Katibu Mkuu Wizara ya Maji naye kumshitaki Mbunge Slaa
Na John Stephen
KATIBU Mkuu wa Wizara ya Maji, Patrick Rutabanzibwa naye amesema kuwa atamshitaki Dk Willibrod Slaa na wenzake kwa kumtuhumu kuwa ni fisadi na kwamba endapo atamuomba radhi, yuko tayari kumsamehe.
Akizungumza katika mkutano na waandishi wa habari kwenye ofisi za wizara hiyo jana, Rutabanzibwa alisema kuwa tuhuma zilizotolewa dhidi yake zimemsononesha na kumsikitisha na kwamba anakusudia kumshitaki Dk Slaa ili kusafisha jina lake.
"Slaa amenitumu kuwa mimi ni fisadi na tuhuma hizo zimenichafulia jina na heshima yangu, lakini akiniomba msamaha nitamsamehe kwa sababu nataka kusafisha jina", alisema Rutabanzibwa.
Rutabanzibwa alisema kuwa kutokana na tuhuma hizo, atachukua hatua za kisheria, ikiwepo kufungua kesi mahakamani ili haki itendeke.
Alisema kesi hiyo ataifungua wakati wowote kuanzia sasa baada ya kumaliza kukusanya ushahidi na hatajiuzulu hata kama ni kwa manufaa ya umma.
"Kazi ninayoifanya si ya kibarua. Nimeteuliwa na Rais na nikijiuzulu nitamwambia nini Rais", Alisema.
Alisema kuwa amechelewa kuzijibu tuhuma hizo kwa sababu alikuwa akitafuta nakala za tuhuma ambazo zilielekezwa kwake na Dk. Slaa.
"Nimechukua muda mrefu bila kujibu tuhuma dhidi yangu lakini jana niliona nakala ya DVD, nikasema leo nijibu", alisema Katibu huyo.
Rutabanzibwa alisema kigezo kuwa alitumia wadhifa wake vibaya kwa kulitia hasara Taifa wakati akiwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini si sahihi na wala hakuna ukweli.
Alifafanua yeye hakuhusika katika kutia saini mkataba wa kuzalisha umeme wa dharura wa IPTL na Serikali na kwamba mkataba huo ulipitishwa na Baraza la Mawaziri na ulifuata sheria ya madini ya Taifa.
"Sikuwa Katibu Mkuu wakati mkataba wa IPTL ukisainiwa Mei 26, mwaka 1995 na niliteuliwa kuwa Katibu wa Wizara ya Nishati na Madini Mei 11, mwaka 1997", alisema Rutabanzibwa.
Rutabanziwa alisema madai kuwa yeye binafsi ana hisa katika Kampuni ya Tanglod inayosimamia hisa za Serikali katika kampuni za madini, si za kweli kwani yeye aliteuliwa na Serikali ili kulinda maslahi ya Taifa.
Katika hatua nyingine, alisema baada ya Dk. Slaa kumtuhumu kuwa ni fisadi amekuwa akipata shida kwa kuwa mitaani watu wanamuita yeye ni fisadi.
"Mitaani watu wananiita mimi ni fisadi, wananiambia kuwa mimi ndio ninayeitafuna nchi", alisema.