Umerejesha matumaini kwa wananchi wazalendo na wanyonge ambao walichagua kukaa kimya wakati rasilimali za nchi yao zilipokuwa zinaporwa huku mapato ya kodi zao yakiwanufaisha wachache huku wao umaskini ukiwaandama na kupata huduma duni za afya, elimu, maji nk
Leo tunashuhudia ulivyoamua kusimama kwa ujasiri na upendo mkubwa kwao kuhakikisha rasilimali za nchi yao zinawapa ustawi wa maisha na kuipa nchi maendeleo. Tumeshuhudia namna ulivyoamua kila senti inayoingia serikalini iende kuboresha maisha ya wananchi wako kwa kupunguza kwa kiwango kikubwa matumizi yenye sura ya anasa na ufujaji kwa viongozi wa serikali.
Hakika imani ni amana. Deni la fedha hulipwa kwa fedha, deni la hisani hulipwa kwa hisani vivyo hivyo deni la imani hulipwa kwa imani kupitia mwenendo na vitendo bora kabisa ili kukidhi matarajio ya waliokupa imani, Rais Magufuli umetulipa imani tuliyokupa.
Matokeo ya haya yote tumeshuhudia elimu bila malipo kuanzia darasa la kwanza hadi kidato cha nne, ujenzi wa reli ya kisasa ya SGR kutoka Dar-Dodoma kilomita takribani 700, usambazaji umeme vijijini kwa gharama nafuu, ununuzi wa ndege sita mpya kwa ajili ya kuliimarisha shirika letu la ndege ATCL, upanuzi wa bandari za Dar es Salaa, Mtwara na Tanga; ujenzi wa miradi ya kuongeza uzalishaji wa umeme nchini kupitia gesi asilia kama kule Kinyerezi II, III, & IV pamoja na maji kama ule wa Stieglers gorge ili kuipa nchi yetu umeme wa uhakika na nafuu. Vile vile tunashuhudia uwekezaji na ujenzi wa viwanda vya kati na vikubwa ukifanyika kwa kasi kubwa maeneo mbalimbali ya nchi yetu hakika unastahili pongezi na sifa.
Kazi yako inastahili heshima mbele za wanadamu na hata mbele za Mungu. Tunakuombea afya njema ili uendelee kuwatumikia watanzania wenzako.
#ChapaKazi