Mbunge wa jimbo la Ngorongoro, Emmanuel Ole Shangay anashikiliwa na Jeshi la Polisi kuanzia jana Agosti 21, 2023 kutokana na tuhuma za kuhusishwa kupanga tukio la kushambuliwa waandishi wa habari.
Shangay alijisalimisha polisi baada ya kupokea wito wa kufika polisi ofisi ya Mkuu wa Upelelezi Mkoa wa Arusha (RCO) na baadae alitakiwa kuripoti kituo cha Polisi Karatu.
Mwenyekiti wa CCM wilaya ya Ngorongoro, Lucas Ole Seina amethibitisha leo Agosti 22, 2023 kwamba ni kweli mbunge huyo alikamatwa alipokwenda kuripoti polisi ili kuhojiwa kwa sababu kuna shida ilitokea mnadani wa Eblini kwa waandishi wa habari kupigwa.
“Baada ya kuhojiwa, ndugu na jamaa waliambiwa waende kesho asubuhi (leo) kwa ajili ya kuwekewa dhamana lakini walipofika asubuhi, hakuweza kujulikana mahali alipo. Kwa hiyo hatujui kama yupo kituoni Karatu au Arusha, kwa hiyo bado tunafuatilia kujua yuko wapi,” amesema Seina.
Hata hivyo, jitihada za Mwananchi kumtafuta Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha, Justine Masejo kuzungumzia kushikiliwa kwa mbunge huyu hazikuzaa matunda.
Hata hivyo, diwani wa CCM kata ya Elelai, James Moringe amedai wakati wakiwa njiani na mbunge huyo kukaribia Karatu katika eneo la Rhotia walisimamishwa na Polisi ambao walimchukuwa mbunge huyo kwenye gari lao.
Wakili Joseph Ole Shangay ambaye alikuwa ameambatana na mbunge huyo amedai baada ya mbunge kufikishwa polisi alielezwa anashikiliwa kwa tuhuma za kujeruhi watu wawili.
Hata hivyo, Wakili anayemtetea mbunge huyo, Simon Mwambo kupitia Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu (THRDC) amesema kuwa walipata taarifa ya mbunge huyo kufikishwa kituo cha Chekereni Arusha.