Vuguvugu la mapinduzi kwa nchi za Afrika zinazoongea Kifaransa linaendelea. Baada ya Burkina Faso, Mali, Niger, Chad na Guinea, sasa ni zamu ya Gabon. Jeshi la Gabon limetangaza kuifurusha serikali ya Rais Ali Bongo baada ya vurugu zilizotokana na matokeo ya uchaguzi.
Jana Tume ya uchaguzi ya nchi hiyo (CGE) ilitangaza Rais Ali Bongo anayegombea awamu ya 3 amepata kura 64.2% huku mpinzani wake mkuu Profesa Albert Ondo Ossa akipata 30.7%. Kufuatia matokeo hayo wananchi waliingia mtaani wakidai kumefanyika udanganyifu, hali iliyosababisha Jeshi kuingilia kati na kupindua serikali.
Taarifa iliyotolewa na Jeshi kupitia kituo cha Televisheni cha Gabon 24 imeeleza kuwa Rais Ali Bongo yupo chini ya ulinzi na serikali imevunjwa. Jeshi pia limetangaza kuvunja bunge na Mahakama, na kuunda baraza la uongozi la mpito la kijeshi, litakaloongoza mpaka utakapopatikana utawala wa kiraia.
"Tumevunja bunge, serikali na mahakama. Hakuna mhimili wowote utakaofanya kazi kuanzia sasa. Jeshi litaongoza nchi kwa kipindi cha mpito hadi hali itakapotulia. Tumefanya hivi kulinda watu wetu na amani yetu" imeeleza taarifa ya Jeshi.
Kufurushwa kwa Rais Bongo kunahitimisha miaka 57 ya familia yake kuongoza taifa hilo. Baba yake Mzee Omari Bongo aliongoza Gabon kwa miaka 43 kuanzia mwaka 1966 hadi mwaka 2009 alipofariki. Baada ya kifo chake mwanae Ali Bongo alichukua madaraka na kuongoza kwa miaka 14 kutoka 2009 hadi leo alipopinduliwa.
Familia ya Bongo inashutumiwa kwa matumizi mabaya ya madaraka na fedha za umma. Mwaka 2019 ndugu wa Rais Bongo, ambao ni Omar Denis Bongo na Paskalina Bongo walituhumiwa kupokea rushwa ya £85M sawa na TZS Bilioni 230 ili kuisaidia kampuni moja ya Ufaransa kuchimba mafuta nchini Gabon.
Pia Rais Bongo anatuhumiwa kwa "nepotism" na kujaza ndugu zake wengi katika nafasi za juu serikalini wakiwemo watoto wake Malika Bongo, Noureddin Bongo, Jalil Bongo, Bilal Bongo na Jean-Valentin Bongo.
Gabon ni nchi ya 6 barani Afrika kufanya mapinduzi hivi karibuni. Nchi nyingine mbili, Guinea-Bissau na São Tome &Principe pia zilifanya mapinduzi lakini yakazimwa. Nchi zote hizo ni makoloni ya zamani ya Ufaransa. Ufaransa inaishutumu Urusi kuwa nyuma ya mapinduzi hayo.!