Malaika Wa Shetani

Malaika Wa Shetani

36.
Alipofika hotelini alimkuta Nuru ameamka kitambo na sasa ameketi kitandani kwa namna ya mtu mwenye wasiwasi na maswali mengi kichwani. Joram alimwendea na kumbusu





shavuni. Nuru hakuonekana kulipokea busu hilo. Busu la pili vilevile halikuzaa matunda yoyote. Joram akacheka na kumwachia. Akaamia kwenye kochi ambako aliketi na kuiwasha sigara yake.

“Huna haja ya kununa. Mke mwenzio amekwishakufa.” “Nani?”

“Betty… Yule msichana wa jana.”

Macho ya mshangao yakamtoa Nuuru. “Amekufa! Amekufaje?” Joram akamweleza kila kitu, pia akampa ile picha aliyoikuta humo ndani. Kwa sauti iliyojaa masikitiko Nuru alinong’ona, “Alikuwa mtu pekee ambaye angeweza kukusaidia, kama kweli angekusaidia. Kinachonishangaza ni hii picha yako. Aliipataje?

Na kwanini awe ameificha? Kama alikupenda si angeiweka

hadharani tu?”

“Yote hayo tutayajua hii karibuni,” lilikuwa jibu pekee la Joram.



***

Waziri Mkuu, Shubiri Makinda alikuwa mtu mwenye historia ndefu kama ilivyo historia ya nchi hiyo ya Pololo, kama si zaidi. Jina lake lilijitokeza katika kila orodha yenye majina mashuhuri ambayo yalihusika kwa njia moja au nyingine, tangu zilipoanza ndoto za uhuru; ndoto zilipotukia kuwa kweli na hadi sasa ambapo serikali huru ilikuwa ikijitawala. Mara nyingi jina hilo lilifuata nyuma ya lile la Shangwe, ingawa mara nyingine lilihama na kushuka chini ya orodha. Kwa sasa lilikuwa la pili kutoka juu.
 
37.
Hayo Joram aliyaona tena baada ya kuanza utafiti wake juu ya nchi na siasa ya nchi hii, hasa akiitafuta nafasi halisi ya Waziri huyo. Haikuwa kazi kubwa kujipatia vitabu vingi ambavyo vimeyaelekeza yote hayo kwa mapana na marefu. Hata hivyo, kama alivyotegemea humu, yote yalikuwa mema yaliyompamba Shubiri Makinda kama mtu mtukufu na mtakatifu sana, ambaye hakuwa mbali sana na malaika. Siku zote alikuwa shujaa, mwenye hekima za ajabu, mpenzi wa nchi na wananchi, mwaminifu kwa Rais, asiye na tamaa wala ndoto za kibinafsi na kadhalika. Kalamu za waandishi wote, walao kwa kukosea, hazikumchora kama binadamu wa kawaida ambaye anaweza kupotoka wala kuropoka.

Kitu pekee kilichomsisimua Joram katika maandishi hayo





duni ni pale aliposoma kuwa Shubiri na Rais Shangwe walikuwa marafiki tangu wakiwa shule ya msingi, kwamba tangu hapo walikuwa pamoja katika kila darasa na kila chuo hadi walipokwenda ng’ambo ambako walirudi na ndoto za uhuru.

‘Yawezekana kuwa madaraka aliyonayo shubiri yanatokana na urafiki wa Rais Shangwe kutokana na tabia ya viongozi wengi wa Afrika kupeana vyeo kama zawadi? Joram alijiuliza wakati akiendelea na uchunguzi wae.

Baada ya kupitia vitabu vyote vilivyoelezea historia ya maisha yake alianza kusoma vile ambavyo viliandikwa na Shubiri mwenyewe. Alikuwa ameandia kitabu kimoja tu kwa lugha ya kiingereza: This way Men. Vingine vyote vilikuwa ni mkusanyiko wa hotuba zake mbalimbali. Katika maandishi hayo Joram aliipata picha ya Shubiri kama mtu mwenye ndoto zote za kujenga nchi ya Ujamaa ingawa mara nyingi aliepuka kutaja Ujamaa huo kwa jina. Zaidi, alionyesha kama mtu ambaye alikuwa akiwalilia watu na taifa zima liongeze juhudi na moyo katika kuinua uchumi, elimu ushirikiano na kujitegemea kikamilifu. Ilikuwa dhahiri kuwa hakuridhika na mafanikio ya nchi yake katika kila fani, akiamini kuwa wangeweza kufanya vizuri zaidi. Katika maandishi hayo Joram hakuona kile ambacho alizoea kukiona katika vitabu na maandishi ya viongozi wengi wengine, tabia ya kuwatupia lawama mfanyakazi na mkulima, kama kwamba wangefanya hivi ingekuwa hivi… na kadhalika. Shubiri alielekea kama mtu aliyesimama njia panda akiangalia kila upande, jambo ambalo lilimfanya Joram ajikute akisahau kuwa anamchunguza Shubiri kama adui na badala yake akaanza kumpenda, mapenzi ambayo yalitoweka mara moja alipopata jalada lenye picha mbalimbali za Waziri Mkuu huyo toka katika ofisi moja ya chama.

Picha zote zilimwonyesha Shubiri kama mtu mkatili asiye na muda walao kumwonyesha meno mpiga picha ili wasomaji wa magazeti waone kuwa anacheka. Karibu picha zote alikuwa mkimya, mtulivu, aonekanaye kama aliyenuna. Kwa nadra sana, kama picha mbili tatu, Joram aliona dalili za tabasamu katika uso wake. Hata hivyo, tabasamu hilo lilikuwa kitu kingine kilichoyavuta macho ya Joram. Lilikuwa tabasamu lililoficha au kufichua kitu kama msiba au maombolezo katika fikra au moyo wake. ‘mtu mwenye jina kubwa na maisha mazuri, mtu anayepokelewa kwa hadhi ya kifalme popote duniani; mtu wa
 
38.
pili kwa ukubwa, katika nchi nzima yenye mamilioni ya watu, vipi awe na msiba rohoni mwake? Mungu ampe nini zaidi?’ Joram alijiuliza.

Aliendelea kuzichunguza picha za Shubiri. Pamoja na kutokuwa na furaha, Joram aliridhishwa na sura yake yenye paji pana la uso, ndevu fupi zilizokizunguka kidevu kinene kilichojaa na kukizingira kinywa ambacho kilionekana kuafikiana na pua yake ndogo nyembamba. Umbo lake refu nene lenye dalili zote za ukakamavu lilikubaliana na suti zake nyeusi ambazo alipendelea kuvaa, suti ambazo zingependeza zaidi kama kando yake kungekuwa na aina fulani ya mavazi ambayo… kama…

Mara Joram akakumbuka kitu kipya. Wako waliosema kuwa nyuma ya kila mwanaume aliyefanikiwa huwa yuko mwanamke. Katika watu waliofanikiwa Shubiri yu miongoni mwao. Kati ya maandishi yote aliyosoma hakukumbuka kuona kitu chochote juu ya ndoa au talaka ya Shubiri. Wala katika picha zote hakupata kuona maelezo yoyote ya mtu na mkewe. Vipi? Shubiri hajaoa? Kisa na mkasa?

‘Waziri Mkuu… kumwaga damu…. Kwa ajili ya mapenzi….’ Maneno ambayo hayati Betty alidai kuyapata toka katika ndoto za mpenzi wake, Patauli Kongomanga, yalimrudia akilini. Mapenzi! Mapenzi yapi? Kitu mapenzi hakikuwemo kabisa katika historia yote ya Shubiri, iliyoandikwa.

Lakini kuna historia ambayo haikuandikwa. Kila binadamu ana mambo yake ambayo angependa kufa kuliko kuyaona yakiandikwa na kusomwa hadharani. Bila shaka

Shubiri, kama binadamu, anayo yake. Ni hayo ambayo Joram aliyahitaji. Si haya ambayo yamechujwa na kutiwa chumvi na sukari ili yapendeze machoni na masikioni mwa dunia.

Joram aliyahitaji hayo mengine. Mara akaona anapoteza bure muda wake kushinda katika maktaba hiyo kwa saa nyingi siku nenda rudi akisoma kile ambacho ameandaliwa, kama kipofu anayepewa fimbo na kuongozwa njia. Akayabwaga majitabu hayo na kutoka zake nje.



***

Uzee ni maktaba isiyo kifani. Kuna wale wazee ambao historia imewasahau au kuwatupa kando wakati ikiendelea na mkondo wake, wazee ambao utake usitake ni kama punje moja ya





mchele uliomo katika gunia; kulifanya liitwe gunia la mchele. Kwa njia moja au nyingine wameshiriki na kuwa sehemu ya historia wakitazama inavyopita taratibu mbele yao, ikibadili sura na kuneemeka au kumeguka hapa na pale. Japo historia imewasahau wazee hao, lakini wao hawakuisahau. I hai katika fikra na mioyo yao.
 
39.
Mmoja kati ya wazee hao alikuwa Pondamali Kalulu. Huyu alijaa habari nyingi za kale. Na alizikumbuka kwa uhakika kama kanda ya video ambayo ikishanasa imenasa. Na hakuna alichopenda zaidi ya kusimulia historia hiyo, kutwa kucha. Pengine ni hilo ambalo lilimfanya ajione sehemu ya historia hiyo. Joram alimfikia mzee huyo baada ya kuongea na watu mbalimbali ambao hawakumsaidia sana zaidi ya kulitaja jina la mzee huyo mara kwa mara. Ndipo akafanya safari hii fupi ya kuuacha mji na kuja huku kitongojini ambako alielekezwa nyumbani kwa mzee huyu. “Naandika kitabu cha historia, kitabu hasa. Unajua hivi vyote vilivyoandikwa havina historia kamili? Nataka kitabu ambacho kimeandikwa kwa msaada wa mtu anayeijua historia. Nimeambiwa wewe unaifahamu, Mzee

Pondamali, utanisaidia?”

Ni hayo tu ambayo yalimfanya babu huyo ajikongoje kuwapeleka Joram na Nuru hadi chini ya mti uliokuwa na kivuli kikubwa, mbele ya nyumba yake, ambapo kulikuwa na viti maalumu vya wacheza bao. Walipokwishaketi alitabasamu akiruhusu meno yake manane tu yaliyosalia mdomoni yaonekane. “Kitabu sio, bwana mdogo? Usiwe na shaka kitabu chako kitakuwa na uhakika. Kitanunuliwa kama peremende. Utakuwa tajiri sana. Lakini mimi sitaki pesa. Nimebakiwa na siku chache za kuishi. Huko niendako pesa hazihitajiki,” aliwatupia tena kicheko kingine wageni wake kabla ya kuuliza, “Unataka kuandika juu ya nini?”

Badala ya kufurahi Joram alisikitika kidogo alipomwona mzee huyo alivyokuwa na hamu ya kuzungumza naye. Hakujua kama maongezi yake yangeweza kumpotezea maisha. Tangu juzi Betty alipouwa kikatili kwaajili ya kuzungumza naye Joram alikwishajenga tabia ya hofu sana kwa maisha ya watu. Hakupenda awe kisa cha mauti ya watu wasio na hatia. Kwa bahati mbaya, hakuwa na njia nyingine ya kuwasaida watu bila ya kuzungumza na watu. Hata hivyo, sasa alikuwa akizungumza





na watu ambao alizungumza nao hadharani bila dalili yoyote iwezayo kumwonyesha mtu anayemchunguza kuwa anapeleleza. Wengine alizungumza nao kwa siri sana. Mfano ni huyu mzee. Akiwa na hakika kuwa kuna watu wanaomchunguza kwa makini, wakiwa na silaha mfukoni, waliondoka na Nuru hotelini kwa mwendo wa mtu na mpenzi wake wanaopunga upepo. Huko mbele walipanda basi na kuteremka mahali ambapo walipenya katika uchochoro hadi mtaa wa pili ambako walipanda basi jingine. Hadi kufika hapo walikuwa wamebadili mabasi mara nne.

Kitu kingine ambacho kilimfanya aongeze uangalifu ni tangazo la mkuu wa polisi baada ya maiti ya Betty kupatikana. Mkuu huyo alitokea katika televisheni akisema kuwa mwuaji angepatikana baada ya muda mfupi kwani watu wengi walimwona akiingia chumbani humo na kwamba wasingesita kumtambua mara watakapomwona tena. Aliongeza kuwa wasanii wa polisi walikuwa wakikamilisha michoro inayoonyesha sura za watu mbalimbali ili mashahidi hao waeleze alivyofanana, picha ambayo ingetolewa gazetini. Lakini saa chache baadaye mkuu huyo wa polisi alibadili kauli na kusema kuwa inaaminika muuaji wa mama huyo ni mwendawazimu mmoja ambaye alikamatwa na jisu lenye damu mtaa wa jirani akikusudia kumwua mtu mwingine. Ni hilo lililomshitua Joram. Alijua kuwa mabadiliko hayo yalifanywa kwa ajili yake na mtu mkubwa serikalini. Rais, au mtu wake wa pili kwa ajili ya kumlinda yeye. Lilimsumbua kwa kuona kuna mtu au watu wanaoangalia kila mwenendo na kitendo chake, jambo ambalo si la kupendeza hata chembe katika shughuli kama hizi. Yeye alikuwa mtu wa kujilinda si kulindwa, na hasa kulindwa na mtu ambaye humfahamu; mtu usiyejua ana nguvu kiasi gani na iwapo ni adui au rafiki.
 
40.

Hali hiyo ilimfanya atembee kwa adhari kama chui aliyejeruhiwa. Watu wa kawaida, wenye macho ya kawaida walimwona kama kijana mwingine wa kawaida ambaye yumo katika matembezi ya kawaida. Aidha, walimwona Nuru kama msichana mzuri mwenye starehe zote akilini na rohoni, fikra zake pekee zikiwa anasa na mahaba. Hawakujua kama wawili hawa walitembea huku miili yao imebeba silaha hatari ambazo zingetosha kuteketeza kikosi cha jeshi ambalo halikufundishwa vizuri. Bastola, silaha ya kawaida, zilikuwa mgongoni mwa Joram

na katika mapaja ya Nuru. Bomu la machozi, hewa ya sumu, vinasa sauti, kamera ndogo za kijasusi pamoja na vikorokoro vingine vilikuwa katika hifadhi nzuri miilini mwao.

Hata hivyo, kitu fulani kilimnong’oneza Joram kuwa iwapo kweli hukumu ya kifo ilikuwa imetolewa dhidi yake, yeyote yule anayeitoa hukumu hiyo alikuwa hakupanga tarehe maalumu ya kifo hicho. Vinginevyo, muuaji asingeshindwa kutumia fursa nyingi zilizojitokeza. Wala isingekuepo haja ya kumwua Betty na kumwacha yeye hai na badala yake kujisumbua kumtisha kwa maneno badala ya risasi. Japo isingekuwa rahisi kumwua Joram kama adui huyo alivyofikiria, lakini bado Joram aliamua kuzidisha uangalifu kwa makini zaidi. Daima macho yake yalikuwa wazi, masikio yakiwa makini na mwili mzima timamu kwa lolote.

“Kitabu chako, bwana mdogo,” Mzee Kalulu alikuwa akiendelea baada ya kujiwashia sigara yake yenye harufu kali. “Kitanunuliwa utashangaa.” Alijiweka vizuri juu ya kiti chake na kuruhusu mapengo yake yaonekane tena kwa tabasamu lake ambalo huko nyuma liliwatesa sana wasichana. “Unajua kuwa nafahamu mambo mengi ambayo hata wazee zaidi yangu hawayafahamu?”

“Kwa mfano,” aliendelea. “Hawa vijana wanaoongoza nchi, kama Rais na baraza lake la mawaziri. Hawa mimi nawafahamu nje ndani. Nazifahamu hata siri zao ambazo kama wangejua kuwa nazifahamu wangeninyonga. Ni siri ambazo wangependa kuzifuta kabisa katika maisha yao.” Alicheka ghafla kabla ya kuuliza, “Unajua kuwa wanachangia mwanamke?”

Mzee hakuhitaji jambo lolote zaidi ya swali hilo kumfanya Joram na Nuru wawe wasikivu zaidi ya walivyowahi kumsikiliza mwalimu yeyote duniani. Hata hivyo, wakiwa watu wanaoifahamu kazi yao vizuri hawakuonyesha dalili yoyote ya kuvutiwa sana na habari au ubaya huo zaidi ya kawaida. “Mwanamke?” Joram aliuliza baada ya kumtazama Nuru na mzee huyo kwa tabasamu. Nani na nani wanaochangia mwanamke?”

“Rais na Waziri Mkuu wake.” “Mwanamke yupi? Hawara…”

“Mke! Mke wao,” Mzee Kalulu alimkatiza Nuru. “Ni hadithi ndefu sana, tamu sana, ya siri sana na ilitokea zamani sana. Wao wanafikiri hakuna mtu anayeifahamu, lakini sisi wazee





ambao tunaona kila kitu tuliona na tunaendelea kuona…” “Wakati huo nilikuwa kijana bado. Wao walikuwa watoto.

Niliwafahamu kwa kuwa mwalimu wao wakiwa darasa la kwanza hadi la nne alikuwa rafiki yangu mpenzi. Alikuwa mwalimu wa ajabu kwa jinsi alivyoipenda kazi yake na wanafunzi wake. Kila nilipotoka zangu nyumbani kwa bwana Pony, aliyekuwa mkuu wa wilaya, mimi nikiwa mtumishi wake nilimkuta Puta, huyo mwalimu rafiki yangu akiwa nyumbani kunisubiri. Tulifuatana kilabuni ambako tulikunywa na kuongea. Wakati huo ukiwa na shilingi mbili utakunywa bia na kuku mzima wa kuchoma, tulijisikia kama tunaoishi peponi. Kila mtu kijijini hapo alituheshimu. Yeye kama mwalimu na mimi mtumishi wa bwana mkubwa. Hivyo, mara nyingi tulilewa kwa kutumia wadhifa badala ya pesa.” Hilo lilimfanya mzee Kalulu atokwe na tabasamu jingine.

“Mwenzangu alikuwa hana maongezi zaidi ya kusimulia mambo ya wanafunzi wake. Huyu hivi, huyu vile, michezo yao, utukutu wao, akili yao darasani na mengineyo. Siku moja alinieleza juu ya wanafunzi wawili ambao anasema siku waliyoanza shule tu, walipigana hata kutoana ngeu, lakini baada ya ugomvi huo sasa ilikuwa imepita miaka miwili wakiwa marafiki, chanda na pete…”

“Watoto hao walikuwa hawaachani popote waendapo. Huyu akitumwa huyu, huyu anatoroka hadi amfuate mwingine. Wala hawanyimani kitu, cha huyu ni cha huyu. Na kwamba kitu kikubwa kilichomfanya mwalimu huyo kuwatia maanani ni akili zao. Walikuwa wakiongoza darasani katika kila mtihani. Huyu akiwa wa kwanza huyu atakuwa wa pili. Wala alama zao hazikutofautiana sana, jambo ambalo lilifanya walimu kushuku kuwa walikuwa wakionyeshana. Lakini baada ya uchunguzi mkubwa ilidhihirika kuwa kila mtu alikuwa na akili zake ingawa wakati fulani walisaidiana.”
 
41.

“Urafiki wao uliendelea hadi walipomaliza shule ya msingi na kuchaguliwa kwenda sekondari. Huko pia walikuwa katika bweni moja. Huko pia akili zao zilichemka na kuongoza si darasani tu bali katika maongezi ya kawaida na mijadala ya hadhara pia. Walipowekwa katika upande mmoja wa kongamano upande wa pili hawakufua dafu. Na walipokwenda pande mbalimbali ulikuwa ubishi mzito ambao haukuelekea kupata mshindi.





Kadhalika, walikuwa mstari wa mbele katika michezo yote, pamoja na gwaride. Uhodari wao haukuchelewa kuwapitia uongozi mwaka wa pili tu wa maisha yao hapo sekondari, mmoja wao akiwa kiranja mkuu.”

“Nilishangazwa na jinsi mwalimu huyo alivyokuwa akipata habari zao za huko sekondari, iliyokuwa maili kumi na tano toka hapo kijijini kwetu. Lakini yeye aliniambia kuwa kila jumapili watoto hao walimtembelea nyumbani kwake na kumsimulia maendeleo yao. ‘Wangefaa kuwa pacha,’ alikuwa akinisumbua mara kwa mara. Nilipolewa nilimwambia awafanye kuwa pacha badala ya kunipigia kelele.” Alitabasamu akimtazama Joram na Nuru kwa shahuku.

“Ikaja siku ambayo rafiki yangu alikuja na habari mpya zaidi. ‘Wanataka kuoa’ alinieleza. “Nani?” nilimwuliza. ‘Wale watoto,’ alinieleza. ‘Wamepata wachumba kijiji cha Pongwe, si unakikumbuka? Harusi yao itakuwa ya ajabu kama walivyo watoto wa ajabu.’ “Kwa nini?” Alinieleza kwamba wamepata wasichana wazuri sana ambao ni pacha, kwamba watoto hao wamefanana sana ambapo huwezi kuwatofautisha. Wasichana hao wamewapenda sana wanafunzi hao na walikuwa tayari kufunga nao ndoa mara tu wamalizapo shule. Ilisemekana kuwa harusi zao zingefanyika pamoja, siku moja.

“Siku chache baadaye mwenzangu alikuwa na habari nyingine ya kusisimua. ‘Wamekwenda Ulaya kuongeza masomo! Aliniambia kwa furaha kana kwamba ni watoto wake. Sikuwa na haja ya kumwuliza ni akina nani hao. Picha zilitokea siku chache baadaye katika magazeti, wakiwemo miongoni mwa watoto wanane waliokuwa wakienda zao kuongeza masomo nje ya nchi. Wakati huo kwenda Ulaya ilikuwa sawa na kwenda peponi, wajukuu zangu mnaweza kufahamu majina hayo yalivyoongeza uzito!”

Mzee alitulia kwa muda akishughulikia sigara yake. Ghafla, aliwakazia macho Joram na Nuru. Kisha akaangua kicheko kabla ya kuongeza kwa sauti ya majivuno, “Halafu na mie nilipata habari ya kumsimulia rafiki yangu huyo.” Alisita tena. “Ilikuwa baada ya miaka minne tu tangu walipoondoka nchini. Nilimkuta bwana

D.C wakifoka kwa ukali huku majina ya wale watoto wawili. Abdul Shangwe na Shubiri Makinda, yakitajwatajwa. Baada ya kuwasikiliza kwa makini nilielewa kilichowafanya wazungu hao





kuwa na wasiwasi. Kweli, walikuwa watoto wa ajabu. Siku hiyo niliona kama saa haziendi ili nirudi nyumbani kumshangaza rafiki yangu kwa habari hiyo mpya. Saa zilienda taratibu zaidi ya kinyonga. Zilipotimu niliendesha baiskeli kama kichaa hadi nyumbani. Nilimkuta rafiki yangu ndiyo kwanza anafika. “Watoto wako wanataka uhuru,” nilimwambia. Nikamweleza kwa tuo kwamba wamerudi nchini na kuanzisha chama cha kudai uhuru; na jinsi chama hicho kilivyokuwa kinaungwa mkono na watu wengi.

“Ilinishangaza kuona rafiki yangu Puta hakushangazwa sana na habari hiyo. Alichofanya ni kucheka kidogo na baadaye kuniuliza ‘Sikukuambia kuwa ni watoto wa ajabu? Uongozi wao pia utakuwa wa ajabu. Shubiri atakuwa Rais wa aina yake,’ alinieleza.”
 
hii copy and past itaakuja kuwaghalimu siku moja....hivi umeomba hidhini ya mmiliki kufanya hichi ulicho fanya...?
 
42.


Habari hiyo zilifuatwa na pilikapilika za vita vya uhuru. Maneno yakiwa silaha, vijana hao walishangaza ulimwengu kwa jinsi walivyoshinda uongo, hila na vipingamizi vyote vya mkoloni. Waliandamwa pia na vitisho vya kuwekwa gerezani na kutishiwa kufa. Hawakukata tamaa. Mmoja alipowekwa gerezani wa pili alisimama hadharani kulaani unyama huo hata mwenzake akaachiwa. Na alipotoka neno la kwanza lililomtoka mdomoni lilikuwa ‘Uhuru.’ Taratibu, wakati wenye roho nyepesi wakianza kukata tama, dalili za uhuru zilianza kujitokeza.

‘Atakuwa Rais wa ajabu!’ mwenzangu aliendelea kunong’ona. ‘Unajua pamoja na shughuli zake nyingi kila anapopata fursa anakuja kunisalimu?’ aliuliza. Hilo kwa kweli sikulitegemea. Wakiwa watu wenye shughuli nyingi, wasiolala usiku na mchana, huku wakiwindwa na serikali ya mkoloni sikuona vipi wangeweza kupata wasaa wa kumtembelea mzee huyo ambaye licha ya kwamba hana lolote la kuwaambia bado waliachana naye miaka mingi ya utoto wao. “Wanakuja?” nilimwuliza. ‘Anakuja, Shubiri anakuja. Hata usiku wa manane anakuja. Na kila akija ananiletea zawadi, walao ndogo. Juzi kaniletea tochi. Unajua hajabadilika kabisa yule mtoto? Tabia yake bado ileile. Mkimya na msikilizaji kuliko alivyo msemaji. Kila akija nategemea awe na la kuniambia, lakini naishia mimi kumsimulia yeye. Na sijui namsimulia nini. Naona kama anafurahia kuisikia sauti yangu tu.’

“Na siku chache mwenzangu alinitembelea katika hali ya





huzuni na msiba mkubwa. ‘Tuna msiba,’ aliniambia, ‘Tumefiwa na mke wetu,’ “Mke yupi?” nilimwuliza. Alinieleza kuwa mmoja kati ya wale pacha wazuri, wachumba wa Shangwe na Shubiri alikuwa amefariki kwa ajali ya kutumbukia mtoni na kuliwa na mamba. “Ni mchumba wa nani aliyepotea?” nilimwuliza. ‘Hilo ndilo tatizo’ alinijibu kwa huzuni kubwa. ‘Wasichana wale wanavyofanana, hakuna anayefahamu nani alikuwa mchumba wa nani zaidi ya msichana mwenyewe. Nina mashaka hata wazazi wao watapata matatizo hayo. Hofu yangu ni kwamba vijana hawa wanaweza kukosana kwa suala hili. Mwanamke ni ibilisi bwana.’ Nilijaribu kumweleza kuwa vijana hao wana akili nyingi na timamu, kamwe wasingeweza kuharibu kazi na hadhi yao kwa jambo dogo kama hilo, lakini mwenzangu hakuelekea kuniamini sana. ‘Pengine uniambie kuwa kwa jinsi wanavyopendana wote wataamua kumwacha msichana huyo,’ alieleza.

“Miezi kadhaa ilipita. Ikafika siku ambayo harusi ya kufana ilifanyika jijini. Abdul Shangwe alimwoa Tunu Mtoro, rafikiye Shubiri akiwa mshenga. Ilikuwa sherehe kubwa ambayo ilikumbukwa na watu kwa muda mrefu.

“Siku chache baada ya harusi hiyo bendera ya mtu mweupe ilishuka na Mtu Mweusi kuchukua nafasi. Wazungu, machozi yakiwatoka, waliporomoshwa toka madarakani. Kiti cha Gavana kilikaliwa na Shangwe, mtu wa pili akiwa Shubiri. Waliitangaza katiba yao mpya, ambayo ilikuwa nuru kwa Mtu Mweusi. Matunda yake ndiyo tunayaona na kuyala sasa…”

Mzee aliposita ili kuwasha sigara nyingine Joram alipata fursa ya kupenyeza swali. “Mzee, yu wapi huyo rafiki yako mwalimu? Siku hizi hakutembelei?” Joram aliuliza.

“Uzee, baba, uzee umemzidi nguvu. Huu mwaka wa nane sasa sijamtia machoni. Lakini hajafa. Kama angekufa ningepata habari mara moja. Yuko hai katika kijumba chake cha mbavu za mbwa kijiji cha Polo ambacho toka hapa ni mwendo mfupi tu.”

Kisha mzee huyo alishituka kidogo baada ya kulitazama jua ambalo lilikuwa likielekea kuaga. “Mungu wangu,” alifoka. “Saa zimekwisha na wala hatujaanza. Anza kuuliza maswali yako. Unataka kuandika kitabu cha nini vile?”



***

Jua lilikuwa likifikia kiota chake cha magharibi wakati Joram





na Nuru walipomwacha mzee huyo kwa ahadi ya kurudi kesho kuanza kuandika kitabu chao. Nuru ya kawaida ilikuwa tayari imemezwa na ile nzito ya dhahabu ambayo pia ilikuwa ikitoweka taratibu na kiza kuchukua utawala. Joram alilifurahia sana giza hilo. Alikuwa ameushika mkono wa Nuru akimwongoza kama mwenyeji, toka kichochoro hadi kichochoro hata walipofika kituo cha basi. Joram hakupenda kubahatisha. Hivyo, ingawa alikuwa na hakika kuwa hakuweza kuonekana na mtu yeyote wa hatari pindi wakimwendea Mzee Kalulu bado walitumia hila nzito za kujihadhari kwa kubadili magari na kujipitisha huku na huko. Walipoingia jijini walichagua baa nzuri ambayo waliamua kuitumia kwa kupozana koo kwa kutumia bia mbilimbili, ambazo ziliwapa hamu ya chakula; kilichohitaji kuteremshwa kwa bia nyingine.
 
43.


Ilikuwa yapata saa nne na robo za usiku walipoifikia hoteli yao. Walipofika mapokezi na kumsalimu msichana aliyekuwa zamu aliwapa ufunguo na ujumbe mfupi ambao uliandikwa juu ya kipande cha karatasi ukisema: Mara ufikapo tafadhali nipigie. Joram hakuitaji kuuliza ni nani aliyeleta ujumbe huo bila jina.

Alikuwa na namba moja tu ya simu. Na asingeweza kutumia simu ya ndani. Hivyo, alimtaka Nuru radhi na kurudi nje ambako alifuata kibanda cha simu. Akazungusha namba hizo moja baada ya nyingine.

Sauti ya mtu aliyeipokea haikuwa ngeni masikioni mwake, “Ulikuwa wapi” iliuliza. “Nimejaribu kukupigia mara tatu bila mafanikio.”

“Nilitoka kidogo.” “Kwenda wapi?”

Hilo lilimshangza na kumkera Joram. “Ni lazima ujue kila ninalofanya na popote niendapo?”

“Ndiyo… hapana… lakini unajua hujanipa taarifa yoyote ya maendeleo yako tangu umeanza kazi? Wakati huohuo Napata taarifa za kutatanisha juu yako. Juzi tu ilikuwa uchukuliwe hati kwa kuua mtu. Mimi sikuamini. Nadhani mambo yanatisha kuliko nilivyofikiria awali. Hivyo, nahitaji kupata taarifa yako mara kwa mara. Sawa?”

Joram hakufahamu kwa nini sauti au amri hii ilimchukiza kiasi hicho. Hakuwa mtu wa kuchukizwa kwa vijambo vidogovidogo kama hivyo. Wala hakuwa mtu wa kufundishwa la





kufanya na mtu yeyote duniani. “Sikia mzee,” alijibu. “Nadhani ulipoamua kunipa kazi hii ulikuwa tayari umearifiwa tabia yangu ya utendaji kazi. Sina tabia ya maneno ila vitendo. Vinginevyo, siwezi kusema lolote.”

Joram akasikia pumzi ikishushwa upande wa pili. Ilifuatwa na kicheko kidogo. “Nadhani nazidi kukuelewa, bwana mdogo. Mimi pia sina muda wa kupoteza. Wasiwasi wangu mkubwa ni juu ya maisha yako. Hawa ni viumbe hatari sana. Siwezi kujisamehe iwapo lolote litakutokea kwa uzembe wangu. Hivyo, napenda sana kuhakikisha nyendo zako hazikupeleki hatarini.”

“Usijali mzee, najua kujiangalia. Mie sio mtoto mdogo.” “Nakutakia kila la kheri.”

Simu ikafa masikioni mwa Joram. Akaitua na kurudi hotelini. Nuru alikuwa tayari ametangulia chumbani. Joram akasubiri lift na kumfuata. Alipowasili chumbani hakumwona Nuru kitandani kama alivyotegemea. Bila shaka alikuwa bafuni. Akaamua kumfuata huko, rohoni akifanya sherehe kidogo kwa matumaini ya kumkuta Nuru kama alivyozaliwa; ili naye avue na kuoga naye, jambo ambalo walikuwa hawajalifanya kwa muda mrefu. Nuru katika ngozi ya Nuru, na ulaini wa mwili huo, vingekuwa burudani tosha ambayo ingeikamilisha siku hiyo na kumfanya asahau uchafu wa siku nzima.

Alikwenda bafuni. Na alimkuta Nuru kama alivyotaka, lakini uso wake ulikuwa na kitu ambacho hakukitegemea. “Vipi?” aliuliza akimfuata pale aliposimama akichungulia ndani ya karo. Joram aliyafuata macho ya Nuru. Mara akakiona kilichomfanya uso wake uwe ulivyokuwa. Kilikuwa kipande cha karatasi, kilicholazwa ndani ya karo kikiwa na maneno yaliyoandikwa kwa wino mzito mwekundu: ‘Joram unatafuta kifo chako.’

Joram alifungua bomba la karo hilo kufanya maji yaloweshe karatasi hiyo. Ilipolainika aliichana vipandevipande na kisha kumgeukia Nuru. “Ni hilo tu lililokufanya upoteze uzuri wa sura yako na kuwa mnyonge kiasi hicho? Alimuuliza kwa mahaba.

“Kwako wewe na hili pia ni mzaha?”

“Sio mzaha. Ni dalili ya uoga. Huoni kama wananiogopa hata wanaanza kunitumia vitisho vya kitoto?”

“Joram!” Nuru alifoka akijitoa katika mikono yake alipojaribu kumkumbatia “Usifanye utani Joram. Kama wameweza kuingia hadi huku na kuacha maandishi kama hayo wangeweza pia





kutega bomu ambalo lingetufanya sasa hivi kuwa marehemu.” “Ndiyo,” Joram alimjibu akitabasmau “Ni hapo ninapowaona

waoga. Kwa nini wasitege bomu badala ya kuleta vitisho vya maneno? Pamoja na kumwuliza Nuru swali hilo lilikuwa likimkereketa. Kwa nini watege maneno badala ya bomu?
 
44.
CONGO ukiuzidisha kwa uongo matokeo yake ni wazimu. Uongo huohuo ukiujumlisha na uongo mwingine matokeo yake ni kitu kilekile cha kutatanisha. Nao ukweli ukiujumlisha na uongo bado jibu utakalopata ni mkorongonyo

wa mambo yasiyo na kichwa wala miguu.

Lakini ukiufanya ukweli uutoe uongo utabakiwa na kitu fulani kinachoeleweka. Ukweli ukiujumlisha na ukweli, utoe uongo, umbeya, unafiki, hila, hisia na mengineyo jibu utakalopata linaeleweka na kukubalika. Daima ndilo linalohitajika.

Hayo yalikuwa yakielea katika ubongo wa Joram Kiango jioni hii, akiwa njiani kuelekea nyumbani kwa Waziri Mkuu. Nuru, alikuwa ubavuni mwake katika kiti cha nyuma ya gari hili walilolikodi.

Hakuona kama ilikuwepo njia nyingine ya kuikamilisha kazi iliyokuwa mikononi mwake bila ya kumwona, kumsikia na kumsikiliza Waziri Mkuu huyo. Kila alichopata kilimfanya azidi kumshuku. Kumsikia tu ndiko ambako kungemfanya ama athibitishe au ayapuuze mawazo yaliyoanza kujengeka kichwani mwake. Ndiyo, Waziri huyo kama binadamu wengine, hasa akiwa kama anavyofikiriwa, asingekosa kuwa na sehemu yake ya uongo pamoja na ile ya ukweli. Baada ya kuipata akiba nyingine ya uongo kama hiyo na ukweli ndipo Joram angekalia meza na kuanza tena mahesabu ya ukweli toa uongo, zidisha





na hisia gawanya kwa hakika na kadhalika. Alikuwa na hakika kabisa kuwa baada ya kazi hiyo kama asingeiona siri iliyofichika basi angeiona njia ambayo ingemwongoza kuifikia.

Safari hii ya kumwendea Waziri Mkuu kiasi ilikuwa kama ya uvamzi. Aliamua kuifanya bila taarifa kwa hofu ya kumfanya ajiandae na kumpokea kiungwana. Joram alipenda kuwapata wasailiwa wake kabla hawajajiandaa. Alichofanya ilikuwa kumnong’oneza Nuru taratibu, “Leo tunamtembelea Shubiri Makinda.”

“Saa ngapi?” “Sasa hivi.”

Dakika mbili baadaye wakawa ndani ya teksi hii ambayo iliendeshwa kwa mwendo wa kistaarabu. Dereva wake, kama walivyo madereva wengi wa teksi, alikuwa mtu mwenye hamu sana ya maongezi, aliongea juu ya kila lililomjia kichwani. Siasa, uchumi, utamaduni, mapenzi, ujambazi na hata yale ambayo hayakumuhusu. Joram na Nuru hawakumtia moyo sana, kwa jinsi ambavyo hawakujiingiza katika maongezi hayo kikamilifu kama alivyotaka. Walichofanya ilikuwa kutia kicheko au neno moja moja ili aendelee. Kimawazo walikuwa mbali sana.

Joram alikuwa akifikiri vipi atakavyomkabili waziri mkuu huyo na kumfanya aseme chochote, licha ya uongo. Si rahisi kumwendea Waziri Mkuu, ambaye fununu zinaonyesha kuwa kwa sababu moja au zaidi anakusudia kumwangamiza Rais wake. Umfikie mbele na kumwuliza maswali ya kijinga. Hiyo isingetofautiana sana na kutia kichwa katika domo la mamba mwenye njaa. Madamu haikuwepo njia nyingine, kazi ya Joram ilikuwa kumfanya azungumze. Hilo ndilo lililomfanya asifanye usiri wowote katika msafara huo kama roho nyingine ilivyomtuma. Alikuwa na uhakika kuwa kuingia kwa Shubiri ingekuwa rahisi kama kwenda kanisani, lakini kutoka… hilo ni jingine lililomsumbua, kubuni mbinu au hila ambayo ingewawezesha kutoka na kuifikia hoteli yake huku wakiwa na roho zao kifuani? Mwilini hakuwa na silaha zozote za haja isipikuwa ile bastola ndogo ambayo maficho yake yasingeweza kufikiwa na wakaguzi wa kawaida. Hiyo tu, silaha nyingine zisingewezekana. Huwezi kwenda kwa Waziri Mkuu na bastola katika mfuko wa koti na ukatarajia kurudi utokako.

Gari liliendelea kutafuna lami, likiiacha mitaa na miji na





kuanza kuvinusa vitongoji vya Borongo, eneo ambalo hukaliwa na wazito wengi. Dereva aliendelea kuzungumza, sasa alikuwa akisimulia jinsi alivyofanya alipomchukua mwanamke mmoja ambaye ana wazimu wa kupenda, “kama alivyodai yeye…” kama huna moyo utaanguka naye nakwambia. Mapaja kayaachia, macho kayalegeza huku mkono wake ukikukuna polepole. Ukimtazama akukonyeza…”

Joram aliinua uso kumtazama alipoikatiza ghafla hadithi yake. Mara alikiona kilichomfanya asite. Hatua chache mbele yake, gari aina ya Dutsan lilikuwa likiwajia kasi kwa mwendo mkali likiwa upande wao kabisa. Lilikuwa tukio la ghafla mno. Haikuwepo nafasi walao ya kufikiria. Alichokifanya Joram ni kufungua mlango ghafla na kumshika Nuru kiunoni huku akiruka nje ya gari. Dakika hiyohiyo mlio wa kutisha ulisikika wakati magari hayo yalipogongana uso kwa uso. Joram aliviringika toka alipofikia na kisha kuinuka ghafla. Aliyatupa macho kwa Nuru na kumwona kama aliyezirahi. Alipoyainua macho kutazama magari yaliyogongana aliambulia kumwona dereva wa gari lililowagonga akiviringika toka alipoanguka na kusaidiwa na dereva mwingine ambaye alisimamisha gari lake ghafla katika eneo hilo kulipanda gari hilo la aina ya Landrover, kabla Joram hajafahamu kinachotendeka aliiona landrover hiyo ambayo ilisimama kwenye gia ikiondoka kwa mwendo wa mshale. Hakujishughulisha kusoma namba ya gari hilo. Akageuka kumtazama Nuru tena. Alimwona akijipindapinda kwa juhudi za kuinuka. Akamwendea na kumsaidia kusimama. Nuru aliinuka kwa shida na kuchechemea hatua mbili tatu kabla hajarudi tena sakafuni.

“Pumzika kidogo,” Joram alimwambia akimtua chini na kutazama kilichokuwa kikimsumbua. Hakuona damu wala dalili yoyote. Pengine ilikuwa hofu tu. Akamwacha hapo na kumwendea dereva wa gari lao. Alikuwa hatazamiki.

Kichwa chake kilikuwa kimekatwa vipande vitatu. Sehemu iliyobaki shingoni ilikuwa ya pua na kinywa ambacho kilikuwa wazi kama kinachocheka kipumbavu na kutema mate ya damu. Kifua chake pia kilikuwa kimefumuliwa na usukani ambao ulivunjika na sehemu yake kupotelea mwilini mwake. Sehemu ambapo palistahili kuwa miguu sasa palijaa damu na mchanganyiko wa kitu kama nyama na mifupa iliyosagwa.





Ilikuwa picha nyingine ya kusikitisha sana. Ilimfanya Joram asikie kichefuchefu. Akafumba macho yake na kugeuka nyuma. Alipomfikia Nuru aliinama na kuutazama mguu wake. Akaona sehemu za magoti zikianza kuvimba.



***

Simu iliita tena. Safari hii iliita kwa muda mrefu, ikatulia kwa dakika mbili na kuanza tena. Joram aliendelea kuipuuza. Aliitazma kwa jicho lililoikinai huku akijaribu kuyalazimisha masikio yake kutosumbuliwa na mlio huo mkali. Iliendelea kuita kinyume cha matarijio yake kuwa mpigaji angechoka. Akainuka na kuiendea, akainua mkono wa simu na kuutia mezani. Kisha, alikirudia kitanda chake na kujilaza tena chali.

Kitanda cha pili kililaliwa na Nuru. Vidonge vya usingizi alivyopewa vilikuwa vikitimiza wajibu kwani kwa muda mrefu sasa alikuwa ametulia kimya katika hali ya utulivu bila ya kujitupa huko na huko kama alivyofanya kabla ya kumeza dawa hizo, kutokana na maumivu makali ya mguu ambao ulikuwa umeteguka gotini.

Hayo yalikuwa matokeo ya ile ajali ya gari nyumba mbili tatu toka nyumbani kwa Waziri Mkuu, ajali ambayo mtu mwenye macho asingeweza kuiita ajali.
 
45.
Hivyo, ilimshangaza Joram alipoona wananchi wengi wakilijia eneo hilo na kulizunguka huku wakitazama kwa macho ya huzuni. Ilimshangaza zaidi polisi wa usalama barabarani walipojitokeza na kuanza kupimapima wakati hata haikuwepo haja. Macho yangetosha kueleza kuwa ilikuwa ajali ya kukusudia. Ajali iliyopangwa. Gari la wagonjwa lilipofika na kumchukua marehemu pamoja na Nuru kwenda hospitalini Joram aliomba kuandamana naye.

“Hapana. Wewe unatakiwa kituo cha polisi,” “Kuna nini?”

“Ushahidi wako unahitajika.” “Nitakuja baadaye.” “Tunakuhitaji sasa hivi.”

Joram aliafiki kwenda nao polisi. Huko aliruhusu kuulizwa maswali yote ya kijinga na aliwapa majibu ya kipumbavu kama walivyotaka. Rohoni alijua fika wangemtafuta dereva wa landrover iliyosababisha ajali hadi kufa na wasingempata. Licha ya namba kuwa za bandia yawezekana pia gari hilo lilikuwa





limeibiwa mahala au kununuliwa maalum kwa shughuli kama hizo. Askari hao walipotosheka na maswali yao na kuchukua jina na anwani yake ya bandia, aliondoka kumfuata Nuru hospitali. Akamkuta tayari amepimwa kwa x-ray na kuonekana ameteguka, ndipo waliondoka kurudi hotelini baada ya matibabu mafupi na kuchukua dawa za kuchua.

“Siku mbili tu kitandani, utakuwa umepona.” Alimweleza Nuru wakati akimsaidia kuvua na kujilaza.

“Siku mbili niwe nimelala tu?” Nuru alilalamika. “Hakuna njia nyingine.”

Na mara tu usingizi ulipomchukua ndipo simu ilipoanza kumsumbua, simu ambayo Joram hakuipenda kuijibu kwani hakuwa na jibu. Alijua ingetoka kwa watu wawili tu, Rais angependa kumwona au yule mtu mwingine ambaye angependa kumtisha. Wote hakuwa tayari kuwajibu. Hakuwa na lolote la kumwambia Rais na asingeweza kumwambia kuwa “Nimeshindwa” hasa baada ya damu nyingi kumwagika kwa ajili yake. Lazima damu hii ilipizwe. Bei ya damu ni damu. Yeyote aliyesababisha kumwagika kwa damu hiyo Joram alimhitaji kwa udi na uvumba kama asingejisamehe kumwacha mtu huyo aendelee kusheherekea hewa safi ya dunia baada ya kumwaga damu nyingi zisizo na hatia.

“… Unakitafuta kifo chako.” Maneno ya mbaya wake yalikuwa wazi masikioni mwake yakikusudiwa kumtisha. Awali yalimchekesha, akijua kuwa ni moja kati ya sura nyingi za woga. Sasa yakimjia akilini, wakati Nuru akiwa chali kitandani, uso wake ukionyesha wazi maumivu yaliyokuwa yakimsumbua japo yumo usingizini ambayo yalimfanya Joram kuhisi kitu fulani kikiibuka tumboni mwake na kujikita moyoni, kitu kichungu, chenye maumivu yasiyoelezeka, kitu ambacho huwezi kukipambanua baina ya hofu na hasira wala asingeweza kukipambanua kwani hakumbuki lini aliwahi kuonja hasira ya hofu na kuijua. Tangu utoto wake hofu kwake ulikuwa msamiati usio na hisia zozote katika nafsi yake.

Ndiyo kifo alikifahamu sana na ni moja kati ya vitu ambavyo hakupenda vimtokee katika umri huu aliokuwa nao. Hakukipenda hasa kwa kutojua kipi humtokea binadamu baada ya roho yake kutengana na moyo. Lakini kuna tofauti kati ya kifo na kifo. Kifo chake yeye binafsi ni jambo ambalo lingemshitua





lakini lisingemtisha. Ni jambo ambalo kila binadamu timamu hana budi kulitarajia kwani hujafa hujazaliwa. Hata hivyo, kifo cha mtu mwingine, asiye na hatia, kwa ajili ya shahuku yake ya kutaka kujua mambo yasiyomhusu ni jambo lililomtesa sana Joram. Kwanza, yule mwandishi wa habari Patauli, kIsha yule msichana, Betty, na leo hii yule kijana mchangamfu, dereva wa teksi. Hayo yalimsumbua sana Joram. Watu wangapi watapoteza maisha yao kabla hajaupata ukweli? Na angeendelea kuketi kizeezee hadi lini akiwatazama watu wanavyouawa kinyama kwa ajili yake? Lini angejibu shambulio?

Akayahamisha macho yake toka kokote yalikokuwa na kuyasafirisha hadi kitanda cha pili, aliuona uso wa Nuru ulivyokuwa, bado dalili zote za maumivu zilikuwa wazi machoni mwake japo alilala kwa utulivu. Akamtazama kwa makini zaidi, utulivu wake ukamtia uchungu mkali moyoni mara alipowaza kile ambacho hakupenda kukiwaza, msichana huyu hivi sasa angekuwa maiti?

Kisha, likamjia wazo jingine zito kuliko la awali. Pengine yule mwuaji hakupenda kuwamaliza? Pengine alichokusudia ni kuwajeruhi tu na kuwatisha kwa kifo cha dereva! Vinginevyo, kwa nini asitumie njia nyingine kuwamaliza wakitapatapa sakafuni baada ya kunusurika?

Maswali hayo yalimwongezea Joram hasira. Aliona dhahiri kuwa adui alikuwa akimchezea kama mtoto mdogo na kumdhihaki kwa vifo vya watu wengine wasio na hatia hali kifo chake kikiendelea kuhairishwa. Ni nani na anachotaka ni nini mtu kama huyu! Na vipi ameondokea kujiamini kiasi hicho? Joram alijiuliza. Au amejiimarisha sana hata anamwona Joram kama chui jike aliyefungwa kamba shingoni, tayari kusulubiwa wakati wowote? Bila shaka machachari yake yote ya kupeleleza kwao yalikuwa mzaha usio na maana yoyote.

Hasira ina nafasi ndogo sana katika kichwa cha Joram. Hutokea kwa nadra sana. Hasira zikimteka akili na kumfanya achukue uamuzi wa pupa. Leo zilimshika. Yeye ni Joram Kiango. Na angeendelea kuwa Joram Kiango kama asingekubali kuwa chui jike au kondoo wa mtu yeyote anayeishi na kamba shingoni. Aliitazama saa yake na kuyasubiri mapambazuko kwa shahuku kubwa. Kesho angekwenda tena kumwona huyo anayejiita Waziri Mkuu. Angemfata ofisini na hakuna mtu





ambaye angemzuia.

Kulipokucha alikuwa mtu wa kwanza kuamka. Kama kawaida yake, alifanya mazoezi ya viungo kwa saa moja, mwili ukiwa umetoka jasho alielekea bafuni ambako alijimwagia maji na kisha kuoga vizuri. Aliporudi chumbani alimkuta Nuru kaamka akijaribu kusimama. “Usifanye hivyo,” Joram alimwonya. “Jipumzishe kitandani tu.”

“Huna budi...”

Haikuwepo haja ya kubishana. Nuru alipojaribu kupiga hatua ya pili tu toka kitandani hapo maumivu makali yalimrudia mguuni. Akaukunja uso wake kwa uchungu na kukirejea kitanda. Macho yake yalitazama mguu wake kwa hasira. “Kitandani siku tatu! Kama maiti,” alinong’ona. Joram alimwendea na kumbusu shavuni. Kisha, alimwacha na kurudi mezani ambako alichukua kitabu cha simu na kuanza kukipekua. Baada ya muda alionekana kuipata namba aliyohitaji. Akainakiri katika daftari lake. Kisha akapiga simu kuagiza chai iletwe chumbani kwao. Chai ilipoletwa alisogeza meza ndogo mbele ya Nuru na kumshawishi kula. Nuru, ambaye alikuwa hajaoga ilibidi apate msaada wa Joram hadi bafuni ambako alijimwagia maji kisha akajikongoja peke yake kurudi chumbani. Alimkuta Joram kaiacha meza ya chakula yuko kwenye simu. Alikuwa akiomba gari la kukodi.

“Unataka kwenda wapi?” Nuru Aliuliza. “Kumwona Waziri Mkuu.”

“Joram!” Nuru alifoka kwa hofu na mshangao. “Bado una hamu ya kumwona. Jana tu tungekuwa maiti kwa ajili ya kutaka kuwona. Nadhani tutafute njia nyingine.”

“Hatuna njia nyingine zaidi ya kumwona. Leo nitamwona. Nitamfuata ofisini ghafla na kutumia mbinu ambayo itaniwezesha kumwona bila kipingamizi chochote,” Joram alimhakikishia.

Alipomwona Nuru akikusudia kuendelea na ubishi alimwacha na kuliendea kabati la nguo. Akatoa suti yake aliyoipenda zaidi. Akachagua viatu maridadi na kuvaa. Akalifungua kasha lake la silaha. Akaitazama bastola yake kubwa 45 kwa tamaa lakini hakuthubutu kuichukua badala yake alirudi kitandani na kupenyeza mkono wake chini ya mto. Ulipotoka ulikuwa umeshikilia ile bastola yake ndogo yenye ukubwa wa kalamu. Akaihifadhi mwilini mwake. Pale ambapo mkono wa binadamu





wa kawaida usingeweza kufika kwa urahisi. Kisha, akachukua ile kalamu yake ambayo haikuwa kalamu ya kawaida bali silaha kali ambayo ingeweza kuua mtu wakati wowote endapo angepata mwanya wa kubonyeza mahala fulani na kuachia hewa ya sumu iliyokuwa imeifadhiwa humo ndani kumfikia binadamu huyo. Aliiweka kalamu hiyo mfukoni. Baada ya kujikamilisha aligeuka kumuaga Nuru. “Nusu saa tu, mpenzi. Baada ya hapo nitarudi hapa mara moja.”

Uso wa Nuru ulikuwa na dalili zote za mashaka. “Joram, nadhani usifanye safari hiyo.”

“Kwa nini?”

“Sijisikii vizuri… naogopa.”

Joram akaangua kicheko. “Huna haja ya kuogopa chochote. Hakuna mtu atakayethubutu kuingia hapa mchana. Na akitokea nadhani hutomruhusu kutoka na roho yake. Bastola yako iko mahala pake. Na sina mashaka kuwa una uwezo wa kuitumia zaidi ya wanawake wote ninaowafahamu. Licha ya bastola kuna bomu la machozi, kuna king’ora cha kumtia hofu, kuna nuru ya kumlewesha, kuna…”
 
46.
“Hujanielewa Joram,” Nuru alimkatiza. “Siyahofii maisha yangu kwa kubaki peke yangu. Nakuhofia wewe… Huko uendako… Nadhani usingeifanya safari hii. Imekuwa ya ghafla mno. Hukuiandaa.”

“Hiyo hasa ndiyo dhamira yangu.” Joram alimjibu akicheka. “Kumwendea bila ya kujiandaa. Niende kama raia yeyote wa kawaida ambaye atatoka ofisini bila ya kumwona Waziri huyo? Kujiandaa nusura kutupotezee maisha jana. Yawezekana tunapojiandaa wenzetu nao wanajiandaa…” alisita kidogo kumtazama Nuru. “Usijali Nuru, muda mfupi baadaye tutakuwa pamoja.

“Joram!”

Joram alimwendea na kumbusu, kisha alitoka nje taratibu. “Joram!”

Hakugeuka kumsikiliza.

Gari lilikuwa likimsubiri nje ya hoteli. Dereva alikuwa mzee mkimya ambaye alikuwa na macho yenye asili kama anayeuonea wivu ujana wa Joram Kiango. Joram alimsalimia na kumpa anuani ya ofisi aliyohitaji. Dereva akalitia moto gari lake. Mara tu gari lilipopamba moto naye alibadilika na kuanza kutokwa





na maongezi kama aliyetiwa funguo. Alizungumza lolote lililomjia akilini akitumia lugha zote za mitaani. Joram alitabasamu na kuendelea kumsikiliza ilhali hamsikii.

Nje ya jengo hilo Joram alimlipa dereva na kuiendea ofisi ya mapokezi. Walikuwa askari ambao maswali yalijaa midomoni mwao kama kanda iliyorekodiwa miaka nenda rudi iliyopita, maswali ya aina ileile, wakitegemea majibu yaleyale. Hivyo, hawakujua wanachokifanya walipojikuta wakijaa hofu ambayo zilimruhusu Joram kuwaendea maofisa wa usalama ambao wangemsikiliza zaidi yao. Askari mmoja alijitokeza kumwongoza katika ofisi yao, walipita hapa na pale na hatimaye, kupanda lifti hadi ghorofa ya nane ambako walifika tena mapokezi. Askari huyo alimwacha Joram hapo.

Maswali mengine yakafuata. Uongo mwengine ukafuata. Hatimaye, fomu nyingine zikajazwa. Zikapelekwa katika nyumba mbalimbali kuchunguzwa. Ziliporejea Joram aliruhusiwa kuendelea na msafara wake. Akajitokeza mtu mwingine kumwongoza. Walipanda tena lifti kushuka chini. Ghorofa ya nne waliteremka. Joram akaelekezwa katika chumba fulani ambacho hakikua na anwani yoyote mlangoni. Aliingia katika chumba hicho kwa mashaka kidogo. Ramani ya ofisi hiyo aliyokuwa nayo kichwani, katu haikuwa na chumba cha aina hiyo, chumba kidogo chenye meza moja tu kubwa iliyozungukwa na viti sita ambavyo havikukaliwa na mtu yeyote. Hewa katika chumba hicho ilikuwa nzito, licha ya mashine ya hewa kufanya kazi kama kawaida. Joram alipiga hatua ya pili kuingia. Ghafla hisia za hatari zikamjia. Akageukua taratibu kumtazama mwenyeji wake. Aliambulia kuona tabasamu la kifedhuli likichanua usoni mwake huku mkono wake ukitoka mfukoni, ukiwa umeshikilia bastola kubwa. Joram alifanya haraka kuupeleka mkono wake kunako silaha yake. Hakuwa mwepesi kiasi hicho kwani mkono huo haukuruhusiwa kutoka kwa jinsi mwenyeji wake alivyoudaka ghafla huku akiisogeza

bastola kifuani mwa Joram.

“Keti,” aliamuru kwa sauti ya utulivu.

Joram hakuwa na la kufanya zaidi ya kumtii. Alikalia kimoja kati ya viti vilivyokuwepo. Akilini alikuwa akijilaani kwa kuruhusu uzembe mkubwa kiasi hicho. “Vipi?” alijitia kuliza. “Sikutegemea mapokezi kama haya katika ofisi kubwa kama hii.





Kama unataka pesa sina chochote.”

Badala ya jibu mwenyeji wake aliangua kicheko ambacho kilikatizwa ghafla pindi mkono wa mtu huyo ulipoinuliwa tena na kubonyeza dude fulani lililokuwa kando ya mlango. Kabla Joram hajajua lipi la kufanya aliambulia kuona chumba kikimezwa na kiza ghafla. Alijitupa kuelekea mlangoni. Haikusaidia. Alikuta tayari mlango umefungwa kwa nje, sauti ya kicheko cha mwenyeji ikipotelea upande wa pili.

‘Nimefanya nini?’ Joram alijiuliza kwa hasira. Upuuzi gani kuacha ajiingize katika mtego ulio wazi kiasi hiki! Uzembe na upofu umemuanza lini? Mikono yake ilitambaa huko na huko ikipapasa hapa na pale. Alipata swichi nyingi ambazo alijaribu kuziwasha. Swichi ya kwanza alipobonyeza tu alihisi chumba kikianza kujawa na joto kali. Akaizima mara moja na kuwasha nyingine; iliyosababisha ubaridi mkali sana. Akaizima na kuendelea kupapasa. Akagusa nyingine. Aliiwasha kwa mashakamashaka. Kiasi hii aliiona imemsaidia. Ilitoa nuru nzito ya bluu ambayo ilimwezesha kuona ingawa kwa tabu kidogo. Akauchunguza mlango. Haikuwepo haja yoyote ya kujaribu kupambana nao. Ulikuwa mlango imara, maalumu kwa shughuli hizo. Akauacha na kurudi mezani. Alijaribu kuvuta droo, lakini zote zilikuwa zimefungwa. Juu ya meza hakukuwa na chochote cha haja; zaidi ya vifaa vya ofisi vya kawaida. Akaiacha meza hiyo na kurudi mlangoni. Alishangaa kuona miguu yake ikiwa mizito mno. Kila hatua aliipiga kwa tabu sana mithili ya mgonjwa wa miaka mingi anayejaribu kukiacha kitanda chake. Sasa hata macho yake aliyaona mazito, yakitokwa na uwezo wa kuona. Tahamaki chumba kilianza kuzunguka machoni mwake.

“Shit,” Joram alifoka kwa hasira akijaribu kujitahidi aufikie mlango. Alikuwa na hakika kuwa hali hiyo ni matokeo ya aina fulani ya sumu ya kulevya au kupumbaza ambayo alikuwa ameichokonoa mwenyewe baada ya kuwasha ile swichi yenye mwanga hafifu. Hivyo, alichohitaji ilikuwa kuifikia swichi hiyo na kuizima. Haikuwa kazi rahisi. Sasa alijiona taabani, kila hatua ikizidi kuwa ngumu kana kwamba mgonjwa huyo anajaribu kuupanda mlima Kilimanjaro. Kizunguzungu kilimzidi. Nayo macho yalikuwa hayataki tena kukaa wazi.

Hatua moja zaidi… Jitahidi tena….





Inua mkono…

Haikusaidia. Miguu ilipoteza uwezo wa kukichukua kiwiliwili chake. Macho yakaishiwa nguvu za kuona. Taratibu alijikuta… akiangukia zulia na kulikumbatia, akili yake ikizama katika usingizi mzito mtamu usio na kifani.



***

Zilimrudia taratibu kama zilivyomtoka. Zilianza fahamu, ambazo zilimfanya ajikumbuke. Zikafuatwa na mwili wake kuupata tena uwezo wake. Aligeuka kutazama huko na huko. Hakushangaa kujikuta katika chumba kingine, bila shaka katika jengo jingine, nje ya mji. Hayo Joram aliyahisi baada ya kusikia utulivu, kinyume cha mjini. Sauti pekee iliyomfikia ilikuwa ya gari moja ambalo lilisikika likipita kwa mbali. Joram alikitazama kwa makini chumba hicho. Kilijengwa kwa kuta nzito za mawe na dari ambalo bila shaka hewa chumbani ilikuwa nzito ingawa mapangaboi ya feni yalikuwa yakifanya kazi.

Chumba kilikuwa na mlango mmoja tu ambao Joram alishangaa kuuona ukiwa wazi. Kisha akageuka kujitazama. Hakufungwa miguu wala mikono. Akainuka mara moja na kugeuka nyuma. Haikuwepo dalili yoyote kuwa analindwa. Akapiga hatua mbili tatu za haraka kuuendea mlango. Mbele ya mlango alisita kidogo. Yawezekana kuwa alikuwa huru kiasi hiki? Alijiuliza. Akaamua kuthubutu. Taratibu akaushika mlango na kuufungua. Ukiwa mlango mzito wa chuma, ulifunguka taratibu. Joram akachungulia nje. Macho yake yakakutana na yale ya pande la mtu ambalo lilikuwa limeketi juu ya kiti nje ya chumba hicho, likivuta sigara kwa utulivu kama linalomsubiri!
 
47.
Lilikuwa pande la mtu hasa. Uso wake, ulifunikwa na ndevu nyingi ambazo zilishuka hadi juu ya kifua chake kipana, ambacho hakikuhifadhika vizuri katika shati lake. Lilikuwa na midomo mipana ambayo ilidhihirisha unyama na ukatili. Mikono yake ambayo ilifunikwa na nywele nyeusi ilikuwa kitu kingine cha kuogofya zaidi. Ilitosha kabisa kuwa nyenzo ambayo ingepoteza maisha ya binadamu kwa kulikaba koo kwa dakika moja tu. Kitu cha kuogofya zaidi katika mtu huyo yalikuwa macho yake. Licha ya kwamba yalitisha sana bado hayakuonekana kama macho ya kawaida. Yalikuwa makavu, baridi, kana kwamba si macho ya binadamu hai bali ambaye ndio kwanza anatoka kaburini katika





nchi ya wafu, macho ya mauti.

Joram alijua kuwa maisha yake yalikuwa mashakani iwapo uhai wake ulikuwa mikononi mwa kiumbe huyu. Kupambana naye isingetofautiana na kuinadi roho yake kwa bei rahisi. Hivyo, hakuiona njia nyingine zaidi ya kujaribu kujenga urafiki na dude hilo, ingawa hakuona vipi lingehitaji urafiki.

“Kaka, samahani,” Joram alisalimu akijaribu kuunda

tabasamu usoni mwake. “Hivi nimefikaje chumbani humu?”

Kitu mfano wa tabasamu kilipenya katika uso huo. Tabasamu kiasi liliufanya uso wake ufanane na uso wa binadamu. Lakini lilidumu usoni hapo kwa sekunde mbili tu, mara likatoweka na kumezwa na ukatili uleule. “Umeamka sio?” sauti yake ilishangaza. Ilikuwa kinyume kabisa na sura yake. Ilikuwa ndogo kama ya msichana.

“Nenda zako,” aliongeza.

Hilo Joram hakulitarajia. Akajifanya hakusikia. Badala yake

akalirudia tena swali lake, “Nimefikaje hapa?”

“Nasema toka, nenda zako,” msichana katika jitu hilo alinong’ona tena.

Kwenda ilibidi Joram ampitie mtu huyo. Macho yake yalionyesha wazi kuwa kuambiwa aondoke ilikuwa dhihaka tu. Jitu lilikuwa likimsubiri kwa shahuku kubwa. Hata hivyo, alijaribu kumpita ili aondoke zake baada ya kuona kuwa jitu hilo halikuwa na dalili yoyote ya kuelekea kuzungumza zaidi. Alipiga hatua moja, ya pili na ya tatu kwa hadhari, ingawa hakuonyesha dalili yoyote. Hatimaye, alimfikia na kumpita kwa hatua moja. Ni hapo kilipofuata kile ambacho alikihofia. Lilikuwa pigo ambalo Joram alilitegemea na alilisubiri ili alikinge au kulikwepa. Lakini hakutegemea kuwa lingekuwa kali na kwamba lingepigwa kwa wepesi kiasi hiki. Alitahamaki teke likimwingia barabara ubavuni na kumfanya apepesuke na kutua sakafuni. Akaviringika na kuinuka hima huku akizipanga, tabasamu la hasira likichanua usoni mwake.

Kitu kingine mfano wa tabasamu kilijitokeza katika uso wa jitu hili, pengine kwa furaha kuona Joram akiwa tayari kupambana. “Unaitwa Joram, sio?” lilikebehi. “Hodari kwa kila kitu. Nilikuwa na hamu kubwa ya kupambana na wewe ana kwa ana. Umetusumbua kwa muda mrefu sana. Kwa nini unakuwa husikii unapoonywa?”





“Kuonywa! Kwa jambo lipi?” Joram alijaribu kuuliza. “Kwa nini unataka kumwona Waziri Mkuu?”

“Kuna ubaya gani ku…”

Joram alikatizwa na pigo jingine kali. Aliliona pigo hilo likija, lakini bado hakuweza kuliepuka. Lilimtia mweleka mwingine na kuinuka harakaharaka, akichupa angani na kuachia teke kali lililokilenga kifua cha jitu hilo. Pigo hilo ambalo jitu hilo halikulitegemea, bado halikumfikia. Alilikwepa kwa wepesi wa ajabu na kujibu kwa teke lake ambalo lilimnasa Joram tumboni. Yalifuata mapamabano makali. Joram alijikakamua na kuutumia ujuzi wake wote wa kareti na judo, akibadili mtindo kwa mtindo. Alipiga kwa nguvu na wepesi kuliko alivyowahi kupigana. Lakini ni vipigo vichache sana ambavyo viliufikia mwili wa jitu hilo. Wakati huohuo Joram alipokea vibao vingi vilivyomlegeza, hata akaanza kutweta huku jasho likimtoka ovyo. Aliongeza jitihada, akipigana kwa nia moja. Bado juhudi zake hazikuzaa matunda. Ilikuwa dhahiri kuwa asingekufua dafu kwa adui yake huyu ambaye alionekana kuufurahia sana mchezo huu, macho yake yakionyesha hamu ya kitu kimoja tu; kuua. Joram alishangaa kwa nini jitu hilo lilikuwa halijafanya hivyo. Pamoja na kumchelewesha sana Joram katika mapambano haya, ilikuwa dhahiri kuwa alikuwa akichelewesha mapambano

hayo makusudi ili auone ujuzi na juhudi za Joram.

Naam, ulifika wakati ambapo jitu hilo lilionekana kukinaishwa na mchezo huo. Likaachia pigo moja ambalo lilimwingia Joram barabara na kumfanya apepesuke na kuanza kuanguka. Lakini jitu hilo halikumruhusu kuifikia ardhi. Lilimrudisha kwa pigo jingine kali zaidi. Ndipo ikafuata mvua ya vipigo, mapigo makali ya harakaharaka; kila pigo likiwa limekusudiwa liingie wapi. Mapigo hayo yalimlegeza kabisa Joram hata akawa hawezi kujitetea wala kukinga. Bado hakuruhusiwa kuanguka, badala yake alisogezwa ukutani ambako aliegemezwa na kuendelea kuadhibiwa.

Maumivu hayakuwa na kifani. Yalimfanya Joram aishiwe hata nguvu za kulalamika na kubaki kimya, kinywa wazi; macho yakiwa yamemtoka pima katika kusubiri vipigo vingine. Mara mbili tatu alielekea kuzirai, lakini fahamu zilikuwa zikimrudia tena; zikifuatwa na maumivu makali. Joram, alitamani afe, ayaepuke mateso hayo. Wala hakufahamu vipi roho yake





iliendelea kuwa sugu kiasi hicho.

Mvua ya mawe iliendelea kumnyeshea. Hatimaye, Joram alielewa kilichokuwa kikimtokea. Adui yake alikuwa hapigi kwa nia ya kuua bali kumchezea tu, na alikuwa akiufurahia sana mchezo wake. Hata upigaji wake ulikuwa wa aina yake. Alijua apige wapi. Na alijua kiwango cha maumivu ambayo Joram aliyapata. Alikuwa akimchezea kwa mapigo hayo, akimlegeza na kumtesa. Joram alipoonyesha dalili za kuzidiwa kupita kiasi lile jitu lililegeza mapigo yake hadi akili zilipomrudia sawasawa, ndipo lilipoanza tena kupiga. Kama mwanamke hodari wa kufanya mapenzi ambaye humchukua mwanaume kimahaba hadi anapokuwa tayari kufika kilele, na kumfanya ahairishe kilele hicho na kuanza upya mara kadhaa hadi wakati unaoruhusiwa kumaliza unakuwa mwisho mtamu ambao huacha kumbukumbu toka fikra za mwanaume huyo. Ndivyo lilivyokuwa jitu hilo. Tofauti ni kwamba yeye alikuwa akiwakilisha burudani hiyo kwa maumivu badala ya starehe. Kipigo kilimlewesha Joram hata akaanza kuyazoea maumivu kiasi cha kutamani kuendelea kupigwa. Hata alipoacha kupigwa alikuwa akitamani kulalamika, amwambie mpigaji huyo aendelee, kama mwanaume anayemwabia yule mwanamke hodari wa mapenzi aendelee.

‘Binadamu gani wa kawaida anayeweza kuwa hodari wa kupigana kwa mapenzi na ukatili kama huyo?’ Joram alijiuliza katikati ya maumivu hayo. ‘Nani? Nani? Ah!’ mara akakumbuka. Ninja! Aliwahi kusoma mahala fulani ninja walivyo wataalamu wa kupigana, upiganaji ulio na utaalamu mkongwe, zaidi, unaojumuisha judo na kareti. Ninjutsu, utaalamu ambao unadaiwa chimbuko lake ni baina ya China na Japan, kwamba pamoja na mazoezi magumu, hila nyingi, mbinu mbalimbali bado unajumuisha uchawi na mazingaombwe pia. Naam, hiyo ndiyo sababu pekee ambayo ilimfanya ashindwe kupambana na mtu huyo kwa kila hali.

‘Ninja katika nchi ya Kiafrika!’ Joram alijiuliza kwa mshangao. ‘anafanya nini…’ na kwa… Mvua ya maumivu iliyokuwa ikiendelea kumnyeshea ilimfanya ashindwe kufikiri vizuri. ‘Oh! Akh! Shida yote hii kwa nini?’ alijiuliza. ‘Akh!’

Kwa nini adhabu kubwa kiasi hiki! Kosa lake ni lipi hasa. Kutaka kumwona Waziri Mkuu! Vipi kumwona Waziri Mkuu iwe kama kuthubutu kumwona Mungu au Shetani? Akh! Oh!
 
48.
NURU alikua amechoka kuitazama saa yake. Masikio yake pia yalichoshwa na subira ya kutegemea simu ile na kumletea ujumbe wowote. Tayari usiku ulikua

umeingia, zaidi ya saa kumi zimepita, Joram, ambaye aliahidi kukaa saa moja, hajatokea! Wala hajaleta ujumbe wowote! Hofu na wasiwasi ambao ulimnasa tangu Joram alipompa kisogo tu, asubuhi, ulikua ukimzidi kila ilipoongezeka dakika moja zaidi pasi ya kutokea kwake.

Na sasa ni usiku!

Hisia zilimwambia kwamba liko jambo. Vinginevyo Joram si mtu wa kuvunja miadi na kumwacha akae roho juu kiasi hicho. ‘lakini ni kitu gani hasa kilichomtokea?’ alijiuliza kwa mashaka, ‘kifo?’ wazo hilo lilimfanya atetemeke ndani ya mwili wake. Nuru hakuwa kipofu, alikua akiona wazi kabisa kuwa shughuli za Joram zilimfanya awe akitembea na kifo chake mkononi kwani alikuwa na maadui wengi kuliko marafiki; wote wakiwa na hatari kuliko hatari yenyewe. Na kati yao wote, adui wa safari hii aliwatangulia kwa madhara. Kwanza, walikuwa hawamfahamu; kisha haikuwa siri kuwa adui huyo alikuwa akiwadhihaki kama mvuvi anayemchezea samaki ambaye tayari amenasa kwenye ndoana yake. Vifo! Ajali! Vifo! Yote hayo machoni mwa Nuru yalikuwa katika jumla ya dhihaka na mateso kabla ya ile adhabu yenyewe,





adhabu ambayo isingekuwa nyingine isipokuwa kifo.

Ndiyo Nuru alimwamini sana Joram. Alimwamini. Alimtegemea, alimheshimu, alimtukuza na zaidi alimpenda kwa ajili ya hekima, ujasiri na vilevile umbile lake. Nuru hakuona kama yuko kijana mwingine wa kiafrika, anayeipenda Afrika na kuthamini utu na haki ambaye angeweza kumzidi Joram. Ni hayo ambayo yalimfanya aitupe kazi yake, aisahau elimu yake, awaasi wazazi wake na hata kutojali uzuri wake ambao wengi wanadai kuwa si wa kawaida ili awe pamoja na kijana huyu ambaye roho yake ameifanya sadaka na mwili wake kafara kwa ajili ya bara la Afrika. Nuru alisherehekea kila dakika ya kuwa naye. Na asingejali kufa naye, huku amemkumbatia. Nuru alimwamini sana. Hofu ya kifo ilikuwa mbali sana na roho yake kila alipokuwa naye. Hata hivyo pamoja na imani yake kwake, safari hii aliona wazi kuwa Joram alikuwa akitapatapa, haoni aendako wala atokako, jambo ambalo lingefanya kifo chake kisiwe tatizo sasa.

Bila hiari aliitupia saa yake jicho jingine. Saa tatu!

Sasa alihisi akitetemeka mwili mzima. Alikisogeza kando chakula alicholetewa na watumishi ili ale. Alijikongoja kuinuka. Mguu uliendelea kumsumbua. Akaamua kuyapuuza maumivu hayo na kwenda hadi bafuni. Ikamshangaza kuona anaanza kurudiwa na uwezo wake. Baada ya shughuli zake za bafuni alirudi chumbani na kuketi kitini akifikiri la kufanya. La kufanya hakuliona. Alikuwa amewaza mengi na kuyawazua yote. Ilimjia kwenda polisi. Hilo alilifukuzia mbali mara moja. Licha ya kwamba Joram asingefurahi kusikia hivyo bado Nuru anaufahamu udhaifu wa kabila la watu hao wanaojiita polisi. Wangeanza uchunguzi baada ya maiti ya Joram kuokotwa barabarani na wasingegundua chochote hadi kiama.

Kumfuata ofisini au nyumbani kwa Waziri Mkuu huyo bado isingekuwa hekima. Kwanza, hajui Joram alitumia hila na njia gani kuingia huko. Zaidi, ingekuwa sawa na kujipeleka mwenyewe kaburini. Asingefurahi adui wajifariji kwa kuua ndege wawili kwa jiwe moja. Subira. Hilo ndilo wazo pekee ambalo aliliona la busara. Subira, hadi kwa wakati unaofaa. Saa kumi tu baadaye. Wakati huo mguu wake utakuwa umepona.

Lakini kusubiri ilikuwa kazi nzito zaidi ya neno lenyewe.





Kusubiri ukiwa chali kitandani ilihali hujui yaliyompata mwenzi na mpenzi wako! Wala hujui lipi linakusubiri! Haikuwa rahisi. Nuru alijikuta hatulii. Alitembeatembea, mara bafuni, mara dirishani; kusikiliza. Na alipotulia kidogo ni wakati alipokuwa akiirudia bastola yake na kuipapasapapasa. Mikono yake haikuchoka pia kuzishika silaha nyingine ili kuhakikisha kuwa ziko timamu kwa matumizi ya dharura.

Saa sita!

Nuru alishangaa. Akaruka toka kitandani na kukimbilia dirishani, bastola mkononi. Hakuona chochote. Akaiendea simu na kuinua mkono wa kusikiliza. Kisha, akakumbuka kuwa hakuwa na mahala popote pa kupiga. Akatulia na kurudi kitandani. Mara akagundua jambo ambalo hakulitegemea. Alikuwa akitembea kwa ukamilifu. Maumivu aliyokuwa akiyasikia yalikuwa ya mbali sana, yasingeweza kumfanya ashindwe kufanya kazi kesho. Akafurahi na kurudi kitandani ambako alijinyoosha, akiisubiri kesho kwa hamu kubwa.

Saa nane! Saa tisa!

Nuru aliduwaa. Kisha, akajisahihisha. Saa tisa! Maana yake bado saa tatu tu kupambazuke, aanze kazi. Hofu ya nini! Akainuka kwenda mlangoni kuhakikisha kuwa ameufunga. Kisha, akavua nguo zake na kujilaza kitandani, mkono wake wa kuume ukiwa umeikumbatia bastola yake. Akazima taa na kujilazimisha kufumba macho.

Hakumbuki kama alipitiwa na usingizi ama la. Alihisi kama anayeona mtu anaingia chumbani humo taratibu. Akafumbua macho na kutazama huku na huko. Hakuona chochote. ‘Upuuzi,’ alinong’ona akiyafumba tena macho yake na kujaribu kuubembeleza usingzi. Mara tu alipotulia hisia zilimrudia tena, kwamba kuna mtu aliyeingia chumbani humo. Alijilazimisha kuzipuuza hisia hizo, lakini hazikuelekea kumtoka. Aliendelea kuhisi kama kuna mtu aliyeingia, anamcheka. Akayafumbua macho yake taratibu na kuitazama nuru nyembamba iliyokuwa ikiingia toka dirishani ambayo haikumwezesha kuona vizuri. Lakini chumba kilikuwa kitupu. Alipotaka kuyafumba tena macho yake alihisi kama aliyeona kitu katika pembe moja ya chumba. Akayakaza macho yake kutazama. Naam, kulikuwa na kitu, kilisimama kimya kama kivuli mfano wa mtu. Kilikuwa





kikitingishika, kikimjia kimya bila kishindo kama mzimu. Nuru akaupeleka mkono wake kuwasha taa ilihali mkono wa pili ukiinuka kulenga bastola. Ndipo lilipotokea jambo la ajabu. Kivuli hicho kilipata uhai ghafla, kikajitupa kitandani na kuunasa mkono wa Nuru ambao ulikuwa na bastola; mkono wa pili ukimziba mdomo ili asiweze kupiga kelele.

Alikuwa binadamu mwenye nguvu za ajabu. Juhudi zote za Nuru kupiga kelele hapa na pale kwa nguvu zake zote zilikuwa kazi bure. Ilikuwa kama anayeupiga mwili wa chuma. Jitu hilo halikuonyesha dalili yoyote ya maumivu. Kinyume chake liliendelea kumnyonga Nuru mkono hadi lilipompokonya bastola na kuitupa kando. Kisha, likaanza kumfunga kamba.

Nuru alipambana kufa na kupona. Alitumia viungo vyake vyote, akirusha mikono na mateke. Alitafuta mwanya azipige sehemu za siri za jitu hilo kwa goti, hakufaulu. Kila pigo lake ambalo lingeweza kuleta madhara lilikingwa kwa uhodari. Nuru akashangaa. Binadamu gani huyo asiyepigwa akapigika? Akajiviringisha shingo kumtazama usoni. Macho yake yalipambana na uso wa kutisha kuliko uso mwingine wowote aliopata kuuona, uso ambao haukutofautiana naye. Yalikuwa macho yake kabisa, macho ya mauti. Yalimtazama Nuru kwa uadui kama yasiyo na uhai wala chembe yoyote ya kuthamini uhai wa mtu mwingine.

Hofu ikamshika Nuru.

“Unataka nini?” alijaribu kufoka. Sauti haikutoka.

Akaacha kupambana na kujilegeza ili kulibabaisha jitu hilo lijisahau, ili aweze kunyoosha mkono wake ufikie chini ya mto lilipokuwa lile bomu lake. Lakini jitu hilo halikuelekea kufanya makosa. Lilimfunga Nuru barabara mikono kwa miguu. Kisha, likaanza kumkunjia katika shuka nyeusi aliyoivuta toka katika kitanda cha pili.

Kidogo hilo lilimfariji Nuru. Pamoja na ukatili wake, pamoja na kutofanya makosa katika mapambano, bado kiumbe huyo ni kiumbe dume. Nuru alijua silaha ambayo inawafaa viumbe hawa. Na alikuwa nayo, silaha ambayo wahenga na wanasayansi wote kamwe wasingeipatia dawa. Ni silaha hiyo ambayo aliitegemea zaidi. Angeitumia. Mwanaume ni mwanaume tu. Huyu asingekuwa tofauti.

Hivyo, hakuwa na hofu sana aliponyanyuliwa na kutupwa
 
49.





beganikwaurahisikamaunyoya,walajituhilolilipoanzakutembea bila kishindo kama kivuli hadi mlangoni ambako liliuchomoa ufunguo wake malaya lililoutumia kuingia, na kuuweka mfukoni. Likaurudisha mlango nyuma yake na kuiendea lifti. Huko chini lilitumia hila ileile kufungua milango hadi nje ya hoteli. Nje ya hoteli kulikuwa na walinzi wawili waliokuwa wanazungumza mbele ya ofisi yao. Nguo nyeusi lililozivaa jitu hilo, na mwendo wake wa utulivu kama mzimu vilimwezesha kupitia hatua chache nyuma yao, kandokando ya ukuta hadi nyuma ya hoteli ambako kulikuwa na gari likiwasubiri. Nuru alitupwa ndani kwa kupitia mlango wa nyuma. Jitu hilo likaingia mlango wa mbele na kulitia gari moto.

‘Ni mwanaume… atafanya makosa…’ Nuru alijifariji.

***

Kama Joram angewahi dakika tano tu angeliona gari lililomchukua Nuru likiondoka. Mwendo wake wa udhaifu na mzunguko wa safari aliyoifanya ni mambo ambayo yalimchelewesha.

Kiasi alijiona kama aliyeko ndotoni au hadithini kuwa hai na huru wakati huo. Kama si ndoto wala mwujiza basi ilikuwa dalili nyingine ya wazi kuwa maadui walimdharau sana hata hawakuiona haja ya kummaliza. Vinginevyo, asingeliacha jengo hilo isipokuwa kwa msaada wa jeneza. Kipigo alichopata toka kwa lile jitu ni kitu ambacho kamwe kisingemtoka akilini katika uhai wake. Roho yake isingeweza kustahimili dakika tatu zaidi ya adhabu ile. Adui yake, kama mpishi hodari ambaye alikuwa akipima chumvi na sukari kwa uhakika, aliacha ghafla kumpiga. Joram aliporomoka na kuanguka sakafuni. Fahamu zikamtoka. Zilipomrudia alijiona yuko palepale alipoangukia, peke yake na maumivu yake. Alitulia kwa muda akisikiliza. Haikumjia sauti yoyote. Taratibu, alijikongoja kuinuka. Akapiga hatua mbili tatu. Kisha, akatulia kusikiliza tena. Bado hakuisikia dalili yoyote ya kiumbe mwingine hai katika jengo hilo. Alikuwa peke yake. Huru! Hakuamini. Akaanza tena kujikongoja kidhaifu hadi alipoufikia mlango wa chumba hicho, akaufungua na kutoka nje taratibu. Alitokea katika chumba kingine ambacho kilikuwa kama ukumbi uliozungukwa na vyumba vingi. Kila mlango ulikuwa na amaelezo yake. Joram aliyasoma maandishi hayo harakaharaka.





Maabara… mkemia mkuu…. Quality Control…

Akajikokota hadi mbele ya mlango wa maabara. Mlango ulikuwa umefungwa. Alipojipapasa mfukoni mshangao wa pili ulimkumba. Funguo zake malaya zilikuwa salama kama ilivyokuwa bastola yake, kalamu yake, ambayo ni tochi na silaha; bomu lake dogo la machozi na vikorokoro vingine. Mshangao wake ulipomtoka nafasi yake ilichukuliwa na hasira. Vipi watu hao wamemdharau kiasi hicho hata wasijisumbue na chochote alichonacho mfukoni! Hasira hizo zikamfanya atabasamu, kiu kubwa ikizidi kuchemka rohoni mwake, kiu ya kuendelea kupambana na watu hao wanaojiamini. Hakuna ambacho Joram anapenda zaidi ya adui wa aina hiyo.

Mawazo hayo yaliupa mwili wake nguvu mpya ambazo hakujua zilikotoka. Akajikuta akitembea kwa uhakika zaidi katika jengo hilo toka chumba hadi chumba, funguo zake zikitimiza wajibu; bastola ikiwa imemtangulia. Baada ya kuingia vyumba vya kutosha alijua hakuna anachotafuta hapo zaidi ya kupoteza muda. Jengo hilo halikuwa na chochote cha haja kwake. Wala halikuwa kambi ya maadui kama alivyofikiria awali. Bali lilikuwa jengo la watu wenye shughuli zao nyingine kabisa, utafiti wa dawa za kienyeji, ingawa maandishi mbalimbali aliyoyasoma katika mafaili yalionyesha kuwa ofisi hiyo ilikuwa imefungwa na wafanyakazi wote kwenda likizo isiyo na malipo baada ya wafadhili wa serikali kushindwa kuihudumia. Bila shaka, maadui hao walilitumia jengo hilo kwa vipindi fulani wanapokuwa na shughuli zao. Hivyo, Joram akatafuta njia ambayo ilimtoa nje ya jumba hilo.

Mbele ya jengo kulikuwa na kichaka kikubwa cha miti, majani na maua mbalimbali; baadhi yakiwa aina ya mitishamba inayotumiwa katika utafiti. Katikati ya kichaka au msitu huo palikuwa na barabara nyembamba yenye kiza inayoelekea barabara kuu. Joram alijishauri sana kabla ya kuamua kuitumia. Ilikuwa nzuri sana, yenye uhakika wa kumfikisha mtu kuzimu haraka kuliko inavyoweza kumfikisha barabarani, hasa kwa jinsi ilivyokuwa na kiza cha kutisha. Adui yake angeweza kuwa popote, na kumwangamiza kwa silaha yoyote. Hakuna pigo baya kama lile ambalo linakupiga bila kutegemea wala kujua litatokea upande upi. Na ni mchezo ambao dude kama lile linalotumia mbinu za kininja linaupenda kuliko michezo mingine, kuua





huku anayeuawa hajui anapigwa na nani.

Hata hivyo, Joram aliamua kuifuata njia hiyo. Alijua kabisa kuwa hiyo haikuwa siku yake ya kufa. Vinginenvyo, angekwishayapoteza maisha yake muda mrefu uliopita.

Kabla ya kuondoka aliyatazama vizuri mazingira ya jengo hilo. Ramani ya nje na ndani ikijichora akilini mwake kikamilifu. Kitu fulani kilimwambia kuwa angerudi tena katika jengo hilo. Hakuwa mtu wa kuchukua kipigo kama kile alichokipokea na kisha akastarehe hotelini. Angekuwa mtu wa aina hiyo asingekuwa Joram Bin Kiango.

Alipiga hatua mbili kuingia kichakani, akasimama kusikiliza. Hakusikia chochote. Halafu akajitazama. Mavazi yake, suti nyeusi aliyoivaa ilimfanya awe sehemu ya kiza hicho. Kitu pekee kilichomtia dosari ni shati jeupe alilolivaa chini ya koti. Akaamua kulifunika vyema kwa koti lake. Kisha, akaanza safari yake kwa utulivu na adhari. Hata alipoifikia barabara tayari alikuwa amepata wazo. Asingekwenda hotelini moja kwa moja. Angemtembelea tena Waziri Mkuu.

Joram alijua fika kwamba kipigo alichokipata hakikukusudia kumwua. Adui alitaka kumtia hofu moyoni mwake ili akome kuendelea na upelelezi wake. Kwa bahati mbaya, hawakujua moyo wa Joram ulivyo. Badala ya kuogopa ndio kwanza walimzidishia ari. Sasa hivi, wakiwa na hakika kuwa yuko mahututi akijuta na kuomboleza ilikuwa nafasi yake nzuri ya kumtembelea Waziri Mkuu.

Barabarani alikaa muda mrefu bila kuona teksi. Saa yake ilikuwa imevunjika kioo katika mapambano, hakuweza kuiamini kama ilikuwa sahihi ilipoonyesha saa saba za usiku. Magari kadhaa ya binafsi yalipita bila kumtupia jicho japo alijaribu kupepea. Teksi mbili tatu pia zilimpita, ingawa moja haikuwa na abiria. Joram akaamua kujivuta taratibu kwa miguu akielekea mjini. Baada ya mwendo wa dakika kumi alifika mahala ambapo aliona gari limesimamishwa kando ya barabara, mlango wa dereva ukiwa wazi. Hatua kadhaa kando ya gari hilo, chini ya mti, Joram aliwaona kwa shida vijana wawili ambao walikumbatiana wima wakifanya wanachokijua. Walikuwa wanaume watupu. Lakini kutokana na mkao hali ilikuwa wazi kuwa mmoja alijifanya mwanaume zaidi ya mwingine, akijaribu kuchukua nafasi ya mwanamke. Hayo Joram aliyathibitisha baada ya kusikia busu





zito likifuatiwa na sauti ya kiume inayojaribu kulia kwa namna ya mahaba.

“Wapumbavu kama hawa wanastahili kurudi makwao kwa miguu,” Joram alisema akiingia katika gari hilo na kufunga mlango taratibu. Kama alivyotegemea swichi ilikuwa imeachwa katika tundu lake. Akaitekenya na kuondoka kwa kasi. Hakujisumbua kuwasikiliza majuha wawili ambao walipiga kelele nyuma yake huku wakimkimbilia. Likiwa gari aina ya Peugeot 505 mpya nalo lilimchukua kwa mwendo aliouhitaji. Dakika kumi baadaye alikuwa mjini. Huko alichukua ramani nyingine ambayo ilimwongoza hadi kwa Waziri Mkuu.

Kama alivyotegemea, walinzi wawili walikuwa wakisinzia katika kibanda cha usalama mbele ya geti la kuingilia katika nyumba hiyo. Lakini waliamka na kuzishika bunduki zao vyema mara tu Joram alipokanyaga breki mbele yao. Waliinuka na kuzielekeza bunduki zao kifuani mwake mara walipomwona akitoka na kuwafuata kwa mwendo wenye uhakika.

“Nani?”

Joram alizidi kuwafuata. “Simama hapohap ulipo.” Alicheka na kuzidi kuwaendea.

“Amri ya mwisho, simama,” askari huyo alifoka akirudi nyuma.

Joram akacheka na kuwatoa wasiwasi. Akasimama na kuwauliza kwa upole, “Vipi? Mapokezi haya hapa hata kwangu?”

“U nani wewe?”

“Tafadhali msijifanye hamnifahamu.”

Askari walishangaa. Yawezekana kuwa wanamsumbua mtu mkubwa sana katika idara ya usalama! Walijiuliza wakiangaliana. “Tunaomba kitambulisho tafadhali,” mwingine aliropoka.

Hiyo ilikuwa nafasi ambayo Joram alikuwa akiisubiri. Alitia mkono mfukoni na kuutoa ukiwa umeshikilia bunda la makaratasi. Aliyachambuachambua taratibu. Akatoa pochi nene ambayo aliifunua na kuchambua kitambulisho chake kimojawapo, ambacho kilikuwa na maelezo mengi yaliyoandikwa kwa herufi ndogondogo sana, makusudi kwa ajili ya kumsumbua msomaji. Akamkabidhi askari aliyekuwa karibu. Askari wa pili alisimama kando akisubiri.

Joram aliutia tena mkono wake mfukoni na kuipata moja kati





ya sigara zake maalumu. Akaitoa na kuiwasha. Aliitia mdomoni na kuvuta moshi, lakini alikuwa mwangalifu sana kuhakikisha haumezi. Alichofanya ni kuupuliza kwa hila usoni mwa askari hao, wakati huohuo akiwa ameziba pumzi. Askari hao wakiwa hawana habari kama wanavuta hewa yenye sumu kali ya kulevya, waliendelea kukikagua kitambulisho cha Joram kwa makini.

“Hiki kina uhusiano gani na Waziri Mkuu?” aliuliza baada ya

kuhangaika na herufi hizo.

Maelezo ya Joram yalikuwa mengi. Ilikuwa hila nyingine ya kuipa muda wa dawa yake ifanye kazi katika miili yao. Wakati huo alikwisha itoa sigara mdomoni mwake na kuacha moshi uendelee kuwaendea askari usoni. Aliyaona macho yao yalivyokuwa yakibadilika harakaharaka kuwa katika hali ya usingizi. Akaendelea kuwasimulia uongo mwingi juu ya udugu wake na Shubiri.

Dakika iliyofuata binadamu hao walikuwa nusu wafu. Walianguka mmoja baada ya mwingine, kila mmoja akianguka taratibu miguuni mwa Joram ambaye alifanya hima kuwabeba hadi katika kibanda chao, akiwafunga kamba mgongo kwa mgongo na kisha kuondoka haraka kuelekea ndani.

Haikuwa kazi ngumu kuingia katika jumba hilo, wala haikuchukua muda kufika chumba ambacho alikihitaji. Ramani ya jengo hilo ilikuwa wazi katika ubongo wake kihisia kama anavyozifahamu nyumba za wakubwa. Mbele ya mlango huo alisita kwa muda kusikiliza. Hakusikia chochote, kinyume na baadhi ya vyumba ambamo alisikia watu wakikoroma au kupumua kwa namna ya usingizi. Hivyo ilimshangaza chumba hiki kuwa kama kilivyokuwa, kimya kiasi hicho. Pengine mzee alikuwa macho akifanya shughuli zake? Alijiuliza. Akainama na kuchungulia katika tundu la ufunguo. Zaidi ya ukimya chumba kilimezwa na kiza kizito. Taratibu, kwa hadhari Joram alizitumia funguo zake malaya kuujaribu mlango. Ni ufunguo wa tatu ambao ulifaulu kufungua. Kabla ya kuingia alisikilza tena. Ukimya ukazidi kumwalika. Kimya kama ukimya wenyewe, aliingia chumbani humo. Alipofika katikati ya chumba aliitumia tochi yake kutazama huko na huko.

Nuru hafifu toka katika tochi hiyo yenye muundo na ukubwa wa

kalamu ilimwezesha kuona wazi kuwa chumba kilikuwa kitupu.





Kitanda hakikuwa na dalili yoyote ya kulaliwa. Makochi yalikuwa yametandikwa kwa utaratibu wa kawaida. Kwa uangalifu na hadhari ileile, Joram akafanya ziara bafuni na chooni. Akafunua hata kabati la nguo lililochimbiwa ukutani, hakuona mtu. ‘Yuko wapi Waziri Mkuu?’ alijiuliza kwa mshangao. Haja yake ilikuwa kumwona ana kwa kwa ana, amsikie na kumsaili.

Joram aliitumia nafasi hiyo ya upweke kupekuapekua, ingawa hakufahamu alihitaji nini hasa. Upekuzi wake haukumpatia chochote cha haja zaidi ya vitabu mbalimbali, hotuba zinazoandaliwa; na maandishi mbalimbali. Yote hayakumsaidia. Hata hivyo, wakati akitoka mguu wake, uligusa karatasi moja ambayo ilidondoka toka katika vitabu hivyo. Akainama na kuiokota. Ilikuwa karatasi ya kawaida ambayo mwandishi aliitumia bila kujua, pengine wakati akiwa na mawazo mengi kwani ilichorwa ovyoovyo na kisha chini ya michoro hiyo yalikuwepo maandishi.

…aondoke madarakani! Ni msaliti na mhaini!

Chini ya maneno hayo kulikuwa na alama ya kuuliza ambayo ilichorwa kwa wino mzito zaidi.

Joram aliyasoma tena maandishi hayo. Bado hakuyaelewa kikamilifu. Akaisokomeza karatasi hiyo mfukoni mwake na kuanza kutoka tena, uangalifu ukiwa umemtawala.

Alipofika kibanda cha askari aliingia na kuwatazama. Mmoja wao alikuwa ameanza kuamka. Joram akamsogelea na kumgusa koo kwa kisu ambacho alikichomoa katika vazi la askari huyohuyo. “Sikia,” alimnong’oneza. “Nitakuchinja usiponiambia aliko Waziri Mkuu.”

“Siwezi kusema… siwezi kumsaliti… ukitaka nichinje,” lilikuwa jibu la askari huyo kwa sauti ya kugugumia.

Joram alimchana kidogo kwa kisu shingoni. Ikamlazimu Joram kucheka kimoyomoyo kwa jinsi askari huyo alivyoshituka na kutoa macho. Alikuwa mwanaume mwingine mwenye moyo wa kike, mwoga kuliko kunguru.

“Nakuchinja.”

“Usinichinje,” alibembeleza. “Sijaona. Wala… yalaa… ngoja niseme.”

Hakuhitaji ushawishi zaidi. Alieleza yote aliyoyafahamu, yote ambayo aliapa kuwa asingeeleza, kwamba huo ulikuwa mwezi
 
50.






wa pili Waziri Mkuu hakiwa halali katika nyumba hiyo, alikuja mchana na kufanya shughuli zake hadi usiku ambapo alitoweka ghafla.

“Analala wapi?”

“Sijui… hakuna anayejua.” MaelezoyakeyalimchanganyaJoramzaidiyayalivyomnufaisha.

Ndipo aliporudi hotelini kwa mwendo wa uchovu na maumivu makali kuliko alivyotegemea. Na ndipo alipofika hotelini na kukuta Nuru akiwa ametoweka. Kichwani mwake mlikuwa na maswali mengi, ‘Kwa nini Waziri Mkuu aihame nyumba yake? Na analala wapi?’ maswali ambayo yalitoweka mara baada ya kuona kuwa Nuru pia alikuwa ametoweka.








ITANDA kilimlaki Joram kwa namna ya mapenzi ambayo huko mbeleni hakupata kuyaonja. Mara tu ubavu wake ulipoligusa godoro hilo laini, huku akiwa na mavazi yake yote; pamoja na viatu; alijikuta akimezwa na lindi zito la usingizi.

Ukweli kwamba Nuru alikuwa mashakani, mikononi mwa watu au mijitu yenye kiu ya damu kama nunda; na ambayo starehe yao kubwa ilikuwa kuua; ukweli kwamba kichwa chake kilikuwa na maswali mengi yaliyohitaji kujibiwa haraka ili kulifumbua fumbo hili ambalo lilimtia Rais wa nchi nzima hatarini; bado haukumpokonya usingizi. Yote yangeweza kusubiri. Usalama wa Nuru haukumtia hofu kuuawa. Alikuwa na hakika kuwa kama yeye ameruhusiwa kuwa hai hadi sasa Nuru pia anasamehewa kwa muda. Kwa sasa hakuna alichokihitaji zaidi ya mapumziko ili aipate tena afya yake ya mwili na akili kwa kiwango chake halisi kumwezesha kumwokoa Nuru na uhuru wa nchi hii. Usingizi ukiwa dawa pekee ya mapumziko, ndipo akalala.

Na alilala…

Usingizi mzito, ambao haukuwa na ndoto zozote, isipokuwa ile aliyoifikiria kama ndoto ambayo ilimfanya adhani kuwa kila mara alikuwa akisikia kengele ya simu. Alipofumbua macho hakuweza kuona chochote kwa jinsi chumba kilivyojaa giza. ‘Vipi?’ Alijiuliza alipowasha taa na kuitazama saa ya ukutani. Alikuwa na hakika kuwa alilala jana, mnamo saa kumi na moja





za alfajiri. Vipi tena saa mbili za usiku? Yawezekana kuwa alilala zaidi ya saa kumi na tano?

Akajizoakitandanihukuakipepesuka.Ndiokwanzaakagundua amedhoofika kiasi gani kwa uchovu, maumivu na pengine njaa ya muda mrefu. Alikuwa mtu mgonjwa. Akakitazama tena kitanda kwa tamaa, na kilimwalika. Hata hivyo, aliishinda hamu hiyo ya kulala tena kwa kujilazimisha kuyavua mavazi yake na kisha kupepesukia bafuni. Maji ya baridi kali, ambayo aliacha yauchezee mwili wake kwa muda wa kutosha, yalimrudishia nusu ya afya yake.

Nusu ya pili ya uhai ilimrudia baada ya kufanya zoezi lake la viungo kwa robo saa.

Sasa alikuwa Joram Kiango tena. Sura yake ilichangamka kama kawaida, ikivutia katika suti yake ya kijivu ambayo aliivaa. Sasa aliiendea simu ili aombe room service wamletee chochote ambacho kingeweza kuila njaa yake. Mara tu alipoifikia simu hiyo ilipata uhai na kuangua kilio. Joram alipuuza. Iliponyamaza aliizungusha namba za huduma hiyo na kuagiza viazi kwa kuku mzima, pamoja na vinywaji mbalimbali.

Mhudumu alileta chakula hicho cha ziada. Matunda ya aina mbalimbali yaliimeza sahani moja pana iliyowekwa kando ya chakula juu ya kimeza kilicholetwa kwa kusukumwa. Pembeni zaidi kulikuwa na kijibahasha ambacho juu kiliandikwa jina lake bandia alilokuwa akilitumia hapo hotelini. Kadhalika, kulikuwa na ujumbe ambao uliandikwa katika karatasi za hapo hotelini.

“Hivi nimepewa hapo mapokezi, mzee,” mfanyakazi huyo alieleza. “Wanasema hawakuweza kuziwakilisha jana kwa kuwa hawakuwa na uhakika kama upo au la, baada ya simu zote kutopokelewa.”

“Vizuri sana,” Joram alimjibu. “Ziache, nitasoma baadaye.”

Mtumishi huyo alipoondoka Joram aliyasogeza kando maandishi hayo. Akijua kuwa asingetegemea habari yoyote njema katika nchi hiyo, hakupenda aipoteze hamu yake ya kula. Hivyo, akakaa mkao wa kula na kuanza kushughulika. Dakika kumi baadaye tayari alikuwa amevichakaza viazi, kumteketeza kuku na kunyanyasa matunda. Akakisindikiza chakula hicho kwa kinywaji. Baada ya hapo ndipo alipozichukua barua hizo na kuanza kuzisoma.

Ujumbe ulikuwa mfupi tu, “Mara tu ufikapo nipigie. Namba





ni ileile.” Joram alijua kuwa unatoka kwa Rais. Hakuwa na la kumwambia, hivyo akaamua kutompigia. Barua ya pili, kifurushi ambacho kililetwa hapo kwa express ya posta kilimchukua muda kufungua kwa jinsi kilivyofungwa kwa gundi lenye uhakika. Ndani mlikuwa na kidole cha mtu. Damu iliyoganda juu ya kidole hicho haikumfanya Joram ashindwe kuona kuwa kilikuwa kidole cha mwanamke.

‘Kidole cha Nuru?’ alijiuliza kwa wasiwasi.

Jibu lilikuwa katika kijikasha hichohicho, katika kijikaratasi ambacho kililetwa hapo kwa express ya posta kilimchukua muda kusoma kwa jinsi mwandiko wake ulivyokuwa mbaya.

… Ni msichana mzuri sana. Hatapendeza iwapo atapoteza vidole vyote. Hivyo, hili liwe onyo la mwisho. Kila siku ambayo utaendelea kuishi katika nchi hii tutamkata kidole kimoja. Na ni msichana ambaye hana hiana. Kabla ya kumkata kidole tunafurahi naye. Kazi anaijua…

Moyo wa Joram ulidunda kwa hasira. Akayasaga meno yake. Hakutegemea kama wangeweza kuwa katili kiasi hicho, hasa kwa mtu asiye na hatia kama Nuru. Asingewaruhusu kumkata kidole kingine. Na kwa kidole hicho walichomkata, kamwe asingejisamehe kwa uzembe huo alioufanya. Wala asingewasamehe washenzi hao.

“Watajuta kuzaliwa,” alinong’ona akiinuka kuanza kuutoka.

Baada ya kupiga hatua mbili kuelekea mlangoni alisita na kujiuliza anakokwenda. Akajikumbusha kuwa alihitaji kuwa na akili zake zote. Kumkata kwao Nuru kidole kimoja kulidhamiriwa kumtisha na kumkoroga akili. Ili alipize kisasi hicho alihitaji kuwa timamu kimwili na kiakili, si kufanya pupa wala papara.

Wazo hilo likamfanya akirudie tena kiti chake na kuketi chini. Kisha, alikichukua tena kidole hicho na kukitazama kwa makini zaidi. Akakirejesha katika kasha hilo na kukificha mahala ambapo watumishi wa hoteli wasingeweza kukiona. Kisha, akainuka na kuanza kutoka, tabasamu likiwa wazi usoni mwake.



***

Kijiji cha Polo kilikuwa pacha kwa vijiji vingi vya nchi masikini duniani. Barabara ya kukifikia isingestahili kuitwa barabara tena kwa jinsi ilivyomezwa na makorongo pamoja na mapori. Na hapo kijijini dalili pekee ya uhai ulikuwa moshi uliokuwa ukitoka





katika vibanda mbalimbali ambavyo wenyewe waliviita nyumba. Vinginevyo, kwa mtu aliyetoka katika mji mkuu, maili chache tu kutoka hapo; alijiona kama anayetoka peponi na kuingia kuzimu; badala ya dunia halisi. Dunia ya wakulima. Uti wa mgongo wa taifa kiuchumi! Giza zito, milio ya bundi na vyura na ukimya wa kutisha ni baadhi tu ya mengi yasiyopendeza yaliyokuwepo.

Ikiwa yakaribia saa nne za usiku, wakati ambapo pirikapirika za starehe zilikuwa zikiendelea mjini hapa, karibu kila mtu tayari alikuwa amejifungia ndani ya nyumba yake; ama anayeiogopa dunia yake, kana kwamba wanauogopa uhai wa usiku kuusubiri mchana ambao daima ulileta nuru ambayo ni neema na matumaini yao pekee, ahadi ya Mungu. Si zile za binadamu ambazo hazikuelekea kutimia. Yako wapi mabomba waliyoahidiwa hata kabla ya uhuru? Uko wapi umeme? I wapi mikopo ya kujenga nyumba bora? Zawadi au ahadi pekee iliyotimizwa ni shule. Lakini hii elimu haitumiwi ili wawaibe vijana wao wenye nguvu na afya toka hapo kijijini na kwenda kuwatumia mijini?

Hayo yalikuwa mawazo ya baadhi ya wanakijiji. Yalikuwa pia mawazo ya Joram Kiango wakati alipokifikisha kijiji hicho na kujikuta kamezwa na kiza hicho cha kutisha.

Sasa alikuwa amefika katikati ya kijiji. Alilizima gari lake na kufikiri namna ya kuanza kuuliza. Aliihitaji nyumba ya mzee Puta.

“Mwalimu Puta?” mtu mmoja ambaye alikuwa anapita hapo kwa bahati alilijibu swali la Joram. “Mbona umefika,” alisema akimwelekeza kwa kidole.

Ilikuwa moja kati ya zile nyumba zinazoitwa “bora” katika nchi kama hizi, nyumba pekee kijijini hapo ambayo ilijengwa kwa saruji na kuezekwa bati, kuta zake zikiwa zinavutia kwa rangi nzuri. Kwa mujibu wa maelezo ya mtu huyo aliyemwelekeza Joram, nyumba hiyo ilijengwa na Waziri Mkuu baada ya kibanda chake kuanza kuutishia uhai mfupi wa mzee huyo. Akiwa mzee mjane, asiye na mtoto, msaada huo kwake ulikuwa kama kapewa uhai mpya.

Kama nyumba nyinginezo, nyumba hii pia ilikuwa kimya, giza likiwa limetawala, wakati Joram alipoifikia na kuugonga mlango. Alipogonga kwa mara ya pili aliisikia sauti dhaifu ikiitikia toka ndani, “Nani?”





“Mgeni” alijibu.

“Mgeni! Unatoka wapi?” “Nifungulie tafadhali.”

Zilipita dakika zaidi ya tano kabla ya taa kuwashwa humo ndani na, hatimaye, mlango kufunguka taratibu.

Puta, umri ulikuwa unamshinda nguvu. Mwalimu huyu ambaye alikuwa mtu mrefu, mwenye mwili mkubwa, sasa alikuwa kama mzigo wa mifupa mitupu ambayo iliunganishwa pamoja na ngozi ambayo pia ilichoka kupindukia. Sauti na uhai kuwa katika umbo hilo dhaifu ilikuwa kama mwujiza. Hayo Joram aliyaona pindi akilitazama umbo la mzee huyo katika vazi lake la usiku; kaptula iliyokunjamana na fulana nyepesi. Alisimama huku akitetemeka, katikati ya mlango kama anayemnyima Joram ruhusa ya kuingia. Badala yake aliuliza tena, “Wewe nani?”

“Mgeni mzee… labda ungenikaribisha ndani ili tuzungumze.

Nimetoka mbali sana…”

“Una shida gani?” Joram alikatizwa. “Ni usiku sana. Siwapendi wageni wa saa hizi. Hawaleti jema lolote.” Sauti yake ilikuwa ikitetemeka kama mwili wake.

“Siwezi kuzungumza hapa nje. Labda niseme tu kwamba ningependa kuzungumza nawe juu ya rafiki yako mpenzi, Waziri Mkuu bwana Shubiri,” Joram alieleza.

Mzee alifanya kama kushituka kiasi, kisha alimkazia macho makali kwa muda. Baada ya muda ambao Joram aliuona mrefu, mzee alisimama kando ya mlango na kutamka neno moja tu, “Ingia.”

Ndani vilevile kulikuwa hakujambo. Taa ya chemli iliyokuwa imewekwa mezani ilimwezesha Joram kuchagua akalie kochi lipi kati ya seti moja unusu iliyokuwemo ukumbini. Aliketi juu ya lile ambalo liliekea mlangoni.

Mzee Puta alimfuata na kusimama mbele yake. “Ulitaka kusema nini juu ya waziri mkuu?’

“Si ungekaa ili tufahamiane vizuri, mwalimu?” Joram alieleza akiachia tabasamu lake bandia kwa nia ya kumtoa wasiwasi mzee. Lakini mzee huyo hakuwa rahisi kiasi hicho. Bado sauti yake ilikuwa na kila dalili ya uadui na kutomwamini Joram.

“Kama ungependa kufahamiana,” alisema. “Ungekuja mchana, si kuvizia saa hizi. Tafadhali, sema unachomtakia Shubiri.”
 
51.


“Namtafuta,” Joram alieleza. “Nahitaji kumwona. Unaweza kunisaidia, mwalimu?”

Mwalimu wa kale alimezwa na kimya kingine. Kisha, akaiendea meza na kuvuta fungameza. Joram alimtegemea kuutoa mkono wake ukiwa na sigara. Lakini kilichotoka humo haikuwa sigara isipokuwa bastola aina ya revolver. Na ilikuwa ikimwelekea Joram kifuani. “Sasa utasema ukweli. Vinginevyo, utatoka huku ukiwa maiti. Sema upesi, wewe ni nani na nani amekutuma?” mzee huyo alinguruma kwa mnong’ono.

Kwanza Joram aliduwaa kwani hilo hakulitegemea. Kisha, akatamani kucheka kwa jinsi alivyomwona mzee huyo akitetemeka mwili mzima kwa kule kuishika tu bastola. Angeweza kuipokonya kwa urahisi wakati wowote bila ya mzee huyo kuwahi walao kuifyatua. Hata hivyo, hakuthubutu kucheka kwa kuchelea kutia mafuta katika mkaa wa moto. Hakupenda kubahatisha, bastola ifyatuke bure na mlio wake kumdhuru mzee wa watu.

Pengine mzee huyo anapenda kuongea na watu katika hali hii, akajikumbusha alivyokuwa akiongea na wanafunzi wake hali fimbo mbili zikimlinda juu ya meza. Hivyo, Joram akaamua kujitia aliyeshtushwa sana na tukio hilo, “Vipi kwani, mzee?”

“Sema wewe nani?’

Joram hakuona ubaya wowote kujieleza. “Naitwa Joram… toka nchi ya Tanzania. Niko hapa kwa ombi la serikali hii kujaribu kupata kiini cha maafa yanayotishia usalama wa nchi hii. Bwana shubiri anahitajika sana…

“Kwa nini unamtafuta usiku?” mzee alikatiza.

Joram alikuwa na jibu tayari. “Namtafuta usiku na mchana.

Nimejar…”

Mzee alimkatisha tena. “Kwa nini kila mtu anamtafuta? Kwa nini mnamwinda kama simba mwenye kichaa wakati yeye ni mtu mkubwa mwenye hadhi na heshima? Inakuwaje hamumfuhati ofisini kwake mchana, wala anapokuwa mikutanoni hadharani bali mnasubiri giza liingie? Hamna shukrani wala fadhila nyie. Mnadhani bila yeye hii ingekuwa nchi? Bila hekima na mapenzi yake kwenu mgekua watu nyie? Mzee akasita kidogo akitweta kwa hasira, jasho jembamba likimtoka usoni. “Naye upole umemzidi,” aliongeza. “Nilimwambia kitambo aiondoe roho hiyo na kuwa mwanaume, hasikii. Sasa anachezewa kama ngedere;





hata na vijitu kama wewe! Nitakuua.”

“Sikia mzee,” Joram alijaribu kusema kwa utulivu kama awali. Lakini mzee alimkatiza kwa ukelele mkali wa hasira uliofuatiwa na machozi mengi. Kwa sauti kali alinguruma, “Nitakuua… naua

mtu…”

“Subiri kidogo mzee, anaweza kufa baadaye. Mimi pia nahitaji kumwona.” Ilisema sauti mpya, yenye uhakika ikitokea katika kimojawapo cha vyumba hivyo. Msemaji alikuwa akiwajia.

Joram na mzee Puta waligeuka kumtazama.

Joram hakuhitaji kuambiwa kuwa alikuwa ana kwa ana na mtu ambaye alihitaji sana kumwona. Hakuoana kabisa na picha zake nyingi katika vitabu na magazeti.

“Ndugu Shubiri,” alisalimu.

“Naama. Hujambo Joram Kiango? Nilikuwa na kiu kubwa ya kuonana nawe,” akamgeukia Puta na kumwambia, “Samahani, mwalimu. Huyu ni Joram Kiango. Anayeweza kufa baadaye…”



***

Hakuna kitu kinachotisha kama kilio cha mzee. Ama kwa kuwa hakupata kumsikia mzee wa umri kama huu akilia kwa sauti ama kwa kuwa hakutegemea mtu ambaye alijitia ushujaa kiasi hicho kulia. Masikioni mwa Joram ulikuwa muziki wa kutisha sana, kama unaoimbwa na mzuka.

Kwa muda alimtazama mzee alivyolia huku akilalamika kwa sauti ambayo iligugumia hata analosema lisisikike. Kisha, ghafla, kama alivyoanza; mzee alinyamaza; mwili wake ukakoma kutetemeka. Akaitazama bastola yake, kisha akamtazama Shubiri.

“Na huyu unamsamehe, mwanangu?” alinong’ona kwa udhaifu. Hakusubiri jibu. “Unamsamehe!” vipi mtoto wewe unakuwa na moyo wa barafu kiasi hicho? Watakuchezea hadi lini? Na wana haki gani ya kukuchezea kiasi hiki?” mzee alisita kidogo. Alipoanza tena kuzungumza sauti yake ilikuwa ya mnong’ono zaidi, kana kwamba aliwasahau Joram na Shubiri na sasa anazungumza peke yake. “Aibu iliyoje. Kila mtu anajua nchi hii ni yako. Kila mtu anakuhitaji. Wala hakuna asiyefahamu kuwa bila wewe nchi hii isingekuwa hapa ilipo. Na hii ndiyo fadhila ya wema wako, kuishi mithili ya popo, huku ukiwindwa kama mhalifu. Nchi hii ni yako mwanangu. Yako… yako… yako,”





alifoka ghafla.

Kisha, alianza tena kulia. Akaitazama tena bastola. Mara akajitupa chini na kuondoka zake kurudi chumbani, huku akipepesuka kwa jinsi macho yake yalivyojaa machozi.

Walipobaki peke yao ndipo Joram alipomkumbuka Waziri Mkuu na kumtazama. Aliona kuwa yeye pia alikuwa ameduwazwa na machozi ya mzee ingawa tabasamu dogo lilienea usoni mwake na kuwa kama lililosahauliwa hapo.

‘Tabasamu katika uso wa Shubiri!’ Joram alishangaa, kitu ambacho hakupata kukiona kamwe katika picha zote zinazotokea magazetini! Vipi wapiga piche wote wasilione tabasamu hili?

“Keti.”

Sauti yake ikamzindua Joram. Akaketi kumwelekea mkuu huyo ambaye tayari alikuwa ameketi, akiipapasa mifuko yake kutafuta sigara. Joram aliwahi kwa kutoa paketi yake na kumchagulia sigara moja. Waziri aliipokea na kuivuta bila ya wasiwasi. Hilo pia lilizidi kutia nyongeza katika mshangao wa Joram Kiango.

Mtu aliyekuwa mbele yake hakuonekana tishio kama alivyostahili kuwa. Hasa alikuwa kama rafiki wa kawaida tu, si Waziri Mkuu wa nchi. Na hasa si yule Shubiri ambaye kila kidole kilikuwa kikimwelekea kutokana na maafa yaliyokuwa yakiikabili nchi, mtu ambaye vifo vingi vilitokea kwa ajili yake, mtu ambaye kumwona tu kumetia roho yake na ya mpenzi wake Nuru katika mashaka makubwa.

Nuru… mara Joram akamkumbuka hasira kali iliumeza moyo wake. Akamkazia Waziri huyo macho yaliyojaa maswali mengi hata asijue aanze na swali lipi na kumaliza na lipi. Ni waziri huyo aliyemrahisishia jukumu hilo kwa swali lake lililoulizwa kwa sauti ya kawaida kabisa. “Bwana Joram Kiango sio? Yule mpelelezi mashuhuri kutoka Tanzania. Ndiye au siye?”

“Nadhani ndiye,” Joram alimjibu.

“Ninayo furaha kubwa kukuona ana kwa ana. Sifa zako ni nyingi sana kijana. Kama waandishi wa habari hawatii chumvi, basi wewe u mtu mwenye roho ya paka.” Akasita kidogo. “Nilikutegemea kuwa jitu la kutisha sana,” aliongeza. “Si mtu wa kawaida, kama ulivyo. Kitu gani kilichokutoa kwenu na hata kuja hangaika katika nchi kama hii?” Aliuliza.

Joram hakujibu mara moja. Sauti ya Shubiri ilikuwa





ikimshangaza. Alikuwa akizungumza bila wasiwasi wowote, wala dalili ya uadui. ‘Mwigizaji mwingine?’ alijiuliza. Hata hivyo Joram alijisikia salama sana kuzungumza naye kuliko alivyopata kujisikia kwa mtu yeyote. Hasira zikazidi kumpanda. Ndivyo walivyo waovu. Huwezi kuwafikiria. Akaamua kutouzunguka mbuyu. Badala yake alieleza kama ilivyokuwa, macho yake yakifanya kazi ya kuuchunguza uso wa Shubiri ili kuona alizipokea vipi habari hizo.

“Niko hapa kwa ombi la serikali yako…” alieleza. Akaendelea kueleza tangu alivyotembelewa na hayati Kongomanga, hayati huyo alivyopoteza maisha yake baada ya kuufikisha tu ujumbe huo; msichana Betty alivyopoteza maisha yake mara tu baada ya kueleza yale aliyoeleza na jinsi maisha yake na Nuru yalivyokuwa mashakani kwa ajili tu ya kujaribu kumwona yeye.

Ilikuwa hadithi ndefu, kisha kama tamu vile masikioni mwa Shubiri aliyekuwa akisikiliza huku tabasamu lake likizidi kuchanua usoni mwake tabasamu ambalo lilipotea na nafasi yake kuchukuliwa na kitu kama mshangao au kutoamini kila Joram alipoeleza juu ya vifo na maafa. Hali hiyo ilibadilika na kuwa kicheko Joram alipogusia suala la mapenzi na kudai kuwa yanaweza kuwa moja ya sababu zinazomfanya yeye Shubiri ashukiwe kuwa kiini cha mauaji hayo.

“Kama mapenzi ama tamaa ya cheo tu hilo si shauri langu. Hata hivyo, kinachonishangaza ni jinsi ulivyo tayari kumwaga damu isiyo na hatia kwa ajili ya kukidhi haja zako, ni dhambi isiyosameheka.”

Maelezo hayo ya Joram yalikikatiza kicheko cha Shubiri. Badala ya kumjibu, aliuliza, “Umesema umekwishamwona Rais?”

“Ndiyo.”

“Naye pia alishangaa?” “Nadhani.”

Baada ya kimya kifupi aliuliza tena, “Na unaonaje? Ni wewe tu uliyekuwa ukinitafuta au kuna watu wengine?”

“Sijui kama wapo.”

“Swali la mwisho tafadhali,” Shubiri alieleza. “Unafikiri vipi. Watu waliokuwa wakikushambulia kila ulipojaribu kuniona nia yao ilikuwa kuua kabisa au kukunyima fursa ya kuniona tu?”

“Nadhani hawakutaka nikuone,” Joram alimjibu. “Wewe





ulitaka?” akaunganisha swali lake. “Nilikuwa na hamu kubwa ya kukuona.”

“Kitu gani kimekufanya hata uihame nyumba yako na

kujificha humu?

“Huwezi kuelewa,” lilikuwa jibu la Shubiri. Kisha, alimezwa na mawazo mengi. Mara akautia mkono wake katika mfuko wa shati na kuutoa ukiwa na karatasi mbili za hundi. Moja aliirejesha mfukoni, ya pili aliiweka mezani na kuandika juu yake. Kisha, alimsogelea Joram na kumpa hundi hiyo.

Joram aliipokea na kuisoma. Iliandikwa jina lake. Paundi za kiingereza elfu kumi. “Za nini?” aliuliza.

“Usumbufu,” Shubiri alimweleza. “Ningekushauri kesho uondoke na ndege ya kwanza kwenda zako kwenu,” aliongeza, “Kucheza na mauti ni jambo jema. Ya Kaisari mwachie Kaisari.” Joram aliitazama tena hundi hiyo. ‘Hakuna pesa zinazonuka,’

aliwaza akiitikia mfukoni.

“Sina budi kukushukuru. Hata hivyo, naomba niulize swali la mwisho kabla sijaondoka.

“Uliza.”

Chochote ambacho kilikusudiwa kuulizwa na Joram hakikuwahi kuulizwa. Mshindo wa kuanguka kitu toka chumbani kwa mzee Puta uliwashitua wote. Wakatazamana. Kisha, Waziri aliinuka na kuelekea chumbani huku, akifuatwa na Joram. Walimkuta mzee akiwa ameanguka chini toka kitandani. Joram aliinama kumgusa kifuani. Uhai ulikuwa umemwacha kitambo. Akamtazama Shubiri kwa macho ambayo hayakuhitaji maelezo zaidi.

“Am… kufa,” Shubiri alitahayari. Machozi yakaanza kumtoka?... sasa nenda zako tafadhali. Nikikuona tena… nitakuua.”

Ilikuwa sauti iliyobeba msiba, huzuni na hasira zake zote. Ilimsikitisha Joram zaidi ya ilivyomtisha. Bila kuaga, taratibu aliinuka na kutoka.
 
52.



ARI lake la kuiba lingeweza kumpeleka popote. Usiku kwake ulikuwa bado mchanga sana na alikuwa na mengi ya kufanya. Sasa angependa kufanya safari ya kumtafuta Nuru na kumtoa katika mikono ya binadamu hao wenye kiu kali ya damu. Lakini alisita kulifanya. Hakuwa na shaka zaidi mateso na majeraha ya hapa na pale Nuru yuko hai na salama. Vinginevyo angekwishapokea furushi la kichwa chake badala ya kidole. Zaidi ya hayo, Joram alikuwa na hakika kuwa maadamu majambazi hayo yalikuwa na Nuru katika himaya yao, yalikuwa na hakika kuwa Joram asingethubutu kwenda kinyume cha maagizo yao. Hivyo, alijiona kuwa alikuwa katika nafasi nzuri ya kwenda atokako na kufanya atakalo katika upelelezi wake. Lakini angekwenda wapi zaidi? Alijiuliza kwa masikitiko. Kama kumwona kwake Waziri kulimwongezea chochote katika uchunguzi wake, basi nyongeza hiyo haikuwa zaidi ya kitu kama kumimina sukari katika bakuli la mboga kwani alichanganyikiwa zaidi. Kwanza, alimwona kwa urahisi zaidi ya alivyotegemea; jambo ambalo, licha ya kushangaza lilimchukiza. Alitegemea kumwona kwa taabu, kama anayeonana na kifo; huku risasi zikimkosakosa. Si kwa ajili ya Waziri Mkuu huyu ambako kulifanya msichana wa watu Betty, auawe kinyama? Si kumwona Waziri huyuhuyu ambako kumeyahatarisha maisha ya dereva asiye hatia. Si





kwa ajili yake huyuhuyu ambako sasa hivi kunamfanya Nuru awe mikononi mwa mauti, tayari kufa wakati wowote? Sio Waziri huyu?...siye?

Na kama ndiye basi imekuwa rahisi kumwona! vipi kuonana naye imekuwa kama kumwona mtu yeyote wa kawaida, si mtu ambaye mauaji ya kutisha yanatokea kwa ajili yake? Na vipi maongezi yake yamekuwa ya kawaida kiasi hicho, sauti yake ikiwa haina dalili yoyote ya hofu wala hatia kwa yote aliyosimuliwa? Zaidi, vipi Waziri huyo aonyeshe kushangaa kwa maelezo ya Joram. Au ni mwigizaji mwingine mzuri?

Kisha, Joram alikumbuka kitu kingine alichokipata katika macho na sauti ya Shubiri. Naam, kulikuwa na kitu zaidi ya mshangao, kitu kama huruma. Shubiri alikuwa kama anayemhurumia Joram zaidi ya anavyojihurumia mwenyewe. Kwa nini? Au angesema mengi iwapo kisingetokea kile kifo cha uzee cha mwalimu Puta?

Maswali yaliongezeka kila dakika, majibu yakiwa ndoto iliyokuwa mbali mno na kichwa chake. Kitu pekee alichokuwa na jibu lake ni kwamba mkasa huo ulimvutia katika kiza kizito zaidi, kinachotisha na kutatanisha.

Laiti ingekuwa hadithi tu, au ndoto, aamke kesho na kujikuta yuko Tanzania, katika chumba chake kilekile chenye kunguni na mbu. Lakini haikuwa ndoto. Alikuwa macho na akishuhudia au kujihusisha na vifo vya kikatili. Watu walikuwa wakiteketea. Nchi ilikuwa mashakani. Nuru alikuwa mikononi mwa mauti. Kisa na mkasa?

Wakati msongamano huo wa mawazo ukikisumbua kichwa chake, Joram alikuwa amekiacha kijiji kitambo na kuingia mjini. Tena, tamaa ilimshika ikimshawishi ageuze gari na kuelekea huko ambako aliamini angeweza kumkuta Nuru, amtoe mikononi mwa wauaji hao kwa gharama yoyote. Lakini roho nyingine ilimshikashika ikimtaka aiharishe safari hiyo na kusubiri wakati unaostahili. Hivyo, akalielekeza gari hotelini kwake. Akaliacha mtaa wa pili na kwenda hotelini kwa miguu.

Mapokezi alipewa karatasi yenye maagizo yaleyale; piga namba ileile mara ufikapo pamoja na kifurushi kingine kidogo. Ndani ya lifti alifungua kifurushi hicho. Mlikuwa na kidole kingine. Hakujishughulisha kukitazama kwa makini. Badala yake aliingia nacho hadi chumbani mwake ambamo alikitupia





mezani na kuwasha taa. Alipoyatupa macho yake kitandani hakuweza kuamini.

Juu ya kitanda hicho alilala mwanamke. Shuka laini alizojifunika hazikufaulu kufanya siri kuwa mwanamke huyo alikuwa kama alivyozaliwa. Mwili wake ulipendeza na kuvutia sana katika shuka hizo.

Hakuwa Nuru. Hilo Joram alikuwa na hakika nalo. Mwanamke huyu ni nani basi na aliingiaje katika chumba hiki ambacho kilikuwa kimefungwa? Na hasa anataka nini? Joram alimtazama kwa muda. Akasogea na kujiketisha juu ya kitanda taratibu. Kwa utulivu huohuo aliivuta shuka toka usoni mwa mgeni huyo na kumtazama. Alikuwa mwanamke wa makamo. Lakini uzuri ulikuwa wazi katika sura hiyo japo macho yalifumbwa. Nywele ndefu laini, nyusi nyingi nyeusi, pua pana iliyonyooka na kinywa kidogo cha kuvutia vilikuwa dalili tosha ya uzuri wa umbile la mwanamke huyo aliyelala kwa utulivu kama yuko kwake.

Joram alikuwa na hakika kuwa mtu huyo yuko macho. Alikuwa na hakika pia kuwa kuna jambo zaidi ya jambo ambalo lilimleta. Hakuonekana kuwa na haraka. Hivyo, Joram aliamua kumpa muda wote anaoutaka kwa kutomwamsha. Badala yake aliinuka taratibu kukiendea kitanda cha pili ili alale.

“Usinikimbie Joram,” sauti ya kike ikanong’ona ghafla.

Joram akageuka kumtazama.

Msemaji alikuwa akitabasamu alipoongeza, “Au naonekana mzee sana kwako?”



***

“Naonekana mzee?” aliuliza tena. Sasa alikuwa amekiacha kitanda chake na kusimama kama alivyozaliwa, akiyaruhusu macho ya Joram kutalii juu ya umbo lake. Alikuwa katika kila hali ya kujiamini, kwamba Joram asingekosa kuridhika na anachokiona. Na alikuwa na kila haki ya kujiamini kwani umri ulikuwa haujadokoa chochote cha haja katika umbo lake. Zaidi ya idadi ya miaka, bado alikuwa msichana. Matiti yake mekundu, laini yanayomeremeta yalikita kifuani kama yanayoshindana na wakati. Kiuno chake chembamba kilichokatika kama kinavyostahili kilikuwa daraja zuri lililounga umbo hilo na mapaja laini ambayo yalimeremeta kwa wekundu. Uzuri huo ulikamilishwa na sura nzuri ya kupendeza, yenye macho ya





kuvutia na kinywa cha kusisimua, kinywa kilichobeba tabasamu ambalo lilipendeza zadi kwa jinsi lilivyokuwa mchanganyiko wa haya, kushawishi na kubembeleza pamoja. Hata sauti yake sasa ilikuwa yenye haiba aliponong’ona, “Kama nimekuudhi…”

Joram hakuyasikia yote. Rohoni alikuwa akitaabika kwa kutiana mieleka na shetani wake ambaye alimtaka ainue mkono na kuugusa mwili huo ambao ulikuwa umejitunuku kwake. Alimtazama mama huyo kwa makini zaidi kwa nia ya kumtia aibu avae, aondoke zake. Lakini haikuwa hivyo. Kinyume chake, Joram alijikuta akizidiwa na tamaa kiasi cha kujikuta akijihurumia zaidi ya alivyokuwa akimhurumia mwanamama huyo. Kisha, Joram alikumbuka jambo. Alikumbuka kuwa alipata kumwona huko mbeleni mama huyo mzuri. Wapi vile? Wapi?

Asingeweza kukumbuka kikamilifu. Akili yake ilikuwa haifanyi kazi kikamilifu. Baadhi ya shurubu zilikuwa zikichezacheza huku nyingine zikikaza kuliko inavyostahili. Hata hakuiamini sauti yake alipouliza, “Kama nimepata kukuona mahala!”

Tabasamu la mama huyo lilipata nguvu zaidi. “Ndiyo,” alijibu akizidi kumsogelea Joram na kuketi kando yake. “Lakini, ya nini?” Aliuliza akiuchukua mkono wa Joram na kuanza kuchezea vidole. “Tuna usiku mrefu sana mbele yetu,” aliongeza taratibu. “Hadi kesho tutakuwa tumefahamiana vya kutosha.” Alikuwa havichezei tena ila kunyonya vidole vya Joram. “Uwe mwanangu mzuri,” sauti yake iliendelea kunong’ona kama kinanda.

Na sasa alikuwa amelishika titi lake na kumnyonyesha Joram. Lilikuwa zito, lililojaa, lenye uhai na joto, titi zuri, la mwanamke mzuri. Joram ni mwanaume shujaa. Lakini ni mwanaume kwanza, shujaa baadaye. Alikuwa na kila chembe ya udhaifu wa kiume. Yawezekana hali hiyo ilisababishwa na kutokuwepo mpenzi wake Nuru? Kwani muda si mrefu alijikuta akishuhudia mavazi yake yakitolewa moja baada ya jingine… alitaabika mikono hiyo laini ilipoanza kuteleza juu ya mwili wake katika kila kichochoro ambacho kilihifadhi faraja iliyoburudisha mwili na kuifariji roho… aliteseka zaidi mikono hiyo ilipoacha kazi hiyo na kinywa kuichukua, kililamba hapa, kunyonya pale na kuonja huku. Kisha…

“Wewe… wewe nani?...” Joram aliuliza kidhaifu. “Baadaye…”





“…Ndiyo… Baadaye.” alijibu akiushuhudia mkono wake mmoja, bila hiari yake, ukiuacha mwili wake na kusafiri hadi katika mwili wa mwanamke huyo, ukitomasa hapa na kupapasa pale. Mkono wa pili ulimtoroka na kusaidia kazi hiyo. Ni hapo lilipotokea jambo ambalo Joram hakulitegemea. Mwanamke huyo aliacha ghafla kufanya alichokuwa akifanya mwilini mwake na kutulia mara tu mguso wa Joram ulipomkolea. Kisha, ghafla mwili huo uliokuwa mtulivu ulianza kutetemeka kwa nguvu, huku akiangua kilio chembamba kwa sauti laini, machozi mengi yakimmiminika.

Kwanza, Joram hakuelewa. Alisita chochote alichokuwa akiutendea mwili wa mwanamke huyo na kumkazia macho ya mshangao. ‘Anakufa?’ alijiuliza. Kisha alielewa. Pamoja na orodha yake ndefu ya wanawake mbalimbali, wenye tabia mbalimbali kitandani huyu alikuwa mwanamke wake wa kwanza ambaye mahaba yangeweza kumwua. Alikuwa na njaa au kiu kubwa ya mahaba, kama mtu ambaye ameokotwa katikati ya jangwa baada ya siku nyingi ya ukosefu wa maji na chakula. Hayo Joram aliyafahamu baada ya kuisikia sauti yake dhaifu ikinong’ona, “Endelea…” mara alipoduwaa.

Aliendelea. Na ilikuwa safari ya kihistoria. Paa lingeweza kufunuka kwa kelele. Kitanda kingeweza kugeuka bahari kwa machozi… lakini aliendelea. Ni baada ya muda mrefu sana, ndipo waliachana lakini bado walikuwa wamekumbatiana.

Joram aliuiba mkono wake mmoja na kuutumia kuvuta kijimeza chenye sigara zake. Akauiba mkono wa pili na kujiwashia sigara moja. Alivuta huku akifikiri. Fikara zake zilikuwa nyingi, za kutatanisha na zilimhusu mwanamke huyo aliyelala ubavuni mwake. Hakuhitaji tena kumwuliza kuwa ni nani. Saa chache walizosumbuana kitandani zilifanya agundue kuwa huyo ni mke wa Abdul Shangwe, Rais wa nchi. Kitandani na mke wa Rais wa nchi! Hilo lilimtisha Joram, lakini halikumsumbua sana. Alijua kuwa mwanamke huyo alikuwa na yake, angeyajua kitambo si kirefu. Ambalo lilimsumbua Joram ni jinsi mwanamke huyo, pindi wakifanya mapenzi alivyosahau kuwa yuko na Joram Kiango, badala yake bila ya kujifahamu alilia “…Shubiri ….Shubiri…” sauti hii haikuwa ya hila. Ilitamkwa kimapenzi kabisa, toka katikati ya fungate la moyo wa mwanamke anayempenda. Ni hilo lililomtatanisha Joram. Alikuwa na kila hakika kuwa Shubiri





anayetajwa si mwingine zaidi ya Shubiri Makinda, Waziri Mkuu. Kwamba kuna mapenzi mazito kiasi hiki, baina ya mwanamke huyu na Shubiri, hilo Joram hakulitegemea. Pamoja na upelelezi wake mgumu, pamoja na vifo vya watu wengi, pamoja na marehemu mmoja kufa baada tu ya kutoa siri ya mapenzi haya bado Joram alikuwa na mashakamashaka juu ya ukweli wa suala hilo, mashaka ambayo yalianza kukamilika usiku huu baada ya kuonana na Shubiri ana kwa ana na kumwona alivyoyapuuza maswali yake yote. Ni hapo Joram alipoanza kushuku kuwa kuna jambo jingine zaidi ya mapenzi na tamaa ya vyeo katika mkasa huu. Lakini sasa mashaka hayo yalielekea kusambaratika tena na kumwacha palepale alipokuwa, katika lindi la bahari ya kutatanisha, yenye kiza na mashaka kwani mapenzi yalikuwa wazi katika macho na sauti ya mwanamke huyu. Mapenzi halisi. Au anaigiza? Aweza kuwa mwigizaji mzuri kiasi hicho? Naye Joram amekuwa kipofu na kiziwi kiasi gani hata ashindwe kuona nuru ya mapenzi halisi katika macho na tetemo la huba katika sauti ya mwanamke huyu? La. Lazima liko

jambo zaidi ya jambo.

Akanyoosha mkono na kupapasa titi lililoshiba, ambalo lilikuwa wazi likimtazama kama linalomdhihaki. Mtoto wa kike aliamka. Akafumbua macho na kuachia miayo mirefu. Kisha, alimtazama Joram. Tabasamu likaumeza ghafla moyo wake, tabasamu refu, pana, ambalo lilisema yote ambayo mwili wake ulipenda kusema. Yote, ingawa yalijumuishwa katika neno moja tu “Ahsante.” Naam, kuridhika kulikuwa wazi katika macho yake, kutosheka kukiwa dhahiri katika sauti yake alipoongeza kwa mnong’ono, “Sikujua, kumbe nimekuwa nikiusumbua bure mwili wangu katika kitanda cha mwanaume ambaye hajui thamani ya mwili wa mwanamke. Nusu ya maisha yangu imepotea bure kabisa. Damu ya ujana wangu imekauka bila thamani. Kama ningejua!”

Joram alimtazama. Macho yake maangavu, japo hayakudhihirisha hasira wala furaha, yalimfanya mama huyu akose raha na kunong’ona kitu kama “Samahani” ingawa Joram hakumsikia vizuri.

“Ulifikiri unafanya nini kujipenyeza chumbani humu kwa siri na kunisubiri uchi kitandani?” aliuliza. Mwanamke huyo alipochelewa kujibu Joram aliongeza, “Na unadhani ni heshima





kwa mke wa Rais wa nchi kubwa kama hii kujiuza kwa bei rahisi kiasi hicho?” mama huyo alipofunua mdomo wake kujibu Joram alimkatiza tena. “Usijisumbue kunidanganya. Naifahamu tabia ya wanawake wa aina yako. Umalaya na uongo ni mchezo wenu wa kawaida.”

Haja yake ilikuwa kumtia hasira na aibu. Kumpokonya ushujaa ambao alikuwa nao kwani Joram alikuwa na kila hakika kuwa tamaa ya mwili lisingekuwa jambo pekee lililomleta chumbani humo. Alikuwa mjumbe. Mjumbe wa nani? Ni hilo alilotaka kulifahamu. Ni hilo lililomfanya amruhusu mwanamke huyo kumchezea kimwili, ili apate siri. Hawakusema kuwa kitanda hakina siri?

“Nadhani huna haki ya kuniita malaya mapema kiasi hicho,” mwanamke alisema. “Kuwa mke wa Rais hakunifanyi kuwa mwanamke, mwenye kila udhaifu wa kike.” Alisita kwa muda. Halafu akaendelea, “Ningeomba uelewe kuwa niko hapa kwa ajili ya kuiokoa roho yako. Sikuwa na njia nyingine zaidi ya kujifanya mwanamke malaya na kumhonga mhudumu mmoja ili aniruhusu kukusubiri chumbani humu.”

“Mume wako…”

“Hana habari. Yuko nje ya nchi. Hukusoma gazeti la jana? Ameenda Ethiopia kuudhuria mkutano wa viongozi wa nchi huru. Nadhani atarudi leo.”

“Walinzi wako…”

“Kwao, sasa hivi niko nyumbani, chumbani kwangu; nikimsubiri mume wangu. Hakuna anayejua kuwa nilitumia mlango wa siri hadi nje ambako nilikodi gari iliyonileta hapa.”

“Na ni kipi kilichokuleta?” “Kuyaokoa maisha yako…” “Ongea kwa tuo, tafadhali.”

Mwanamke alimtazama Joram kwa utulivu. Kisha akatabasamu. “Kijana mzuri,” alisema. “Kwanza umejuaje kuwa mimi ni mke wa Rais?” aliuliza.

“Kwa jinsi unavyotapatapa kitandani kama samaki anayekaangwa hai,” Joram aliamua kumtusi tena. “Hakuna ambaye angeshindwa kufahamu.”

Kwa mshangao wake Joram hilo pia halikumkera mwanamke huyo. Ndio kwanza alicheka na na kusema, “Hujui. Usiku wa leo umekuwa wa aina yake katika maisha yangu. Sikutegemea…”
 
53.


“Nielewe kuwa ulikuja kufaidi, au kuyaokoa maisha yangu?” “Kuyaokoa.”

“Kwa vipi?”

Ndipo ilipokuja ile hadithi ndefu, ya kale, ambayo Joram aliisubiri kwa hamu. Mwanamke alieleza taratibu bila haraka, tangu alipozaliwa akiwa pacha, yeye na ndugu yake Lulu; yeye akiitwa Tunu… “Tulipendana kama tulivyofanana. Tulikuwa radhi kuichangia punje ya mhindi kuliko kumwacha mmoja ale, mwingine akose.”

“Watu walisema kuwa tulikuwa wasichana wazuri. Walitutazama kwa tamaa na mshangao, jambo ambalo lilitufanya tuwe na kiburi sana, tukimringia kila mwanaume aliyemtaka yeyote kati yetu. Tuliringa sana, na tungeendelea kuringa kama asingetokea Abdul na Shubiri. Vijana hao, wazuri wa sura na tabia; wakiwa wanapendana kama tulivyopendana siye; tulijikuta tumefanya nao urafiki; urafiki uliozaa uchumba. Kama ndugu yangu Lulu asingekufa, tungefunga ndoa siku moja, saa moja…” “Kitu gani kilichosababisha kifo cha Lulu?” Joram alitaka

kujua.

“Mapenzi.” “Mapenzi?”

Tunu alisita kujibu na kumkazia macho Joram. “Unaweza kutunza siri?” aliuliza. “Jibu la swali lako ni siri ambayo nimeishi nayo miaka nenda rudi. Sijapata kumwambia mtu yeyote. Kila mtu anaamini kuwa alikufa kwa ajili ya kuchukuliwa na mto. Ni mimi tu ninayefahamu kuwa haikuwa ajali. Alijiua. Maiti yake ilitafunwa siku nyingi bila kuonekana. Ikaaminika kuwa ameliwa na mamba au viboko waliokuwa chini ya mto huo.”

Sauti yake ilimshangaza Joram. Kama kweli walipendana kiasi hicho vipi anazungumza kujiua kama anayesema “Kulala” I wapi dalili yoyote ya majonzi inavyowastahili wapendanao? Kwa sauti aliuliza, “Alijiua… kwa ajili ya mapenzi! Nifafanulie tafadhali.”

“Nisirinyinginenzitoambayonakuibia,”alieleza.“Nimekwambia kuwa tulimpenda Abdul na Shubiri? Sio kweli sana. Ukweli ni kwamba tulimpenda mmoja wao. Wote tulimpenda sana Shubiri. Lakini ilikuwa siri yetu. Tuliificha vilivyo. Tusingeweza kuwavunja mioyo kwani wao walikuwa zaidi ya chanda na pete. Hivyo, tukalazimika kuendelea kukubali uamuzi wao wa kutugawa kama mifugo Shubiri akiwa amenichagua mimi na





Abdul akimtaka ndugu yangu Lulu.

“Nadhani waliyapenda majina yetu tu kwani, kama nilivyosema awali, kwa sura tulikuwa sarafu kwa ya pili. Hivyo, tulikuwa tukiwachezea tulivyopenda. Leo mie nilijifanya Lulu, Lulu akawa Tunu, tukaandamana nao na kufanya yote waliyotaka kufanya. Hawakuiona tofauti yoyote, hata kitandani. Tungeweza kuendelea na mchezo wetu huo milele kama kisingetokea kipingamizi cha ndoa. Ingetulazimu kutengana. Tunu angelazimika kuwa Tunu na Lulu, Lulu. Ni hapo ulipozuka msiba wa mapenzi. Nani akawe Tunu wa Shubiri? Wote tulimpenda. Tukaamua kumkataa Abdul na kuolewa uke wenza kwa Shubiri lakini tulipomwambia hilo kwa siri, alitucheka na kutuomba tuache upuuzi. Tarehe ya harusi ilipokaribia ndipo Lulu alipoamua kujiua.”

Alisita kidogo, Joram alipokosa swali aliongeza, “Mimi nikiwa mchumba halisi wa Shubiri nilijikuta nikiwa na furaha kwa kifo cha ndugu yangu. Hata hivyo, furaha hiyo iliyeyuka nilipotakiwa na wazazi wangu kuolewa na Abdul badala ya Shubiri. Kisa? Atakuwa Rais wa nchi. Nilipomtaka Shubiri ushauri nilikuta nae kapambazika kama wazazi wangu “Siwezi kumyang’anya Rais mke,” alisema. Nilipomweleza kuwa mimi ni Tunu si Lulu hakunisikia. Baada ya kulia sana ndipo nilipoyaona machozi katika macho yake. Nikajua kuwa alinipenda sana. Ati ni hilo tu lililonifanya nikubali kuolewa na Abdul baada ya Shubiri kunisihi sana. Hata hivyo, ingawa miaka nenda rudi imepita, lakini bado nampenda Shubiri zaidi. Naye ananipenda. Iko siku haki itatawala ki-mapenzi baina yake na miye. Abdul amenikinaisha kabisa. Laiti angeupasua moyo wangu na kuuona ukweli huo, angeninyonga au kujinyonga mwenyewe.”

Alikuwa akisema kweli tupu. Hilo Joram hakuwa na shaka nalo. Mwanamke huyu asingekuwa hodari wa kutunga hadithi na bado awe fundi wa kuigiza kwa kiwango hicho. “Kwa nini humpendi Abdul? Ana kosa lipi?” alimwuliza.

“Ni mzembe sana kitandani. Anavyosifiwa hovyo na watu na kupendwa amefikia hatua ya kujipenda sana. Hata mwili wa mwanamke ukiwa uchi kando yake haupendi kama anavyojipenda. Inachukiza zaidi anapotaraji kusifiwa hata kwa uzembe huo, kisha asifiwe na mkewe.”

Joram alimwelewa. Baada ya kumtazama, tena kwa makini zaidi, aliuliza swali jingine, “Nadhani hukuja hapa kuniibia siri





hizo. Ulitaka kunionya. Sio?”

“Nimekuja kukuomba urudi kwenu. Maisha yako yapo hatarini sana, panda ndege ya kwanza leo hiihii.

Joram akacheka. “Usijisumbue kunitisha kwa maneno. Kwa taarifa yako nimekwishatishiwa kwa silaha na damu. Sitishiki kwa urahisi.”

“Sikusudii kukutisha. Nimekuja kukuomba.”

Joram akacheka tena, kicheko kingine cha kebehi. “Na unaweza kuniambia mapenzi yako kwangu yalianza lini, hata uhatarishe ndoa na hadhi yako kwa ajili ya kunionya?” alisukuma swali jingine. Alipoona Tunu akibabaika kulijibu aliongeza, “Pengine hilo si swali la maana kwa sasa. La muhimu, ambalo lingenifanya niamue kuondoka hapa ni iwapo utaniambia ukweli, ni nani aliyekutuma kwangu?”

“Nadhani, kulingana na sifa nilizozisikia juu yako umekwishamfahamu.”

“Sijamfahamu.”

“Ni mpenzi wa moyo wangu. Kila mtu anampenda kama ninavyompenda miye. Siku mbili tatu zijazo atachukua uongozi wa nchi hii. Siku chache baadaye tutakuwa mume na mke…”

Alikuwa akiongea kama anayeota, kana kwamba anaiomba miungu hilo litokee, si kama mtu anayewakilisha ujumbe muhimu ambao ametumwa kuuwakilisha. “Ni yeye aliyekutuma kuufikisha ujumbe huo kwangu?” Joram alimwuliza.

“Ndiyo,” alijibiwa. “Usiwe na shaka. Nenda zako uwanja wa ndege na utamkuta mkeo akikusubiri.”

“Ni yeye aliyekuambia hilo pia?” Tunu alikubali kwa kichwa.

Jibu lake lilimshangaza Joram. “Amekuambia lini maneno hayo?”

“Jana.”

“Saa ngapi?” “Usiku wa jana.”

Joram hakuhitaji kuongeza swali jingine ili kuthibitisha kuwa mwanamke huyo sasa alikuwa akisema uongo. Alikuwa na hakika kuwa Shubiri asingekuwa mwepesi kiasi hicho, katika usiku mmoja aonane na mke wa Rais wake kwa siri; usiku huohuo asafiri hadi kijijini ambako alijificha kwa sababu isiyoeleweka. Kilichomshangaza Joram ni kwa nini mwanamke





huyo alikuwa akimdanganya ilihali muda mfupi uliopita alikuwa akisema ukweli mtupu.

Huku akitabasamu Joram alisema, “Mama, hivi nimewahi kukuambia kuwa u-mwaname mzuri sana kwa sura?”

Pamoja na kushangazwa kwa badiliko hilo la ghafla, la mkondo wa maswali ya Joram, bado alionyesha kuburudishwa sana na maelezo hayo. Kama mwanamke yeyote mwingine yeye pia alipenda sana kusifiwa uzuri.

“U-malaya mzuri sana, wa sura na umbile,” Joram aliendela. “Hata hivyo, sina budi kukuambia kuwa roho yako ni mbaya kuliko shetani.” Akasita na kuacha tusi hilo lizame katika akili ya Tunu. “Ndiyo, shetani ni afadhali kuliko wewe…”

“Tafadhali,” Tunu alibadilika. “Sidhani kama una haki wala hadhi ya kunitukana kiasi hicho. Kujitupa kitandani mwako kusikufanye usahau kuwa mimi ni mke wa mkuu wa nchi hii. Tamko langu moja linatosha kukutupa gerezani kwa maisha yako yote yaliyosalia.”

“Linatosha pia kunitupa kaburini kama ulivyokusudia.” Tunu alionekana kama ambaye hakumwelewa Joram. “Wengi umekwishawapeleka kuzimu kabla ya wakati wao.

Mimi umeamua kunichelesha kidogo na kujisingizia mapenzi. Kama inavyomstahili kabisa shetani mzuri wa kike.”

“Sikuelewi…”

“Huwezi kuelewa.” Sasa alikuwa kama anafoka. “Utanielewa vipi wakati kuua mtu asiye na hatia kwako ni mchezo mdogo tu? Utaelewa vipi wakati kumtesa mwanamke mwenzio ni jambo dogo sana kwako?”

“Bado sijakuelewa.”

“Huwezi kuelewa,” Joram alisema tena akiinuka na kuiendea meza. Alimrudia Tunu huku akiwa ameshikilia lile kasha aliloletewa. Akalifungua na kutoa kidole, ambacho sasa kilianza kuelekea kuvunda. Akakisogeza mbele ya macho ya Tunu na kumwonyesha huku akisema, “Labda utafurahi zaidi kukiona hiki?”

“Nini hicho?” “Kidole.”

“Cha?” “Binadamu.”


Tunu alionekana kubadilika. Kitu kama kichefuchefu

kilionyesha dalili katika uso wake kiasi cha kumfanya ashindwe kutamka lolote ingawa alimtazama Joram kwa macho yenye maswali elfu moja.

“Ni kidole cha mpenzi wangu,” Joram alimpa moja ya majibu ya maswali hayo ambayo hayakutamkwa. “Hana hatia. Mmemteka nyara na kumtesa kiasi hiki bila kosa lolote, nia yenu ikiwa kunitisha niondoke nchini. Kwa taarifa yako, ukitaka kamwambie pia aliyekutuma, kwamba siondoki katika nchi hii bila kulipwa vidole vya mpenzi wangu na damu za watu wengi wasio na hatia. Ningependa pia mjue kuwa bei ya damu ni damu na deni la damu hulipwa kwa damu.”

Ilikuwa dhahiri kwa Joram Kiango kuwa Tunu hakuelewa chochote ambacho alieleza. Macho yake yalionyesha mshangao na kushitushwa sana na maelezo hayo lakini hakuna alichokielewa. Akaomba aelezwe kitu kizima, kwa tuo. Ndipo Joram akamsimulia, tangu alivyoitwa toka Tanzania; mjumbe huyo alivyoyapoteza maisha yake; Betty alivyochinjwa kama kuku; dereva teksi alivyouawa na wao kuponea chupuchupu; mateso aliyoyapata; mwalimu Puta alivyofariki kwa hasira na akamaliza kwa kumkumbusha juu ya vidole vya Nuru ambavyo vilikatwa bila huruma. “Nadhani umeelewa kwa nini unastahili kuitwa mwovu kuliko shetani. Kuwa kwako katika njama chafu kama hizi kunakufanya uwe mwanamke wa mwisho kwa roho nzuri ambaye anaishi duniani. Kwa kweli, nilistahili kukuua, mara tu nilipokutia machoni,” Joram alimaliza.

Macho yalimtoka pima Tunu. Alionekana kama ambaye hakushangazwa tu bali kutishwa sana na hadithi hiyo, kana kwamba hakuitegemea wala kuamini. Mara chozi lilimtoka na kuteleza juu ya shavu lake. Likafuatiwa na la pili. Joram aliamua kuitumia nafasi hiyo. “Kuyafanya maisha ya binadamu kama mifugo ni dhambi sana. Mtu yeyote ambaye anayafanya, pamoja na kujificha kwake katika fumbo lisiloelezeka, bado nitamtia mikononi na kuhakikisha anayalipia madhambi yake yote hapahapa duniani. Wewe uko katikati ya mgogoro huu, mpenzi u-kama ufunguo ambao unaweza kurahisisha kazi yangu. Unaonaje kama utaniambia kinachotokea?”

Tunu alijaribu kutabasamu, tabasamu ambalo lilimgomea na kufanya sura yake iwe katikati ya kicheko na kilio. Alijaribu kusema, neno likakataa kutamkika. Akausogeza mkono wake





na kuvuta saa yake ya dhahabu ambayo ilikuwa juu ya kijimeza. Alitahayari kuona kuwa ilikuwa yakaribia saa kumi na mbili za asubuhi. Mara moja akaamka na kuanza kuvaa nguo zake, suruali ya degrizi na tisheti nyepesi ya kijani ambayo iliyafanya matiti yake yasimame na kuvutia sana. Alizishughulikia nywele zake harakaharaka; kisha, akavaa miwani yake myeusi na kukifunika kichwa chake kwa kofia kubwa ya jua. Akasimama mbele ya kioo kujitazama. Aliyekuwa akionekana katika kioo hicho hakuwa mwingine wa mjini ambaye vijana wangemwita changudoa. Hakuna mtu ambaye angediriki kumshuku. Alimgeukia Joram na kumnongoneza kwa sauti ambayo ilimtoka kwa dhiki “Bado nakushauri urudi kwenu.”

“Siwezi…”

Tunu alisita na kufikiri kwa makini. Kisha, aliitazama tena saa yake. “Mungu wangu, muda umekwenda,” aliropoka. Akamgeukia Joram na kusema, “Unajua kuwa unacheza na kifo?”

“Siogopi kufa!”

“Ningependa kukusaidia,” aliendelea. “Ni hadithi ndefu sana. Muda haunitoshi. Unaweza kufika mtaa wa Lolongo, nyumba namba arobaini leo saa nne? Nitakuibia siri ambazo zitaitingisha nchi hii.”

Joram alikubali.

“Na iwapo utabadili mawazo na kwenda zako kwenu bado nitashukuru sana,” aliongeza. “Kwani kila dakika unayoishi katika nchi hii inakusogeza karibu zaidi na mauti yako.”

“Nitafika…” Joram alisisitiza. “Saa nne sio?”

***

Kwa Joram kiango, kuisubiri saa nne haikuwa kazi ndogo. Zaidi ya saa tano zilihitaji kuuawa kabla ya kuifikia saa nne. Saa tano ukiwa chali juu ya kitanda, katika nchi hiyo ambayo ilinuka maafa, ilikuwa sawa na kukisubiri kifo miaka mitano juu ya kitanda hichohicho.

Hata hivyo, hakuwa na jingine la kufanya. Kufunga virago vyake kwenda uwanja wa ndege kama alivyoshauriwa, ingekuwa aibu ambayo hakuwa tayari kuifanya. Angekuwa radhi kufa na kuzikwa ugenini zaidi ya kukimbia baada ya kufanywa juha kiasi hicho kwa sababu ambayo hakuifahamu, hasa baada ya maisha





ya watu wengi kuteketea kwa ajili yake. Na hasa kwa kuwa hakuwa na uwezo wa kuishinda kiu yake kubwa ya kulifumbua fumbo hili la kutatanisha.

Kwamba Nuru alikuwa huru, akimsubiri uwanja wa ndege hilo lilimsisimua Joram lakini halikumvutia. Pamoja na ukweli kwamba alifurahi Nuru kuwa hai, bado asingeruhusu kuwa chambo ambacho kingemshawishi kuondoka katika nchi hiyo kabla hajalipwa maovu yote aliyotendewa. Nuru si mgeni Tanzania. Acha atangulie. Watakutana baadaye, kama si Dar es salaam hata mbele ya milango ya kuingilia ahera.

Saa moja kasoro Joram alikiacha kitanda na kuingia bafuni. Toka huko alivaa na kwenda chumba cha maakul ambako alijiamsha kwa staftahi kamili, kisha akapitia magazeti mawili ya kila siku. Habari zilizoongoza gazeti hilo zilikuwa suala ambalo lilimfanya Joram alivamie gazeti hilo mara moja na kurudi nalo chumbani ambako aliketi na kulisoma kwa makini.

WAZIRI MKUU KUJIUZULU?

…Katika barua hiyo ambayo ndugu Shubiri amemwandikia Rais amedai kuwa hana sababu maalumu ya kujiuzulu kwake isipokuwa kujipumzisha tu. Akiwa mtu ambaye ni mmoja kati ya nguzo za nchi hii, aliyepigania uhuru tangu utoto wake na ambaye alifikiriwa kuongoza iwapo Rais atapumzika, uamuzi wake wa ghafla umemshangaza kila mtu. Gazeti hili limewasiliana na mawaziri wengi na kuwataka mawaidha yao. Kila mmoja ameonyesha kushangazwa na uamuzi huo. Rais alipohojiwa hakuwa na la kusema isipokuwa kwamba ameshangazwa na uamuzi huo na kuongeza kuwa leo saa nne za mchana kamati kuu ya nchi itakutana katika ukumbi wa Makao Makuu kulijadili suala hilo…

Joram aliisoma tena habari hiyo. Hakuelewa. Ulikuwa mwanzo au mwisho wa mchezo huu wa kutatanisha? Alijiuliza. Hakupata muda wa kujijibu. Mlango wake ulikuwa ukigongwa kwa nguvu. Kabla hajaitikia ulifunguka.

Waliingia askari wawili wenye vyeo vya Captain, bastola zao zikining’inia viunoni. Walimkagua kwa macho na kisha mmojawao, ambaye Joram aliona kuwa alifanana sana na samaki, alimwuliza kwa ukali, “Wewe ni Joram Kiango?”

“Kama ndiye?”

“Tumeamriwa kukuondoa nchini mara moja. Na ni kwa
 
Back
Top Bottom