Mohamed Said
JF-Expert Member
- Nov 2, 2008
- 21,967
- 32,074
Mchango wa kujenga club ya Sunderland Msimbazi Street katika miaka ya 1970
Majuzi hapa kulikuwa na Simba Day.
Nimekaa leo asubuhi na kuwaza vipi Simba ilikotokea.
Sijui kama Simba walifanya kisomo, yaani khitma ya kuwarehemu
viongozi, wachezaji na wapenzi wa club toka enzi za Sunderland.
Ikiwa walifanya kisomo naamini kabisa katika majina ambayo
yaliyotajwa moja litakuwa la Ayubu Kiguru.
Aliitwa Ayubu Kiguru kwa kuwa mguu wake mmoja ulikuwa na
athari.
Hii ilikuwa miaka ya 1960.
Mimi bado mtoto na nikipenda Sunderland na nikimjua Ayubu kwa
karibu sana na sababu ni kuwa Ayubu alikuwa na ubao wa biashara
Soko la Kariakoo na mjomba wangu Bwana Khamis Salum na yeye
alikuwa na ubao wake si mbali na ubao wa Ayubu Kiguru.
Ayubu alikuwa na sura jamil na alikuwa mweupe wa rangi.
Mungu alimjaalia Ayubu kipaji cha kuongea na kubishana.
Soko la Kariakoo enzi hizo lilikuwa moja ya vituo vya ushabiki wa mpira
Dar es Salaam.
Yanga na Sunderland walitawala soko na Yanga washabiki wao wengi
walikuwa na biashara ya kuuza samaki kiasi ikawa watani wao wakiwaita
Yanga, ''Wauza Samaki.''
Siku ya mechi ya Sunderland na Yanga moto ulikuwa unawaka sokoni pale
toka mapema asubuhi.
Ushabiki huo utaendelea kwa juma zima takriban baada ya mechi.
Sasa ikitokea kuwa Yanga imefungwa na Sunderland washabiki wa Yanga
walikuwa tabuni kwa juma zima pale sokoni wakipigwa makombora na
Ayubu Kiguru.
Ayubu alikuwa na uwezo wa yeye peke yake kuwanyamazisha Yanga wote
pale sokoni kwa maneno yake, kejeli na kebehi lakini katika namna ambayo
mtu hawezi kughadhibika bali ni kucheka tu.
Enzi zile za Ilala Stadium kelele za kuzomea zikizidi kutoka uoande wa Yanga
Ayubu atasimama kuwaelekea Yanga na atatoa maneno watu watacheka.
Yanga maneno yakiwaingia kisawasawa na sasa wamepwelewa hawana la
kusema basi watamwambia, ''Wewe Ayubu nani atakuweza bwana kiwete
wewe nyie mlojaaliwa na Allah ni mdomo tu.''
Ayubu alikuwa pia ni bingwa wa matusi.
Jibu litakalotoka litamaliza ubishi wote watu watatawanyika watamuacha
Ayubu anapanga nyanya zake huku amevaa jezi ya Hamisi Kilomoni.
Ilikuwa Sunderland ikishinda Ayubu anachukua kikombe anakujanacho
sokoni anakiweka mbele ya ubao wake watu wanapita wanatunza.
Ayubu alikuwa akitukana lakini si kutokana na hamaki wala hasad ya nafsi.
Ilikuwa ndiyo kusherehesha ushabiki wa Yanga na Sunderlaand wala mtu
haendi Msimbazi Polisi kushitaki kuwa katukanwa na Ayubu Kiguru.
Ilikuwa ''ambition,'' yangu siku moja nivae jezi ya Sunderland lakini kipaji kilikuwa
kidogo nikaishia mchangani.
Rafiki yangu marehemu Jumanne Masimenti (Cosmopolitan FC, Simba na
National Team) siku moja tushakuwa wakubwa kanambia, ''Wee ungecheza
mpira gani bwana uko mazoezini sisi tunapiga danadana, wewe uko pembeni
ushavaa jezi unasoma kitabu. Mchezaji mpira gani anakwenda mazoezini na
vitabu?''
Matokeo ndiyo haya leo niko JF hapa nadarsisha historia.