Kwa kawaida kinga ya mwili huulinda mwili dhidi ya vitu mbalimbali vyenye kuleta athari kwa afya kama vile vimelea vya magonjwa kama vile bakteria na virusi, lakini wakati mwingine pia na vitu ambavyo havina madhara yoyote kwa mwili, ambavyo huitwa allergens (mzio).
Aleji au mzio (allergy) ni matokeo ya kinga ya mwili inapofanya kazi ya ziada ya kupambana na kitu chochote ambacho kwa ujumla huwa hakina madhara kwa mwili pale inapotokea kimeingia ndani ya mwili au kimegusa sehemu fulani ya mwili.
Kinga ya mwili inapoamua kufanya kazi ya ziada husababisha mtu kuwa na dalili za aleji au mzio katika mwili wake kwa kuona dalili mbalimbali
Vitu vinavyosababisha mzio
Baadhi ya vitu vinavyosababisha mzio ni pamoja na vumbi, baadhi ya dawa zenye madini ya sulfer, vyakula, kung’atwa na wadudu kama vile nyuki na baadhi ya uyoga.
Wapo pia watu ambao wanapatwa na mafua karibu kila siku na wengine kushindwa kuvaa aina fulani ya nguo na vitu kama saa,hereni na cheni, kwani mara nyingi husababisha kuwashwa na kuvimba mara wavivaapo.
Watu wenye mzio huwa na hisia zisizo za kawaida za mwili dhidi ya vitu vinavyowaathiri na pindi mwili unapokumbana na vitu vinavyosababisha mzio, mfumo wa kinga wa mwili huzalisha kemikali mbalimbali, mfano histamine ambazo hupambana na mzio.
Mara nyingine watu hupata ugonjwa wa mzio pindi wanapokutana na aina fulani ya mazingira kama yenye vumbi, baridi ya wengine hupatwa na mzio wanapopigwa na jua kali au msuguano wa ngozi unaweza kuwasababishia dalili fulani za mzio.
Dalili zake
Mara nyingi dalili hutegemeana na mgonjwa ana aina gani ya mzio.
Kama mtu atakuwa na mzio katika mfumo wa hewa, huweza kupata matatizo ya kupumua anapokutana na mazingira yenye vumbi, hali inayomsababishia kupiga chafya mara kadhaa, kutokwa na makamasi, kuziba pua, muwasho kwenye pua na koo au kupumua kwa kutoa sauti kama filimbi, kuumwa na kichwa mara kwa mara, kizunguzungu, pumu, kuhisi joto katika mwili na mfadhaiko.
Endapo macho yataguswa, mhusika huhisi hali ya macho kuchoma, kutiririkwa na machozi na muwasho kwenye macho na pindi anapojikuna, macho huvimba na kuwa mekundu.
Iwapo mtu atakula kitu ambacho ana aleji au atakunywa dawa zenye sulfer na zina mzuru kila azitumiapo, anaweza kuwa na dalili kama ya kuharisha, kichefuchefu, kutapika, kusokotwa au kuumwa na tumbo na hata hali mbaya ya kutishia maisha.
Vitu vinavyosababisha aleji vinapogusa ngozi ya binadamu, vinaweza kusababisha ngozi kuwa na mabaka, kubabuka, kuvimba, muwasho, kutoa vipele, malengelenge, michubuko na ngozi kuwa nyekundu.
Zipo aleji zinazohusisha mwili mzima zinaweza kuwa na mkusanyiko wa dalili zote alizozitaja na wakati mwingine mtu anaweza kuwa na aina fulani ya nguo, hivyo vyema kuziepuka ili kupunguza tatizo hili.
Maambukizi
Kwa kawaida ugonjwa wa mzio huwa ni wa kuzaliwa nao na hauambukizi ikiwa mtu katika familia ana ugonjwa huo, hawezi kumuambukiza mtu mwingine.
Jinsi ya kufanya vipimo
Mara nyingi mgonjwa wa mzio hupimwa kwa kutumia damu kwa sababu katika damu inaweza kutoa majibu ya mgonjwa juu ya mzio alionao na hii ni baada ya mgonjwa kuelezea vitu gani vinavyomsababishia matatizo mara avitumiapo.
Na hii ni kwa sababu kuna baadhi ya mambo yanayoweza kumsababishia mtu dalili zinazofanana na za mtu aliye na aleji ya kitu fulani
Kwa mfano, matumizi ya aina fulani ya dawa yanaweza kumsababishia mtu mikwaruzo au michubuko katika ngozi inayofanana na aleji nyingine, au mtu anaweza kuwa na mafua au kikohozi kwa sababu ya maambukizi ya bakteria au virusi na si kwa sababu ya aleji.
Anasema mara nyingine wanapopima damu huangalia ongezeko la immunoglobin E ambayo huashiria uwapo wa vitu vinavyosababisha aleji na kipimo cha damu chenye kuonesha ongezeko la eosinophil iwapo kuna aleji, ambayo ni sehemu ya chembe nyeupe za damu.
Matibabu
Shambulio kali la aleji linaweza kusababisha mhusika kulazwa hospitali na lisipodhibitiwa, kifo kinaweza kutokea kutokana na kupata shida katika upumuaji wake, lakini hii hutokea mara chache kwa wagonjwa wenye mzio katika chakula na mfumo wa hewa.
Anasema tiba kubwa ni kupunguza uwezekano wa kupata
aleji kwa kutambua na kuepuka kitu au vitu vinavyokusababishia hali hiyo.
Kama ni chakula au dawa au kemikali, mgonjwa anatakiwa kuepuka kabisa matumizi yake, na kama ni vumbi ajitahidi kukaa nalo mbali
zipo pia aina mbalimbali za dawa zinazotumika kutibu na kuzuia aleji, kulingana na jinsi daktari atakavyoona inafaa kwa kuzingatia ukali wa tatizo, dalili zake azipatazo mgonjwa, umri wa mgonjwa pamoja na hali yake ya kiafya kwa ujumla.
Anasema pia wagonjwa hawa hupewa dawa maalum kwa ajili ya kutuliza mcharuko mwilini ambazo huwa katika miundo mbalimbali zikiwamo za kupaka, matone, kuvuta, sindano au vidonge.
Kwa wale wenye mafua na kuziba kwa pua, hushauriwa kutumia dawa zinazosaidia kufungua pua, hata hivyo, dawa hizi hazina budi kutumiwa kwa uangalifu hasa kwa watu wenye magonjwa ya shinikizo la damu au moyo.
Anasema wagonjwa hawa hupewa dawa pia kwa ajili ya kuzuia vitu vinavyosababisha aleji.
Aina nyingi za aleji hutibika kwa urahisi kwa kutumia dawa. Wapo baadhi ya watu hususan watoto wanaoweza kujenga hali ya aleji dhidi ya aina fulani za vyakula, hali wanayoweza kuendelea nayo hadi ukubwani na kwa kawaida, kitu kikimletea mtu aleji utotoni, huendelea kumuathiri daima
Madhara yatokanayo na mzio
Madhara ya mzio ni pamoja na kupata shambulio kali ambalo linaweza kusababisha kifo kama matibabu hayatafanywa haraka.
Kuna baadhi ya watu ambao wakila baadhi ya vyakula huvimba mwili na kushindwa kupumua mpaka kuhitaji kulazwa hospitali na kusaidiwa kupumua kwa mashine.
Madhara mengine ni pamoja na shida ya kuvuta pumzi au kushuka kwa shinikizo la damu (kupata shock).
Namna ya kujikinga na aleji
Kuna baadhi ya wagonjwa hupata madhara makubwa ya kuungua nje na ndani pindi wanapotumia dawa ambazo zina sulfer na huwasababishia mzio ambao usipotibiwa kwa haraka, kifo kinaweza kutokea.
“Steven Johanson’s syndrome ni mzio hatari na wa kipeke kuliko aina zote na mgonjwa anapopata aina hii ya mzio na ngozi yake huungua nje na ndani na endapo akichelewa kupewa matibabu huweza kupoteza maisha
Jinsi mzio unavyonyima uhuru wa kufanya kazi
Evelyn Menas mkazi wa Mtoni Kijichi, anasema yeye mara nyingi hupata tatizo la mzio akikaa au kupita eneo lenye vumbi au kutokwa na jasho mwilini, mambo yanayomnyima uhuru wa kufanya kazi katika baadhi ya mazingira.
“Nikitokwa jasho mwili huwasha, najikuna, kukosa uhuru na mara nyingine ninapokuwa sehemu yenye hewa iliyo na asili ya vumbi, napiga chafya mfululizo, kuwashwa uso na macho yanavimba na huwa nashindwa kupumua vizuri kwa sababu pua zinaziba,” anasema Evelyn.
Anasema anajitahidi kuhakikisha chumba anacholala kinakuwa safi muda wote, lakini hali inakuwa ngumu akiwa katika vyombo vya usafiri kama daladala iliyojaza abiria kupita kiasi, kupita sehemu yenye harufu mbaya, au kutimuliwa vumbi barabarani.
Ushauri
Ni vizuri watu wakazingatia na kufanya utafiti ili kuweza kugundua ni kitu gani kinawasababishia mzio au kufika katika kituo cha afya kinachotoa huduma ya vipimo waweze kufanyiwa vipimo na kupata ushauri wa kitaalamu.
Na endapo mtu atatumia dawa zenye madini ya sulfer zikamletea madhara, anatakiwa awahi kumuona daktari ili kuepusha madhara yanayoweza kujitokeza.
Mzio au aleji ni matokeo ya mpambano uliopitiliza kati ya kinga ya mwili na kitu chochote ambacho kwa ujumla huwa hakina madhara kwa mwili, inapotokea kimeingia ndani ya mwili au kugusa sehemu fulani ya mwili.
Katika mjumuisho wa haya yote hali inaelezeka kuwa mzio ni hali inayotokea wakati seli za mwili wa binadamu zinapokataa kitu ambacho kwa mtu wa kawaida hakina madhara. Mzio hujitokeza kwa alama au dalili mbalimbali na huleta matokeo yenye ishara nyingi mwilini.
Kuna aina mbili kuu za mizio zinazosababishwa na kitu ambacho kiko nje ya mwili na husababishwa na mazingira ya nje ya mwili. Aina nyingine kuu ya mzio ni ile ambayo iko ndani ya mwili wako ambayo inaweza kuletwa na kinasaba cha kurithi au na kitu kilichoko ndani ya mwili.
Mzio wa ngozi au aleji inayojitokeza kwenye ngozi ni tatizo linaloweza kukupata kutokana na mwili kutopenda kitu Fulani kutokana na sababu kadhaa ikiwemo hewa na hata chakula tunachokula.
Kuna vitu ambavyo huibua mzio kama vumbi katika nyumba, mavi ya panya, manyoya ya wanyama na hewa yenye aina ya spiriti. Mzio unaweza kukufanya uwe na ukurutu, mafua, pumu na hata kuvimba kwa mwili ambapo pia wapo watu ambao hupata tatizo la ngozi, kuwashwa na hata kuvimba.
Katika dunia ambayo inatamba na teknolojia, tatizo la mzio ni kubwa na hasa kutokana na kemikali zinazotumika katika vyakula na hata urembo vinapotibua kemikali zinazotengeneza aleji katika mwili.
Wakati kitu chochote kinaweza kuwa alejeni lakini kuna vitu vingine ambavyo husababisha mzio zaidi kupita kiwango cha kawaidacha hali ya hewa.
Alejeni zinaweza kuwa vumbi na mazingira yaliyochafuliwa kwa unga wa mimea na maua, vipodozi na marashi ya kujipaka au ya kupuliza, vyakula mbalimbali kama mayai, karanga, kemikali zinazotumika kuhifadhia vyakula na vinywaji ambazo mtu huzila kwenye chakula au kuzinywa kwenye vinywaji hivyo.
Mzio unaweza kusababishwa na mabaki au uchafu wa kemikali kutoka viwandani, moshi wa magari machakavu, mwanga wa jua, nyuzi za nguo zinazotengenezwa viwandani, baadhi ya dawa, manyoya, sufi ya ngozi za wanyama, wadudu mbalimbali kama mchwa na mende, manyoya ya paka na mbwa na hata harufu inayotokana na rangi mbalimbali.
Mzio unaosababishwa na dawa
Katika hali ya ufahamu zaidi unatakiwa kufahamu kuwa hali ya Mzio unaosababishwa na dawa au drug allergy ni hali isiyo ya kawaida inayooneshwa na mfumo wa kulinda mwili kutokana na dawa.
Aleji ya dawa si sawa na athari ya dawa, inayoweza kujitokeza baada ya kula dawa ya aina fulani, ambayo kwa kawaida huambatanishwa na maelezo ya dawa. Mzio unaosababishwa na dawa pia ni tofauti na sumu ya dawa ambayo hutokea pale dawa inapotumiwa kwa kiasi kikubwa ambapo dawa hizo zimetajwa kuwa ni aina za antibiotiki.
Uwezekano wa aleji kujitokeza ni mkubwa zaidi pale dawa inapotumiwa mara nyingi, inapopakwa juu ya ngozi au kudungwa mwilini kwa sindano, kuliko wakati inaponywewa kupitia mdomo kwa maana na maneno mengine tunaweza kusema kuwa, mzio wa dawa humaanisha kuwa mwili umekataa dawa fulani au haupatani nayo.
Dalili za aleji inayosababishwa na dawa kwa kawaida hutokea katika kipindi cha saa moja baada ya kutumiwa kwa dawa. Mara chache aleji huweza kutokea baada ya masaa, siku au wiki kadhaa.
Miongoni mwa dalili za mzio wa dawa ni vipele vya ngozi, muwasho, kuvimba, macho kutoa machozi na ngozi kubadilika rangi. Dalili nyinginezo za aleji ya dawa ni homa, kuvimba, kubanwa na pumzi, mafua na kupumua kwa kutoa sauti kama mtu anayepiga filimbi hali inayojulikama kitaalamu kama wheezing.
Mara chache mzio wa dawa huweza kusababisha madhara makubwa kwa mtu ambapo mwili huonesha dalili ya jumla inayohatarisha maisha ijulikanayo kama Anaphylaxis ambayo hukwamisha utendaji wa mfumo wa mwili.
Viashiria vya hali hiyo ni kubwanwa njia ya hewa na koo, suala linalopelekea kushindwa kupumua. Kichefuchefu au maumivu ya tumbo yasiyo ya kawaida, kuharisha au kutapika, kizunguzungu au kuhisi kichwa chepesi, mwili kudhoofika na mapigo ya moyo kwenda mbio. Pia mwenye hali hiyo presha yake hushuka, huwa na dalili za kifafa na kupoteza fahamu.
Vilevile kuna matatizo ambayo yanaweza kujitokeza baada ya siku au wiki kadhaa baada ya kutumia dawa, ambayo yanaweza kubakia kwa muda mrefu hata baada ya kuacha kutumia dawa. Matatizo hayo yametajwa kuwa ni ugonjwa wa Serum ambao husabisha homa, maumivu ya viungo, vipele, kuvimba na kichefuchefu pamoja na ukosefu wa damu ambapo chembe nyekundu za damu hupungua na pia kuvimba figo na kutokewa na vipele vinavyoambatana na matatizo katika seli nyeupe za damu.
Muhimu kujua ni kwamba utatumia dawa na kwa bahati mbaya zikakuletea aleji unapaswa kumuona daktari mara moja au kwenda hospitali haraka ili kupata matibabu na kuondoa aleji na iwapo utapata dalili zinazoashiria Anaphylaxis kama tulivyoeleza kabla unapaswa kuomba haraka msaada wa kitiba ili kuokoa maisha.
Cha zaidi unapaswa kuacha kutumia dawa iliyokusababishia dalili kali za mzio pindi tu unapobaini tatizo hilo baada ya kubaini tatizo hilo.