LGE2024 Mdau, yapi maoni yako ya Jumla kuhusu Uchaguzi wa Serikali za Mitaa uliofanyika Novemba 27, 2024?

LGE2024 Mdau, yapi maoni yako ya Jumla kuhusu Uchaguzi wa Serikali za Mitaa uliofanyika Novemba 27, 2024?

Uchaguzi wa Serikali za Mitaa 2024

JamiiTalks

JF Advocacy Team
Joined
Aug 7, 2018
Posts
685
Reaction score
1,124
MJADALA_2.jpg
Uchaguzi wa Serikali za Mitaa 2024: Changamoto, Mafanikio, na Mustakabali wa Demokrasia Yetu

Novemba 27, 2024, Watanzania walishiriki katika Uchaguzi wa Serikali za Mitaa kwa lengo la kuchagua viongozi wa vijiji, vitongoji, na mitaa. Uchaguzi huu, kama chombo muhimu cha kukuza ushiriki wa wananchi katika uongozi wa maeneo yao, umekuja na matukio mbalimbali yanayostahili kujadiliwa kwa kina.

Maswali Muhimu:​

  1. Mchakato wa Uchaguzi: Je, uchaguzi ulikuwa wa haki na huru? Kuna changamoto zipi zilijitokeza kabla, wakati, na baada ya upigaji kura?
  2. Ushiriki wa Wananchi: Je, mwitikio wa wananchi ulikuwa wa kuridhisha? Ni kwa nini baadhi ya watu hawakushiriki ipasavyo?
  3. Nafasi ya Vyama vya Siasa: Vyama vya siasa vilipata nafasi gani katika kushawishi uchaguzi huu? Je, wagombea wa vyama vyote walipata haki sawa?
  4. Ushiriki wa Vijana na Wanawake: Je, makundi haya yalihamasishwa ipasavyo kushiriki au kugombea nafasi za uongozi?
  5. Mafanikio na Mapungufu: Ni nini kilichofanikiwa, na ni maeneo gani yanahitaji kuboreshwa kuelekea uchaguzi mkuu wa 2025?
  6. Mustakabali wa Demokrasia: Je, uchaguzi huu umeonesha ukuaji wa demokrasia nchini au bado kuna changamoto kubwa zinazohitaji kushughulikiwa?

Tunakaribisha mawazo, uzoefu, na mapendekezo yenu. Tafadhali shiriki kwa hoja za msingi na mifano halisi ili kujenga mjadala wenye tija kwa maendeleo ya nchi yetu.

Kushiriki mjadala kupitia XSpaces ya JamiiForums ingia hapa

Kupata taarifa na matukio ya kimkoa kuhusu Uchaguzi Serikali za Mitaa ingia hapa: LGE2024 - Special Thread: Orodha ya Mijadala ya Mikoa yote Tanzania Bara inayoshiriki katika Uchaguzi wa Serikali za Mitaa 2024

========================================

MAONI YA WACHANGIAJI WALIOPO KWENYE MJADALA

Esther Thomas - Naibu Katibu Mkuu ACT Wazalendo Bara


"Kwa kilichotokea katika Uchaguzi wa Serikali za Mitaa 2024, imeonesha hatuko tayari kwa Demokrasia ya Nchi huru na Haki"

"Mambo yalivyoonekana katika Uchaguzi wa Serikali za Mitaa yametuonesha tuna safari ndefu sana kufikia safari yetu ya kuwa Nchi ya Demokrasia"


"Uchaguzi ulisimamiwa kwa asilimia kubwa na Watumishi wa Umma, hivyo unapozungumzia watu waliofanya hujuma ni Watumishi wa Serikali, mfano Watendaji wa Kijiji, Walimu, Jeshi la Polisi"

"Wananchi wanapaswa kufahamu wahujumu wa Uchaguzi uliopita ni Watumishi wa Umma na aliyeharibu uchaguzi wote ni Serikali, kwa kuwa msimamizi wa Uchaguzi ni Idara ya Serikali"

"Kilichofanyika wakati wa Uchaguzi kinaonesha hata TAMISEMI wenyewe hawakujiandaa, kulikuwa na baadhi ya vitu havina maandalizi"

"Pia, ujumbe mwingine ni kuwa Serikali inaonesha haipo tayari kwa maendeleo ya Wananchi, walichokifanya ni kuwa wao walihitaji kupata madaraka na sio kwaajili ya Wananchi"

"Kutokea kwa Vitisho, Kutekwa, Kupigwa yanaonesha kuwa Wananchi wanafikishiwa ujumbe wa kutosema chochote au kulalamika, badala yake wawe tayari kutawaliwa"

"Viongozi walioteuliwa (Nawaita hivyo kwa kuwa sioni kama wamechaguliwa) sioni kama wanaweza kuwa na ujasiri wa kusimama hadharani na kuzungumzia maendeleo ya maeneo yao kwa kile kilichotokea katika Uchaguzi"

"Mtu anapokaa mezani kuzungumza na wewe kutafuta utatuzi sio dhaifu, hilo ndilo ambalo linaonekana upande wa pili kuwa kile ambacho kinafanyika wanadhani sisi ni dhaifu"

"Unapoona suala la utekaji unahisi halikuhusu, siku likitokea kwako au kwa mtu wako wa karibu au mtu unayemfahamu ndio utafahamu kuwa ni jinsi gani watu wanapata maumivu"

"Yote hayo yanatokana na kukosekana kwa Uwajibikaji wa Kikatiba na kufinywa kwa Demokrasia"

"Wasifurahie kushinda kwa Asilimia 99 wakati wanashindana kukimbia na mtu ambaye wamemkata miguu, watambue kuwa ipo siku huyo ambaye amekatwa miguu atapona na ndipo watatambua kuwa walikuwa wanashindana na Mtu wa aina gani"

John Pambalu - Mwenyekiti BAVICHA Taifa

"Kilichotokea katika Uchaguzi wa Serikali za Mitaa 2024 pamoja na matukio yake ikiwemo kutumia Wanafunzi kujiandikisha Kupiga Kura, Wizi wa Kura, Mauaji, imetufanya CHADEMA kutoa wito kwa Wadau mbalimbali kuwa ni wakati sahihi kuunganisha nguvu ili kupambania Katiba Mpya"

"Wadau wote kwa pamoja tunahitaji kuwa pamoja na kupata Katiba Mpya, ambayo italeta Haki na Usawa kwa watu wote"

"Hilo likiwa gumu basi tufanye mabadiliko madogo (minimum reform), ili tushughulikie masuala yetu Kikatiba, kwa kuwa inawezekana ikawa ngumu kutimiza hilo kabla ya Uchaguzi ujao"

"Inahitajika presha ya Umma katika kudai mabadiliko, ili Watawala wajione hawatakuwa salama na utulivu kama hakutakuwa na mabadiliko ya Katiba"

"Ninapozungumzia nguvu ya Wadau inatakiwa wale wote wanaofanya uhuni wakiwa katika nafasi Serikalini wajue kuwa Umma unahitaji mabadiliko na wajue Wananchi wanahitaji Uchaguzi Huru na Haki"

"Uchaguzi uliopita inawezekana tuliwaonesha kuwaamini na tukajisahau lakini kilichotokea katika Uchaguzi wa Serikali za Mitaa (2024) kimeonesha hawa watu ni walewale"

"Tunatakiwa kuunganisha nguvu tukiweka pembeni itikadi za Kisiasa na nyingine, zikiwemo za Kiimani ili tuwe kitu kimoja"

"Historia ya Vyama vya Upinzani kupinga Vyama vingine vya Upinzani inaonesha imekuwepo kwa miaka mingi, ilikuwa hivyo pia hata wakati wa harakati za kudai uhuru wa Nchi mbalimbali"

"CHADEMA tumesimamisha Wagombea lakini wamekutana na Upinzani kutoka kwa Vyama kadhaa vidogo vya Upinzani, ACT pia nao walikutana na changamoto kama hiyo"

"Kuna mauaji yametokea wakati wa Uchaguzi, lakini huwezi kusikia wanaoona Uchaguzi ulikuwa wa Haki wanadema chochote katika hilo, wanatafuta kile wanachoona wao kinafaa"

"Uchaguzi huu ulikuwa unatuma ujumbe kuwa bila kuwa CCM huwezi kupata Madaraka, ndio maana unaona wameshinda kwa 99%"

"Napongeza baadhi ya Watu mashuhuri wakiwemo kina Mzee Butiku na Viongozi wengine wa Dini walijitokeza na kukemea kilichofanyika wakati wa Uchaguzi (Serikali za Mitaa 2024), kuwa haukuwa sawa na Haki haikutendeka"

"Natoa wito kuwa kuna haja ya kuwa Wamoja na kuunganisha nguvu kujadiliana kuhusu Haki na Demokrasia kwa kuwa ni suala la Kitaifa, suala la uwepo wa Vyama vya Upinzani vinavyoweza kupinga vingine vya upinzani hilo lipo kihistoria"

Idd Mkanza - Katibu Mtendaji Jumuiya ya Vijana wa CUF

"Uchaguzi uliopita (Serikali za Mitaa 2024) CCM imeshinda kwa 99% lakini kuna Vijiji vingi ambapo mbali na wale walioenguliwa kulikuwa na maeneo mengi ambapo Wapiga Kura waliingia wakakuta wagombea ni wa Chama kimoja"

"Kuna watu wengi wamekatwa kwa makusudi. Wanatumia muda mwingi kufanya Kampeni lakini mwisho wake hakuna wanachokipata"

"Nadhani ni wakati wa Jumuiya za Kimataifa kusitisha misaada Nchini kwa kuwa tunachokifanya ni kuwadanganya wao na kuidanganya Dunia"

"Mfano; Wilaya ya Mtwara Vijijini, milango ilifunguliwa Saa Mbili asubuhi hadi saa Sita Mchana, kulikuwa na Kura batili na Mamlaka za Ulinzi zilihusika kusaidia hilo"

"Tunahubiri Demokrasia wakati kuna vitu vingi ambavyo haviendani na uhalisia, sisi kama Chama tunatarajia kutoa tamko kuhusiana na kilichotokea katika Uchaguzi wa Serikali za Mitaa 2024"

"Umuhimu wa kuwa na Serikali za Mitaani ni kumfanya Mwananchi awe karibu na Serikali yake na kushiriki katika kufanya maamuzi"

Majalio Kyara - Katibu Mkuu Sauti ya Umma

"Tunatakiwa kumshukuru Mungu kwa kumaliza Uchaguzi kukiwa na hali ya Amani na Salama"

"Niwapongeze TAMISEMI kwa kuwa walitushirikisha kuanzia mwanzo, japokuwa katika utekelezaji kuna mambo ambayo hata sisi yalitubana"

"Haiwezekani jambo kubwa kama hili likose changamoto, lakini kinachotakiwa kuangaliwa ni kuwa changamoto ni kubwa kiasi gani?"

"Pamoja na hivyo tunapokuwa tunalalamika tunatakiwa kujiuliza pia, Je, hakukuwa na mazuri? Au kila kitu kilikuwa kibaya?"

"Kuna tukio lilitokea Muheza, Jeshi la Polisi lilitutaka tuondoke sehemu tulipokuwa tunapiga Kampeni, baadhi ya Watu wakasema tusiondoke, tubaki ili tupate ‘kiki’ kwa kubishia maelekezo"

"Hatukufanya hivyo, tulifuata maelekezo kwa kuwa tulikiuka, hatukufuata maelekezo mapema, tukalazimika kuondoka hapo kwa amani"

"Jambo lingine ni kuwa sisi Wanasiasa tunatakiwa kuwa makini na maamuzi yetu wakati wa kutunga Sheria na Kanuni"

"Wenzetu CHADEMA walikuwa wanajiona wanaenda wao tu, walisema Vyama ni Viwili tu CCM na CHADEMA, sasa hivi wanarudi nyuma na wanataka ushirikiano, walitaka kupambana wao lakini tungeweza kwenda pamoja tangu kipindi hicho tungefika mbali"

"Mazingira ya kujitenga na kujiona bora yalikuwepo tangu wakati wa UKAWA, hakukuwa na umoja, kulikuwa na mazingira ya kujitenga na ndio maana hakukuwa na mafanikio"

"Kauli ya CHADEMA Taifa kuhusu Uchaguzi (wa Serikali za Mitaa 2024) imesema haukuwa Huru na wa Haki, wakati huo CHADEMA Kinondoni walisema Uchaguzi ulienda vizuri"

"Matukio ya Watu kuuawa wakati wa Uchaguzi yamekuwa yakitokea sehemu tofauti hata katika Nchi nyingine, tunachotakiwa kujiuliza ni je, kulikuwa na mazuri mangapi na mabaya mangapi, kisha ndio tunaweza kutoa kauli kwa ujumla"

"Kuna wakati sisi Wanasiasa tunajichanganya, unamsikia mtu anasema Uchaguzi huu usisimamiwe na TAMISEMI, usimamiwe na Tume Huru ya Uchaguzi, lakini kuelekea Uchaguzi Mkuu wanasema, Uchaguzi usisimamiwe na Tume Huru ya Uchaguzi. Unajiuliza hawa watu wanataka nini? Huo ndio ninaosema ni ubinafsi"

"Viongozi wanasahau kuwa katika Chama kila mmoja anafiti kwa sehemu yake, ndio maana ninasisitiza umoja wa Vyama, wao (CHADEMA) walikuwa wanataka kufanya kila kitu wao ndio maana wameenda imefika hatua unaona wanashindwa kuendelea, wanaturudia"

"Kuna siku nilimwambia Mnyika (CHADEMA), kuwa nyie mnafanya Maandamano lakini mnafeli, na nikamwambia mbona mnafeli hata kabla ya kuanza maandamano?"

"Kuhusu Takwimu kuwa kuna Vyama vya Upinzani vilipinga Vyama vingine vya Upinzani, hizo ni historia tu, sasa hivi tunatakiwa kuishi tulivyo kulingana na uhalisia"

Thobiasi Mgisha (Mdau)

"Tuna mchakato wa Uchaguzi ambao hauna mazingira ya Haki, Wapinzani wanatakiwa kujipanga na kujianda kutokana na hali halisi iliyopo, kwa kuwa CCM haiwezi kujitokeza na kusema "Tumeshindwa Uchaguzi"

"Kote Duniani, sehemu wanapopambania Haki dhidi ya Chama Tawala, Dola ya Wapinzani ni Wananchi, hiyo ipo hivyo katika Nchi nyingi"

"Hali ilivyo inaonesha Wapinzani hawajawapa Wananchi elimu na uelewa wa nini wanatakiwa kukifanya, wanatakiwa kutengeneza msingi wa Umma kuelewa umuhimu na nguvu yao"

"Katika Uchaguzi uliopita (Serikali za Mitaa), kulikuwa na upigaji kura wa Ndio na Hapana, jiulize huo upande wa Hapana unasimamiwa na nani?"

"Mara baada ya Rais Samia kuruhusu uwepo wa Mikutano ya Kisiasa ambalo ni suala la Kikatiba, napongeza ACT Wazelendo na CHADEMA kwa kuwa ndani ya muda mfupi waliweza kuwa ‘active’ na kuwajibika kufanya shughuli zao inavyotakiwa"
 
1, Uchaguzi haukuwa huru na haki, Wakati wa mchakato wa kujiandikisha kulitokea dosari nyingi zilizoonekana kuwa za Makusudi kama kuandikisha watu waliochini ya umri wa miaka 18(wanafunzi) hapa mwanangu aliye chini ya miaka 18 aliandikishwa shuleni.

-Kutokutumika kitambulisho wala uthibitisho wowote wa kuwa anayeandikishwa ni mkazi wa mtaa au kitongoji husika na ana umri unaostahili hii ilikuwa ni njama ya kuweka watu.

-Kujitokeza dosari ya waandika wapiga kura kuongeza idadi ya watu(rejea vio zilizagaa mitandaoni)

2.Kwa upande wangu naona mwitikio wa watu ulikuwa mdogo sana, pengine huu uchaguzi unaweza kuwa umevunja rekodi ya mwitikio mdogo wa watu licha ya TAKWIMU kuonesha uandikishwaji ulikuwa wa kiwango kikubwa(TAKWIMU hizo zina dosari nyingi kuonesha hazikuwa halisi)

- Watu hawakushiriki ipasavyo kwa sababu TAMISEMI walionesha kulazimisha kusimamia uchaguzi na kuonesha dhahiri nia ya kusababisha ushindi wa kishindo kwa chama walichokuwa wanakitaka wao( Moja kwa moja ni CCM ukizingatia waziri wa wizara husika ni mwanachama wa CCM)

3. Vyama vilipata nafasi ila si nafasi sawia, kuna namna ya kuvikandamiza vyama pinzani ilijitokeza, rejea tukio la Polisi kuwakamata viongozi wa CHADEMA na ACT kwa kigezo cha CHADEMA kuingilia mkutano wa ACT licha ya ACT kuridhia eneo lao litumike na CHADEMA.

4. Uhamasishaji wa vijana na wanawake haukuwa mkubwa, hakukuwa na msisitizo wa kuwahamasisha makundi ya vijana na wanawake kushiriki, sikuona TAMISEMI wala vyama vikisisitiza kwa kina juu ya hilo

5, Kwenye uchaguzi huu CCM wamefanikiwa kupora haki ya Watanzania ya kuchagua viongozi wao, aidha wamefanikiwa kuuonesha Umma kuwa wao hawawezi kuiacha demokrasia ifanye kazi yake. Wanaipora na kushangilia ushindi wa asilimia 99 huku wakidhani wamefanikiwa kumbe wamejiabisha kwa kuwa wanaonesha walivyo waoga, hawakubaliki, na muda wao wa kuongoza umepita isipokuwa wanatumia nguvu ya Jeshi la polis kubaki madarakani

Aidha, Kuwe na tume huru na siyo jina Tume huru, tume itakayo kuwa haifungamani na chama chochote, watu wa tume wasiwe wa kuteuliwa, waombe nafasi hiyo( Wanaowasaili wawe nje ya mfumo wa siasa) na wasiwe wa kudumu wawe kwa ajili ya uchaguzi huo tu.

Vyama vya siasa viachwe viwe huru kutekeleza wajibu wao bila jeshi la polisi kuingilia kwa kuweka upendeleo kwa chama kimoja na kuingilia uhuru wa vyama vingine huku likijidai kuwa na intelijensia ya kubaini uhalifu unatarajiwa kufanywa na vyama vya upinzani huku likiacha matamshi ya kuonesha uvunjifu wa sheria dhidi ya vyama pinzani yanayotolewa na wafuasi wa CCM.

6. Kuna changamoto kubwa zinazohitaji kushughulikiwa, Mifumo ya uchaguzi wa Tanzania ipo kwa ajili ya kumfanya aliye na madaraka aamue nani ashinde na nani ashindwe kwa kuwa kila kitu kinakuwa chini ya mamlaka ya unayeshindana naye ambaye yuko madarakani.
 
Kwa kifupi hakukuwa na uchaguzi bali kulikuwa na ujinga, upuuzi, upumbavu, uuaji, utesaji, upotevu wa pesa za umma na muda chini ya usimamizi wa CCM, serikali na vyombo vya dola.
Kuanzia zoezi zima la uandikishaji, ugombea, upigaji kura, uhesabuji kura na kutangaza matokeo vyote vilikuwa ni vitu vya kuigiza ujinga na upuuzi mtupu.

Ushauri:
Uchaguzi wote ufutwe kabisa na usiwepo tena mpaka tuwe na mifumo huru ya kuweza kusimamia na kutenda haki kwa watu wote.
 
Uchaguzi wa Serikali za Mitaa 2024: Changamoto, Mafanikio, na Mustakabali wa Demokrasia Yetu

Novemba 27, 2024, Watanzania walishiriki katika Uchaguzi wa Serikali za Mitaa kwa lengo la kuchagua viongozi wa vijiji, vitongoji, na mitaa. Uchaguzi huu, kama chombo muhimu cha kukuza ushiriki wa wananchi katika uongozi wa maeneo yao, umekuja na matukio mbalimbali yanayostahili kujadiliwa kwa kina.

Maswali Muhimu:​

  1. Mchakato wa Uchaguzi: Je, uchaguzi ulikuwa wa haki na huru? Kuna changamoto zipi zilijitokeza kabla, wakati, na baada ya upigaji kura?
  2. Ushiriki wa Wananchi: Je, mwitikio wa wananchi ulikuwa wa kuridhisha? Ni kwa nini baadhi ya watu hawakushiriki ipasavyo?
  3. Nafasi ya Vyama vya Siasa: Vyama vya siasa vilipata nafasi gani katika kushawishi uchaguzi huu? Je, wagombea wa vyama vyote walipata haki sawa?
  4. Ushiriki wa Vijana na Wanawake: Je, makundi haya yalihamasishwa ipasavyo kushiriki au kugombea nafasi za uongozi?
  5. Mafanikio na Mapungufu: Ni nini kilichofanikiwa, na ni maeneo gani yanahitaji kuboreshwa kuelekea uchaguzi mkuu wa 2025?
  6. Mustakabali wa Demokrasia: Je, uchaguzi huu umeonesha ukuaji wa demokrasia nchini au bado kuna changamoto kubwa zinazohitaji kushughulikiwa?

Tunakaribisha mawazo, uzoefu, na mapendekezo yenu. Tafadhali shiriki kwa hoja za msingi na mifano halisi ili kujenga mjadala wenye tija kwa maendeleo ya nchi yetu.

Jiunge na mjadala huu, tusaidie kubaini njia bora ya kuimarisha demokrasia yetu!
Uchaguzi gani mkuu, hapakua na uchaguzi bali drama,
 
Hakuna uchaguzi uliofanyika labda useme uteuzi ambao umefanywa na Tamisemi kwa maagizo na usimamizi wa CCM.
Kwahiyo hoja ya kujadili uchaguzi haina mashiko.
 
Kiufupi tu ccm wamevuruga mchakato kuanzia mwanzo hadi mwisho haukuwa uchaguzi bali ni wizi wa wazi wazi na ubakaji wa demokrasia.

Ccm sio chama cha siasa ni chama dola kinachotumiwa na watawala kulinda maslahi yao binafsi.

Majina feki waliongeza mengi tu..kura feki zilipigwa nyingi tu..wagombea wa upinzani walienguliwa makusudi kabisa.

Chaguzi zimekua sehemu ua kuhalalisha ubakaji wa demokrasia

Bila katiba mpya na tume huru ya uchaguzi sahauni kupata demokrasia ya ukweli zaidi ya maigizo kutoka ccm na vibaraka wake.
 
Kuna Chizi mmoja alienda kupiga kura baada ya kumaliza akaondoka bila kuweka kidole kwenye wino alichosema kwa wale wasimamizi ni amepiga kura ila hamjui yule aliempigia wa Chama A yeye amependa tu zile rangi za majani ya maboga, akatembea akawaacha huku nyuma wasimamizi wanacheka alipofika mbele akawa anaendelea kuwaambia watu kwamba amepiga kura ila hajachovya kidole walipoona wale wa maboga maboga wakaona hili dili wakamwambia Chizi huyo aende tena akapige tena kura nyingine kwa yule yule aliempigia mwanzo maana akienda si hajachovya kidole kwa hio akienda hawatojua km ameshapiga, Chizi akagoma

Uchaguzi ulikua wa ovyo sana
 
Bila hii kitu, tutaendelea kuburuzwa mpaka tuongee au tunene kwa lugha
2Q==.jpg
 
Uchaguzi wa Serikali za Mitaa ulifanyika kwa uhuru, haki na uwazi. Pongezi kubwa sana kwa Serikali ya Mama Samia!!
 
Back
Top Bottom