Polisi waruhusu maandamano ya kudai Zanzibar ni nchi
Rais Amani Karume wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar.
Na Salma Said, Zanzibar
JESHI la Polisi Zanzibar, limetoa kibali cha kufanyika maandamano ya kutetea Zanzibar kuwa ni nchi yaliyoandaliwa na Chama cha National Reconstruction Alliance (NRA), visiwani hapa.
Taarifa ya polisi iliyotolewa visiwani hapa jana ilisema kwamba, maandamano hayo yameruhusiwa kufanyika keshokutwa na yataanza saa 2:00 asubuhi katika Viwanja vya Kombawapya hadi Kibanda Maiti Uwanja wa Demokrasia.
Hata hivyo, Jeshi la Polisi limetoa masharti kwa wahusika, ikiwa ni pamoja na wahusika kutochukua silaha ya aina yoyote wala kubeba mabango katika maandamano hayo.
Kwa mujibu wa barua hiyo yenye kumbukumbu No. W/MJN/SO.7/2A/106, pia Polisi imewataka waandaaji kuhakikisha wanawadhibiti wanachama wao wasiharibu mali za raia na wananchi katika maeneo ambayo yatapitia.
"Kusiwepo na lugha ya matusi kwa viongozi wa serikali, vyama vya siasa kwa nia ya kuleta jazba, ugomvi na kupelekea kuhatarisha amani na utulivu," inaeleza barua hiyo ambayo Mwananchi imeiona ikiwa imeandikwa Agosti 7, mwaka huu na kusainiwa na Mkuu wa Polisi wa Wilaya ya Mjini, Mkadam Khamis Mkadam.
Aidha, viongozi wa NRA wametakiwa kuhakikisha vyombo vya habari vinaruhusiwa katika maandamano hayo vikiendelea kufanya kazi zao bila ya kuwepo vikwazo vyovyote.
Akizungumza na waandishi wa habari, Naibu Katibu Mkuu wa NRA Zanzibar, Suleiman Gaddafi, alisema matayarisho ya maandamano hayo yamekwishakamilika ikiwemo kuwaalika viongozi wa vyama vingine ili kuongeza nguvu ya mahudhurio.
Alisema takriban vyama vyote vilivyopata usajili wa kudumu nchini vimekaribishwa katika maandamano hayo isipokuwa Chama Cha Mapinduzi (CCM), wamesema hao hawatashiriki kwa vile wanaunga mkono uamuzi wa Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, kwamba suala hilo waachiwe wanasheria wa pande mbili kulishughulikia.
"Naibu Katibu Mkuu wa CCM nilipokutana naye ili kumkaribisha katika maandamano hayo amenijibu chama chake hakiko tayari kwa vile kinaamini suala hilo linashughulikiwa kama ilivyoagizwa na serikali," alisema Gaddafi. Alisema pamoja na msharti magumu yaliyowekwa na polisi, wanashukuru kwa kuruhusiwa kufanya maandamano hayo kwa vile yatatoa fursa kwa wananchi wa Zanzibar kuonyesha ni jinsi gani walivyokerwa na kauli ya Pinda kwamba Zanzibar sio nchi. Gaddafi alisema, maandamano hayo si ya itikadi ya chama na kwamba wananchi wote wa Zanzibar wanaruhusiwa kushiriki bila kujali tofauti zao za kisiasa kwa vile suala hilo linahusu nchi na sio chama.Awali, maandamano kama hayo yalikuwa yafanyike Zanzibar, lakini yalishindikana baada ya Spika wa Baraza la Wawakilishi, Pandu Ameir Kificho, kugoma kuyapokea.
Alikataa kupokea maandamano hayo yaliyokuwa yamalizikie katika Viwanja vya Baraza la Wawakilishi kwa maelezo kwamba, katika kipindi hicho Viwanja vya Baraza vilihitaji mazingira ya utulivu kutokana na wajumbe kuendelea kujadili bajeti ya serikali, kwa hiyo haikuwa jambo la busara kuruhusu mikutano ya watu katika viwanja hivyo.
Maandamano hayo yalikuwa yameandaliwa na Wazanzibari wanne kwa niaba ya wenzao 10,000 wanaotetea kuwa Zanzibar ni nchi licha ya kufikiwa kwa Muungano wa Tanganyika na Zanzibar mwaka 1964.
Tangu Pinda atoe kauli kwamba Zanzibar si nchi akiwa bungeni akinukuu Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kumekuwa na mjadala mkali kutoka kwa watu mbalimbali, baadhi wakimuunga mkono ilhali wengine wakimpinga.
Pinda hadi sasa amekwishapingwa na viongozi waandamizi ndani ya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, akiwamo Naibu Waziri Kiongozi na Waziri wa Habari, Utamaduni na Michezo, Juma Shamhuna, Mwanasheria Mkuu wa SMZ, Iddi Pandu Hassan na wawakilishi kadhaa.