Mfanyabiashara mashuhuri Z'bar achochea ufa wa Muungano
Na Salma Said, Zanzibar
MFANYABIASHARA mashuhuri Zanzibar, Mohammed Raza, amewashauri Wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kutoka visiwani hapa, warudi makwao kwa vile hawaiwakilishi nchi.
Kauli hiyo imekuja siku chache baada ya Jeshi la Polisi visiwani hapa kupiga marufuku maandamano yaliyoandaliwa na Chama cha National Reconstruction Alliance (NRA), yaliyotarajiwa kufanyika jana.
Raza alisema pia, wafanyakazi wote wa taasisi za Muungano wanaoiwakilisha Zanzibar katika serikali ya Muungano, wanapaswa kurudi nyumbani kwa vile visiwa hivyo siyo nchi.
Licha ya Raza kuwataka Wabunge wa Zanzibar kurejea kwao kwa hoja kuwa wanaiwakilisha Zanzibar, ukweli ni kuwa, Wabunge kutoka Zanzibar na Tanzania Bara huingia katika Bunge la Jamhuri ya Muungano kuwakilisha majimbo yao.
Vile vile, kauli ya Raza ya kuwataka wafanyakazi wa taasisi za Muungano wanaoiwakilisha Zanzibar kurejea kwao haina ukweli wowote kwa kuwa hakuna wafanyakazi wanaotoka Zanzibar kuiwakilisha katika Muungano.
"Wabunge wote wa Zanzibar warudi makwao. Wasiende Dodoma. Kwa sababu hawawakilishi nchi pamoja na wafanyakazi wote wa taasisi za Muungano warudi kufanya kazi kwao hadi hapo itakapojulikana moja wapo kama ni nchi au si nchi, alisema Raza, ambaye ni Kada wa Chama Cha Mapinduzi (CCM).
Akizungumzia kauli kwamba, wanaozungumzia Zanzibar ni nchi kuwa ni wahaini, Raza alisema Wazanzibari wote kwa sasa ni wahaini na wataendelea kuwa hivyo hadi suala hilo litakapopatiwa ufumbuzi.
Tunaambiwa Zanzibar siyo nchi. Je, mwaka 1964 Wazanzibari tuliuzwa kwa Watanganyika? alihoji na kuongeza: Tuambiwe basi kama tuliuzwa kwao.
Raza, ambaye aliwahi kuwa Mashuhuri kwa Michezo wa Rais wa awamu ya tano Zanzibar, Dk Salmin Amour Juma, alisema kuitwa wahaini hakuwezi kuua mjadala huo kwani Wazanzibari wana machungu ya tangu kusainiwa kwa mkataba wa Muungano na waasisi wawili, Mwalimu Julius Nyerere na Abeid Amani Karume, ambao wote wameshafariki.
Sisi Wazanzibari sote ni wahaini, nikiwamo mimi na tutaendelea kuwa wahaini kwa kusema Zanzibar ni nchi. Sote wahaini ndio na hilo tumethibitishiwa na Baraza la Wawakilishi kwamba, Zanzibar ni nchi na hakuna kitakachobadilisha hilo, alisema.
Alidai, kuwa vikao vilivyofanyika kuidhinisha kwamba Zanzibar si nchi, havikuwa halali kwa kuwa havikupata ridhaa ya Wazanzibari.
Vikao hivyo vilivyoidhinisha sio halali kwa sababu havikupata theluthi tatu ya Wazanzibari. Katiba lazima ipatikane kwa theluthi tatu ya Wazanzibari. Kwanza, hakuna mkataba ulioondosha Zanzibar kuwa nchi, hakuna makubaliano hayo, hakuna, alisisitiza Raza.
Alisema Katiba ilivunjwa wakati wa kupitisha mabadiliko, ambayo yalimwondolea madaraka Rais wa Zanzibar asiwe Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuwa mabadiliko hayo hayajapata ridhaa ya Wazanzibari inavyotakiwa kwa mujibu wa sheria.
Alisema, wakati umefika kwa Wazanzibari kudai hati ya makubaliano ya Muungano ili kujua ukweli wa mambo, ambayo yameanza kutokota jikoni hivi sasa sambamba na kutaka kura ya maoni juu ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar.
Alisema, makubaliano ya Muungano hayakuwa sehemu kubwa iibane sehemu ndogo wala Muungano haukuwa kwa mmoja mume na mwingine mke, bali ulikuwa kati ya nchi mbili zilizo huru zenye kujitawala, tena kwa muda maalumu na siyo milele.
Hatukuungana kama mke na mume wala kama mkubwa na mdogo. Tumeungana nchi mbili huru na zenye kujitawala. Hatukuungana kama nchi hii ina watu wengi hii kidogo ahhh hapana, alisema na kuongeza:
Kama ni hivyo, basi tuachieni Wazanzibari tujitegemee kwa njia nzuri, tusije tukapigana mizinga, tusigombane. Tuachieni Zanzibar. Kwa nini mnatung'ang'ania?" alihoji Raza, ambaye katika siku za karibuni amelivalia njuga suala la Muungano bila kutumia vikao rasmi vya chama chake.
Alidai kuwa, umefika wakati kwa suala hilo kujadliwa na kupatiwa ufumbuzi wa haraka na hakuna suala la kudhibitiwa watu na kukemewa na lazima demokrasia ipewe nafasi yake.
Matusi yamekuwa mazito mno. Mara tunaambiwa wimbo wetu wa taifa kama kwaya, mara rais wetu kama rais wa timu ya mpira, mara bendera kama ya
simba..ahhh! Tuheshimiane. Mambo ya kutukanwa hatutaki. Maneno yanayojitokeza hivi sasa, ni matusi kwa Wazanzibari wenzetu. Wajifunze lugha ya kusema na sio matusi, alisema kwa hasira.
Raza, alisema mjadala kuhusu suala hilo, umekuja siku mbaya, ambayo CCM inateremka kilima, ambacho karibuni wananchi wataingia katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2010, ambao hautakuwa na Ilani wala sera kwa kuwa suala hilo litakuwa limewagawa wanachama, akiwamo yeye.
Aliwataka polisi kuacha kuingilia siasa, badala yake wafanye kazi zao za kulinda raia na mali zao, ikiwa ni pamoja na kuwapa haki Wazanzibari kufanya maandamano yao kwa amani, kwani hiyo ndio njia pekee ya kufikisha ujumbe kwa viongozi wao waliowachagua kwa kura.
Alipoulizwa kama wako tayari kupokea ushauri wa Raza, Mbunge wa Ziwani, Ali Said Salim (CUF), alisema hawawezi kurudi kwa vile wanachokiwakilisha bungeni, ni Zanzibar.
Hata hivyo, Salim, ambaye pia ni Naibu Msemaji wa Kambi ya Upinzani Bungeni wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, alisema kisiasa Zanzibar, ni nchi, lakini kikatiba ya Jamhuri ya Muungano, si nchi.
"Kama Zanzibar siyo nchi, Rais anawakilisha kitu gani? Hatuwezi kurudi kwa sababu tunawakilisha Zanzibar," alisema Salim.
Alisema anamshangaa Raza kuibuka leo wakati alipokuwa Mshauri wa Rais wa Zanzibar, aliridhia marekebisho ya Katiba, ambayo yalimwondolea madaraka Rais wa Zanzibar kuwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, licha ya wapinzani kupinga suala hilo kwa nguvu zao zote.
Tuma maoni kwa Mhariri