Ni ajabu kwamba wanasiasa wakuja juu sana kulinda kitumbua chao cha SIASA kisiguswe na viongozi wa dini. Lakini wakati huo huo wanampigia makofi kiongozi mwenzao wa siasa anayetumia vitabu vya dini kutimiza malengo ya kisiasa. Na mbaya zaidi anafanya hivyo kwa kupotosha, tena kwa makusudi.
Makamba ametumia vibaya maandiko matakatifu juu ya kubatiza kwa maji na kubatiza kwa moto na huo ni upotoshaji wa makusudi au kukejeli kitabu cha Biblia Takatifu ambayo ameifanya bila kujali kama ataumiza hisia za waumini wanaotumia na kuiheshimu Biblia. Kwa kufanya hivyo, anashindwa hata kuwaheshimu Wakristo ambao ni wana CCM.
Iwapo mzee huyu ana uwezo wa kuona ubaya wa kufanya hivyo, na iwapo anaheshimu misingi ya kuheshimu imani za wengine, jambo la kwanza anapaswa kuwaomba radhi Wakristo, iwapo alifanya hivyo bila kukusudia. Jambo la pili ni kwamba, iwapo anataka kuendelea kuitumia biblia kwenye jukwaa kubwa namna hiyo kama afanyavyo, basi aende chuo cha Biblia, akafundishwe Biblia na wenye Biblia yao. Najua kila mtu anaweza kununua Biblia kama anavyoweza kununua novel, lakini Makamba haiamini Biblia, kwani kama angeiamini angebatizwa, kwa hiyo Biblia sio yake. Ni hatari sana kutumia kitabu cha imani ya watu wengine unavyotaka wewe. Sote tunajua Salman Rushdie alinunua Quran Tukufu kama vile kununua novel na akakitumia alivyotaka yeye, matokeo yake? Aliwaudhi wenye kitabu chao.
Naomba niishie hapa ili nisije nikaamsha hisia kali.
Makamba, kama unaamini Salman Rushdie alifanya kosa, iheshimu Biblia!