Analogia Malenga
JF-Expert Member
- Feb 24, 2012
- 5,108
- 10,191
Abiria ndani ya ndege ya Kampuni ya Precision, jana waliingiwa na hofu ya usalama wao baada ya injini moja kuzima ikiwa angani.
Ndege hiyo yenye namba PW 467 ikitokea Kahama, ikielekea Dar es Salaam kupitia Mwanza, ilizima injini baada ya dakika 51 kuruka kutoka uwanja wa ndege wa Mwanza.
Hofu ilianza kutokea baada ya abiria mmoja, kijana wa kizungu, kuanza kupiga kelele, akiwaeleza wenzake waliokuwa wameketi jirani, kwamba injini imezima.
Baadaye abiria wengine waliingiwa hofu, huku baadhi wakisali, wakilia na wengine kuonekana wamejiinamia, huku wamefunika nyuso zao.
Baada ya abiria kuonekana 'wakipaniki' ndipo rubani wa ndege hiyo alitangaza kuwepo kwa hitilafu hiyo huku akieleza kwamba hali siyo ya kutisha sana.
"Abiria wetu wapenzi, ndege yetu imepata tatizo la kiufundi, injini moja imezima, lakini hakuna haja ya kuwa na wasiwasi kwani, tunapanga kutua katika kiwanja jirani na hapa tulipo," alisema rubani huyo.
Hata hivyo, tulizo la mwana anga huyo halikuleta afueni ya wasiwasi kwa abiria wengi, waliendelea na hofu yao, huku wengine waliokuwa hawajatambua kinachoendelea wakiungana na wengine kusononeka.
Rubani alirejea tena kwa tangazo; "Abiria wetu wapendwa, tunasikitika kwa kilichotokea, nawaomba kuwa watulivu wakati sasa tunajiandaa kutua Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro. Tutatua ndani ya dakika 20."
Baada ya muda huo, ndege hiyo ilitua salama katika uwanja huo na abiria walishangilia. Wengine walipiga kofi, wengine wakipiga kelele za shangwe na wengine wakimshukuru Mungu.
Mmoja wa abiria aliyekuwamo ndani ya ndege hiyo, Simon Mkina, aliandika katika ukurasa wake wa Twitter na taarifa hiyo kusambaa dunia nzima, huku akipongezwa kwa kutoa taarifa hiyo mapema.