Kuna mtu nimeona ameandika huko fb namnukuu hapa
RAI YANGU KWA SERIKALI JUU YA MFUMO WA AJIRA ZA WALIMU NA WATENDAJI WA AFYA TAMISEMI
Leo nataka nichangie mawazo yangu kwenye mfumo wa ajira wa TAMISEMI. Kwa nia njema serikali kupitia wizara ya OR-TAMISEMI iliandaa mfumo wa ajira kwa walimu na watendaji wa afya kwa nia njema kabisa ikiwa malengo ni kuendana na dunia ya leo ambayo takribani huduma nyingi zinafanyika wavuni. Lakini pia kupitia mfumo huo wa ajira husaidia kupunguza gharama na muda. Kubwa zaidi kutumia mifumo kama hiyo husaidia kutokomeza janga la rushwa. Hivyo naipongeza sana serikali kwa maono haya mazuri sana.
Sambamba na hilo, bado kuna changamoto katika zoezi zima la ajira za walimu na watendaji wa afya. Kwa mawazo yangu nimeona bado hatujafikia lengo la kuanzisha ile mifumo. Sijajua kuna watu wanafanya hujuma au ni wapi tunakwama ili tuweze kufika pale tulipopataka. Jambo ninaloliona ni kwamba, mfumo wa ajira umeandaliwa kwa namna ambayo wasiokua na sifa mfumo unawakataa. Hii ina maana kwamba wote wanaokubaliwa na mfumo wana sifa linganifu za kuwa walimu au watendaji wa afya hapa kwetu Tanzania. Sijajua ni mfumo ndio unawachagua wale wanaotakiwa na kuwaacha wengine au ni watu hupembua kutoka kwenye wale wenye sifa ambao mfumo umewakubali ili kujaza nafasi wazi za ajira? Hili bado sijalipatia ufumbuzi. Muhimu ni kwamba, vyovyote itakavyokua bado kutakua na udhaifu katika kuwachagua watakaojaza nafasi hizo kutoka kwenye kundi la wengi ambao mfumo umewakubali muda wa kuwa hakuna kigezo kingine kinachotumika kuwachuja.
Nikilinganisha na mfumo wa ajira wa sekretarieti ya ajira, ambapo waombaji hujisajili na kisha tangazo la kazi likitoka hutuma maombi na kisha mfumo huwateua watu wote wenye sifa na kuitwa kwenye usaili. Kisha kupitia usaili hupatikana wenye sifa zaidi ya wengine. Na inapotokea watu walioomba ni wengi basi hupangwa saili zaidi ya moja ili kupunguza idadi yao. Kwa mfumo huu hata mtu akikosa nafasi moyo wake unasuuzika kuwa amekosa kwa haki, hivyo kumfanya asiwe na wasiwasi au mafundo moyoni mwake dhidi ya serikali yake.
Tukija kwenye mfumo wetu wa ajira za walimu na watendaji wa afya, huku mambo ni tofauti kabida. Ni ukweli usio na shaka kuwa wanaoomba nafasi huwa ni wengi sana na hata ambao mfumo umewakubali kuwa wana sifa pia huwa wengi. Lakini mbali na wingi huo, hatujawahi kusikia walimu hao wakiitwa kwa ajili ya usaili. Hii ina maana kwamba huchaguliwa baadhi tu ili wajaze nafasi wazi za kazi zilizotangazwa. Hili huleta maswali hasa kwa wenye weledi wa mambo na wale wenye kupenda kujihosha kwa kufukiria nje ya boksi. Kwamba hawa waliochaguliwa wana sifa gani za ziada za kuwazido wengine? Na hali wote wana sifa sawa linganifu? Jambo hili huacha manung'uniko kwa wengine waliokosa nafasi ya kazi kiasi wengine hufikiria kuwa huenda udanganyifu umefanyika na wengine wakaenda mbali wakasema huenda hao waliopata kuna chochote kitu walichokitoa.
Ili kukata mzizi wa fitina, kwa maoni yangu ningeshauri baada ya kupata idadi ya walioomba kujaza nafasi hizo wenye sifa linganifu, waitwe kwenye usaili ili walinganishwe na kupitia usaili wachukuliwe walimu wenye uwezo zaidi ya wengine kama wanavyofanya sekretarieti ya ajira. Ingawa hili litaongeza gharama kidogo, lakini manung'uniko yatakayofutwa kwenye vifua vya wengi dhidi ya serikali ni bora zaidi ya gharama zitakazotumika kwa ajili ya usaili.
Pamoja na hayo yote, mtaani kuna idadi kubwa ya wahitimu wa vyuo vikuu na vyuo vingine, ambao hawawezi kuisha kwa nafasi chache zinazotolewa na serikali. Lakini pia kuna ambao walihitimu miaka ya nyuma tangu 2012 kama nilivyosikia kutoka kwa Waziri mwenye dhamana na wengine wapo waliohitimu mwaka jana. Kutoa nafasi za kazi kwabwote hao kuanzia 2012 hadi 2020 kwa mara moja bado nahisi inaleta shida na sinto fahamu, lakini pia ndio maana wahusika hupata kazi ngumu ktk kuamua nani apewe na nani asubiri.
Katika kutatua hili, mimi ninashauri serikali kupitia wizara husika ingetoa mgawanyo wa nafasi za kazi zinazotolewa kwa miaka ya wahitimu. Kwa mfano, hivi karibuni wizara imetangaza nafasi elfu sita, hivyo kwa mawazo yangi naona ni vema ingepanga kuwa nafasi hizi zitawahusu wahitimu wa mwaka 2012 hadi 2015 kwa mfano ili wale waliohitimu kuanzia mwaka 2016 waendelee kusubiri zikitoka nafasi zingine zitawahusu wao. Na hivyo ifanyike kila zinapotokea nafasi za ajira hasa kwa kada ambazo wahitimu ni wengi sana kama walimu. Hili litasaidia mambo yafuatayo;-
a) Kupunguza idadi ya waombaji hivyo kurahisisha zoezi
b) Kutoa nafasi kwa wahitimu wa zamani ambao huenda muda unavyokwenda wakapoteza sifa ya kuajiriwa na serikali
c) Kutokana na uchache wa waombaji, kuiwezesha wizara kuandaa zoezi la usaili kwa watakaoomba
d) Kuondosha mshuguliko na gharama kwa wahitimu wa miaka mingine kwani hawatashugulishwa na kuomba nafasi hizo kwa kutambua kuwa haziwahusu. Kuna suala ambalo wengi hatulizingatii, huu mfumo wa kuomba ajira kupitia wavuni unagharimu sana vijana wetu hasa wale waishio vijijini ambako miundombinu ya kuwawezesha shuguli hizo ni hafifu, au sehemu zingine hamna kabisa hivyo huwalazimu kusafiri kwenda mijini kupata huduma ya kompyuta, na ku scna vyeti nk.
Haya ni maoni yangu binafsi, mwingine anaweza akatoa ya kwake kwa vile anavyoona yeye inafaa. Unaweza ukakosoa lakini kwa hoja, ingawa sauti yangu ni ndogo lakini ninaamini itawafika walengwa. Huenda rai yangu ikifanyiwa kazi ikaleta natija.
Imeandikwa nami;-
Msusa. M. Msusa
Masasi Mjini
29/05/2021
+255 714 291 319