Lycaon pictus
JF-Expert Member
- Jan 31, 2021
- 9,189
- 16,128
Hotuba hii ilitolewa kama kijitabu TANZANIA ITAJENGWA NA WENYE MOYO. Unaweza kukisoma bure ndani ya app ya Maktaba Sauti. Inapatikana playstore.
Oktoba 23, 1966.
Wananchi,
Jana tumefukuza wanafunzi wapatao 393 kutoka katika vyuo mbali mbali vya Dar es Salaam baada ya maandamano yao ya kupinga mpango wa Serikali wa National Service. Tumeamua vijana hao, waliokuja mpaka Ikulu wakipinga mpango wa National Service, na kusema maneno machafu- machafu, waondoke warudi majumbani kwao.
Wanafunzi gani.
Kwanza nataka kuwaambieni, wananchi, kwamba wanafunzi hao wametoka katika vyuo mbali mbali, na majina ya vyuo hivyo yametangazwa. Baadhi yao wametoka katika Chuo Kikuu pale mlimani, wengine wametoka katika Chuo kile cha Ufundi hapo nyuma yenu, wengine wametoka katika Chuo cha Madaktari kule Mhimbili, na wengine wametoka katika Chuo cha Waalimu, kule Chang'ombe. Vile vile kuna waliotoka katika Chuo cha Biashara hapo nyuma ya Chuo cha Ufundi na wachache wametoka katika shule za sekondari. Lakini walio wengi, zaidi ya nusu ya wote wale waliokuja Ikulu, na ndio tuliowaambia warudi majumbani kwao, wametoka katika Chuo Kikuu kule mlimani.
Walio wengi walikataa.
Nataka kueleza pia kwamba katika Chuo Kikuu wamebaki vijana wengine wa Kitanzania waliokataa kuwaunga mkono wenzao katika maandamano yale. Walio wengi walikataa. Katika chuo hiki hapa cha ufundi, walio wengi walikataa. Katika chuo cha waalimu cha Chang'ombe walio wengi walikataa. Katika vyuo hivyo vingine vyote nilivyovitaja, walio wengi walikataa. Nataka kuwapa pongezi vijana hao wa vyuo hivyo vyote ambao najua walishawishiwa na wenzao kwa kukataa kuingizwa katika maandamano ya kupinga National Service. Pia nawapa pongezi vijana wa shule za sekondari wote, sio wa hapa Dar es Salaam tu bali na wa shule za sekondari za Tanzania nzima kwa kukataa kuingia katika jambo hili baya. Wengine nimesema nao mimi mwenyewe, na wengine wamehutubiwa na wenzangu Mawaziri, nao hawakubali upuuzi huu ambao umekaa miezi mingi sana katika Chuo chetu Kikuu. Jana upuuzi ule ukadhihirika uwanjani kule Ikulu.
Maana ya "National Service".
Vijana walikuja Ikulu kuja kupinga mpango wa National Service. Wananchi sasa nataka kuwaelezeni kwa utaratibu kadiri nitakavyoweza maana ya National Service. National Service maana yake nini? Najua wote vijana mliofanya maandamano haya ya leo ya kuniunga mkono, na vijana wengine kadhalika, mnaelewa maana ya National Service na mkapinga fikara za kuikataa—ndiyo maana muko hapa. Mnapinga upuuzi ule wa jana. Lakini hata hivyo nataka kuwaelezeni ninyi na nchi nzima, National Service maana yake nini.
Wananchi National Service hatukuanzisha sisi. Mataifa mengi duniani yana National Service. Taifa linawaambia vijana wake: Tunataka vijana mlitumikie Taifa lenu. Taifa linadai utumishi toka kwa vijana. Linadai huduma kwa vijana. Na vijana wanaitika. Taifa linawadai huduma vijana na vijana wanaitika wito huo kwenda kulihudumia Taifa, kwa kazi yo yote ambayo Taifa linahitaji ifanywe. Narudia nikisema mipango kama hiyo hatukuanza sisi. Mataifa mengi duniani yana National Service.
Kwa desturi "National Service" au huduma wanayoitiwa vijana hawa wa mataifa haya mengine duniani, ni huduma ya kivita. Wanaitwa vijana wafundishwe kwa kazi ya kivita. Ikiwa kesho na kesho kutwa hapana budi basi waende wakapigane, waue au wauawe—hiyo ndiyo National Service ya kawaida katika mataifa mengine duniani. Na wanapoitwa jinsi hiyo wakaingia katika National Service, vijana hao wote wanafanywa ni sawa sawa. Atakuja mwingine labda ametolewa katika ualimu, mwingine labda alikuwa fundi chuma, mwingine labda ni daktari. Huyu udaktari wake kasomea miaka saba, yule ualimu wake akasomea miaka mitatu, na kadhalika, lakini wote hao watakapoingia katika kundi lile la National Service, wakishafika pale basi wote sawa. Wote wanakuwa ni askari wa kawaida, hakuna mmoja anayehesabiwa digrii, la; japokuwa aingie na digrii ishirini. Ukisha fika pale wewe, na mwingine wote ni praivet, yaani ni askari wa chini kabisa. Pengine unaweza ukaambiwa wewe ni mwalimu, kazi ako utafundisha, lakini utafundisha kama praivet, askari wa chini kabisa. Pengine wewe ni daktari ukaambiwa adhali umesomea udaktari, sasa kazi yako hapa jeshini itakuwa kutibu askari, lakini utatibu kama praivet, askari wa chini kabisa. Kama umepata bahati ya kumzidi mwenzio, ni kwa sababu katika hali yako ya u-National Service umefanywa koplo. Hapo utamzidi mwenzio. Ukifanywa sajin ndiyo kabisa. Lakini kama wewe si koplo, wala si sajin, wala si meja, hata ungekuwa na digrii thelathini, wewe ni praivet tu, na hali yako pale ni ya ki-praivet tu, askari wa chini kabisa. Ndiyo kawaida ya National Service.
National Service yetu.
Na sisi wananchi, tumeanzisha National Service hapa. Tunayo National Service; vijana wale mnawaona pale, ni vijana wa National Service. Tofauti ya kweli baina ya National Service yetu na zingine ni nini. Kwanza, ya kwetu si ya kivita; ni ya ujenzi. Tumewaita vijana waingie katika National Service, na kazi tutakayowapa ni ya ujenzi katika nchi. Wamekwisha anza na tunao, wengine karibu watamaliza miaka yao miwili. Tunawafanyaje mle katika National Service? Wanatumika sawasawa. Wameingia katika National Service mle, wote wamehesabiwa kuwa sawasawa. Kila mmoja anapata posho Sh. 20/- kwa mwezi na tumekuwa tukiwapa hivyo tangu wameanza, siyo kwamba tutakuja kuanza baadaye. Tumekwisha fanya hivyo kwa miaka miwili yote waliomo katika National Service. Lakini hapo walipo katika National Service wanapitana. Wachache ni "leader", yaani viongozi, na wengine ni National Service tu, bila jina la zaidi. Lakini wote wale ni National Service na waulizeni wenyewe kama katika kupitana huko kuna apataye zaidi; mimi sijui.
Nilikuwa pale Ruvu juzi nikiwakagua vijana wale wa kike na wa kiume, wanaomaliza miaka yao miwili. Wengine wananiuliza, "Mwalimu iko ruhusa tukimaliza miaka miwili turudie tena?" Hao wanafanya kazi yao ya National Service ya kawaida. Halafu tangu mwaka juzi, mara tu baada ya maasi yale ya askari, ikawa tumepitisha vijana wetu katika National Service, ndiyo wakachaguliwa kutoka katika National Service kuingia katika jeshi la ulinzi.
Jeshi la ulinzi hili la sasa ni la wananchi wa Tanzania. Wamo mle vijana wa National Service. Baadhi ya wale vijana wenu waliomo katika jeshi la ulinzi ni vijana wa National Service. Wengine karibu watamaliza miaka yao miwili. Kule tunawafanya wote sawa.
Hawapati mishahara.
Ijapokuwa kule kuna mishahara-shahara, praivet mshahara fulani, koplo mshahara fulani, sajin mshahara fulani, lakini tangu tangu tumeanza mpango huu mpya, wao wanapata 40 kwa mia tu ya mshahara ule. Hatuwatofautishi hawa kwa namna yo yote, madhali ni vijana wa National Service.
Vijana wenye elimu hawaji.
Lakini tuliona kwamba vijana waliokwisha kuingia katika National Service hivi sasa ni vijana ambao, au wana elimu ndogo, au hawakusoma kabisa, au hawana kazi, au hawakusomea kazi yo yote. Hao ndio wanaoingia katika National Service. Na National Service ni kazi ya vijana, ni mahali pa vijana kwenda kutumikia Taifa. Tukaona vijana wenye elimu hawaji. Waliosomea kazi maalum hawaji. Mwenye kitumbua na kazi yake mahali, haji. Tukaona kuwa jambo hili lina kasoro. Vipi waliokwisha tumikiwa vizuri sana na Taifa wao ndio hawaji kulihudumia Taifa katika National Service, ila wale ambao hawakugharimiwa na Taifa wao ndio wanakuja? Tuligundua kwamba mpango huu una walakini.
Mpango una walakini.
Kwa hiyo tukaanza kutafuta njia ya kuwaleta wenye elimu na wenye kazi, nao waje wakalihudumie Taifa. Tukaamua kupitisha sheria, kwamba kijana ye yote anayetoka akimaliza masomo yake katika shule hizi kubwa, au akishamaliza kusomea kazi yo yote, kabla hajaanza kazi yake kwanza atumike katika National Service. Tukasema, tutawatumikishaje hao vijana waliosoma? Tukasema tutafanya hivi, kwamba tutaugawa muda wao vijana hawa wa kuwa katika National Service. National Service yenyewe ni miezi ishirini na minne, yaani miaka miwili. Lakini tutaugawa muda huo katika sehemu mbili; miezi sita kijana atakuwa yumo katika kambi, pamoja na wenzake wote. Kama ni mwalimu, au ni daktari, au ni fundi wa aina yo yote, atakuwa katika kambi katika muda wa miezi sita pamoja na wenzake wengine wote. Anapata posho ya shilingi ishirini kwa mwezi. Halafu akishamaliza yale mafunzo yake ya miezi sita ya kambini atakwenda kufanya kazi yake ya kawaida kwa muda wa miezi kumi na minane iliyobaki. Kama ni mwalimu, atakwenda darasani kufundisha; kama ni fundi wa aina nyingine yo yote, atakwenda kufanya kazi yake; nasi tutaukubali ule udaktari, au ualimu wake kuwa kama ni kazi ya National Service. Tutahesabu ile miezi yake kumi na minane pale Muhimbili kwamba ile ni National Service. Ikiwa yuko Muhimbili anatibu sawa sawa kama daktari mwingine tutahesabu ile kazi yake katika muda wa miezi kumi na minane ya kuwa ni National Service.
Posho yao.
Tukasema, posho je! Muda ule wa miezi sita ya kwanza anapokua kambini atapata posho ya kawaida. Lakini atakapokuwa anafundisha darasani mtu huyu, posho yake iweje? Tukasema kama yuko darasani anafundisha, au ni daktari katika hospitali, au yuko mahala pengine tutampa posho yake namna hii. Kwanza tutampa kima cha chini cha mtumishi wa Serikali Dar es Salaam ambazo ni shilingi mia moja na themanini kwa mwezi, hizo tutazichukua tutaziweka kando, kuwa fungu lake la kwanza. Sh. 180/- ana hakika atazipata. Halafu mathalani kama ni mwalimu, tunajua mshahara wa mwalimu asiyekuwa National Service. Katika mshahara huo tunazitoa zile Sh. 180/-. Tukishaziondoa zile Sh. 180/- zile zilizobaki tunampa 40 kwa mia.
Kwa mfano. Mwalimu atakayemaliza masomo yake pale Chuo Kikuu, na ambaye siyo National Service, kwa kawaida ni shilingi 1,320/- kwa mwezi. Sasa akienda katika National Service tutampa nini? Kwanza kabisa tutampa Sh. 180/-. Halafu zile tunazitoa katika shilingi 1,320/-. Katika zile zinazobaki Sh.1, 140/-, tunampa 40 kwa mia yake, ambazo ni Sh. 456/-. Kwa hiyo, anapata kwanza 180/- halafu 456/-. Ukijumlisha utaona anapata 636/-, hii ndiyo posho yake atakapokuwa anatumika katika National Service.
Lakini haijatosha, haiishii hapo hapo tu. Tunampa kwanza Sh. 636/-, posho, mwalimu aliyemo katika National Service; halafu tunampa nyongeza ya kodi ya nyumba, ambayo itafika kiasi cha Sh. 132/-. Halafu tunampa nguo za National Service, wanasema hii ni kiasi cha Sh. 26/- kwa mwezi. Kwa hiyo kwa jumla mwalimu huyo anapata Sh. 794/-. Na hiyo ni posho ya kijana wa National Service kila mwezi. Tuseme Sh. 790/-.
Nataka muelewe wananchi, nataka muelewe nini wasilolitaka vijana hawa! Huyu analihudumia Taifa anapewa Sh. 790/- posho tu, na bado haijatosha; wananchi, bado haijatosha! Katika hizo Sh. 790/- anazopata hatumkati hata senti moja ya kodi, hatumkati kodi ila kama amenunua bia, maana katika kila chupa ya bia kuna kodi ya Serikali. Lakini bila hivyo Sh. 790/- za posho ya kijana wa National Service hizi haziguswi; ni posho siyo mshahara. Siyo mshahara maana siku hizi Tanzania kwa waheshimiwa kama wale, hakuna mishahara midogo ya namna hiyo? Hakuna!
Wananchi, hivyo ndiyo National Service tunayoisema, ambayo waheshimiwa hawa wanaikataa. Kijana atakwenda kambini miezi sita pamoja na wenzake. Atatoka pale atakwenda darasani au hospitali kwenda kufanya kazi yake. Kama ni mwalimu nasema atakuwa anapata kiasi cha Sh. 800/-, posho, hazikatwi kodi hizo. Hiyo na ule ualimu wake au uganga wake ndiyo tutakaoupokea, kwamba ndiyo huduma anayohudumia Taifa. Hatumpeleki vitani au kumwambia akachimbe mfereji—atafanya kazi yake ile ile aliyoisomea. Wala hatutamchukua huyu kijana kabla hajamaliza masomo yake. Tulisema tuache kwanza amalize masomo yake. Tungeweza tukamchukua kwanza akamaliza National Service yake halafu ndiyo akaenda kule kumaliza masomo yake, lakini tukasema hapana, tusimkatishe masomo yake. Acha asome amalize, halafu ndiyo akafanye National Service. . . . . . . . .
Oktoba 23, 1966.
Wananchi,
Jana tumefukuza wanafunzi wapatao 393 kutoka katika vyuo mbali mbali vya Dar es Salaam baada ya maandamano yao ya kupinga mpango wa Serikali wa National Service. Tumeamua vijana hao, waliokuja mpaka Ikulu wakipinga mpango wa National Service, na kusema maneno machafu- machafu, waondoke warudi majumbani kwao.
Wanafunzi gani.
Kwanza nataka kuwaambieni, wananchi, kwamba wanafunzi hao wametoka katika vyuo mbali mbali, na majina ya vyuo hivyo yametangazwa. Baadhi yao wametoka katika Chuo Kikuu pale mlimani, wengine wametoka katika Chuo kile cha Ufundi hapo nyuma yenu, wengine wametoka katika Chuo cha Madaktari kule Mhimbili, na wengine wametoka katika Chuo cha Waalimu, kule Chang'ombe. Vile vile kuna waliotoka katika Chuo cha Biashara hapo nyuma ya Chuo cha Ufundi na wachache wametoka katika shule za sekondari. Lakini walio wengi, zaidi ya nusu ya wote wale waliokuja Ikulu, na ndio tuliowaambia warudi majumbani kwao, wametoka katika Chuo Kikuu kule mlimani.
Walio wengi walikataa.
Nataka kueleza pia kwamba katika Chuo Kikuu wamebaki vijana wengine wa Kitanzania waliokataa kuwaunga mkono wenzao katika maandamano yale. Walio wengi walikataa. Katika chuo hiki hapa cha ufundi, walio wengi walikataa. Katika chuo cha waalimu cha Chang'ombe walio wengi walikataa. Katika vyuo hivyo vingine vyote nilivyovitaja, walio wengi walikataa. Nataka kuwapa pongezi vijana hao wa vyuo hivyo vyote ambao najua walishawishiwa na wenzao kwa kukataa kuingizwa katika maandamano ya kupinga National Service. Pia nawapa pongezi vijana wa shule za sekondari wote, sio wa hapa Dar es Salaam tu bali na wa shule za sekondari za Tanzania nzima kwa kukataa kuingia katika jambo hili baya. Wengine nimesema nao mimi mwenyewe, na wengine wamehutubiwa na wenzangu Mawaziri, nao hawakubali upuuzi huu ambao umekaa miezi mingi sana katika Chuo chetu Kikuu. Jana upuuzi ule ukadhihirika uwanjani kule Ikulu.
Maana ya "National Service".
Vijana walikuja Ikulu kuja kupinga mpango wa National Service. Wananchi sasa nataka kuwaelezeni kwa utaratibu kadiri nitakavyoweza maana ya National Service. National Service maana yake nini? Najua wote vijana mliofanya maandamano haya ya leo ya kuniunga mkono, na vijana wengine kadhalika, mnaelewa maana ya National Service na mkapinga fikara za kuikataa—ndiyo maana muko hapa. Mnapinga upuuzi ule wa jana. Lakini hata hivyo nataka kuwaelezeni ninyi na nchi nzima, National Service maana yake nini.
Wananchi National Service hatukuanzisha sisi. Mataifa mengi duniani yana National Service. Taifa linawaambia vijana wake: Tunataka vijana mlitumikie Taifa lenu. Taifa linadai utumishi toka kwa vijana. Linadai huduma kwa vijana. Na vijana wanaitika. Taifa linawadai huduma vijana na vijana wanaitika wito huo kwenda kulihudumia Taifa, kwa kazi yo yote ambayo Taifa linahitaji ifanywe. Narudia nikisema mipango kama hiyo hatukuanza sisi. Mataifa mengi duniani yana National Service.
Kwa desturi "National Service" au huduma wanayoitiwa vijana hawa wa mataifa haya mengine duniani, ni huduma ya kivita. Wanaitwa vijana wafundishwe kwa kazi ya kivita. Ikiwa kesho na kesho kutwa hapana budi basi waende wakapigane, waue au wauawe—hiyo ndiyo National Service ya kawaida katika mataifa mengine duniani. Na wanapoitwa jinsi hiyo wakaingia katika National Service, vijana hao wote wanafanywa ni sawa sawa. Atakuja mwingine labda ametolewa katika ualimu, mwingine labda alikuwa fundi chuma, mwingine labda ni daktari. Huyu udaktari wake kasomea miaka saba, yule ualimu wake akasomea miaka mitatu, na kadhalika, lakini wote hao watakapoingia katika kundi lile la National Service, wakishafika pale basi wote sawa. Wote wanakuwa ni askari wa kawaida, hakuna mmoja anayehesabiwa digrii, la; japokuwa aingie na digrii ishirini. Ukisha fika pale wewe, na mwingine wote ni praivet, yaani ni askari wa chini kabisa. Pengine unaweza ukaambiwa wewe ni mwalimu, kazi ako utafundisha, lakini utafundisha kama praivet, askari wa chini kabisa. Pengine wewe ni daktari ukaambiwa adhali umesomea udaktari, sasa kazi yako hapa jeshini itakuwa kutibu askari, lakini utatibu kama praivet, askari wa chini kabisa. Kama umepata bahati ya kumzidi mwenzio, ni kwa sababu katika hali yako ya u-National Service umefanywa koplo. Hapo utamzidi mwenzio. Ukifanywa sajin ndiyo kabisa. Lakini kama wewe si koplo, wala si sajin, wala si meja, hata ungekuwa na digrii thelathini, wewe ni praivet tu, na hali yako pale ni ya ki-praivet tu, askari wa chini kabisa. Ndiyo kawaida ya National Service.
National Service yetu.
Na sisi wananchi, tumeanzisha National Service hapa. Tunayo National Service; vijana wale mnawaona pale, ni vijana wa National Service. Tofauti ya kweli baina ya National Service yetu na zingine ni nini. Kwanza, ya kwetu si ya kivita; ni ya ujenzi. Tumewaita vijana waingie katika National Service, na kazi tutakayowapa ni ya ujenzi katika nchi. Wamekwisha anza na tunao, wengine karibu watamaliza miaka yao miwili. Tunawafanyaje mle katika National Service? Wanatumika sawasawa. Wameingia katika National Service mle, wote wamehesabiwa kuwa sawasawa. Kila mmoja anapata posho Sh. 20/- kwa mwezi na tumekuwa tukiwapa hivyo tangu wameanza, siyo kwamba tutakuja kuanza baadaye. Tumekwisha fanya hivyo kwa miaka miwili yote waliomo katika National Service. Lakini hapo walipo katika National Service wanapitana. Wachache ni "leader", yaani viongozi, na wengine ni National Service tu, bila jina la zaidi. Lakini wote wale ni National Service na waulizeni wenyewe kama katika kupitana huko kuna apataye zaidi; mimi sijui.
Nilikuwa pale Ruvu juzi nikiwakagua vijana wale wa kike na wa kiume, wanaomaliza miaka yao miwili. Wengine wananiuliza, "Mwalimu iko ruhusa tukimaliza miaka miwili turudie tena?" Hao wanafanya kazi yao ya National Service ya kawaida. Halafu tangu mwaka juzi, mara tu baada ya maasi yale ya askari, ikawa tumepitisha vijana wetu katika National Service, ndiyo wakachaguliwa kutoka katika National Service kuingia katika jeshi la ulinzi.
Jeshi la ulinzi hili la sasa ni la wananchi wa Tanzania. Wamo mle vijana wa National Service. Baadhi ya wale vijana wenu waliomo katika jeshi la ulinzi ni vijana wa National Service. Wengine karibu watamaliza miaka yao miwili. Kule tunawafanya wote sawa.
Hawapati mishahara.
Ijapokuwa kule kuna mishahara-shahara, praivet mshahara fulani, koplo mshahara fulani, sajin mshahara fulani, lakini tangu tangu tumeanza mpango huu mpya, wao wanapata 40 kwa mia tu ya mshahara ule. Hatuwatofautishi hawa kwa namna yo yote, madhali ni vijana wa National Service.
Vijana wenye elimu hawaji.
Lakini tuliona kwamba vijana waliokwisha kuingia katika National Service hivi sasa ni vijana ambao, au wana elimu ndogo, au hawakusoma kabisa, au hawana kazi, au hawakusomea kazi yo yote. Hao ndio wanaoingia katika National Service. Na National Service ni kazi ya vijana, ni mahali pa vijana kwenda kutumikia Taifa. Tukaona vijana wenye elimu hawaji. Waliosomea kazi maalum hawaji. Mwenye kitumbua na kazi yake mahali, haji. Tukaona kuwa jambo hili lina kasoro. Vipi waliokwisha tumikiwa vizuri sana na Taifa wao ndio hawaji kulihudumia Taifa katika National Service, ila wale ambao hawakugharimiwa na Taifa wao ndio wanakuja? Tuligundua kwamba mpango huu una walakini.
Mpango una walakini.
Kwa hiyo tukaanza kutafuta njia ya kuwaleta wenye elimu na wenye kazi, nao waje wakalihudumie Taifa. Tukaamua kupitisha sheria, kwamba kijana ye yote anayetoka akimaliza masomo yake katika shule hizi kubwa, au akishamaliza kusomea kazi yo yote, kabla hajaanza kazi yake kwanza atumike katika National Service. Tukasema, tutawatumikishaje hao vijana waliosoma? Tukasema tutafanya hivi, kwamba tutaugawa muda wao vijana hawa wa kuwa katika National Service. National Service yenyewe ni miezi ishirini na minne, yaani miaka miwili. Lakini tutaugawa muda huo katika sehemu mbili; miezi sita kijana atakuwa yumo katika kambi, pamoja na wenzake wote. Kama ni mwalimu, au ni daktari, au ni fundi wa aina yo yote, atakuwa katika kambi katika muda wa miezi sita pamoja na wenzake wengine wote. Anapata posho ya shilingi ishirini kwa mwezi. Halafu akishamaliza yale mafunzo yake ya miezi sita ya kambini atakwenda kufanya kazi yake ya kawaida kwa muda wa miezi kumi na minane iliyobaki. Kama ni mwalimu, atakwenda darasani kufundisha; kama ni fundi wa aina nyingine yo yote, atakwenda kufanya kazi yake; nasi tutaukubali ule udaktari, au ualimu wake kuwa kama ni kazi ya National Service. Tutahesabu ile miezi yake kumi na minane pale Muhimbili kwamba ile ni National Service. Ikiwa yuko Muhimbili anatibu sawa sawa kama daktari mwingine tutahesabu ile kazi yake katika muda wa miezi kumi na minane ya kuwa ni National Service.
Posho yao.
Tukasema, posho je! Muda ule wa miezi sita ya kwanza anapokua kambini atapata posho ya kawaida. Lakini atakapokuwa anafundisha darasani mtu huyu, posho yake iweje? Tukasema kama yuko darasani anafundisha, au ni daktari katika hospitali, au yuko mahala pengine tutampa posho yake namna hii. Kwanza tutampa kima cha chini cha mtumishi wa Serikali Dar es Salaam ambazo ni shilingi mia moja na themanini kwa mwezi, hizo tutazichukua tutaziweka kando, kuwa fungu lake la kwanza. Sh. 180/- ana hakika atazipata. Halafu mathalani kama ni mwalimu, tunajua mshahara wa mwalimu asiyekuwa National Service. Katika mshahara huo tunazitoa zile Sh. 180/-. Tukishaziondoa zile Sh. 180/- zile zilizobaki tunampa 40 kwa mia.
Kwa mfano. Mwalimu atakayemaliza masomo yake pale Chuo Kikuu, na ambaye siyo National Service, kwa kawaida ni shilingi 1,320/- kwa mwezi. Sasa akienda katika National Service tutampa nini? Kwanza kabisa tutampa Sh. 180/-. Halafu zile tunazitoa katika shilingi 1,320/-. Katika zile zinazobaki Sh.1, 140/-, tunampa 40 kwa mia yake, ambazo ni Sh. 456/-. Kwa hiyo, anapata kwanza 180/- halafu 456/-. Ukijumlisha utaona anapata 636/-, hii ndiyo posho yake atakapokuwa anatumika katika National Service.
Lakini haijatosha, haiishii hapo hapo tu. Tunampa kwanza Sh. 636/-, posho, mwalimu aliyemo katika National Service; halafu tunampa nyongeza ya kodi ya nyumba, ambayo itafika kiasi cha Sh. 132/-. Halafu tunampa nguo za National Service, wanasema hii ni kiasi cha Sh. 26/- kwa mwezi. Kwa hiyo kwa jumla mwalimu huyo anapata Sh. 794/-. Na hiyo ni posho ya kijana wa National Service kila mwezi. Tuseme Sh. 790/-.
Nataka muelewe wananchi, nataka muelewe nini wasilolitaka vijana hawa! Huyu analihudumia Taifa anapewa Sh. 790/- posho tu, na bado haijatosha; wananchi, bado haijatosha! Katika hizo Sh. 790/- anazopata hatumkati hata senti moja ya kodi, hatumkati kodi ila kama amenunua bia, maana katika kila chupa ya bia kuna kodi ya Serikali. Lakini bila hivyo Sh. 790/- za posho ya kijana wa National Service hizi haziguswi; ni posho siyo mshahara. Siyo mshahara maana siku hizi Tanzania kwa waheshimiwa kama wale, hakuna mishahara midogo ya namna hiyo? Hakuna!
Wananchi, hivyo ndiyo National Service tunayoisema, ambayo waheshimiwa hawa wanaikataa. Kijana atakwenda kambini miezi sita pamoja na wenzake. Atatoka pale atakwenda darasani au hospitali kwenda kufanya kazi yake. Kama ni mwalimu nasema atakuwa anapata kiasi cha Sh. 800/-, posho, hazikatwi kodi hizo. Hiyo na ule ualimu wake au uganga wake ndiyo tutakaoupokea, kwamba ndiyo huduma anayohudumia Taifa. Hatumpeleki vitani au kumwambia akachimbe mfereji—atafanya kazi yake ile ile aliyoisomea. Wala hatutamchukua huyu kijana kabla hajamaliza masomo yake. Tulisema tuache kwanza amalize masomo yake. Tungeweza tukamchukua kwanza akamaliza National Service yake halafu ndiyo akaenda kule kumaliza masomo yake, lakini tukasema hapana, tusimkatishe masomo yake. Acha asome amalize, halafu ndiyo akafanye National Service. . . . . . . . .