Riwaya: Mkimbizi

Riwaya: Mkimbizi

SEHEMU YA KUMI NA MOJA

“Hallow Tigga...” Alinisemesha huku akitabasamu na akinitazama kwa makini. Sikuwa na la kusema. Nilimeza funda kubwa la mate na kutembeza macho yangu mle ndani. Nilikuwa nimenasa. Hakukuwa na namna yoyote ya kutoroka kutoka mle ndani. Nilimtazama Kelvin.
“Ah! Dokta Lundi..umefika hatimaye...” Alisema kumuambia yule mtu aliyejiita Dokta Martin Lundi. Badala ya kumjibu, Dokta Martin Lundi alinikazia macho yake ya kuogofya na kuniuliza.
“Oke Tigga, ni ushahidi gani huo unaodai kuwa unao?”
Nilibaki nikimkodolea macho kwa mshangao. Nikamtazama Kelvin, naye alionekana kushangaa tu. Alimtazama yule muuaji aliyeamini kuwa ni tabibu, kisha akanitazama, akamtazama tena yule muuaji.
“Eeh...dokta, sijui mnatarajia kufanyia wapi hayo matibabu...” Kelvin alimuuliza Martin Lundi muongo kwa mashaka kidogo.
“Huyo sio daktari Kelvin! Ni muuaji huyo!” Nilibwatuka kwa hasira. Dokta Lundi alitoa tabasamu lake baya kabla ya kusema, “Tigga, Tigga, Tigga...usiwe na wasiwasi, nitakupatia dawa sasa hivi na utajisikia vizuri tu...”
Ingawa nilikuwa nimejawa na woga usio kifani, nilijikuta nikimbetulia midomo kwa kukereka na kumtupia swali.
“Kwa hiyo sasa nimekuwa Tigga na sio Sylvia tena, eenh? Hivi unadhani unamlaghai nani hapa wewe?”
Yule dokta laghai alijitia kutikisa kichwa kwa huzuni huku akinitazama kwa makini. Kelvin alionekana kutoelewa afanye nini. Dokta Lundi alinisogelea taratibu huku wale watu wake wawili wakijizatiti mlangoni ili nisijaribu kutimua mabio. Na kwa hakika nilikua nimekwama. Nilijilazimisha kufikiria jinsi ya kujiokoa sikupata jibu. Niliufikiria ule mkanda wa video na nikajihisi kizunguzungu. Ikiwa watafanikiwa kunipokonya ule ushahidi, basi nimekwisha.
“Mnh! Paranoid Schizo...” Dokta Lundi alianza kusema uongo wake huku akinisogelea lakini sikumpa nafasi.
“Toka na uzushi wako hapa! Hakuna cha Paranoid Schizo-nini wala nini hapa! Uongo mtupu! Na wewe unajua hilo! Mimi ni mtu na akili zangu na nimewaona mkiua mtu, na najua kuwa ndio mliowaua wenzangu kule msituni...sasa mnanitaka na mimi kwa kujitia eti madaktari, kwenda zako huko!” Nilimbwatukia kwa kelele huku nikirudi nyuma.
Dokta Lundi alighadhibika na kunitolea macho. “We’ Tigga...” Alianza kunikemea, lakini nilimkatisha tena.
“Utawadanganya hao hao lakini sio mimi...kaa mbali nami!” Nilimwambia huku nikimwoneshea Kelvin aliyekuwa akizidi kushangaa. Sijui ilikuwaje hata nikapendana na jitu bwege kama hili!
“Tigga ana ushahidi kuwa mliua mtu Dokta...nadhani labda tungehakikisha juu ya hilo kabla hamjamchukua...” Kelvin aliropoka kwa kitetemeshi.
“Sawa kabisa Kelvin...Tigga, hebu tuoneshe huo ushahidi wako!” Dokta Lundi aliniambia huku akizidi kunisogelea na uso wake ukionesha mashaka, kama kwamba anajishauri iwapo aamini kuwa inawezekana nikawa kweli na kitu kama hicho au la. Nilitazama huku na huko sikuona pa kukimbilia.
“Ah! Tangu lini mwehu...Paranoid Schizo-nini sijui huko, akawa na ushahidi wa kumtia wasiwasi mtu mwenye akili timamu kama wewe dokta? Mi’ si mwehu bwana? Then why are you so worried about my evidence, eenh?” Nilimuuliza huku nikizidi kurudi nyuma, nikimaanisha kwa nini ushahidi wangu uwatie hofu wakati wanajua kabisa kuwa mimi ni mwehu. Niligota ukutani. Dokta Lundi alitoa amri na kwa hatua moja kubwa mmoja wa wale vibaraka wake alinirukia pale nilipokuwa. Nilipiga yowe huku nikiruka pembeni lakini yule jamaa alikuwa mwepesi. Alinidaka na kunikamata mikono yangu kwa nguvu. Nilimpiga teke la ugoko, akaguna kwa maumivu na kulegeza mikono yangu. Nikamchapa kofi la uso. Kelvin aliropoka neno, Dokta Lundi akamfokea. Yule jamaa alinichapa kofi kali sana la uso lililonipeleka chali kitandani kwa Kelvin na kunigaragaza mpaka upande wa pili wa kitanda, huku mkoba wangu ukianguka sakafuni.
Nilijiinua huku nikisikia kizunguzungu kutoka nyuma ya kitanda na kujikuta nikikamatwa kwa nguvu na wale wasaidizi wa Martin Lundi ambao waliniinua mzima mzima na kunikalisha kwenye kochi lililokuwa mle ndani. Nilihisi mchirizi wa damu ukinichuruzika kutoka puani kutokana na kofi lile. Nilitoa ulimi wangu kuramba eneo nililohisi kuwa lina damu juu ya mdomo wangu na nikahisi ladha ya chumvi-chumvi.
“Heey! Sasa mbona mnampiga? Hivi ndivyo mnavyo wahudumia wagonjwa nyie!” Kelvin aliwafokea wale watu na kumtazama Dokta Lundi ambaye alikuwa akinitazama kwa hasira bila ya kusema neno.
“Dokta! Ongea na watu wako! Hawawezi kumfanya hivi mchumba wangu hata kama ni mgonjwa wa akili...”
“Mimi sio mchumba wako Kelvin, na wala sio mgonjwa! Haya ndio uliyoyataka, sasa unalalama nini? Kwa nini hukutaka kuniamini tangu mwanzo...”
“Kelele!” Dokta Lundi alifoka.
“Ebbo! Yaani mnakuja kunitolea amri nyumbani kwangu? Haiwe....” Kelvin alianza kumaka, lakini Dokta Lundi alimchapa kofi la uso lililompeleka mpaka ukutani.
“Shut Up!”
Na hapo hapo mmoja wa wale wasidizi wa Martin Lundi alimrukia na kumkamata mikono kwa nyuma. Ikawa sote tumeshikwa na wale wasaidizi wa Martin Lundi.
Nilimtazama Kelvin kwa kukata tamaa. Alibaki akitembeza macho huku na huko asijue afanye nini.
“Unasema ulituona tukiua mtu?” Martin Lundi aliniuliza nikiwa nimebanwa na yule msaidizi wake pale kwenye kiti. Sikumjibu. Alinipiga kofi la shavu lililotia vimulimuli machoni mwangu. Kelvin aliropoka kitu, lakini sikuelewa ni kitu gani. Nilimtazama yule muuaji kwa ghadhabu.
“Ndio, nimewaona! Wewe pamoja na mwenzako mwenye mguu mbovu na mwingine mwenye macho kama nyoka! Mlikuja na helikopta na wewe ndio ulikuwa ukiendesha, uongo?” Nilimtemea yale maneno kwa hasira. Jamaa alinitazama bila ya kusema neno lakini niliona kuwa uso wake ulibadilika na aliamini kuwa nilikuwa nasema kweli.
“Uongo?” Nilimuuliza tena. Nilipigwa kofi jingine kali la uso lililotawanya maumivu makali usoni mwangu, na nililia kwa uchungu.Lakini sikukata tamaa.
“Kwa nini mlimuua yule mtu Lundi? Au na yeye alikataa kukubali kuwa ni mgonjwa wa akili kama mimi?” Nilizidi kumkemea kwa hasira yule muuaji muongo.
“Hah! Ni kweli hayo maneno Dokta?” Kelvin aliropoka kutoka kule alipokuwa ameshikiliwa na yule kibaraka mwingine. Dokta Lundi alimwendea kwa kasi na kumtamdika ngumi ya uso huku akimkemea.
“Hebu Nyamaza wewe!”
Alinirudia pale nilipokuwa nimeshikiliwa kwenye kiti na kuniuliza. “Na unasema kuwa una ushahidi wa tukio hilo?”
“Kwa hiyo ni kweli?” Kelvin aliuliza kwa kihoro huku akimkodolea macho yule daktari bandia, damu ikimchuruzika kutoka kwenye kona ya mdomo wake.
“Nina ushahidi wa mkanda wa video!” Nilimtemea tena maneno kwa hasira huku nikimsogezea uso wangu kwa kumsuta. Hapo hapo alibamiza kofi jingine kali la uso na kunidaka koo kabla sijataharuki. Kelvin alijikurupusha kutoka kule alipokuwa ameshikwa lakini niliona kuwa yule mtu aliyemshika alikuwa amemzidi nguvu. Alianza kupiga kelele lakini haraka jamaa alimbana koo na kumzuia kupiga kelele.
“Nautaka huo ushahidi sasa hivi!” Dokta Lundi muongo aliniambia kwa hasira. Nilimtazama kwa kiburi bila ya kusema neno. Alizidi kunitazama kwa ghadhabu.
“Au unadanganya wewe? Huna cha ushahidi wala nini...!” Aliniambia huku bado akiwa amenikaba.
“Mimi sio muongo kama wewe! Lakini kwa kukuridhisha tu, tufanye ninakudanganya na wala sijawaona mkishuhudia wakati bastola ya macho ya nyoka ilipoutoa uhai wa yule mtu kule msituni, na wala sina ushahidi wowote!” Nilimjibu. Dokta Martin Lundi alichanganyikiwa kwa jibu hili. Alinitazama halafu akamgeukia Kelvin, kisha akanitazama tena.
“We’ unao ushahidi, uko wapi?” Alisema na kuniuliza kwa jazba. Nilimchekea mbele ya uso wake bila ya kumjibu. Yule kibaraka wake alinibamiza kofi la kichwa, na hapo hapo Dokta Lundi aliniinua na kunibamiza ukutani huku akiwa bado amenikaba koo.
“Tuoneshe huo mkanda sasa hivi!” Alinifokea. Sikumjibu. Alimuamrisha yule msaidizi wake anikamate, naye akaunyakua ule mkoba wangu na kumimina vitu vyote vilivyokuwa ndani yake juu ya kitanda. Aliiona ile video kamera ya Gil. Aliokota kile kisu kidogo nilichonunua kwenye treni na kukitazama, kisha akanitazama.
“Unatembea na visu mwanamke? Kwa hakika wewe ni muuaji!” Alisema kwa kebehi. Kisha aliichukua ile kamera na kuanza kuitazama taratibu, akiigeuza huku na huko. Moyo ulikuwa ukinidunda vibaya sana na watu wote mle ndani walibaki kimya. Nilimtazama Kelvin na nikaona kuwa alikuwa akiikodolea macho ile kamera kama kwamba ilikuwa ndio tegemeo pekee la kuokoa maisha yake. Muda huu yule jamaa aliyekuwa amemkaba alikuwa amelegeza kabali, naye akaropoka.
“Kumbe ni kweli...!”
Akili ilikuwa ikinitembea haraka sana. Niliangaza mle ndani nikitazama uwezekano wa kujiokoa. Ulikuwa mdogo sana.
Mtu aliyejiita Dokta Martin Lundi alifungua sehemu ya kuingizia mkanda kwenye ile kamera na kutazama ndani yake, na wote mle ndani wakawa wanamtazama yeye.
Hamna mkanda!
Aliinua uso wake kwa ghadhabu na kunitazama.
“Hamna mkanda wa video humu!” Aliniambia kwa ghadhabu.
“Ulitegemea nini Dokta Martin Lundi?” Nilimuuliza kwa kejeli.
“Kwa hiyo hamna ushahidi wa mkanda?” Aliniuliza.
“Sijui, we’ si ndio dokta bwana! Unajua kila kitu. Hadi umeweza kujua kuwa mimi ni mwehu bila hata ya mi’ mwenyewe kujua...” Nilitoa majibu ya kejeli huku akilini nikitafuta namna ya kujiokoa.
Dokta Lundi alipekua kwenye rundo la vitu vilivyotoka kwenye mkoba wangu akitafuta mkanda wa video asiupate. Alitoa bastola na kunigeukia kwa ghadhabu. Kelvin aliguna kwa woga baada ya kuona ile bastola.
“Where is the tape?” Aliniuliza kwa hasira. Nilijua pale nikizidisha jeuri yule mtu angeweza kuniua kweli. Njia pekee ilikuwa ni kuendelea kumfanya yeye ahitaji ule mkanda kutoka kwangu.
“Mkanda ninao na nimeuficha...” Nilipigwa kofi jingine na kujipigiza kisogo changu ukutani. Yowe la uchungu lilinitoka.
“Umeuficha wapi mwanamke?”
“Nimeukabidhi kwa wakili, akiwa na melekezo kuwa auwakilishe kwenye vyombo vya dola na vituo vya televisheni iwapo nitashindwa kuwasiliana naye kwa siku mbili mfululizo, au nitakapofikwa na umauti kwa namna yoyote ile.” Nilimjibu kwa kujiamini huku nikimtazama usoni.
Jamaa alichanganyikiwa.
“Muongo mkubwa! Where is the tape?” Alibwata akisisitiza nimwambie ni wapi ulipo ule mkanda wa video huku akiniwekea bastola yake kwenye paji la uso.
“Mimi sio muongo kama wewe! Huo ndio ukweli, kama huamini basi...fanya utakalo!”
“N’takuua wewe!”
“Kwani hiyo si ndio kazi yako? Nimeshuhudia kwa macho yangu kule porini, na wakili wangu ameshuhudia hilo kupitia kwenye ule mkanda wa video niliomkabidhi.”
Kelvin alicharuka.
“Kumbe nyie ni wauaji! Niacheni! Niacheni!” Alijikurukupusha na kumsukuma yule mtu aliyemkamata. Jamaa alipambana naye kwa muda na kufanikiwa kumbwaga chini na kumbana sakafuni.
“Hapana. Huo mkanda uko humu humu ndani...” Martin Lundi alisema, na kumgeukia yule kibaraka aliyekuwa amenishika mimi, ”...hebu pekua humu ndani mpaka uupate!” Aliamrisha. Kiza kilikuwa kimeanza kuingia, na yule jamaa aliwasha taa za mle ndani na kuanza kupekua. Alipekua kila mahali huku Kelvin akilalamika akiwa amebanwa sakafuni jinsi vitu vyake vilivyokuwa vikitupwa tupwa hovyo mle ndani. Jamaa alipekua kila mahali. Kabati lilichambuliwa hovyo hovyo, chini ya kitanda, bafuni, akatoka na kuingia jikoni, sebuleni.
Alirudi bila mafanikio.
“Mkanda uko wapi we’ binti?” Aliuliza Martin Lundi.
“Kama nilivyokuambia. Kwa wakili wangu.”
Alitikisa kichwa kwa masikitiko.
“Twende kwa wakili wako!” Aliniamrisha.
“Mnh! We’ unadhani mi’ mwehu kama unavyonipakazia?Itabidi uniue kwanza ndio nikupeleke huko kwa wakili wangu, na ukiniua taarifa zitatapakaa kwenye vyombo vya habari kama mvua!”
Alinipiga kofi kali la mdomo. Na wakati huo huo Kelvin alipata upenyo, kwani alimtupa pembeni yule jamaa aliyekuwa amembana pale chini na kusimama. Jamaa alijitahidi kumkamata tena lakini Kelvin alimwahi na kumsukumia teke la kifuani lililomtupa ukutani. Kisha akamrukia Dokta Lundi huku akipiga kelele za ghadhabu. Dokta Lundi aligeuka akitanguliza bastola yake, nami niliruka pembeni na kufyatua ile swichi ya kuwashia feni.
Mlio wa bastola ulivuma ndani ya kile chumba na kiza kikatawala ghafla kikiambatana na yowe la uchungu kutoka kwa Kelvin. Nilijitupa sakafuni na kujibiringishia chini ya kitanda wakati wale wauaji wakipiga kelele za kuchanganyikiwa.
“Washa taa!” Dokta Lundi alibwata, lakini mmoja wa watu wake alipiga kelele kuwa ni kiza nyumba yote.
“Pumbavu! Yuko wapi mwanamke!”
Nilisikia Kelvin alikilia kwa maumivu na nikaingiwa na woga mkubwa. Bila shaka alikuwa amejeruhiwa na bastola ya Dokta Lundi.
Oh! Mungu, Ni mabalaa mpaka lini sasa?
Na mara nilisikia kelele kutokea kule nje.
“Kelvin! Kelvin! Fungua! Sasa mbona umefyatua hiyo swichi tena?”
Ilikuwa ni sauti kutokea nje ya nyumba! Ndio kitu nilichokuwa nakitarajia. Nikiwa nimejilaza chini ya uvungu nilinyamaza kimya nikisikiliza. Ilikuwa ni heka heka mle ndani wakati wale wauaji wakikimbia hovyo huku na kule.
“Twendeni! Kuna watu wanakuja...Shit!”
“Sasa huyu mwanamke?”
“Tutampata tu...Let’s Go!”
Nilisikia vishindo vyao vikitoka nje ya chumba, na huko sebuleni nilisikia kelele nyingine, bila shaka walikutana na watu waliokuwa wanaingia sebuleni kwa Kelvin kuja kujaribu kurekebisha hitilafu ya umeme.
“Heyy! Nyie nani...”
“Toka!”
“Yallaaaa! Wezii!”
“Ohh! Shiit! Let’s Gooooooo!”
Nilisikia vishindo na mikiki mikiki huko nje, na wakati huo huo Kelvin alizidi kulia mle ndani. Nilitoka kule uvunguni na kumuendea pale niliposikia sauti yake ikitokea.
“Kelvin! Kelvin...? Vipi?” Nilimsogelea huku nikipapasa kutokana na kiza.
“Wamenipiga risasi! Nakufa Tigga....sa...sama...hani kwa kuto...kuamini!”
“Aaaah! Kelvin! Nyamaza ngoja nitafute msaada...”
“Nenda Tigga! Wata...rudi! Mi’ nakufaaaa!”
Hii nini tena sasa?
Nilisikia mlipuko wa bastola huko nje na nikaruka kwa mshituko huku yowe likinitoka. Watu walipiga mayowe huko nje.
“Nenda Tigga!”
Nilikurupuka bila ya kujijua. Nilikimbilia kwenye kitanda cha Kelvin na kutoa tochi niliyojua kuwa huwa inakaa kwenye droo ya kando ya kitanda kile. Niliwasha tochi ile na kuvikusanya vitu vyangu haraka haraka na kuvitia kwenye mkoba wangu, pamoja na ile kamera ya Gil. Nilikimbilia bafuni kwa Kelvin na tochi mkononi. Niliichukua sabuni kubwa aina ya Geisha ambayo Kelvin hupenda kuongea na kuitumbukiza kwenye mkoba ule na kutoka mbio. Kelvin alikuwa akigaragara pale sakafuni huku damu ikimvuja ingawa sikuweza kujua jeraha lilikuwa wapi hasa. Huko nje nilisikia gari ikitia moto na kuondoka kwa kasi. Nilimuinamia Kelvin na kutaka kumsemesha, lakini alinihimiza niondoke.
“Go Tigga...watu watajaa sasa hivi!”
Na hata aliposema maneno yale, nilianza kusikia ving’ora vya gari ya polisi kwa mbali.
“Iam so sorry dear!” Nilisema kwa sauti ya chini na kuiacha ile tochi ikiwaka mle ndani kando ya Kelvin nami nikatoka mbio nje ya nyumba ile huku nikitiririkwa na machozi nikiwa na mkoba wangu mgongoni.

***DUH!
 
SEHEMU YA KUMI NA MBILI

Na hata aliposema maneno yale, nilianza kusikia ving’ora vya gari ya polisi kwa mbali.
“Iam so sorry dear!” Nilisema kwa sauti ya chini na kuiacha ile tochi ikiwaka mle ndani kando ya Kelvin nami nikatoka mbio nje ya nyumba ile huku nikitiririkwa na machozi nikiwa na mkoba wangu mgongoni.

PEKE YANGU

Nilikurupuka kutoka usingizini huku nikipiga yowe kubwa. Niliketi kitandani na kuangaza huku na huko ndani ya chumba ambacho kilikuwa kigeni kwangu. Jasho lilikuwa likinitoka na koo lilinikauka. Ilikuwa ni ndoto ya kutisha iliyojumuisha matukio ya kuogofya niliyoyaona kule msituni siku si nyingi zilizopita ambayo ilinifanya nikurupuke namna ile kutoka usingizini. Kwa sekunde kadhaa nilizidi kuduwaa pale kitandani bila ya kujua nilikuwa wapi na nilifikaje mahala pale, kisha nikakumbuka. Niliteremka kutoka kitandani na kuelekea juu ya meza iliyokuwamo mle ndani na kuchukua chupa ya maji ya Uhai na kuyabugia kwa pupa. Nilirudi na kuketi kitandani na kuitafakari ile ndoto.
Niliota matukio ya kule msituni na jinsi nilivyokuwa nikihangaika kuifukuza ile midege iliyokuwa ikiwadonoa wale wenzangu waliouawa kule msituni, na nilipokuwa nikiwafukuza, mmoja wa midege ile alikuwa ameng’ang’ana kuudonoa uso wa bwana Ubwa Mgaya, ila nilipomsogelea, bwana Ubwa Mgaya aligeuka na kuwa Kelvin.
Oh! Mungu wangu!
Nilimfikiria Kelvin na moyo ulianza kunipiga kwa nguvu. Sijui ana hali gani huko aliko! Bila shaka atakuwa amekufa, kwani nilimwacha bila msaada wowote...
Lakini kwa nini hukutaka kuniamini Kelvin?
Nilipotoka mbio pale nyumbani kwa Kelvin sikuwa na uelekeo maalum na sikujua nilikuwa nakimbilia wapi. Ila kitu kilichonisaidia ni kuwa kule nje kulikuwa kuna mtafaruku mkubwa uliotokana na ule mlipuko wa risasi kutoka kwenye bastola ya wale wauaji niliofanikiwa kuwakurupusha kwa kutawanya kiza katika nyumba ile. Nilitoka mbio kwa muda mfupi na nilipopotelea mtaa wa pili tu nilianza kutembea haraka haraka huku nikilia peke yangu kwa kwikwi. Kiza kilikuwa kimeingia na eneo la sinza ndio lilikuwa linaamka. Watu walikuwa wamejaa katika mabaa mengi yaliyotapakaa eneo lile huku muziki ukisikika kutoka kila kona.
Nilikuwa nimechanganyikiwa vibaya sana, na nilijaribu kufikiri ni kitu gani nilitakiwa kufanya lakini iliniwia vigumu sana. Akili ilikuwa imekufa ganzi. Nilijilazimisha kuogopa swala la Kelvin kupigwa risasi na wale wauaji, lakini cha ajabu nilijikuta siogopi kabisa. Hisia zote zilikuwa zimekufa ganzi.
Nilizidi kukata mitaa ya sinza bila ya kujijua hadi nilipojihisi kuchoka. Niliangallia saa yangu ikaniambia muda ulikuwa ni saa tatu kasoro robo za usiku.
Sasa niende wapi Mungu wangu saa hizi!
Nilijua kuwa kwa hali iliyofikia, nilitakiwa kuripoti kituo chochote cha polisi kujisalimisha na kupata msaada. Lakini kila nilipokumbuka maelezo ya Kelvin kuwa Dokta Lundi alifika ofisini na hatimaye nyumbani kwake akiwa na askari wa jeshi la polisi, niliingiwa woga na wasiwasi mkubwa iwapo huko nitapata msaada ninaouhitaji. Kwa kadiri nilivyoelewa, pamoja na kuwa nawindwa kwa nguvu sana na wale wauaji wabaya, pia nilikuwa natafutwa na polisi sio tu kwa kile kimuhemuhe nilichozusha kule kwa mkuu wa wilaya, bali pia kama muhusika wa yale mauaji yasiyo na maana kule msituni. Kwenda kituo cha polisi kwa sasa ni sawa na kujipeleka mwenyewe kwa Pilato. Nilidhani kuwa njia salama kwangu ni kwenda kwa mtu mkubwa kabisa katika jeshi la polisi nikiwa na ule ushahidi wangu wa mkanda wa video, vinginevyo ule mkanda unaweza ukapotelea mikononi mwa Dokta Martin Lundi muongo, na huo ndio utakuwa mwisho wangu.
Sasa niende wapi?
Swala la kwenda nyumbani kwangu halikuwepo kabisa, kwani bila shaka kama wale watu wabaya walikuwa wameamua kunifuatilia kwa nguvu kiasi kile, basi huko ndio wangekuwa wamepiga kambi kabisa.
Nilifikiria kwenda nyumbani kwa mama yangu Tabata, lakini nilihisi kuwa nako ningemkuta Dokta Lundi na vibaraka wake wakinisubiri. Nilifikiria kwenda kwa mmoja kati ya marafiki zangu wachache, lakini sikulipenda kabisa wazo la kumgongea mtu usiku kama ule na kumpelekea mashaka yangu. Nilikimbilia kwa Kelvin na matokeo nimeyaona, sasa itakuwaje nikienda kwa mmoja wa hao marafiki zangu halafu Dokta Lundi akaniibukia huko huko? Ingawa unaweza kuona kuwa nilikuwa nampa huyu Martin Lundi uwezo mkubwa wa ki-Mungu wa kuweza kunifikia mahala popote niwapo, lakini kwa wakati ule akili yangu ilikuwa imeingiwa na woga mkubwa kabisa. Nilikuwa ni mtu niliyejawa wasiwasi wa hali ya juu.
Paranoid?
Niliamua kupitisha usiku ule wa mashaka kwenye nyumba ya wageni, ambamo baada ya kujitahidi kupata usingizi kwa shida, nilijikuta nikikurupushwa na ndoto ile ya kutisha.
Mwili ulinisisimka.
Ndani ya masaa sabini na mawili mlolongo mzima wa maisha yangu ulikuwa umebadilika kwa namna ya ajabu kabisa. Ndani ya muda huo, maisha yangu yaliyokuwa yamepambwa na ndoto nzuri sana za mafanikio na matarajio makubwa, yaligeuka na kuwa ndoto moja ya kutisha sana iliyogubikwa mashaka mazito.Ndani ya masaa hayo nilikuwa nimevunja uchumba kama masikhara, na bila shaka mtu aliyekuwa mchumba wangu alikuwa amepoteza maisha.
Kwa nini?
It is always the very good times of one’s life that normally turns into one’s very bad times in no time…
Nilianza kulia upya.
Nililia kwa unyonge na upweke. Nililia kwa kusikitikia maisha yangu yaliyoharibiwa bila sababu. Niliwalilia wenzangu niliokuwa nao kule msituni, waliouawa bila hatia.
Nilimlilia Kelvin.
Nililia sana na kwa muda mrefu. Kisha nilijilaza kitandani, huku nikijihisi mchovu kuliko kawaida.
Nilipitiwa na usingizi.
Lakini muda si mrefu baadaye nilishtushwa na vishindo na kelele nje ya chumba changu. Nilikurupuka nikiwa makini ghafla. Nje ya chumba kile nilisikia kelele za watu waliokuwa wakifoka na kushurutisha wapangaji wengine wafungue milango yao. Nilihamanika vibaya sana. Niliangaza huku na huko ndani ya chumba kile nisione pa kukimbilia. Kile chumba kilikuwa ni kama kile cha Kelvin, kikiwa na bafu lake kwa ndani, ila mlango wa kutokea ulikuwa ni mmoja tu. Nilinyakua koti langu la jeans na kulivaa haraka haraka na kuanza kuvuta viatu vyangu kutoka chini ya kitanda huku moyo ukinienda mbio wakati niliposikia mlango wa chumba changu ukigongwa kwa nguvu.
“Nani?” Niliuliza kwa sauti ya kitetemeshi huku nikihangaika kuvaa viatu.
“Polisi! Fungua!” Sauti kali ilijibu kutoka nje ya mlango ule na kuamrisha.
Mungu wangu, nimenyakwa! Nilienda haraka mpaka pale mlangoni, nikiacha kuvaa viatu na kuuliza kwa mashaka.
“Mnataka nini...?”
Mlango ulipigwa ngumi kwa nguvu.
“Hebu fungua mlango mwanamke...!Upesiiii, Ebbo!”
Nilifungua mlango haraka kwa woga na nilijikuta nikisukumiwa ndani kwa nguvu na askari wawili wakiingia mle ndani, mmoja akiwa mwanamke. Nilirudi nyuma na kubaki nikiwakodolea macho kwa woga. Yule askari wa kiume alipita moja kwa moja hadi kule bafuni na kukagua huku na huko, na kurudi pale chumbani. Yule wa kike aliliendea kabati la nguo la mle ndani na kulifungua. Hakukuta kitu, hivyo akarudi na kusimama mbele yangu.
“Ni..niwasaidie nini afande...” Niliuliza kwa wasiwasi. Badala ya kunijibu wale askari walikuwa wakinitazama huku nyuso zao zikificha hisia zozote ambazo ningeweza kuzisoma, kisha yule mwanaume aliongea.
“Uko peke yako humu?”
“Ndiyo...”
“Mwanamke peke yako gesti?” Yule mwanamke alidakia. Hili sikulijibu.
“Wewe ni nani, na kwa nini uko hapa saa hizi?” Yule askari wa kiume aliniuliza. Sikusita, nilitoa jibu hapo hapo.
“Naitwa Mwajabu, nimelala hapa gesti kwa sababu sina mwenyeji hapa mjini nami ni msafiri...”
“Ukilala ndio huwa unavaa nguo namna hii? Je ukioga?” Yule askari wa kike aliniuliza.
“Nimevaa nguo baada ya nyie kuanza kunigongea...ndio maana nilichelewa kufungua mlango.” Nilimjibu.
“Una kitambulisho?”
“Sina.” Walitazamana, kisha wakaniamrisha nitoke nje. Huko nilikuta askari wengine wapatao wanne, mmoja kati yao akiwa mwanamke. Wapangaji wengine walikuwa wamesimamishwa nje ya milango ya vyumba vyao, nami nikaamriwa nisimame mbele ya mlango wangu. Nikiwa nimejawa wasiwasi na udadisi, niliwatazama wale wapangaji wengine waliotolewa vyumbani mwao. Wengi wao walikuwa wawili-wawili,yaani mume na mke, na walikuwa wakilalamika kwa kuingiliwa faragha yao, hasa wanaume ambao bila shaka walikuwa pale kwa kujiiba wakisaliti ndoa zao.
Nilimgeukia yule askari wa kike.
“Afande kwani kuna nini...mbona mnadhalilisha watu namna hii?”
“Huu ni msako wa machangudoa...na wewe ni mmoja wao kwa hiyo usijitie kutoelewa hapa!”
Eh! Kwanza kichaa...Paranoid Schizophrenia...sasa changudoa! Ni nini hiki?
“Hah! Mi’ sio changudoa...mi’ ni msafiri...”
“Wasafiri huwa hawakai kwenye viji-gesti vya vichochoroni kama hivi, halafu huwa wanatembea na vitambulisho. Tulia hapo tuelekee kituoni sasa hivi!” Alinijibu yule askari wa kike halafu akawaendea wale askari wengine na kuanza kuwaeleza vitu ambavyo sikuweza kuvielewa huku akinioneshea kidole. Wawili kati ya wale askari niliowakuta pale kwenye korido nje ya chumba changu walinisogelea taratibu huku wakinitazama kwa makini. Kwa namna fulani nilihisi kuwa pale mimi ndio nilikuwa kusudio la msako ule, ila nilishindwa kuelewa ni vipi walijua kuwa nipo kwenye ile gesti, ambayo kwa hakika ilikuwa vichochoroni.Na kama hivyo ndivyo, basi kwa hakika lile kundi la Dokta Martin Lundi lilikuwa hatari sana. Na kama haikuwa njama ya Martin Lundi muongo, basi ilimaanisha kuwa ule ulikuwa ni msako wa polisi kweli, ambao kwa vyovyote mwisho wake ilikuwa ni kupelekwa kituoni tu. Sikuwa na shaka hata kidogo kuwa iwapo nitafikishwa kituoni tu, basi nitakuwa kwenye mashaka mazito.
Mungu wangu, hivi nitaweza kuondokana na balaa hili mimi?
“Enhe, msichana, mbona uko hapa gesti peke yako?” Mmoja wa wale askari wengine, mwanaume aliniuliza. Nilitaka nimuulize iwapo hilo lilikuwa ni kosa, lakini kabla sijajibu, yule askari mwingine wa kike alidakia. Nilimhisi kuwa na umri wa kati ya miaka thelathini na tatu au na tano. Alikuwa na sura ya kuvutia, na yale mavazi yake ya kiaskari yalimkaa vizuri sana, hasa suruali yake ambayo ilionesha jinsi alivyojaaliwa makalio mazuri ya kuvutia.
“Na usituletee habari ya kuwa eti u-msafiri...msafiri huna hata mzigo?”
Nilibaki nikiwakodolea macho wale askari nisijue la kuwaeleza. Na wakati bado naendelea kushangaa, yule askari mwanamke alinisukumia tena chumbani mwangu na kufunga mlango kwa ndani, akimuacha yule mwenzake kule nje. Bila ya kunitazama alitembeza macho mle chumbani na kuniuliza. “Umesema unaitwa nani?”
“Mwajabu...”
Aliliendea kabati la nguo la mle ndani na kulifungua kwa kutumia fimbo yake na kuchungulia ndani bila ya kushika kitu. Hakukuwa na kitu. “Unasema we’ ni msafiri...unatokea wapi na unaelekea wapi?” Aliuliza tena bila ya kunitazama huku akielekea kule bafuni.
“Natokea Mkuranga...naenda Zanzibar...” Jibu lilinitoka kama kwamba nilikuwa nasema ukweli. Yule askari aliguna na kurudi kando ya kitanda changu. Akiendelea kutonitazama, alilisukuma kwa fimbo yake begi langu dogo lililokuwa pale kitandani, kisha alilichukua na kukung’uta vilivyokuwamo ndani yake pale kitandani.
“Zanzibar unaenda kufanya nini?” Aliniuliza huku akipekua vile vitu vilivyomwagika pale kitandani. Aliinua ile kamera ya Gil na kuitazama kwa makini.
“Ku...kununua nguo za biashara...”
Aliifungua ile kamera sehemu ya kuwekea kaseti na kuchungulia ndani. Ilikuwa tupu. Nilikuwa nikitazama kila kitendo chake kwa makini huku moyo ukinienda mbio. Yule askari wa kike aliiweka kitandani ile kamera, na kuanza kupekua vitu vyangu vingine kwa muda na kwa utaratibu wa hali ya juu. Nilizidi kupata wasiwasi kwani huyu askari alionekana kuwa anajua anachofanya na sio anayebahatisha tu ambaye ningeweza kumlaghai kirahisi. Aliinua tena ile kamera na kuitazama kwa makini, huku akiigeuza huku na huko. Hatimaye aliiweka kitandani na kunitazama usoni kwa mara ya kwanza tangu aingie mle ndani.
“Oke, sasa mchezo basi Tigga, where is the tape?” Aliniuliza huku akiwa amenikazia macho kiaskari hasa, akimaanisha nimweleze ni wapi ulipo ule mkanda wa video wenye ushahidi wa mauaji ya yule mtu asiye na jina kule msituni.
Mshituko nilioupata kwa swali lile ulikuwa mkubwa sana. Niliruka kama kwamba nimepigwa kofi na kubaki nikimkodolea macho yule mwanamke aliyevaa mavazi ya kiaskari, kama kwamba nilikuwa nimeona jini.
Mimi nilijitambulisha kwake kwa jina la Mwajabu, sasa yeye ameniita kwa jina langu halisi na anajua juu ya ule mkanda wa video! Kwa hiyo muda wote ule alikuwa akijua kila kitu!
Hii ni njama ya Dokta Martin Lundi muongo! Oh, My God! Sasa nitapata wazimu!
Nilimtazama kwa kihoro yule mwanamke.
Hii ni babu kubwa! Na huyu naye ni mwenzao?
“Mbo..mbona sikuelewi Afa...nde?” Nilijitutumua kumuuliza huku nikirudi nyuma kwa woga.
“Usinitanie mimi wewe! Lete huo mkanda sasa hivi!” Yule askari alinifokea na hapo hapo alinitolea bastola na kuniwekea usoni. Sikumjibu kitu. Nilibaki nikiukodolea macho mdomo wa ile bastola huku moyo ukinienda mbio. Tulibaki tukitazamana kwa muda huku yule askari akinihemea usoni kwa hasira. Alipoona bado namkodolea macho bila kumjibu, alinidaka koo na kunisukumia kitandani.
“Tunajua kuwa unao huo mkanda...tunautaka...na nakuahidi kuwa tutayafanya maisha yako yawe mabaya sana hapa duniani mpaka utautoa!” Alinifokea kwa sauti ya chini huku akinitomasa puani kwa mdomo wa ile bastola yake.
Hii ilikuwa ni mara ya kwanza kwa hawa watu kujidhihirisha kwangu, nami sikuweza kuiachia nafasi hii, ingawa nilikuwa nimetishika vibaya sana.
“Kwani nyie ni kina nani? Wewe sio askari...ni mmoja wao!. Mnataka nini kutoka kwangu?”
“Kauli ya kijinga na swali la kijinga! Mimi sio askari wakati unaniona kuwa ni askari? Unauliza tunataka nini wakati nimekwambia tunautaka huo mkanda! Mjinga sana wewe!”
“Nyinyi?Nyie ni kina nani?”
“Si kazi yako kujua.......where is the tape Goddamn it?” Yule askari wa kike alinijibu kwa ghadhabu huku akisisitiza nimpatie ule mkanda wa video. Aliniudhi.
“Mnh! Mi’ naona wewe ndio mjinga. Sasa nikikupa huo mkanda halafu mimi hatima yangu itakuwa nini?” Nilimuuliza kwa kebehi. Alinibamiza kofi kali sana la ghafla na macho yalinichomachoma kwa machozi machanga. Nikiwa sijawahi kupata kipigo cha aina yoyote ile kwa miaka mingi sana, vipigo nilivyopata siku ile viliniuma sana. Kwanza Dokta Lundi na vibaraka wake, halafu huyu mwanamke mwenye mavazi ya kiaskari.
“Mi’ n’takuua ukinichezea we’ mtoto, lete huo mkanda...”Alinikemea kwa sauti ya chini huku akinididimizia bastola yake kooni.

***Makubwa!
 
SEHEMU YA KUMI NA TATU

“Mnh! Mi’ naona wewe ndio mjinga. Sasa nikikupa huo mkanda halafu mimi hatima yangu itakuwa nini?” Nilimuuliza kwa kebehi. Alinibamiza kofi kali sana la ghafla na macho yalinichomachoma kwa machozi machanga. Nikiwa sijawahi kupata kipigo cha aina yoyote ile kwa miaka mingi sana, vipigo nilivyopata siku ile viliniuma sana. Kwanza Dokta Lundi na vibaraka wake, halafu huyu mwanamke mwenye mavazi ya kiaskari.
“Mi’ n’takuua ukinichezea we’ mtoto, lete huo mkanda...”Alinikemea kwa sauti ya chini huku akinididimizia bastola yake kooni.
“Sina mimi huo mkanda!...kwani rafiki yako Martin Lundi muongo hajakueleza?”
Yule askari alisonya kwa hasira na kuikoki bastola yake huku akiididimiza kwa nguvu katikati ya koo langu na kuniambia kwa ghadhabu. “Usicheze na serikali Tigga...sisi tuko kila mahali, huwezi kutukwepa.Salama yako ni kutoa ushirikiano unaohitajika...”
“No! Wewe sio askari na wala nyie...sijui ni watu gani, lakini nyie sio serikali...serikali haiko hivyo...”
“The tape Tigga! Nautaka huo mkanda wa video sasa hivi!”
“Swala hilo nilishalimaliza kwa rafiki yako Martin Lundi muongo...kanda iko kwa wakili wangu!” Nilimkemea huku nikimsogezea uso wangu kwa kiburi. Yule askari alitoa sauti ya kukereka kwa jibu lile na kutaka kusema neno lakini ghadhabu zilimkaba kooni hivyo alibaki akinitumbulia macho kwa hasira, akijaribu kuamua achukue hatua gani badala ya kunilipua kwa ile bastola yake. Tulitazamana, na katika muda ule niliona kuwa yule dada alikuwa tayari kunilipua kwa risasi, kwani jibu langu lilimghadhibisha vibaya sana.Nilishuhudia midomo ikimcheza kwa hasira na macho yakimwiva.
Nilibaki nikimtazama kwa woga mkubwa na wasiwasi usio kifani. Bado shavu lilikuwa likinichonyota kutokana na kofi lake kali. Tulibaki tukitazamana kwa muda mrefu,hakuna mmoja kati yetu aliyesema neno.
Na mara yule askari wa kiume aliita kutokea nje ya chumba changu akimhimiza yule mwanadada waondoke nami pamoja na wale wapangaji wengine walioshindwa kujieleza vizuri kule nje kuelekea kituoni.
“Dakika moja afande!” Yule mwanadada askari alimjibu kwa sauti huku bado akiwa ananitazama usoni kwa macho ya ghadhabu. Hatimaye alishusha pumzi ndefu, na huku akilegeza mdidimizo wa bastola yake shingoni kwangu alinong’ona kwa hasira.
“Unafanya kosa kubwa sana Tigga, na utajuta kwalo!”
Kisha alisonya na kuiweka bastola yake kwenye mkoba wake na kuelekea mlangoni kwa mwendo wa haraka akiniacha nikiwa nimeduwaa mle chumbani nikimtazama huku nikijitahidi kumeza mate bila mafanikio. Alipofika mlangoni nilimsikia yule askari wa kiume alimuuliza juu yangu. Yule mwanadada aliyevaa mavazi ya kiaskari alisimama mlangoni na kunitazama kwa muda, kisha akamjibu huku bado akiwa ananitazama.
“Hana matatizo huyu...ni msafiri anayeelekea Zanzibar. Lets get out of here!” Kisha alifunga mlango taratibu na kutoweka.
Nilibaki nikiwa nimeduwaa.
Heh! Hawa watu...ni watu gani hawa? Kwa nini wanakuwa na uwezo wa kunifuatilia namna hii? Na vije wanakuwa na namna ya kujiingiza kwenye nyanja za kiserikali namna hii? Hivi yule mwanamke ni askari kweli au bandia?
Yaani kichwa kilinizunguka kwa maswali hayo kwa muda mrefu nikiwa nimekaa pale kitandani bila ya kupata dalili ya uelewa. Lakini swali kubwa zaidi lililobaki kichwani mwangu lilikuwa moja tu: kwa nini yule dada askari hakunikamata na kunipeleka kituoni?
Naam. Kwa hakika hili kwangu lilikuwa ni a hundred dollar question, kama wamarekani wanavyopenda kusema. Kwa nini yule dada asinikamate na kuniweka chini ya ulinzi? Kwani baada ya kituko kile, sikuwa na shaka kuwa alikuwa ana taarifa zote za tafrani niliyoizusha na kizaazaa nilichoacha kule Manyoni kwa mkuu wa wilaya.
Sasa kwa nini ameniacha?
Kadiri nilivyozidi kujiuliza maswali hayo, ndivyo taratibu nilipoanza kupata mwanga.
Nilijishawishi kuwa wale watu wanaonisakama hawakuwa wakifanya hivyo ili wanitie kwenye mikono halali ya sheria, bali walikuwa wananitaka kwa sababu yao binafsi, ambayo ni kuupata ule mkanda wenye ushahidi wa madhambi yao niliojinadi kuwa ninao.
Kitu kingine ambacho kilijitokeza ni kwamba wale watu...watu gani...? walikuwa na uwezo wa kutumia mamlaka za nyanja mbalimbali za kiserikali kwa maslahi yao.
Sasa hii ilibadilisha lile swali langu la msingi: hawa watu ni akina nani?
Niliwaza na kuwazua lakini bado niliishia kujiongezea maswali mengi yasiyo na majibu. Lakini kitu kimoja kilibaki akilini mwangu. Ule mkanda wa video ndio ulikuwa salama yangu,kwani nilikuwa na hakika kabisa kuwa wale watu hawashindwi kabisa kuniua, lakini hawatoweza kufanya hivyo mpaka waupate ule mkanda. Kabla ya hapo hawatathubutu kuniua, labda wajithibitishie kuwa hakuna mtu mwingine yeyote anayejua juu ya mambo yaliyomo ndani ya mkanda ule zaidi yangu.Lakini hilo wazo halikunipa amani hata kidogo, hasa nilipomkumbuka yule mtu niliyempachika jina la macho ya nyoka. Yule jamaa ni kichaa, angeweza kuniua wakati wowote, kama jinsi alivyomuua yule mtu asiye na jina kule msituni.
Nilikumbuka maneno makali ya yule askari wa kike aliyetoka mle chumbani muda si mrefu uliopita.
“...na nakuahidi kuwa tutayafanya maisha yako yawe mabaya sana hapa duniani mpaka utautoa!”
Kufikia hapa niliamua kuwa sina ujanja bali niendelee kukimbia tu mpaka nipate mtu nitakayeweza kumuamini na ule mkanda na ambaye ataweza kunisaidia, kwani lile swala sikuwa na uwezo wa kupambana nalo peke yangu.
Lakini ni nani wa kunisaidia? Na ni nani wa kumuamini?
Mambo yaliyonikuta kwa Mkuu wa Wilaya na kwa Kelvin yalinifanya nizidi kujiona kuwa bado niko peke yangu, nisiye na kimbilio.
Na yote hii ni kwa ajili mambo niliyoyaona na ambayo sasa yako kwenye ule mkanda wa video. Sikusubiri zaidi.
Nilikurupuka ghafla na kuanza kukusanya vitu vyangu vilivyotawanywa hovyo pale kitandani na kuvishindilia kwenye begi langu. Niliichukua ile sabuni aina ya Geisha niliyoichukua bafuni kwa Kelvin na kwa kutumia kile kisu changu kidogo,nilifuatisha mchinjo mwembamba sana nilioukata kuuzunguka mgongo wa ile sabuni wakati nilipokuwa nimejifungia bafuni kwa Kelvin kabIa ya kuanza kuoga, na kuitenganisha ile sabuni kwa ubapa na kubaki na vipande viwili mithili ya silesi mbili za mkate. Katikati ya kila ubapa wa ile sabuni kwa ndani nilikuwa nimechimba kwa kisu kiasi cha kuweza kuzamisha ile kaseti ndogo kabisa ya video. Kwa mikono iliyotetemeka na huku moyo ukinipiga kwa nguvu, niliitoa ile kaseti ambayo hapo awali nilikuwa nimeizungushia nailoni ya sabuni kabla ya kuizamisha kwenye kishimo nilichochimba kwenye moja ya bapa mbili za ile sabuni niliyoikata kistadi na kuibananisha tena kwa maji kidogo na kuuficha ule mchinjo kwa rojo zito la sabuni ile baada ya kuiloweka na kukauka.
Ile kaseti ilionekana safi na salama, wala haikuonekana kuathirika na kificho kile kilichoiokoa kutoka kuangukia mikononi mwa dokta Martin Lundi na kuendelea kuiokoa tena kutoka kuangukia mikononi mwa yule askari wa kike aliyeahidi kuyafanya maisha yangu yawe mabaya mpaka atakapoitia mkononi ile kaseti.
Kwa kutaka kuhakikisha, niliingiza kwenye ile kamera ya marehemu Gil na kuirudisha mwanzo kidogo, kisha nikabonyeza sehemu iliyoandikwa “play”.
Kwenye kile kijiruninga kidogo cha kamera ile, nilimuona tena yule mtu asiye na jina akimg’ang’ania koo macho ya nyoka...
Niliizima na kutumbukiza ile kamera pamoja na ile kaseti ndani ya mkoba wangu.
Nilivaa viatu vyangu na kutoka haraka mle ndani bila kujali kuwa ulikuwa usiku.
Kwa wakati ule jambo la muhimu kwangu lilikuwa ni kuwa mbali na eneo lile kwa kadiri iwezekanavyo.

--

Nilipitisha sehemu iliyobaki ya usiku ule Club Billicanas, ambako nilijichimbia kwenye kona pweke ndani ya ukumbi ule na kuduwaa nikiangalia jinsi vijana wenzagu wakijirusha na kufurahi pamoja na wapendwa na marafiki zao. Baada ya kukurupuka kutoka pale kwenye ile gesti, sikuwa na kimbilio lolote la haraka nililoweza kulifikiria kwa wakati ule. Ingawa nilibahatika kupata watanashati kadhaa waliojitokeza kutaka kucheza nami na wengine hata kujaribu kunitongoza, sikuwa na hamu kabisa ya kujipumbaza na furaha zile, hivyo niliwakatalia kistaarabu na kuendelea kukaa kimya peke yangu ndani ya ukumbi ule.
Akili yangu ilikuwa imepigwa na bumbuwazi kwa jinsi mambo yalivyozidi kuniendea vibaya, kwani nilijiona nikizidi kudidimia katika dimbwi la uadui na tuhuma zisizo na msingi, bila ya matumaini ya kujinasua kutoka katika dimbwi lile. Na ilionekana kuwa kadiri mambo yalivyozidi kusonga mbele, ndivyo ule mtandao dhalimu wa akina Martin Lundi ulivyozidi kupanuka.
Angalau pale ndani ya ule ukumbi maarufu wa starehe sikuwa na wasiwasi wa kukurupushwa na vibaraka wa yule mtu anayejiita Martin Lundi, au wana usalama ambao nao nilikuwa na imani kuwa walikuwa wakinisaka. Nilikuwa na hakika kabisa kuwa katika mawazo yao wasingetarajia kabisa kwamba katika mazingira kama niliyokuwa nayo ningeweza hata kufikiria kwenda sehemu kama Club Billicanas.
Na kuanzia hapo niliamua kuwa salama yangu ilitegemea katika kufanya yale ambayo wao hawayatarajii.
Wao.
Nilimfikiria yule mwanadada aliyevaa mavazi ya kiaskari aliyeacha kuniweka chini ya ulinzi muda mfupi uliopita...
Wao ni nani? Who are these people?
Alfajiri kulipopambazuka nilitoka pamoja na washabiki wengine wa starehe waliokesha pale ukumbini na kuchukua teksi mpaka nyumbani kwa mama yangu Tabata,nyumba ambayo tuliachiwa na marehemu baba yetu.
Niliondoka pale nyumbani baada ya kuanza kazi na kwenda kupanga nyumba ya msajili maeneo ya Upanga ili niweze kujitegemea, nikimwacha mama na dada yangu wakiishi pale nyumbani. Kwa kuwa naye hakuwa ameolewa, na ajira yake hakikumuwezesha kupanga nyumba na kujitegemea kama mimi, dada yangu aliendelea kuishi na mama pale nyumbani.
Ilikuwa ni saa kumi na mbili kasoro robo wakati mama aliponifungulia mlango nami nikaingia ndani ya nyumba ile niliyolelewa tangu utoto wangu. Mama alionekana wazi kuwa ameshitushwa na ujio wangu, na mara nilipoingia ndani alifunga mlango haraka na kuniongoza hadi chumbani kwake ambako tulikumbatiana kwa nguvu huku sote tukibubujikwa na machozi kimya kimya. Nilimuuliza iwapo Koku, dada yangu alikuwepo nyumbani. Aliniambia kuwa alikuwa ameshatoka kwenda kazini. Koku alikuwa ni nesi wa hospitali ya wilaya ya Temeke. Nilibaki nikiangaza mle ndani huku nikitokwa na machozi. Kwa namna fulani nilihisi amani kwa kuwepo tu pale nyumbani na mama yangu.
“Oh! Tigga mwanangu! Ni nini tena kimekukuta mwanangu?” Mama alilalamika kwa sauti ya chini huku akibubujikwa na machozi. Sikuweza kujibu. Sasa nilikuwa nikilia kwa nguvu nikiwa nimemkumbatia mama yangu. Hapa nilikuwa nimepata liwazo nililokuwa nikilihitaji sana tangu nikutane na mtihani huu mgumu kabisa katika maisha yangu.
“Matatizo makubwa yamenikuta mama...” Nilibwabwaja kwa simanzi.Nilitaka kumueleza juu ya Kelvin, lakini jibu lake lilinishitua.
“Najua mwanangu...pole sana. Lakini unahitaji kitu cha kula...na mapumziko.”
“Unajua...?” Nilimuuliza huku nikimtazama kwa mashaka. Tulitazamana, na niliona kuwa alikuwa akinitazama kwa huzuni kubwa...
“Walikuja hapa...wakanieleza kila kitu...” Alinifafanulia huku akiniketisha kitandani kwake.
Hapo nilikuwa makini kupita kawaida. Walikuja hapa...wakanieleza kila kitu...
“Nani walikuja mama? Dokta Lundi? Dokta Martin Lundi alikuja hapa?”
“Ndio mwanangu...Dokta Lundi alikuja, akanieleza yote yaliyotokea...”
Nilimtazama mama yangu na nikahisi moyo ukiniisha nguvu. Kwa jinsi mama alivyokuwa akiongea, niliona kuwa lolote ambalo alikuwa ameelezwa na huyu mtu anayejiita Martin Lundi, alikuwa amelielewa vizuri sana na hakuwa na shaka nalo kabisa.
Eh! Mungu wangu!
Sikuwa na shaka hata kidogo kuwa Martin Lundi muongo atakuwa ameleta uongo na fitna zake kwa mama yangu, lakini nilikuwa na hakika kabisa kuwa mama asingeweza kumkubalia ule uongo wake kirahisi. Lakini kilichonishangaza ni kuona kuwa mama alikuwa anaongea kama kwamba alikuwa amemuamini! Nilimeza funda la mate, ambayo niliyahisi machungu kuliko kawaida.
“A...alikuja na polisi...?” Nilimuuliza mama kwa wasiwasi. Mama alinitazama kwa mshangao mkubwa sana. Kama kwamba alikuwa anamshangaa mtu mwenye wazimu.
“Polisi? Kwa nini aje na polisi? Hapana, alikuja na madaktari wenzake...”
Nilibaki mdomo wazi. Kwa hiyo hapa hakuja na askari. Ni uongo gani uliotumia kwa mama yangu Martin Lundi?
“Na akakueleza kila kitu...?”
“Yes, my love. I am so sorry for you, lakini usiwe na wasiwasi, mama yako hatokuacha peke yako. Na nitahakikisha kila kitu kinakuwa sawasawa.”
“How, mama? Utahakikishaje kuwa kila kitu kinakuwa sawa...? Kwani umeelezwa nini na Dokta Lundi? Yule ni muongo sana mama, isije ikawa...”
“Usiwe na wasiwasi mwanangu...mimi nitakuwa na wewe kila hatua mpaka mwisho.”
Nilichoka!Nilitaka kumuuliza alikuwa anamaanisha nini kwa kauli ile, lakini hakunipa nafasi. Aliinuka kwenda kunitayarishia chai nami nikaingia bafuni na ule mkoba wangu ambako nilioga haraka haraka na kupiga mswaki kwa kutumia kidole na kusukutua kwa dawa ya meno. Niliogopa hata ile kuwaza tu kuwa na mama naye atakuwa amekolezwa ule ujinga wa Dokta Lundi. Nilitaka kuamini kuwa alikuwa upande wangu na aliazimia kunisaidia mpaka mwisho wa mkasa huu.
Lakini hivyo ndivyo alivyokuwa akimaanisha kwa kauli yake ile?
Au alikuwa anamaanisha vinginevyo?
Nilipotoka nilimfuata mama jikoni ambako alikuwa akimalizia kukaanga mayai. Nilikunywa chai kule kule jikoni huku akilini nikiwa najaribu kutafakari ni nini maana ya yale maneno ya mama. Baada ya kunywa ile chai na kushiba kisawasawa, nilianza kujihisi usingizi mzito. Nilikumbuka kuwa sikuwa nimepata muda wa kulala sawasawa tangu niingie hapa jijini kutoka kule Manyoni ambapo balaa lote hili lilipoanzia. Nilijilazimisha kupingana na usingizi ule na kumkabili tena mama yangu.
“Mama...umesema Dokta Lundi amekueleza kila kitu...amekueleza nini?” Hatimaye nilimuuliza mama yangu. Alinitazama kwa muda, kisha alishusha pumzi kabla ya kunijibu taratibu.
“Amenieleza kuhusu...kuhusu yaliyotokea kule msituni Tigga. Lakini amenihakikishia kabisa kuwa yote yaliyotokea kule si jukumu lako! Niliogopa sana mwanangu, lakini Dokta Lundi is such a humble man...(ni mtu mkarimu sana...) ameahidi kukusaidia kwa kadiri ya uwezo wake...”
Mwili ulinifa ganzi na nikahisi ile nyumba ikizunguka. Yaani mama alikuwa anaamini kuwa Dokta Lundi ni mtu mzuri mwenye nia ya kunisaidia!
Sikuamini.
“Mama! Unataka kuniambia kuwa umeamini aliyokueleza Dokta Lundi?” Nilimuuliza kwa jazba huku nikiinuka kutoka kwenye kiti nilichokuwa nimekalia na kumsogelea huku nikimtazama kwa makini. Mama alinitazama kwa mashaka huku akijishughulisha kusogeza vile vyombo nilivyokuwa nikilia pale mezani.
“Sasa kwa nini nisimuamini Tigga mwanangu? Yule ni mtu mwenye nia ya kusai...”
“Yule ni mtu mwenye nia ya kuniua mama! Na usimruhusu kabisa aje karibu na wewe, atakudhuru! Dokta Martin Lundi ni muuaji mama, na mimi nimemuona kwa macho yangu akishirikiana na wenzake kumtesa na hatimaye kumuua mtu kule msituni.” Nilimkatisha mama yangu kwa hasira.
Kwa nini watu wanapenda kumuamini Martin Lundi muongo?
“Hapana Tigga...hayo yote yamo katika fikira zako tu mwanangu...ni kutokana na...”
“Paranoid Schizophrenia?” Nilimkatisha mama yangu kwa uchungu, kabla hajamalizia ile kauli yake, na kuendelea; ”Hivyo ndivyo Dokta Lundi alivyokueleza mama? Kuwa hayo mambo ni fikira zilizojengeka bila msingi kichwani mwangu kutokana na huo ugonjwa unaosemekana kuwa ninao?”
“Tigga mwanangu, usiifanye hii hali iwe ngumu kuliko inavyohitajika...”
ITAENDELEA
 
SEHEMU YA KUMI NA NNE

Kwa nini watu wanapenda kumuamini Martin Lundi muongo?
“Hapana Tigga...hayo yote yamo katika fikira zako tu mwanangu...ni kutokana na...”
“Paranoid Schizophrenia?” Nilimkatisha mama yangu kwa uchungu, kabla hajamalizia ile kauli yake, na kuendelea; ”Hivyo ndivyo Dokta Lundi alivyokueleza mama? Kuwa hayo mambo ni fikira zilizojengeka bila msingi kichwani mwangu kutokana na huo ugonjwa unaosemekana kuwa ninao?”
“Tigga mwanangu, usiifanye hii hali iwe ngumu kuliko inavyohitajika...”
Nilitoa sauti ya kukata tamaa na kutikisa kichwa kwa masikitiko makubwa.
“Mama! Hivi kuna historia ya wazimu katika familia yetu? Kuna mtu yeyote...babu au bibi fulani huko nyuma, aidha upande wako au wa baba ambaye alipata kuugua wazimu?” Nilimuuliza kwa jazba. Mama alibaki akinitazama tu huku akivisogeza sogeza vile vyombo bila uelekeo maalum. Lile swali lilionekana kuwa lilimchanganya kidogo na niliona wazi kuwa wazo hilo halijawahi kumpitia kichwani mwake hata kidogo.
“Ennh, mama, hebu nieleze hilo...sijawahi kusikia hata siku moja...au mlituficha?” Nilizidi kumsukumia maswali.
“Hakuna Tigga, lakini...”
“Unaona? Mi’ najua magonjwa kama hayo yana namna ya kurithishwa katika familia, au nakosea?”
Mama hakunijibu. Niliona alikuwa amechanganyikiwa na nilimwonea huruma sana.
Nilihisi chuki ya hali ya juu kwa yule mjinga anayejiita Dokta Lundi kwa kutufikisha katika hatua hii mimi na mama yangu. Lakini kwa nini mama asiuone uongo huu? Mimi ni mwanae for God’s sake!
Nilimsogelea na kumuambia kwa kuomboleza: “Mama. Naomba uniamini mimi mwanao. Dokta Lundi ni muongo tena muongo mkubwa sana! Na wala sidhani kama ni dokta kweli yule. Anachofanya ni kupita akinipakazia uzushi wa ugonjwa huo wa uongo ili kuninyima nafasi ya kusikilizwa na kuaminika mahala popote nitakapokwenda. Na hiyo ni kutokana na mambo niliyoyaona kule msituni na ambayo nina ushahidi usiopingika...ushahidi ambao utamuathiri sana huyo Dokta Lundi na wenzake!”
Niliona kabisa kuwa hali ile ilikuwa ikimchanganya vibaya sana mama yangu, na nilizidi kumuonea huruma lakini ilibidi nimueleweshe.
“Mama, mi’ n’na ushahidi wa kuthibitisha kuwa Dokta Lundi si mtu mwema kama anavyotaka wewe umuone...”
“Amenionesha picha za kule msituni Tigga...watu wameuawa Tigga! Kama kuku...!Inatisha sana!” Alisema kwa sauti ya chini huku akilengwa na machozi.
“Na akakuambia kuwa ni mimi ndiye niliyewaua wale watu?” Nilimuuliza mama kwa uchungu. Hakunijibu, lakini katika macho yake niliona kuwa nilikuwa nimeuliza jibu. Iliniuma sana.
“Mama! How can you believe such rubbish?” Nilibwata huku nikitupa mikono yangu hewani,nikimuuliza ni vipi anaweza kuamini upuuzi kama ule, kisha nikaendelea kwa sauti ya chini huku nikisisitiza kauli yangu kwa mikono yangu.
“Mama...ni yeye pamoja na wenzake watatu ndio waliofanya yale mauaji kule msituni! Na hakuna mtu yeyote anayejua hilo isipokuwa mimi. Huoni kuwa anafanya kusudi kunipakazia ugonjwa huo ili taarifa nitakazotoa dhidi yake na wenzake zitiliwe mashaka na kila mtu? Si unaona jinsi wewe mwenyewe unavyoshindwa kuniamini? Hivi ndivyo anavyotaka, na ndivyo inavyokuwa kila mahali niendapo mama!How can you believe him mama?” Nilimueleza kwa hisia kali huku nikihoji uhalali wa mama yangu kuamini uongo wa Martin Lundi kirahisi namna ile.Na hata pale nilipokuwa nikiongea maneno yale, nilijihisi uchovu na usingizi mzito. Nilipiga mwayo mrefu na kujibwaga tena kwenye kiti. Mama alinisogelea na kunipapasa kichwani.
“Pole sana Tigga. Unaonekana una usingizi, kwa nini usijipumzishe kidogo halafu tutaongelea hili jambo baadaye?” Aliniambia kwa upole. Na hii ndio tabia ya mama yangu ambayo toka utotoni mwangu nilikuwa siipendi. Akiwa na jambo lake basi yuko radhi mliahirishe kwa muda kuliko kukubaliana na wazo jingine, akitumaini kuwa baada ya muda utakuwa umeelewa “ujinga” wako na kukubaliana na mawazo yake.
Sasa mimi sina muda wa kupoteza namna hiyo mama!
Nilimtazama mama yangu kwa kukata tamaa, na mwayo mwingine ukanitoka. Sikuwa nimepata usingizi wa kutosha usiku uliopita. Lakini huu sio wakati kulala!Dokta Lundi akitokea...
“Tafadhali usimruhusu Dokta Lundi anikamate mama...please!” Nilimwambia kwa sauti ya chini huku nikihisi macho yakiniwia mazito kuliko kawaida.
“Mi’ nakutakia yaliyo mema kwako mwanangu, na si vinginevyo.” Mama alijibu, lakini kauli ile haikunipa amani hata kidogo.Nilijilazimisha kuinuka na kwenda kujilaza kwenye kochi refu lililokuwa pale sebuleni huku nikiwa nimeukumbatia mkoba wangu. Mama alinishauri nikalale chumbani, lakini sikukubali, nilimwambia kuwa nataka kujipumzisha kwa dakika chache tu.
Nadhani nilisinzia kwa dakika chache sana, kisha nikahisi nikipambana na usingizi ule mzito, nikijitahidi usinielemee.
Lazima niamke! Lazima niamke!
Wazo hilo lilikuwa likinijia tena na tena ilhali usingizi ukizidi kunielemea.Kwa mbali nilisikia sauti ya mama yangu ikinisemesha. Niliinuka ghafla na kutazama kila upande, lakini nilikuwa peke yangu pale sebuleni. Ilikuwa ndoto? Hapana, nilisikia sauti ya mama ikitokea sehemu ndani ya nyumba ile. Alikuwa akiongea na nani? Aliniambia kuwa Koku alikuwa ameshaenda kazini, sasa huyo anayeongea naye ni nani? Niliinuka taratibu na kuelekea kule niliposikia sauti yake ikitokea.
Nilimkuta akiwa katika chumba cha kulia chakula. Alikuwa amekaa kwenye kiti akiwa amenigeuzia mgongo na alikuwa anaongea na simu, na alikuwa akimbembeleza kitu fulani huyo aliyekuwa akiongea naye. Nilisimama kando ya mlango wa kuingilia kule alipokuwepo na kujaribu kusikiliza maongezi yale huku moyo ukinienda mbio.
“...nataka nijue ni wapi hayo matibabu yatakapofanyika na mimi nataka niwepo...”
Usingizi ulinikauka mara moja, nikazidi kusikiliza.
“...yeye yupo hapa, lakini lazima na mimi niwepo...”
Moyo ulinilipuka na kuongeza mapigo.
Mama alikuwa anaongea na Dokta Martin Lundi!
Nilichanganyikiwa.
Haraka nilirudi kule sebuleni na kulinyakua lile begi langu dogo. Nilitembea haraka kuelekea mlango wa nyuma wa nyumba ile, na nilipopita tena kwenye ule mlango wa kuingia chumba cha kulia chakula, mama alikuwa ameshamaliza kuongea na simu.
“U...unaenda wapi Tigga...usingizi umeisha mara hii?” Aliniuliza huku akinisogelea. Moyo uliniuma kuliko kawaida. Sikuweza kumtazama.
“Na...naenda kulala chumbani...” Nilimjibu bila kumtazama na bila kupunguza mwendo wangu. Mwisho wa korido kabla ya kuufikia mlango wa nyuma wa nyumba ile kulikuwa kuna chumba cha wageni. Nilipokifikia nilisimama nje ya mlango wa chumba kile na kumgeukia mama yangu. Alikuwa amesimama akinitazama.
“Ennh...naomba uniamshe ifikapo saa saba...” Nilimwambia kwa sauti ya chini huku nikifungua mlango wa kile chumba.
“Sawa mama...” Alinijibu, kisha akanisogelea kwa hatua za haraka, nami nikamsubiri huku nikitazama sakafuni. Alinikumbatia kidogo na kunibusu kwenye paji la uso.
“Lala unono mwanangu...yote yatakwisha tu, muamini mama yako.”
Sikujua nimjibu nini, lakini machozi yalinitiririka nami nikageuza uso wangu ili asione jinsi nilivyoumia.Niliingia ndani ya kile chumba na kusimama nyuma ya mlango kwa ndani nikisikilizia mienendo ya kule nje huku moyo ukinipiga sana. Hakuna kilichotokea, kisha nikasikia maji yakimwagika jikoni na vyombo vikigongana. Nikahisi mama alikuwa akiosha vyombo jikoni.
No time to waste!
Nilitoka nje ya chumba kile taratibu na kufungua mlango wa kutokea nyuma ya nyumba ile taratibu mno. Nilitoka nyuma ya nyumba yetu na kuruka michongoma iliyofanya uzio wa kuizunguka nyumba ile na kutokea mtaa wa pili.
Huku nikitiririkwa na machozi, nilitembea kwa mwendo wa kasi kuelekea nisiKokujua.
Nilikimbilia kwa Kelvin, nikakutana na usaliti nisioutegemea na roho iliniuma sana. Lakini hili la kukuta usaliti kama ule kwa mama yangu liliniuma zaidi. Sasa nitakimbilia wapi? Kwa nini hawa akina Martin Lundi wanakuwa na uwezo wa kuwarubuni watu mpaka wanafikia hatua ya kunigeuka namna hii?
Au inawezekana ikawa ni kweli mimi nina huo ugonjwa ninaosemekana kuwa ninao na mambo yote ninayoamini kuwa nimeyaona ni fikara zangu tu zenye maradhi?
Lakini nilipopapasa begi langu na kuigusa ile kamera ya marehemu Gil, nilipata hakika kuwa niliyoyaona yalikuwa ni kweli tupu.
Sasa ni nini hii?
Hata mama yangu! Oh, My God!
Ama kwa hakika sasa nilikuwa peke yangu, nisiye na kimbilio.
Ili iweje sasa?
Nilijua kuwa mama alifanya vile akiwa na imani,kuwa ananisaidia, kwamba anafanya kwa faida yangu.
Lakini sivyo mama! Martin Lundi ni muongo na muuaji! Nitawezaje kusema hadi niaminike?
Nilikuwa nikiwaza mambo hayo na mengi mengine huku nikipotelea mitaa ya nyuma kutoka ule uliokuwamo nyumba yetu. Sikuwa na uelekeo maalum, na kwa wakati ule sikujali. Jambo pekee nililojali kwa wakati ule ni kujiweka mbali na mikono ya yule mtu mbaya anayejiita Martin Lundi, na kundi lake.
Bila ya kujua nilikuwa nimezunguka na kufuata mtaa uliotokea mwanzoni mwa ule mtaa ambao nyumba yetu ilikuwepo. Nikiwa nimesimama mwanzoni mwa mtaa ule, niligeuka kutazama upande ilipokuwepo nyumba yetu ambapo ni katikati ya ule mtaa. Nilishuhudia kwa kihoro magari matatu yakisimama kwa kasi na vishindo nje ya nyumba yetu na watu wakiremka na kukimbilia nyumbani kwetu, huku wengine wakiizingira nyumba ile kwa nje. Nilidhani nilimuona Dokta Lundi miongoni mwao. Lakini kwa umbali ule sikuweza kuwa na uhakika. Niliogeza hatua na kupotea eneo lile nikimwomba Mwenyezi Mungu amsaidie mama yangu.
iv.

S
iwezi kuelezea jinsi nilivyoumizwa na kitendo cha mama yangu kuamua kumuamini yule shetani anayejiita Martin Lundi na kupuuzia kabisa utetezi wangu. Kwa kweli hakuna maneno ambayo ninaweza kuyatumia hata yakatosha kuonesha ni kiasi gani jambo lile lilikuwa limeniumiza, kwani ilikuwa ni kupita kiasi. Ni kweli kuwa pale nilipogundua kuwa Kelvin aliamua kunisaliti kwa yule shetani Martin Lundi hata nilipompa maelezo yangu, niliumia hata nikahisi kama kuna ndoana iliyokuwa ikiuvuta moyo wangu kwa nguvu kubwa; lakini kuumia nilikoumia kutokana na hali iliyotokea pale kwa mama yangu, kulikuwa ni zaidi ya hivyo.
Lakini sikuwa na la kufanya, lililotokea lilikuwa limetokea, na aliyelifanya ni mama yangu.
Angalau kwa Kelvin niliweza kuamua kuvunja uchumba na kuachana naye, lakini huyu alikuwa mama yangu! Mama aliyenizaa kwa uchungu mwingi. Sasa vije mtu kama Dokta Lundi akaweza kumrubuni, kumlaghai na kumshawishi hata akaweza kumuamini yeye na akashindwa kuamini maelezo ya mwanae mwenyewe ambaye alipata uchungu usio mfano wakati akimzaa?
Nilishindwa kuelewa, na nilizidi kuchanganyikiwa iliponibainikia kuwa hata ningefanya nini, nisingeweza kumfuta asiwe mama yangu kama jinsi nilivyoweza kumfuta Kelvin kutoka katika maisha yangu (sijui naye yu hali gani huko aliko). Hivyo nilimwomba Mwenyezi Mungu amnusuru mama yangu na ghadhabu za Dokta Lundi baada ya kufika pale nyumbani na kukuta kuwa nimewatoroka kwa mara nyingine tena, wakati yeye aliwapigia simu na kuwahakikishia kuwa nilikuwepo pale nyumbani.
Baada ya kuwashuhudia kwa mbali akina Martin Lundi wakiizingira nyumba yetu, nilielekea moja kwa moja kituo cha basi na kupanda basi nililolikuta likipakia abiria pale kituoni bila ya kujali lilikuwa likielekea wapi, lengo likiwa ni kupotea kabisa eneo lile. Na njia nzima wakati basi lile likifanya safari yake ambayo nilikuja kuelewa baadaye kuwa lilikuwa likielekea posta, nilikuwa ni mtu niliyepigwa bumbuwazi. Woga ulinitawala kupita kiasi kwani sasa ilikuwa imenifunukia wazi wazi kichwani mwangu kuwa katika janga hili nilikuwa peke yangu.
Nilikwangua akili yangu nikijaribu kutafuta ni hatua ipi ifuate lakini niliambulia ukungu tu. Nilifikiria kumfuata dada yangu Koku kazini kwake, lakini nililifuta wazo hilo haraka, kwani nilijua kuwa asingeweza kunisaidia lolote katika mazingira yale. Nilijua iwapo mama ameamua kuchukua msimamo aliouchukua katika swala langu, hakuna shaka kabisa kuwa na yeye atakuwa na mtazamo ule ule.
Nilidhani kuwa Koku angeweza kusaidia kwa kumbana Dokta Lundi kwa maswali ya kitaalamu juu ya ule ugonjwa anaonipakazia na hatimye kubainisha uongo wake, lakini kama angefanya hivyo, basi hata mama angekuwa na mtazamo tofauti. Lakini pia nilikumbuka kuwa, dada yangu alikuwa ni nesi wa kawaida tu.Yumkini akawa hana uwezo na utaalamu wa kuuelewa ugonjwa ule kama jinsi alivyouelewa Dokta Martin Lundi muongo.
Sasa nifanye nini...?
Niliamua kwenda ofisini kwangu, katika jumba la Makumbusho ya Taifa. Huenda huko nikapata baadhi ya majibu ya maswali yangu. Kwani si huko ndipo iliposemekana kuwa ile barua ya uongo iliyopelekwa kwa mkuu wa wilaya ilikuwa imetokea? Sasa niliona kuwa iwapo nilikuwa nashutumiwa kwa mambo yasiyo na msingi, basi ni wajibu juu yangu kutafuta kiini cha shutuma hizo. Shutuma za kuwa nilikuwa mgonjwa wa akili zilikuwa ni nzito na mbaya sana. Nilijua kuwa ile barua ilikuwa imeghushiwa, na hata kule ofisini haijulikani kuwa kulikuwa kuna barua kama ile. Lakini sikuwa na namna ya kujithibishia hilo isipokuwa kwenda ofisini. Aidha nilijua kuwa kwa vyovyote iliniwajibikia kuripoti pale ofisini baada ya kutoka kwenye ile safari iliyozaa balaa niliyotumwa na ofisi. Sikujua ningekutana na nini huko nilipoazimia kwenda, lakini sikuona njia nyingine ya kuanza kutafuta ukweli wa mambo yale ya uongo niliyopakaziwa zaidi ya ile.
Niliingia ndani ya jengo la ofisi yetu na kuelekea moja kwa moja ofisini kwa afisa utumishi, ambaye ndiye muangalizi wa maswala yote ya wafanyakazi na ajira zao, lakini kabla sijaifikia ofisi yake niliwahiwa kwenye korido na baadhi ya wafanyakazi wenzangu ambao walinizingira kwa maswali kemkem kuhusu matukio ya huko msituni. Wapo walionipa pole, wapo walioulizia ilikuwaje hadi wenzangu wakaangamia kule porini, wengine walikuwa wakiniambia kuwa kwa kujipeleka pale ofisini nilikuwa nimejitia kwenye mtego na kunishauri niondoke haraka, huku wengine wakionesha wazi kuwa walikuwa wakiniogopa. Sikuweza kujibu swali hata moja, kwani yalikuwa yakija bila mpangilio maaluim, nami nilianza kuingiwa na woga na kujuta kwa nini niliamua kwenda pale ofisini. Niligundua kuwa habari zangu zilikuwa zimefika pale ofisini, na kwamba kwa ujumla ilieleweka kuwa Tigga si mtu salama tena kuwa karibu naye. Hili nililibaini kutokana na hali iliyojitokeza pindi nilipoingia pale ofisini, kwani wenzangu walikuwa wakiniuliza maswali yale na kunipa pole huku wakinitazama kwa wasiwasi, na muda wote walikuwa kikundi, hakuna hata mtu mmoja aliyekuwa tayari kukaa na mimi peke yake. Nikiwa nimezingirwa na wale wafayakazi wenzangu pale kwenye korido, nilimuona Mkurugenzi wa Idara ya Makumbusho akitoka ofisini kwake, iliyokuwa kwenye ghorofa ya kwanza, na kuchungulia pale chini nilipokuwa nimezongwa na wafanyakazi wenzangu. Tulitazamana kwa muda, kisha alirudi ofisini kwake na kufunga mlango.
Hatimaye nilifanikiwa kujichomoa kutoka kwenye lile kundi la wafanyakazi wenzangu na kuingia ofisini kwa afisa utumishi.
ITAENDELEA
 
SEHEMU YA KUMI NA TANO.

. Nikiwa nimezingirwa na wale wafayakazi wenzangu pale kwenye korido, nilimuona Mkurugenzi wa Idara ya Makumbusho akitoka ofisini kwake, iliyokuwa kwenye ghorofa ya kwanza, na kuchungulia pale chini nilipokuwa nimezongwa na wafanyakazi wenzangu. Tulitazamana kwa muda, kisha alirudi ofisini kwake na kufunga mlango.
Hatimaye nilifanikiwa kujichomoa kutoka kwenye lile kundi la wafanyakazi wenzangu na kuingia ofisini kwa afisa utumishi.
“Heey! Tigga! Karibu mrembo...karibu...” Suleiman Kondo, afisa wetu wa utumishi alinikaribisha huku akiweka chini simu aliyokuwa akiongea nayo muda mfupi kabla ya ujio wangu, naye akiinua mwili wake mkubwa na mzito na kusimama kwa heshima yangu. Hili ni jambo ambalo halijawahi kutokea.Hata siku moja Suleiman hajawahi kunikaribisha kwa kusimama, leo vipi hadi kusimama? Nilitembeza macho haraka mle ndani na kugundua kuwa ile simu aliyokuwa akiongea nayo ilikuwa ni ile niliyoijua kuwa huwa ina mawasiliano ya moja kwa moja na ofisi ya Mkurugeenzi.
“Nimekuja kuripoti Suleiman...na kuleta taarifa za maafa yaliyotokea huko Manyoni.” Nilimwambia.
“Oke...karibu na pole sana Tigga. Tumeingiwa na msiba mkubwa...wenzetu wametutoka...what happened out there Tigga?” Suleiman alisema kwa huzuni huku akinitazama usoni, na kunitupia swali akitaka nimweleze ni kipi kilichotokea kule msituni. Sikufanya haraka kumjibu bali akilini mwangu nilikuwa nikijaribu kuisoma hali ya mle ndani iwapo ilikuwa na maslahi nami au bado nilikuwa nakabiliwa na vikwazo kutoka kwa watu wangu. Niliketi kwenye kiti mbele ya meza yake na kwa mara nyingine Suleiman alitaka kujua ni kipi kilichojiri kule Manyoni. Lakini kabla sijamueleza kilichojiri Manyoni, nilimuuliza swali langu la msingi.
“Suleiman...hivi kuna barua yoyote iliyotoka hapa ofisini kwenda kwa mkuu wa wilaya Manyoni wakati tukiwa kule?”
Suleiman alionekana kutoelewa maana ya swali lile, lakini niliona kuwa hakuwa akielewa lolote juu ya kuwepo kwa barua hiyo.
“Si kuna barua iliyotoka hapa ambayo mlipewa kwa ajili ya kuiwasilisha kwa Mkuu wa wilaya baada ya kufika huko?” Alinijibu kwa swali. Nilimjibu kuwa ni kweli, lakini nilikuwa nauliza kuwa iwapo kuna nyingine iliyotumwa kwa fax kutokea pale ofisini kwenda kule kwa mkuu wa wilaya baada ya sisi kufika kule.
“Hakuna. Ni wapi umepata mawazo hayo, na ni nani aliyeandika barua hiyo?” Alinijibu kwa uhakika kabisa na kunihoji zaidi.
“Nimeiona hiyo barua kwa mkuu wa wilaya na imesainiwa na Mkurugenzi mwenyewe...nimeiona saini yake kabisa!” Nilimjibu kwa uhakika.
“Hakuna, haiwezekani. Barua zote za Mkurugenzi huwa nazitayarisha mimi, sekretari wake anazitaipu kwa kompyuta, na yeye anasaini tu...huo ndio utaratibu, na hakuna barua yoyote iliyotoka hapa kwenda Manyoni baada ya nyie kuondoka.” Suleiman alinijibu, nami nilimuelewa kwani huo ndio utaratibu uliokuwepo pale ofisini.
Kwa hiyo ile barua ya akina Martin Lundi ilikuwa imeghushiwa.
“Hebu nieleze ni nini hasa kilichotokea huko Manyoni Tigga? Kwa sababu hapa wamekuja wana usalama wakikusaka kuhusiana na mauaji ya wenzetu kule msituni, na tuhuma nyingine za ajabu sana kuwa ulifanya fujo katika ofisi ya mkuu wa wilaya...infact, wamesema kabisa kuwa wewe ni fugitive from justice, sasa hiyo ni hali mbaya sana Tigga, na inatuweka sisi kama waajiri wako katika wakati mgumu sana.”
Nilimtazama Suleiman kwa muda nisijue nimueleze nini, kwani yale maneno yake yalinitisha sana, ingawa taarifa yake haikuwa ngeni kabisa akilini mwangu.
Fugitive from Justice Nililitafakari lile neno na mwili ukanisisimka.
Mkimbizi kutoka katika mikono ya sheria.
“Naona ni bora nikitoa maelezo ya safari yetu na mambo yaliyotokea kwa Mkurugenzi, Suleiman...nadhani na wewe utahitajika uwepo.” Nilimwambia huku nikiinuka. Suleiman alionekana kusita kidogo, kisha akaafikiana nami, lakini kwa mashaka. Sikuelewa ni kwa nini alisita, ila niliona kuwa sikuhitajika kutumia muda mwingi sana pale ofisini. Baada ya kutoa maelezo yangu niliazimia kuchukua likizo ili nipate muda wa kuzidi kutafuta namna ya kukabiliana na mtihani huu ulionikabili, na kujaribu kutafuta ukweli wa matukio yale ya ajabu.
Tulipoingia ofisini kwa Mkurugenzi tu nilihisi kuwa nilikuwa nimeingia kwenye matatizo, kwani moja kwa moja niliona kuwa yule mzee wa makamu ambaye tulizoea kumwita “mkuu” tukimaanisha mkuu wa idara, alikuwa ameshadhamiria kunituhumu, bila shaka akiwa na taarifa za mambo niliyofanya kule Manyoni, na zile taarifa potofu zilizotoka kwenye gazeti siku chache zilizopita. Baada ya kumuamkia aliniuliza iwapo ndio siku ile nilikuwa nimeingia kutoka Manyoni, nikamjibu kuwa niliingia jijini jioni ya siku moja iliyopita. Yule mzee ambaye huwa tunamuogopa sana kutokana na mtindo wake wa uongozi ambao ni wa ukali na amri, alimwita katibu muhtasi wake na kuniambia nitoe maelezo ya safari yangu na mambo yote yaliyotokea huko Manyoni, wakati yule katibu muhtasi wake akinukuu maelezo yangu kwenye kompyuta.
Nilieleza mkasa wote wa safari yetu na mambo yote yaliyotokea kule Manyoni tangu pale nilipoishuhudia ile helikopta ikitua kule msituni, jinsi akina Ibrahima Geresha walivyowekwa chini ya ulinzi na wale watu wabaya ambao mmoja wao hivi sasa nilimjua kwa jina la Martin Lundi. Wote walikuwa kimya kabisa wakisikiliza maelezo yangu, nami nilikuwa makini sana kwa kutoeleza mambo niliyoongea na yule mtu asiye na jina kule msituni wakati wale wauaji walipoondoka na wenzangu.Nikawaelezea jinsi nilivyorudi kule kambini kwetu na kuwakuta wenzangu wakiwa wameuawa na kudonolewa na ile midege mibaya. Hapa nilishindwa kujizuia, na machozi yalinitoka upya, na mara kadhaa nililazimika kushindwa kuendelea na maelezo yangu nikielemewa na kwikwi, na niliona hata yule katibu muhtasi wa kamishna naye alikuwa akitirikwa na machozi. Nilielezea jinsi nilivyolikuta begi langu nje ya hema na jinsi nilivyoweza kufika hadi ofisini kwa mkuu wa wilaya, na mambo yaliyotokea huko.
Hapa niliona kuwa Kamishna alizidisha umakini, na nikaelezea juu ya ile barua iliyotumwa kwa fax kwa mkuu wa wilaya ikisemekana kuwa imetokea pale ofisini.
“Hakuna barua ya aina hiyo msichana! Huo ni uzushi sasa!” Hapo Kamishna aliingilia kati kwa ukali. Nilimtazama kwa kutoelewa.
“Uzushi kivipi mkuu...? Kwamba hiyo barua haikuwepo, au unadhani kuwa mimi ninazusha juu ya kuwepo kwa barua hiyo?” Nilimuuliza kwa mashaka.
“Uzushi! Hakukuwa na barua ya aina hiyo iliyotoka hapa ofisini kwenda huko kwa Mkuu wa wilaya...labda wewe unataka kutuchanganya tu kwa kuleta hadithi za barua za ajabu ajabu...”
“Aaah! Mkuu! Ni wewe ndiye uliyesaini ile barua, na sehemu ya maelezo yangu yaliyotolewa kwenye ile barua yalikuwa ni yale yanayoweza kupatikana kwenye faili langu la ajira hapa ofisini!” Nilimjibu kwa jazba, kisha nikaendelea kuwaeleza jinsi nilivyoikana ile barua mbele ya mkuu wa wilaya kuwa ni ya kughushi. “Hakukuwa na barua ya aina hiyo!” Kamishna alizidi kusisitiza, kisha akaendelea, “Unaweza kutuonesha hiyo barua?”
Nilimjibu kuwa niliiacha pale pale kwa mkuu wa wilaya, na nikamwambia kuwa nina imani itakuwepo kwa mkuu wa wilaya iwapo wataamua kuifuatilia, kwani kule walikuwa wameamini kabisa kuwa ilikuwa imetokea pale ofisini.
Mkuu alinitazama kwa muda huku nikiona wazi kuwa alikuwa haniamini. Kisha bila ya kusema neno aliniashiria niendelee na maelezo yangu.
Nilieleza kisa chote hadi kufikia pale nilipoingia ofisini asubuhi ile.
Baada ya hapo ofisi yote ilibaki kimya. Kamishna alinitazama kwa muda mrefu wakati yule binti aliyekuwa akinukuu maelezo yangu akitoa nakala ya yale maelezo na kumkabidhi. Aliyatazama kwa muda na kunipatia akiniambia niyapitie iwapo yalikuwa ni sawa na nilivyoeleza. Nilisoma maelezo yale yaliyotoka kurasa saba, na kutoa marekebisho machache ambayo yule dada aliyarekebisha kwenye kompyuta yake na kutoa nakala nyingine ambayo ilikuwa sawa.
Kwa makusudi kabisa nilikuwa nimeacha kuelezea juu kuwepo kwa mkanda wa video uliokuwa na ushahidi wa yale mauaji ya kule msituni.
Niliweka saini yangu chini ya maelezo yale. Kisha Suleiman Kondo naye alisaini kama shahidi aliyekuwepo wakati nikitoa maelezo yale, na Kamishna mwenyewe. Yule dada aliambiwa arudi ofisini kwake na kuendelea na kazi zake.
Kilichofuatia ni mahojiano marefu baina yangu na Kamishna ambayo kwa ufupi yalikuwa yanahitaji kuelewa mtazamo wangu juu ya swala lile. Kwa nini yale mauaji yatokee, kwa nini wale wauaji waghushi ile barua iliyokuwa ikinitangazia mimi ule ugonjwa wa akili, kwa nini mkuu wa wilaya alionekana kuwaamini zaidi wale madaktari badala yangu. Sikuwa na majibu ya kuwatosheleza juu ya mengi ya maswali yao, kwani mimi mwenyewe nilikuwa natafuta majibu hayo, ila jibu kubwa nililowapa lilikuwa ni juu ya sababu nilizodhani kuwa ziliwafanya wanipakazie ule ugonjwa wa uongo, kuwa walifanya kusudi kunipakazia ugonjwa huo ili taarifa nitakazotoa dhidi yao na mambo niliyoona wakiyafanya kule msituni zitiliwe mashaka na kila mtu.
Swali kubwa kabisa aliloniuliza mkuu wangu wa kazi ni kwa nini muda wote tangu mambo yale yalipojitokeza sikuenda kuripoti polisi. Hili kwake lilikuwa ni jambo la muhimu sana, na alishindwa kuelewa kuwa kama sikuwa na matatizo, kwa nini nilishindwa kwenda polisi.
“Mkuu wale watu tayari walikwishaonesha kuwa wana namna ya kuingiliana na vyombo vya dola kwa maslahi yao! Nilishindwa kwenda polisi kienyeji tu bila ya kuwa na uhakika wa hali nitakayoikuta huko...” Nilijaribu kuwaelewesha lakini niliona kuwa swala lile lilikuwa gumu kueleweka. Sikuweza kuwaeleza kuwa nilishindwa kwenda polisi kwa sababu nilikuwa nahofia usalama wa ule mkanda wa video wenye ushahidi, kuwa huenda ungeangukia mikononi mwa askari mwenye uhusiano na wale wauaji. Kwa usalama wangu, sikuwaeleza kabisa juu ya kuwepo kwa huo mkanda tangu mwanzo, sasa wangeelewa vipi? Ilikuwa ni hali ngumu.
“Tigga, samahani sana binti, lakini lazima nikueleze kuwa hii taarifa yako ni ngumu sana kuiamini...mimi binafsi naiona kama masimulizi ya filamu ya kubuni tu.” Hatimaye Mkurugenzi aliniambia, na nikaona na afisa utumishi wetu, Suleiman Kondo naye akitikisa kichwa kuafikiana naye.
“Sasa nifanyeje wakuu wangu? Maana mi’ nimekuja kwenu kwa msaada...” Nilisema huku nikiwatazama kwa zamu. Badala ya kunijibu, Mkurugenzi aliinuka na kuingia chooni, ambacho kilikuwa kimejengwa humo humo ndani ya ofisi yake.
Kama Masterbedroom ya Kelvin...
Tulibaki na Suleiman Kondo mle ofisini, nami nikajaribu kumdadisi juu ya hatua iliyopaswa kufuatwa.Lakini Suleiman alionekana kuwa na mashaka sana na kuongea lolote na mimi tukiwa peke yetu. Nilianza kujiuliza kwa nini, lakini mara nilipata jibu na moyo ulinifa ganzi.
Mkurugenzi alitoka kule chooni na kuingia tena pale ofisini akiwa amefuatiwa na afisa wa jeshi la polisi!
“Ni wajibu wangu kukukabidhi kwenye mikono ya sheria Tigga, sehemu pekee ambayo nadhani swala lako linaweza kushughulikiwa ipasavyo.” Mkurugenzi aliniambia huku akimtanguliza yule afisa wa polisi.
Mate yalinikauka na nikapigwa na butwaa. Nilimtazama kwa mshangao, kisha nikamtazama yule askari na kumgeukia Suleiman Kondo ambaye alinitazama kidogo na kuinamisha kichwa. Nikamgeukia tena yule afisa wa jeshi la polisi.
“Mkurugenzi...” Nilianza kuongea kwa sauti ya kukwaruza huku moyo ukinipiga vibaya sana na huku nikisimama kutoka kwenye kiti changu.
Haraka sana yule afisa wa polisi alipiga hatua kubwa na kuwahi kusimama mlangoni akinizuia nisitoke mle ndani.
Nilikuwa nimenaswa, na hata wazo hilo liliponijia, akili yangu ilienda kwenye ule mkanda wa video uliokuwa ndani ya mkoba wangu uliokuwa ukining’inia begani kwangu.
“Sina la kukueleza Tigga, na naomba uelewe kuwa hapa natimiza wajibu wangu. Na kwa mujibu wa sheria za kazi, kuazia muda utakaokuwa chini ya ulinzi, ajira yako itasimama mpaka hapo itakapoamuliwa vinginevyo, Suleiman atakupatia barua rasmi kukuarifu juu ya hilo na taratibu nyingine za kisheria.” Mkurugenzi aliniambia kwa upole lakini kwa mkazo usioyumba kabisa.
“Lakini...lakini...si mmepata maelezo yangu? Kwa nini tena nikamatwe...?”
“Tigga Mumba?” Yule askari aliongea kwa mara ya kwanza. Nilimgeukia huku macho yakiwa yamenitoka pima. Nilimtazama kwa umakini. Alikuwa amevaa mavazi wanayovaa askari wa ngazi za juu katika jeshi la polisi. Alikuwa mrefu na nilimhisi kuwa alikuwa katika umri wa kati wa ujana.
Alikuwa na sura ya kuvutia hasa, na tofauti na askari wengi, yeye alikuwa amechonga ndevu zake vizuri katika ile staili ya Timberland ambayo mabrazameni wengi huwa wanaipenda. Sasa askari gani ananyoa ndevu kwa staili ya timberland!
Hivi huyu ni askari wa kweli au ni miongoni mwa wale wanaomsaidia Martin Lundi moungo?
Nilimkumbuka yule askari wa kike aliyeacha kunikamata kule gesti usiku uliopita.
“Mkurugenzi! Hu...huyu si askari wa kweli! Anaweza kuwa miongoni mwao! Usimruhusu anichuku...”
“Kuanzia sasa nakuweka chini ya ulinzi kwa kosa la kutoroka mikono halali ya sheria ambayo ilikutaka uisaidie polisi katika swala la mauaji yaliyotokea Manyoni.” Yule afisa alinieleza kwa ukakamavu bila ya kujali mapingamizi yangu.
“Lini? Lini nilitoroka mikono ya sheria? Huo ni uongo! Uongo mkubwa...” Nilibwata huku nikihaha mle ndani ilhali yule askari akiwa amedhibiti njia yangu ya kutorokea.
“Pia nakuweka chini ya ulinzi kwa kosa la kufanya vurugu zilizomsababishia mkuu wa wilaya ya Manyoni maumivu makali wakati ukiwa katika harakati za kuikimbia mikono ya sheria huko Manyoni.” Aliendelea kunisomea makosa yangu yule afisa wa polisi ambaye kwa hakika nilimuona kuwa ni muongo tu kama wale wengine.
Miguu iliniisha nguvu nikajikuta nikijibwaga kwenye kiti.
Yule askari alininyanyua kwa nguvu kutoka pale kwenye kiti na kuniongoza nje ya ofisi ile akiwa amenishika mkono wangu kwa nguvu juu kidogo ya kiwiko changu.
Oh! Mungu wangu, huu ndio mwisho wangu!
--
Yule afisa wa polisi aliniongoza kuniteremsha ngazi kuelekea ghorofa ya chini ambapo ndio kulikuwa na uelekeo wa kutoka nje ya jengo lile. Kwenye ngazi tulipishana na binti mmoja wa kampuni ya ufagizi iitwayo WE KLEEN OFFICE CLEANERS na ambayo ilikuwa mkataba wa kufanya usafi na ufagizi katika ofisi yetu. Nilijionakama niliyekuwa ndotoni na sikuwa na ujanja. Mkono ulionikamata ulikuwa imara na wenye nguvu, na niliongozana na yule askari huku nikijaribu bila mafanikio kuilazimisha akili yangu inishauri ni hatua gani nichukue ili kujikomboa kutoka katika mtego ule.
Wafanyakazi wenzangu walikuwa wakinichungulia kutoka kwenye milango ya vyumba vyao vya ofisi kwa wasiwasi uliochanganyika na udaku. Nilizungusha macho na kumtazama tena yule askari aliyenikamata. Mimi ni mrefu kuliko wasichana wengi, lakini huyu bwana alikuwa mrefu zaidi kwani niliona kuwa kichwa changu kilikuwa kinaishia juu kidogo ya bega lake. Nilipata harufu ya marashi ghali sana ya kiume ikitokea kwenye mavazi yake ya kiaskari, na hapo nikawa na hakika kabisa kwamba yule mtu hakuwa afisa wa jeshi la polisi kweli, na hata kama alikuwa ni afisa wa kweli, basi alikuwa ni miongoni mwa wafuasi wa Martin Lundi, na si vinginevyo.
Nifanye nini Mungu wangu!
ITAENDELEA
 
SEHEMU YA KUMI NA SITA.

. Mimi ni mrefu kuliko wasichana wengi, lakini huyu bwana alikuwa mrefu zaidi kwani niliona kuwa kichwa changu kilikuwa kinaishia juu kidogo ya bega lake. Nilipata harufu ya marashi ghali sana ya kiume ikitokea kwenye mavazi yake ya kiaskari, na hapo nikawa na hakika kabisa kwamba yule mtu hakuwa afisa wa jeshi la polisi kweli, na hata kama alikuwa ni afisa wa kweli, basi alikuwa ni miongoni mwa wafuasi wa Martin Lundi, na si vinginevyo.
Nifanye nini Mungu wangu!
Tulipofika mwisho wa zile ngazi tulikata kushoto ambapo aliniongoza kufuata kijikorido kidogo kilichoelekea kwenye mlango mdogo wa dharura ambao ulitokea moja kwa moja kwenye sehemu ya kuegeshea magari ndani ya uzio wa jumba la makumbusho. Mbele yetu, upande wa pili wa ile korido niliona kuna mfanyakazi mwingine wa ile kampuni ya kufanya usafi pale ofisini akiwa ameinama akipiga deki. Kwa pale tulipokuwa, niliweza kuona tu yale maandishi makubwa kwenye mgongo wa fulana yake yaliyokuwa yakiitambulisha ile kampuni ya usafi na ufagizi. Na hata pale tulipochukua uelekeo wa ule mlango mdogo wa dharura, naye aliinuka na kubeba ndoo yake ya maji pamoja na mifagio yake maalum ya kupigia deki na kuelekea kule tulipokuwa tukielekea na kuanza kupiga deki ile korido ndogo tuliyokuwa tukiiendea. Tulizidi kuelekea kule mlangoni huku yule afisa akianza kuchomoa pingu kutoka kwenye mfuko wa suruali, nami nikaingiwa na woga maradufu. Sijawahi kufungwa pingu hata siku moja maishani mwangu, na sio siri, pingu bora uisikie tu watu wakiitaja, lakini kuiona kwa macho inatisha si mchezo. Nilianza kutetemeka huku miguu ikiniwia mizito kuliko kawaida.
“Tembea vizuri mwanamke...!” Yule afisa alinikemea huku akinivuta mkono wangu kwa mkono wake mmoja hali ule mwingine ukiweka pingu yake sawa. Na hapo hapo wote tulishitushwa na kishindo kikubwa. Yule mfagizi alikuwa akiinua ndoo yake ili kutupisha, lakini ghafla ile ndoo ilimponyoka na kuanguka sakafuni kwa kelele kubwa huku ikimwaga na kurusha maji sehemu yote, akilowanisha miguu ya suruali yangu na ya yule askari.
Niliruka kwa mshituko huku nikitoa sauti ya woga hali yule afisa wa polisi akiropoka neno la kulaani kitendo kile naye akiruka pembeni bila kuniachia na kutazama jinsi suruali yake ilivyotota maji. Aliinua uso wake kwa hasira na kumtazama yule mfagizi na hapo hapo yeye na mimi wote tuliachia midomo wazi kwa butwaa.
Macho ya nyoka alikuwa ametupa ile mifagio yake na sasa alikuwa ametuelekezea bastola kubwa iliyotisha huku akiwa amekenua meno kwa ghadhabu. Yule afisa wa polisi alikunja uso kwa hasira na mshangao.Alinigeukia, akaona jinsi nami nilivyohamanika, akamgeukia tena yule mtu mwenye bastola mbele yetu.
Nilichoka!
Yaani kumbe muda wote ule nilikuwa nikimtazama macho ya nyoka na sikumjua. Nilipeleka macho kwenye ile fulana nyeupe aliyovaa, ikiwa na maandishi WE KLEEN OFFICE CLEANERS kifuani, na suruali ya jeans nyeusi ambayo ndio sare wanazovaa wale wafanyakazi wa ile kampuni ya usafi na ufagizi.
Eeh! Hawa watu ni kiboko!
“Wewe ni nani...na Unataka nini...? Mimi ni afisa wa ngazi ya juu wa polisi, na nakuamuru uweke chini hiyo silaha yako upe...” Yule afisa wa polisi alianza kumuambia yule muuaji huku akiwa ameinua mikono yake usawa wa mabega yake kuonesha kuwa hakuwa na silaha, akiachia ile pingu yake ianguke sakafuni, lakini macho ya nyoka alimkatisha kikatili.
“Kimya! Sitojali iwapo ni afisa wa ngazi ya mbinguni au ya ardhini! Usipotii maelekezo yangu nakuua sasa hivi!” Alimfokea, na niliona wazi kuwa alikuwa hatanii. Bila kujijua nilijikuta nikijificha mgongoni kwa yule afisa wa jeshi la polisi huku nikijiuliza kuwa iwapo naye alikuwa ni mfuasi wa Martin Lundi, vije tena Macho ya nyoka amtishie bastola? Sikuwa na shaka kabisa kuwa mimi ndiye niliyekuwa nikitakiwa pale, na si yule askari. Nilipata wazo kuwa muda wote Macho ya nyoka alikuwa akinisubiri pale ofisini akijifanya naye ni mfagizi akijua kuwa kuna siku ningetokea. Bahati leo nimetokea na kukutwa na huyu askari, kwani sasa ilinijia wazi kuwa yule mtu alikuwa ni askari wa kweli.
“Oke...haina haja ya kugombana. Unataka nini...?” Yule askari alimuuliza Macho ya nyoka kwa tahadhari kubwa huku akimtazama usoni.
“Namtaka huyo mwanamke, na sitaki uniingilie, kwani sitasita kukuua!” Macho ya nyoka alifoka.
“Hapana! Usimkubalie! Ni muuaji huyo...” Niliropoka kwa jazba huku nikimng’ang’ania mgongoni yule askari.
“Kelele malaya wee! Kuja hapa! Upesi!” Macho ya nyoka alinikemea huku akiniashiria nimfuate kwa ile bastola yake.
“Sijui unamtakia nini huyu binti, lakini najua kuwa unafanya kosa kubwa sana. Huyu binti yuko chini ya ulinzi, na we’ unataka kumtorosha...mna uhusiano gani?” Yule afisa alimuuliza taratibu huku nikiuhisi mwili wake ukikakamaa.
“Sina uhusiano naye wowote! Huyo ni muuaji...namjua sana! Ndiye aliyeua...anataka kuniua!” Nilipayuka kwa jazba kumuambia yule askari huku nikimtazama Macho ya Nyoka kwa hofu kubwa. Nilijaribu kuangaza nyuma yetu kuona iwapo akina Suleiman waliweza kutuona, lakini tulikuwa tumeshapinda kona na hivyo watu wote waliokuwepo kule upande wa vyumba vya ofisi hawakuweza kutuona. Tulikuwa tumejinasa wenyewe kwenye kona ya muuaji.
“Afande kaa chini! Msichana njoo kwangu haraka!” Macho ya Nyoka aliamrisha huku nikimuona akiukaza ule mkono uliokuwa umeishika bastola hali macho yake ya kuogofya yakitoa mng’ao wa chuki kubwa. Sikuwa na shaka kabisa kuwa tukizidi kubisha tu ataua mtu.
Huyu ni muuaji wa kuzaliwa hasa...
Na nilipokuwa nikimtazama, nilipata hisia isiyo shaka kabisa kuwa alikuwa anatafuta sababu tu ya kuua mtu.
“Mimi chini sikai, Utafanyaje?” Yule askari alimuuliza kwa sauti ya upole sana, kama kwamba alikuwa anaongea jambo la kawaida na mtu asiye hatari, nami nikazidiwa na woga.
“Hah! Atakuua huyo afande! Atatuua sote...” Niliropoka kwa woga, na hapo nilishitukia kitu kama upepo tu kikipita kwa kasi na bastola ya macho ya nyoka ikisambaratika sakafuni kwa kelele, kwani yule afisa alirusha teke lililoipangusa ile bastola kutoka mkononi mwake kama mzaha. Mimi na Macho ya Nyoka tulijikuta tukizubaa kwa kama sekunde hivi wakati akili zikijaribu kuelewa kilichotokea, kisha Macho ya Nyoka alikurupuka ghafla huku akinguruma kwa ghadhabu kuirukia bastola yake iliyotupwa sakafuni, lakini yule afisa wa polisi alikuwa amejiandaa kwani alimrushia teke la kifua lililomtupa yule muuaji hadi ukutani, naye akajirusha kuiwahi ile bastola ya yule muuaji.
Macho ya nyoka alijiinua haraka na kujirusha miguuni kwa yule afande kabla hajaifikia ile bastola, na wote wawili wakapiga mwereka mzito pale sakafuni. Sasa na mimi nilizinduka na nikaanza kupiga kelele, nikiwa nimejibanza kwenye kona ya ile korido huku macho yakiwa yamenitoka pima nikishuhudia wale wanaume wakigaragazana sakafuni kila mmoja akijaribu kumzuia mwenzake asiiwahi ile bastola. Kwa pale nilipokuwa nimesimama, niliona kuwa Macho ya Nyoka alikuwa amemlalia juu yule askari huku akinyoosha mkono wake kuiwahi ile bastola, wakati yule askari akiuvuta mkono wa Macho ya Nyoka usiifikie ile bastola. Na wakati huo huo niliona kwa mkono wake mwingine akijaribu kutoa bastola yake iliyokuwa kiunoni mwake, lakini mguu wa Macho ya Nyoka ulikuwa umeubana ule mkono hivyo ilimuwia vigumu kufanikisha lengo lake.
Hapo ilinijia kumbukumbu ya lile tukio la kule msituni baina ya Macho ya Nyoka na yule mtu asiye na jina. Tukio lililopelekea yule mtu kupoteza maisha yake. Kumbukumbu ile iliniletea woga mkubwa na nikahofia kushuhudia tena tukio kama lile.
Kwa nini kifo kinifuate kila mahali?
Nilikurupuka kutoka kwenye kona ya ile korido nilipokuwa nimejibanza na kujaribu kuwaruka wale jamaa ili niiwahi ile bastola, na wakati huo huo yule muuaji alijiinua akijaribu kuinuka na miguu yangu ikampamia kwenye ubavu wake nami nikapiga mwereka mkubwa huku nikiachia yowe la woga. Nilijiinua kwa kupepesuka na kuegemea ukuta huku macho yakinitembea. Macho ya Nyoka alikuwa ameshainuka akiwa ameikamata tena ile bastola yake na sasa ilikuwa ikimuelekea usoni yule askari ambaye alibaki akiwa amepiga goti pale sakafuni huku akitweta, akimtazama kwa hasira. Niliona kuwa alikuwa hana ujanja. Macho ya Nyoka hakutaka kuongea zaidi. Na niliona kuwa alikuwa ameghadhibika kupita kawaida.Akili yake ilikuwa imemuelekea yule askari na kwa muda ule alikuwa hana habari na mimi. Alifyatua kitunza usalama cha ile bastola na uso wake ulimbadilika. Macho ya Nyoka alikuwa ameazimia kuua!
Huku nikiwa nimetumbua macho na moyo ukinipiga kwa woga niliinyakua ile ndoo ya bati aliyokuwa akipigia deki na kumpiga nayo kichwani kwa nguvu zangu zote huku nikitoa ukelele wa hasira iliyochanganyika na woga. Macho ya Nyoka alitoa mguno hafifu na miguu ikamlegea huku bastola ikimtoka mkononi na damu ikimchuruzika kutoka upande wa kichwa chake pale pigo langu lilipotua. Haraka sana yule afisa wa polisi aliruka na kumshindilia ngumi ya taya iliyopeleka chini mzima mzima, na wakati huo huo kelele za wafanyakazi wenzangu pale ofisini zilinijia huku wengine wakianza kuja eneo lile mbio wakiwa wamejaa udadisi mkubwa.
Nilibaki nikitazama kwa woga wakati yule afisa wa polisi akimnyanyua Macho ya Nyoka aliyeonekana wazi kuwa amepumbazwa na mapigo yale na kumbandika ile pingu iliyokuwa inifunge mimi mkono mmoja na kumgeuza kwa nguvu kimgongo mgongo ili amfuge na ule mkono wa pili kwa nyuma.
Hilo lilikuwa kosa.
Macho ya Nyoka aligeuka na pigo zito ambalo mpaka sasa siwezi kuelewa kama lilikuwa ni ngumi, teke au kiwiko cha mkono. Nilichoona ni yule afisa wa polisi akitoa yowe huku akijipinda kwa maumivu na kupepesuka. Hapo hapo Macho ya Nyoka aliruka na kumtamdika teke la kichwa lililompeleka ukutani kwa kishindo yule askari. Nilipiga kelele na hapo hapo wale wafanyakazi wenzangu pamoja na wale wafanyakazi wengine wa ile kampuni ya usafi walitimua mbio kurudi walipotoka huku kila mmoja akipiga kelele kivyake. Macho ya nyoka aliruka hatua mbili za nyuma nyuma na kunigeukia huku akininyooshea kidole kwa hasira bila ya kusema neno, na katika macho yale, niliona ahadi isiyotamkwa ya kifo cha mateso kutoka kwa Macho ya Nyoka. Kisha aligeuka na kutimua mbio kutoka nje ya jengo lile kutumia ule mlango wa dharura tuliokuwa tukiuelekea hapo awali.
“Don’t Move!” Yule afisa wa polisi alininyooshea kidole na kuniambia huku akiikwapua ile bastola ya macho ya nyoka na kutoka mbio kumfuata yule muuaji, akimpigia kelele asimame.
Sikuzubaa. Nililiweka sawa begi langu mgongoni na kutimua mbio kuelekea upande wa lango kuu la kuingilia na kutokea ndani ya jengo lile, nikipuuzia kabisa ile amri ya yule afisa wa polisi. Mazingira yalikuwa hayaeleweki, nami sikuwa tayari kuhatarisha usalama wangu zaidi katika mazingira kama yale. Suleiman Kondo alinipigia kelele nisikimbie lakini sikumjali. Niliendelea kutimua mbio.
“Mkamateni huyooo!” Suleiman Kondo alipiga kelele na nikaona wafanyakazi wenzangu pamoja na baadhi ya wale wafanyakazi wa ile kampuni ya usafi ambayo Macho ya Nyoka alifanikiwa kujipenyeza ili aweze kunivizia pale ofisini wakitanda mbele yangu na kunizibia njia.
“Tigga don’t run! Hii ni kwa usalama wako!” Suleiman Kondo alinipigia kelele huku akihangaika kunikimbilia kwa taabu kutokana na mwili wake mzito. Nilipagawa. Niligeuka na kutaka kurudi kule nilipotokea, nako nikakuta kuna baadhi ya wafanyakazi wakiwa wamefanya ukuta. Nilichanganyikiwa, jasho likinivuja na moyo ukinienda kasi kuliko ilivyowahi kutokea. Nilikuwa kama chui aliyezingirwa na wawindaji wenye ghadhabu. Nilimgeukia Suleiman Kondo, nikaona alikuwa ameungana na Mkurugenzi wakinikodolea macho.
“Tigga! Usifanye tena kosa hilo...uko chini ya ulinzi! Utazidi kujiwekea mazingira mazito!” Suleiman alinipigia kelele. Na hata pale Suleiman alipomalizia kauli yake nilisikia mlipuko mkubwa wa bastola kutokea kule nje ambapo yule afisa wa jeshi la polisi alikuwa akikimbizana na Macho ya Nyoka huku vilio vya woga vikitawala mle ndani kutoka kwa wafanyakazi wenzangu. Sikutaka kusubiri kujua ni nani aliyepigwa risasi kati ya yule askari na yule muuaji niliyempachika jina la Macho ya Nyoka.Nilikwapua mtungi mkubwa wa maua uliokuwa pale kwenye korido kama sehemu ya mapambo ya ofisi na kwa nguvu zangu zote niliutupia kwenye dirisha kubwa la kioo lililokuwa karibu yangu na kulipasua vibaya, likiacha uwazi mpana sehemu iliyokuwa na kioo.
Kelele zilitawala mle ndani nami nikajitupa nje ya dirisha lile na kuangukia nje ya jengo ambako nilijiinua haraka na kutoka mbio. Nilijipenyeza kwenye uzio wa nyuma ya jengo lile uliofanywa kwa aina ya miti kama michongoma na kutokea kwenye eneo la wazi lililokuwa limetapakaa majani yaliyokuwa yakitunzwa vizuri. Nilizidi kutimua mbio huku akili ikinizunguka bila ya kujua ni kwa nini niliamua kufanya vile na nini ingekuwa matokeo yake.
Lakini nilichojali ni kuwa mbali na eneo lile ambalo lilishaingia walakini kuhusiana na usalama wangu. Nilikimbia nikijipenyeza kwenye uzio mwingine wa miti na kutokea kwenye mtaa mmoja mfupi na uliokuwa kimya sana. Nilihaha kwa muda, nikiangaza kulia na kushoto, kisha nikachomoka kasi kuelekea kushoto kwangu na kukutana na barabara nyingine ya lami, ambapo pia nilikutana na njia panda. Nilitimua mabio kuelekea kulia huku magari yakinipigia honi na nikisikia msuguano wa tairi za gari wakati zikifunga breki kwa ghafla. Sikugeuka nyuma wala sikupunguza mwendo.Nilikua natoka kasi kweli kweli. Niliibukia katika eneo nililolifahamu ambapo nililiona jengo la Internationa House likiwa kulia kwangu. Nilikunja kushoto kwenye makutano ya ile barabara niliyotoka nayo na ile ya kuelekea kwenye lile jengo la International House na Holiday Inn na kuanza kutembea kwa mwendo wa haraka huku nikikimbia kidogo kidogo, nikichukua uelekeo wa jengo la PPF Tower. Jasho lilikuwa likinitirirka vibaya sana na sina hata haja ya kukuambia jinsi moyo ulivyokuwa ukinipiga.
ITAENDELEA
 
SEHEMU YA KUMI NA SABA.

Sikugeuka nyuma wala sikupunguza mwendo.Nilikua natoka kasi kweli kweli. Niliibukia katika eneo nililolifahamu ambapo nililiona jengo la Internationa House likiwa kulia kwangu. Nilikunja kushoto kwenye makutano ya ile barabara niliyotoka nayo na ile ya kuelekea kwenye lile jengo la International House na Holiday Inn na kuanza kutembea kwa mwendo wa haraka huku nikikimbia kidogo kidogo, nikichukua uelekeo wa jengo la PPF Tower. Jasho lilikuwa likinitirirka vibaya sana na sina hata haja ya kukuambia jinsi moyo ulivyokuwa ukinipiga. Miguu ilikuwa ikinitetemeka na nikahisi maumivu kwenye sehemu ya juu ya mkono wangu wa kulia. Nilipojitazama nikaona kuwa nilikuwa nimejichanja na kipande cha kioo pale niliporuka dirishani. Kioo kilichana mkono wa lile koti langu gumu la jeans na kwa kiasi kikubwa kabisa lile koti lilipunguza makali ya kile kioo na hivyo kupunguza ukubwa wa lile jeraha ambalo lilikuwa likichuruzika damu kidogo, lakini hilo nililiona kuwa ni swala dogo sana. Niliangaza huku na huko, kila mara nikitaraji kusikia mtu akinipigia ukelele kuwa nisimame au akiwapigia kelele wapita njia wengine kuwa wanikamate.
Nililipita duka la Imalaseko na kuongeza kasi kuelekea barabara kubwa ya Azikiwe. Hatua kadhaa mbele yangu niliona daladala kubwa aina ya Isuzu Journey likisimama kwenye makutano ya ile barabara niliyokuwapo na ile ya Azikiwe kuelekea posta ya zamani, na kondakta akinipigia kelele akiniuliza iwapo nilikuwa ni msafiri. Kwa rangi ya mstari wa lile basi, niliona kuwa lilikuwa ni basi linalofanya safari za Mwananyamala-Posta.Sikufikiri zaidi, nilimpungia mkono anisubiri huku nikiongeza mbio.
Kwa wakati ule, basi lolote lingekuwa muafaka kwangu. Niliparamia lile basi kwa pupa nalo likaondoka kwa kasi eneo lile kuelekea maeneo ya posta ya zamani, huku yule kondakta akishangilia na kurukaruka mlangoni, nami nikijibwaga kwenye kiti nikitweta huku nikijifuta jasho kwa mkono wa koti langu. Tulipofika eneo la posta ya zamani nilipatwa na kihoro baada ya kuona tukisimamishwa na askari wa usalama barabarani. Niliangaza huku na huko na nikaona magari yote yaliyokuwa pale barabarani yalikuwa yamesimama, yakifanya foleni kubwa. Nilichanganyikiwa vibaya sana. Niliinuka na kutaka kuteremka, lakini konda alinizuia, akiniuliza iwapo nilikuwa nataka kuwalipisha faini ya elfu ishirini kwa kuteremsha abiria sehemu isiyo kituo, tena mbele ya wana usalama. Niliketi kwenye kiti huku akili ikinizunguka.
Ina maana huu ni msako kwa ajili yangu?
Nilitoa kichwa nje ya dirisha na kutazama kule mbele tulipokuwa tukielekea. Mwili ulinifa ganzi niliposhuhudia askari wa jeshi la polisi zaidi ya sita wakiwa wameshika bunduki aina ya SMG wakiwa wametanda mbele ya barabara, baina yao wakiwamo askari wa usalama barabarani.
Nimekwisha!
Nilimgeukia konda na kumuuliza kwa sauti ambayo nilishindwa kuamini kuwa ni yangu.
“Ni...ni kitu gani? Kuna nini mbona tumesimamishwa?”
Konda alinitazama kwa muda kabla ya kuniuliza. “Anti vipi...? Una haraka sana nini?” Nilimtazama kidogo kisha nikapeleka uso wangu pembeni, asije akanishika sura halafu akaja kuniletea matatizo hapo baadaye.
“Hao ni wenye nchi wanapita dada yangu, eeeh!” Yule konda aliniambia baada ya kuona kuwa sikumjibu hapo awali, kisha akaongezea. “Hii ndio Bongo dadaangu, Ohooo! Namna hii mtu hata umpe nini hakubali kuachia madaraka. We’ watu wote tunasimamishwa ili mkuu apite bwana! Hata ingekuwa mimi siachii ngazi mwanangu!” Abiria waliangua kicheko nami nikabaki nimeduwaa huku nikihisi moyo ukinipiga kwa nguvu.Kwa hakika nilikuwa nimeshikwa na woga mkubwa.
Kumbe ni msafara wa kiserikali tu!
Nilishusha pumzi za faraja kwani nilijua kama ule msako ungekuwa kweli ni kwa ajili yangu basi nisingekuwa na namna ya kujiokoa. Muda si mrefu ving’ora vilisikika na msafara mrefu wa magari ya kifahari ambayo hayakuwa na shaka kuwa ni ya serikali ulipita, nasi tukaruhusiwa kuendelea na safari yetu muda mfupi baadaye. Nilitahamaki kuona lile basi likikunja kuelekea maeneo ya feri badala ya kule posta ya zamani kama nilivyotarajia. Kumbe lilikuwa ni basi la Mwananyamala-Kivukoni. Hii ilikuwa ni mbaya kwangu, kwani nilitaka nipotee lile eneo la mjini haraka iwezekanavyo. Sasa hii ya kuelekea Kivukoni tena si ndio ninazidi kujizamisha ndani ya mji kabisa. Nilitaka kumpigia kelele konda aniteremshe, lakini nikachelea kuonekana kituko bila sababu.
Niliamua kutulia kufuata safari ya lile basi. Potelea mbali.
Nilipofika Kivukoni niliteremka baada ya kuona lile basi lilikuwa linaendelea kusubiri abiria wajae ndio lianze safari yake ya kuelekea Mwananyamala. Niliamua kutafuta basi lolote litakalonitoa katika yale maeneo ya katikati ya mji na kunirudisha uswahilini ambapo ningeweza kupotea kirahisi, ingawa sikuwa na wazo nielekee wapi hasa. Nilianza kuangaza huku na huko pale kituoni nikitafuta basi lolote ambalo lilikuwa liko tayari kuondoka eneo lile wakati niliposhituka kwa kihoro baada ya kuona umma wa watu ukinijia mbio kama kwamba walikuwa wanamkimbiza mwizi.
Moyo ulinilipuka na woga ukanitawala.
Ni nini tena? Wamenijuaje?
Nilianza kukimbia kidogo kidogo huku akili ikinizunguka kwa woga na mwili ukiniingia baridi.
Lakini mbona walikuwa wananikimbiza kimya kimya? Au...?
Na hata pale nilipokuwa nikijitahidi kukimbia kwa wasiwasi na woga mkubwa, nilishuhudia wale watu wakinipita bila hata kunijali na badala yake wakiendelea kutimua mabio kuelekea mbele.
What is happening...?
Niliendelea kukimbia huku nikiangaza huku na huko, nikijaribu kuwatazama wakimbiaji wenzangu kwa mshangao nisijue kinachoendelea, halafu nikaelewa.
Wanakimbilia pantoni!
Kama mwehu nami nikakaza msuli na kutimua mbio kwa nguvu zangu zote kuikimbilia ile pantoni. Niliiwahi nikiwa miongoni mwa watu wa mwisho kabisa, na muda si mrefu ile pantoni ikauacha ukingo wa bahari na kuanza safari ya kuelekea Kigamboni. Nilijiegesha kwenye kona moja mle ndani na kujikunyata nikilitazama jiji la Dar es Salaam likirudi nyuma taratibu wakati ile pantoni ikikata maji kuelekea upande wa pili wa bahari ya Hindi.
Mwili wote ulikuwa ukiniuma na miguu ilikuwa ikinivuta kuliko kawaida. Nikiwa ndani ya pantoni nilitoa kitambaa changu cha kichwa na kujifunga kichwani, nikizificha kabisa zile nywele zangu za rasta.
Niliteremka upande wa pili wa bahari na kujiunga na msururu mrefu wa wasafiri wenzangu kuelekea katikati ya kitongoji kile cha Kigamboni. Sikuweza kabisa kuiruhusu akili yangu iyatafakari matukio ya asubuhi ile, kwani nilihisi kuwa ningeweza kulipuka wazimu ghafla. Nilipitia kwenye maduka ya pale karibu na kipando cha pantoni na kununua nguo za kubadili kwani zile nguo zangu zilikuwa zimeanza kutoa harufu ya jasho, na pia nilijua kuwa kufikia sasa nilikuwa najulikana nguo nilizovaa, hivyo polisi wangekuwa wanamsaka mwanamke aliyevaa suruali na koti la jeans, kijitopu chekundu kwa ndani, akiwa amesuka nywele katika mtindo wa rasta. Kwa kuwa bado nilikuwa na pesa za kutosha, nilinunua nguo kadhaa za kubadili na kuongeza begi jingine dogo ambamo niliweka zile nguo zangu mpya. Niliingia duka la dawa na kununua dawa ya kidonda, bandeji, mswaki na dawa ya meno.
Kisha nilikodi teksi na kumuambia dereva anipeleke kwenye nyumba nzuri ya wageni iliyotulia. Alinipeleka kwenye nyumba moja ya wageni ambayo niliafikiana naye kuwa ilikuwa imetulia. Nikijiandikisha kwa jina la Nuru bint Shaweji, nilikodi chumba cha self contained kwa muda wa siku tatu. Kazi yangu nilijiandikisha kama mwanafunzi wa chuo cha elimu ya sayansi ya bahari cha Zanzibar. Sababu ya ujio wangu pale Kigamboni ikiwa ni kuandika juu wa mwenendo wa pwani ya Kigamboni. Maelezo yote haya nilijua kuwa ni upuuzi na uongo mtupu, lakini ilikuwa ni vigumu kwa yule jamaa wa mapokezi, ambaye alionekana kuwa hakwenda shule kiasi cha kuweza kuelewa mambo kama yale, kuyatilia maanani na kuyafuatilia.
Nilijifungia chumbani kwangu na kuelekea moja kwa moja bafuni ambapo nilioga kwa muda mrefu. Kisha niliosha na kufunga kidonda changu, kabla ya kujibwaga kitandani na kuchapa usingizi mzito.
v.

J
ambazi lauawa na pingu mkononi.
Kilikuwa ni kichwa cha habari kilichochukua uzito wa juu kabisa katika moja ya magazeti ya kila siku yanayotoka jioni. Moyo ulinilipuka na kuanza kunienda mbio, huku nikishuhudia lile gazeti likitetemeka mikononi mwangu wakati nikikodolea kwa kutoamini kichwa kile cha habari.
Ilikuwa ni majira ya saa moja za jioni wakati nikiwa napata mlo wa jioni kwenye mgahawa wa ile nyumba ya wageni wakati nilipoona kile kichwa cha habari kutoka kwenye moja ya magazeti yaliyokuwa yakitembezwa na kijana mmoja ndani ya mgahawa ule. Nilinunua haraka lile gazeti huku hamu ya kula ikiniisha. Niliinamia sahani yangu ya chakula na kukichezea chezea kwa muda kile chakula, kisha nikarudi chumbani kwangu upesi na kuanza kuisoma habari ile.
Macho ya Nyoka ameuawa!
“Haiwezekani! Haiwezekani auawe kirahisi namna hii! Macho ya Nyoka! Labda ungeniambia Dokta Martin Lundi, ningeweza kuamini, lakini sio Macho ya Nyoka!” Nilikuwa nijisemea peke yangu mle ndani huku nikitikisa kichwa kukana habari ile huku nikiiona kwa macho yangu pale gazetini.
Hapana bwana, kwangu hilo lilikuwa haliwezekani kabisa. Yule mtu ni muuaji wa kuzaliwa. Yaani yeye ndiye mwenye kazi ya kuua watu, sasa iweje tena yeye ndio auawe kirahisi namna hii?
Sio Kweli. Hii ni mbinu yao tu ya kutaka kunilaghai ili nijiamini kuwa niko salama halafu wanikamate kirahisi. Macho ya Nyoka ndiye mtu niliyemuhofia kuliko wote miongoni mwa wale wauaji niliowaona kule msituni, na nilishapata hisia kuwa kama sitanusurika na maisha yangu katika kindumbwendubwe hiki, basi ni Macho ya Nyoka ndiye atakeniua. Sasa tena hii habari...hapana si kweli!
Macho ya Nyoka afe! Sikuamini.
Lakini gazeti ndivyo lilivyoandika!
Macho ya Nyoka aliniahidi kifo cha mateso makubwa kwa macho tu na nikaelewa bila shaka yoyote ni nini alikuwa akiniahidi! Yaani hakutamka hata neno moja! Macho tu, na ujumbe ukafika!
Nilikumbuka yale macho yake jinsi yalivyoniahidi kifo pale aliponitazama kwa chuki huku akininyooshea kidole kabla hajatimua mbio kumkimbia yule afisa wa polisi, pingu ikimning’inia katika mkono mmoja.
Eti amekufa!
Nilikumbuka ule mlipuko wa bastola niliosikia ukitokea kule nje walipokuwa wakikimbizana, baada ya yule afisa wa polisi kuniamuru nisiondoke wakati akimfuata mbio yule muuaji. Nami nikaamua kutimua mbio kutoka eneo lile bila ya kujali kelele za Suleiman Kondo kuwa nisikimbie.
Pamoja na kuona kuwa kile kilichosemekana kutokea kuwa hakiwezekani, sikuweza kujizuia kuisoma ile habari iliyoandikwa gazetini kuhusu tukio lile lililotokea asubuhi ya siku ile pale ofisini kwetu.
Na hata nilipomaliza kuisoma kwa mara ya pili, bado nilibaki mdomo wazi na kujiuliza iwapo nilitakiwa niiamini au nisiiamini habari ile.
Kwa mujibu wa gazeti lile, ni kwamba jambazi hilo ambalo bado jina lake halijatambulika, liliuawa katika mapambano na polisi baada ya kufanikisha kutoroka kwa mwanamke ambaye alikuwa ametiwa mbaroni na polisi kuhusiana na mauaji ya kutatanisha ya watafiti wa Idara ya Makumbusho ya Taifa pamoja na watu wengine huko Manyoni.
Kutokana na maelezo ya gazeti lile, nilielewa kuwa Macho ya Nyoka alipokuwa akikimbizwa na yule askari, aliamua kusimama ili apambane naye, ambapo alitoa bastola (hii itakuwa nyingine, ambayo bila shaka alikuwa nayo – kwani ile bastola yake ndiyo aliyokuwa akiitumia yule askari baada ya kuangushwa chini katika mapambano), lakini kabla hajaitumia, yule askari alimuwahi kwa risasi ya mguu, na alipozidi kujaribu kumtupia risasi ndipo yule askari alipompiga risasi nyingine(sikumbuki kusikia mlipuko wa pili wa bastola, lakini wakati huo mimi ndio nilikuwa nimehamanika nikitafuta namna ya kutokomea kutoka eneo lile) iliyompata kifuani na kumuua.
Just like that...!Yaani hivi hivi tu!
Baada ya hapo gazeti lilielezea tena habari za yale mauaji ya kule Manyoni, na kutaja kuwa mwanamke aliyetoroka katika tukio lile bado anatafutwa na polisi na kutaja jina langu halisi, huku likinukuu taarifa ya polisi kuwa mwananchi yeyote atakayemuona au kuwa na habari zozote za mahala anapoweza kupatikana mwanamke huyo, atoe taarifa katika kituo chochote cha polisi kitakachokuwa karibu naye.
Kwa kuwarahisishia kazi wananchi, wasifu wangu wote ulielezwa gazetini, ikiongezewa na taarifa ya nguo nilizokuwa nimevaa siku ile pamoja na mtindo wa nywele niliokuwa nimeusuka. Nilishukuru mungu kuwa ingawa nilipoingia pale kwenye ile nyumba ya wageni nilikuwa nimevaa zile jeans zangu, nywele zangu za rasta nilikuwa nimezifunga ndani ya kilemba ambacho hadi muda ule nilipokuwa nakula pale kwenye mgahawa bado kilikuwa kichwani mwangu, na nilikuwa nimebadilisha nguo.
Zaidi ya hapo, picha yangu yenye ukubwa wa pasipoti iliwekwa pale gazetini, picha ambayo sikuwa na shaka ilitoka pale ofisini. Ni picha ambayo niliipiga siku chache baada ya kumaliza masomo yangu Chuo Kikuu, niliyoiwasilisha pale ofisini wakati naanza kazi kwa ajili ya kuwekwa kwenye faili langu binafsi la ajira. Katika picha ile nilikuwa naonekana mdogo zaidi, mwembamba zaidi, na zaidi ya hapo nilikuwa nimekata nywele zangu na kuziacha ndogo ndogo sana, ikiwa si siku nyingi tangu nitoke kwenye msiba wa baba yetu, ambapo kutokana na msiba ule, nilinyoa nywele zote.
Haikuwa picha ya kunitia shaka sana, lakini niliogopa kupita kiasi, kwani sasa jina langu lilikuwa hadharani, na wajihi wangu ulikuwa gazetini kwa kila mwenye macho kuuona.
Nitakimbilia wapi sasa?
Bila hata kufikiri zaidi nililitupa pembeni lile gazeti na kuanza kufumua zile rasta.
Hivi ni kwa nini haya mambo yanatokea?Ndilo swali lililokuwa likijirudia tena na tena kichwani mwangu tangu nilipoamka kutoka kwenye ule usingizi mzito ndani ya ile nyumba ya wageni. Na baada ya kusoma zile habari za kwenye lile gazeti, nilijikuta nikizidi kujiuliza lile swali. Na kila nilipojiuliza swali lile,nilijikuta nikijiuliza swali jingine kubwa na gumu zaidi. “Kwa nini mambo yale yanikute mimi katika watu wote?”
Kwa kweli wakati natimua mabio baada ya tukio la pale ofisini, sikuwa na hakika kama nilikuwa nachukua uamuzi wa busara, kwani nilipoyatafakari upya matukio yote yaliyotokea pale ofisini siku ile, nilipata hisia kuwa huenda yule afisa wa jeshi la polisi alikuwa ni askari wa kweli, na kwamba hata kama alikuwa na nia ya kunikamata kwa makosa yale aliyonitamkia pale ofisini kwa Mkurugenzi, kutokea kwa Macho ya Nyoka na matendo yaliyofuatia, kungeweza kabisa kumbadilisha mawazo na labda angeweza kuwa ndiye mtu wa kunisaidia, hasa nikizingatia kuwa yule alikuwa ni afisa wa ngazi ya juu katika jeshi la polisi.
Lakini kwa wakati ule ningeyajuaje hayo? Ningeweza kuyachezea bahati nasibu maisha yangu? Hapana, bora nilivyokimbia.
Lakini kila nilipozidi kutafakari tukio la pale ofisini na uamuzi niliochukua, ilinifunukia wazi kuwa sasa nilikuwa naendeshwa na hisia zaidi kuliko kitu kingine chochote. Kuwa ujumla wa matukio yote yaliyonikuta huko nyuma hadi kufikia sasa, umepelekea hisia zangu zote kufikia hatua ambapo zilikuwa zinaanza kutekeleza matendo ya kujihami na kujiokoa kwanza, halafu kutafakari juu ya hatua hizo baadaye. Baada ya matukio ya kule kwa mkuu wa wilaya nilipokimbilia kutafuta msaada, na yale ya kule kwa Kelvin na nyumbani kwa mama yangu, nilikuwa nimejitosheleza fika akilini mwangu kuwa sehemu pekee yenye usalama kwangu ni pale nitakapokuwa peke yangu. Na kwamba kila nitakayemdhania kuwa huenda akawa na msaada kwangu, anaondokea kuwa upande wao.
ITAENDELEA
 
SEHEMU YA KUMI NA NANE.

Baada ya matukio ya kule kwa mkuu wa wilaya nilipokimbilia kutafuta msaada, na yale ya kule kwa Kelvin na nyumbani kwa mama yangu, nilikuwa nimejitosheleza fika akilini mwangu kuwa sehemu pekee yenye usalama kwangu ni pale nitakapokuwa peke yangu. Na kwamba kila nitakayemdhania kuwa huenda akawa na msaada kwangu, anaondokea kuwa upande wao.
Wao.
Wao ni akina nani?
Na yule afisa wa polisi naye...
Macho ya Nyoka alikuwa tayari kabisa kumuua yule askari...sasa amekufa yeye!
Kwa hakika nilijua kuwa kama sikuchukua uamuzi wa haraka na kumbamiza Macho ya Nyoka na ile ndoo, bila shaka ningeshuhudia yule askari akiuawa mbele ya macho yangu.
Kadiri nilivyolitafakari tukio lile, nilijishawishi kuwa kwa wakati ule, nilikuwa nimechukua uamuzi wa busara sana kukimbia kutoka eneo lile, kwani kwa mambo niliyoyashuhudia kutoka kwa akina Martin Lundi, isingekuwa ajabu kabisa kukuta kuwa yule askari na Macho ya Nyoka walikuwa kitu kimoja, na walikuwa wanajifanya kutupiana mateke mbele yangu ili nijenge imani kwa yule askari wapate kunichukua kirahisi.
Lakini sasa nilielewa vinginevyo.
Kwa hakika yule alikuwa ni askari wa kweli, lakini hata kama ningebaki pale ofisini kama alivyoamrisha, angenielewa na kunisaidia? Au ndio ingekuwa kama yale ya kule kwa Mkuu wa Wilaya?
Kadiri nilivyoitafakari ile hali huku nikiendelea kuzifumua zile rasta, ilinijia wazi kuwa ingawa kifo cha Macho ya Nyoka kilitakiwa kiwe faraja kwangu, bado hakikuleta unafuu wowote katika hali yangu, kwani bado nilikuwa natafutwa na Dokta Martin Lundi na wenzake waliobaki. Tena sasa baada ya kifo cha mwenzao na kuelezwa gazetini kwa mazingira yaliyopelekea kifo chake, nilikuwa na hakika kabisa kuwa watazidisha bidii za kunisaka kwani nilikuwa na hakika kabisa wao hawakutaka kabisa nitiwe mbaroni na polisi wasio upande wao ili waweze kupata na kupoteza ule ushahidi ambao ulikuwa na madhara makubwa sana kwao. Lakini kama hiyo haitoshi, na polisi nao kwa upande wao walikuwa wanaendelea kunisaka. Sasa sijui kwa nini gazeti liliandika kuwa Macho ya Nyoka alikuwa amekuja kunitorosha, wakati yule afisa aliona wazi kuwa yule muuaji hakuwa na nia ya kunitorosha kwa urafiki baina yetu bali kwa sababu nyingine tu. Vyovyote itakavyokuwa, mbele ya yule afisa wa polisi na jeshin lake, bado nilikuwa mkimbizi kutoka kwenye mikono ya sheria, tena niliyekaidi amri ya kutotoroka niliyopewa na yule afisa wakati akimfukuza yule muuaji.
Lakini yule afisa wa polisi akiendelea kuniwinda ajue kuwa anaweza kuendelea kuniwinda kwa sababu niliokoa maisha yake...
Kwa siku mbili mfululizo sikutoka nje ya chumba changu zaidi ya kwenda kula na kurudi tena chumbani. Uzuri wa mambo ni kuwa pale pale kwenye ile nyumba ya wageni kulikuwa kuna sehemu ya mgahawa, hivyo sikupata taabu ya kutembea umbali mrefu kutafuta chakula. Kwangu, hizo zilikuwa ni siku mbili za tathmini ya matukio yote yaliyonitokea na jinsi nitakavyokabiliana nayo.
Siku yangu ya kuondoka pale kwenye ile nyumba ya wageni, niliongeza siku nyingine tatu, nikidai kuwa nilikuwa bado nina kazi za kuandika. Wakati huu nilikuwa nimeshanunua madaftari na makaratasi pamoja na kalamu kadhaa ili kweli nionekane mwanafunzi niliye kwenye utafiti. Na ili nisijiletee mashaka, nilikuwa nikitoka nje na kwenda kuzubaa pwani iliyokuwa karibu na ile nyumba ya wageni, na mara nyingine nikitembea tu mle mjini. Na mara zote nilizotoka, nilihakikisha kuwa nilikuwa na madaftari yakionekana wazi kwenye mkoba wangu.
Katika kipindi hiki, nilitumia muda wangu mwingi kadiri nilivyoweza kuangalia televisheni iliyokuwamo mle chumbani, hasa taarifa za habari ili nijue iwapo kuna habari zaidi juu yangu katika vyombo vya habari na kama zipo, zimetolewa kwa mtazamo gani. Aidha nilikuwa nikinunua magazeti kila siku nilipotoka kwenda kupata kiamsha kinywa asubuhi na kuyasoma kwa makini kutafuta habari zozote zilizohusiana na matukio niliyokumbana nayo. Lakini katika siku zilizofuatia, habari zile zilionekana kufifia kabisa.
Kama mvua iliyonyesha ghafla wakati wa kiangazi, halafu ikapotea na kukiacha kiangazi kiendelee kutawala.

--

Ukimya uliotawala baada ya habari ya kuuawa kwa Macho ya Nyoka ulinitia wasiwasi sana. Haikuniingia akilini kabisa kuwa baada ya taarifa kama ile, na taarifa zangu zikiambatana na picha yangu kutolewa gazetini, mambo yawe kimya kiasi kile. Nami nilizidi kuchoka kukaa katika ile hali ya wasiwasi na kujificha nikipita nikijibandika majina yasiyo yangu kwa woga wa kukutwa na watu wa Dokta Lundi au wana usalama.
Na kadiri nilivyokuwa nikiendelea kujificha katika ile nyumba ya wageni, nilikuwa nazidiwa na hamu na duku duku la kutaka kujua hali ya mama yangu ikoje hasa baada ya kukutana na dokta Lundi siku ile nilipowatoroka pale nyumbani. Nilitamani pia kumpigia simu dada yangu labda angenipa habari zozote lakini nilishindwa kutokana na woga kuwa huenda namba ya simu nitakayotumia ikafuatiliwa na kugundulika kuwa nimepiga kutokea Kigamboni halafu wakaniibukia kule kule Kigamboni. Nilishindwa pia kutafuta habari za Kelvin kwa sababu hiyo hiyo, ingawa naye nilikuwa na shauku kubwa ya kujua ni nini ilikuwa hatima yake.
“Lakini kwa nini niendelee kuishi maisha haya ya kikimbizi namna hii?” Nilijisemea peke yangu nikiwa chumbani mwangu pale kwenye ile nyumba ya wageni na kusonya kwa hasira na kuchanganyikiwa. Niliinuka kutoka kitandani nilipokuwa nimejilaza na kwenda kusimama nikiegemea ukuta huku nikiwa nimetumbukiza mikono yangu kwenye mifuko ya suruali ya michezo niliyokuwa nimeivaa.
“Na nitaendelea kuwindwa namna hii mpaka lini?” Nilijisemea tena kwa hasira na kutoa msonyo mkali. Nilitembea mle ndani huku nikiwa nimezamisha mikono yangu mifukoni nikitafakari ile hali niliyokuwa nayo.
“Halafu kibaya ni kwamba hao wanaoniwinda wananijua fika, lakini mimi siwajui…naona watu wananikimbiza, wanaua watu, wanawarubuni ndugu na jamaa zangu nao wanigeuke…lakini wao ni akina nani hasa sijui!” Niliguna na kujibwaga tena kitandani kwa kukata tamaa.
Muda ulikuwa ni kama saa kumi na mbili za jioni na kwa mbali nilisikia sauti ya adhana ikiwakumbusha waislamu kwenda msikitini kwa swala ya jioni.
“Lakini tatizo hasa ni nini…? Kwa nini yale mauaji yalitokea kule msituni? Kwa nini ilikuwa muhimu kwa Dokta Lundi kunipakazia mambo ya uongo namna ile…?”
Niliinuka na kuliendea begi langu na kuitoa ile kamera ya Gil, na kwa mara ya kwanza tangu nitoke kule Manyoni nilikaa chini na kuutazama upya ule mkanda tangu mwanzo hadi mwisho. Nikilirudia upya lile tukio la kule msituni. Nilipomaliza kutazama yale mambo ya ajabu niliyoyarekodi kule msituni nilijikuta nikibubujikwa na machozi bila kupenda. Lakini pia kulitazama tena lile tukio kuliniletea mwanga mpya katika uelewa wangu wa tukio lile na nikajikuta nikiurudisha tena nyuma ule mkanda na kuuangalia upya kutokea mwanzo hadi mwisho huku nikitafakari matukio mengine yaliyonitokea ambayo hayakuwamo mle kwenye ule mkanda.
Niligundua kuwa kumbe wale wauaji, akina Martin Lundi, wote walikuwa wamevaa glovu mikononi mwao, kitu ambacho sikuwa nimekiona hapo mwanzo.
Ina maana walikuwa wamedhamiria kuwa wasiache ushahidi wowote wa kuhusika kwao aidha na kifo cha yule mtu, au tukio zima la pale msituni.
Nilirudia ile sehemu nilipokuwa naongea na yule mtu asiye na jina kule msituni, ambapo hapa nadhani nilirekodi bila ya kujijua, kwani ile kamera ilikuwa imeelekea ardhini kwenye mchanga, na ilichorekodi kilikuwa ni yale mazungumzo yaliyotokea baina yetu pale mchangani. Na nilipokuwa nikitazama ule mkanda ukionesha michanga tu ya pale alipokuwa amelala yule mtu na sehemu kidogo ya bega na mkono wake, nilikuwa nayasikia upya yale maongezi kutoka kwenye ile kamera.
“Usiongee! Tulia, nitakusaidia”
Halafu nilisikia miguno ya yule mtu kisha nikaona zile namba ambazo yule mtu aliziandika mchangani na kunisistizia nizitazame.
Niliusimamisha ule mkanda na kukimbilia kalamu na kijitabu kidogo kilichokuwa mezani, nikarudi pale nilipoiacha ile kamera na kuinakili ile namba huku moyo ukinienda mbio.
Nikaendelea kuangalia ule mkanda.
“Sawa...nimeshaona! Hizi namba ni za nini? Na wewe ni nani...kwa nini wale watu wamekufanya hivi? Umewafanya nini? Ni nani wale?”Ilifuatia sauti ya yule mtu akikohoa kwa taabu, ikifuatiwa na pumzi zake akitweta kama mtu aliyemaliza mbio ndefu.
“Find the Bastard!”
“Yes! Usiwe na wasiwasi nitahakikisha wanafikishwa mbele ya sheri...’
“...at the Rickshaw...!”.
“Rickshaw? Rickshaw iko wapi ?”
Niliisimamisha tena ile kaseti na kuandika tena kwenye kijitabu changu:
Bastard.
Rickshaw.
Nikaendelea kuutazama tena ule mkanda.
Zilifuatia sauti za yule mtu akigumia kwa taabu, nami kumbukumbu zangu zikanionesha picha ya yule mtu alipokuwa akitapatapa huku akitupa kichwa chake huku na huko na nikakumbuka jinsi nilivyopandwa na woga nilipodhani kuwa yule mtu ndio alikuwa anakata roho.
“Wewe ni nani...ndugu zako ni nani?”
Niliusimamisha ule mkanda na kuandika kwenye kijitabu changu:
Wewe ni nani? – No answer. Mr. Who?Mr. Nani? Question Mark! =Mr. Q?
Nikabonyeza sehemu inayotakiwa na ule mkanda ukaendelea.
“Get the key....the bastard!”
“Key…? What key…?”
Niliisimamisha ile kaseti na kuandika tena kwenye kijitabu changu:
Key – Ufunguo. ???
Nikaendelea kuutazama ule mkanda.
“At the Rickshaw…!”
“I don’t understand!”
“Please…Go now!”
“Lakini bado sijaelewa…nataka kukusaidia! Au hujui Kiswahili…? Can’t you speak Swahili?”
“Find the bastard!”
Niliisimamisha tena na kuandika kwenye kijitabu changu:
Find the Bastard! – Mtafute Mwanaharamu? (M. Lundi&wenzake???)
Nilibaki kimya kwa muda mrefu huku nikitafakari wakati picha ya siku ile msituni ikinijia akilini na nikakumbuka jinsi yule mtu alivyonitazama huku akitoa kitu kama tabasamu dogo sana baada ya kuniambia yale maneno.
“Now why did you smile like that Mr. Q, eenh?” Nilijisemea mwenyewe kwa sauti ya chini, nikimuuliza yule marehemu huko aliko kwa nini alitabasamu namna ile baada ya kunieleza maneno yale. Nilikaa nikitafakari kwa muda mrefu sana, huku nikichorachora vitu visivyoeleweka katika kile kijitabu changu. Kisha niliamua kuendelea kuuangalila ule mkanda.
“Okay...I can speak english....who are you? Who are those people…? Do you have any relatives….? I can help you…I want to help you!”
“Please Go...watakukuta!”.
“Watakuua...wacha nijaribu kukusaidia”
“I don’t care...you go find the bastard!”
Hapa niliusimamisha tena ule mkanda na kuandika kwenye kijitabu changu:
Mr.Q hajali kama angeuawa?? Anachojali = Find the Bastard!!!!
Who is the Bastard? – M. Lundi, Kigulu,Macho ya Nyoka(Dead?) Au kuna kitu kingine?
Hapa nilitafakari tena kwa muda mrefu, na ingawa sehemu hii yote ya mkanda nilikuwa nimerekodi sauti tu, wakati picha ikionesha michanga tu ya pale mchangani alipokuwa amelala yule mtu asiye na jina(nilishampachika jina la Mr.Q), bado niliikumbuka vizuri sana sura yake ilivyokuwa pale alipomaliza kusema yale maneno na jinsi alivyojitahidi kutabasamu tena halafu akazidiwa na kikohozi kikali na damu ikaanza kumtoka mdomoni. Hapa mkanda ulisimama kabisa kurekodi na hakukuwa na picha wala sauti yoyote, nami nikakumbuka kuwa ni wakati huu ndipo nilipomwinua kichwa chake ili damu isimpalie na kuanza kumfuta ile damu kwa mkono wa shati langu. Nilikumbuka waziwazi kuwa nilipofanya hivi, yule mtu alinishika mkono kwa nguvu na kunitolea macho huku akinisisitizia kuwa niondoke eneo lile haraka kabla wale wauaji hawajanikuta na kuniua.
Na kweli masikini, nilipoondoka na kumwacha pale, wale wauaji walirudi na kumkuta akiwa anagaa gaa pale mchangani.
Nililia kwa uchungu baada ya kuona ni jinsi gani yule mtu alivyonisisitiza niokoe maisha yangu ingawa alijua kuwa yeye angekufa muda wowote.
“Lakini kwa nini uliniita? Hukutaka nikuokoe, bali ulitaka kunieleza kitu…?” Nilimuuliza yule marehemu huko aliko kwa fadhaa huku nikibubujikwa machozi na nikihisi donge kubwa likinikaba kooni.
“Sasa mbona hukunieleza kitu chochote cha maana, Mr. Q?” Nilimuuliza tena kwa uchungu huku nikibubujikwa na machozi. Nilitazama vitu nilivyoandika kwenye kile kijitabu changu. Hakukuwa na kitu chochote kilichokamilika ambacho kiliniwezesha kujua ni nini yule mtu alitaka kunieleza. Kwa muda mrefu nilibaki nikikodolea macho vitu nilivyoandika kwenye ule ukurasa wa kile kijitabu changu, na bado sikupata jibu la moja kwa moja.

456718
Bastard.
Rickshaw.
Wewe ni nani? – No answer. Mr. Who? Mr. Nani? Question Mark! = Mr. Q?
Key – Ufunguo.???
Find the Bastard! – Mtafute Mwanaharamu?(M. Lundi&wenzake???)
Mr. Q hajali kama angeuawa?? Anachojali = Find the Bastard!!!!
Who is the Bastard? – M. Lundi, Kigulu, Macho ya Nyoka (Dead?) Au kuna kitu kingine?

Nilidhani ningeweza kupata mwelekeo fulani kutoka kwenye ule mlolongo wa vitu nilivyoandika kutoka kwenye kauli za yule mtu aliyeuawa msituni. Nilihitaji kutafakari zaidi.
Hatimaye niliamua kuendelea kuutazama ule mkanda na nilipofikia katika sehemu ambapo yule mtu niliyembatiza jina la Mr. Q alimrukia Macho ya Nyoka na kuanza kupambana, niliusimamisha tena ule mkanda na kubaki nikikodoa macho kwa mshangao mkubwa huku akili ikinizunguka. Kitu nilichokiona pale, ingawa nilishakiona kwa macho yangu kule msituni, na nikakiona tena kwenye ule mkanda mara ya kwanza, kilinishitua na kuniletea mtazamo mpya kabisa katika swala zima la mkasa huu ulioniangukia.
Ilikuwa ni vigumu kuamini, lakini ndivyo ilivyoelekea.
Niliirudisha tena ile sehemu na kuiangalia upya.
Ni kweli kabisa nilichogundua, na hata pale ugunduzi ule uliponiangukia, nilijikuta nikishikwa na butwaa nisijue la kusema.
Mr. Q alimrukia Macho ya Nyoka kusudi ili auawe!
Naam! Ndivyo haswa.
Nilihisi mwili ukinisisimka na hapo hapo vipele vya baridi vilinitoka mwilini.
Kwa nini Mr. Q aamue kufanya vile? Kwani bila shaka na yeye alijua kuwa katika wale watu watatu, Macho ya Nyoka ndiye aliyekuwa anaelekea kuua bila hata ya sababu, hivyo akaamua kumpa sababu ya kumuua na ndivyo ilivyotokea!
Nilifikiria maana ya kitendo hiki huku maswali yakinielemea.
Kwa nini aamue vile? Kwa nini aamue vile wakati ule, na si wakati wowote kabla ya hapo?
Kutokana na tukio lile kama jinsi nilivyojikumbusha kwa kuutazama tena ule mkanda, ni kwamba yule mtu aliteswa sana kabla ya kuletwa pale msituni, na kama aliteswa, lazima kuna sababu ya kuteswa huko.
Nilikumbuka kuwa kuna wakati kabla ya yule mtu kumrukia Macho ya Nyoka na hatimaye kuuawa, alimtemea mate Kigulu ambaye alikuwa akimuuliza kitu fulani, na kisha akamtupia mchanga usoni, na wakati kigulu anajipangusa mchanga, yeye alimrukia Macho ya Nyoka.
Ambaye wakati huo alikuwa pembeni kabisa tena na bastola yake alikuwa ameiweka mfukoni baada ya kukemewa na wenzake alipokuwa akimtishia Mr. Q kwa bastola ile.
Hii ilimaanisha kitu kimoja tu...
Yule mtu alikuwa anawachokoza kusudi ili wamuue!
ITAENDELEA .
 
SEHEMU YA ISHIRINI

“Mimi ni Aulelia kweli, lakini wewe sikujui! Na naomba usinicheleweshe!” Alinijibu kisha aliondoka kwa mwendo wa haraka akiniacha nikiwa nimepigwa na butwaa.
Hii ni nini tena?
Nilimtazama yule mtu ambaye tulikuwa pamoja kwa muda mwingi wakati tukiwa chuoni na nilishindwa kuelewa ni nini maana ya tukio lile. Na hata pale nilipokuwa nikimkodolea macho, nilimshuhudia akifungua mlango wa gari yake aina ya RVR ambayo niliijua fika hadi namba na kuondoka eneo lile kwa kasi. Na wakati gari ile ikinipita kwa kasi, Aulelia alinigeuzia uso wake kunitazama na nikaona alikuwa akibubujikwa na machozi.
Mungu wangu! Martin Lundi amemfikia na yeye?
Niliondoka eneo lile nikiwa nimezidi kuchanganyikiwa.Moyo uliniuma vibaya sana kutokana na kitendo alichonifanyia rafiki yangu Aulelia.
Kwa nini Aulelia, eenh? Why do you have to do this to me?
Sikuwa na shaka kuwa tabia ya Aulelia niliyoishuhudia muda mfupi uliopita ilitokana na yale mambo yaliyonikuta. Lakini Aulelia ni mtu mwenye uelewa wa hali ya juu, si kawaida yake kufanya kitu kama kile bila ya kuwa na uhakika nacho. Nilikuwa na imani kabisa kuwa hata kama angesikia taarifa kuwa nimekuwa kichaa ninayeua watu hovyo, Aulelia angetaka kuongea na mimi na kuelewa ni yepi hasa yaliyonisibu na kujihakikshia mwenyewe kuwa kweli nimekuwa mwehu, badala ya kunikana moja kwa moja kwa maneno ya kuambiwa tu au ya kusoma magazetini. Lazima kuna kitu zaidi.
Ni nini? Sikuwa na la kufanya zaidi ya kurejea kwenye eneo langu la maficho kule Kigamboni. Siku yangu ilikuwa imepotea bila mafanikio yoyote.

--

Safari yangu kurudi kwenye ile nyumba ya wageni kule Kigamboni ilikuwa kama ndoto. Sikumbuki chochote kilichotokea humo njiani, ila nilijikuta tu nimefika na kupitiliza moja kwa moja chumbani kwangu na kujifungia. Usiku ule nilisumbuliwa zaidi na mawazo juu ya tabia aliyoonesha rafiki yangu kipenzi Aulelia Mushi nilipokutana naye pale mjini. Sikuwa na shaka hata kidogo kuwa yule ni yeye, kwani hata gari aliyoondoka nayo ilikuwa ni ile ambayo mimi niliijua siku zote kuwa ni yake, hata namba za ile gari ni zile zile za gari lake. Nikiwa nimejilaza kitandani nikiwaza juu ya mambo haya, nilisikia wahudumu wa ile nyumba ya wageni wakifungua chumba kilichokuwa kikitazamana na kile nilichokuwa nimepanga na kumkaribisha mpangaji mpya kwenye chumba hicho. Mawazo yangu yalirudi kwa rafiki yangu Aulelia Mushi.
Sasa kwa nini amefanya vile?
Sikupata jibu la kuniliwaza, na nilibaki na uchungu mkubwa moyoni kwani tukio lile lilinikumbusha kuwa bado nilikuwa mkimbizi nisiye na kimbilio, na kwamba sehemu pekee inayonifaa ni pale nitakapokuwa peke yangu.
Zaidi ya hapo mawazo yangu yalisumbuliwa na tatizo la upungufu wa pesa uliokuwa unaelekea kunikumba. Kwa hali hii nitakimbilia kwa nani anipe pesa? Na bila pesa nilikuwa sina ujanja wa kujiokoa kutoka katika msako wa akina Martin Lundi. Nitakimbilia kwenye nyumba gani ya wageni au hoteli bila ya pesa?Hapo niliamini kuwa hawa akina Martin Lundi walikuwa ni watu hatari sana wanaopangilia mambo yao kwa wigo mpana sana, kwani kwa kunichukulia kikadi changu cha benki, walihakikisha kuwa wamenizibia kabisa mianya ya kujipatia pesa na hivyo kuyafanya maisha yangu kuwa magumu sana. Nilikumbuka maneno ya yule askari wa kike aliyeniibukia kule kwenye nyumba ya wageni maeneo ya sinza:
...na nakuahidi kuwa tutayafanya maisha yako yawe mabaya sana hapa duniani mpaka utautoa!
Na ilielekea kuwa kweli.
Sijui kwa nini hawakuzichukua na zile pesa taslimu zilizokuwa kwenye begi langu kule msituni, labda kwa kuwa nilikuwa nimezishindilia chini kabisa ndani ya begi lile nao hawakuwa na muda wa kulipekua sana. Na pia hakuna ambaye angetarajia kuwa ningeweza kuwa na pesa kiasi kama kile porini namna ile. Nilikumbuka kuwa marehemu Ibrahim Geresha alichukua pesa kidogo sana, na sehemu kubwa ya posho yake ya safari alimwachia mkewe kwa matumizi ya familia yake. Sasa mimi sikuwa na familia ya kuiachia pesa, hivyo nikaenda nazo msituni.
Na ndio zilizonisaidia mpaka kufikia hapa. Ingawa bado nilikuwa na pesa za kuniwezesha kujikimu kwa siku kadhaa zijazo, lakini niliona ni bora ningeanza kufanya utaratibu wa kutafuta pesa mapema kabla hazijanikaukia kabisa. Niliikumbuka akaunti yangu kule benki. Nilikuwa na zaidi ya Milioni moja na nusu kwenye ile akaunti, lakini ndio sikuwa na namna ya kuzipata bila ya ile kadi yangu ya benki.
Njia ya kujitia kuwa kadi imepotea isingenisaidia kwani utaratibu niliujua wazi. Nilitakiwa nitoe ripoti polisi, nipewe RB ya upotevu wa kitambulisho cha benki, ndipo Benki wangeweza kunipatia kadi nyingine. Kinyume na hapo hakukuwa na namna.
Na swala la kwenda polisi kutoa ripoti ya kupoteza kitambulisho cha benki lilikuwa haliwezekani kabisa, kwani huko kulikuwa ni kujipeleka kwenye mdomo wa mamba, kwani nisingeweza kwenda polisi kwa jina la Nuru Bint Shaweji, nilitakiwa niende kwa jina langu halisi, Tigga Mumba, ambalo ndilo lililokuwa kwenye kadi yangu ya Benki na ambalo linatambulika kule benki.
Pia ni jina ambalo kufikia sasa sikuwa na shaka kwamba lilikuwa maarufu katika vituo vyote vya polisi sio tu jijini, bali pia hata mikoani.
Sasa nifanyeje?
Niliamua kwenda benki siku iliyofuata na kubahatisha kutoa kiasi cha pesa kutoka kwenye akaunti yangu. Namba yangu ya akaunti nilikuwa naikumbuka kwa kichwa, na kulikuwa kuna dada ambaye nilikuwa nimezoeana naye sana pale benki, kwani mara nyingi nikienda kutoa pesa huwa namuachia na yeye bakshishi kidogo, hivyo kila mara niingiapo pale benki huwa akinichangamkia sana.
Nilitaraji kuwa zile bakshishi nilizokuwa nikizitoa kwa yule dada huenda zikanisaidia kupata pesa bila kulazimika kutoa kitambulisho changu cha benki.
Baada ya hapo ningemfuatilia rafiki yangu Aulelia Mushi ili nijue kiini cha ile tabia ya ajabu aliyonionesha pale tulipokutana. Huenda ningepata mwanga wa kunikurubisha katika ufumbuzi wa mtihani ulionikuta.
Kwa muda ule nilisahau kabisa maswala ya The Rickshaw, The Bastard na Key.

--

“Eem…Samahani kidogo anti, lakini itabidi nipate kibali cha kukupatia pesa kutoka kwa bosi wangu, si unajua tena…mambo ya procedure?” Yule dada niliyekuwa nimetaraji kuwa angekuwa mwepesi kunielewa pale benki na kunipatia pesa bila usumbufu na vipingamizi aliniambia huku akitabasamu kijinga, uso wake ukionesha wazi kuwa hakupenda kabisa hali ile.
“Aaah! Ni lazima ufanye hivyo? We’ si unanifahamu anti? Na hiyo ndiyo akaunti yangu…mi’ nakuja hapa benki mara kibao tu kuchukua pesa kwa hiyo akaunti…” Nilimjibu huku nikianza kujutia uamuzi wangu wa kuja hapa benki. Nilikuwa nimecheza bahati nasibu mbaya sana kuja hapa, kwani pia ingewezekana hata hapa benki wakawa na habari zangu na hivyo kunifanya niwe nimejiingiza mwenyewe kwenye mdomo wa Mamba.
Lakini ningeishi vipi bila pesa?
“Akaunti iko sawa kabisa Anti, na mi’ nakujua vizuri na sina shaka na wewe…”
“Sasa tatizo ni nini?” Nilimkatisha kwa swali.
Nilipofika pale benki nilijaza fomu ya kuchukulia pesa na kufoleni kwenye dirisha alilokuwa yule dada niliyemkusudia tangu siku iliyopita. Aliponiuliza juu ya kadi yangu ya benki nilimwambia kuwa nilikuwa nimeisahau nyumbani kwa mama yangu Morogoro nilipoenda likizo na kwamba nilikuwa nimeagiza mtu aniletee, lakini kwa sasa nilikuwa na shida kubwa sana ya pesa na hivyo nikamwomba anisaidie. Aliniuliza kuwa nilikuwa na uhakika kuwa sijaipoteza nami nikamhakikishia kabisa kuwa nilikuwa nimeisahau pamoja na baadhi vitu vyangu kule Morogoro na nimewasiliana nao wakanithibitishia kuwa ipo na italetwa.
Nilimuona yule dada akisita huku akijaribu kuamua iwapo adharau procedure kwa muda na anisaidie. Niliona wazi akilini mwake alikuwa akizikumbuka zile bakshishi nilizokuwa nikimkatia kila nilipokuwa nikienda kuchukua pesa pale benki.
“Naomba unisaidie Anti, Please!” Nilimwambia kwa kuomboleza huku moyo ukinidunda.
Yule dada alisita kwa muda. Kisha nilimuona akianza kuigonga muhuri ile fomu yangu nami nikabana pumzi, lakini mara aliingia dada mwingine pale kwenye kaunta ya yule dada.
“Bosi anakuita…sasa hivi!” Alimwambia na kutoka. Yule dada alinitazama na kutabasamu kisha akaniomba radhi na kuelekea sehemu ya ndani ya ile benki ambapo wateja hatukuweza kuona kilichokuwa kikitendeka. Nilibaki nikisubiri pale kwenye foleni huku moyo ukinienda mbio na wasiwasi ukinipanda. Nilisikia manung’uniko ya wateja waliokuwa nyuma yangu, kwani nilikuwa nimetumia muda mrefu na yule dada pale dirishani, lakini sikujali.
Baada ya muda yule dada aliyekuja kumwita mwenzake alinijia na kuniomba niongozane naye kuelekea sehemu ya ndani alikoelekea yule dada aliyekuwa akinihudumia. Hapo machale yalinicheza na nikataka kutimua mbio, lakini sikuweza kufanya hivyo kwani mlangoni kulikuwa kuna askari mwenye silaha na zaidi ya hapo watu waliojaa mle ndani wangeweza kunikamata kwa urahisi sana.
“Ku…kuna nini, something wrong?” Nilimuuliza kwa wasiwasi iwapo kulikuwa kuna tatizo lolote huku nikiangaza huku na kule nikijaribu kumtafuta yule dada aliyekuwa akinihudumia hapo mwanzo.
“Hakuna tatizo la kukutisha dada yangu, ni kuweka taratibu sawa tu. Nifuate tafadhali.” Yule dada alinijibu huku akiongoza njia. Nilihisi mwili ukiniisha nguvu na kwa mara nyingine nilijutia uamuzi wangu wa kuja hapa benki. Nilimfuata yule dada huku nikiwa nimeingiwa na woga wa ajabu, akilini mwangu nikijua fika kuwa huko niendako nilikuwa naenda kukutana tena na yule muuaji muongo, Martin Lundi.
Niliingizwa kwenye ofisi moja nzuri sana iliyokuwa nyuma ya ukuta wa zile kaunta za kuhudumia wateja na mtu mmoja mrefu na mtanashati sana alikuwa ameketi kwenye kiti kizuri sana nyuma ya meza kubwa na safi. Mlangoni mwa ofisi ile kulikuwa kumeandikwa “Branch Manager” nami moja kwa moja nikaelewa kuwa huyu ndiye alikuwa meneja wa tawi lile la benki. Baada ya kunifikisha ndani ya ile ofisi yule dada aliyenileta aliondoka na kuniacha pamoja na wale niliowakuta mle ndani.
Nilibaki nikiwa nimesimama kizembe nikisubiri maelekezo, lakini yule bwana tuliyemkuta mle ndani alikuwa akinitazama tu bila ya kusema neno. Yule dada aliyekuwa akinihudumia pale kaunta alikuwa amesimama kando ya ile meza na ile fomu yangu niliyoijaza ilikuwa juu ya meza ya meneja wa tawi. Kibao kidogo kilichokuwa juu ya meza ile kilimtambulisha yule bwana kama Dick Bwasha. Nilipotembeza macho mle ndani, niligundua kuwa kulia kwa meza ya yule meneja wa tawi, kulikuwa kuna vijiruninga vidogo ambavyo vilimwezesha yule meneja kuona kila kilichokuwa kikitendeka kule kwenye kaunta za kuhudumia wateja. Nilimgeukia yule dada aliyekuwa akinihudumia pale kaunta na nikaona alikuwa amebadilika na uso umemsawajika vibaya sana. Alikuwa ametishika vibaya sana, nami nikaanza kugwaya nisijue nitafanyaje. Muda huo yule bwana alimwashiria yule dada atoke nje ya ile ofisi naye aliondoka haraka akiniacha na yule mtu mle ndani. Hatimaye yule meneja wa tawi aliniashiria niketi kwenye kiti kilichokuwa mbele ya meza yake nami nikatii.
“Ulikuwa unataka kumfukuzisha kazi yule binti bila ya sababu. Ukisahau kitambulisho chako cha benki unatakiwa urudi ukakifuate ndio uje benki kutoa pesa. Na ukikipoteza, unatoa ripoti polisi, unapewa RB, unakuja hapa, unatengenezewa kadi nyingine kisha unachukua pesa. Huo ndo utaratibu.” Dick Bwasha akiniambia huku akiwa ameninyanyulia nyusi na akinitazama usoni. Uso wake ulikuwa umejaa jeuri na kila alipoongea alibetua midomo yake kama kwamba anasikia kichefuchefu. Hii ilitia dosari kubwa katika utanashati wake. Nilibaki nikimkodolea macho kwa muda kabla sijapata neno la kusema.
“Lakini nilikuwa nimeomba msaada tu! Nina shida sana ya pesa na kitambulisho nimekisahau nje ya mkoa, nisingeweza kurudi kukifuata wakati nimeshikwa na shida ya dharura.” Nilimjibu huku nikizidi kupata hofu ya kuendelea kubaki na yule mtu mwenye majivuno na kiburi kikubwa kabisa ndani ya chumba kile.
“Hilo halitawezekana!” Alinijibu kwa mkato huku akinibetuliwa midomo yake mibaya na kuniinulia nyusi zake nene kwa kiburi cha hali ya juu. Nilimtazama kwa muda huku hasira zikinipanda.
Kwani imekuwaje? Mimi sikuona kama lile lilikuwa ni swala kubwa sana kiasi cha kuanza kujibizana na meneja wa tawi.
“Lakini kuna pesa zangu kwenye benki yako! Zaidi ya milioni na nusu, sasa unataka kuniambia kuwa siwezi kuchukua kilicho changu kwa vile tu…”
“Sio kwa utaratibu uliotaka kuutumia. Sisi tuna taratibu zetu bwana!”
“Sasa kwa nini umeagiza niletwe huku ofisini kwako? Kwa sababu nilitaraji nimeletwa huku ili nipate msaada ambao labda wale wahudumu wa kule kaunta hawana mamlaka nao!” Nilimjibu kwa mshangao. Yule bwana alinitazama kwa kiburi huku akitafuna tafuna kalamu yake na domo lake likifanya tabasamu la kuchukiza.
“Unataka msaada?” Aliniuliza huku akiendelea kutafuna tafuna kalamu yake na akinitazama kwa macho ya matamanio, na kuendelea; “Itabidi nawe ukubali kusaidia.”
Alinichefua!
Yaani huyu bwana alikuwa anataka kutumia nafasi hii kuniletea mzuka wake wa ngono!
“Sikiliza Mista, nilitegemea tatizo langu lingeeleweka na kupatiwa ufumbuzi kwa taratibu zinazoeleweka. Sioni sababu ya kujirahisi kwako kwa pesa yangu mwenyewe bwana! Kama we’ una mzuka wa ngono si ukatafute machangudoa waliojaa tele huko mitaani!” Nilimkemea kwa hasira, wakati yeye akibaki akinitazama tu huku akiendelea kunichekea akitafuna tafuna kalamu yake.
Nilizidi kuchukia.
“Na nitahakikisha kuwa naifunga akaunti yangu na nahamia benki nyingine, Benki gani inakuwa na watendaji wasio na adabu hata kidogo!” Nilimwambia kwa ghadhabu.
“Mnnhu! Mi’ n’lidhani utaenda polisi kupeleka mashitaka ya unyanyasaji wa kijinsia!” Dick Bwasha aliniambia kwa kebehi huku akinitazama machoni na sura yake ikiendeleza ile cheko yake ya kebehi, na aliposema vile, alitilia msisitizo sana neno “polisi”. Sikumuelewa, tulibaki tukitazamana kwa muda, kisha nikaamua kuondoka eneo lile. Nilipeleka mkono wangu kwa nia ya kuinyakua ile fomu yangu ya kuchukulia pesa iliyokuwa pale mezani huku nikiinuka. Lakini mkono wa Dick Bwasha ulichomoka ghafla na kuukamata mkono wangu, akinizuia nisiichukue ile fomu. Niliruka kwa mshituko huku nikiachia yowe la woga.
“Not so fast young lady!” Dick Bwasha alinikemea huku naye akisimama kutoka kwenye kiti chake na kunikunjia sura yake kwa ghadhabu, ile cheko yake ya kejeli na mchezo-mchezo ikiyeyuka kabisa usoni mwake, akimaanisha kuwa nisifanye haraka kuondoka.
“Hey! Niachie!” Nilimwambia kwa hasira huku nikijaribu kuunasua mkono wangu kutoka mkononi mwake. Dick Bwasha alizunguka ile meza kwa wepesi wa ajabu na kuja hadi pale kwenye kiti nilichokuwa nimekalia hapo awali na kunikalisha huku akiniinamia na kunisemea karibu sana na sikio langu.
“Unataka msaada, n’takusaidia. Lakini na wewe lazima ukubali kunisaidia bibie, unasemaje?”
Mwili ulinifa ganzi. Huyu bwana ana wazimu au kitu gani?

***MNH! Kwanza Aulelia, na sasa Dick Bwasha. Nini kingine?

TUKUTANE KESHO SAA MOJA ASUBUHI IN SHAA ALLAH!
 
Back
Top Bottom