Uongo mwingine wa dikteta uchwara huu hapa.
Odinga afichua aliyoteta na JPM
Raila Odinga
Na Ratifa Baranyikwa,
MWANASIASA maarufu nchini Kenya, Raila Odinga, amesema amemuuliza Rais John Magufuli kuhusu hatua yake ya kuzuia mikutano ya vyama vya upinzani hususani Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema).
Odinga ambaye anaongoza muungano wa vyama vya upinzani nchini Kenya (CORD), alisema tofauti na maelezo anayoyasikia nje, katika mazungumzo yao Rais Magufuli alimwambia hajapiga marufuku mikutano ya kisiasa ikiwemo ile ya wanasiasa au viongozi wa juu wa kitaifa wa vyama vya siasa wasio na majimbo.
Alisema badala yake alimwambia amepiga marufuku mikutano ya kubeba watu kwenye mabasi kutoka eneo moja kwenda jingine kwa madhumuni ya kufanya vurugu.
Odinga aliyekuwa nchini kwa shughuli binafsi, yeye na familia yake, aliyasema hayo katika mahojiano maalumu yaliyofanyika mwanzoni mwa wiki hii katika Hoteli ya Hyat Dar es Salaam na wahariri wa magazeti ya Kampuni ya New Habari (2006) Ltd.
Katika mahojiano hayo yaliyoanza kuchapishwa wiki hii na gazeti dada la MTANZANIA JUMAPILI la RAI, Odinga pia alizungumzia mwenendo wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na hatua ya wabunge wa upinzani kususia vikao vyake, lakini pia uamuzi wa Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa, kujiunga upinzani na kisha kuwania urais katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka jana.
Odinga anayetambulika kama baba wa demokrasia katika siasa za Afrika Mashariki, alilazimika kufichua siri ya mazungumzo baina yake na Rais Magufuli baada ya wahariri kutaka kujua kama alikutana na rafiki yake huyo na kuzungumzia joto la siasa za hapa nchini.
Katika majibu yake kuhusiana na swali hilo, Waziri Mkuu huyo wa zamani nchini Kenya, alikiri kukutana na Rais Magufuli Jumapili ya Agosti 14 mwaka huu Ikulu, Dar es Salaam na kula naye chakula cha jioni kisha kuzungumza mambo yao ya kirafiki na yale ya kisiasa lakini yasiyohusu urais.
“Jana mimi nimeongea na Rais yeye ameniclaim tofauti okey…amesema hajawanyamazisha wasiongee, anasema wanataka kufanya maandamano katika jimbo zile zingine ambazo hawana watu na kutaka kubeba watu kwa mabasi yeye alisema wakitaka hivyo wafanye kwao na si kubeba watu kutoka eneo hili kwenda eneo lingine, sasa sijui ukweli mimi maana mimi si Mtanzania.
“Anasema hajawakataza kama wakifanya eneo lao wanaweza kufanya lakini kubeba watu kutoka jimbo hili kwenda jimbo hili na mabasi kwenda kuleta vurugu ndio anasema amekataa,” alisema.
Alipoulizwa kama pengine Rais Magufuli amemweleza msimamo wake wa kupiga marufuku siasa za ushindani hadi mwaka 2020 pia ulilenga kuwazuia viongozi wakiwemo wale wa juu wa kitaifa wa vyama vya upinzani wasio na majimbo, Odinga alisema huku akimalizia na kicheko;
“Anasema hajakataa.”
Akisisitiza kile alichoelezwa na Rais Magufuli ambaye ni rafiki yake wa siku nyingi, Odinga alizungumzia uhuru wa kutoa maoni akisema wapinzani kazi yao ni kupinga na si kushangilia na kwamba hiyo ndiyo demokrasia.
Alisema kutokana na kile alichomweleza Rais Magufuli, hadhani kama alikuwa na madhumuni ya kuwanyamazisha wapinzani.
Awali wakati akijibu swali hilo, Odinga ambaye miezi mitatu iliyopita alikuja nchini na kukutana na Rais Magufuli nyumbani kwake Chato, ziara ambayo ilizua gumzo hapa nchini na Kenya, alianza kwa kusifu kazi iliyofanywa na kiongozi huyo ya kusafisha hekalu lake pindi tu alipoingia madarakani Novemba mwaka jana.
“Kwanza nimshukuru sana Rais Magufuli kwa yale aliyofanya, tangu ashike hatamu ya utawala Tanzania kuna maendeleo mengi ambayo yamefanyika kwa mfano ile vita dhidi ya ufisadi, uzembe na kuleta nidhamu kwa upande wa kutoa huduma kwa wananchi.
“Sasa waliolala usiwaamshe (kicheko), lakini mimi sioni kama kuna shida kubwa, kama upande huo wapinzani wanatafuta relevance sasa kwa hivyo nilikuwa sitaki kujiingiza katika mambo ya ndani ya Tanzania,” alisema.
Wakati haya yakitokea sasa kwa takribani miezi mitano kumekuwa na vita baridi ya kisiasa kati ya Serikali ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) na vyama vya upinzani vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa).
Msingi wa vita yenyewe ni madai yanayotolewa na Ukawa, hususani Chadema kwamba Taifa limeporwa haki na demokrasia na Serikali inayotawala.
Kutokana na hilo hivi karibuni Chadema walitangaza kufanya mikutano na maandamano nchi nzima ifikapo Septemba mosi mwaka huu kupitia operesheni waliyoibatiza jina la Umoja wa Kupambana na Udikteta Tanzania (Ukuta).
Hatua hiyo ya Chadema ilionekana wazi kumkera Rais Magufuli ambaye akiwa katika ziara ya chama chake mkoani Singida takribani wiki mbili zilizopita alikaririwa akisema yeye si mtu wa kujaribiwa na kwamba mwanasiasa atakayeandamana kinyume na maagizo yake atakiona cha mtema kuni.
Rais Magufuli alisema mtu pekee anayeweza kupita kila mahali ni yeye peke yake kwa sababu ni rais huku pia akiruhusu mikutano kwa wabunge wenye majimbo tu.
Juni mwaka huu, Rais Magufuli alitangaza kupiga marufuku mikutano ya siasa za ushindani hadi mwaka 2020, akiwataka watu kufanya kazi.
Odinga afichua aliyoteta na JPM
SOURCE: Mtanzania