Simulizi - change (badiliko)

Simulizi - change (badiliko)

CHANGE

Story by Elton Tonny

Urafiki, Familia, Mapenzi, Mahaba, Tamaa, Hila, Usaliti, Unyanyasaji, Ukatili, Mauaji, Mambo yasiyotazamiwa, Mambo yenye kuhofisha

R-rated 18+

Enjoy!

★★★★★★★★★★★★★★★★★

SEHEMU YA ISHIRINI NA MBILI

★★★★★★★★★★★★★★★★★


Namouih alifika nyumbani kwake kwenye mida ya saa tatu asubuhi hiyo, naye akaelekea chumbani na kumkuta mume wake akiwa tayari kuondoka, lakini haikuwa kuondoka kwenda kazini. Alikuwa ameweka nguo chache kwenye begi dogo la mgongoni na baadhi ya vifaa muhimu vya kikazi, jambo lililomwambia Namouih kwamba mume wake alikuwa anataka kufanya safari fupi ya kikazi. Efraim Donald alimlaki Namouih kwa furaha baada ya kuwa amerudi, naye akamuuliza ikiwa mambo yalikwenda vizuri jana akiwa na rafiki yake.

Kwa kutotaka kuingiza zile habari za ugomvi uliotokea usiku, Namouih akaamua kuficha ukweli na kusema, "Ndiyo. Mambo yalikwenda vyema."

"Angalau umetuliza akili kidogo eh?" Efraim Donald akamuuliza.

Namouih akatikisa kichwa kukubali na kuangalia chini kama kuonyesha hana raha.

"Ona Namouih... najua tuna mambo mengi sana ya kuzungumzia ila kuna huu mkutano mkubwa umejitokeza... masuala yale yale ya mikataba na nini... kwa hiyo nafikiri ndani ya wiki nitakuwa nimerudi. Naomba univumilie... tutaongea vizuri sana nikirudi," Efraim akamwambia huku akiwa ameyashikilia mabega ya mke wake.

"Ni sawa Efraim. Nitasubiri," Namouih akamwambia.

"Nitakaporudi nafikiri maandalizi yatakuwa yameshakamilika... nataka hii party mwaka huu iwe spectacular... utafurahia sana honey," Efraim akasema.

"Party?" Namouih akauliza akiwa hajaelewa.

Efraim Donald akaachia tabasamu na kuuliza, "Umesahau?"

"Nini?"

"Birthday yako inakaribia Namouih," Efraim akamkumbusha.

Namouih akatazama pembeni na kuachia tabasamu hafifu, naye Efraim Donald akacheka kidogo.

"Mambo yamekuwa mengi, siyo rahisi kukumbuka yaani. Ulikuwa unafanya maandalizi ya birthday
party?" Namouih akauliza.

"Yeah. Na ninataka mwaka huu ndugu zetu wote wawepo huku," Efraim akasema.

Namouih akatabasamu huku akimwangalia kwa hisia.

"Mama, Zakia, Sasha, Nasma, na washkaji zako wote nawaleta huku... ahah... nataka yaani ifunike sherehe zingine zozote za kuzaliwa nchi nzima," Efraim akamwambia.

"Ahahah... haiwezi kuzidi sherehe zingine zote. Kuna watu wana pesa zaidi yaani siku ya kuzaliwa mtu ananunuliwa ndege," Namouih akasema.

"Aa, hayo ni akina Beyonce na Jay-Z tu ndiyo wanafanya, ushaona wapi kwa nchi yetu? Wewe subiri tu, nimekuahidi utaifurahia, utafurahia kweli," Efraim akasema.

Namouih akatikisa kichwa kukubali na kusema, "Sawa. Asante Efraim."

Efraim Donald akambusu mke wake mdomoni, na Namouih akatania kwamba hakuwa ameosha mdomo kwa hiyo busu hiyo isifike mbali. Mume wake akacheka na kumkumbatia, kisha akaanza
kuondoka na kwenda mpaka nje ili kupanda gari; alikokuwa anasubiriwa na Suleiman. Kupitia dirishani, Namouih alisimama kwenye kiubaraza kidogo kwa nje huko huko juu na kumpungia mkono wa kwa heri mume wake, kisha Efraim Donald akaingia ndani ya gari na kuondoka hapo hatimaye.

Namouih alibaki amesimama sehemu hiyo akiwaza mambo mengi. Ni ile hali fulani ya kuhisi hatia
kwamba ingawa alikuwa amemwambia mume wake jambo zito sana siku iliyotangulia, bado
mwanaume huyo alimtendea vizuri na angalau kwa wakati huu alionyesha nia ya kutaka kurekebisha mambo. Lakini bado Namouih hakuwa ameridhika mpaka suala lile lililoisumbua ndoa yao litatuliwe kwa usahihi, kwa hiyo ingawa alihisi ni kama anamsukuma mno mume wake, bado angeendelea kushikilia msimamo huo mpaka kieleweke kweli.

Akarudi tu ndani baada ya hapo na kwenda kuoga, kisha akavaa nguo nzuri sana za kikazi na kujitengeneza vizuri sana kichwani na usoni kuumeremetisha urembo wake, halafu akaamua kumpigia tu rafiki yake ili kumjulia hali. Blandina alipopokea simu, aliongea kwa shauku nyingi sana akisema yeye na Draxton walikuwa wamerudiana tena, na ingawa alihisi kwamba furaha yake ilipita kiasi mno lakini bado alijihisi vizuri sana moyoni. Aligusia pia suala la jinsi alivyoamka na kujikuta hana jeraha kichwani, naye Namouih akamwambia tu Draxton alipofika pale walipokuwa usiku wa
jana alimsaidia kwa dawa, bila kusema kwa undani ni dawa gani hiyo. Blandina akasema kwamba
wangekutana baadaye ofisini kwa kuwa alijisikia vizuri sana kufanya kazi leo.

Jinsi Blandina alivyokuwa anamwongelea mwanaume wake, kwamba amempikia, jana alimwokoa, na kumbeba mpaka chumbani, bila kusahau busu kali waliyopeana asubuhi hiyo, ilimfanya
Namouih acheke sana. Akafurahi kwa ajili ya rafiki yake na kumpa hongera, kisha wakaagana kwa
wakati huo, na mwanamke huyu akaelekea chini kupata kiamsha kinywa alichoandaliwa na Esma.
Akatumia muda mfupi kucheza na paka wake wa kufugwa, na baada ya hapo akaelekea kazini pia.

★★

Watu wengi ndani ya kampuni aliyofanyia kazi Namouih walifurahi sana kumwona tena, na wengi
walitumia muda wao kuzungumza naye wakimjulia hali na kuuliza jinsi alivyookoka kifo kwenye ile "ajali" iliyompata. Aliongea kwa ustaarabu na kuwashukuru wengi waliomtumia salamu zao, na sasa alikuwa amerudi kazini tena kuendelea kufanya kazi kwa bidii, hivyo bila kukawia akaingia ofisini kwake na kumkuta Blandina akiwa humo. Marafiki hawa wakakumbatiana kwa upendo mwingi sana, na Blandina alionekana kuwa na furaha isiyo na kifani, kwa hiyo wangezianza kazi
zao huku wanapata maongezi kuhusu mambo yaliyotokea jana usiku mpaka Blandina akajikuta
anaamkia mikononi mwa Draxton wake asubuhi hii.

Waliendelea na kazi za hapa na pale mpaka imefika mida ya saa saba mchana, ndiyo Namouih akawa amemwita Blandina na kumkumbusha kuhusu kukutanika kwao na marafiki zao wale wawili
waliokuwa wanakuja upande huu wa jiji leo kuwatembelea. Blandina alikuwa ameshasahau kabisa kuhusu hilo, naye akamwambia Namouih kwamba kwa sababu alikuwa amesahau, tayari alikuwa
ameshafanya mipango ya kukutana na Draxton mchana huo kwa hiyo alihisi asingeweza kwenda kule walikopanga kukutana na rafiki zao hao. Namouih akamwambia haikuwa na shida, kwamba waende kukutana na rafiki zao huko kwa muda huu kabla Draxton hajaja kumpitia, au angempitia wakiwa huko huko.

Wazo la pili lilionekana kuwa zuri hasa kwa sababu Blandina alitaka sana pia kuwaona mashosti zake wale, kwa hiyo akatoka na kumpigia simu Draxton ili amjulishe kwamba angekwenda sehemu fulani ya jiji, kwa hiyo ampitie akiwa huko. Draxton kama Draxton hakuwa na shida, naye akasema kuna mambo alikuwa anamalizia kisha ndiyo angempitia kwa hiyo wangeonana baadaye. Basi baada ya hayo, Blandina akamjulisha Namouih, ndiyo marafiki hawa wakaondoka pamoja kuelekea kule walikoahidiana kukutana na marafiki zao; Dantu na Marietta.

★★

Marafiki hawa wawili walikwenda pamoja kwenye eneo la kati la jiji ambako kulikuwa na hoteli fulani ya kifahari sana iliyopewa jina Zakhem. Haikuwa hoteli kwamba ni hoteli iliyopokea wageni wa kulala, bali hoteli maalumu kwa ajili ya vyakula vizuri sana na vya gharama. Ilikuwa ni kama mgahawa lakini kwa sababu ya kiwango chake kikubwa cha umaridadi iliitwa hoteli, na Namouih
pamoja na Blandina wakawa wamefika hapo na kwenda ndani kutafuta sehemu za kukaa.

Walikaribishwa vyema, nao wakapewa meza moja iliyozungukwa na viti kama masofa, kisha wakaagiza vinywaji vya juice za cream na chips fulani kavu sana zenye pilipili kali (chilli fries), nao
wakaanza kula taratibu huku wakiwasubiria marafiki zao ambao tayari walikuwa wamekwishawasiliana nao. Hatimaye Dantu na Marietta wakawa wamefika, nao wakapokelewa kwa shangwe sana kwa kuwa ni muda mrefu ulikuwa umepita bila ya wao kuonana. Waliishi mkoa tofauti na huu na walifanya kazi kwenye maduka makubwa ya vito vya gharama na masuala ya mitindo na urembo, hivyo walikuwa aina ya wanawake wenye nguvu kipesa.

Dantu alikuwa mweupe, mtu wa zenji, na ingawa alikuwa na miaka 40 lakini alionekana kuwa kama na miaka 25 kutokana na kujua kupangilia mwonekano wake kwa uzuri wa hali ya juu. Alikuwa
mwanamke mwerevu sana na ndiyo alikuwa amevalishwa pete siku za hivi karibuni na mpenzi wake wa muda mrefu mwenye pesa pia, na tayari alikuwa na mtoto mmoja wa kike pamoja na huyo huyo mchumba wake. Marietta yeye alikuwa mwanamke mzuri sana pia, mwenye miaka 35, aliyekuwa na mashauzi mengi hatari. Alipenda sana kuponda raha na alikuwa na akili nyepesi, yaani mjanja. Umbo lake lilikuwa namba nane, na urefu wake ulikaribiana na urefu wa Namouih
hasa kama angevaa viatu virefu, na alikuwa bado hajaolewa wala kuwa na mtoto.

Ujio wao ulifanya wote wachangamke na kuanza kuongelea mambo mengi sana yenye kufurahisha na hata kuhuzunisha, kama suala la kifo cha Felix, na wanawake hao pia wakaagiza vyakula na juice ili kujiunga pamoja na wenzao kwenye makamuzi. Maongezi yalipohamia kwenye maisha ya mapenzi, wote waliwazungumzia wanaume wao na namna wanavyoumiza vichwa sana lakini hakukuwa na namna ila kukomaa tu na mahusiano. Blandina alianza kumwongelea Draxton wake
pia, akimsifia kuwa mtu mzuri mno ambaye hajawahi kukutana na aina yake hata mara moja. Alikuwa anamwongelea vizuri sana kwa mashoga zake hasa kwa kuwa Marietta aliulizia mno habari zake. Blandina angesema kwamba Draxton alimfaa kabisa hata kuolewa naye, na Namouih akawa kimya tu kuelekea maongezi yaliyomhusu mwanaume yule ingawa alijua vitu vingi kumhusu.

Baada ya muda mfupi, Blandina akapigiwa simu, ikiwa ni Draxton, ambaye alimjulisha kwamba tayari alikuwa sehemu ya nje ya jengo hilo kumpitia, hivyo mrembo atoke ndani hapo. Baada ya Blandina kukubali na kukata simu, Dantu na Marietta wakaanza kumshinikiza amlete Draxton ndani hapo ili nao wamwone pia kwa sababu walitaka tu hata kusikia sauti yake. Namouih akaingilia kati na kuwaambia halingekuwa jambo zuri kumsumbua kaka wa watu, lakini wenzake wakampondea, wakisema aache ubahili wa macho kwa kuwa yeye tayari aliwahi kumwona. Wakamshawishi Blandina atunge kisingizio chochote tu cha kumwambia Draxton ili amlete ndani hapo, naye Blandina akakubali na kuondoka. Hata hivyo na yeye Blandina alitaka mashoga zake wamwone mwanaume wake mubashara ili awadolishie kwa njia fulani, kama ujuavyo mambo ya wanawake.

Akatoka mpaka nje na kuliona gari la mwanaume wake likiwa limeegeshwa usawa wa barabara,
naye akaliendea na kuingia ndani yake, akitazamwa na watu kadhaa kutokana na mwonekano wa shepu nono aliokuwa nao. Draxton alikuwa ameketi kwenye siti ya usukani huku akimwangalia kwa upendezi, naye Blandina akampa tabasamu la madoido.

"Tukazurure sasa," Draxton akamwambia.

"Ndiyo, ila kuna ishu imezuka..." Blandina akasema.

"Mm-hmm..."

"Kuna rafiki yangu mwingine... ana mzigo wangu. Anatoka huko juu anakuja kunipitishia, kwa hiyo
naomba tumsubirie kidogo," Blandina akamwambia.

"Sawa, haina shida," Draxton akamwambia kwa upole.

"Twende ndani basi, tukamsubirie..."

"Huko ulipokuwa?"

"Yeah."

"Si ni bora tu tukikaa humu?"

"Ndiyo ila, nimewaacha rafiki zangu pale. Itakuwa nzuri zaidi tukienda kukaa nao kwa ufupi."

Draxton akapandisha nyusi huku akimtazama kama anauliza 'kweli?'

"Ahahah... na ndiyo, nataka wakujue pia. Dantu kavishwa pete juzi juzi, twende hata ukampe hongera," Blandina akasema.

Draxton akavuta pumzi na kuishusha huku akisema, "Okay."

Blandina akafurahi na kumsogelea karibu zaidi, naye Draxton akambusu mara tatu mdomoni. Lipstick nyekundu ya Blandina ikabaki mdomoni mwake Draxton, naye Blandina akaifuta taratibu huku wakiangaliana kwa hisia.

"Twende."

Blandina akamwambia hivyo na kuketi vizuri kwenye siti yake. Draxton akazima gari lake na
kushuka, halafu akazungukia upande wa Blandina na kukuta anashuka pia. Akaifunga milango na wote wakaanza kuelekea kwenye hoteli ile huku wameshikana mikono. Draxton alikuwa amevalia koti gumu jeusi (leather jacket) lililokuwa juu ya T-shirt nyeupe aliyovaa kwa ndani, suruali ya jeans ya rangi nyeusi na viatu vyeusi chini. Blandina alitembea naye kwa ukaribu sana, akijivunia kuangaliwa na baadhi ya watu eneo hilo ingawa hakuonyesha hilo.

Wakafika sehemu ya ndani na kuanza kuelekea pale alipowaacha rafiki zake. Tayari rafiki zake
Blandina walikuwa wamemwona Draxton pindi alipoingia tu, nao wakawa wanasema kweli jamaa alionekana kuwa ngangali sana mbali na kuwa na sura nzuri. Namouih alikuwa anamtazama kwa
umakini, akipendezwa kwa kiasi fulani na mwonekano wa mwanaume huyo. Draxton tayari alikuwa
ametambua uwepo wa Namouih kwenye mchanganyiko wa watu hapo baada ya kuivuta harufu yake mapema, na hakuwa ametarajia kumkuta hapo pia, lakini kuvunga kwamba hawakuwa na akili
moja juu ya jambo fulani ilikuwa kitu muhimu kwa wawili hawa.

Blandina akawa amemfikisha mwanaume wake walipokuwa Dantu, Marietta, na Namouih, nao
wakasalimiana vizuri. Blandina akaketi kwenye sehemu yake na kumwachia nafasi Draxton ili naye
akae, na mwanaume akaketi. Harufu nzuri ya Draxton iliwavutia sana wanawake wote, na Marietta akaanza kumsemesha.

"Draxton... agiza chochote... me nitalipa," akasema kiutani.

Wengine wakacheka, naye Blandina akasema, "Tayari unataka kumuiba!"

"Siyo hivyo, ila we' ukichelewa lazima me nijiongeze," Marietta akamwambia.

"Umekwama baby. Drax, huyu ni Marietta na Dantu. Yule pale nafanya naye kazi hata simkumbuki jina lakini," Blandina akawatambulisha wenzake, nao wakacheka kwa namna alivyomtania Namouih.

"Nimefurahi kuwafahamu. Hongera pia Dantu kwa kuwa unaelekea kuwa jiko rasmi," Draxton akaongea.

"Ahahahah... asante. Amekwambia huyu eeh?" Dantu akauliza.

"Ndiyo," Draxton akajibu.

"Nasikia ulivunja rekodi ya Namouih ya kutopoteza kesi hata moja," akasema Marietta.

Wengine wakacheka kidogo, kisha Namouih akasema, "Yeah. Draxton ni bingwa."

Draxton akamwangalia machoni, naye Namouih akatabasamu kwa mbali na kuangalia chini.

"Mwitie mhudumu basi," Marietta akamwambia Blandina.

"Oh no, niko sawa. Tunamsubiri tu rafiki yenu, akifika tunaondoka," Draxton akasema.

Blandina akawatazama wenzake na kukodoa macho kidogo huku amejishika shingoni, njia fulani ya kuwaambia kwamba hicho ndiyo kisingizio alichokuwa amempa jamaa. Wenzake walipoelewa hilo, wakaanza kusema 'aaaah sawa' kwa kupishana, jambo lililofanya Namouih acheke kidogo.

"Vipi? Mbona unacheka?" Draxton akamuuliza.

"Aa... hamna kitu. Nilikuwa tu nimekumbuka kitu fulani... kabla hujafika tulikuwa tunazungumzia
kuhusu wasanii. So nimekumbuka tu," Namouih akaongea kwa kujihami ili abadili mawazo upesi.

"Okay sawa. Wasanii na vituko vyao eh?" Draxton akauliza.

"Yeah, ila sana sana kuhusu mafanikio. Tulikuwa tuki-discuss nani angefika mbali sana kama Mdee na Mondi walivyofanikiwa kufanya kwanza," Blandina akamwambia.

"Siyo Diamond na Vanessa Mdee peke yao, ni basi tu kwa sababu wewe unawashobokea sana,"
Marietta akamwambia.

"Nani mwingine amefika mbali kabla yao? Kisanaa tu?" Blandina akauliza.

"Wapo wengi mbona? AY, K-Lynn, Kanumba... tena Kanumba ndiyo alikuwa kubwa yao," Marietta
akasema.

"Ee... ndiyo ni kweli, Kanumba. Imagine kama angekuwepo mpaka sasa hivi. Alikuwa na kipawa kizuri sana cha kutunga story," Dantu akasema.

"Eee kweli. Nani mwingine angetop hao watatu? Eti Draxton? We' unafikiri nani?" Marietta akauliza.

Draxton akatabasamu tu.

Namouih alikuwa anamtazama kwa umakini sana.

"Haionekani kama unafatiliaga sana wasanii, eti shem? Oh, ni sawa nikikuita shem?" Marietta
akamuuliza.

Wengine wakacheka kidogo, naye Draxton akasema, "Ndiyo ni sawa, shem."

Blandina akaachia tabasamu la furaha sana.

"Najua wasanii pia Marietta, na mimi kwa upande wangu nafikiri ingekuwa ni Sharo Millionea," Draxton akamwambia.

"Oh, maskini! Umenikumbusha mbali sana," Dantu akasema kwa shauku.

Namouih akaachia tabasamu hafifu huku akimtazama Draxton, na marafiki zake wakaanza kuongelea kuhusiana na jinsi msanii huyo alivyokuwa vizuri aana.

"Alikuwa na style nzuri mno. Angekuwa mbali sana kuliko hata huyo ndomo wako!" Marietta
akamwambia Blandina.

"Thubutu! We' si ndiyo wale vibishoo vya bandia aliowaimba ndiyo maana hazipandi fresh," Blandina akasema.

"Na ndiyo maana haukuagi tu. Draxton usipoangalia atakuja kukufanya kuwa henpecked huyu,"
Marietta akasema.

"Kweli eti? Bora tu nimteme mapema kabla haijawa too late," Draxton akaongea kiutani.

"Halafu uende kwa nani?" Blandina akamuuliza.

"Marietta," Draxton akamwambia na kuwafanya wengine wacheke.

"Weee, 'ntamuua," akasema Blandina.

"Ahahahah... atanilinda Draxton. Tunazaa na watoto tunakimbia, unakuja kutukuta Haiti," Marietta
akasema.

"Koma. Drax angalia huyu asije akakupulizia unga," Blandina akasema.

Maongezi yao haya ya kuzoeana yalifanya wachangamke, naye Dantu akauliza, "Una miaka mingapi Draxton?"

Namouih akamwangalia Draxton kwa umakini, akisubiri kusikia jibu lake.

"Ishirini na tano," Draxton akasema.

"Eh! Kumbe? Unaonekana mkubwa!" Dantu akasema.

"Na ni lazima awe na mambo kubwa," Marietta akasema kiutani.

Wote wakacheka kwa pamoja, na Namouih akamsukuma Marietta kidogo begani.

"Ahahah.... Kwa hiyo Draxton, uko tayari kufanya commitment kwa Blanding'a?" Dantu akamuuliza.

Lilikuwa swali ambalo Draxton hakutarajia kabisa, naye akaangalia chini kidogo.

"Halafu nimeshakukataza kuwa unaniita hivyo," Blandina akamwambia Dantu.

"Oh, am sorry Blanding'aaa," Dantu akamtania tena.

"Blandina mali safi bwana, shem hatachelewesha. Draxton wachawi wengi, inabidi umweke huyu ndani mapema kabla hawajamroga kukuacha," Marietta akasema.

Blandina na Dantu wakacheka kidogo, naye Draxton akatabasamu pia. Namouih akamwangalia Draxton na kutambua kwamba tabasamu hilo lilikuwa la kujilazimiaha, naye akagundua kwamba maongezi hayo kuhusu ndoa yalimfanya asijihisi wepesi.

"Drax wazoee tu hawa, wanaongea mno," Blandina akamwambia.

"Yeah, Marietta ana point. We ni mali safi Blandina. Lakini bado nitakimbia naye kwenda Haiti," Draxton akatania.

Wanawake wakacheka, naye Blandina akampiga Draxton begani kidogo.

"Kuna stage tano za uhusiano. Kujuana, urafiki, kupendana, commitment, na ndoa. Mie na Blandina tupo ya tatu, na tutaruhusu muda upite ili kuona kama tunafaana vya kutosha kufika mpaka ya tano," Draxton akasema hivyo na kukiingiza kiganja chake ndani ya kiganja cha Blandina.

Dantu akatabasamu na kusema, "Unaongea vizuri sana."

"Ndiyo, kisomi zaidi. Blandi lazima aringe," Marietta akasema, nao wakacheka pamoja.

Draxton akaendelea kuonyesha ustaarabu wake mzuri, lakini Namouih akiwa ameshaona jinsi hali
hii ilivyomkosesha amani kwa kiasi fulani, akaamua kukatisha mkutano huu kwa njia isiyo ya moja kwa moja.

"Blandina... mpigie basi nanii... muulize amefika wapi," Namouih akasema.

"Oh, sawa. Babe, ngoja nimpigie huyu. Nakuja," Blandina akamwambia Draxton.

Draxton akatikisa kichwa kukubali, naye Blandina akanyanyuka na kwenda pembeni kuigiza kwamba alikuwa anampigia huyo rafiki mwingine.

Dantu na Marietta wakaendelea kumsemesha Draxton, lakini Namouih akatambua kwamba
umakini wa mwanaume huyu ulikuwa kwa Blandina ingawa hakumwangalia. Si ndiyo akawa
amekumbuka kwamba jamaa anaweza kusikia mbali! Maigizo ya Blandina hayakuwa na faida yoyote kwa kuwa Draxton akamwangalia Namouih kwa ufupi na kuachia tabasamu hafifu, kisha akatazama chini tu. Namouih akaibana midomo yake na kufunika uso kwa kiganja akihisi aibu kiasi, na hakuna yeyote kati ya rafiki zake aliyegundua yaliyoendelea baina ya wawili hawa.
Namouih akawa anajizuia kutoa tabasamu la wazi, naye Draxton akaendelea tu kushiriki maongezi
na rafiki zao.

Blandina akarejea kutoka alipokuwa amesimama, naye akamwambia kwamba rafiki yake huyo amesema kwamba angechelewa sana kwa hiyo wangeweza tu kuondoka sasa. Marafiki zake walikuwa wakidhani kwamba uzushi huo mdogo ulifanikiwa kwa asilimia zote, kwa sababu waliridhika kumwona "shem" na haikuonekana kama alijua walichofanya, ila Namouih alielewa wazi kwamba Draxton alijua. Mwanaume akamwambia Blandina tu sawa, yaani haina shida, kisha
wakawaaga wengine na kuanza kuondoka hatimaye.

Marietta akawa akimsifia sana Draxton, akiwaambia rafiki zake yaani kwa mwanaume mzuri kama huyo ikiwa Blandina angezubaa basi yeye angepita naye. Namouih alitaka hata kumzuia asiongee hivyo kwa kuwa alielewa kwamba Draxton angemsikia, lakini kwa hapo ingekuwa kazi bure maana
Marietta aliendelea tu. Namouih kujua Draxton kutokuwa mtu mwenye makuu wala gubu lolote
kulimfanya atulie tu, na alizidi kupendezwa sana na jinsi mwanaume yule alivyoonyesha usawaziko na kujitahidi kushughulika na hali hii iliyokuwa tata kwake kwa njia nzuri.

★★

Muda ulisonga sana siku hii, na Namouih alikuwa ameachana na Dantu pamoja na Marietta tayari,
ambao walielekea kule walikochukua chumba cha kulipia kwa muda ambao wangekuwa jijini. Blandina na Draxton walikuwa wameachana pia baada ya kufanya mizunguko mingi pamoja, na mwanamke huyo alirudi tena kazini pamoja na Namouih ili kufunga kazi zao zingine. Namouih yeye akawahi kuondoka ikiwa imefika mida ya saa kumi na moja, na Blandina angemalizia muda
uliobaki wa saa moja kwa kuwa kazi zao zilikwisha muda wa saa kumi na mbili; yaani kwa upande wao wa kazi za kisheria.

Namouih hakuwa amekwenda kupumzika nyumbani, bali alikuwa anakwenda pale Draxton
alikopangishwa vyumba. Walikuwa wameshawasiliana kwa ujumbe na kukubaliana kukutana huko ili wazungumze kuhusiana na suala la kifo cha Felix, kwa kuwa Draxton alikuwa amepata mambo fulani katika uchunguzi mdogo aliokuwa ameufanya. Hawakutakiwa kumwambia Blandina kuhusiana na hili kwanza ili wafanye mambo kwa umakini, kwa hiyo rafiki yake hakujua kama anakwenda nyumbani kwa mpenzi wake kwa muda huo.

Akawa amefika nje ya nyumba hiyo, na kwa kupendeza, Draxton tayari alikuwa amesimama nje akionekana kuwa anamsubiri. Namouih akatabasamu tu baada ya kumwona, kisha akashuka kutoka ndani ya gari baada ya kuliegesha. Leo Namouih alikuwa amevaa nguo fulani iliyounganika kama suti ya kike iliyobana na kuishia magotini, nyeupe yenye mistari myekundu na myeusi ya drafti, iliyokuwa imeacha uwazi katikati ya matiti yake na kuyafanya yaonekane kwa juu kiasi, hivyo alikuwa anaonekana kuwa mtamu balaa! Draxton yeye sasa alikuwa amevalia tu T-shirt nyeupe yenye mikono mifupi na kaptura ya kijani, akionekana kuwa makini sana kama vile amemsubiri mwanamke huyo hapo kwa hamu, na Namouih akawa amemfikia karibu.

Draxton akajisawazisha namna alivyokuwa amesimama huku akionekana kuivuta harufu nzuri ya
mwanamke huyo, na Namouih akatabasamu na kupitisha kidole chake kwenye nywele yake
iliyokuwa imedondokea usoni na kuirudisha nyuma kwa njonjo.

"Samahani..." Draxton akasema hivyo, akimaanisha suala la yeye kushindwa kujizuia kuvuta harufu
nzuri ya mwanamke huyu.

Namouih akatabasamu kidogo na kusema, "Usijali. Nimeshazoea."

Draxton akatikisa kichwa kuonyesha uelewa, kisha akamwambia amfuate ili wakaongelee kule ndani. Sehemu hiyo ya nje ilikuwa na watu kadhaa waliowaangalia sana hasa kutokana na Namouih kuonekana kuwa wa matawi na mrembo mno, na wawili hawa wakaelekea ndani huku wazushi wakianza kusema huyo mwanamke "sugar mommy" alikuwa amepelekwa kupigwa miti huko ndani; kama kwa lugha ya waswahili. Namouih akapelekwa mpaka ndani kwake Draxton, ikiwa ndiyo mara ya kwanza kabisa kuingia hapo, na kiukweli alivutiwa na namna palivyopangiliwa vizuri. Akaketi kwenye sofa moja, kisha Draxton akamletea juice ya baridi kwenye glasi na kumwekea mezani.

"Asante," Namouih akasema huku akitabasamu.

"Karibu. Hapa ndiyo mageto," Draxton akasema.

"Ahahahah... mara ya kwanza nimekukuta hapa unakumbuka ilivyokuwa?"

"Ahahah... ulikuwa mkali kweli!"

"Mimi au wewe?"

"Ahahahah... basi wote."

Namouih akatabasamu na kunywa juice kidogo. Alipomwangalia tena Draxton, akaona akiwa kama
ameinamisha uso na kukaza macho yake kwa umakini, halafu akaachia tabasamu la chini kiasi lililofanya Namouih atambue kwamba kuna kitu fulani kilikuwa kinaendelea.

"Vipi Draxton?" Namouih akauliza.

"Naam?"

"Kwa nini una... tabasamu namna hiyo?"

"Aa... hakuna kitu wala... usi..."

"Niambie," Namouih akasema huku naye akitabasamu.
Draxton akaangalia pembeni na kutabasamu tena, kwa njia iliyoonyesha kuna jambo lilikuwa
linamfurahisha sana.

"Niambie basi... nini kinakufurahisha?"

"Ni... majirani... humo ndani. Wanatuongelea," Draxton akamwambia.

"Ahahah... kweli? Unawasikia?"

"Ndiyo."

"Wanasemaje?"

Draxton akatabasamu na kutikisa kichwa chake.

"Tell me," Namouih akamsisitizia huku akitabasamu.

"Wanaongea sana. Wanafikiri mimi na wewe tumekuja ku... you know..."

"Ahahahah... ni Rehema na Salhat eeh?"

"Unawajua?"

"Ahahah... ndiyo. Nimeshakutana nao. Nafahamu wana maneno mengi sana. Wameshawahi kuona umemleta Blandina hapa kwa hiyo lazima waongee tu..."

"Yaani!"

"Ahahahah... piga picha kama Blandina angejua nimekuja huku now, au mara ghafla aje anikute
hapa..."

"Ahah... angeshangaa ila na yeye ndiyo angetakiwa kueleza kwa nini alinidanganya kwamba rafiki yake anamletea mzigo ili tu wenzake wanione..."

Namouih alikuwa anakunywa juice wakati huu, naye akaishusha huku akicheka sana kwa kusikia kauli hiyo.

"Niligundua umetambua kwamba alikuwa anazuga tu, yaani Draxton nilihisi aibu," Namouih akamwambia.

Draxton akacheka kidogo.

"Haikukukera kabisa kwamba alikuzingua namna hiyo?" Namouih akamuuliza.

"La. Nafurahi Blandina akionyesha anajivunia kuwa na mimi. Angalau yeye hafichi mambo mazito kama ilivyo kwangu," Draxton akamwambia.

Namouih akawa anamwangalia kwa uelewa.

"Okay, tuachane na hayo. Back to Felix," Draxton akasema.

"Right."

"So, usiku huo tulikutana pub moja hivi, nilikuwa na Blandina, tukaongea kifupi sana, na... kiukweli nilitambua alitenda kwa njia fulani ya udadisi kwangu mimi ingawa sikujua alikuwa ameanza kunipeleleza. Sikuwa nimeamua kufuatilia vifo vya wasichana waliokuwa wanakufa kila mwezi kwa njia ile ile mpaka jambo hilo lilipompata Agnes. Nilipoenda pale ile siku huyo msichana ameuliwa, ilikuwa ni ili kumsaidia... lakini pia kuona kama ningepata harufu ya mhusika," Draxton akaeleza.

"Harufu?"

"Ndiyo. Uwezo wangu wa kuvuta harufu unaniruhusu kufuatilia ilikoelekea, na nilijaribu kufuatilia ya
mhusika wa mauaji ya Agnes lakini nikashindwa kufikia mwisho wake. Ilikuwa ni kama... ilipotea tu... kitu ambacho siyo cha kawaida. Mwanzoni nilidhani ningepata harufu ya mtu aliyemtoa Agnes kifungoni siku hiyo au yeyote yule regardless lakini... hiyo harufu ili-vanish tu. Ni ngumu sana kujua ni nani kwa njia hiyo tena ikija kwa Felix, na siwezi kupata njia nyingine hasa kwa kuwa mwili wake umeshazikwa," Draxton akamwambia.

"Ulijuaje kwamba harufu ya aliyemuua Felix ndiyo harufu ile ile ya muuaji wa Agnes sasa?"

"Felix alikatwa tumbo akiwa bado na nguo, tofauti na Agnes na wasichana wengine. Kwenye taratibu za kuuhifadhi mwili wake niliweza kuipata harufu hiyo kwenye nguo yake waliyoitupa tu. Nilikuwa nimejitahidi sana kufatilia hii harufu kwa uwezo wote nilionao... lakini na penyewe haikuwa na matokeo mazuri..."

"Ulifanya hayo yote lini?"

"Siku ya kuamkia.... baada ya kifo chake. Nilijaribu kila mara Namouih... nilitaka sana kujua nani alimfanyia vile lakini ikashindikana, na sikutaka wenye mamlaka wanikute nikifanya uchunguzi huo, na maswali na nini... unaelewa...."

"Ndiyo naelewa. Nilikuwa nafikiri hukuwepo msibani na Blandina kwa sababu ulijificha kumbe... inabidi nirudie kukuomba tena samahani kwa kukufanyia nilivyokufanyia siku ile msibani ulipo...."

"Namouih usiwe na hofu, hiyo imeshapita. Unatakiwa ujue kwamba kuna jambo fulani ambalo liko
tofauti kati ya hivi vifo vyote ikilinganishwa na kifo cha Felix," Draxton akamwambia.

Namouih akabaki kumtazama kwa umakini, akiweka usikivu wa hali ya juu.

"Dhumuni la kumuua Felix lilikuwa tofauti na lile kwa wasichana wengine wote kufikia Agnes.
Nimefatilia taarifa za baadhi ya wasichana hao na kugundua kwamba wote wamekufa tarehe 19 ya kila mwezi, hata na Agnes pia. Nachojaribu kusema ni kwamba, kila mara msichana anapouawa kwa njia hiyo, hana nguo, tarehe ni moja kwenye kila mwezi, lengo ni moja. Lakini Felix kafa kwa njia hiyo hiyo, ana nguo, tarehe tofauti,...."

"Lengo tofauti," Namouih akamalizia maneno ya Draxton.

"Ndiyo. Kwa nini lengo liwe tofauti? Ni kwa sababu tofauti, lakini mhusika ni yule yule. Ikiwa tutasema ni kwa sababu Felix alikuwa anapeleleza vifo hivi, hiyo hainge-make sense kwa kuwa
wanaofatilia ni wengi. Kwa nini iwe yeye? Aliyemuua Felix ni yule yule aliyemuua Agnes, lakini kwa Felix ilikuwa ni kwa sababu ya KIBINAFSI, na siyo kwa MPANGILIO kama ilivyo kwa wasichana," Draxton akaeleza.

Namouih akatazama chini na kutikisa kichwa chake kwa uelewa, kisha akasema, "Nilikuwa hata
sijatambua kwamba tarehe ni ile ile ya mwezi kila mara msichana anapouawa namna hiyo. Tarehe 19. Kwa nini tarehe 19?"

"Kwa hapa ni ngumu sana kumpata huyu mtu, maana haachi clue zozote, ni maeneo tofauti-tofauti ya mkoa, na ndiyo sababu maaskari wanashindwa kujua aliko."

"Kwa hiyo unasema kwamba tutatakiwa kusubiria mpaka tarehe 19, msichana mwingine afe, ili
tufatilie kwa ukaribu?"

"Ndiyo inavyoonekana. Wengi hawajatambua kuhusu hili, na sijui tu ni kwa nini lakini wanalichukulia kijuujuu mno. Kila mara likitokea, linakaziwa attention, kidogo tu wanasahau, repeat," Draxton akasema.

"Ni kwa sababu pia lilikuwa limefichwa kwa muda mrefu..."

"Ndiyo. Lakini anayefanya hivi atakuwa anatumia nguvu ya ziada," Draxton akaongea kwa umakini.

"Unamaanisha nini? Kama uchawi?" Namouih akauliza.

"Inawezekana. Lakini nisemeje.... uchawi ulioenda shule," Draxton akamwambia.

Namouih akainamisha uso wake kwa njia ya huzuni.

"Uko sawa?" Draxton akauliza kwa upole.

"Yeah. Ni kwamba tu... nikimfikiria mke wake Felix... Oprah... na watoto wake yaani, nakosa amani every time nikikumbuka kwamba kwa njia kubwa nilisababisha wakampoteza...."

"Usiwe unasema hivyo. Haukumuua wewe. Tu-focus tu kwenye kumpata muuaji wake ili yeye ndiyo aje kuikosa hiyo amani vizuri," Draxton akamwambia.

Namouih akamwangalia na kutikisa kichwa kukubali. "Asante sana Draxton. Unanisaidia sana,"
akamwambia.

"Ingekuwa vizuri kama taarifa za ndani zaidi tungezipata kutoka kwa maaskari, ila...."

"Tutazipata sasa?"

Draxton akatikisa kichwa kwa njia ya kusikitika.

"Ni kama usemavyo, wanachukulia haya mambo kijuujuu tu ndiyo maana sifikirii hata kama tutapata lolote," Namouih akasema.

"Hatuwezi kuwa na uhakika, only time will tell. Acha tu tuwe na subira, huenda isiwe lazima kusubiri mpaka tarehe 19 na tukapata jambo fulani," Draxton akamwambia.

Namouih akatikisa kichwa kukubali.

Wawili hao wakaendelea na maongezi ya hapa na pale kuhusiana na jambo hilo ambalo bado lilikuwa na utata mwingi sana, kwa kuwa haikujulikana kama hata wangeifikia hatamu waliyoihitaji ili maswali mengi yaweze kujibiwa na haki itendeke ipasavyo, lakini matumaini ya kupata ushindi walikuwa nayo, hivyo wangetakiwa kuendelea kusubiri kuona matokeo ya uchunguzi wao kulielekea suala hilo zito....


★★★★


Kwake Efraim Donald. Mume huyu wa mwanasheria mahiri Namouih alifanikiwa kufika kule alikokwenda baada ya kuaga kuondoka kwa ajili ya safari, akiwa ametumia ndege ya kibinafsi. Ilikuwa ni sehemu ambayo angetumia muda wake kukutana na wafanyabiashara wengine wakubwa kwa ajili ya kupanga makubaliano mapya ya kazi zao ili kuongeza ukuzi wa biashara zake. Lakini hii haikuwa sehemu yoyote tu, alikuwa ametoka ndani ya nchi na kwenda nje kabisa,
kule Nairobi, Kenya. Alichukua chumba kwenye hoteli fulani ya kifahari, kisha akawasiliana na mtu
muhimu aliyetaka kuzungumza naye kabla ya kuanza kufanya mikutano hiyo, na alikuwa ni rafiki yake wa karibu zaidi, yaani Mr. Godwin Shigela.

Godwin alifurahi sana baada ya kujua kwamba rafiki yake alikuwa huko pia, naye akamwambia wakutane mahali fulani kulikokuwa na nyumba kubwa za starehe mida ya usiku ili wajumuike na kufurahia maongezi na vinywaji. Efraim Donald alihitaji sana kuzungumza na rafiki yake huyo kwa
sababu kwa kipindi kirefu hawakuonana, na ni yeye hasa kuliko mtu mwingine yeyote ndiyo
angemwelewa vizuri sana kwa mengi aliyotaka kuzungumzia. Hivyo ilipofika mida ya kwenda huko
akachukua gari la muda ambalo alikodi kutumia kwa muda ambao angekuwa huku na kuelekea huko kukutana na rafiki yake.

Alifika na kumkuta Godwin akiwepo tayari, naye akampokea vizuri sana. Mwanaume huyo alikuwa mfupi kiasi kumfikia Efraim Donald begani, mwenye mwili mpana na mikono imara, naye alikuwa mweusi na kichwani alinyoa kipara. Wakati huu alikuwa amevalia nguo za kawaida tu; shati jeupe a mikono mifupi akichomekea ndani ya suruali ya jeans na viatu vyeusi chini. Huu ulikuwa ukumbi wa starehe, kukiwa na watu wengi walioponda raha tu kwa kucheza muziki taratibu, kunywa
vinywaji, na kujiburudisha na wanawake. Godwin akamwongoza Efraim mpaka sehemu maalumu
iliyokuwa na sofa pana jekundu lililozunguka meza nyeusi iliyokuwa na chupa nyingi za vinywaji na glasi kadhaa, naye akaketi psmoja naye hapo.

Kulikuwa na wanawake wanne sehemu hiyo, weusi, warembo, waliovalia vigauni vifupi sana na
kufanya ieleweke wazi kwamba walikuwa ni vyombo vya starehe tu hapo kwa ajili ya pesa, na wawili wakaanza kumshika-shika Efraim kwa njia ya kuamsha hisia za mahaba, lakini mwanaume huyo alionyesha kutopendezwa na jambo hilo hata kidogo. Godwin akamtathmini sana na kutambua kwamba akili ya rafiki yake ilikuwa sehemu nyingine kabisa hata alipojaribu kunwongelesha kwa shauku, hivyo akawaambia warembo hao wawapishe kwanza, nao wakatii na kuondoka.

Godwin akamsogelea Efraim karibu zaidi na kusema, "Vipi kaka? Hao manze hawajakupa entice nzuri tuite wengine?"

Efraim Donald akatabasamu kidogo na kunywa kileo chake.

"Nilikuwa natarajia uje na amsha yako hapa ila umeshaanza kunifanya nihisi usingizi," Godwin akasema.

Efraim Donald akamtazama.

"Mambo yamekaaje?" Godwin akauliza kwa umakini.

Efraim Donald akatikisa kichwa kuonyesha mkazo mwingi, kisha akasema, "Mke wangu Godwin...
mke wangu ameanza kupotea."

"Oh come on bro... umekuja all the way to Nairobi kuanza kuongelea stress za mke wako? Hebu jaribu kuvaa viatu vyangu hapa me nimekuandalia quality time nzuri halafu...."

"Siyo kihivyo, Godwin. Namouih... ameanza kuona vitu ambavyo hatakiwi kuona," Efraim akasema.

Godwin akaweka sura makini zaidi, kisha akasema, "Ina maana bado ndoto zinamsumbua? Ameanza kuona nini?"

"Vitu vingi. Mara vivuli, mara yuko mochwari, mara aone wafu, mara akutane na jitu linalokunywa damu... unaelewa nachomaanisha?"

"Donald acha masihara. Namouih ndiyo alikuwa perfect kabisa. Haiwezekani uwe umebakiza muda
mfupi tu halafu ndiyo aanze kuona haya mambo. Ina maana hata baada ya kumwondoa yule mwanaume bado haikutoa vikwazo vyake?"

"Namouih hakuwa na uhusiano huyo mwanaume Godwin... ndiyo sababu bado aliendelea kusumbuliwa na ndoto mbaya hata nilipomuua," Efraim Donald akasema.

"Kwa hiyo ulimuua kazi bure tu?"

"Nilidhani ni huyo maana nilipomfatilia nilimwona naye hiyo siku... aagh, inakera sana... ikiwa
atatambua kinachoendelea kabla ya mzunguko kukamilika sijui itakuwaje," Efraim akaongea kwa
hasira.

Godwin akamshika begani na kusema, "Calm down. Unatakiwa tu kumfatilia ili ieleweke ana-cheat na nani, halafu ummalize huyo mtu."

"Namouih hani-cheat Godwin. Yaani kila sehemu yuko msafi..."

"Hilo linawezekanaje? Angeweza vipi kuota ndoto mbaya kama hajaanza kuku-cheat?"

"Hii haihusishi ku-cheat kwa kufanya mapenzi. Godwin... kuna mtu inaonekana Namouih amempenda... lakini hata yeye mwenyewe hajajua hilo. Inakuwa ngumu kujua ni nani kwa sababu hiyo ndiyo maana nashindwa kumwondoa..."

"Hupaswi kusema neno kushindwa mbele ya meza yetu. Amka mwanaume! Ongea na roho yako
ikuonyeshe huyo mtu ili umwondoe mapema maana ukijiremba utasababisha kila kitu kiporomoke,
na huo utakuwa ni uzembe wako. Nilikwambia mapema kabisa... sasa now utafanya nini? Ikifikia hatua Namouih akauona uso wako kwenye hizo ndoto je?"

Efraim Donald akamwangalia kwa hisia kali na kusema, "Sitaruhusu hilo litokee. Nimemuua Felix lakini haijasaidia lolote, ndiyo maana natakiwa kuwa mwangalifu sana ili nisikosee next time. Namouih ameshaongea mpaka kuhusu kutaka kutoka nje ya ndoa na talaka kwa sababu simpi haki yake, na hiyo ni moja kati ya mambo yanayochangia hili tatizo. Kama amempenda mtu fulani bila yeye mwenyewe kujua hiyo inamaanisha nitapaswa kutulia kusikilizia hali, maana mzunguko hauko mbali kuisha... nimebakiza msichana mmoja tu wa kuua... yaani mpaka nahisi hasira kaka... why now? Wakati niko karibu sana? Agh..."

"Kaka, fanya ukweli. Hakikisha hilo tatizo linaondoka upesi. Najua ni jinsi gani unataka sana kumla yule mwanamke heheheh..." Godwin akasema huku akicheka.

"Yaani! Huwezi amini kaka... Namouih ni mwanamke mmoja nayeweza kusema ni mtamu sana
ingawa bado sijamuonja, ndiyo maana nataka kuhakikisha haya yanaisha kabla sijampoteza..."

"Usiwaze kumpoteza. Kila kitu kitakwenda sawa, cha muhimu ni kuendelea kutokosea mahesabu. Na usipuuzie ushauri wangu... mwombe Subiani msaada... atakusaidia kujua nani ameuteka moyo wa mke wako ili...."

"Godwin, sitakiwi kufanya hivyo. Task ya kuondoa tatizo ni yangu, nikijipeleka mbele yake nitaombwa malipo zaidi, kitu ambacho ni ngumu wakati unajua nina mzigo mkubwa kukamilisha kabla ya.... yaani... I don't know," Efraim akaongea kwa mkazo na kupiga fundo mbili za haraka.

"Kaza moyo mwanaume. Hata mimi nilipita pagumu sana, lakini si unaniona sasa hivi nilipo? Hapo ulipo kwa sasa yaani bado sana... utajiri juu yako ni mwingi mno ukikamilisha hili zoezi. Njia uliyochagua ni ngumu mno, lakini hakuna kurudi nyuma sasa. Komaa. Hakikisha hilo tatizo
linaondoka. Mwangalie mke wako kwa makini, macho yake tu yatakuonyesha ni nani anayemwangalia zaidi ili umnase," Godwin akasema.

"Sawa. Nitalifanyia kazi ipasavyo. Ila... kuna jambo fulani yaani linanipa raha sana kila nikifikiria... ni raha fulani hivi nataka niipitie kwanza kabla ya kuendelea na haya yote... inaonekana kuwa tamu mno... Subiani ataipenda sana," akasema Efraim na kuanza kutabasamu.

"Hautaniambia ni raha gani hiyo?" Godwin akauliza.

"Nitakuja kukuonyesha tu. Bonge moja la show nataka kufanya... hahahahah..." Efraim Donald akaongea huku akinywa.

Wanaume hawa wakacheka kwa pamoja na kuongeza vinywaji ili waendelee na maongezi yao.

Mambo hayo! Hapa ndiyo msemo wa usilolijua ni sawa na usiku wa giza utafaa kutumika kwa asilimia zote. Katika mzunguko mkubwa wa mambo mengi mabaya, sikuzote msababishi hutokea pale pale ambapo wengine hupaona kuwa pazuri sana, na katika kisa hiki chote, ni mwanaume huyu ndiye aliyekuwa msababishi wa hayo yote. Efraim Donald hakuwa namna alivyoonekana kwa nje tokea mwanzo alipoingia kwenye maisha ya mwanadada Namouih. Huyu alikuwa ni mtu mbaya sana mwenye kila aina ya sifa kuitwa mkatili wa hali ya juu, na alificha mambo mengi ya kikatili kwa msaada wa roho mwovu na mkubwa sana, mwenye nguvu nyingi, ambaye kwa wengi
hufahamika kama JINI SUBIANI. Ilikuwaje mpaka maisha ya mwanaume huyo mwenye nyuso mbili yakawa namna hiyo? Na lengo lake kumwelekea Namouih lilikuwa nini?


★★★★★★★★★★★★

ITAENDELEA

★★★★★★★★★★★★


Huo ndiyo mwisho wa msimu wa kwanza wa hadithi hii ya CHANGE. Sehemu za mwendelezo wa hadithi hii kali zitaanzisha msimu wa pili. Ni story nzuri na ndefu sana. Waweza ipata nakala yote kwa gharama nafuu sana. Karibu WhatsApp au kwa E-mail yangu.

WhatsApp no: +255 678 017 280

e-mail: eltontonny72@gmail.com
IMG_20230108_235349_632.JPG
 
CHANGE

Story by Elton Tonny

Urafiki, Familia, Mapenzi, Mahaba, Tamaa, Hila, Usaliti, Unyanyasaji, Ukatili, Mauaji, Mambo yasiyotazamiwa, Mambo yenye kuhofisha

R-rated 18+

Enjoy!

★★★★★★★★★★★★★★★★★

SEHEMU YA ISHIRINI NA TATU

★★★★★★★★★★★★★★★★★


EFRAIM DONALD


Tupate mwanga zaidi kuhusiana na maisha halisi ya mwanaume huyu. Efraim Donald alikuwa ndiyo mzaliwa wa kwanza katika familia yenye watoto watatu. Mama yake, Halima, alikuwa ameachwa na mwanaume ambaye hakumwoa kisheria abaki kulea watoto hao peke yake tangu Efraim alipokuwa na miaka 9 tu, na hiyo ikamwacha Halima apitie mambo mengi magumu kwa sababu ya kutoweza kupata kipato cha kutosha kuwahudumia watoto wake kwa mahitaji yao mengi muhimu. Angalau alijikongoja kwa kufanya biashara za kuuza shanga, rozali, na urembo wa shingoni uliomhitaji afanye kazi kwa muda mrefu kuvitengeneza vitu kama hivyo kwa kuwa alitumia mbegu za matunda na mimea, lakini bado kipato kilikuwa kidogo sana.

Maisha yao yalikuwa magumu. Wakati mwingine ilibidi Efraim Donald aache kwenda shule ili amsaidie mama yake kwa kazi kama kuuza barafu, mkaa mdogo mdogo aliookota-okota na hata kufanyia watu kazi zao ili wamlipe chochote walichoweza. Alikua kwa kusontewa sana vidole kama mtu ambaye amelaaniwa, yeye pamoja na familia yake, kwa sababu hata ndugu zao wengi hawakujihusisha nao. Wadogo zake wote walikufa Efraim alipokuwa na miaka 19 baada ya kupatwa na ajali ya kuangukiwa na jengo walipokuwa wamesimama usawa wake. Kufikia kipindi hicho, Efraim Donald alikuwa mitaani tu akifanya shughuli zozote zile ili kumsaidia mama yake, na alikuwa amejitahidi sana kuwa na moyo wenye ukarimu kwa wengi hata kuwadaidia kwa vitu vingi lakini yeye kwa upande wake hakuwa akifanikiwa.

Baada ya vifo vya wadogo zake, Efraim Donald aliamua tu kuhama mji waliokuwepo na ili kwenda kutafuta maisha jijini, akimwacha mama yake huko, na ndiko alikoanza kufanya biashara za hapa na pale. Aliuza karanga, alipiga debe, alifanya udalali mdogo mdogo wa kila aina, hadi kuna mara ambazo alijiingiza katika mambo mengi haramu; yote hiyo ili kupata maisha aliyotaka sana ili kujiondoa pale pabaya alipokuwa. Angeona namna ambavyo watu au watoto wa watu wenye pesa waliishi na kujiahidi kwamba ipo siku angekuwa na maisha ya namna hiyo. Ingawa alikuwa kwenye mstari mbaya kimaisha, hakufanya mambo ambayo yangemwathiri vibaya kiakili au kimwili, kama kuvuta bangi au kutumia madawa ya kulevya, kwa sababu pamoja na vidogo alivyofanikiwa kupata alikuwa na akili nzuri sana ya kuendesha maisha yake kwa mpangilio ili asije kukata tamaa.

Lakini ilifikia kipindi akahisi kuchoka, kwa sababu umri ulienda, na mambo mengi hayakwenda vizuri sana. Alikuwa akifanya kazi kama kinyozi kwenye saluni ndogo alipokuwa na miaka 35, na ndiyo iliyokuwa inamsaidia sana hata kutengeneza mitaji ya kufanya biashara za pembeni, huku akimhudumia na mama yake aliyekuwa kule kule mkoani kwao. Alikuwa amepita kwa wanawake kadhaa ambao mwisho wa siku wangeachana naye kutokana na yeye kuonekana hana uwezo wa kuwamudu, na ni moja kati ya mambo mengi yaliyomkosesha amani ya moyoni kwa sababu ya kujiona ni kama hafai.

Basi, siku fulani alikuwa amekwenda kuonana na mwanaume mmoja kijana aliyefanya kazi kwenye kituo cha kujaza mafuta, au sheli, ambaye alikuwa na pesa yake ya kukopeshwa ili amrudishie. Yaani, Efraim Donald alimdai mwanaume huyo pesa, na ilikuwa imepita miezi miwili akiwa anamzungusha tu kwa kusema angemlipa wakati aliomba akopwe kwa wiki moja tu, na sasa Efraim alikuwa na uhitaji wa hali ya juu uliomnyima budi ya kwenda kumfata ili akaichukue; kwa kuwa ilionekana wazi kwamba alikuwa anakwepwa.

Alifika sehemu hiyo ya shell na kumkuta huyo mwanaume, naye akamwambia kilichompeleka hapo ni uhitaji wake wa kupata hela siku hiyo hiyo, na hakuwa na njia nyingine ya haraka kwa sababu alichotaka kufanyia kazi kilikuwa cha lazima. Lakini mwanaume huyo akaanza kumwambia kwamba hakuwa na hela, kwamba hata yeye ana wakati mgumu sana kwa hiyo hangeweza kumsaidia, ila Efraim akamweleza kuwa kilichompeleka hapo haikuwa kuomba msaada bali kuchukua kilicho halali kwake. Jambo hili likazua ugomvi mkubwa kwa sababu mwanaume yule alionyesha dharau sana, na ilimtia Efraim Donald ghadhabu nyingi kiasi kwamba akaanza kupigana naye kwa hasira. Walipigana mpaka kuumizana haswa, na ndipo maaskari wa ulinzi wakawa wamefika hapo ili kuwaachanisha.

Wakati hayo yalipokuwa yanaendelea, kuna gari la kifahari lilikuwa limefika sehemu hiyo ili kujazwa mafuta, na aliyekuwa mwendeshaji ni yule yule Godwin Shigela. Aliweza kuona ugomvi huo, hasa kwa sababu watu wengi walijaa sehemu hiyo, naye alikuwa ameanza kuliondoa gari lake hapo ili akatafute sehemu nyingine ya kuweka mafuta lakini baada ya kumwona askari mmoja akimwongoza Efraim kuelekea upande mwingine wa eneo hilo, akaghairi kuondoa gari lake hapo. Ni kwamba alikuwa amemtambua, na ilikuwa imepita muda mrefu sana bila ya wawili hawa kuonana. Walisoma wote sekondari mpaka kufikia kidato cha nne ndipo wakaachana, na walikuwa ni marafiki wale wa kawaida tu siyo kwamba walipatana kwa ukaribu sana, lakini baada ya kumwona Efraim ndani ya shida hiyo, Godwin akataka kumsaidia.

Efraim Donald pamoja na yule mwanaume waliyepigana walipelekwa kwenye ofisi ya kituo cha mapolisi na kukalishwa ili ijulikane nini kilikuwa chanzo cha wao kupigana namna ile na adhabu gani ichukuliwe dhidi yao, na Efraim alieleza mengi sana kwa hisia kali kwa sababu ni yeye ndiye aliyeona kwamba hakutendewa haki. Lakini maaskari wa hapo wakawa wanasema eti yeye ndiyo mbaya kwa kuwa alimfata mtu kazini na kuanzisha vurugu, kwamba kama ni hayo mambo ya kibinafsi angemsubiri huyo mwenzake aondoke kazini ili ndiyo akamdai kuliko kuanza kupigana naye pale.

Maaskari walikuwa wanataka wawili hao watoe faini kubwa sana kwa sababu ya vurugu zile la sivyo wangewaweka ndani, na bila kukawia, mwanaume yule aliyekuwa anadaiwa na Efraim Donald akatoa faini kwa upande wake. Maaskari walitaka kila mmoja wao atoe laki moja, lakini mwanaume huyo akasema yeye alikuwa na elfu sabini tu na akawaomba waikubali, hivyo wakamkubalia na kumwachia. Efraim Donald alimwangalia sana mwanaume huyo, kwa sababu yeye alikuwa anamdai elfu hamsini, lakini akaona asimlipe makusudi kabisa ila kwenye kutoa faini ili kujiokoa akatoa kiasi cha juu. Aliingiwa na hasira zaidi, lakini hapo hakuwa na njia ya kujitoa kwa sababu hakuwa na pesa hata kidogo, kwa hiyo angefungiwa ndani ya gereza dogo na kuambiwa angekaa humo kwa siku mbili zaidi.

Lakini Efraim hakuwa bado amepelekwa ndani na maaskari hao ili kufungiwa pale Godwin Shigela alipofika na kuwaambia maaskari kwamba amekuja kumtolea dhamana rafiki yake. Efraim Donald alipomwangalia Godwin kwa mara ya kwanza, alihisi ni kama anamjua ingawa hakumkumbuka vizuri sana, na mwanaume huyo akawapa maaskari laki tano baada ya wao kumwambia ni laki moja tu ndiyo iliyohitajika. Ingawa ilionekana kama ametoa pesa kwa njia fulani ya dharau, wakazipokea, kisha wakamwachia Efraim Donald na kumwonya asirudie tena kufanya jambo kama alilofanya leo.

Baada ya hapo, Godwin Shigela akaongozana na Efraim mpaka kwenye gari lake, huku mwanaume huyu akiwa bado na maumivu mwilini na majeraha usoni ya kuvimba, naye Godwin akamwambia aingie ndani ya gari lake ili waongee vizuri.

"Dah, kaka pole sana aisee. Nimekuona hapo sheli nimekukumbuka sana... Efraim bwana. Za siku?" Godwin akasema.

"Siwezi kusema ni nzuri maana na hali uliyonikuta nayo ndiyo kama hivyo. Mambo hayajawa mepesi kwangu kaka," Efraim akamwambia.

"Pole sana," Godwin akasema.

"Ila unajua... nahisi kama nakufahamu sijui... tulisoma wote au?" Efraim akauliza.

"Ndiyo, ni muda mrefu. Mimi ni Godwin. Tumemaliza form four pamoja."

"Ooh sawa... Godwin Shigela... walikuwaga wanakuita mmasai mfupi..."

"Ahahahah... ndiyo mimi."

"Aisee... ni muda mrefu. Sikumbuki watu wengi niliosoma nao yaani..."

"Hiyo ni kawaida. Lakini vipi wewe? Maisha... yaani, tulipomaliza tu mitihani ukapotea, sikukuona hata Grad. Uliendaga wapi?"

"Aah... mambo mengi mazito ndugu yangu, basi tu. Kipindi hicho mambo hayakuwa rahisi kwetu kama tu yalivyo magumu sasa hivi, nilimaliza form four kwa msoto pia, na bado nilifeli... nilifiwa na wadogo zangu wawili ndani ya siku moja tu... kwa hiyo, kidogo nikahama kuja kutafuta maisha jijini hapa... ni mambo mengi... mambo mengi sana siyo rahisi kuelezea yote kaka," Efraim akasema kwa hisia.

"Pole sana. Ngoja twende hapo hospital angalau wakufanyie..."

"Hapana, hapana, niko sawa Godwin. Nashukuru sana kwa msaada wako. Sijui hata nitaweza vipi kukulipa kaka maana... uwezo wenyewe hata sina," Efraim akasema.

"Nilikuwaga nakuona hata shuleni kaka, hukuwa... ukijichangsnya na watu, we' ulikuwa wa kuja, kuandika, na kuondoka. Najua mlikuwaga na maisha magumu sana, na roho imeniuma kuona kwamba bado mambo siyo rahisi kwako... nataka nikusaidie rafiki yangu," Godwin akasema.

Efraim Donald akatabasamu na kusema, "Nitashukuru sana kaka. Nahitaji kupata angalau kazi itakayoni-boost haraka maana mama umri unaenda, na bado me mwenyewe nina mambo mengi ya kurekebisha... wakati mwingine najitahidi kuwa mwema lakini malipo ni ubaya tu... inachosha sana. Sa'hivi ningekuwa hata na watoto watatu kaka lakini mama zao wakatoa mimba... na nani wa kuwalaumu? Hata kama wangezaa, ningesaidia vipi kuwatunza? Mpaka nahisi aibu yaani..."

"Usihisi hivyo, lakini ninaelewa unachopitia. Hata mimi sikupita sehemu rahisi, ila sikukata tamaa. Nawe pia usikate tamaa, utatoka tu," Godwin akamwambia.

"Asante sana Godwin..."

"Huyo mwanaume uliyegombana naye, ni mtu wa karibu?"

"Ni mpumbavu sana huyo. Nilimkopesha pesa maana alikuwa na shida akaahidi kurudisha ndani ya wiki... sa'hivi imepita miezi kaka... namwomba ananipiga chenga, mama yangu anakosa hata hela kidogo ya kula kwa sababu mimi nimejifanya mwema kwa mtu halafu nikalipwa fadhila kwa kutemewa mate usoni. Afu' alivyo na dharau anasema 'kwani hamsini pesa gani' wakati anaiomba alikuwa anatoa hadi na machozi, sa'hivi kapata yeye hataki kurudisha wema... yaani najiona fala sana Godwin... samahani kwa maneno yangu lakini...'

"Hapana usijali, naelewa. Ngoja nikwambie kitu. Usije ukafikiri kwamba maisha kwa watu ambao tayari wana pesa ni rahisi, wengi wao huwa wanazipata kwa njia ya mkato. Wengine wezi, wengine mashoga, wengine wafisadi, wengine wanafanya umalaya tu, na wanaonekana kufurahia maisha yao kwa kuwa wanaishi wakijua kwamba hicho walichonacho kinaweza kupotea muda wowote, ndiyo maana hawaachi kuyaishi kwa njia hiyo. Usije hata siku moja kudhani kwamba wema unaoonyesha utalipwa kwa wema, kwamba labda ndiyo utatajirika sasa... hapana. Ukikaa kusaidia watu wakati wewe mwenyewe una shida, hautafika popote kaka, kwa hiyo inabidi uanze kuishi kwa njia ya kichoyo, lakini... lakini Efraim, ile ambayo itakufanya hata ukitoa pesa nje, kwako wewe ndiyo zinazidi kuongezeka mfukoni."

Godwin alisema maneno hayo kwa uzito sana, naye Efraim akawa ameangalia chini kwa umakini akiwa anajaribu kuyaelewa kiundani zaidi.

"Unamaanisha nini... kichoyo?" Efraim Donald akauliza.

"Unataka nikusaidie ili uache kuishi namna hii... na uanze kuishi maisha mazuri kwa muda wote uliobakiza hapa duniani Efraim?" Godwin akauliza.

Efraim Donald akamwangalia tu usoni kwa umakini, kisha akatikisa kichwa kukubali.

Godwin akatabasamu kwa mbali na kumshika begani, kisha akasema, "Furahia kukutana nami Efraim, kwa sababu ukihakikisha unafuata kwa umakini kile nitakachokwambia, utaishi maisha mazuri sana... na utapata chochote kile unachotaka kwa ajili yako mwenyewe."

Efraim Donald akatega sikio lake kwa umakini, na mwanaume huyo akaanza kumwelezea mambo mengi ambayo kiukweli yalimchanganya sana mwanzoni, na baada ya kueleweshwa vizuri hata zaidi, mwanaume huyu akawa kama mtu aliyeachwa katikati ya barabara iliyomtaka achukue uamuzi wa kutumia upande fulani ili aweze kufika alikotaka kwenda, kwa kuwa mambo mengi yalikuwa ni mazito sana. Godwin alimhakikishia kwamba hakukuwa na haja ya kuhofu lolote lile, kwa sababu hata yeye alifanikiwa kupitia njia kama alizomwambia, hivyo akampa muda wa kufikiria aliyomwambia kisha angemjulisha. Akamwachia mwanaume huyu kiasi cha shilingi laki tano, kama tu alivyowapa maaskari wale, jambo lililomwambia Efraim Donald kuwa Godwin alikuwa akipata pesa nyingi sana, naye akawa ameingiwa na tamaa ya kutaka kujichumia pesa kama hivyo ili aachane na maisha aliyoyaona kuwa batili mno.

Wawili hawa wakaachiana namba za mawasiliano, hususani namba za Godwin kwa Efraim ili akiwa tayari kuafikiana na ushauri wake basi amtafute ili amwelekeze mambo mengi vizuri hata zaidi. Mwanaume huyo akampeleka Efraim mpaka kule alikoishi, kisha akamuaga huku akisema angesubiri kwa hamu kusikia jibu lake kwa uchanya, naye akaondoka na kumwacha Efraim Donald anatafakari kila kitu alichotoka kuambiwa.


★★★


Ilipita kama wiki baada ya Efraim Donald kuachiwa laki tano na Godwin Shigela, na sasa mwanaume huyu alikuwa ameamua kwenda nyumbani, yaani mkoani kwa mama yake ili akamsalimie kwa sababu hawakuwa wameonana kwa muda mrefu. Halima alimpokea mwanaye kwa furaha, na kufikia kipindi hiki mwanamama huyo alikuwa akiishi kwenye nyumba ya kupanga pamoja na vijana wengine watatu wa kiukoo, ambao walimsaidia katika shughuli zake za hapa na pale. Hata baada ya Efraim kufika na kutazama jinsi ambavyo mama yake aliishi, aliingiwa na simanzi kwa kuwa alihisi ni kama alishindwa kubadili maisha ya mzazi wake kuwa bora hata baada ya miaka mingi kupita.

Akiwa huku, yeye Efraim Donald alikaa kwenye chumba cha kulipia kwenye nyumba ya wageni kwa kutoa elfu sabini ili akae hapo kwa wiki, na ndiyo angekuwa anakwenda kwa mama yake ili kumtembelea kisha baada ya hapo angerudi jijini kwao. Dhumuni la yeye kuja huku ilikuwa ni ili azungumze kwa kina na mama yake kuhusu badiliko alilotaka kufanya maishani, na aliamini mama yake angemwongoza vizuri ili aweze kufanya maamuzi sahihi. Baada ya kukaa hapo kwa siku mbili, siku ya tatu alimwita mama yake ili aende pale alipochukua chumba waweze kufanya maongezi kwa kina. Halima alikwenda huko mida ya jioni baada ya kumaliza shughuli zake ndogo ndogo, naye Efraim akampokea vizuri na kuagiza chakula kizuri kwa ajili yake.

"Kwa hiyo tokea alipotoa mimba yako, mpaka leo hamjaonana tena?" Halima akawa anamuuliza huku akiendelea kula taratibu.

"Hapana, hatujaonana. Rafiki yake tu aliniambia hayo, hata nilipomtafuta sikumpata. Ila mara ya mwisho tumeonana aliweka wazi kabisa kwamba hawezi kuendelea kuwa na mwanaume suruali kama mimi... na inawezekana tayari alikuwa ameshampata huyo mwanaume wake mwingine ndiyo maana akaitoa mimba..." Efraim akamwambia.

"Mpumbavu sana. Yaani mwanangu, wanawake wa siku hizi ni wapumbavu sana, wanachoangalia ni pesa tu na si kingine. Ningekuwa na mjukuu wa tatu sasa hivi mimi aagh..." Halima akaongea kwa kuudhika.

Efraim Donald akatabasamu kwa mbali.

"Vipi kazi lakini?" Halima akauliza.

"Hivyo hivyo tu," Efraim akajibu.

"Uliponiambia kuhusu yule mshenzi aliyekudhulumu hela yaani nilitamani nije huko nimnyonge kwa mikono yangu mwenyewe! Watu wanafikiri hela zinaokotwa sijui? Na wewe Efraim uwe unaanglia, watu wengine siyo wa kuwaamini, hiyo hela ungetuma huku tukatumia badala ya kumpa huyo mjinga," Halima akasema.

"Ahahahah... unapenda hela mama..."

"Siyo kupenda hela, kulikuwa na shida. Angalau we' ndiyo unaweza kunisaidia..."

"Najua. Samahani. Mambo ni mengi afu'... magumu."

"Yaani! Sijui mpaka lini jamani, ah-ah," Halima akaongea na kuendelea kula.

Efraim Donald akamwangalia kwa umakini sana, kisha akasema, "Nafikiri nimepata njia ya kubadili maisha yetu mama."

Halima akamtazama kwa umakini pia, kisha akasema, "Nakusikiliza."

"Kuna... rafiki yangu... anaweza kunionyesha njia fulani ya kupata mali... haraka," Efraim akasema.

"Ahah... Efraim... hebu achana na hayo mambo. Nimeshakuelewa vizuri, na ndiyo maana nakwambia achana nayo. Mengi tunayasikia sijui mzee nani anafanya nini, lakini hakuna lolote huko. Unafikiri kama wangekuwa na huo uwezo kungekuwa na umasikini hapa nchini? Na wenyewe wanatafuta hela kwa hao hao wanaowaahidi hela nyingi, ni akili hiyo?"

"Hapana mama, siyo hivyo. Hii ni tofauti."

"Kivipi?"

"Ikiwa nitakubali kufanya jambo hilo... kuna malipo fulani natakiwa kutoa... lakini siyo pesa," Efraim akasema.

"Malipo yasiyo ya pesa? Efraim... unaongelea masuala ya kafara?" Halima akauliza huku akikiweka chakula pembeni.

Efraim Donald akabaki kumtazama tu usoni.

"Jamani! Mwanangu imeshafika mpaka hatua hiyo?"

"Mama, hapa kuna nafasi ya mimi kufanikiwa kweli... nachotaka kukwambia siyo masihara..."

"Najua siyo masihara kwa sababu nakujua vizuri. Akili yako ikishataka kitu yaani ndiyo utakazia hicho hicho tu, hautasikiliza la mwadhini wala mnadi suala. Efraim hayo mambo siyo, na unaweza ukajiweka kwenye matatizo makubwa sana ukiamua kufuata hiyo njia..."

"Hapana mama, niamini. Huyu rafiki yangu nayekwambia... amefanikiwa sana. Na... sidhani kama mambo ni mazito kihivyo maana...."

"Ukiambiwa unitoe mimi kafara je?" Halima akamkatisha.

"Mama..." Efraim akamwita kwa upole.

"Yaani Efraim kwa kweli sielewi. Mimi nitakupa support kwa mambo mengi sana kwa sababu... najua tulikotoka... ila sasa hivi nikiona unakoelekea siyo kuzuri lazima nikwambie kwamba sitaweza kukuunga mkono kabisa... yaani kwa jambo hilo siwezi," Halima akasema.

Efraim Donald akaishika mikono ya mama yake na kumwambia, "Mama, sikuombi uniunge mkono, ninakwambia tu kwamba ninataka kujaribu hii bahati ili nione itanifikisha wapi. Sitakubali kukuweka sehemu mbaya nikigundua kwamba kuna vitu haviwezekani kufanywa, na ninakuamini sana ndiyo maana nimeona nikwambie. Sipendi kabisa kukuona unaendelea kuteseka toka zamani wakati mimi nipo na ninaweza kufanya jambo la kukuinua mama yangu. Nakuahidi kila kitu kitakuwa sawa. Naomba tu uniamini."

"Efraim... Efraim... Efraim mwana wangu! Haya. We' fanya unayotaka kufanya, ila usisahau maneno yangu. Mimi nitaendelea tu kukaa namna hii hii maana sijabakiza muda mrefu wa...."

"Usiseme hivyo mama. Utaishi maisha marefu na mazuri. Nakuahidi. Nitafanikiwa," Efraim akasema kwa ushawishi.

Halima hakuwa na namna ila kumwacha mwana wake afuate kile ambacho akili yake ilikuwa imemtuma, na ingawa aliogopa kwa ajili yake, yeye pia alitaka kuona namna ambavyo mambo yangekwenda ikiwa mtoto wake angechukua hatua hiyo. Kwa maneno mengine ni kama akili zao zilifanana hasa kwa sababu walielewana kwa mengi sana kutokana na magumu waliyopitia maishani.

Baada ya hayo, Efraim Donald akamweleza sasa kwamba bado hakuwa ameongea na Godwin tena baada ya msaada aliompatia wiki iliyopita, na ndiyo alikuwa anafikiria kumtafuta ili waongee tena. Akamhakikishia mama yake kuwa ikiwa njia ambazo angeonyeshwa zingezidi matarajio yake basi angeahirisha kufuata suala hilo na kumwomba tu Godwin amsaidie kupata kazi nzuri, na kwa hilo mama yake akawa ameridhia.


★★★


Efraim Donald alirejea jijini alikoishi baada ya safari yake kwenda kumwona Halima, na sasa alikuwa ameiweka akili yake sawa zaidi baada ya kuongea na mama yake na kuamua kumtafuta Godwin Shigela. Mwanaume huyo alifurahi sana na kumwambia Efraim wakutane siku na saa fulani, naye Efraim Donald akaridhia na kuanza kujipanga kwenda kukutana naye. Alielewa kwamba bila shaka angekutana na mambo mengi ambayo yangemfanya awe kama mgeni, lakini akajiahidi kusimama kiume ili akutane nayo na kushughulika nayo kwa njia ambayo ingempa faida kweli.

Wawili hawa walikuja kukutana kwenye siku ambayo Godwin aliamua kumtembeza Efraim kwenye sehemu kadhaa kati ya nyingi ambazo alimiliki kutokana na utajiri mwingi aliojichumia, kisha akakaa naye na kuanza kumweleza namna ambavyo alifanikiwa kupata hayo yote kwa kipindi kifupi sana. Alimwambia kwamba kupata vitu hivyo haraka haikumaanisha vilikuja kimuujiza tu, lakini yeye Efraim kama mtu mzima angepaswa kutambua kwamba kila kitu kilitakiwa kuonekana kuwa halali kwa nje hata kama njia za ndani zilikuwa za mkato, na akasema njia aliyokuwa ametumia haikuwa ya mchezo hata kidogo. Akamwambia kwamba kuna nguvu kuu zilikuwa zinahusika, na wengi waliotaka kujiingiza katika jambo kama hilo waliambulia patupu kwa sababu hawakuwa na mioyo mikuu ya kuchukua hatua nzito ambazo zilihitajika ili kuwafanya wafanikiwe kweli; na baadhi yao hata walikufa.

Efraim Donald alikuwa ametarajia kuambiwa vitu kama hivyo, lakini bado alihitaji kujua kwa undani ni mambo kama yapi yaliyohusika. Godwin akasema ndiyo hicho sasa. Hangejua ni mambo gani ambayo yangehusika mpaka aingie huko ili kufanya makubaliano na "watu" waliotoa msaada huo, kwa hiyo alitakiwa kujua kwamba akienda huko, chochote kinaweza kutokea. Hakukuwa na mambo yanayofanana kwa watu waliojihusisha na jambo hilo, kwa hiyo hata yeye angekutana na jambo tofauti. Godwin akamwambia asiwe na hofu kubwa labda ingemlazimu kufanya jambo baya mno, lakini akamwambia hapo kikubwa ni kuwa tayari kwa ajili ya lolote. Ikiwa kwa sasa angehisi kwamba hangeweza, basi angetakiwa kuacha. Lakini kama alikuwa anaenda, angetakiwa kuhakikisha anaiweka akili yake tayari kutimiza chochote kile ambacho angeombwa kufanya.

Efraim Donald alionyesha kuwa na uhakika baada ya kumwambia Godwin kwamba yuko tayari, hivyo aonyeshwe mambo hayo yalikuwa ni nini. Godwin akampongeza kwa hilo, kisha akamwambia kwamba angemkutanisha na "mawakala" wa mtu fulani muhimu sana ambaye ndiyo alikuwa chanzo kikuu cha kuwawezesha wapate utajiri, na ni mawakala hao ndiyo ambao walimwakilisha, na ikiwa angejitoa kwao kwa asilimia zote basi angepata faida kubwa sana. Akamwonya pia, akisema alitakiwa kuwa mwangalifu mno ili chochote kile ambacho YEYE Efraim Donald angechaguliwa kufanyia kazi, ahakikishe anakitimiza kwa nguvu zake zote kwa sababu ikiwa asingefanikiwa basi kungekuwa na madhara.

Baada ya kuwa amemwelewesha waziwazi lakini kwa njia yenye mafumbo mengi, Godwin akampeleka Efraim sehemu yenye kumbi ya starehe ili wajifurahishe pamoja, naye akamfanyia mpango ili apate vitumbuizo kutoka kwa wanawake kadhaa na ajichagulie yeyote aliyetaka ili kufanya naye mapenzi. Ilikuwa moja kati ya njia nyingi ambazo Godwin alitumia kumwonyesha kwamba angefurahia vitu vingi vizuri kama angefanikiwa kufata maagizo yake, na mambo hayo yalikuwa yameanza kumwingia vyema Efraim Donald ndani ya moyo wake baada ya kuonyeshwa raha ambazo angezipata kwa sehemu tu, hivyo akawa anataka kuzipata hata zaidi.


★★★


Baada ya siku chache, Godwin Shigela akamtafuta Efraim Donald na kumwambia kwamba sasa ulikuwa umewadia wakati wa kwenda kukutana na "mawakala" wale ili mpango uanze kazi. Efraim alielewa kwamba vitu hivi huenda hata vingehusisha masuala ya kuzimu huko, lakini tayari alikuwa ameshaazimia moyoni mwake kuwa angefanya yote yaliyo ndani ya uwezo wake kuhakikisha anafanikiwa. Ni maisha magumu yenye kumchosha sana aliyokuwa amepitia, kwa hiyo kama hii ndiyo ilikuwa nafasi aliyoshushiwa ili ayaonje na kuyaishi yale maisha mazuri zaidi, yeye alikuwa nani kuikataa?

Alijiandaa vyema na kukutana na rafiki yake, kisha Godwin Shigela akampeleka mpaka sehemu ya mbali ya jiji hilo iliyokuwa na hospitali ndogo iliyojengwa zamani sana. Walikuwa wamekwenda usiku, usiku wa saa nane, kwa hiyo walifika huko yapata saa tisa usiku. Eneo hilo halikuwa na makazi mengi sana karibu ingawa kuna watu waliishi kwenye mitaa yake, naye Godwin akamwambia kwamba hapo ndiyo mahali ambapo kulikuwa na "mlango" muhimu wa kuwakutanisha na hao mawakala. Efraim Donald hangehitaji kuuliza maswali kama hao mawakala ni nani, na walimfanyia kazi nani; tayari alielewa kabisa kwamba huu mchezo wote ulikuwa na jina moja tu la aliyekuwa kama mhusika mkuu: Lucifer.

Godwin akamwambia Efraim kwamba "mlango" huo wa kuwapeleka kwa mawakala wale ulikuwa ndani ya chumba kimoja cha mochwari, ambako hakuna mtu yeyote aliyetakiwa kuingia kwa wakati huu isipokuwa yeye, kwa sababu tayari alikuwa na makubaliano na mtunzaji wa hifadhi za maiti; kumaanisha alikuwa na funguo kwa ajili ya kuingia ndani huko. Hata mtunzaji huyo hakujua kuhusiana na habari hizi lakini Godwin alikuwa ameshamnunua, yaani alikuwa anamlipa pesa ili asiseme kwamba kuna mtu ambaye huenda pale mara kwa mara kwa ajili ya kufanya biashara zisizoeleweka.

Wawili hawa wakaelekea mpaka upande wa vyumba vya mochwari, naye Godwin akampigia simu mhifadhi huyo na kumwambia yuko nje na aje kumruhusu apite kwa kufungua geti. Kulikuwa na kamera za ulinzi za CCTV pia kwa ndani na nje kwa hiyo mhifadhi yule alitakiwa kuhakikisha zinazimwa kwa wakati huu mpaka Godwin amalize biashara zake. Baada ya mhifadhi huyo kuwafungulia, marafiki hawa wakaelekea mpaka kwenye chumba kile ambacho Godwin alidhamiria kumpeleka Efraim, kisha akatangulia kwenda ndani huku Efraim akifata nyuma taratibu. Mwanaume huyu hakuwa na woga wa kuona maiti wala nini baada ya kuingia, ila bado alijiuliza maswali mengi sana kuhusu "mlango" huo, na hivyo angetakiwa kusubiri kuona matokeo ya mambo haya yote.

Mlango wa kuingilia ndani ya chumba hicho ulifungwa kwa nje na yule mhifadhi, wawili hawa wakiachwa ndani humo ambapo palikuwa na meza kadhaa zilizofunika miili michache pamoja na masanduku makubwa yenye majokofu ya kuhifadhi miili ya maiti, na kiukweli harufu ya ndani hapo haikuwa nzuri hata kidogo. Kulikuwa na giza kiasi katika chumba hiki lakini mambo yalionekana vyema kama kwa mwanga wa mbali wa tochi. Godwin akafika usawa wa ukuta na kusimama, akimwambia Efraim asimame pembeni yake, naye akatii. Akamuuliza ikiwa yuko tayari, na baada ya Efraim kutikisa kichwa kukubali, Godwin akamwambia aunganishe viganja vyake na kufumba macho, kisha akae kwa kutulia. Alikuwa ameshamwambia kwamba asishangae endapo angekutana na hali iliyobadilika, kwa hiyo Efraim akawa ameiandaa akili yake kwa chochote kile ambacho angeona.

Godwin akaanza kuongea maneno fulani ambayo hayakueleweka hata kidogo masikioni mwa Efraim, na mwanaume huyu akaendelea kusimama kwa utulivu zaidi akisubiri maagizo mengine. Ndipo akaanza kuhisi kama upepo mkubwa ukipuliza sehemu aliyokuwepo, lakini tena ni kama alikuwa kwenye sehemu isiyotoa sauti yoyote hata kidogo. Aliingiwa na msisimko zaidi baada ya kuanza kusikia sauti kama hatua za mtu anayetembea kumwelekea, lakini akajitahidi kutofumbua macho yake hata mara moja. Sauti hizo zikageuka kuwa kama sauti za matone ya maji yakidondoka kidogo kidogo ndani ya tenki lenye maji, na ndipo sauti nzito ikasikika ikifanya kama mguno wa mtu aliyeridhika.

"Hmmmm... Efraiiimmm..."

Jina lake lilitajwa kwa njia nzito sana, na wasiwasi mwingi ukamwingia mwanaume huyu kwa kutotambua nani aliyetamka jina lake.

"Piga magoti..."

Mnong'onezo huo kutoka kwa Godwin ulipenya vyema masikioni mwa Efraim, naye akatii na kupiga magoti chini kabisa.

"Godwinnn... mwana wa Isaya Shigelaaah..."

Sauti hiyo nzito ikasema maneno hayo.

"Ni mimi... mtumishi wako," Godwin akatamka maneno hayo.

Efraim Donald alikuwa ameingiwa na wasiwasi mwingi sana kufikia hapa, akijiuliza ikiwa bado alitakiwa kuendelea kufumba macho au la.

"Umeniletea zawadi Godwinnn..." sauti hiyo ikasema.

"Nimeleta zawadi bwana wangu. Ni zawadi ambayo itakupa kilicho bora kwa njia yoyote unayotaka..." Godwin akasema.

"Hmmmm... Efraiiimmm..." sauti hiyo ikaita.

Efraim Donald, akiwa bado amefumba macho yake, akajiongeza na kusema, "Ndiyo, bwana wangu..."

Sauti hiyo ikaanza kucheka sana kwa njia iliyomuumiza Efraim masikio, lakini akajitahidi kujikaza na kuendelea kushikanisha viganja vyake huku akiwa amefumba macho.

"Fungua macho yako Efraiimmm..."

Baada ya sauti hiyo kusema hivyo, Efraim Donald akafumbua macho yake na kushangazwa sana na mazingira aliyojikuta katikati yake. Ilionekana ni kama yuko msituni, pakiwa na uoto mwingi wa asili, na mbele yake vilisimama viumbe vitatu virefu sana vilivyofunikwa kwa nguo nyeusi juu mpaka chini. Hakuelewa walifikaje hapo, lakini akajitahidi kujikaza zaidi na kuonyesha ujasiri na uhakika. Akaangalia pembeni na kumwona Godwin akiwa amepiga magoti kando yake, na rafiki yake huyo akamtikisia kichwa kumwonyesha kwamba wako pamoja.

"Unajua uko mbele ya nini Efraiimmm...?" sauti hiyo ikauliza.

Efraim aliweza kutambua sasa kwamba huyo kiumbe aliyesimama katikati ya wale wawili ndiye aliyeongea, akiwa kama mwakililishi na wakala mkuu wa mzee mwenyewe, naye Efraim akasema, "Ndiyo bwana wangu. Niko mbele ya sehemu takatifu."

Sauti hiyo ikacheka kwa njia iliyojaa hila nyingi sana, naye Efraim akamwangalia Godwin kiufupi, ambaye alimwonyesha kwa ishara ya macho kuwa anajitahidi.

"Utanipa nini Efraiiimmm...?" sauti hiyo ikauliza.

"Chochote kile utakacho bwana wangu..." Efraim akajibu huku mapigo yake ya moyo yakidunda kwa nguvu sana.

"Na wewe unataka nini, mwanangu?" sauti hiyo ikauliza.

"Ninahitaji... kupata pesa na... mali nyingi sana... bwana wangu..." Efraim akasema.

"Hmmmm... ni mambo ambayo wengi hutaka... lakini nahitaji kujua kwa nini unayataka..." sauti hiyo ikasema.

"Ninataka kuboresha maisha yangu... ninataka nisiendelee kuonekana kuwa kitu cha kudharaulika bwana wangu... nipate heshima... si heshima kama unayostahili wewe... yaani heshima isiyoweza kukaribiana na yako... bali heshima ile itakayozidi kukupa utukufu wewe pekee bwana wangu..." Efraim Donald akasema.

"Hmmmm... maneno mazuri sana. Nimekuangalia Efraim... kwa muda mrefu. Wewe ni kiumbe wa pekee... na upekee wako utakufikisha mbali ikiwa tu utafanya kile ulicholetwa duniani kufanya.... NIABUDU MIMI EFRAIIMMM!"

Sauti hiyo ilinena hayo kwa uzito sana, naye Godwin akainama zaidi kama anasujudu, kitu kilichomfanya Efraim Donald atende namna hiyo hiyo pia.

"Unajua kazi ya wafanyakazi wa mochwari ni nini?" sauti hiyo ikauliza.

Efraim Donald akatulia tu akiwa bado amesujudu bila kutoa jibu.

"Kazi yao ni kupunguza uzito wa hofu inayosababishwa na kifo, na wakati huo huo wakipata faida kutokana na msiba unaowapata wengine. Wanawachukua watu waliokufa na kuwapendezesha; wanazitengeneza nywele zao, wanawavalisha nguo safi, halafu mwishowe wanakuja kutupwa chini ya ardhi chafu. Ila unafikiri hao wafu huwa wanajali hilo? Hapana... hawajali. Lakini watu wa mochwari hawafanyi hayo kwa ajili yao. Wanafanya hayo kwa ajili ya wale wanaowaombolezea. Wanawarahisishia kusema kwa heri, kama njia ya kutoa kitulizo cha kihisia. Wanawasaidia kukubaliana na ukweli wa kwamba mpendwa wao amewatoka daima, na wakati huo huo wakiingiza malipo mifukoni mwao. Sababu bila shaka ni hofu. Watu huogopa kifo, na pale mtu wa karibu anapokufa inawalazimu kukumbuka na kukubali kwamba nao pia watakufa. Wanyama hawana hili tatizo. Muda mchache wa maumivu makali sana yenye kupelekea kifo ndiyo utakaomfanya mnyama atambue uzito wa jambo hilo... lakini wanadamu... mnaishi maisha yenu yote mkielewa kwamba muda wowote ule, bila onyo, bila sababu, maisha yenu yanaweza kukata. Hiyo ndiyo sababu mna mifumo kama hii ya mochwari... ili kusaidia kupambana na hali hiyo ya hofu ipasavyo..."

Efraim Donald hangeweza kuelewa ni kwa nini kiumbe huyo aliongea maneno hayo, lakini alijua lazima kulikuwa na ujumbe muhimu aliotakiwa kuelewa hapo.

"Nitakupa unachotaka Efraiimmm... ikiwa utanitumikia kwa njia nayotaka," sauti ya mwakilishi ikasema.

"Ndiyo bwana wangu... nitakutumikia wewe tu," Efraim akasema akiwa bado amesujudu.

"Hmmmm... ninakupa utumishi Efraiimmm... utumishi kwa mmoja wa wanangu... mtumikie... mpe anachotaka kwa wakati anaotaka... mfurahishe... na kila kitu unachokitaka utapewa..." sauti hiyo ikasema.

"Ndiyo bwana wangu... niko tayari..." Efraim Donald akasema kwa uhakika.

"Vizuri. Ninakupa mmoja wa wanangu... msababishaji wa ajali... mzuiaji wa hedhi kwa mwanamke... mpenzi wa damu changa ya mwanamke... mtumikieee... mfurahishe... apate nguvu zaidi... aniongezee nguvu maradufu... nami nitakupa kila kitu unachotaka..." sauti hiyo ikamwambia.

"Ninakubali utumishi huo bwana wangu... nitafanya unavyoniagiza," Efraim Donald akasema.

Sauti hiyo ikacheka kwa kishindo sana, kisha ikasema, "Inuka."

Efraim Donald akajinyanyua taratibu na kurudia kupiga magoti, vile vile na Godwin pia, kisha kiumbe huyo akaonekana kunyoosha mkono wake, sijui mkono, sijui nini; akiuelekeza kwa Efraim Donald, na hapo hapo mwanaume huyu akaanza kuhisi kizunguzungu cha hali ya juu, kama vile kuna vitu vilikuwa vikiingia ndani ya kichwa chake kwa kasi sana, na kwa muda huo aliweza kupatwa na vitu kama maono mengi sana yaliyomwelezea vitu vingi mno, kisha hisia hiyo ikakoma ghafla, naye akabaki kupumua kwa njia ya kichovu.

Aliponyanyua macho yake kumtazama yule kiumbe, akajikuta akiwa ndani ya chumba kile cha mochwari, na hapo hapo bega lake likashikwa. Akageuka kwa kasi na kukuta ni Godwin ndiye aliyemshika, naye Efraim akatulia na kukaa chini kwanza.

"Uko sawa?" Godwin akamuuliza.

Efraim Donald akatikisa kichwa kukubali.

"Umeonyeshwa vitu... vitu vingi sana unavyohitaji kufanyia kazi, siyo?" Godwin akauliza.

"Ndiyo. Nafikiri najua nachopaswa kufanya sasa," Efraim akajibu.

"Na?" Godwin akauliza.

Efraim Donald akaachia tabasamu lililoonyesha hila, kisha akasema, "Nafikiri nita-enjoy."

Godwin akatikisa kichwa chake huku akitabasamu kwa furaha sana, kwa kuwa sasa alitambua kwamba aliweza kumbadili rafiki yake awe aina ya mtu ambaye yeye pia alikuwa amegeuzwa kuwa. Akamsaidia kunyanyuka na kumwambia waondoke hapo upesi, na angemwelezea mambo yote aliyoona na aliyotakiwa kuanza kufanyia kazi ili zoezi lake la kupata mali nyingi lifanikiwe haraka sana. Mambo yote haya yalikuwa yenye kutisha sana, lakini kwa sasa Efraim alikuwa ameshabadilishwa moyo kwa njia kubwa mno, na angehakikisha anafanya kila kitu ili kukamilisha mambo yote aliyotakiwa kufanya kwa umakini wa hali ya juu.



★★★★★★★★★★★★

ITAENDELEA

★★★★★★★★★★★★


Usikose sehemu za mwendelezo wa hadithi hii kali ya CHANGE. Ni story nzuri na ndefu sana. Waweza ipata nakala yote kwa gharama nafuu sana. Karibu WhatsApp au kwa E-mail yangu.

WhatsApp no: +255 678 017 280

e-mail: eltontonny72@gmail.com
 
Sahamani mkuu, kwakua nachanganya stori ndni ya stori ila uzuri ni kwamba wewe ni muhusika wa yote mawili,, napenda kuuliza INVISIBLE 3 isubiriwe mpaka lini?
 
Mkuu Elton Tonny hongera sana kwa kazi nzuri, nimeanza kuamini nyuma ya mafanikio ya watu wenye pesa nyingi, mafanikio makubwa na majina yanayovuma sana kuna mambo mazito ya siri nyuma yake. Hii historia ya Efraimu Donald ni funzo zuri sana kwa sisi Vijana tunaotaka mafanikio na umaarufu. 🤔🤔

Ni Muumini wa scriptures
Keep your lives free from the love of money and be content with what you have, because God has said, "Never will I leave you; never will I forsake you." 6So we say with confidence, "The Lord is my helper; I will not be afraid.
Hebrews 13:5 😂😂😂
 
Back
Top Bottom