Simulizi - DYLAN

Simulizi - DYLAN

Huyo ndiye Beatrice ninayemfahamu. Madhara makubwa kabisa ya Obsession ni "HERI TUKOSE WOTE FURAHA" Obsession haimuchagi mtu salama hata kidogo
 
DYLAN

Story by Elton Tonny

Familia, Kazi, Urafiki, Mapenzi, Tamaa, Hila, Unyanyasaji, Usaliti, Visasi, Mauaji, Mambo Yasiyotazamiwa

(R-rated 18+)

Enjoy!

★★★★★★★★★★★★★★★★★★

SEHEMU YA AROBAINI NA MBILI

★★★★★★★★★★★★★★★★★★


Dylan aliendesha kwa spidi zote kiasi kwamba mpaka Gilbert akahofia huenda wangeanguka. Lakini alielewa kuwa kijana wake alihofia zaidi usalama wa wanawake kule nyumbani, hivyo ingekuwa lazima afanye mambo kwa uharaka. Gilbert alipigiwa simu na baba yake, ambaye alikuwa akiuliza kulikoni maana waliondoka na kuwaacha ukumbini bila maelezo yoyote ya ni wapi bibi harusi alikuwa; hasa familia ya bwana harusi ndiyo iliyokuwa na maswali mengi sana. Gilbert akamwambia ndiyo wanaelekea huko kumfata, hivyo akamwomba baba yake awatulize watu pale ukumbini.

"Inashangaza sana!" akasema Gilbert baada ya kumaliza kuzungumza kwenye simu.

"Kuhusu Beatrice kutoroka gerezani?" akauliza Jafari.

"Ndiyo lakini... hasa ni kwa nini mpaka sasa hatukuwa na taarifa zozote kuhusu hilo wakati limetokea jana," akasema Gilbert.

"Me mwenyewe nashangaa! Hizi zingekuwa habari muhimu sana ambazo tungesikia haraka lakini..."

"Wewe nani amekwambia?" Dylan akamkatisha Jafari.

"Kuna askari magereza huko ninajuana naye. Ndiyo kanipigia akaniambia. Anasema walikuwa wanataka wamkamate tena kimya kimya lakini muda umeenda na hawajafanikiwa... yaani ni kama amepotea tu," Jafari akaeleza.

"Inabidi tuwaambie polisi..."

"Hakuna chochote ambacho hawajui baba. Kutegemea msaada wao ni kazi bure...tutapaswa kushughulika na haya sisi wenyewe," Dylan akasema.

"Vipi tusipowakuta huko nyumbani Dylan? Je, kama Beatrice amewa...." Gilbert akashindwa kuendelea.

Dylan akatoa simu yake mfukoni na kumpigia Bosco.

"Bro..."

"Bro vipi? Mbona mmeondoka huku sherehe inakuwaje sasa watu wamechizi, nini kinaendelea?" Bosco akauliza kwenye simu.

"Beatrice ametoroka jela, tunahofia anaweza akawa amefika home..."

"What? Ametoroka vipi? Nani ame..."

"Nisikilize bro. Nahitaji unisaidie. Unajua la kufanya. Niko naelekea huko sasa hivi... please," Dylan akasema.

"Okay. Nanyanyuka now," Bosco akasema.

"Asante," Dylan akasema na kukata simu.

"Nani ulikuwa unaongea naye?" Jafari akauliza.

"Plan B," Dylan akajibu kimkato.

Walifika mpaka usawa wa nyumba ya Gilbert na kuegesha gari pembeni, nao waliweza kuona taa za nyumba zikiwa zimewashwa. Sehemu hii ya nje haikuwa na mtu hata mmoja aliyepita, hivyo wakapeana tahadhari kuwa waangalifu sana watakapoanza kuelekea kule ndani. Wakashuka na kuanza kutembea vizuri polepole, wakiangalia huku na kule kuona kama kuna nuksi yoyote. Walipofika usawa wa geti, waliona kwamba mlango mdogo wa geti wa kuingilia hapo ulikuwa na uwazi, hivyo Jafari akaokota jiti fulani nene lililokuwa chini na kulishikilia kwa ajili ya kujihami; kwa kuwa hakuwa amebeba bastola yake.

Dylan akalisukuma taratibu, kisha akaingia kwa umakini sana. Ile anapiga macho pembeni chini aliweza kuona mwili wa mlinzi wa Gilbert ukiwa umelala na damu nyingi kutokea kifuani zikiwa zimetapakaa chini. Akafumba macho kwa kusikitika, na ni hapa ndipo Gilbert pia akaingia na kushtushwa sana na jambo hilo. Sasa wakawa wamethibitisha kuwa bila shaka Beatrice alikuwa nyuma ya hili, na wasiwasi uliwajaa walipowafikiria wapendwa wao.

Nje hapo waliweza kuziona gari maalum zilizokuwa zimetengenezwa kwa urembo kwa ajili ya Camila na wapambe wake wachache. Jafari akatoa ishara kwa kiganja chake kuwa waelekee ndani kule kwa kuachana-achana, ili kama hatari ikitokea kwa mmoja basi mwingine awe nyuma kumsaidia. Dylan akatangulia, kisha Gilbert akafuata. Alifika usawa wa mlango na kuusukuma, kisha akaingia ndani hapo na kubaki mdomo wazi kwa mshangao. Alishindwa hata kuendeleza umakini aliokuwa nao na kuanza kutembea taratibu akiwa amefadhaishwa na yale aliyoona.

Kulikuwa na miili sita ikiwa bila uhai hapo chini; wanawake watano, mwanaume mmoja, na damu nyingi zilikuwa zimetapakaa. Dylan aliweza kuwatambua wanawake wale wanne kuwa ndiyo baadhi ya wapambaji waliokuwepo nyumbani hapo leo, na mmoja alikuwa ni msichana wa kazi wa Grace, yaani Matilda, ambaye alikuja huku pia kumsaidia boss wake. Mwanaume yule alikuwa ndiyo dereva ambaye angewaendesha kuelekea hotelini. Wote walikuwa na matundu ya risasi kwenye miili yao. Gilbert naye akawa amefika, na ni itikio hilo hilo alilokuwa nalo Dylan ndilo lililompata pia. Alighafilika sana. Akaanza kuelekea upande wa jikoni kuweza kuangalia mambo huko yalikuwaje.

Dylan alipoanza kuangalia usawa wa ngazi, aliweza kuona michirizi ya damu ikitokea juu kule, naye akazielekea na kutazama juu. Aliweza kuona miili mingine miwili katikati ya ngazi kuelekea juu, bila shaka wasichana, ambao walivalia gauni zenye kufanana, na hili likamwambia Dylan kuwa hao walikuwa ni baadhi ya wapambe wa bibi harusi (au wacheza show), na inaonekana walikuwa wakimkimbia mtu huyu aliyewapiga risasi watu wote ndiyo nao wakapigwa migongoni. Mauaji haya yalielekea chumbani. Hivyo Dylan akaanza kupanda upesi akiwa na hofu kubwa mpaka alipokaribia milango ya chumba ambacho michirizi ya damu nyingi ilitokea.

Alipotaka kuifungua, Gilbert akaja nyuma yake akiwa ameshika visu viwili na kumpatia kimoja, bila shaka akiwa amevichukua kutokea jikoni kule chini. Waliangaliana kwa huzuni sana, kisha wakafungua mlango kwa kasi na kuingia; kukuta miili mingine ya wasichana wanne waliovalia sare zile zile, ikiwa imezagaa humo na kutapakaza damu kila kona. Yaani ilikuwa ni kama bafu la damu humo ndani!

Gilbert na Dylan walichoka. Watu walikuwa wamekufa kama wadudu bila hatia yoyote, na tena kikatili sana. Ikabidi tu wajikaze na kuendelea kutafuta vyumba vingine kuona kama wangeweza kumpata Grace, Jaquelin na Camila, lakini hawakufanikiwa kuwaona. Wote walihisi kukata tamaa. Wakarudi mpaka sehemu ile ya sebule, naye Dylan akapiga magoti chini karibu na mwili wa Matilda, machozi yakianza kumtoka. Gilbert naye alikuwa amesimama usawa wa mwana wake akiwa na huzuni nzito.

"Watu hawa walikuwa wamemkosea nini?" Gilbert akanena kwa sauti ya chini.

"Kama anaweza kuua mpaka mtoto wake wa kumzaa mwenyewe... huyo mwanamke siyo mtu..." Dylan akasema kwa huzuni.

"Camila atakuwa wapi Mungu wangu? Jaquelin... Grace... yaani.... aisee! Tutafanya nini sasa?" Gilbert akauliza kwa kupoteza matumaini.

Haikuwa imeingia akilini mwa Dylan kutambua kwamba ni kama Jafari hakuwepo. Ile tu wazo hilo lilipoingia kichwani kwake, akataka kugeuka ili kuangalia uwepo wa mwanaume huyo pale aliposikia sauti ya maumivu kutoka kinywani mwa baba yake!

"Aaaagh!"

Akageuka upesi kumwelekea Gilbert na kukuta amedondoka chini, na ile anaangalia sehemu ya hapo kumwona adui, akahisi kitu fulani kizito kinapiga kichwa chake na kusababisha giza zito lifunike macho yake! Akadondoka chini na kupoteza fahamu zake pale pale.


★★★★★★


Harleen: Huwa...unanifikiria kama ulivyokuwa unanifikiria kipindi hicho? You know..me..coming out of the pool...wet...

Dylan: Kwa nini unauliza?

Harleen: Curiosity...

Dylan: Curiosity killed the cat...

Harleen: Ahahahah...

Dylan: I'll be honest. Nilipenda kukuangalia sana kwa kuwa vinguo vya kuogelea vilifanya sehemu kubwa ya mwili wako ionekane. Sikuwahi kuona msichana akiwa bila nguo, na wewe ulikuwa umekaribia jambo hilo. Uli...ulinisisimua...

Dylan: Si ndiyo huyo weasel uliyekuwa unamsemea?

Fetty: Ndiyo...

Dylan: Anajifanyaga anajua sana huyo. Yaani huwa namnyoosha, mpaka nitahakikisha hicho kitambi kinaporomoka...

Fetty: Ndiyo, anaonekana ni mwenye hila sana. Nilikuwa nakwambia...

...: Sir Dylan...helicopter imefika...

Dylan: Already?!

...: Ndiyo sir...

Fetty: Ni marafiki tu wa kawaida...

Gilbert: Nafurahi kwamba unatengeneza marafiki sasa. Itapendeza ukiwa unawaleta muwe mnajifurahisha...

Jaquelin: Halafu wakiichoma nyumba moto?

Dylan: Usijali mama. Hekalu lako litasimama daima...

Jaquelin: Una miaka mingapi?

Fetty: 25...

Camila: Unaonekana mkubwa, ila kumbe mdogo...

Dylan: Ninataka kumweka Fetty awe assistant manager kwenye Dy-Foods Restaurant...

Jaquelin: Ataweza assistancy, au unataka tu kumsumbua mtoto wa watu? Ili akiboronga, uwe na mtu wa kulalamikia...

Dylan: Hamna. Ni ili tumbo lako likikoroga, ukimbilie Dy-Foods kula bamia...

Dylan: After seeing you earlier...solo me quedo el requerdo de la felicidad intensa que me hiciste sentir (baada ya kukuona tena muda ule...nilirejewa na kumbukumbu ya furaha kubwa sana uliyonipa kipindi kile).

Camila: Oh Dylan... De que servirán requerdos cuando ya no estés conmigo (kumbukumbu zitasaidia nini wakati hauko nami tena?)

Dylan: What do you mean?

Camila: I'm engaged, Dylan (nina mchumba, Dylan).

Harleen: Usijisikie vibaya lakini Dy...

Dylan: No, no, no. Sijisikii vibaya. Baada ya hiyo mechi kali hivyo nitajihisije vibaya?

Killmonger... Killmonger... Killmonger...

Harleen: Ahahah...sawa. Bila shaka unasikia njaa, siyo? Twende ukale kitu fulani...

Dylan: Ningependa kukula wewe tena...

Gilbert: Unataka kuwa mvuta bangi?

Dylan: Siyo mimi... ila inaonekana ndo' nyie mnachokitaka...

Gilbert: Hapana Dylan. Tunafanya hivi ili uweze kuwa na maisha bora baadae. Na usiamini ulichosikia, kwa sababu wavuta bangi wako kila sehemu, lakini unanionaje mimi, navuta bangi?

Dylan: Siwezi kujua... huu utawala wa Kikwete labda kuna bangi zinanukia siku hizi!

"Dylan... Dylan... Dylan amka!"

Queen: Una moto mwingi sana ndani yako Dylan ambao niliona ni kama unapotea tu bure huku... I wanted to help make it so your talent doesn't go to waste...

Dylan: Na ili upate pesa nyingi kupitia kwangu...

Queen: Ahahahah... yeah...

Dylan: So what happens now?

"Dylan... Dylan mwanangu amka! Tafadhali amka! Dylan!"

Dylan: Asante sana kwa kila jambo ulilofanya kwa ajili yangu... wewe ni wa muhimu sana kwenye maisha yangu Grace.... Nakupenda....

"Dylan amka!"

Dylan akafumbua macho yake kwa kushtuka sana! Akayafumba tena baada ya kuhisi maumivu kichwani kwake, na hakuweza kutambua alikuwa wapi kutokana na kichwa chake kuzunguka sana. Lakini pamoja na haya yote, wakati huu alikuwa anayaona mambo kwa njia tofauti sana. Yote hayo yaliyopita kichwani kwake yalikuwa ni sehemu za kumbukumbu za maisha yake ya nyuma, na sasa baada ya kufumbua macho, kumbukumbu zake ZOTE zikawa zimerejea! Hii ilitokana na kupigwa kwa kichwa chake kwa nguvu mno wakati yuko nyumbani pamoja na baba yake na Jafa... Subiri kwanza!

Akatazama eneo alilokuwa, naye akatambua alikuwa kwenye jumba fulani kubwa na kwenye chumba kipana sana; ijapokuwa kulikuwa na giza. Pembeni yake kulikuwa na mtu mwingine, na kwa uhakika zaidi baada ya kumtazama kwa kulizoea giza aliweza kutambua kuwa ilikuwa ni baba yake. Aliisawazisha vizuri akili yake, naye akatambua kwamba alikuwa amelazwa chini, huku mikono yake ikifungwa kwa nyuma pamoja na miguu yake. Gilbert alikuwa anamuuliza ikiwa yuko sawa, na baada ya kumwangalia vizuri pia akatambua naye alikuwa amefungwa namna hiyo hiyo.

Dylan akajiviringisha ili aweze kujinyanyua na kukaa, lakini ilikuwa ngumu sana. Akashindwa na kuambulia maumivu tu zaidi kwenye viwiko vya mikono yake na kichwani. Gilbert akamwambia atulie kwanza maana alijiumiza sana, na kwa kuwa walitakiwa kujua hasa yaliyotokea, ingebidi waongee pamoja. Dylan alikuwa akipumua kwa hasira sana chini hapo, na baba yake vile vile alikuwa amelala hivyo hivyo kwa kufungwa. Kulikuwa na giza humo hivyo hawakuweza kuonana vizuri, na mbu wengi waliwasumbua sana.

"Ahhh...ssss... kichwa kinauma sana!" Dylan akasema.

"Pole Dylan... hata mimi vile vile..." Gilbert akajibu.

"Tumekuwa hapa kwa muda gani?" Dylan akauliza.

"Sijajua... ila toka nilivyoamka ni kama saa limepita na wewe ndiyo ukaamka..."

"Huyo malaya kama alikuwa anataka kutuua tungekuwa tushakufa..."

"Anachotaka ni nini hasa?"

"Kisasi... kutuumiza nafsi... nafikiri anapanga jambo fulani... ndiyo sababu tuko hapa..."

"Hiyo ikimaanisha Jaquelin na wengine watakuwa hai si ndiyo?"

"Inaonekana... siwezi kusema kwa uhakika..."

"Agh... jamani! Ilifikiaje hatua hii! Mimi ndiyo nimesababisha haya yote... ikiwa jambo lolote baya litawapata sitajisamehe kamwe..."

"Hatupaswi kukata tamaa, sikuzote kuna njia... Tutatoka tu..."

"Yaani... sijui hata Jafari wamemweka wapi... naomba Mungu wasiwe wamemuua kijana wa watu..."

"Jafari...."

Dylan akaanza kutafakari jambo fulani baada ya baba yake kumtaja Jafari.

"Baba... ulimwona aliyekupiga?" Dylan akamuuliza.

"Hapana... sikumwona..."

"Jafari alikuwa wapi wakati..."

Kabla Dylan hajamaliza kuongea, taa za jengo hili zikawashwa na kufanya mambo yaanze kuonekana vyema ndani hapo. Mwanzoni iliwaumiza wawili hawa macho, lakini wakaanza kuzoea na kujaribu kupeleka shingo zao huku na huku ili kutazama sehemu hii waweze kumwona mtu aliyewasha. Gilbert alikuwa wa kwanza kumwona mwanaume fulani akiwa amemshikilia Camila, akiwa amevaa gauni lake lile lile zuri la sherehe, huku akiwa amefungwa mikono kwa nyuma na mdomoni kuwekewa kitambaa cheupe kuziba sauti yoyote ambayo angetaka kutoa.

"Camila!" Gilbert akaita kwa sauti yenye hofu.

Dylan akageuzia shingo yake upande huo pia na kumwona shangazi yake mdogo akiwa ameshikwa namna hiyo. Simanzi nzito ilimwingia kwa kuwa sasa aliweza kumkumbuka vizuri sana. Akawa anamwangalia kwa hisia sana bila kuweza kunyanyuka ili kwenda kumpatia msaada. Papo hapo wakaingia wanaume wengine watano wenye miili mikubwa ya mazoezi. Wawili walikuwa wakiwavuta Jaquelin pamoja na Grace; wakiwa wamewafunga namna hiyo hiyo pia kama Camila. Dylan akaanza kufurukuta chini hapo baada ya kuona jinsi Grace alivyokazwa huku akiwa na ujauzito. Alimwonea huruma sana mpenzi wake na kuhisi hasira kubwa sana kuelekea wanaume wale.

"Washenzi nyie! Waachieni haraka! Nitawaua wote!" Dylan akaapaza sauti huku bado akihisi maumivu ya kichwa.

Wanaume wale watatu waliokuwa wamewashikilia wanawake wakasimama kwa kupangana, na wengine wawili wakatembea kufikia usawa wa Gilbert na Dylan, huku mmoja akiwa amesimama tu akiwaangalia na tabasamu la hila. Huyu alikuwa ndiyo yule bodyguard wa karibu wa Beatrice, yaani Seba. Mmoja wa wale wanaume waliowafikia Dylan na Gilbert akampiga Dylan hapo hapo chini teke la tumboni lililomsababishia maumivu makali sana, nazo sauti zilizozibwa za vilio kutoka kwa Jaquelin na Grace zikasikika.

"Tafadhali jamani msiwaumize hawa wanawake! Ona yule pale ni mjamzito... anahitaji...."

"Funga domo lako!" mwanaume mmoja akamkatisha Gilbert.

"Acheni jamani! Kama ni sisi mnatutaka sawa, waachieni hao hawana kosa lolote lile..." Gilbert akaendelea kuwaomba.

"Kwani nani kasema kuna mtu mwenye makosa?"

Sauti hiyo ilisikika kutokea nje ya mlango wa kuingilia hapo, nao wote waliifahamu vizuri sana. Wakatazama upande huo, na hapo hapo akaingia Beatrice mwenyewe! Alikuwa amevalia nguo nyeusi juu mpaka chini zenye kuubana mwili wake (koti la kike na suruali ngumu), machoni akivaa miwani nyeusi, na miguuni mabuti ya kike marefu pia. Akafika mpaka usawa aliosimama Seba pale katikati, kisha akaachia tabasamu la kujivuna.

"Beatrice! Niaje mrembo? Nilifikiri ulitakiwa kuwa jela..." akasema Dylan kikejeli.

"Clearly sipo huko sasa!" akasema Beatrice kwa sauti tulivu.

"Ahahah... umependeza kinoma yaani! Nifungulie basi tupige selfie angalau," akasema Dylan.

Beatrice akacheka kwa dharau.

"Unanikumbusha mambo mengi kuhusu baba yako enzi zile za ujana wetu... alikuwa cheesy kama wewe ulivyo," akasema Beatrice.

"Beatrice tafadhali, usifanye lolote baya kwa mtu yeyote. Najua hii ni kuhusu mimi na wewe, tuyamalize mimi na wewe tu. Waachie wengine nakuomba tafadhali," Gilbert akamwambia.

"Sielewi unamaanisha nini! Mimi nilitaka tu tuwe pamoja leo hapa... kama reunion... marafiki tufurahie mambo mazuri... mbona unaongea utafikiri mimi ni adui yako?" Beatrice akasema kwa kejeli.

"Unajikuta jambazi sugu kama wa kwenye movie fulani ya kifilipino eti? Wewe uta...."

Kabla Dylan hajamaliza kuongea akapigwa teke lingine tumboni.

"Dylan!" Gilbert akamwita kwa hofu.

Mwanaume aliyempiga Dylan akamnyanyua na kumsimamisha kwa lazima. Kwa sababu alikuwa amefungwa, hakuweza kusimama vizuri, hivyo aliumia sana kwa sababu kamba zilikuwa ngumu mno. Beatrice akatoa bastola kutoka nyuma ya kiuno chake, na kuwafanya wote washikwe na hofu.

"Huu siyo wakati wa kujifanya unajua sana kuongea. Ikiwa hutaki kuona nalipasua hili tumbo lenye mjusi wako humo ndani, funga bakuli lako," Beatrice akamwonya Dylan, akimaanisha tumbo la Grace.

Dylan alihisi hasira kali sana. Alitaka sana kumshika mwanamke huyo amfundishe adabu. Lakini akiangalia na hali walizokuwa nazo, haingekuwa rahisi kufanya lolote lile. Kihalisi alichokuwa anafanya ilikuwa kumpotezea muda Beatrice akiwa na lengo lake akilini, lakini sasa ingembidi tu atulie maana mwanamke huyu hakuwa na akili sawa. Beatrice akaelekea upande aliosimama Jaquelin, na baada ya kumfikia, akakishusha kitambaa kilichokuwa kimemziba mdomo.

"Hi Jacky... nimekumiss shosti," Beatrice akamwambia.

Jaquelin alikuwa anamwangalia huku anapumua kwa hofu sana.

"Heeey vipi? Mbona presha? Its me your friend! Unatakiwa ufurahi kuniona... au... nimekuwa nweusi sana? Ahahahah..." Beatrice akasema kwa kejeli.

Yeye pamoja na mabaunsa wake wakawa wakicheka.

"Beatrice... kama niliwahi kukukosea..."

"Aa-aaa mambo gani hayo! Acha kuwa p(....) bwana! Jaquelin nayemjua mimi hajing'atagi kifala namna hiyo. Ongea kama Jaquelin nayemjua!"

"Please Beatrice... mwachie Grace na Camila. Wewe ni mama pia... unajua Grace anakaribia kujifungua hapaswi kuwa chini ya pressure kubwa kiasi hiki... nakuomba... nitafanya lolote lile... please mwachie binti yangu... Beatrice tafadhali...." Jaquelin akaomba huku analia.

"Hmmmm... unatia huruma. Na uko sahihi... mimi ni mama. Na ndiyo maana niko hapa. Kwa kuwa nyie ndiyo mmesababisha mpaka mtoto wangu amekufa!!!" Beatrice akafoka usoni mwa Jaquelin.

"Beatrice..." Gilbert akamwita.

"Yes honey..." akaitika.

"Tafadhali... yote yaliyotokea hayakuwa fair. Please... tunaweza kuongea vizuri. I know you Beatrice. Najua unaweza kubadili..."

"Oh no no no no no... see Gil hapo ndo unapoboronga. Mimi siyo Beatrice yule unayemfahamu. Uliyekuwa unacheza naye kitandani wakati Jacky akiwa vibandani..." akasema Beatrice.

"Nini?" Jaquelin akashangaa.

"Oh... ulikuwa hujui? Mimi na Gilbert ni waaaay back. Tumepeana mapenzi matamu every time... kipindi hicho umekuwa bonkers. Na iliendelea kwa miaka mingi shosti. Hahah... Unajua alichokuwaga ananiambia? Mimi ndiyo nina nyama tamu kuliko hata yako! Ahahahah... aaahh the days..." Beatrice akaongea kwa kejeli.

Jaquelin akamtazama Gilbert kwa huzuni sana. Fikira ya kwamba hakujua kuhusu mambo hayo muda wote huu ilimvunja sana moyo. Angeweza kuweka pembeni ukweli wa kwamba mume wake aliwahi kutoka nje ya ndoa, kama yeye tu, lakini kujua kwamba mwanamke aliyetoka naye alikuwa rafiki wa karibu kwa muda mrefu kulimuumiza sana. Gilbert akamwangalia mke wake akisononeka sana moyoni mwake, akishindwa hata aongee nini.

"Mwanzoni ilikuwa ni kuhusu mimi na wewe tu Gil, lakini sasa hivi mambo yamepanuka. Sikuhitaji tena, nataka tu uone jinsi gani inavyoumiza kuwapoteza watu unaowapenda kama mlivyonifanya niwapoteze wangu..." Beatrice akasema.

"Lakini Harleen ulimuua wewe mwenyewe!" Dylan akamwambia.

"Ndiyo. Hata na baba yake pia," Beatrice akasema, kiutulivu kabisa.

Wote wakashangaa.

"Nini? Ulimuua Alfred?" Gilbert akauliza.

"Oh acha kujifanya kama ulikuwa unamjali sana wakati ulikuwa unanila nikiwa naye bado. Hiyo niliifanya kwa ajili yako... nikitumaini utamwacha huyu mshenzi na kuja kwangu, lakini ukajifanya unampenda zaidi ya mimi. Na Harleen... isingekuwa ya king'ang'anizi cha mwanao mpaka sasa angekuwa hai..."

"King'ang'anizi gani? Me ndiyo nilikutuma ufanye haya yote?" Dylan akauliza.

"Nani alikwambia uokoke ile ajali, eeh? Ulipaswa kufa kwenye helicopter ile lakini ukajifanya mgumu sana. Now we're here..." Beatrice akasema.

"Beatrice..." Gilbert akamwita kwa hisia.

Beatrice akatabasamu, kisha akaanza kuelekea kwa Grace. Dylan akapandwa na hofu sana.

"Na wewe... kujiingiza kwenye mambo yasiyokuhusu... umejiweka kwenye list nzuri ya watu nitakaofurahia sana kuwaondoa hapa duniani... wewe na haka kautumbo kako kenye..." akawa anaitembeza bastola juu ya tumbo la Grace.

"Beatrice no..." akasema Jaquelin.

"Beatrice..." akaita Gilbert.

"Aunty Beatrice tafadhali usifanye... please usifanye hivyo!" Dylan akamwomba huku chozi likimtoka.

"Aunty Beatrice! Wow ni muda mrefu sijasikia umeniita hivyo. Imekuwaje?" Beatrice akasema.

"Nimekumbuka kila kitu. Nimekumbuka jinsi ulivyokuwa mzuri kwetu... tokea tulivyokuwa wadogo. Tafadhali aunty Beatrice... usifanye hivi... hatutaenda polisi tena... tuta... tutakuacha hatutakubughudhi kabisa... please!" Dylan akaendelea kumwomba kwa hisia.

Beatrice akawa anacheka tu, kisha akakitoa kitambaa kilichokuwa kimeziba mdomo wa Grace na kumwekea bastola karibu na taya yake.

"Ongea maneno ya mwisho kwa mpenzi wako dear..." Beatrice akasema.

"Beatrice! Mguse Grace haki ya Mungu I'm going to kill you! Nitakuua! Nita...aaargh!!"

Dylan akiwa anamwambia hivyo kwa hasira akapigwa tena na mwanaume yule mpaka akadondoka chini. Grace alikuwa analia kwa hofu na kushindwa kupumua kwa utaratibu mzuri, mpaka akawa akihisi kichomi. Beatrice akaushusha mkono ulioshika bastola kutoka usoni mwa Grace huku akicheka kwa dharau sana. Alijiona kuwa mwenye nguvu mno na alifurahia sana kuona watu hawa wakiteseka.

"Such drama..." Beatrice akasema.

Dylan akawa anapumua kwa nguvu chini pale huku analia kwa hasira.

Beatrice akamwangalia kwa umakini sana, kisha sura yake ikageuka na kuwa serious, na papo hapo akainyanyua bastola na kufyatua risasi mbili bila kusita! Jaquelin akapiga kelele akiwa ameshtushwa sana na jambo hili. Dylan na Gilbert walitoa macho kwa taharuki kubwa, wakiwa kama hawaamini kilichotokea.



★★★★★★★★★★★

ITAENDELEA

★★★★★★★★★★★

WhatsApp +255 787 604 893
 
Beatrice wa visasi. Revenge time pasipo kuwa na cha kupoteza. Grace anakufa kizembe kabisa. Mungu asaidie Queen na Bosco wajue hili chimbo kabla kina Jaquiline hawajalambishwa shaba. Riwaya kali sana hii, halafu mkuu Elton Tonny una ngeli imenyooka sana. Hongera kwa utunzi mkali
 
Huyo ndio kubwa la maadui Beatrice, the one woman on herself acting briliantly; Sasa haoni haja ya kujificha tena, now anataka kile alichokifil tangia alipomuua mumewe alafu mwanae aliyempenda sana anataka na wengine wakifil in the same way. Tunaelekea kutamu zaidi
 
Beatrice wa visasi. Revenge time pasipo kuwa na cha kupoteza. Grace anakufa kizembe kabisa. Mungu asaidie Queen na Bosco wajue hili chimbo kabla kina Jaquiline hawajalambishwa shaba. Riwaya kali sana hii, halafu mkuu Elton Tonny una ngeli imenyooka sana. Hongera kwa utunzi mkali
👊 kula gwara. Shukran kwa pongezi zako mkuu
 
Huyo ndio kubwa la maadui Beatrice, the one woman on herself acting briliantly; Sasa haoni haja ya kujificha tena, now anataka kile alichokifil tangia alipomuua mumewe alafu mwanae aliyempenda sana anataka na wengine wakifil in the same way. Tunaelekea kutamu zaidi
Maneno mazuri sana. Kutamu ndiyo sehemu inapoelekea. Kesho naangusha dude kali 👐
 
DYLAN

Story by Elton Tonny

Familia, Kazi, Urafiki, Mapenzi, Tamaa, Hila, Unyanyasaji, Usaliti, Visasi, Mauaji, Mambo Yasiyotazamiwa

(R-rated 18+)

Enjoy!

★★★★★★★★★★★★★★★★★

SEHEMU YA AROBAINI NA TATU

★★★★★★★★★★★★★★★★★


"No... no... no.... Camila... no!" Gilbert akawa anaongea huku akilia.

Mwili wa Camila ulianguka chini baada ya risasi hizo kumpiga kifuani. Damu nyingi zilianza kumtoka na kusambaa kwenye nguo yake nyeupe iliyokuwa kwa ajili ya bibi harusi. Tena, Beatrice akawa ameua mtu asiyekuwa na hatia; kama kujifurahisha tu. Midomo ya Dylan ilianza kutetemeka sana akimwangalia shangazi yake kipenzi chini hapo, ambaye hakuwa na uhai tena. Grace alikuwa akilia sana huku mikono yake ikitetemeka kwa hofu kubwa, naye Jaquelin akawa analia pia huku akiiita jina la wifi yake.

Beatrice akapuliza tundu la bastola yake, kisha akasema, "Huyo hakuwa na faida yoyote kwangu. Angalau sasa wamebaki watakaoburudisha zaidi au siyo?"

Wanaume wake wakaanza kucheka.

Gilbert alilia sana. Dylan alishindwa hata kutoa sauti ya kilio na kubaki anadondosha tu machozi huku anautazama mwili wa Camila.

"Okay tuendelee. Mmmm... sijui nani afate sasa hivi. Jaquelin... Grace... kijacho... ohohohoh... kweli nikimuua Grace na kijacho anaenda... kwa hiyooo... nimpasue tumbo, nimtoe kijacho, halafu tupige selfie aliyokuwa anaitaka Dylan, then nimuue mama mbele ya kijacho... au huko nitakuwa nimepita mbali sana? Possibilities nyingi yaani dah..." Beatrice akaongea kwa dharau huku watu wake wakicheka kwa sifa.

"Beatrice... mdogo wangu alikukosea nini? Kwa nini umeamua kuwa mnyama kiasi hiki? Kama kuna mtu unataka kuua niue mimi! Kwa nini unawaumiza wengine..." Gilbert akaongea kwa huzuni.

"Don't be a p***y Gilbert! Nafikiri... itafaa sa'hivi tukipiga kura labda, au mnaonaje? Nitaanza na wewe Gilbert. Ungependa nani afate kati ya mkeo, au mpenzi wa mwanao? Mmm?"

Dah! Huyu mwanamke alichosha. Dylan akafumba macho kwa nguvu na kuanza kuivuta mikono yake kwa nguvu sana ili akate kamba. Zilikuwa ngumu mno kiasi kwamba mpaka akaichubua mikono yake akijaribu tu kuzikata, lakini akashindwa. Akapiga kelele za hasira huku analia kwa uchungu.

"Oooh... jomonii... usilie mtoto. Huo ni mwanzo tu," Beatrice akasema kikejeli.

"Boss..." Seba akamwita Beatrice.

"Usijali Seb, mapolisi hawawezi kuja sasa hivi hata kama wangesikia huo mlio. Hapa tutacheza mpaka chakunaku," akasema Beatrice.

"Ahahah... ahahahah...."

Wote waliokuwa hapo walianza kumshangaa Dylan, kwa sababu alikuwa anacheka.

"Well, well, well... naona show imeanza kukuingia vyema dogo," Beatrice akamwambia.

"Ahah... siyo kihivyo. Nilikuwa tu... nawaza... haya yote unayoyafanya, hivi David atataka tena kuwa na mama kama wewe?" Dylan akamuuliza.

Swali lake lilimfanya Beatrice akerwe kiasi.

"Nini?" Beatrice akauliza.

"Ahahah... fanya ufanyavyo... lakini ipo siku dogo atajua uliwaua dada yake na baba yake... na hawa watu wengine wote. Na hiyo siku ukiwa naye nimeshaiona yeye pia atafata... tena nafikiri kwa akili yako kama ya bata mzinga utachukua oven umwingize humo aive then awe ndiyo supper! Ukifika huo mlo usisahau kunialika..." Dylan akamwambia.

Wazazi wake, Grace, na hata wale wanaume walikuwa wakijiuliza alikuwa na tatizo gani. Walishindwa kumwelewa kwa sababu wakati huu ambao Beatrice alikuwa akijitahidi kumvunja moyo, yeye ni kama alizidi kuwa imara. Beatrice akamtathini kwa sekunde kadhaa. Aliwaza kijana huyu kuna kitu alikuwa anafanya zaidi ya kile ambacho alionekana anafanya. Mwanamke huyu alikuwa mwerevu sana kutambua kwamba kuna sababu iliyomfanya Dylan atende hivyo.

"Unajua... toka tulivyoanza kuongea... umekuwa ukijaribu tu ku.... unanipotezea muda!" Beatrice akasema baada ya kutambua hilo.

Dylan akawa anamwangalia kwa mkazo kutokea chini pale.

"Kwa nini unafanya hivyo?" Beatrice akamuuliza.

"Beatrice... tafadhali nakuomba umwachie Grace... anahitaji huduma...."

"Kaa kimya Gilbert! Wewe... niambie unapanga nini? Umejifungia bomu hapo? Au unawasubiri mapolisi? Niambie kwa nini unajifanya mjanja sana..." Beatrice akamwambia Dylan.

Alipoona Dylan amekaa kimya tu, akainyoosha bastola yake kuelekea kichwa cha Grace!

"Beatrice!" Gilbert na Jaquelin wakasema kwa hofu.

Dylan akawa anapumua kwa hofu pia.

"Sihitaji kura tena. Unafata sweetheart," Beatrice akamwambia Grace.

"No... don't..." Dylan akamwomba.

"Fine. Niue. Niue tu! Itakupa faida gani? Kwamba umeongeza namba za vifo kwenye ledger yako iliyojaa umwagaji damu? Go ahead... shoot me!" Grace akamwambia kwa hasira.

Kwake yeye ilikuwa imefikia "too much!" Beatrice akaikoki bastola yake akionyesha utayari wa kumtandika Grace risasi. Dylan, Gilbert na Jaquelin walikuwa wakiomba kwa sauti za juu kwamba Beatrice asifyatue risasi, na papo hapo mlio mkubwa wa risasi ukasikika!

Wote walishtuka sana, kwa sababu risasi hiyo ilikuwa imeipiga bastola ya Beatrice na kufanya aidondoshe pembeni. Yeye pamoja na wanaume wake pia walishangaa sana na kuangalia upande wa kuingilia jengoni humo, nao wakaweza kuwaona wanaume wanne wakiwa wanaingia; watatu wakiwaelekezea bastola na mwingine akiwa bila bastola. Dylan aliingiwa na matumaini baada ya kumtambua mwanaume huyo ambaye hakubeba bastola kuwa ni Bosco.

Beatrice aliduwaa! Akabaki kuwaangalia wanaume hao waliokuwa na miili mikubwa na wenye sura zisizotaka mchezo kabisa.

"Wekeni vyuma vyote chini! Mikono kichwani!" mmoja wao akawaamrisha wanaume wa Beatrice.

Wale wawili waliokuwa wamesimama pembezoni mwa Gilbert na Dylan wakaweka mikono yao vichwani kwa njia ya kujisalimisha, na wawili waliokuwa usawa wa Grace na mwili wa Camila wakafanya hivyo hivyo pia; ikionyesha hawakuwa na bunduki. Lakini yule aliyemshikilia Jaquelin akaendelea kumng'ang'ania na kutoa vitisho kwamba angemuua ikiwa wangeendelea kuwaonyeshea bastola namna hiyo, kwa hiyo eti wazishushe.

Baunsa huyu aliyekuwa ametoa amri kwa wanaume wa Beatrice akamwelekezea bastola jamaa huyo kwa makini sana na kufyatua risasi iliyompata kupitia shavu usoni! Wote walishtuka sana, kwa sababu alionyesha shabaha ya hali ya juu mno. Ni Beatrice na Seba peke yao ndiyo waliokuwa na bastola, hivyo Seba akaitoa yake taratibu huku akipiga mahesabu ya kufanya ujanja fulani.

"Tupa chini... usijifanye mjanja!" baunsa huyo akamwambia Seba.

Hakuwa na jinsi tena ila kutii kwa sababu bastola zote zilielekezwa kwake. Akairusha pembeni mwa jengo, na hapo hapo Bosco akamkimbilia Dylan ili kwenda kumfungulia kamba haraka. Wanaume wale walioingia na Bosco wakawaamrisha wanaume wa Beatrice walale chini upesi. Wote wakatii na kulalia matumbo yao huku mikono wakiwa wameiweka vichwani, wakimwacha Beatrice amesimama tu. Wanaume wawili waliokuwa pamoja na Bosco wakawafuata Grace na Jaquelin ili kuwafungulia kamba na wao pia, huku yule baunsa mmoja akimwelekezea Beatrice bastola. Jaquelin akamfata Grace na kumshika vizuri akimuuliza kama alihisi maumivu sehemu.

"Dylan pole sana bro... tumekutafuta sana... nilimtafuta Queen akakutrack lakini baadae tukakupoteza... nafikiri hawa walitupa simu yako kwo' Queen akatugawa ili tukutafute sehemu za karibu..." Bosco akawa anamwambia Dylan baada ya kumfungulia kamba na kuanza kumfungua Gilbert pia.

Dylan akasimama. Alikuwa anamtazama mtu mmoja tu... Beatrice. Beatrice alimwangalia Dylan kwa hofu sana, kwa sababu mwanaume alikuwa anamtazama kwa njia ya hasira nyingi mno. Hangeweza kumwacha salama mwanamke huyo aliyethubutu kumuua shangazi yake kipenzi na kutishia kumuua mtu aliyempenda sana, yaani Grace, hivyo alikuwa anawaza kumshika ili amfunze somo ambalo hangesahau.

Ile Dylan alipoanza kumfata Beatrice, akashtuka baada ya kuona kama mtu fulani anakuja taratibu nyuma ya yule mwanaume baunsa aliyekuwa amemwelekezea bastola Beatrice kutokea kule aliposimama. Lakini hakuweza kutoa onyo mapema kutokana na kumshangaa kiasi. Mviziaji huyo akamkaba mwanaume yule na kumwekea bastola kichwani, na kisha akaipiga pembeni sana bastola aliyoishika mwanaume huyo. Baada ya wote kumtazama kwa makini wakatambua ilikuwa ni Jafari.

"Nyie wawili tupeni bunduki zenu, la sivyo nampasua huyu kichwa!" Jafari akawaamrisha wale wenzake na baunsa huyo.

"Jafari... unafanya nini?" Grace akauliza kwa mshangao.

Kila mtu alishangaa sana.

"Mmenisikia? Zitupeni!" Jafari akafoka.

Wale wanaume wawili hawakutupa silaha zao, bali wakamnyooshea Jafari kwa ujasiri kabisa. Dylan akawa anamtazama Jafari kwa njia ya kawaida tu. Beatrice akatabasamu kiasi na kumwangalia Dylan kwa kiburi.

"Jafari... nini una..." Gilbert akasema.

"Ni yeye ndiye aliyetupiga vichwa wakati tuko nyumbani baba. Na yeye ni puppet wa huyu mwanamke!" Dylan akasema.

"Unbelievable!" Grace akasema kwa kushangaa sana.

"Sihitaji kuwaelezea chochote. Nyie wawili shusheni bastola zenu la sivyo nitamuua huyu! Nina mafunzo..." Jafari akanena.

"Kweli Jafari na yote tuliyofanya pamoja unaamua kunisaliti? Amekununua kwa shilingi ngapi huyu mwanamke?" Grace akamuuliza.

"Haikuhusu..." Jafari akamjibu.

Beatrice alikuwa anampa ishara mwanaume wake mmoja alielala chini kwamba aichukue bastola ile aliyoidondosha chini baada ya kuwa imepigwa na risasi muda ule. Ilikuwa imedondokea karibu na usawa wake, hivyo jamaa akawa anapiga hesabu za kuichukua upesi ili aitumie.

"Hainihusu? Kwa nini? Eeh? Sema Jafari! Ni nini ambacho hauja.... aah.... aaaah!"

Grace akiwa hajamaliza kuongea akaanza kutoa vilio hivyo. Wote walipomtazama, waliweza kuona kama maji yakitiririka kutokea katikati ya miguu yake na kumwagikia chini. Akalegea sana na kumfanya Jaquelin ampe egamio huku naye akihofia usalama wa Grace.

"Grace..." Dylan akaita kwa wasiwasi.

"Maii yamepasuka! Mtoto anakuja!" Jaquelin akaonya.

"Grace... Jafari... nahitaji... Grace..." Dylan akaanza kubabaika.

Hiki ndiyo kikengeusha fikira alichokihitaji mwanaume yule wa Beatrice pale chini. Akajiviringisha haraka na kuichukua bastola ile, kisha akamfyatua risasi ya ubavuni mwanaume mmoja kati ya wale wawili waliokuwa wameelekeza bunduki kwa Jafari. Jaquelin akapiga kelele huku akiwa bado amemshikilia Grace ambaye alikuwa akilia kwa kuhisi uchungu. Dylan na Beatrice wakainama chini, na wakati mwanaume yule alipotaka kumfyatua risasi yule mwanaume wa pili aliyekuja na Bosco, Gilbert akamwahi na kumrukia mkono ulioshika bastola na kufanya ipige risasi kwenye paja la mwanaume huyo, hivyo bastola ya mwanaume huyo ikadondokea pembeni. Bosco akamfata Gilbert pia ili amsaidie kumdhibiti mwanaume huyo.

Mwanaume ambaye alikuwa amekabwa na Jafari akajitoa kwa nguvu mikononi mwake na kuanza kupigana naye, lakini Jafari akamzidi ujanja na kumfyatua risasi ya kifua na kufanya adondoke chini. Ile Jafari anatazama juu akakutana na teke la tiki-taka kutoka kwa Dylan, ambaye aliwahi upande wake haraka sana. Jafari akaweweseka na kurudi nyuma, kisha akataka kumwelekezea Dylan bastola ili ampige na yeye risasi lakini kwa mtindo wa sarakasi Dylan akawa amemrukia na kuutandika mkono huo kwa teke; hivyo bastola ya Jafari ikadondokea pembeni.

Wakati Gilbert na Bosco walipofanikiwa kumdhibiti mwanaume yule pale chini, Gilbert akampatia bastola ile Bosco na kumwambia amchunge ili yeye akatoe msaada kwa Grace, lakini ni hapa hapa ndipo Beatrice alikuwa ameshaiwahi bastola ile iliyodondoka ya yule mwanaume aliyepigwa risasi pajani. Dylan sasa alikuwa anamchangamkia Jafari kwa kumtandika ngumi zisizo za kitoto kutokana na hasira kali aliyokuwa nayo kumwelekea kwa sababu ya usaliti wake. Lakini Jaquelin akamwita kwa sauti ya juu kumkumbusha kwamba Grace alihitaji sana msaada, hivyo Dylan akaona aachane na Jafari kwa kuwa alikuwa ameshadebweda balaa.

Ni wakati amegeuka ili amfate Grace upesi, pale alipoona mkono wa Beatrice ulioshika bastola ukiwa umemwelekea baby mama wake. Akatoa macho na kuanza kukimbia haraka ili akamzibe, lakini akawa amechelewa. Beatrice alifyatua risasi kumwelekea Grace, akiwa amelilenga tumbo lake kabisa! Mshtuko ulikuwa ni mkubwa kwa Dylan baada ya kusikia mlio huo wa risasi kiasi kwamba hata hakuona mambo vizuri, lakini baada ya Beatrice kuwa amefyatua hiyo risasi papo hapo sauti za juu za milio ya risasi zikazidi kusikika tena. Risasi kumi na mbili!

Hakuna aliyeelewa kilichoendelea mpaka wote walipomtazama Beatrice na kukuta akiwa ametobolewa-tobolewa mwilini kwa risasi nyingi, na mwili wake ukadondokea chini kwa kishindo baada ya kula risasi kumi na mbili *****! Dylan, Bosco, Jafari, na wanaume wale waliobaki pale chini wote walitazama kutokea upande wa kuingilia kwenye jumba hilo, na hapo wakaweza kumwona, si mwingine, ila Queen mwenyewe! Alikuwa ameelekeza bastola upande ule alipodondokea Beatrice, na wote wakatambua kwamba ilikuwa ni yeye ndiye aliyemtandika risasi hizo zote.

Dylan aliangalia upande wa mama yake na Grace, na hapo akaweza kuona kama mtu fulani akiwa amewakumbatia Jaquelin na Grace. Kwa haraka akatambua kwamba ilikuwa ni Gilbert, baba yake, naye Dylan akanyanyuka na kwenda hapo upesi. Gilbert alikuwa na tundu la risasi nyuma ya mgongo wake, na hii ikamwambia Dylan kwamba wakati Beatrice alipofyatua risasi ile kumwelekea Grace, baba yake alijiweka hapo ili impige yeye badala. Alihuzunika sana.

Grace bado alikuwa anaugulia maumivu ya uchungu mwingi sana uliokuja kabla ya wakati mwafaka, naye Jaquelin alikuwa akilia sana kwa sababu mume wake alikuwa hoi na risasi mgongoni. Dylan akashindwa afanye nini. Ajigawe vipi? Wanaume kadhaa wakaingia, wakiwa ni watu wa Queen, nao wakawafuata pale na kuanza kutoa msaada, huku wengine wakiwadhibiti wale wanaume wa Beatrice. Bosco akasaidiana nao ili wambebe Grace na kumwahisha kwenye gari apelekwe hospitali upesi.

Jaquelin akabaki chini hapo akiwa amemshikilia Gilbert, ambaye sasa hakuwa hai tena. Alikuwa akilia kwa uchungu mwingi sana, naye akawa anamwambia Dylan aende hospitali tu kwa sababu Grace angehitaji awepo kule. Dylan akanyanyuka na kusimama, akiwa ameghafilika sana, na hapo Queen akaja nyuma yake na kumshika begani.

"Queen..." Dylan akashindwa kuongea zaidi.

"Its okay. Go. Nitakuwa pamoja nao," akamwambia Dylan.

Dylan akaanza kuondoka upesi kuwahi kwenye gari lile walilompeleka Grace, na baada ya kufika akaketi karibu yake, nalo likaondolewa hapo ili kuwahi hospitali. Jaquelin akabaki tu anamlilia mume wake kwa huzuni, akihisi kama vile mambo haya yote ni ndoto. Queen akapiga simu polisi na kuwaambia kuhusiana na tukio hilo hapo. Akahakikisha Jafari na wale wanaume wengine wamefungwa vizuri sana hapo, naye akachuchumaa karibu na Jaquelin na kumtazama kwa makini.

"Najua huu ni wakati mgumu kwako, lakini mapolisi wakifika...."

"Usijali.... hhhh... najua la kufanya..." Jaquelin akamkatisha Queen huku akiwa bado analia.

Queen akatikisa kichwa taratibu kuonyesha ameelewa. Kwa kuwa hakutaka kujionyesha kwa mapolisi ambao bila shaka wangeanza kumfatilia-fatilia, akaondoka haraka na kumwachia Jaquelin walinzi wake wawili kabla ya mapolisi kufika.

Grace alifikishwa hospitali baada ya dakika kadhaa, na kufikia wakati huu alikuwa akitokwa na damu kwa sababu ya mkazo mwingi aliopitia siku hiyo. Wakamwahisha kwenye chumba cha dharura, nao madaktari wakaingia ili kuanza kutoa msaada haraka. Bosco alikuwa pamoja na Dylan, akimtia moyo kuwa kila jambo lingekwenda sawa tu, ijapokuwa Dylan alikuwa amepasuka sana moyo. Alikuwa analia mno. Baraka, Harleen, Matilda, Camila, baba yake, na wengine wote Beatrice aliowaua kikatili ni mambo yaliyomfanya augue sana moyoni mwake, hasa kwa kuwa aliona sababu ilikuwa ni yeye. Hakutaka kumpoteza na Grace, wala mtoto. Hivyo ndiyo kati ya mambo yaliyobaki ambayo yangempa nguvu ya kusonga mbele, kwa hiyo kama angewapoteza, basi angekata tamaa ya maisha.

Baada ya muda fulani, daktari akatoka kwenye chumba kile, naye Dylan pamoja na Bosco wakamfuata huku Dylan akiuliza hali ya Grace na mtoto. Daktari akashusha pumzi, kisha akamshika Dylan begani kwake.........


★★★★★


MIAKA MINNE BAADAE.....


"Harakisha bwana, muda umeenda!" akasema Shani.

"Mama usikonde, mambo yako fresh hata kama nikikawia dakika 20 bado watakuwa hawajafika," Steven akamwambia mama yake.

"Yaani kweli nimewezaje kusahau kumnunulia Yogurt... na alishaniambia kanapenda kweli!" Shani akasema.

"Steven kimbilia haraka sasa..." Leila akamwambia mdogo wake.

Steven akatoka upesi kwenye nyumba yao na kuelekea dukani.

"Okay wali, nyama, tambi, chips, marage, njegele, kuku, soseji, juisi na...."

"Mama jamani kila kitu kiko sawa. Ni Yogurt kwa ajili ya dogo tu ndiyo imekosekana... Steven anaiwahisha... hapa kila kitu kiko safi wakifika ni kujinoma tu," Leila akamwambia mama yake.

"Sawa. Hawatachukua muda mrefu, me naenda kujiandaa," akasema Shani, na kisha kuelekea juu chumbani.

Hii ilikuwa ni siku nzuri sana kwao kwa kuwa walikuwa na wageni muhimu ambao waliwasubiri kwa hamu sana. Shani ndiye aliyeonyesha furaha kubwa kwa kuwa alitazamia kwa hamu sana wageni hao wapendwa wafike, hivyo vyakula viliandaliwa kwa kila aina ya ufundi wanaojua wanawake wazoefu kwenye mapishi. Bado walikuwa kwenye nyumba yao hii mpya iliyokuwa ya familia ya Gilbert kipindi cha nyuma, na kufikia wakati huu palikuwa pamebadilika haswa na kupendeza hata zaidi kwa mazingira yake.

Kufikia kipindi hiki, Shani alikuwa amefungua mgahawa mzuri jijini huku, naye Leila alikuwa ndiyo msimamizi mkuu wa Dy-Foods Restaurant, ule mgahawa wa Fetty. Fetty yeye aliondoka kwenda kuendelea na masomo zaidi, hivyo alikuwa ameuacha mgahawa wake chini ya uangalizi muhimu wa Leila, ambaye pia alikuwa rafiki yake sana wakati huu. Hakuubadili jina mgahawa huo kwa kuwa "Dy-Foods" ingemkumbusha sikuzote alikotoka na mtu muhimu aliyempatia fursa hiyo ya kuumiliki. Steven alikuwa mkubwa sasa, mwenye miaka 16, akiwa kidato cha nne.

Baada ya Steven kuwa amerudi na vile alivyoagizwa, wote wakakaa kwa utayari wakiwasubiri wageni wafike. Hazikupita dakika nyingi sana nao waliweza kusikia 'horn' mbili za gari nje ya geti, naye Steven akatoka upesi kwenda kulifungua. Shani na Leila walitoka mpaka usawa wa sehemu pana pale nje ya kuegeshea magari na kusimama, wakiwa wanatazama kwa hamu getini. Baada ya Steven kufungua geti, likaingia gari ndani hapo, aina ya Range Rover SV Luxury 2022, lenye rangi nyeusi, lililokuwa linangaa kama ndiyo limetoka dukani!

"Aisee! Cheki gari hiyo..." Leila akamwambia mama yake.

"Inaonekana ya gharama," akasema Shani.

"Sana."

Gari likaingia moja kwa moja mpaka sehemu ya kuegeshea, kisha Steven akafunga geti na kuanza kuelekea upande huo wa gari. Mlango wa nyuma ulianza kufunguka, kisha akashuka mwanamke ambaye walimfahamu vizuri sana. Shani na Leila wakaanza kumfata huku naye akiwaelekea na tabasamu la furaha.

"Wow... jamani Jaquelin!" Shani akasema kwa furaha.

"Shani mpenzi, za siku nyingi?" akasema Jaquelin akiwa amemfikia na kumkumbatia.

"Safi tu. Yaani jamani... karibu sana mpendwa," Shani akasema.

"Asante dear," Jaquelin akamwambia.

Leila akamsalimu Jaquelin vizuri naye akamwitikia. Ni hapa ndipo wakawaona wengine kutokea kwenye gari wakija upande wao pia, nao wakafurahi sana.

"Kaka Dylan!" Steven akaita kwa furaha.

"Steven huyo! Vipi jembe?" Dylan akamsalimu pia na kugongesha kiganja chake kwake alipomkaribia.

"Wow! Dylan... Grace jamani!" Shani akawafata na kumkumbatia Grace kwa upendo.

"Hee! Kaone na haka!" akasema Leila.

Ndiyo. Ilikuwa ni Grace na Dylan, wakiwa na mtoto wao mdogo wa kike. Leila akambeba msichana huyo na kuanza kuchezea mashavu yake makubwa. Kalikuwa kanakula pipi tu huku kakiwa hakaelewi somo! Kalikuwa kazuri sana kama mama yake. Na kalipendeza mno kwa gauni la rangi ya pink na viatu vyeupe vilivyowakawaka kila wakati ambapo kangekanyaga chini. Nywele zake zilikuwa ndefu na laini, nazo zilisukwa kwa mtindo fulani kama rasta.

Grace huyo! Alikuwa amefanikiwa kujifungua msichana huyu usiku ule ambao ulikuwa wenye kuhofisha sana aliowahi kupitia kwenye maisha yake. Sasa alikuwa mama, na mke wa Dylan. Walifunga ndoa mwaka mmoja uliopita wakati binti yao alipokuwa na miaka mitatu, nao wakaendelea na maisha mazuri yaliyojaa upendo mwingi sana na furaha. Baada ya ndoa yao walikwenda fungate (honeymoon) la muda mrefu sana pamoja na binti yao huyu nje ya nchi, kule Indonesia, nao wakaendelea kukaa huko kwa miezi mingi mpaka waliporejea nchini tena wiki moja iliyopita kufikia siku hii.

Hapa sasa ndiyo walikuwa wamekuja kuwatembelea marafiki zao wapendwa baada ya kutoonana kwa kipindi hicho chote. Grace alikuwa amevaa gauni refu la rangi ya maziwa lenye urembo wa maua maua, lililokuwa na mpasuo mrefu pia kufikia pajani, na miguuni akivaa viatu vidogo vya matembezi. Usoni alipendeza sana pia na kuonekana kama mwanadada wa umri mdogo tu, na nywele zake alikuwa amezisukia kwa "weaving" la nywele za kizungu lililofanya aonekane kama mmarekani mweusi. Pesa hizo! Dylan pia alikuwa amependezea kwa kuvaa shati nyepesi yenye maua-maua na suruali nyeusi ya jeans, pamoja na sneaker kali nyeupe.

"Jamani mashavu! Hujambo? Eeh? Amekua!" Shani akawa anamsemea mtoto.

"Nakwambia kagoma kukaa na mimi eti anamtaka mama yake tu... nimemwambia nimemgaya," Jaquelin akasema, na wote wakacheka.

"Halafu jina lake huwa linanitoka jamani. Nakumbuka ni gumu kweli..." akasema Shani.

"Siyo hata gumu, ni uzee wako tu," Steven akamwambia mama yake, na wote wakacheka.

"Katoto, eti waitwa nani? Eeh? What is your name?" Shani akawa anamuuliza mtoto.

Kenyewe kakawa kanamwangalia tu huku kanamumunya pipi.

"Ni nani kweli? Me mwenyewe limenitoka..." akasema Leila.

"Marcelyn," akajibu Grace.

"Wow! Zuri kweli," akasema Leila.

"Jamani karibuni ndani..." Shani akasema.

"Asante. Pamebadilika sana huku. Tokea mara ya mwisho nimefika..." Jaquelin akawa anasema.

Wote wakaelekea ndani huku wakiongea kwa furaha. Walifika na kuketi pamoja kwenye masofa na kuongea kwa ufupi, kisha Leila akawakaribisha mezani ili waweze kupata chakula pamoja. Muda wote Shani na wengine waliojaribu kumsemesha Marcelyn, dogo alikuwa haongei chochote ila kufanya tu michezo yake ya kitoto bila kujali muda! Wakakaa naye mezani tayari kwa ajili ya kula huku wakifurahia maongezi.

"Eti jamani... yaani mbali kote kule! Mgeenda hata pale Ushirombo kuna sehemu nzuri za kutembelea," akawa anasema Steven, na wote wakacheka.

"Ushirombo pazuri eeh?" akauliza Grace.

"Acha! Indonesia hapaoni ndani," akajibu Steven.

"Tutakuja kumpeleka Celyn apaone... ole wako sa' nikute ni msitu tu," Dylan akamwambia Steven kiutani.

"Huko Indonesia ni pazuri sana?" akauliza Leila.

"Ndiyo kuna sehemu nyingi ni nzuri sana. Kuna mahoteli na vivutio vya watalii wengi," akasema Grace.

"Kule wanaongeaga kiingereza kwani?" akauliza Shani.

"Kwa wageni wanaofika kwenye hoteli kama hizo kiingereza ni must, baada ya kuzoea hapo inategemea na mnakaa muda gani unaweza hata kujifunza lugha yao," akasema Dylan.

"Mpe Shani zile picha... mwonyeshe," Jaquelin akamwambia Grace.

Grace akachukua simu yake na kutafuta picha za sehemu waliyokaa kule Indonesia na kumpatia Shani atazame. Leila na Steven pia wakawa wanaziangalia.

"Eh! Pazuri sana!" akasema Shani.

"Ahahahah... kaone ka Meriselin hapo kanarukaruka," akasema Steven.

"We naye unaharibu jina la mtoto afu' ulikuwa unasema mama mzee kumbe we ndo' kibabu!" Leila akampa ukweli, na wote wakacheka.

"Panaitwaje? Hii hoteli yaani mliyokuwepo na eneo lake?" Shani akauliza.

"Ni villa... hoteli kubwa yaani... inaitwa Kamuela Seminyak, kule Bali," akajibu Grace.

"Bonge la jitu!" akasema Steven.

"Tuambieni mlifanya mambo gani huko..." akasema Leila kwa shauku.

"Mh! Vitu vingi sana. Tulitembelea beach nyingi za kule, kuogelea baharini, kujifunza tamaduni zao... na nyingi ni nzuri sana. Tulifanya matembezi kwa helicopter... yaani mambo mengi sana..." akawa anasema Dylan.

"Ahahahah... mara ya kwanza Celyn amepanda helicopter alimng'ang'ania baba yake mpaka kidogo amchanie shati!" Grace akakumbushia, nao wote wakacheka.

"Hadi raha. Na sisi tutaenda siku moja," akasema Steven.

"Ndiyo mtaenda tu," akasema Dylan.

"Lazima ilikuwa pesa ndefu sana kukaa muda wote huo huko..." akasema Leila.

"Ndiyo. Sema kuna extradi...."

"Mommy..." Marcelyn akamkatisha Grace.

"Yes darling?" akaitika.

"I want pizza," kakasema.

Wote wakawa wanakaangalia huku wanatabasamu.

"You want pizza? Okay. Finish this first, then we'll get some pizza, alright? (unataka pizza? sawa maliza hii kwanza, halafu tutafata pizza eti?)" Grace akamwambia.

"Okay," kakakubali na kuendelea kula soseji.

"Wacha! Amekuelewa!" Steven akasema.

"Ahahahah... ndiyo," Grace akajibu.

"Kaka Dylan, Indonesia inanihusu. Nataka nami nikirudi nisijue kiswazi hata chembe, yaani itasaidia mama asiwe ananisemesha kabisa!" Steven akatania, nao wote wakacheka.

Waliendelea kufurahia chakula, na baada ya kumaliza wakaanza kuongea mambo mengi hata zaidi.

Baadae wakubwa wakawa wameketi pamoja kwenye masofa, huku Steven akiwa na Marcelyn sehemu ya chini pembeni akicheza pamoja naye. Shani akawa anaongelea kuhusu maisha yao huku tokea Dylan na Grace walipoondoka, akigusia jinsi yeye na Jaquelin walivyokuwa mashosti haswa. Akamzungumzia na Emilia pia, ambaye sasa alikuwa chuo kikuu akisomea udaktari.

"Emilia ni smart sana kama mimi tu mama yake," Shani akawa anasema.

"Kweli," Leila akaongea kwa njia ya kejeli.

Dylan na Grace wakatabasamu.

"Muda unapita haraka sana," akasema Jaquelin.

"Yeah," Dylan akakubali.

"Vipi kuhusu David? Yule kijana yuko wapi siku hizi?" akauliza Grace.

"Nasikia yuko kule Nairobi. Aliachiwa fortune kubwa na mama yake kwa hiyo he's living the life," akasema Jaquelin.

"Atakuwa mkubwa sasa hivi," akasema Grace huku anamwangalia Dylan.

"Ndiyo, hajamwacha sana Steven," Jaquelin akasema.

Wote wakawa kimya kwa ufupi, wakimtazama Marcelyn akicheza.

"Unajua... huwa natamani sana... Baraka na Gilbert wangekuwepo kuiona hii siku," akasema Shani kwa hisia.

"Wanaiona. Wao ndiyo wanatuangalia kutoka juu," akasema Jaquelin.

"Ndiyo," akasema Grace.

"Ahah... inaonekana mama siku hizi ameanza kusoma Bible," Dylan akatania.

"Ahahahah... hakuwahi kuisoma kwani?" akauliza Shani.

"Walikuwa wananisema sana huyu na baba yake ikabidi nianze," akasema Jaquelin.

"Umeimaliza?" akauliza Shani.

"Nilisoma kama mistari miwili hivi... mpaka leo sijagusa tena..."

"Haya sasa..." akasema Dylan, nao wote wakacheka pamoja.

Dylan alikuwa amekaa karibu na Grace huku mke wake huyo akiwa amemwegamia kidogo, lakini sasa akajitengeneza vizuri na kuweka mkao uliowaambia wanawake hao kuwa alitaka kusema jambo fulani la muhimu, hivyo wakamwangalia kwa umakini.

"Kuna vitu huwa vinakuja na kwenda... kama vile muziki fulani mzuri ukiingilia kipindi fulani unakuwa bonge la buzz, lakini baada ya muda mwingine unakuja na kuufunika..." akaanza kusema.

"Ahahah... ndiyo ni kweli," akasema Leila.

"Ila kama ni kitu fulani kisichofunikwa hata kama muda mrefu utapita kadiri gani... ni upendo wa mzazi kwa mwanaye. Kuna jamaa aliwahi kusema, 'huwa hatujui kikamili upendo wa mzazi mpaka na sisi watoto tukija kuwa wazazi pia...'"

"Ndiyo... kweli kabisa..." Shani akakubali.

"Yeah... kwa hiyo ingawa hata hatutaweza kuonana tena na wazazi, au wapendwa wetu... upendo wao kwetu ni kitu ambacho hakitaweza kamwe kufutika wala kusahaulika. Baba, aunt Camila, na Baraka... wote tuko nao bado... kwa kuwa wataendelea kuishi mioyoni mwetu milele. Mambo yote yaliyotokea, mazuri na mabaya, yametufikisha sisi sote kwenye wakati huu. Kwa hiyo tunapaswa kuendelea kuishi kwa kushukuru juu ya kila zawadi Mungu alizotupatia, na kujitahidi kuonyesha upendo mwingi hata zaidi kwa wenzetu..." Dylan akaongea kwa busara.

"Uko sahihi Dylan," akasema Jaquelin.

Grace akatabasamu na kusema, "Maneno mazuri love... asante sana. Zawadi kubwa tuliyonayo ni uhai, na pia..."

"Marcelyn hahahah..." akamalizia Shani.

Wote wakatabasamu kwa furaha na kumwangalia mtoto. Yeye pia alikuwa amegeuka na kuwaangalia baada ya kusikia jina lake likitajwa na Shani, hivyo wakaanza kumsemesha. Dylan na Grace wakashikana viganja vyao kwa upendo na kumtazama binti yao huku wanatabasamu, naye Marcelyn akatabasamu pia kwa furaha.



★★★★★★★★★★★★

MWISHO

★★★★★★★★★★★★
 
Dah...ahsante sana kwa kutupa burudani kali hii, ambayo ingetengenezewa tv show kabisa na kuwa kali kuliko hizi tunazoziona kwenye local tv na maisha magic bongo. Hongera sana mkuu Elton Tonny kwa muda wako na kwa kutuburudisha kupitia kipaji chako. Ubarikiwe
 
Dah asante sana kaka bonge la Stori mafunzo ya kutosha ila Fetty kama bado hajaolewa mwambie natafuta mke maana anaonekana ni wife material af bonge la pic...
 
Dah...ahsante sana kwa kutupa burudani kali hii, ambayo ingetengenezewa tv show kabisa na kuwa kali kuliko hizi tunazoziona kwenye local tv na maisha magic bongo. Hongera sana mkuu Elton Tonny kwa muda wako na kwa kutuburudisha kupitia kipaji chako. Ubarikiwe
Shukran kwako pia kwa kuwa nami tokea mwanzo
 
Dah asante sana kaka bonge la Stori mafunzo ya kutosha ila Fetty kama bado hajaolewa mwambie natafuta mke maana anaonekana ni wife material af bonge la pic...
Nimeshamcheki kwa sms kumwambia kuna jibwa huku lina njaa naye kwo atoke huko upesi sana 😂
 
Back
Top Bottom