Simulizi: Harakati za Jason Sizya

Simulizi: Harakati za Jason Sizya

taharuki..jpg

297

Hata hivyo, ilionekana pia kundi hili lililokuwa na watu ndani ya Serikali ya Msumbiji waliotumika kutaka kuvuruga uhusiano mzuri uliokuwepo kati ya Tanzania na Msumbiji, uhusiano ulioasisiwa na Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere na mwasisi wa chama cha kupigania uhuru wa Msumbiji, ‘FRELIMO’, Eduardo Chivamba Mondlane tokea mwaka 1962, kisha uhusiano huo ukatiliwa nguvu na Rais wa kwanza wa Msumbiji, Samora Machel.

Kwa taarifa hizi Idara ya Usalama la Taifa iliamua kuweka utaratibu na kugawana malengo ya kushughulikia. Ili kurahisisha mizunguko ya mjini na ufuatiliaji wa ‘leads’ nyingi kwa wakati mmoja, wakuu walikubaliana kukipanua zaidi kikosi kazi na kukigawanya katika makundi mengine madogo madogo ya utendaji.

Kila kundi lilikuwa na maofisa kumi na mbili waliotoka Idara ya Usalama wa Taifa (TISS), Idara ya Upelelezi wa Makosa ya Jinai (CID), Kikosi cha Siri cha Ulinzi (SS) na Idara ya Ujasusi ya Jeshi la Wananchi wa Tanzania (MI).

Kisha kila kundi lilipaswa kupewa magari maalumu mawili hadi matatu ambayo serikali ilikuwa mbioni kuyakodi, kwa msaada wa nchi marafiki, kutoka mawakala mbalimbali jijini Dar es Salaam, yakiwa na namba za kiraia. Baada ya mgawanyo wa vikundi kukamilika, maofisa walipaswa kugawana majukumu kulingana na mkakati wa utendaji.

Hata hivyo mgawanyo huu usingeliathiri kundi letu la ‘Nge’ lililokuwa na jukumu la kufuatilia mawasiliano yote yaliyofanywa na watuhumiwa, kuanzia mawasiliano ya simu za mkononi, barua pepe na hata account zao kwenye mitandao ya kijamii. Kwa jinsi tukio lilivyofanyika, tulikuwa na kila sababu ya kuamini kwamba wahusika walikuwa na mtandao mkubwa, uliohusisha washiriki na wafadhili walioko nje ya nchi, na walikuwa na mawasiliano ya kila aina.

Kwa kuwa sikuwa nimeshiriki kwa ukaribu zaidi kwenye shughuli za kundi langu la ‘Nge’ kutokana na jukumu zito nililopewa, Tunu alinifahamisha kuhusu hatua kubwa iliyokuwa imepigwa na kundi letu katika kufuatilia kwa umakini kumbukumbu zote za simu zilizopigwa ndani na nje ya nchi katika kipindi cha miezi mitatu iliyokuwa imepita na jumbe mbalimbali zilizotumwa kwa njia ya simu na intaneti.

Tunu pia alinionesha taarifa ya awali aliyokuwa ameipata ya kundi la pili lililojulikana kama “Spider” (Buibui) ambalo maofisa wake walitakiwa kufanya uchunguzi wa haraka wa eneo la tukio kabla halijavurugwa, na kupata maelezo ya mashahidi kabla hawajatoweka na kuiwasilisha taarifa hiyo kwenye task force. Kiukweli kundi hili lilikuwa limepiga hatua kubwa katika uchunguzi wao. Walijigawa katika makundi mawili, moja lilifuatilia majeruhi waliolazwa katika hospitali za Muhimbili, Mwananyamala na Agakhan kwa ajili ya matibabu.

Waliwahoji, wakachukua maelezo yao kwa kufuata taratibu za kisheria na kuwatambua wale waliokuwa na taarifa muhimu ambazo zingeweza kusaidia katika upelelezi. Kwa vile wengi wa majeruhi hao walikuwa wameshatambuliwa, na taarifa zao kuchukuliwa muda mfupi baada ya mlipuko kazi ya kuwapata ilikuwa rahisi.

Wengi wa watu hao hawakuwa na maelezo mengi kwani walishitukizwa na mlipuko kiasi kwamba hawakujua ni kitu gani hasa kilichotokea. Hata hivyo baadhi yao waliweza kueleza kwa ufasaha hali ilivyokuwa. Mmojawapo wa watu waliokuwa na kumbukumbu nzuri ya tukio hilo ni mzee Julius Mhilu, mwandishi mkongwe wa riwaya na mwongozaji wa filamu aliyekuwa katika harakati za kugombea daladala la kueleka Tabata.

Katika maelezo yake mzee Mhilu aliwaeleza maofisa wa kikosi kazi kwamba, wakati akigombea daladala la Tabata lililokuwa jirani la jengo la Alpha Mall, ghafla aliona mwanga mkali kama wa radi ambao ulifuatiwa na muungurumo mkubwa ulioambatana na vumbi, vipande vya vioo na vitu vinginevyo vilivyorushwa kwa nguvu.

Vitu hivyo vilimpiga na kumchana sehemu ya kifua chake na mikono aliyokuwa ameitumia kujiziba uso wake. Kwa sekunde kadhaa aliduwaa asijue la kufanya na alipopata fahamu alijiona akiwa chini, damu imetapakaa kila mahali. Alipoangalia vizuri alimwona kila mtu aliyekuwa eneo lile akivuja damu.

Kikosi kazi pia kilimhoji Adam Chande, mmiliki wa duka la nguo (Kidoti Boutique) ambaye alieleza kuwa wakati wa tukio, yeye pamoja na mkewe Halima walikuwa wanafika katika eneo hilo.

Wakati anakunja kona ili kuingia mtaa ambao jengo la Alpha Mall lilikuwepo, akiwa umbali wa mita kama thetathini hivi, ghafla ulitokea muungurumo mkubwa uliopasua vioo vya gari lake na kuvisambaza ndani ya gari. Alipotazama kwa umakini mbele yake kuona nini kilichotokea, alishituka kuona damu ikimminika.

Alipomtazama mkewe akamwona akiwa amepatwa na mshtuko mkubwa na kupoteza fahamu na alikuwa amejeruhiwa eneo la usoni na kifuani. Kwa sekunde kadhaa aliendelea kusikia mfululizo wa miungurumo mingine midogo dogo iliyofanana na milio ya bunduki. Baadaye alitambua kuwa milipuko hiyo ilisababishwa na kupasuka kwa matairi ya magari yaliyokuwa yakiungua kwenye maegesho ya magari nje ya jengo lile. Kwa vile majeraha aliyopata hayakuwa mabaya sana, Adam Chande aliweza kuwasaidia wengine waliojeruhiwa.

Mtu mwingine aliitwa Sarah Hillary, ambaye alikuwa mhudumu mgahawa wa kisasa wa Nuru Café uliokuwa kwenye ghorofa ya pili ya jengo lile. Sarah alikieleza kikosi kazi kuwa kupona kwake ulikuwa muujiza mkubwa kwani mlipuko wa bomu ulimfanya apoteze fahamu kabisa na alipozinduka alijikuta akiwa amefunikwa na kifusi, huku mwili wake ukiwa umelowa kitu kinachofanana na Mafuta.

Sekunde chache baadaye alipata fahamu vizuri na kutambua kuwa yale hayakuwa mafuta bali ilikuwa damu iliyochanganyika na vumbi la kifusi. Wakati akihangaika kujiinua ndipo watoa msaada walipofika na kuondoa kifusi kilichokuwa kimemfunika yeye na wenzake.

Akiwa anapelekwa kwenye gari la wagonjwa, Sarah aliona vipande vya nyama na viungo vya watu vilivyosambaa kila mahali hali iliyomfanya asite kukanyaga eneo hilo na alipoangaza zaidi alimwona bosi wake, meneja wa mgahawa huo akiwa ameungua mwili mzima.

Mtu mwingine aliyehojiwa na kikosi kazi aliitwa Halima Mlacha, mmoja wa wanasheria wa kampuni ya Kitomari Advocates iliyokuwa na ofisi zake ndani ya jengo la Alpha Mall. Halima alieleza kuwa dakika takriban kumi kabla ya mlipuko alitoka kwenda kununua chakula kwenye mgahawa mmoja uliokuwa katika jengo la Makumbusho Plaza baada ya kugundua kuwa alikuwa hajala.

Mara tu baada ya kununua chakula hicho, Halima alianza kurudi kwenye lile jengo taratibu lakini kabla hajaenda zaidi akasikia mlipuko mkubwa uliotingisha kila mahali. Kwa sekunde kadhaa alijikuta amebutwaa asijue kilichotokea; lakini ghafla akaona moto mkubwa ukiwaka kwenye jengo la Alpha Mall. Alishitushwa sana kuona jengo likiporomoka na magari yakiungua moto huku na damu nyingi ikitapakaa na viungo vya binadamu vikiwa vimesambaa kila mahali.

Maelezo yalikuwa mengi kwani kikosi kazi hiki pia kiliwahoji mamia ya watu wengine waliokuwepo katika eneo la tukio. Watu walioonekana kuwa na taarifa za maana waliorodheshwa na kupangiwa siku ya mahojiano. Kwa vile wengi wa watu hao bado walikuwa katika hali mbaya ki afya, yaani kimwili na kisaikolojia, hivyo iliamuliwa kuwa mahojiano ya pili yakafanyikie kwenye makazi yao au mahali pengine ambapo wangejisikia huru kuzungumza kwa uhuru, bila hofu.

Endelea...
 
taharuki..jpg

298

Kundi lingine lililokuwa na wataalamu wa uchunguzi wa milipuko (Bomb Squad – Evidence Response Team) na wachunguzi wa eneo la tukio (Forensic experts), kati yao walikuwepo wataalamu watatu waliokuwa wamebobea na wenye uzoefu mkubwa katika medani hiyo, wakiongozwa na Ofisa Usalama wa Taifa, Sunday Msuya, lilifanya uchunguzi wa kina katika eneo la tukio.

Sunday Msuya aliyewahi kushiriki kikamilifu katika uchunguzi wa mlipuko wa bomu uliotokea mwaka 1998 katika ubalozi wa Marekani jijini Dar es Salaam, chini ya vikosi vya Marekani, alikuwa mbobevu, mwenye elimu na uzoefu wa hali ya juu katika kazi za kijasusi.

Licha ya kushiriki katika operesheni nyingi ndani ya nchi pia alikuwa amefanya kazi katika nchi kadhaa za nje na kukamilisha malengo ya Idara ya Usalama wa Taifa kwa ufanisi mkubwa. Sunday Msuya alikuwa na uzoefu wa zaidi ya miaka therathini katika Idara, muda uliomwezesha kujiwekea rekodi nzuri sana ya utendaji bora.

Chini ya Sunday Msuya ilikuwa rahisi kiasi fulani kwa maofisa wa kundi hili kuchunguza mlipuko kwa kuwa maofisa wengi wa Idara Usalama wa Taifa na wale wa Idara ya Ujasusi Jeshini, wakati mafunzo, hufundishwa namna ya kutengeneza na kutumia mabomu madogo kwa kutumia vitu vinavyopatikana nyumbani… na katika somo la ulinzi wa viongozi pia hufundishwa kukagua na kutambua mabomu ya kutegwa katika vyombo vya usafiri na majengo, na njia rahisi ya kuyategua.

Lakini kwenye uchunguzi wa milipuko mikubwa kama huu uliotokea kwenye jengo la Alpha Mall maofisa wengi hawakujua lolote la maana zaidi ya nadharia ya juu juu bila mazoezi yoyote ya vitendo. Maofisa wa CID ndio hawakuwa na utaalamu wowote wala vifaa vya uchunguzi wa aina hii, hali iliyochangiwa kwa kiasi kikubwa na amani iliyokuwepo nchini, pamoja na mwelekeo wa nchi kiuchumi, kisiasa na kijamii uliifanya nchi kujiamini na kujisahau katika mambo mengi.

Hali hii ilimfanya Sunday Msuya kuandaa taarifa ya jinsi ya kutengeneza bomu kubwa lenye mlipuko wa nguvu ya paundi elfu moja (1000 pounds) kwa kutumia vifaa vinayopatikana kwa urahisi.

Lengo la taarifa hiyo lilikuwa kuwapa picha maofisa ya aina ya vifaa walivyotakiwa kuvisaka katika eneo la tukio vikiwa vizima, vipande, au mabaki ya vifaa vilivyoteketezwa kwa moto. Vipande hivyo vilikuwa muhimu sana katika kutambua aina ya bomu, na hata kikundi au mtu aliyelitengeneza. Ingawa kila kikundi cha kigaidi kina namna yake ya kutengeneza mabomu, vifaa vya msingi huwa ni vile vile (TNT, methane gas, liquefied petroleum gas, detonator, simu au radio, saa n.k).

Hata hivyo, kila kikundi huwa kina namna yake ya kuunganisha (setting) na kulipua mabomu. Vikundi vingi hupendelea kutumia vitu vya ziada kama goroli, misumari, vipande vya nondo na kadhalika kwa lengo la kuacha alama (signature) katika eneo la tukio.

Kisha Sunday Msuya aliwaelekeza maofisa wa kundi lake utaratibu unaotumika katika kukagua eneo ulipotokea mlipuko wa bomu, vifaa vinavyohitajika, na namna ya kushughulika na kila kipande cha ushahidi kinachopatikana ili kiweze kusaidia uchunguzi na kukubalika mahakamani. Eneo walilolifanyia uchunguzi lilikuwa na nusu kipenyo cha maili moja kutoka kwenye kitovu cha mlipuko. Hii ilikuwa na maana kuwa walilazimika kukagua eneo la duara lenye mzunguko wa mita za mraba 5,000.

Ukubwa wa eneo hilo ulikadiriwa kutokana na uzito wa mlipuko uliosababisha kurushwa mbali kwa vipande vya bomu hususan nyaya, vifaa vya radio au simu, mabaki ya tanki lenye vumbi la mlipuko, viungo vya binadamu, na vitu vingine vilivyohitajika kusaidia uchunguzi.

Maofisa waliligawa eneo la tukio katika sehemu kuu mbili: sehemu ya kwanza ilianzia mahali kilipokuwa kitovu cha mlipuko hadi umbali wa mita ishirini na tano kwa mzunguko. Eneo hili walikabidhiwa wataalamu waliobobea wa milipuko kushughulika nalo. Kwenye kitovu cha eneo hilo kulikuwa na shimo lenye kipenyo cha takriban mita tatu.

Wataalamu hao walisogeza vumbi la udongo mweusi lililokuwa limeziba eneo ili waweze kuona vitu vilivyofukiwa, kazi iliyofanyika kwa tahadhari ya hali ya juu ili kuepusha uharibifu wa ushahidi. Kila kipande cha ushahidi kilichoonekana kilipigwa picha na kuorodheshwa katika daftari. Baada ya vumbi la juu na mchanga kupekuliwa, na kusogezwa pembeni, wataalamu hao walitumia majembe, sululu na makoleo kutanua upana wa shimo, na kuongeza kina chake. Katika kila hatua waliyochimba walikusanya udongo, vyuma, mabati na vitu vingine vilivyopatikana humo na kuvipeleka sehemu maalumu iliyotengwa kwa ajili ya uchunguzi zaidi.

Hapo udongo ulichujwa kwa machekeche makubwa yaliyotengenezwa kwa mbao na nyavu. Udongo laini ulitupwa pembeni; lakini kila kipande cha chuma, waya, kifaa cha radio au simu, bati, plastiki au chochote kilichoonesha dalili ya kuweza kusaidia uchunguzi kilichukuliwa. Baadaye ukaguzi wa pili ulifanyika ambapo vipande vilivyoonesha umuhimu zaidi vilipewa namba, vikapigwa picha, na kuorodheshwa katika daftari maalumu la vidhibiti kabla ya kukabidhiwa kwa wataalam wa uchunguzi wa eneo la tukio (Forensic Experts) kwa ajili ya uchunguzi zaidi.

Sehemu ya pili ya eneo ilianzia mita ishirini na tano kutoka kwenye kitovu cha mlipuko kuendelea mbele, umbali wa maili moja mzunguko kila upande. Eneo hili walikabidhiwa maofisa wengine wa usalama kushughulika nalo. Kazi kubwa ilikuwa kupekua kila inchi ya eneo hilo kwa lengo la kupata ushahidi uliorushwa mbali.

Maofisa hawa hawakupaswa kuchimba mahali popote. Walichotakiwa ni kutembea taratibu, kuangalia kwa umakini na kutambua kila kipande cha ushahidi kilichoonekana. Kwa hiyo hawakuwa na haja ya kubeba zana kama majembe, sululu au makoleo kama wenzao; badala yake walivaa glavu mikononi na kubeba ndoo za plastiki, mifuko ya karatasi na plastiki, fimbo za kusogezea majani, na wachache walikuwa na kamera za kupigia picha.

Kazi yao ilihitaji umakini wa hali ya juu na ilikuwa yenye kuumiza mno viungo vya mwili hasa mgongo, shingo na macho. Walihakikisha kuwa kila inchi ya maeneo hayo ilikuwa inakaguliwa kwa kadri ilivyowezekana. Ili kuhakikisha umakini wa upekuzi wa eneo lote, walitumia njia kuu mbili. Njia ya kwanza ilihusisha upekuzi mzunguko (spiral search).

Upekuzi huu ulifanyika kwa maofisa kujipanga mstari na kulikagua eneo la tukio kwa kulizunguka taratibu kuanzia kwenye kitovu cha mlipuko, kuelekea nje kama buibui anavyotengeneza utando wake. Na njia ya pili ilikuwa ya upekuzi mraba (square search).

Upekuzi huu ulifanywa kwa kuligawa eneo linalopekuliwa katika vyumba vidogo, vya futi moja moja. Vyumba hivyo vilihesabiwa na jumla yake ikagawanywa kwa idadi ya wapelelezi waliokuwepo. Hata hivyo, kila ofisa aliweza kupewa vyumba vichache au vingi zaidi kutegemeana na mazingira na vikwazo vilivyokuwepo katika eneo lenyewe.

Eneo lenyewe lilikuwa kubwa, na kwa kiasi fulani lilikuwa limevurugwa na watu waliokuwa wakiishi au kupita wakiwa matembezini. Kwa hiyo kila kipande cha chuma, waya, plastiki, au kiungo cha mtu kilipoonekana kilipigwa picha kikiwa chini, kabla ya kuokotwa, na kuingizwa kwenye ndoo ya plastiki au mfuko wa kubebea. Hatua hiyo ilikuwa muhimu sana katika kuthibitisha mahali kilipookotwa, umbali kiliorushwa kutoka eneo la tukio, na uhusika wake katika tukio zima…

“Kinachokera ni kwamba, waliopanga tukio hili na kugharimia utekelezaji wake sasa hivi wapo mahali fulani wanacheka na kufurahia maisha, who knows! Wakati sisi tunahangaika na kuomboleza, wao wanaendelea na maisha kama kawaida. What a shame!” nilisema kwa sauti tulivu iliyobeba huzuni.

Tunu alinitazama kwa umakini kwa kitambo pasipo kusema kitu, kisha alinyanyua juu mabega yake na kubetua midomo. Nikaangalia saa yangu ya mkononi na kushtuka kidogo. Ilikwisha timia saa tatu na robo za usiku.

* * *

Usichoke kuendelea kuzifuatilia harakati hizi za Jason Sizya...
 
Mtanisamehe kidogo wakuu, nalazimika kuipitia upya na kurekebisha baadhi ya vitu kabla sijaiposti humu, maana iligusa mambo ya ndani mno ya... ah... ngoja niishie hapa😔...
 
Mtanisamehe kidogo wakuu, nalazimika kuipitia upya na kurekebisha baadhi ya vitu kabla sijaiposti humu, maana iligusa mambo ya ndani mno ya... ah... ngoja niishie hapa😔...
mkuu sasa lini utakua tayari tuweke amsha amsha ya bando hapa samahani kwa kuuliza
 
taharuki..jpg

299

Mpango haramu!




Saa 3:30 usiku…

NILIAGANA na Tunu kwenye baraza ya nyumba yake huku akinisisitiza kuwa makini kwenye upelelezi wangu, nikaliendea gari langu lililokuwa kwenye maegesho ya magari ndani ya uzio wa nyumba yake na kufungua mlango halafu nikaingia ndani huku akili yangu ikiwa hoi kwa kulemewa na mtiririko wa mawazo juu ya matukio yasiyoeleweka, hisia mbaya za kuonekana kushindwa kujua mahali alipo Gahizi ziliendelea kuutafuna mtima wangu.

Maswali mseto yaliendelea kuzunguka akilini mwangu, kubwa likiwa: ni akina nani waliomkodi Gahizi kufanya ugaidi na kumuua Waziri wa Mambo ya Ndani, Ummi Mrutu? Hata hivyo, sikutaka kujikatisha tamaa na hivyo nilijipa moyo kuwa majibu yote ningeyapata ndani ya kipindi kifupi. Niliwasha gari langu na kulitoa nje ya uzio wa nyumba ya Tunu kisha nikaingia barabarani katika Barabara ya Kaunda nikiianza safari yangu taratibu kuelekea nyumbani kwangu eneo la Upanga, katikati ya jiji la Dar es Salaam.

Muda huo katika eneo la Oysterbay hasa barabara ile ya Kaunda kulikuwa na magari machache. Wakati nikiingia katika barabara ile, mbele yangu, hatua kama thetathini hivi, nikaliona gari aina ya Jeep Wrangler jeusi lenye vioo vya giza likiwa limeegeshwa kando ya barabara jirani na mgahawa wa Kaffé Koffee.

Kitendo cha kuliona lile gari kikafungua mlango wangu wa sita wa fahamu na kunifanya nipunguze mwendo nilipolifikia ili kulitazama vizuri gari lile. Hata hivyo taa za ndani ya gari hilo zilikuwa zimezimwa na hali ile haikuniwezesha kuona nani alikuwemo mle ndani ya gari ingawa hisia zangu ziliniambia kuwa ndani ya lile gari kulikuwa na mtu au watu waliokuwa wakinitazama.

Hisia hizo zilianza kunishawishi nitake kusimama au nigeuze gari langu na kulirudisha kule nilikotoka ili nipate nafasi nzuri ya kuendelea kulichunguza vizuri lile gari. Lakini nikajionya na kusita kufanya vile kwa kuhisi kuwa kitendo hicho kingewafanya watu waliokuwemo ndani ya lile gari washikwe na shaka na hivyo kujijengea tahadhari.

Sikusimama. Hata hivyo, macho yangu yalijikuta yakivutwa na namba za lile gari aina ya Jeep Wrangler. Namba zake zilikuwa ngeni machoni mwangu na zisizofanana kabisa na namba za magari yaliyosajiliwa Tanzania. Kabla sijazikariri vizuri ili kujua lilikuwa limesajiliwa nchi gani, nikashtuliwa na mlio wa simu yangu ya mkononi iliyoanza kuita kwa fujo.

Na hivyo mawazo yangu niliyarudisha mle ndani ya gari huku nikiitazama ile simu na hapo nikaliona jina la Kamishina Zuberi Koba, Mkurugenzi wa Makosa ya Jinai (DCI). Mshtuko ukanipata kidogo huku moyo wangu ukipiga kite kwa nguvu, kwa vile nilikuwa sijatarajia simu yoyote kutoka kwa Kamishina Koba hususan muda ule.

Muda ule nilikuwa nimelipita jengo ya Digital Waves Africa Limited na kisha lile la African Reflection Foundation (ARF) yaliyokuwa upande wangu wa kulia, na nilikuwa usawa wa mgahawa maarufu wa Peacock Cafe uliokuwa kushoto kwangu.

“Jason!” sauti nzito ya Kamishina Koba iliunguruma upande wa pili wa simu baada ya kuipokea na kuiweka kwenye sikio langu.

“Naam! Shikamoo, Kamishina!” nilimsalimia Kamishina Koba mara tu nilipoisikia sauti yake ikipenya kwenye ngoma ya sikio langu.

“Marhaba, Jason!” sauti ya Kamishina Koba ilisikika vyema kwenye sikio langu. “Vipi mbona umekuwa kimya hadi leo? Si kawaida yako au hujafanikiwa kunusa uvundo wowote kwenye hili sakata? Kabisa yaani…!”

“Sijafanikiwa bado, Kamishina… Ila najua muda si mrefu ukweli unaweza kujiweka bayana,” nilimweleza Kamishina Koba, na hapo nikamsikia akishusha pumzi.

Sasa nilikuwa nalipita jengo la mgahawa maarufu wa Kichina wa Red Dragon na kisha nikaanza kulipita jengo la Prestige Properties.

“Kwani uko wapi saa hizi maana nilipita ofisini kwako sikukukuta!” Kamishina Koba aliniuliza kwa sauti yake nzito na tulivu. “Sijui naweza nikakuona?”

Kauli ile ya Kamishina Koba ilinishtua kidogo. “Anataka nini huyu mzee?” nilijiuliza pasipo kupata jibu, maana kutembelewa na Mkurugenzi wa Makosa ya Jinai wa Polisi ofisini kwako bila taarifa yoyote, wakati hakuna kazi aliyokupa, si jambo la kawaida kabisa!

Yeah… Unaweza ukaniona,” nilimjibu kwa sauti tulivu huku nikilikwepa swali la nilikuwa wapi, na kisha nikawa kama niliyegutuka kidogo, nikasema, “Ila si kwa sasa, Kamishina.”

“Kwa nini si sasa! Kwani wewe uko wapi?” Kamishina Koba aliniuliza tena. Sikujua nimjibu nini kwa kuwa sikuwa tayari kuonana naye muda huo. Hivyo nikawa kimya kidogo.

Wakati huo huo gari moja aina ya Toyota Hilux double cabin la rangi ya maruni lililokuwa likiendeshwa kwa mwendo wa kasi, huenda hata bila sababu za msingi, likanipita kwa kasi na kukata kona ghafla likiingia upande wangu huku likiwasha taa za pembeni kuashiria kuwa lilitaka kuelekea kushoto kuifuata Barabara ya Laiboni.

Ilibidi nikanyage breki za ghafla kupunguza zaidi mwendo wangu na kuliacha liingie katika barabara ile, wakati huo huo nikivitazama vioo vya ubavuni vya gari langu kuchunguza kama kulikuwa na gari lolote ambalo ningelitilia shaka kuwa lilinifuatilia nyuma yangu.

Kwa kufanya vile niligundua kuwa hali ilikuwa shwari kwani hakukuwa na gari lolote lililokuwa likinifuatilia, na jambo lile likanifurahisha sana.

“Jason?” sauti ya Kamishina Koba ilipenya kwenye siko langu na kunizindua toka kwenye mawazo, na hapo nikakumbuka kuwa alikuwa ameniuliza swali ambalo sikuwa nimelijibu.

Err… naam, Kamishina! Ulikuwa unasema…?” nilisema kwa kubabaika kidogo na kushusha pumzi.

“Naona uko barabara una-drive!” Kamishina Koba alisema. “Basi kama leo haiwezekani nitakutafuta hata kesho…”

“Kuna shida yoyote, mkuu?” nilimuuliza Kamishina Koba kwa wasiwasi.

“Hakuna. Usijali,” Kamishina Koba alisema na kukata simu, na kwa kiasi fulani maneno yake yakanifanya nibaki njia panda huku nikishindwa kuelewa nini kilichokuwa kikiendelea!

Niliitupia jicho saa ya ndani ya gari kwenye dashibodi na kugundua kuwa ilikuwa inaelekea kutimia saa nne kasoro robo za usiku wakati nilipokuwa nikilivuka jengo la Harambee Plaza zilipo ofisi za Ubalozi wa Kenya na Benki ya KCB kisha nikakata kuingia kushoto nikiiacha barabara ile ya Kaunda na kuingia Barabara ya Ali Hassan Mwinyi. Na hapo nikayatumbukiza tena mawazo yangu kwenye tafakari nzito ya kufikiria namna nitakavyoanza kazi ya kumsaka gaidi Gahizi popote alipo.

Wakati nikiendelea na safari yangu huku nikijaribu kutafakari kwa kina kuhusu kazi iliyokuwa mbele yangu nikakumbuka wajibu wangu na kuangalia tena nyuma kupitia vioo vya ubavuni vya gari langu, na hapo nikaliona lile gari jeusi aina ya Jeep Wrangler lililokuwa limeegeshwa kando ya Barabara ya Kaunda jirani ya mgahawa wa Kaffé Koffee, sasa lilikuwa nyuma yangu.

Endelea...
 
taharuki..jpg

300

Tukio lile likanishtua kidogo na hivyo nikapunguza mwendo kidogo ili niweze kuliona vizuri lile gari nyuma yangu na mara hii nikapata hakika kuwa gari lile lililokuwa nyuma yangu lilikuwa ndiyo lile lile lililokuwa limeegeshwa jirani na ule mgahawa, muda mfupi uliokuwa umepita.

Sikujua kwa nini hisia mbaya zilianza kunipata, hata hivyo nilichukua simu yangu na kumpigia Tunu, alipopokea nikamtaarifu kuhusu hisia zangu kuwa kulikuwa na gari lililonifungia mkia, huku nikiendelea kulitazama lile gari kupitia vioo vya ubavuni vya gari langu na kujaribu kuupisha utulivu kichwani mwangu. Muda huo nilikuwa nalivuka jengo la ofisi za kampuni ya ulinzi, G4S Secure Solutions (Tanzania) Ltd.

Na kabla ya kufanya uamuzi wowote nilitaka kwanza kupata hakika kama nilikuwa nafuatiliwa au lile gari lilikuwa kwenye ratiba ya safari zake. Nilipozifikia ofisi za TANAPA Dar es Salaam nikataka niingie kushoto kuifuata Barabara ya Laiboni ambayo ingenirudisha tena kule nilikotoka, hata hivyo nikasita kufanya hivyo na kuamua kuendelea mbele nilikilivuka jengo la British Legion Tanganyika Club na kisha nikayavuka makazi ya Balozi wa Uingereza nchini Tanzania. Halafu nikazivuka taa za kuongezea magari barabarani na kuingia upande wangu wa kulia nikiifuata Barabara ya Kinondoni licha ya kwamba zile taa za kuongozea magari barabarani hazikuniruhusu kupita.

Kisha nikaongeza mwendo huku nikipanga kujizungusha zungusha kwenye mitaa kadhaa ya eneo la Kinondoni huku macho yangu yakiendelea kulitazama lile gari nyuma yangu kupitia vioo vya ubavuni vya gari langu. Kwa kufanya vile ningegundua kuwa nilikuwa nafuatiliwa na lile gari au la! Na baada ya hapo ningejua nini cha kufanya.

Niliendelea kuendesha gari langu kwenye barabara ile ya Kinondoni nikiyavuka majengo ya balozi za Spain na Switzerland na mbele zaidi niliyavuka majengo ya makao makuu ya Ecobank na lile la Kituo cha VFS Global Canada Visa Application – Tanzania kisha nikaanza kupunguza mwendo nikiwa na nia ya kuingia upande wa kulia kuifuata Barabara ya Burundi inayokatisha mitaani.

Nililisubiri gari moja lililokuwa likitokea upande wa Kinondoni lipite kisha nikaingia kwenye barabara ile ya Burundi na kuongeza mwendo kidogo huku macho yangu yakiendelea kutazama kwenye vioo vya ubavuni vya gari langu. Sikuliona lile gari na hali ile ikanipa matumaini kuwa mambo yalikuwa shwari, kwa mara ya kwanza nilidhani hisia zangu hazikuwa sawa na nikaanza kujilaumu kuwa nilikuwa nikipoteza muda wangu kwa kufanya uchunguzi usio na tija.

Hata hivyo nilipokuwa nafika mwisho wa ile barabara usawa wa jengo la Global Alliance for Improved Nutrition (GAIN) Tanzania, na kabla sijaingia Barabara ya Kilimani iliyokuwa ikikatisha kutoka kulia kwenda kushoto, nikatazama tena nyuma na kugundua kuwa hisia zangu hazijawahi kunidanganya, kwamba nilikuwa sahihi kulitilia shaka lile gari aina ya Jeep Wrangler jeusi, kwani nililiona likiingia kwenye ile Barabara ya Burundi na kunifuata kwa nyuma likiwa katika mwendo wa kasi.

Kwa kutaka kujiridhisha zaidi nikakunja kushoto nikiifuata barabara ile ya Kilimani nikiyavuka majengo ya Hospitali ya Tanzania Nordic (TANZANORD HOSPITAL) huku nikiendesha gari langu kwa mwendo wa kasi. Mbele kidogo nikakutana na barabara nyingine ya Tunisia, wakati nikikata kuingia kushoto kuifuata barabara ile ya Tunisia nikaliona tena lile gari aina ya Jeep Wrangler likiingia katika barabara ya Kilimani na kukunja kona kushoto likinifuata.

Tukio lile likanifanya nishikwe na hasira, nikaichomoa bastola yangu kutoka mafichoni na kuiweka kando yangu tayari kukabiliana na jambo lolote ambalo lingejaribu kutishia usalama wangu. Sasa niliamua kumshikisha adabu huyo mtu au watu walioamua kunifuatilia. Harakati zangu zilinifikisha mwisho wa barabara ile ya Tunisia na kuikuta tena Barabara ya Kinondoni, nikaingia katika barabara ile kwa mwendo wa kasi huku nikiyapita makaburi ya Kinondoni, nikayavuka magari mawili yaliyokuwa mbele yangu nikiwa katika mwendo wa kasi hadi nilipokifikia kituo cha daladala cha Kinondoni Makaburini nikapunguza kidogo mwendo.

Sasa nilipanga kuwaweka karibu zaidi wale watu nyuma yangu kwani hadi kufikia hapo nilishakuwa na uhakika kuwa nilikuwa nimefungiwa mkia. Muda huo simu yangu ikaanza kuita, nilipoitazama nikaliona jina la Tunu, nikaipokea na kumweleza kuhusu gari lile na mahali nilipokuwa. Sasa nikapata wazo jingine wakati nilikuwa nafika kwenye Soko la TX la Kinondoni, nikakanyaga breki huku tayari nikifyatua kabali ya mkanda wa kiti changu niliojifungua, na kulisimamisha gari langu kando ya barabara ya Kinondoni jirani na Soko la TX.

Kisha nilikiachaa kiti changu na kusogea kwenye kiti cha abiria na kufungua mlango, nikashuka haraka kupitia mlango ule wa abiria na kwenda kujibanza kwenye ukuta wa jengo lililokuwa jirani na soko hilo.

Muda mfupi uliofuata lile gari aina ya Jeep Wrangler likawa limefika eneo lile likiwa katika mwendo wa kasi na mara dereva wa gari lile alipoliona gari langu akupunguza mwendo huku akionekana kama aliyekuwa akipita, na hapo nikashuhudia vioo vya upande wa kushoto vya lile gari vikishushwa haraka, mitutu miwili ya bunduki ikachomoza.

Tayari nilishahisi hatari nikaishika vizuri bastola yangu huku macho yangu yakiwa makini kutazama kule kwenye lile gari. Nilichokishuhudia ni mirindimo mfululizo ya risasi iliyolengwa kwenye gari langu upande ule wa dereva na kutoboa vibaya bodi la gari langu huku kile kioo cha ubavuni cha gari langu, sehemu ya dereva, kikiondoshwa kwa kuchanguliwa vibaya na risasi.

Kisha nikashuhudia watu wawili wakishuka haraka toka kwenye lile gari aina ya Jeep Wrangler wakiwa wameshika bunduki aina ya SMG mikononi na kulizingira gari langu huku wakiendelea kuachia risasi kwenye lile gari. Hali ile ya milio ya risasi ilisababisha kuwepo kwa hali ya taharuki eneo lile na kuwafanya watu waliokuwa eneo lile waanze kukimbia ovyo kusalimisha roho zao huku wakipiga mayowe ya hofu.

Wakati huo nami nilikuwa nimeikamata vizuri bastola yangu mkononi, nikavuta kilimi cha bastola yangu kwa mmoja wa wale watu wawili walioshuka toka ndani ya lile gari wakiwa na bunduki, kitendo kile kikaruhusu risasi mbili zichomoke kwa kasi na kuchana anga huku mlio mkali wa risasi ukisikika na kumwingia yule mtu upande wake wa kushoto wa kifua, msukumo wa risasi zile ukamnyanyua juu na kumtupa nyuma katikati ya barabarani. Hakuweza hata kufurukuta.

Endelea...
 
taharuki..jpg

301

Na hapo nikamwona yule mwenzake akitaharuki lakini sikutaka kumpa nafasi ya kunishambulia pale nilipokuwa nimejibanza, nikaachia risasi nyingine iliyoingia upande wake wa kulia wa kifua, kwenye bega lake. Akapiga yowe kali la maumivu huku akitupwa chini, bunduki ikamtoka na kuanguka kando. Sikuwa na shida ya kumuua yule mtu kwani nilihisi kuwa tungehitaji kumpata japo mmoja wao akiwa hai kwa mahojiano ili kujua ni nani aliyewatuma kunifuatilia, na kwa sababu gani!

Kuona hivyo dereva wa lile gari akataka kuliondoa gari lake ili kukimbia, lakini tayari nilishamshtukia na wakati lile gari likianza kuondoka kwa kasi, nikaachia risasi tatu makini, risasi moja ikienda kwenye gurudumu la mbele la upande wa kushoto na mbili zikipasua kioo cha nyuma cha upande huo wa kushoto na kukipasua. Sikujua kama risasi zile zilikuwa zimempata dereva au la! Lakini nilichokishuhudia muda ule ni lile gari kupoteza mhimili na kuyumba kisha likaelekea kwenye mtaro wa maji taka uliokuwa kando ya barabara ile na kupinduka.

Hata hivyo, ilinishangaza kuona kuwa pamoja na hali ile lakini injini ya lile gari ilikuwa bado ikiunguruma na magurudumu yakiendelea kuzunguka kwa kasi. Yule mwanamume niliyemchakaza kwa risasi kwenye bega lake la kulia alikuwa akijaribu kuinuka ili aiokote baunduki yake lakini nikamuwahi, bastola yangu ikiwa mkononi.

Nilifika eneo lile na kuziokota haraka haraka zile bunduki zao, nikazining’iniza kwenye bega langu la kushoto huku bastola yangu nikiwa nimeishika kwa mkono wa kulia nikimnyooshea yule mtu nikiwa nimemkazia macho. Na hapo nikamwona akigeuka taratibu kunitazama, hata hivyo hakuweza kufanya chochote kwani ilionesha kuwa alikuwa kwenye hali ya kutaabika na maumivu makali.

Nilimtazama kwa makini huku nikijaribu kumkazia macho kuitazama vizuri sura yake. Hata hivyo sura yake ilikuwa ngeni kabisa machoni mwangu. Yule mtu alipoona namtazama kwa udadisi zaidi nikayaona namna macho yake yalivyojawa na hofu ambayo ilimfanya ayakwepeshe macho yake na kutazama pembeni.

“Mnataka kuniua nimewafanya nini?” nilimuuliza yule mtu huku macho yangu yakitambaa haraka kulikagua eneo lile kwa tahadhari, kama scanner, ili kuona kama kulikuwepo na mtu mwingine ambaye angeweza kuwa na ushirika na wale watu.

Muda ule mashuhuda walikuwa wameanza kukusanyika eneo lile wakitaka kufahamu vizuri nini kilichokuwa kimetokea. Nikiwa bado nimeikamata vyema bastola yangu mkononi pasipo kuitilia maanani halaiki ya watu iliyokuwa ikizidi kuongezeka eneo lile, niliendelea kumkazia macho yule mtu aliyelala pale barabarani. Yule mtu hakunijibu na badala yake aliendelea kunitazama kwa hofu huku akilalamika maumivu ya bega lake la mkono wa kulia.

Nilipomtazama yule mwingine niliyekuwa nimemchapa risasi mbili za kifuani nikamwona akiwa amelalia dimbwi la damu hatikisiki, tayari alikuwa amekufa. Nikayarudisha haraka macho yangu kwa yule mwenzake na kumuuliza kwa ukali, “Nakuuliza wewe, nimewafanya nini hadi mnataka kuniua?”

Yule mtu aliendelea kuwa jeuri kwa kukaa kimya kisha alijiinua toka pale chini na kukaa, muda wote alikuwa akiuma meno yake na kukunja sura yake katika namna ya kukabiliana na maumivu makali ya jeraha lake. Nikamsogelea karibu na kumzaba kofi la nguvu ili kumuweka sawa.

“Nyinyi ni akina nani?” nikamuuliza tena yule mtu kwa hasira huku nikifikiria namna ya kumfanya azungumze.

Hata hivyo kabla hajanijibu nikalishuhudia gari aina ya Mercedes Benz jeusi lenye vioo vyeusi likija kwa mwendo wa kasi huku likiyapenya magari mengine yaliyokuwa yamesimama barabarani, taa za gari lile zilikuwa zimewasha zote na lilikuwa likipiga honi mfululizo kuyataka magari mengine yapishe na kuegeshwa pembeni. Kisha likafunga breki mbele yangu.

Nikawa makini kulitazama lile gari huku nikijiandaa kwa lolote endapo ingetokea hali ya kutishia usalama wangu. hata hivyo nilijikuta nikisita kidogo baada ya kulitambua lile gari, lilikuwa gari la Tunu.

“Sisi ni askari,” yule mtu aliongea kwa tabu baada ya kumwona Tunu akishuka toka kwenye gari lake na kuja haraka pale tulipokuwa. Kwa kutambua kuwa yule mtu alikuwa askari ikanishtua kidogo. Hata hivyo sikujali sana.

“Kuna mwingine kule kwenye gari,” nilimwambia Tunu huku nikimwonesha kule kwenye lile gari aina ya Jeep Wrangler lililopinduka kwenye mtaro wa maji taka, kisha nikageuza shingo yangu kuitazama sura ya yule mwenzake aliyelalia dimbwi la damu nikahisi moyo wangu ukiyasahau mapigo yake kwa muda, na yalipoanza tena nikashusha pumzi.

Sasa sura yake ilijaa machoni kwangu na hasira kunichemka kifuani. Alikuwa ni yule mwanamume mfupi ambaye nilimwona kwenye gari aina ya Range Rover Velar la rangi nyeupe, usiku wa siku ulipotokea mlipuko wa bomu pale Alpha Mall.

Nilikuwa naitazama sura ya Deogratius Samson Rutashobya, ofisa wa usalama wa taifa. Hasira zikazidi kunipanda, nikamrudia yule mwanamume niliyekuwa namhoji na kumchapa tena kofi la nguvu usoni kwake na hapo nikaona kamasi nyepesi za damu zikianza kumtoka puani.

“Kwa hiyo askari wa siku hizi mnaua watu wema wasiokuwa na makosa, sivyo! Kwanza ni nani aliyewatuma mnifuatilie ili kuniua?” nilimuuliza yule mtu kwa hasira wakati akigugumia maumivu.

“Hatujatumwa na mtu yeyote,” yule mtu aliongea kwa tabu huku akilalama kwa maumivu.

“Sasa kwa nini mnifuatilie kama jambazi? Na kama kweli nyinyi ni wanausalama kweli kwa nini msishughulike na wahalifu na badala yake mnatumika kuua raia wanyonge?” nilimuuliza tena yule mtu lakini nikagundua kuwa alikuwa amepoteza fahamu kutokana na maumivu na kupoteza damu nyingi.

Sikutaka kupoteza muda hivyo nikaanza upekuzi makini kwenye nguo zao nikianza na yule mtu niliyekuwa nikimhoji, nikamkuta akiwa na simu ya mkononi aina ya Samsung na kitambulisho cha kazi kilichomwonesha kuwa alikuwa ni askari wa cheo cha mkaguzi wa polisi (inspector) kutoka kitengo nyeti cha CID makao makuu.

Kisha niliufuata mwili wa Deogratius Rutashobya na kuupekua, nikamkuta pia akiwa na simu ya mkononi aina ya Iphone 13 na kitambulisho kilichomwonesha kuwa alikuwa Ofisa Usalama wa Taifa, pia nilipata kadi ndogo ya kibiashara (business card) yenye anwani fulani. Nikaichukua kadi ile na kuitia mfukoni kwangu huku simu zao nikiwa nimezishika mkononi, na wakati nikijishauri nini cha kufanya mara nikamwona Tunu akirejea pale nilipokuwa nimesimama.

“Vipi amekufa au mzima?” nilimuuliza Tunu huku nikimtazama kwa umakini.

“Amekufa! Risasi zimepenya kwenye fuvu lake la kichwa,” Tunu alinijibu. Na mara lile kundi la mashuhuda waliokuwa wamejazana kushangaa likaanza kusogea kando taratibu na kutengeneza nafasi nzuri ya kupita.

Nilipotazama vizuri nikaliona gari la polisi lililokuwa limewasha king’ora na muda huo polisi watano waliruka toka kwenye lile gari na kusambaa haraka eneo lile wakiwa wamebebelea bunduki aina ya Sub Machine Gun na vifua vyao vimekingwa na mavazi maalumu yanayozuia risasi (bullet proof). Askari hao walikuwa na sura za kazi. Niliwatambua mara moja kuwa ni polisi wa kutoka Kituo cha Polisi cha Oysterbay.

Nikageuka kumtazama Tunu katika namna ya kumuuliza iwapo ni yeye aliyekuwa amewasiliana nao, akanielewa na kubetua kichwa chake kukubali.

* * *

Usichoke, endelea kufuatilia hadi mwisho...
 
Kwa leo tuishie hapa, Mungu akipenda pengine kesho nikaachia episodes zingine. Itabidi mnivumilie kidogo maana huku Kilwa nilipo kwa sasa kuna changamoto lukuki, isitoshe ninabanwa sana na majukumu na wakati mwingine sipati network...
 
Dah! Humu kumepoa sana kana kwamba watu mmeamua kunisusia 😔, ni watu wachache sana wanaotia moyo... nafikiria nikiimaliza season hii ya Taharuki niachane na harakati hizi za Jason Sizya, ingawa bado kuna season kibao huko mbele...
 
taharuki..jpg

302

Saa 6:30 usiku…

Manyunyu hafifu ya mvua yalikuwa yanadondoka ardhini, upepo nao ulivuma kwa hasira ukitokea upande wa baharini na kufanya baadhi ya takataka zilizoonekana katika Mtaa wa Bahari kupeperuka juu. Manyunyu haya ya mvua na upepo, kwa pamoja, vilisababisha baridi kali la aina yake lililopenya kwenye ngozi yangu na kunifanya nitembee huku nikiwa nimejikunyata na kuweka mikono yangu mifukoni.

Jinsi muda ulivyozidi kwenda ndivyo baridi lilivyozidi kuwa kali na kunifanya nishangae sana, kama si kuhamaki, kwani sikuwahi kulihisi baridi kali kama hili jijini Dar es Salaam, na hata upepo wa aina hii ulikuwa aghalabu kutokea ndani ya jiji hili lenye watu wengi zaidi nchini na lililosifika kwa hali ya hewa ya joto kali tofauti na hali niliyokuwa nikiishuhudia usiku huu.

Kama hii haitoshi, giza nalo lilikuwa limetamalaki, giza totoro, ambalo lilimudu kufifisha mwanga uliothubutu kutoka katika baadhi ya taa toka kwenye majumba ya kifahari ya mtaa huu wa Bahari, eneo la Mbezi Beach, na kufanya mwanga huo wa umeme uonekane kama ni chemli zisizo na mafuta ya kutosha.

Kwangu, hiki kilikuwa kichekesho cha mwaka, kwamba jiji kongwe katika Afrika ya Mashariki na lango kuu la kibiashara nchini Tanzania lilikuwa halina taa za barabarani? Ah, hapana… taa zilikuwepo, isipokuwa zilikuwa haziwaki! Kwa nini? Wenye jibu la swali hilo walikuwa ni maofisa wa Manispaa ya Kinondoni au wale wa Shirika la Ugavi wa Umeme Nchini, Tanesco.

Lakini, kwani ni nani alisema kuwa matajiri hawa wangelithubutu kuwasha chemli ikiwa umeme ungekatika ilihali kulikuwa na umeme uliotumia mwanga wa jua (solar) na kwa wengine wangeweza kutumia taa za Kichina za solar au betri zilizozagaa kila kona ya Jiji la Dar es Salaam katika maduka?

Ingawa baridi lilikuwa kali na upepo halikadhalika, lakini pengine vyote kwa pamoja havikuisumbua sana akili yangu kwa wakati huu, jambo lililonitatiza ni kuhusu kile nilichokuwa nikienda kukitafuta huko mbele! Moyo wangu ulikuwa ukienda mbio sana na sikuweza kuhisi nini ambacho kingenitokea mbele yangu, hata hivyo hilo halikunizuia kuendelea na harakati zangu.

Muda huu nilikuwa nimetoka Kituo cha Polisi cha Oysterbay kuandikisha maelezo juu ya shambulio la risasi dhidi yangu kutoka kwa watu watatu waliotambulika kuwa wanausalama, ambao kati yao ni mmoja tu aliyekuwa bado mzima na alikuwa amelazwa katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili kwa matibabu.

Nilipotoka kituo cha polisi Tunu alinichukua kwa gari lake hadi nyumbani kwake Barabara ya Kaunda, Oysterbay, na kuniazima gari lake binafsi aina ya Toyota Premio la rangi ya fedha baada ya gari langu kuchakazwa vibaya kwa risasi kwenye shambulio lile la risasi kule kwenye Soko la TX Kinondoni.

Ni gari hili la Tunu nililolitumia kunifikisha pale Mbezi Beach na kisha nikaliegesha kwenye maegesho ya ukumbi wa burudani wa Sea Breeze uliokuwa kwenye makutano ya Barabara ya Mwai Kibaki na Mtaa wa Bahari.

Nilimtafuta mlinzi wa eneo lile na kumpatia noti ya shilingi elfu tano ili kunilindia gari langu kwa muda mfupi, fedha ile ilimfanya akenue meno yake kwa furaha. Halafu nikafunga vizuri milango ya gari, kisha nikaanza kutembea taratibu nikiufuata mtaa ule wa Bahari, bastola yangu ikiwa nyuma kiunoni.

Safari ya kuja Mbezi Beach ilikuwa imeibuka ghafla baada ya kugundua kuwa dereva aliyekuwa akiendesha lile gari la wavamizi, aina ya Jeep Wrangler, alikuwa ni SSP Yusuf Kambi, yule mtu niliyemwona kwa mara ya kwanza kwenye msiba nyumbani kwa Waziri Ummi Mrutu akiwa amevalia suti nyeusi, kofia ya pama nyeusi na macho yake akiwa kayaficha kwa miwani myeusi, kisha akaondoka na mwanamke fulani mrefu mweupe mwenye hijabu, wakiwa na gari la kifahari aina ya BMW X6 la rangi nyeusi na safari yao kuishia kwenye jumba la kifahari lenye nambari 89.

Niliamua kwenda Mbezi Beach kwenye makazi yake ambayo aliyatumia mara chache kufanya mambo yake. Niligundua kuwa SSP Kambi aliishi peke yake na hakuwa na mke, kwa hivyo, hiyo ilikuwa nafasi yangu muhimu kwenda kufanya uchunguzi wa siri kubaini nini kilikuwa kimejificha nyuma ya shambulio lile dhidi yangu, na iwapo lilikuwa na uhusiano wowote na lile tukio la kigaidi la kulipuliwa kwa jengo la Alpha Mall.

Wakati nikitembea taratibu katika mtaa ule huku manyunyu ya mvua na baridi vikiendelea kunitesa kiaina, nilizungusha macho yangu kutazama huku na kule katika kuhakikisha usalama wangu, lakini sikuweza kuona chochote cha kutishia usalama wangu katika barabara ile, ingawa hali ile haikutosha kunihakikishia kuwa nilikuwa katika mazingira salama.

Niliendelea kutembea nikiyapita majumba ya kifahari yaliyozungukwa na miti mirefu na kuta ndefu zenye mifumo maalumu ya ulinzi, hata hivyo majumba yale yalikuwa na giza kutokana na miti ya kivuli kutanda. Niliuvuka mtaa wa kwanza ulioingia kushoto, na kisha niliufikia mtaa wa pili nikaingia upande ule wa kushoto nikiifuta barabara tulivu ya mtaa wenye majumba ya kifahari yaliyozungukwa na miti mirefu na kuta zenye usalama wa uhakika.

Barabara ya mtaa ule ilikuwa tulivu mno huku giza likiendelea kutamalaki na kufanya mwanga wa taa za umeme toka kwenye majumba yale kupenyeza mwanga hafifu pale mtaani. Hata hivyo nilijihisi kama niliyekuwa nikionekana vizuri na mtu yeyote aliyekuwa mafichoni akinitazama. Kwa mbali niliweza kuzisikia sauti kali za mbwa waliokuwa wakibweka katika nyumba za eneo lile bila sababu za msingi.

Mtaa ule ulikuwa tulivu mno na wenye ukimya wa aina yake kiasi kwamba wakati nilipokuwa nikikatisha nilijikuta nikisita na kusimama baada ya kuhisi kuwa kulikuwa na mtu kama si watu waliokuwa sehemu fulani kwenye miti wamejibanza. Hisia zangu ziliniambia hivyo, nikasimama kwa utulivu chini ya mti mkubwa uliokuwa kando ya barabara ya mtaa ule huku nikiyatembeza macho yangu kwa umakini kulikagua vizuri eneo lile.

Hata hivyo sikumwona mtu yeyote isipokuwa manyunyu hafifu ya mvua na hisia za upepo uliokuwa ukiendelea kuvuma na kuyumbisha matawi ya miti iliyokuwa eneo lile. Hatimaye nilizipuuza hisia zangu na kuendelea mbele na safari yangu nitembea taratibu, na nikiwa mbioni kuifikia nyumba nambari 89 ya SSP Kambi hisia kama zile za awali zakanijia tena, lakini mara hii kwa namna tofauti kidogo, kwani nyuma yangu nilihisi kama vile kulikuwa na mtu fulani aliyekuwa akinifuatilia.

Endelea...
 
taharuki..jpg

303

Hisia hizo zilinifanya nichepuke na kujibanza kwenye mti mmoja mkubwa uliokuwa jirani na eneo lile huku nikiwa nimeikamata vyema bastola yangu mkononi. Kutoka pale nyuma ya mti ule nilipojibanza, niligeuka taratibu na kutazama kule nyuma nilipotoka huku nikiwa makini zaidi kuyatembeza macho yangu katika vipenyo vyote vya eneo lile.

Bado sikuweza kumwona mtu yeyote na hali ilikuwa tulivu kama ilivyokuwa mwanzo. Hata hivyo sikutaka kuridhika mapema kuwa hali ilikuwa shwari, hivyo nikaendelea kujibanza nyuma ya ule mti kwa muda mrefu zaidi huku nikitarajia kumwona mtu yeyote akijitokeza. Lakini hali ilikuwa tofauti kwani hakukuwa na mtu yeyote aliyejitokeza na hali ile ikanifanya nijione kuwa mwenye wasiwasi mwingi na woga usiokuwa na sababu za msingi.

Hatimaye niliyaacha maficho yale na kutembea taratibu, safari hii sikutaka tena kugeuka nyuma ingawa nilikuwa nimejizatiti kwa kila hali kukabiliana na hatari yoyote ambayo ingejitokeza. Kisha nililifikia geti kubwa jeusi la nyumba niliyoikusudia, nyumba ya SSP Kambi.

Hata hivyo, ukuta mrefu na wenye seng’enge maalumu juu yake inayomzuia mtu yoyote kupenya kwa urahisi endapo angefanikiwa kufika juu ya ukuta huo ilinikatisha tamaa juu ya namna ya kuingia ndani ya nyumba ile. Nilisimama nikageuka kutazama huku na huko, sikumwona mtu yeyote.

Nilitazama juu ya geti ili nibaini kifaa ambacho kingekuwa kikifanya kazi ya kuchukua picha lakini sikuona kitu chochote zaidi ya taa moja kubwa. Nikatabasamu na hivyo nilitamani sana kulisogelea lile geti na kugonga nikiamini mle ndani kungekuwa na mlinzi tu, lakini nikajionya na kughairi.

Kikubwa nilichofikiria ni kutaka kufahamu hali ya usalama wa eneo lile, hivyo nikaachana kwanza na lile geti na kutembea kwa utulivu kando kando ya ukuta wa ile nyumba chini ya vivuli vya miti katika namna ya kufanya tathmini ya mazingira yale. Lakini vile vile nilitaka kuvuta uwepo wa kiumbe hai chochote ambacho kingekuwa eneo lile kikinitazama.

Hatimaye nikafika mwisho wa ukuta wa ile nyumba pasipo kuhisi uwepo wa mtu yeyote eneo lile. Hali bado ilikuwa shwari na kwa mbali niliendelea kuzisikia sauti za mbwa waliokuwa kwenye nyumba za jirani na eneo lile wakibweka japo nyumba zote za eneo lile zilikuwa zimetawaliwa na ukimya wa aina yake. Nilipoitazama saa yangu ya mkononi nikagundua kuwa ilikuwa tayari imetimia saa saba na dakika tano usiku. Sasa mvua ilikuwa imeongezeka na kuwa kubwa kiasi.

Kule mwisho wa ukuta kulikuwa na upenyo ambao ungeniwezesha kuizunguka ile nyumba, nikaanza kuzunguka huku nikiuchunguza ule ukuta na nilipoona kuwa hapakuwa na mwanya wowote wa kuniruhusu kuingia ndani ya nyumba ile nikapata wazo jipya. Niliitazama ile miti mikubwa iliyoizunguka ile nyumba nikiwa nimepata wazo kuwa ningeweza kuyatumia matawi ya ile miti iliyokuwa ndani ya uzio wa nyumba ambayo yalikuwa yametokea kwa nje ya ule ukuta mrefu wa ile nyumba.

Hali ile ilinipa faraja kiasi nilipogundua kuwa nilikuwa na uwezo wa kuyatumia matawi yale kupenya na kuingia mle ndani ya ile nyumba. Hata hivyo wazo hilo lilifutika baada ya muda mfupi nilipogundua kuwa nisingeweza kuingia ndani kwa kupitia njia ile, kwani matawi hayo yalikuwa juu na ingenilazimu kuyarukia, jambo ambalo lingeweza kumshtua mlinzi wa nyumba ile ambaye niliamini alikuwemo ndani ya uzio wa nyumba hiyo.

Nilikuwa bado nina dhamira ya kuingia mle ndani ya ile nyumba. Nikaamua kurudi tena kule mbele, na nilipolifikia tena lile geti nikasimama huku nikigeuka na kuyatembeza macho yangu huku na kule katika namna ya kujiridhisha na hali ya usalama wa eneo lile. Hali bado ilikuwa shwari na sikuweza kuhisi kitu chochote katika geti la nyumba ya jirani upande wa pili wa barabara lililokuwa likitazamana na lile geti la nyumba nambari 89.

Sasa nilibaki njia panda, nafsi moja ikiniambia niondoke na kurudi asubuhi lakini nafsi nyingine ikinitaka kuendelea na harakati za kutaka kuingia ndani kwani kazi ilipaswa kufanywa usiku huo huo pasipo kungoja, hata hivyo ile sauti iliyonitaka niingie ndani ilionekana kushinda, nikaamua kuwa liwalo na lile lakini nisingeweza kuahirisha jambo nililoliazimia tangu mwanzo. Nikalisogelea lile geti na kugonga taratibu.

Ni kama vile yule mtu aliyekuwa ndani alikuwa akinisubiri tu nigonge kwani muda ule ule niliona kidirisha kidogo kwenye geti dogo kikifunguliwa na sura ya mtu ikichungulia.

“Nani?” yule mtu aliniuliza kwa sauti yake nzito inayokwaruza.

“Ni mimi, samahani kumetokea tatizo huku,” nilisema kwa namna ya kutaka kumwaminisha yule mtu kuwa nilikuwa mwenyeji wa eneo lile na kuwa kulikuwa na tatizo.

“Wapi? Kwani we nani?” yule mtu aliniuliza tena kwa sauti iliyobeba wasiwasi.

“Dah, kuna tatizo ndugu yangu, tafadhali nisaidie,” nilisema huku nikijitia kuwa na hofu. Nilimsisitiza nikijiambia kuwa endapo angekataa kufungua ningetafuta namna nyingine ya kufanya au kuondoka ili nirudi asubuhi.

Kikatokea kimya cha kitambo fulani, huenda yule mtu alikuwa akijishauri. Na nilipoanza kukata tamaa nikaliona geti dogo likifunguliwa taratibu kisha nikajikuta nikitazamana uso kwa uso na mtu mmoja wa miraba minne aliyejazia kisawa sawa na ambaye alikuwa na macho yenye kuashiria shari muda wote. Mtu huyo alikuwa amevaa kofia ya bareti iliyokibana kichwa chake na koti refu jeusi lililomfika magotini, na alikuwa ameshika bunduki mkononi.

Alinitazama kwa umakini kuanzia juu hadi chini. Mara moja nikapata picha kwamba yule mtu alikuwa ndiye mlinzi wa nyumba ile.

“Nikusaidie nini?” yule mtu aliniuliza huku akinikazia macho yaliyowaka kwa ghadhabu.

“Nahitaji msaada wako, kaka…” nilimjibu kwa nidhamu nikijitahidi kuonesha hali fulani ya uoga halafu nikimwonesha kwa ishara upande wangu wa kushoto.

Kauli ile ilimfanya jamaa yule aniangalie kwa umakini akionekana kufukiria kwa sekunde kadhaa. “Kuna nini?” aliniuliza huku akiwa bado ananitazama kwa umakini. Kisha nikamwona akitoa shingo yake kuchungulia kule nilikomwonesha. Muda huo nilikwisha andaa ngumi nzito tayari kabisa kumtandika kichwani, ngumi ambayo niliamini ingempeleka chini na kumpoteza fahamu.

Kwa kasi ya aina yake nilimpiga ngumi nzito ya shingoni iliyomfanya apepesuke na kuyumba huku akirudi ndani ya uzio. Kufumba na kufumbua nikaruka na kumpiga mateke mawili makali yaliyompata sawa sawa kichwani na kumpeleka chini. Bunduki yake ikaanguka mita chache toka alipokuwa ameangukia. Niliifuata ile bunduki na kuinama ili niiokote lakini kabla sijaiokota yule mtu aliinuka mzima mzima na kuruka juu ili aweze kunikanyaga mgongoni.

Endelea...
 
taharuki..jpg

304

Bahati yake ilikuwa mbaya kwa sababu nililing’amua hilo mapema na kumkwepa kitendo kilichomfanya ajibamize ukutani kwa kishindo. Hata hivyo nilistaajabu sana kwa wepesi wa mtu yule wa miraba minne. Akiwa bado ameegemea ukuta akigugumia kwa maumivu, nilimrukia tena kwa teke kali sana la shingo lililomrusha mita kadhaa kisha akatulia. Nilikuwa na imani kuwa asingeamka kwa pigo lile hadi zipite saa tano.

Nilisimama na kumwangalia yule jamaa aliyekuwa amelala kimya pale chini. Nilikuwa nahema kwa nguvu. Kisha nilimwendea pale chini kwa tahadhari na kumchunguza. Nikagundua kuwa tayari alikuwa mbali na dunia hii kwani teke lile lilikuwa limekata kabisa mawasiliano baina ya kichwa na sehemu nyingine za mwili.

Nilimpekua haraka haraka na kumkuta na kete kadhaa za bangi, shilingi elfu kumi na mbili na kitambulisho cha kazi kilichomtambulisha kwa jina la Jackson Nyembo, na alikuwa mwajiriwa wa kampuni ya ulinzi ya Gadi Security Agency kama mlinzi maalumu.

Nilimrudishia vitu vyake katika mfuko wake. Kisha niliangaza huku na kule katika namna ya kuchunguza kama kulikuwa na chochote ambacho kingeweza kunisaidia lakini sikuona chochote cha kunisaidia kwa wakati ule. Nikalifunga lile geti halafu nikamburuta yule mlinzi na kumficha nyuma ya kibanda cha mlinzi.

Mara nikashtushwa na sauti ya muungurumo wa gari lililokuwa likija upande ule, hivyo nikachepuka na kujibanza kwenye kona moja ya kile kibanda cha mlinzi huku nikiusikilizia ule muungurumo, nikalisikia lile gari likipita na kuendelea mbele. Sikuweza kufahamu lilikuwa gari gani. Nilisubiri pale kwa sekunde kadhaa nikiwa makini, kabla sijaanza kufanya mjongeo wowote.

Niliyatembeza macho yangu kupeleleza mandhari ya ile nyumba. Ilikuwa nyumba kubwa ya kisasa lakini si ya ghorofa na ilikuwa na madirisha makubwa ya kisasa na baraza kubwa mbele yake. Nje ya nyumba ile upande wa kulia kulikuwa na nyumba nyingine ndogo ya mfanyakazi na kando yake kulikuwa na banda la wazi la kuegeshea magari. Nilipochunguza vizuri nikaona magari mawili ya kifahari. Gari moja lilikuwa aina ya Range Rover Velar la rangi nyeupe lenye vioo vyeusi visivyoonesha ndani na jingine ni lile BMW X6 la rangi nyeusi ambalo pia lilikuwa na vioo vyeusi.

Sehemu nyingine ya mandhari ya nyumba ile ilizungukwa na bustani nzuri ya maua ya kupendeza na katikati ya bustani ile kulitengenezwa njia nzuri ya kutembea kwa miguu kwa vitofali vidogo vinavyovutia huku nyumba ikizungukwa na miti kadhaa ya kivuli ikiwemo mitatu mikubwa ambayo matawi yake yalikuwa makubwa na yalikuwa yametengeneza giza fulani lililonipa hisia kuwa mtu yeyote angeweza kujibanza bila kuonekana.

Kwa sekunde kadhaa niliendelea kujibanza pale kwenye kibanda cha mlinzi huku nikiupisha utulivu kichwani mwangu, hali ilikuwa ya ukimya mno jambo lililonipa hisia kuwa mle ndani ya ile nyumba hapakuwa na mtu yeyote. Hatimaye niliondoka pale kwenye kibanda na kuelekea upande wa kushoto. Bastola yangu ikiwa imetulia vyema kwenye kiganja cha mkono wangu wa kushoto.

Sikutaka tena kurudi nyuma hivyo niliamua kusonga mbele nikitembea kwa tahadhari kuizunguka ile nyumba katika namna ya kupata uhakika wa hali ya usalama wa eneo lile. Kiza kilichotokana na matawi makubwa ya miti ya vivuli iliyoizunguka nyumba ile kilinipa ahueni kidogo ya kufanya mjongeo makini.

Wakati nikikatisha chini ya ile miti nilishuhudia upande ule wa kushoto wa ile nyumba kulikuwa na bwawa dogo la kuogelea lililozungukwa na vitanda vizuri vya kujipumzisha chini ya miamvuli mikubwa ya kivuli. Nikajibanza kwenye mti mmoja uliokuwa jirani huku nikiyapa macho yangu utulivu wa kufanya uchunguzi wa mazingira yale.

Mvua ilikuwa imeacha kunyesha na hivyo kunifanya niwe na tahadhari ya hali ya juu kwani hatua zangu zingeweza kusikiwa na mtu, endapo kungekuwa na mtu yeyote aliyelala mle ndani. Baada ya kusimama pale kwa sekunde chache hatimaye niliondoka na kuelekea nyuma ya ile nyumba ambako kulikuwa na karo la kufulia nguo na kuoshea vyombo na pembeni yake kulikuwa na kamba maalumu za kuanikia nguo.

Nilizifuata ngazi za varandani za kuelekea mlango wa nyuma wa nyumba na nilipoufikia ule mlango wa nyuma nikajibanza kwa utulivu nikisikilizia huku nikiangaza macho yangu huku na kule katika namna ya kuchunguza hali ya usalama wa eneo lile. Hali bado ilikuwa ya ukimya mno na sikuona dalili zozote za upinzani katika harakati zangu. Nikauchunguza kwa makini ule mlango wa nyuma na kugundua kuwa ulikuwa umefungwa kwa funguo.

Sikuwa na funguo malaya ambayo ingeweza kufungua vitasa vingi, hivyo sikutaka kuhangaika na ule mlango ambao ungenipotezea muda mwingi, nikawaza haraka haraka nikitafuta njia mbadala ya namna rahisi zaidi ya kuingia mle ndani. nikajisogeza pembeni mwa ile varanda kwenye dirisha. Hapo nikalichunguza lile dirisha kwa utulivu na kugundua kuwa lilikuwa dirisha la sehemu ya jiko la ile nyumba.

Nilijaribu kulifungua kwa hila lakini sikuweza kwani lilifungwa ndani kwa komeo. Nikawaza namna ya kufanya na kukumbuka kuwa nilikuwa na kisu kidogo cha springi ambacho mwisho wa mpini wake kulikuwa na kipande kidogo cha almasi kwa ajili ya kukatia vioo, hivyo nilikitoa na kuzungusha duara kwenye sehemu ya kioo usawa wa komeo la lile dirisha kisha nikakitoa kile kipande cha kioo nilichokizungusha na kupenyeza mkono wangu kufyatua komeo na kulifungua lile dirisha.

Muda mfupi uliofuata nikawa nimefanikiwa kulifungua lile dirisha na kuingia mle jikoni. Kwa dakika chache nilitulia mle jikoni huku masikio yangu yakiwa makini kusikiliza sauti na macho yangu yalikuwa makini kuyapeleleza mazingira ya chumba kile cha jiko.

Baada ya kuyatembeza macho yangu nikiyatathmini kwa haraka mazingira ya mle jikoni nikaondoka eneo lile na kupita kwenye ukumbi wa chakula na niliposonga mbele nikajikuta nikitokea kwenye sebule kubwa iliyokuwa na makochi makubwa manne ya sofa ya vitambaa vyeusi yaliyopendeza huku yakiwa yamepangwa katika mtindo wa kuizunguka meza fupi nyeusi ya kioo iliyokuwa katikati ya sebule ile.

Wakati nikipiga hatua zangu kuyatathmini vizuri mandhari yale mbele yangu nikaiona milango miwili ya kioo, nikaufuata mmoja nikiamini ungenipeleka kwenye vyumba vya kulala, sikujua kama ulikuwa umefungwa au ulirudishiwa tu. Niliufikia nikausukuma na kutokea kwenye ukumbi mpana na hapo nikaiona milango mitatu.

Endelea...
 
taharuki..jpg

305

Niligundua kuwa mlango wa kwanza ulikuwa wa kwenye maliwato ya jumuia, nikaachana nao na kuufuata mlango wa pili uliofunikwa na pazia refu, nikasogeza pazia pembeni na kushika kitasa kisha nikakinyonga taratibu huku nikiusukuma mlango, ukafunguka na kuniruhusu kuingia ndani. Kwa kupitia mwanga hafifu uliopenya niliweza kuona mle ndani.

Kilikuwa chumba kikubwa chenye kitanda kipana cha futi sita kwa sita. Kitanda hicho kilikuwa kimefunikwa vizuri kwa shuka nzuri na mito ya kuegemea. Kwa upande wa mbele kitanda kile kilitazamana na kabati kubwa la nguo ambalo milango yake ilikuwa imefungwa.

Nililifungua lile kabati na kuona nguo nyingi za kiume, zikiwemo sare maalumu za polisi zenye tepe na alama ya ngao na nyota moja mabegani, zilizokuwa zimetundikwa kwenye kining’inizo maalumu cha nguo kilichokuwa ukutani. Nikaachana kwanza na lile kabati na kupiga hatua zangu taratibu hadi kando ya kitanda huku nikiyatembeza macho yangu mle ndani. Nikauona mlango mwingine uliokuwa kwenye kona ya chumba kile kwa upande wa kulia na kugundua kuwa ulikuwa wakuelekea kwenye chumba cha maliwato.

Nilielekea kwenye mlango ule na kuusukuma, macho yangu yakajikuta yakitazamana na sinki kubwa la kuogea pamoja na choo cha kukaa cha marumaru kilichopakana na bomba dogo la maji.

Nikiwa nimeanza kuridhishwa na hali ya usalama wa mle ndani nikaanza kufanya upekuzi kwenye kile chumba nikianza na pale kitandani. Hakukuwa na kitu chochote cha maana. Kisha jitihada zangu nilizihamishia kwenye lile kabati la nguo lililokuwa likitazamana na kitanda cha mle ndani.

Nilipochunguza kwa makini na kuona droo mbili, kwenye droo ya kwanza niliikuta bastola ndogo aina ya 25 Revolver na magazini mbili zilizojaa risasi na mafaili matatu yenye taarifa zinazohusu upelelezi wa kesi za dawa za kulevya zilizokuwa zikishughulikiwa kwenye mahakama za Hakimu Mkazi Kisutu na Kinondoni. Droo ya pili ilikuwa imefungwa. Nikatia utundu wangu na ndani ya muda mfupi nikawa nimefanikiwa kuifyatua kabari ya droo ile na kuifungua.

Mle ndani hakukuwa na kitu kingine zaidi ya bahasha moja ya kaki ya ukubwa wa A4, niliichukua bahasha ile na kuanza kuichunguza. Ilikuwa bahasha nyepesi yenye kitu mfano wa karatasi nyepesi ndani yake na juu ya bahasha ile hakukuwa na maelezo yoyote.

Niliichukua bahasha ile na kuifungua kwa pupa, ndani yake kulikuwa na karatasi mbili, moja ilikuwa barua ya maelekezo maalumu iliyotakiwa kumfikia Mr. Andrew Adonis, Meneja wa Alpha Commercial Bank tawi la jijini Dar es Salaam. Karatasi nyingine ilikuwa ndogo na nilipoitazama vizuri nikagundua kuwa ilikuwa hundi na ilikuwa na jina la Yusuf Ismail Kambi.

Kilichonishangaza zaidi ni kiasi cha fedha kilichokuwa kimeandikwa kwenye hundi ile kilikuwa kikubwa mno kuweza kutolewa na tawi la benki kama lile. Shilingi milioni mia tisa na hamsini! Si kiasi kidogo. Nikashikwa na kihoro cha kutaka kujua huyu SSP Yusuf Kambi alikuwa amefanya kazi gani hata alipwe kiasi kikubwa cha fedha namna ile? Na fedha zile zilikuwa zinatoka wapi? Nilijiuliza bila kupata majibu.

Chini ya hundi ile kulikuwa na tarehe ambayo ilionesha kuwa hundi ile ilikuwa imesainiwa siku hiyo hiyo ikiwa na saini iliyoandikwa kwa hati safi. Niliitazama saini ile kwa umakini, hata hivyo sikuweza kufahamu ilikuwa ya nani kwa kuwa ilikuwa ngeni kabisa machoni mwangu.

Niliitazama ile hundi kwa namna ya kuitathmini kana kwamba ndiyo kitu pekee nilichokuwa nikikihitaji. Kisha barua na ile hundi nikavirudisha kwenye bahasha na kuendelea kufanya upekuzi, hata hivyo sikuona kitu kingine cha kunivutia. Nikaitazama saa yangu ya mkononi na kugundua kuwa ilikwisha timia saa nane na nusu, nikaamua kutoka ndani ya chumba kile na kuelekea kwenye chumba kingine.

Humo pia nilikuta kitanda kikubwa na kabati la ukutani lakini hakukuwa na chochote cha maana kwani ilionesha wazi hakukuwa na mtu aliyekuwa akilala mle. Nikatoka na kurudi sebuleni nikiwa na mpango wa kwenda kwenye ule mlango mwingine wa kioo niliouona kule sebuleni.

Na hapo nikajikuta nikiwa uso kwa uso na ACP Richard Mwamba, Mkuu wa Upelelezi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam (ZCO) aliyekuwa ameketi kwenye sofa pasipo wasiwasi wowote, ni kama aliyekuwa akinisubiri kwani aliponiona akasimama katikati ya ile sebule huku uso wake ukichanua kwa tabasamu. Bastola aina ya 25 Revolver ikiwa mkononi.

ACP Mwamba alikuwa mrefu mwenye mwili ulioshiba mazoezi ya uhakika na alikuwa amevaa T-shirt nyekundu na suruali ya bluu ya dengrizi. Nilishtuka kidogo kumwona pale muda huo.

“Habari yako, Mr. Sizya?” ACP Mwamba alinisalimia huku akinitazama kwa tabasamu lililojaa dharau, kisha akaniuliza, “Nimekushtua, eh?”

Sikumjibu. Ili kuitowesha hofu iliyoanza kuzitawala hisia zangu nilipiga moyo konde huku nikiupisha utulivu kichwani mwangu. Kisha nilianza kupiga hatua kwa kujiamini nikitaka kuelekea kwenye mlango wa kutokea lakini ACP Mwamba akanielekezea mtutu wa bastola yake kichwani.

“Tulia hivyo hivyo… hatua moja tu nafumua kichwa chako kwa risasi,” sauti yake kavu ilinionya. Kisha akaongeza, “Niambie umefuata nini humu ndani?”

Nilimtazama nikiwa nimekunja uso wangu, nikataka kumjibu lakini nikajizuia na kubaki kimya. Nilijua kabisa kuwa ACP Mwamba hakufahamu kuwa nilikuwa Ofisa Usalama wa Taifa bali alinifahamu kama mwandishi wa habari za uchunguzi. Kwa kumwona pale nilijua kuwa alikuwa kundi moja na akina SSP Yusuf Kambi waliotaka kuniua, kwani japokuwa alisifika sana kwa kupambana na wahalifu jijini Dar es Salaam yakiwemo majambazi sugu lakini ni watu wachache sana tulioufahamu ukweli kuwa, alikuwa mmoja wa wanausalama mafisadi wasio na maadili.

Kikapita kitambo fulani cha ukimya huku tukitazamana kwa macho ya tahadhari. ACP Mwamba aliutazama mkono wangu wa kushoto ulioshika bahasha kisha akayarudisha macho yake usoni kwangu.

“Umekuja kufanya nini hapa?” ACP Mwamba aliniuliza tena huku akiwa amenikazi macho.

“Na wewe upo hapa kufanya nini?” nilimuuliza huku nikimtazama moja kwa moja machoni, akili yangu ilianza kufanya kazi haraka sana.

“Hiyo si kazi yako,” ACP Mwamba alinijibu kwa dharau. “Kwani hujui mimi ni nani?”

“Najua…” nilimjibu. “Wewe ni askari shupavu unayesifiwa kupambana na wahalifu sugu mchana, lakini usiku unashiriki kwenye uhalifu!”

Kwa kusema vile nikaamwona ACP Mwamba akishtuka kidogo japo alijitahidi kuuficha mshtuko wake. Alitaka kusema neno lakini akasita na kushusha pumzi. Kikapita kitambo kingine cha ukimya huku tukitazamana katika namna ya kusomana. Akili zetu zilikuwa zinaongea mengi kuliko midomo.

Endelea...
 
Back
Top Bottom