Simulizi: Harakati za Jason Sizya

Simulizi: Harakati za Jason Sizya

I know, ila sometimes nakuwa sina bando au matatizo ya umeme. Nitajitahidi, kama nitaweza nitupie jioni hii, vinginevyo tukutane hapa kesho...
Bishop weka namba yako hapa,sisi wapenda riwaya tutajitahidi kukuwezesha!
 
utata.JPG

370

Wazimu wa hatari!




Saa 7:55 usiku…

HATIMAYE tulitoka ndani ya uzio wa ile nyumba yenye mitambo ya mawasiliano na kuondoka tukijigawa kila mmoja na njia yake, hatukutaka kuongozana kwa sababu za kiusalama. Wakati nikitembea kichwa changu kilijaa maswali mengi juu ya yote tuliyokuwa tukiyapitia kwenye operesheni ile hasa aina ya watu tuliokuwa tukipambana nao.

Kitendo cha kukuta mitambo ya mawasiliano, tena ya kisasa, kwenye ile nyumba kilikuwa kimeibua mjadala mkubwa kichwani mwangu. Nilijikuta nikiwa na maswali kadhaa; nyumba hiyo ilimilikiwa na nani? Mitambo ile ya mawasiliano ilifungwa lini? Kwa ajili gani? Maswali haya pamoja na ule ukweli kwamba aina ya watu tuliokuwa tukipambana nao kila tulipopita ilitufanya kutafakari mara mbili juu ya uzito wa jambo tulilokuwa tukilichunguza.

Na hivyo, kabla hatujaondoka kjwenye nyumba ile yenye mitambo ya mawasiliano, Daniella alimpigia simu usiku ule ule mkuu wa kikosi maalumu cha kushughulika na operesheni hatari (SOG), Kanali Othman Mjaka, na kumweleza yote yaliyotokea na yaliyokuwa yakiendelea ndani ya nyumba ile kisha alimwomba atume haraka makomando wa SOG kuilinda nyumba ile, kwa sababu nyumba ilihitaji askari makini wenye mafunzo ya hali ya juu ya ukomando kuilinda.

Kanali Mjaka alishtushwa sana na taarifa zile na kuahidi kutekeleza ombi letu mara moja huku akituambia kuwa angewasiliana na mkurugenzi mkuu wa Idara ya Usalama wa Taifa usiku ule ule, si hivyo tu, pia aliahidi kufika mwenyewe Mtwara mara moja.

Baada ya kuachana na Daniella nilitembea nikiifuata barabara ya mtaa ule wa Duara, lengo langu likiwa nifike mwisho wa mtaa ule na kuchukua uelekeo wa kule tulikokuwa tumeliacha gari letu. Muda wote nikitembea mkono wangu mmoja nilikuwa nimeutumbukiza kwenye mfuko wa koti langu kuikamata bastola yangu vyema.

Niliitazama saa yangu ya mkononi nikaona kuwa dakika moja tu ilikuwa imebakia kutimia saa nane za usiku, nikajiambia kuwa bado tulikuwa na kazi ngumu ya kuhakikisha tunazijua mbivu na mbichi kabla hakujapambazuka.

Muda ule barabara ile ilikuwa katikati ya giza isipokuwa mwanga hafifu wa taa zilizowaka toka kwenye nyumba kadhaa katika mtaa ule. Mtaa ule na mingine ya jirani usiku huu ilikuwa pweke sana na yenye ukimya wa kutisha na hali ile ilinipa hadhari na hofu kidogo. Nilikuwa nakaribia kufika mwisho wa ule mtaa na kisha nivuke ng’ambo ya pili ya Barabara ya Njombe.

Kabla sijafika kule ili nikunje kuelekea kule tulipokuwa tumeliacha gari letu nikakumbuka kutimiza wajibu wangu wa kujilinda kwa kugeuka nyuma kuhakikisha kuwa hakukuwa na mtu au watu waliokuwa wakinifuatilia. Wakati akili yangu ikiamini kuwa mambo yalikuwa shwari hisia zangu ziliniambia kuwa nilikuwa najidanganya.

Kiasi cha umbali usiopungua mita hamsini nyuma yangu niliwaona watu watatu wakiwa katika mavazi meusi wakiharakisha kuja uelekeo wangu. Moyo wangu uliingiwa na baridi ya ghafla ingawa sikuwa na uhakika kuwa watu wale walikuwa wakinifuata mimi lakini nafsi yangu iliniambia lazima nichukue tahadhari.

Shaka ilikuwa imeniingia, wasiwasi juu ya jambo la hatari ukazidi kuzitekenya fikra zangu, nywele zikanicheza na kijasho chembamba kikaanza kunitoka. Ingawa sikuwa mgeni na namna ile ya ufuatiliwaji katika harakati zangu kadhaa za kijasusi nilizowahi kupitia lakini nilitaka kutafuta uhakika juu ya hisia zangu.

Ili kupata uhakika nilianza kuivuka ile barabara na kuhamia upande wa pili huku tayari kidole changu cha shahada kikiwa kimeshagusa triger ya bastola yangu mfukoni.

Muda huo huo nikaisikia sauti ya Daniella akanitaarifu kupitia kifaa maalumu cha mawasiliano kilichopachikwa kwenye sikio langu kuwa kulikuwa na watu wawili walikuwa wakimfuatilia kwa nyuma na kwamba walikuwa wamevaa mavazi meusi. Mara moja nikatambua kuwa watu hao walikuwa kundi moja na hawa waliokuwa wakinifuatilia.

Nilimweleza kuwa nami nilikuwa nikifuatwa na watu watatu nyuma yangu. Tukakubaliana tuwachezeshe nachi na wakati huo nikitafuta namna ya kufika kule tulikoacha gari letu bila watu hao kupafahamu kisha niwasiliane na Daniella kujua uelekeo wetu ni upi. Safari hii mimi ndiye niliyekuwa na ufunguo wa gari.

Wakati nikivuka ile barabara nikageuka tena nyuma kuwatazama wale watu na hapo nikawaona wawili kati ya wale watu nyuma yangu nao wakivuka ile barabara kunifuata. Akili ya haraka ikanijia kichwani, sikumaliza kuvuka ile barabara, badala yake nikarudi ule upande niliotoka na safari hii macho yangu yalikuwa makini zaidi kuzitazama nyendo za wale watu.

Wale watu na wao wakarudi haraka wakihamia upande wangu. Sasa nikaanza kuchanganya miguu yangu kuelekea mbele. Na hapo nikawaona wale watu na wao wakianza kukimbia taratibu wakinifuata na hapo nikaanza kutimua mbio utadhani niko kwenye mashindano maana niliamini kuwa uzembe wowote ungesababisha balaa kwangu.

Hata hivyo wale watu walionekana kuwa makini sana na nyendo zangu kiasi cha kutonipa nafasi ya kuwatoroka kirahisi na badala yake walijigawa, mmoja akahamia upande wa kushoto, mmoja akabaki nyuma yangu na mwingine akahamia upande wa kulia na mbio zao zilikuwa za uhakika.

Hatua chache mbele yangu nilikiona kibarabara chembamba cha mtaa kilichoingia upande wa kushoto, hivyo nilipiga mahesabu kuwa mara baada ya kukifikia kile kimtaa ningepata nafasi nzuri ya kupambana na wale watu kwa vile kulikuwa na sehemu nzuri ya kujibanza.

Hata hivyo kabla sijatimia azma yangu wale watu nyuma yangu wakawa ni kama walioshtukia dhamira yangu ya kutaka kuwatoroka kupitia kile kimtaa hivyo wakaanza kunifyatulia risasi. Lakini walikwisha chelewa kwani niliwahi kujitupa chini haraka na kujiviringisha kama gurudumu la gari nikipotelea kwenye kimtaa kile, hivyo risasi zao zikaambulia patupu na hakuna iliyonipata.

Kisha niliinuka na kukimbia haraka sana nikaenda kujibanza kwenye mti mmoja mkubwa huku nikitweta, mapigo ya moyo wangu yalienda mbio isivyo kawaida na kijasho chepesi kilinitoka mwilini.

Mara nikasikia vishindo vya watu wakija upande ule na sasa nilikuwa na uhakika kuwa wale watu walikuwa mbioni kunifikia, nikaikamata vyema bastola yangu mkononi na kuchungulia kwenye ile kona ya kichochoro. Nikamwona mtu mmoja akiambaa ambaa na ukuta wa nyumba moja akija pale kwenye mti mkubwa nilipojificha.

Sikumkawiza niliachia risasi moja makini iliyokifumua kichwa chake, ikamsomba kimo cha mbuzi na kumtupa chini chali, na ule ndiyo ukawa mwisho wake.

Kabla wale wengine wawili hawajajua nini wafanye nikaruhusu risasi nyingine itoke na kumchapa yule mtu wa pili risasi ya kifuani, sehemu ya moyo, naye akarushwa hewani na kutupwa chini kinyumenyume akiwa maiti. Kuona vile yule mtu wa tatu akasita kunifuata na badala yake nikamwona akirudi nyuma haraka na kupotelea gizani.

Endelea...
 
utata.JPG

371

Sikutaka kuamini kuwa baada ya yule mtu wa tatu kukimbia basi hali ilikuwa shwari, hivyo nilitoka pale mafichoni na kuanza kutimua mbio huku bastola yangu nikiwa nimeikamata vyema mkononi, nilikatiza vichochoro nikaelekea upande wangu wa kushoto, nia yangu ilikuwa niende nikatokezee katika barabara moja ambayo ingeniongoza hadi mahali tulikoliacha gari letu.

Wakati nikitimua mbio niligeuka nyuma kuangalia usalama lakini sikuweza kuona kitu wala kusikia sauti ya chochote cha kunishtua zaidi ya mitupo ya mapigo yangu ya moyo na vishindo vya hatua zangu ardhini.

Kabla sijafika mbali sana katika mbio zangu hisia mbaya zilianza kunijia akilini kuwa nilikuwa naelekea kwenye mdomo wa mauti, na hapo nikapunguza mwendo huku nikianza kuziogopa hisia zangu. Niligeuka tena kutazama nyuma lakini sikuona kitu chochote cha hatari na hapo nikajiona kama niliyeanza kuwa mwoga pasi na sababu.

Baada ya mbio za kitambo fulani nikawa nimefika mahala tulipoliacha gari letu, nikasimama sehemu na kuangaza macho yangu huku na kule katika namna ya kuhakikisha eneo lilikuwa salama. Sikuona chochote cha kunitisha, hali ilikuwa shwari kabisa.

Niliwasiliana na Daniella kujua kama alikuwa amefanikiwa kuwadhibiti wale watu wawili waliokuwa wakimfuatilia. Daniella aliniambia kuwa yalitokea mapambano makali kati yake na wale watu na akafanikiwa kumuua mtu mmoja na yule mwenzake alimvunja kiuno, na sasa alikuwa anataka kumhoji ili kupata taarifa muhimu.

Nikiwa sasa najipongeza kufikia sehemu tulipoacha gari letu, taratibu nikaanza kupiga hatua zangu kuelekea kwenye mlango wa mbele, upande wa dereva, wa gari letu lakini nikiendelea kuwa makini sana. Macho yangu yaliendelea kutambaa yakiangaza huku na kule. Bado sikuona dalili yoyote mbaya au uwepo wa kitu cha hatari eneo lile. Hali ilikuwa tulivu mno.

Kabla sijalifikia gari niliamua kubonyeza kitufe cha rimoti kilichounganishwa na funguo za gari na sauti ndogo ya kuashiria kuwa milango ilikuwa imefunguka ikasikia. Hata hivyo wakati nilipokuwa katika harakati za kutaka kushika kitasa cha mlango wa gari ili nifungue macho yangu yakajikuta yakivutiwa na kitu fulani cheupe kilichokuwa chini, karibu na gurudumu la mbele la gari, upande ule wa dereva, nikawasha simu yangu na kumulika sehemu ile.

Na hapo nikakiona kipande cha karatasi kilichoonekana kama kiliwekwa hapo makusudi kikiwa na ujumbe, nafsi yangu ikatamani sana kujua karatasi ile ilikuwa na ujumbe gani, ulitoka kwa nani na ulikusudiwa umfikie nani?

Hivyo haraka nikainama ili kuiokota ile karatasi, na muda huo huo nikasikia sauti mbaya ya mpasuko mkubwa wa kioo cha dirisha la gari letu. Sauti ile na mpasuko wa kioo cha dirisha ilinifanya mara moja nitambue kilikuwa kitu gani na hivyo nikawahi kujitupia kando.

Kumbe kitendo kile cha kuinama ili niichukue ile karatsi kilikuwa kimeniokoa mbali na risasi hatari ya mdunguaji iliyonikosa kichwa changu na kuishia kukisambaratisha kioo cha dirisha upande ule wa dereva, huku chenga chenga za vioo zikimwagika na kusambaa kila mahali.

Kitendo kile kilifanya ile karatasi initoke mkononi mwangu na kudondoka chini. Sikuwa na muda wa kuiokota na badala yake kwa wepesi sana niliviringika pale chini kama gurudumu la gari huku nikiwa siamini kama nilikuwa nimesalimika katika shambulizi lile. Risasi ya pili ikatua kando yangu wakati nikiviringika pale chini kuufuata mti mmoja mkubwa uliokuwa kando.

Zilikuwa risasi za mdunguaji ambaye sikuwa na shaka yoyote kuwa kwa muda mrefu alikuwa akinitazama tangu nikifika eneo lile.

Wakati nilipokuwa nikijificha nyuma ya mti ule mkubwa, risasi nyingine ya tatu ikapunyua nywele zangu, na hapo nikaanza kuona hatari ikinikaribia, hivyo nikawahi kujitupa tena chini na kuangukia mbali kabisa kwenye mtaro na kisha nikajiviringisha chini mtaroni nikijikinga kwenye ukuta fulani mfupi dhidi ya risasi za yule mdunguaji huku nikiikamata vyema bastola yangu mkononi.

Nikiwa pale nyuma ya kijiukuta kile nilitambua kuwa bunduki aina ya US Barrett M82, itumiwayo wa wadunguaji hatari duniani ilikuwa kazini. Ili kuyaokoa maisha yangu sasa nikawa na kazi moja tu; ya kuhama toka sehemu moja kwenda nyingine, kutoka mti mmoja kwenda mti mwingine huku akili yangu ikiwa makini zaidi kuchunguza risasi zile zilikuwa zikitokea upande gani toka eneo lile.

Sikuchukua muda kugundua kuwa upande wa pili wa eneo lile, tulipokuwa tumeacha gari letu, juu ya mti mmoja mkubwa wa kivuli uliokuwa ndani ya uzio wa jengo moja la ghorofa moja, ndipo risasi zile zilipokuwa zikitokea. Niligundua haraka baada ya kuuona mtutu wa bunduki namna ulivyokuwa ukitema cheche.

Na hivyo baada ya kugundua upande ambao risasi zilitokea nikaikamata vyema bastola yangu mkononi kisha nikachungulia na kuachia risasi moja yenye shabaha makini, mara nikaona risasi ile ikiniletea matunda kwani nilisikia sauti hafifu ya mtu aking’aka kwa maumivu, halafu bunduki ikaanguka chini huku yule mdunguaji akifuatia kwa kutanguliza kichwa chake. Risasi yangu ilikuwa imepita jichoni na kulifumua fuvu la mdunguaji yule.

Muda ule ule nikaisikia sauti ya Daniella ikivuma kwenye kifaa cha mawasiliano sikio kwangu.

March, are you there? ...unanisikia?” sauti ya Daniella iliongea akiniita kwa codename, yaani jina bandia la March.

Mimi na Daniella tulikuwa tumekubaliana kwenye operesheni ile kuitana majina kufuatia miezi tuliyozaliwa, hasa mmoja anapokuwa kwenye matatizo au anapohisi mwenziwe yuko kwenye matatizo. Mimi nilikuwa nimezaliwa mwezi wa tatu (March) na Daniella alizaliwa mwezi wa tano (May).

Hata hivyo nilitambua haraka kuwa sauti ya Daniella ilikuwa imetawaliwa na wasiwasi mwingi. Nikadhani labda alikuwa amefikwa na jambo la hatari.

March unanipata?” sauti ya Daniella ilijirudia, na safari hii kwa nguvu kidogo.

“Ndiyo, nakupata May, any trouble?” nilimuuliza Daniella kwa wasiwasi. Nikamsikia akishusha pumzi za ahueni.

“Huku kwa sasa hali ni shwari ila nahisi huko kwako bwawa limeingia luba,” Daniella aliongea kwa wasiwasi.

Yes! Adui waliweka mtego kwenye gari letu, hapa nilikuwa napambana na mdunguaji…” nilisema huku nikisimama kwa tahadhari na kuhama eneo lile haraka kisha nikaanza kunyata nikielekea upande mwingine huku bastola yangu ikiwa mkononi na macho yangu yakiwa makini kuli-scan eneo lote. “…kioo cha gari letu kimechakazwa.”

Japokuwa sasa risasi zilikuwa zimekoma lakini sikuwa na imani kabisa kama hali katika eneo lile ilikuwa shwari. Niliamini bado kulikuwa na watu wengine eneo lile na hivyo nikajibanza nyuma ya gogo kubwa la mti uliokatwa. Macho yangu yalikuwa makini kutazama kule kwenye lile jengo la ghorofa moja.

Oh my God! Umesalimika?” Daniella aliwahi kuniuliza kwa taharuki.

Endelea...
 
utata.JPG

372

“Niko salama. Ila nimemshusha mdunguaji lakini cha moto nimekiona,” nilisema.

“Uko wapi sasa?” Daniella aliniuliza.

“Bado nipo eneo hili nyuma ya gogo la mti,” nilisema huku macho yangu yakiwa makini kutazama huku na kule.

Okay! Hold on, March, I am coming right now,” Daniella alisema na kisha nikasikia sauti ya mitupo ya hatua zake na mihemo yake wakati akikimbia.

Be careful, May, hali bado ni tete sana,” nilimuonya Daniella.

Don’t worry, I know how to take care of myself,” Daniella alisema, na mawasiliano yetu yakaishia hapo.

Mara nikaikumbuka ile karatasi iliyoniponyoka wakati nikishambuliwa na risasi za mdunguaji. Hivyo sikutaka kusubiri, na badala yake haraka nikajitoa nyuma ya lile gogo la mti kisha nikatimua mbio kwa tahadhari kuelekea kule kwenye gari. Nikafanikiwa kufika na kuinama ili niiokote ile karatasi.

Niliweza kuiokota lakini kabla sijasimama nikasikia sauti ya mvumo wa kitu fulani kikija kwa kasi eneo lile. Akili yangu ilikuwa inafanya kazi haraka na niliitambua sauti ile hatari ya mvumo kwani niliwahi kuisikia mara mbili katika harakati zangu za kijasusi, hivyo nikawahi kuchupa nikijitupia chini nyuma ya mti mkubwa.

Kombora zito la silaha kali aina ya LPG lilikuwa limetumwa pale kwenye gari nilipokuwa na kunikosa, badala yake likasambaratisha gari letu, nililiona gari letu likinyanyuliwa juu na kisha kubwagwa chini huku sauti kali ya mlipuko wa lile bomu ikisikika.

Nikiwa pale nyuma ya mti mkubwa nikaanza kusikia mvua ya risasi ikirindima eneo lile kwa mipigo ya ufundi, nikatambua kuwa nilikuwa napambana na watu wengi na kuwa bunduki US Barrett M82 zilikuwa kazini.

Niliangaza macho yangu kutazama mbele ya barabara iliyokatisha eneo lile upande wa kushoto, juu ya lile jengo la ghorofa moja nilikoamini kwamba risasi zile zilikuwa zikitokea. Hisia zangu zilikuwa sahihi kwani nilimwona mtu mmoja akihama kutoka sehemu moja kwenda nyingine, juu ya lile ghorofa.

Muda mfupi uliofuata mashambulizi ya risasi yakakoma kisha eneo lile likawa kimya kabisa. Hata hivyo sikufikiria kuondoka pale nilipokuwa nimejificha. Niliendelea kujificha huku masikio yangu yakiwa makini kusikiliza sauti yoyote yenye kuashiria hatari.

Nikiwa bado nimejificha pale nyuma ya mti nikasikia kishindo cha muanguko wa kitu kizito kama mtu kule kwenye lile jengo la ghorofa moja. Kishindo hicho kiliambatana na sauti ya mtu huyo kung’aka kwa maumivu. Kama umeme nikawahi kujitupa kwenye mtaro na kujiviringisha chini mtaroni.

Mara nikasikia kishindo kingine cha muanguko wa kitu kule kule kwenye lile jengo la ghorofa moja. Na kishindo kingine tena cha tatu kilichoambatana na yowe kali la mtu. Nikajiviringisha haraka na kutokea upande wa pili wa ule mtaro bastola yangu ikiwa imetuama vyema kwenye kiganja cha mkono wangu, huku nikiangaza macho yangu huku na kule. Sikuona mtu yeyote.

Nikasikiliza kwa umakini nikihisi labda wale adui walikuwa wanaruka toka ghorofani ili kuja kupambana nami ana kwa ana, lakini sikuweza kusikia sauti nyingine na badala yake nikahisi kuguswa na kitu cha baridi nyuma ya shingo yangu, kitu ambacho moja kwa moja nilitambua kuwa ulikuwa ni mtutu wa bunduki. Mwili wangu ukaingiwa na baridi. Nilichofanya ni kutulia tu kama maiti. Sikutikisika wala kuinua mkono wangu uliokuwa na bastola.

“Jason!” niliisikia sauti ya Daniella ikiniita nyuma yangu.

Na hapo nikageuka kutazama nyuma yangu na kumwona Daniella akiwa amesimama kwa ukakamavu, mkono mmoja kashika bunduki aina ya US Barrett M82 na mkono mwingine ameshika yale mafaili mawili mekundu tuliyoyachukua toka kwenye ile nyumba yenye mitambo ya mawasiliano.

Nilitambua kuwa ile bunduki aliitoa kwa wale adui waliomfuatilia mwanzo, na hivyo moja kwa moja nikatambua kuwa vile vishindo vya muanguko wa kitu nilivyovisikia ilikuwa ni kazi ya Daniella akiwashughulikia adui zetu kwa shabaha maridadi.

“Daniella!” niliita huku nikiinuka haraka toka pale chini nilipokuwa nimejificha.

“Hapa si mahali salama, tuondoke haraka,” Daniella aliniambia na kuitupa ile bunduki chini, akabakiwa na bastola yake na yale mafaili mawili mekundu, kisha akaanza kutimua mbio kuelekea upande fulani. Sikuwa mbishi nikamfuata nyuma.

Wakati nikitimua mbio kuondoka eneo lile masikio yangu yalikuwa makini kusikiliza sauti yoyote yenye kuashiria hatari, mara nikasikia vishindo vya watu wakitimua mbio kuja eneo lile. Niligeuza shingo yangu kutazama nyuma nikaona kundi la watu wasiopungua watano wakiwa na mavazi meusi na bunduki za kivita wakitufuata.

Wakati tukikimbia risasi zilianza kuvuma karibu yetu na moja ikanipunyua begani lakini sikusimama. Tulizidi kutokomea kizani tukiivuka barabara ya Mtaa wa Nyali, tukapinda upande wa kushoto bila kujua tulipokuwa tunaelekea. Nilichofanya ni kumfuata Daniella tu. Sikuamini macho yangu kwa jinsi Daniella alivyokuwa akizifahamu njia na vichochoro vya mji wa Mtwara.

Watu hao hawakuonesha kukata tamaa wala kukubali kutukosa, walizidi kuja nyuma yetu kwa kasi sana lakini kwa vile tulishawaacha mbali hawakufanikiwa kutupata. Tulikimbia hadi tukafika eneo moja lilipokuwa na uzio wa seng’enge zenye miiba na urefu wa kama mita mbili hivi kwenda juu, nikamwona Daniella akipaa juu kama kishada huku akijiviringisha sarakasi kama gurudumu na alipotua chini alikuwa tayari yupo upande wa pili wa uzio ule wa seng’enge.

Mimi hata sikujua nilirukaje ila nilishtukia tu nipo hewani nikipaa kama karatasi kwenye upepo huku risasi zikinikosa kosa na kisha nikaangukia upande wa pili wa uzio ule. Bila ya kufanya ajizi nikainuka haraka na kuendelea kutimua mbio nikimfuata Daniella huku risasi zikiendelea kunikosa. Niliamini kuwa ni Mungu tu aliyekuwa akiniokoa nisipatwe na risasi zile.

Tulizidi kusonga mbele na hatimaye tukatokea kwenye barabara moja tulivu sana iliyopita kwenye eneo pana lenye miti mingi mikubwa, nilipotazama vizuri nikagundua kuwa lilikuwa eneo la Mtwara Technical Teachers Training College, na hapo tukaliona lori moja la Dangote lililokuwa limebeba mifuko ya saruji likiwa katika mwendo wa kujikongoja.

Nilishangaa usiku ule kuliona lori lenye saruji katika barabara ile na sikuelewa lilikuwa linaelekea wapi, na hapo nikakumbuka kutazama saa yangu ya mkononi na kugundua kuwa ilishatimia saa nane na dakika hamsini za usiku. Tukaongeza kasi ya mbio na kulirukia lile lori nyuma ambako tulijibwaga juu ya mifuko hiyo ya sementi huku tukitweta.

Lile lori lilizidi kusonga mbele likiyavuka majengo mengine ya taasisi za elimu kama Mtwara Sisters Secondary School na Architects and Engineers Mtwara na kwenda kutokea kwenye barabara nyingine ambayo sikuifahamu kisha likaingia kushoto kuifuata barabara ile hadi tulipokwenda kutokea kwenye makutano ya Barabara za Bandari na Shangani.

Endelea...
 
utata.JPG

373

Tukaliona lile lori likiingia upande wa kulia kuifuata Barabara ya Bandari tuliendelea kuwa makini, tukayavuka majengo kadhaa kama St. Michael Pre and Primary School, Chuo Kikuu Kishiriki cha Stella Maris Mtwara, Cathedral Mtwara Catholic, eneo pana lenye msitu mdogo la JWTZ Mtwara, na baada ya mwendo mfupi hivi tukaliona lile lori likianza kupunguza mwendo, na hapo Daniella akanipa ishara kuwa tushuke.

Tuliruka haraka na kuanza kutembea haraka na kukatisha barabara ile ya Bandari tukaufuata mtaa fulani upande ule wa kulia, muda wote tulikuwa kimya na mara tukatokezea kwenye kanisa moja kubwa huku macho yetu yakiwa makini kuangaza huku na huko katika namna ya kuthibitisha kuwa hakukuwa na mtu aliyekuwa akituzingatia.

Niligundua kuwa lile lilikuwa kanisa kwani niliona bango kubwa mbele ya jengo, lililokuwa limeandikwa Living Paradise Ministries. Lilikuwa jengo kubwa lenye paa refu na imara, na ukutani kulikuwa na madirisha makubwa marefu ya vioo vyenye rangi. Tukalipita lile kanisa na kwenda moja kwa moja upande wa nyuma wa kanisa hilo ambako kulikuwa na nyumba mbili kubwa za kisasa.

Zilikuwa nyumba za kisasa zilizozungushiwa uzio wa ukuta mrefu na geti jekundu mbele yake. Tulilipita lile geti huku tukilitazama halafu tukageuka kukazitazama nyumba za jirani za eneo lile ambazo zilikuwa kimya kabisa na wenyeji wake walikuwa wametopea katika usingizi.

Tukawa kama tunauzunguka uzio ule wa ukuta kwa upande wa kulia tukiliachaa lile geti kubwa la mbele, tulipokuwa eneo la nyuma tukatazama huku na huko na haraka tukaukwea ule uzio kininja na kutua ndani ya bila vishindo.

Mara tu tulipoingia mle ndani ya uzio macho yangu yalizunguka haraka kuyachunguza vizuri mazingira ya nyumba zile mbili. Kulikuwa na miti mitatu mikubwa, miwili ilikuwa ya mwembe na mti mmoja sikuelewa ulikuwa mti gani. Katika kutazama zaidi nikagundua kuwa mti mmoja wa ulikuwa mbele ya nyumba iliyokuwa mwanzoni na mti mwingine ulikuwa ubavuni mwa nyumba ile. Mti wa tatu ulikuwa mbele ya nyumba ya mwisho.

Jason, are you okay?” hatimaye Daniella aliniuliza kwa sauti ya kunong’ona huku akinitazama mwilini kwa namna ya kunikagua, wakati tukiwa tumesimama ndani ya uzio wa lile kanisa.

I’m okay,” nilijibu kwa ufupi huku nikigeuza shingo yangu kutazama huku na huko kwa tahadhari kubwa. “Mbona tumekuja hapa?”

“Hapa ni kwa mjomba wangu, tunatakiwa kupata sehemu tulivu ili kuyachunguza haya mafaili,” Daniella alisema huku akinionesha yale mafaili mawili mekundu halafu akashusha pumzi. “Siamini kama tumesalimika maana hawa jamaa wamejipanga vilivyo”

“Unamwamini mjomba wako?” nilimuuliza Daniella kwa wasiwasi kidogo nikitaka kupata hakika.

Absolutely!” Daniella alisema kwa kifupi na kunipa ishara nimfuate. Alionekana kutotaka kuzungumza mengi kuhusu mjomba wake jambo lililonifanya kuwa na shaka kidogo.

Hata hivyo nilimfuata, tukaipita ile nyumba iliyokuwa mwanzoni na kuelekea kwenye ile nyumba ya mwisho ambayo ilikuwa na madirisha makubwa ya kisasa na baraza kubwa mbele yake iliyopangwa seti moja ya makochi ya sofa.

Chini ya mti wa mwembe uliokuwa mbele ya nyumba ile ya mwishoni kulikuwa na viti vya kupumzikia jirani na banda la wazi la kulaza magari ambalo ndani yake kulikuwa na magari mawili yaliyoegeshwa, gari moja lilikuwa aina ya Toyota Landcruiser GX V8 la rangi nyeusi na lingine Toyota Prado TX la rangi ya fedha.

Mandhari ya eneo lile ilikuwa nadhifu sana iliyozungukwa na bustani nzuri ya maua ya kupendeza na katikati ya bustani hiyo kulikuwa kumetengenezwa njia nzuri ya kupita gari au kutembea kwa miguu kwa vitofali vidogo vilivyokuwa vinavutia.

Nilisimama pale mbele ya nyumba wakati Daniella akielekea kwenye dirisha moja na kuanza kugonga taratibu. Baada ya kugonga mara kadhaa hatimaye tkasikia sauti ya kiume kutokea ndani ikasikika ikiuliza, “Nani?”

“Ni mimi Daniella, nahitaji msaada wako mjomba,” Daniella alisema na kushusha pumzi za ndani kwa ndani.

Kisha kukawa kimya kabisa, na baada ya takriban dakika moja na nusu tukasikia kitasa cha mlango mkubwa wa mbele kikizungushwa halafu muda huo huo mlango ule ukafunguliwa. Mwanamume mmoja mtu mzima aliyevaa pajama akachungulia na kutuona. Alikuwa mrefu na mwenye mwili wa ukakamavu, kichwa chake kilianza kutawaliwa na mvi.

Alimtazama Daniella kisha macho yake yakahamia kwangu, na hapo nikamwona akishtuka kidogo, hata hivyo aliumeza mshtuko wake na kushusha pumzi.

“Karibuni ndani,” sauti yake tulivu ilitukaribisha huku mikono yake ikiwa imeshika Biblia.

“Ahsante!” tuliitikia huku tukiingia ndani, nikajikuta nikitokezea kwenye sebule kubwa iliyosheheni samani za gharama kubwa.

Pale sebuleni tulipita, tukaelekea kwenye mlango mmoja wa kioo, yule mzee aliufungua ule mlango halafu akatukaribisha ndani, na hapo nikajikuta nikitokea kwenye chumba kipana cha ofisi binafsi ya mzee yule.

Ile ofisi ilikuwa kubwa na ya kisasa yenye tarakilishi na vifaa muhimu vya kiofisi. Upande wa kulia kulikuwa na kabati moja la mbao na makabati mawili mengine ya chuma. Sakafuni kulikuwa zulia zuri la rangi nyekundu.

Upande wa kushoto ukutani kulikuwa na rafu ya mbao iliyopangwa vitabu vya dini na pembeni ya rafu ile ukutani kulikuwa na runinga kubwa. Mara moja tu tulipoingia mle ndani hali ya hewa nyepesi ikanifanya niyatembeze macho yangu mle ndani na hapo nikakiona kiyoyozi kimoja ukutani. Mara moja nikatambua kuwa ilikuwa ni sehemu aliyoitumia kwa maongezi ya faragha na wageni wake.

Yule mzee alitukaribisha kwenye viti viwili vilivyotizamana vilivyokuwa mbele ya meza kubwa yenye vitabu vingi vya kiroho, majarida na maandalio ya masomo ya kanisa, wakati yeye akiketi nyuma ya meza ile, kwenye kiti kikubwa cha kiofisi cha kuzunguka na chenye magurudumu madogo yaliyokiwezesha kuhama toka sehemu moja kwenda nyingine.

Nasi tukaketi kwenye viti vilivyotazamana huku nikiyatembeza macho yangu taratibu kuyatazama mandhari ya chumba kile. Halafu nikamwona yule mzee akiiweka Biblia yake juu ya meza huku akiendelea kututazama kwa umakini, na hapo nikapata nafasi nzuri ya kumchunguza vizuri mzee yule, nikatambua kuwa umri wake ulikuwa ni miaka sitini na ushee.

Tulimsalimia yule mzee kwa adabu, akaitikia huku akitutazama kwa utulivu na hapo nikajua kuwa bila shaka alikuwa ameshangazwa na ugeni wetu muda ule. Kisha alimuuliza Daniella kwa taharuki, “Daniella, mbona mmenijia usiku huu, halafu mmeingiaje humu ndani wakati geti limefungwa?”

“Ah, mjomba bwana…” Daniella alisema huku akiviminyaminya vidole vyake mikononi kama mtoto anayedeka, “hayo tutayaongea, mjomba, ila tambua huko mjini hali si shwari kabisa!”

Endelea...
 
utata.JPG

374

Yule mzee alimtazama Daniella kwa utulivu pasipo kusema neno. Sasa Daniella akaanza kutoa utambulisho mfupi. Na hapo nikafahamu kuwa yule mzee aliitwa Askofu Jerome Masinde, kaka wa mama yake Daniella, na alikuwa Askofu Mkuu wa Living Paradise Ministries.

Nilishtushwa kidogo na jina la mwisho la askofu yule, ‘Masinde’, kwa kuwa lilifanana na jina la mwisho la Rais Albert Masinde, ambaye ndiye sababu ya sisi kuwepo pale Mtwara.

Halafu Daniella alinitambulisha kwa yule askofu, katika namna ya kunipamba zaidi, na kwamba tulikuwa tumefika pale kwake usiku huo kutafuta hifadhi baada ya kushambuliwa. Hata hivyo, Daniella hakuwa amegusia suala la kutoweka kwa Rais Masinde.

Maelezo ya Daniella yalikuwa yamenyooka na hivyo wakati akimalizia kutoa utambulisho Askofu Masinde aliinuka na kunipa mkono japokuwa niliona mashaka kidogo katika uso wake.

“Na wewe ni mpelelezi?” hatimaye Askofu Masinde aliniuliza huku akinitazama usoni.

“Ndiyo! Mimi ni mpelelezi” niliongea kwa utulivu.

“Nilikufahamu tangu nilipokuona kwa mara ya kwanza. Mara nyingi nimekuwa nakutana na wapelelezi na baadhi yao wakitaka kunipeleleza juu ya huduma yangu,” Askofu Masinde aliongea kwa utulivu huku akigeuka kumtazama Daniella.

“Kwa hiyo, mko hapa kwa ajili ya upelelezi juu ya kitu gani hasa?” Askofu Masinde alimuuliza Daniella huku akimtazama kwa umakini.

Mimi na Daniella tulitazamana, hisia zangu ziliniambia kuwa tulipaswa kumwamini yule mzee na kumweleza ukweli kwani huenda angekuwa na msaada mkubwa kwetu hasa ikizingatiwa kuwa alikuwa mtumishi wa Mungu. Kwenye kazi za kishushushu wakati mwingine unapaswa kujiumbua (kusema ukweli wa kazi yako) ili upate taarifa muhimu unazozitaka. Hivyo nikaamua kumgusia juu ya kutekwa kwa Rais Masinde.

Mara tu nilipoongea juu ya kutekwa kwa Rais Askofu Masinde alinitazama kwa mshangao. “Albert ametekwa…!” aliongea kwa utulivu huku akitafakari.

“Ndiyo, na Idara ya Usalama wa Taifa haifahamu Rais alipo. Siku ya kwanza tu ya ziara yake hapa Mtwara akatekwa na kupelekwa kusikojulikana,” niliongea kwa utulivu.

Askofu Masinde hakusema neno, alikunja sura yake na kutazama dirishani kana kwamba alihisi uwepo wa mtu aliyekuwa akisikiliza maongezi yetu. Nilipomtazama vizuri nikatambua kuwa fikra zake hazikuwa pale bali zilikuwa kilomita nyingi nje ya chumba kile. Kisha kilipita kitambo fulani cha ukimya.

“Ulikuwa unafahamu kuhusu jambo hili?” nilijikuta nikisukumwa nafsini mwangu kumtupia swali lile Askofu Masinde huku nikimtazama usoni kwa makini. Swali langu likamfanya alegeze kidogo uso wake na kutabasamu kisha akakohoa kidogo kusafisha koo lake na hatimaye kuvunja ukimya.

“Ndiyo nafahamu,” Askofu Masinde alijibu na kutufanya mimi na Daniella tushikwe na mduwao wa aina yake na kwa sekunde kadhaa tukamtazama katika namna ya kutoamini maneno yale.

Loh! Hatimaye nilishusha pumzi taratibu na kuulegeza uso wangu huku nikiliruhusu tabasamu jepesi kuchomoza usoni mwangu kisha nikaketi vizuri kwenye kiti changu.

“Albert ni rafiki yangu mkubwa…” Askofu Masinde aliongea kwa utulivu. “Na alikuwa akifika hapa kunisalimia kila mara akija Mtwara.”

“Nataka kufahamu ni mazingira gani yaliyokufanya utambue kuwa Rais ametekwa?” nilimtupia swali lingine Askofu Masinde, swali lile lilimfanya aupishe utulivu kidogo huku akionekana kufikiri jambo kisha akaniambia.

“Ilikuwa kama saa saba za usiku niliposhtushwa kutoka usingizini na mlio wa simu yangu maalumu iliyokuwa mezani chumbani kwangu…” Askofu Masinde alisema huku akionekana kuzidi kuvuta kumbukumbu.

Hata hivyo nilimkatisha. “Simu hiyo ilitoka kwa nani?”

“Ilikuwa ni simu ya Albert, kutoka kwenye namba yake maalumu ambayo hakuwa akiitumia ovyo bali kwa watu maalumu sana na kwa shughuli maalumu, na mzungumzaji alikuwa ni Albert mwenyewe,” Askofu Masinde alisema na kuweka kituo.

Maelezo yale yalikuwa yameanza kunivuta hivyo nilimtazama Daniella, ambaye muda wote alikuwa mtulivu akimtazama mjomba wake kwa shauku kama mwewe aliyeona kifaranga cha kuku, kisha nikaiegemeza vizuri mikono yangu pale juu mezani huku nikimtazama yule mzee kwa umakini.

“Una hakika kuwa sauti ya mzungumzaji kwenye hiyo simu uliyopokea ilikuwa ni ya Rais Masinde mwenyewe?” nilimuuliza Askofu Masinde katika namna ya kutaka kupata uhakika.

“Nina uhakika kabisa kwani sauti ya Albert naifahamu vizuri sana kama ninavyoifahamu mistari ya kiganja changu,” Askofu Masinde alisema huku akichombeza utani.

“Mara baada ya kuipokea hiyo simu Rais alikueleza nini?” hatimaye Daniella aliuliza kwa mara ya kwanza.

“Sauti yake ilikuwa imetawaliwa na kitetemeshi cha hofu na mashaka wakati aliponieleza kuwa maisha yake yalikuwa hatarini, kwani makazi yake yalikuwa yamevamiwa na watu wasiojulikana, hivyo alinitaka kumsaidia na kumwombea kwa Mungu aepushiwe na mabaya,” Askofu Masinde alisema na hapo maelezo yake yakawa yameamsha hisia tofauti nafsini mwangu, sasa niliamua kuuruhusu utulivu kichwani mwangu huku nikitafakari kwa kina juu ya maelezo yale.

Hatimaye nikamuuliza, “Halafu nini kilifuata baada ya hapo?’’

“Nilimdadisi kwa kumuuliza kuwa ni kipi kilichokuwa kimemfanya ahisi kuwa alikuwa amefanyiwa uvamizi, akanieleza kuwa nyumba yake ilikuwa imezingirwa na wavamizi hao wasiojulikana na nje kulikuwa na majibizano ya risasi kati ya walinzi wake na wavamizi hao,” Askofu Masinde alisema na kuweka kituo kisha alitutazama kwa zamu kama mtu afikiriaye jambo.

“Wakati akikupigia simu alikuwa wapi?” hatimaye niliuliza Askofu Masinde kwa shauku baada ya kuhisi kuwa ukimya ulikuwa mbioni kushika hatamu mle ndani.

“Muda huo alikuwa amekimbilia chooni…” Askofu Masinde alisema.

“Baada ya hapo alikueleza nini?” Daniella aliwahi kumuuliza Askofu Masinde.

Askofu Masinde alimtazama Daniella kwa utulivu kisha akasema, “Hiyo ndiyo ilikuwa mara yangu ya mwisho kuisikia sauti ya Albert, kwani wakati nilipokuwa nikijiandaa kutia neno ghafla sauti yake ilitoweka hewani na simu yake ilikatwa kabisa na sikuweza kusikia chochote. Nilipoipiga ikawa haipatikani,” Askofu Masinde alisema kwa huzuni. “Hofu ikanishika, sikupata tena usingizi na badala yake nikaamka kutoka kitandani na kuanza kuomba nikimlilia Mungu amwepushie mabaya yote.”

Nilipomtazama Askofu Masinde usoni nikagundua kuwa uso wake ulikuwa umejawa sana na simanzi na hapo nikajua kuwa alikuwa amehuzunishwa sana na tukio lile la kutekwa kwa Rais.

“Kuanzia siku hiyo nimeshindwa kabisa kupata usingizi, na sasa nipo kwenye maombi maalumu na mfungo usio na kikomo kuomba rehema za Mungu ili amwepushe Rais wetu wa mabaya yoyote,” hatimaye Askofu Masinde alisema tena na kushusha pumzi.

“Kuna mtu mwingine yeyote uliyemweleza habari hizi za kutekwa kwa Rais?” nilimuuliza tena Askofu Masinde.

“Hapana! Ila mke wangu alipatwa na shaka lakini nikalazimika kumweleza uongo kuwa Rais alipata dharura na hivyo aliamua kukatisha ziara yake na kuondoka haraka usiku huo,” Askofu Masinde alisema.

Endelea...
 
utata.JPG

375

“Unaweza kuniambia urafiki wenu ulianzaje, na kama mna uhusiano wa kindugu maana majina yenu ya mwisho yanafanana!” hatimaye nilivunja ukimya na kumuuliza Askofu Masinde kwa shauku huku nikimtazama. Akacheka kidogo.

“Urafiki wetu ulianzia Sekondari ya Tabora tulikosoma darasa moja kuanzia kidato cha kwanza hadi cha nne na baadaye tukakutana tena Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Kuhusu mfanano wa majina yetu ya mwisho ndiyo sababu kubwa iliyotufanya kuwa karibu zaidi, na wengi hudhani sisi ni ndugu lakini ukweli hatuna undugu wowote,” Askofu Masinde alisema.

“Niseme tu tukio la kutekwa kwa Rais wetu limeishtua sana Idara ya Usalama wa Taifa na kutushangaza sana kwani hadi sasa nikifikiria bado sioni sababu yoyote walau ya kuhisi tu inayoweza kuhalalisha tukio la kinyama kama hili,” nilisema kwa huzuni, kisha nikaendelea.

“Mimi na Daniella tutajitahidi kufanya kila liwezekanalo katika kuhakikisha kuwa Rais wetu anapatikana kabla ya kesho mchana na yeyote aliyehusika na kitendo hiki cha kiharamia anaijutia nafsi yake.”

Na hapo maelezo yangu yalikuwa ya uhakika na kwa namna moja au nyingine yalionekana kumfurahisha sana Askofu Masinde kiasi cha kumfanya atabasamu.

“Ila nafahamu nini kinachoendelea, hili ni jambo hatari sana na linaweza kuyagharimu maisha yenu msipokuwa makini,” Askofu Masinde aliongea kwa utulivu huku maelezo yake yakiibua shauku ya aina yake usoni mwangu hali iliyonifanya niketi vizuri na kumtazama kwa umakini.

“Unafahamu nini?” nilimuuliza kwa udadisi na hapo yule mzee akanitazama kwa utulivu kabla ya kuvunja ukimya.

“Najua lipo jambo kubwa lililofichika nyuma ya kutoweka kwa Albert ambalo kwa namna moja au nyingine lina maslahi makubwa kwa nchi kubwa na baadhi ya wakubwa katika nchi hii,” Askofu Masinde alisema.

“Kwa nini unasema hivyo?” nilimuuliza Askofu Masinde kwa shauku, nilipomtupia jicho Daniella nikamwona naye akiketi vizuri kwenye kiti chake kwa shauku ya kusikia nini Askofu Masinde angesema.

“Sura yako inanifanya nijisikie kukuamini, na kwa kuwa Daniella amekusifia na anaonesha kukuamini sana kiasi cha kukuleta hapa… basi nitawaeleza ninachokijua,” Askofu Masinde alisema kisha akatuuliza kama tulikuwa tunafahamu kuhusu uandaaji wa muswada fulani kuhusu haki za binadamu. Tukakubali kuufahamu muswada huo ila hatukujua uliishia wapi.

“Huko ulikoishia ndiyo hasa shida ilikoanzia…” Askofu Masinde alisema na kuendelea, “Uandaaji wa muswada huo ulikumbwa na changamoto nyingi ukipingwa kutoka kila kona na makundi mbalimbali ya wananchi, viongozi wa dini n.k. Ndani ya muswada huo kuna vipengele ambavyo vinatambua haki za makundi ya watu wanaojihusisha na mapenzi na ndoa za jinsia moja, haki ya kutoa mimba pamoja na mambo mengine kadhaa ambayo yanakwenda kinyume kabisa na utamaduni wetu au mafundisho ya dini.”

Niliduwaa kidogo, na nilipomtazama Daniella nikamwona naye pia ameduwaa.

“Sijaelewa…” Daniella alianza kusema. Kisha alinyamaza ghafla huenda alifanya vile ili afikiri kwanza kabla ya kutia neno lolote katika kikao kile kisicho rasmi.

“Usiwe na haraka…” Askofu Masinde alimwambia Daniella kisha akaongeza, “bado kuna mengi yatakayokusisimua mno.”

Daniella alitaka kusema neno lakini Askofu Masinde alimkatisha kwa mkono kisha akaendelea, “Kumekuwa na shinikizo kubwa toka kwa nchi za Magharibi zikizitaka nchi zote za Afrika kuhakikisha kwamba zinapitisha sheria za kutambua haki za binadamu, na hapa wanalenga makundi hayo niliyoyaeleza. Nchi kadhaa za Afrika tayari zimekwisha pitisha sheria hiyo na chache ikiwemo Tanzania bado hatujafanya hivyo japokuwa lipo shinikizo kwamba muswada wa sheria hiyo upelekwe bungeni ili kutimiza matakwa hayo ya nchi tajiri.”

“Wazimu wa hali ya juu,” Daniella alifoka.

“Ni wazimu kweli kweli!” Askofu Masinde aliunga mkono maneno ya Daniella. “Waasisi wetu wametuachia taifa lenye maadili mema na linaloheshimika lakini tunataka kulifanya liwe la ovyo. Nilimwambia Albert akiruhusu jambo hili litokee nchini basi atakuwa amejitia laana kubwa na vizazi vinavyokuja havitamsamehe.”

“Sasa…” Daniella alianza kusema na kushusha pumzi. “Muswada huu unahusiana vipi na kutekwa kwa Rais?”

“Ni kwa sababu yeye amekataa kuupitisha na kwenye kikao cha Baraza la Mawaziri alitangaza kuufuta na kuufunga kabisa mjadala wake…” Askofu Masinde alisema huku sura yake ikichanua kwa tabasamu. “Amekataa kuona vizazi vijavyo vinarithi taifa ambalo limebomolewa misingi yake japo anafahamu mapambano na mataifa haya si kitu chepesi.”

“Kwa hiyo unahisi waliomteka Rais ni mataifa ya Magharibi?” Daniella aliuliza huku mshangao ukiwa haujamtoka usoni.

Precisely…” Askofu Masinde alijibu kwa kujiamini. “Kuna jumuia fulani ya siri inayoitwa ‘Triangle’ iliyoanzia nchini Italia kabla haijasambaa katika nchi hizo ndiyo wenye kushinikiza jambo hili, na walipanga kumtumia Rais.”

Oh my God!” Daniella alimaka.

“Ukweli hao Triangle ndio walimweka Albert madarakani. Walitumia nguvu yao hadi akapitishwa ndani ya chama japo wakubwa ndani ya chama walikuwa hawamkubali, kisha akachaguliwa kwa kishindo akiibuka mshindi kwa kura nyingi. Walimpa nafasi hiyo kubwa kwa sharti moja kwamba wataitumia ofisi yake katika kufanikisha mambo yao, na hivi ndivyo wamekuwa wakifanya kwa marais wengi wa Afrika,” Askofu Masinde alisema kwa utulivu kana kwamba alikuwa anaongelea mambo ya kawaida tu.

Mimi na Daniella tukatazamana na kushusha pumzi. Ni kweli bado kulikuwa na mengi ya kusisimua mno.

“Baada ya kuupata mzizi mkuu ambao ni Rais, Triangle wakaanza kusambaza mizizi midogo midogo katika sehemu mbalimbali za bungeni na kwenye taasisi nyeti za ulinzi na usalama… ili kutengeneza mmea wenye afya. Kwa taarifa yenu jumuia hii ya siri imeliteka Bunge kwani asilimia kubwa ya wabunge ni wafuasi wa Triangle kwa kuwa waligharamiwa kampeni zao na kusaidiwa kushinda, si hivyo tu, kila mwezi kuna kiasi kikubwa cha fedha wanakipokea kwa siri…” Askofu Masinde alisema, na hapo nikang’aka.

What!” nilimaka kwa mshtuko mkubwa.

“Kitendo cha kuyateka mabunge katika nchi za Kiafrika kumewasaidia kuweka urahisi wa kupitisha miswada mbalimbali inayowasilishwa bungeni. Kwa Tanzania hadi sasa, mawaziri wengi ni wafuasi wa Triangle hata baada ya Rais Masinde kuvunja serikali na kuwaondoa aliyekuwa Waziri Mkuu, Festus Mponjoli na wale mawaziri watano bado kuna mawaziri wengi tu wafuasi wa Triangle. Kwa ufupi ni kwamba jumuia hii imeishika nchi hii na wanaipeleka namna watakavyo…” Askofu Masinde aliendelea kueleza lakini Daniella akamkatisha kwa hasira.

No! this is impossible!” Daniella alisema kwa hasira.

“Halafu kibaya zaidi, hata mke wa Rais, Juliana, naye ni mfuasi wa Triangle,” Askofu Masinde alisema kwa huzuni.

Endelea...
 
utata.JPG

376

Oh my God!” mimi na Daniella tulijikuta tukisema kwa mshangao mkubwa halafu tukaangaliana. Macho yetu yalipokutana yaliongea mengi sana ambayo midomo isingeweza kuyatamka.

Even President’s wife?” niliuliza kupata uhakika huku mshangao ukiwa haujanitoka usoni.

Yes, even his wife…” Askofu Masinde alisema kwa utulivu.

“Wazimu wa hatari!” Daniella alisema kwa hasira.

Kisha kilitokea kitambo kifupi cha ukimya mle chumbani, kila mmoja alikuwa anatafakari kivyake, na baada ya muda kidogo Daniella akauliza, “Imekuaje hadi mke wa Rais akaingia katika kundi hili?”

“Swali lako linahitaji maelezo marefu kulijibu… historia ya Albert na Juliana ni ndefu kidogo… ni Juliana aliyemshawishi Albert kuingia kwenye siasa na ni yeye aliyemuunganisha na hao Triangle. Mambo haya nitayaeleza wakati mwingine…” Askofu Masinde alisema.

Nilimtazama Askofu Masinde kwa namna ambayo nilishindwa kujizuia kushangaa maana niligundua kuwa alikuwa anayafahamu mambo mengi sana ya kisiasa, kiuchumi na kiintelijensia yaliyokuwa yakiendelea nchini na duniani. Sikuwa nimeshangazwa na ufahamu wake kuhusu mambo hayo ila ule uwezo wake wa kuchambua mambo ndiyo ulinifanya nijione bado sana katika shughuli za ujasusi na nilitakiwa kurudi shule kujifunza zaidi.

Katika maongezi yake mzee yule alikuwa anakufanya utamani kuendelea kumsikiliza kwa jinsi alivyodadavua mambo.

“Samahani, mjomba… wewe ni nani hasa?” nilimuuliza Askofu Masinde huku nikimtazama kwa umakini usoni.

“Kwa nini!” Askofu Masinde aliniuliza kwa mshangao.

“Kwa sababu wewe si askofu tu… I need to know, who precisely are you?” niliongea huku nikimkazia macho. Nilipomtupia jicho Daniella nikamwona akiyakwepa macho yangu na kuinamisha uso wake kutazama chini, nikajua alikuwa anafahamu kitu ila hakutaka kuniambia.

Kwanza Askofu Masinde aliachia tabasamu kisha akakohoa kidogo kurekebisha sauti yake. “Mimi ni Askofu Mkuu wa Living Paradise Ministries…” Askofu Masinde alisema.

“Hilo najua…! Hata hivyo si lazima uniambie kama unadhani hisia zako hazitaki kuniamini!” nilimwambia Askofu Masinde huku nikiupisha utulivu kichwani mwangu. “Ila nashukuru sana kwa maelezo yako ambayo yametupa picha kamili ya nini kipo nyuma ya sakata hili.”

Askofu Masinde alishusha pumzi ndefu kisha akacheka kidogo na kujiweka vizuri kwenye kiti chake, “Nashangaa kwa nini Daniella hajakwambia… kwa kifupi nimekuwa ndani ya Idara ya Ujasusi kwa miongo minne nikitumika kama covert officer under church umbrella. Ingawa nimestaafu lakini bado natumika.”

Dah! Sasa nilitambua kuwa miaka yote Askofu Masinde alikuwa ofisa kificho chini ya mwamvuli wa kanisa! Nilijikuta nikiachia tabasamu kabla sijasema, “Nilihisi jambo kama hili” kisha nikaongeza, “Sasa kwa nini hukuchukua hatua ya kuyaripoti mambo haya kunakohusika baada ya Rais kutekwa?”

Swali langu lilimfanya Askofu Masinde acheke kidogo. “Nadhani unajua kanuni ya ujasusi ya kutomwamini kila mtu, hata marehemu. Tatizo kubwa ni nani wa kumwamini! Dunia hii imekuwa na matukio ya ajabu sana kwa zama hizi. Watu wengi wamejikuta wakijitumbukiza kwenye ibada za kishetani ili mambo yao yawanyookee kama wanavyodhani. Dini ya kishetani imeanza kuzoa maelfu ya wanasiasa, wasanii, wanamichezo na hata baadhi ya viongozi wakubwa wa kidini hapa nchini.”

“Unafahamiana na Othman Mwambe?” nilimuuliza tena Askofu Masinde. Nikamwona akionekana kushtuka kidogo, hata hivyo aliumeza mshtuko wake na kuachia tabasamu.

“Kwa nini umeniuliza hivyo?” Askofu Masinde aliniuliza huku akinitazama machoni.

“Yeye pia anafahamu mengi, kama wewe… alikuwa ndani ya idara ya ujasusi kwa miongo minne, kama wewe… ingawa amestaafu lakini bado anatumika, kama wewe… na pia ni rafiki wa karibu wa Rais Masinde, kama wewe…” nilisema kwa sauti tulivu.

Askofu Masinde akacheka sana na kicheko chake kilipokatika akaniambia, “Una akili nyingi sana… umekutana wapi wa Othman?”

“Nimekutana naye leo, usiku huu, nyumbani kwake,” nilimjibu huku nikimtazama usoni.

“Mnafahamiana muda mrefu?” Askofu Masinde aliniuliza kwa mshangao.

“Sikuwa nikimfahamu kabla ila harakati hizi zimenikutanisha naye leo baada kunitafuta ili anipe taarifa fulani, ingawa nilijua yapo mambo mengi hakutaka kuniambia,” nilisema.

“Amekwambia nini?” Askofu Masinde aliniuliza kwa shauku huku akinitazama machoni katika namna ya kuyasoma mawazo yangu.

Kwanza nilishusha pumzi ndefu kisha nikaelezea yale niliyoambiwa na mzee Othman Mwambe. Nilipomaliza maelezo yangu Askofu Masinde akabetua kichwa chake kuafiki.

“Othman ni rafiki yangu mkubwa, kama ilivyo kwa Albert… yeye pia tulikuwa darasa moja Tabora…” Askofu Masinde alisema kisha akaitazama saa iliyokuwa imetundikwa ukutani na kushtuka.

Nami nilipopeleka jicho langu kuitazama saa ile nikashtuka, ilikwisha timia saa kumi na dakika tano. Tulikuwa tumeongea kwa muda mrefu sana.

“Muda wangu wa maombi umefika, nitawaacha humu ili nikaombe kwanza kisha nitarejea,” Askofu Masinde alisema na kunyanyuka toka kwenye kiti chake. “Endeleeni kuyatafakari hayo niliyowaambia, lakini mkumbuke kuwa hamuwezi kupambana na shetani kama hamna Mungu. Taifa hili linawategemea maana msipolipigania linakwenda kubomolewa na ndani ya miaka michache ijayo ile misingi yote imara iliyosimamisha taifa hili itabomolewa na zitaletwa tamaduni mpya kabisa ambazo hazikuwahi kuonekana.”

Lakini kabla hajatoka alituomba tufumbe macho kwa dakika chache, tukafanya hivyo. Kisha alitufanyika sala fupi ya kutuombea ulinzi na alipomaliza akatupa mkono wa baraka na kutoka akituacha.

Baada ya kubakia peke yetu tuliamua kuyafungua yale mafaili mekundu ili tujue kilichoandikwa.

* * *

Endelea...
 
utata.JPG

377

Utata!




Saa 10:30 usiku…

“SIJAWAHI kuwaza kama kuna watu wana wazimu wa namna hii! This is pure insanity!” Daniella alifoka kwa hasira. “Hili ni swala la kufa mtu au kupona. Nitahakikisha wote waliofanya hujuma hii vichwa vyao vinakuwa halali yangu, sitojali wadhifa wala cheo cha yeyote aliyehusika.”

Tangu alipopitia kilichoandikwa kwenye yale mafaili mekundu tuliyoyatoa kwenye ile nyumba yenye mitambo ya mawasiliano, Daniella alionekana kuvurugika kichwa kiasi cha kuchanganyikiwa kama alivyokuwa. Hata macho yake yalibadilika na kutoa cheche.

Muda huu Daniella alikuwa amesimama baada ya kiti chake kutokalika tena, mara kwa mara akipiga hatua kuelekea dirishani ambako alisimama akichungulia kama kwamba wakati wowote alitegemea kuona uovu aliokuwa akiutarajia kutokea. Uovu ambao hakuujua ingawa hakuwa na shaka kuwa, bila kumkomboa Rais Masinde, basi kungetokea uovu wa kutisha kuliko mengi yaliyokwisha tokea.

Mimi pia niliamini kuwa lolote lingeweza kutokea. Dunia hii iliyojaa waovu, kama alivyosema Askofu Masinde, nchini mwetu walikuwemo wa kutosha! Watu waliokuwa tayari kuhakikisha damu inamwagika, wakifurahia kitendo chochote cha unyama, watu waliokuwa wakitabasamu walipoona maafa na kushangilia waliposhuhudia mauaji.

Walikuwa tayari kumtoa yeyote kafara, hata kama ni mzazi au mtoto wa kuzaa, sembuse kumteka kiongozi wa nchi aliyechaguliwa kidemokrasia na wananchi ili tu waipeleke nchi halijojo!

“Lakini hawa wanataka nini hasa? Je, wanadhani wao wana hakimiliki ya nchi hii?” nilijiuliza huku donge la hasira likinikaba kooni.

Niliyatazama tena yale mafaili mekundu yakiwa juu ya meza, nikalivuta moja na kulifungua kisha nikalirudisha baada ya kugundua kuwa lilikuwa ni lile lenye hotuba za Rais zikiwa na saini yake chini. Aidha zilikuwemo nyaraka mbalimbali za Ikulu zilizoandikwa ‘Top Secret’ ambazo bila shaka zilikusudiwa kwa ajili ya macho ya Rais pekee na wateule wake wachache.

Kisha nililichukua lile faili lingine na kulifungua, nikayapitia tena haraka haraka yaliyoandikwa mle ndani. Kulikuwa na mkataba hatari ambao Rais alitakiwa kuupitia upya na kuridhia makubaliano na jumuia ya Triangle.

Na mambo yaliyoainishwa ndani ya mkataba ule ni kuwa mkuu wa nchi aliyesaidiwa na Triangle alitakiwa kupitisha sheria zao na kutambua haki za watu wanaofanya mapenzi ya jinsia moja, utoaji mimba na kuhakikisha katika nchi yake wafanyabiashara wakubwa wa dawa za kulevya hawaguswi wala kubughudhiwa na kwamba ahakikishe wanatengenezewa miundombinu mizuri ya kuweza kuifanya kazi yao kwa uhuru.

Jambo hili lilitiliwa mkazo kwa kuwa dawa za kulevya kilikuwa chanzo kikubwa cha mapato kwa Triangle kwa kuwa wafanyabiashara wa mihadarati walitoa kiasi kikubwa cha fedha ambazo ziliisaidia jumuia hiyo iweze kujiendesha.

Hivyo, Rais Masinde ndiye aliyetakiwa kuhakikisha anawasimamia wafanyabiashara wote wa mihadarati nchini, walio chini ya jumuia ya Triangle na kuhakikisha biashara zao zinakwenda vizuri na wanalipa michango yao kwa jumuia hiyo ya siri kwa wakati.

Hata hivyo nyaraka zilionesha kuwa haikuwa kazi ngumu kwa nchi za Afrika kukubaliana na Triangle kwani walitumia kigezo cha umasikini wa nchi hizi kuzishinikiza zifuate masharti yao. Tayari nchi nyingi za Afrika zilikuwa zimekubaliana na mkataba huo na kutunga sheria kukubaliana na mambo hayo. Nchi pekee ambazo ziliwapa ugumu mkubwa kuingia hazikuzidi tatu, Tanzania ikiwemo.

Hivyo, kwa sababu hiyo Iliundwa timu ya watu kumi ambayo ilitakiwa kuhakikisha Rais Masinde anafikia makubaliano hayo, iwe kwa hiyari au kwa kulazimishwa. Miongoni mwa watu hao kumi, mke wa Rais Masinde, Mama Juliana Masinde alikuwa mmoja wao! Jina la Juliana lilikuwa namba mbili likitanguliwa na jina la Tiger!

Orodha iliendelea kwa namba tatu Yusuf Taifa, mkuu wa kikosi cha siri cha ulinzi wa Rais; namba nne Festus Mponjoli, aliyekuwa Waziri Mkuu. Kisha kuanzia namba tano hadi kumi yalikuwa majina mageni kabisa kwangu. Hata hivyo niliamini kuwa majina yote yalikuwa halisi isipokuwa jina namba moja tu halikuwa halisi, sikujua kwa nini hawakutaka utambulisho wa mtu huyo ufahamike!

Timu hii haikutakiwa kuishia kumshinikiza Rais tu aridhie makubaliano hayo, ilitakiwa kuhakikisha mtu yeyote anayechaguliwa kuwa Rais, Makamu wa Rais, Waziri Mkuu, Mawaziri wote, Katibu Mkuu Kiongozi, viongozi wa taasisi nyeti za ulinzi na usalama kama Jeshi, Polisi, Usalama wa Taifa n.k. wawe ni wafuasi wa Triangle. Lengo kubwa ni kuotesha mizizi yao na kuiona Tanzania ikibadilika na kuwa Tanzania Mpya!

Mwishoni mwa mkataba ule kulikuwa na maelezo ya kuridhia yaliyomtaka Rais Masinde kuweka agano la kuwa mtiifu na kufuata maelekezo yote anayopewa, mbele ya mkuu wa Triangle, mnamo Novemba 23, saa tano kamili asubuhi na kama angeshindwa kutekeleza hayo basi adhabu yake ingelikuwa kifo!

“Ama kweli kikulacho ki-nguoni mwako…” hatimaye Daniella alisema kwa uchungu. “Kumbe mke wa Rais anafahamu mahala alipo Rais. Kujifanya sijui yupo depressed, hayupo kwenye mood ya kuongea na kuwa ni mtu wa kulia na kujitenga tu… yote haya ni maigizo!”

Nilibaki kimya nikijaribu kutafakari, maana katika operesheni zote nilizotumwa kuzifanya, hii ilikuwa ni utata!

She’s going to pay, I swear!” Daniella alisema kwa kusisitiza.

* * *

Endelea kuufuatilia mkasa huu wenye utata...
 
Back
Top Bottom