Simulizi: Nini maana ya mapenzi

Simulizi: Nini maana ya mapenzi

SEHEMU YA 251


Kesho yake mamake alienda kanisani ila Erica alibaki nyumbani kama kawaida na mtoto wake huku akifanya shughuli za hapa na pale, simu yake iliita tena akaiangalia ni namba ya Erick, akaipokea,
“Erica, leo nimeamua kwenda kanisani kwaajili yako, jibu lako ndio litategemea uamuzi wangu. Niambie ukweli Erica, una mtoto?”
“Ndio nina mtoto”
Simu ikakatika, Erica akajaribu kupiga tena ile namba ya Erick ila hakuipata hewani kabisa, wasiwasi ulimshika Erica maana hakujua ni nini kimempata Erick, alijikuta akijawa na mashaka kupita maelezo,
“Mungu wangu, ukweli humuweka mtu huru au ukweli humuongezea mtu matatizo? Sasa Erick wangu kakumbwa na nini? Mungu wangu, sijui nani ataweza nieleza habari za Erick”
Siku hiyo hakuwa na raha kabisa siku nzima na kila alipojaribisha namba ya Erick bado hakuipata hewani na kumfanya kuwa na mashaka zaidi.
Hata mama yake aliporudi aligundua hali ya Erica,
“Ndiomana nakwambiaga uwe unaenda na kwenye ibada, wewe ni mtu gani kila siku mawazo?”
“Hapana mama, ila ngoja nikuulize jambo. Ukweli humuweka mtu huru au ukweli humuongezea mtu matatizo?”
“Kwanini ukweli ukuongezee matatizo? Ukweli ni mzuri sana na hukuweka huru, hebu fikiria ungekuwa unakuja kwa mama yako na kuniambia ukweli, mama kuna mwanaume hivi na hivi na vile, mimi kama mama ningekushauri kuhusu huyo mwanaume. Unafikiri ingefikia hatua ya Angel kutokuwa na baba? Katika maisha tunatakiwa kujifunza kusema ukweli maana unapokuwa mkweli ni rahisi kusimamia maneno yako ila njia ya muongo ni fupi maana kuna muda utasahau hata ulikuwa unaongelea nini?”
“Sasa mama, kuna ukweli wa kuumiza, unawezaje kumwambia mtu ukweli wa kuumiza wakati unajua unaumiza?”
“Sasa hapo penye ukweli wa kuumiza unatakiwa kupata ushauri kwa mtu anayeelewa kuongea na mtu mwingine ambaye atatoa ukweli kwa ushauri. Ukijua ni kitu cha kuumiza, hutakiwi kutoa ukweli kwa kukurupuka, unatakiwa kupata ushauri kwanza na ukishindwa hata mtumie mtu mwenye busara kusema. Mfano madaktari wetu wamejifunza kuongea na mgonjwa na endapo wakimpima mtu na kugundua kaathirika huwa hawakurupuki tu na kusema una ukimwi maana wanajua ule ni ukweli ila unaumiza na ukikurupuka kumwambvia mtu unaweza kumpoteza maana ile mara ya kwanza mtu kuambiwa una ukimwi huwa inachangaya akili hatari mtu huwa anatamani hata kufa. Ila madaktari wetu hutumia kauli za busara na upendo kiasi kwamba mtu Yule aliyeathirika anapoambiwa ana ukimwi huwa tayari ameshaweza kukubaliana na hali yake na kuona kuna watu wameathirika na bado wanaishi vizuri tu. Ukijua kabisa ukweli huu unaumiza basi usiutoe kwa pupa”
Erica akainama chini kidogo kwani jinsi alivyomjibu Erick ni kwamba aliutoa ukweli kwa pupa na hakujua ni kipi kinaweza kutokea kwa Erick, alimuuliza tena mama yake
“Na kama hukujua hilo ukajikuta umetoa ukweli kwa pupa itakuwaje?”
“Kuna ukweli gani umeutoa kwa pupa? Unajua unaposema ukweli inategemea na mtu unayemwambia huo ukweli, mfano una mpenzi anakupenda sana na anakujali kwa kila kitu ila umejikuta humpendi basi tafuta namna ya kumfikishia huo ujumbe sio unakurupuka na kumwambia sikupendi, sikutaki yani hujui tu utasababisha nini kwa Yule mtu labda kama hakuwa na upendo na wewe ila anayekupenda sana unaweza fanya akawa kichaa wengine ndio huchukua hata jukumu la kujiua kama hajapata watu wazuri wa kumshauri. Ukweli ni mzuri sana ila jifunze kutoa ukweli katika staili inayofaa, na uangalie huo ni ukweli wa aina gani, kama wa kuumiza basi tafuta namna ya utaratibu kufikisha ujumbe kwa muhusika”
Erica alishajiona amekosea alivyomueleza Erick, aliumia sana moyoni ila ndio alishamueleza na kumfanya akose raha kabisa.
Siku hiyo alikuwa na mawazo sana, hata usiku hakushika simu wala chochote ila usingizi ulimpata kwenye mida ya saa tisa.
 
SEHEMU YA 252

Kulipokucha mama yake alienda kumkurupua,
“Wewe Erica, huendi kazini?”
Alikurupuka na kwenda kuoga kwaajili ya kwenda kazini, alijiandaa na kwenda kazini kama kawaida ila alikuwa kazini na mawazo sana.
Alifika na kufanya kazi zake kama kawaida, ila hata James alijua kuwa ana mawazo, alimuita ofisini kwake na kumuuliza kuwa mbona anaonekana hayupo kawaida, ila Erica naye alimuuliza James,
“Mfano bado hujaoa, na kuna mwanamke unampenda sana ila unakuja kugundua huyo mwanamke ana mtoto na mtoto kapata ndani ya mahusiano yenu na mwanaume mwingine, utajisikiaje?”
“Eeeh bhana eeeh! Hilo jambo limewahi kunitokea, inauma asikwambie mtu yani inauma sana tena usikute ulimuomba mzae akagoma halafu akaenda kuzaa na mjinga yani inauma sana.”
“Sasa wewe ilivyokutokea ilikuwaje?”
“Unajua mara nyingi kwasababu ya Yule mwanamke mmoja nimeona wanawake wote hawafai wakati Bite wangu yupo tofauti kabisa, yani ukimfanyia hivyo jamaa yako unamchukiza sana tena anaweza kukuchukia milele. Ndio imetokea kwako hiyo Erica nini? Maana nimeambiwa huyo uliyezaa nae hakujali, je ulikuwa na mpenzi kabla yake ndio kakuchukia?”
“Yani mwanaume ninayempenda ndio kajua ukweli kuwa nina mtoto, na amechukia sana”
“Ndio swala linakupa mawazo hilo Erica?”
“Naumia sana, sababu nampenda”
“Hebu ondoa hayo mawazo, tena ondoa mawazo hayo kabisa kichwani mwako. Huyo mwanaume hawezi hata kukuoa maana tayari ushaingia doa, mwanaume atakayeweza kukuoa ni Yule atakaye kukuta na mtoto kwasasa na akakupenda hivyo hivyo ila kwa huyo uliyetia doa sahau. Ila usijali Erica, naomba leo usiondoke mapema nikupeleke mahali ukarelax kidogo”
Erica alimuitikia ila akajua kama kawaida shemeji yake ameshaanza upuuzi wake, kwahiyo alimuitikia ili kumridhisha tu.
Alimaliza kazi zake leo ila hakwenda kumuaga James na kuondoka zake kurudi nyumbani kwao.
Akiwa njiani akakutana na Dora, ambapo alimsalimia na kumkumbatia,
“Erica unaenda wapi?”
“Naenda nyumbani”
“Unakumbuka kuwa ni leo jioni ndio ulisema tuje ofisini kwenu? Yani nipo na wenzangu wale pale ndio tunaelekea ofisini kwenu sasa wewe ndio unaondoka tena jamani!”
“Ila wapo wenzangu”
“Ndio Erica, ila uwepo wako ndio mzuri zaidi. Naomba tuongozane pamoja tafadhali”
“Basi ngoja na mimi nikuombe kitu”
“Niombe tu”
“Naomba mkimaliza useme kuwa unataka kwenda na mimi nyumbani na usiondoke hadi tuondoke wote, hata wenzio waondoke tu”
Ilibidi Dora akubali maana kiukweli alihitaji sana waweze kuongea na wafanyakazi wa ile ofisi, kisha wenzie Dora walifika pale na safari ya kurudi kazini kwa James iliwadia.
 
SEHEMU YA 253


Walifika kisha Erica alienda kumwambia James kuwa wale watu wa kuongea na wafanyakazi wake wamefika, James alimwambia Erica aweze kuwaambia wafanyakazi wote ili wakutane kwenye chumba cha mkutano maana tangazo alishabandika toka wiki iliyopita kuwa karibia na muda wa kutoka kutakuwa na semina fupi, sema tu Erica mwenyewe alisahau.
Aliwaambia kisha wote wakajiandaa na muda ulipofika wakaenda kwenye chumba cha mkutano ambapo wale wakina Dora walipewa muda wa nusu saa tu ya kuzungumza mambo yao, na waliyazungumza walipomaliza waliwashukuru kila mtu alirudi sehemu ya kazi yake kwaajili ya kufunga na kuondoka maana muda wa kazi nao ulikuwa umeisha. Kwahiyo wale wengine waliondoka kisha kumuacha Dora pale akimsubiria Erica.
Kisha Erica akataka kwenda kumuaga shemeji yake maana hakuweza kuondoka kama mwanzo sababu tayari alishaonekana kwenye kikao, ila kabla hajaenda kumuaga shemeji yake alimwambia,
“Erica nisubiri, kumbuka kuna kitu nilikwambia kuwa kuna mahali tutaenda”
“Aaaah shemeji, kuna rafiki yangu ananisubiri niende nae nyumbani”
“Rafiki yako yupi huyo?”
“Ni mmoja kati ya wale waliokuja kwenye semina”
“Mwambie atakufata siku nyingine”
“Aaaah shemeji, leo kaacha shughuli zake zote kwaajili yangu, itawezekanaje kumwambia hivyo? Sio vizuri eti”
“Basi nisubiri nae, nikamilishe kazi hapa mara moja”
Erica hakumuelewa shemeji yake kwakweli, ila ilibidi afate maagizo yake maana licha ya kuwa shemeji yake wakati huo huo ni bosi wake.
Kwahiyo Erica alienda kwa Dora na kumwambia kuwa wasubiri mara moja, muda kidogo James alimaliza kazi zake na kumwambia Erica amfuate pamoja na rafiki yake.
Walipofika nje, James alijitambulisha kwa Dora,
“Hey, Dora mimi naitwa James nadhani unanifahamu kama mmiliki wa hii kampuni ila pia mimi ni shemeji yake Erica. Jina lako nimelisikia kwenye utambulisho wenu na Erica ameniambia kuwa wewe ni rafiki yake wa dhati na kaniambia kuwa leo unataka kwenda nae kwao ila mimi nahitaji kumpeleka mahali shemeji yangu akatulize akili yake kidogo maana imevurugika. Kama hutojali basi tuungane”
Dora hakujua kama akatae au akubali maana kwenye makubaliano na Erica ni kuwa ajifanye kwamba anamsubiria Erica kwenda nae nyumbani, ila kwa hoja ile hakujua kama akubali au akatae, Erica akaamua kujibu,
“Ila shemeji…”
James akamkatisha Erica na kusema,
“Erica wewe nyamaza, mimi nimemuuliza Dora, je yupo tayari kuungana na sisi au la”
Dora alikubali ili kujua kuwa Erica na shemeji yake wamepanga kwenda wapi. Basi wakapanda kwenye gari ili kuelekea ambako anapajua James.
 
SEHEMU YA 254

Wakiwa kwenye gari James akawaambia,
“Sasa tutangulie sehemu moja hivi, wanapikaga kitimoto kitamu hiko balaa. Twendeni tukale kitimoto”
Erica akamwambia shemeji yake,
“Hapana mimi silagi kitimoto”
“Kwanini huli kitimoto?”
“Basi tu imetokea huyo mdudu huwa sili”
James akamuuliza na Dora,
“Wewe je?”
“Mimi nakulaga”
“Basi tutapanga siku nyingine tukale mimi na wewe, yani Erica ana mambo ya kishamba hadi yanakera. Basi twendeni tukale nyama ya mbuzi hadi tusahau matatizo”
Napo Erica akapinga,
“Hapana huwa sili mbuzi”
“Una matatizo gani wewe Erica? Kwahiyo nyama gani unapenda?”
“Napenda kuku na samaki”
“Basi twende mahali kuna mishikaki ya kuku mitamu sana, yani wanajua kuchoma hao balaa huko tunakula huku tunaangalia bendi”
“Shemeji kumbuka nina mtoto mdogo bado ananyonya, ananisubiri nyumbani, si vizuri nianze kuzurula zurula”
“Erica usiwe hivyo jamani, mimi nitakurudisha hadi kwenu. Nahitaji tu ukatulize mawazo yako, tafadhali usiniuzi na mimi”
Kwakweli Erica hakujisikia kabisa kwenda mahali na shemeji yake ila kwavile shemeji alionekana kadhamiria siku hiyo kutoka na Erica hakuwa na namna zaidi ya kumsikiliza mambo mengine.
Wakafika kwenye hiyo hoteli ambako walikuwa wanachoma kuku huku kuna bendi inatumbuiza, walienda kukaa kwenye viti na kuagiza nyama kisha wa vinywaji akaja, James akaagiza pombe yake, Dora nae akaagiza bia yake, Erica akaagiza soda. James akamzuia muhudumu kwenda kumletea kwanza,
“Erica usituletee nzi hapa, utaagizaje soda?”
“Shemeji, giza lishaingia sasa hao nzi watoke wapi? Halafu niagize nini zaidi ya soda?”
“Agiza bia, yani usiagize juisi wala soda, sitaki kuchafuliwa meza”
“Sinywagi pombe”
“Ila kuna pombe laini”
“Hapana sinywi pombe, hata hivyo nina mtoto mdogo bado ananyonya mwanangu siwezi kuchanganya maziwa yangu na vilevi. Sinywi pombe nampenda mwanangu”
James akamuangalia Erica na kuruhusu muhudumu amletee kinywaji anachotaka, na alipoletewa tu na kumiminiwa kwenye glasi, James akachukua na pombe yake kuimimina kwenye glasi ya Erica,
“Shemeji ndio unafanya nini?”
“Erica, kunywa pombe sio zambi hata hivyo pombe ukichanganya na soda haileweshi”
Erica akakumbuka mara ya kwanza kunywa pombe alishawishiwa na Derick na kuambiwa kuwa ile pombe haileweshi, halafu akanywa na kulewa na kisha kufanya mapenzi na Derick hadi kupata mimba na kuja kupata dhambi ya kutoa maana alibeba mimba ya ndugu yake, halafu shemeji yake bila aibu anamshawishi anywe pombe, akaona ni ujinga.
Akawaza ni kwa jinsi gani atamkwepa shemeji yake, aliamua kumuaga kuwa anaenda chooni na akirudi atakuja kunywa.
 
SEHEMU YA 255

Alienda chooni Erica na kupita mlango wa nyuma halafu kuondoka zake, yani alimuacha shemeji yake na Dora, kwa muda huo hakujali kuhusu Dora alimuacha mwenyewe ajiokoe maana amekubali tu wito hata asioujua chanzo chake.
Erica alienda hadi nyumbani kwao na kumkuta mama yake ambaye alimfokea sana,
“Yani Erica mpaka muda huu kweli? Saa nne hii jamani? Hiyo kazi kazi gani, mbona siku zote unawahi kurudi, huna uchungu na mtoto wako?”
“Namuhurumia mama ila leo tulikuwa na kikao ofisini, halafu tulivyotoka foleni. Najua mara nyingine nawahi ila leo bahati mbaya mama. Nisamehe mama”
“Haya nenda ukaoge uje kumchukua mtoto ukamlaze”
Basi Erica alienda kuoga kisha akaenda kumchukua mtoto wake na kwenda kumlaza, yeye hakuweza hata kula maana hakujisikia tena ila mama yake alimwambia kuwa anatakiwa kula kwahiyo akala kidogo na kwenda chumbani.
Wakati yupo chumbani leo alijikuta gafla alijikuta akimkumbuka Bahati hadi moyo ulimuuma maana ndiye mwanaume aliyekuwa tayari kumfanya mtoto wake kuwa na baba, tofauti na Erick aliyemzimia simu maana aliamini kuwa Erick alimzimia simu.
Ingawa siku zote hakumpata Bahati hewani ila siku hiyo alipiga na simu ya Bahati iliita, na muda kidogo ilipokelewa na ilipokea sauti ya kike na kumfanya Erica kidogo ajiume ume,
“Bahati yupo?”
“Anaoga, kwani una shida gani?”
“Shida natakiwa niongee nae yeye”
“Mimi ni mke wake kwahiyo unaweza kunieleza shida yako”
“Mmmh! Nyie wanawake wengine ndiomana mnaachikaga nyie, kupokea simu ya mume wako ndio nini?”
“Wewe inakuhusu nini? Huyu ni mume wangu mie, chochote chake nina uhuru nacho umesikia eeeh! Tena usinipandishe mashetani yangu nikuangushie matusi saizi”
Erica kusikia matusi akakata ile simu,
“Hivi kweli au naota? Yani muda mwingine nakuwa mgumu kuamini kuwa Bahati kaoa ingawa nilimshuhudia kwa macho yangu. Kweli mwanaume sio ndugu yako, yani Bahati alivyonigeuka gafla loh hadi nashindwa kuamini”
Aliwaza ya Bahati pale kisha akawaza ya shemeji yake na kulala.

Kulipokucha alijifanya kuwa anaumwa na hatoweza kwenda kazini, ilibidi mama yake amuache kalala kisha akamtumia ujumbe shemeji yake,
“Jana nilishikwa na tumbo la kuhara, sikuweza tu kukwambia ila nilikuwa na hali mbaya sana ndiomana nikaondoka, sasa leo ndio tumbo linaniuma balaa”
Akamtumia ujumbe huo na baada ya muda kidogo shemeji yake alimjibu,
“Pole sana”
Erica alishukuru uongo wake umetenda kazi muda huo na kuendelea kulala kujitoa kwenye uchovu.
Kwenye mida ya mchana, Erica alipokea ujumbe toka kwa Dora,
“Siamini Erica kama umeamua kunilipizia mambo yale ya zamani kwa stahili hii wakati ulisema umenisamehe dah! Siamini kabisa”
Kabla hajatafakari ule ujumbe alisikia mtu akigonga mlango wao, akainuka na kwenda kumfungulia. Alipofungua tu ni Tumaini aliingia ndani na baada ya kuingia alimnasa kibao Erica, na kabla Erica hajakaa sawa alishtukia tu kibao cha pili kikiingia kwenye shavu lake.
 
SEHEMU YA 256

Kwenye mida ya mchana, Erica alipokea ujumbe toka kwa Dora,
“Siamini Erica kama umeamua kunilipizia mambo yale ya zamani kwa stahili hii wakati ulisema umenisamehe dah! Siamini kabisa”
Kabla hajatafakari ule ujumbe alisikia mtu akigonga mlango wao, akainuka na kwenda kumfungulia. Alipofungua tu ni Tumaini aliingia ndani na baada ya kuingia alimnasa kibao Erica, na kabla Erica hajakaa sawa alishtukia tu kibao cha pili kikiingia kwenye shavu lake.
Kwakweli Erica alikuwa akiugulia vile vibao na kushangaa tu kuwa imekuwaje kupigwa kiasi kile, kumbe mama Erica alikuwa ameenda dukani kwahiyo muda ule amerudi aliweza kushuhudia mwanae akizabwa vibao.
Tumaini akamzaba kibao kingine Erica kabla hata hajajiweka sawa, muda kidogo alienda mbele ya Erica mamake na Erica kisha akamkunja Tumaini na kumzaba vibao vinne mfululizo kisha akamuachia na kumuuliza,
“Wewe binti umezaa? Unaujua uchungu wa mtoto wewe? Utakuja vipi nyumbani kwangu na kumnasa mwanangu vibao?”
Kisha akamgeukia Erica na kumwambia,
“Hivi mwanangu Erica una akili wewe? Mtu anaweza vipi kukupiga nyumbani kwenu?”
Akamuangalia tena Tumaini aliyekuwa akiugulia vile vibao alivyopigwa na mama yake Erica, kisha akamuuliza
“Haya niambie kilichokufanya umpige mwanangu ni nini? Sijali kuhusu urafiki wenu, sijali kama mmechukuliana wanaume huko, ila hapa ni nhumbani kwangu na huyu ni mwanangu, uchungu wa Erica naujua mimi na si mwingine. Haya sema kilichokuleta”
Tumaini alikaa chini na kuanza kulia ila mama Erica alimuangalia tu na Erica alipotaka kuinama ili ambembeleze mamake alimzuia, na kumwambia akae pembeni na wamuache Tumaini alien a atasema kinachomsibu.
Ila kabla hawajafanya lingine lolote, Tumaini alianza kuongea
“Umenipiga mama ila umenipiga kimakosa, ungejua kwanza binti yako alichokifanya kwangu ndio ungenipiga. Mama kwa baba yangu nina kaka mmoja tu ambaye nasaidiana nae kwa shida na raha, sasa mwanao huyu alichomfanya kaka yangu ni Mungu anajua, asanteni sana Mungu atanilipia”
Tumaini akainuka na kuondoka, Erica alitaka kumfata nyuma ila mama yake alimrudisha ndani na kuingia nae sebleni kisha akamkalisha chini na kuongea nae.
“Haya niambie hayo uliyomfanya kaka yake huyu ni yapi? Na je huyo kaka yake ndio baba yake Angel?”
“Hapana mama sio”
“Haya ni yapi umemfanyia?”
“Mama, ngoja nikwambie ukweli maana nimejifunza kusema ukweli hata kilichoniponza sasa ni kusema ukweli”
“Niambie sasa sio unazunguka zunguka”
“Mama, kaka yake na Tumaini niliwahi kuwa na mahusiano nae ila yupo Afrika kusini, sasa aliachana na mimi sababu ya huyu huyu dada yake alimpa maneno ya unafki. Nikawa na baba Angel ambaye amenitenda, sasa kipindi hiki kaka yake kanitafuta mwenyewe kwenye simu ila hakujua kama nina mtoto, ndio juzi kaniuliza kuwa una mtoto? Nikamjibu ndio, basi akakata simu na sikumpata tena hewani”
“Yani hiyo ndio sababu ya huyu kukupiga?”
“Ndio hivyo hivyo mama”
“Kwahiyo wewe kuwa na mtoto ndio jambo la kusema umesababisha matatizo kwa kaka yake?”
“Hata mimi sielewi mama”
“Ila mwanangu hebu uache ujinga mara nyingine, hivi unaachaje mtu akuzabe vibao kwenye nyumba yenu? Huo si ujinga huo?”
“Lakini mama, si imeandikwa mtu akikupiga kofi upande wa kushoto mgeuzie na wa kulia”
“Mungu wangu, nina mtoto mjinga haijapata kutokea, ndiomana nakwambiaga uwe unasikiliza mahubiri, usikie watumishi wa Mungu wakifafanua neno. Hivi dunia ya leo ilivyo eti ukipigwa shavu la kushoto geuza na la kulia, si utaonewa sana wewe! Nimekusomesha ili kufuta ujinga kwenye akili yako hiyo, kama hadi umemaliza chuo na una ujinga wa namna hiyo inamaana akili yako ilikuwa mbovu zaidi, pengine nisingekusomesha ningekuwa najuta tu. Kwa stahili hiyo si utateswa sana mwanangu, hebu achaga ujinga, kwanza neno lolote ukilisikia njoo uniambie mama yako nikuelekeze vizuri ila ukichukulia kwa pupa na akili zako hizo si nitakukosa wewe. Ndio nyie mkianza kuokoka sababu hamjui kuchambua maandiko unashangaa unakutana na wale manabii wa uongo wanaanza kukufundisha lete pesa zote kwa Mungu, unashangaa unakufa masikini sababu tu hukutumia akili. Tumepewa akili na utashi, kila jambo linaloingia kwetu lazima tulitafakari ndiomana kuna watu wa kutafakari neno maana ukitumia kwa akili zako yani utaona dini ni ngumu kuifuata ila ukijua kutafakari neno utaenenda sawa sawa na mapenzi ya Mungu. Sitaki tena kuona ujinga wa namna hii, mtu anakupiga nyumbani kwenu, sio kwao hapa pa kujichukulia sharia, hapa ni kwenu una uwezo wa kumtimua ila sio kumuachia akupige”
“Sawa mama nimekuelewa”
“Tena unielewe vizuri na habari zako za kutangatanga na wanaume sitaki, ukipata mchumba mlete nyumbani, habari za kutanga tanga utamleta mdogo wake Angel asiye na baba pia. Hivi hujisikii kuwa huna furaha kuona mtoto hana baba, ni mama mama mama, jamani hakuna raha kama mtoto kuona mama na baba, akijisikia anasema baba, akijisikia mama, ila mtoto ni mama mama mama, inauma sana. Usirudie tena makosa, hurumia kizazi chako”
Erica alimuitikia mama yake kwani maneno ya mama yake yalimuingia vilivyo, kisha akaendelea na kazi zingine hata akasahau tena habari ya Dora mpaka usiku uliingia.
 
SEHEMU YA 257

Alipoenda kulala wakati anashika simu ndio akakutana na ule ujumbe wa Dora, akawaza sana
“Mmmmh shemeji kamfanya nini Dora mpaka kalalamika hivi”
Akaamua kumpigia simu Dora kumuuliza na kumpa pole, Dora alivyopokea Erica alianza kuongea nae,
“Dora, nisamehe rafiki yangu. Nilikusamehe kwa moyo mmoja hata sijadhamiria kwa chochote, kwani shemeji kakufanya nini?”
“Njoo kesho nyumbani unione”
“Nyumbani kwenu ni wapi? Nitakuja asubuhi kabla ya kwenda kazini”
Dora akamuelekeza Erica nyumbani kwao kwa njia ya ujumbe kisha Erica alisema kuwa ataenda kesho yake kabla ya kwenda kazini.
Kisha aliamua kulala, ila alipigiwa simu akashtuka na kuangalia simu yake, akaona ni namba ya Bahati akajua kuwa Bahati amejirudi na kupokea ile simu ambapo alianza kuongea mwenyewe moja kwa moja,
“Kwakweli Bahati umeniudhi kupita kitu chochote maishani, kwanini unifanyie hivi kwanza? Uko wapi ule upendo uliosema mpaka kufa kwako utanipenda tu? Kwanini Bahati”
Ila cha kushangaza akasikia sauti ya mwanamke ile ya jana ambaye alijitambulisha kama mke wa Bahati,
“Dada sikia nikwambie, kama ulikuwa na mahusiano na Bahati ni huko mwanzoni ila sasa hivi Bahati ni mume wa mtu. Jifunze kuwa na heshima na ndoa za watu, mimi na mume wangu tunapendana na wala hajawahi kuniambia kama alipenda mdudu kama wewe. Naomba umkome mume wangu”
“Lakini mimi sijapiga simu, umenipigia simu mwenyewe”
“Ndio nimekupigia simu ili kukujua mwizi wangu usiyeheshimu ndoa za watu. Jifunze kuelewa kuwa Bahati kaoa sasa, huo usumbufu wa kijinga hatuutaki tuache na mume wangu tufurahi, ndoa yenyewe bado change hii unataka uiwekeee kigundu! Utukome”
Erica aliamua kukata ile simu maana aliona ni itamfanya awe na hasira za bure tu na aache kuwaza mambo ya maana aweze ujinga wa kugombana na mke wa Bahati. Kisha akasema,
“Sijawahi kugombana na mwanamke yeyote sababu ya mwanaume, hebu anitolee balaa mie”
Kisha kabla ya kulala akafungulia redio na kusikiliza mahubiri kidogo,
“Jifunze kuombea wengine, Mungu atafungua milango ya baraka kwako pale unapowaombea wengine. Sio unajikumbuka wewe tu, ila kumbuka na wengine”
Erica akazima redio na kusema,
“Hawa wahubiri nao kila leo wana jipya, kwahiyo wanataka nimuombee mke wa Bahati? Nimuombee nini sasa? Wanaona kabisa nimemaliza kuongea na adui yangu eti jifunze kuombea wengine. Jamani mambo mengine, ngoja nilale zangu mie”
Kisha akaamua kulala tu.
 
SEHEMU YA 258


Asubuhi na mapema aliamka na kujiandaa kwenda kazini ila kama alivyopanga kuwa hatoenda kazini kwanza hadi apitie kwakina Dora, kwahiyo alimtumia shemeji yake ujumbe kuwa anapitia hospitali halafu ndio ataenda kazini, shemeji yake alimjibu kawaida tu kuwa poa. Hakujiuliza sana akaona labda shemeji hataki kumuhoji hoji sana.
Erica alienda hadi kwakina Dora ambapo alipofika kituoni alipiga simu halafu mdogo wa Dora alifika na kumpeleka hadi kwakina Dora, ambapo aliingizwa hadi chumbani alikolala Dora kisha Yule mdogo wake alimuacha na Dora na kutoka nje.
Erica alikaa karibu na Dora na kumpa pole huku akimuuliza kipi kimetokea,
“Erica sikutegemea Yule shemeji yako ni mshenzi kiasi hiki”
“Mmmh Dora usitukane tafadhari”
“Nisitukane kitu gani? Unajua alichonitenda? Tena ngojea nikuonyeshe namna ya kumtusi”
Dora alianza kuporomosha matusi na kumfanya hadi Erica aogope, kisha akamwambia,
“Dora, ukiendelea na hayo matusi kwakweli sitaweza kuvumilia, unajua kabisa mimi na matusi ni mbalimbali”
“Mbona ukayafanya hadi ukapata mimba na kuzaa”
“Dora, Dora nakuhurumia ndiomana niko hapa, sijaja unipe matusi au unionyeshe uwezo wako wa kutukana. Sijalelewa hivyo tafadhari, kama hayo mengine niliyofanya yaache nilifanya ila siwezi hayo ya kuongea. Wewe nishakupa pole, nimekuuliza nini kimekusibu unaanza kuporomosha matusi hivi hata ukifika mahakamani ukaporomosha hivyo matusi ni nani ataonekana mwenye makosa kati yako na shemeji yangu?”
“Haya yaishe ila shemeji yako kanifanyia kitu kibaya sana, hadi nikawaza kuwa labda umemtuma anifanyie vile maana wewe ulikimbia na kuniacha nae”
“Hapana, mimi tumbo lilinishika na muda ule ningemuaga shemeji angekataa tu si unaona alikuwa akinibishia nisiondoke”
“Haya bhana, shemeji yako Yule nina haki ya kumuita mshenzi maana alichonifanyia hakifai hata kidogo.Tulikunywa pombe na shemeji yako pale balaa, na wewe hukutokea, nilikuwa nimelewa haswaa nikaamua kumuaga kuwa naondoka ila shemeji yako akasema twende club, sababu nilikuwa nimelewa nikaenda nae, huko nako tulikunywa sana na nilikuwa nimelewa sana. Shemeji yako akanichukua sijui akanipeleka chumba cha hoteli kumbuka nilikuwa nimelewa, shemeji yako akanibaka na kunifanyia mchezo mbaya maana alinifanya kinyume na maumbile”
Erica akashtuka na kushangaa sana,
“Kheee shemeji ndio ana tabia chafu kiasi hiko?”
“Ndio hivyo, tena alivyo mshenzi sababu nilikuwa sijitambui kanitoa pale hotelini na kaenda kunitupa karibu na mtaro, watu ndio wameniokota na kunileta nyumbani. Kwakweli alichonifanyia shemeji yako hapana, nimeenda kushtaki polisi ila shemeji yako kanikana kabisa kuwa hafahamu chochote kuhusu mimi, yani Erica nimeumia sana, shahidi yangu ni wewe maana kesi ipo mahakamani”
Kwakweli Erica alisikitika sana maana alichofanyiwa rafiki yake hakikuwa kitendo cha utu hata kidogo, ingawa rafiki yake huyo amewahi kumtendea mambo mabaya ila yeye hakupanga vitu vibaya kwa huyo rafiki yake. Erica alikuwa kimya tu kisha Dora aliendelea kuzungumza,
“Eraca tafadhari nakuomba uwe shahidi wangu maana ni wewe tuliyekuwa pamoja na ndio unajua kuwa uliniacha na shemeji yako. Kanifanyia kitendo cha kikatili sana, sina nguvu sasa nalala tu unadhani kubakwa ni jambo rahisi? Raha ya mapenzi ufanye kwa utayari ila sio kwa kubakwa halafu kitu kinachoniuma zaidi ni kile kitendo cha kuniingilia kinyume cha maumbile, Erica inauma asikwambie mtu”
“Pole sana rafiki yangu yani nawaza nakosa hata jibu”
“Nisaidie rafiki yangu, nahitaji kupata haki kwa kindendo nilichotendewa, najua huyu mtu ni shemeji yako ila kumbuka kuwa mimi ni mwanamke mwenzako”
“Naelewa Dora, nitakusaidia. Pole sana”
Kisha Erica aliamua kumuaga Dora, na kumuachia hela kidogo kwaajili ya kumsaidia saidia,
“Sina pesa ndugu yangu, ila pokea hiki kidogo”
“Nashukuru Erica, ila usiache kuja mahakamani kutoa ushahidi nakuomba”
“Usijali nitafika”
Kisha Erica akaondoka na kumuona shemeji yake ni mtu asiyefaa kabisa kwenye jamii maana hakuelewa ni kwanini katenda kitu kama kile kwa Dora. Alitembea njiani akielekea kituoni huku akiongea mwenyewe,
“Yani wanaume sijui wana akili gani jamani? Kweli kabisa shemeji anafanya ujinga kiasi hiki! Nawachukia wanaume mie, siwataki kabisa, bora niishi mwenyewe kwa stahili hii sio kwa haya jamani, dada yangu namuhurumia maana sijui awe na moyo wa aina gani kuweza kupokea upuuzi huu alioufanya mumewe”
Wakati anaongea peke yake, kuna gari ilikuja na kupaki mbele yake. Mwenye gari alishusha kioo na kumsalimia Erica,
“Habari yako binti”
“Salama”
“Si unaenda stendi, twende nikusogeze”
“Hapana, asante nafanya mazoezi ya kutembea”
“Aaah! By the way naitwa Jimmy, sijui wewe unaitwa nani?”
“Naitwa Erica”
“Sawa Erica, basi naomba namba zako”
Akakumbuka maneno ya mama yake na kumwambia,
“Hapana, siwezi kukupa namba. Mimi ni mke wa mtu, na sipendi kuongea kwenye simu na mtu mwingine zaidi ya mume wangu”
“Hebu acha kunichekesha Erica, umesikia wake za watu huwa hawatoi namba? Unajua namba yako naitaka ya nini? Pengine ni maswala ya kazi? Sio kila mwanaume anayetaka namba zako ni ana lengo la kukutongoza, hebu futa hiyo fikra kwanza. Utakosa bahati kwa kujifanya oooh mimi mke wa mtu. Shauri yako, mimi nahitaji namba yako maana kuna kazi nataka kukushirikisha”
Erica akafikiria kidogo na kuamua kumtajia mtu Yule namba yake sababu mtu Yule alionekana ni mtu wa makamo na mwenye heshima zake, kisha akaagana na Erica.
 
SEHEMU YA 259


Erica alielekea ofisini, na alipofika kwenye meza yake tu James alimuita, kiukweli Erica alienda ofisini kwa James ila hakuwa na amani anayokuwaga nayo siku zote. James alimsalimia kisha akamwambia,
“Najua Yule mjinga kashakuelezea habari za kijinga ndiomana umekuja bila amani”
“Hapana shemeji ila kwanini umefanya vile?”
“Erica, wewe ni msomi ila nashangaa umeanza vipi urafiki na Yule msichana asiye na akili hata kidogo”
“Hata kama hana akili ndio umfanyie vile kweli?”
“Erica, unanifahamu vizuri shemeji yako na unamfahamu vizuri mke wangu Bite, hivi nina mke mzuri kama Bite halafu nikafanye ujinga na Yule rafiki yako mjinga mwenye sura nzito kama uji kweli? Nampenda sana mke wangu, Bite wangu mzuri bhana, hawezi kufanana na ujinga ujinga ule”
“Mmmh shemeji, kumbuka nilikuacha nae”
“Sikia Erica, labda kama umepanga na Yule mjinga wako kunichafua jina langu ila kumbuka mimi ni shemeji yako tena ni mume wa dada yako mzazi ambaye umezaliwa nae tumbo moja. Ukisikiliza maneno ya kijinga unataka nini kwangu? Huwa nakusaidia kwa moyo mmoja na hata sina lengo baya, nilikwambia mambo ya kijinga niliyoyafanya mwanzo hayapo tena kwangu, nianze vipi kwa rafiki yako asiye na mvuto Yule!”
Erica alikuwa kimya tu akimsikiliza shemeji yake anavyojitetea, kisha James akaendelea kuongea,
“Sikia siku ile ilivyokuwa, baada yaw ewe kuondoka na hukurudi tena nikakupigia simu hukupokea. Nikaenda kuangalia chooni ila kuna mtu alikuona akasema kuwa uliondoka, nilirudi na kukaa na Yule mjinga, nikamtaarifu kuwa umeondoka ila hakuwa hata na mashaka aliendelea kunywa pombe na kula nyama. Msichana hajielewi hata robo Yule, anakunywa kila kilevi, castle lite twende, dompo twende, valuer twende mpaka konyagi jamani Yule rafiki yako kashindikana. Namwambia mimi naondoka anadai yeye anaendelea kupombeka ikabidi kwa huruma yangu nimuachie hela hata akimaliza kulewa akodi tax arudi kwao, nilimuachia elfu hamsini nikaondoka zangu. Nashangaa kuitwa polisi eti nina kesi ya kubaka sijui kumuingilia mtu kinyume na maumbile na kumtupa, jamani Yule binti sina hamu nae loh! Ataje aliokuwa nao kwenye ulevi wake, muda huo nilikuwa na familia yangu mie nalala na mke na mwanangu halafu yeye ananiletea habari za kijinga kiasi hiko”
“Kheee kumbe ndio ilivyokuwa?”
“Ndio hivyo Erica, najua atakuwa amekulisha sumu ili kuniona mimi mbaya. Hivi rafiki yako anachofanya si kunichafulia jina jamani! Mimi nina kampuni yangu na nina pesa zangu halafu kijitu cha ajabu ajabu kinataka kunichafulia jina jamani dah! Hivi nikitaka mwanamke mimi naweza kukosa? Kama pesa ninayo, mgonjwa mkubwa wa mwanamke ni pesa, licha ya hivyo machangudoa wamejaa tele si ningewachukua na kufanya nao ujinga huo kama nahitaji kufanya ujinga ila mimi siwezi kufanya hivyo, naiheshimu familia yangu Erica, nampenda dada yako naomba uelewe na uondoe dhana potofu kuwa mimi naweza kufanya ujinga wa namna ile. Erica wewe ni binti uliyesoma, achana na marafiki wasiojielewa”
Erica alimsikiliza shemeji yake kisha akamuaga kuwa anaenda kufanya kazi sasa, ila James aliendelea kuongea na kumwambia,
“Unapokuwa kwenye kazi zako hapo jaribu kufikiria kama mimi naweza kufanya ujinga ulioambiwa na rafiki yako. Sipendi kusingiziwa mimi, nampenda sana mke wangu”
Erica alienda kukaa na kuendelea na kazi zake ila kiukweli mpaka muda huo hakujua wa kumuamini ni nani kati ya Dora na shemeji yake James maana wote walionekana kuwa wanaongea ukweli.
Erica alifanya kazi zake na alipomaliza alimuaga shemeji yake na kwenda zake kwao.
 
SEHEMU YA 260

Alifika kwao akitafakari mambo ya Dora na shemeji yake James ila hakupata jibu na hata hakujua kuwa akienda mahakamani atasema nini maana hakujua ukweli, ukizingatia ukweli waliujua wenyewe wawili kwahiyo kwa Erica ilikuwa kitendawili kikubwa sana.
Basi akaoga na kula kisha kwenda chumbani kwake na mwanae, muda kidogo akapigiwa simu, namba ilikuwa ni ngeni akapokea na kuanza kuongea nayo,
“Hallow, nani mwenzangu?”
“Mimi Jimmy, Yule umekutana naye mchana. Unaendeleaje muda huu?”
“Salama tu”
“Mbona mimi huniulizi kuwa naendeleaje?”
Erica akaona mitego hiyo, ila akaamua kujigelesha na kumuuliza,
“Unaendeleaje?”
“Kiukweli siendelei vizuri maana nina mawazo haswaaa”
“Aaah pole”
“Asante, ila hujaniuliza ni mawazo ya nini?”
“Haya, ni mawazo ya nini?”
“Erica, tangu nimekuona ile asubuhi sina raha kabisa, nipo kazini nakuwaza tu wewe. Nakupenda Erica”
“Ila si nimekwambia mimi ni mke wa mtu?”
“Kwani mke wa mtu kitu gani Erica? Kwani ukinipa naondoka nayo jamani? Si inabaki kwako? Niponye mtoto wa mwanamke mwenzio”
Erica akakata ile simu na akaizima kabisa kwani hakutaka gasia maana kwake zilikuwa gasia zile ukizingatia alishaanza kukataa habari za wanaume, ingawa hakujua kati ya shemeji yake na Dora ni nani mwenye makosa.
Aliamua kulala, wakati amelala akajiwa na njozi kuwa Erick yupo hospitali na ana hali mbaya sana, aliamka na kuhema sana alijikuta tu akipiga magoti na kuomba,
“Eeeh Mungu nakuomba mtetee Erick na afya yake, sikukusudia mimi kumfanya aumwe au awe katika hali mbaya. Nakuomba Mungu wangu nisamehe kwa yote niliyoyatenda, naomba itetee afya ya Erick. Amen”
Alirudi tena kitandani akachukua simu yake na kuiwasha, ila alipoiwasha tu kuna ujumbe uliingia kuwa amepokea muda wa maongezi wa shilingi elfu kumi, alipoangalia aliona umetokea kwa Yule mzee Jimmy, ila kwa muda huo Erica hakutaka kufikiria kuhusu Yule mzee, kwahiyo alimpigi Tumaini ili kujaribu kuulizia hali ya Erick ingawa hakujua kama Tumaini angepokea simu yake au la ila kwa muda mfupi tu Tumaini alipokea ile simu na alivyopokea tu akamwambia Erica,
“Nakutumia namba za hospitali upige mwenyewe simu uongee na Erick, sitaki kusema chochote mimi”
Tumaini akakata simu halafu akamtumia namba Erica, ambapo Erica alizipiga zile namba na kuomba kuongea na Erick ambapo Erick alipewa ile simu,
“Ni wewe Erica kweli ndio umepiga muda huu?”
“Ndio ni mimi Erick, nakuombea upone baba yangu”
“Erica umeniita baba?”
“Ndio, wewe ni mwanaume na unauwezo wa kunilea kwahiyo wewe ni kama baba kwangu”
“Siamini Erica, ila nitakutafuta kesho”
Erick alionekana kuongea kwenye hali ya furaha sana hapo mwishoni kwahiyo akaagana na Erica na kukata simu, kisha Erica akalala sasa.

Kulipokucha kama kawaida akajiandaa na kwenda kazini, alifika na kufanya kazi zake, ila kwenye mida ya saa nne alipigiwa simu na Yule meneja wa benki akimtaka Erica aende muda huo, kwahiyo Erica alienda kumuaga bosi wake kisha kwenda huko benki.
Alifika na kuingia ofisini kwa meneja,
“Nimekuita hapa, maana leo kuna kikao cha bodi na wakurugenzi wote watakuwepo. Niliwasilisha kuhusu swala la mwanao na wamempenda sana, tunahitaji mwanao awe balozi wa akaunti ya watoto hapa benki”
Kwakweli Erica alijihisi furaha sana moyoni mwake, na hata hakupinga kuhusu swala hilo kisha baada ya lisaa limoja Yule meneja akamwambia Erica kuwa aende nae kwenye kikao ili amtambulishe na kisha kesho yake amlete mtoto wake, Erica alikubali na kuanza kufatana na Yule meneja.
Kisha walipokarinia Yule meneja akamwambia Erica,
“Inabidi uwe na majibu mazuri maana leo na mkurugenzi mkuu yupo”
“Sawa”
Wakaingia ndani, Erica akaona kuna wababa watano, kisha kuna mmoja alikuwa amekaa kwenye kiti cha mbele ambapo Yule meneja alimwambia Erica kwa taratibu,
“Yule wa mbele ndio mkurugenzi mkuu”
Erica alipomuangalia vizuri, akagundua ndio Yule mzee Jimmy.

ITAENDELEA
 
Back
Top Bottom