Simulizi : Ukweli Wenye Kuuma (Painful Truth)

Simulizi : Ukweli Wenye Kuuma (Painful Truth)

SEHEMU YA 31

“Hapana. Bado haitosaidia. Nitaua tu. Hiyo ndio sababu ambayo inanifanya kutokuingia katika mahusiano” Andy alisema.
Moyoni alipanga kabisa tena kwa moyo mmoja kutokujiingiza katika mahusiano lakini kila alipokuwa akiwangalia msichana Annastazia Kapama alionekana kuanza kuusaliti moyo wake. Hakuona kama angeendelea kuwa katika msimamo ambao alikuwa amejiwekea.
Annastazia Kapama alikuwa ni msichana aliyetoka nchini Tanzania ambaye baba yake alikuwa Waziri wa Mambo ya Ndani na Nje, Bwana Simon Kapama. Ingawa walikuwa wamezaliwa watatu katika familia yao lakini Annastazia ndiye ambaye alikuwa akipendwa zaidi.
Bwana Kapama hakutaka watoto wake wasome nchini Tanzania jambo ambalo lilimpelekea kuanza kuwasomesha nje ya nchini katika nchi za Marekani, Uingereza na India. Kapama alikuwa msichana mwenye mvuto mkubwa shuleni hapo kiasi ambacho wavulana wengi walikuwa wakitamani sana kuwa nae.
Umbo lake lilikuwa la kimisi huku uso wake wa upole ndio ulikuwa chachu kubwa ya uzuri wake. Mashavuni mwake, vishimo viliwili vilikuwa vikionekana lakini kila alipokuwa akicheka au kutabasamu, vishimo vile vilionekana vizuri zaidi.
Muda wote Annastazia alikuwa mcheshi hali ambayo ilimfanya kupata marafiki wengi shuleni hapo. Japokuwa wanafunzi wengi walikuwa wakijaribu bahati zao kwa Annastazia lakini kamwe hakuonekana kuwa msichana mwepesi kabisa.
Katika kipindi chote cha maisha yake, Annastazia alitamani sana kuwa mwanasiasa kama alivyokuwa baba yake. Kila siku alikuwa akisoma vitabu vilivyokuwa vimeandikwa na wanasiasa wengi ili kujua walianzia wapi mpaka kuwa wanasiasa wakubwa.
Kama ilivyokuwa kwa Andy na ndivyo ilivyokuwa kwa Annastazia, kamwe hakutaka kujiingiza katika mahusiano ya kimapenzi, kwake aliyachukia mapenzi kama alivyokuwa akimchukia adui yake aliyemtishia kumuua.
Katika kila kona, alikuwa akiyaepuka mapenzi. Ilikuwa ni kawaida kuongea na Annastazia kuhusu mambo mengine na kuondoka huku akiwa amekasirika mara tu utakapoanza kuzungumzia mapenzi. Hakujiona kuwa tayari kuingia katika mapenzi, alijiapiza kuitunza bikira yake mpaka kwa mwanaume ambaye angetokeza kumuoa.
Kadri siku zilivyozidi kwenda mbele na kuzidi kuangaliana, kuna vitu ambavyo vikaanza kujitokeza ndani ya mioyo yao. Mara ya kwanza hawakuwa wakivifahamu vitu hivyo mpaka pale ambapo walianza kukaa pamoja na kuanza kuzungumza. Kila mmoja akaanza kujisikia furaha kila alipokuwa akiongea na mwenzake kiasi ambacho kama walikuwa mbali hawakujisikia kuwa na furaha kabisa.
Mara ya kwanza walionekana kutokujua ni kitu gani kilikuwa kikiendelea lakini mara walipoanza kugusana, miili yao ikaanza kujisikia hali ya tofauti. Ukaribu wao ukaanza kuongeeka kiasi ambacho wanafunzi wakaanza kujua ni kitu gani kilikuwa kinaendelea katika maisha yao. Andy akawa haambiwi kitu chochote juu ya Annastazia lakini nae Annastazia akawa haambiwi chochote juu ya Andy.
Kwa mara ya kwanza katika maisha yao wakajikuta wako ndani ya gari peke yao na kuanza kugusanagusana mpaka pale tamaa ya mwili ilipowashika. Hakukuwa na kilichoendelea zaidi ya kuanza kufanya ngono.
Andy akawa ameitoa bikira ya Annastazia lakini nae Annastazia akawa amemkaribisha Andy katika ulimwengu wa ngono. Kuanzia siku hiyo ndipo ukaribu wao ulipozidi zaidi na zaidi, walipendana na kuthaminiana kupita kawaida.
“Utanioa?” Annastazia alimuuliza Andy.
“Unaniuliza au unaniambia?”
“Nakuuliza”
“Hapana. Hapo umeniambia” Andy alimwambia Annastazia na kisha wote kukumbatiana.
Katika kipindi hicho hakukuwa na mtu aliyekuwa akifikiria kama watu walikuwa wakilia katika mahusiano, hawakukumbuka kama kuna watu walikuwa radhi kuua mara tu wanaposalitiwa, wao kwao waliona mahusiano
 
SEHEMU YA 32

kuwa ni furaha ambayo ingedumu katika maisha yao yote. Wakajisahau kama kulikuwa na maumivu makali katika mahusiano ya kimapenzi.

Kama ni jeuri ya fedha basi kijana George alikuwa akiongoza nchini Tanzania. Yeye alikuwa mtoto wa tajiri wa Bwana Mtimbi ambaye alikuwa akimiliki kiasi kikubwa cha fedha. Ukiachilia mbali utajiri huo mkubwa aliokuwa akimiliki baba yake, pia alikuwa akijivunia sana kutokana na baba yake kuwa Waziri wa Nishati na Madini nchini Tanzania.
Maisha ya starehe ndio ambayo alikuwa amezoea kuishi toka katika kipindi ambacho alikuwa amepata ufahamu wa kujitambua. Alikuwa akimshawishi sana baba yake amnunulie magari ya kifahari na kutokana na mapenzi makubwa ambayo alikuwa nayo baba yake, alikuwa akimnunulia.
Mitaani watu hawakuwa na amani hata kidogo, George na marafiki zake walikuwa wakileta fujo na magari yao ya kifahari ambayo yalionekana kuwa kero kwa Watanzania ambao asilimia themanini walikuwa wakiishi katika maisha ya dhiki.
Alizaliwa huku akiwa amezikuta fedha na hata wakati huo alikuwa akikua huku akiziona fedha, kwake hakuwahi kuzitafuta fedha hizo zaidi ya kuzitumia kadri ya uwezo wake. George alikuwa miongoni mwa watoto wa viongozi ambao walikuwa wakipenda sana starehe, ilikuwa ni bora umnyime kitu chochote lakini si kumnyima kwenda klabu nyakati za usiku au kulala na wasichana watatu kila ifikapo mwisho wa wiki.
Mtanzania gani ambaye alikuwa akiishi Dar es Salaam hakuwa akimfahamu George? Kila mtu alikuwa akimfahamu kijana huyo ambaye sifa zake chafu zilikuwa zikiendelea kutapakaa katika kila kona jijini Dar es Salaam.
George akajikuta akiwa ameanza kuyanufaisha magazeti na vyombo vingine vya habari. Kuonekana kwa picha yake katika magazeti na kuandikwa maneno yaliyojaa kashfa kuliyafanya magazeti hayo kununuliwa kupita kawaida.
Baba yake, Bwana Mtimbi alijitahidi kumuita George mara kwa mara na kuongea nae lakini wala hakuonyesha mabadiliko yoyote zaidi ya kuendelea kuwa vile vile huku wakati mwingine akionekana kuzidisha. Ingawa baba yake alikuwa na hasira juu ya tabia zake lakini hakuwa na la kufanya zaidi ya kumuacha afanye kile ambacho alikuwa akijisikia kufanya.
Fedha zikamtia wazimu George, akaonekana kuchanganyikiwa, kila siku alikuwa akipamba vichwa vya habari katika magazeti mengi jijini Dar es Salaam. George akaonekana kuishusha heshima ya baba yake, watu wakaonekana kumdharau kwa kuwa tu alishindwa kabisa kumdhibiti kijana wake ambaye kadri siku zilivyozidi kwenda mbele na ndivyo ambavyo aliendelea kuvuma kwa kashfa.
“Unafikiri nisipofanya haya sasa hivi nitayafanya kipindi gani? Umri unaenda, na ujana ni maji ya moto, acha nihangaike nayo” Hayo yalikuwa maneno ambayo mara kwa mara yalikuwa yakitoka kinywani mwa George.
Ingawa kila siku alikuwa akifanya mambo mengi ya starehe pamoja na kutembea na wasichana wengi lakini kila siku moyo wake ulikuwa kwa msichana mmoja tu, Annastazia Kapama. Akili yake ilikuwa imechanganyikiwa juu ya binti huyo, kwake, lengo lake halikuwa kumchezea na kisha kumuacha kama wasichana wengine, kwa Annastazia, alitaka kumuoa kabisa na kuachana na mambo mengine.
Kwa mara ya kwanza alikutana na Annastazia katika kipindi ambacho watoto wa Mawaziri walikuwa wamekutana katika sherehe ya kumpongeza mtoto wa Waziri Stefano, Anania. Siku hiyo ndio alikuwa amemuona Annastazia, akauhisi moyo wake ukimpenda kwa moyo wa dhati.
George hakutaka kuchelewesha muda, alichokifanya ni kumfuata Annastazia
 
SEHEMU YA 33

na kumuelezea kile ambacho alikuwa akikihisi moyoni mwake. Annastazia hakuonekana kuwa mwepesi hata mara moja, akamkataa George.
George akaonekana kuumia hali ambayo ilimfanya kukosa raha kila siku. Unyonge ukaanza kumtawala moyoni, mapenzi yakaonekana kuanza kumtesa. Alishindwa kulala vizuri wala kula vizuri kwani kila alipokuwa akiufikiria uzuri wa Annastazia halafu akifikiria kwa jinsi alivyokataliwa, hakuona sababu yoyote ya kumfanya kuwa na furaha.
Kila siku alikuwa akimfuata shuleni St’ Marys lakini napo haikuonekana kumsaidia. Annastazia aliendelea kumkataa George, hakuvutiwa nae hata siku moja. George hakuonekana kukata tamaa, kwake aliamini kwamba asilimia kubwa ya wasichana hukaza siku ya kwanza na hatimae kuulegeza msimamo wao.
Kila siku aliendelea kumfuatilia Annastazia lakini bado msimamo wake ulikuwa vilevile. Hapo ndipo George alipoamua kubadilika, skendo mbalimbali ambazo alikuwa nazo aliziona kuanza kumharibia. Alichokifanya kwa wakati huo ni kutoa kiasi fulani kwa waandishi wa habari kwa ajili ya kuandika mambo mengi juu yake kwa ajili ya kumsafisha.
Wiki nzima magazeti ya udaku yalikuwa yakiandika kuhusu mabadiliko ambayo alikuwa ameamua kuyafanya George juu ya maisha yake. Kwa mara ya kwanza wananchi walionekana kutokuamini lakini ya mwezi mzima wakaonekana kuamini kutokana na magazeti yale kuendelea kumsafisha zaidi na zaidi.
“Nimeamua kubadilika. Nimekubali kwamba yale niliyokuwa nikiyafanya yalikuwa ni ujinga mbele zenu na hata mbele ya jamii” George aliwaambia wazazi wake.
Bado harakati zake za kumtafuta Annastazia na kumuweka katika himaya zilikuwa zikiendelea kila siku lakini Annastazia hakuonekana kukubaliana nae hata mara moja japokuwa alikuwa akijua kwamba George alikuwa amebadilika.
Moyo wa George ukaonekana kupatwa na pigo kubwa mara baada ya kufahamu kwamba Annastazia alikuwa akikaribia kuelekea nchini Marekani masomoni. Akaongeza nguvu zaidi za kumwambia kuwa nae lakini bado Annastazia alikuwa akikataa.
“Nakuomba Annastazia. Nitakuwa tayari kuwa mwaminifu juu yako mpaka utakaporudi” George alimwambia Annastazia kwa sauti ya chini iliyokuwa ikimaanisha.
“Sikutaki George. Muda wangu wa kuwa na mwanaume haujafika” Annastazia alimwambia George.
“Ninakupenda Annastazia, ninakupenda sana” George alimwambia Annastazia.
“Sikutaki” Annastazia alimwambia George na kisha kuwasha gari lake na kuondoka.
Siku hiyo ilikuwa pigo kubwa kwa George, alipata muda mwingi wa kuongea na Annastazia lakini bado alionekana kuwa mgumu kukubaliana nae. Usiku hakulala, alikesha kama popo huku akimfikiria Annastazia ambaye alikuwa ameuteka moyo wake kupita kawaida.
Kuanzia siku hiyo hakuweza kumuona tena Annastazia mpaka pale aliposikia kwamba alikuwa amesafiri kuelekea nchini Marekani kuanza masomo. George akakosa amani, alichokifanya kwa wakati huo ni kuwaleza wazazi wake juu ya kile ambacho kilikuwa kimetokea.
“Unampenda kweli?” Mzee Mtimbi aliuliza.
“Ninampenda. Niko tayari kumuoa hata atakaporudi” George alimjibu baba yake.
Kwa hali ambayo alikuwa akionekana nayo George ilikuwa ni vigumu sana kwa Bwana Mtimbi kuvumilia, alichokifanya ni kuanza safari kuelekea nyumbani kwa Bwana Kapama na kuwaelezea vyote ambavyo George alikuwa amemwambia.
Bwana Kapama na mkewe wakaonekana kufurahia kwani kutokana na wao kuwa marafiki, waliona urafiki ungeongezeka zaidi kama watoto wao wangeungana na kuwa kitu kimoja. Wote wakakubaliana, kilichotakiwa
 
SEHEMU YA 34

mahali hapo ni kumsubiria Annastazia arudi kutoka masomoni na kisha kumwambia kile ambacho kilikuwa kimeendelea.
“Utaweza kumsubiri mpaka miaka miwili ipite?” Bwana Kapama aliuliza.
“Ni michache sana. Hata ukisema mitano, niko tayari” George alisema.
“Kwa hiyo tumpe taarifa juu ya kinachoendelea?”
“Hapana. Nataka tumfanyie ‘suprise’”
“Ila si mpaka ninyi mkubaliane?”
“Ndio. Ila naona kama ninyi wazazi mkihusika, hakutokuwa na tatizo halafu mtakuwa mmenipa urahisi” George aliwaambia.
Hapo ndipo uvumilivu wa George ulipoanza. Mwezi wa kwanza ukakatika, wa pili ukakatika na wa tatu nao ukakatika. Uvumilivu bado ulikuwa ukiendelea moyoni mwake. Hatimae mwaka ukakatika. George hakutaka kuwa na uhusiano na msichana yeyote, alikuwa akimsubiria Annastazia.
Miezi bado iliendelea kukatika na hatimae miezi tisa kukatika. Ni miezi mitatu tu ndio ambayo ilikuwa imebaki hata kabla Annastazia hajarudi nchini Tanzania na kuanza maisha mapya huku lengo lake likiwa ni kujifundisha kuhusu siasa na miaka mitano ijayo agombee ubunge katika uchaguzi mkuu.
“Kama nimeweza kuvumilia kwa muda wa mwaka mmoja na miezi tisa, hakika miezi mitatu haitonishinda, nitaendelea kumsubiria” George alijisemea.
Kuhusika kwa wazazi wa pande zote mbili ndio ilikuwa sababu ambayo ilimpa nguvu kwa kuona kwamba kwa vyovyote vile ni lazima Annastazia angekubali na kuwa nae kabla ya kumuoa na kuwa mume na mke.
****
Mapenzi kati ya Andy na Annastazia yalikuwa yakiendelea kama kawaida, kwao mapezi yalionekana kuwa na furaha na kamwe hawakuipa mioyo yao kufikiria kama kuna watu walikuwa wakiumizwa katika mahusiano.
Walipendana na kuthaminiana huku wakipeana ahadi za kuishi milele huku wakiwa pamoja. Maneno yale ambayo yalikuwa yakitoka mara kwa mara vinywani mwao yalikuwa yakionekana kuendana sana na matendo ambayo walikuwa wakiyaonyesha. Mitihani ya mwisho ikafika na hatimae kumaliza. Andy hakuwa na jinsi, alichokifanya ni kumpeleka Annastazia nyumbani kwao na kumtambulisha kwa wazazi wake.
“Umeamua kumchukua Mtanzania kama mama yako?” Bwana Wayne aliuliza.
“Ndio. Nimefuata kile ambacho baba alikifuata nchini Tanzania” Andy alijibu na kuwafanya wote kuanza kucheka sebuleni pale.
“Tuna mapenzi ya kweli sana. Ninauunga mkono uamuzi wako mtoto wangu” Bi Happy alimwambia Andy.
Annastazia alionekana kuwa na furaha, kutambulisha ndani ya nyumba ya tajiri Wayne ilionekana kuwa furaha kwake na kuwa kitu ambacho hakuwahi kukitarajia katika maisha yake. Kitu ambacho alikiahidi mbele ya uwepo wa watu hao ni kumpenda Andy kwa moyo wa dhati katika maisha yake yote.
Wote wakajiona kuwa huru, wakawa radhi kuyaonyesha mapenzi yao mbele ya mtu yeyote, kitendo cha wazazi wa Andy kukubali kilionekana kuwapa faraja kupita kawaida. Kazi ilikuwa imebaki moja tu, kuwaelezea wazazi wa Annastazia kile ambacho kilikuwa kimetokea katika maisha yake katika kipindi ambacho alikuwa nchini Marekani.
“Itanibidi kuelekea nchini Uingereza, kuna vitu inabidi niende kuviangalia. Waambie wazazi wako kila kitu na kunipa taarifa ya kilichoendelea” Andy alimwambia Annastazia.
Baada ya siku tatu, Andy akasafiri kuelekea nchini Uingereza kama moja ya matembezi yake kabla ya kujiunga na chuo cha Oxford ambacho kila siku kilikuwa kichwani mwake. Hakuwa na wasiwasi na mpenzi wake, kitu ambacho alikuwa akikiamini ni kwamba wangekubaliwa na hatimae kufunga ndoa katika kipindi ambacho watakuwa wakiendelea na masomo ya chuo.
Siku nne baadae, Annastazia akaanza safari kuelekea nchini Tanzania. Moyo wake ulikuwa ukimfikiria mpenzi wake na namna ambayo angewaambia wazazi wake.
 
SEHEMU YA 35

Hakufikiria kama wazazi wake wangekataa kutokana na baba yake Andy kuwa maarufu na tajiri mkubwa duniani.
Kitu ambacho alikuwa akikitaka kwa wakati huo ni kuwaeleza juu ya moyo wake. Katika kipindi chote ambacho aikuwa chuoni, kamwe hakuwahi kumfikiria George ambaye alikuwa akimsumbua sana, moyo wake ulikuwa ukimfikiria mtu mmoja tu, Andy.
Mara baada ya kumaliza kila kitu alichokifuatilia nchini Uingereza, Andy akaamua kuanza safari kuelekea nchini Tanzania huku lengo lake likiwa moja tu. Katika maisha yake yote, alichagua kuwa raia wa Tanzania, aliamua kuchukua uraia wa mama yake kwa kuwa alitaka kuwa karibu sana na Annastazia.
Kila kitu alikuwa akikifanya kwa siri kubwa sana. Kwa sababu alikuwa na vyeti vya kuzaliwa wala hakuwa na pingamizi lolote, alihesabika na kuwa mmoja wa Watanzania kama ilivyokuwa kwa Watanzania wengine.
Hakutaka kuwasiliana na Annastazia katika kipindi ambacho alikuja nchini Tanzania kisiri, alichokifanya mara baada ya kumaliza taratibu zote ni kurudi nchini Marekani na kuamua kuwaambia wazazi wake. Bwana Wayne akaonekana kukasirika lakini hasira zake hakutaka kuzionyesha waziwazi kwa sababu alijua kwamba mtoto wake alikuwa amefanya uamuzi ambao aliuona kufaa katika maisha yake.
“Maisha yangu yatakuwa nchini Tanzania tu. Nitahitaji kuwa karibu na mpenzi wangu” Andy aliwaambia wazazi wake ambao wala hawakuwa na kipingamizi zaidi ya kumtaka kuanza masomo ya chuoni huku kiu yake ikiwa ni kutaka kuwa dokta wa viumbe hai, yaani wanyama na binadamu kwa ujumla.
“Nadhani hapa ndipo Annastazia atajua ni kwa jinsi gani ninampenda’ Andy alijisemea huku akiziangalia picha za Annastazia katika kompyuta yake.

Annastazia akawa na kiu kubwa ya kutaka kuwaona wazazi wake, kilikuwa kimepita kipindi kirefu sana pasipo kuwaona zaidi ya kuongea nao simuni tu. Ndani ya ndege alionekana kuwa na presha kubwa, aliiona ndege ikienda kwa mwendo wa taratibu sana.
Kwanza alikuwa na kiu kubwa ya kuwaambia wazazi wake juu Andy ambaye alionekana kuwa kila kitu kwake. Alikuwa na uhakika wa asilimia mia moja kwamba wazazi wake wangekuwa pamoja nae bila kipingamizi chochote.
Ndege ilichukua masaa kadhaa na ndipo ikaanza kutua katika uwanja wa ndege wa Mwl Julius Kambarage Nyerere ndani ya jiji la Dar es Salaam. Annastazia akaanza kuchungulia kwa nje kupitia kidirisha kidogo ambacho kilikuwa katika upande wake.
Ndege ikasimama na hatimae abiria kuruhusiwa kutoka ndani ya ndege hiyo. Annastazia aliuona mwili wake ukimtetemeka huku kwa mbali kijasho kikionekana kumtoka. Katika kipindi hicho, alikuwa na kiu kubwa sana ya kuwaona wazazi wake kwa mara nyingine tena.
Abiria wakaanza kuteremka katika ngazi za ndege ile huku wakitakiwa kutotoka nje ya jengo la uwanja wa ndege kabla ya mizigo yao kuchunguzwa. Wakatoka mikono mitupu ndani ya ndege ile huku gari maalumu likifika mahali hapo na kuchukua mizigo yao.
Akaanza kupiga hatua za haraka haraka, ingawa alikuwa amebakiza hatua chache kuwaona wazazi wake lakini kwake zikaonekana kuwa hatua nyingi. Alimuona abiria aliyekuwa akitembea mbele yake kutembea kwa mwendo wa taratibu kupita kawaida, alitamani kumpita na kuwa wa kwanza.
Mara baada ya mizigo kuchunguzwa, abiria wakaichukua mizigo yao na kuelekea sehemu ambayo ndugu zao na marafiki walikuwa wamekaa wakiwasubiri. Ghafla, Annastazia akaanza kukimbia kuwafuata wazazi wake na kisha kuwakumbatia kwa furaha.
 
SEHEMU YA 36

Kuwaona wazazi wake kwa mara nyingine lilionekana kuwa tukio kubwa na la kipekee katika maisha yake, furaha ikaonekana kumzidi, akajikuta akianza kutokwa na machozi. Wakakumbatiana kwa sekunde kadhaa na kisha kuachiana.
Hapo ndipo alipogundua kwamba wazazi wake walikuwa wamekuja na mtu mwingine mahali hapo, huyu alikuwa George. Annastazia akaonekana kushtuka, hakuamini kumuona George mahali hapo. Huku akionekana kushangaa, akayapeleka macho yake kwa wazazi wake, tabasamu pana yalikuwa yakionekana nyusoni mwao.
“Karibu Annastazia...” George alimkaribisha Annastazia.
“Asante” Annastazia alisema na kisha kulichukua begi lake.
Furaha yote ambayo alikuwa nayo katika kipindi kichache kilichopita ikatoweka moyoni mwake, uwepo wa George mahali pale ulionekana kumkasirisha. Kwa kipindi hicho alikuwa akikumbuka mbali sana toka katika kipindi ambacho George alikuwa akimfuatilia na kumkataa.
Wakaingia ndani ya gari, Annastazia hakutaka kuongea tena, muda wote macho yake yalikuwa yakiangalia nje kupitia dirishani. Alionekana kukasirika, uwepo wa George mahali pale ulionekana kumkasirisha kupita kawaida.
Gari likafunga breki nje ya nyumba kubwa ya kifahari, geti likafunguliwa na gari kuingizwa ndani. Annastazia akateremka na moja kwa moja kuelekea chumbani kwake. Bado alionekana kutokuwa katika hali ya kawaida, mama yake akaanza kupiga hatua kumfuata kule chumbani alipokuwa.
Annastazia alikuwa amelala kifudi fudi huku uso wake ukiangalia pembeni, mama yake akaingia na kukaa karibu nae pale kitandani. Bado ukimya ulikuwa umemtawala Annastazia, hakuongea kitu chochote kile zaidi ya kumwangalia mama yake kana kwamba hakuwa akimfahamu.
“Mbona umebadilika hivyo?” Bi Sara aliuliza.
“Nahitaji muda wa kupumzika mama” Annastazia alimwambia mama yake.
Ingawa Bi Sara alionekana kufahamu kile ambacho kilikuwa kimememsababisha binti yake kuwa katika hali hiyo, akaamua kutoka ndani ya chumba kile na kuelekea sebuleni. Uso wake ulikuwa ukionyesha tabasamu pana, kwake aliona kwamba kazi wala haikuwa kubwa kama ambavyo walikuwa wakifikiria kabla.
“Kidogo uwepo wako umeonyesha mafanikio” Bi Sara alimwambia George.
“Mmh!”
“Mbona unaguna?”
“Inawezekana kweli? Hali yake haikuwa ya kawaida kabisa” George alisema.
“Hiyo niachie mimi. Unajua imekuwa kama suprise kwake, hata kama ningekuwa mimi ningekuwa katika hali kama yake” Bi Sara alimwambia George.
Siku hiyo Annastazia hakutoka chumbani kwake, alijifungia muda wote. Moyo wake bado haukuwa na furaha hata kidogo, kadri picha ya George ilivyokuwa ikimjia kichwani mwake ilionekana kumkasirisha. Moyo wake haukutokea kumpenda George wala kuvutiwa nae.
Wazazi wake hawakutaka kuvumilia kumuona akiwa kwenye hali hiyo, walichokifanya ni kumuita na kuongea nae sebuleni. Annastazia hakutaka kuwaambia ukweli wazazi wake japokuwa alikuwa akifahamu fika kwamba wazazi wake walikuwa wakifahamu kila kitu.
“Ni mchoko tu” Annastazia aliwaambia.
Huo ndio ukawa mwanzo wa maisha yaliyokuwa na karaha, Annastazia hakuwa na raha tena, uwepo wa George ambaye alikuwa akifika nyumbani hapo mara kwa mara ulionekana kumkasirisha kupita kawaida. Hakumpenda kabisa George ingawa wazazi wake walikuwa wakiulazimisha ukaribu kuwepo miongoni mwao.
Kila alipokuwa akija George nyumbani hapo, Annastazia alikuwa akiitwa na kuachwa sebuleni pamoja na George. Muda wote wa kukaa hapo sebuleni Annastazia hakuwa akiongea kitu chochote kile zaidi ya kuangalia televisheni.
Mapaka kufikia hatua hiyo tayari akaona kulikuwa na kila dalili za pingamizi kutoka kwa wazazi wake kama tu angewaambia kuhusu Andy, alichoamua ni kukaa kimya. Kamwe George hakuchoka kuja nyumbani hapo, kila siku alikuwa akifikia nyumbani hapo.
 
SEHEMU YA 37

Bwana Kapama na mkewe, Bi Sara walikuwa wakihakikisha kwamba ukaribu huo unazidi zaidi na zaidi. Baada ya miezi miwilili, Annastazia akajikuta akianza kuongea na George bila kupenda. Wazazi wake wakaona jambo hilo kutokutosha, wakazidi kuwafanya watu hao kuwa karibu zaidi na zaidi hasa mara walipokuwa wakiwapa safari za kwenda katika mikoa ya jirani kama Morogoro na Dodoma huku wakati mwingine wakiwataka kwenda Zanzibar kwa ajili ya matembezi.
Ingawa mara kwa mara alikuwa akiwasiliana na Andy lakini katika hali ambayo hakuweza kuitegemea, akaanza kumsahau Andy. Andy akaanza kuanza kupiga hatua kutoka nje ya moyo wake huku George akianza kuingia ndani.
Baada ya mwezi moja akaanza masomo chuo kikuu huku akisomea sheria. Wazazi wake hawamkutaka kwenda kusoma mbali na Tanzania kwa kuhofia kwamba angeweza kumsahau George hali ambayo ingewasababisha kuanza upya kazi yao.
Mara kwa mara Annastazia alikuwa pamoja na George ambaye alikuwa akimng’ang’ania kama ruba, hakutaka kumpa nafasi ya kupumzika kwani alihofia kumpoteza kwa mmoja wa watoto wa Kitanzania waliokuwa wakiishi Dar es Salaam ambao walikuwa wakisifika kwa tabia za kuchukua wasichana wa watu bila kujali utajiri au elimu.
Kwa mara ya kwanza Annastazia akaruhusu kinywa chake kunyonyana na kinywa cha George. Hapo ndipo alipochanganyikiwa zaidi mpaka kufikia hatua ya kumsahau Andy huku akionekana kusahau kama alikwishawahi kukutana na mtu ambaye alikuwa na jina hilo katika dunia hii.
“Nataka kukuoa haraka iwezekanavyo” George alimwambia Annastazia.
“Hapana. Ni lazima nisome kwanza hata kabla ya harusi” Annastazia alimwambia.
“Kusoma si umekwishasoma mpenzi. Au unataka usome mpaka wapi?” George aliuliza.
“Nitakapoanza kuchukua degrii” Annastazia alijibu.
George hakuwa na jinsi, alichokifanya ni kuwa mvumilivu. Miezi ikakatika huku akionekana kuwa na kiu ya kutaka kumuoa Annastazia na hatimae kumuita mke wake halali wa ndoa. Mwaka wa kwanza ukakatika, mwaka wa pili nao ukakatika, bado George alikuwa na kiu kubwa ya kumuoa Annastazia.
Hatimae mwaka wa tatu ukatimia na kukatika, Annastazia hakuwa na jinsi, kama ambavyo alikuwa ameahidi na ndivyo ambavyo ilitakiwa kuwa. Wakawaambia wazazi wao juu ya hatua ambayo walikuwa wamefikia. Kila mmoja akaonekana kufurahishwa na hatua ile.
“Sisi kama wazazi tunawapa Abdul zote” Wazazi wa pande zote mbili walisema.
Harakati za harusi zikaanza kwa haraka sana. Magazeti yakaanza kuandika hatua kwa hatua jambo ambalo liliwafanya watanzania kuwa na hamu kubwa ya kutaka kuiona harusi hiyo ikifanyika. Fedha zilimwagwa na viongozi mbalimbali wa nchi hii huku harusi ikitarajiwa kuwa ya kifahari kuliko zote ambazo ziliwahi kufanyika katika ardhi ya Tanzania.
Annastazia akaonekana kupata jina kubwa nchini Tanzania mara baada ya kutangaza nia yake ya kuwania kiti cha ubunge wa Kinondoni. Kila mtu alionekana kumkubali Annastazia kutokana na kuwa na changamoto kubwa na elimu aliyokuwa nayo. Ukiachilia hayo yote, jina la baba yake lilikuwa likizidi kumbeba zaidi na kumuweka juu.
Kila kitu ambacho kilitakiwa kufanyika kilifanyika kwa haraka haraka. Mpaka mwezi unakatika kila kitu kilikuwa tayari. Tarehe ya harusi ikapangwa na wasimamizi wa harusi ile wakaandaliwa kabisa. Wapambaji wa ukumbi na wanaharusi walikuwa wameitwa kutoka nchini Afrika Kusini, hakukuwa na sababu ya kuwatumia wapambaji wa hapa na wakati kiasi kikubwa cha fedha kilikuwa kimeandaliwa.
“Siamini kama wiki ijayo tunakwenda kuwa mume na mke” George
 
SEHEMU YA 38

alimwambia Annastazia.
“Ninataka kuwa na familia yangu sasa” Annastazia alimwambia George.
Wiki moja ikaonekana kuwa kubwa kwa wachumba hao, kila mmoja alionekana kuwa na oresha ya kuona wanafunga ndoa na kuwa mume na mke. Walijua kwamba walikuwa wamepitia mambo mengi katika maisha yao ya nyuma lakini kwa wakati huo walitakiwa kusahau kila kitu.
Siku ambayo ilikuwa ikisubiriwa na Watanzania ikawaida. Watu zaidi ya elfu mbili walikuwa wamekusanyika ndani ya kanisa la Praise And Worship lililokuwa Mwenge jijini Dar es Salaam. Watu zaidi ya elfu saba walikuwa wamebaki nje huku wakifuatilia kile ambacho kilikuwa kinaendelea kupitia televisheni ambazo zlikuwa zimewekwa nje ya kanisa hilo.
Kama kawaida yao, waandishi wa habari hawakuwa nyuma, walikuwa wakiendelea kuchukua na kupiga picha kila tukio ambalo lilikuwa likiendelea mahali hapo. Kila mtu kanisani alionekana kuwa na furaha, kitendo cha kupata nafasi ya kuhudhuria harusi hiyo kilimpa furaha kila mmoja.
Bwana Kapama, Bwana Mtimbi na wake zao walikuwa katika viti vya mbele kabisa huku wakifuatilia kila kitu ambacho kilikuwa kikifanyika kanisani hapo. Viongozi mbalimbali walikuwa wamekusanyika kanisani hapo huku rais wa nchi akiwa mmojawapo. Harusi ilionekana kujaza viongozi wengi wa nchi.
Wanakwaya bado walikuwa wakiendelea kuimba huku wakivuta subira kuwasubiri maharusi. Zilipita dakika thelathini, vigele gele vikaanza kusikika kutoka nje ya kanisa. Hakukuwa na cha kujiuliza kwani kila mtu alijua fika kwamba maharusi walikuwa wamekwishafika mahali hapo.
Kwa haraka bila kupoteza muda, mchungaji Samuel akachukua kipaza sauti na kuwataa maharusi kuingia kanisani hapo. Muziki ukaanza kupigwa na maharusi kuanza kuingia huku wakisindikizwa na watoto waliokuwa na maua. Hatua zao zilikuwa za taratibu sana, flashi za kamera zilikuwa zikiendelea kuwamulika.
Nyuso zao zilikuwa zimetawaliwa na furaha, tukio ambalo lilikuwa linatokea kwa wakati huo lilionekana kuwa tukio moja kubwa na la kukumbukwa kutokea katika maisha yao. Walitumia dakika kadhaa mpaka kufika mbele ya kanisa lile.
Mchungaji akasimama mbele yao. Kitu cha kwanza alichokifanya kabla ya kufungisha ndoa ile ni kuanza kusoma Neno la Mungu. Wanaharusi walikuwa na hamu ya kufungishwa ndoa jambo ambalo waliona kama mchungaji akichelewa kuwafungisha ndoa.
Mchungaji alihubiri Neno la Mungu kuhusu ndoa, ni ndani ya dakika tano tu akawa amekwishamaliza na kutaka pete ziletwe mahali hapo. Mchungaji akazichukua zile pete na kuanza kuziangalia, aliporidhika, akakipeleka kipaza sauti karibu na kinywa chake.
“Kabla sijafungisha ndoa hii, kuna mtu mwenye kuweka kipingamizi ndoa hii isifungwe mchana wa leo?” Mchungaji aliuliza.
Kila mtu kanisani hapo akaanza kuangalia huku na kule kuona kama kulikuwa na mtu ambaye alikuwa amesimama. Kanisa zima lilikuwa kimya, hakukuwa na mtu ambaye alikuwa amesimama. Mchungaji akarudia kwa mara ya pili napo hakukuwa na mtu ambaye alisimama. Mchungaji akaona kutokutosha, akarudia kwa mara ya tatu.
Hakukuwa na mwanaharusi yeyote ambaye alionekana kuwa na wasiwasi mahali hapo ingawa macho yao yalikuwa yakiangalia kila upande huku nyuso zao zikiwa zimetawaliwa na tabasamu. Annastazia hakuonekana kuamini mara baada ya macho yake kutua usoni mwa mtu ambaye alikuwa akimfahamu vilivyo japokuwa alikuwa katikati ya umati wa watu huku akiwa amevaa miwani, alikuwa ANDY.

Andy hakutaka kupoteza muda, akaanza masomo katika chuo kikuu cha Oxford kilichokuwa nchini Uingereza huku akisomea udaktari juu ya viumbe
 
SEHEMU YA 39

hai wakiwemo binadamu na wanyama. Kila mwanachuo ambaye alikuwa akichukua masomo ambayo alikuwa akichukua alionekana kumuogopa Andy ambaye sifa zake zilikuwa zikivuma kwamba alikuwa hatari.
Kila siku alikuwa akiwasiliana na Annastazia huku akiendelea kumwambia ni kiasi gani alikuwa akimpenda na wala hakutaka uhusiano wao uishie hapo, alitaka awe nae katika maisha yake yote. Baada ya ukali wake darasani kukubalika na kila mwanachuo, wasichana wakaanza kumpenda Andy, wakaanza kujaribu bahati zao.
Msichana wa kwanza ambaye alikuwa akitamani sana kuwa pamoja na Andy alikuwa Marie. Kila siku Marie alikuwa akifanya vitu vingi kama kumpigia simu usiku, kumtumia meseji za mapenzi na hata kumpelekea zawadi za mapenzi lakini Andy hakuonekana kukubaliana nae kwani bado moyo wake ulikuwa ukimpenda sana Annastazia na kamwe hakutaka kumsaliti kama alivyomuahidi.
Marie hakukata tamaa, kila siku alikuwa akijaribu kumfuatailia Andy lakini juhudi zake zote zikagonga mwamba. Mpaka mwaka wa kwanza unaisha bado Marie alikuwa akiendelea kumfuatilia Andy ambaye alionekana kuwa mgumu kujiingiza katika mahusiano ya kimapenzi pamoja nae.
Hapo ndipo Andy alipoanza kuyaona mabadiliko makubwa katika mahusiano yake ya kimapenzi na Annastazia. Kuwasiliana kwa simu kukaanza kupungua na si kama zamani. Alijitahidi sana kumpigia simu lakini wala simu haikuwa ikipatikana.
Alichokifanya yeye ni kuanza kuwasiliana nae kwa kutumia mtandao wa Facebook. Aliwasiliana nae zaidi na zaidi, akakuta mawasiliano yakiwa yamekatika ghafla. Alichokifanya ni kuanza kulitafuta jina la Annastazia Kapama lakini wala hakupatikana hali iliyomaanisha kwamba alikuwa amekwishamblock katika mtandao huo.
Andy akaonekana kukasirika, hakuamini kile ambacho kilikuwa kimetokea, alichokifanya ni kuhamia katika mtandao wa Skype lakini napo huko hali ilikuwa ile ile, katika kila kona ambazo alikuwa akimtafuta Annastazia, hakumuona.
Picha zake alizokuwa nazo katika laptop yake ndio zilikuwa kumbukumbu ambazo alibaki nazo. Kila apokuwa akiziangalia picha zile usiku alijikuta akilia. Hakuamini kama angeweza kumpoteza Annastazia katika hali kama ile ambayo ilitokea.
Maisha yake akayaona yakibadilika, mbele yake akaanza kuona giza. Alitamani sana asafiri na kuelekea nchini Tanzania ambako huko angeweza kuonana na Annastazia na kuanza kuongea nae lakini jambo hilo likaonekana kuwa gumu sana kwake kutokana na masomo ambayo yalikuwa yakimtaka kutokupoteza muda.
Msichana wa pili ambaye alikuwa akimhitaji sana Andy chuoni pale alikuwa Patricia, msichana ambaye alikuwa miss wa vyuo vikuu nchini hapo. Andy bado aliendelea kuwa na msimamo ule ule, kamwe hakutaka kumkaribisha msichana yeyote moyoni mwake na wakati bado alikuwa na Annastazia.
Moyoni alijua fika kwamba bado Annastazia alikuwa kwake na kamwe hakutakiwa kumsaliti hata mara moja, kwake aliona lisingekuwa jambo jepesi lenye kuvumilika kama Annastazia angesikia kwamba amemsaliti.
Kila mwanachuo alimuona Andy kuwa mjinga, uzuri ambao alikuwa nao Patricia ilionekana kuwa ni zaidi ya uzuri, kila mvulana chuoni hapo alikuwa akimhitaji msichana huyo ambaye halikuwa hasikii chochote kwa Andy.
Kama kawaida yao wasichana, Patricia akaanza vituko, kila siku alikuwa akileta vituko vya mahaba kwa Andy lakini wala Andy hakuonekana kujali, kitu ambacho alikuwa akikijali ni masomo na uhusiano wake kwa Annastazia tu.
Uwezo wake mkubwa wa darasani na kufahamu mambo mengi ndio ambao uliwasababisha Waingereza kuanza kumwangalia kwa jicho la tatu. Wakaamua kumuajiri katika hospitali yao huku wakimlipa mshahara mkubwa sana.
Andy alionekana kuwa mtu wa ajabu katika kufahamu mambo mengi
 
SEHEMU YA 40

kuhusiana na mwili wa binadamu. Wagonjwa mbalimbali ambao walikuwa na magonjwa sugu walionekana kupata suruhisho hasa pale ambapo Andy alipoanzisha dawa yake aliyoiita Androone ambayo ilikuwa ikitibu magonjwa mengi katika mwili wa binadamu.
Dawa hiyo ikaanza kutangazwa katika kila kona duniani, watu wakaanza kuinunua kwa gharama kubwa ambapo Andy akaanza kuingiza kiasi kikubwa katika akaunti yake. Japokuwa Andy alikuwa ameanza kiutani lakini baadae akajikuta akianza kuingiza fedha nyingi sana.
Ni ndani ya miezi sita tayari alikuwa ameingiza zaidi ya paundi milioni mia tano. Maisha kwake yakaanza kubadilika, akaanza kujituma zaidi na zaidi kwani hakutaka kuridhika hata mara moja. Alijua fika kwamba alizaliwa katika ukoo uliokuwa na fedha lakini kamwe hakutaka kufikiria kuhusu fedha hizo, alihitaji kuwa na fedha zake mwenyewe.
Wamarekani wakaonekana kushtuka, kitendo cha Andy kuwa nchini Uingereza na wakati baba yake alikuwa Mmarekani kikaonekana kuwakasirisha, walichokifanya ni kuongea na Bwana Wayne ambaye akaongea na mtoto wake na kisha kurudi nchini Marekani.
Ugomvi ukaanza kutokota kati ya mataifa haya mawili, Uingereza ikaanza kuichukia Marekani kwa kuwa walikuwa wamepokonywa kitu ambacho kilikuwa na uhakika wa kuingiza kiasi kikubwa cha fedha nchini mwao. Andy akawa amerudi nchini Marekani na kuanza kufanya kazi katika hospitali ya Midtown Care ambao ilikuwa ikimlipa kiasi kikubwa cha mshahara mara tatu ya kile alichokuwa akilipwa nchini Uingereza.
“Kuna kazi tunataka kufanya” Mwanaume mmoja alimwambia Andy mara baada ya kuonana nae nyumbani kwake.
“Kazi gani?” Andy aliuliza huku akionekana kuwa na wasiwasi.
“Ninataka kuingiza fedha, kwa hiyo kuna kitu ninahitaji kukifanya” Mwanaume huyo, Dawson alimwambia Andy.
“Bado haujawa muwazi. Kitu gani?” Andy aliuliza.
“Nataka unitengenezee virusi fulani ambavyo vitakuwa vikiingia katika mwili wa mwanadamu kwa njia ya ngono. Tena viwe virusi hatari zaidi ya hivi vya UKIMWI” Dawson alisema.
“Mmmh!” Andy aliguna.
“Usijali. Nitakupa malipo mazuri sana” Dawason alimwambia Andy.
“Umenichanganya. Sasa faida yako hapo itapatikana vipi?” Andy aliuliza.
“Nataka pia unitengenezee dawa yake ya kuua virusi hivyo. Hiyo dawa niwe naimiliki mimi. Kwa kila mtu ambaye atakuwa akiingiwa na virusi hao, dawa nitakuwa nayo mimi, kwa hiyo mimi ndiye nitakayeingiza fedha” Dawson alimwambia Andy.
“Nipe muda nijifikirie” Andy alimwambia Dawson.
“Lakini itawezekana?”
“Asilimia mia moja” Andy alijibu na Dawson kuondoka.

****
Andy bado alikuwa akihitaji fedha za kutosha, japokuwa alikuwa akiingiza kiasi kikubwa cha fedha lakini hakuonekana kuridhika hali ambayo ilimfanya kukubali kuvitengeneza virusi ambvyo alikuwa akivihitaji Bwana Dawson.
Kwanza akalipwa nusu ya malipo na kisha kazi kuanza mara moja. Andy alichukua muda mrefu katika kutegeneza virusi ambavyo baadae vilitakiwa kusambazwa dunia nzima hata kabla ya dawa yake kutangazwa, hivyo ndivyo ilivyotakiwa na Bwana Dawson.
Andy akaanza kushinda katika maabara yake iliyokuwa ndani nyumba yake, masaa yote alikuwa bize akitengeneza virusi hivyo ambavyo vilitakiwa kusambazwa kwa njia ya ngono. Kazi haikuwa ndogo hata mara moja, kila virusi ambavyo alikuwa akivitengeneza vilionekana kuwa si imara, hivyo vilikufa mapema.
Andy akaona kazi kubwa kubwa sana jambo ambalo lilimhitaji kuwa na utulivu zaidi. Wakati mwingine alikuwa akikataa kula mpaka pale ambapo kila kitu kitakapokamilika lakini mwisho wa siku alijikuta akila kutokana na kutumia masaa mengi sana bila mafanikio yoyote yale.
 
SEHEMU YA 41

Andy alitamani kuomba ushauri kutoka kwa madaktari wengine lakini jambo hilo lilionekana kuwa gumu kutokana na usiri mkubwa uliokuwepo katika kutengeneza virusi vile. Andy alishinda maabara huku wakati mwingine hata akikatisha kazi zake za kuelekea kazini.
Fedha ambazo alikuwa ameahidiwa kilikuwa kiasi kikubwa cha fedha, alijua fika kwamba alikuwa akienda kuiteketeza dunia lakini kwake hakuonekana kujutia jambo lolote lile, kiasi cha fedha ndicho ambacho kilikuwa kikihitajika kuongeza fedha katika akaunti yake.
Bado kazi ile ilionekana kuwa ngumu kupita kawaida lakini bado alikuwa akiendelea kukomaa kila siku. Kuanzia saa mbili usiku mpaka saa tano usiku ndio ulikuwa muda wake wa mapumziko ambao alikuwa akiutumia katika kupekuapekua mambo mbalimbali katika kompyuta yake.
Andy alitumia kipindi cha wiki tatu na nusu na ndipo alipofanikiwa kuvitengeneza virusi hivyo ambavyo vilionekana kuwa na nguvu kubwa kuliko hata virusi vya UKIMWI. Virusi hivi ambavyo alikuwa amevitengeneza vilionekana kumshangaza hata yeye mwenyewe kwa jinsi vilivyokuwa, vilikuwa vimeambatana ambatana hali iliyomfanya kuvipa jina la Katerpilar.
Furaha ikaonekana kurudi kwa Andy, kidogo akaanza kujisikia amani moyoni mwake, kitendo cha kutengeneza virusi vile kilionekana kuwa kitendo ambacho kilimpa mafanikio makubwa katika kazi yake. Alishinda ndani akila na kunywa huku virusi vile akivihifadhi vizuri hata kabla hajamkabidhi Bwana Dawson kazi yake.
Siku hiyo alishinda akipekua pekua mambo mbalimbali katika mtandao wa Internet. Hapo ndipo alipofikiria kuanza kumtafuta Annastazia katika sehemu mbalimbali hasa katika mitandao ya nchini Tanzania. Hakuwa na uhakika kama angeweza kumuona au kusoma tetesi zozote kuhusiana na msichana huyo ila kitu ambacho alikitaka kukifanya na kuridhika nacho ni kumtafuta tu.
Katika kila website ambayo alikuwa akifungua, hakweza kumuona Annastazia kabisa jambo ambalo lilimfanya kukata tamaa. Hakujua ni kwa jinsi gani angemuona msichana huyo na kumwambia kuhusiana na jinsi alivyokuwa akimhitaji katika maisha yake.
Katika kupekua pekua ndipo alipokutana na tangazo kubwa ambalo lilikuwa likihusu harusi kubwa ya watoto wa Mawaziri ambayo ilitakiwa kufanyika nchini Tanzania. Ingawa alionekana tangazo hilo kutokumhusu lakini akaonekana kuvutiwa nalo hali iliyomfanya kuanza kulisoma.
Andy akaonekana kushtuka kupita kawaida mara baada ya macho yake kutua katika jina ambalo alikuwa akilifahamu vizuri kabisa, lilikuwa jina la ANNASTAZIA KAPAMA. Andy hakutaka kuishia hapo, tayari akaonekana kuwa na mashaka na jina lile hali iliyomfanya kuanza kulibofya jina lile na picha ya Annastazia kutokea.
Andy akaonekana kushtuka, moyo ukaonekana kumuuma kupita kawaida. Alilirudia tangazo lile mara mbili mbili huku akionekana kutokuyaamini macho yake. Hakuamini kama Annstazia ambaye alikuwa akimpenda kwa moyo wake wote alikuwa ameamua kufunga ndoa na mwanaume mwingine na kumuacha peke yake.
Andy akajikuta akiifunika laptop yake na kisha kuinamisha kichwa chini. Mawazo juu ya Annastazia yakaanza kujirudia kichwani mwake, akaanza kukumbuka mambo mengi ambayo alikuwa amefanya na Annastazia toka siku ya kwanza ambayo alikutana nae shuleni mpaka siku ya mwisho kuachana nae, hakuonekana kuamini kama Annastazia alikuwa amemsaliti na kuamua kwenda kwa mwanaume mwingine.
Andy akajikuta akianza kutokwa na machozi, na baada ya sekunde kadhaa akaanza kulia kwa sauti kama mtoto mdogo. Alijuta kwa nini aliamua kuingia katika mahusiano na msichana yule ambaye alimuonyeshea mapenzi na baadae kumletea maumivu makali. Andy hakutaka kukubali, hakutaka kuona
 
SEHEMU YA 42

harusi ikifungwa na yeye kuwa nchini Marekani, alichokifanya ni kusafiri kuelekea nchini Tanzania.
Ndege ilipotua katika uwanja wa Mwl Julius Kambarage Nyerere, akachukua teksi ambayo ilimpeleka mpaka katika hoteli ya kimataifa ya Serena. Alichukua chumba kimoja na kutulia ndani. Kutokana na harusi ile kuwa kubwa na ya kifahari, ilikuwa ikitangazwa mara kwa mara katika vyombo vya habari ambapo kila wakati Andy alipokuwa akiziona taarifa zile alikuwa akilia kama mtoto.
Maisha yake akayaona yakianza kubadilika, ‘Mauaji’ ndio neno ambalo lilikuwa limeanza kumtawala moyoni mwake, isingewezekana hata mara moja kumuacha msichana yule hai na wakati alikuwa amemuumiza kupita kawaida. Alichotaka kukifanya kwa wakati huo ni kushiriki katika harusi hiyo kwa kuamini kwamba angeweza kumuona Annastazia japo kwa mara moja.
Siku zikakatika na hatimae siku ile kufika. Andy akachukua teksi na kisha kuanza kuelekea katika kanisa lile. Uwepo wa watu wengi ulionekana kumuumiza kwa kuona kwamba kama angekuwa yeye basi watu wangekuwa wengi zaidi ya wale ambao walikuwa wamekusanyika kanisani mule.
Alichokifanya ni kutafuta kiti kimoja kilichokuwa katikati ya viti vingine na kutulia. Muda ulizidi kwenda mbele mpaka katika wakati ambao maharusi wakaanza kuingia ndani ya kanisa lile. Andy akayapeleka macho yake kwa maharusi wale, hasira zikamkaba zaidi mara baada ya kumuona Annastazia akiwa ndani ya shela huku George akiwa pembeni yake.
Andy akainamisha kichwa chake chini na machozi kuanza kumtoka tena, hakuamini kama kweli katika maisha yake alikuwa amesalitiwa. Hakuamini hata kidogo kama Annastazia alikuwa ameamua kumuacha na kumchukua mwanaume mwingine.
Andy akaanza kulia kwa sauti ya chini, moyo wake ulikuwa katika maumivu makali kupita kawaida. Kumuona Annastazia akiolewa na mwanaume mwingine kulimuumiza kupita kawaida. Maharusi wakafika mbele na mchungaji kuanza kuhubiri.
Muda wote Andy alikuwa akimwangalia Annastazia huku akilia, hakuamini kile ambacho alikuwa akikiona mbele yake. Akajiona kutokuwa na kosa lolote kama itatokea siku akimuua Annastazia ambaye alikuwa ameuumiza moyo wake kupita kawaida.
“Kabla sijafungisha ndoa hii, kuna mtu mwenye kuweka kipingamizi ndoa hii isifungwe mchana wa leo?” Mchungaji aliuliza.
Kila mtu kanisani hapo akaanza kuangalia huku na kule kuona kama kulikuwa na mtu ambaye alikuwa amesimama. Kanisa zima lilikuwa kimya, hakukuwa na mtu ambaye alikuwa amesimama. Mchungaji akarudia kwa mara ya pili napo hakukuwa na mtu ambaye alisimama. Mchungaji akaona kutokutosha, akarudia kwa mara ya tatu.
Andy hakutaka kusimama, aliendelea kubaki pale kitini huku akiendelea kumwangaia Annastazia ambaye alikuwa akiangalia huku na kule. Macho yake yakagongana na Annastazia ambaye wasiwasi ukaongezeka zaidi. Mara baada ya mchungaji kuona kwamba hakukuwa na mtu yeyote mwenye kipingamizi, akaifungisha ndoa ile.
Annastazia akajikuta akipoteza furaha yote ambayo alikuwa nayo, kitendo cha Andy kuwa ndani ya kanisa lile akiangalia harusi ile hata yeye kilionekana kumuumiza na kumkumbusha mbali sana. Annastazia alitamani kumfuata Andy na kumuelezea hali ambayo alikutana nayo Tanzania aliporudi lakini hakuwa na nafasi ile tena.
Andy akasimama na kuanza kuondoka. Mikono yake alikuwa amekunja ngumi kwa hasira. Moyo wake ulikuwa na maumivu makali ambayo aliamini kwamba hakuweza kuyapata kabla. Alimchukia Annastazia kuliko wanadamu yeyote katika dunia hii, alikuwa tayari kumuua muda wowote ule.
Akaingia katika teksi ambayo alikuja nayo na kisha kuanza kupelekwa
 
SEHEMU YA 43

hotelini. Muda wote alikuwa katika hasira kali, alionekana kuvimba kupita kawaida. Mauaji ndiyo ambayo alikuwa akitaka kuyafanya kwa wakati huo. Alipofika hotelini akaingia chumbani na kutulia kitandani.
Bado moyo wake ulikuwa katika maumivu makali, akasimama na kuanza kutembea tembea huku na kule huku akikipiga ngumi kiganja chake kila wakati. Muda wote huo, machozi yalikuwa yakimtoka na baada ya muda kuanza kulia kama mtoto mdogo.
Kifo ndicho kitu ambacho kilistahili kumkuta Annastazia, alipanga kumuua katika kifo cha aina yake kwa kutumia mikonoyake mwenyewe, hakuona sababu ya kumuacha msichana huyo hai, alitaka kumuua kwa gharama yoyote ile.
“Nitakuua...nitakuua...NI LAZIMA NITAKUUA ANASTAZIA....” Andy alisema huku akiendelea kulia kwa maumivu makali moyoni mwake.

Je nini kitaendelea?
Je Andy ataweza kumuua Annastazia kama alivyojiapiza?
Je Andy ataweza kutengeneza virusi hao kwa lengo la kuiteketeza dunia?
 
SEHEMU YA 44

Bwana Wayne alikuwa ametulia kwenye kiti cha baiskeli yake huku macho yake yakiangalia televisheni. Pembeni alikuwepo mkewe, Bi Happy ambaye alikuwa amekilaza kichwa chake kochini. Katika kipindi chote ambacho walikuwa pamoja, maisha yao yalikuwa na furaha japokuwa Bwana Wayne hakuwa na uwezo wowote kitandani.
Uwepo wa mtoto wao, Andy ulikuwa ukiwapa furaha kila siku, mafanikio ya Andy yalikuwa yakimfurahisha kila mmoja. Walijivunia kuwa na mtoto kama Andy ambaye kadri siku zilivyokuwa zikizidi kwenda mbele alikuwa akizidi kusikika katika mafanikio ya watu na kuwa faraja katika mioyo ya wagonjwa.
Bwana Wayne akaonekana kushtuka, akajiweka vizuri na kuikazia macho televisheni. Mkewe, Bi Happy akaonekana kushtuka pia, akakiinua kichwa chake na kuanza kumwangalia mumewe usoni. Alipomuona anaiangalia televisheni ile na yeye akayapeleka macho yake katika kioo cha televisheni ile.
Tangazo la ibada kubwa ya kipekee lilikuwa likionekana katika televisheni ile. Bwana Wayne bado alikuwa akiendelea kuliangalia tangazo lile huku akiyasikiliza maneno ambayo yalikuwa yakitangazwa. Wenye shida na matatizo mbalimbali walitakiwa kuwepo katika ibada hiyo ambayo hufanyika kila Jumapili katika kanisa la Salvation from Christ lililokuwa hapo hapo jijini New York huku mchungaji Gibson Gabriel akitarajia kufanya maombezi siku hiyo.
“Ni lazima twende huko mke wangu” Bwana Wayne alimwambia mkewe, Bi Happy.
“Kwenye hiyo ibada?”
“Ndio. Ninaamini kwamba ugonjwa wangu utaponywa tu” Bwana Wayne alisema.
Moyoni mwake alikuwa na imani asilimia mia moja kwamba ni lazima ugonjwa wake ule ungekwenda kuponywa kama tu angekwenda kufanyia maombezi katika ibada hiyo. Kuanzia hapo siku ya Jumapili akaanza kuiona iko mbali.
Kiu kubwa ya kutaka kushiriki katika ibada hiyo ya maombezi ilikuwa imemkaba kooni, alitamani siku hiyo iwe siku ya maombezi ili aweze kwenda katika maombezi hayo ili nae apate uponyaji ambao angekwenda kuukumbuka katika maisha yake yote.
Ni kweli kwamba ilikuwa imepita miaka ishirini na tano wala hakuwahi kuingia kanisani lakini kwa kipindi hicho wala hakuwa na ujanja wowote ule ilimbidi kuingia kanisani kwani uponyaji ndicho kitu ambacho alikuwa akikihitaji sana.
Siku zikakatika mpaka kufikia siku ambayo alikuwa akiihitaji sana. Asubuhi na mapema akaanza kujiandaa na mkewe, Bi Happy na kisha kuanza kuelekea katika kanisa hilo. Bado imani kubwa ilikuwa moyoni mwake kwamba kama angefanyiwa maombezi basi alikuwa akienda kupokea uponyaji mkubwa maishani mwake.
 
Back
Top Bottom