Simulizi ya Kijasusi: Kiguu Na Njia

Simulizi ya Kijasusi: Kiguu Na Njia

SEHEMU YA 111

kuona dalili za udenda zikielekea kudondoka toka mdomoni mwake. Sikuwa na hakika kama niliona vizuri.
“Itabidi tuzungumze kama wanaume baadaye,” aliniambia. “Unatarajia kuondoka lini?”
“Sina haraka,” nilimjibu. “Nitapenda kufika Arusha pia
kabla ya kurejea maporini,” niliongeza.
“Nitakupeleka.” Alidakia. “Mimi ni mwenyeji Arusha kuliko hapa Moshi. Hutohitaji kulala au kula hotelini.”
Mchaga aliangua kicheko cha dhihaka, kicheko kilichofuatiwa na “Ndugu yangu umekwisha. Mpare ajitolee kukupeleka Arusha, akupe malazi na chakula! Kuna jambo hapo,” alisema.
“Atakwisha yeye,” nilijibu, “Maana siye Wamanyema tuna historia ya kula watu. Nitamla mzimamzima kabla yeye hajanila,” kauli ambayo iliniangusha kicheko kirefu.
“Lakini Wapare unawajua vizuri? Wana maradhi yasiyo na dawa ya uchoyo. Wewe na yeye mtakufa njaa hata kabla hujafikiria kumla, huku mkiwa na fedha mfukoni,” aliongeza na hivyo kuongeza kicheko. Sikujua mengi juu ya Wapare zaidi ya ukweli kuwa ni kabila jingine kubwa la Kilimanjaro, wanaishi katika miteremko ya milima ambayo ni sehemu ya mlima Kilimanjaro, na kwamba wao pia wamegawanyika katika sehemu kuu mbili, Wapare wanaozungumza Kingweno, wanaoishi kaskazini na Wachasu waishio Usangi, Kusini. Lugha zao zina aina fulani ya kulandana na zile za Wataveta na Asu wa Kenya.
Enzi za kale Wapare walisifika kwa uganga wa mvua na uhunzi. Uhakika kuwa kabila hili ni la kale ni pale nilipowahi kuona kitabu kitakatifu cha Biblia iliyoandikwa kwa lugha ya Kipare, kilichochapishwa mwaka 1910. Pamoja na ujio huo



wa dini za kisasa Wapare waliendelea na tiba mbalimbali za asili kama maziwa ya Konda badala ya mama kumtibu mtoto mwenye wintu, maradhi ya sangasi yaliyoharibu vinywa vya watoto, majani yaliyoitwa more yaliyotibu ‘Kirumu,’ ‘kiruti’ au ‘kinyoka’, maradhi ya macho kwa watoto wadogo.
Historia ya dini za kigeni Upareni inaanza na mmisheni Jakob Janssen Dannholz, Mjerumani wa madhehebu ya kiluteri ambaye mwaka 1908 alianzisha ‘kazi ya bwana’ huko Mbaga, Upare ya kusini. Aliishi hapo hadi mwaka 1907 alipokamatwa na kuchukuliwa na Waingereza kama mfungwa wa kivita hadi katika kambi yao ya Misri ambako alifariki mwaka mmoja baadaye. Alifariki na umri wa miaka arobaini lakini kazi aliyoianzisha iliishi, ikakua na inaendelea kukua hadi leo.
Kinyume na makabila mengi nchini, wanawake wa Kipare walikuwa mstari wa mbele, pengine kuliko wanaume zao, katika harakati za kupigania uhuru na haki zao. Kumbukumbu zangu toka vitabuni zilinikumbusha mwaka 1946, kule Usangi, pale maelfu ya akina mama walipoibuka na kuanzisha vurumai kubwa wakipinga kulipa kodi. Tukio hilo liliibuka pale Chifu mmoja alipotembelewa na mkuu wa wilaya kwa ajili ya majadiliano. Umati wa wanawake wapatao mia tano waliizingira nyumba hiyo kutaka ufafanuzi juu ya utaratibu wa kodi ambao hawakuafikiana nao. Mkuu huyo alipojaribu kuondoka bila kuwapa ufafanuzi walipandwa na hasira, walianzisha nyimbo huku wengine wakiipiga mawe nyumba hiyo ya Chifu. Tukio hilo lilifuatiwa na maelfu ya wanawake kujiunga katika vuguvugu hilo ambalo lilitikisa serikali ya mkoloni.
Kama Wachaga, Wapare pia walikuwa katika mstari wa





mbele katika kuiunga mkono TAA na baadaye TANU katika mapambano ya kudai kujitawala. Hali hiyo inachukuliwa kuwa ilisaidia kuondoka wazo la kuibuka kwa chama cha kikabila ambacho kingeweza kuwa chini ya ‘PARE UNISI’ ambayo ilikuwa na nguvu nyingi kutokana na mchango wa kiuchumi iliyotokana na kilimo cha mibuni, katani na chai.

“Unasemaje?”

Mpare alinizindua. Nikamtazama.

“Naona uko mbali sana,” aliongeza. “Nilikuuliza unadhani tuondoke lini kwenda Arusha?”

“Nilikuambia sina haraka, kwani hatuonani tena baada ya leo?” nikamuuliza.

“Tutaonana. Bila shaka yoyote.”

Mara akina mama walikwenda stendi kumpokea mwalimu wakaanza kurudi, mmoja baada ya mwingine. Hawakuwa na furaha kama ile waliyoonyesha wakati wakinipokea mimi. Hatukuchelewa kuelewa sababu.

Mwalimu Nyerere hakutokea.

Mchaga aliyekuwa kimya muda mwingi, akishughulikia kinywaji chake alitabasamu kidogo akinitazama. Kisha akasema, “Maadam Nyerere hakuja, na wewe umefanana naye, tutaendelea kukuita Nyerere. Unasemaje?”

Sikumbuki kama nilimjibu.
 
SEHEMU YA 112










SURA YA KUMI NANE

Za Moshi

oshi na Arusha ni miji jirani sana, ikiwa imetenganishwa kwa umbali wa kilometa 75 tu na hivyo kufanya safari toka mji huu hadi
ule iwe takriban dakika sitini kwa gari lisilo na matatizo.
Safari ya Arusha na Moshi ni burudani tupu. Japo barabara haikuwa nzuri sana, lakini kule kupita katikati ya mashamba makubwa ya mibuni na migomba, vijiji vichache vikichomoza hapa na pale ilikuwa burudani ya macho. Ilikuwa alfajiri moja tulivu na angavu sana. Anga lilitakata pasi ya wingu lolote. Jua lililokuwa likichomoza Mashariki liliufanya mlima Kilimanjaro ambao tuliupa kisogo usimame pale, taji lake jeupe kichwani, juu ya kiwiliwili chake cha kijani, ukiwa umetuinamia kama mzimu au malaika aliyekuwa akitutakia heri katika safari yetu. Sikuchoka kugeuka mara kwa mara kuutazama uzuri huo wa pekee.
Hata kabla Kilimanjaro haujatokomea nyuma yetu, ulijitokeza mlima mwingine mbele yetu. Kama Kilimanjaro, ulisimama kando ya mji wa Arusha, kwa maringo na utukufu wa aina yake. Japo mbele ya Kilimanjaro mlima huu ulikuwa kama mtu na mdogo wake, bado utukufu wake ulikuwa palepale. Sikuhitaji kuambiwa kuwa huu ulikuwa mlima



Meru, fahari nyingine ya Tanzania. Ukiwa umepanda juu ya usawa wa bahari kwa mita 4565 mlima huu ulimwaga hewa safi yenye ubaridi mwanana uliopenya katika miili ya wakazi wa Arusha na vitongoji vyake hadi kuitikisa mifupa ya wageni wa mandhari hiyo.
“Naona tayari umeanza kumsahau mrembo mmoja umeanza kumtamani mrembo mwingine. Vipi, unafikiria kumpanda?”
Nikazinduka na kumtazama msemaji. Alikuwa rafiki yangu mpya, yule Mpare, ambaye toka tukio lile la mimi kufananishwa na Nyerere na kumsimulia kwa ufupi maisha yangu ya maporini aliniganda kama kupe. Siku zote tatu nilizokaa mjini Moshi alikuwa nami kama kuku na vifaranga vyake. Sikupata kujiuliza nani alikuwa kuku nani kifaranga kati yetu. Lakini ile tabia yake ya kuwa nami bega kwa bega, tukiachana wakati wa kulala, nikiamka tayari ananisubiri, nilianza kupata hisia pamoja na yeye kujifanya kuku ilielekea kuwa yeye ni kifaranga asiyetaka kumpoteza mama yake.
“Mrembo gani?.... Kumpanda nani?” nilimuuliza kwa mshangao.
“Mrembo Kilimanjaro, dada mtu. Mara tu ulipomwona mdogo wake, Meru, tayari umehamishia mapenzi yako kwake. Hilo liko wazi katika macho yako. Ukipenda tunaweza kufanya mipango tuupande. Sio mrefu kama Kilimanjaro,” alijibu.
Niliyatafakari maneno yake kwa muda. “Kama ningepata fursa hiyo ningeitumia kupanda mama wa milima yote Afrika, mwenye sifa zote za pekee duniani, Kilimanjaro; ili nipate kitu cha kuwasimulia wajukuu zangu pale nitakapozeeka,” nilimweleza.
“Wajukuu! Uliniambia hujaoa.”





“Iko siku nitaoa. Nitapata watoto na baadaye wajukuu,” nilimjibu, jibu ambalo lilifanya mada hiyo iishie hapo.



* * *​

Arusha ilinisisimua kwa mengi. Mji mdogo ndiyo, lakini ulikuwa na pilikapilika nyingi, wageni wengi. Ukiwa mji wa mpakani, ukiwa umetenganishwa na Nairobi kwa kijiji mashuhuri cha Namanga. Wageni wengi walioitembelea Arusha walikuwa wafanyabiashara, watalii na wataalamu mbalimbali wakiwa katika pilikapilika hii na ile. Wahindi wachache walikuwa na biashara zao lakini sehemu kubwa ya biashara ilishikwa na wenyeji, Wachaga, Wapare na Waarusha wachache.

Wamasai walinisisimua pia. Ingawa kiasili wao ndio wenyeji hasa wa mji huu lakini kama wanavyoishi mbungani ndivyo walivyokuwa wakiishi hapa. Siku zote walionekana wageni wa mji, wakifanya kazi yao nje kabisa ya mji ambako wao na ng’ombe wao walijiona huru zaidi. Hata ujio wao mjini kwa mahitaji muhimu kama chumvi na vipande vya nguo walivyozowea kuvaa, bado vaa yao, upande mmoja wa mwili ukiwa wazi, sime kiunoni kana kwamba muda wote wako vitani huku kiswalhili na lugha nyingine zinazotumiwa na wengi kikiwapiga chenga. Kuwepo kwao mjini kulifanya waonekane kama watu waliopotea njia.

Mpare, wakati fulani aliponiona ninavyowashangaa, alinisimulia kisa kimoja cha kuchekesha juu ya Wamasai. Kwamba katika jitihada za kuwalazimisha kuvaa nguo za kisasa serikali ilipata kutoa amri ya wauzaji wote wa maduka kutomuuzia kitu Mmasai ambaye hakuvaa ama suruali ama kaptula ndani ya shuka lake.
 
SEHEMU YA 113

Hatua hiyo iliwaudhi sana Wamasai. Hata hivyo, ili wapate huduma hizo kijiji kilibuni mbinu ya kununua kaptula moja ambayo kila aliyekuwa na shida mjini aliiazima. Kwa aibu, kaptula hiyo ilivaliwa nje kabisa ya kijiji. Na baada ya manunuzi anaporejea nyumbani Mmasai aliivua kaptula hiyo nje ya kijiji kabla ya kuirejesha.
Sikushangazwa kabisa na habari hiyo, kwa jinsi nilivyowafahamu Wamasai.
Kama ilivyokuwa Moshi, Mpare hakuwa Mpare wa kawaida Arusha vilevile. Hatukulala hotelini. Alinipeleka kwa ndugu zake, maeneo ya Kaloleni ambako alinitambulisha kama rafiki yake ‘mpenzi.’
Alinitembeza maeneo mbalimbali ya mji, Oljoro, Kijenge, Mianzini na kwingineko. Alinifikisha hadi Namanga, Mpakani, ambako alijaribu kuomba ili turuhusiwe kuvuka mpaka na kuikanyaga ardhi ya Kenya walau kwa dakika kumi, tukakataliwa. Wakati tukirejea, kwa hasira zake za kukataliwa kuvuka mpaka aliamua kubadili uelekeo wa safari yetu. “Twende zetu Ngurdoto, tuburudishe macho yetu,” alisema.
sana katika mbuga, misitu mito na ziwani. Nimeona wanyama na ndege wengi sana. Lakini sikupata kuona wanyama wa kuvutia kama tumbili weupe, lino wekundu, mbega na ndege wengi kama niliowaona Ngurdoto. Niliwaona kereng’ende, kibeti, aina mbalimbali za vibisi, kicheleko na wengine wengi ambao waliifanya Ngurdoto kuwa mahala pa kusisimua.
Mandhari ya eneo hilo pia ni kitu kingine cha kuvutia. Ikiwa karibu kabisa na mji wa Arusha, katikati ya milima mikubwa maarufu ya Kilimanjaro na Meru Ngurdoto ilikuwa zawadi nyingine ya asili kwa nchi na vizazi vyake.



Tulirejea mjini jioni sana. Kwa ushauri wake tulikula chakula cha usiku hotelini. Tukashushia kwa vinywaji. Yeye bia za moto, mie fanta mbili za baridi. Kama ilivyokuwa katika mambo mengine, alisisitiza kulipia vinywaji na chakula hicho peke yake. Nikakataa katakata na kulipia. Kisha nilimwambia, “Nadhani umefika muda wa kuzungumza ana kwa ana kama wanaume wawili. Umekuwa mwema kwangu kwa muda mrefu. Umelazimisha urafiki na udugu hadi nikaukubali. Niambie, unahitaji nini sasa kutoka kwangu?”
Mpare alitazama huko na huko kuona kama tulikuwa katika faragha. Hakuridhika. Akanishauri tuhamie katika kona ya baa hiyo iliyokuwa na meza mbili tatu zisizo na watu. Tukahama. “Nataka tuwe marafiki,” alisema baada ya kuketi.
“Nadhani tumeshakuwa.” “Nataka tuwe ndugu,” aliongeza.
“Nadhani tumeshakuwa,” nilimjibu tena.
Alisita kwa muda kabla hajasema, “Nataka tuwe wasiri. Kwa mwanamume udugu na urafiki havitoshi. Tuwe kitu kimoja. Langu liwe lako, lako liwe langu. Tuafikiane hilo kwanza, kisha tuchukue hatua ya pili.”
Nilimtazama kwa mshangao uliochanganyika na mashaka. Alikuwa akizungumza kwa makini na msisitizo kuliko ilivyokuwa kawaida yake.
“Hatua ya pili ni ipi?” Nilimuuliza.
“Nataka tutafute pesa. Nataka tuwe matajiri. Mimi nawewe,” alijibu mara moja.
“Kwani hatutafuti?” Nilimuuliza.
Swali hilo lilimfanya aangue kicheko. “Tunatafuta ndiyo. Lakini tunazotafuta ni fedha za kula tu, fedha za kubadili mboga na mashati. Mwanamume anahitaji fedha zilizotakata.



Unaona maghorofa yake yanayopanda?” aliuliza akinielekeza nje ya dirisha ambako jengo la ghorofa nne lilikuwa likijengwa. “Lile linajengwa na binadamu kama mimi na wewe.​
Nataka miaka miwili ijayo tuwe na majengo kama yale. Tuwe na magari ya maana. Tuweze hata kununua ndege.”
Nikacheka.
“Usicheke. Hii sio ndoto. Nyota yangu na yako zinafanana. Naona waziwazi mimi na wewe tukiogelea katika bahari ya pesa. Tunajenga… tunalimisha mashamba makubwa… tunakwenda kutembea Ulaya…”
Alizungumza huku akitazama angani, macho kayakodoa kama anayekiona hicho anachozungumza. Nilitamani kucheka tena, lakini kitu fuani kilinizuia. Kitu ambacho sikuweza kukipambanua kati ya hofu na mashaka juu ya rafiki yangu huyo.
“Nitakusimulia hadithi moja,” alisema ghafla. “Sio hadithi ya kupendeza sana, lakini itakufanya uelewe kwa nini nahitaji fedha za maana. Yuko bwana mmoja,” alianza hadithi yake. “Alizaliwa katika familia moja masikini sana. Kwa bahati mbaya sana, familia hiyo ilizungukwa na familia yenye kipato kikubwa, familia ambazo zilisomesha watoto wao nje ya nchi, zilijenga nyumba za maana na kushindana katika kubadili magari na mavazi. Masikini na huyu na ndugu zake wote waliishia kuajiriwa katika mashamba ya majirani hao ambao waliwanyanyasa na hata kuwapiga makofi hadharani. Hali hiyo ilimfanya jamaa huyu asononeke na kukosa raha.”
“Siku moja bwana huyu masikini alikuta baba yake akiwa amepiga magoti mbele ya mtoto wa tajiri yao mmoja, huku akisihi na kubembeleza. Kisa? Masikini baba yake alikuwa amefukuzwa kazi kwa kushindwa kufika kazini
 
SEHEMU YA 114

jana yake kutokana na maumivu ya mgongo. Baba alikuwa akijaribu kumsihi mtoto huyo wa tajiri abadili uamuzi wake na kumruhusu kuendelea na kazi ya shamba. Kijana huyo hakukubali, badala yake alimtukana kwa kila neno chafu alilolifahamu hata masikini mzee akawa akitokwa na machozi.” “Ilikuwa picha ya kusikitisha sana kwa yule kijana.​
Alimfuata baba yake na kumwinua huku akimwambia, “Kufukuzwa kazi sio mwisho wa dunia. Nenda nyumbani kapumzike,” kauli ambayo yule mtoto wa tajiri aliisikia.
Akageuka na kumwambia, “Na wewe pia umefukuzwa kazi. Toka leo msikanyage katika mashamba yetu.”
“Masikini kijana yule maisha yakawa magumu sana. Alikuwa ndio kwanza ameoa na kupata watoto wawili mapacha. Alishindwa kuwalisha. Watoto wakapata utapiamlo na kufa mmoja baada ya mwingine. Mama wa watoto alishindwa kuvumilia. Alilia kwa wiki mbili. Asubuhi moja ya wiki ya tatu mama huyo alikutwa akining’inia kwenye paa la nyumba yao. Alijinyonga kwa kamba ya katani.”
“Uchungu, aibu na hasira vilimfanya baba huyo aondoke nyumbani na kwenda mjini kutafuta kazi. Hakuwa na elimu ya kutosha, hakuwa na ndugu mwenye madaraka, hivyo suala la kazi likawa ndoto. Masikini aliishia kuambulia vibarua vya hapa na pale, ambavyo havikumsaidia sana. Wakati akihangaika huko mjini alipokea habari mbaya moja baada ya nyingine. Mama yake alikuwa amefariki kwa malaria. Hakwenda, kwa aibu ya kwenda mikono mitupu. Baba yake naye akafa. Hakwenda, kwa sababu zilezile. Familia yao sasa ilibakiwa na watu watatu tu, bibi mzaa baba, kikongwe ambaye kila usiku ulipoingia waliamini kuwa kesho asingeamka kutokana na malalamiko ya maumivu ya miguu na mgongo



yaliyokuwa yakimsumbua. Wengine walikuwa wadogo zake wawili, msichana aliyekuwa kiwete na mvulana ambaye ndiye aliyekuwa akichangia kuleta walao vibaba vya unga vilivyowawezesha kuvuta siku.”
“Yule bwana, masikini, hadi leo anahangaika mijini akijaribu kushika ama hiki ama kile bila mafanikio,” alimaliza hadithi yake na kunikazia macho.
“Hii ni hadithi ya kweli,” baadaye alisema. “Na wahusika wake ni wa kweli. Mhusika mkuu ni mmi.”
“Wewe?” Niliuliza kwa mshangao.
“Naam, mimi mwenyewe. Na, kwa kweli, hicho ulichokisikia ni moja ya kumi tu ya mateso na aibu zitokanazo na umasikini ambazo nimepata kukutana nayo. Kinachoitesa roho yangu sana ni huyo bibi na wajukuu zake ambao wanaishi kwa kudra ya mwenyezi mungu. Tatizo lolote linalohusiana na pesa linaweza kumfanya yeyote kati yao au wote wapoteze maisha kama mende au kunguni mikononi mwa binadamu.”
Sikupata kujua kama nilikuwa na huruma. Lakini nilipohisi machozi yakinilengalenga kwa simulizi hiyo nilijua kuwa nimeshikwa na huruma. Akili ikahama na kunifanya niifikirie familia yangu huko Buha. Pengine ina hali kama hiyo. Pengine haipo tena, wote wamekufa kwa shida hii au ile! Chozi moja liliteleza ghafla na kulifikia shavu langu. Nililifuta mara moja kwa kiwiko cha mkono na kisha kutoa leso yangu ambayo haikutoka mkononi mwangu kwa muda mrefu.
Tulipigwa na kimya cha muda mrefu, kimya ambacho Mpare alikiondoa pale aliposema baadaye, “Ninaposema nimejaribu kila kitu maana yake ni kila kitu. Nimejaribu biashara lakini bila mtaji ni biashara gani utafanya? Nimejaribu kutafuta kazi. Bila elimu utapata kazi gani ya maana? Lilipokuja





vuguvugu la siasa na kupigania uhuru nilikuwa mstari wa mbele kujiunga, kwa matarajio kuwa nitakuwa mmoja wa wachache watakaowahi kula matunda ya uhuru. Lakini humo pia nimekata tamaa. Elimu yangu ya ngumbaru, niliyoipata kwa taabu haikufua dafu mbele ya wenzangu ambao tayari wamejipanga vizuri. Hata pale unapokuwa na wazo la maana bila elimu au pesa kamwe hutasikia wala kusikilizwa.” Alisita kwa muda. Alipozungumza tena ilikuwa kama aliyenisahau, na kuzungumza peke yake. “Nimepoteza watoto niliowapenda. Nimempoteza mke niliyempenda. Nimepoteza wazazi. Siwezi kupoteza tena nafasi ya kutajirika.”

Akanigeukia ghafla na kusema, “Nitakuwa tajiri. Nitafuta aibu zangu zote. Wewe utanisaidia. Tutapaa kama mlima Kilimanjaro. Wote waliokuwa wakitupuuza watainua nyuso zao kutushuhudia.”

“Ulisema juu ya tatizo la mtaji. Umeshaupata?” nilimuuliza.

Kwa mara ya kwanza katika kipindi kirefu nilimwona akitabasamu. “Naam, mtaji ninao tayari,” alijibu baadaye.

“Uko wapi?”

“Wewe ni mtaji.” Alijibu.

“Mimi! Nilishangaa “Unajua sijakuelewa?”

Akatabasamu tena kabla hajasema, “Utanielewa. Ni rahisi sana. Kwa ujuzi wako wa mambo ya porini, kwa uzoefu wako wa masuala ya mbugani na msimamo ambao nauona katika macho yako, naamini tukishikana ni mtaji tosha.”

Bado sikumwelewa.

Akafafanua, “Tunahitaji bunduki moja tu na risasi tano. Risasi moja ikilenga shabaha tayari tumetajirika. Bunduki ninayo, risasi ninazo. Kitu gani kitanizuia?”
 
SEHEMU YA 115

Bado sikuwa nimemwelewa. Nikamtumbulia macho ya kumtaka ufafanuzi.
“Nadhani nizungumze kwa tuo. Nisikilize kwa makini, tafadhali,” alisema akijiweka vizuri juu ya kiti na kukivuta karibu yangu zaidi.

* * *​
Niliwapenda wanyama wa porini. Niliwapenda sana. Kukuru, kakara, tumbili na nyani wakicheza juu ya miti, mara waruke toka tawi hadi tawi au toka mti hadi mti, kwangu ilikuwa burudani safi sana. Niliwahusudu chui, ngozi zao za madoa yanayopendeza na mwendo wao wa maringo porini, pasi ya kishindo, kana kwamba wao ni malkia wa nyika ni mambo ambayo yalinisisimua sana. Nilivutiwa na simba, wafalme wa mwituni, kwa ubabe na jeuri yao hasa wale wa Serengeti ambao hupanda miti na kupumzika juu yake kama chui. Niliwapenda twiga na shingo zao ndefu, niliwapenda hata fisi wala mizoga. Kwa ujumla, niliwapenda wanyama wote.
Niliwapenda pia ndege, tai mvumilivu ambaye anaweza kumfuata mnyama na hata binadamu mgonjwa kwa siku kadhaa hadi atakapozidiwa na kukata roho ndipo humvamia na kumla, njiwa ambao huburudisha kwa sauti zao nzuri, korongo na jamii zake zote, korongo mfuko shingoni, korongo uso mwekundu na wengineo. Nilimpenda pia bundi na hadithi zake zenye mapokeo anuwai.
Samaki wa majini, wadudu wa ardhini pia ni viumbe niliowapenda. Kila mmoja ambaye ungemtazama kwa makini na kufuatilia nyendo zake, kama unazo fikra usingekosa kujifunza jambo toka kwao. Nyuki na malkia wao, ambao kwa umoja wao hujengwa himaya kubwa na kutuwezesha kupata



asali. Mchwa ambao pamoja na udogo wao hujenga vichunguu, kinyonga mwenye uwezo wa kubadili rangi ya mwili wake kama anavyojisikia, jongoo menye miguu elfu moja na moja lakini asiyeweza kukimbia, nyoka asiye na mguu hata mmoja, mwepesi wa kuteleza maporini kama mshale.
Zaidi ya wanyama niliyapenda mazingira yanayowawezesha kuishi: misitu murua yenye mimea na vivuli wanavyohitaji, mito na mabwawa yanayowapatia maji na hifadhi kwa wale waishio majini, mawe, milima na mabonde ambayo ni sehemu ya maisha yao na kadhalika. Licha ya mazingira haya hifadhi ya wanyama bado ni kivutio muhimu cha watalii, ambao kutembelea kwao nchini kuna maana ya kuleta pesa. Aidha, mazingira ni urithi wa watoto na wajukuu wetu ambao wana haki ya kufaidi kama tunavyofaidi sasa.
Niliwaza yote hayo nikiwa chali kitandani, usingizi ukiwa umenikimbia usiku kucha. Ilikuwa baada ya Mpare, ambaye jina lake halisi lillikuwa Daniel Mbonea.
Alikuwa ameibuka na wazo la mradi wa hatari, unaoshawishi na kutisha pamoja, mpango wa kunitaka tushirikiane katika uwindaji wa wanyama pori na kujipatia nyara ambazo zingetupatia utajiri wa harakaharaka.
“Kila kitu katika wanyama ni pesa,” alikuwa amesisitiza. “Ukimwua tembo pembe zake ni pesa. Ukimwua chui na hata mamba ngozi zao ni pesa. Lakini tunayemtaka zaidi ni kifaru. Ukiwaua wawili tu, umasikini kwa heri. Wako wengi huko mbungani. Lazima tuwatafute.”
Wazo hilo sikupata kulifikiria. Kwa kila namna lilinitisha, nikijua kuwa si kazi ya hatari kwa maisha yetu tu, bali kwa vyovyote vile ni kinyume na sheria. Nilimkumbusha hilo. Lakini Mpare alicheka tu, kisha akaniuliza, “Hivi unafahamu





hawa waliotajirika wamefanya kazi gani?” Nikamjibu kuwa sijui.

“Huwezi kujua. Hutapata kujua. Na wao hawatajua utajiri wetu umetoka wapi. Mwanamume anahitaji kuthubutu. Hii ni nafasi yetu ya pekee.”

Nilikuwa na mengi ya kufikiri. Awali ya yote lilikuwa lile pendekezo la akina Bibi Titi Mohamed la kunitaka nirudi nyumbani nikaanzishe tawi la TANU ili kujiandaa kwa uhuru ambao alisisitiza kuwa ‘umenukia.’ Kimsingi nilikuwa tayari nimeafikiana naye. Si kwa ajili ya kwenda kufanya siasa pekee. Nia yangu kubwa ilikuwa kufika nyumbani kwetu kuwajulia hali wazazi wangu. Akiba yangu ya pesa haikuwa ndogo. Ningeweza kabisa kuwajengea nyumba bora zaidi, kuwanunulia mavazi mapya na kumpatia baba baiskeli. Nilimwambia hivyo Mpare. Lakini alinicheka tena kabla ya kuniuliza, “Baada ya kujenga hiyo nyumba?”

Sikumjibu haraka. Akaamua kujibu kwa niaba yangu. “Baada ya nyumba utarudia kwenye umasikini wako. Hutakuwa na kitu tena. Kwa maana hiyo ni kwamba huna kitu. Lazima tutafute pesa zilizotakata. Achana na vijisenti ambavyo havitabadili maisha yako.”

Ndipo nikamwomba aache nilifikirie wazo lake hadi kesho, fikra ambazo zilifanya nipoteze usingizi wangu kucha na kubakia nikitapatapa kitandani kuubembeleza.

Nilishawishika.



* * *​

Kuwinda sio lelemama. Sio kuingia porini, kuona mnyama, kuelekeza bunduki na kuifyatua peke yake. Ni zaidi ya hapo. Kuwinda kuna miiko na maadili yake. Mimi sikuwa
 
SEHEMU YA 116


mwindaji. Lakini sehemu kubwa ya maisha yangu nikiwa nimeitumia maporini nilikuwa nimeona mengi na nimejifunza mengi, mengi tosha kunipa ujanja na maadili ya porini.
Kwa mfano, usiku mmoja tukiwa katika barabara moja mbovu, ya mkato katika maeneo ya Makuyuni, nilishangaa kuona njia imeziba ghafla. Nikasimamisha gari na kumuuliza mmoja wa abiria wangu kuna nini mbele yetu. Aliangalia mara moja tu na kuniambia “Tembo.”
Kumbe tembo mkubwa alikuwa amesimama katikati ya njia akitutazama. Baada ya muda alianza kutusogelea taratibu. Nikaweka gia ya kurudi nyuma na kuanza kurudisha gari taratibu. Tembo alizidi kutusogelea. Kwa wasiwasi nilijikuta nimerudisha gari vibaya na kuingia shimoni. Tembo aliendelea kuja taratibu. Mara nikamsikia abiria wangu mwingine akiuliza kama kulikuwa na mtu mwenye kiberiti. Nilikuwa nacho. Nikampa. Kwa mshangao wangu alishuka nje ya gari na kuwasha sigara. Moshi na harufu ya sigara ulipeperushwa na upepo kuelekea aliko tembo, tulimwona akisita. Kisha tembo yule aligeuka na kuondoka zake taratibu kama alivyokuwa akija.
Tembo hapendi harufu ya sigara.
Katika tukio jingine niliwahi kulala ndani ya hema langu mapumzikoni, huko Ngorongoro. Nyakati za alfajiri nilipata hisia kuwa mambo si shwari. Nikafungua macho kutazama nje. Pazia la hema langu lilikuwa limefunguka. Simba wawili, dume na jike waliketi pale mlangoni wakinitazama. Walipoyaona macho yangu waliinuka na kuondoka zao polepole. Niliwatazama hadi walipotokomea porini.
Wanyamawanajuabinadamunidhaifu,hawamshambulii bila sababu.



Nilimsimulia hayo Mbonea. Hayo na mengine mengi. Nilimwambia kimaadili ni mwiko kumuua mnyama mwenye mtoto au watoto.
“Hutakuwa umeua mnyama mmoja tu, bali wengi. Baadhi ya wanyama wachanga huweza kutembea dakika tatu tu baada ya kuzaliwa. Wanamhitaji mama kwa maziwa na ulinzi. Ukimwua mama umewaua wao pia,” nilimfafanulia.
“Binadamu tunamwogopa sana simba, pengine na chui,” nilimweleza. “Lakini wanyama wote ni hatari. Nyati, kwa mfano, ni mnyama mwenye hasira na hila nyingi. Ukimpiga risasi ukamwona ameanguka usije ukamsogela. Wakati mwingine hata ukiwa umemkosa au kumjeruhi atajiangusha chali na kujifanya kafa. Ukimsogelea unakufa wewe. Kifo cha nyati ni mpaka pale utakapoona amejikojolea.”
“Mkojo huo wa nyati akiwa hai ni silaha kali sana.” Niliongeza. “Kama utakuwa umepambana na nyati halafu unamkimbia na kupanda juu ya mti atakachofanya ni kuukojolea mkia wake na kisha kurushia mkojo huko aliko. Mkojo wake unawasha sana. Ukikupata kwa vyovyote utaachia mti na kuanguka chini, ambako utamkuta akikusubiri. Atakusagasaga kwa miguu na pembe zake hadi ahakikishe umekufa.
Mpare Mbonea alishangaa. Ilikuwa dhahiri kuwa hilo hakulijua.
“Tembo hata kama hujampiga risasi, ukimwona kaanguka usimwogope. Tembo akianguka haamki, huwa ndio mwisho wa maisha yake. Ndiyo maana tembo hata akilala hulala wima, ama kwa kujiegemeza kwenye mti au kwa tembo wawili kuegemeana.”
Hilo pia Mbone hakulijibu. Alizidi kuduwaa.





“Huyu tunayemwinda ni mkali zaidi na wa hatari zaidi,” niliongeza. “Kwa bahati hana akili nyingi. Kifaru ana nguvu nyingi sana na kasi ya ajabu. Akikuona unatishia maisha yake atainama na kukujia kwa kasi, macho kayafumba, kwa lengo la kukuchoma lile pembe lake. Ukiona hivyo ondoka haraka sana eneo hilo. Wawindaji wajanja hulipata pembe lake kirahisi sana kwa njia hiyo. Wao husimama mbele ya mti mkubwa. Faru anapokuja huondoka mara moja kwa hasira zake na hujikuta amechomeka pembe lake katika shina la mti huo na kulididimiza. Katika jitihada za kuitoa mara nyingi pembe hiyo hung’oka, kifaru hutokwa na damu nyingi na baadaye kukata roho.

Mwindaji hujipatia hitaji lake kwa urahisi kabisa.” Mbonea alinisikiliza kwa makini sana, kana kwamba nilikuwa nikimfundisha namna ya kuingia katika ufalme wa mbinguni. Alinisikiliza. Lakini sina hakika kama alikuwa akinisikia, kwani mara alipopata nafasi ya kwanza aliivunja kanuni ya kwanza kabisa ya uwindaji. Kitendo hicho kiliniua kwa mara ya pili katika maisha yangu.
 
SEHEMU YA 117

SURA YA KUMI NA TISA

Pembe Za Faru


W
anasema ‘za mwizi arobaini’. Sisi hatukuzihitaji arobaini hizo. Siku ya tatu tu, toka tulipoanza shughuli hizo, ilitosha kabisa
kututia hatiani.
Tukio hilo lilianza hivi;
Baada ya kufika na Mbonea, aliniacha Arusha na kwenda Kilimanjaro. Aliporejea jioni hiyohiyo, akiwa na ‘vifaa’ vyake; viatu aina ya safari, suruali na shati la kaki, mfuko wa ngozi na zaidi ya yote silaha. Alikuwa na bunduki kuukuu ambayo aliielezea kama hazina yake pekee itakayomtoa katika lindi la umasikini. “Hii ndio baba, ndio mama. Nina hakika haitaniangusha,” alisema wakati akiitoa katika mfuko wake na kunikabidhi ili niikague.
Alfajiri ya siku iliyofuata tuliuacha mji wa Arusha, tukiifuata barabara ya Dodoma. Tulivipita vitongoji vya Ngarenaro, Sombetini na Majengo. Tukafika Kisongo na kuiacha njia ya Monduli kulia hadi tulipofika Makuyuni. Hao tungeweza kuelekea kulia vilevile na kufika Mto wa Mbu, Karatu na hatimaye Ngorongoro ambako nilitarajia tuanzie shughuli zetu. Tulipita kwa chini na kuliona ziwa Manyara kwa mbali kabla ya kuingia Magugu na hatimaye Babati.



Mbonea alisisitiza sana juu ya kuwatafuta vifaru kabla ya wanyama wengine. “Pembe zao ni almasi!” “Zinatafutwa sehemu mbalimbali za dunia.” Tukiipata walao moja tu….”
Nilitamani kucheka. Kwangu mimi kifaru ni mnyama mwenye sura mbaya na umbile lisilovutia kuliko wanyama wengine wote. Alivyokuwa na bahati mbaya zaidi pembe zake hizo kubwa na ndogo, zinazodaiwa kuwa za thamani zimeota juu ya pua, katikati ya uso wake. Wataalamu wanasema pembe hiyo ni mkusanyiko wa aina fulani ya nywele, zinazoota toka kwenye fuvu lake la kichwa jambo ambalo hupelekea kupoteza pembe hizo apoteze pia uhai wake.
Mbonea alinisikiliza kwa shahuku. Lakini nilihisi shahuku yake kubwa ilikuwa ni kumwona kifaru na kumpiga risasi, si vinginevyo.

* * *​
Kifaru anaweza kuishi kati ya miaka 35 hadi 40, umri ambao humwezesha kufikia uzito wa tani moja na nusu hadi mbili. Pamoja na uzito huo anaposhambuliwa hukimbia kwa kasi kati ya kilomita arobaini na tano au hamsini kwa saa. Kifaru hana makuu. Pamoja na machachari yake yote chakula chake pekee ni majani, hata yale yenye miiba. Si msumbufu, kwani muda mwingi wa mchana hupenda kujipumzisha kando ya mito au mabwawa. Hali hiyo hufanya kazi ya kumwinda isiwe ngumu kama inavyotarajiwa.
Imani ya muda mrefu juu ya pembe zake hizo, kuwa hutengeneza dawa fulanifulani muhimu kwa binadamu pamoja na mapambo murua ni sababu iliyofanya aanze kuadimika sana duniani. Ukweli huo niliufahamu fika kupitia matangazo ya watetezi wa wanyama katika vyombo vya habari. Na hivyo





ikawa sababu mojawapo iliyonifanya kushiriki katika jukumu hili huku roho ikinisuta.

Lakini pindi maji ukishayavulia nguo huna budi kuyaoga. Sikuona kama ingekuwa uugwana kubadili uamuzi, hasa nikiwa tayari humo porini. Nilimwelekeza Mbonea maeneo yote ambayo yalikuwa na sifa za kuishi vifaru. Nilimkumbusha mara kwa mara kuwa makini. “Macho ya kifaru ni dhaifu kidogo kuona mchana. Lakini pua zake ni makini sana. Akipata harufu yako kabla hujamwona na akishuku kuwa una nia mbaya ujue kuwa utakufa wewe badala yake,” nilimwambia.

Nikaongeza, “Lakini kifaru si wa kuogopa zaidi. Yupo askari wake. Huyu ni ndege ambaye muda wote hukaa juu ya miili ya vifaru akidonoa wadudu wanaomsumbua. Wakati mwingine hata pale kifaru anapokuwa na jeraha ndege hawa huliongeza kwa kulidonoadonoa. Kifaru humvumilia. Pengine analazimika kumvumilia kwa kuwa hana la kufanya. Ndege huyo huona mbali sana na humshtua kifaru kwa mlio wake mara anapohisi dalili za hatari kwa bosi wake.”

Wataalamu wanakubaliana kuwa Ngorongoro ni moja ya miujiza kadhaa ya dunia. Wanaikadiria kuwa ni mwujiza wa nane duniani. Miujiza mingine ikiwa pamoja na ile ya yale majengo yaliyopo Misri. Piramidi, ambayo yalijengwa miaka ipatayo 4700 iliyopita lakini yangali hai hadi leo. Mojawapo ambayo yametumia mawe na miamba yenye uzio wa tani moja hadi mbili kila moja na kupaa juu urefu wa meta 140. Ikizingatiwa kuwa wakati huo hakukuwa na vifaa maalumu vya ujenzi kama leo, majengo hayo yaliyoandaliwa kama hifadhi ya miili ya farao yanamshangaza kila mtu anayeyaona. Sanamu ya mmoja wa miungu ya wagiriki, Zeus, akiwa amekaa juu ya kiti chake cha enzi, chenye ukubwa wa meta 12, ikiwa
 
SEHEMU YA 118

imeundwa kwa meno ya tembo na kupambwa aina mbalimbali za madini ni mwujiza mwingine wa dunia.
Muujiza wa Ngorongoro unatokana na maumbile yake. Wakati eneo hili ambalo limo katika Bonde la Ufa linakadiriwa kuwa na ukubwa wa kilometa za mraba 8,300 zenye wanyama pori wapatao 300,0000 ndani ya eneo hilo kuna kilometa za mraba zipatazo 250 za kushangaza ziadi. Eneo hili, katika mabadiliko mbalimbali ya maumbile ya dunia lilididimia kwa kiasi cha meta 600 toka usawa wa ardhi. Humo ni shamba pekee la wanyama. Zaidi ya wanyama wapatao 20,000 wakiwemo vifaru weusi, nyati , pundamilia, tembo, fisi na wanyama wengine tele. Wamo pia ndege anuai na wadudu.
Ikiwa kama bustani ya aina yake, eneo hilo lenye maji tele, lishe ya kutosha na mazingira ya kuvutia limefanywa na wanyama hao kama makazi yao ya kudumu ingawa wanao uwezo wa kutoka na kuingia.
Kama ambavyo eneo hili humshangaza kila binadamu anayeliona kwa mara ya kwanza ndivyo lilivyomshangaza rafiki yangu Mbonea. Nilihisi kuona kitu kama machozi yakimlengalenga katika macho yake na dalili za udenda kumtoka pale tulipoingia na kuwaona wanyama mbalimbali wakiendelea na shughuli zao bila ya kututilia maanani. Twiga mmoja aliyekuwa akinyonyesha aligeuka kutuangalia kidogo kisha akaendelea kula juu ya kilele cha mti. Swala mmoja alikurupuka toka kichakani na kukimbia hatua kadhaa kabla hajasimama, kututazama kwa muda kabla na kisha kutokomea tena vichakani. Kwa mbali sana, tuliweza kuona kundi kubwa la nyati likipunga upepo huku vitoto yao vikiruka huku na huko katika michezo yao ya kawaida.
Mbonea alizidi kushangaa. Alishindwa kustahimili,



chozi likamdondoka. Alijaribu kulifuta harakaharaka, lakini haikuwa kabla ya kuliona, jambo lililofanya niangue kicheko. “Tunawatafuta faru,” nilimkubusha. “Sio kitoweo. Kwa hiyo, punguza papara.”
Tulizurura maporini humo kwa siku nzima. Tulipita katika mito ya layara, oljiro na Mungo. Tulipita kandokando mwa ziwa Makkat na katika bwawa la Mandus. Tuliingia hata katika msitu wa Lerai. Tuliwaona wanyama wengi sana isipokuwa yule tuliyemwitaji, kifaru. Ilikuwa siku mbaya.
Siku ya pili ilianza kwa namna ya pekee. Ilikuwa angavu sana na hata hali ya hewa haikuwa ya ubaridi mkali. Tulifuata barabara ya Lemaka iliyotupeleka tena kwenye ziwa Makkat ambako tulikuwa tumeona dalili za wanyama hao vikiwemo kinyesi na nyayo. Wakati tukiwa umbali wa kilometa moja toka ziwani hapa nilisikia milio ya ndege, askari wa vifaru ikitokea vichakani. Kisha niliwaona ndege hao wakiruka angani na kutokomea.
“Wapo,” nilimwambia Mbonea. “Kwa bahati mbaya, wameshapata hisia za hatari. Lazima tuwe waangalifu sana,” nilimsisitizia. Hata hivyo, nilikuwa na mshangao kidogo. Ndege hao walikuwa wametuona sisi kweli au hatari nyingine? Maana tulikuwa mbali na pale walipotokea.
Tulitembea kwa hadhari kuelekea huko, mitutu ya bunduki zetu ikiwa imeelekezwa mbele, tayari kufyatuliwa iwapo lingetokea lolote lile. Tulipofika pwani ya ziwa tuliambaa nayo kuelekea upande wa kulia walikorukia ndege. Hata kabla hatujapiga hatua ishirini tulimwona kifaru mmoja akiwa amesimama katika hali ya tahadhari akiangalia tunakotokea. Alikuwa na mtoto, kifaru mdogo ambaye alisimama katikati ya miguu ya mtoto wake.



Mara nikamwona Mbonea akipiga goti chini na kulenga shabaha. “Usimwue… ananyonyesha…” nilijaribu kumwambia. Sauti yangu ikimezwa na mlio mkubwa wa ghafla kutoka kwenye bunduki yake. Alikuwa na shabaha ya pekee. Risasi ilipenya katika paji la uso la kifaru huyo bila kuharibu pembe zake. Kifaru alitapatapa kwa muda akipigania roho yake kabla hajaanguka chini. Risasi ya pili, iliyomwingia tumboni ilimfanya akate roho palepale.
“Umefanya nini?” nilimuuliza kwa ukali. “Nilikuonya mapema kuwa mnyama anayenyonyesha! Kinda yule atafanya nini peke yake katika mazingira haya?”
Mbonea alikuwa akitabasamu, tabasamu pana ambalo sikupata kuliona huko mbeleni katika uso wake. Badala ya kunijibu nilimsikia akisema, “Mmoja tayari! Bado wawili tu tumekuwa matajiri!”
Nilikuwa nimekasirika kiasi kwamba nilitamani kumlenga bunduki yangu na kuifyatua. Majuzi tu alikuwa akilalamika watoto wake pacha waliopoteza maisha kwa utapiamlo leo anaacha mtoto wa faru apoteze maisha kwa njaa, baridi au kukosa kiongozi wa kumsaidia mbinu za kuishi porini.
Mbonea alijua nimekasirika. Hakujua kama alinikasirisha zaidi pale aliposema “Toto la kifaru litakufaa nini rafiki yangu. Hata pembe halina. Achana nalo, tushughulikie mali yetu.”
Wakati huo ‘toto’ hilo la kifaru lilikuwa limehisi kuwepo kwa jambo baya lililomtokea mama yake. Lilionyesha kushangazwa na damu. Likamzunguka mama yake mara tatu na kujaribu kumtikisa kabla halijaanza kulia kwa sauti yake mbaya, sauti ambayo masikioni mwangu ilitia huzuni kubwa.
 
SEHEMU YA 119

Sijui nini ambacho kingefuata baina yangu na rafiki yangu Mpare kama jambo jingine, kubwa zaidi, lisingetokea. Tulijikuta ghafla tumezingirwa na kundi la askari wa wanyama pori wasiopungua sita, kila mmoja akiwa na bunduki mkononi. Na kila bunduki ikiwa imetuelekea.
“Tueni bunduki zenu chini na muweke mikono yenu juu mara moja!” mmoja wao alitoa amri.
Tulitazamana na Mbonea kwa mshangao. Hatukuwa na namna yoyote ya kupambana nao wala kukimbia. Tukaziangusha bunduki na kuweka mikono yetu juu ya vichwa.
“Washenzi wakubwa nyie,” askari yule aliendelea kufoka. “Tumemlinda kifaru huyu kwa miaka nyie mnamuua kama mchezo. Mtakuwa mfano mzuri sana kwa jamii. Kama hamjafungwa maisha, miaka ishirini kwa kila mmoja wenu haitamkosa.”
Walizichukua bunduki zetu. Wakatutia pingu za mikono kisha tukaanza kusukumwa kuelekea walikoificha gari yao. Tukatupwa ndani ya gari, ikatiwa moto na kuelekezwa mjini Ngorongoro ambako tulifungiwa katika kijichumba kidogo kwa siku tatu kabla ya kupelekwa Arusha. Tulifunguliwa mashataka.

* * *​
Kabla ya kesi yetu kuanza kusikilizwa tulikaa rumande kwa wiki tatu nzima, tukiwa tumewekwa katika chumba cha watu hatari sana. Chumba hicho kilijumuisha watu watatu wa kesi za mauaji, watu watano wanaotuhumiwa kwa kujaribu kuvunja benki kwa nia ya kuiba, mmoja aliyekamatwa akimnajisi ng’ombe na wengine tele wenye tuhuma hii au ile.



Mmoja kati ya watuhumiwa hao nadhani alikuwa kichaa. Siku zote , wakati wote, alikuwa mtu wa kupiga kelele. Na kauli yake ilikuwa moja tu; ‘Nitaua mtu. Kama si leo kesho!’ Kauli hiyo ilinitisha sana kwani sikujua alikusudia kumwua nani. Hakimu anayesikiliza kesi yake, askari aliyemkamata au yeyote kati yetu mahabusu wenzake. Macho yake yalikuwa yanatisha, sura yake ikitangaza shari kama shetani mwenyewe. Kwa kweli alininyima raha na kufanya nijitahidi kila ilivyowezekana kumkalia mbali.
Hiyo ndiyo jumuiya mpya niliyojiunga nayo, jumuiya ya wahalifu, jumuiya ya waasi wa sheria. Mimi, Petro Mtukwao Kionambali Kalimanzira tayari nilikuwa mmoja wao. Machoni mwa jamii nilikuwa mtu duni, asiyefaa kuishi uraiani bali gerezani kusubiri hukumu kamili.
Ilinisikitisha zaidi pale watuhumiwa hao walipotupokea kwa furaha kana kwamba sisi ni mashujaa. “Jengo hili limejengwa kwa ajili ya wanaume kama nyie,” mmoja wao alisema. “Bila nyie, polisi na mahakimu wangekufa njaa, kwani hakuna mtu ambaye angekubali kuwalipa mishahara bure!”
Sikumwelewa.
Wala hakunijali. Aliendelea na mawaidha yake ya kishetani, “Wanaletwa hapa watu kwa makosa ya kitoto kabisa. Eti jitu zima limepiga hadi kumwua mkewe au mwanawe. Eti jitu na akili zake limeiba kuku wa jirani. Nyie wanaume bwana! Kuingia msituni, kupambana na wanyama hatari kama faru ili mpate zile pembe zake ni uanaume. Kukamatwa kwenu ni ajali kazini tu. Kama msingeshikwa mngekuwa matajiri wakubwa kutoka nchi hii.”
Hiyo ndiyo jela! Hakuna siri! Toka siku ya kwanza tulipoingia tayari tulikuwa gumzo. Kila mmoja alionyesha dalili



ya kutupongeza! Laiti wangejua nilivyokuwa najisikia moyoni! Nilikuwa taabani kwa aibu na kukosa raha. Sikutegemea kamwe maishani nifanye kitendo chochote, ama kwa makusudi ama kwa bahati mbaya, ambacho kingeniweka upande wa pili wa sheria. Nilikuwa na nilitegemea kuwa mtu mwaminifu na mwadilifu katika uhai wangu wote. Nilijuta kukutana na Mbonea. Nilijuta zaidi kumsikiliza. Nilitamani kumchukia maisha yangu yote. Nilitamani kumwambia hayo.
Hata hivyo, Mbonea hakuwa katika hali ya kuambiwa hayo. Toka tulipokamatwa muda wote alikuwa mtu wa kutokwa machozi. Mara nyingi, kwa sauti inayotetemeka, nilimsikia akinong’ona, “Bibi yangu kikongwe atafanya nini jamani… dada yangu kiwete ataishi vipi…” alisema huku akifuta machozi. Kwa muda huo mfupi Mbonea tayari alikuwa amekonda na kupungua uzito kwa zaidi ya kilo kumi. Hakupata usingizi. Alikula kwa shida baada ya ushawishi mwingi. Ndiyo, ni yeye aliyeniingiza katika mkasa huo. Lakini kwa jinsi alivyokuwa akitia huruma nilijikuta nikimhurumia kuliko hata nilivyojihurumia mimi.
Mbonea alikuwa na ndugu wengi. Alitembelewa na watu mara kwa mara na kujadiliana nao hili na lile. Nilishangaa alivyokuwa haonyeshi nia ya kunishirikisha katika maongezi hayo, ambayo nilitarajia yangelenga katika kutafuta ufumbuzi wa tatizo letu. Sikuwa na la kufanya. Nikabakia na uyatima wangu nikiyaweka yote mikononi mwa Muumba.
Kabla ya kupelekwa mahakamani, tulihojiwa na watu mbalimbali, polisi, wanasheria na hata watuhumiwa wenzetu. Kila mmoja alikuwa na ushauri wake kwetu. Polisi na wanasheria wa serikali walinishauri kukiri kosa ili kupunguza uzito wa adhabu. Wanasheria wengine walinishauri kukataa
 
SEHEMU YA 120

katakata kuhusika na suala hilo. Watuhumiwa na wenye uzoefu wa masuala ya kesi pia walinionya juu ya athari za kukubali kosa kubwa kama lile. Hali iliyofanya nijione kuwa nachangwanywa akili.
Tatizo jingine lilikuwa mshitakiwa mwenzangu. Kila nilipomtaka tukae na kuweka mkakati wa pamoja alikuwa akiishia kulia tu. Hatukupata hata mara moja kukaa na kuzungumza lolote kwa tuo. Mbaya zaidi ni pale ambapo tulikuwa tukihojiwa na hata kuandika maelezo kila mmoja kwa wakati wake. Sikujua amejieleza vipi na kuandikisha lipi, kama ambavyo niliamini yeye hakujua nilichoeleza.
Hatimaye, siku ya siku ikafika. Tulichukuliwa na lori la polisi toka gereza la Kilimwanga, tulilokuwemo na kupelekwa mahakamani mjini Arusha. “Pilato” alikuwa mzungu, mtu mfupi; mwembamba mwenye sura ya kitoto. Isipokuwa kwa miwani mizito na joho alilovaa isingekuwa rahisi kumfananisha na hakimu. Nilikuwa nimepata sifa nyingi za hakimu huko gerezani. Nusu ya wafungwa wote ni yeye aliyewahukumu. Nilikwishaambiwa mapema kuwa kama tungemkuta hakimu huyo, ambaye gerezani walimwita “Fisi maji” kwa ukali wake, gereza lisingeweza kutuepuka. Ajabu ni kwamba kwa sura hakuonekana katili kama alivyoelezewa.
Siku hiyo mahakama ilikuwa na kesi nyingi, kubwa na ndogo. Lakini nadhani kesi yetu ndiyo iliyomvutia zaidi maana niliona kesi nyingi akiziendesha harakaharaka. Zingine alizihairisha na nyingi alizitolea hukumu bila umakini mkubwa, huku mara kwa mara akitupa jicho upande wetu kama anayetusubiri kwa hamu.
Saa na hatimaye dakika ikawadia. Tukiitwa kwa majina, mmoja baada ya mwingine na kusimamishwa kizimbani. Mimi



nikitetemeka kidogo, mwenzangu akitetemeka na kupepesuka kama jani la mwembe.
Hakimu alivua miwani na kututazama kwa takribani dakika nzima, kabla hajaivaa tena na kusoma jalada la tuhuma zetu lililokuwa mbele yetu. “Petro Mtukwao Kionambali… Daniel Mbonea mnashtakiwa kwa kuingia katika hifadhi ya taifa ya Ngorongoro kwa makusudi ya kufanya vitendo vya uharamia. Kosa la pili, kwa makusudi vilevile mlimuua mnyama aitwaye kifaru kwa kumpiga huku mkijua fika kuwa kifaru huyo ni mmoja wa wale wanaolindwa na serikali kwa gharama kubwa ili kuifadhi viumbe hao walio hatarini kutoweka. Aidha, kosa lenu la tatu ni kumwua kifaru huyo huku mkijua na kuona wazi kuwa alikuwa na mtoto mchanga ambaye alimtegemea. Kwa maana hiyo mmehatarisha maisha ya kichanga huyo pia.” Hakimu alivua tena miwani yake na kunikazia macho,​
“Petro Mtukwao Kionambali… ni kweli au si kweli?”
Nikageuka kumtazama mwenzangu. Alikuwa akinitazama pia, ingawa macho yake yalijaa machozi. Kwa namna fulani alikuwa kama anayenisihi jambo fulani. Sikujua ni jambo lipi. Nikainuka na kumtazama hakimu. “Ni kweli Mheshimiwa,” nilijibu.
Nilipata hisia kuwa kila mtu katika chumba hicho cha mahakama, ikiwa pamoja na hakimu mwenyewe, alipigwa na butwaa. Hakimu aliinama, akaandika jambo katika faili lake, kisha akainua tena miwani na kumkazia macho Mbonea. “Daniel Mbonea, mashtaka haya ni kweli au si kweli?”
“Sio kweli, Mheshimiwa,” Mbonea alijibu kwa sauti iliyokuwa na uhakika kinyume na hali yake.
Hakimu aliandika jambo. Akainua tena uso wake na kututazama kwa zamu kabla hajauliza, “Nataka kufahamu



kitu kimoja. Kati yenu nani aliyefyatua bunduki, ambayo risasi yake ilimuua kifaru yule?”
Tulitazamana tena na Mbonea. Alikuwa amebadilika tena. Anatetemeka na anapepesuka nusura aanguke chini. Macho yake yalijaa huruma na simanzi. Niliweza kuyasoma mawazo yake katika macho yake hayo; bibi yangu kikongwe atafanya nini jamani… dada yangu kiwete ataishi vipi… ujumbe ambao ulinifikia bila sauti. Ukanitia huruma. Bila kujua nilifanyalo, niliinua tena mkono wangu na kumjibu hakimu, “Ni mimi Mheshimiwa.”
Nilisikia sauti za kitu kama, “Ah!” zikiwatoka watu wawili watatu chumbani humo. Wengi wao walinikazia macho ya mshangao na kutoyaamini masikio yao. Hata hakimu alionekana kutoamini kile alichokisikia. Akaandika alichokuwa akikiandika. Kisha aliahirisha kesi kwa kupanga tarehe ya hukumu.
Tukarudishwa mahabusu. Huko nilikuwa gumzo kubwa. Kila mtu aliyesikia kilichotokea mahakamani alitaka kuniona kwa macho na kuisikia sauti yangu.
“Pole sana, mdogo wangu,” mzee mmoja aliyekaa rumande kwa miaka tisa sasa aliniambia. “Hivi hujaambiwa kuwa hata kukubali kosa ni kosa? Maana yake ni kwamba ulifanya kosa huku ukijua kuwa unafanya kosa. Adhabu yake ni kubwa sana. Humu, wewe anza kutafuta kona yako ambapo utalala kwa miaka ishirini. Halafu huonekani kama mtu wa kumudu chawa, kunguni na chakula cha ajabu kinachotolewa.” Nadhani nilikuwa nimechanganyikiwa kwani haikuniingia akilini uzito wa mkasa uliokuwa mbele yangu hadi siku ya hukumu. Hakimu, akiwa mkali kama pilipili, alitumia zaidi ya dakika arobaini kuelezea athari za ujangili​
 
SEHEMU YA 121

kwa wanyamapori hasa wale adimu kama faru. Alitoa mifano ya nchi mbalimbali za dunia ambazo zimeweka sheria kwa ajili ya kuwalinda wanyama ambao wanazidi kutoweka siku baada ya siku.
“Tumeirithi nchi hii ikiwa na mazingira murua, wanyama na ndege tele. Tumerithi hayo kwa kuwa babu zetu hawakuwa waharibifu wala katili kwa wanyama. Tunahitaji watoto na wajukuu zetu nao warithi hali ile tuliyoikuta. Kwa bahati mbaya baadhi yetu wametia pamba masikioni mwao. Wanapuuza jitihada zote za serikali na dunia kwa matarajio ya maslahi yao binafsi. Hawa lazima wawe mfano kwa wengine kwa kupewa adhabu kali,” hakimu alisema.
“Kesi iliyo mbele yangu inamhusu Petro Mtukwao Kionambali na Daniel Mbonea. Hawa walikamatwa na askari wa wanyamapori waliokuwa wakitelekeza jukumu lao la kumlinda kifaru huyu mwenye mtoto. Kwa ukatili mkubwa walimpiga risasi na kumwua.”
“Katika maelezo yao hapa mahakamani na hata yale ya awali, Mbonea alikataa kuhusika na mauji haya. Anasema kuwa alimtembelea rafiki yake huyo mbugani baada ya kufahamiana naye mjini Moshi na Arusha bila kujua kuwa kazi yake ni uwindaji wa vifaru. Kuwa kifaru yule mwenye mtoto alipotokea alimwona akiandaa bunduki na kutaka kumwua. Alimtahadharisha lakini Kionambali hakumsikiliza. Alifyatua risasi na kumwua kifaru yule. Kwa upande wake Kionambali mwenyewe katika maandishi na maelezo ya ana kwa ana mahakamani amekiri yote yaliyotokea. Hivyo, mahakama inamwachia huru Daniel Mbonea. Aidha, inamuhukumu Petro Mtukwao kifungo cha kwenda jela miaka ishirini na kazi ngumu na viboko kumi, ili awe mfano kwa wengine.”



Sikuelewa. Nilimwona Mbonea akibebwa juujuu na ndugu zake huku wakishangilia. Mimi nilitiwa pingu, nikasukumwa kuelekea kwenye gari la magereza ambako nilipandishwa na kurejeshwa Kilimanga ambako nilivuliwa mavazi ya uraiani na kuvishwa yale ya gereza yenye namba na tarehe yangu ya kufunguliwa. Niliondolewa katika chumba cha mahabusu na kuelekezwa katika selo nyingine ambayo ingekuwa makazi yangu hadi mwisho wa kifungo changu. Kama ile ya mahabusu hii pia haikuwa na kitanda wala godoro. Nilipewa blanketi kuukuu na kuelekezwa mahala pa kulala. Juu ya sakafu ngumu. Kona moja ilikuwa na kijichumba kidogo chenye harufu kali ambacho kilitumiwa kama choo na bafu. Mlikuwa na bomba lakini halikupata kutoa walao tone moja la maji!
Nilitoka nje na kuketi mahala fulani nikiwa nimejiinamia. “Pole sana,” nilisikia sauti ikiniambia. Nikatazama. Alikuwa yule mzee wa miaka tisa mahabusu. “Nilikuuliza kama unamwamini mshtakiwa mwenzako hukupata kunijibu,” alisema na kuendelea, “Yule kakuuza rafiki yangu. Kesi yenu ilikuwa mbaya sana. Ilikuwa lazima mtu afungwe. Amekuchezea akili umefungwa wewe, yeye ametoka.”
“Kwa vipi?” niliuliza “Mbona mtu mwenyewe alikuwa mtu wa kulialia muda wote?”
“Kulia!” mzee alisema akicheka. “Kama alikuwa analia kweli basi yalikuwa machozi ya mamba. Alikuwa akikuchota akili huku akikucheka. Kwa bahati mbaya, wewe ulishiriki kumrahisishia azma yake kwa kukiri hili na lile. Hilo limemfanya atoke haraka kuliko alivyotegemea.”
Machozi ya mamba! Niliwaza kwa mshangao.

20
Ben R. Mtobwa











SURA ISHIRINI

miaka ishirini


M
fikiriemtotomdogosanawakiume, aliyeondoka kwao zamani sana kuiokoa roho yake, mtoto ambaye alifuatana na babu yake, wakavuka
misitu na nyika, milima na mabonde, mito na mabwawa hadi nchi ya mbali. Huko mtoto aliona nuru mpya elimu. Akaanza kusoma huku akiwa na matumaini.
Mtoto huyu, ambaye kwa miaka nenda miaka rudi alikuwa hajazitia machoni sura za wazazi wake wapenzi, wala kuonana na babu yake kipenzi, majuzi tu alikwishafikia uamuzi wa kurejea nyumbani. Na alitarajia kupokelewa kishujaa kwani akiba yake benki ilikuwa ya kuridhisha. Angeweza kujenga nyumba ya kisasa na kutoa zawadi nyingine tele ambazo zingefanya ukoo mzima umshangilie. Lakini, kwa mara nyingine tena likatokea jambo jingine, kubwa kuliko yote yaliyopata kutokea. Na sasa yuko kifungoni. Hategemei kutoka kabla ya miaka ishirini! Hategemei kuwakuta wazazi wake wakiwa hai! Yeye mwenyewe hategemei kutoka akiwa hai!
Mtoto huyo ni mimi, Petro Mtukwao Kionambali. Tayari miezi miwili ilikuwa imepita toka nianze kutumikia kifungo. Miezi miwili! Ilibakia miezi isiyopungua mia mbili thelathini na nane, nikiwa ndani ya chumba hiki kinachonuka, nikilala juu
 
SEHEMU YA 122

ya sakafu hili gumu na kula chakula chao kisikolika! Mara kwa mara wafungwa wenzangu walinishauri nijitahidi kuyazoea maisha ya jela, lakini yalikuwa hayazoeleki. Binadamu gani atazoea kula mlo mmoja, tena usioridhisha, kwa siku? Binadamu gani atazoea kula saa kumi na moja jioni, katika chumba kisicho na madirisha na kutoipata tena hewa ya nje hadi kesho yake?
Niliteseka sana kialikili zaidi ya kimwili. Nilitafakari kwa nguvu zangu zote na kushindwa kabisa kutambua kitu gani kinafanya siku zote niwe kondoo wa kafara. Sikuweza kuelewa kwa nini nilikwenda Kilimanjaro na kukutana na ‘Mpare’ Daniel Mbonea. Sikuweza kuelewa kwa nini nilikubali kushawishika hata nikafuata ushauri wake na kuahirisha dhamira yangu ya kurejea nyumbani Buha na badala yake kuingia naye porini kuwinda nyara za serikali. Zaidi sikuweza kuelewa kabisa sababu iliyofanya nijisikie kumhurumia kiasi cha kumlinda kwa kujitoa kuwa ni mimi niliyefyatua risasi ya kumwua kifaru kutokana na madai yake ya kutegemewa na bibi kizee na dada kiwete? Mie pia si nilikuwa na babu kizee na ndugu vilema wengi tu ambao walinitegemea. Machozi yake ya mara kwa mara? Mie pia ningeweza kutokwa na machozi siku nzima kama ningependa. Kwa kweli sikuweza kabisa kuelewa sababu.
Hisia za siku nyingi, ambazo nilianza kuzisahau zilinirejea. Hirizi iliyopotea! Nilianza kueleka kuamini kuwa chanzo cha balaa na mikosi yangu ni kuipoteza hirizi ile ambayo babu alinihusia kuitunza. Una alama… alama ya shari... Niliyakumbuka tena maneno niliyoambiwa kule Sumbawanga na Mbeya. Pengine ni kweli? Pengine alama hii ndiyo iliyomvuta Mbonea? Iwe kweli iwe uongo, niliwaza,



kwa vyovyote vile ilihusiana na hirizi yangu iliyopotea. Kama ningekuwa nayo, niliendelea kuwaza, mtu yeyote mwenye nia mbaya nami asingenisogelea. Kamwe nisingewekwa alama!
Majuto ni mjukuu! Niliwaza. Nilikuwa na miaka isiyopungua ishirini ya kuishi katika gereza hilo huku nikiwaza hayo. Mawazo ambayo yangeweza kunitia kichaa. Lazima nijifunze kuachana nayo. Lazima nipate jambo jipya la kuwaza badala ya kukodolea macho kalenda nikiitafuta siku ambayo ingechapishwa baada ya miaka ishirini.
Nilijitahidi pia kumfukuza Mbonea katika fikra zangu. Bwana huyu alikuwa mtu wa ajabu sana. Alikuwa mnafiki asiye na haya kuliko binadamu wote niliopata kuwafahamu. Siku tatu tu baada ya yeye kupata uhuru wake na mimi kuanza kutumikia kifungo alikuja gerezani kuniona. Niliarifiwa kuwa nilikuwa na mgeni, sikuambiwa mgeni huyo alikuwa nani. Pengine nisingekwenda. Nikamkuta kakaa kitako akinisubiri. Alikuwa anang’ara mwili na mavazi, hali iliyofanya nijishuku kuwa nanuka jasho na uchafu wa nguo zangu.
Nilimwona akitafuta chozi la kunionyesha uchungu aliokuwa nao kwangu. Halikotoka. Sikuwa tena mgeni wa machozi yake ya mamba. Nilitamani kucheka. Hakunipa nafasi hiyo. Aliinuka na kunikumbatia bila ridhaa, kisha akanipa mkono wake wa kulia ambao muda wote alikuwa ameufumba. Nikaupokea na kubaini kuwa katika kunipa mkono huo alinipa kitu fulani kilichokuwa kiganjani. Nikaufungua mkono kutazama. Alikuwa amenipa kipande cha aina fulani ya jani.
“Nini hiki?” Nilimuuliza “Jani.”
“Jani la nini?”
“Jani la isale,” alinijibu.





Nililifahamu jani hilo. Isale ni majani uhimu sana kwa Wachaga. Hutumiwa kupanda katika mipaka ya mashamba, kuepusha migongano. Lakini jani hilo pia hutumiwa kwa upatanishi. Mchaga anapomfuata mwenzie kwa suala zito kama kuombana radhi, kudaiana na hata ndoa huweka jani hilo mkononi na kumshikisha mwenzi huyo kabla ya mazungumzo ya siri. Mara nyingi baada ya kitendo hicho mazungumzo huwa ya amani na mafanikio kwa pande zote mbili.

“Unanipa isale ya nini?” nilimuuliza.

“Nataka kukuomba radhi kwa yote yaliyotokea,” alisema. “Nataka tuendelee kuwa ndugu. Ndiyo, uko ndani niko nje. Nitautumia uhuru wangu huko nje kuhakikisha hukai ndani zaidi ya miezi mitatu. Nitahakikisha…”

“Umenipa isale ya nini?” nilimkatiza kwa ukali kidogo. “Mimi sio Mchaga na wewe sio Mchaga pia, kama ulikuwa ukisema ukweli.”

Mbonea alikohoa kidogo kabla hajanijibu akisema, “Ni kweli mimi sio Mchaga. Lakini sisi Wapare wa Ugweno tuna tamaduni nyingi zinazofanana na Wachaga. Moja ni jani hili. Tunalitumia katika upatanishi na mengineyo.”

Nilimtazama kwa makini mtu huyu. Alikuwa Mbonea yuleyule mwenye sumu ya nyoka na hila za kinyonga. Sikuona sababu za kuendelea kumsikiliza. Nikamwambia, “Sikiliza Mbonea. Mimi sio malaika. Mimi sio Yesu Kristo ambaye aliwaelekeza wanafunzi wake wakipigwa shavu moja wakinge na la pili. Mimi ni binadamu kama wewe. Naomba uondoke. Naomba usikanyage tena hapa kwa niaba yangu.”

Nadhaini hakunielewa. Nilimwona kaduwaa, hajui lipi zaidi aseme. Nilimwacha katika hali hiyo na kurudi katika ‘utumwa’ wangu wa miaka ishirini.
 
SEHEMU YA 123

Siku mbili tatu baadaye nilipata ugeni mwingine. Huyu alikuwa mwanamke. Alikuwa mnene, maji ya kunde. Sura yake nzuri haikuwa na dalili zozote za dhiki wala misukosuko ya maisha. Alifuatana na watoto wawili wa miaka saba au minane, mapacha.
“Mgeni wangu?” Nilimuuliza. “Ndiyo. Wewe si Petro Kionambali?” “Ndiye.”
Basi mimi ni mgeni wako. Nimetumwa na rafiki yako Daniel Mbonea nikuletee chakula. Ameniagiza nikutembelee mara mbili kila wiki na kukuletea mahitaji yako yote muhimu.
“Mbonea!” Nikaropoka. “Wewe ni nani kwake?” “Mimi ni mkewe.”
Sikuyaamini masikio yangu, “Mkewe?” Nikauliza kuhakikisha. “Mke wa ngapi?”
“Kwani alikuambia anao wake wangapi?” “Ninachofahamu ni kwamba hana mke. Mkewe alifariki
zamani kwa kujinyonga.”
Ikawa zamu ya mama huyo kushangaa. “Mkewe alijinyonga?”
Kisha akaangua kicheko. “Bila shaka alikuwa akikutania. Tumeoana toka tukiwa vijana, sasa tunaelekea uzeeni. Hana mke mwingine, hana mke aliyepata kujinyonga.”​
Niliduwaa kwa muda. “Na hawa watoto? Unataka kuniambia kuwa ni wake?”
“Ndiyo. Ni watoto wetu. Alikuambia hana watoto?” Nilishindwa kumwambia kuwa kwa mujibu wa
Mbonea mwenyewe watoto wake pacha walikufa zamani kwa utapiamlo. Nilishindwa kuuliza juu ya bibi kizee na dada yake kiwete wanaomtegemea. Sikuhitaji kuhakikishiwa kuwa yote



aliyosema ulikuwa uongo, uongo mtupu, uongo uliokusudiwa kunitia huruma ili nishawishike kushirikiana naye katika dhamira yake chafu ya kutafuta utajiri.
“Mama, nashukuru sana,” nilimwambia. “Naomba umrudishie chakula chake. Halafu, tafadhali mwambie, sihitaji msaada wake wa aina yoyote si leo si kesho wala keshokutwa.”
Nikageuka na kuondoka zangu.
Nilimwacha mama huyo kaduwaa, haelewi kinachoendelea. Laiti angejua kuwa aliolewa na nyoka…

* * *
Gerezani kuna kiu. Kwangu kiu hiyo haikuwa ya vinywaji baridi au vinywaji laini. La, hasha! Ilikuwa kiu ya habari. Gerezani kuna njaa. Lakini njaa yangu mimi haikuwa ile ya chakula chao kibovu, ilikuwa ya kuona na kusikia kile kinachoendelea nje ya ukuta huo imara wa gereza la Kilimoanga. Kwangu hiyo ilikuwa adhabu kubwa zaidi na inayonitesa zaidi. Kwa nia ya kukidhi adha hiyo nilijenga urafiki na mfungwa mmoja kwa namna ya ajabu. Alikuwa na redio ndogo.
Kwa bahati mbaya, bwana huyu alipenda sana kusikiliza muziki. Mara kwa mara alitafuta stesheni zinazopiga muziki wa kina Mbaraka Mwinshehe na Salumu Abdallah. Nyimbo za ‘malaika’, ‘wanawake wa tanzania’, ‘mwanameka!’ ‘shida na Marijani Shabani’ zilikuwa mdomoni mwake kila dakika kufuatia mipigo redioni. Ilikuwa kazi ngumu kumshawishi mara chache aniruhusu kusikiliza taarifa za habari na vipindi vingine makini zaidi.
Ni kwa kupitia redio yake hiyo nilipofahamu kuwa Zanzibar, nchi ambayo ilitawaliwa na waarabu kwa muda mrefu, nayo ilikuwa ikiwaka moto kwa vuguvugu la kudai kujitawala.



Chama kilichoitwa Afro Shiraz kilikuwa kimeanzishwa na kuwapa taabu kubwa watawala.
Aidha, nilibaini kuwa hesabu ya watu ilifanywa mwaka 1957chini Tanganyika ilionyesha kuwa tulikuwa 9,087,6000 kati ya hao 364,072 au asilimia 4 tu wakiishi mijini.
Mwaka wa 1958 zikasikika habari za Julius Nyerere kushtakiwa mahakamani kwa kuandika katika gazeti la TANU, sauti ya TANU. Habari ambazo magavana wawili wa wilaya walidai kuwa ziliwadhalilisha. Nyerere alishinda shitaka moja na kutiwa hatiani kwa shitaka la pili. Adhabu yake ilikuwa kifungo cha miaka sita jela au faini ya shilingi 3,000/= alilipa faini. Kama asingelipa uenda tungejumuika naye gerezani humo.
Tukio hilo lilikuwa kama chachu ya matukio tele ya kisiasa yaliyoendelea kutumbuiza maisha yetu gerezani humo. Zilisikika habari za TANU kuchachamaa katika kudai uhuru. Zikasikika habari za chama kipya, ANC, kilichoongozwa na Zuberi Mwinyishehe Mtemvu, pia kiliomba ridhaa ya wananchi kuongoza serikali. Hatimaye, ikaja ile siku ya siku, desemba 9, 1961 tulikesha tukisikiliza redio, sauti ya Dar es salaam iliyokuwa ikitangazwa na bwana mmoja, Hamza Kasongo, kusheherekea uhuru. Ilipotimia saa sita za usiku tulisikiliza taarifa za bendera ya malkia wa Uingereza ikishushwa na ile ya Tanganyika ikipandishwa, Julius Nyerere akiwa Waziri Mkuu wa kwanza.
Pilikapilika hizo hazikuwa Tanganyika pekee. Kenya na Uganda pia kulikuwa kukiwaka moto. Lakini tukio lililonigusa ni lile la visiwa vya Zanzibar, Unguja na Pemba. Huko nako kulikuwa na purukushani kali za kisiasa. Mtu mmoja aliyeitwa Abeid Aman Karume na chama chake cha Afro Shiraz alikuwa
 
SEHEMU YA 124

akusuguana na vyama vya ZPPP na ZNP. Uchaguzi uliojaa hila ulifanyika na kutoa madaraka kwa vyama vile vilivyokuwa na ushawishi mkubwa wa Waarabu dhidi ya Afro Shiraz iliyoshindwa kwa asilimia 54.3 januari 12, 1964 visiwa hivyo vililipuka, Waarabu wakatimuliwa, Karume na chama chake wakachukua uongozi.
Aril 21, 1964, pamoja na kuwa mfungwa nililala nikiwa Mtanganyika, kesho yake nikaamka nikiwa Mtanzania. Hiyo ilifuatia Muungano wa Tanganyika na Zanzibar ambao uliambatana na kubuniwa kwa jina jipya la nchi.
Nikiwa mfungwa kutokana na tuhuma za kuharibu maliasili na urithi wa taifa masikio yangu hayakuwa wazi kwa habari za kisiasa pekee. Nilitegemea siku hiyo habari zote zilizohusiana na mazingira, misitu na viumbe wake, maziwa na vyote vilivyomo na hata hali ya hewa. Kila nilipofanikiwa kupata gazeti nilifurahi zaidi na kulisoma lote, ikiwa pamoja na mashairi na kujaribu kujaza mafumbo.
Kupitia gazeti moja zile jitihada zilizobuniwa mwaka 1954, za kupandikiza aina mpya ya samaki katika ziwa Nyanza, ambalo sasa liliitwa Victoria, lilikuwa limetiliwa mkazo zaidi mwaka 1960 na kwamba jaribio hilo lilianza kutoa matunda. Hata hivyo, kulikuwa na malalamiko mengi toka kwa wana mazingira mbalimbali duniani kuwa samaki hao ambao ni wakubwa zaidi walikuwa wakiwateketeza samaki wa asili kwa kuwala. Hali ambayo ilielezewa kuwa iliashiria kuwa aina zipatazo hamsini za samaki wa ziwa hilo zilikuwa hatarini kutoweka.
Kwa upande mwingine nilijifunza kuwa serikali ilikuwa imeongeza jitihada za kuwalinda wanyama, miti na misitu asilia. Pamoja na Serengeti maeneo kama Ngorongoro, Ziwa Manyara,



Tarangire, Mikumi, Rubondo, Udzungwa na mengineyo tayari yalisajiliwa kama hifadhi maalumu za taifa. Maeneo mengine yalikuwa pamoja na Selow, Kilimanjaro, Gombe, Mahele na Katavi.
Hali kadhalika, mapori na misitu kadhaa ilihifadhiwa kwa ajili ya urithi. Selow yenye ukubwa wa takriban kilomita za mraba 50,000 ikiwa na maana kuwa inazishinda nchi kama Switzerland au Denmark kwa ukubwa lilikuwa eneo mojawapo. Ikiwa haina mtu anayeishi huko wala shughuli zozote za kibinadamu zinazofanyika, Selow inakadiriwa kuwa na tembo wapatao 60,000, nyati 160,000, viboko 40,000 na simba 5000. Pamoja na wanyama wengine anuai Selow inakisiwa kuwa na aina 440 za ndege. Ziwa Tagalala mto Rufiji, miti ya miombo na migunga pamoja na misitu inayoambaa na mito ni baadhi ya vivutio vinavyotajwa katika hifadhi hiyo.
Mapori mengine yaliyoifadhiwa yalikuwa pamoja na Moyowosi, Bugiri, Rungwa, Maswa, Kisiwa cha Saa Nane, Mkomazi na Ugala. Pia Usangu, Mpanga, Rukwa, Swaga, Ikorongo ni miongoni mwa mapori hayo.
Huko Zanzibar pia jithada tele zilikuwa zikifanyika kulinda mazingira ya nchi kavu na bahari. Pomboo, viumbe wa majini ambao wataalam hawapendi kuwaita samaki kwa kuwa wananyonyesha watoto wao, walikuwa wakitafutiwa namna ya kuwalinda. Vifo vya mara kwa mara vya viumbe hao, ambao ni wahamajihamaji vilikuwa vikisumbua sana vichwa vya wana mazingira. Viumbe hao, ambao wanafundishwa kwa urahisi hasa pale wanapochupa toka majini kama golikipa anayedaka mpira wanaweza kuwa kivutio kikubwa cha watalii.

* * *​





Pamoja na ‘alama’, kama kweli nilikuwa nayo nyota yangu ya kupendwa na watu bado ilikuwa iking’ara, hali ambayo naamini ilichangia kufanya niweze kuyamudu maisha ya gerezani humo hadi mwisho wa kifungo. Wakati wenzangu wengi walipigwa kama ng’ombe, baadhi wakifa kwa kutiliwa maanani wanapougua, mimi hali ilikuwa tofauti. Nilipendwa na mkuu wa gereza. Nilipendwa na maafisa wake pia. Nadhani kale ka usomi kangu kalisaidia. Mara kwa mara nilipewa kazi ya ukarani, kujaza fomu, kurekodi matumizi au mahitaji, kuandaa taarifa za wafungwa wenzangu na kadhalika. Kazi hizo zilipokuwa finyu nilipewa udobi wa kunyoosha nguo za askari magereza. Mara nyingine nilipewa kazi ya kutunza bustani ya mkuu wa gereza ambazo ziliambatana na kudokolewa chakula cha binadamu toka jikoni mwake.

Sherehe za uhuru na zile zilizofuatana mara kwa mara ziliambatana na kuachiwa kwa baadhi ya wafungwa wenye makosa madogomadogo au ambao tarehe zao za kufunguliwa zilikaribia. Bahati hiyo mimi haikunipitia. Uzito wa kosa langu haukuruhusu kunijadili katika kundi hilo. Kama ungeruhusu naamini nisingekuwa na sababu ya kusubiri tarehe iliyobandikwa kifuani pangu.

Uhuru wenyewe ulianza kunitia mashaka kabla sijauonja. Tulitarajia uhuru ulikuwa mwisho wa kero zote za Mtanganyika, ambaye sasa aliitwa Mtanzania. Tulidhani uhuru ungekuwa mwanzo wa neema na faraja kubwa nchini. Haikuwa hivyo. Nyimbo za hali ngumu ya maisha toka huko uraiani zilitushangaza sana wafungwa. Tulishangaa zaidi pale kasi ya watuhumiwa waliokuwa wakiletwa gerezani ilipoongezeka badala ya kupungua, wengi wakiwa watu wenye makosa ya ovyoovyo yaliyoashiria jambo moja kubwa ‘njaa!’
 
SEHEMU YA 125

huyu kampiga mke wake hadi kumwua kwa kupoteza shilingi mia! Yule kafungwa kwa kuiba kuku wa jirani. Na Yule? Yeye alitupa kitoto kichanga jalalani!
Kasi hiyo, ilifanya selo zifurike, tuanze kulala ‘mzungu wa nne’. Huyu aliweka kichwa huku yule kule. Chakula kiliongezeka ubaya, hata hewa katika selo ilibadilika na kuwa nzito kutokana na kutumiwa na watu wengi kuliko ilivyokusudiwa.
Nadhani ni hali hiyo iliyoibua tatizo jingine zito zaidi, ‘maradhi.’ Zamani kidogo ugonjwa mkubwa gerezani ulikuwa malaria. Mara yaliingia maradhi mapya ya kipindupindu. Ugonjwa hatari wa kuharisha ambao ulimchukua binadamu siku mbili tu kupoteza maisha.
Wafungwa wengi walipoteza maisha, kutwa watu sita au zaidi hadi ulipodhibitiwa kwa vidonge vya kufunga tumbo. Tuliambiwa ugonjwa huu hatari chanzo chake kilikuwa uchafu. Lakini kutokana na shida ya maji gerezani humo, naamin tuliobakia hai ilikuwa kwa kudra za Mwenyezi Mungu zaidi ya jitihada kujikinga.
Habari za kipindupindu humo nje ya gereza pia zilivuma sana. Dar es salaam, Dodoma, Singida na kwingineko kipindupindu kiliteketeza maisha ya watu kama watu wa kusini wanavyoshambulia ‘dagaa nchanga’ au Wahaya wanavyowaonea ‘nsenene’. Sikuelewa hata kidogo kila nilipofikiria hilo. Watanzania tuteketee kwa uchafu kwa ajili ya uhaba wa maji! Nchi ambayo imezungukwa na maji kila upande, ikajaliwa mito, maziwa, mabwawa na chemchemi tele! Kwa kweli sikuweza kuelewa.
Wakati bado natafakari hilo, likaja jingine la kutisha zaidi, UKIMWI. Ugonjwa ambao wataalamu walidai kuwa



ulitokana na wadudu wanaoitwa HIV ambao hushambulia chembechembe nyeupe ambazo ni kinga ya mwili wa binadamu na kumwacha wazi kwa ugonjwa wowote kumtia mweleka wa mwisho. Niliwaona baadhi ya wafungwa wenye UKIMWI. Wanatisha kuliko chochote kile ulichopata kukiona. Nywele zao zilinyonyoka, mwili kuota mapele huku tumbo likiwa halina uwezo wa kuhifadhi chochote kutokana na kuharisha. Kama kipindupindu kiliogopwa kwa kuua haraka UKIMWI uliogopwa zaidi kwa kuchelewesha sana kumwua mteja wake huku ukimpa kila aina ya mateso.
Wajuzi wa masuala ya tiba walitueleza kuwa njia kubwa zaidi ya maambukizi ya UKIMWI ni katika kujamiiana bila kutumia kinga. Jambo ambalo mtu yeyote angeweza kulielewa mara moja na kujiepusha nalo. Lakini taarifa ya tatizo hilo huko nje lilikuwa kubwa na la kutisha kupita kiasi. Haikupita siku mbili bila kumsikia mfungwa mmoja wapo akiangua kilio. Kisa? Kafiwa na mdogo wake, mtoto wake, mke wake au rafiki yake. Taarifa za wasichana kujiuza katika majumba ya starehe, akina baba wenye pesa kuwarubuni wanafunzi, kuzagaa kwa mabaa na sehemu za starehe mitaani na vishawishi tele vya anasa ziliendelea kutufikia gerezani humo kwa kiwango kilekile cha kukua kwa kasi ya UKIMWI. Hali iliyoashiria kitu kimoja tu, hali ngumu maisha. Kwa lugha nyepesi; njaa!
Wakati huo tarehe yangu ya kumaliza kifungo ilizidi kukaribia. Siyo siri kwamba nilianza kuyaogopa maisha ya huko uraiani zaidi ya gerezani. Kama mazingira ya gerezani humo yangeweza kuboreshwa kidogo tu siyo siri, ningefikiria suala la kubaki gerezani humo wa makini zaidi.

21
Ben R. Mtobwa











YA ISHIRINI NA MOJA

Mfungwa Mikono Musoma


W
anahistoria wanatukumbusha kuwa adhabu ya kifungo, ambayo mimi na wenzangu gerezani humu tulikuwa tukiitumikia,
ilianzishwa huko Ulaya yapata miaka 300 iliyopita.
Awali ya hapo mhalifu, au mtuhumiwa aliyepatikana na hatia ama alinyongwa ama alitoswa baharini au kuachwa katika visiwa vya mbali visivyo na watu.
Hapa Afrika pia tulikuwa na adhabu zetu mbalimbali. Mhalifu alilazimishwa kutoa baadhi ya mali zake kama adhabu, kutengwa na jamii yake hata kufukuzwa kijijini. Wakati mwingine alitungiwa nyimbo za mafumbo ambazo ziliimbwa katika sherehe na hivyo kumdhalilisha sana mbele ya jamii. Hali hiyo ilipunguza sana tabia ya uhalifu.
Hivyo, wageni walipoingia na kutushawishi kufuata dini na tamaduni zao kwa upande mmoja, upande wa pili walitushurutisha kutii sheria na adhabu zao. Moja ya adhabu hizo ni hili la gereza. Unakamatwa na mtu anayeitwa polisi, unapelekwa kwa mtu anayeitwa hakimu, kufumba na kufumbua uko mikononi mwa bwana magereza; ukifanya kazi ambazo hulipwi na kupewa chakula ambacho hushibi.
Ni katika hali hiyo tuliposhangazwa siku moja alipoletwa​
 
Back
Top Bottom