Simulizi ya Kijasusi: Noti Bandia

Simulizi ya Kijasusi: Noti Bandia

SEHEMU YA 42 & 43


"Pole sana bosi wangu, naona kikao kilikuwa kirefu kupita maelezo", alisema, mama huyu askari mwenye cheo cha Staff Sajenti, lakini aliheshimiwa sana kutokana na utendaji kazi wake uliotukuka.

"Ndiyo mambo ya kazi. Sikiliza Linnah, naomba nisaidie kazi moja muhimu sana, niitie Sajenti Peter Twite aje ofisini kwangu haraka, ikiwezekana aingie kwa siri. mtu zaidi yako asijue", niliagiza halafu nikaingia ofisini kwangu.

Nilipanga kumtumia Peter kufanya kazi maalumu, kazi ya kimafia, ambayo ingetusaidia kumaliza jambo hili haraka. Baada ya muda mfupi Peter aliingia ofisini kwangu.

"Jambo Afande?" alinisalimia.

"Jambo. Habari ya toka usiku wa jana, Peter ujumbe wako ulinisaidia sana, maana sikujua lolote litatokea, sijui ingekuwaje?", nilimuuliza.

Peter akatumia muda huo kueleza mambo yalivyokuwa uwanja wa ndege, akaeleza jinsi alifika uwanja wa Julius Nyerere kwa ajili ya kunipokea, uwanja wa ndege alikutana na watu ambao aliwatilia shaka, kutokana na uzoefu wake wa kazi baada ya kuwawafanyia utafiti alibaini kuwa walikuwa katika mpango wa kumsubiri mtu.

"Ilikuwa vigumu saba kuwabaini, baada ya kutulia na kusoma mazingira ya uwanja wa ndege, nilibaini magari mawili aina ya BMW, moja likiwa limeegeshwa karibu kabisa na sehemu ya kutokea abiria na lingine liliegeshwa sehemu ya kutokea magari. Ulipoanza kutoka wewe watu wawili walilikimbilia gari la mbele, ambalo lilianza kuondoka, lingine likasuri gari ulilopanda liondoke ndipo wao walifuate gari hilo kwa nyuma. Haraka nikakutumia ujumbe wa tahadhari".

"Ama kweli ulifanya kazi ya ziada, sikuwa na mashaka kabisa, bila wewe pengine siku ya leo ingekuwa ya maombolezo kwangu, asante Peter", nilimshika mkono.

"Usijali mkuu, haya ni matunda yako, kumbuka wewe ndiye uliyenifundisha haya, ulinifundisha jinsi ya kunusa harufu mfano wa mbwa, Nikushukuru kwa kunifikisha hapa", alisema Pete.

"Tuachene na hilo, sasa nataka ufanye kazi moja ya muhimu sana, nimemwambia Mzee Emilly kuwa mapambano yameanza, ni mapambano makali ambayo yafaa tuyapigane sasa, hakuna jinsi, kazi yako tafuta vijana watano, wawe raia wa kawaida tu, lakini waendesha bodaboda jijini, ingia nao mkataba, lakini wapatie pamit na alama ili wasisumbuliwe na migambo. Pikipiki zao waziegeshe kwenye barabara kubwa tano za jiji. Yaani Morogoro road, Ali Hassan Mwinyi, Nyerere road, Kilwa road na Bibi Titi Mohamed, ukimaliza hilo tuwasiliane nitakuelekeza kazi nyingine", niliagiza.

"Nitalifanya hilo haraka sana bosi", alisema Peter.

"Ok, usikose kunijulisha, kumbuka kuwafahamisha kuhusu matumizi ya pikipiki hizo, maana tumepanga kuwatumia wao katika kazi fulani, isifike wakati wakatushangaa, kazi kwako".

Niliwasiliana na Luteni Claud Mwita kumuuliza kama uwepo wake eneo hilo umebaini nini akanidokeza kuwa watu ni wengi, pamoja na kufanikiwa kufahamiana na Sajenti Julius Nyawaminza, wameimalisha ulinzi katika eneo hilo.

Simba, Nyati na Chui, wao walikuwa eneo hilo wakitembea hatua kadhaa kwenda upande mwingine na kurejea kwenye pointi huku silaha zao ndogo, zikiwa tayari zimeondolewa usalama. Risasi zikiwa chemba tayari kwa lolote.

Baada ya kupanga mipango yangu, niliyoofanya kimya kimya, nilifungua mkoba wangu mdogo, nikatoa kamba niliyoinunua Kariakoo. Ilikaribia kuwa saa moja ya usiku, giza lilianza kuifukuza nuru, niliwasiliana na wenzangu. Claud Mwita, Julius Nyawaminza na Fred Libaba nikawaomba tuonane kwenye Mghahawa wa YWCA uliopo hapo Posta Mpya kwa ajili ya chakula cha jioni.

Pamoja na kwamba Mghahawa huu uko karibu kabisa na kituo cha Daladala cha Posta Mpya, wengi hawakupajua, lakini pia niliwahadharisha wenzangu kuwa makini. Nilishauri kila mmoja achukua chakula na atumie meza tofauti, baada ya hapo tutakuwa na mazungumzo yetu binafsi nje ya eneo hilo.

Taratibu nilifungua mlango wa ofisi yangu nikachungulia kwa nje, nilitafuta sehemu ya siri nikazificha funguo za gari, halafu nikawasiliana na David, mmoja wa vijana wanaofanya kazi karibu yangu, nikamfahamisha mahali nilikohifadhi funguo hizo ili azichukue na kuipeleka gari kwa aliyeniazima, rafiki yangu Edgar.

Hapakuwa na dalili yoyote ya kuwa na mtu, hata Linnah alikuwa ametoka na kufunga ofisi yake, nilitoka haraka na kuivamia lifti iliyonishusha ghorofa ya kwanza. Nilitembea haraka hadi kwenye maegesho ya magari, sikutaka kupoteza muda, nilichungulia upande wa pili lilipo jengo la ofisi za benki ya CRDB. Baada ya kujiridhisha kuwa hakukuwa na mlinzi eneo hilo wakati huo, nikairejesha kamba yangu kwenye mkoba, baada ya kujiridhisha kuwa hakuna kikwazo cha kunisumbua.
 
SEHEMU YA 44 & 45

Niliangalia nyuma na upande wangu wa kulia na kushoto, sikumuona mtu, lakini kwa vile jengo hili linalindwa kwa kamera maalumu za usalama, nililazimika kufanya jambo moja ili kamera hizo zisinione. Nilisogea kwenye kivuli, nyuma ya magari kadhaa yaliyoegeshwa hapa, nikatumia nafasi hiyo kujirusha chini, upande wa jengo la CRDB. Haikuwa shida kwangu kuruka sehemu kama hiyo.

Lango la kutokea bado lilikuwa wazi na kwa vile kuna ofisi zingine juu ya ghorofa hili, nilitoka na kuwapita walinzi na baadhi ya askari polisi waliokuwa kwenye kibanda chao cha ulinzi. Nielekea shell ya Gapco, nikakavuka barabara na kuingia YWCA, Wenzangu wote walikuwa wamefika na tayari walikuwa wamepata chakula.

Tulisalimiana na kupeana ishara, kwa vile Mghahawa huu ni wa kujihudumia mwenyewe, na njaa ilikuwa karibu iniue nilielekea kwenye dirisha la huduma, nikaagiza chakula, ambacho nilikula haraka haraka, ili kwenda sawa na wenzangu, ambao kila mmoja alikuwa na hamsini zake.

Wakati huo Carlos Dimera alikuwa akiwasiliana na wakala wa kusafirisha mizigo kutoka Bogota, nchini Corombia, wakala akimjulisha kuwa baada ya masaa ishirini na nne mzigo huo ambao ni dawa za kulevya, utakuwa umewasili kwenye uwanja wa ndege wa Julius Nyerere, Dar es Salaam.

"Tunahitaji maelezo kutoka kwenu, hivi tunavyoongea hapa shehena ya dawa za kulevya imetua salama katika uwanja wa ndege Addis Ababa, nchini Ethiopia. Tumelazimika kupitishia mzigo nchini Ethiopia badala ya Ouagadougou, nchini Burkina Faso kama ilivyokuwa awali kwa sababu za usalama, taratibu zote za mzigo kuondoka Ethiopia kesho zimekamilika, kazi kwenu, vipi hali ya usalama huko?", Carlos Dimera aliulizwa.

"Dar es Salaam, Tanzania hali si mbaya sana, japokuwa kuna mawingu na mvua za hapa na pale, lakini haziwezi kutuzuia kuendelea na majukumu yetu. Kuna wingu moja limetanda angani kuashiria mvua, lakini wataalamu wa hali ya hewa hapa Tanzania wanasema wingu hilo halina madhara, waganga wako kazini kuhakikisha wingu hilo halidondoshi hata tone moja la maji, kuhusu hali ya uwanja wa ndege wa Dar es Salaam ni nzuri sana, tunausubiri", alieleza Carlos Dimera kwa simu ya mkononi.

"Oke, lakini kuweni makini sana katika jambo hili, nasikia serikali ya Tanzania sasa hailali?."

"Kuhusu hilo ondoa shaka kaka, niko na mtandao unaoeleweka, mtandao wa vijana wa mjini ambao nimewafundisha mbinu za kila aina, hata hili wingu lililotanda angani mwisho wake wa kutanda na kuleta hofu ni leo, wingu hili halitakuwepo tena", alisisitiza Carlos.

Baada ya Carlos Dimera kumaliza kuongea na simu hiyo, aliingiwa na hofu kidogo, alisimama akatembea hatua mbili, halafu akajiuliza maswali kadhaa, akainua simu yake ya mkononi na kuongea na Nombo.

"Uko wapi Mr. Nombo?", alihoji Carlos Dimera.

"Niko katikati ya mji bosi, nimelazimika kuja huku kuongeza nguvu kwa vijana, kazi hii lazima iishe leo bosi, kuna habari mpya?", Nombo alihoji.

"Hakuna habari mpya, isipokuwa wakala wa kusafirisha mizigo anauliza, hatua gani tumefikia, mzigo umewasili salama Addis Ababa, Ethiopia, yamebaki masaa ishirini na nne tu mzigo uwasili Dar es Salaam, na wingu bado limetanda angani, unadhani kuna uwezekano wa kuliondoa?", Carlos Dimera aliuliza.

"Tulia bosi, tumuombe Mungu atasaidia, maana uwezekano ni mkubwa mno, kwa vile hujafika kwenye uwanja wa mapambano, ungeshuhudia adui alivyowekwa kati, hakika jengo lote la Benjamin Mkapa liko chini ya usalama wetu, kila anayetoka na kuingia anaonekana, kuhusu hilo usijali, leo ndiyo mwisho wa wingu hili, labda utokee muujiza gani".

"Niwatakie kazi njema, jitahidini bwana jambo hili liishe mapema leo, vinginevyo nitume kikosi kazi?, hawa jamaa zetu wapo tu wanasubiri kazi kama hizi, mkishindwa semeni", aliuliza Carlos.

"Hakuna sababu, mapambano ya mchana yangeleta shida kidogo, maana watu walikuwa wengi eneo hili, lakini sasa hali iko shwari, hili giza litatusaidia pia. Kunywa, kula ukiamini kuwa kazi hii imekwisha", Nombo alieleza, Carlos akapata faraja na matumaini.

Baada ya sisi wote kupata chakula cha jioni kwenye Mghahawa huu wa YWCA, tulitoka mmoja baada ya mwingine kama tulivyoingia, lakini tukiwa nimewapa ishara ya kukutana sehemu nyingine ambayo tutafanya mazungumzo na kupanga mipango yetu kwa siri.
 
SEHEMU YA 46




Kabla ya kutoka ndani, niliwasiliana na Mama Feka, ili kujua wapi amefika, akanifahamisha kuwa amefika salama Jijini Dar es Salaam. Nilimfahamisha kuwa nitamtafuta kesho, hivyo atafute hoteli itakayomfaa apumzike kwani alikuwa amesafiri kwa muda mrefu.

Wakati tunatoka ndani ya Mghahawa huu wa YWCA, nilisikia kelele za risasi, zilizosikika kutoka upande wa pili, zikafuatiwa na harufu ya baruti. Kwa sisi wazoefu wa mambo ya silaha, mara moja nikahisi jambo. Watu walikimbia kuelekea upande tuliokuwa, ghafla kwa muda mfupi hali ya usalama ilikuwa imetoweka katika eneo la Posta Mpya.

Tuliangaliana na wenzangu, moyo wangu ukaingiwa na hofu, nikahisi jambo la hatari limemtokea David. Tulianza kusogea taratibu eneo la tukio. Nilifungua mkoba wangu nikatoa moja ya kofia zangu za kuficha sura, nikaivaa ili kuficha sehemu ya uso wangu.

"Tukimbie, majambazi yamevamia na kuua watu, mwenyezi mola tusaidie", mama mmoja wa makamo alisikika huku akikimbia kuyanusuru maisha yake.

"Sijawahi kuona unyama kama huu, binadamu kumuua binadamu mwenzao tena mbele ya watu utadhani wanaua mnyama", alieleza mzee mmoja aliyekuwa amelala kwenye mfereji wa barabara ya Azikiwe.

Toyota Carina TI, ambayo David alikuwa akiendesha kutoka kwenye maegesho ya magari ghorofa ya kwanza, ishambuliwa na kuteketezwa vibaya kwa kombora ambalo halikujulikana, David aliuawa katika shambulizi hilo. Waliofanya shambulizi hilo hawakufanya makosa. Nilisikitishwa sana, lakini kwa kiasi fulani nilijiona mwenye bahati, maana kazi yangu sasa ingekuwa rahisi au ngumu zaidi.

Polisi hawakuchelewa kufika eneo la tukio, waandishi wa habari pia waliwasili na kamera zao, mimi na wenzangu Claud Mwita, Julius NYawamizna na Fred Libaba tuliangalia tukio hilo kwa dakika kadhaa tukiwa mbali kiasi, halafu tukapeana ishara ya kuondoka eneo hilo. Hata kama ungekuwa mtaalamu wa hisia kiasi gani hakika usingeweza kubaini ishara zetu, labda uwe mmoja kati yetu.

Kutokana na uzito wa tukio hilo, niliwasiliana na Peter Twite, nikamfahamisha klichotokea, nikamwelekeza mambo ya matatu ya kufanya, afike haraka eneo la tukio na kutoa taarifa kwa Kanali Emilly, ahakikishe majina ya marehemu hayaripotiwi kwenye vyombo vya habari, ofisi anayotoka marehemu iwe siri na mwili wake uhifadhiwe mahali salama mpaka tutakapomaliza kazi.

Baada ya kutoa agizo hilo kwa Twite, tulikubaliana kuonana kwenye Mghahawa wa Chief Pride, uliopo mtaa mdogo wa Chaga, katikati kabisa na barabara za Jamhuri, upande wa kushoto na Libya, upande wa kulia. Tulipanda ngazi hadi ghorofa ya kwanza, hapakuwa na wateja zaidi ya meza na viti. Wakati tunapanda ngazi, muhudumu alitufuata kwa nyuma, tulipoketi akawa tayari kutusikiliza. Tuliagiza vinywaji kila mmoja alichoona kinamfaa.

"Nadhani hapa patatufaa kwa mazungumzo, au mnasemaje bosi?", Fred alihoji baada ya muhudumu wa Mghahawa huu kuondoka.

"Pamoja na kwamba sijaelewa lolote kuhusu kilicho mbele yetu, lakini kwa utulivu huu, nashauri tuifanye sehemu hii iwe kwa ajili ya kukutana tukiwa na dharura. Naamini kazi tuliyoitwa kuifanya itakuwa ngumu, lakini tutashinda", alieleza Claud.

"Sikilizeni, naamini mpaka sasa adui zetu wanasherehekea ushindi wakidhani nimekufa, David ameuawa kinyama, wamemuua wakidhani ni mimi, sasa kabla jua la kesho halizachomoza, yatupasa kufanya kazi ya ziada, kujua wauaji wanapatikana wapi, wanafanya nini? Sababu zilizowasukuma kutushambulia, tukilijua hilo, kazi yetu itakuwa rahisi, tofauti na hapo tutakuwa tunajisumbua kutwanga maji ndani ya kinu", niliwaeleza.

Vinywaji vililetwa mezani, tukaanza kunywa huku kila mmoja akieleza mpango kazi wake. Baada ya kila mmoja kutoa mchango wake huku Fred akijaribu kuweka kumbukumbu ya maandishi, nikakumbuka kuhusu, Carlos Dimera.

"Wakati mwingine linapotokea tukio la kushitua kwa aina hii, akili yangu hulazimika kufanya kazi ya ziada. Fred..., unaweza kumfahamu mzungu mmoja anaitwa, Carlos Dimera?".

"Yaa. Ndiyo, Carlos Dimera namjua, huyu jamaa ndiye tajiri mwenye kile kiwanda cha kutengeneza tembe za malaria, Huyu jamaa anatajwa kuwa mtu safi na mwaminifu kwa serikali, pia anatajwa kuwa mstari wa mbele katika kusaidia jamii, ana nini?", Fred alihoji.

"Yatupasa kumchunguza haraka iwezekanavyo. Nimewahi kusikia minong'ono kuhusu yeye, lakini nisimchumie dhambi, nataka kujua anaishi wapi, anapendelea mambo gani?", nilimuuliza Fred.
 
SEHEMU YA 47

"Huyu Carlos, anaishi Mikocheni A, ukiziacha taa za usalama barabarani za Morocco, barabara ya kwanza kabisa ingia kulia, nimewahi kuonyeshwa na rafiki yangu mmoja Inspekta wa polisi. Anasema walikwenda kupokea msaada wa Pikipiki kumi za kuwasaidia polisi kufanya doria, ndipo nilipobaini kuwa ni mtu safi. Ni matajiri wachache sana wenye moyo wa kusaidia suala la usalama wa raia", alifafanua Fred.

"Siyo sababu, yafaa achunguzwe, na kazi hii lazima tuifanye usiku huu, huyu jamaa kwa nyakati fulani, binafsi nilijaribu kufuatilia nyendo zake, sikupata mambo makubwa sana, lakini nilipata mashaka kidogo, sasa nitamfuatilia kwa undani zaidi ili nijiridhishe", nilisema.

"Inspekta Judith, aliyenionyesha nyumbani kwake alinidokeza kuwa wakati anawakabidhi Pikipiki hizo, Carlos mwenyewe aliwaeleza polisi kuwa binafsi anachukia sana vitendo vya uhalifu, akaahidi kutoa magari mawili maalumu kusaidia doria, ndiyo maana najiuliza", Fred alieleza.

"Siyo sababu, wahalifu wana mbinu nyingi, hujaona wachawi walivyo wakarimu, anakufanyia vitendo vya ushirikiana huku akikuonyesha wema. Hata ukielezwa kuwa huyu ndiye mchawi wako huwezi kuamini, kutoa msaada haitoshi kukufanya uwe mwaminifu", Nyawaminza alieleza.

"Hakika", Claud alisapoti.

"Ndugu zangu, Claud na Julius, kwanza poleni kwa safari, niwaombe radhi kwa safari ya kushitukiza, nimelazimika kuwaita ili tusaidiane kupigana vita iliyoko mbele yetu", nilitumia nafasi hiyo kuwaeleza kila jambo, kuanzia wazee walioibiwa kwa mtindo wa noti bandia na jinsi dawa za kulevya zinavyoingizwa nchini na kuchangia kuharibu maisha ya ambani ni nguvu kazi ya taifa na kizazi cha sasa.

"Tuko pamoja".

"Kuanzia sasa, mtaziacha kazi zenu zote, mtayaacha majukumu yenu yote, tukabiliane na jambo hili, si kazi rahisi kama tunavyodhani, kuwakabiri watu hawa ni sawa na kuwa mkononi na tiketi ya kwenda ahera, kwa vile tuliapa kuilinda Jamhuri yetu, hatuna budi kuifanya kazi hii", niliwaambia huku wote wakiniangalia kwa macho makavu.

"Hakuna shaka kuhusu hilo Kamanda", alieleza Claud, Julius akatikisa kichwa kuunga mkono.

Nikatumia nafasi hiyo pia kuwaeleza wenzangu kuhusu ujio wa shemeji yangu Mama Feka, nikawaeleza nilivyopanga kumtumia mwana mama huyu.

"Ataweza?", alihoji Nyawaminza huku akicheka.

"Naamini ataweza, Mama Feka ni mmoja kati ya wanamke jasiri sana", niliwahakikishia, halafu nikamgeukia Fred, "Sikiliza Fred, hawa jamaa watafutie mahali pa kulala leo, kuanzia kesho hatutakuwa na muda wa kulala, lakini iwe maeneo ya Sinza, Kinondoni au hata Kijitonyama, mimi nitakwenda nyumbani kwangu wakati huu, kuna vifaa vyangu vya kazi nitachukua halafu nitamtafuta Carlos, hata wewe pumzika maana kesho utakuwa na kazi nyingi zaidi".

"Asante", Fred alishukuru.

"Angalizo, jambo hili bado ni siri, pale ofisini hakuna anayejua mpango huu zaidi ya Mzee Emilly, Twite na wewe Fred, hatuna sababu ya mtu mwingine kujua, ndiyo sababu ya kuwaita hawa jamaa, Claud na Nyawaminza. Of rekodi", nilionya.

"Nimekusoma", alieleza Fred.

"Fred, wakati unakwenda kulala, hakikisha unapata ratiba ya huyu Carlos, ujuwe ni mtu wa aina gani, anapenda nini, ana msimamo gani, nani rafiki zake wa karibu na hiki kiwanda chake kinakidhi haja? tumia akili zaidi kuliko nguvu".

Wakati huo kulikuwa na sherehe kubwa nyumbani kwa Carlos Dimera, vinywaji vya kila aina vilikuwa mezani, nyama za kila aina zilitafunwa, muziki laini ukipenya katika masikio ya watu hawa, kila mmoja akiyatafakari maisha baada ya kazi nzito.

"Umefanya kazi nzuri sana Nombo, kuanzia sasa mshahara wako unaongezwa mara mbili zaidi, lakini hata, Simba, Nyati na Chui pia posho zenu zimeongezwa, mmefanya kazi nzuri sana. Kumfuatilia adui kuanzia usiku wa jana, leo asubuhi, mpaka jioni mnamaliza kazi ni jambo kubwa mmefanya. Kuondoka kwa mbwa huyo ni ushindi kwetu", Carlos Dimera alieleza.

"Wakati mwingine lazima ujifanye kama mwendawazimu ili kazi yako iwe nzuri. Nguvu ya Nombo kwenye uwanja wa mapambano imesaidia sana, milango yote ya kuingia na kutoka ilikuwa chini yetu, tulisubiri mpaka mwisho, alipotoka tu akakutana na kifo, wakati ndugu zake wakiomboleza sisi tunakula raha", Nyati alieleza.
 
SEHEMU YA 48


"Sasa ni wakati wa kula na kunywa, kazi yenu imenifurahisha sana, sina budi kuwaambia nawapenda sana, shehena kubwa ya dawa za kulevya yenye utajiri, itaingia Dar es Salaam, kesho alasiri, taratibu zote za kupokea mzigo huo zimefanyika, kunyweni lakini msilewe", Carlos alishauri. Wakaendelea kunywa huku wengine wakicheza muziki.

Wakaendelea kula, kunywa na kucheza muziki

Ilikaribia kuwa saa sita na nusu za usiku, niliposhuka kwenye taksi iliyonitoa katikati ya mji, nilipenya uchochoroni, nikapita nyuma ya Kanisa la KKKT, lililopo Kijitonyama, nikaambaa na ukuta wa kanisa hili nikaibukia kwenye barabara ya vumbi inayoelekea nyumbani kwangu. Nilitembea haraka haraka, nilipoufikia mti ulio karibu na nyumba yangu nikasimama na kuufanya kuwa ngao yangu.

Eneo hili lilikuwa kimya kabisa, ni nyumba yangu pekee iliyokuwa katika hali ya giza. Hii ilitokana na familia yangu kutokuwepo. Baada ya kujiridhisha kuwa hali ilikuwa shwari, nilinyata mfano wa paka, nilipoufikia ukuta wa nyumba, nilitoa funguo za mlango wa siri ulioko nyuma ya ya nyumba, nikaufungua taratibu, nikaurejesha kama ulivyokuwa, nikasubiri kwa sekunde kadhaa halafu nikasogea na kuingia.

Kwa vile hali ya usalama haikuwa nzuri, familia yangu niliihamishia sehemu nyingine, nilitumia nafasi hiyo kukagua usalama wa eneo la nyumba yangu, nilipohakikisha kuwa hakuna dalili zozote za hatari, nikauendea mlango wa nyumba, nikaufungua kwa tahadhari nkajitosa ndani.

Ndani ya Nyumba hii kulikuwa kumepekuliwa sana, kabati ya nguo iliyoko chumbani kwangu ilikuwa imepekuliwa na baadhi ya nguo na vitu vyangu vingine kuachwa bila kuvirejesha mahali pake. Nadhani waliamua kuviacha hivi baada ya kujiridhisha kuwa waliniua katika shambulizi la Posta kwa hiyo waliamini kuwa siko tena duniani. Lakini walikosea jambo moja. Hakuhakikisha nani alikuwa akiendesha gari lile walilolishambulia.

Kiasi fulani nilicheka mwenyewe, maana nilijua sasa kazi imeanza, niliyakumbuka maneno ya Rais wa kwanza wa Tanzania, Hayati Mwalimu Julius Nyerere, alipokuwa akitangaza vita dhidi ya majeshi dhalimu ya Ndul Iddi Amin Dada wa Uganda. Kilichonisisimua zaidi ni pale Mwalimu aliposema, 'RAFIKI ZETU WALIOKUWA WANASEMA MWALIMU ACHA, SASA WAKAE PEMBENI, WATUPISHE, MAANA HATUTAWASIKILIZA TENA, ILI SASA UBISHI UISHE'.

Maneno haya ya Mwalimu Nyerere yaliniongezea hamasa, nililiendea kabati langu maalumu lenye dhana zangu muhimu za kazi, kabati hili lilikuwa sehemu ya siri, nikalifungua kabati hilo lililoko ukutani, nikatoa fulana mbili maalumu zisizopenya risasi (bletproof), nikazihifadhi vizuri kwenye mkoba wangu, halafu nikatoa bastola mbili aina ya M9 zisizotoa sauti, zote zikiwa zimejazwa risasi kumi na mbili kila moja kwenye magazini zake, nikazifutika kwenye mapaja yangu, moja kulia na nyingine kushoto. Nikatoa magazini zingine nne zenye risasi za ziada, mkasi wa kukata vyuma na kisu kidogo nikaviweka kwenye mkoba wangu.

Kichwa changu kilijawa na mambo mengi, nilijiuliza hili na lile, nikishika hili na lile. Niliwakumbuka wenzangu, Luteni Claud Mwita, Fred Libaba na Julius Nyawaminza, moyo wangu ukajawa na matumaini ya ushindi. Maana kila mmoja alikuwa na hamasa ya kuingia kwenye uwanja wa mapambano.

Baada ya kutoa vifaa hivyo, nilirudi hatua moja nyuma, nikasimama nikitafakari nini kingine kitanisaidia zaidi katika mapambano na watu hawa, nikaikumbuka ngazi yangu ambayo mimi huitumia kupanda au kushuka kwenye majengo makubwa. Pamoja na kwamba nilikuwa na kamba maalumu niliyoinunua Kariakoo kwa ajili ya kazi hiyo, nikalazimika pia kuichukua ngazi. Usidhani ni mzigo mkubwa, ilikuwa ngazi ya kisasa kabisa, unaweza kuiweka hata kwenye mkoba wako na mtu asijuwe ulichobeba.

Sasa nilikuwa tayari kwa mapambano na watu hawa, nilipiga magoti chini nikamuomba mungu wangu, nikawaomba bibi na babu zangu ili wanisaidie. Nikayakumbuka maneno mazuri ya waswahili, 'AKUANZAE MMALIZE' nikaapa kufa au kupona. Ama zangu ama zao.

Baada ya kupiga maombi, nilitoka ndani ya nyumba yangu na kuacha kila kitu kama nilivyokikuta, Hasira na woga vyote vilikuwa ndani ya nafsi yangu, nikajiuliza iwapo nitaishia njiani katika vita hivi nani atakuja kuviendeleza. Imani ikanijia kuwa iko siku atapatikana kijana mkeleketwa wa atakayewasha moto na kuendeleza mapambano hadi kieleweke.
 
SEHEMU YA 49


Saa yangu ya mkononi ilinieleza kuwa ni saa nane kasoro dakika chache usiku, nilipenya kwenye uchochoro nikatokea Chuo cha Ustawi wa Jamii, eneo hili lilikuwa na wasichana kadhaa wanaouza miili yao, waliponiona walinigombea, lakini mimi sikuwajali, niliwapita kimya kimya nikatafuta taksi iliyonishusha karbu na taa za usalama barabarani za Morocco.

Muda huu magari yalikuwa machache barabarani, baada ya kushuka kwenye taksi iliyonileta, nilitembea haraka kurudi nyuma, kama Fred alivyokuwa amenielekeza, nilianza kuhesabu nyumba moja baada ya nyingine, nikiitafuta nyumba ya Carlos Dimera, hatmaye nikaiona.

Eneo hili lilikuwa limezungukwa na miti mingi, kwa vile nilikuwa nimevaa nguo nyeusi, nililipita geti kuu la kuingilia ndani. Nilifanya hivi ili kuona kama kulikuwa na mtu yeyote eneo hilo. Baada ya kujiridhisha nilirudi nikinyata taratibu na kwa tahadhari kubwa, nikauparamia mti uliokuwa karibu na ukuta, nikatulia juu kwa sekunde kadhaa, nikiangalia ndani ya ngome hii. Nilipoona hali ni shwari niliifungua ngazi yangu, nikaifunga juu, halafu nikashuka taratibu kwa hadhari, hatimaye nikajitosa ndani.

Mwanga mkali wa taa ulilifanya eneo hili kuwa la usalama wa kutosha, muziki laini ulisikika ndani ya jengo lililokuwa mbele yangu. Nililala kifudifudi, nikakuloo hadi nyuma ya dirisha lililokuwa na kelele ya muziki, nikautumia mti mkubwa uliokuwa eneo hili kujikinga ili nisionekane.

Chumba hiki kilikuwa kimejaa watu, Carlos Dimera alikuwa ameketi juu ya kiti kikubwa, huku wasichana wawili warembo wakifanya kazi ya kumpepea asipate jasho, vijana kadhaa walikuwa wakicheza muziki, huku wengine wakipata vinywaji.

"Jamani, makamanda wangu, mmeinjoi hamjainjoi?" Carlos aliwauliza vijana wake.

"Tumeinjoi sana bosi, tumekunywa, tumekula, tunacheza muziki", walisema.

"Kama nilivyosema, mzigo unaingia usiku, sasa sitaki mlewe, tuna jukumu kubwa mbele yetu, Teacher amekufa sawa, lakini hatujui nani atafanya nini, au siyo jamani?", Carlos Dimera alieleza.

"Hakika, lakini nikutoe hofu bosi, kifo cha Teacher kitasababisha wengine waogope kabisa, ni mtu mwendawazimu ambaye ameona kilichompata mwenzake, halafu aingie kichwa kichwa, itawachukua muda", Nombo alidakia.

"Ndiyo, lakini mnajua wanaweza kujiuliza kwanini Teacher ameshambuliwa na kuuawa kinyama namna ile?", Carlos Dimera aliuliza.

"Maswali lazima yawepo, nakuhakikishia mzigo utaingia na kusambazwa kwa amani kama ilivyokuwa, huyu mshenzi alikuwa kikwazo kikubwa kwetu, kifo chake ni faraja kubwa katika familia yetu", Hawa Msimbazi alieleza.

Nilikaa kimya nikiwasiliza washenzi hawa, nilijiuliza kwanini hawakuweka ulinzi wa aina yoyote katika eneo hili, lakini nikabaini kuwa hofu ya kuvamiwa na mimi ilikuwa imewatoka baada ya kubaini kuwa niliuawa katika shambulizi lile.

"Kanali Emilly ameagiza lazima wwatu hawa akamatwe wakiwa na ushahidi, vinginevyo tutakuwa tumefanya kazi ya bure", nilijisemea mwenyewe, maana bila hivyo walikuwa katika himaya yangu, ningewaita wenzangu tukawatia mikononi, lakini tutakuwa tumefanya kazi ya bure.

"Wakala anasubiri taarifa kutoka kwangu ili mzigo uondoke Addis Ababa, Ethiopia. Hatutaki kufanya makosa, shehena iliyopo stoo ni ndogo, mzigo unaotarajiwa kuingia ni mkubwa kiasi cha matumizi ya miezi sita, kazi kwenu, kuingia kwa mzigo huu kutawafanya wote kuuaga umasikini", aliwaeleza Dimera.

"Bosi, tumejipanga vizuri mno, waswahili wanasema kila anayetaka cha uvunguni sharti ainame, maana yangu ni kwamba, kila atakayeonekana kuingilia anga zetu, mauti yatamkuta, Teacher ni mfano wa kuigwa na wenzake", Jakna alifafanua.

"Basi, maneno yenu yamenitia nguvu, Jakna, unajua utaratibu wa kupokea mzigo, panga halafu utanijulisha, nitawasiliana na wakala ili kuwajulisha hali halisi ya Dar es Salaam. Kama ilivyo kawaida yetu, Hawa Msimbazi, utasimamia taratibu za kupokea mzigo. Sitaki mpango wetu huu uferi", alisisitiza.

Walizungumza na kujadili mambo mengi huku nikiwasikiliza, nilimshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha kufika hapa na kusikia upuuzi wao, ilionekana kuwa hofu yao ilikwisha kabisa baada ya kufanya shambulizi lililomuua kijana wetu David.

Dakika kumi zilikuwa zimenitosha kabisa, baada ya kudaka baadhi ya maneno ambayo niliamini yatanisaidia katika kazi yangu, nilijitoa taratibu, nikapita sehemu ile ile ya awali, nikatoa ngazi yangu na kuondoka eneo hili salama usalimini. Nikiamini kuwa habari hizi zitamshangaza sana Fred.
 
SEHEMU YA 50


Baadhi ya maofisa walikuwa wameugeuza uwanja wa ndege kuwa njia ya kupitisha dawa za kulevya. Raymond Keneko, alikuwa Afisa Mwandamizi Kitengo cha Ukaguzi wa mizigo. Kiutendaji ukimuona utaamini kuwa ni mtu makini, mwenye msimamo wa kati, asiyeyumbishwa katika kazi zake. Lakini alikuwa mmoja wa watu hatari, dhaifu waliopenda kupokea zawadi kutoka kwa wafanyabiashara wakubwa, bila kujua kuwa zawadi hizo ni kishawishi.
Ndiyo kwanza Kenoko alikuwa amefikisha umri wa miaka arobaini na saba. Akiwa mmoja wa watumishi wachache wa uwanja wa ndege waliokuwa wakipokea pesa nyingi kutoka kwa mzungu Carlos Dimera, kila wakati mzigo wa dawa za kulevya unapokuwa njiani kuletwa Jijini Dar es Salaam.
Asubuhi hii wakati Kenoko akipata kifungua kinywa nyumbani kwake, alipokea ujumbe kutoka Hawa Msimbazi, ukimjulisha kuwa malighafi za kiwanda cha kutengeneza vidonge vya malaria zilizokuwa zimekwama nchini Ethiopia baada ya kukosa usafiri sasa tayari kuletwa Tanzania. Kutokana na uzito wa ujumbe huo, Raymond Kenoko alilazimika kuacha kila kitu mezani, akafanya maandalizi yake na kuondoka haraka kuelekea kazini.
Mkewe na watoto waliyajua vizuri majukumu yake, hivyo hawakushangazwa na kitendo cha kuacha chakula mezani. Alipofika ofisini, aliwapanga vizuri watu wake, aliweka kila jambo katika mstari, akipita kila idara inayohusika na ukaguzi wa mizigo akiweka mambo sawa. Baada ya kila jambo kuwa limefanikiwa, aliwasiliana na Hawa Msimbazi.
"Nakujulisha kuwa kazi yangu imekwisha, kazi imebaki kwenu dadangu, njia zote za kuingia na kutoka ziko wazi. Mwambie Carlos asihofu, kila idara imejulishwa kuhusu kuingia kwa mzigo huo, bahati nzuri ni kwamba wakuu wa idara zote wamepewa amri kuushughulikia mzigo wenu haraka, wanasubiri mgao wao", Raymond Kenoko alimjulisha Hawa Msimbazi.
"Umesomeka kakangu, Carols mwenyewe amesema malipo yako yataongezwa, kazi unazofanya kwa upande wetu zinastahili nyongeza, mimi kama mwakilishi wake, naahidi kuongeza posho zaidi", alisema na kukakata simu. Kisha aliwasiliana na Carlos Dimera.
"Habari ya asubuhi bosi?", Hawa alimsalimia Carlos.
"Niko salama, una habari gani nzuri?", alihoji Carlos Dimera.
"Habari nzuri ni kwamba Uwanja wa ndege kumeeleweka. Taratibu zimekwenda vizuri, Mr. Raymond anasema kwa upande wao hakuna shaka, kazi imebaki kwetu, tena amenihakikishia kuwa idara zote zinazohusika kupokea mizigo zimejulishwa kuhusu kuingia kwa mzigo huo, hali ni shwari".
"Nimekupata Condeliza Rise, maana hauna tofauti kabisa na mwana mama wenye jina hilo, kazi alizofanya akiwa Waziri wa Mambo ya Nje Marekani, zilitosha kumfanya awe kivutio kwa wanawake wenzake duniani. Ngoja niwasiliane na wakala ili mzigo usafirishwe kwa ndege ya usiku leo.
"Fanya hivyo bosi, kilichonisisimua zaidi ni kwamba, huyu Raymond ambaye ndiye Afisa mkaguzi, anasema njia ziko wazi".
"Asante Hawa, wapange watu wako vizuri mkaupokee mzigo huo, sitaki kusikia jambo baya limewakuta", Carlos alibainisha.
"Tuko tayari kwa mapokezi na kwa lolote, napata faraja kwamba, Raymond amesema hali ni nzuri kuliko wakati wote, hususan baada ya Waziri aliyekuwa akiwafuatilia na kuweka kamera za CCTV uwanjani hapo kuhamishiwa wizara nyingine, hii imetuongezea nguvu na matumaini", Hawa alisema.
"Oke, niwatakie kazi njema na mapokezi mema, lakini tuwasiliane, kila hatua mtakayokuwa mnijulishe, lolote laweza kutokea", Carlos alieleza wasiwasi wake.
"Ni kweli bosi. Tutakujulisha", aliongeza Hawa Msimbazi. Baada ya Carlos kuongea na Hawa. Alifanya mawasiliano ya mwisho na wakala.
"Habari ya asubuhi kaka?", Carlos Dimera alisalimia.
"Huko Tanzania ni asubuhi, Addis Ababa ni mchana, tunakula chakula, leta taarifa?".
"Ndio maana nikakupigia. Najulisha kuwa hali ya Dar es Salaam ni shwari kabisa, vijana wako tayari kupokea mzigo, kulikuwa na mvua za rasharasha na mawingu ya hapa na pale, lakini sasa yamedhibitiwa, itakuwa vizuri mzigo ukiingia Dar es Salaam leo usiku. Hali ni nzuri", Carlos Dimera alieleza.
"Mzigo uko tayari, kilichokuwa kikisubiliwa ni taarifa za awali kutoka kwenu, hata hivyo Mamlaka za usalama nchini hapa Ethiopia zilianza kuhoji kuwepo kwa mzigo huu, lakinimaofisa wetu makao makuu Bogota, Colombia waliwasiliana na mamlaka za hapa na kuzijulisha kuwa mzigo huu unaopita, naamini utaingia leo Dar es Salaam", alieleza wakala.
"Asante na samahani kwa kuchelewa kutoa taarifa za awali, hii imetokana na hali ya usalama nchini Tanzania kuwa si ya kuaminika wakati huu, kiasi fulani mambo hayaeleweki. Serikali ya sasa haitabiriki, kwa kuwa mipango imekaa vizuri sasa tuko tayari kupokea mzigo, ambao utawafanya vijana wengi wa nchi hii kupoteza mwelekeo baada wakivuta dawa hizi za kulevya", Carlos alieleza na kukata simu.

ITAENDELEA
 
SEHEMU YA 51

Ndio kwanza nilikuwa nimeamka kutoka usingizini, kuchelewa kwangu kuamka si kwamba mimi ni mtu mvivu, la hasha, hali hii ilitokana na mimi kuchelewa kulala usiku kutokana na kazi nilizofanya. Kama wewe ni binadamu mwenye huruma, utaona ni jinsi gani mimi nilistahiri kulala mpaka muda huu.
Ilinilazimu kulala KB Hoteli iliyoko Mabibo ili asubuhi niweze kuonana na shemeji yangu Mama Feka, ambaye pia alifikia katika hoteli hii. Kilichonitoa usingizini ni kelele ya mwito wa simu iliyopigwa na Peter TWite, Vinginevyo ningeendelea kuuchapa usingizi, nilijivuta taratibu na kupokea simu.
"Jambo Mkuu", sauti ya Peter ilipenya masikioni mwangu.
"Oh Peter, Jambo. Habari ya asubuhi".
"Habari nzuri mkuu, nakujulisha kazi uliyonituma, vijana wako kwenye pointi kama ulivyoshauri, kuwatambua kila mmoja amevaa fulana na kofia nyeusi za NSSF. Ili kuepusha usumbufu, nimewajulisha wavae kofia ziangalie nyuma, maana anaweza kutokea mtu mwingine amevaa vile ikawa shida", Peter alieleza.
"Asante Peter, kama nilivyokufahamisha, usishughulike na jambo lolote mpaka nitakapokujulisha, usizime simu, usiwe mbali na eneo lako, kuna kazi moja itabidi uifanye majira ya saa tisa alasiri hivi. Usiniangushe", nilisisitiza.
"Siwezi, siwezi kabisa kukuangusha mkuu. Utakapokuwa tayari kunituma kazi yoyote utanifahamisha, nafahamu wakati tuliomo bosi, niamini tafadhali".
"Usijali Peter, wewe endelea mpaka nitakapokujulisha vinginevyo".
"Tuko pamoja".
Niliwasiliana na Luteni Fred Libaba nikamjulisha mahali nilipokuwa, niliagiza awachukue Luteni Claud Mwita na Sajenti Julius Nyawamiza, awalete KB Hoteli chumba namba kumi, floo ya pili. Nikamjulisha kuwa wakifika wanipigie simu. Ningia maliwatoni, nikafanya usafi wa mwili wangu, nilikoga, nikanyoa ndevu na kujiweka vizuri, halafu nikashuka chini kwa ajili ya kifungua kinywa.
Sebastian alikuwa mmoja wa rafiki zangu, kazi yake ilikuwa dereva taksi, alifanya kazi zake sehemu mbalimbali za Jiji la Dar es Salaam. Kijana huyu ndiye aliyenileta hapa usiku, nikamfahamisha pia anifuate saa mbili asubuhi na tayari alikuwa amefika kunichua.
"Umelala saa ngapi Seba?", nilimuuliza.
"Hizi kazi zetu hatuna muda wa kulala, dereva taksi halali kaka, unaposubiri wateja, ndiyo nafasi ya kulala hiyo", alieleza Sebastian.
"Nitakuwa na wageni, nahitaji kutumia gari yako kwa shughuli zangu binafsi. itakuwa siku ya leo na kesho, nitakulipa", nilimwambia.
"Hakuna shaka kaka, funguo za gari hizi hapa, ukimaliza mambo yako utanijulisha, iwe siku mbili, wiki au mwezi".

Baada ya kupata kifungua kinywa, nilisimama, wakati najiandaa kurejea chumbani kwangu, Fred, Claud na Nyawaminza waliingia.
"We Fred, ina maana mlikuwa karibu sana?", nilimuuliza.
"Hata sisi tumelala Mabibo, niliwaambia wenzangu, Teacher asipolala Sinza, basi atalala Mabibo, utabiri wangu umekuwa sahihi", alieleza Fred.
Tulipanda ngazi tukaingia chumba namba kumi, "Karibuni, baada ya kutoka nyumbani kwa Carlos usiku, niliona vyema kulala hapa. shemeji yangu Mama Feka yuko chumba namba nane, kwa kuwa tumekutana wote hapa, ngoja nimwite aje mbele yenu, itakuwa vizuri mkimfahamu", niliwaeleza wote wakatingisha vichwa kukubaliana nami.
Nilisimama kwa sekunde kadhaa nje ya mlango wa chumba namba nane, nilijiuliza maswali kadhaa, ambayo majibu yake yalielekea kunishinda. Nilijiuliza kuhusu kazi ninayotaka kumtuma mwana mama huyu, ni sahihi au namuingia katika matatizo. Hata hivyo nilipiga moyo kinde, nikagonga mlango, akaniruhusu kuingia. Mama Feka alikuwa amevaa kaptula na fulana, zilizomfanya apendeze sana.
 
SEHEMU YA 52

Jasho jingi lilikuwa likimtoka mwilini kwa sababu ya mazoezi, aliponiona akasitisha mazoezi na kunisalimia, "Sema shem wangu, umelala salama?".
"Niko salama kabisa shem, ama kweli wewe ndiye Cnthia Rothrock wa ukweli, nimelala hapa chumba namba kumi, niko na wenzangu, wanahitaji kukuona, ukimaliza mazoezi yako, njoo room namba kumi tuzungumze kidogo", nilimwambia.
"Dakika moja", alisema Mama Feka nikatoka nje na kumwacha akijiandae. Maana vitu vingine vya shemeji sina ruhusa ya kuviona.

"Tumsubiri kidogo, anakuja, alikuwa katika mambo ya kujiweka sawa kiafya", niliwajulisha wenzangu, waliokuwa kimya, wakainua vichwa vyao juu kuonyesha ishara kuwa wamenielewa.

Wakati tunamsubiri Mama Feka, niliona ni vyema nitumie nafasi hii kuwaeleza habari ya usiku. "Fred, niliwahi kukwambia siku zote usiamini maneno ya mtu, wakati tunamsubiri Mama Feka, labda nitumie nafasi hii kukujulisha kuwa Carlos Dimera si binadamu wa kawaida, ni aina ya mnyama tena hatari zaidi ya chui", akanitolea macho na kunishangaa.

"Ehee, imekuwaje bosi, maana kiasi fulani umenishitua?", alihoji Fred kwa shauku kubwa.

"Sikiliza Fred, huyu mzungu rafiki yako, au sijui ni nani kwako, anamiliki kikosi kikubwa cha uhalifu hapa jijini, sasa nakwambia tukifanya mchezo tumekwisha, take care", nilimwambia.

"Si rafiki yangu kabisa, kumbuka nilikwambia habari za huyu mzungu nilielezwa na rafiki yangu mmoja wa polisi, binafsi sijawahi hata kukutanishwa nae", alijitetea.

"Basi elewa hivyo, mimi nilimtilia shaka mapema kabisa, ndiyo maana nimejiridhisha baada ya kufika nyumbani kwake usiku. Huyu mzungu ndiye chanzo cha mambo yote ya uhalifu hapa jijini, sasa nasema ama zake ama zangu, amejiandaa vizuri sana, lakini sisi pia tuko vizuri, au vipi jamani?", niliwauliza wenzangu huku wote wakiniunga mkono.

"Sasa ajiandae kukutana na mkono wa sheria, watu kama hawa siku zao ni arobaini, mwisho wake umetimia, kama ulivyosema, ama zake ama zetu, naamini tutashinda", Julius Nyawaminza alieleza kwa hasira.

Niliwaeleza kila jambo, jinsi nilivyoingia nyumbani kwa Carlos Dimera, hali ya ulinzi ilivyokuwa na mipango yao ya uhalifu waliyokuwa wakipanga. "Walikuwa katika sherehe, eti wakisherehekea kifo changu, cha ajabu hawakuweka ulinzi wa aina kabisa, wameamini nimekufa, siku wakiniona watatamani ardhi ipasuke".

"Kama ndivyo kwanini tusiwakamate mapema ili kuokoa muda?", Claud alihoji na kuongeza, "Maana kila kitu kiko wazi, sasa sijui tunasubiri nini mkuu?".

"Ni kweli kabisa Claud, kama inawezekana wakamatwe wakati ni huu sasa", Nyawaminza alirukia kuunga mkono maneno ya Claud.

"Hapana, tusikurupuke kufanya jambo ambalo halina tija kwa taifa. Sikilizeni, ingekuwa kazi ni kuwakamata tu, ningewaita hata usiku tukawamata kama kuku, lakini tutakuwa tumefanya kazi ya bure, lazima muelewe kuwa nchi yetu inatawaliwa kwa mjibu wa sheria, huwezi kumtia mtu hatiani bila kuwa na ushahidi. Fred... unadhani inawezekana, haya sawa, tutamfikisha mahakamani kwa kosa lipi?", niliwauliza.

"Hakika bosi, itakuwa vigumu kumkamata mtu bila ushahidi, nashauri tufanye kila njia wakamatwe na ushahidi", alishauri Fred, wote tukamuunga mkono.

"Leo tutafanya kazi moja ndogo, lakini yenye faida kubwa kwetu. Fred jiandae tutakwenda kumkamata mtu mmoja anaitwa Raymond Kenoko, huyu jamaa ni Afisa wa Uwanja wa ndege, Claud na Nyawaminza nitawaelekeza cha kufanya, halafu...", kabla sijaendelea mlango uligongwa, Mama Feka akaingia.

"Habarini za asubuhi", Mama Feka alisalimia.

"Oh, nzuri, nzuri", tulimwitikia kwa pamoja. suluali ya blue na fulana ya njano, alizovaa zilimfanya apendeze sana, aliingia na kusimama mfano wa mtu anayesubiri kupandishwa kizimbani.
 
SEHEMU YA 53



"Pole na safari shem wangu, pole kwa kukukatisha usingizi wako, pole kwa kila nililokukosesha kulifanya asubuhi ya siku ya leo", nilimuomba radhi.

"Usijali shem", Mama Feka alisema kwa mkato huku akitabasamu.

"Jamani, huyu mwana mama ni shemeji yangu kabisa, ametoka Nyamuswa kwa ajili ya kushiriki mahafari ya chuo kikuu huria, lakini kabla hajafika huko chuoni nikamuomba aonane na sisi kwa ajili ya mambo fulani fulani ambayo tutamuomba atusaidie", niliwaeleza wenzangu wakatingisha vichwa.

"Kazi gani tena shem? Mbona unanitisha jamani".

"Usiogope molamu, labda nieleze moja kwa moja utanielewa". Nilitumia nafasi hiyo kuwatambulisha wenzangu kwake ili awafahamu, halafu niliendelea. "Hapa jijini limeibuka kundi moja hatari la wafanyabiashara wa dawa za kulevya, hawa jamaa ndiyo wanauzia watu madini feki kama umewahi kusikia, wanateka watu na kuwapora mali zao mchana na usiku, wanaibia watu kwa mtindo wa noti au dolla bandia, mji umechafuka kwa ajili yao, sasa sisi hatukubaliani nao", nilimwambia.

"Umenikumbusha mbali, mwanangu aliwahi kuibiwa kwa mtindo wa madini feki, wakachukua ada yote ya shule, hao watu ni wauaji kabisa", alieleza Mama Feka.

"Pole, sasa kinara wao yuko hapa ni mzungu, huyu mzungu ndiye anafadhili mambo haya, lakini kumkamata imekuwa ngumu kidogo", nilieleza.

"Kuna ugumu gani shem?, mtu kama huyo si anakamatwa tu jamani, mwanangu alilia sana siku hiyo, alikuja na chupa akidai ameuziwa madini, iliniuma sana jamani, kwa hiyo ulitaka nieleze ilivyokuwa?", aliuliza.

"Hapana shem, kuna jambo moja la msingi sana ambalo tumelijadili na wenzangu kwa muda mrefu, baada ya kutafajari kwa kina, tukaishia kukuchagua wewe utusaidie kufuatilia mambo fulani, ambayo yatatuwezesha kumtia hatia mtu huyo", nilimwambia akacheka.

"Ehe, mnataka mimi nifanye nini?", alihoji.

"Tunataka tukutume ujiingize upande wake iwe rahisi kwetu kumkamata na ushahidi, unasemaje shem?", nilimuuliza.

"Heeee, shem hivi inawezekana mtu akajipeleka mwenyewe jehanam, si hatari hiyo, kwanza mimi nimekuja Dar kwa kazi nyingine, aaah itakuwa ngumu, hivi nitaanzaje kujiingiza huko?", alilalama Mama Feka huku akisimama.

Nilishika kichwa, nikainamisha uso wangu chini, nilianza kutafakari hili na lile nikitafuta majibu lakini nikakosa. Wenzangu, Claud Mwita, Julius Nyawaminza na Fred Libaba nao walikuwa kimya wakiniangalia.

"Keti tafadhali shem". Nilitumia nafasi hiyo kumweleza mambo mengi yanayoweza kumfanya binadamu akaonekana shujaa kwa watu, nilimuomba arejee alipokuwa ameketi. Nikasimama, nilitembea kutoka kona moja ya chumba hiki kwenda upande mwingine.

"Samahani shem, si kusudio langu kukuingiza kwenye moto, kukutuma ujiingize upande ule si kwamba tutakuacha tu, tutakuwekea ulinzi wa hali ya juu, tutakufuatilia wakati wote, kuhusu usalama wako ondoa shaka", nilieleza.

"Sawa, lakini nitaanzaje kujiingiza upande wao, kwanza wataniamini vipi?".

"Tunataka kujaribu kitu kimoja, tumepata taarifa kuwa huyu mzungu Carlos Dimera, anapenda sana wasichana wazuri, kila anapowaona hupagawa, ndiyo maana nikasema kwako itakuwa rahisi atanasa, na akinasa hatutakuacha tu, tutakufuatilia kila hatua utakayokuwa", nilimwambia.

"Mmmm, sasa naanza kukuelewa, unataka nitumie mbinu zangu huyo mzungu Carlos anipende au sivyo?".

"Ndivyo tunavyotaka", Nyawaminza aliyekuwa kimya kwa muda mrefu akitafakari aliongeza.

"Majaribu haya, sina jinsi, niko tayari kuwasaidia sasa natakiwa kufanya nini?".

"Tutakuwezesha kwa pesa na mavazi. Tumepata ratiba kuwa huyu mzungu kila siku lazima afike Msasani Shopaz Plaza kwa ajili ya kununua vitu vidogovidogo vya kula, halafu huenda Seaclif Hoteli, akitoka hapo, hujirusha kwenye muziki, California Dreema. Shem, hakikisha wewe pia unapatikana maeneo hayo, akikuona tu atakushobokea, lakini uwe mwangalifu sana", nilimuasa.
 
SEHEMU YA 54

"Kazi hiyo niachie mimi, nawahakikishia huyu mzungu kwangu atanasa, chezea Cnthia wewe, niko tayari kuanza kazi hiyo", alisema Mama Feka hofu ikiwa imemtoka.

Niliwasiliana na Peter Twite kumjulisha hatua tuliyokuwa, nilitumia nafasi hiyo kumwelekeza ratiba ya kazi atakapokuwa na Mama Feka. Tulimpangia kazi ya kumpeleka sehemu alizopangiwa, yaani Shopaz Plaza, Seaclif Hoteli na California Dreema.

Wakati vyombo vya ulinzi na usalama nchini vikifuatilia kwa makini na karibu matukio ya kutisha ya uhalifu yaliyokuwa yakiendelea Jijini Dar es Salaam. Watu kadhaa walifika vituo vya polisi kutoa maelezo ya jinsi walivyo tapeliwa.

Mfanyabiashara John Roman, afika Kituo Kikuu cha Polisi, Sokoine Drive, baada ya kuibiwa kwa njia ya mtandao, Shaaban Ismail, baada ya kubaini kuwa ameibiwa, alifika haraka kituo cha polisi Oysterbay, ambapo maofisa wa polisi walichukua maelezo yak.

John Roman ni mmiliki wa klabu ya 'Toroka Uje' ambaye aliibiwa pesa nyingi kwa njia ya mtandao. Alifika polisi akionyesha namba za simu za nje zilizotumika kuwasiliana nae na kumfanya atume pesa nyingi, akiwaomba polisi watumie uwezo kuzifuatilia namba hizo.

Akihojiwa na polisi wa zamu waliokuwa kituoni hapo, John Roman alieleza kuwa, awali alipokea ujumbe kutoka Benki ya Maendeleo ya Afrika ADB, ukimweleza kuwa ameteuliwa kuwa mrithi wa Hayati John Bryson wa Uingereza, aliyekuwa na akaunti katika benki hiyo, lakini alifariki dunia na kuacha pesa nyingi..

Maelezo ya John Roman yalimshawishi Afisa wa Polisi kumhamishia chumba maalumu cha mahojiano, afisa huyo alifanya hivyo baada ya kuvutiwa na taarifa hiyo. Alipoingia ndani ya chumba hicho, askari huyo alimtaka bwana John Roman kulielezea vizuri kuhusu tukio hilo.

"Nimekuleta katika chumba hiki ili tuweze kuzungumza kwa uwazi zaidi, tukio hili ni moja ya matukio ya uhalifu yanayotokea karibu kila siku, naomba uanze kueleza toka mwanzo wa tukio hili mpaka sasa, usifiche kitu na usione aibu. Eleza mpaka ulivyofika hapa", Inspekta Judicate alieleza, akijiweka sawa kuandika maelezo yake.

"Ni hadithi ndefu Afande, lakini nitahitahidi kueleza kama ilivyo, naamini polisi mba mbinu zetu ambazo zitasaidia kuwakamata watu hawa. Maana kichwa changu hakifanyi kazi vizuri, nimevurugwa", John Roman alieleza.

"Usijali, maji yakimwagika hayazoleki, lakini maelezo yako yataisaidia polisi katika upelelezi wa tukio hili, cha msingi usifiche jambo", Inspekta Judicate alimhakikishia.

"Asante sana Afande, nakumbuka siku tatu zilizopita nilipokea ujumbe kupitia email yangu, ukiuliza kama mimi ndiye John Roman raia wa Tanzania Bara, nilipojibu ndiyo, nilipokea ujumbe mwingine ukiniuliza nahusika na biashara gani, nilipojibu kuwa namiliki klabu. Hawakutuma ujumbe tena, isipokuwa walinipigia simu wakitumia namba za nje ya nchi", alinyamaza kidogo ili kumeza mate, baada ya kutafakari aliendelea.

"Afande, watu hawa ni wajuzi wa hali ya juu, aliyenipigia simu alijitambulisha kwa majina ya Roggers Peter, akidai kuwa ndiye Mtendaji Mkuu wa Benki ya Maendeleo ya Afrika, ambayo Makao Makuu yake ni Ouagadougou nchini Bukinafaso, Afisa huyu alinieleza kuwa benki imenichagua mimi kuwa mrithi wa mali za marehemu John Bryson, raia wa Uingereza aliyekuwa na pesa nyingi katika benki hiyo, nilipohoji inakuwaje niteuliwe kuwa mrithi wa mali za mtu nisiyemjua, Afisa huyo alinieleza kuwa huo ni mpango wa siri wa benki na kwamba watanitumia nyaraka mbalimbali za marehemu John Bryson, ikiwa
 
SEHEMU YA 55

pamoja na hati ya kifo ili nizitumie kupokea pesa hizo kama urithi alioniachia. Lakini akaniasa kuwa mwaminifu, akidai kuwa kuna dola milioni sita za kimarekani ambazo zitaletwa Tanzania kwa jina langu, nitazipokea uwanja wa ndege, halafu tutagawana", alieleza.

Inspekta Judicate aliyekuwa akiandika maelezo hayo kwa haraka na kwa umakini, aliuliza "Kumbe Makao Makuu ya Benki hii yako Bukinafaso?"

"Hata mimi ndiyo nafahamu hivyo, maana sikuwa na uhakika".

"Oke. Kwa jinsi inavyoelekea ni kweli watu hawa ni wajuzi katika kutenda uhalifu, ehee, ikatokea nini sasa?".

"Nilishawishika kwenda kwenye mtandao, kama unavyojua dunia sasa ni kijiji, sikuchelewa nikaandika neno Mtendaji Mkuu wa ADB, likatokea jina la Roggers Peter, nikaanza kuyaamini maneno ya mtu huyo, baada ya muda nikapokea taarifa na nyaraka mbalimbali za marehemu John Bryson, ikiwa pamoja na hati ya kifo, ikieleza kuwa alifia nchini Uingereza na kuzikwa huko", alinyamaza kidogo kupisha kama kuna swali.

"Hizo nyaraka ulizipokea kwa njia gani?", Inspekta Judicate alihoji.

"Documenti zote za tukio hili zilitumwa kwa njia ya mtandao, na kweli zilikuwa zinaendana na tukio lenyewe, ilifika wakati nikaanza kuwaamini, mimi ni mtu makini sana lakini sijui nilipatwa na jinamizi gani?", alieleza John Roman huku akitoa nyaraka hizo na kuzikabidhi kwa Inspekta Judicate.

Inspekta Judicate alizipitia documenti hizo moja baada ya nyingine, akiziangalia kwa makini, halafu akaziweka kando.

"Ehee, nini kikatokea sasa, maana unanieleza hadithi ambayo hakika ni tamu masikioni mwangu, endelea?".

"Jana asubuhi, nilijulishwa kuwa benki imewatuma maofisa wake wawaili, Mohamed Mussa na Seif Mtigino kusafirisha pesa hizo hadi Dar es Salaam, nilitakiwa kufika uwanja wa ndege saa sita mchana kwa ajili ya kupokea pesa hizo. Kwa kuwa pesa zina mambo mengi, nilimuomba Afisa wa Jeshi la Ulinzi, Kapteni Masey anisimamie kupokea pesa hizo, lakini alinikatalia, akidai kuwa huo ulikuwa utapeli, kiasi fulani nilimlaumu, lakini sasa nimeamini kuwa alikuwa na nia njema", alieleza John Roman.

"Afisa huyo wa Jeshi hakukueleza chochote zaidi ya kusema uache ni utapeli, kama wewe mwenyewe ulivyosema hapa?".

"Afisa huyo yeye alikataa tu, akidai kuwa hao ni matapeli na kwamba hawezi kupoteza muda wake kunipeleka kwa matapeli eti nikatapeliwe, lakini pia alinisihi niachane na mpango huo, lakini sikumwelewa, ndiyo nazinduka usingizini sasa baada ya kuwa tayari nimeibiwa, tena nakumbuka alinieleza kuwa Benki ya Maendeleo ya Afrika ni kwa ajili ya maendeleo ya nchi za Afrika tu, haiwasiliani na mtu mmoja mmoja, pia alieleza kushangazwa na mtindo wa kusafirisha pesa hizo kuja Tanzania, ningemsikiliza hakika nisingekutwa na jambo hili", alieleza machozi yakimtoka.

Inspekta Judicate alikuna kichwa cheke, huku kalamu yake ikiwa mdomoni kwa mshangao, alimwangalia John Romani kwa macho makali. "Kumbe ulipewa darasa la kutosha na bado ukaendeleza ujinga wako, aisee wewe ni kichwa maji kweli, lazima ufahamu kuwa maofisa wa Jeshi wana mbinu nyingi, kama alivyokushauri ungemsikiliza, au ungetoa taarifa kituo chochote cha polisi".

"Ni kweli, hata mimi najiuliza sasa, sijui niliingiwa na tamaa au shetani gani, maana wakati wote mimi ni mtu makini sana", alieleza John Roman.

"Wewe si mtu makini, ungekuwa makini usingekaidi ushauri wa Afisa wa Jeshi", Inspekta Judicate alieleza kwa sauti ya kukatisha tamaa. Alimwangalia John Roman kwa macho yake makali, macho ya mwanamke Afisa wa polisi, aliyewiva katika utendaji kazi wake.
 
SEHEMU YA 56


"Ni kweli Afande, unajua linapotokea jambo kama hili ndiyo mtu unajifunza, kwa kuwa limetokea sina jinsi kujifunza". alieleza John Roman kwa unyenyekevu.

"Ehee, kwa hiyo hizo dola ndiyo zikaletwa Dar es Salaam au ilitokea nini tena?", alihoji Inspekta Judicate kwa shauku.

"Ilipofika saa tano jana, nilipokea simu nyingine kutoka kwa mtu aliyejitambulisha kwa majina ya Mohamed Mussa, akadai kuwa yeye Afisa kutoka ADB, akanijulisha kuwa ndege iliyokuwa ikitoka Bukinafaso kuelekea Dar es Salaam, Nchini Tanzania imepata hitlafu ikiwa angani na kutua kwa dharura katika uwanja wa ndege wa Entebe, Nchini Uganda, hivyo, akashauri nitume haraka dola elfu ishirini za Marekani ili waweze kuondoka Entebe kuja Dar es Salaam, wakidai kuwa visa zao zikiisha kabla ya kufika Dar es Salaam, itabidi warudi tena Bukinafaso, jambo ambalo wao binafsi hawapendi litokee".

"Ukatuma pesa hizo?".

"Mdiyo, ikanilazimu kuwatumia hizo pesa".

"Kwa nini hukuwaambia watumie pesa walizokuwa wakisafirisha kuleta Dar es Salaam. Maana kama ni pesa walikuwa nazo tena nyingi. Dola milioni sita ni pesa nyingi, ni zaidi ya shilingi bilioni kumi za Tanzania, inakuwaje utume pesa?", Inspekta Judicate alihoji.

"Niliwashauri watumie pesa hizo walizokuwa wakisafirisha, lakini wakadai kuwa taratibu za Benki haziruhusu pesa hizo kufunguliwa mpaka zifike sehemu husika, nikawaeleza kuwa mimi ni mlengwa wa pesa hizo, naruhusu zitumike, lakini hawakunielewa, wakadai kuwa zikifunguliwa itakuwa vigumu kupokelewa na wakala wa Dar es Salaam, atakayethibitisha kama pesa hizo zimefika salama Tanzania, ikanilazimu kutuma kiasi hicho haraka iwezekanavyo", alieleza.

"Mama yangu, baada ya kutuma pesa hizo ikatokea nini?", Inspekta Judicate alihoji.

"Baada ya kutuma pesa hizo. Simu zao hazikupatikana, kuanzia ya aliyejiita Mtendaji Mkuu wa ADB, pamoja na maofisa wote waliohusika kunipigia simu, lakini pia nilipotoa taarifa kwa mamlaka zingine ili kuzuia pesa hizo zisichukuliwe, nilikuwa nimechelewa, hali halisi ndiyo hivyo Afande", alieleza John Roman.

"Mmmm, iko kazi, maana inawezekana watu hawa wako hapa hapa Dar es Salaam, naamini pia wanakufahamu, ndiyo maana wakaweza kupata hata namba zako za simu na majina yako, ok, ngoja tujaribu jinsi ya kukusaidia, pia taarifa hii tutaipeleka kwa wenzatu wa usalama ili nao waifanyie kazi", Inspekta Judicate alieleza huku akisimama.

"Nitashukru", John Roman nae alisema huku akimshika mkono wa wakaagana.

Wakati huo, Mama Feka alikuwa amewasili kwenye maegesho ya magari ya Msasani Shopaz Plaza, alifika eneo hili mapema kwa ajili ya kazi moja, kumshawishi Carlos Dimera ampende. Alikuwa ameketi ndani ya gari aina ya Ford Pick Up yenye rangi ya kijani, ambayo vioo vyake vilikuwa vyeusi, hivyo si rahisi kuonekana kwa mtu anayepita nje.
 
SEHEMU YA 57


Aliketi kwenye viti vya nyuma vya gari hii Doble Cabine, huku wakiteta mawili matatu na Peter Twite, aliyemleta hapa. "Cha msingi uwe makini sana na watu hawa, naamini Teacher hawezi kumtuma mtu asiyemwamini, amekuamini ndiyo maana amekutuma katika kazi hii", Peter Twite alimwambia Mama Feka.

"Nitajitahidi sana, naamini siwezi kuwaangusha, sijui kitokee nini, lakini nitajitahidi kupambana, najiamini", Mama Feka alimwambia Peter. Alichukua picha ya Carlos Dimera iliyokuwa kwenye mkoba wake, akaingalia kwa mara ya mwisho, halafu akairejesha mahali ilipokuwa.

"Baadaye", Mama Feka aliaga.

"Kila la heri, usiogope, maana kila utakapokuwa tutakuwepo pia", Peter alieleza, Mama Feka akashuka kwenye gari na kuingia upande wa Supermaket hii kubwa iliyoko Barabara ya Kawe, Dar es Salaam.

Dakika kadhaa baadaye, Carlos Dimera aliwasili eneo hilo, akifuatana na mpambe wake, Jackna, walipoukaribia mlango wa kuingilia ndani, Jackna alikimbia na kuufungua mlango huo, ili Dimera aweze kupita. kama ilivyo kawaida yao, Walipoingia ndani haraka Jackna, alianza kusukuma tololi, akiwa nyuma ya bosi wake, ambaye wakati huo alikuwa akichagua vitu kadhaa anavyopenda kununua katika Supermaket hii.

Mama Feka aliyekuwa upande huo, akitafuta jinsi ya kuwasiliana na watu hawa, alibeba kikapu mkononi, akasogea mpaka kwenye pembe ya mwisho ya Supermaket, mapigo ya moyo yakamwenda mbio, akajiuliza mawili matatu, akapata jibu. Haraka akazunguka upande wa pili, alipofika sehemu ya makutano, hakuchelewa, akamgonga Jackina kama bahati mbaya, vifaa vyake zikamwagika chini.

"Vipi wewe kaka unatembea kama kipofu?", Mama Feka alihoji.

Jackina alihamaki, haraka akainua mkono wake juu ili aushushe katika mashavu ya Mama Feka, lakini Carlos Dimera alikuwa mwepesi akaudaka mkono wa Jackina na kumzuia.

"Jackina, acha bwana, usipende kuwapiga watoto wazuri kama huyu, Mungu aliwaumba ili waupendezeshe ulimwengu", Carlos Dimera alisema huku akitembea taratibu kuelekea kwa Mama Feka. "Pole sana, usijali kwa lililotokea", hakafu akamgeukia Jackina, "Haraka okota vitu vyake, nitamlipia bili". Jackina aliinama na kuokota vitu vilivyokuwa vimemwagika na kuvirejesha katika kikapu.

"Utaongeza nini malkia ili nikulipie bili?", Carlso Dimera alimuuliza Mama Feka aliyekuwa amesimama akiwaangalia kwa hasira.

Alichukua kikapu chake, akatembea hatua mbili, halafua akawageukia na kusema, "Sikiliza kaka, mimi sibabaiki na rangi yako, kwetu si masikini kama unavyodhani, sina shida ya kulipiwa bili, tunajiweza ndiyo maana nikaja hapa, kaa na pesa zako, lakini pia mwambie huyu bwege wako avae miwani ili siku nyingine aweze kuona".

"Shika adabu yako we malaya", Jackina alifoka.

"Malaya ni wewe unayetembea kama kipofu",

"Nyamaza Jackina, mbona hunielewi, usipende kugombana na wasichana", Carlos alimtuliza Jackina huku Mama Feka akiondoka. "Ni msichana mzuri sana", aliongeza Carlos.

"Lakini, anaonekana kuwa hana adabu bosi".

Kama ilivyo kawaida yake, Carlos Dimera, aliwasili katika Hoteli ya Seaclif, ambako hukutana na wageni kutoka nje ya nchi, ambao hufika nchini kwa ajili ya biashara haramu ya dawa za kulevya. Mara hii alifika hapa ili kuonana na mtu maarufu sana duniani, mtu ambaye vyombo vya habari vya dunia humtaja karibu kila siku.

Hakuwa mwingine, huyu ni Emilio, mtoto wa Pablo Escoba, aliyekuwa mwanasiasa, mbabe wa dawa za kulevya, raia wa Colombia ambaye historia inaonyesha hakuwa na mfano. Kijana huyu Emilio, alikuwa amewasili nchini kwa ajili ya kuonana na Carlos Dimera. Alimtambua Carlos kama mtu wa karibu, kutokana na historia zao.
 
Back
Top Bottom