Simulizi ya kipelelezi: Idaiwe maiti yangu

Simulizi ya kipelelezi: Idaiwe maiti yangu

FEBIANI BABUYA

JF-Expert Member
Joined
Mar 5, 2022
Posts
1,916
Reaction score
3,850
STORY: IDAIWE MAITI YANGU
MWANDISHI: FEBIANI BABUYA
STORYTELLER: BUX THE STORYTELLER
WHATSAPP: 0621567672
EMAIL: thomasibabuya@gmail.com
AGE: 18+

********************
SEHEMU YA KWANZA
ANZA NAYO................

NDOTO YANGU NDANI YA MSITU WA KUTISHA

MSITU WA MAU, KENYA.

Ndani ya msitu mmoja uliokuwa na miti mirefu iliyoshonana, katikati kabisa ya msitu huo palikuwa na nyumba ndogo ambayo ilijengwa kwa mbao iliyo onekana kabisa kwamba ilikuwa imetelekezwa kwa muda mrefu kama sio mhusika kuijenga kwa ajili ya kazi yake maalumu. Msitu ulikuwa kimya, ni sauti za ndege tu ambazo zilikuwa zikipenya ndani ya eneo hilo tulivu, hakukuwa na upepo uliokuwa unasikika kwa sababu ya maeneo mengi kushonana kiasi kwamba ilikuwa ni ngumu upepo kupenya mpaka chini.

Kwenye nyumba ambayo ilitelekezwa hilo eneo kulikuwa na watu kadhaa ambao walikuwa wamevaa nguo za jeshi. Ndani kabisa ya hiyo nyumba kulikuwa na mateka mmoja ambaye alikuwa amefungwa vyema kwa minyororo kwenye mwili wake. Mwili wake ulikuwa umechoka, alikuwa anavuja damu kwenye maeneo mengi ya mwili huku watu kadhaa ambao walikuwa kwenye yale mavazi ya jeshi wakiwa wamelazwa kwenye vitanda nje kidogo ya chumba hicho wakiendelea kuvuja damu.

Ni wachache ambao walikuwa ni wazima wa afya kabisa na wengine ndio ambao walikuwa naye ndani ya hicho chumba bwana huyo aliyekuwa amechakaa kwa kipigo ambacho alikipata. Pembezoni mwa hicho chumba alikuwepo mwanamke mmoja ambaye alikuwa mrembo kwa mwonekano wake japo haukuwa ukiridhisha kutokana na mazingira ambayo alikuwepo na kukosa mahitaji ya mhimu kuuweka mwili wake kwenye hali ya usafi zaidi. Mwanamke yule hakuonekana kupendezeshwa na kilichokuwa kinaendelea ndani ya lile eneo ila hakuwa na namna angeweza kufanya hivyo alitoka kwa hasira na ghadhabu kwenye nje kupunga upepo huku akiwaacha watu wale wafanye kile ambacho walikuwa wamedhamiria kukifanya humo ndani.

Ndani ya hicho chumba walibakia wanaume watatu, wawili walikuwa wamesimama pembezoni wakiwa wameegamia ukuta na mmoja ndiye ambaye alikuwa amesimama mbele ya bwana huyo aliyekuwa amefungwa kwenye kiti. Mwanaume ambaye alikuwa amesimama mbele yake, alivaa mavazi ya jeshi kasoro upande wa juu, kifuani kwake alikuwa amevaa vesti ya rangi nyeusi na kwenye mkono wake alikuwa ameishika sigara ambayo alikuwa anaivuta kwa mbwembwe iliyo changanyikana na gadhabu huku moshi akiwa anampulizia huyo mtu wake usoni.

Alitoa ishara kwa mwanajeshi mmoja, hakusita zaidi ya kulibeba dumu kubwa ambalo lilikuwa pembeni yake, dumu lilijaa mafuta ya petroli ambayo aliyamiminia kwenye mwili wa mwanaume ambaye alikuwa amefungwa kwenye kile kiti kwa umakini bila kumwaga mwaga hovyo chini. Alipo ona inatosha alisogea pembeni na kulipeleka lile dumu mbali ili isije kuwa hatari hata kwa upande wao pia, mwanaume yule ambaye alikuwa anaendelea kuivuta sigara yake aliinama kidogo mpaka alipokuwa ameketi bwana yule kwenye kiti.

"Wakati napewa kazi ya kukutafuta kwa namna na gharama yoyote, binafsi nilijua kwamba ingenichukua zaidi ya mwaka mzima au zaidi kukupata ukizingatia umetafutwa kwa miaka zaidi ya mitano na hukuwahi kujulikana kwamba ni wapi uliwahi kuwepo. Maajabu nimekupata ndani ya muda mfupi tu kiasi kwamba kazi imekuwa rahisi lakini kwa upande wako mambo hayawezi kuwa rahisi kwa sababu unatakiwa kufa leo kwa maumivu" mwanajeshi yule alivuta tena sigara na kuutoa moshi kwa mara nyingine kwa kejeli na majivuno.

"Hii usiichukulie personal ndugu yangu, hii ni kazi na walio nituma ndio wanahitaji iwe hivi kwahiyo kama nisipo kuua mimi ndiye nitakufa. It's over" aliongeza sentensi fupi kisha akasimama, alivuta sigara yake kwa mara nyingine na kuiachia kwenda kwenye mwili wa yule mwanaume ambaye alianza kupiga kelele baada ya moto kuwaka na kuanza kuuunguza mwili wake. Mwanajeshi yule aliitoa simu yake akapiga picha za kutosha na kuchukua video fupi kabla uso wa mwanaume yule haujaharibika kisha aliichomoa bastola kwenye kiuno chake, aliikoki kwa kuigongesha kwenye buti lake na kumimina risasi zote kwenye kichwa cha mwanaume ambaye alikuwa anawaka moto baada ya kuzidisha makelele.
Utulivu ulichukua nafasi, mwanajeshi mmoja alisogea na kuanza kuuzima ule moto ili usije ukaleta madhara kwenye hiyo nyumba kwa ujumla lakini kipindi anaendelea na zoezi hilo, walisikia mlio wa risasi eneo la mbali na hiyo nyumba. Hiyo hali haikuwa ya kawaida kwenye eneo kama lile, ni eneo ambalo hakuna mtu mwingine angeweza kufika kwa wakati huo, ni eneo ambalo hakuna binadamu alikuwa na ujasiri wa kwenda kufanya hata utalii kwa sababu lilikuwa linatisha na liliaminika kwamba lilikuwa na viumbe hatari ndani yake, sasa wakati huo hiyo risasi ilipigwa na nani? Kiongozi wao ambaye ndiye alitoka kumuua yule mateka wao alitoka humo ndani kwenda nje kujua ni kipi kilikuwa kinaendelea.

Kutokana na baridi kali ambalo lilikuwa huko, watu wengine ambao walikuwa pale nje ambao nao walikuwa kwenye mavazi ya jeshi walikuwa wakiota moto huku yule mwanamke ambaye alionekana wazi kwamba hakupendezwa na kile ambacho kilikuwa kinafanyika pale akiwa amejitenga mwenyewe na kuegamia kwenye mti mmoja ambao ulikuwa karibu na pale ambapo wenzake walikuwa wakiota moto na kuchoma nyama. Wote ambao walikuwa nje waliusikia ule mlio wa risasi hivyo kila mtu alitahayari kutaka kujua kwamba ni kipi kilikuwa kinaendelea.
Hawakukaa tena bali kila mtu alisimama wakiwa wanaangaza huku na huko lakini hawakuona kitu ndipo mmoja wao alishtuka baada ya kuona kuna mwenzao amekosekana hilo eneo.
"Jordan yuko wapi?" yule aliyeshtuka aliuliza kwa wasiwasi akiwa anamwangalia kila mmoja wao usoni ili kuhakiki kuhusu huyo ambaye alikuwa anamuulizia.

"Alisema anataka kupunga upepo nje kidogo ya hapa hivyo aliingia huko msituni" sauti ya mmoja wao ndiyo ambayo iliamsha hisia ambazo hazikuwa sawa, kiongozi wao huyo aliinyanyua simu yake kupiga kwa kutumia radio call ambayo kila mmoja wao alikuwa anatembea nayo. Simu hiyo iliita mara tatu mfululizo bila kupokelewa, jambo hilo lilitoa ishara mbaya, hapakuwa pema hivyo alimtaka mwanamke yule ambaye hakuwa kwenye mood nzuri kuangalia kwa kutumia kumpyuta yake kujua huyo mwenzao yuko wapi kwa wakati huo.
Alikimbilia ndani na kuhaki mfumo wa mawasiliano kupitia kifaa cha mwenzao, alionekana kuwa mita miambili kutoka walipokuwa wao na kifaa hicho kilionekana kusimama sehemu moja bila kujongea, hawakuwa na muda wa kusubiri, kiongozi wao aliwataka wajiandae kwenye kuangalia hali ya mwenzao kwa sababu ukimya kama huo haukuwa utaratibu kwenye kazi yao, maana yake hakukuwa na usalama kwa mwenzao na walitakiwa kumsaidia kwa haraka kama kuna shida yoyote ingekuwa imempata.

Walitembea kwa umakini kwa dakika mbili ndipo walifika ile sehemu ambayo ilionyesha kwamba kulikuwa na kifaa cha mawasiliano cha mwenzao, kifaa kilikutwa kikiwa kwenye nyasi pembeni yake kukiwa na damu ambayo ilionyesha kuendelea kuelekea mbele ikabidi waifuate. Hatua kumi kutoka hapo ndiyo sehemu ambayo waliukuta mwili wa Jordan shingo yake ikiwa na alama za kutoboka na kichwa kikiwa kimepasuka kwa nyuma. Jordan alikuwa amekufa na kichwa chake kilionekana kujibamiza kwenye mti sehemu ambayo ilikuwa na damu na nywele kiasi. Bastola yake ilikuwa pembeni ya mwili wake, aliyekufa alikuwa ni miongoni mwa watu wa kuaminika vilivyo, kifo chake tena cha ghafla namna hiyo ni ishara kwamba walikuwa wameupokea ugeni ambao hawakuutarajia kwa sababu mtu ambaye aliwaleta ndani ya hilo eneo walitoka kumuua muda sio mrefu. Sasa huyo mtu mwingine ambaye aliingilia hiyo shughuli alikuwa ni nani? Ilizaliwa hofu na maswali ambayo hata wao hawakuelewa namna ya kuweza kuyapatia majibu yake.


"Kuna mtu mwingine ndani ya huu msitu na huenda mpaka muda huu anatuona kwa kila tunacho kifanya hapa" aliongea kiongozi wao huku akiwa anainama kuufanyia uchunguzi mwili wa mwenzake. Mwili ulikuwa bado wa moto, ni ishara kwamba ni muda mfupi; ulipita tangu mtu huyo aweze kuuawa, alitoa ishara ya vijana wake kuweza kutawanyika kwa ajili ya kumsaka mgeni ambaye alikuwa ameingia ndani ya msitu bila wao kuwa na taarifa na kuanza kuwapunguza.
Yalikuwa ni majira ya jioni jua likiwa linazama hivyo chini ya msitu kulikuwa na mwanga kwa mbali ambao kadri dakika zilivyokuwa zinasonga ulikuwa unafifia taratibu. Mwanajeshi mmoja akiwa anatembea, alishangaa kuna shilingi ya zamani ambayo ilikuwa inang'aa ikitua mbele ya macho yake.

Hakuelewa ilirushwa na nani na ilitokea wapi hivyo alisogea ili kuweza kuyashuhudia hayo maajabu, akiwa ameikaribia na kuinama ili aipate mwili wake ulihisi uzito ambao haukuwa wake, akajua kabisa kwamba kulikuwa na ongezeko la mtu mwingine karibu yake. Aligeuka haraka akiwa ameinyoosha bastola yake ila hakuona kitu ikamlazimu kuyarudisha macho yake haraka kwenye ile shilingi ambayo ilikuwa nyuma yake.
Wakati anageuka alikutana na kitu cha ajabu, alifanikiwa kuyafungua macho yake mara moja tu pekee, kwa sababu ile shilingi hakuiona tena na alipo jaribu kuweza kuangalia alihisi kama kuna kivuli ndipo akayafumbua macho yake baada ya kuhisi kulikuwa na kivuli kutokea juu kwenye mti. Ni kweli kuna mwanaume alikuwa amenasa kwenye mti kwa kutumia miguu yake huku mikono ikiwa imeleelekezwa chini. Wakati anapata mshtuko, alihitaji kuielekezea bastola yake kuelekea kwa yule mtu, kwa bahati mbaya kidole kilizama kwenye koromeo lake na kulivunja, alirudi nyuma akiwa ameishika shingo yale ila hakumaliza hata sekunde tano, alikufa baada ya ile shilingi kuzamishwa kwenye paji yake la uso na kifua kilivunjwa kwa ngumi ambayo ilimgandamiza kwenye ule mti kiasi kwamba hata mifupa ya uti wake wa mgongo ikavunjika vibaya.

Ukimya wake uliokithiri ndio ambao ulimsogeza yule mwanamke ambaye alikuwa mtaalamu wa kompyuta karibu na eneo hilo, aliitoa sauti ya mshtuko huku moyo wake ukianza kwenda na kupiga kwa nguvu. Hakutarajia kukutana na kitu kama hicho kwa mara nyingine tena, ni muda mfupi walitoka kushuhudia mwili wa Jordan lakini haikuchukua muda mwingine tena mwenzao alikuwa ameuliwa kikatili kama mwanzo lakini huyo wa pili kwenye paji lake la uso iliachwa shilingi ambayo ilibaki imeshikilia hapo ikiwa inang'aa isivyokuwa kawaida.

Ile hofu yake ilimfanya aanze kurudi nyuma huku akiwa anaitoa simu yake mfukoni baada ya kugundua kwamba hata kile kifaa cha mawasiliano kwenye sikio lake hakikuwepo huenda ni kwa sababu alikisahau kule kwenye kumpyuta. Alisimama na kujibanza kwenye mti baada ya kuhisi kama kuna kitu kilikuwa kimempita kwa kasi nyuma ya alipokuwepo yeye, jambo hilo alihisi ni ndoto ila aliamini kwamba ni kweli baada ya kuiona ile simu yake ambayo alikuwa ameishika mkononi ikiwa imepasuka baada ya kubamizwa kwenye mti. Lilikuwa ni jambo la haraka kufanyika kiasi kwamba yeye mwenyewe alibaki anashangaa asijue tukio hilo lilitokeaje na kwanini aliyelifanya hakumdhuru yeye? Hakuwa na muda wa kusubiri zaidi ya kuanza kukimbia kuelekea upande ambao walikuwepo wenzao wakiwa wanaendelea kumsaka mtu ambaye bila shaka naye alikuwa anawasaka ndani ya msitu huo mzito.

Ndiyo kwanza tunaifungua sehemu ya kwanza kabisa ya simulizi hii, ungana nami mpaka mwisho ili tuweze kwenda sawa pamoja.

FEBIANI BABUYA.
idaiwe%20Maiti3.jpg
 
STORY: IDAIWE MAITI YANGU
MWANDISHI: FEBIANI BABUYA
STORYTELLER: BUX THE STORYTELLER
WHATSAPP: 0621567672
EMAIL: thomasibabuya@gmail.com
AGE: 18+

********************
SEHEMU YA PILI
SONGA NAYO................

Alisimama na kujibanza kwenye mti baada ya kuona jambo la kutisha mbele kidogo kutoka pale ambapo alikuwepo. Mwanaume ambaye kwenye mwili wake alivalia koti refu la rangi ya ugoro, suruali ya jeans ambayo ilifanania na koti lake pamoja na buti kubwa ambalo ni maarufu kama American boot huku uso wake ukiwa umefunikwa kwa kitambaa chenye rangi ya ugoro na kichwani akiwa na kofia aina ya NY ndiye ambaye alikuwa anayafanya matukio hayo ndani ya huo msitu. Kusita kwake ni kwa sababu alimuona mtu huyo akiwa anaufanya ukatili kwa wenzake.

Bwana yule alikuwa anatembea kama mashine, miguu yake ilikuwa myepesi isivyokuwa kawaida lakini spidi yake ndiyo ambayo ilikuwa inatishia usalama wao. Alijigeuza kwenye mti ambapo alipishana na risasi ambayo ilitua hapo, alijitokeza kwa kujiviringisha chini lakini wakati anajitokeza ni shilingi ambayo ilikuwa inaongea lugha moja na mkono wake, shilingi hiyo ilitua kwenye jicho la mwanajeshi mmoja ambaye alianza kupiga makelele bila utaratibu huku silaha yake ikiwa inarusha risasi hovyo kila mahali. Mwanaume huyo alijinyanyua pale chini kama mzimu na kutua pembeni kidogo mwa yule mwanaeshi aliyekuwa na shilingi kwenye jicho lake.

Alizikutanisha ngumi zake mbili kwenye shingo ya mwanajeshi yule, alitulia na kushuka chini taratibu lakini alitumiwa kama ngao kwani mwanaume huyo alimrusha kwa viganja vyake vya mkono kwa nguvu na kwenda kumzoa mwenzake mmoja wakadondokea mbali. Yeye hakuwa na muda wa kupoteza, alitembea kama mzimu kiasi kwamba hata wapiga risasi hawakuelewa wapige wapi kwani alikuwa anawachanganya kiasi kwamba kama wangekurupuka basi wangejikuta wanaanza kuuana wao wenyewe kwa wenyewe. Mwanaume huyo aliruka sarakasi za haraka haraka na kudunda kwenye mti mmoja, alitua chini kwa kutumia goti lake moja ambapo wakati anatua alikuwa ameichomoa bastola kwenye buti lake, risasi zilipigwa kwa muda mfupi mno ambazo zilitua kwenye kichwa cha mwanajeshi mmoja. Alikufa pale pale na wakati wanaangalia risasi zilipo tokea ili waweze kumshambulia, hakuwepo lile eneo, alikuwa ametoweka. Yule mwanajeshi ambaye alikuwa ni mwanamke alikuwa akiyashuhudia yote hayo akiwa haamini huku akiwa amejibanza kwenye mti.

Licha ya kuangalia kwa umakini ila hakuelewa mwanaume huyo alipotelea wapi, ni muda mfupi tu alishuhudia mwenzake akipigwa risasi nyingi za kichwa. Jambo ambalo alilifanya ni kuhamisha uso wake kumwangalia mwenzake ambaye mpaka wakati huo alikuwa amekufa, wakati anayarudisha macho yake mahali ambapo yule mwanaume alikuwepo, hapakuwa na mtu, ni miti tu na nyasi zilikuwa zikimwangalia na kumzomea.

Lilikuwa jambo la ajabu kwake kiasi kwamba alijikuta ana muda mchache wa kuweza kuyapata majibu ya maswali mengi na sio maswali tu bali maswali ambayo yalikuwa ni magumu kwake.
Swali la kwanza ni kwamba, alikuwa ana uhakika kuwa ni huyo mtu ndiye ambaye alimpitia na kuiharibu hiyo simu, kama ni hivyo maana yake alikuwa ana nafasi ya kumuua, sasa kwanini alimuacha hai tofauti na wenzake ambao alikuwa anawaua kikatili? Alijikuta anapoteza ile nafasi ya kujiamini kwenye moyo wake, alijihisi yupo mikononi mwa ibilisi na hakuwa na msaada kwani huenda alishamkana Mungu kwenye maisha yake sasa msaada huo angeupatia wapi na ameshaingia kwenye mikono ya baradhuli shetani? Akiwa anazidi kujipa presha kubwa ya kumfanya atokwe na jasho jingi kwenye msitu ambao ulikuwa na baridi ya kutosha ndipo likaibuka swali la pili kwenye kichwa chake.

Huyo mwanaume alikuwa ni nani? Ni swali ambalo hakulipa muda mrefu kwenye akili yake kwani hakuwa na huo uwezo wa kuweza kulijibu hivyo akajikuta anahamia kwenye swali namba tatu ambalo huenda ndilo lilikuwa mhimu zaidi kuliko yote kwa wakati huo. Ni kwanini huyo mwanaume alikuwa anawaua watu hao, na sio kuwaua tu kwanini alikuwa anawaua kikatili namna hiyo mithili ya mtu ambaye alikuwa na uhasama nao mkubwa? Hilo swali hata hakupewa muda wa kutosha wa kuweza kulitafakari kwa sababu alishtushwa na sauti ya mlio wa kitu, hakikuwa kitu bali kichwa cha mtu kikiwa kinapasuka baada ya kubamizwa kwenye mti kisha buti likatua kwenye kichwa hicho. Yule mwanamke hakuvumilia kushuhudia tukio lile, alijikuta anayafumba macho yake huku chozi likimtoka.
Mwanaume yule alikuwa ni miongoni mwa binadamu wachache ambao walikufa kikatili yeye binafsi kuwahi kuwashuhudia.

Hakuelewa yule mwanaume alitokea wapi bali alimuona tu wakati anamzoa mwenzake kwa miguu yake miwili ambayo aliipitisha shingoni na kumrushia hewani bila shaka alikuwa anaichanganya akili yake. Wakati mwanajeshi yule anashuka chini akiwa anaomba msaada ndipo alikutana na bwana yule ambaye alimdaka kwa nguvu kwa mikono yake na kumtua kwenye goti lake, uti wa mgongo ulikuwa haufai mpaka muda huo na ndipo hapo alipomrushia kwa nguvu kwenye mti kisha akafuatisha buti lake ambalo lilikipasua kichwa kama vile kondomu ilijazwa maji halafu ikatupwa chini.

Zile kelele ziliwaleta wenzake ambao walikuwa wamebaki wawili tu pekee, aliyekuwa mbele alikuja kwa kasi bila mahesabu wala kumuona mhusika wao. Ile kasi yake ilimfanya aanze kutembea kwa kusita sita, sio kwamba alipenda bali shilingi ilipitishwa kwenye koo lake ikatokea nyuma na kwenda kukita kwenye mti. Ile kusita sita kutembea ni kwa sababu alikuwa ameshikilia koo lake akiwa anahangaika huku hawezi hata kutoa sauti ya kuweza kuhitaji msaada ndani ya eneo hilo. Mwanaume yule alikuwa amemfikia ambapo aliizungusha shingo yake kama ananyonga jogoo la pasaka na ni wakati ambao hata yule kiongozi wao alikuwa amefika hapo.
Alipokelewa kwa mtama mzito ambao almanusura umfanye sura yake idondokee kwenye jiwe kubwa lakini alitanguliza mkono ambapo alijivuta na kujigeuza kwa sarakasi safi lakini silaha ilikuwa imedondokea upande mwingine hivyo alichomoa kisu kwenye kiuno chake na kukielekezea kwa mwanaume yule ambaye hakuonekana kumchukulia kwa uzito. Aliangalia pembeni na kupigwa na butwaa kwa namna miili ya vijana wake ilivyokuwa imezagaa pale chini, hakuweza kukubaliana na jambo hilo hivyo alipata hasira kali ambayo ilimfanya kujiinua kwa ngumu na kujipinda kwa sarakasi ambayo iliutanguliza mguu mmoja, ulimkosa mwanaume yule na mguu wa pili ukawa unakuja shingoni lakini nao alifanikiwa kuukwepa hivyo mkono ukawa unafanya kazi kubwa baada ya kujipinda na kurusha kisu chake.

Mkono wenye kisu ulikutana na bega la mwanaume yule kiasi kwamba akarudi nyuma kidogo, aliyainua macho yake ila awamu hii ni yeye ambaye alichelewa hivyo alikutana na ngumi ya kwenye taya ambayo ilimfanya kudondosha meno mawili chini aliyo yatema kwa ghadhabu. Alirusha mkono wenye kisu lakini alitumia hasira zaidi ya akili, mkono ulidakwa na kugeuzwa kwa nguvu kiasi kwamba ulivunjwa bila huruma, kisu kilimponyoka kikawa kimetua kwenye mikono ya mwanaume huyo ambacho alikitumia kumkita mwanajeshi huyo kwenye moyo wake kwa nguvu mpaka pale alipohakikisha amekichana chana kifua chake ndipo alikizamisha kisu hicho kwenye koo la mwanajeshi huyo na kumtupa akiwa ni maiti tayari. Wakati analitekeleza tukio hilo alikuwa anaaangalia pale ambapo mwanajeshi yule wa kike alikuwa amejibanza, bila shaka alijua kabisa kwamba mtu huyo alikuwa anajua kwamba yeye amejificha pale.

Hali ya kuangaliwa na muuaji yule ilizidi kumharibu akili yake, alikuwa hawezi kufanya jambo lolote kwa ambayo alioyaona pale hata silaha yake hakuwa nayo muda huo. Ni hofu ndiyo ambayo ilikuwa imeiteka sehemu kubwa ya moyo wake na asingeweza kufanya jambo lolote lile. Mwanaume yule alivua kile kitambaa chake usoni ili kumuonyesha sura yake halisi mwanamke yule. Asalaleee! Alikuwa ni yule mwanaume ambaye muda mchache uliokuwa umepita alitoka kumshuhudia akichomwa moto na kuuawa kwa petroli ndani ya ile nyumba, sasa kivipi tena awe hai? Alichanganyikiwa.

Alijikuta anatetemeka mpaka akadondoka chini akiwa ameishiwa nguvu kabisa, kivipi mtu ambaye alitoka kuuawa muda mfupi uliopita aonekane tena akiwa mwenye afya njema kabisa? Ulikuwa ni mzimu wake au walikuwa mapacha? Hilo jambo alilipinga kwa sababu mtu huyo hakuwa na ndugu hata mmoja hapa duniani na aliyekuwa hai ni yeye tu, sasa huyo alikuwa ni nani? Kupiga kwake magoti kulikuwa na sababu kubwa mbili, sababu ya kwanza ni kuchanganyikiwa kuhusu mtu yule lakini sababu ya pili alikuwa anajua sheria za wauaji, hata kama alikuwa na mpango wa kukuacha hai ila ukifanya kosa la kuiona sura yake tu basi ni lazima akuue. Alikuwa na uhakika kwamba mtu yule asingeweza kumuacha hai na kwa yale ambayo alimshuhudia akiyafanya! Hakutaka hata kuhangaika kuweza kupambana naye alijua ni lazima afe.
Mwanaume yule alimsogelea mwanamke yule mpaka pale jirani ambapo alikuwa amepiga magoti akiwa analia, alimwangalia kwa umakini sura yake na kuhakiki kama alikuwa amemuona vizuri usoni.

"Binti kama wewe hautakiwi kuwepo maeneo kama haya, sio salama kwa maisha yako. Ni jambo la hatari kubwa nchi hii ikianza kuwapoteza warembo wa aina yako kwa uzembe wa watu wachache. Naenda kuua wenzako wote ambao wamebaki kwenye ile nyumba ila wewe nitakuacha hai, nakuacha hai kwa sababu moja tu, wewe hautakiwi kufa kwa sasa ila zingatia hiki ambacho naenda kukwambia hapa "Watu ambao wamekutuma wewe na wenzako bila shaka wametumiwa video na picha na kuambiwa kwamba nimekufa hivyo mimi ni mfu kwako pia, hatakiwi kujua binadamu yeyote hata kwenye maisha ya huko baadae kwamba mimi bado nipo hai, kama ikitokea hivyo basi nitakuja kukutafuta kwenye maisha yako na kuua kizazi chako na familia yako yote kiasi kwamba jina la familia yako litafutika kana kwamba halikuwahi kutokea hapa duniani" Mwanajeshi yule akiwa anahitaji kuuliza angalau swali moja tu pekee kujua ni sababu zipi ambazo zilifanya yeye asiweze kuuliwa kwa wakati huo, alipokea kofi kali ambalo lilimtoa damu puani na kufanya shavu lake kuwa jekundu ghafla. Akiwa hajakaa sawa alikutana na mguu ambao ulikomaa kwenye tumbo lake, alinyanyuliwa na kupigwa na kiganja kwenye kifua chake kiasi kwamba alitapika damu nyingi kwenye mdomo wake. Alianza kuelemewa na ndipo mwanaume huyo alipopipitisha vidole vyake viwili kwenye shingo ya huyo mwanamke aliyepoteza fahamu hapo hapo.

Alimtupia chini na kumwangalia kwa umakini kwenye pua yake, bado alikuwa anahema kwa mbali hivyo alikuwa hai. Kufanya hivyo ilikuwa ni kumsaidia mwanajeshi huyo kwani kama ingetokea akakutwa akiwa hai na wenzake wote wameuawa kikatili basi lazima ingemletea shida kwa kutengeneza maswali kwa wapelelezi kwamba ni kwanini wenzake wote walikufa ila ni yeye pekee ndiye alipona? Kama angekutwa akiwa mzima kabisa basi lazima angekuwa mshukiwa wa kwanza ila kupigwa namna hiyo hata kama angezinduka bado asingekuwa kwenye hali nzuri hivyo hata kama angeomba msaada basi naye angechukuliwa kama mhanga ambaye huenda muuaji kwa bahati mbaya alisahau kuweza kumuua hivyo hakuna mtu ambaye angekuja kuwa na mashaka naye. Baada ya kuhakikisha amelimaliza jambo hilo, mwanaume huyo alitoweka taratibu akipotelea kwenye ile nyumba ambako kulikuwa na wanajeshi kadhaa ambao walikuwa majeruhi na wasingeweza kutembea kwa kuumizwa vibaya.

Sehemu ya pili inafika mwisho hapa, panapo majaaliwa tukutane ndani ya sehemu ya tatu kuweza kujua safari ya huyu muuaji mpya msituni.

FEBIANI BABUYA.
 
As usual mwamba katika ubora wako. Heshima zangu nyingi kwako mkuu kwa kipawa adhimu ulichojaliwa na Mungu kwenye utunzi.
Kazi iendelee
 
STORY: IDAIWE MAITI YANGU
MWANDISHI: FEBIANI BABUYA
STORYTELLER: BUX THE STORYTELLER
WHATSAPP: 0621567672
EMAIL: thomasibabuya@gmail.com
AGE: 18+

********************
SEHEMU YA TATU
SONGA NAYO................
"It's him, it's him" Ni mwanamke mmoja alikurupuka kutoka kwenye ndoto ya kweli ambayo haikuwa njema kwake akiwa anasisitiza kwamba ni yeye, ni yeye. Aliyekuwa anaota ndoto hiyo alikuwa ni yule mwanamke ambaye ndiye pekee alifanikiwa kuishi na kuachwa hai kule msituni. Ni masaa mengi yalikuwa yamepita lakini tukio lile halikufutika kwenye kichwa chake ndiyo maana hata alipo shtuka wakati huo alitoka kulikumbuka lile tukio huku akiwa anapiga makelele kutoka kwenye kitanda ambacho alikuwepo. Sarah ndilo lilikuwa jina lake halisi mwanamke huyo, ndiye pekee aliishi miongoni mwa wale wanajeshi wote ambao walikuwa wametumwa kuweza kumtafuta mwanaume yule ndani ya msitu ule mzito.
Mwili wake ulikuwa unatoka jasho kila mahali kiasi kwamba alilowanisha mpaka shuka ambalo alikuwa amelalia. Bado hakuwa na utulivu, alikuwa akitetemeka na kila alipo likumbuka tukio lile alizidi kuwa na wasiwasi zaidi ya mwanzo. Alijipapasa kila sehemu ya mwili wake na kugundua kwamba alikuwa salama kabisa lakini mwili wake ulikuwa na maumivu makali ndani yake ambayo bila shaka aliyapata kutoka kwa mtu yule. Akiwa kwenye kitanda hicho alihisi kuna hatua za mtu zinamsogelea kwa sababu alikuwa anashangaa yuko wapi wakati huo, bado akili yake haikuwa imetulia vizuri.
Mbele yake alimuona mwanajeshi mmoja ambaye hawakusafiri naye kwenda kuifanya ile kazi ambayo iliwapeleka ndani ya ule msitu. Mwanaume yule alikuwa na kikombe cha maji mkononi mwake ambapo alimpatia Sarah aweze kunywa ili kutuliza akili yake. Aliyagida maji yote na kutua kikombe chini akiwa anahema.
"Maneno ambayo umeyaongea hapa nimeyasikia mimi pekeyangu, hakuna mtu mwingine yeyote yule hivyo nahitaji uniambie ukweli kwamba ni nani huyo ambaye amekujia ndotoni kiasi kwamba umeogopa namna hiyo?" Sarah alishtuka, hakutarajia kukutana na swali kama hilo kwa wakati huo, lilikuwa ni jambo la hatari kama ukweli ungejulikana kwamba mhusika wao hakuwa amekufa bali alikuwa hai na mzima wa afya kabisa.
"Hakuna kitu ni ndoto ya kutisha tu Nick"
"Sio kweli, kwa mwanajeshi kama wewe huwezi kuota ndoto ya kufikirika ikakupa hofu namna hiyo na ukumbuke wewe ndiye pekee ambaye umekutwa upo hai ndani ya ule msitu. Unataka kuniaminisha kwamba mhusika ambaye amefanya tukio hili alifanya makosa ya bahati mbaya kukuacha wewe pekeyako hai na wengine wote wakauawa tena kikatili namna ile? Kumbuka kwamba baada ya hapa unaenda kwenye chumba cha mahojiano ili ukaeleze nini kilitokea kule kwa sababu mtu ambaye mlimfuata alikufa, sasa huyo ambaye aliua watu wote kasoro wewe alikuwa nani na kwanini ni wewe pekee ndiye ambaye ulifanikiwa kuishi kule? Niambie ukweli ili nijue namna sahihi ya kuweza kukusaidia" Sarah alimwangalia kwa umakini bwana huyo tena kwa utulivu wa hali ya juu.
"Unahisi kuna nini labda Nick?"
"Hakuna utulivu nadhani taarifa imefika mpaka kwa mkuu wa majeshi juu ya kilicho tokea, kila mtu anahitaji kujua ni jambo gani lilifanyika mpaka kufikia hatua ya yale yote kutokea nje ya mpango ambao ulikuwepo" Sarah bado ni kama alikuwa gizani, alitamani kumsimulia bwana huyo juu ya kile ambacho kilitokea lakini nafsi yake ilikuwa inagoma, aliikumbuka kauli ya yule mwanaume ambaye alimuacha hai kule msituni alivyo mpa maelekezo kama angeweza kusema jambo hilo mahali popote na kile ambacho angekifanya! Nafsi yake iligoma kabisa kuwa shahidi na kuelezea kwamba alimuona mtu wa aina kama ile akifanya tukio la namna ile.
"Kitu cha mwisho ninacho kikumbuka ni kwamba nilikuwa napigwa na kiongozi wangu kule msituni mpaka nikapoteza fahamu" alidanganya
"Sijakuelewa bado, yaani kwamba Michael ndiye ambaye alikuzimisha wewe?"
"Ndiyo"
"Hili linawezekanaje?"
"Tulipishana nilipo mwambia kwamba kile ambacho tunakifanya hakikuwa sahihi, yule alikuwa binadamu mwenzetu hivyo tungetumia njia nyingine kumuua sio ile na hatukuwa na uhakika asilimia miamoja kama kweli alikuwa na mtuhumiwa wetu hapo ndipo ugomvi ulipo anzia" mwanaume huyo ambaye alijulikana kama Nick alitabasamu kwa sababu Sarah alikuwa anamdanganya mchana kweupe.
"Sarah kama ulizimia maana yake hukuona kile ambacho kilitokea, nilipo kueleleza kuhusu mauaji ya wenzako haujaonyesha hata mshtuko ikiwa na maana kwamba ulishuhudia kilicho tokea na huenda ndicho ambacho kimekupa hofu namna ile. Najua unanidanganya lakini kwenye mahojiano usije ukafanya huo upumbavu kwa sababu utaingia kwenye matatizo mazito, itengeneze stori yako vizuri ili ukaeleweke, wanajeshi waliokufa ni wengi hivyo usitegemee kwamba itakuwa kirahisi tu namna hiyo lazima watataka kujua kila ambacho kilitokea na siku ambayo utakuwa tayari kuniambia kilicho tokea basi nitafute nitakusikiliza na kuangalia namna ya kukusaidia" Nick alimpiga piga begani Sarah kwa sababu alijua kabisa anamdanganya hivyo alimpa msaada wa kutaka aitengeneze vizuri hadithi yake hiyo ili asije kujiingiza kwenye shimo baya. Sarah alihema kwa nguvu, jambo hilo hakuwa tayari kumwambia mtu yeyote yule kwa gharama na namna yoyote ile.

******************
Sarah Martin, ndilo lilikuwa jina lake mwanamke pekee ambaye alifanikiwa kupona ndani ya ule msitu ambako wenzake wote waliuawa kikatili. Msitu wa Mau, upatikanano nchini Kenya ndiko ambako mambo yote hayo yaliweza kutokea, msitu wa Mau ndio msitu mkubwa na mnene zaidi ndani ya nchi ya Kenya na ndiko ambako mambo yote hayo yaliweza kufanyika. Sarah baada ya kuzimishwa ndani ya ule msitu baadae alikuja kuzinduka hali yake ikiwa ni mbaya ndipo alipoamua kupiga simu makao makuu kuweza kuomba msaada na kuelezea kwamba hakuwa na uhakika kama kuna mwingine alikuwa amepona zaidi yake.
Msaada ulifika lakini ilikuwa ni baadae sana, kitu ambacho kilishuhudiwa ndani ya hilo eneo kilikuwa kinatisha kwa sababu yalikuwa ni mauaji tu pekee ambayo yalitamalaki na mtu ambaye alikuwa hai alikuwa ni huyo mmoja tu pekeyake. Sarah wakati huo ndipo aligundua sababu halisi ya muuaji yule kuweza kumpiga namna ile kiasi kwamba alipoteza mpaka fahamu. Kuwa kwenye hali kama ile haikuwa sababu pekee ya kufanya jambo hilo liishe kirahisi, ilikuwa ni lazima afanyiwe uchunguzi wa kutosha pamoja na kuhojiwa kwa kina ili aweze kueleza kinaga ubaga kwamba ni jambo gani lilitokea huko wakati ni wazi mhusika wao walifanikiwa kumkamata na kumuua na ushahidi wote wa picha na video ulikuwepo.
Baada ya kuzinduka tu Sarah ndipo alikutana na mwenzake huyo Nick ambaye alimpa ushauri wa kuweza kuitengeneza vizuri hadithi yake ya uongo hiyo kwani kama wakubwa wake wangegundua kwamba kuna kitu anakificha basi alikuwa anapewa kesi nzito ya kuwauza ama kuwasaliti wenzake. Alijua yeye kuumia pekee na ndiye ambaye alipona isingekuwa rahisi kuwaaminisha wakubwa zake kwamba lile tukio yeye hakuelewa lilitokeaje, alitakiwa kulidadavua kwa kina Sarah ila abadani hakuwa tayari kuelezea uhalisia wa namna tukio hilo lilivyo fanyika.
Sarah baada ya mahojiano alikuwa amerudi nyumbani kwao, kambi yao ilikuwa ndani ya jiji la Arusha lakini yeye alikuwa amejenga ndani ya Moshi ambako ilikuwa ni asili ya mama yake mzazi. Kwenye jumba lake alikuwa akiishi yeye, mama yake pamoja na mdogo wake mmoja ambao walikuwa wakimtegemea yeye kwa kila kitu kuanzia kuvaa mpaka kulala. Majira ya jioni alikuwa amerudi nyumbani kwao baada ya kupata nafuu na kupewa likizo kambini, kurudi kwake nyumbani kulimpa nafasi ya kutuliza akili yake na kutafakari mambo mengi ambayo yalikuwa yametokea. Aliwahi kuwepo kwenye baadhi ya mataifa ambayo hayaishi vita kila siku na mauaji yalikuwa yanafanyika kwa wingi ila jambo ambalo alilishuhudia kwa wenzake lilimtisha na kumfanya kila akilikumbuka mwili wake kuanza kutetemeka kwa nguvu kiasi kwamba ikawa kama ni ndoto mbaya kwake ambapo kuna wakati ilikuwa inamfanya atetemeke.
Alikuwa dirishani juu ya nyumba yake hiyo ya ghorofa moja akiwa amelifunua pazia na kuuangalia kwa mbali mlima mkubwa na mrefu zaidi ndani ya bara la Afrika ambao ulikuwa unavutia na kuifanya mandhari hiyo kuwa bora na ya kupendezesha kwenye macho yake, fahari ya mlima Kilimanjaro. Mkononi mwake alikuwa ameshika kikombe cha kahawa ili kuweza kushindana na baridi kali ambalo lilikuwepo huko Moshi. Mkono wake ulikuwa unatetemeka kiasi kwamba yeye mwenyewe akawa anajishtukia, alishtuka baada ya kusikia sauti nyuma yake kiasi kwamba mpaka kile kikombe kikataka kumponyoka! Ilikuwa ni sauti ya mama yake.
"Una shida gani binti yangu? Sijawahi kukuona una wasiwasi kiasi hiki kwenye maisha yako tangu siku umezaliwa, nini kinakusumbua mama yangu?" ilikuwa ni ghafla na hakutarajia kitu kama hicho hivyo alipata wasiwasi mno kiasi kwamba alikosa jibu la haraka la kumjibu mama yake. Alijichekesha ili kumtoa wasiwasi mama yake lakini hali ya mkono ndiyo ambayo ilikuwa inamdhalilisha, ilimlazimu kukitua chini kikombe hicho kwenye meza ndogo ambayo ilikuwa karibu na dirisha kisha akasogea kumkumbatia mama yake.
"Nawaza kuhusu kazi mama, kazi yetu hii imebeba hatima ya maisha ya watu wengi kwenye mikono yetu hivyo kila wasaa nawaza nisije kufanya kosa la namna yoyote ile nikashindwa kuyaokoa maisha ya watu wengi"
"Binti yangu wewe ni moja kati ya wazalendo wakubwa kwenye taifa hili, tangu ukiwa mdogo siku zote umekuwa ukijitoa kwa watu kwa ukubwa hata kama wewe utaumia na ndiyo maana kwenye kabati lako umejaza zawadi za mfanyakazi bora ambazo ulikuwa unapewa na viongozi wako hivyo mimi nakuamini kuliko mtu yeyote yule na unatakiwa kujua kwamba wewe ni bora kwa kila kitu" mama yake alimpa maneno mazito na yenye ujumbe ulioshiba kumpa tumaini mwanae.
"Asante mam...." hakuimalizia sentensi yake alihisi kuna kitu hakipo sawa, alichomoka kwenye mkono wa mama yake na kukimbilia nje akiwa anaichomoa bastola kwenye kiuno chake. Haikuwa kawaida kuhisi jambo zito namna hiyo huku moyo ukiwa unamuenda mbio kwa nguvu, ni hisia ambazo zilimpa hali hiyo akajua kabisa hapakuwa sawa kwenye hiyo nyumba yao lakini baada ya kufika nje aliona kivuli kikiwa kinaishia kwenye mti fulani ambao ulikuwa karibu na uzio mrefu wa fensi. Alitamani kumfuatilia mtu huyo lakini alisita baada ya kukutana na begi hivyo akalifungua haraka kujua kulikuwa na nini ndani yake, hakuwa na wasiwasi ya kukutana na kitu cha ajabu kwa sababu hakuwahi kuwa kwenye ugomvi na mtu yeyote yule na hakuna mtu ambaye alikuwa anajua ni wapi yeye anaishi.

Ni nani tena huyu ambaye amemtembelea Sarah mpaka nyumbani kwake ikiwa ndo kwanza amerudi? Alikuwa na lengo naye lipi? Unatamani kujua kwamba lile begi lilikuwa na kitu gani ndani yake?

Kwa leo sehemu ya tatu inaishia hapa, tukutane ndani ya sehemu ya nne wakati ujao.

FEBIANI BABUYA.
 
STORY: IDAIWE MAITI YANGU
MWANDISHI: FEBIANI BABUYA
STORYTELLER: BUX THE STORYTELLER
WHATSAPP: 0621567672
EMAIL: thomasibabuya@gmail.com
AGE: 18+

********************
SEHEMU YA NNE
SONGA NAYO................
Baada ya kufungua ndani ya begi hilo alikutana na mabunda mengi ya pesa yakiwa yamepangana lakini juu yake kulikuwa na bahasha moja ngumu ambayo ndiyo aliiona kuwa ya mhimu kwa wakati huo. Aliifungua hiyo bahasha ndipo ndani yake akakutana na karatasi nyeupe iliyokuwa imeandikwa kwa maandishi makubwa "Hizi pesa ni zawadi kwa mama, umefanya jambo kubwa kutosema kile ambacho ulikiona kule. Kuna siku nina uhakika maisha yatakuja kutukutanisha tena ila kwa kilicho tokea ndani ya ule msitu IDAIWE MAITI YANGU sio mimi. Hili jambo hakikisha unalifukia kwenye moyo wako, kila utakapo hitaji kulisema hadharani basi ikumbuke kwanza familia yako" Ujumbe huo uliishia hapo, ulimuogopesha na kumpa hofu, alikimbilia lile eneo ambalo aliona kile kivuli kinaishia akiwa na begi mkononi lakini hakuona kitu chochote kile.
Hali hiyo ilimuongezea hofu na kumpa ishara kwamba ina maana mtu huyo alikuwa akimjua vizuri kiasi kwamba hata kwake alipafahamu mpaka hivyo kama angetaka kumuua lingekuwa jambo la muda mfupi tu. Mpaka wakati huo alikuwa ana maswali mengi kichwani mwake kuweza kutaka kujua kwamba yule mtu alikuwa ni nani haswa na aliyekufa alikuwa nani? Alibaki anasonya na kuogopa kwa sababu asingeweza kujijibu hayo maswali hivyo akawa anarudi kinyonge ndani ambapo alikutana na mama yake lakini alimpisha bila kuongea jambo lolote lile.

**************
Saa nane na dakika kumi na tano usiku, simu ilikuwa inaita ndani ya jumba moja la kifahari ambalo lilikuwa maeneo ya Mbweni Dar es salaam. ulikuwa ni wakati wa kupumzika huo lakini ilionekana kuwa simu ya mhimu zaidi, hilo jumba lilikuwa linamilikiwa na mkurugenzi wa usalama wa taifa wa Tanzania Micho Othman. Simu ilipokelewa na aliyekuwa katibu wake yeye akiwa amepumzika lakini uzito wa simu hiyo ndio ambao ulifanya iwe lazima kwa mheshimiwa huyo kuamka ili kwenda kuisikiliza. Alikereka kuamshwa majira hayo ambayo alipenda kutulia na familia yake ila hakuwa na namna.
Simu hiyo ya majira ya usiku ilikuwa inatokea Kenya, ndani ya makao makuu ya shirika la kijasusi la nchi hiyo National Intelligence Service (NIS) yapatikanayo ndani ya jiji kubwa la Nairobi. Uzito wa mtu ambaye alimpigia hiyo simu ilionyesha kabisa kwamba kulikuwa na shida mahali kwa sababu isingekuwa rahisi kupigiwa simu na mtu huyo bila sababu za msingi za kufanya hivyo. Aliipokea simu hiyo na kuiweka sikioni
"Bwana Odhiambo ni usiku sana saivi na unajua kabisa muda kama huu inatakiwa nipate muda wa kutulia na familia yangu"
"Ni sahihi lakini sio kama kuna tatizo Micho na wote tunalijua hilo"
"Nakusikiliza"
"Unajua lolote juu la kilicho tokea ndani ya msitu wa Mau?"
"Hapana, huo ni msitu wako kwenye nchi yako sasa mimi nahusikaje na nchi yako Odhiambo?"
"Shida sio wewe kuhusika na msitu wangu shida ni kile ambacho kimetokea huku kinakuhusu hata wewe moja kwa moja"
"Ni usiku saivi ebu nenda kwenye hoja yako moja kwa moja unataka nini?"
"Kuna mauaji yamefanyika ndani ya huu msitu"
"Sasa mimi nahusika vipi?"
"Haya mauaji ni ya wanajeshi wa Tanzania" Micho alibakia kimya kwa muda kwanza asijue ni kipi ambacho alitakiwa kukijibu.
"Ni wanajeshi wangapi wamekufa?"
"Sina idadi kamili ila hawapungui kumi na watano"
"Unajua kilicho sabababisha mauaji yao na walikuwa wanafanya nini huko?"
"Kwa taarifa za awali inaonekana kwamba kuna mtu ambaye walikuja kumtafuta huku alikuwa anaishi kwa siri na baadae walifanikiwa kumpata wakamuua ila jambo la kushangaza ni kwamba wote wamekutwa wameuawa kasoro mtu mmoja tu ndiye amepona. Inanishangaza mkuu wa usalama nchini hauna hizi taarifa?" hilo swali ndilo ambalo lilimpa hasira kiongozi huyo wa usalama nchini, ni kweli hakuwa na hizo taarifa ina maana ni kwamba alifichwa na watu wawili, raisi pamoja na mkuu wa majeshi.
"Una jina la huyo aliyepona?"
"Sarah Martin"
"Unataka nini Odhiambo kulimaliza hili?"
"Ndicho ambacho huwa nakupendea, unajua kabisa kwamba taifa lako litatuletea picha mbaya kwa kuvamia kwenye msitu wetu bila kibali na kufanya mauaji huko hivyo itaonekana ni sisi tunaua raia wetu au wananchi wetu lakini kwa sababu wewe ni mtu mwenye busara unalielewa hili na lazima kuna gharaam zitumike ila leo sijakupigia kwa ajili ya kukwambia tunacho kitaka ili kulimaliza hili, leo nilitaka tu uwe na hizi taarifa. Kuna siku nitahitaji kitu kutoka kwenu na nitakupa taarifa mapema ya nini unatakiwa kukifanya"
"Kwanini hizi taarifa usingempatia mkuu wa majeshi au raisi maana sihusiki sana huku?"
"Mimi na wewe wote tunajua kwamba jeshi huwa linetekeleza tu ila jukumu la usalama wa nchi lipo kwenye mikono yako wewe hapo hivyo wewe ndiye ambaye unapaswa kuzungumza na hao watu wako huenda wakawa na majibu sahihi na mpaka walikuficha wewe basi kuna jambo halikuwa sawa kwenye kazi hiyo"
"Unamjua aliye waua watu hao?"
"Hapana ila zungumza na huyo binti atakupa majibu sahihi" simu ilikatwa, mkurugenzi aliketi kwenye kiti hata ile hamu ya kuendelea kulala iliisha kabisa. Alizihitaji taarifa za binti huyo ziletwe haraka mezani na kuweza kujua yuko wapi wakati huo kwani ilikuwa ni mhimu kuongea naye kabla hajaongea na mtu mwingine yeyote yule.

Sarah Martin, ana miaka 35 ni moja kati ya wanajeshi hodari na wenye mafunzo ya juu ndani ya jeshi la nchi ya Tanzania. Mwanamke huyu pia ni moja kati wa wadunguaji bora na wa kutegemewa jeshini. Amezaliwa Makongorosi Chunya ambako alianzia shule yake ya awali huko ila baada ya baba yake kufariki walihamia ndani ya jiji la Mbeya maeneo ya Nzovwe. Huko aliishi yeye, mama yake na mdogo wake ambapo baada ya kuhitimu elimu ya sekondari aliweza kujiunga moja kwa moja na JKT pale pale Nzonvwe ambapo safari ya maisha yake ilianzia hapo akiwa kama mwanajeshi.
Alikuwa ni miongoni mwa wanajeshi wenye umri mdogo kuaminiwa kufanya oparesheni ngumu za kijeshi ambapo ameenda kwenye nchi nne barani Afrika; Alienda Nigeria kubambana na kundi la Boko Haramu, alienda Congo kama sehemu ya wanajeshi ambao waliungana na Interpol kwenda kupambana na waasi. Alikuwepo kwenye ile oparesheni ya kupambana na Al-shabaab lakini pia alikuwepo Msumbiji kupambana na waasi ambao walisababisha hali ya hatari ambayo ilidhaniwa ingeweza kuupindua utawala ulipo madarakani.
Baada ya kutoka huko alipewa likizo kisha mwaka mmoja baadae akajumuishwa kwenye kikosi maalumu ambacho kilikuwa kinatambuliwa na mkuu wa majeshi na ndicho ambacho anafanya nacho kazi mpaka sasa. Japo alizaliwa Mbeya ambako ndiko asili ya baba yake lakini kwa sasa anaishi Moshi ambako ndiko iliko asili ya mama yake. Taarifa za mwanamke huyo zilikuwa zinasomwa na moja ya vijana wake usiku huo huo kwenye Ipad kubwa, zilikuwa zinajitosheleza kuujua uwezo wa mwanamke huyo ambaye alidaiwa kwamba ni pekee ambaye alifanikiwa kupona kwenye ule msitu huko iliko dhaniwa kwamba watu wengi walikuwa wamepoteza maisha.
"Kwa sasa yuko wapi?"
"Tumejaribu kudukua mawasiliano yake, inaonekana yupo Moshi muda huu"
"Andaeni helikopita nataka niende huko mwenyewe" mheshimiwa hakuwa na muda wa kusubiri kupambazuke, lilikuwa ni jambo la dharura na yeye ndiye ambaye angekuja kuzipokea lawama zote kama kuna kitu kingeenda vibaya hivyo aliona ulikuwa ni wakati sahihi wa yeye mwenyewe kudili na jambo hilo kabla ya kuwashirikisha watu ambao walimficha oparesheni nzima mpaka kufikia wakati huo.

Kuna mengi ya kuyafunua humu ndani, ndiyo kwanza sehemu ya nne, tukutane ndani ya sehemu inayo fuata.

FEBIANI BABUYA.
 
Daaah tangia asubuh napita pita apa mkuu umeweka fupi fupi sana ongezeaa ata mbili zingine mkuu
 
Back
Top Bottom