Simulizi ya kipelelezi: Idaiwe maiti yangu

Simulizi ya kipelelezi: Idaiwe maiti yangu

STORY: IDAIWE MAITI YANGU
MWANDISHI: FEBIANI BABUYA
STORYTELLER: BUX THE STORYTELLER
WHATSAPP: 0621567672
EMAIL: thomasibabuya@gmail.com
AGE: 18+

********************
SEHEMU YA SABINI NA TISA
SONGA NAYO................


******
Ezra Ethan alipigika isivyokuwa kawaida, hali yake haikuwa nzuri sana hivyo ilimlazimu The Future kumbeba ili ampeleke hospitali lakini akiwa anakaribia kufika hospitali nafsi yake iligoma kufanya hilo jambo. Kwenda hospitali ingekuwa ni hatari mno kwa upande wao, kwanza yeye mwenyewe alikuwa mhuni wa mtaani ambaye mara kadhaa alikoswa koswa na mkono wa dola, kujipeleka hospitali ingekuwa mwanzo wake wa kuingia kwenye mikono ya watu hao ukizingatia angeambiwa kwamba afuate taratibu za kipolisi ili mtu wake aweze kutibiwa.
Uamuzi huo ndio ambao ulimfanya kughairi jambo hilo, aliamua kwenda nyumbani kwake kwa ajili ya kumtibia mtu huyo mwenyewe japo lilikuwa jambo la hatari mno endapo angemfia mkononi mwake, hakujua angejieleza vipi kuhusu jambo hilo. Lakini wakati wanafanya hayo yote, kuna jambo moja la mhimu ambalo walikuwa wamelisahau, wakati tukio lile linafanyika ni kwamba kuna watu walikuwa wanarekodi hususani wananchi wa lile eneo.

Kama ilivyo kawaida ya watanzania kupenda kutrendisha vitu ndilo kosa ambalo mwananchi mmoja wa Tabata alilifanya. Baada ya The Future kuingia lile eneo na bastola yake, alipiga risasi kuwatawanyisha wale watu lakini muda huo huo bwana huyo aliiachia video mtandaoni, video ambayo ilimtokea puani. Ilichukua dakika hamsini tu kijana huyo kutafutwa na watu ambao hawakuwa wakijulikana wakimtaka aeleze kwa upana kuhusu video hiyo kwa kuhisi kwamba huenda alikuwa anafahamiana na wahusika wa kwenye tukio.
Kipi kiliwavutia watu hao? Kuonekana kwa sura ya Othman chunga ndiyo ilikuwa sababu. Othman sura yake ilisambaa zaidi kwenye lile tukio la mauaji ya waziri wa mambo ya ndani hivyo alikuwa anatafutwa na watu wa pande mbili, moja ni serikali hususani shirika la TIGI ambalo lilikuwa na hamu ya kumpata kwani kupatikana kwake ungekuwa mwanzo wa urahisi wa kumpata mhusika wao Gavin mwenyewe.
Lakini kundi la pili halikuwa la kiserikali, hawa walikuwa ni watu ambao ndio haswa walikuwa wamempoteza mtu wao, waliamini kwamba kulikuwa na muunganiko mkubwa wa hayo matukio hivyo kijana huyo angekuwa msaada mkubwa kwao kuweza kumpata mdau wao ambaye alionekana kuwachanganya kwa muda mrefu bila mafanikio.

Haikuwa hivyo tu bali tukio hilo pia lilinogeshwa na uwepo wa ofisa wa polisi, ofisa wa polisi ambaye alizuiliwa kwenye hizo kesi alikuwa anatafuta nini mpaka ikafikia hatua ya yeye kupigana na Othman tena muuaji wa kiongozi mkubwa kama waziri wa mambo ya ndani? Isingekuwa rahisi namna hiyo, ilikuwa ni lazima asakwe mhusika kwa namna moja ama nyingine. Kijana yule licha ya kujieleza sana kwamba yeye alichukua ni video tu hakuna ambalo alikuwa analijua, aliupa ulimwengu kitu cha kukizungumzia ila yeye aliuawa na kwenda kutupwa kwenye jalala la takataka kwa sababu hakuwa na faida tena. Maisha yake yakawa mafupi akiwa ameyafupisha kwa mkono wake mwenyewe na ujinga wake.
Kifo cha kijana huyo ikawa kama ishara ya hatari mbele ya maisha ya Ezra na kuna kosa kubwa moja ambalo alilifanya, sura yake ilitambulika eneo la tukio halafu alikuwa na simu yake mfukoni, simu ambayo ilikuwa hewani. Makosa madogo madogo ndiyo ambayo huwa yanawaletea watu shida kwenye maisha yao hilo ndilo ambalo lilimkuta yeye, wakati huo alikuwa amepoteza fahamu kwani alipoteza damu nyingi baada ya kuumia kule kiasi kwamba hakuwa akijitambua tena.

Ezra alishtuka baada ya muda mrefu, mwili ulikuwa unauma kila sehemu. Hakujua kwamba alikuwa wapi kwa sababu akili yake bado haikutulia huku kichwa kikiwa kinamuua isivyokuwa kawaida. Alianza kuyakumbuka mapigo ambayo alikuwa anayapokea kutoka kwa mtu wake, moyo ulianza kumuenda mbio sana kiasi kwamba alihisia amevamiwa tena, aliyafumbua macho yake akiwa anavuja jasho na kuhema kwa nguvu mithili ya mtu anayesakwa na umoja wa mataifa, yaani hana pa kukimbilia tena, hakuw sawa.

Alihamaki baada ya kugundua kwamba mbele yake kulikuwa na mtu, mtu ambaye alikuwa amempa mgongo akiwa analizungusha bisu kubwa pembeni. Alimeza mate kwani hakujua ni nani, akili ilimrudisha eneo la tukio akakumbuka kabisa kwamba aliyekwenda kumuokoa alikuwa ni The Future, ila mtu huyo hakuonekana kuwa ni yule ambaye alimuokoa wakati ule ndiyo maana hofu iliongezeka. Alifundishwa hivyo kwenye kazi yake, ni kosa kuwa na amani sehemu ambayo hauna uhakika na usalama wako.
Nafsi yake ilionyesha kuwa na mashaka mengi na mtu ambaye alikuwa pembeni yake hakuonekana kuwa na muda naye licha ya kujikohoza ili kumshtua mtu huyo juu ya uwepo wake hapo. Akiwa anataka kutoka kitandani ili kama kuna hatari aweze kujihami, mwanaume huyo ambaye alikuwa amempa mgongo alibonyeza rimoti ambayo ilikuwa kwenye mkono mwingine. Skrini kubwa ambayo ilikuwa ukutani iliwaka, kuwake kwake kukamfanya Ezra kuyatupa macho yake, jambo ambalo alilishuhudia lilimfanya aanze kurudi nyuma.
Ilikuwa inaonekana video fupi ikimuonyesha The Future akiwa anauawa kikatili mno, alijaribu kupigana na mwanaume ambaye alikuwa mbele yake ila alionekana kuwa kama mtoto mdogo, mwanaume huyo alionekana kuwa mkatili isivyokuwa kawaida. Sehemu ya moyo ilitobolewa vibaya mpaka mtu huyo akautoa moyo na kuukanyaga kwa mguu wake. Ezra alijikuta chozi linashuka, mtu ambaye aliuawa ndiye ambaye alimuokoa yeye na bila shaka alikufa akiwa anamlinda yeye, sasa yeye alikuwa wapi? Jibu angelipata muda mchache ambao ulikuwa unafuata.

Akiwa amehamaki kwa uchungu na masikitiko ilikuja video nyingine, hiyo ilimkosesha kabisa nguvu kiasi kwamba alikaa mpaka chini kabisa akianza kujifikiria mara mbili mbili na kutukana kwa hasira. Ilikuwa video ya Brian, yule kijana wa IT ambaye ndiye alimsaidia kumpa ramani ya mambo yalivyokuwa yanakwenda lakini kijana huyo alimuonya mapema kuachana na vile vitu kwa sababu alimhakikishia kwamba kuwafuatilia wanasiasa hakujawahi kuwa na mwisho mwema hata siku moja hivyo kama amepewa nafasi ya kukaa kando na hayo mambo alitakiwa kufanya hivyo.

Lakini kwa sababu yeye alikuwa anawaza kupata vyeo na kujibebea ujiko hakuwa tayari kuufuata ushauri huo Ezra, moyo ulikuwa unasukumwa na nguvu kubwa ya kuyapata mafanikio ya haraka, alitamani kuwa mtu mkubwa na kutambulika ila mambo hayo yalimtokea puani. Kijana huyo aliuawa kwa kupigwa risasi nyingi kichwani bila huruma kiasi kwamba hata kichwa kilipondeka pondeka vibaya na kwa mtu ambaye hakuwahi kumjua basi asingeitambua kabisa sura yake. Hayo mambo yote yalitokea kwa sababu yake yeye, kama zisingekuwa tamaa zake watu hao wawili wangekuwa hai mpaka wakati huo hivyo hilo jambo lilikuwa kwenye mkono wake.

Ezra hata ule ujasiri kama ofisa wa polisi uliisha, alijikuta anaanza kulia kama mtoto mdogo, kila binadamu ni muoga mbele ya kifo. Akili yake ilikuwa inampa hiyo taarifa, hakuelewa yule mtu alikuwa ni nani hasa mpaka kufanya ukatili wa namna ile ila alikuwa anahisi kwamba huenda ni wale watu ambao walikuwa wanamfuatilia.
“Nimepata taarifa kutoka kwenye kituo chako kwamba ulikuwa mtu wa kwanza kufika kwenye tukio la kuuliwa kwa waziri wa mambo ya ndani. Lakini nmeshangazwa zaidi baada ya kukuona kwenye video ile ukiwa na yule yule muuaji wa waziri tena wewe mwenyewe ukiwa kwenye hali mbaya wakati unapigana naye. Unaweza kuniambia kwamba huyo mtu mnafahamiana vipi na umempataje?”
“Kwanini umewaua?”
“Nadhani kwa sasa unatakiwa kuyahofia zaidi maisha yako bwana mdogo” mwanaume huyo aliongea bila kugeuka, alibaki amekaa vile vile.
“Mpuuzi mkubwa wewe, nitakuua kwa mkono wangu” Ezra alifoka akijinyanyua na kutaka kumrukia mwanaume yule japo hakuwa na nguvu za kutosha. Mwanaume yule alisimama ghafla na kuukunjua mguu wake ambao ulikuwa ndani ya buti kubwa, mguu ule ulitua kwenye shavu la Ezra akatema meno mawili na kwenda kujibamiza ukutani akigugumia maumivu ambayo yalikuwa yanatembea mwilini mithili ya mtu aliyepigwa na shoti ya umeme.
Hakumkopesha, bwana yule aligeuka akiwa anaivuta bastola kiunoni, aliachia risasi moja ambayo ilitua kwenye goti la kulia. Alilia kwa sauti kwani hakutarajia kuongezewa maumivu ya namna hiyo, mwanaume ambaye alikuwa amegeuka, sura yake haikuwa ngeni sana, alikuwa ni Bashir, yule kijana wa mkuu wa majeshi. Aliirudisha bastola kiunoni huku mkono mmoja akiwa anaendelea kukizungusha kisu chake kwa nguvu.

79 inafika mwisho.

FEBIANI BABUYA.
 
STORY: IDAIWE MAITI YANGU
MWANDISHI: FEBIANI BABUYA
STORYTELLER: BUX THE STORYTELLER
WHATSAPP: 0621567672
EMAIL: thomasibabuya@gmail.com
AGE: 18+

********************
SEHEMU YA THEMANINI
SONGA NAYO................


“Nadhani kwa sasa tunaweza kuongea kwa heshima, nakuuliza swali rahisi tu unaanza kunipigia makelele. Unahisi kwamba mimi najali lolote kuhusu maisha ya wale watu ambao wamekufa labda? Mimi sijali lolote kuhusu wewe kuwajua hao vijana” alizamisha tena kisu kwenye mfupa lile eneo ambalo risasi imepenya, Ezra alijinyonga nyonga pale alipokuwa lakini hakuwa na la kufanya.
“Nilipata taarifa zake kutoka kwa rafiki yangu wa pili ambaye alimuua”
“Umepataje taarifa zake?”
“Niliunganisha na yule The Future ambaye alikuja kuniokoa ndiye ambaye alinipa maelekezo kuhusu maisha ya Othman na mzee mmoja ambaye ndiye amenipa mwongozo”
“Yeye alimjuaje?”
“Kwa sababu yeye na baba yake wamewahi kuwa marafiki na kufanya kazi pamoja”
“Na kule ulikuwa unaenda wapi?”
“Nilikuwa naenda kumtafuta”
“Ulijuaje kama atakuwepo kule?”
“Kwa sababu ni maelekezo ambayo nimepewa na mzee huyo kwamba atakuwa huko kwa sababu ni nyumbani kwao. Alikuwa anaenda kuangalia kaburi la baba yake”
“Una uhakika na hizi taarifa?”
“Ndiyo”
“Nipe maelezo zaidi juu ya yale ambayo unayajua kuhusu yeye”
“Inaonekana kwamba hawa vijana wapo chini ya Gavin Luca na hayupo mmoja, wapo wengi”
“Kivipi?”
“Walikusanywa vijana wote ambao familia zao ziliuliwa na viongozi wa serikali hivyo wapo kwa ajili ya kulipa kisasi”
“Dhidi ya nani?”
“Viongozi wa serikali”
“Na sababu za wewe kumfuatilia mtu huyu mwisho wake ulitaka uwe nini?”
“Kumpata Gavin”
“Halafu?”
“Nilitegemea jambo hili lingenipa umaarufu na kupata nafasi kubwa ya kuaminika kwa wakubwa”
“Kwahiyo haya unayafanya uli upate cheo?”
“Ndiyo”
“Bwana mdogo huna mambo ya mhimu ya kufanya?”
“Naomba nipe nafasi ya mwisho nitakaa mbali na haya mambo”
“Kwa taarifa ambazo nimefuatilia ni kwamba mara ya kwanza ulipewa onyo na nafasi ya kukaa mbali na haya mambo lakini ulipuuzia leo unahitaji mimi nikupe nafasi nyingine?”
“Zilikuwa ni tamaa tu, naahidi siwezi kurudia tena”
“Bahati mbaya sana mimi sio mtu wa kutoa misamaha kama unahitaji misamaha ulitakiwa kwenda kutubu kanisani” mwanaume huyo aliunguruma akiwa anaitoa picha ya mwanamke, Sarah na kumuonyeshea kijana huyo.
“Unamfahamu huyu mwanamke?”
“Ndiyo”
“Unamfahamuje?”
“Ni mwanajeshi lakini ni moja kati ya wadunguaji hodari kwenye hili taifa ambaye watu wengi wanatamani kuwa kama yeye kwa sababu huwa anatumika kama mfano tukiwa tunafundishwa kulenga shabaha”
“Nadhani umeliewa swali langu”
“Nimesikia kwamba ndiye muuaji wa mke wa raisi”
“Unajua ninakoweza kumpata?”
“Hapana”
“Huyo mzee ambaye unadai ulielekezwa kwake anaitwa nani?”
“Mzee Miraj”
“Nampatia wapi?” ilikuwa ni sauti ya mamlaka hivyo hakuwa na namna zaidi ya kuitii kwa adabu kwani alijua kabisa bwana huyo hakopeshi hivyo alijibu kila ambacho alikuwa anaulizwa tena kwa usahihi kabisa.
“Unajua bwana mdogo ulitakiwa ufuate ushauri wa watu ambao walikuonya kabla. Mimi nafanya kazi na wanasiasa ila naichukia sana siasa, haya maisha ni rahisi kama ukiamua kufuata yanayo kuhusu ila unapo amua kujiingiza kwenye mambo kama haya halafu unajua kabisa una maisha magumu na hakuna mtu hata mmoja ambaye yupo nyuma yako kwa ajili ya kukulinda ni jambo la hatari sana. Maisha yanakupa nafasi moja tu, ukiitumia vibaya basi ujue kabisa kwamba hautaipata nafasi nyingine tena ndo inakuwa imeisha.

Lakini licha ya hayo yote ukajitwika ugwiji na kuhisi wewe ndiye unajua sana, ukajiona kwamba wewe ndiye una tamaa ya kupanda vyeo mwisho wa siku unaenda kufa bila hata kuviona hivyo vyeo vyako ambavyo unavililia. Na watu wenye tamaa tamaa za kipuuzi kama nyie mnatakiwa kufa kwa maumivu ila nakuonea huruma umepata maumivu ya kutosha kwahiyo nitakuua haraka tu” yalikuwa ni maneno ya kutisha bwana huyo akitoa somo dakika za mwisho lakini alimhakikishia mtu wake kwamba ilikuwa ni lazima aweze kumuua, yaani hakukuwa na namna ya kwamba angemuacha hai, hilo ndilo lilikuwa jambo la hatari zaidi.

“Hapana usiniue tafadhali, naahidi nitabadilika kuanzia leo. Sitaweza tena kufanya jambo kama hili kwa mara nyingine tafadhani nipe nafasi ya mwisho”
“Bwana mdogo una maneno ya mwisho labda ya kuongea?”
“Usiniu…….” Hakumsikiliza tena, alimfumua na risasi zote ambazo alikuwa nazo na kutoweka hilo eneo, kazi ambayo ilimpeleka huko ilikuwa imeisha, alitoa maagizo kwa vijana wake kwenda kuutupa huo mwili barabarani ili kila mtu auone lakini hiyo ingekuwa meseji pia kwa wenzake ambao wangetaka kuingia kwenye msala kama wa kwake.


******
Ile video haikutua kwenye mikono ya Bashir tu ambaye aliifanyia kazi. Shirika la kijasusi la nchi pia lilikuwa likifuatilia kwa ukaribu sana taarifa hiyo, hivyo baada ya kuiona video hiyo walikuwa makini kufuatilia kila hatua kuweza kujua ni jambo gani ambalo lilitokea huko mpaka mambo yakaishia kwa namna ile.
Yule ofisa wa polisi Ezra walikuwa wakimjua vizuri sana, alikuwa ni kijana ambaye alikuwa ana maono makubwa kuhusu jeshi la polisi ila alikuwa anaponzwa na kitu kimoja, alikuwa na tamaa isiyo mfano, alitamani kufika mbali kwa muda mfupi jambo ambalo lingemletea matatizo makubwa kwenye maisha yake ila yeye wala hakuonyesha kuwa na wasiwasi juu ya jambo hilo.
Taarifa hizo mtu ambye aliamua kuzifanyia kazi ya haraka alikuwa ni Dayana, mwanadada huyo alijua wenzake wapo kwenye majukumu mengine ya kufanya upelelezi mkali hivyo alitaka kufanya kila namna kuhakikisha kwamba anajua alipo bwana Ezra, kumpata ungekuwa mwanzo mzuri wa kuweza kupata habari na taarifa za tukio ambalo lilikuwa likiendelea. Namna pekee ya kumpata kijana huyo ilikuwa ni kudukua namba yake na jambo hilo alilifanyia akiwa ndani ya kituo kikuu cha Osterbay ambapo ndipo kijana huyo alikuwa akifanyia kazi, alikuwa sambamba na mkuu wa kituo kwa sababu alianza kukusanyia taarifa hapo.
Jambo la kwanza ambalo lilimshangaza ni kuona kijana huyo alikuwa akifanya kazi nje ya maagizo ya mkubwa wake, kesi hizo alizuiliwa kabisa kuzifuatilia lakini hakujali bali aliangalia kile moyo wake unamwambia jambo ambalo lilipelekea kuyapoteza maisha ya watu wawili kipuuzi tu.
Simu yake ilionekana maeneo ya Upanga lakini baada ya muda ikaonekana ipo Mbagala, jambo hilo lilimshtua Dayana ikamlazimu kuingia kwenye gari huku nyuma kukiwa na gari ya polisi kuelekea ndani ya eneo hilo ambako ndiko simu ya kijana huyo ilikuwa inaonekana kuwepo. Saba saba kwa Mpili ndipo simu hiyo ilikuwa imegotea, wakati wanakaribia kufika sehemu hiyo waliona watu wengi wakiwa wamesimama pembezoni mwa barabara, watu walijaa eneo hilo na baada ya kuona gari ya polisi walianza kusogea pembeni kwa ajili ya kuwapisha.

Watu hao walikuwa hapo kwa ajili ya kuushangaa mwili wa mtu ambao ulitupwa eneo hilo, mwili huo ulikuwa umechakaa mno kiasi kwamba ulikuwa unatisha hata kuutazama. Mwili ulikuwa ni wa Ezra Ethan yeye akipenda kujiita Double E, zile ndoto zote ambazo alikuwa nazo, ule umaarufu wote ambao alikuwa anausaka ulikuwa umelala na mwili wake, hakuwa hai tena zaidi ilibaki kuwa historia. Swali la msingi likabaki kwamba ni nani alimuua? Kwenye ile video alionekana mwanaume mmoja akimpa msaada, huyo ndiye ambaye alitakiwa kutafutwa ili kuweza kutoa majibu kamili.
“Alikuja kwangu akiwa kijana mdogo baada ya baba yake kufa, aliniomba niwe mwalimu wake nikafanya hivyo. Nimemkuza kwenye misingi ya kipolisi mpaka anakuwa mkubwa akaja kuipenda kazi hii kwa moyo wake wote, alikuwa kijana mtiifu na kijana ambaye alikuwa na njaa ya mafanikio. Hakuwahi kukubali kushindwa jambo lolote mahali popote ambapo angekuwepo, alijiona kuwa mshindi wa kila jambo ambalo alikuwa analifanya
Wakati namuingiza kwenye idara ya polisi nilijitahidi kumlea kwenye misingi iliyo bora, nilimuonya kuhusu siasa na matokeo yake, kila kitu nilimpa somo kuhusu namna ya kuishi ila huenda nilisahau kumpa somo kubwa zaidi la kuinamisha kichwa chini mbele ya wenye vyeo, hakutakiwa kuwa namna hii anapo jiingiza kwenye mikono ya wanasiasa. Wanasiasa hawapendi watu mashujaa, njaa ya kijana wangu ilimfanya kutokuwa mtu wa kusikiliza jambo lolote kutoka kwa mtu mwingine. Hilo ndilo kosa ambalo nitalijutia mpaka siku naingia kaburini” alikuwa anaongea kwa uchungu mkuu wa kituo baada ya kuukuta mwili wa kijana wake ukiwa umedhalilishwa barabarani watu wakipiga picha na kuchukua video.
“Amekufa akiwa bado mdogo sana, kwa ari ambayo alika nayo kwanini usinge jaribu kumleta kwenye shirika letu huku?” Dayana aliongea akiwa anauzunguka huo mwili na kuangalia makovu ambayo yalikuwepo.
“Kwa sababu aliwahi kukataa kabisa kuhusu hilo. Kama nilivyo kwambia hapo mwanzo kwamba kuna sehemu kama mlezi wake nilifeli, nimemfundisha vitu vingi sana kwenye maisha ila nilisahau jambo ambalo huenda ndilo la msingi zaidi. Nilisahau kumfundisha namna ya kuinamisha kichwa na ndiyo sababu hakutaka kabisa kuwepo sehemu kama ya kwenu hiyo.
Shida kubwa kwake ni moja, alipenda umaarufu, alipenda jina lake liwe linatoka kwenye sehemu ambazo watu wanaona. Nyumbani kwake amejaza nishani kibao kwa sababu ya kuwa mfanyakazi bora, jina lake lilikuwa likitajwa sana kwa sababu alikuwa anafanya kazi kubwa na wenzake wanaona, hiyo ndiyo ilikuwa adhma yake kubwa na ndicho ambacho kilimuua hata baba yake mzazi, nadhani inatembea kwenye damu hii. Kazi yenu ninyi ni kazi kubwa sana na ndio ambao mnahakikisha kama taifa tupo salama kwa masaa ishirini na manne kwa sababu bila taarifa zenu muda wote tupo hatarini lakini nani anajali kuhusu hilo?
Hakuna anayejali kwa sababu kazi kubwa ambayo mnaifanya haiwekwi wazi inabaki kuwa siri, watu wanasubiri tu tatizo litokee ndipo waje kuwalaumu tena kwa kuwatukana, yeye hakupenda hayo maisha kabisa. Alitaka kuwepo sehemu ambayo angeonekana muda wote kwa anacho kifanya kisha ashangiliwe”

80 inafika mwisho.

FEBIANI BABUYA.
 
STORY: IDAIWE MAITI YANGU
MWANDISHI: FEBIANI BABUYA
STORYTELLER: BUX THE STORYTELLER
WHATSAPP: 0621567672
EMAIL: thomasibabuya@gmail.com
AGE: 18+

********************
SEHEMU YA THEMANINI NA MOJA
SONGA NAYO................


Mkuu huyo wa kituo wakati akiwa anaendelea na maongezi yake akimuelezea huyo kijana wake ambaye alikutwa amekufa muda huo Dayana mawazo hayakuwa hapo tena, alikuwa mbali kwa wakati huo kwa sababu ujumbe ambao uliingia kwenye simu yake ndio ambao uliweza kumteka na kuyahamisha mawazo na fikra zake.
Alipokea taarifa ambayo haikuwa njema, taarifa hiyo ilimshtua zaidi ya namna alivyokuwa anafikiria lakini kabla hajaongea jambo lolote lile mkuu wa kituo naye alisimama na kuangalia kwenye simu yake, bila shaka naye kuna ujumbe alikuwa ameupata wakati huo. Mkuu wa kituo alimgeukia Dayana na kumwangalia usoni, jasho jembamba lilianza kumtoka usoni akiwa mwingi wa mashaka na hofu, alionekana kukata tamaa.
“Kuna nini?” Dayana alimuuliza bwana huyo, hakumjibu kwa mdomo bali kwa vitendo, alimuonyesha simu yake ili aweze kujionea mwenyewe kwa macho yake ndipo akahamaki, yalikuwa ni mauaji mengine.
Yule bwana ambaye kwenye ile video alioneka akimsaidia afisa huyo wa polisi naye ulikutwa mwili wake, lakini maiti haikuwa hiyo tu bali kulikuwa na zingine mbili. Nyingine ilikuwa ni ya kijana wa kuitwa Brian ambaye alikuwa ana duka lake maeneo ya Kariakoo na mwingine ni kijana ambaye alikutwa ametupwa kwenye jalala na kwa taarifa za haraka alikuwa ni yule ambaye alidaiwa kuhusika kurekodi ile video wakati Ezra anapigana na Othman.
“Huyu mpuuzi ni lazima ndiye kamuua kijana wangu, baada ya kuona ameshindwa kumuua pale ameamua kuwatafuta watu wote ambao wameunganika kwenye hili tukio na kuwaua. Naapa siwezi kumuacha hai lazima nimuue kwa mkono wangu” alikuwa anaapa kwa jazba mkuu wa kituo, Dayana alibaki anamwangalia huku akimsikitikia na kumrudishia simu yako.
“Unajau moja kati ya misingi mikubwa ya mtu kuingia kwenye kazi hizi?”
“Ndiyo, awe mzalendo, muadilifu lakini ajue majukumu sahihi ya kazi yake”
“Kuingia kwenye jeshi la polisi ni rahisi sana ndiyo maana umenipa majibu mepesi mepesi tu lakini kuingia kufanya kazi kama yangu hii na hata yako jambo hili ni mhimu. Usipende kuendeshwa na mihemko kama mtoto wa kike, kuangalia tu video tayari ushahukumu na kutaka kufanya uamuzi, unaweza ukafanya maamuzi sahihi wa idadi ya watu milioni moja kweli wewe kama tu tukio hili unakurupuka namna hiyo?” hakuonekana kuwa mtu wa kutumia akili bwana huyo, alikuwa anaendeshwa na mihemko zaidi ambayo ilikuwa ni hatari kwenye ufanyaji wa maamuzi.

“Ukiangalia kwa umakini kuhusu ushahidi uliopo inakupa jibu moja kwa moja kwamba ni yeye”
“Unahisi kijana wako alikuwa anatafutwa na mtu mmoja? Kwa sababu angekuwa hai yye ndiye alitakiwa kuwa mshukiwa namba moja na hata hivyo anabaki kuwa hivyo. Swali la msingi ni kwamba alijuaje kuhusu watu hawa na hizi taarifa alizipatia wapi? Wewe mwenyewe umezungumza kuhusu wanasiasa hapa, una uhakika gani kwamba sio mwanasiasa ambaye amehusika na hili? Kuna watu wengi ambao wanajaribu kuzima ukweli ambao huenda siku zijazo ukafichuka. Ukijua sababu ya kilicho mpeka kule, ukajua watu ambao walikuwa wanahusika kwenye hiyo sababu na ambao huenda kuna kitu walitaka kisijulikane basi utapata majibu kwamba kijana wako ameuawa na nani”
“Mimi nilijua hili jambo litakuwa chini yenu?”
“Mimi sihusiki na uchunguzi wa kesi za vifo vya maaskari, nitaingia kwenye suala lako kama kutakuwa na taarifa za mhimu ambazo nitazihitaji kutoka huko” Dayana alimaliza na kumuacha bwana huyo akiwa mdomo wazi huku yeye akiingia kwenye gari yake aina ya V8 nyeusi na kutoka hilo eneo kwa kasi kiasi kwamba aliwashangaza watu ambao walikuwa jirani na eneo hilo kwa sababu alionekana kabisa kwamba alikuwa analiwahi jambo fulani la mhimu sana mahali.

Taarifa ambayo iliingia kwenye simu ya Dayana haikuwa njema, ilikuwa ni taarifa mbaya kwake kwa sababu Ismail Mhammed yule tajiri wa Zanzibar alikutwa ameuliwa kikatili mwili wake ukiwa umetupwa pembezoni mwa bahari. Kwenye kifua palitobolewa na shilingi ikawa imapachikwa eneo hilo ikiwa inang’aa sana.
Aliwahi hospitali mahali ambako mwili ulikuwa umepelekwa, hakuelewa ilikuwaje mpaka mtu huyo akakutwa ameuliwa tena ndani ya Tanzania bara wakati mara ya mwisho walimfuatilia mpaka walipo hakikisha ameingia ndani ya boti kwa ajili ya kurudi Zanzibar baada ya kumaliza kumhoji. Jambo hilo lilikivuruga mno kichwa chake lakini akiwa kwenye huo mshangao alipata habari nyingine tena ya kifo.
Aliyekuwa mchumba wa zamani wa Zara ambaye alishindwa kumvumilia mrembo huyo kwa maelezo ambayo yalitolewa na dada yake Zara naye alikutwa akiwa ameuawa kwa kukatwa kichwa chake Zanzibar, jambo hilo lilianza kuashiria hali ya hatari. Kifo cha Ismail alijiona yeye ndiye ambaye alikuwa na hatia kwa sababu ndiye alitoa wazo la kuweza kumteka bwana huyo ambaye ni kweli aliwapa taarifa nyingi sana lakini ziliishia kuyaondoa maisha yake, huenda kama wasingemteka asingekufa! Lakini pia alipingana na jambo hilo kwa sababu kama mkwewe wa zamani aliuliwa Zanzibar maana yake hata yeye pia wakati wake wa kufa ulifika hivyo hata kama angekuwa wapi bado angeuliwa tu kwa namna yoyote ile.

“Why Gavin Luca?” aliongea kwa sauti akiwa anabamiza mkono kwenye usukani wake. Alikuwa anaendesha gari kwa mwendo mkali mno, alifika hospitali na kuwakuta wenzake ambao walijifanya kuwa wafanya biashara wenzake na mfanya biashara huyo ambaye alikuwa ni tajiri mkubwa na ilikuwa inasubiriwa tu taarifa kutoka serikalini ili kifo chake kitangazwe rasmi.

Dayana aliukagua mwili huo kwa umakini, haukuwa na alama sehemu yoyote ile, muuaji alikuwa makini, alikuwa anamjua ambaye alihusika kwenye jambo hilo ndiyo maana hakutaka kabisa hata kuumiza kichwa kujiuliza.
“I need him now?” aliongea kwa sauti kali akiwa anafoka, akasahau kwamba alikuwa hospitali lakini Bariki Dumba akiwa kwenye suti yake safi na begi mithili ya mnunuzi wa madini alimsogele mwanadada huyo na kumpa kikaratasi kidogo ambacho kilikuwa na maelezo. Aliipokea barua hiyo akiwa anauma meno, alikuwa ana hamu kubwa ya kukutana na bwana huyo wa kujiita Gavin, ni yeye ambaye alikuwa anawafanya wasilale na muda wote waishie kupewa lawama tu. Mungu alikuwa amejibu maombi yake kama ambavyo alitarajia Gavin alikuwa ametuma ujumbe huo kwa mwenzao kuwapa taarifa kwamba usiku wa siku hiyo alikuwa na maongezi nao yaani hilo kundi la THE INVISIBLE.

Dayana alibaki amepigwa na butwa kabla hata ya kumaliza kusoma, alimgeukia bwana huyo ndipo akakumbushwa kwamba ile siku pale uwanja wa ndege bwana yule aliiba kitambulisho cha mmoja wao, kufanya hivyo maana yake alizipata taarifa zake zote mpaka wakati huo ndio maana alijua kila kitu kuhusu hilo kundi lao hivyo kwenye kikaratasi hicho kulikuwa na maelezo kwamba bwana huyo alihitaji kufanya nao mazungumzo ya amani kwa sababu hakuona kama wanahusika kwenye jambo hilo. Kama wangekubali kukutana naye basi angewaacha hai ila kama wangegoma basi yeye asingekuwa na chaguo lingine zaidi ya kuwaua.

“Hahahha hahahaha hahahaa hatimaye nimekupa Gavin, naapa kwa jina la mama yangu kaburini sitakuacha, I’m going to kill you myself” uje ujumbe kwake aliutafsiri kama dharau kubwa, ilikuwa ni dharau kwa sababu raia hakuwa na hiyo jeuri ya kulitishia shirika la kijasusi na kudai kwamba analipa nafasi.
“Pumbavu zake!” Dayana alitamka tena akiwa ameghafilika, mwanaume huyo alikuwa akiwaumiza sana vichwa, hakuwa tayari kumuona anafanya huo upuuzi tena. Habari hiyo kwake ilikuwa ni njema mno kwa sababu alikuwa anaenda kulitaua tatizo ambalo lilikuwa ni kero kwao kwa muda mrefu na yeye binafsi alikuwa amemchoka bwana huyo, hayo mazungumzo hata yasingefanyika bali angehakikisha anamfanya Gavin kujuta maisha yake yote na hakuwa na mpango wa kumkamata tena bali aliapa kwamba angemuua kwa mkono wake mwenyewe.
“We are ready and we’re going to do this” aliongea kijasiri lakini moyoni hakuwa na amani, hakuwa na amani kwa sababu alikuwa anaenda kukutana na binadamu aliye daiwa kuwa hatari mno, binadamu ambaye aliwadanganya kuhusu kifo chake, binadamu ambaye alikuwa anaimbwa kila kona lakini zaidi ndiye alikuwa mtu tajiri zaidi ndani ya bara zima la Afrika baada ya kurithi utajiri wa baba yake. Isingekuwa kawaida kukutana na mtu wa namna hiyo, alikuwa anajiamini mbele ya vijana wake ila kuna namna kwenye moyo wake hakuwa na amani na nafasi ya uwoga kidogo ilikuwa inamvamia taratibu.

81 inafika mwisho.

FEBIANI BABUYA.
 
STORY: IDAIWE MAITI YANGU
MWANDISHI: FEBIANI BABUYA
STORYTELLER: BUX THE STORYTELLER
WHATSAPP: 0621567672
EMAIL: thomasibabuya@gmail.com
AGE: 18+

********************
SEHEMU YA THEMANINI NA MBILI
SONGA NAYO................


********
Sarah kwa mara yake ya kwanza alikuwa anakutana na Gavin Luca kwa ajili ya kufanya mazungumzo ya kawaida ukiacha mara ya kwanza ambayo walikutana kule msituni na mwanaume huyo akafanya ukatili ambao ulimuacha mdomo wazi Sarah lakini bahati ilikuwa upande wake yeye kwa sababu alifanikiwa kumuacha akiwa mzima kabisa wa afya. Mwanaume huyo alikuwa anaiangalia picha moja ya mwanaume ambaye alikuwa kama yeye lakini hatua za binti zilimfanya aitoe na kuihifadhi sehemu safi ambalo ilitengenezwa vizuri.
“Angekuwa kama unavyo niona hivi kama angekuwa hai mpaka leo. Tumepishana dakika kadhaa tu na kaka yangu, mtu ambaye binafsi nakiri kwamba alikuwa bora kwa kila kitu kunizidi mimi, Mungu alimpendelea vitu vingi kiasi kwamba hata haya maisha ya mavurugu hakuyazoea wala kupenda lakini hivi ninavyo ongea na wewe hayupo kwa sababu kuna watu waliona kuishi kwake ni usumbufu, wakayabeba maisha yake.” Alizungumza akiwa anageuka kuangaliana na mwanamke huyo lakini Sarah hakuwa na huo ujasiri wa kutazamana na hicho kiumbe.
“Usioniogope Sarah mimi ni mwanadamu kama wewe tu ambaye nimezaliwa na mwanamke pia, mimi sio mashine kiasi kwamba nimetengenezwa kama watu ambavyo wanazusha kwenye mitandao. Kama ilivyo asili kwamba kila kizaliwacho ni lazima kife hivyo hata mimi nitakufa kama watu wengine ni muda wangu tu huenda bado haujafika”
“Kama wewe upo hai yule ambaye alifia kule msituni ni nani?” Sarah aliuliza akiwa anatetemeka lakini mwanaume huyo siku hiyo hakuwa kama yule mkatili, alikuwa mkarimu hivyo alimkaribisha binti huyo kiti kwa sababu alijua kabisa ana maswali mengi ambayo alihitaji kuyapatia majibu kuhusu yeye.
“Unatakiwa kuijali afya yako kwanza kabla ya kuwaza jambo lingine lolote lile, unaendeleaje kwa sasa?”
“Mimi ni mzima wa afya kabisa”
“Lakini hauonekani kuwa mzima wa afya kama ambavyo unajitanabaisha Sarah”
“Maana yangu ni kwamba nitakuwa sawa”
“Kabla ya kukujibu maswali yako nina swali moja la mhimu hapa ambalo nataka unithibitishie”
“Unaweza ukauliza tu”
“Ni kweli mkuu wa majeshi ndiye alikutuma wewe ukamuue mke wa raisi?” Sarah jambo hilo lilimshtua hakutegemea kama angeulizwa hilo swali na huyo bwana.
“Ndiyo, ndiyo” alijibu kwa kubabaika.
“Kwa sababu zipi?”
“Hata mimi sijui mpaka nilipo jikuta naingia kwenye kesi hii na nilifanya yote ili tu kuhakikisha kwamba familia yangu inakuwa salama”
“Naweza nikakupa nafasi kama ukitaka”
“Unamaanisha nini?”
“Naweza nikakuletea mkuu wa majeshi ukajua wewe mwenyewe cha kufanya naye”
“Kirahisi tu hivyo?”
“Ndiyo maana nimekwambia nakupa hiyo nafasi ila kama hauitaki unaweza ukaikataa pia hakuna tatizo”
“Kama ni kweli, ningependa iwe hivyo”
“Leo usiku naenda kukutana na TIGI”
“Unamaanisha shirika letu la kijasusi?”
“Ndiyo”
“Sidhani kama ni wazo zuri kwa sababu wale watu wanakutafuta kuliko hata pesa na ukijitokeza tu mbele yao basi kuna hatari kubwa unaweza usirudi tena”
“Mimi naenda kuwapa nafasi ya kuwaacha hai, hakuna hata mmoja ambaye anatakiwa kuingilia kwenye kazi ambayo nataka niimalize ndani ya siku chache zilizo bakia. Hilo ndilo jambo ambalo nataka kukutana nao ili tuingie makubaliano, siwaoni wakiwa watu ambao wanastahili kufa kwa mkono wangu lakini kama atatokea yule ambaye atahitaji ilwe hivyo basi nitafanya hivyo kwa sababu kwenye maisha yangu huwa sina nafasi ya pili kwa sababu ya kuokoa muda na watu wajifunze.

Huwa ninatoa nafasi moja tu na baada ya hapo ukishindwa kuitumia nafasi hiyo basi usitegemee kama kuna nafasi nyingine unaweza ukaipata tena kutoka kwangu. Kuhusu usalama wangu hata usiwaze kabisa kwa sababu wale ni wadogo sana, hakuna hata mmoja kati yao ambaye anaweza kufanikiwa kuigusa hata kola tu ya shati yangu ila naona wanakuja kwenye njia yangu sitaki lawama hapo baadae”
“Unapaswa kuwa makini sana kwa sababu kuanzia jeshini mpaka kwa watu wa usalama wanasubiri ufanye kosa moja tu wapite na wewe. Kwenye kila sehemu ambayo unakuwepo unatakuwa kuwa makini kuliko unavyo fikiria kwa sababu hawa watu wamewaweka watu wao kila kona kitu ambacho kinawafanya kupata taarifa nyingi kwa wakati mmoja tena haraka sana”
“Turejee kwenye swali lako la msingi” Gavin alionekana kuyapuuzia mawazo ya Sarah hivyo akamtaka warudi kwenye msingi wa maada ya kwanza ili waweze kumaliza moja.
“Ni muda mrefu sasa umekuwa ukituchanganya kiasi kwamba mpaka leo kuna watu wanaamini wewe umekufa, kuna watu hawajui kama mpo wawili lakini mwisho wa siku kuna mtu tulimuua ambaye ana mfanano na wewe. Nataka kujua kama wewe upo hai na mzima wa afya kabisa, yule mtu ambaye alikufa siku ile tulimuua kule msituni ni nani? Sarah aliliweka swali lake vizuri zaidi, ila alikuwa na tahadhari kwa kila alichokuwa anakitamka kwenye mdomo wake.
“Yule ambaye alikufa kule msituni anaitwa Haizulu Mtemwa, ni mwanaume ambaye amezaliwa huko Mbeya vijijini. Nilikutana naye miaka sita iliyopita, huyu bwana ni moja kati ya wahanga wa ile serikali ambayo ilimfanyia ushenzi baba yangu, ni moja ya watu ambao walidhulumiwa maeneo na mali zao zote ambazo baba yake mzazi alihangaika kuzitafuta kwa jasho enzi za uhai wake.
Kuna oparesheni maalumu ambayo niliianzisha ya kutaka kusaidia watu wote ambao walikuwa wahanga wa ile serikali, nilikuwa naangalia watu ambao waliathirika kwa ukubwa na ile serikali, mpaka sasa nimefanikiwa kuzisaidia familia elfu kumi na tano ambazo nazikumbuka kichwani lakini huyu bwana kesi yake ilikuwa ni tofauti kabisa na wengine kwani alikuwa mtu mwenye uchungu mkubwa kwenye maisha yake.
Familia yake haikuishia tu kufanyiwa ukatili wa kuweza kusimulia bali mke wake alibakwa mbele ya macho yake na hata alipo jaribu kwenda kushtaki juu ya jambo hilo yeye ndiye aliishia kufungwa jela. Hilo nimegusia la familia yake yeye mwenyewe ukiacha ya baba yake, akiwa jela ndipo alipatwa na makubwa zaidi ya yale ambayo aliyaacha wakati anaondoka, jela alikaa mwaka mmoja tu akaachiwa kwa sababu kesi yake danadana zilikuwa nyingi.
Bwana huyo alimkuta mkewe ameuawa na familia yake yote isipokuwa binti yake ambaye aliishia kuwa wa mtaani, hakuwa na mtu wa kumjali wala kumhudumia hivyo alikuwa akila jalalani na makombo ya vyakula, najua hauna mtoto bado ila kama ungekuwa naye haya ambayo nakwambia abadani usingetamani uje kuyasikia kwa mwanao. Bwana yule lile jambo lilimfanya atake kujiua wakati ule ule, alilia kama mtoto mdogo kukutana na hali ambayo alikuwa anaishi nayo mwenyewe. Alimchukua mtoto wake na kuanza kuhangaika naye mpaka safari yake ilipotua Iringa mjini akiwa anampambania mtoto wake mimi nilimpatia huko.
Hakuna mwanaume anakuwa na hasira ya maisha kama mwanaume ambaye ana sababu ya msingi ya kuweza kuishi hususani kama ana mtoto ambaye ametoka naye mbali. Yule bwana alikuwa anafanya kazi ngumu isivyokuwa kawaida kwa ajili tu ya binti yake lakini kwa bahati mbaya sana wakati yupo jela alipata kansa kutokana na maisha ambayo alikuwa anayaishi kule hakulijua hilo mpaka hali yake ilipo anza kubadilika badilika na ndio wakati ambao mimi niliipata historia ya familia yake kwa mkono wangu ndipo nikafanya uamuzi wa kumuweka karibu yangu.

82 inafika mwisho.

FEBIANI BABUYA.
 
STORY: IDAIWE MAITI YANGU
MWANDISHI: FEBIANI BABUYA
STORYTELLER: BUX THE STORYTELLER
WHATSAPP: 0621567672
EMAIL: thomasibabuya@gmail.com
AGE: 18+

********************
SEHEMU YA THEMANINI NA TATU
SONGA NAYO................


Baada ya kumkuta kwenye hali ile iliniuma sana, nilimpatia kila kitu kwenye maisha yake, nilimpatia mali nyingi sana ambazo zote ziliandikwa kwa jina la binti yake. Nilimtaka ataje vitu vyote ambavyo alikuwa anatamani kuvifanya kwenye maisha yake na mimi ningevifanya kwa naiba yake. Yule ndiye mtu wa kwanza kwenye maisha yangu mimi kumuamini na kumpatia siri zangu zote, yule alikuwa anajua kila kitu kuhusu mimi, hakuna taarifa yangu hata moja ambayo hakuwa nayo ila alikuwa na ombi moja kwangu baada ya kugundua ile mipango yangu ambayo ilikuwa mezani.
Haizulu hakutaka kufa bila kuwa msaada kwangu, aliomba angalau angepumzika kwa amani kama angekufa akiwa anarudisha asante kwangu ndipo yeye akaja na lile wazo la mimi kwenda huko Kenya ndani ya ule msitu wa Mau. Sasa kwanini nilitakiwa kwenda mimi lakini ambaye amekufa kule ni yeye? Kipindi kile kuna baadhi ya watu walianza kusambaza taarifa maeneo mbali mbali wakieleza kwamba sisi tulizaliwa wawili hivyo aliyekufa hakuwa mimi, habari hizo wengi walizupuuzia lakini zilikuwa za kweli na mpango wake ndio ambao umenifanya nikapiga hatua kubwa sana.
Kuna watu ambao mimi nawatafuta lakini kwa miaka yangu yote ambayo niliwatafuta sikuwahi kuwapata mpaka nilipo ikamilisha ile adhma yake ya yeye kujiua kwa ajili yangu, sasa ilikuaje? Mpango ulikuwa ni kwamba tuvujishe siri kwa baadhi ya watu kwamba mimi Gavin Luca nipo hai, tulijua kabisa kwamba zile habari zingewagawa kwenye makundi mawili, kundi moja lingekuwa ni lile kundi ambalo lingeamini moja kwa moja lakini kundi la pili ni lile kundi ambalo lisingeamini kuhusu taarifa hizo, sasa hesabu zetu zilikuwa kwenye hilo kundi ambalo lingeamini habari hizo na kama lisingeamini basi tulihitaji tu wachukue tahadhari maana yake wasingeacha jambo hilo lipite na bila shaka nyie kama jeshi mliingia kwenye kundi ambalo sisi tulikuwa tumelilenga.
Tulielewa kabisa kwamba kama kundi hilo moja lingeamini basi mara moja ungeanza msako ili kuhakikisha hakuna makosa yanafanyika huku nikiwa naonekana mara moja moja baadhi ya maeneo ili kuwahakikishia kwamba BADO NINAISHI mkaingia kwenye huo mtego. Lengo lilikuwa kwamba wakati ambao mngekuwa mnanitafuta mimi mngeanza kujiaminisha kwamba mimi nipo hai hivyo mngepambana muweze kunipata lakini baada ya kunipata ni lazima watu kadhaa watake kuniua ili kumaliza utata huo hivyo baada ya mimi kufa mngehisi yale yote yameisha tayari. Mimi nilinufauika vipi na hilo?
Siku zote adui yako akishajua amekumaliza huwa anaanza kutamba, atataka mitaa iitambue furaha yake kwa sababu ile hatari yake haipo tena na hapo niliamini kwamba lazima kuna makosa wangeyafanya ningeanza kuwapata watu wangu ambao walijificha kwa miaka yote ambayo niliwasaka bila mafanikio yoyote yale. Nilikuwa na uhakika taarifa za kifo changu zingewaibua wengi kwenye maficho na hao wangenisaidia mimi kufika na kumpata yule ambaye najua ndiye alikaa chini akauandaa huu mchezo mzima.
Na ndio ule wakati ambao kijana Michael alikabidhiwa kile kikosi wewe mwenyewe ukiwemo kuanza kunitafuta mpaka mlipo fanikiwa kumpata Haizulu mkidhani ni mimi. Wakati tumeuandaa ule mchezo ilinilazimu nimfue kwanza ili asiwe lege lege, angekuwa legelege lazima mngeshtuka kirahisi ndiyo maana hata siku mnampata mliwapoteza watu wenu kadhaa, hakuwa mtu dhaifu kwa sababu nilimtengeneza kwa mikono yangu mwenyewe. Baada ya kukamilika kwake ndipo tukamfanyia oparesheni ya kumbambikia sura yangu, tulihakikisha kunakuwa na mfanano mkubwa kwenye kila kitu ili asije kushtuka mtu yeyote yule. Huo ndio ulikuwa mpango wake yeye kutoa asante kwangu kwa sababu alijua amebakisha miaka michache ya kuishi hivyo aliitafuta furaha ya kufa nayo na hilo kwake akaona kabisa kwamba linamfaa.
Hilo ni jambo ambalo binafsi nililipinga sana ila alisisitiza kufanya hivyo, kwake aliona kama ni neema na bahati ya pekee kufanya na kulitimiza hilo kwa sababu hisia za moyo wake zilikuwa zinamtuma kufanya kitu kama hicho. Nadhani kwa sasa utakuwa umepata jibu kuhusu mkanganyiko wako wa kujua kwamba mlimuua nani badala yangu mimi”

Mwanaume aliidadavua historia na fumbo zito ambalo lilikuwa linawaumiza watu kwamba ni kwanini mtu huyo walimuua halafu bado akaonekana akiwa hai tena, kiukweli hakuna mtu ambaye alikuwa anaamini kwamba ni sayansi watu walihisi ni mzimu wake labda lakini hapo alifunguka akili na kuelewa mchezo mzima ulisukwa vipi na watu hao wenye akili zao ambao waliuandaa nao ukakubali kama walivyokuwa wameutaka uwe.
“Hii ndiyo stori ya kutisha zaidi kuwahi kuisikia kwenye maisha yangu, moyoni nazidi kujawa na hofu, mlifanya jambo la hatari sana kwa mwanadamu wa kawaida hakuna ambaye anaweza kuja na mpango kama huo”
“Mhhhh bibie kwenye kuzunguka kwangu dunia nimegundua kwamba matukio makubwa ya kutisha watu wengi hawayajui kwa sababu mnasubiri yaripotiwe kwenye vyombo vya habari ndipo myasome. Huu ulimwengu una sehemu za kutisha na binadamu ambao ni hatari hata kuongea nao tu, nimeishi China kwa miaka kadhaa, kuna mambo nimeyashuhudia kule sikuwahi kuhisi kwamba yanawezekaan hapa duniani. Siku zote mwanadamu huwa anapenda kukiamini kitu mpaka akili yake inapo ishia, eneo ambalo akili yake haiwezi kufika hata akiambiwa vipi huwa hawezi kukubali kwa sababu anahisi ni zile nomino za dhahania na watu wa hivyo wengi huwa wanajifanya wajuaji na wabishi sana”

“Bado haiifanyi stori kama hii kuwa ya kawaida, kila mtu mpaka sasa huwa anajiuliza lile jambo linawezekana vipi, ndiyo maana licha ya kuonekana maeneo kadhaa ukiwa unaua watu, kuna watu bado wanaamini kwamba wewe umekufa na hawakubali kabisa kama upo hai, kwa sasa naanza kuwaelewa ni kwanini wanafikiria hivyo”
“Na hilo ndilo nilikuwa nalitaka tangu mwanzo kwa sababu limenifanya nimewapata watu wangu wengi sana na hivi sasa natarajia kumaliza kazi hii sitaki kuja kuanza kuua watu tena ndiyo maana sitaki kuacha mtu hata mmoja nyuma kwa sababu najua haya mambo yatakuja kurudi upya tena. Nataka nihakikishe nawamaliza wote ndipo naenda kupumzika jumla na sitakuja kuonekana sehemu yoyote ile duniani”
“Unampango wa kufanya jambo gani mpaka usije kuonekana tena?”
“Hilo haupaswi kulijua kwa sababu halina faida yoyote kwako”
“Naweza kujua kwamba yule binti aliishia wapi, kwa sababu kama baba yake alijitoa kifo lazima alikuwa na imani kwamba anamuacha binti yake kwenye mazingira mazuri na ya kueleweka ili asije kuteseka”
“Yule ni binti ambaye ataishi maisha mazuri na kizazi chake chote, ana bima ya maisha na nimempeleka mbali sana kiasi kwama hakuna mtu atakuja kujua kama aliwahi kuwepo labda kama atakuja kuamua kurudi mwenyewe tena Tanzania kipindi akiwa mtu mzima ila kwa sasa hakuna mtu anaweza kumpata. Nilifanya kama namsaidia ni binti yangu”

“Nashukuru sana kwa kuniamini na kuwa muwazi kwangu mpaka umenipa taarifa kama hizi ambazo huenda sikustahili kabisa kuzipata ama kuwa nazo ila jambo kubwa zaidi ambalo huwa linanifanya nikilala niwe na mawazo mengi ni lile la wewe kunipa nafasi ya kuishi wakati ulikuwa na uwezo mkubwa tu wa kuweza kuyabeba maisha yangu. Nimejiuliza sana hili swali kiasi kwamba nilitamani siku moja niweze kuonana na wewe ili nikuulize moja kwa moja huenda kama ukinijibu moyo wangu unaweza kutulia kwa sababu nitaijua sababu ya mimi kupata nafasi nyingine ya kuishi ukiacha lile la kunipa pesa nyingi ambazo zijawahi kuzishika kwa pamoja mimi kama mimi tangu nizaliwe. Begi lilikuwa na zaidi ya pesa za kitanzania milioni mia tano, hili nalo lilinitisha sana” Sarah bado alionekana kuwa na mengi ya kuzungumza na mtu huyo hivyo nafasi hiyo hakutaka kuweza kuichezea vibaya, alihitaji kuitumia vyema kumaliza dukuduku lake ambalo alikuwa nalo moyoni.
“Moja ya vitu amnavyo nimewalisha hata vijana wangu ni kufanya maamuzi ukiwa na uhakika na taarifa sahihi za unacho kiamualia hayo maamuzi yako. Hautakiwi kufanya maamuzi kwa sababu tu umejisikia kufanya hivyo, hilo ni jambo la hatari na unaweza kuja kujuta ukiwa umechelewa hivyo binafsi huwa sishauri kabisa mtu kufanya hilo kosa. Mimi mpaka nafikia uamuzi wa kufanya yale maamuzi tayari nilikuwa najua aina ya watu ambao nilikuwa nawaua, nilikuwa nina taarifa zao wote ndiyo maana hata taarifa za kujua wapi nilipo kule msituni ni mimi nilizivujisha nikaamua hata kufanya jukumu la kuhifadhi silaha na kuacha ujumbe kule kwa sababu nilijua kuna watu wataupata ili uendelee kuwachanganya zaidi.
Niliisoma historia nzima ya maisha yako, niliona jinsi ambavyo umeteseka kufika pale ulipo, hakika kwa mtoto wa kike ulikuwa unastahili pongezi zisizo na mipaka, ni mabinti wachache wana huo uthubutu. Lakini hilo pekee halikuwa jibu la kukupa nafasi nyingine ya kuishi kwa sababu kuna watu wamekua kama wewe lakini baadae wakaja kuwa washenzi hawa huwa siizingatii sana historia zao, kama anastahili kufa basi ni lazima tu afe. Jambo la msingi zaidi ambalo lilinivutia kwako ni uzalendo wako kwa taifa lako, jinsi ulivyo mwema na mpenda kusaidia watu. Huwa unajitoa hata kwa kidogo ulicho nacho. Huna kikubwa ila umekuwa msaada kwa watu wengi, hupendi kuona mtu anaonewa kwenye haki yake, hupendi kuwa sababu ya matatizo kwa watu.

83 inafika mwisho.

FEBIANI BABUYA.
 
Hii kitu ina mafunzo mengi sana hata kwenye maisha yetu ya kawaida kabisaa ya kila siku.
Kazi safi sana mkuu
 
Stori tamu sana
Umeniacha na arosto mkuu ifanye kuisogeza kidogo wikiendi hii mkuu
 
Back
Top Bottom