Siri: Kiini cha mgogoro unaofukuta ndani ya Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) Dayosisi ya Konde

Siri: Kiini cha mgogoro unaofukuta ndani ya Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) Dayosisi ya Konde

ULAFI WA FEDHA "SADAKA", UCHU WA MADARAKA, MAJUNGU, VISASI NA HILA CHANZO CHA MIGOGORO INAYOIDHOOFISHA MAKANISA YA KIPROTESTANT HUSUSANI KKKT. JE NINI KIFANYIKE?

Na Remmy Cameroon

Nimesema mara si moja na leo narejea tena kusema hili peupe. Zipo sababu nyingi sana za migogoro ndani ya Kanisa lakini kwa makanisa ya Kiprotestant (Protestant Churches) ikiwemo KKKT sababu Kuu iliyoko uchi ambayo hata ukiivika nguo haifichiki wala kusitirika ni ulafi wa fedha "sadaka" na uchu wa madaraka. Hiki ndicho chanzo kikuu cha migogoro inayoitafuna, kuibomoa na kuidhoofisha KKKT.

Jinamizi la migogoro, vita, chuki, mapigano na mauaji wamekuwa ndugu pacha usioweza kuwatenga na Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT). Ni kama pande mbili za sarafu zisizoweza kutenganishwa.

Ndani ya KKKT njia ya rahisi sana ya kupata madaraka ni kuanzisha mgogoro ndani ya Dayosisi na Suluhu ya mgogoro huo inakuwa ni ama kuanzushwa Dayosisi Mpya au Askofu aliyepo madarakani na washirika wake kufukuzwa kama MBWA KOKO, kudhalilishwa, kutukanwa na hata kuvuliwa Uchungaji na hatimaye kupoteza hadhi ya kuwa Askofu.

Dayosisi nyingi kama sio zote ndani ya KKKT huwa hazianzishwi kwa hitaji la waumini au matakwa ya waumini bali kwa matakwa ya Viongozi waliojawa uchu na uroho wa madaraka na ulafi wa fedha "sadaka". Waumini huwa wanatumika kama magreda tu ya kuchimba barabara na Dayosisi ikishapatikana waumini hupakiwa pembeni hawana sauti wala nguvu ya kumhoji tena Askofu na washirika wake.

Labda tujikumbushe kidogo tu kwa uchache migogoro ndani ya KKKT.

1. Mgogoro wa uchu wa madaraka uliopelekea vita ya kukatana mapanga, mashamba kuchomwa moto, mazao na mali kuharibiwa wakati wa harakati za Viongozi wachache waliokuwa na uchu wa madaraka wakishinikiza kujitenga kutoka Dayosisi ya Kaskazini ili kuanzisha Dayosisi ya Meru kati ya mwaka 1990 hadi 1993.

Baadhi ya Wachungaji waliokuwa na uchu wa madaraka na ulafi wa sadaka walianzisha vuguvugu la kujitenga kutoka Dayosisi ya Kaskazini wakipinga mgawanyo usio sawa wa rasilimali na miradi. Huku waumini Kondoo wakitumiwa kama kichaka, mwavuli na ngao yao katika vita hii ya kusaka kushibisha MATUMBO yao.

Hii ni moja ya Dayosisi iliyozaliwa kwa ncha ya upanga, kwa kima cha damu huku Viongozi wake mikono yao ikinuka damu na machozi ya watu na wao Viongozi wakifunika mikono yao unayonuka damu kwa kutumia majoho meupe na yale ya damu ya Mzee.

Katika vita hii ya Dayosisi ya Meru kiliumana kweli kweli, waliokuwepo katika uwanja wa mapambano hususani mstari wa mbele wa mapambano ungeweza kudhani ni vita vya kidini baina ya dini mbili tofauti au madhehebu mawili tofauti kumbe ni vita vya wenyewe kwa wenyewe ndani ya KKKT.

Polisi hususani kikosi cha kutuliza ghasia "FFU" kilikuwa na kazi ya ziada wakati ule hadi aliyekuwa Waziri wa mambo ya ndani na Naibu Waziri Mkuu, Augustine Lyatonga Mrema alipoamuru nguvu ya dola kupita kiasi kutumika ili kuepusha mauaji na madhara zaidi kuendelea kutokea.

Wachungaji waliokuwa na uchu wa kupata madaraka walipopata walichokihitaji vita vikakoma, wakati wao wanafurahia madaraka yaliyotokana na kima cha damu, waumini wakabaki wakiugulia kutazama makaburi ya wapendwa wao, ulemavu wa kudumu walioupata wakigombea Dayosisi na uharibifu wa Mali.

2. Mgogoro mwingine unaofanana na huo ni wa Dayosisi ya Pare, uliotokana na vuguvugu la Wachungaji wa KKKT upande wa Wilaya ya Mwanga kufanya mchakato wa kuzaliwa kwa dayosisi mpya ya Mwanga, ambao baadaye ulizimwa na KKKT makao makuu wakati huo Mkuu wa KKKT akiwa ni Askofu Malasusa.

Hali hiyo iliibua mvutano wa miaka 18 uliosababisha matukio ya uvunjifu wa amani, zikiwamo nyumba kuchomwa, watu kutupwa gerezani, kushtakiwa mahakamani hadi mwaka 2016 ambapo dayosisi hiyo ya Mwanga ilizaliwa na kuhitimisha safari ya miaka 18 iliyoshuhudiwa wachungaji wakitengwa na Kanisa.

Dayosisi ya Pare ilizaliwa kwa kima cha damu na jasho. Waumini masikini wamebaki na makovu ya kupigwa, kuchomewa nyumba na hata kufungwa gerezani huku Wachungaji wakigawana vyeo na kufurahia sadaka za waumini masikini.

Katika mgogoro huu Viongozi wachache sana wenye uchu wa madaraka waliwatumia waumini na kuwapiganisha wenyewe kwa wenyewe ili kuhakikisha wanapata madaraka.

Waumini hususani kutoka wilaya ya Mwanga wakiaminishwa kuwa Askofu wa Dayosisi ya Pare ndiye anayehujumu maendeleo ya miradi ya Dayosisi iliyopo Wilaya ya Mwanga hivyo wakaahidiwa Dayosisi ikipatikana miradi yote itafufuka mara na waumini watapata kazi.

Matokeo yake Dayosisi ikapatikana, hakuna mradi uliofufuka wala kuanzishwa hata wa choo cha shimo, wenye uchu wa madaraka wakayapata wanakula maisha huku waumini waliopiganishwa wakibaki mdomo wazi na zaidi sana wakitwisha mzigo wa kulipa madeni yaliyokopwa na Viongozi wa Dayosisi ya Pare kwa kichaka cha Kanisa lakini mikopo hiyo ikienda kufaidisha familia zao na sio Kanisa.

Katika mgogoro huu Viongozi mbali mbali walidhalilishwa, kutukanwa, kupigwa na hata kufukuzwa huku mamia ya waumini wakijeruhiwa, mali kuharibiwa, miradi ya Kanisa ikiwemo shule, hospitali na vyuo kuhujumiwa.

Waumini wakitumika kama wapiganaji wa mstari wa mbele chuki zikapandikizwa. Ndugu na ndugu wakawa hawasalimiani wala kuzikana. Jirani na jirani wakawa hawasalimiani.

Ni wakati wa mapambano makali ya kusaka Dayosisi ya Mwanga kiliundwa kikosi cha mapambano kilichoitwa Kosovo kikiwa mahsusi kwa ajili ya kuwashughulikia wote waliokuwa wanapinga namna Dayosisi ya Mwanga inavyotafutwa.

3. Mgogoro mwingine ulioibuka ulikuwa ni Dayosisi ya Kaskazini Mashariki mwaka jana na kushuhudiwa Ofisi ya Mkuu wa Kanisa ikiunda kamati ya maaskofu wastaafu wanne, kusimamia uchaguzi wa askofu mpya wa dayosisi hiyo.

Mgogoro wa wenyewe kwa wenyewe ndani ya Dayosisi ya Kaskazini Kati ukichochewa na kikundi cha watu wenye maslahi binafsi walioitwa "Wanaharakati wa wa Dayosisi". Hakuna asiyejua kuwa msingi wa mgogoro huu ni uchu wa madaraka tu. Dayosisi hii ilikuwa ikiongozwa na Askofu Stephen Munga.

Hata hivyo, licha ya uchaguzi wa askofu kufanyika na Askofu Mbilu kuchaguliwa kuwa Askofu Mpya, mgogoro uliendelea kwani Novemba mwaka huu halmashauri kuu ya dayosisi hiyo ilimsimamisha uchungaji Askofu Munga sambamba na wachungaji wengine saba akiwemo mkewe Mch. Dk. Aneth Munga waliokuwa enzi za Dk Munga.

Kwa tukio hilo Askofu Munga anapoteza sifa ya kuwa "Askofu Mstaafu" hivyo hawezi kutokea kama Askofu katika tukio lolote.

4. Mgogoro wa wenyewe kwa wenyewe kati ya Jimbo la Mufindi na Dayosisi ya Njombe: Ukifuatilia mgogoro uliopo baina ya Jimbo la Mufindi na Dayosisi yao ni kuwa tayari kuna Wachungaji ndani ya Jimbo la mufindi tayari wameshajipanga kuutaka Uaskofu na madaraka mengine hivyo wanataka Dayosisi kwa jasho na damu. Tunavyojadili hapa tayari Mkuu wa Jimbo la Mufindi ameshajipanga kuwa Dayosisi ikipatikana yeye ndiye Askofu na ameshapanga safu ya atakaowapa madaraka lakini kwa sharti la kuhakikisha kwanza wanamketisha katika kiti cha Uaskofu. Rushwa ya ahadi ya madaraka na vyeo. Ni ulafi tu wa sadaka.

Wakati huo huo Askofu wa Dayosisi ile naye anaona mapato (sadaka) yatapungua hivyo anaweka ngumu yeye na washirika wake ili ulaji wao usiguswe. Ni ulafi wa sadaka na uchu wa madaraka mtupu.

5. Mbali na huo, uliwahi kuibuka mgogoro ndani ya Dayosisi ya Ziwa Tanganyika, ulioanza 2017 kati ya washarika wa Mpanda na uongozi wa dayosisi, ambapo washarika walipinga kuhamishwa kwa mchungaji wao, Calvin Kessy.

Mgogoro huo ulifikia hatua mbaya Mei 2018, baada ya baadhi ya waumini kumzuia Askofu wao, Ambele Mwaipopo kuingia Usharika wa Sumbawanga mjini na inaelezwa tukio hilo liliambatana na msafara wake kurushiwa mawe. Orodha ni ndefu. Hata mgogoro wa sasa wa Dayosisi ya Konde msingi ni huu huu tu wa ulafi wa Fedha na uchu wa madaraka.

Usisahau mgogoro wa kusaka Dayosisi Mpya ya Manyara uko jikoni nako Wachungaji wameshajipanga kwenye safu za uongozi. Naambiwa pia ndani ya Manyara hiyo hiyo kuna Jimbo ambalo nalo linataka Dayosisi yake. Vita vya madaraka na fedha hivi, hakuna mgogoro wa kiimani au namna ya kuabudu hapa.

Hili nalirudia tena na kulisema kwa kinywa kipana. Dayosisi nyingi ndani ya KKKT huwa hazianzishwi kwa hitaji la waumini au matakwa ya waumini. Hata hii migogoro inayoendelea kinachotakiwa na hawa viongozi walafi na wenye uchu wa madaraka ni kuzaliwa Dayosisi mpya ili wao na magenge yao, wake zao na watoto wao wale na kuishi kwa anasa. Waumini huwa wanatumika kama magreda tu ya kuchimba barabara na Dayosisi ikishapatikana waumini hupakiwa pembeni hawana sauti wala nguvu ya kumhoji tena Askofu na washirika wake.

Wakati wa mapambano ya Dayosisi waumini hutumiwa kama Askari mazuzu ambao huoiganishwa wao kwa wao, kuuana wao kwa wao, jirani na jirani kutosalimiana wala kuzikana. Baada ya kupigania Dayosisi ikipatikana wapiganaji hawa wa mstari wa mbele huwekwa pembeni na wenye MATUMBO makubwa huketi mezani pamoja wakila sadaka zitokanazo na waumini ambao hukamuliwa hadi watoe damu ili mradi wakubwa wanenepeshe MATUMBO yao, wajilimbikizie mali na kuishi maisha ya anasa.

Fuatilia Maaskofu wengi wa KKKT ni mabwenyenye na matajiri kupindukia ambao hata ukiwaletea CAG waeleze chanzo cha ukwasi na utajiri wao hawawezi kukueleza.

Wakati waumini wakiishi maisha ya umasikini, hushurutishwa kutoa fedha kwa kile kinachoitwa sadaka ambazo Maaskofu huzitumia kwa anasa wao na wake zao na watoto wao.

Watoto wengi wa Maaskofu wa KKKT hawaishi hapa Tanzania wanaishi na kusoma Ulaya na Marekani. Na wale wachache wanaosoma Tanzania utawakuta seminary na private schools kubwa kubwa kama sio international school. Malipo ya ada za hawa watoto zinatokana na sadaka za waumini masikini ambao watoto wao hata kumudu gharama za shule za Kata ni kitendawili.

Msingi wa haya yote ni vita ya madaraka, uchu wa madaraka, ulafi wa fedha, kutotosheka na ubinafsi uliopindukia ndani ya KKKT.

Mifano ni mingi bado hatujasau mgogoro ndani ya Dayosisi ya Mashariki na Pwani miaka ya hivi karibuni ulioishia kwa kumng'oa Askofu na washirika wake. Nani amesaa mkasa wa Askofu Jeremiah Mngwamba na sasa mgogoro unaofukuta chini ya Askofu Malasusa?

Naam na sasa huko Dayosisi ya Konde moto unawaka. Hakuna asiyejua kuwa mafuta pekee yanayongojwa ni kuanzishwa kwa Dayosisi ya Mbeya Mjini.

Ndio, kinachotakiwa hapa ni Dayosisi ya Mbeya Mjini ndio maana unaona licha ya Mkuu wa KKKT Askofu Fredrick Shoo kuongoza mchakato wa kupatikana Askofu Mpya Mwakihaba bado mgogoro ndio kwanza umelipuka zaidi.

Ukitazama asili ya migogoro hii na mingine mingi ndani ya KKKT chanzo chake sio kuhitilafiana kiimani wala namna ya kuabudu au kuinjilisha wala kubatiza bali vyanzo vya migogoro ndani ya KKKT asili yake ni uchu wa madaraka, ulafi wa Fedha "sadaka za waumini masikini" waliogeuzwa mitaji ya Viongozi wachache ndani ya Kanisa.

Migogoro yote inayotokea ndani ya KKKT ukifuatilia kwa undani ni ugomvi wa Fedha "sadaka", tamaa ya madaraka, yule anataka kuwa Askofu, mwingine anataka kuwa msaidizi wa Askofu, yule anataka kuwa Mkuu wa Jimbo na yule anataka kuwa Katibu Mkuu wa Dayosisi, Mchungaji yule anajua fulani akiwa Askofu au Mkuu wa Jimbo na yeye atapewa kitengo ndani ya Dayosisi au Jimbo au hata kuhamishiwa usharika wenye makusanyo makubwa sana ya sadaka kila jumapili. Wengine washaahidiwa mukifanikisha Mimi nikakalia kiti cha Askofu wewe ndiye utakuwa Mkuu wa Chuo, wewe utakuwa Mkuu wa shule, wewe utakuwa dean of students, wewe utakuwa Mkuu wa hospitali n.k. Ni vita vya madaraka hakuna kingine.

NINI KIFANYIKE?

Japo tumechelewa sana lakini niseme tu kuwa ni wakati umefika sasa kwa Walutheri kufanya yafuatayo:

1. Katiba Mpya: Tuwe wakweli katiba ya sasa ya KKKT na Dayosisi za KKKT ni mbovu na ina mapungufu mengi yanayoacha wazi mianya na milango ya migogoro. Tutafakari kama Katiba yetu ya sasa bado inakidhi mahitaji ya wakati huu. Nimesoma baadhi ya Katiba za madhehebu mbali mbali, Katiba ya KKKT na Katiba za Dayosisi mbali mbali za KKKT ni miongoni mwa Katiba mbovu na zenye mapungufu mengi sana yanayofanya mfumo wa kuendesha Kanisa usiwe na tofauti kubwa na mifumo ya kuendesha serikali za Kiafrika. Katiba zinaacha mianya ya kusababisha migogoro kila uchwao.

Migogoro yote hii katika hizi dayosisi hakuna hata mmoja unahusisha tofauti za kiimani, namna ya kuendesha ibada, namna ya kuabudu au mafundisho bali maslahi fulani fulani ya vitu vya kidunia hususani uchu wa madaraka na ulafi wa Fedha "sadaka" za waumini. Tusipo tafakari tujue kuwa madhara yanaweza kuwa makubwa sana. Tunaweza kupuuza ushauri huu wa kuandika Katiba Mpya lakini hatuwezi kukwepa matokeo ya kupuuza hili.

2. Mamlaka na madaraka ya Askofu wa Dayosisi yapunguzwe na yaundiwe chombo cha kuyadhibiti. Kuna kosa kubwa sana la uongozi ndani ya KKKT. Maaskofu wa Dayosisi zote wana mamlaka ya juu kabisa ndani ya Dayosi wanazoongoza na hawaingiliwi na Mkuu wa KKKT kwa nguvu ila ni kushauri tu.

Maaskofu ndani ya Dayosisi zao ni zaidi ya miungu watu, hawagusiki, ni untouchable, hawa wanafanya watakalo, wakihojiwa wanafukuza Mchungaji kazi na Mchungaji akisema fwii anavuliwa na huo uchungaji wake kabisa. Yani Mchungaji wa KKKT hana tofauti na Mbunge wa Tanzania maana Mbunge akifukuzwa uanachama amepoteza Ubunge na KKKT ni hivyo hivyo Wachungaji sio wanafukuzwa tu hadi kuvuliwa uchungaji kwa sababu zisizo na msingi. Hii inafungua mianya ya migogoro.

3. Mfumo wa kuwapata Maaskofu wa KKKT: Aidha namna hawa Maaskofu wanavyopatikana inafungua mianya ya rushwa, tamaa, uchu wa madaraka, chuki na visasi. Leo anashinda Askofu huyu kwa figisu, Wachungaji wengine wanabaki majeruhi moyoni wana chuki na uchungu. Kesho wataacha kuandaa zengwe la kukutoa wewe Askofu na kundi lako ili wao nao waingie na washirika wao?

Na hii imekuwa shida kubwa kila shida ikitokea inaanzishwa Dayosisi nyingine ndiyo inakuwa suluhu au Askofu anafurushwa madarakani ili Askofu mwingine aliyekuwa anaumezea mate Uaskofu aingie.

Ninaona imefika muda mamlaka iwe kama Kanisa lilivyo sajiliwa na raslimali za Kanisa zinavyoandikishwa kwamba ni za KKKT. Mmiliki mkuu awe ni mkuu wa Kanisa.

Mfumo unaotumika sasa wa kumchagua Askofu kwa kampeni na Kura za Wachungaji ufutiliwe mbali, mfumo huu unachochea uchu wa madaraka, rushwa hususani rushwa ya kuahidiwa vyeo au kupangiwa usharika wenye waumini wanaotoa sadaka kubwa kubwa na migogoro isiyoisha.

Nashauri Maaskofu wateuliwe na Askofu Mkuu wa KKKT kisha kuundwe Baraza la Maaskofu na Wachungaji "watu wazima" ambapo Baraza hili litakuwa na jukumu la kuomba kwa Mungu na hatimaye kupiga Kura ili kuidhinisha jina la Askofu. Aidha Askofu Mkuu wa KKKT awe na mamlaka kamili ya kuteua na kumtengua Askofu wa Dayosisi au kumpangia Dayosisi nyingine. Sio Askofu akae kwenye Dayosisi moja kama Chifu wa eneo hilo hadi astaafu. Maaskofu wasigeuze Dayosisi mali zao wabadilishiwe vituo vya kazi ndani ya Dayosisi zote ndani ya nchi.

4. Wadhifa wa sasa wa Mkuu wa KKKT ubadilishwe na kuwa Askofu Mkuu wa KKKT mwenye mamlaka kamili na achaguliwe kutoka miongoni mwa Maaskofu na wakuu wa majimbo kulingana na sifa za Elimu na uzoefu zitakazowekwa.

Mkuu wa KKKT atamkwe kuwa ni Askofu Mkuu wa KKKT na awe msemaji wa juu na wa mwisho katika Kanisa na aundiwe vyombo vitakavyomsaidia kusimamia majukumu yake kwa HAKI. Askofu Mkuu wa KKKT akiongea au kutoa maelekezo mjadala uwe umefungwa.

5. Mfumo wa sasa wa kumchagua Mkuu wa KKKT una mapungufu makubwa sana yanayoacha Kanisa likiwa na makundi, majeraha, chuki na wakati mwingi mfumo huu hujaa harufu ya rushwa hususani rushwa ya kuahidiana madaraka na fursa fulani fulani hususani kwa Maaskofu na Wachungaji wanaopiga Kura.

Katika hili nadhani nisiseme sana maana kila mtu anajua abracadabra zilizotokea katika chaguzi za hivi karibuni kumpata Mkuu Mpya wa KKKT kutoka kwa Mkuu aliyekuwepo Askofu Malasusa hadi kuchaguliwa Mkuu mpya wa sasa Askofu Shoo. Majeruhi na migawanyiko ile ya wakati wa uchaguzi bado inalitafuna Kanisa. Maaskofu na Wachungaji wako pamoja lakini hawako kwa Umoja.

5. Nidhamu ya Wachungaji: Ndani ya Sharika nyingi kuna tatizo kubwa sana la nidhamu ya Wachungaji. Na kumekuwapo na ubutu wa Maaskofu wengi kushughulika na nidhamu za Wachungaji kwa sababu Maaskofu wanawatazama Wachungaji kama wapiga Kura wao. Maaskofu wanawaza Uchaguzi ujao, wakiwaza hivyo wanakumbuka huyu Mchungaji alinipigia Kura na kushawishi Wachungaji wenzake wampigie Kura au alimuahidi madaraka au kumpangia usharika wenye "ulaji wa sadaka au miradi ya Kanisa" unadhani akikumbuka hayo yote anaweza kumshughulikia Mchungaji huyo?

Wachungaji wanafuja fedha za waumini masikini, wanawaezeka mimba mabinti na wake za watu mitaani hakuna hatua yoyote inayochukuliwa zaidi sana Mchungaji anahamishiwa usharika mwingine akachafue tena huko.

Wapo baadhi ya Wachungaji kuliko Askofu amhamishe kutoka usharika wenye ulaji hususani maeneo ya mijini ni bora aende kwa sangoma na kalumanzila akajipatie kinga huko.

Hili linaleta matabaka makubwa sana, wapo Wachungaji ni untouchable, hawagusiki, hawahamishiki wala kusemesheka wana ma God fadher. Yani ili umguse Mchungaji fulani ni hadi Askofu au Mkuu wa Jimbo fulani atakapotoka madarakani.

6. Nidhamu ya Maaskofu: Vivyo hivyo kwa Maaskofu. Kuna Maaskofu mafisadi, wamejilimbikizia mali na kuishi kwa anasa huku waumini wakitwisha na kurithishwa mzigo wa madeni.

Inafikia mahali Askofu anapostaafu au anapojua kuwa sasa eneo fulani linajitenga kuwa Dayosisi anafuja mali yeye na washirika wake kiasi kwamba Askofu ajaye akiingia ofisini akaunti zote ni nyeupe, miradi yote imekufa, madeni yamekopwa kila kona kwa kutumia mali za Kanisa kama shule, vyuo na hospitali lakini mkopo uliokopwa hauonekani ulichofanyia bali ametia kwenye mfuko wake akale raha na familia yake.

Vyuo, shule na hospitali nyingi za dayosisi za KKKT huwa zinakufa kwa style hii. Kama huelewi nasema nini nenda waulize Dayosisi ya Mwanga ilirithi madeni kiasi gani ambapo baadhi ya shule almanusura zipigwe mnada na Benki. Waumini wakatwishwa mzigo walipe mamilioni yale. Askofu na washirika wake walitenda ufisadi huu si bado wapo ofisini? Nani wa kuwagusa hawa miungu watu kwa Katiba hii sasa ya KKKT na Katiba ya Dayosisi?

Unauliza nasema nini? Hebu jisomee na kufuatilia mradi wa Hotel ya Corridor "Corridor Spring Hotel ulivyowaheshesha waumini? Waliotafuna fedha zile kwani hawajulikani? Nani wa kuwagusa hawa miungu watu kwa Katiba hii ya sasa ya KKKT?

Nani wa kuwagusa hawa Maaskofu ambapo anajua hata akistaafu anabaki na mali alizoiba Kanisani? Ukiwauliza wanakuambia kwa jeuri hatugusiki kwa sababu Mkuu wa KKKT sio Askofu Mkuu na hana mamlaka kamili ndani ya Dayosisi zetu isipokuwa kushauri tu.

7. Uwiano mbovu baina ya mishahara na marupurupu ya Maaskofu, Viongozi wa Dayosisi, wakuu wa Majimbo, Wachungaji na Wainjilisti.

Kama ambavyo ni tabu kwa Watanzania kujua mshahara, marupurupu na posho za Rais wao ndivyo ilivyo ngumu kwa waumini wa KKKT kufahamu mishahara, posho na marupurupu ya Viongozi wao wa Kanisa kuanzia Mkuu wa KKKT, Askofu wa Dayosisi na Viongozi wengine wa Dayosisi, wakuu wa Jimbo na Wachungaji. Unauliza nasema nini? Nami nakuuliza unajua Askofu wako anajilipa mamilioni mangapi kila mwezi kama mshahara, posho na marupurupu? Je Mchungaji wako?

Maaskofu wamefanya mishahara, posho, marupurupu yao kuwa siri Kuu "top secret".

Kazi ya muumini ni kutoa tu sadaka, kwamba wanalipana mamilioni mangapi kama mishahara, posho na marupurupu mengine sio kazi yao. Ni siri ya kambi.

Wainjilisti wa KKKT wanafanya kazi kubwa sana lakini kutokana na ubinafsi na ulafi wa Fedha wa Maaskofu na Wachungaji, nasikitika kusema kuwa wainjilisti wetu wanaishi katika hali ya umasikini, ufukara na uduni uliopindukia huku Maaskofu na Wachungaji wengi wakiishi kwa raha na anasa kutokana na kujilimbikizia mafungu makubwa makubwa ya uwiano wa sadaka.

Ni aibu kuwa ndani ya usharika unamkuta Mchungaji analipwa shilingi 500,000 " laki 5" tena ambayo haikatwi kodi wala tozo yoyote ile lakini ukakuta mwinjilisti wake analipwa kati ya shilingi 30,000 hadi 50,000 "elfu 30 hadi elfu 50" kwa mwezi na hata hiyo hana uhakika wa kuilipwa. Wainjilisti wetu wamechakaa, wamegeuka ombaomba lakini hebu tazama maisha ya anasa wanayoishi Maaskofu na Wachungaji na familia zao. Halafu mtu wa namna hii anasimama madhabahuni bila aibu anahubiri habari za kumpenda jirani yako kama nafsi yako na kwamba kile hupendi kukitendewa basi nawe usimtendee mwenzako.

Hiki ni kiwango cha juu cha ubinafsi ambacho KKKT inafaa kukitazama na kukirekebisha kwa sababu maslahi duni ya Wachungaji na wainjilisti yamekuwa kichocheo kikubwa cha wao kurubuniwa na kununulika kirahisi sana na Viongozi wachache matajiri wenye tamaa ya madaraka hivyo kuwatumia kama vyombo vya kutengeneza na kuchochea migogoro katika Sharika na sana sana katika Dayosisi.

Nimalizie kwa kusema kuwa kwa Katiba hii ya KKKT na Katiba za dayosisi za KKKT migogoro ndani ya Kanisa hili hitokaa ikome na siku za usoni Kanisa hili litapoteza umaarufu wake maeneo mengi zaidi na pengine kuja kuwa Kanisa DHAIFU na la hovyo likidhoofishwa na migogoro ya kila uchwao.

Asomaye na afahamu. Kama KKKT tunaweza kupuuza waraka huu lakini kamwe hatuwezi kukwepa madhara yatokanayo na kupuuza warak huu. Nimeyaeleza haya kwa uwazi kwa sababu Mimi ni muumini HURU wa KKKT na nimeyasema haya kwa fikra HURU maana naelewa nini kinaendelea ndani ya Kanisa letu hili la KKKT.

Nawatakia heri, fanaka na baraka za sikukuu ya Pasaka.

#KKKT #Migogoro #Dayosisi_ya_Konde
#Mwaikali

Remmy Cameroon
Sauti ya wasio na sauti
 
Du, Mkuu wa kanisa awe Askofu mkuu.Hapo ndipo migogolo itakuwa mikubwa zaidi.
Nakubaliana na wewe marekebisho yawepo kwenye katiba.
Mfano hoja ya Konde iliachwa mwanya na Katibu Mkuu wa KKKT.
Yeye ndiye mtendaji mkuu wa kila siku.Jambo la utawala limekaa kisheria kisha kiutume.Hivyo konde walihamisha jambo la kisheria kuwa la kichungaji bila kuzuiliwa na;
Katibu mkuu Konde
Katibu mkuu makao makuu.
 
Askofu Mwakali na Mchungaji mmoja Mkuu wa Jimbo wanasema wajumbe wa huo mkutano Mkuu hawakupatikana kwa kufuata Katiba ya Konde inavyo ainisha.

Wanasubiri barua ya kuongoa Askofu Mwaikali wapange next move.
Hao wajumbe atawalipa nani kwenda kusikiliza mtu ambaye hana mamlaka kisheria.
Hata wapambe wote mwishowe wataungana na mamlaka mpya.
Mwaikali atabaki pekee yake.
 
Gitifii na Remmy Cameroon hiki mlichokileta hapa ni kazi ya Mungu na isindikizwe na Neno kutoka Ester 4:14.

Sasa niongezee. Baadhi ya Watumishi wa kanisa hili ni manabii wa uongo na hapo ndipo linazaliwa tatizo jengine la Kanisa hili.. Hakuna utaratibu wa Kiroho wala kimwili ulio wazi wa kuwa shughulikia.

Sifa za hawa Watumishi baadhi ambao ni Manabii wa uongo/Falseprophetes.
-Wanatumikia Mabwana wa tatu. Mungu, fedha kwa maana ya mali na siasa. Huyu bwana siasa ni mtoto wa matokeo ya tamaa ya kujilimbikizia mali.Yesu Kristo kasema wazi huwezi kuwa tumikia mabwana wawili wao wamejiongeze na huyu wa tatu..

- Baadhi yao they are cult leaders, wanao fanya occult practices , unzinzi wa kutisha ie kutembea na wake za watu na mbinu za fasle teaching. Mbinu ya kutumia upendo kuficha uongo aka lie and love.
Utakuta madhabahuni mara kadhaa yanatumika mahubiri ya vitisho ili kuwatishia waumini kwa kutumia yale Maneno ya Mungu ya usimguse mpakwa mafuta wa Bwana. Basi waumini wanawaona ni miungu watu. Kulitumia Neno la Mungu kwa ulaghai ili kusukuma maslahi yao nalo ni tatizo linaloendelea kuota mizizi siku baada ya siku.

Ukweli ni kwamba baada ya kushushwa kwa Roho Mtakatifu hapa duniani kila aliye mpokea Bwana Yesu na kufuata yale maagizo aliyo yatoa ya jinsi ya kufanyika Wana wa Mungu waliookoka na wao ni wapakwa mafuta kupitia Roho Mtakatifu. Warumi 8:11/2Wakorintho 2:21-22/1John 2:27/2Timotheo 1:14/1John 1:20 nk.

Yesu Kristo alisema kwa uwazi mmepewa bure toeni bure. Hii haiondoi umhimu wa kutoa sadaka. Lakini Neno la Mungu linafundidha kwa uwazi ni sadaka gani na itolewe vipi? Kanisa la KKKT halizingatia hayo wanazo sadaka zao za bahasha. Sadaka hizi zinatumika kutishia waumini wao na wanaambiwa na viongozi wa madhabahuni Ili uhudumiwe lazima utoe hizo sadaka. Na huduma zinazo tumika kutishia ni ugonjwa -kuombewa, sakaramenti na kifo - kuzikwa kwa ibada.

Vitisho kwa watumishi wa ngazi za chini ndio nyumbani kwao. Hasa wale wanaonekana kuwa na karama za Kiroho kuzidi wakubwa wao. Watahamishiwa makanisa yasio na ulaji yale yanayo toa sadaka chache kama kuwakomoa. Inafika mpaka mahali ziko Dayosisi zimetumia ndio sivyo fedha za mafao ya uzeeni za watumishi wake. Lakini kwa vitisho huwezi kuwasikia hao watumishi wakinyanyua midomo kuuliza kuhusu hatima yao ni ipi?

Mapendekezo. Nitatoa machache.
- Neno la Mungu liko wazi kuhusu huduma ya kanisa inavyo taka kuendeshwa Matendo ya Mitume 6:1-7. Hapa kulitokea mgogoro na ukapatiwa utatuzi kwa kufunga na kuomba. Kwa nini katiba za KKKT na Dayosisi zake hazilifuati na kulizingatia hili kwa usahihi wake?

- Viongozi wa Kanisa wa Kiroho wawekwe mbali na utawala wa fedha na mambo mengine yote ya kiuchumi maana hapo ndipo tatizo kubwa lilipo. Sifa zitakazo wapata wasimamiaji wa mambo ya fedha(Sadaka) zitumike hizo za Acts 6:1-7 na za taaluma ya Elimu ya darasani na utaratibu wa kuwapata uwe huohuo.

- Mitaala wanayo tumia katika vyuo vya thiologia vya Kanisa iangaliwe na kupitiwa ili iandaliwe upya. Watakao iandaa walipe uzito wa juu sana suala na kuomba na kufunga ili wapate kuongozwa na Holy Spirit sio akili zao. Vyuo vinazalisha Watumishi waliobobea umwilini zaidi kuliko Wakiroho.

Mali za Kanisa ziwe chini ya Baraza la Wadhamini sio Askofu Mkuu wa Kanisa. Wadhamini hao wapatikane kwa utaratibu huo wa Acts 6:1-7 na Maandiko mengine yenye sifa hizo na zikiongezewa na sifa za taaluma ya Elimu ya Darasani
 
SIRI imefichuka, kwamba kiini cha mgogoro unaofukuta ndani ya Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) Dayosisi ya Konde, Mbeya, kinatajwa kuwa ni kuficha udanganyifu kwenye mkopo uliochukuliwa na Kanisa hilo, takribani miaka minane iliyopita.

Raia Mwema ilielezwa kuwa baadhi ya viongozi wa Dayosisi ya Konde, wanatuhumiwa kughushi nyaraka za Kanisa, ikiwamo mihutasari wa vikao vya Bodi kwa lengo la kuwezesha kutolewa mkopo huo (miaka 8 iliyopita).

Taarifa kutoka ndani ya Kanisa hilo zinasema, baadhi ya wakubwa ndani ya KKKT wameanzisha mgogoro katika Dayosisi ya Konde, ili kuficha udhaifu wa deni la takribani Sh bilioni 4.7 zinazodaiwa Kanisa na benki ya kibiashara ya CBA.

Benki ya CBA Commercial Bank of Africa-ilitoa kwa Kanisa Sh bilioni 1.7, kufadhili ujenzi wa ukumbi katika chuo kikuu cha Makumila, tawi la Mbeya, kilichoko Uyole (kilikufa kwa ubadhirifu), ambacho zamani kilitambulika kama Chuo cha Ualimu Uyole.

Hata hivyo, mkopo huo haukutumika kama ulivyopangwa, badala yake waliokuwa viongozi wa Kanisa, walizielekeza kwenye matumizi mengine binafsi ambayo hayakufahamika na Kanisa. Mpaka sasa, deni la Benki kwa KKKT, Dayosisi ya Konde limefikia Sh. bilioni 4.7 na tayari benki hiyo, imekwenda mahakamani na kupata amri ya kulipwa deni lake.

Mkopo huo, ulichukuliwa wakati Dayosisi ya Konde, ikiongozwa na Askofu Israel Mwakyolile (Msaidizi wake akiwa Mwakihaba aliyeteuliwa kuwa Askofu sasa), huku Mkuu wa KKKT, akiwa Askofu Dk. Alex Malasusa, ambaye alimaliza utumishi wake kwa mujibu wa Katiba ya Kanisa hilo mwaka 2015.

Nyaraka ambazo gazeti Raia Mwema imezipata, zinaonesha kuwa Kanisa lilitumia majengo ya hoteli ya Matema Beach yaliyopo Ziwa Nyasa Kyela, kama dhamana ya kujipatia mkopo benki.

"Askofu Mwakyolile akishirikana na Mchungaji Mwakihaba walichota fedhia za mkopo, lakini ghafla Mwakihaba ameteuliwa na Askofu Shoo kuwa Askofu wa Konde katika mazingira ya kutatanisha," alieleza mmoja wa wachungaji wa Kanisa hilo

Kwa mujibu wa mtoa taarifa, kinachomponza Askofu Mwaikali, ni msimamo wake wa kugoma kusaini nyaraka za kuitoa hoteli ya Matema Beach kwa "wafanyabiashara wawili mashuhuri jijini Mbeya (wamiliki wa hoteli kubwa jijini Mbeya), ambao wamekubali kulipa deni la benki (nyongeza kwa ahadi ya kusimamia hoteli kwa miaka 100).

Benki ya CBA ilipeleka shauri mahakamani kulishitaki Kanisa. Wakati huo Malasusa aliishaondoka madarakani na Askofu Shoo Akakana kulijua hilo deni.

Kanisa likaunda Tume iliyoongozwa na Askofu wa Singida, Alinikisa Mkumbo, ikabaini 'madudu' yaliyomgusa Askofu Mwakyolile na kustaafu kabla ya wakati.

Askofu Shoo alishikilia msimamo, kuwa mkopo si wa Kanisa, lakini akaamua kuwaacha akina Mwakyolile kwa sababu binafsi, Hili linalotokea sasa, chanzo chake ni hicho"

Baraza la Maaskofu la KKKT, linatarajiwa kukutana Dodoma, Jumatatu ijayo ambako moja ya ajenda zinazotarajiwa kutawala, ni mgogoro ulioibuka kwenye Dayosisi ya Konde

Kwa mujibu wa taarifa kutoka ndani ya Kanisa hilo, maaskofu karibu wote, wamekasirishwa na kitendo cha mkuu wao wa Kanisa, Askofu Dk Fredrick Shoo kuchochea mgogoro kwenye Dayosisi hiyo na makanisa mengine ya KKKT.

"Haya mambo yakiachwa hivi, kesho hawa watu wanaweza kutengeneza magenge na kuwang'oa maaskofu wasiowataka," alieleza Askofu mmoja wa KKKT, ambaye hakupenda kutajwa gazetini.

Alisema, "tunakwenda Dodoma, tukiwa tunakumbuka madhila yaliyompata mwenzetu. Tunakwenda tukiwa wamoja na tunataka vitendo hivi vya kupinduana kinyemela vikomeshwe kwenye Kanisa letu.

Chanzo: Raia Mwema, Machi 26, 2022

NB
Kwanini Shoo kajiingiza kwenye mgogoro? Baadhi wanadai siku zote toka achaguliwe Askofu Mwaikali na baadhi ya maaskofu wasomi wamekuwa tishio kwa Askofu Shoo kuchukua nafasi yake.


View attachment 2165336

Weledi wa Gazeti la Raia Mwema umeporomoka sana kwani kwenye habari nyeti kama hii wangetakiwa kuwahoji watuhumiwa wote kama askofu Shoo, Mwalasusa na wengine waliowataja. Kuhusu kikao cha huko Dodoma walichoandika ni uchochezi kwavile hawawezi kuwaeka uthibitisho wa walichoandika.
 
Hivi KKKT mbona kila Mara migogoro ya kimaslahi? Inanikumbusha deni la Arusha...wakubwa wanapiga mabilioni, halaf waumini wanachangishwa kwa lazima kulipa deni walilokula wakubwa. Dini ni ujinga..
 
Hao maaskofu wana usomi gani ambao Askofu Shoo hana?

Cheo cha Shoo si kina muda? Na tayari ameongoza vipindi viwili? Kwa nini ahofie nafasi yake ambayo kikatiba hawezi kugombea tena?
Mkuu wa kanisa huwa hagombei.
Majina hupendekezwa na ndani ya maaskofu kisha kuyapigia kura hadi liibuke moja
 
Ni vizuri ukaitafuta vizuiri historia ya waluteri,.na pia ukaitafuta pia historia ya wakatoriki na siyo kama unavyosimulia humu,Sina hakika kama hata makao ya ukatoliki yalitokana na hongo iliyotolewa na Benito Mussolini aliyekuwa mtawala wa Italy enzi hizo,ili linyamaze atakapoanza kuua watu.
Kanisa Katoliki chini ya papa ilikuwa na maeneo Mengi katikati mwa Italy kama himaya yake.Wakati Italy inaungana ,maeneo hayo yalitwaliwa pamoja na Roma lakini mle Roma ndo Kuna Vatican city ambako papa alijifungia na kugoma kutoka.Kwa kuhofia mataifa yanayomuunga mkono papa,waitaliano waliamua kumzingira tu bila kuingia Vatican city kumkamata.Kwa Miongo kadhaa,pande hizo mbili zilikuwa na uhasama mkubwa Sana.Benito Mussolini alimuwakilisha mfalme Victor Emmanuel III kusain mkataba wa Lateran na papa wakatambuana na kukubaliana mambo kadhaa ya kidiplomasia ndipo Vatican city ama Holy see ikabaki kuwa Dola ndani ya Dola la Italy.
 
Back
Top Bottom