Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) limetangaza kwamba klabu ya Simba na kiungo Ramadhani Singano ‘Messi' watakaa na kujadili mkataba wao upya.
Katibu Mkuu wa TFF, Mwesigwa Selestine amesema wamegundua mikataba miwili alionao Messi na walionao Simba, ina matatizo.
"Hivyo tumekubaliana waanze mwanzo kujadili tena ingawa ni muhimu kuzingatia mkataba mama," alisema Mwesigwa.
Suala la kuzingatia mkataba mama ambao ndiyo ule wa Simba, nalo limeonekana kuzua utata jambo ambalo limezidi kuwachanganya hata waandishi lakini katibu huyo alipoulizwa, alijibu.
"Hatujaja hapa kutangaza mshindi ni nani, kwa kifupi ni vizuri waanze upya na kujadili kuhusiana na mkataba mpya," alisema.
Messi alikuwa na mkataba unaoiisha 2015, wakati Simba wana mkataba unaoisha 2016 jambo lililozua tafrani kati yao.
Licha ya Mwesigwa kukiri kulikuwa na mapungufu pande zote mbili baada ya kikao hicho cha pande zote pamoja na Sputanza, bado alishindwa kuweka wazi kama Messi bado ni mchezaji wa Simba au makubaliano yanamfanye awe huru.
"Siwezi kuweka hadharani masuala yanayohusu mkataba, hiyo ni siri kati ya mchezaji na klabu," alisisitiza.
Hiyo ni nukuu kutoka kwenye Blog ya Salehjembe.