Tukibaki Hai, Tutasimulia

Tukibaki Hai, Tutasimulia

TUKIBAKI HAI, TUTASIMULIA - BONUS!


Na Steve B.S.M




Nini kilimkuta Dr. Jean?

Magazeti yaliandika na vyombo vingine vya habari vikaripoti ya kwamba mwanaume fulani amekutwa akiwa ameuawa kwa kufumuliwa ubongo wake kwa risasi.

Mwanaume huyo hakufahamika ni nani kwani uso wake haukutambulika kwa namna alivyoharibika. Mwili wake ulichukiliwa na kupelekwa kwenye mahifadhi salama na baadae, kwa kutumia kadi ya gari, mwili huo ukatambulika kuwa ni wa Dr. Jean Broomfield, mtaalamu wa maabara anayefanya kazi katika maabara kuu ya serikali, huko Brookhaven.

Lakini ni nani aliyemuua bwana huyo?

Maramoja shughuli za upelelezi zilianza na mawasilano alofanya bwana huyo yakaanza kuchunguzwa, nani alikuwa mtu wa mwisho kuongea naye, alikuwa wapi siku nzima, je kuna watu ambao amewahi kuhitilafiana nao kwa namna yoyote ile? Vipi huko kazini? Kuna lolote la kushuku?

Wana-usalama waliingia kazini kukusanya taarifa hizo nyeti ili wajue pa kuanzia, kitambo kidogo Dr. Lambert akatiwa nguvuni kwaajili ya mahojiano zaidi yeye akiwa miongoni mwa watu waliowahi kuhitilafiana na marehemu muda si mrefu toka yalipotokea mauaji hayo.

"Serious?" Dr. Lambert aliuliza akiyatoa macho kuwatazama wanausalama waliosimama mbele yake, mabwana hao walikuwa wamevalia suti wote wawili, mmoja nyeusi na mwingine ya kahawia iliyokoza.

"Ndio," afisa mmoja akajibu, "kwa maelezo tuliyoyapata kazini kwako, hivi majuzi ulisikika ukigombana na bwana huyo hivyo tunahitaji maelezo toka kwako."

Dokta hakuwa na namna, akaongozana na mabwana hao na baada ya lisaa limoja la mahojiano akaachiwa huru. Alipotoka akanyookea nyumbani kwake, huko aliandika barua ndefu ambayo aliikabidhi kesho yake kazini kwenye mamlaka husika, hoja ni moja, anataka kuacha kazi rasmi.

"Kwanini umefikia maamuzi haya ghafla hivi?" Mkemia mkuu alimuuliza, "Imebaki miezi michache tu, hukuona haja ya kungoja?"

"Nimechoka sana," Dr. Lambert akajitetea, "nadhani sasa ni muda wangu muafaka wa kupumzika."

Kidogo simu yake ikaita, akaitazama simu hiyo na kuipuuzia kisha akaendelea na maongezi yake kana kwamba hakuna kilichotokea.

" ... Kama nilivyokuambia, nadhani nitaeleweka na uongozi."

Akaaga na kwenda zake, alipofika nje ya jengo akachomoa simu yake mfukoni na kupiga namba ile ambayo hakuipokea hapo awali, akasema,

"Niambie ... Nangoja, bado sijapata taarifa ...." Maongezi yake hayakukata akawa tayari ameshaingia kwenye gari, si punde gari likaondoka zake.

Katika anga za upelelezi, kabla siku haijaisha, ikawa ipo bayana kwamba aliyeongea mara ya mwisho na Dr. Jean alikuwa ni mwanamke ambaye bado hakujulikana ni nani. Kwa msaada wa IP Address, mtu huyo alipiga simu akiwa maeneo mawili tofauti na alitumia namba ambayo ilisajiliwa kwa majina bandia.

Walitazama kwenye kamera iliyokuwepo kwenye eneo husika lakini hamna walichoambulia, watu walikuwa wengi kiasi kwamba ilikuwa ngumu kumbaini muuaji achilia mbali watu hao hawakuonyesha dalili zozote za kutiliwa shaka.

Katika sintofahamu hiyo, mtu mmoja, majira ya jioni, alipiga simu kituo cha polisi akajitambulisha kama raia mwajibikaji, hakutaja jina lake halisi na sauti yake haikuwa inatambulika kama ya mwanaume ama mwanamke, ilikuwa imetibuliwa na 'effects'.

Mtu huyo akasema anajua aliyemuua Dr. Jean, yeye alimshuhudia kwa macho yake akifanya hivyo kisha akatokomea, lakini uzuri alifanikiwa kurekodi kwa kutumia simu yake.

"Tafadhali, unaweza ukajitambulisha na ukatusaidia kuipata video hiyo?" Aliuliza mtu wa mapokezi kwenye 'line' hii ya polisi, 911, lakini ajabu mtu huyo hakujibu na badala yake akakata simu. Aliikata katika muda ambao haukutosha kabisa ku-track mahali alipokuwa.

Swala likabaki bwana huyo ni nani? Kweli alikuwa na video hiyo? Kama anayo kwanini aliamua kuficha utambulisho wa sauti yake na utambulisho wake binafsi? Hamna aliyejua.

***

Gari la polisi lilikatiza likiwa linawaka taa za bluu na nyekundu. King'ora chake kilikuwa kikali sana lakini hakikudumu muda mrefu kwani gari hilo lilikatiza kwa haraka sana. Si muda mrefu kikawa kinasikika kwa mbali huko kikiishia.

Mitchelle alilitazama gari hilo akiwa amejiegesha kwenye gari yake katika kiti cha dereva, gari hilo lilipokatiza akageuza shingo yake na kutazama pembeni, hapo alikuwa ameketi Dr. Lambert akiwa amelaza kichwa chake kwenye kiti.

"Sijaelewa kabisa," alisema Mitchelle kwa sura ya tafakari. "Nilikuwa nipo karibu kukutana naye. Aliponiambia amefika nikatoka kwenye gari kumfuata lakini ajabu nikasikia sauti ya bunduki, kabla sijafanya jambo eneo lile lote likawa vurugu, watu wanakimbia huku na kule. Niliporusha macho nikabaini tukio lilipigwa katika gari la bwana yule, kioo chake kilitapakaa damu, lakini kwa vurugu ile ya watu wakikimbia kwa hofu, sikujua nani aliyefanya tukio!"

Akashika paji lake la uso kwa kulifinyanga kisha akasema tena jambo,

"Sijui nani aliyemuua, sijui alikuwa anataka nini? ... Pengine anatuma ujumbe, lakini ujumbe gani? Na kwa nani?"

Dr. Lambert akauliza, "kuna mtu mwingine alikuwa anafahamu kuwa mnakutana?"

Mitchelle akamhakikishia hakukuwa na yeyote yule ajuaye, labda kwa upande wa dokta lakini kwake yeye hapana, chakustaajabisha ni kwamba hata ule mzigo ambao bwana huyo alikuwa amekuja nao kwaajili ya kumkabidhi, nao haukupatikana katika gari! Ina maana ulibebwa na mtu yule aliyefanya mauaji?

Mitchelle alitikisa kichwa chake kisha akamuuliza Dr. Lambert kama ana kile kilochowaleta hapo, Dr. Lambert akampatia mkoba na kumwambia kila kitu kipo humo,

"Hizo zitakufaa kwa muda wote utakaokuwa safarini."

Mitchelle akatazama na kuhakikisha, kila kitu kilikuwa sawa, akalifunga begi kisha akampatia Dr. Lambert 'cheque' ambayo imejaa madola ya kutosha, Dr. Lambert akahakiki na kisha kwenda zake.

Mitchelle alimtazama bwana huyo akiishia alafu akaanza kutafakari yake, kichwani alikuwa na mambo mengi, mojawapo ni safari yake ya hivi karibuni lakini jingine ni utata .... Usiku wa kuamkia leo aliota ndoto ambayo hakuelewa inahusu nini, kila alipotafakari ndoto hiyo alijikuta hamna anachoambulia.

Alishusha pumzi ndefu, akalaza kidogo kiti chake, hapo akawa 'comfortable' zaidi, akaendelea kuwaza kuhusu ndoto yake.

Kwa kawaida mtu hawezi kuota kitu ambacho hajawahi kukiona au hajawahi kupata kukifahamu lakini kwake ilikuwa tofauti kwani alikuwa anaota mambo mapya, watu wapya, maeneo mapya. Kila alipowaza vitu hivyo amevionea wapi hakuwa anapata majibu.

Baada ya kuona anapoteza muda kwa kuwaza kitu kisichoeleweka, akawasha gari lake aondoke. Akiwa anayoyoma, Dr. Lambert ambaye alikuwapo katika gari lake umbali mdogo tu toka na hapo, akamtazama mwanamke huyo akienda zake kisha akapiga simu yake.

Simu ilipopokelewa naye akasema,

"Hallo!"

Kisha akawasha gari yake na kuondoka. Aliondoka kwa kasi tusisikie hata nini alizungumza humo.


***

Manhattan, New York. Majira ya asubuhi ya mapema.


Bwana mwenye kiwaraza kipana aliingia katika gari yake tayari kwaajili ya kwenda kazini. Alitengenezea koti lake vema kisha akanyoosha mkono wake wenye funguo, akauchomeka lakini kabla hajawasha gari simu yake ikaita, ilikuwa ndani ya koti lake kubwa la suti, akaitoa na kuitazama kwa ufupi kabla hajaipokea na kusema,

"Naam."

Bwana huyu alikuwa ndo yule mkuu wa kitengo cha upelelezi pale kituo kikubwa cha New York. Hapa ni nyumbani kwake, yu ndani ya uzio akitazamia kwenda kwenye majukumu yake ya kila siku.

"Mtu wako amekwishafariki," sauti ilimwambia kwenye simu, kidogo akakwama, uso wake umeganda kana kwamba mtu aliyekaushwa na umeme.

"Nimepata taarifa kutoka kwenye vyanzo vya uhakika," sauti ya kwenye simu iliendelea kutoa maelezo, "amepata ajali na kufia humo."

Kidogo kukawa kimya.

"Hallo? Unanisikia?"

Mkuu wa kitengo akakurupuka akisema,

"Naam! Naam! Nakusikia, umesema amefariki?"

"Ndio, amefariki kwa ajali. Nadhani sasa huko alipo atakuwa ameelewa kwanini nilikuwa namwonya, bahati mbaya ameshakawia."

Simu ikakata, ikamwacha bwana huyu katika bumbuwazi, ni kana kwamba ubongo wake ulikuwa unachelewa kuchakata taarifa, baadae kama baada ya dakika nne hivi ndo' bwana huyu akarejea katika ulimwengu wetu wa kawaida. Alitafuta namba katika simu yake kisha akapiga, simu haikupatikana.

Akajaribu tena, mara tatu, lakini simu haikuwa inapatikana. Akawaza inamaana kweli bwana yule amefariki?

Akawasha gari kwenda kazini, njiani mawazo yamemjaa haswa. Alipofika tu kituoni akafanya kila analolijua ili kupata taarifa lakini kila jitihada alofanya haikuzaa matunda, Mpelelezi hakupatikana na kwa mujibu wa habari alizozithibitisha Mpelelezi alikuwa amekwishafariki!

Kwa kutumia 'tablet' yake alitazama video iliyonaswa na kamera zilizokuwapo katika eneo husika, akahakikisha ya ajali hiyo. Kwa namna alivyoona, hakukuwa na uwezo wa kupata mwili wa Mpelelezi wenye kutambulika kwa chochote, gari lilikuwa limesinyaa mno, hata kuupata mfupa wenye urefu wa sentimeta tatu haikuwa inawezekana.

Bwana huyu akahuzunika sana, hata jicho lake la kushoto likadondosha chozi. Ubaya ni kwamba hakupata wasaa mwema wa kumuaga bwana huyo, mbaya zaidi namna alivyompatia mapumziko ya lazima ilikuwa ni kinyume na taratibu za ofisi, alilifanya hilo kwa utashi wake tu baada ya shinikizo, sasa atasemaje?

Kiti hakikukalika, kila alipokaa alisimama akatembea kwenda mbele na kurudi nyuma, hakujua afanye nini? Kichwa kilikwama kwa muda.

Baada ya dakika kadhaa mlango ukagongwa, akajikuta anashtuka. Hakujua anashtuliwa na nini lakini moyo wake ulimwenda mbio sana, akajikaza na kusema,

"Karibu!"

Akaingia bwana mmoja mwembamba na mrefu sana, alikuwa amevalia shati la bluu na tai ya njano yenye vidoadoa vyeusi, bwana huyo alikuwa ameshikilia bahasha ya kaki, size A4, uso wake umejichonga, taya zake zimejaa mithili ya perege.

Akasema,

"Picha hizi hapa." Akimkabidhi mkuu wake bahasha kisha akasimama hapo kana kwamba sanamu fulani la dukan, Mkuu akazitazama picha hizo moja baada ya nyingine, alipofika kwenye picha ya tatu bwana huyu aliyelizileta akasema,

"Aliyefanya mauaji ya Travis alikuwa ni mwanamke, unaweza ukatambua hilo kwa picha hiyo ya nne na tano, kimo chake na upana wa mabega yake, ingawa amejificha uso, iko bayana kuwa ni mwanamke."

Wakati huo Mkuu alikuwa akitazama picha anayosimuliwa kuihusu, katika picha hiyo alionekana mtu aliyevalia kofia nyeusi aina ya pama, koti jeusi la ngozi na mikono yenye gloves. Mtu huyo alionekana akiwa ameipa mgongo kamera iliyomnasa.

Picha zilizofuatia hazikuwa bayana sana kwani mlengwa aliyefanya tukio alizidi kupotelea akienda mbali na eneo la tukio, Mkuu akazitupia picha hizo mezani kwake kisha akashika kiuno chake, mambo yalikuwa yanazidi kuwa mengi, katika kipindi alichokuwa anamhitaji Mpelelezi zaidi kilikuwa ni hiki, na Mpelelezi mwenyewe ndo' huyu aliyeambiwa amefariki.

Basi akachoka zaidi.

"Kwahiyo Travis kauawa na mwanamke?" Mkuu akasema katika namna ya kutafakari, bwana yule aliyemletea picha hizo akamwambia,

"Ndio, ni mwanamke, bila shaka atakuwa ni mtu mwenye mafunzo ya hali ya juu. Namna alivyoficha utambulisho wake dhidi ya kamera lukuki zilizokuwapo hapo inathibitisha kabisa jambo hilo."

Mkuu akauliza,

"Kuna cha ziada cha kusaidia kumtambua?"

"Ndio!" Bwana akajibu, jibu lake likamfanya Mkuu amtazame akiuliza,

"Nini hiko?"

"Plate number," bwana akajibu kisha akamwonyesha mkuu wake moja ya picha alomkabidhi.

"Ukitazama vema hapa utaona gari aina ya van nyeusi, hiyo ndo' gari aloondoka nayo muuaji."

"Ushaitazama usajili wake?"

Mkuu akauliza upesi.


***
 
TUKIBAKI HAI, TUTASIMULIA - BONUS


Na Steve B.S.M




Usiku haukuwa umeisha, ndo' kwanza ilikuwa saa nne ya dakika za mapema. Richie alitoka kuoga akiwa anajifutafuta na taulo, amevalia nguo ya ndani rangi ya machungwa, miguu yake myembamba ipo wazi ikipuyanga na vinyweleo.

Alipomaliza kujifuta alitupia taulo kitandani kisha akaenendea mafuta ya ngozi, alichovya kidole lakini kabla hajajipakaa simu ikaita. Hakujua simu ipo wapi, alisahau alipoiweka, akarusha macho yake hapa na pale bahati akaiona, ilikuwa kwenye kona ya kitanda, shida nguo zilikuwa zimetanda sana kana kwamba kitanda kimechapwa na bomu, akainyaka simu hiyo na kuitazama, alah! Alikuwa ni Jamal, akastaajabu ni nini muda huu?

"Hello!" Akasema akiketi kitandani, "... Saa hii? ... Serious? ..." Simu ikakata, akatahamaki kwa sekunde, upesi akajivika suruali na shati, nguo zote hizo aliziokota kwenye kile kifurushi kilichokuwepo kitandani kwake, sijui kama nguo hizi zilikuwa safi au lah, alishuka chini upesi na alipofika nje ya ghorofa hili analokaa aliangaza na kidogo tu akamwona Jamal, mwanaume huyo alikuwa amesimama akiegemea moja ya gari, kwa namna alivyoegema hapo unaweza kudhani huo usafiri ni wake, alipomwona Richie anamjia akasimama.

"Ni nini hiko muda huu?" Aliuliza Richie, Jamal kabla hajaongea akatazama kwanza pembeni yake kana kwamba mtu anayehofia usalama wake kisha akasema,

"Richie, najua hili litakuwa 'too much' kwako lakini naomba unisaidie, tafadhali."

Wakati huo wa mazungumzo yakiwa yanaendelea, kuna mtu fulani alikuwa akiwatazama ndani ya gari.

Mtu huyo alitazama vinywa vya watu hawa na kwa kuutumia mkono wake wa kushoto akawa ananakili jambo kwenye 'notebook' yake, alilifanya zoezi hilo kwa sekunde kadhaa kisha akaifunga notebook na kuiweka kwenye 'dashboard'.

Muda mchache ulofuatia, kama dakika zisizozidi tatu, Jamal akamwona mtu fulani akiwa anaingia ndani ya jengo hili la ghorofa, mtu huyo alikuwa mrefu amevalia 'hood' nyeusi iliyofunika kichwa chake, mikono yake ameizamisha kwenye hood hiyo, mwendo wake wa kasi ya wastani, kichwa amekiinamishia chini.

Jamal hakumjali sana bwana huyo kwani hapa wanaishi watu wengi sana, ni ghorofa yenye 'floors' nyingi na vyumba vingi pia, akamchukulia kama mkazi tu wa eneo hili, akapuuza na kuendelea na maongezi yao kama kawaida, baada ya dakika mbili maongezi yakasimama kwa Richie kusema,

"Ningoje hapa, simu yangu niliiacha ndani."

Bwana huyo akatoka zake kuelekea ndani, alikwea ngazi upesiupesi, akashika korido na kuimaliza haraka, kidogo tu huyu hapa mlangoni mwake, chumba namba 43, akachomoa ufunguo mfukoni mwake na kuuchomeka kwenye kitasa, mara mlango ukafunguka wenyewe! Akahamaki, ina maana sikuufunga mlango kwa funguo? Alisema na nafsi yake, akausukuma mlango na kuingia ndani, akatazamatazama, akajiaminisha kila kitu kipo shwari, akaelekea chumbani kwake kuichukua simu iliyomleta huku.

Aliufungua mlango akayatupia macho yake kitandani, akaiona simu, lakini nyuma ya mlango kulikuwapo na mtu amesimama hapo na yeye hakuwa anafahamu jambo, akaichukua simu yake na kuiweka mfukoni, kugeuka, kabla hajaondoka hapa, akashuku kitu mlangoni.

Aliutazama mlango kwa sekunde tano, kuna kivuli kilikuwapo hapo, kivuli kisichoeleweka, moyo ukaguta, haraka akili yake ikamkumbusha yale ya mlango kuwa wazi, hofu ikamvaa, alihisi mwili mwake umepitwa na baridi fulani jepesi ambalo halieleweki, akaupiga moyo konde, mimi ni mwanaume, alisema na nafsi yake, akausogelea mlango taratibu, alipoufikia, katika kiza cha kivuli kile, akaona kiatu cha mtu, buti kubwa jeusi, moyo ukaita pah!


....


Jamal alitazama saa yake ya mkononi, muda ulikuwa umeenda, toka Richie amemuaga kwenda kuchukua simu sasa yapata nusu saa, akajiuliza bwana huyo anafanya nini muda wote huo? Alingoja kidogo, mwishowe akakata shauri kwenda kumwona.

Aliingia ndani akashika ngazi, alizikwea haraka akiziruka mbilimbili, muda si mrefu akawa ameishika korido ya kumpeleka kwa Richie, alipopiga hatua nne akamwona bwana yule aliyevalia hood nyeusi, bwana huyo alikuwa anamjia, uso wake, kama kawaida, ulikuwa unatazama chini, mikono yake ipo ndani ya nguo yake hiyo.

Jamal alimzingatia bwana huyu lakini hakuambulia kitu, hakumwona uso wala hakujua ngozi yake, alichoambulia ni harufu tu wakati akipishana naye, alimsindikiza kwa macho mpaka alipokata kona na kutokomea zake.

Alipofika kwenye mlango wa makazi ya Richie akagonga, kimya, akagonga tena lakini mara hii mlango ukafunguka wenyewe, akashangaa, akausukuma mlango huo na kuingia ndani, akaangaza, hamna kitu, akaita lakini napo kimya, akarudia kuita mara tatu, bado kimya, akaanza kuingiwa na hofu, kutazama mlango wa chumbani upo wazi, taratibu akaujongea na kuusukuma, lah! Akamwona Richie akiwa amelala chini!

"Richie!" Aliita lakini bwana huyo hakuonyesha dalili ya uhai, alikuwa ametulia tuli kana kwamba maiti ndani ya jeneza, upesi akamsogelea na kumtikisa, akampima mapigo yake ya moyo kwa masikio, akabaini bwana huyo alikuwa hai ila ni ufahamu amepoteza, basi upesi akatoa simu yake mfukoni na kupiga 911 kwaajili ya kuomba msaada wa dharura.


......


"Hallo!" Redio ndogo ilitamka ndani ya gari, "kuna mtu amezirai hapa, na mapigo yake ya moyo yako chini sana!" Redio iliendelea kutamka, na bwana aliyevalia hood alikuwa akiskiza kila jambo, ametulia kwenye kiti cha dereva alichokilaza chini kiasi.

Maongezi yaliendelea kidogo katika redio kisha kukawa kimya, baada ya dakika chache sana sauti ya king'ora ikaita kwa mbali, sauti hiyo ikawa inaongezeka kadiri na muda unavyozidi kwenda, kidogo tu eneo hili likaanza kuwakawaka kwa rangi nyekundu na bluu, mara 'ambulance' hii hapa, watu wawili wakashuka upesi na kwenda ndani ya ghorofa hili.

Wakati haya yanatokea, bwana yule mwenye hood alikuwa anatazama kila kitu. Muda si mrefu wale watu waliongia ndani wakatoka na mwili katika 'machela' yao, nyuma wakifuatwa na Jamal. Ilipofikia hapo, bwana huyu ndani ya hood akawasha gari yake na kuondoka zake, akiwa anaenda, Jamal akalikodolea gari hilo ambalo lilikatiza kwa ukaribu kwa kasi yake ya wastani lakini hakuambulia kitu, gari lilikuwa na vioo vyeusi ti, alichobaini ni gari hilo halikuwa na namba zozote za usajili.


***


Uwanja wa Kimataifa wa New York, saa tano asubuhi.


Taksi yenye rangi nyeupe iliingia katika eneo la uwanja wa ndeges ehemu mahususi kwaajili ya kupakulia wateja. Taksi hiyo ilisimama akashuka mwanamke fulani aliyevalia mithili ya walimbwende, nywele zake ni ndefu na ni nyeupe pe, miwani yake ya jua iliziba karibia robo ya uso wake, 'lips' zake zilikuwa zinang'aa na zimelowana, hakika alivutia.

Mwanamke huyu ambaye mwonekano wake ni mpya kabisa machoni petu alikuwa na mwendo mithili ya twiga mwenye kufuata maji ya mtoni, alitembea pasipo papara, kila hatua akiihesabu, kila alipokatiza kati ya watu alionekana wa tofauti kwa namna alivyonawiri, na yeye ni kama vile alilitambua hilo, akaringa.

Mkoba wake wa thamani uliokuwapo begani ulitetemeka, akaufungua na kutoa simu yake, akaitazama kwa kusimama, akatazama nyuma na pembeni yake kisha akapokea simu hiyo,

"Naam," alisema kisha akaendelea na mwendo, mwendo wa madaha kama kawaida, alizungumza na simu hiyo kwa hatua kama tano hivi kisha akasimama, akauliza,

"Umetuma saa ngapi?"

"Tazama kwenye barua pepe yako, utaona," sauti ilimjibu upande wa pili kisha simu ikakata, kabla hajapiga hatua nyingine akafungua 'inbox' ya barua pepe yake, huko akakutana na 'links' mbili za mtandao, akapiga simu.

"Nimeona," alisema kisha akakata simu yake na kuirejesha kwenye mkoba alafu akaendelea na safari yake, baada ya mlolongo mfupi wa abiria akawa sehemu ya ukaguzi, hapo alikuwapo mwanamke mmoja wa makamo ya miaka arobaini, amevalia miwani ambayo ameishusha chini ya pua, macho yake ni kuyarembua lakini kayakaza kuwatazama abiria, ukimtazama vibaya waweza sema anatazama kwa madharau.

Aliipokea 'passport' ya mwanamke huyu kisha akaikagua kwa macho yake, alipomaliza akamtazama mwanamke huyu na kumwamrisha avue miwani yake, mwanamke akatii, akaivua na kumtazama, alikuwa na macho ya kijani, sawa sawia na picha ilokuwepo kwenye 'passport' yake, basi mkaguzi alipojiridhisha akamruhusu aende zake, mwanamke huyo akatabasamu akirudishia miwani yake usoni kisha akasema,

"Tchao!"

Akaenda zake kwa mwendo wake wa madaha, mkononi mwake alikuwa amebebelea tiketi ya ndege kubwa ya Uchina, ndege zao la Boeing yenye uwezo wa kubeba abiria lukuki, humo alijikalia katika kiti cha dirishani na safari ikaanza si muda, ndege ilipong'oa nanga kuidaka anga mwanamke huyu alishusha pumzi ndefu, hatimaye aliiacha ardhi ya Marekani.

Baada ya masaa na masaa ya kudumu angani, hatimaye ndege hii kubwa ilitua salama ndani ya Taiwan katika uwanja wa kimataifa wa Taoyuan, kutokana na utofauti wa ukanda wa muda ulokuwepo baina ya pande hizi mbili, yaani New York na Taipei, Taiwan, ndege hii ilifika katika muda salama kabisa, jua linaangaza vya kutosha, mwanamke huyu akapokelewa na mwanaume aliyekuwa anamngoja muda wote huo, mwanaume huyo alikuwa ameegamia gari kubwa nyeusi, modeli ya Alphard, alipomwona mwanamke huyu alimtambua upesi akampungia mkono, mwanamke akamjia.

"Muda mrefu hatujaonana!" Mwanaume huyo alimpokea mgeni wake kwa kumkumbatia, hapa kwa karibu ndo' akaonekana vema, alikuwa ni Taiwan, mwanamke alipoingia ndani ya gari akavua wigi lake na kunyofoa sura bandia alokuwa amebandika, hapo akawa mtu mpya kabisa! Usingeweza sema ni mwanamke yule tuliyemwona kule New York, walikuwa watu wawili tofauti, wa kule ni mwanamke mgeni machoni petu ila huyu wa sasa ni mwanamke tunayemfahamu, mwanamke tuliyemwona si mara moja ama mbili, alikuwa ni Mitchelle!

Aliuliza,

"Kila kitu kipo sawa?"

Taiwan akamjibu, "sawa sawia."

Mitchelle akasema,

"Nataka kuwaona Truce na Kiellin. Tunyookee huko saa hii."

Taiwan akakaa kimya.

"Umenisikia?" Mitchelle akauliza.


***
 
Back
Top Bottom