Tukibaki Hai, Tutasimulia

Tukibaki Hai, Tutasimulia

Kwa hiyo mpelelezi ndio amekufa mazima? 😔😔😔
 
TUKIBAKI HAI, TUTASIMULIA -- 33



Na Steve B.S.M






New York Police Department, New York, Saa mbili asubuhi.



Bwana alifungua mlango akaingia ndani ya ofisi ya Mkuu wa Upelelezi, akasalimu na kuketi, mkononi mwake alikuwa amebebelea faili moja aliloliweka mezani na kusema,

"Nimefanikiwa kupata mwanya mdogo."

Bwana huyo alikuwa ndo' yule aliyepewa kazi ya kufuatilia mauaji ya Travis, bwana aliyeuawa muda mfupi baada ya kuwasiliana na Mpelelezi kisha gari lake likaandikwa kwa maandishi ya damu, jina lake Michael Summer, ilikuwa rahisi kumtambua sababu alibebelea kijibao kidogo kinachomtambulisha jina kifuani mwake.

"Nini umepata?" Mkuu aliuliza akijaribu kulifungua faili aliloletewa mezani, bwana Michael akamwambia,

"Usajili wa gari ile iliyombeba muuaji ni ya kampuni moja ya usafi inayoitwa RICKY & PAT CLEANING', nilifuatilia katika kampuni hiyo kuhusu gari lao wakaniambia hawana taarifa, gari hilo ni miongoni mwa magari yao chakavu ambayo huifadhiwa kabla ya muda wa kwenda kuharibiwa moja kwa moja."

Mkuu aliendelea kutazama faili, bwana Michael akaweka kituo kifupi katika maelezo yake akimtazama, zikapita kama sekunde sita hivi za ukimya. Mkuu akasafisha koo lake, kuna picha aliiona katika faili hilo, picha ya mwanaume aliyekuwa ndani ya gari, mwanaume mwenye asili ya bara la Ashia, akauliza,

"Na huyu ni nani?"

Bwana Michael akamwambia ni mkurugenzi wa kampuni hiyo, kwa jina anaitwa Ricky Wang, nimejaribu kuonana naye lakini sijabahatika, nimeambiwa amesafiri kwenda kwao, pengine ningeonana naye ningepata taarifa zaidi maana walisema baadhi ya taarifa ni 'confidential' kwa mkurugenzi."

"Kingine?" Mkuu akauliza akiwa anaendelea kutazama faili.

"Kingine ni kuhusu bwana huyo, Ricky Wang," bwana Michael akajibu, "nimetazama usahili wake kwenye 'database', ana nyaraka zote rasmi za kufanya kazi nchini hapa lakini si raia wa Marekani, kama ni hivyo natilia mashaka umiliki wa kampuni yake labda tu kama kuna Mmarekani ambaye yupo naye ubia."

"Naye ni nani?" Mkuu akauliza, macho yake ameyabandua toka kwenye faili.

"Sijamjua, na hilo ni moja ya kitu ambacho ningetaka kumuuliza bwana huyo lakini hayupo, pengine ingeweza kutoa 'lead' fulani."

"Sawa, kuna la ziada?" Mkuu akauliza.

"Nadhani nitalipata n'takapofanikiwa kumpata mlinzi wa zamu, yeye anaweza kutusaidia kujua gari hilo lilitokaje katika yadi kwenda kutekeleza mauaji."

"Gari hilo limeonekana tena?"

"Halikurudi tena yadi lakini ukifungua huko mbele," akasimama kuonyeshea ndani ya faili, "gari hilo limenaswa na kamera za barabarani likiwa linaelekea Pennsylvania."

Mkuu akatazama picha hiyo kwa umakini, gari hilo lilionekana kwa mbali kiasi cha kutoweza kupata taarifa nyingi, akafunga faili na kulirejesha kwa bwana Michael.

"Kazi nzuri, Michael. Fuatilia gari hilo kwa kuwasiliana na mamlaka ya Pennsylvania, utanijuza kila utakachopata."

Michael akanyanyuka na kwenda zake.


****


Taiwan, masaa manne kabla ya Mnada mkubwa kufanyika.



Mitchelle alitazama nguo yake iliyokuwa inametameta ikiwa inaning'inia kwenye enga. Nguo hiyo ilimvutia machoni na aliamini atakapoiweka mwilini basi kila mtu atapata kuona uzuri wake, gauni lilikuwa maridadi sana, mtindo wake wa kipekee na namna litakavyokuwa linahakisi taa zile zinazomulika mnadani vinaweza kukupatia picha kichwani juu ya namna mambo yatakavyofana.

Alishatengeneza nywele zake vema, na vitu kama vile usafiri, mavazi na mzigo unaotakiwa kwenda kuuzwa mnadani ulikuwapo kitandani, upo tayari kabisa, upo ndani ya 'safe' ya chuma yenye kufunguliwa kwa tarakimu za siri, tarakimu anazozifahamu Mitchelle pekee.

Kila kitu kilikuwa vema, naam, lakini si kwamba kila kitu kilikuwa kimekamilika, la hasha, Mitchelle alitazama saa mkononi mwake, ilikuwa ni saa moja kamili ya usiku, muda muafaka, aliponyanyua tu kichwa chake akasikia kengele ya mlangoni, akajikuta anatabasamu kwa mbali, akaelekea mlangoni huko akakutana na bwana mmoja akiwa amebebelea mkoba, bwana huyo alikuwa amevalia kofia nyeusi na ni kana kwamba alilenga kutojulikana kwani alikuwa anatazama chini.

"Kila kitu kipo humo!" Akasema akikabidhi mkoba, Mitchelle akaufungua mkoba kuhakiki, akaona kila kitu kipo vema, basi akamkabidhi bwana huyo begi alilopokea na kufungua kutazama, alipoona kila kitu kipo sawa alishukuru kwa kutikisa kichwa kisha akaenda zake, hakuteta mengi, alijipakia katika pikipiki kubwa alokuja nayo akatia moto, hapo nje akakutana na gari linalotaka kuingia, gari hilo lilikuwa limewabebelea Bwana Taiwan pamoja na Yu, watu hao waliangalia pikipiki hiyo ikipita na kuishia zake wasimtambue hata aliyekuwa anaendesha maana alivalia helmet nyeusi yenye kioo cheusi.

"Ni nani huyu?" Taiwan akauliza, lakini hakuna aliyekuwa anajua kati yao, waliishia kumtazama bwana huyo akienda mwishowe wakaendelea na yaliyowaleta hapa, kuonana na Mitchelle.

Waliingia ndani moja kwa moja wakaketi sebuleni, kidogo tu Mitchelle akatoka akiwa ameng'aa ndani ya gauni lake maridadi, gauni lililofunika kifua na mikono yake huku likiacha mgongo ukiwa wazi kwa kiasi fulani, chini amevalia viatu vyenye visigino virefu, viatu ambavyo ukimtazama unaweza kujiuliza anatembeaje, mkononi amebebelea mkoba, mkoba wenye mali ya pesa ndefu ikiwa ndani ya 'safe' ya chuma.

"Hello, boys!" Alisalimu kisha akatabasamu, Taiwan na mwenzake wakastaajabu kwa uzuri wa mwanamke huyo, hakika alipendeza na alivutia kuendelea kumtazama, wakampa sifa zake.

"Ahsanteni sana, leo ni siku muhimu kwetu, na tuifanye ikawe hivyo!"

Wakatoka kulifuata gari, wakakwea na safari ya kuelekea mnadani ikaanza, ilikuwa ni mapema lakini ndo' utaratibu wenyewe haswa kwa wale ambao walitakiwa kukabidhi mizigo kwaajili ya mauzo, mizigo hiyo ilibidi ifike mapema ili kutoathiri ratiba ya mnada ukizingatia mahudhurio yalikuwa ni ya watu wazito, si vema kuwapotezea muda wao.

Mitchelle aliketi nyuma ya gari pamoja na Taiwan kulia kwake, katikati yao kuna mzigo wa thamani, huku Yu akiushikilia usukani kuelekeza chombo, kila kitu kilikuwa vema, gari lilienda katika mwendo wa usalama na kwa makadirio ya mwendo huo basi ingewapata lisaa limoja kuwasili wanapoelekea.

Baada ya muda mchache wa kuwa barabarani, kama dakika kumi na tano kupita, gari likakwama kwenye foleni, ilikuwa ni foleni kubwa iliyotembea mita kadhaa, magari yamesimama hamna linalosogea wala kujigusa, Taiwan akang'aka,

"Hili foleni limetokea wapi tena?"

"Huwa kuna foleni majira haya?" Mitchelle akauliza.

"Hapana," Taiwan akamjibu, "nashangaa hili limetokea wapi!"

"Pengine kuna ajali mbele," Yu akachangia akigeuza shingo yake kuwatazama walioketi nyuma, "na kama ni kweli basi tutakaa muda mrefu sana hapa."

Taiwan akashusha kioo na kuchungulia mbele, kidogo akaufungua mlango akatoka ndani kwenda kutazama, alitembea hatua kadhaa mbele kisha akarejea na kusema foleni ni kubwa na ameambiwa sasa yapata robo saa foleni hilo halijasogea hata inchi moja, kuna ajali mbaya imetokea hapo mbele ikihusisha magari makubwa, hapo Yu akashauri,

"Vipi tukitumia njia mbadala? Hamna anayejua hapa tutakaa kwa muda gani, huenda tukachelewa."

Mitchelle akaunga mkono hoja, hakutaka kupoteza muda wake hapo, upesi gari likachekechwa kutoka hapo kwenye foleni alafu likageuza kurudi lilipotokea, mwendo wa kama dakika tatu gari likashika njia ndogo kuelekea mashariki mwa jiji, barabara hiyo ilikuwa ni 'one-way' na ilikuwa nyeupe kiasi cha kuruhusu mwendo wa kujiachia, wakatembea huko mpaka mahala fulani walipokuta njia panda, wakakata kushoto, kidogo uso kwa uso na gari kubwa linalobeba taka, gari hilo lilikuwa limejiegesha katika namna ambayo gari lingine lisingeweza kukatiza, lilimeza barabara nzima likikaa kiubapa.

RICKY & PAT CLEANING Co.

Lilisomeka mbavuni, maneno makubwa meupe yanayoonekana vema.

"Shit!" Yu akabamiza usukani, akageuza shingo kutazama nyuma akaona ni kweupe, akaweka 'reverse' gari likaanza rudi nyuma, halijafika popote likatokea gari jingine na kuliweka gari hili kati, gari hilo lilikuwa kubwa jeusi lenye ngao kubwa ya chuma, tairi zake ni nene na ndefu kama trekta, lipo hewani sana wakilitazama gari la wakina Mitchelle kwa chini.

Milango ikafunguka wakashuka watu watano, watu hao walikuwa wamevalia kombati na kapelo nyeusi, kisha nyuso zao zikafunikwa na 'mask' zinazoziba kidevu, mashavu mpaka pua yakabakia macho tu, macho yenyewe hayakuonekana vema sababu ya kushushwa kwa kofia mpaka chini, watu hao walikuwa wamebebelea bunduki nzito nzito zilizoshikiliwa na mikono yote miwili miwili, wakanyooshea bunduki hizo kwenye gari alilomo Mitchelle kisha wakaamuru kila mmoja atoke ndani upesi!

"Ukifanya janja yoyote huu ndo' utakuwa mwisho wa maisha yenu, hatupo hapa kuleta matani!" Mmoja alifoka, Yu akatoka kwenye gari akiwa ameweka mikono yake kichwani, kidogo naye Taiwan akatoka akiwa ameiweka mikono yake juu, nyuso zao zinatweta kwa hofu, naye Mitchelle akatoka akiwa amefanya hivyohivyo, mikono yake iko juu.

"Mzigo uko wapi?" Mmoja akafoka, kabla hajajibiwa akalisogelea gari na kutazama, akauona mzigo kwenye kochi, akaunyaka na kumtupia mwenzake wa nyuma kwaajili ya kuukagua, yeye akanyoosha mdomo wa bunduki kwa mateka wao, yule bwana aliyetupiwa mzigo akaufungua upesi na kukutana na 'safe' ya chuma, hakuweza kuifungua, akapayuka,

"Nahitaji passcode!"

Basi bwana yule aliyekaribu na Mitchelle alimtazama mwanamke huyo akamwonyeshea mdomo wa bunduki usoni na kumwambia,

"Sema passcode upesi."

Mitchelle akamuuliza,

"Aliyekutuma anajua mimi ni nani?"

"Sema Passcode!" Bwana akafoka, saa hii akasogea karibu zaidi na mhusika wake, bunduki yake tayari ameshaikoki kwaajili ya shambulizi, Mitchelle akamtazama Taiwan, macho yake yalikuwa makali yakibanwa na ndita. Aliurejesha uso wake kwa mvamizi aliyemwonyeshea bunduki alafu akamtajia Passcode, yule mwenye mzigo akaweka passcode hizo na mara kukawa kimya, 'safe' haikufunguka.

"Nahesabu mpaka tatu, toa passcode!" Bwana yule akafoka tena, sauti yake haikuwa na utani na kidole chake kilikuwa kinakaribia kufyatua 'trigger' ya bunduki, Mitchelle akarudia tena passcode, ikaingizwa lakini 'safe' haikufunguka, bwana aliyemnyooshea bunduki akampa nafasi ya mwisho,

"Taja passcode!"

Saa hii aliuweka mdomo wa bunduki kwenye paji la uso la mwanamke huyo, na macho yake yakagongana ana kwa ana na macho ya Mitchelle, Mitchelle akarudia tena passcode, ilikuwa ni ileile alosema mwanzo, akasema,

"Weka tena!"

Passcode ikawekwa, mara hii 'safe' ikafunguka, lakini walichokutana nacho hakikuwa kile walichotaraji, halikuwa jiwe la thamani kama walivyodhani, la hasha, ilikuwa ni bomu ambalo muda wake umebakia sekunde mbili tu lipate kulipuka, swala la kufumba na kufumbua, bomu likaparachuka kwa mlipuko mkali!

Mabwana wanne walisambaratika hovyohovyo, vipande vya mwili vilishindana kuacha mwili, sehemu yote ikatapakaa damu.

Bwana yule aliyekuwa anamnyooshea bunduki Mitchelle alikuwa chini akiugulia maumivu, kichwa chake kilikuwa kinavuja damu, kofia yake ilirukia pembeni kichwa chake kikaachwa mavumbini, alijaribu kunyanyuka lakini hakuweza, kwa mbali alimwona mtu anamjia, hakumtambua vema, macho yake yalikuwa na ukungu, mtu huyo alipomsogelea karibu ndipo akamjua kuwa ni Mitchelle, akajitahidi haraka kuisogelea bunduki yake lakini hakufanikiwa, alipigwa risasi mbili akatulia hapohapo chini akigugumia maumivu.

"Nilikuuliza, aliyekutuma ananijua mimi ni nani?" Mitchelle alisema akisogea kwa madaha, "maana laiti angelinijua basi asingelituma watu watano, angelituma jeshi zima."

Baada ya kusema hayo alkfumua kichwa cha bwana huyo kwa risasi alafu akapokea simu yake iliyokuwa inaita kwenye mkoba,

"Mzigo ushafika tayari," sauti ya kiume ilisema, aliyekuwa anaongea upande wa pili alikuwa ni yule bwana aliyeondoka na pikipiki majira yale akipishana na wakina Taiwan mlangoni, alimalizia, "na mnada utaanza si punde, wahi." Kisha simu ikakata.

Mitchelle akaruka maiti zilizokuwapo hapo chini, akawafuata Taiwan na Yu, walikuwa wamelala wakijishika panapouma, akawamalizia risasi zake zote kisha akashika njia kwenda zake mnadani.

Alitembea kwa madaha kana kwamba ametoka tafrija.



****
 
Bado hadithi hii haijaanza rasmi, hata mgogoro mkuu haujaibuka kujulikana, muda si mrefu tutajua mwenendo wake kamili.

Unaikumbuka RICKY & PAT CLEANING?Mpaka sasa imeshafanya matukio mangapi?

[emoji2729]Mauaji ya Mpelelezi.

[emoji2729]Mauaji ya Travis.

[emoji2729]Jaribio la kumuua Mitchelle.
 
TUKIBAKI HAI, TUTASIMULIA - 34



Na Steve B.S.M



Prado kubwa nyeusi isiyokuwa na plate number ilikuja na kusimama kando ya barabara, akatoka mwanaume mrefu, mbavu nene, amevalia miwani yenye glasi nyeupe, nywele kazilaza nyuma, mwili kauvesha suti kali rangi yake nyeusi ti, kuanzia shati mpaka tai yake vyote ni rangi nyeusi.

Bwana huyo mwenye asili ya uchina, kwa mwonekano wa macho yake, alikuwa anatafuna kijiti cha kuchokonolea meno yake madogomadogo huku sura ameikunja. Mwili wake mnene ulivyoshuka kwenye gari chombo hicho kilihema kwa kuutua mzigo, kikanyanyuka maradufu kikikaa katika mazingira yake halisi, alitengenezea koti lake akipandisha mabega kisha akaufuata uchochoro nyuma yake akifuatwa na vijana wawili, nao walivalia suti nyeusi lakini mashati yao yalikuwa meupe kwa rangi, vijana hao walipokuwa karibu na bwana huyu walionekana kama watoto kwa maumbo yao madogo.

Walitembea kidogo tu wakajikuta katika sehemu ile ambapo dhahma ilitokea muda si mrefu, eneo ambalo Mitchelle aliwamaliza wanaume kadhaa ndani ya muda usiozidi dakika moja, hapo wakasimama na kutazama maafa kwa macho ya hasidi, bwana yule mnene mwenye miraba minne akachuchumaa kumtazama kwa ukaribu mmoja wa mabwana wale ambao sasa wameshakuwa wafu, akamgeuza kwa mkono mmoja, maiti ikabinuka kama bua la muhindi, akaikagua aking'atang'ata kijiti chake mdomoni alafu akasimama na kupiga simu, kabla haijapokelewa akatokea bwana mmoja kutoka kwenye ile gari ilowaleta wale mabwana watano kuja kumvamia Mitchelle, bwana huyo alikuwa amevalia kombati jeusi lakini hakuwa na kinyago kama wale wenzake walouawa, bila shaka alikuwa ni dereva, hata mahali alipotokea katika gari hili palieleza hilo, uso wake umeparamiwa na hofu na punde tu alipotoka kwenye gari alimkimbilia bwana yule wa miraba minne na kumweleza namna gani walivyoangamizwa,

"Ilikuwa upesi sana! Hatukuwa na namna yoyote ya kujitetea ..." Wakati huo bwana yule mnene alikuwa anangojea simu ipokelewe, kidogo ikapokelewa, akaeleza yaliyojiri, sauti ya kwenye simu ikamuuliza,

"Kuna aliyebakia?"

Bwana yule wa miraba minne akamtazama bwana yule aliyemkuta katika eneo hili kisha akajibu hakuna aliyebakia, bwana yule aliyebakia akatahamaki kusikia hivyo, hofu ikampara mara mbili yake, akataka kujaribu kuongea lakini bwana yule wa miraba minne akamkatiza kwa kumwonyeshea kidole basi akanyamaza upesi.

"Inabidi twende kwenye mpango namba mbili," bwana wa kwenye simu alizungumza na kuagiza, "tekelezeni mpango huo sasa, lazima tufanikishe hili, hii ni nafasi yetu ya dhahabu." Alafu simu ikakata, bwana huyo mnene akairejesha simu yake mfukoni alafu akachomoa bunduki yake aliyoichomeka nyuma ya kiuno akamwonyeshea bwana huyu aliyebakia, akasema,

"Umesikia? Hamna aliyebaki!"

Kisha akamfyatulia risasi na kumwacha bwana huyo katika dimbwi zito la damu, risasi ilipenya na kutoboa fuvu lake kisha ikasambaratisha kabisa ubongo wake, akalala mfu.


***


"Karibu sana, madam," mwanaume aliyevalia suti nyekundu alimkarimu Mitchelle kwa tabasamu mwanana, mwanaume huyo alikuwa ni miongoni mwa wanaume lukuki waliokuwapo hapa kwaajili ya kuwakaribisha wageni, ukumbi ulikuwa unawakawaka kwa mataa ya rangi mbalimbali, waalikwa na wageni rasmi tayari wameanza kujisogeza wakiingia kila upande.

"Ahsante sana!" Mitchelle alimjibu bwana huyo huki akitabasamu kwa mbali kisha akaufuata mlango mmoja wa ukumbi huu, kulikuwa na milango mitano na kila mmojawapo ukiwa na mfumo mkali wa ulinzi, walisimama hapo wanaume waliovalia suti na vifaa vya mawasiliano masikioni, miongoni mwao walikuwapo wanaume walioshikilia vyombo maalum vya ku-scan wanaokatiza hapa, hapo kama una kifaa chochote chenye kutia walakini wa kiusalama basi vifaa hivyo vingelia ukazuiwa na walinzi.

Kama ilivyo kwa wengine, Mitchelle alikaguliwa mkoba wake kisha na yeye pia, hakukuwa na chaajabu hapa, alikatiza mlangoni lakini kabla hajaendelea ndani zaidi alitakiwa kupachika mikono yake miwili katika skrini fulani iliyounganishwa na mtambo wa utambuzi, hakutegemea hili, alisimama hapo akiitazama mashine hii mlinzi akamsihi afanye upesi,

"Weka mikono yako kwaajili ya 'fingerprint', ma'm."

Mitchelle hakuwa na namna, akajipachika mikono na mtambo ule ukasoma mikono yake, uliscan juu mpaka chini kisha chini mpaka juu, hamna kilichosoma, ikaendelea tena kuscan lakini hamna taarifa ilokuja, iliishia kuwasha taa nyekundu na kuandika 'unknown', yaani isiyofahamika, mlinzi akasogea karibu, akatazama, akagusagusa mashine hiyo na kumtaka Mitchelle arudie tena zoezi hilo, akafanya hivyo lakini bado hamna kitu kilichosoma, alama zake za vidole hazikuwa zinatambulika kabisa.

"Samahani sana, madam," akasema mlinzi, "nadhani itakuwa tatizo la mtandao," kisha akatabasamu kidogo kwa haya, "usijali, wewe nenda, hizi taarifa zimenakiliwa, mtandao utakapokuwa imara basi tutapata kuzitunza." Mitchelle akashukuru na kwenda zake, kwa mwendo wake wa madaha aliingia ukumbini na kunyookea moja kwa moja mahali maalum palipoandaliwa kwaajili ya watu waliokuwa wanauza mali zao katika mnada huu, alifika hapo kwa maelekezo ya 'ushers' waliokuwamo humu, kwa kibali alichokuwa nacho akaketi hapo na kukunja nne kiustaarabu akiusoma mchezo, kidogo tu, hazikupita hata sekunde kumi akaja mhudumu, alikuwa amevalia shati jeupe na 'bow tie' nyeusi kuendana na suruali yake ya kitambaa, mkono wake wa kuume alikuwa amebebelea 'tray' yenye glasi kadhaa za vinywaji, akamuuliza Mitchelle nini angependa kutumia.

"Naomba whisky, tafadhali," Mitchelle aliagiza, mhudumu akamchagulia glasi mojawapo na kumpatia akisema, "karibu."

Mitchelle alitazama akaona 'tattoo' ndogo chini ya kiganja cha mhudumu huyu, ilikuwa ni picha ya ndege aina ya tai akiwa ameachama mbawa zake, hakujali sana, akabeba glasi yake na kuiweka mezani, hakutaka kuipeleka kinywani upesi, hakuwa na kiu kiasi hiko.

Kadiri muda ulivyoenda ndivyo na watu walivyokuwa wanazidi kuingia katika ukumbi huu, kama dakika ishirini mbele kukawa kumejaa pomoni, kila mtu amekaa katika nafasi yake, wanunuaji katika mahali pao na wauzaji pia vilevile, wahudumu wakawa 'busy' kwelikweli kuhudumia umati huu, wanazurura huku na kule wakibebelea trey zao za vinywaji, walinzi nao hawakuwa nyuma, walikuwa wanakatiza huku na kule kuhakikisha usalama upo.

Ukitazama kwa harakaharaka tu, haikuhitaji jicho la umakini, ukumbi ulikuwa umefurika watu wa kariba na asili tofautitofauti, wazungu walikuwapo hapa, waarabu, wahindi, wachina na hata watu wenye asili ya Afrika, watu hao kwa hadhi zao kubwa walikuwepo hapa kufanya biashara kubwa, kitambo kidogo bwana 'auctioneer', yaani mwendesha mnada akaingia akiwa amebebelea kipaza sauti, alikuwa ni bwana mmoja mfupi, amevalia suti ya kijani, nywele kazitengeneza vema na mwendo wake ni wa kitaaluma, akasalimu na pasipo kupoteza muda mnada ukaanza, mali ya kwanza iliweekwa sokoni watu wenye kuipenda wakaweka madau yao.

Kila kitu kilikuwa kinaonekana kwenye skrini kubwa ilokuwapo jukwaani, bidhaa inayonadiwa na pia mnadi mwenyewe hivyo kila mtu alikuwa na uwezo wa kuona kila kinachoendelea pasipo kujali yupo kona gani ya ukumbi, ikafuatia bidhaa ya pili, ikiwa inanadiwa mhudumu akamfuata Mitchelle baada ya kuona glasi yake ni tupu, alikuwa ni bwana mwingine sio yule aliyemhudumia hapo mwanzo, bwana huyu alikuwa na sura nyembamba yenye janja ndani yake, mwingi wa tabasamu na ushapu, hakuuliza, moja kwa moja akatoa glasi na kumpatia Mitchelle, Mitchelle akaipokea na kushukuru kwa tabasamu, mhudumu akaenda zake.

Kabla Mitchelle hajaweka kinywaji hiko mdomoni alipata kuhisi harufu yake, akatambua ilikuwa ni whisky, kidogo akasita, mhudumu yule alifahamu vipi kuwa anakunywa whisky kati ya vinywaji vyote vilivyokuwapo katika trey? Alijiuliza, aligeuka kutazama kando yake, mhudumu mwingine alikuwa anakatiza, akamwita kwa kichwa, mhudumu akasogea kumskiza, akamwagiza kinywaji bila kusema cha aina gani, wakati huo alikuwa ameficha glasi yake ya mwanzo alopewa, mhudumu akampatia glasi ya whisky, alimtazama mkono wake wa kuume akaona 'tattoo' ileile alokuwa nayo mhudumu wa kwanza, mchoro wa tai aliyeachia mbawa zake, hapa akapata walakini, lakini zaidi kilichompatia mawazo ni saa ya mhudumu huyo, saa hiyo ilikuwa katika mtindo wa 'stopwatch' ikihesabu dakika kushuka chini, kwa muda alotazama zilikuwa zimebakia dakika kumi na tano tu dakika hizo zikwishe.

Akatazama saa yake ya mkononi, akatazama ratiba ya mnada na kubaini baada ya dakika kumi na tano zifuatazo itakuwa ni zamu ya bidhaa yake kuwa sokoni kwaajili ya mnada, upesi akanyanyuka aende maliwatoni, alitembea kwa mwendo wa wastani, mwendo usoleta mashaka, alipotoka tu eneo lenye watu wengi kushika eneo tulivu akafungua pochi yake na kuchukua kitu humo, kitu alichokifichama na kiganja chake, alipoingia tu maliwatoni akafuata sinki na kutema kinywaji kilichomo mdomoni mwake kisha akakigusa na kijifaa kidogo cha chuma, kile kifaa alichokitoa kwenye pochi yake, mara kifaa hiko kikatoa sauti ndogo 'beep-beep, upesi akakirejesha katika pochi yake alafu akachana gauni lake kwa chini kutengeneza mpasuo mpaka pajani.

Alishatambua hamna usalama hapa, huu wote ulikuwa ni mtego, hakuelewa kwasababu gani lakini kwa mambo aloyaona na kuyakokotoa, hapa hapakuwa na usalama kuwapo, kuna kitu kikubwa kilikuwa kinafuatia, akahamishia mkoba wake mkono wa kuume alafu akaufuata mlango wa choo.

Kule ukumbini mhudumu mmoja alimfuata mwenzake akamnong'oneza sikioni,

"Hayupo."

Mwenzake akatupa macho yake kwenye kiti alichokuwa ameketi Mitchelle, kilikuwa kitupu, akatembea upesi kwenda hapo, alipofika akatazama chini akaona glasi zote za whisky alizoletewa mwanamke huyo, glasi hizo bado zilikuwa na kinywaji pomoni, ina maana hazikunyweka, upesi akatoa taarifa kwakupitia kifaa chake cha mawasiliano sikioni, wanaume wawili wa jeshi hili la wahudumu wakaelekea chooni haraka, walitazama chooni lakini hawakumwona mtu, wakafuata korido kusaka huku na kule, kidogo wakakutana na mwili wa mwenzao upo chini unavuja damu!

Mwili huo ulikuwa na majeraha kadha wa kadha ya kukatwakatwa na kitu cha ncha kali, na tukio halikutokea muda mrefu kwani bwana huyo aliyekatwa ndo' alikuwa akiishilia hapa, anarukaruka kama kuku aliyekatwa shingo.

"Code red!" Bwana akasema na kifaa chake cha mawasiliano, "Code red!" Akarudia tena kutoa taarifa wakiongeza mwendo kukimbia, kidogo wakapata taarifa kwamba kuna tukio limetokea katika ofisi ya mnada, haikupita muda wakawa wamefika huko, walikuta watu watatu wameuawa, wakapewa na taarifa kuwa mzigo wa Mitchelle ulishachukuliwa akiondoka pia na mizigo mingine ya thamani, mitatu kwa ujumla, na habari mbaya ni kwamba mwanamke huyo bado hakuwa amepatikana.

Mitchelle, akiwa amebebelea mizigo miwili mkononi, alitoka nje ya ukumbi huu kwa kupitia mlango wa dharura ya moto, alitembea kwa haraka akielekea kaskazini mwa ukumbi lakini kabla hajafika mbali simu yake ikaita kwenye mkoba, akajibana mahali apate kuitazama, namba mpya, akapokea na kuiweka sikioni,

"Boss," sauti ilisema kwenye simu, maramoja akaitambua sauti hiyo ni ya Jennifer, mwanamke anayemfanyia kazi nyumbani kule Marekani, akapigwa na butwaa, "Jennifer?"

"Ndio, ni mimi, boss."

Mara ikaongea sauti ya kiume, "ukitaka mwanamke huyu awe salama, rejea ukumbini."

"Wewe ni nani?" Mitchelle akafoka, kabla hajajibiwa akaisikia tena sauti nyingine ya kiume, mara hii aliitambua kuwa ya Dr. Lambert, akazidi kuduwaa.

"Utarudi, ama?" Sauti ngeni ikauliza, Mitchelle akajikuta akipatwa na kigugumizi cha kinywa.




****
 
Back
Top Bottom