Tarehe 19 Desemba, 1968 serikali kama vile imegutushwa na taarifa ya Kwikima, iliipa BAKWATA Cerificate of Exemption na kuifungia EAMWS.[SUP]72[/SUP] Waziri wa Mambo ya Ndani Said Ali Maswanya kwa niaba ya serikali alitoa taarifa fupi:
Waziri wa Mambo ya Ndani kwa kuamriwa na Rais anatangaza kuwa tawi la Tanzania la East African Muslim Welfare Society na Baraza la Tanzania la la East African Muslim Welfare Society ni jumuiya zisizotambulika kisheria chini ya kifungu 6 (i) cha Sheria ya Vyama.[SUP]73[/SUP]
Kwa tangazo hilo la Rais wa Tanzania, Julus Nyerere, Waislam walinyimwa nafasi ya kukutana na kuzungumza kuhusu tatizo ambalo kwa kweli liliwahisu Waislam peke yao. Kwa ajili hii basi Waislam walinyimwa nafasi ya kujadili na kulitolea uamuzi tatizo hilo.
Viongozi wa EAMWS waliitwa mbele ya Kabidhi Wasii ambae ndiye alikuwa amekabidhiwa na serikali jukumu la kusimamia shughuli za kufunga rasmi shughuli za EAMWS. Viongozi walifahamishwa kuwa chini ya sheria ya vyama mali zote za EAMWS zitauzwa na madeni yatalipwa kutokana na fedha hizo na fedha zitakazobaki watapewa wanachama. Serikali ilikuwa haiwezi kufanya kama sheria ilivyokuwa imeelekeza. Ilikuwa jambo zito sana kwa serikali ya Nyerere kuonekana anasimamia kuuzwa kwa mali za Waislam. Viongozi wa EAMWS walipoitwa kwa Kabidhi Wasii mara ya pili walifahamishwa kuwa serikali imebadilisha mawazo yake kutekeleza amri kama sheria inavyosema kwa ajili hiyo basi imefanya mabadiliko ya sheria ya vyama ambayo yanaiwezesha sasa kutoa mali ya EAMWS na kukabidhi BAKWATA. Hivi ndivyo mali za EAMWS zilivyochukuliwa na kupewa BAKWATA bila ya ridhaa ya Waislam wenyewe. Hivi ndivyo shule zote zilizojengwa na EAMWS pamoja na mradi wa Chuo Kikuu cha Kiislam kilipoanguka katika mikono ya kundi la Adam Nasibu. BAKWATA haikuwa na uwezo wa kuendesha mipango yoyote na taratibu shule na miradi yote ya elimu ikafifia na mwishowe kufa kabisa. Hivi ndivyo halikadhalika moto wa Waislam uliowashwa kwa kupatikana kwa uhuru waliopigania hadi ukapatikana ulivyokufa. Moto huu ulikuja ukawaka tena, lakini hiki ni kisa kingine. Insha Allah Mwenyezi Mungu akipenda tutakuja kukieleza.
Huu ndiyo ukawa mwisho wa kile kilichokuwa kikijulikana kama mgogoro wa Waislam ulivyomalizika. Mgogoro ambao ulianza pale mwalimu wa shule ya msingi asiyefahamika na yeyote alipofanya maandamano katika mitaa ya Bukoba akimuunga mkono Julius Nyerere na Azimio lake la Arusha na ukaishia kwa mwalimu huyu akiwa na nafasi juu katika jumuiya ya Kiislam ambayo ilikuwa ikichukiza machoni mwa Waislam. Mwalimu huyu ambae sasa amekuwa Makamu Katibu Mkuu wa BAKWATA alianza kazi yake kwa kuwashutua Waislam. Katika mkutano wa waandishi wa habari Adam Nasibu aliiomba TANU na ASP kujikinga na watu wanaohujumu umoja wa nchi kupitia dini. Akaendelea na kusema kuwa BAKWATA ni sawa na Baraza la Kikristo la Tanzania. [SUP]74[/SUP] Kwa kuwa Waislam walinyimwa fursa ya kujadili "mgogoro' hivi sasa kilichobaki na dhana tu, kuwa nini kingelitokea endapo wangeliruhusiwa kufanya mkutano ule ulioitishwa na EAMWS. Waislam wa Bukoba ambao ilitaarifiwa kuwa walifanya maandamano kuunga mkono Azimio la Arusha hawakutayarisha maandamano ya kuunga mkono BAKWATA. Dar es Salaam na katika miji mingi ya Tanzania, neno BAKWATA halina tofauti na tusi. Kumuita Muislam kuwa yeye ni mwanachama wa BAKWATA ni sawa na kumuita Mkristo mfuasi wa Yuda Iscariot, aliyemsaliti Yesu kwa vipande thelathini vya fedha.