SEHEMU YA KUMI
*******************
"Samahani kaka, nilikuona kuwa una busara ndiyo maana nilikuomba unisindikize ili nipate kukusimulia yanayonisibu hivi sasa, maana sina wa kuongea naye kwa pale nyumbani kwa hili zaidi ya ma-mkubwa ambaye naye hayupo huru sana kwakuwa mama ni boss wake"
Hamida alianza 'kufunguka' akielezea kisa chake, tulikuwa bado tupo maeneo ya supermarket kwa pembeni kulikuwa na sehemu ya kukaa na kupata viburudisho baridi kama ice cream ama vinywaji baridi, kahawa chai na kadhalika.
Nilikuwa namsikiliza kwa makini huku nikijitahidi kuonesha uso wenye busara muda wote. Tulikuwa tumekaa kwa kuangaliana huku tukiwa tumetenganishwa na meza ndogo.
Kwa mara nyingine hapa nilimfaidi Hamida kwa kumuangalia usoni bila wasiwasi (bila kuibia) na kuona uzuri alionao. Naye wala hakuwa na hofu yoyote juu yangu aliendelea kutiririka...
"Mie ndio kwanza nimetoka chuo Kenya, nilikuwa campus ya Mombasa KUC kwa masomo ya diploma ya miezi kumi na minane, nilimaliza Jangwani girls mwaka majuzi."
"Sasa wiki mbili zilizopita ililetwa posa kwa baba, nikiposwa mie, posa ilitoka Oman. Dada yangu Sabra naye ameolewa huko huko. Sasa tatizo siyo posa maana mie tayari nimeshakuwa, nahitaji kuanza maisha yangu, lakini shida ipo kwa mhusika wa posa yenyewe, mie simpendi..."
Alimeza mate kisha akaendelea....
****
Hapa nilikuwa nafaidi vitu vingi, kuwa karibu naye, alikuwa ananukia uturi mzuri sana, udi si udi, misnk si misnk lakini ni harufu iliyotulia na kutamani kuendelea kuinusa muda wote...
****
"Simpendi kwa sababu anaonekana yupo umri kama wa baba, yani mbabu haswa.."
Alisema kwa kusisitiza huku akiingiza mkono mmoja kwenye mkoba wake na kutoa bahasha ya khaki, ndani yake akatoa picha mbili, moja full size na nyingine ni half size (siyo passport size lakini)
"Hebu ziangalie hizi picha..."
Akanipatia, nikaziangalia kwa makini na kuona kuwa ni kweli asemacho Hamida.
"Enhe, sasa wazazi wameamuaje?" Nilidadisi
"Baba, mama na kaka wote wanataka niolewe, mama Fungameza haoneshi upande wowote, lakini najuwa yupo upande wangu maana naye ndoa yake ilimsumbua sana hadi aliomba talaka na kurudi kwetu.
" He kumbe!" Nikijifanya sijui...
"Ndiyo, mie nimezaliwa nimemkuta ma-mkubwa yupo kwetu, tuko naye miaka mingi" aliongeza kisha akaendelea...
"Baba anasema mara oooo, yule tajiri kwao huko, mara oooo, tuna udugu naye kiukoo mara oooo eti nitakaa na dada yangu mji mmoja, yani vijisababu ambazo mie hata sivikubali" aliongea huku kwa mara ya kwanza nilimuona anabinua mdomo kwa kuonesha hasira zake (bila kudhamiria)
"Sasa kali kupita yote eti mie niwe mke wa tatu, yaani pale alipo ana wake wawili mie binti mdogo hivi nikawe mke wa tatu, aku, bikra yangu nitamzawadia nimpendaye" alisema huku akionekana kuchukizwa
"Kwani dini inasemaje kuhusu uke wenza na kuolewa na mtu mzima, maana mie ndio kwanza najifunza, nawe ni mwalimu wangu..." Nikatabasamu kidogo kisha akadakia...
"Kidini wala si haramu, mtu waweza kuoa ama kuolewa na mwenza wa umri wowote ili mradi mume aweze kutumiza mambo manne muhimu kwa mke..."
"Enhe, yapi hayo mwalimu wangu" nilimuuliza
"Mie siyo mwalimu wako, mzee Burhani atakutafutia, mie nimekusaidia tu pale ninapopajuwa..." Alisema
"Ndiyo mwalimu wangu tena, hata kama umenifundisha kipindi kimoja" nilisema huku nacheka kwa mbaaali.
"Jambo la kwanza ni kuweza kukidhi haja ya ndoa kwa maana ya jimai" alisema
"Hebu fafanua hapo wala sijaelewa..." Nilimuuliza, akainama chini kidogo na kusema...
"Awe na uwezo wa kufanya tendo la ndoa, jimai ni tendo la ndoa"
"Ahaaaa, enhe?!" nilielewa sasa nakumuacha aendelee...
"Jambo la pili ni mume awe na uwezo wa kumlisha mke" kisha akasita kidogo halafu akaendelea
"Yaani aweze kuhemea (kutafuta) na kuleta rizki halali nyumbani kwa ajili cha chakula" alimaliza
"Hapo sasa nimeelewa maana nilitaka kukuuliza swali la ufafanuzi" nilichagiza.
"Muoaji pia awe na uwezo wa kumvisha mke, yaani aweze kumpatia nguo kiasi cha kumsitiri maungo mkewe" alitulia kisha akaendelea...
"Jambo la nne ni aweze kumpa malazi mkewe, yani awe na sehemu ya kulala., hayo ndiyo mambo manne muhimu yatakiwayo" alimaliza.
"Ahaaa, sasa mchumba wako anakosa lipi kati ya hayo?" Nilimuuliza
"Kwa maelezo ya baba inaonekana yote anaweza kutimiza lakini mie siiweki rehani bikra yangu kwa mbabu, nijitunze weeee kisha niangukie kwa babu, tena uke wenza!" Aling'aka.
"Kwani uke wenza si inaruhusiwa kwa dini yetu?!" Nilionesha kuiva kwa imani.
"Ndiyo, inaruhusiwa lakini mie hata sikubali, ningekuwa tayari nimeshaolewa na kuachika labda ningekubali, ama ningekuwa mjane labda..."
Alitulia kisha akaendelea
"Ndiyo naenda kumwambia Shangazi nione naye atasimamia wapi" alimaliza.
"Du, pole sana" nilimpa pole huku nikimrudishia zile picha.
"Sijapoa bado, ndiyo maana nimekuomba uje unisikilize kisha unishauri" alisema na kushusha pumzi ndefu kisha kutulia.
"Eee kweli, hili jambo ni zito kwako, na linahitaji busara kubwa katika kuliendea"
Nilisema kama mshauri vile kumbe nami ni mmoja wa waposaji watarajiwa, nilikuwa napima tu anapenda nini na vitu gani.
"Kwani wewe katika makuzi yako hukuwahi kupata boyfriend uliyempenda, ili umwambie aje atoe posa nyumbani?" Nilimuuliza huku namuangalia kwa makini usoni.
Akawa anafikisha vidole huku ameinama kiasi na kusema...
"Wakati nipo form two, kulikuwa na mwanafunzi wa Almuntazir wa A-level, alikuwa ananipenda sana, tulikuwa tunakaa wote Magomeni, yeye alikuwa akiishi mtaa wa suna, alikuwa ana baiskeli nami nilikuwa nayo hivyo mara nyingi tulionana njiani, akajenga mazoea, Jangwani nzima walikuwa wanadhani nimetembea naye lakini ukweli ni kwamba hatuwahi kufanya lolote zaidi ya barua za mapenzi, ila aliahidi akimaliza masomo ya chuo atakuja kuniona. Lakini bahati mbaya alifariki kwa ajali ya gari. Baba yao alikuwa na kiteksii datsun cha mashindano ndio walikuwa wanafanya mazoezi kwa ajili ya mashindano ya Safari Rally yaliyofanyika mwaka juzi, aliumia vibaya sana kwa ajali, mgongo ulivunjika, alipelekwa India kwa matibabu zaidi lakini mwaka jana alifariki" alikatisha huku machozi yakimtoka bila kujuwa.
"Ooh masikini, pole sana Hamida" Nilisimama na kumfuata na kumkumbatia kwa nyuma yeye akiwa bado amekaa na kuinama, kisha nikampa handkerchief.
Pakawa na kimya fulani hivi kisha nikakata ukimya kwa kuendelea kumshauri...
"Pole sana Hamida, Mungu amuweke mahali pema peponi amin" nilisema na kumuuliza...
"Hakukuwa na mwanmume mwingine aliye kutaka ama kukuposa?"
"Wanaonitaka wapo wengi tu, sisi watoto wa mzee Burhani tuna sifa ya tabia njema kule mtaani, tuna malezi bora ya kiislamu..." Akasita kidogo kisha akasema
"Ila sasa nami nimechoka kukaa ndani nataka nianze maisha yangu..."
"Sisi mara nyingi tunaolewaga wenyewe kwa wenyewe, Dada yangu Warda ameolewa Mwanza kwa baba yetu mwingine, Sabra naye Oman kwa ndugu mwingine, lakini yeye angalau mumewe amemzidi miaka sita tu..."
Alijifuta usoni vizuri kwa kitambaa kisha akaendelea...
"Hivyo kwa kujibu swali lako ni kwamba hakuna, labda mbabu wa Oman... Hahahhaha" akacheka.
Sasa ikabaki zamu yangu ya kumshauri. Nitamshauri nini zaidi ya 'kuvutia ngozi' upande wangu!
"Okay, sasa wewe uende kwa Shangazi, mueleze yote, utapata busara zake, nami nipe muda kidogo hadi Ijumaa ijayo nitakupa majibu muafaka wa namna bora ya kukwepa usilotaka." Nilimaliza kibaharia namna hiyo.
Akanishukuru sana kwa ushauri wangu, tukainuka na kuita teksi ili itutoe pale...
"Tupeleke mtaa wa Kimweri na Ghuba Msasani" alisema Hamida
Dereva aliondoa gari na tukaanza kuelekea huko.
"Hivi kumbe unaweza kuletewa picha ukaambiwa ni mchumba, ukamkubali, kama ni picha ya zamani je!" Nilimuuliza Hamida kuondoa ukimya garini.
"Hapo sasa, maana waoaji wa mbali anaweza kuwakilishwa na mtu aliyemridhia, siku ukienda kwa mumeo unashangaa na roho yako unakutana na kibabu!"
Tukacheka wote kwa pamoja.
Dereva wa teksi naye alikuwa 'mfukunyuku' akaweka kanda ya Robert Nesta Marley, wimbo ulioanza unaitwa Turn your light down low!
Ulipofika sehemu ya kibwagizo nikajikuta nami naimba kwa sauti ya chinichini...
[emoji443][emoji441] "....I want to give you some love!, I want to give you some good good lovin'....
" .... Never try to resist oh no!, never never try to resist no more!..."
Pakawa na ukimya tena hadi wimbo mwingine ukaja...
"[emoji443][emoji441] I wanna love you, and treat you right, I wanna love you and treat you alright...."
"Is this love is this love is this love that I'm feelin...'"
"....Everyday and every night, we'll be together..."
"...We will share the shelter of my single bed, we'll share the same room..."
Yani nikajikuta niko so high, Hamida ametulia kama hasikii kitu...
Baada ya kona mbili tatu tukafika mtaa wa Ghuba jirani na msikiti...
"Mie nashukia hapa"
Alisema Hamida, kisha akaniambia nyumba ya tano kutoka msikitini upande ule ndio kwa dada yake baba"
Alishuka na nikamsaidia kushusha bidhaa alizomnunulia aunt yake.
"Twende Moroco" nilimuambia dereva baada ya kumuacha Hamida pale.
Nilikuwa najuwa kesho Jumatatu tutaonana 'darasani'
Moroco nilishuka, nikasubiri Uda kisha nikarudi hadi magomeni nikaenda straight nyumbani
James Jason