SoC01 Umuhimu wa kuwa na Dira ya Maendeleo ya Taifa inayotekelezeka kwa wakati na kwa kuzingatia rasilimali zilizopo

SoC01 Umuhimu wa kuwa na Dira ya Maendeleo ya Taifa inayotekelezeka kwa wakati na kwa kuzingatia rasilimali zilizopo

Stories of Change - 2021 Competition

Abrianna

JF-Expert Member
Joined
Mar 30, 2021
Posts
4,696
Reaction score
15,390
Utangulizi
Dira kwa maana fupi ni muelekeo. Dira ya Maendeleo ya Tanzania (Tanzania Development Vision (TDV) 2025 ilianzishwa mwaka 1994 na kuzinduliwa rasmi mwaka 1999 ambapo utekelezaji wake ulianza mwaka 2000 lengo kuu likiwa kuongoza harakati za maendeleo ya uchumi na jamii zitakazoiwezesha Tanzania kufikia uchumi wa kati na kuondokana na umaskini uliokithiri ifikapo mwaka 2025. 'www.tanzania.go.tz' (tovuti kuu ya serikali)

Melengo makuu matano yalioainishwa katika Dira ya Maendeleo 2025 ni pamoja na kuboresha hali ya maisha ya kila Mtanzania, kuwepo kwa mazingira ya amani usalama na umoja,kujenga utawala bora,kujenga jamii iliyoelimika na kujenga uchumi imara unaokabiliana na ushindani. (Nukuu kutoka Dira ya Maendeleo ya Taifa 2025).

Katika andiko hili, nitaangazia malengo makuu matano kama yalivyoainishwa katika Dira ya Maendeleo 2025. Andiko langu litaangazia pia utekelezaji wa malengo haya na uhalisia wa maisha ya Mtanzania.

Katika uhalisia, Maendeleo ya Nchi yetu kwa asilimia kubwa yamekua yakitegemea Ilani ya chama tawala pamoja vipaumbele vya Rais aliye madarakani. Mfano halisi ni ununuzi wa ndege na ujenzi wa madaraja ambao uliingiza nchi katika madeni makubwa na umaskini. Ni wazi kwamba Dira ya Maendeleo ni kijarida tu ambacho kimetengenezwa kutimiza wajibu lakini hakina nafasi kubwa katika utekelezaji wa shughuli za maendeleo.

Serikali imeunda mipango mingi kwa ajili ya utekelezaji wa maendeleo kama vile mpango wa maendeleo wa miaka mitanpo (Five Year Development Plan), MKUKUTA, Mpango wa Big Results Now (Matokeo Makubwa Sasa), Mpango wa maboresho ya utumishi wa Umma,pamoja na Maleongo ya Maendeleo ya Millenia chini ya nchi za Umoja wa Mataifa.

Katika mipango tajwa, yote ina malengo yanayolandana kwa maana ya kutokomeza umaskini kwa kuboresha huduma za afya, elimu, nishati, kilimo, maji, biashara, mahusiano ya kimataifa, ajira, kuboresha utumishi wa umma, kuweka usawa wa kijinsia pamoja na mengine mengi.

Hebu tuangazie miaka kumi nyuma tulinganishe na utekelezaji wa Dira ya Maendeleo ya Taifa 2025 na hali halisi ya Watanzania mpaka leo hii.

Hali ya maisha ya Mtanzania imezidi kuwa duni pamoja na kwamba nchi yetu ipo katika uchumi wa kati wa chini, Mtanzania wa kawaida anashindwa kumudu gharama ndogo za mlo wa siku ilhali tunatangaziwa uchumi wetu umekua kwa asilimia 7% ( NBS 2019/2020).

Katika kujenga utawala bora, hali imezidi kuwa tete, ni wazi kwamba utawala wa sheria umekua jambo gumu katika nchi yetu hali inayopelekea kutokuwajibika kwa pamoja na ubadhirifu wa mali za umma (Rejea ripoti ya CAG 2020).

Katika Dira ya Mendeleo 2025, serikali imeonyesha nia ya kujenga jamii iliyoelimika na inayojifunza kila siku kulingana na mazingira na nyakati tulizopo, tukirudi kwenye uhalisia, kiwango cha ubora wa elimu zetu hakikidhi viwango vitakavyowawezesha wasomi wetu kuingia katika ushindani ndani na nje ya Tanzania, shule zetu nyingi hazina waalimu wa kutosha wala vifaa vya kufundishia, matamko ya kisiasa kwa upande mwingine yamekua yakiathiri mifumo ya elimu.

Kwa mfano mnamo mwezi Desemba 2020, Rais JPM aliagiza somo la historia ya Tanzania lianze kufundishwa katika shue za msingi mpaka sekondari, Wizara ya elimu iliandaa machapisho kwa ajili ya somo husika lakini baada ya Rais Samia kuingia madarakani somo hilo lilisitishwa rasmi.

Kwa upande mwingine serikali ilichangia kupotosha jamii badala ya kuelimisha. Nitoe mfano mdogo wa janga la Covid 19. Serikali ilisimama kidete kuuaminisha umma kwamba janga hili ni vita ya mabeberu dhidi yetu badala ya kutumia wataalamu wa afya kutoa elimu kuhusu namna bora ya kujikinga ili kuepuka maambukizi. Serikali ilienda mbali zaidi na kuhamasisha tiba mbadala na njia za asili ambazo zilitumika katika vituo vya afya pia.

Kauli ya serikali pamoja na viongozi wakuu wa nchi imeleta mkanganyiko pamoja na hisia tofauti juu ya janga hili na kusababisha watu kuishi pasipo kuchukua tahadhari hata baada ya serikali kubadili msimamo na kuamua kufuata njia za kitaalamu. Ukijaribu kuongea na watanzania kumi, tisa kati yao wanaogopa chanjo na kuamini kwamba mabeberu wanataka kutumaliza.
1626861526209.png
1626861576665.png

(picha kutoka mtandaoni)

Katika uboreshaji wa utumishi wa umma, vilio vimekua vingi, utekelezaji wa dhima hii umesahaulika kwa miaka zaidi ya mitano iliyopita, vilio vingi vya wafanyakazi kuhusu nyongeza za mishahara pamoja na kupanda madaraja, makato makubwa, na mishahara duni ambayo haikidhi maisha ya kila siku.

Mambo ya muhimu yaliyotajwa katika utekelezaji wa malengo ya milenia ni pamoja na kukuza mahusiano ya kimataifa, kutokomeza umaskini wa kipato na njaa. Kwa kipindi cha miaka mitano iliyopita, Tanzania imepuuza kwa kiasi kikubwa sana mahusiano ya kimataifa kutokana na misimamo ya kiongozi aliyekua madarakani. Vipato vya wananchi vimeshuka kutokana na tozo kubwa katika bidhaa na huduma, mfumuko wa bei umeathiri pembejeo za kilimo na bidhaa mbalimbali, uonevu kwa wafanyabiashara,ubambikaji wa kesi na kodi uliosababisha biashara nyingi kufungwa. Tunao mfano halisi wa sasa katika tozo ya miamala ambayo imeleta taharuki kubwa kwa wananchi masikini ambao hata kula yao ni ya tabu.

Mapendekezo
• Serikali ianzishe taasisi maalumu kwaajili ya kuandaa na kusimamia Dira ya Maendeleo ya Taifa. Chombo hicho kiwe na kazi ya kuandaa, kusimamia pamoja na kuishauri serikali iliyopo madarakani bila kujali chama.Taasisi hii ihakikishe sera sera na mipango ya taasisi mbalimbali za serikali pamoja na wizara zina uelekeo mmoja na zinashirikiana ka ukaribu. Kwa mfano suala la kuzalisha wahitimu wenye weledi ni lazima liendane na uboreshaji mfumo wa elimu, kwa hiyo ni lazima wizara ya kazi na wizara ya elimu zishirikiane kubaini mapungufu yanayoonekana kwa wahitimu wanaoajiriwa ili waweze kubaini njia bora ya kuboresha.

Taasisi hii ipewe mamlaka ya kusimamia serikali kama ilivyo bunge na mahakama na kwamba ilani ya chama cha kiongozi aliyeko madarakani ilenge kutafuta au kuonyesha njia sahihi za kuipeleka nchi kule ambako dira inaonyesha, hii itasaidia kutekeleza miradi iliyoachwa au iliyoanzishwa na kiongozi aliemaliza muda wake, mfano wakati Rais JPM naingia madarakani alisitisha ujenzi wa bandari ya Bagamoyo kwa madai kwamba mikataba ilikua mibovu na iliyojaa unyonyaji, siku chache baada ya Rais Samia kuingia madarakani mapitio ya ujenzi wa bandari yameanza, hii ni kwa sababu hakuna mfumo wa kusimamia viapaumbele vya maendeleo ya Taifa badala yake kila kiongozi anajiamulia kile anachopenda.

• Ipatikane katiba imara ambayo itasaidia kudhibiti na kusimamia viongozi walioko madarakani na hata baada ya kustaafu kama ilivyo kwa nchi nyingine kama Marekani na Afrika ya Kusini. Hii itahakikisha viongozi wote wanafanya kazi kwa kuheshimu haki za binadamu na sheria na taratibu zilizopo bila kuathiri malengo ya Taifa kwa ujumla. Katiba imara pia itasaidia kuweka uwajibikaji na usawa kati ya watumishi/viongozi, kuondoa ubadhirifu na matumizi mabaya ya madaraka.

• Serikali ijikite zaidi katika kuvumbua vyanzo vipya vya mapato badala ya kujikita katika kuongeza kodi katika huduma mbalimbali za kijamii ili kupunguza mzigo mkubwa wa kodi kwa wananchi na badala yake wananchi wapate unafuu wa maisha. Mfano sekta ya utalii na madini zinaweza kuwa vyanzo vizuri vya mapato kama tukiweka usimamizi mzuri na mifumo ya kuaminika ili kuepusha mianya ya ubadhirifu. Pia serikali ijikite katika kuboresha mfumo wa elimu ili kuruhusu vijana wengi kujiajiri katika nyanja mbalimbali badala ya kutegemea ajira kutoka serikalini.

• Bajeti za maendeleo zilizoidhinishwa na bunge zisitumike kinyume na lengo ili tuweze kutekeleza mipango iliyopangwa katika mwaka wa fedha wa serikali. Huko nyuma tulishuhudia pesa zikipelekwa katika matumizi ambayo hayakuidhinishwa na bunge hali iliyochangia kukwamishwa kwa miradi mingi ya maendeleo iliyoidhinishwa na bunge. Bajeti inayoidhinishwa pia iende sambamba na Dira ya Maendeleo ya Taifa.

• Serikali iunde mfumo shirikishi utakaosaidia wananchi kushiriki katika kuonyesha vipaumbele vya maendeleo pamoja na utekelezaji. Hii itasaidia wananchi kuwa wasimamizi wa moja kwa moja wa miradi ya maendeleo inayotekelezwa katika maeneo yao.

• Serikali iwatumie wataalamu wa masuala ya uchumi walioko nchini badala ya kutumia wanasiasa pekee katika kuandaa bajeti na matumizi ya serikali, pia serikali ijenge utamaduni wa kuwatumia wataalamu waliobobea katika fani mbalimbali nchini katika kuandaa na kusimamia sera mbali mbali kwaajili ya kukuza uchumi na kuleta maendeleo ya Taifa pamoja na kuheshimu mawazo na maelekezo ya wataalamu katika sekta mbalimbali hata pale yanapotokea majanga yanayohitaji ufumbuzi wa kitaalamu. Kwa kufanya hivi, tutapunguza au kudhibiti matamko ya kisiasa katika mambo nyeti yanayohitaji ufumbuzi wa kitaalamu kama vile Afya, Elimu na Uchumi.

Hitimisho
Natoa wito kwa viongozi/wenye mamlaka, na watunga sera wa nchi, maamuzi yoyote wanayofanya yanaathiri au kufaidisha jamii nzima, wao ni sehemu ya jamii na hivyo wataathirika au kufaidika na maamuzi hayo kwa namna moja au nyingine. Ni vyema kufanya uchambuzi yakinifu kabla ya kufanya maamuzi ili kuepuka athari zozote zitakazoisababishwa na maamuzi yao ikiwa ni pamoja na kurudisha nyuma maendeleo ya Taifa.

Asanteni Sana​
 
Upvote 1.3K
Bandiko zuri, kwangu mimi cha msingi sana sio kuwa na mipango mizuri - mambo mazuri sote tunayajua na tunayatamani. Mengi yao yako ndani ya uwezo wetu. Mengi pia yamekuwa copied kutoka kwingine palipo na mazingira kama yetu. Ili kufikia malengo ya dira hizo tumeshindwa kufanya haya:
a) Financial discipline - kuna maneno sana wakati wa kupitisha dira hizi. Hakuna nidhamu ya pesa kuhakikisha inakamilika, hata pale tunapokuwa na pesa za kutosha kukamilisha.
b) Uwajibikaji. Uwajibikaji kwetu ni kufukuzwa kazi jambo linapoharibika na inaishia hapo. Hatuwajibiki kiasi cha kuhoji kwanini tumeshindwa. Ulishawahi kusikia mbunge akihoji kwanini mradi haukufanywa japo ulitengewa pesa??? Wengi wakiambiwa "utakuwa katika budget ya mwaka huu" basi wanatulia na kutoa sifa kemkem. Je nini ilikuwa sababu ya mradi huo kutofanyika mwaka wa fedha uliotangulia? Inabaki bila majibu!
Umeongea point nzuri sana, kwenye suala la financial dicipline tumefeli pakubwa sana ndio maana kila kukicha tunaona ubadhirifu mkubwa ndani ya ofisi za umma na hakuna hatua zinazochukuliwa matokeo yake wananchi wanaumia na tozo nyingi au kuchangia shughuli za maendeleo wakati pesa hizo zinaishia mikononi mwa wachache

Tukija kwenye suala la uwajibikaji, kuna tatizo kubwa, imefika mahali watawala wanajitengenezea sheria za kuwalinda ili wasiwajibishwe kwa matendo yao.

Tunahitaji marekebisho makubwa sana ya katiba yatakayoweka vipengele vya kuwawajibisha wabadhirifu pamoja na watawala bila kujali nafasi zao, pia tunahitaji katiba itakayopunguza mamlaka ya Rais ili kuweka usawa au uwiano katika utendaji ndani ya ofisi za umma

Mwisho tunahitaji vyombo huru vyenye mamlaka kikatiba kwa ajili ya kufuatilia mipango ya maendeleo na fedha zilizotengwa kwa ajili ya mipango hiyo, taarifa za kila mara juu ya maendeleo ya miradi zitasaidia kuweka rekodi ya namna fedha za maendeleo zinavyotumika na ikibainika uzembe au ubadhirifu basi hatu zichukukiwe, kama ulivyosema kwamba pesa zinatengwa ila miradi haitekelezwi na hakuna anaehoji
 
Tuko pamoja Nimefika Siongapore hilo Port lao c mchezoo c la kitoto Meli inapokuja kushusha mzigo basi ni moja kwa moja inafika port na kupakuliwa mzigo baada ya masaa mawili meli inasepa.Leo kwetu eti meli inakaa nangani kwa wiki mzima hakuna nafasi huu ni ushamba Dunia haiko hivyo .Leo tuna nchi tano tumepakana nazo tunashindwa kuwa na port ya kisasa .Sisi kila tukiamka asubuhi tunawaza umeme tu na maji ushawaka , maji wamekata ,maji hayatoki ,umeme ushazimwa huo unawaka ,huu ni ujinga wa hali juu .KWENYE MITI HAKUNA WAJENZI.Ndio TZ kwa kweli inatia uchungu sana sana tukiona nchi za watu zilivyoendelea they are so proud .Raisi Mama Samia Watoe Viongozi washamba wende wakatembee special nchi za Asia wakaone maendeleo pengine watapata wivu wa kuiga wa maendeleo.Ni mengi sana.
Kuna shida kubwa sana, tunahitaji kujifunza kutoka kwa wenzetu na tunatakiwa tutafute namna bora ya ku-utilize our resources, tuna wataalamu wa kutosha lakini hatuwatumij badala yake tunawatumia wanasiasa katika mambo sensitive

Wataalamu wetu wengine wanamshauri Rais vibaya au pengine hawana exposure ya kutosha
 
Yaani hii ni nchi pekee ambapo unaagiza gari bei ya gari milioni 7 lakini kodi milioni 10 yaani utafikiri hayo magari wanaunda wao!! Nilikuwa napitia gharama za miamala hizi mpya kwenye chati ya TIGO nikabaki numeduwaa kwa sababu yaani toza ya serikali iko juu kuliko gharama za wenye kampuni daaah...
Kwamba kodi ni kubwa kuliko bei ya gari? 🤣🤣🤣 inasikitisha na kuchekesha sana mkuu
 
Hao akina babu T jambo la kushangaza ni kwamba hapo walipo tumewaweka sisi wenyewe.[emoji28]
Hatujawaweka, wabunge wengi wa sasa hawakuwekwa na wananchi bali waliwekwa na chama chao au mwenyekiti wao, wananchi walidhulumiwa haki yao ya kuwachagua viongozi wanaowataka, ndio maana tunasema tunahitaji katiba mpya na tume huru labda vitasaidia kuwapa wananchi mamlaka tena
 
Andiko zuri, mwandishi anafaa kuchukua nafasi ya mzee wa tozo! Watu wenye akili wapo mtaani huku kina Babu T wako mjengoni! Nchi hii bhana .........
Asante mkuu, kweli tunahitaji mabadiliko, tena tuanze na pale mjengoni maana wao ndio wanaopitisha maamuzi haya ambayo yanaumiza wananchi, mjengoni wanatakiwa kuwepo wawakilishi wa wananchi na sio wawakilishi wa serikali ili waweze kusimamia maendeleo ya nchi ikiwemo Dira yetu ya maendeleo
 
Mkuu unamuwajibishaje mtu uliyemkabidhi cheo/ wadhifa kama ngekewa? Hana mpango wowote wa atakachofanya kwenye hiyo nafasi.

Kama ulivyopendekeza, nafasi itangazwe, vigezo vitolewe, unaulizwa ukiipata hii nafasi tutarajie yapi kutoka kwako? Mtu ajivishe kamba mwenyewe shingoni.

Uwezekano wa kuongezwa mkataba utegemee utakavyoweza kufanya kazi vizuri na kutekeleza malengo ya hiyo nafasi. Hii nchi itabadilika.
Exactly!!
 
Yaani hii ni nchi pekee ambapo unaagiza gari bei ya gari milioni 7 lakini kodi milioni 10 yaani utafikiri hayo magari wanaunda wao!! Nilikuwa napitia gharama za miamala hizi mpya kwenye chati ya TIGO nikabaki numeduwaa kwa sababu yaani toza ya serikali iko juu kuliko gharama za wenye kampuni daaah...
Aibu sana mkuu, sijui ni nani anawashauri hawa wasimamizi wa taasisi husika, kuhusu kwenye tozo mimi nimeachana kabisa na biashara za mobile money, sasa wamehamia kwenye mabenki, nitakua naficha pesa zangu kwenye kububu cha mama P,

Ninachojiuliza, hivi Rais anapoteua hawa wakuu wa taasisi au idara mbalimbali huwa anaangalia uwezo wao au anateua tu kwa sababu zake binafsi? Mtu kama huyu Mwigulu Nchemba anaejiita daktari wa uchumi, ni daktari wa uchumi kweli au alipatia elimu yake majalalani kama kabudi,? Hakuna proffeaionalisim kabisa, kuna vyanzo vingi vya mapato kama kwenye sekta za madini walitakiwa wazibe mianya ya wizi badala yake anataka kuplunder pesa wa wanchi kwa kupitia tozo
 
Binafsi naona tatizo limeanzia alipotuachia mkoloni. Mambo mengi na mifumo ya kiserikali katika nchi za kiafrika ni urithi kutoka kwa wakoloni waliotawala nchi husika. Huu mfumo wetu wa uongozi ni mfumo wa kifalme kutoka kwa malkia Elizabeth, nakunaliana na mleta maada juu ya umuhimu wa marekebisho lakini kama ilivyo kwa Queen Elizabeth wa UK ni ngumu sana watawala kukubali kutawaliwa tena kwa hiari yao Rai yangu kwa wananchi wenzangu ni tufanye kazi kwa bidii tu. Asante.
 
Umeongea point nzuri sana, kwenye suala la financial dicipline tumefeli pakubwa sana ndio maana kila kukicha tunaona ubadhirifu mkubwa ndani ya ofisi za umma na hakuna hatua zinazochukuliwa matokeo yake wananchi wanaumia na tozo nyingi au kuchangia shughuli za maendeleo wakati pesa hizo zinaishia mikononi mwa wachache

Tukija kwenye suala la uwajibikaji, kuna tatizo kubwa, imefika mahali watawala wanajitengenezea sheria za kuwalinda ili wasiwajibishwe kwa matendo yao.

Tunahitaji marekebisho makubwa sana ya katiba yatakayoweka vipengele vya kuwawajibisha wabadhirifu pamoja na watawala bila kujali nafasi zao, pia tunahitaji katiba itakayopunguza mamlaka ya Rais ili kuweka usawa au uwiano katika utendaji ndani ya ofisi za umma

Mwisho tunahitaji vyombo huru vyenye mamlaka kikatiba kwa ajili ya kufuatilia mipango ya maendeleo na fedha zilizotengwa kwa ajili ya mipango hiyo, taarifa za kila mara juu ya maendeleo ya miradi zitasaidia kuweka rekodi ya namna fedha za maendeleo zinavyotumika na ikibainika uzembe au ubadhirifu basi hatu zichukukiwe, kama ulivyosema kwamba pesa zinatengwa ila miradi haitekelezwi na hakuna anaehoji
Andiko lako linaweza tafsiriwa kama bandiko lenye viashiria vya kigaidi lina lenga kuweka usawa ambao unatafsiriwa kama viashiria vya ugaidi!
 
Binafsi naona tatizo limeanzia alipotuachia mkoloni. Mambo mengi na mifumo ya kiserikali katika nchi za kiafrika ni urithi kutoka kwa wakoloni waliotawala nchi husika. Huu mfumo wetu wa uongozi ni mfumo wa kifalme kutoka kwa malkia Elizabeth, nakunaliana na mleta maada juu ya umuhimu wa marekebisho lakini kama ilivyo kwa Queen Elizabeth wa UK ni ngumu sana watawala kukubali kutawaliwa tena kwa hiari yao Rai yangu kwa wananchi wenzangu ni tufanye kazi kwa bidii tu. Asante.
Nakubaliana na wewe, tunafanya kazi kwa bidii lakini hata kile tunachppata wanakipora kwa mgongo wa tozo halafu wanatumia kujifurahisha na kujilipa mishahara mikubwa tena hata kodi wamesameheana, sioni kama tunahitaji kufanya kazi tu bali tunahitaji pia tuone matunda ya kazi yetu, tunahitaji kurekebisha hii mifumo tuliyoachiwa na wakoloni ili tuweke mifumo ambayo ni rafiki kwa mazingira yetu na kwa nyakati hizi.

Wananchi wanahitaji unafuu wa maisha, unafuu wa kodi, unafuu wa bei za bidhaa,na pia wanahitaji maidha bora.
 
Inawezekana kabisa, tumetoka kwenye ufisadi kukaja kwenye uhujumu ichumi na sasa tupo kwenye ugaidi, sijui what will be next....

Kwa sasa tumepiga kambi kwanza kwenye tozo wakati tunaangalia what is next.

Unakuja kutahamaki, uchaguzi umewadia, hakuna cha kuwaambia wananchi, inabidi tu mbinu zitumike kutangazwa washindi.
 
Back
Top Bottom