SoC01 Umuhimu wa kuwa na Dira ya Maendeleo ya Taifa inayotekelezeka kwa wakati na kwa kuzingatia rasilimali zilizopo

SoC01 Umuhimu wa kuwa na Dira ya Maendeleo ya Taifa inayotekelezeka kwa wakati na kwa kuzingatia rasilimali zilizopo

Stories of Change - 2021 Competition

Abrianna

JF-Expert Member
Joined
Mar 30, 2021
Posts
4,696
Reaction score
15,390
Utangulizi
Dira kwa maana fupi ni muelekeo. Dira ya Maendeleo ya Tanzania (Tanzania Development Vision (TDV) 2025 ilianzishwa mwaka 1994 na kuzinduliwa rasmi mwaka 1999 ambapo utekelezaji wake ulianza mwaka 2000 lengo kuu likiwa kuongoza harakati za maendeleo ya uchumi na jamii zitakazoiwezesha Tanzania kufikia uchumi wa kati na kuondokana na umaskini uliokithiri ifikapo mwaka 2025. 'www.tanzania.go.tz' (tovuti kuu ya serikali)

Melengo makuu matano yalioainishwa katika Dira ya Maendeleo 2025 ni pamoja na kuboresha hali ya maisha ya kila Mtanzania, kuwepo kwa mazingira ya amani usalama na umoja,kujenga utawala bora,kujenga jamii iliyoelimika na kujenga uchumi imara unaokabiliana na ushindani. (Nukuu kutoka Dira ya Maendeleo ya Taifa 2025).

Katika andiko hili, nitaangazia malengo makuu matano kama yalivyoainishwa katika Dira ya Maendeleo 2025. Andiko langu litaangazia pia utekelezaji wa malengo haya na uhalisia wa maisha ya Mtanzania.

Katika uhalisia, Maendeleo ya Nchi yetu kwa asilimia kubwa yamekua yakitegemea Ilani ya chama tawala pamoja vipaumbele vya Rais aliye madarakani. Mfano halisi ni ununuzi wa ndege na ujenzi wa madaraja ambao uliingiza nchi katika madeni makubwa na umaskini. Ni wazi kwamba Dira ya Maendeleo ni kijarida tu ambacho kimetengenezwa kutimiza wajibu lakini hakina nafasi kubwa katika utekelezaji wa shughuli za maendeleo.

Serikali imeunda mipango mingi kwa ajili ya utekelezaji wa maendeleo kama vile mpango wa maendeleo wa miaka mitanpo (Five Year Development Plan), MKUKUTA, Mpango wa Big Results Now (Matokeo Makubwa Sasa), Mpango wa maboresho ya utumishi wa Umma,pamoja na Maleongo ya Maendeleo ya Millenia chini ya nchi za Umoja wa Mataifa.

Katika mipango tajwa, yote ina malengo yanayolandana kwa maana ya kutokomeza umaskini kwa kuboresha huduma za afya, elimu, nishati, kilimo, maji, biashara, mahusiano ya kimataifa, ajira, kuboresha utumishi wa umma, kuweka usawa wa kijinsia pamoja na mengine mengi.

Hebu tuangazie miaka kumi nyuma tulinganishe na utekelezaji wa Dira ya Maendeleo ya Taifa 2025 na hali halisi ya Watanzania mpaka leo hii.

Hali ya maisha ya Mtanzania imezidi kuwa duni pamoja na kwamba nchi yetu ipo katika uchumi wa kati wa chini, Mtanzania wa kawaida anashindwa kumudu gharama ndogo za mlo wa siku ilhali tunatangaziwa uchumi wetu umekua kwa asilimia 7% ( NBS 2019/2020).

Katika kujenga utawala bora, hali imezidi kuwa tete, ni wazi kwamba utawala wa sheria umekua jambo gumu katika nchi yetu hali inayopelekea kutokuwajibika kwa pamoja na ubadhirifu wa mali za umma (Rejea ripoti ya CAG 2020).

Katika Dira ya Mendeleo 2025, serikali imeonyesha nia ya kujenga jamii iliyoelimika na inayojifunza kila siku kulingana na mazingira na nyakati tulizopo, tukirudi kwenye uhalisia, kiwango cha ubora wa elimu zetu hakikidhi viwango vitakavyowawezesha wasomi wetu kuingia katika ushindani ndani na nje ya Tanzania, shule zetu nyingi hazina waalimu wa kutosha wala vifaa vya kufundishia, matamko ya kisiasa kwa upande mwingine yamekua yakiathiri mifumo ya elimu.

Kwa mfano mnamo mwezi Desemba 2020, Rais JPM aliagiza somo la historia ya Tanzania lianze kufundishwa katika shue za msingi mpaka sekondari, Wizara ya elimu iliandaa machapisho kwa ajili ya somo husika lakini baada ya Rais Samia kuingia madarakani somo hilo lilisitishwa rasmi.

Kwa upande mwingine serikali ilichangia kupotosha jamii badala ya kuelimisha. Nitoe mfano mdogo wa janga la Covid 19. Serikali ilisimama kidete kuuaminisha umma kwamba janga hili ni vita ya mabeberu dhidi yetu badala ya kutumia wataalamu wa afya kutoa elimu kuhusu namna bora ya kujikinga ili kuepuka maambukizi. Serikali ilienda mbali zaidi na kuhamasisha tiba mbadala na njia za asili ambazo zilitumika katika vituo vya afya pia.

Kauli ya serikali pamoja na viongozi wakuu wa nchi imeleta mkanganyiko pamoja na hisia tofauti juu ya janga hili na kusababisha watu kuishi pasipo kuchukua tahadhari hata baada ya serikali kubadili msimamo na kuamua kufuata njia za kitaalamu. Ukijaribu kuongea na watanzania kumi, tisa kati yao wanaogopa chanjo na kuamini kwamba mabeberu wanataka kutumaliza.
1626861526209.png
1626861576665.png

(picha kutoka mtandaoni)

Katika uboreshaji wa utumishi wa umma, vilio vimekua vingi, utekelezaji wa dhima hii umesahaulika kwa miaka zaidi ya mitano iliyopita, vilio vingi vya wafanyakazi kuhusu nyongeza za mishahara pamoja na kupanda madaraja, makato makubwa, na mishahara duni ambayo haikidhi maisha ya kila siku.

Mambo ya muhimu yaliyotajwa katika utekelezaji wa malengo ya milenia ni pamoja na kukuza mahusiano ya kimataifa, kutokomeza umaskini wa kipato na njaa. Kwa kipindi cha miaka mitano iliyopita, Tanzania imepuuza kwa kiasi kikubwa sana mahusiano ya kimataifa kutokana na misimamo ya kiongozi aliyekua madarakani. Vipato vya wananchi vimeshuka kutokana na tozo kubwa katika bidhaa na huduma, mfumuko wa bei umeathiri pembejeo za kilimo na bidhaa mbalimbali, uonevu kwa wafanyabiashara,ubambikaji wa kesi na kodi uliosababisha biashara nyingi kufungwa. Tunao mfano halisi wa sasa katika tozo ya miamala ambayo imeleta taharuki kubwa kwa wananchi masikini ambao hata kula yao ni ya tabu.

Mapendekezo
• Serikali ianzishe taasisi maalumu kwaajili ya kuandaa na kusimamia Dira ya Maendeleo ya Taifa. Chombo hicho kiwe na kazi ya kuandaa, kusimamia pamoja na kuishauri serikali iliyopo madarakani bila kujali chama.Taasisi hii ihakikishe sera sera na mipango ya taasisi mbalimbali za serikali pamoja na wizara zina uelekeo mmoja na zinashirikiana ka ukaribu. Kwa mfano suala la kuzalisha wahitimu wenye weledi ni lazima liendane na uboreshaji mfumo wa elimu, kwa hiyo ni lazima wizara ya kazi na wizara ya elimu zishirikiane kubaini mapungufu yanayoonekana kwa wahitimu wanaoajiriwa ili waweze kubaini njia bora ya kuboresha.

Taasisi hii ipewe mamlaka ya kusimamia serikali kama ilivyo bunge na mahakama na kwamba ilani ya chama cha kiongozi aliyeko madarakani ilenge kutafuta au kuonyesha njia sahihi za kuipeleka nchi kule ambako dira inaonyesha, hii itasaidia kutekeleza miradi iliyoachwa au iliyoanzishwa na kiongozi aliemaliza muda wake, mfano wakati Rais JPM naingia madarakani alisitisha ujenzi wa bandari ya Bagamoyo kwa madai kwamba mikataba ilikua mibovu na iliyojaa unyonyaji, siku chache baada ya Rais Samia kuingia madarakani mapitio ya ujenzi wa bandari yameanza, hii ni kwa sababu hakuna mfumo wa kusimamia viapaumbele vya maendeleo ya Taifa badala yake kila kiongozi anajiamulia kile anachopenda.

• Ipatikane katiba imara ambayo itasaidia kudhibiti na kusimamia viongozi walioko madarakani na hata baada ya kustaafu kama ilivyo kwa nchi nyingine kama Marekani na Afrika ya Kusini. Hii itahakikisha viongozi wote wanafanya kazi kwa kuheshimu haki za binadamu na sheria na taratibu zilizopo bila kuathiri malengo ya Taifa kwa ujumla. Katiba imara pia itasaidia kuweka uwajibikaji na usawa kati ya watumishi/viongozi, kuondoa ubadhirifu na matumizi mabaya ya madaraka.

• Serikali ijikite zaidi katika kuvumbua vyanzo vipya vya mapato badala ya kujikita katika kuongeza kodi katika huduma mbalimbali za kijamii ili kupunguza mzigo mkubwa wa kodi kwa wananchi na badala yake wananchi wapate unafuu wa maisha. Mfano sekta ya utalii na madini zinaweza kuwa vyanzo vizuri vya mapato kama tukiweka usimamizi mzuri na mifumo ya kuaminika ili kuepusha mianya ya ubadhirifu. Pia serikali ijikite katika kuboresha mfumo wa elimu ili kuruhusu vijana wengi kujiajiri katika nyanja mbalimbali badala ya kutegemea ajira kutoka serikalini.

• Bajeti za maendeleo zilizoidhinishwa na bunge zisitumike kinyume na lengo ili tuweze kutekeleza mipango iliyopangwa katika mwaka wa fedha wa serikali. Huko nyuma tulishuhudia pesa zikipelekwa katika matumizi ambayo hayakuidhinishwa na bunge hali iliyochangia kukwamishwa kwa miradi mingi ya maendeleo iliyoidhinishwa na bunge. Bajeti inayoidhinishwa pia iende sambamba na Dira ya Maendeleo ya Taifa.

• Serikali iunde mfumo shirikishi utakaosaidia wananchi kushiriki katika kuonyesha vipaumbele vya maendeleo pamoja na utekelezaji. Hii itasaidia wananchi kuwa wasimamizi wa moja kwa moja wa miradi ya maendeleo inayotekelezwa katika maeneo yao.

• Serikali iwatumie wataalamu wa masuala ya uchumi walioko nchini badala ya kutumia wanasiasa pekee katika kuandaa bajeti na matumizi ya serikali, pia serikali ijenge utamaduni wa kuwatumia wataalamu waliobobea katika fani mbalimbali nchini katika kuandaa na kusimamia sera mbali mbali kwaajili ya kukuza uchumi na kuleta maendeleo ya Taifa pamoja na kuheshimu mawazo na maelekezo ya wataalamu katika sekta mbalimbali hata pale yanapotokea majanga yanayohitaji ufumbuzi wa kitaalamu. Kwa kufanya hivi, tutapunguza au kudhibiti matamko ya kisiasa katika mambo nyeti yanayohitaji ufumbuzi wa kitaalamu kama vile Afya, Elimu na Uchumi.

Hitimisho
Natoa wito kwa viongozi/wenye mamlaka, na watunga sera wa nchi, maamuzi yoyote wanayofanya yanaathiri au kufaidisha jamii nzima, wao ni sehemu ya jamii na hivyo wataathirika au kufaidika na maamuzi hayo kwa namna moja au nyingine. Ni vyema kufanya uchambuzi yakinifu kabla ya kufanya maamuzi ili kuepuka athari zozote zitakazoisababishwa na maamuzi yao ikiwa ni pamoja na kurudisha nyuma maendeleo ya Taifa.

Asanteni Sana​
 
Upvote 1.3K
Ahsante kwa mada nzuri...
Lakini pia vyama vya Siasa vinabidi ndiyo vyewe wajibu wa kusimamia dira ya Taifa asa chama kinachokua madarakani. Tukipigie kura chama kitakachoweza kusimama na dira ya Taifa..
Ni kweli kabisa, ila vyama vyetu hivi vinasimamia fikra za mwenyekiti badala ya dira ya Taifa
 
Tanzania inateswa na mfumo uliosimikwa awamu ya kwanza ambapo Rais alitengenezwa akawa kama Baba wa familia. Hamna mifumo thabiti inayo weza kumuwajibisha. Kiongozi mkuu wa nchi anakuwa nusu na robo mungu mtu. Sijui tutafanya kitu gani kugeuza hali hii ili Rais awe mtumishi wa watu aliye aminiwa na wenzake awaongoze.

Ukisikia Mawaziri na viongozi wengine wanavyo ongea kuhusu miradi kwa mfano. Rais ametuletea hiki na hiki na bado ameahidi atatuletea na kufanya hiki na hiki. Kama vile hizo fedha zinazotumika kufanyia hayo maendeleo zinatoka mfukoni kwa Rais kumbe uhalisia ni fedha za wananchi wenyewe walizo changishwa kupitia kodi, tozo au kutoka kwenye raslimali nchi. Aina hii ya kuwapumbaza wananchi matokeo yake ni kuwafanya matahira na kukosa uchungu hata wanapoona fedha zao zinatapanywa. Kwanza walio wengi hawajui ni fedha zao wanafikiri niza Rais na serikali wanaona ni ujuha kumuingilia anayetumbua chake. Nani wa kutoa elimu kuwashika masikio wananchi. Tutasubiri mpaka Yesu arudi halitokei kwa hiari unless hatua za makusudi zimechukuliwa na wenye nyoyo za kizalendo.

Itungwe sheria na mechanisim ya kumlazimisha Rais kufuata dira ya Taifa atake asitake. Dira ya taifa iambatane na njia za utekelezaji wake zinazotoa mwanya wa kuhuhishwa kisheria. Bunge liweze kuisimamia serikali na yawekwe mazingira ya kisheria yanayo zuia Serikali kupitia Rais kuligeuza hili bunge kuwa ni kama muhuri wa kuidhinisha mambo ya Rais anavyotaka yeye. Hili linawezekana kama maslahi ya Wabunge yatatengwa na utegemezi kutoka serikalini. Maana hapo ndipo serikali ilipo shika kwenye mpini na bunge kwenye makali ya upanga. Wanaogopa kuiwajibisha serikali kulinda maslahi yao. Jambo baya zaidi ni la Mawaziri kutokana na Wabunge na kutegemea fadhila za Rais kuteuliwa nafasi hizo. Utaratibu huu umewafanya wabunge kujipendekeza kwa Rais na kusema kweli kunawafanya watende dhambi ya unafiki kila itwayo leo. Wakati mwengine huwahujumu Mawaziri wakitegemea watatenguliwa na wachukue nafasi za wahusika. Kwenye mfumo kama huu unategemea dira ya taifa iwe effective?! Kwa shida sana na kwa nguvu nyingi.
 
Na akishindwa tu kuifuata akina Colonel Mamady Doumbouya wafanye yao potelea mbali liwalo na liwe! [emoji51][emoji51][emoji51]
View attachment 1927112

Hatutaki hii dhambi ya kula nyama za watu itokee Tanzania. Mungu wa Mbinguni atuepushe na haya mambo na awasaidie viongozi wetu waombe hekima itokayo kwa Mungu katika kutungoza. Wakishindwa kufanya hivyo watufute wenye hizo Hekima wawazunguke. Modekai wa Biblia alipewa Pete yenye Muhuri wa Mfalme aandike Waraka uende kwenye himaya yote ya mfalme enzi zake. Yusufu alipewa uongozi akiwa utumwani Misri akawa Mkuu wa Misri yote kasoro Mfalme na wa familia yake tu. Akaweza liokoa Taifa la Misri ya Farao wa wakati ule kwa janga la njaa ya miaka saba mfululizo. Mifano michache tu hii.
 
Bado cpati majibu,kwa nn serikali imewabana wananchi wa chini kulipa kodi nyingi na sio kubana matumizi serikalini,kuna matumiz mengi sana serikalini ambapo mengi ni matumiz mabovu ya fedha,lakin kipigo kimegeuzwa kwa wananchi .
Ukiuliza vizuri watakuambia wao ndio watendaji wakuu,ila kiukweli kuna sehemu serikali inatumia pesa nyingi pasipo sababu za msingi,mfano kwenye misafara ya viongozi,baraza kubwa la mawaziri, mishahara mikubwa,posho za vikao bungeni,yote haya bado hawaridhiki wengine wanataka hata kuongezewa,ukija upande wa pili wa shilingi wananchi wana vipato vidogo,maisha duni lakini kodi na tozo kibao, wanasiasa wa Tanzania hawako kwa maslahi ya nchi hii.
 
Kwa sababu sisi wananchi tumekubali kubambikiwa tozo zote, hauwezi kuhoji wala kupinga hizi tozo za uonevu matokeo yake zitaletwa nyingine nyingi tuu
Mfano mwingine wa mambo ya ajabu ni mchango wa mwenge,niikuwa nasikia tu watumishi wanalalamika sana kuhusu hii ishu lakini mwaka huu nimeshuhudia mwenyewe,watumishi wanaonewa sana,vitisho kibao kutoka kwa wakurugenzi na wakuu wa wilaya mpaka unajiuliza mbio za mwenge zipo kila mwaka kwanini wasipange bajeti yake inayojitosheleza badala ya kuwakamua watumishi.?
 
All in all katiba ifanyiwe marekebisho hii italeta freedom kila sector kufanya biashara kwa haki kwa kila mtanzania bila usumbufu,hii itapelekea vyombo vya habari kuwa huru na kusemea pale ambapo viongozi wamekosea.
Ni kweli kabisa lakini je ni nani atasimamia mchakato huo wa katiba mpya?
 
Abrianna umeandika mengi yenye uzito, pia umependekeza sana taaluma ipewe upekee kwa uzito wake kama ukivyo ndani ya jamii.
Hebu tujiulize, mimi wewe na wachangiaji wengine? Je, ni wataalumu gani hawa unaotaka waaminiwe na kupewa nafasi?
Mnakumbuka Wataalam wetu akina Kabudi, Mpango, Kitila Mkumbo, na wengineo wengi ambao walipewa hizo nafasi lakini wakageuza utaalam wao kuwa dekio la uchafu wa wanasiasa? Mbaya zaidi na wao wakajigeuza vijakazi wa hao wanasiasa?
Mkuu nchi hii ina wataalamu wengi sana ukitoa hao ambao umewataja hapo juu, tatizo la nchi hii ni serikali kushindwa kutambua mchango wa wataalamu hao, inawezekana kabisa wataalamu wa nchi hii wanaishauri serikali vizuri kabisa,lakini kwakuwa wanasiasa wa nchi hii ni wabinafsi,wamekuwa wagumu sana kupokea mapendekezo ya wataalamu katika mambo mbalimbali rejea sakata la Rais Magufuli na Ndugulile,Mwele Malechela wa NIMR,yote hayo yalitokea sababu wanasiasa wa nchi hii wanajifanya wanajua kila kitu.
 
Kuna watu wakiona umekosoa serikali kwa namna yoyote wanakuhusisha na upinzani au unatuhumiwa kumkosoa magufuri, tujifunze kuishi nao tu ndio njia lahisi
Kweli kabisa yaani.
Watanzania tu shida sana,yani ukishauri serikali kidogo tu utaambiwa wewe CHADEMA, vivyo hivyo hata kwenye mpira ukikosoa Yanga,unaambiwa wewe unashabikia simba,sijui tuna matatizo gani sisi.
 
Huko objective badala yake umekopi na kupaste ngonjera za wapinzani. Nikupe mfano. Unasema ununuzi wa ndege na ujenzi wa madarasa ni hasara. Unakua na mtazamo kama ceo wa kampuni badala ya kutazama nchi. Nchi kuna mambo yanawekezwa kwa long term benefit. Kwa nchi kubwa kama tanzania usafiri wa anga unachochea sekta nyingi kukua. Na hasa nchi kama yetu yenye vivutio vya kitalii. Hasara ya airline inaweza fidiwa kwa overall benefit kwenye kukua uchumi. Hili la madarasa unaonyesha uelewa mdogo kwa mambo ya uchumi. Nchi sio kampuni ya biashara. Lengo ni kuwaletea wananchi maendeleo. Kuna maeneo serikali inabidi kuwekeza kwa kua kibiashara wawekezaji wanaangali short term results.
Siwezi comment kila kitu ila kwa hayo machache unaweza kupata kitu.
Asante mkuu kwa mchango wako lakini je kwa mtazamo wako unayaonaje mapendekezo ya mleta mada,je yakifanyiwa kazi yanaweza kuleta mabadiliko chanya katika nchi?
 
Serekali nadhani ilikuwa na chuo cha mipango na wizara ya mipango hawa ndio wapo responsible kwa dira ya.maendeleo taifa
Vyuo vipo na vinatoa maafisa mipango wengi tu na wengine ni waajiriwa serikalini,shida ni kwamba hao maafisa mipango wenyewe wanafanya kazi kama walivyo watumishi wengine serikalini,umesema kwamba hao ndio responsibile kuanda dira ni wazo zuri ila nina uhakika bila kuwepo wataalamu wengine katika kuanda hiyo dira ya maendeleo pamoja back up ya serikali kuu na katiba imara,hawa hawawezi kufanya kitu chochote kikubwa.
 
Tume huru ya katiba na mahakama huru,Ambayo haifungamani na chama chochote,hi italeta amani Zaid kwa wana inchi,mfano mzuri South Africa.
Shida ni kwamba hata mahakama zetu hazipo huru, sehemu pekee tunayoitegemea kupata haki nayo tumeanza kuiogopa
 
Kweli kabisa yaani.
Watanzania tu shida sana,yani ukishauri serikali kidogo tu utaambiwa wewe CHADEMA, vivyo hivyo hata kwenye mpira ukikosoa Yanga,unaambiwa wewe unashabikia simba,sijui tuna matatizo gani sisi.
Ndio maana tunaongezewa tozo kila siku na bado tunanyamaza maana ukisema utaambiwa wewe ni mpinzani hutaki kuchangia maendeleo ya nchi
 
Vyuo vipo na vinatoa maafisa mipango wengi tu na wengine ni waajiriwa serikalini,shida ni kwamba hao maafisa mipango wenyewe wanafanya kazi kama walivyo watumishi wengine serikalini,umesema kwamba hao ndio responsibile kuanda dira ni wazo zuri ila nina uhakika bila kuwepo wataalamu wengine katika kuanda hiyo dira ya maendeleo pamoja back up ya serikali kuu na katiba imara,hawa hawawezi kufanya kitu chochote kikubwa.
Maafisa mipango wapo na Tume ya mipango ipo, ila hiyo dira wanayoiandaa na mipango wanayoipanga haina usimamizi, hata wao wenyewe hawawezi kuisimamia itekelezwe kwa wakati, unadhani nini kifanyike?
 
Mkuu nchi hii ina wataalamu wengi sana ukitoa hao ambao umewataja hapo juu, tatizo la nchi hii ni serikali kushindwa kutambua mchango wa wataalamu hao, inawezekana kabisa wataalamu wa nchi hii wanaishauri serikali vizuri kabisa,lakini kwakuwa wanasiasa wa nchi hii ni wabinafsi,wamekuwa wagumu sana kupokea mapendekezo ya wataalamu katika mambo mbalimbali rejea sakata la Rais Magufuli na Ndugulile,Mwele Malechela wa NIMR,yote hayo yalitokea sababu wanasiasa wa nchi hii wanajifanya wanajua kila kitu.
Wakati mwingine wataalamu wanaogopa kuishauri serikali maana wanaweza wakaonekana wanapingana na Fikra za mkuu wa nchi na wakaonekana wahaini au wasaliti, kwa kifupi wataalamu hawapewi nafasi ya kutosha kushiriki kwenye maendeleo ya nchi, na hata wanapopewa wanashiriki kwa woga au wanaweka taaluma pembeni wanafanya kazi kisiasa
 
Ni kweli kabisa lakini je ni nani atasimamia mchakato huo wa katiba mpya?
Mchakato wa katiba mpya umetupiliwa mbali kwa kigezo kwamba tunainua uchumi kwanza, na yeyote anaeleta habari za katiba mpta anashughulikiwa. wananchi nao wamekaa kimya kiasi kwamba serikali inaona kwamba katiba mpya sio kipaumbele cha wananchi
 
Back
Top Bottom