Utajiri wa rafiki yangu ulivyofanya nikamuamini Shetani

Utajiri wa rafiki yangu ulivyofanya nikamuamini Shetani

Nisikuchoshe na usinichoshe, tusichoshane!.

Kwanza kabisa nipende kuwashukuru wote ambao mmeendelea kuwa na mimi bega kwa bega tangia mwanzo wakati naanza kusimulia visa vya maisha yangu ambayo nimeyaishi na kuyapitia kama mwanadamu.

Simulizi yangu ya kwanza kabisa hapa JF imefahamika kama "TULICHOMFANYA YULE MCHAWI HATOKUJA KUSAHAU KAMWE" hii inapatikana kwenye jukwaa hili la Entertainment, simulizi hii iliangazia namna tulivyopata shuruba ya ushirikina wakati ambao nilienda kumsalimia baba yangu mdogo aliyekuwa mwalimu katika shule moja ya sekondari huko mkoani Tabora, kiukweli ni mkasa ambao sitokuja kuusahau kamwe kwasababu ndipo niliamini wachawi wapo na uchawi upo!

Simulizi ya pili ilikuwa ni muendelezo baada ya hiyo ya kwanza, simulizi hii ya pili niliona nianze kusimulia baada ya mimi kwenda shule ya upili(Advance)na wakati nilipomaliza matokeo yangu hayakuwa mazuri hivyo nikatimuliwa na Mzee(Baba)yangu nyumbani nikaingia mtaani kupambana, simulizi hii inafahamika kama "NILIVYONUSURIKA KIFO BAADA YA MZEE KUNITIMUA NYUMBANI" na inapatikana kwenye jukwaa la Habari na Hoja Mchanganyiko.

Sasa leo nimeona niwaletee na niendelee na masimulizi ya maisha yangu ili kuwapa hamasa vijana wenzangu kuweza kupambana na kutokata tamaa mapema! Dhumuni la masimulizi yangu ni kutoa funzo kwa watu na sipo hapa ili kujipatia fedha kwa njia ya ulagahai, mimi binafsi ninajiweza kwasababu ni mpambanaji na sihitaji hata mia mbovu ya walalahoi wenzangu!.

Mimi binafsi ni mfanyabiashara, nimejiajiri kwa kutoa huduma ya usafirishaji wa abiria almaarufu kama Bodaboda, shughuli zangu huwa nazifanyia hapa Bunju, ingawa ki makazi naishi Mbezi Inn ila kikazi nafanyia Bunju. Sasa kama mtakumbuka kwenye simulizi ya mwisho nilisema ya kwamba, baada ya kuwa tumeuza lile duka la vipodozi ambalo tulikuwa tumefungua na rafiki yangu kipenzi Mtatiro (Kwa sasa anaishi nchini Uganda), tuliamua kugawana fedha kila mtu afe na chake, mimi niliamua kurudi zangu Tarime-Sirari, baada ya kukaa kule kuna ndugu yangu(Mtoto wa Baba yangu mkubwa) tuliwasiliana naye akaniambia nije Dar es salaam ili tufanye biashara ya uuzaji wa vyombo vya ndani kwasababu kwa wakati huo ilikuwa na pesa(Kwa maelezo yake).

Niliianza safari ya kuja Dar es salaam, sasa nilipofika Dar es Salaam pale Ubungo(Kipindi stendi bado haijahamia Mbezi), ile nimefika mida ya saa 5 usiku nikampigia simu mwenyeji wangu lakini majibu toka kwenye simu ni kwamba "Namba unayopiga kwasasa haipatikani, jaribu tena baadae", niliendelea kuipiga ile simu lakini majibu yalikuwa ni hayo hayo!.

Kwakuwa nilikuwa nimechoka, niliamua kumsikiliza moja ya watu ambao walikuwa wakinisumbua ili wabebe mzigo wa begi langu ili niwalipe posho, mpaka wakati huo nilikuwa makini sana kujilinda mimi binafsi pamoja na mzigo wangu, kilichofanya nikawa makini kupita kiasi ni stori ambazo mara zote nimekuwa nikizisikia kuhusu Jiji la Dar es Salaam na vioja vyake.

Mimi " Mwanangu vipi!?"

Jamaa " Poa bro"

Mimi "Mbona mnavurugu, shida ni nini?"

Jamaa " Si huyu msenge, nimemwambia wewe ni wakwangu lakini hataki kusikia"

Mimi "Ok mnasemaje"

Jamaa "Bro we nipe begi mi nikubebee, achana na huyu muhuni atakuibia"

Mimi " Sasa wote mnang'ang'ania mzigo, nimpe nani na nimwache nani?"

Mimi "Sa sikia, begi langu nitalibeba mwenyewe, achaneni na mimi"

Baada ya kusikia lafudhi yangu na namna nilivyochukia nadhani waliamua kutii sheria bila shuruti, waliondoka wakiwa wananiangalia kwa uchungu na maumivu makali ya kukosa posho! Kiukweli muda huo nilichokiongea ndicho nilichokuwa nikikimaanisha, kutokana na sifa mbaya za mkoa wa Dar es Salaam nilikuwa nimesema yeyote ambaye angejitia kimbelembele kunikaba au kuniibia, basi siku hiyo ndiyo ingekuwa mwisho wa maisha yake! Jeuri na kiburi cha kikurya vilinitia morali maradufu na niliwaona wale vijana wa pale stendi ni kama wanawake tu wasiokuwa na uwezo wa kunifanya chochote!.

Niliamua kujisogeza mpaka kwenye geti la kutoka nje, nilipotoka nje nilikuwa nikiendelea kushangaa pilika pilika namna zilivyokuwa za kutosha pale stendi, kiukweli sikuwahi kuona mji uliokuwa na pilika nyingi kama Dar es Salaam.

Mwanza nimekaa lakini hakukuwa na harakati za kutosha kama Dar es salaam. Nilichukua simu yangu nikawa nampigia tena mwenyeji wangu lakini simu yake ikawa haipatikani. Nilichukia sana kwasababu nakumbuka nilivyofika Singida alinipigia simu nikamwambia ya kwamba nimefika Singida na akawa amesema ikifika mida ya saa 2 usiku angekuwa amekuja pale stendi ili anisubiri nikifika tuondoke wote.

Kuna jamaa mmoja alikuwa kando ya geti la kutokea nje ya stendi pale Ubungo nilimsogelea nikawa namuuliza kuhusu Guest House yeyote iliyokuwa karibu ili niende nikalale na ikiwezekana asubuhi niendelee kumtafuta jamaa.

Jamaa "Sasa tutafanyaje ndugu!"

Aliendelea "Mwenyeji wako hajatokea?".

Mimi "Nimempigia simu lakini hapatikani!"

Jamaa "Duuuu mbona ni hatari!"

Aliendelea "Sasa sikia, wewe nyooka na hii barabara, unaona kwenye ile njia?"

Mimi "Ndiyo"

Jamaa "Hebu subiri"

Jamaa " Hassaniiiiiii"

Baada ya ya kuita hilo jina muhusika alifika

Jamaa "Hassani hebu nenda kampeleke huyu jamaa pale kwa Asteria, ukifika mwambie jamaa anataka chumba"

Aliendelea "Kaka nenda na jamaa atakupeleka kwenye Lodge ambayo kuna usalama na vyumba vipo vya kutosha, ila utamlipa maana kuna umbali"

Mimi "Hakuna tatizo"

Basi yule jamaa aliyeitwa Hassan akanichukua akanivusha barabara tukaikamata njia ya Ubungo Maziwa kuelekea kwenye hiyo lodge ambayo nimeambiwa kuna usalama na vyumba vya kutosha. Wakati tunakwenda na Bwana Hassan tulikuwa tunapiga stori za hapa na pale huku mikono yangu ikiwa bize imeng'ang'ania begi kwasababu ndilo lililokuwa na hela pamoja na nguo za kubadilisha, kiukweli nilikuwa nimesema endapo yeyote angejipendekeza kunikaba angejuta kuzaliwa.

Baada ya mwendo mrefu kidogo hatimaye tukawa tumefika kwenye Bar moja iliyokuwa inapiga mziki kwa sauti kubwa huku kukiwa na watu wengi.

Hassan " Nisubiri hapa nakuja"

Nilimsubiri Hassan pale nje baada ya kufika kwenye hiyo Bar na baada ya dakika 15 akawa amekuja kunichukua na kuongozana nae kuingia ndani. Tulipofika ndani ambako kulikuwa na kaunta, Hassan alinichukua tena kuelekea Uani ambako nilikuta kuna vyumba vingi ambavyo vilikuwa havipungui 10.

Sasa baada ya kufika pale Uani alikuja mwanamke mmoja mweusi mnene na ndiye aliyekuwa akiitwa Asteria, alimuita Hassan Pembeni wakawa wanaongea, sikufahamu kitu walichokuwa wanazungumza kwa wakati huo. Baada ya yale mazungumzo Hassan alirudi kwangu.

Hassan "Sasa bro,mimi nadhani nikuache wewe upumzike, niangalizie basi ustaarabu"

Mimi "Chumba changu cha kulala ni kipi?"

Hassan "Atakuonyesha Asteria, wala usijali kaka hapa ni nyumbani"

Baada ya maneno ya kutia moyo ya Hassan nikachomoa shilingi elfu 5 nikawa nimempatia kama posho ya kunipeleka hapo Guest.

Hassan "Aaah kaka hela gani hii?"

Mimi "Hela gani kivipi?"

Hasaan "Aaaah Kaka yaani nikutoe kule stendi na nimeacha shughuli zangu halafu unanipatia buku tano? Hebu ongeza ongeza kaka angalau kesho niamkie supu"

Sikutaka mambo mengi na yule Jamaa ikabidi nizame tena mfukoni nikatoa elfu 5 nyingine nikampatia, hivyo kufanya jumla kuwa elfu 10.

Baada ya jamaa kuondoka lile eneo nikamfuata yule demu aliyeitwa Asteria ili aje anionyeshe chumba niingie kulala kwasababu nilikuwa nimechoka.

Asteria "Kaka ina maana Hujaambiwa huu si muda wa kulala?"

Mimi "Si muda wa kulala?"

Mimi "Si muda wa kulala kivipi?"

Asteria "Kaka hapa huwa hatulazi watu ila tunakodisha!"

Aliendelea "Hivi vyumba vinakodishwa kwa dakika na masaa, labda usubiri mpaka saa 9 wateja wakipungua ndipo tutakukodishia ulale"

Kiukweli baada ya ile kauli niliishiwa nguvu ghafla, sasa baada ya kuniambia maneno yale yeye aliondoka akaenda kuendelea na shughuli zake akaniacha pale Uani nikiwa sijui cha kufanya, sasa ndipo nilikuja kugundua ya kwamba, vile vyumba vilikuwa vinatumika kwenye biashara ya short time(Biashara ya Ngono),sasa kumbe ile Bar niliyopelekwa, pale nje kulikuwa na wanawake wanaouza miili yao(Dada Poa) na vile vyumba vilitumika kwa shughuli ya short time.

............................................................................................


Utajiri wa rafiki yangu ulivyofanya nikamuamini Shetani - 02.

Kwakuwa muda ulikuwa umekwenda sana na kwakuwa nilikuwa mshamba wa jiji, niliona ni vema nisihangaike kuzurura huo usiku bali niendelee kusubiri na kuvumilia hadi muda ambao yule muhudumu aliniambia vyumba vingekuwa tayari kwa kukodishwa.

Sasa pale ndani kulikuwa na madumu ya maji yaliyokuwa na maji na mengine yalikuwa tupu, niliamua kuvuta dumu moja lililokuwa tupu nikakalia, wakati nimekaa nilichukua tena simu yangu nikaanza kumpigia mwenyeji wangu lakini bado hakukuwa na mafanikio, niliwaza nimpigie mama yangu lakini kwakuwa ilikuwa usiku sana sikutaka kumsumbua. Niliendelea kuvumilia pale uani huku nikishuhudia madada poa ambavyo wakibadilisha wanaume kama mvua, ilikuwa kila baada ya dakika moja kuna ambao walikuwa wanatoka vyumbani na wanaume na wengine wakiingia, ilikuwa ni kuingia na kutoka! Kelele za muziki na mioshi ya sigara ilifanya nikalichukia lile eneo kwa ule muda lakini sikuwa na namna ilibidi nivumilie tu angalau pakuche.

Baada ya uvumilivu wa muda mrefu, ilipofika muda wa saa 9 usiku, yule muhudumu aliyeitwa Asteria alikuja akawa ameniambia ni muda sasa wa mimi kuingia kulala!.

Asteria "Kaka chumba hiki hapa nadhani unapaswa ulipie ili uweze kulala"

Mimi "Ni shilingi ngapi?"

Asteria "Ngoja nikuitie mtu anayehusika na vyumba"

Asteria " Aminaaaa"

Aliendelea " Wewe Aminaaa"

Amina "Abeeeee"

Asteria "Haya mteja wako huyu"

Amina " Anataka chumba?"

Asteria "Eeeh"

Amina "Jamani mapema yote hii!"

Asteria "Huyu kaka amesubiri sana msaidie bhana"

Amina "Haya anipe Elfu 20"

Basi kwakuwa nilikuwa nimechoka sikutaka kabisa majibizano na mtu,nilichomoa elfu 20 nikampatia huyo muhudumu kisha nikaingia zangu kwenye chumba nilichokuwa nimeonyeshwa na Asteria.

Nilipoingia mle ndani kwenye kile chumba kiukweli hakustahili mwanadamu mwenye akili timamu kulala kwasababu kilikuwa kichafu sana, uchafu ninaouzungumzia hapa si uchafu wa takataka bali ulikuwa uchafu wa taka mwili, nilikuta kondomu zimetupwa ovyo japo kulikuwa na kidastibini kidogo lakini sijui ilikuwa ni dharau au ni nini maana kondomu zilitupwa tu chini zikiwa na shahawa ndani yake, dirisha la kile chumba pia kulikuwa na pazia lililokuwa chafu kupita kiasi, nilipotazama ukutani ndiyo usiseme, nadhani ule ukuta watu waliokuwa wakiingia mle ndani walikuwa wakiiutemea mate au kuukojolea kwasababu ulikuwa umejaa michirizi ya rangi ya kahawia na njano iliyokuwa imekauka na hivyo kuufanya ukuta kuonekana mchafu.

Godoro lenyewe pia lilikuwa na kava tu llililokuwa limechakaa na lilikuwa limechoka hatari! Kiukweli kutokana na ile harufu ya ule uchafu nilitoka ndani nikaelekea kwenye korido aliyokuwa amekaa yule dada aliyeitwa Amina.

Mimi "Sista mbona kile chumba ni kichafu!"

Amina "Kaka vyumba vyote hapa ndivyo vilivyo kama hutaki kulala unaweza kukaa nje!"

Mimi "Kwani hakuna chumba ambacho angalau ni kisafi?"

Amina "Hebu twende"

Basi yule dada alinyanyuka kwenye kiti akawa ametangulia na mimi nikamfuata nyuma kama mtu na mke wake!.Alianza kufungua chumba kimoja baada ya kingine vile ambavyo havikuwa na watu.

Amina "Je hiki kitakufaa?"

Nilikisogelea kile chumba na kutazama kwa ndani ili nione kama kitafaa.

Mimi "Angalau hiki"

Amina "Sawa"

Niliingia ndani ya kile chumba nikafunga mlango kisha nikakaa zangu kitandani nikiendelea kukitazama. Kile chumba hakikuwa na tofauti kubwa na kile cha kwanza sema hiki cha pili angalau sikukuta kondomu chini na godoro lake halikuchoka sana kama lile la kwanza, japo kulikuwa na kiharufu fulani cha kukera lakini sikuwa na namna ilibidi nivumilie pakuche!. Nilivua viatu kisha nikapanda kitandani kujiegesha, mle ndani hakukuwa na shuka wala taulo, mimi niliamua kulala na nguo zangu angalau zikanisitiri na kiubaridi kile cha Alfajjri.

Mida ya saa 3 asubuhi nilishitushwa na kelele za watu wakiwa wanafokeana hapo nje, niliamka zangu nikavaa viatu kisha nikachukua begi langu nikalitia mgongoni nikatoka nje, nilipotoka nje nikawakuta kina dada wawili wakiwa wanatambiana kwa matusi kedekede! Niliwashangaa namna walivyokuwa wakiporomosheana matusi ya nguoni bila aibu, sikutaka kupoteza muda kwenye mambo ya kijinga, niliondoka zangu kuelekea nje nione nitaianza vipi siku kwenye hili jiji ambalo ndiyo ilikuwa mara yangu ya kwanza kufika!.

Nilichukua simu yangu nikaanza kumtafuta mwenyeji wangu lakini simu haikupatikana hewani kabisa, kiukweli nilibaki najiuliza maswali mengi sana ambayo hayakuwa na majibu. Jamaa ndiye aliyefanya mimi kuondoka Tarime na kuja Dar es Salaam na wakati nikiwa kwenye gari tulikuwa tukiwasiliana naye kutwa nzima, sasa sikufahamu ni kitu gani ambacho kilimpata hadi asipatikane kwenye simu. Niliamua kumtafuta mama yangu na kumueleza kila kitu kilichokuwa kimetokea.

Mama "Sasa utafanyaje?"

Aliendelea "Ndugu wa upande wa baba zenu niliwahi kuwaambia huwa wana tabia za kijinga lakini huwa hamnisikii!"

Mama "Sasa kama mliongea na akajua unaenda kwanini hapatikani kwenye simu?"

Aliendelea "Mpigie mjomba wako Nicholaus"

Mimi "Sinaga namba yake mimi"

Mama "Hebu subiri"

Basi baada ya mazungumzo ya muda mfupi na mama yangu alikata simu, Mama yangu alishangaa sana mimi kwenda Dar es Salaam bila taarifa na kibaya zaidi alikuwaga hapendi kabisa sisi wanae kwenda upande wa baba zetu kwasababu hawakuwaga na msaada zaidi ya masimango na manyanyaso.

Baada ya dakika kama 10 kuna namba ngeni ilinipigia simu ikabidi nipokee kwa uharaka na nilidhani uenda atakuwa jamaa ametumia namba nyingine.

Sauti ya Kiume "Wewe uko wapi?"

Mimi "Nani mwenzangu?"

Sauti ya kiume "Mjomba wako Nico hapa"

Mimi " Ooh Anko shikamoo!"

Anko Nico "Kwahiyo sikuhizi umesahau kikurya hadi uniamkie Kiswahili?"

Mimi "Hapana Anko"

Anko Nico "Haya bhana"

Aliendelea "Wewe unakujaje mjini bila taarifa? Au unadhani hapa ni Mogabiri?"

Mimi "Niliwasiliana na Kileri Anko sema nilipofika nimejaribu kumpigia hapatikani!"

Anko Nico "Huyo Kileri ni nani?"

Mimi "Ni mtoto wa Ba'mkubwa"

Anko Nico "Hapa ni mjini hebu acha ujuaji wa kijinga, sema uko maeneo gani nitume mtu aje akachukue"

Basi nilisogea eneo moja nikamuuliza jamaa mmoja pale ni wapi akawa ameniambia ni Ubungo Maziwa, ndipo nilimpa Anko Nico taarifa.

Anko Nico "Uliza mtu yeyote hapo jirani akuonyeshe jengo la Ubungo Plaza lilipo na uende hapo ukasubiri kuna mtu namtuma anakuja kukuchukua"

Mimi "Sawa anko"

Niliuliza watu bahati nzuri nikawa nimeonyeshwa jengo la Ubungo Plaza na nikaliona kwakuwa lilikuwa refu, nilitembea mdogo mdogo huku nikiwa makini sana na begi langu mgongoni asije kibaka yeyote akanikwapua akakimbia. Nilipofika hapo Ubungo Plaza nilimpigia Anko Nico simu kisha akawa ameniambia kuna mtu amempatia namba yangu ya simu akifika hapo atanipigia simu.



............................................................................................




Utajiri wa rafiki yangu ulivyofanya nikamuamini Shetani - 03


Nilisimama pale kando ya lile jengo la Ubungo Plaza huku nikiendelea kuwa makini sana, baada ya muda wa nusu saa kuna namba nisiyoifahamu ikanipigia.

Mimi "Hallo"

Yeye "Hallo, mambo vipi"

Mimi "poa, nani?"

Yeye " Ah mh! Wewe si ndiye mgeni wa Mzee Nicolaus?"

Mimi "Ndiyo"

Yeye "Ameniambia upo Ubungo Plaza nije nikuchukue"

Aliendelea "Umesimama eneo gani?"

Mimi "Nipo mbele ya hili jengo kaka, mbele kabisa ya mlango wa kuingia"

Yeye "Ok sasa vuka barabara uje upande wa pilipili unaiona hii gari nyeusi Prado imepaki hapa pembeni?"

Aliendelea "wewe si ndo umevaa shati la damu ya mzee na suruali ya kaki?"

Mimi "Ndiyo kaka, umeniona?"

Yeye "Nishakuona, vuka uje nakusubiri"

Nilivuka ile barabara kwa umakini mkubwa huku nikiendelea kushangaa magari namna yalivyokuwa mengi barabarani, wakati nimefika jiji la Dar es Salaam hii barabara ya kutoka Manzese hakukuwa imejengwa miundombinu ya Mwendokasi, hivyo haikuwa rahisi kuivuka ile barabara kwasababu magari yalikuwa rafu sana!. Nilipofika kwenye ile gari jamaa aliyonielekeza niliisogelea kisha nikamgongea kioo akawa amekishusha.

Jamaa "Shwari?"

Mimi "Swari kaka"

Jamaa "Ok Ingia twende"

Nilipanda kwenye ile gari nikaa mbele ili iwe rahisi kuyatazama maeneo ya jiji kwa uzuri zaidi. Wakati tupo kwenye gari hatukuwa na stori sana kwasababu jamaa muda wote alikuwa akiongea na simu.

Baada ya dakika kadhaa tukawa tumefika kwenye nyumba nzuri mno iliyokuwa na geti, ndipo jamaa alipiga honi akawa amefunguliwa geti, baada ya mimi kuteremka jamaa aliondoka na ile gari. Kiukweli ile nyumba ilikuwa nzuri sana na nilipokuwa mwenyeji ndipo niligundua Anko Nico alikuwa akiishi eneo la Ununio -Bahari beach.

Historia fupi ya Anko Nico.

Kiukweli mimi tangu nimekuwa, wajomba zangu nimekuwa nikiwaona Tarime wakiwa wamepita kumsalimia dada yao(Mama yangu), sikuwahi kuzifahamu familia zao na hata makao yao, na mara zote wakati wanapita hapo Tarime huwa wanakuja wenyewe. Hivyo ilikuwa tu ni eidha mama atuambie kuna mjomba wako anaishi sehemu fulani na mwingine yupo sehemu fulani.

Kaka zake mama ambao ni wajomba zangu, wapo wanne(4), Mmoja yupo Serengeti ni muajiriwa wa Tanapa, Mwingine ni Mwanajeshi aliwahi kuwa hapo Lugalo lakini siku hizi amehamishiwa Kigoma, mwingine anaishi na familia yake huko Botswana na mwingine ndiye huyu ambaye nilikuwa kwake, kwa bahati nzuri wote nimewahi kuwaona ila sikuwahi kuishi nao.

Kumekuwa na sintofahamu mara zote katika familia mbili na huwa sifahamu shida ni nini, kwa upande wa kina Baba nilikuwaga nikizingua au kufanya kosa lolote, wakati baba akiniadhibu alikuwa akiniambia nimechukua akili za kipumbavu za ujombani, vilevile mama nae alikuwa akisema upande wa kina baba wana roho mbaya na tabia za kipumbavu, sasa sikuwahi kufahamu ni kitu gani kilikuwa kinaendelea kati ya familia hizi mbili.

Anko Nico alikuwa ni Contractor na Mkewe hadi leo ninapoandika yupo anafanya kazi wizara ya Afya, Anko Nico kwasasa ni marehemu, hivyo mkewe ndiyo kila kitu kwenye familia yake kwasasa.

Nimeona nitoe historia fupi kidogo ili huko mbele maswali yapungue.

Basi baada ya kuachwa pale ndani ya fensi kulikuwa na ukimya wa ajabu, ni ndege tu ambao nilisikia wanalia kwenye miti, kiukweli mazingira yale ungedhani wanakaa mawaziri au viongozi wenye vyeo vikubwa Serikalini kwasababu kulikuwa kuzuri na kutulivu mno! Baada ya muda nikiwa nashangaa, mlango ulifunguliwa akawa ametoka nje binti mmoja aliyekuwa amevalia mavazi ya jikoni(Yale mavazi yanavaliwa na wapishi wakiwa jikoni wanapika).

Yule binti "Karibu"

Mimi " Ahsante"

Yule binti "Unaitwa nani?"

Mimi "Umughaka"

Yule binti "Kumbe ndiyo wewe!"

Tulipofika ndani nikaa kwenye kochi nikawa nashangaa namna watu walivyokuwa wakiishi, wakati naendelea kushangaa mara simu ya mezani ikawa inaita, yule binti akawa amekuja kuipokea.

Yule binti "Eeh amefika baba"

Aliendelea "sawa baba"

Baada ya yale maongezi yule binti akawa ameikata ile simu na kuondoka kwenda kuendelea na alichokuwa anakifanya.

Yule binti alipoivishwa chakula kilitengwa na kunitaka niende nikajisevie, nilinyanyuka zangu nikaenda kupakua msosi na kuanza kula, nilipomaliza kula yule binti alinionyesha chumba ambacho nilipaswa kwenda kuoga na ndipo ningelala kwa siku hiyo, sasa nilipofungua na kuingia ndani nilimkuta mzee mmoja akiwa amelala huku ikionekana kabisa afya yake imedhoofika kwasababu nilikuta amewekewa mpira wa kukojolea, yaonyesha hata kokojoa mwenyewe tu alikuwa hawezi.

Nilipoufungua ule mlango na kuingia ndani akawa ameshituka na kugeuka kwa shida kunitazama.

Mimi "Shikamoo"

Mzee "Marhaba"

Baada ya salamu sikuwa na stori zaidi ya kuendelea kumshangaa mzee huku na yeye akinitazama kwa umakini. Kwakuwa alikuwa amewekewa mpira wa kukojolea nilifahamu kabisa ni mgonjwa na hivyo ikabidi nimpe Pole.

Mimi "Pole sana mzee wangu"

Mzee "Pole ya nini mwanangu!"

Mimi "kwa maumivu mzee"

Mzee "Aaah haya nilishayazoea muda tu"

Aliendelea "wewe ni nani?"

Mimi "Mimi naitwa Umughaka, Nicolaus ni mjomba wangu"

Mzee "Oooh sawa"

Kwa namna mzee alivyokuwa akiongea alionyesha kabisa ni mtu kutokea pande za kaskazini mwa nchi yetu.

Nilivua nguo nikawa nimeingia bafuni kuoga, sasa wakati nikiwa bafuni nikawa nasikia simu yangu inaita mpaka ikakata, nilipomaliza kuoga moja kwa moja nilienda kuitazama na ndipo nikakuta ni mtoto wa baba mkubwa Kileri alikuwa akinipigia. Nilibadili nguo kisha nikampigia.

Kileri "Mwanangu nisamehe sana, uko wapi?"

Mimi "Nipo kwa Anko Nico"

Kileri "Maeneo gani kaka nije kukuchukua"

Mimi "Usijali niko salama kabisa kaka, nadhani nikitoka huku nitakufahamisha"

Kileri "Daaah nisamehe sana kaka, simu yangu huwa inasumbua betri, jana ilizima"

Mimi "Ungetumia hata simu ya mtu kaka"

Kileri "Tatizo namba yako sijaikariri kaka!"

Mimi "Usijali kaka hakuna kilichoharibika"

Kileri "Poa mwanangu lakini hakikisha huchelewi ili tupambane"

Mimi "Nikitoka huku nitakushitua"

Baada ya yale maongezi na Kileri nilitoka mle chumbani nikarudi zangu sebuleni. Nilikaa pale sebuleni huku nikiendelea kutazama luninga, mida ya saa 9 alasiri kuna mabinti wawili waliingia ndani, mmoja akiwa mkubwa na mwingine mdogo, japo kuwa wote walikuwa na miaka zaidi ya 18 lakini kuna mmoja alikuwa mkubwa kuliko mwenzie, wale mabinti walikuwa watoto wa mjomba Niko na kiukweli sikuwahi kuwafahamu na wao walikuwa hawanijui, waliniangalia na mmoja akanisalimia ila mmoja alikula buyu na kuzama ndani!.

Ilipofika mida ya saa 1 usiku, kuna gari iliingia ndani ya fensi ya ile nyumba na haukupita muda akawa ameingia ndani mke wa Anko Nico ambaye nimewahi kumuona mara moja tu pale Tarime wakiwa wamekuja mmewe kumsalimia mama.

Mke wa Anko "Habari ya siku"

Mimi "Nzuri, shikamoo"

Mke wa anko "Marhaba"

Aliendelea "Tarime wazima?"

Mimi "Wazima kabisa"

Mke wa anko "Wifi yupo?"

Mimi "Yupo mzima kabisa"

Mke wa anko "Karibu"

Baada ya salamu yule mke wa anko alizama ndani kwake huko. Ile familia ilikuwa ni familia ambayo ilikuwa haijali kabisa na kila mmoja alijali mambo yake.

Ilipofika mida ya saa 2 mjomba nae akawa amefika.Tuliongea mambo mengi sana na Anko Nico na alitaka kufahamu nimekuja Dar es salaam kufanya shughuli gani kwasababu aliniambia huu mji bila kuwa na kazi ni vema ningerudi Tarime kuliko kudhani kungekuwa na mteremko wa maisha mazuri. Baada ya kumwambia kilichokuwa kimenileta alielewa na akawa kimya.

Maisha ya hapo nyumbani kwa Anko yaliendelea kama kawaida na sasa nikaambiwa niwe namuangalia yule mzee na kumbadilishia mpira, kumuogesha na hata kwenda chooni nihakikishe niwe namtazama, ingawa alikuwa akijiweza kwa kujikokota lakini alihitaji uangalizi, sasa kumbe yule mzee alikuwa ni baba yake na mke wa mjomba Nico.

Niliona nikiondoka pale kwa Anko na kwenda kwa Kileri nitakuwa kama nimewadharau na niliona naweza kupata tatizo halafu ikala kwangu kwasababu ya kuondoka kwa ujuaji, nilisubiri Anko aniambie sasa ni muda wa kuondoka nikaendelee na shughuli zangu baada ya kunifadhili kwa makazi kwa muda.

Kwakuwa muda na siku zilikuwa zimekwenda, Kileri aliniambia kama inawezekana nimuelekeze maeneo nilipokuwa aje achukue ile hela ili akanunue mzigo wa kutosha aongeze kwenye duka kama tulivyokuwa tumekubaliana ili biashara iendelee kufanyika, sikuwa kabisa na shaka kwasababu niliamini ni mtoto wa baba yangu mkubwa na kwetu anafahamika na mimi kwao nafahamika, hivyo niliona ni vema nimwambie aje mpaka Ununio kuchukua ile hela akaendelee kufanya biashara na faida tuwe tunagawana.

Mipango yote ya ufanyaji wa biashara na upatikanaji wa faida tulikuwa tumeisuka tangu nikiwa Tarime, basi jamaa alikuja nikawa nimempatia ile yote milioni 9 akawa ameondoka.

Maisha yalisonga na jamaa akawa ananipa mrejesho kuhusu biashara na kiukweli kwa mujibu wa maelezo yake ilikuwa inachanganya vibaya hivyo sikuwa na shaka.

Pale kwa Anko walikuwa wakiondoka asubuhi nilikuwa ninabaki mimi na yule binti wa kazi huku mimi nikiendelea kumuangalia yule mzee na kuwa kama mtu wa usafi nje ya nyumba. Kadiri siku zilivyokuwa zinasonga ndipo na mambo yalianza kubadilika, kuna siku nilikuwa nikimsalimia mke wa anko anajifanya hajasikia salamu anasepa, nilidhani huenda ilikuwa ni kawaida kwa mtu mzima kuwa na mawazo kumbe haikuwa kama nilivyodhani.

Kuna siku aliporudi kutoka kazini kwake nikawa nasikia anamgombeza sana mjomba huko chumbani kwao na sikufahamu ni kitu gani kilikuwa kikiendelea.



.............................................................................................



Utajiri wa rafiki yangu ulivyofanya nikamuamini Shetani - 04.


Sasa muda ambao mke wa anko anafika pale nyumbani mimi nilikuwa nyuma ya nyumba ambapo kulikuwa kuna kama kibustani kidogo ndani yake kulikuwa kumepandwa miwa ambayo ilikuwa imekuwa mikubwa na hakukuwa na walaji, niliona nikate zangu muwa nikaa chini nikaanza kutafuna, kumbe aliingia chumbani anakolala yule mzee ambaye ni baba yake na akakuta amejisaidia kitandani na hakukuwa na mtu aliyemwangalia na kumjali, kwa mawazo yake yeye alidhani mimi nimemuona yule mzee na nikamuacha kama alivyo ili aendelee kuteseka!.

Akili na mawazo yake yalimtuma vibaya kwasababu sikuwa nimeingia mle chumbani tangia mchana, pia yule mzee alikuwaga kama na kakiburi fulani hivi ambako kalikuwa ka kijinga, anaweza kuwa amebanwa na haja kubwa wala asiite mtu yeyote, utakuta ameinyanyuka ameingia chooni na amechafua vibaya bila hata kuflashi. Inawezekana alifanya makusudi siku ile ili kunikomoa.

Kumbe muda huo Anko anapewa makavu laivu ilikuwa ni hiyo ishu na bahati mbaya sana Anko wangu alikuwaga hakoromi kwa yule mwanamke bali hasira za kugombezwa na mkewe zilikuwaga zinaishia kwa wanae au mimi kwa wakati ule nipo kwake.

Muda huo ambao nipo zangu natafuna miwa sina habari, kumbe alimwambia yule mfanyakazi akaingia mle ndani akatoa yale mashuka akawa amemnyanyua mzee akampeleka bafuni mzee akajisafisha kisha akatandika shuka safi na kuweka mazingira ya chumba poa.

Mimi sikufahamu chochote kwasababu nilipomaliza kula miwa nikazunguka kule mbele ya nyumba ndipo nikakuta gari ya mke wa anko ikiwa imepaki nikajua atakuwa amerudi, sikutaka kuingia ndani kwasababu ilikuwa bado mapema, niliingia stoo nikachukua fagio la nje nikaanza kufagia pale nje.

Nilipomaliza niliingia ndani kuoga na kubadili nguo ili nije nikae sebuleni nitazame luninga, wakati naingia mle ndani nilikuta mzee amelala na kitandani kukiwa na shuka nyingine, sikufahamu kumbe dakika chache zilizopita hali ya mle ndani haikuwa nzuri, sasa huo usiku anko alivyorudi ndipo mkewe akamuamshia mtiti!.

Baada ya hayo malumbano Anko alivyorudi sebuleni alikuwa amebadilika na sikutaka kusema chochote mimi niliendelea kutazama luninga, chakula kilipotengwa alielekea kula na alipomaliza aliingia chumbani kwake!. Mkewe yeye sikuonana nae kwa siku hiyo.

Asubuhi kama kawaida wao waliondoka wakawa wamelekea kazini, pale nyumbani nikawa nimebaki mimi, yule binti wa kazi pamoja na mtoto mkubwa wa anko ambaye naye aliondoka ilipofika mida ya saa 3 asubuhi. Sasa baada ya yule mtoto wa Anko kuondoka, yule binti wa kazi alikuja kuniita nikanywe chai, muda huo nilikuwa nje napambana kung'olea nyasi kwenye maua yaliyokuwa kando ya fensi.

Binti wa kazi " Hivi jana ulikuwa wapi?"

Mimi "Jana?, Jana saa ngapi?"

Binti wa kazi " Aliporudi Mama"

Mimi "Nilikuwa kule Bustanini"

Binti wa Kazi "Jana mama kagomba"

Mimi "Alikuwa anagomba kuhusu nini?"

Binti wa kazi "Aliporudi aliingia chumbani kwa babu akakuta babu kajinyea, alikuwa anakuulizia mimi nikajua labda umetoka!"

Mimi "Alijenyea saa ngapi? Mbona mchana nilipotoka ndani alikuwa tu vizuri"

Binti wa kazi "Alikusema maneno mabaya sana, we acha tu"

Mimi "Mimi siyo mjinga nimuone huyo mzee akiwa anashida niache kumsaidia, mbona siku zote namuosha na kumpeleka chooni na mpira nambadilishia!"

Mimi "Jana nilikuwa bustanini na sikutoka nje kabisa"

Mimi "Kwani kabla sijaja hapa nani alikuwa akimuangalia mzee?"

Binti wa kazi "Nani zaidi yangu? Wanae tu wala hawana time na babu yao"

Baada ya mazungumzo ya muda kadhaa nilinoti kitu kwa yule dada wa kazi ambacho hakutaka kabisa kuniambia, kwa kifupi yule mke wa anko inaonekana alitoa shiti nyingi dhidi yangu, niliamua kutulia na kutafakari.

Sikwenda kwa Anko huenda kwakusema nimepigwa na maisha ili anifadhili la hasha, nilienda pale kwasababu wakati nafika mjini mwenyeji wangu alikuwa hapatikani, sasa kuna muda nilikuwa nashangaa wanavyonichukulia ni kana kwamba nimepigwa na maisha!.

Baada ya kupata kifungua kinywa niliamua nimsubiri Anko akitoka kazini ile jioni nimuage na kesho yake nisepe niwaache wapambane na matatizo yao na roho zao mbaya. Kweli, usiku ule kabla ya kula tukiwa pale sebuleni tukiangalia taarifa ya habari, nilimwambia kesho mimi nitaondoka.

Anko Nico " Utaondoka kwenda wapi?"

Mimi "Nitaenda kwa yule mtoto wa baba mkubwa"

Anko Nico " Sawa siye tupo"

Baada ya hayo mazungumzo niliona kabisa nilikuwa sitakiwi. Ukiachilia Anko, lakini mkewe na watoto wa Anko walikuwa ni watu ambao hawana time na mtu, tangia nimefika hapo hawakuwahi hata kusema na mimi wala kujua hali ya maisha ya shangazi yao, walikuwa ni watu ambao hawakuwa na muda kabisa, pengine uzungu uliwaharibu au walirithi tabia za kwao mama yao.

Kesho yake nilimuaga yule mzee pamoja na yule binti wa kazi nikaondoka zangu, nilipotoka nje nilitembea hadi kituo cha daladala nikapanda kuelekea Tegeta.

Kwakuwa nilikuwa nimeshawasiliana na Kileri akawa ameniambia anakaa Kivule na hivyo ilipaswa nipande magari yatakayonifikisha Ubungo stendi ya daladala na nikifika hapo nipande za Gongo la Mboto nikashukie Banana kisha nichukue za Kivule.

Namshukuru Mungu nikawa nimefika na jamaa akaja kunichukua tukaelekea kwake. Nilipofika kwa jamaa nilikuta anakaa kwenye nyumba ambayo bado haijaisha na nilikuta mafundi wakiwa wanaweka vigae kwenye vyumba baadhi.

Kileri "Karibu wa kwetu, hapa mimi ndipo naishi na familia yangu"

Mimi "Hongera kaka umejitahidi"

Kileri "Kawaida tu, naipeleka mdogo mdogo mpaka itaisha, mjini hapa ukiwa na kwako unaepuka usumbufu wa kodi"

Baada ya mazungumzo ya hapa na pale, jamaa akawa ameniambia kesho yake tungeenda Tandika ambako alidai ndiko anakofanyia biashara ili nikajionee namna biashara ilivyoshamiri.

Ilipofika asubuhi tuliondoka kuelekea huko Tandika kama alivyokuwa ameniambia. Tulipofika hapo Tandika kuna duka moja la vyombo tuliingia lakini kuna kitu kikanishangaza.



..........................................................................................


Utajiri wa rafiki yangu ulivyofanya nikamuamini Shetani - 05


Jamaa wa duka "Oooh poti mtu mbaya"

Kileri "We mpemba acha zako"

Aliendelea "Jamal yuko wapi?"

Jamaa wa duka "Hapo nje hayupo?,alikuwa anaongea na simu hapo nje"

Kileri "Sijamuona"

Jamaa wa duka "Vipi unataka mzigo?"

Kileri "Ngoja kwanza nichonge na Jamal"

Yalikuwa ni mazungumzo kati ya Kileri(Mtoto wa baba yangu mkubwa) na Jamaa mmoja mwenye asili ya Pemba tuliyemkuta kwenye duka kubwa la vyombo vya ndani hapo Tandika.Sasa nilibaki kushangaa yale mazungumzo kwasababu Kileri alichokuwa ameniambia ni kwamba tulikuwa tunakwenda kuliona duka letu(Mimi na yeye) ambalo tulikubaliana kufungua.Nialiamua kutulia uenda hapo tulipita kwa rafiki zake ambao alikuwa akifahamiana nao hivyo tungeondoka muda si mrefu kuelekea kwenye duka lenyewe.

Baada ya dakika kadhaa kuna Jamaa mwingine aliingia dukani ambaye pia alikuwa na asili ya pemba na Kileri alipomuona alimuita ili waongee nje lakini jamaa ni kama akawa anamkataa!.

Jamaa "Tatizo lako poti mpaka tuanze kusumbuana kwenye simu,mzigo tunakupa lakini kona nyingi"

Kileri "Jamal eeh hebu njoo tuzungumze kaka"

Jamal " Kama ni hii ishu ya vyombo sitakuelewa lakini kama ni ishu nyingine sawa"

Kileri "We siunanijua lakini mimi ni mtu wa dili!"

Basi yule jamaa aliyeitwa Jamal alitoka nje na Kileri akawa ameniambia nimsubiri abonge kwanza na jamaa.Mimi nilikaa pembeni ambako sikuweza kusikia walichokuwa wanazungumza,baada ya mazungumzo ambayo Kileri alikuwa anamsisitiza sana jamaa,walimaliza ndipo jamaa(Jamal) alikuja akaingia dukani kisha wakawa wanaongea na Kileri kama mwanzo.

Jamal " Sasa nadhani Poti hesabu zetu tutazipiga mwezi ujao ili tujue tunafanyaje katika gawio,au unasemaje?"

Kileri "Mi nakuamini sana Jamal hapo hakuna tatizo"

Aliendelea "Basi sawa mi naondoka"

Baada ya mazungumzo yale mafupi Kileri aliniambia tuondoke zetu,sasa tukiwa njiani Jamaa alikuwa akinieleza mambo mengi ambayo sikuyaelewa na mimi niliamua kunyamaza ili niuone mwisho wake utakavyokuwa kwasababu wahenga wanasemaga "Njia ya muongo ni fupi".
Kileri "Wa kwetu lile duka ndipo nimeweka mtaji wako na wangu,hivyo hao jamaa mara nyingi ndio ninaofanya nao biashara na niwatu wema sana"

Mimi "Kama ndivyo haina shida"

Mimi "Kwahiyo faida tunagawanaje?"

Kileri "Faida tunaigawana kulingana na mtaji,kama ambavyo duka unaliona lilivyokubwa na bado kuna stock nyingine iko stoo,hivyo kila mtu huwa anapata chake kulingana na mtaji"

Aliendelea "Mimi sikutaka kuwaambia ya kwamba nipo na mdogo wangu ila pesa niliyowapa waiweke kwenye mtaji wao wanafahamu kama niya kwangu,hivyo tukigawana faida sisi ndiyo tutakuwa tunagawanya faida yetu tunagawana"

Mimi "Kama ndivyo ni jambo jema"

Kileri "Pia mwanzo nilikuwaga nachukua vyombo kwa mkopo natembeza barabarani na majumbani lakini baada ya kupata mtaji niliona niongee na jamaa wakakubali na ndiyo maana wakati tunaongea nilikushauri uje huku tuifanye hii biashara kwasababu ina faida sana"

Hatimaye tulipanda gari tukawa tumeondoka kurudi nyumbani,muda huo mimi nilikuwa naendelea kushangaa pilika pilika za watu katika jiji la Dar es salaam.

Tulivyofika nyumbani kwa jamaa,yeye alitoka akawa ameelekea kusiko julikana mimi nikabaki pale nyumbani huku nikiendelea kutazama mazingira ya hapo nyumbani,mafundi siku hiyo hawakuja kuendelea na ujenzi lakini walikuwa wamemaliza kiweka vigae vyumba viwili.

Mke wa Kileri "Shem ingia ndani tule"

Mke wa jamaa baada ya kuivisha chakula cha mchana akawa amenikaribisha ndani.

Mke wa Kileri "Baba Nyangi ameenda wapi?"

Mimi "Tumefika wote lakini naona sijui atakuwa ametoka!"

Mke wa Kileri "Hawezi kuona kuna mgeni akatuliza miguu"

Mimi "Ngoja nimpigie simu uenda atakuwa jirani"

Mimi "Ndugu pande zipi?,msosi tayari huku"

Kileri "Nyie kuleni wa kwetu nimetoka kidogo ila sichelewi kurudi"

Mimi "Sawa kaka"

Basi sie tuliendelea kula chakula kama kawaida.Ilipofika usiku mida ya saa 2 jamaa bado alikuwa hajatokea,nakumbuka baada ya kumaliza kula niliingia chumbani kutulia kwasababu ile nyumba hakukuwa na umeme hivyo walikuwa wanatumia taa ya mafuta au siku nyingine mshumaa,sasa sikutaka kukaa sana sebuleni kwasababu hakukuwa na cha maana zaidi ya kushangaa kenchi.

Sasa nikiwa nimepitiwa na usingizi,niliamshwa ghafla na kelele za mtu akiita kwa nguvu.Nilipoangalia saa ilikuwa mida ya saa 5 usiku.Nilipoendelea kusikiliza kwa makini kumbe ilikuwa ni sauti ya Kileri,sasa kumbe jamaa alikuwa amelewa chakari na alikuwa akimuita mkewe amfungulie.

Kileri "Wewe mama Nyangi "

Aliendelea "Mama Nyangi fungua mlango"

Baada ya mkewe kuwa kimya,jamaa alikuwa akifyonza huku akiendelea kugonga geti kwa nguvu,sikufahamu kama mkewe ni kweli alikuwa hasikii au aliamua tu kujikausha.Ilibidi niamke nitoke kwenda kumfungulia jamaa geti kwasababu ilikuwa usiku.

Mimi "Kaka nadhani shemeji atakuwa amepitiwa na usingizi"
Kileri "Wakwetu ngoja niingie kulala tutaonana asubuhi"

Jamaa alikuwa amelewa sana na hata kutembea vizuri akawa anashindwa.Sasa baada ya kuingia chumbani ile nimenilaza kidogo nikaanza kusikia anamfokea mkewe akitishia kumpiga,mkewe nae hakuwa mnyonge kwani alikuwa akimjibu kwa hasira na namna ambavyo nilielewa ni kwamba,jamaa tabia ya ulevi ilikuwa ni kawaida yake na yule mwanamke alionekana kumchoka kwasababu hakuwa na msaada wowote.Baada ya muda ulipita ukimya na nilifahamu jamaa atakuwa alilala fofofo.

Asubuhi nilipoamka sikumuona jamaa na baada ya kumuuliza mkewe akawa ameniambia aliwahi kuamka saa 12 asubuhi akaondoka.Sasa niliamua kuchukua jembe nikaenda kumsaidia mkewe ambaye alikuwa anapalilia bustani aliyokuwa amelima bamia pamoja na matemebele sasa tukiwa pale bustanini,mkewe akawa ananiambia kuhusu tabia za jamaa na aliamua kuniambia nikiwa kama mdogo wake na ndugu yake wa karibu ikiwezekana nimshauri jamaa.

Mke wa Kileri "Shemeji usingeamka ungeacha alale nje,mimi unadhani naamkaga usiku?"

Aliendelea "Tena nadhani alirudi kwa ajili yako,mara zote akijua amelewa huwa harudi kwasababu anajua hata akirudi nani wa kumfungulia geti?,kuna siku amerudi sikumfungulia alilala nje ndipo akaanza tabia akienda huko kulewa harudi hadi kesho yake"

Mimi "Aisee mbona ni hatari"

Mke wa kileri "We acha tu shemeji napitia mambo magumu sana kama mwanamke"

Mimi "Mbona Kileri hakuwaga na hizi tabia?"

Mke wa Kileri "Wewe kileri umeanza kumjua tangu lini unasema hizo tabia alikuwa hana?"

Mimi "Kileri nimekaa sana kwao maana ni kwa baba yangu mkubwa hivyo ninamfahamu vema na hakuwaga na tabia hizi za ulevi"

Mimi "Labda alipokuja Dar ndipo amenza hizi tabia"

Mke wa Kileri "Ndugu yako amenikuta Nauza dagaa kutoka Mwanza na nilikuwa na mtaji mkubwa tu,nilipoingia na Kileri kwenye mahusiano nikajua ni mwanaume nimepata kumbe nilikuwa najidanganya"

Aliendelea "Nilikuwa nampatia hela nikijua mwenzangu anaongezea mtaji kwenye biashara kumbe pesa yote niliyokuwa nikimpatia yeye alikuwa akiipeleka kwa malaya zake"

Mke wa kileri "Nilipokuja kugundua shem nakwambia ilikuwa ugomvi mkubwa sana,baadae aliniomba msamaha ikabidi nimsamehe tuendelee kuishi ila sikumpatia hela yangu tena"

Aliendelea "Hii nyumba unayoiona niliijenga na kuisimamia mimi kwa pesa yangu ya niliyokuwa naipata kwenye biashara ya dagaa,japo kiwanja ni cha kwake lakini naamini nisingejenga angekuwa amekwisha kiuza"

Baada ya maelezo ya mkewe kidogo nikabaki kushangaa kwasababu mimi niliamini ile nyumba itakuwa imejengwa na ndugu yangu kumbe haikuwa kama nilivyodhani,yule mwanamke alikuwa ni mzuri japo ilionekana kabisa maisha mabaya naya umasikini ndiyo yalikuwa yakimchosha.

Mke wa Kileri " Tangia mwezi uliopita naona analeta mafundi wanakarabati humo ndani kwa kuweka vigae na hata kile choo anekijenga upya maana cha kwanza kilikuwa cha mabati"

Aliendelea "Mimi hata simuulizi shem maana niliyofanya yanatosha,na yeye sasa ni zamu yake"

Mimi "Kwani Kaka yeye ukiacha biashara ya vyombo huwa anafanya kazi nyingine"

Mke wa Kileri "Biashara ya vyombo?,ndiyo alikwambia anafanya biashara ya vyombo?"

Mimi "Ndiyo,hivyo ndivyo ninavyofahamu"

Mke wa Kileri "Biashara ya vyombo alikuwa anaifanya hata kabla hatujaishi wote,kupitia biashara hiyo ya vyombo ndipo mimi na yeye tulikutana kwasababu alikuwa anapenda sana kunipitishia vyombo kwenye banda langu"

Aliendelea "Kwa namna alivyokuwa mpole na mnyenyekevu nikajua mwanaume ndiyo huyu"

Mimi "Kwahiyo auzi tena vyombo?"

Mke wa Kileri "Biashara ya vyombo kidogo impeleke jela shem,kuna vyombo sijui alikuwaga anakopa kwa tajiri sasa kumbe alikuwa anauza na hela hapeleki hivyo mwenye vyombo vyake akataka kumfunga ndipo ikabidi nichukue hela yangu nikampatia alipe hela ya watu na wakati huo ndiyo tulikuwa wapenzi"

Baada ya maelezo ya mke wa kileri kiukweli moyo wangu uliuma sana kwasababu niliamini hela yangu jamaa atakuwa ameila!.

Mke wa kileri "Angekuwa anafanya kazi kila siku tushindie matembele?"

Aliendelea "Binti yake tu hata viatu vya shule saa nyingine ni mtihani,hadi niwapigie simu ndugu zangu nianze kuomba omba"

Mimi "Mimi nilijua anafanya biashara ya uuzaji wa vyombo na hata kuja Dar nimekuja kwa shughuli hiyo!"

Mke wa Kileri "Kama alikwambia hivyo alikudanganya"

Mimi "Jana tulienda Tandika kwenye duka moja la vyombo akadai hela niliyompatia ameiweka hapo pamoja naya kwake ili kuongeza mtaji na faida ikipatikana tutakuwa tunagawana na wale jamaa"

Mke wa kileri "Ulimpatia shi ngapi shem?"

Mimi "Nilimpatia milioni 9"

Mke wa kileri "Mungu wangu!, unasemaaa!"

Mke wa Kileri alipata mshangao baada ya kusikia nimempatia mume wake pesa nyingi kiasi hicho!.

Mke wa Kileri "Mbona mimi sijamuona na hela?"

Aliendelea "Hiyo hela shemeji andika maumivu,hiyo atakuwa amepelekewa hawara yake"

Mke wa Kileri " Ndiyo maana naona anajitutumua kuweka vigae ndani nikawa najiuliza huyu katoa wapi hela"

Aliendelea "Mwanaume hana chochote cha maana anachofanya na watu walishamfahamu hawampi hata kazi kwasababu ya ujuaji wa mjini(utapeli)"

Kiukweli niliumia moyo sana na nilimwambia mkewe akae kimya asimwambie chochote lakini mkewe akuvumilia ile hali akaamua siku hiyo hiyo kumtwangia simu,jamaa alipojua mkewe amefahamu hakuwahi tena kurudi nyumbani kwa takribani wiki mbili.

Kwakuwa sikuwa na kazi ilibidi niingie mtaani kuanza kusaka kazi ya kufanya ili kujipatia kipato.



............................................................................................





Utajiri wa rafiki yangu ulivyofanya nikamuamini Shetani - 06.


Fedha niliyokuwa nimeitafuta kwa jasho na damu na baada ya kuuza mali za duka letu la vipodozi tukawa tumegawana na rafiki yangu kipenzi ikawa imeishia mikononi mwa ndugu yangu ambaye niliamini tungefanya biashara ikashamiri kama alivyokuwa akiniambia lakini haikuwa kama nilivyodhani!.Nilipanga niendelee kuwa subira uenda mwisho wa mwezi angeenda kwa wale jamaa pale Tandika akapewa faida ya pesa aliyokuwa ameweka hapo dukani kama alivyoniambia,niliamua kuupa muda nafasi ingawa Jamaa baada ya kupewa taarifa na mkewe kuhusu hizo hela alikata mawasiliano kabisa kwa takribani wiki mbili.

Sikutaka kabisa kukaa kizembe pale kwa Kileri,niliamua kuzunguka kutafuta kazi ya kufanya angalau nianze kutengeneza pesa,sasa niliamua kutembea mdogo mdogo kama naelekea Banana na kuna mahali nilifika nikakuta jamaa wanafyatua tofali za blocks,eneo lile halikuwa mbali na nyumbani kwa kileri,ilikuwa takribani mita kama 1000 hivi,nilijisogeza mpaka pale nikawa nimeongea na jamaa mmoja ambaye ndiye alionekana kuwa kiongozi wa ule mradi.

Mimi "Kaka kwema"

Jamaa "Kwema,vipi hali"

Mimi "Safi kaka"

Mimi "Naweza kupata angalau kibarua kaka?"

Jamaa "Kibarua kama kipi unaweza!"

Mimi "Chochote tu kaka"

Jamaa "Unao uzoefu wa kufyatua tofali?"

Mimi "Hapana kaka ila kubeba na kupanga naweza"

Jamaa "Unaitwa nani?

Mimi "Naitwa Umughaka"

Jamaa "Ok sawa"

Aliendelea "Sudiiiiiii !"

Jamaa "Sudi eeeh !"

Sudi "Nambie "

Jamaa "Njoo mwanangu"

Sudi "Nambie "

Jamaa "Jamaa anahitaji kibarua,vp kuna sehemu umchomeke?"

Sudi "Hapa nafasi haziishagi ni nguvu zake tu"

Jamaa "Sawa muangalizieni"

Sudi "Mbona kama umependeza,unataka leo leo au ulikuja kucheki kwanza"

Mimi "Kaka nipo tayari kwa kazi"

Sudi " Hizo nguo huzipendi au!"

Mimi "Nitavua nitabaki na bukta"

Sudi "Sawa,twenzetu"

Baada ya maongezi ya muda mfupi,jamaa aliyeitwa Sudi alinichukia mpaka eneo la kazi kisha nikavua nguo zangu nikawa nimebaki na bukta(boksa),sasa Sudi akawa ameniambia nitakuwa nachukua tofali zitakazokuwa zinafyatuliwa na mashine na kisha kwenda kuzipanga kwenye eneo la wazi lililokuwa limetengwa kwa kazi hiyo.

Niliifanya ile kazi kuanzia muda ule hadj jioni mida ya saa 12,kiukweli haikuwa kazi ya kitoto hata kidogo,kwakuwa niloshafanya kazi nzito na ngumu kuliko ile,sikuona tatizo lolote japo jamaa waliponiangalia walidhani mimi ni lele mama lakini nilipoanza kupiga mzigo hawakuamini!.Eneo lile kulikuwa na kinyumba kidogo na kwa nyuma kulikuwa kumejengwa choo pamoja na bafu,hivyo baada ya kumaliza kazi nikawa nimeingia kuoga,nilipomaliza kuoga,yule jamaa ambaye nilienda kumuomba kazi aliinita akanipatia elfu 3 ambayo ni kama posho ya kibarua.Ilikuwa ni hela ndogo sana lakini sikukata tamaa kwakuwa kwa wakati huo sikuwa na kazi yoyote!.

Baada ya malipo niliondoka zangu kwa kutembea kurudi kwa Kikeri ambapo ndipo nilipokuwa nimefikia.

Niliendelea kuifanya ile kazi kwa siku kadhaa,sasa ilikuwa kwamba mteja amiweka oda ya tofali tunapakia na kwenda kushusha tulikuwa tunapewa posho ya upakiaji na ushushaji elfu 2 kila mmoja,hivyo ukijumlisha na ile posho ya ufyatuaji na ubebaji kwenda kuanika ambayo ilikuwa buku 3,kwa siku nilikuwa napata zaidi ya elfu 10,kwasababu kwenye upakiaji na ushushaji kwa siku tulikuwa tunapata oda hata za wateja 3 hadi 4 kwa siku.

Kuna siku nilipomaliza kazi nimerudi nyumbani pale kwa ndugu yangu Kileri nikamkuta yupo,sasa sikutaka kuzungumza nae pale ndanj ilibidi nimwambie shemu tunatoka kidogo.Dhumuni la mimi kumtoa pale nyumbani nilitaka anieleze ukweli kuhusu ile hela kwasababu ilikuwa ni mwezi umekatika na hakukuwa na mrejesho wowote kuhusu faida kama alivyokuwa ameniambia.

Mimi "Ndugu yangu hujanipa mrejesho wowote kuhusu biashara"

Kileri "Kaka wewe acha tu"

Aliendelea "Kiukweli kaka niwe mkweli,wewe ni ndugu yangu sitaki kukuficha"

Kileri "Ile hela ulinipa nilienda kulipa deni nililokuwa nadaiwa na yule jamaa(Jamal) na kuna kiasi cha fedha niliona nijengee choo kilichokuwa cha mabati"

Aliendelea "Juzi kabla hujaja mama yake mke wangu alisema anakuja sasa nikaona nitengeneze angalau vyumba viwili niweke vigae ili kuwe na muonekano kaka"

Mimi "Kaka ni heri ungeniambia tangu mapema nikiwa Tarime kwamba unashida na hela ningekutumia kwakuwa wewe ni ndugu yangu"

Mimi "Lakini kitendo cha kufanya mimi kuja huku nikiamini tunakuja kufanya biashara wakati ni uongo,umenikosea sana ndugu yangu"

Kileri "Nitampigia Marwa nyumbani nimwambie aniuzie vile vi ndama vyangu halafu nitakulipa,wewe ni ndugu yangu"

Mimi "Wewe acha tu,kama ipo ipo tu kaka!"

Mimi "Wala usijali kuhusu hiyo hela"

Kiukweli nilijisikia hasira sana na nilijiona ni mpumbavu sana kumpatia Kileri ile hela ambayo haikufanya jambo la maana zaidi iliishia kwa wanawake zake na utumbuaji wa starehe,sikukata tamaa niliamini kama niliweza kuipata hiyo hela basi nitaweza kuipata nyingine.Japo alijitahidi kunieleza maneno mengi lakini bado nilimuona ni muongo kwasababu mkewe alikuwa ameniambia kila kitu.

Niliendelea kupambana katika ile kazi ya tofali pasipo kukata tamaa,nilikuwa natafuta hela angalau nikapange chumba changu ili niweze kujisogeza zaidi.Kuna siku nikiwa na jamaa zangu kwenye gari tukiwa tunapeleka tofali kwa mteja,kuna jamaa mmoja nae alikuwa mfanyakazi mwenzangu hapo site alikuwa akituambia kama vipi twende kwenye mradi wa nyumba huko kigamboni uliokuwa ukifahamika kama DEGE.

Mwakisaka " Mwanangu kama mko tayari kesho tuibuke Dege kuna jamaa zangu wako kule wanasema kuna hela nzuri"

Mimi "Dege ndo wapi?"

Mwakisaka "Kigamboni huko kuna nyumba zinajengwa kama utitiri!"

Aliendelea "Halafu kule vibarua kwa siku waliniambia wanakula elfu 15"

Zomela "Tatizo kigamboni ni mbali,hiyo hela inaishia tu kwenye nauli"

Mwakisaka "Sasa hiyo nauli kwani unaenda wapi?,watu huko wamepiga kambi halafu wewe unaongelea masuala ya nauli tena"

Aliendelea "Mimi kesho ngoja niende nikacheki"

Zomela "Tatizo huko unaweza kwenda ukakosa na ukirudi huku nako unakuta wameweka mtu mwingine,tena nianze kufanya kazi kutafuta kazi"

Mwakisaka "Kwani utasema unaenda wapi?,kule tunaenda kimya hivyo si rahisi mtu kujua,tukipata ndo hivyo tusipota tunarudi"

Zomela "Hao jamaa zako wanauhakika?,siyo tunachoma nauli tu!"

Mwakisaka "Aliye tayari kesho twende tukikosa tunarudi"

Baada ya yale mazungumzo nilimwambia Mwakisaka mimi nitakuwa tayari kuungana nae na kuelekea huko Kigamboni kusaka kibarua cha elfu 15.

Mimi "Kwahiyo tutakutana wapi?"

Mwakisaka "Kwani siunasimu?"

Mimi "Ndiyo"

Mwakisaka "Nigei namba yako asubuhi nitakushitua"

Nilimpatia namba yangu ya simu Mwakisaka kisha tukaendelea na mambo mengine.

Ilipofika alfajiri mida ya saa 11,Mwakisaka alinipigia simu na akawa ameniambia tuonane pale Banana na nikifika nimwambie,kweli nilianza kuhangaika na usafiri wa kunitoa huko kivule ambao ulikuwa wa changamoto sana,nilihangaika kupambania usafiri hadi saa 12 asubuhi ikanikuta bado sijapata gari,nilikuja kupata gari imejaa ikabidi nining'inie hivyo hivyo kibishi ilimradi nifike.Nilipofika pale Banana nilimpigia Mwakisaka ambaye yeye alikuwa amefika kitambo akinisubiri mimi!.

Mwakisaka "Shwari?"

Mimi "Shwari kaka"

Mimi "Zomela yuko wapi?"

Mwakisaka "Yule hawezi kwenda,ameshapazoea pale kwa Mushi kama kwao"

Aliendelea "Hapa itabidi tupande magari ya kivukoni"

Tulikaa pale stendi tukawa tunasubiri magari ya kivukoni yaliyokuwa yanatokea Gongo la mboto ili tupande tuondoke,gari nyingi zikawa zinapita zimeshona watu kama utitiri,kiukweli nilikuwa nashangaa sana ile hali kwakuwa hata Mwanza sikuwahi kuona gari zinajaa kiasi kile!.

Baada ya muda kupita kuna gari ambalo lilikuja likiwa angalau na nafasi ya kusimama na tukapanda hilo.



...........................................................................................



Utajiri wa rafiki yangu ulivyofanya nikamuamini Shetani - 07.


Kwakuwa Mwakisaka ndiye aliyekuwa mwenyeji wangu sikuwa na hofu kabisa kwasababu ni mtu ambaye tulifanya nae kazi kwa muda mfupi na alikiwa mtu mwema,baada ya kufika kivukoni(feri)tulikata tiketi za kivuko na tukawa tumefanikiwa kuvuka ng'ambo ya pili,baada ya kufika upande wa pili yaani Kigambo,jamaa aliniambia inapaswa tupande gari zilizokuwa zinaelekea Kibada kwa kuwa ndiyo njia yenyewe hiyo.

Tulifanikiwa kufika hapo kwenye mradi mkubwa kabisa uliofahamika kama DEGE ECO VILLAGE,kiukweli nilikuwa nashangaa sana namna ambavyo watu wanatumia fedha,ule mradi ndugu zangu ulikuwa mkubwa mno,na kwa waliobahatika kufika huko au wanaotokea huko watakubaliana nami.

Hatukutaka kupoteza muda kabisa ilibidi Mwakisaka aniambie tuulizie namna ya kupata kibarua kwasababu tulikuta watu wakiwa wanachakalika kinoma.Kuna jamaa tulimfuata tukaanza kumuulizia namna ya kupata kibarua siku hiyo.

Jamaa "Hapa kwetu yupo foreman ambaye ndiye msimamizi wetu,ukienda kule mbele pia wanae foreman wao"

Mwakisaka "Foreman wenu yuko wapi tujaribu kuongea nae?"

Jamaa "Nadhani atakuwa anazungukia maeneo anayosimamia,subirini tu hapa atakuja"

Tulisogea kando tukawa tunaendelea kuushangaa ule mradi wakati huo tunamsubiri mtu tuliyeambiwa ndiye foreman wa hapo tulipofikia.Baada ya muda wa nusu saa jamaa mmoja mweusi aliyekuwa mnene na kitambi cha kutosha akawa amekuja na ndipo yule jamaa alitukonyeza ya kwamba jamaa ndiye foreman wa lile eneo.Tulimfuata na kumjulia hali jamaa kisha Mwakisaka akaanzisha maongezi nae.

Mwakisaka "Kaka tunatafuta kazi ya kibarua "

Foreman "Aliyewaambia hapa tunaajili vibarua nani?"

Mwakisaka "Hakuna mtu aliyetuambia kaka tumekuja kuona kama tutapata"

Foreman "Hapa hatuajiri kwa sasa,siku tukiajiri vibarua mtapata taarifa"

Baada ya yale majibu ya kukatisha tamaa Mwakisaka aliamua akae kimya kisha jamaa akaanza kuondoka kuzunguka nyuma ya yale majengo yaliyokuwa mbele yetu.Sasa yule jamaa aliyekuwa kibarua pale akawa amemuita Mwakisaka akamwambia bila pesa ni ngumu sana kupata kibarua kwasababu hata wao walihonga ndipo kupata kibarua,jamaa akasema twende tukaongee nae kikubwa.Nilimwambia Mwakisaka hiyo kazi ya kuongea na jamaa aniachie mimi,akikataa basi tungerudi zetu kwa Mushi kule kivule kuendelea na ufyatuaji wa tofali.

Niliamua kuzunguka ule upande alokuwa amekwenda yule foreman na bahati nzuri nilimuona akiwa anaingia kwenye jengo moja,nilitembea kwa haraka ili kumuwahi kabla hajafika kwa watu wengi ikawa shida kuzungumza nae.

Mimi "Kaka kakaa"

Foreman "mmmh nambie"

Mimi "Kaka tusaidie ndugu yangu na kama ni chochote tutakupatia"

Foreman "Wewe si ndo upo na yule mwenzio nimewaambia hamna kazi!"

Mimi "Kaka tusaidie ndugu yangu!"

Foreman "Nyie mnatokea wapi?"

Mimi "Wote tunatokea kivule"

Foreman "Kivule?,sasa kivule hadi kuja kufanya kazi huku hamuoni tutasumbuana?"

Aliendelea "Ni bora hata mngekuwa hapa maeneo ya jirani"

Mimi "Tutaweka kambi maeneo haya kaka wala hilo lisikupe taabu"

Foreman "Hapa jirani haturuhusu watu kukaa kwasababu za kiusalama"

Mimi "Sijamaanisha hapa kwenye mradi kaka,tuta tafuta eneo maeneo ya jirani tutaweka kambi"

Foreman "Tukubaliane,mtanipa elfu tano tano kila siku kwa muda wa wiki moja"

Aliendelea "Na iwe siri,ikiwa vinginevyo mi nitawaruka na kuwageuka"

Mimi "Hakuna tazizo kaka"

Foreman "Kamuite mwenzio mje niwakabidhi huku juu!"

Niliondoka kumfuata Mwakisaka na kumueleza kila kitu jamaa alichosema na jamaa akaniambia hakuna tatizo;Tuliondoka kumfuata yule foreman ambaye alituchukua mpaka kwa jamaa wengine akamuacha hapo Mwakisaka kisha akaniambia tena nifuatane nae,mimi pia akawa amenipeleka kwenye kikosi kingine.
Tukaanza kuifanya kazi ya kibarua rasmi na kwa siku tukawa tunapewa elfu 15,ishu ya kula pamoja na maji ya kunywa ilikuwa ni juu ya yako wewe kibarua uzuri ni kwamba,kwenye kundi ambalo mimi nilikuwepo walikuwa wamejitolea kuchanga fedha na kununua vyakula kisha kuna mtu walikuwa wanamlipa anakuja kuwapikia,hivyo na mimi baada ya kuingia kwenye kundi la wale jamaa niliamua kuchangia elfu 10 kwa kila wiki kwa ajili ya huo mpango.

Miongoni mwa wale jamaa pia walikuwa wametengeneza matenti ya maturubai kuishi hapo maeneo ya jirani,niliamua kichangia fedha na mimi ili kukaa hapo,sasa bahati nzuri ni kwamba wikiendi tulikuwaga tunapumzika na hiyo niliitumia kwenda kufata virago vyangu kwa kaka Kileri na kurudi kambini,sikutaka kabisa kuhangaika na mambo ya jiji la Dar es salaam,fokasi yangu ilikuwa ni kwenye kufanya kazi na kutunza malipo yangu kwenye simu.

Nilipopambana ndani ya miezi mitano kwenye ule mradi nilipata kiasi kisichopungua Tsh milioni 1.3,sasa nilimuomba Mwakisaka aniambie ni eneo gani ni zuri kwa kupanga chumba na angalau linakuwa na maisha nafuu kwa hapa Dar es salaam.

Mwakisaka "Mwanangu mimi nakaa Gongo la mboto na nikuzuri sana"

Mimi "Kwahiyo kipindi kile ulikuwa unatoka Gongo la Mboto mpaka Kwa Mushi?"

Mwakisaka " Nilikuwa nakaa kulekule kivule kwa ndugu yangu mmoja"

Aliendelea "Kama unataka chumba we sema nimpigie simu jamaa mmoja pale kitaa akutafutie chumba"

Mimi "Nahitaji kaka"

Mwakisaka "Basi ngoja nitamcheki mshikaji"

Kweli,baada ya Mwakisaka kuwasiliana na jamaa yake na kumjulisha nilikuwa nahitaji chumba jamaa alianza kutafuta na akasema endapo angepata basi angetujulisha.
Baada ya siku tatu yule jamaa aliyepewa kazi na Mwakisaka ya kutafuta chumba akawa amesema nyumba imepatikana maeneo ya mwisho wa lami lakini ni vyumba viwili ambavyo malipo ilikuwa ni elfu 45 kwa kila chumba na ilipaswa kulipwa kwa miezi 6.

Mwakisaka "Jamaa anasema nyumba imepatikana Gongo la mboto mwisho wa lami"

Mimi "Mwisho wa lami ni maeneo ya wapi?"

Mwakisaka "Hapo hapo Gongo la mboto sema ni mbele kidogo"

Mimi "Sawa,na wewe ndiyo unaishi huko?"

Mwakisaka "Hapana,mimi naishi Mzambarauni"

Mwakisaka "Ila jamaa anasema amepata chumba na sebule kwa elfu 45 kwa kila kimoja na inalipwa miezi 6,vp?"

Mimi "Sawa,hakuna tazizo"

Mwakisaka "Ngoja nimwambie amwambie mwenye nyumba atulie kesho kutwa tukakicheki"

Mwakisaka aliwasiliana na yule jamaa akawa amemwambia amwambie mwenye nyumba jumapili tungeenda kukitazama ikiwezekana nilipie kabisa.

Namshukuru Mungu baada ya kwenda kuingalia ile nyumba niliipenda na nikawa nimelipia miezi sita,hela iliyobaki nikanunua godoro na mashuka nikawa nimeyaweka na mimi kufunga chumba kisha kurudi Kigamboni kuendelea na kibarua.

Kila nilipokuwa ninapata hela nilikuwa nikinunua kitu kimoja baada ya kingine na kuweka ndani na hatimaye vyumba vikawa na muonekano mzuri,kiukweli pamoja na mateso ya kushinda juani niliyokuwa nayapitia kule kigamboni lakini nilihakikisha najinyima kiasi kwamba hadi malengo yangu yatimie.

Ule mradi wa Dege kuna muda ukawa umesimama kidogo hivyo kwa muda ule nikaenda kukaa kwangu nilikokuwa nimepanga,sasa pale nilipokuwa naishi kulikuwa na geti na tulikuwa wapangaji kadhaa na kila mtu alikuwa na ishu zake.

Sasa kuna jamaa mmoja alikuwa akiitwa Steve yeye tulitokea kushibana sana na tukawa marafiki,jamaa alikuwa akifanya kazi kampuni ya Tigo kama msajili line za simu,kwakuwa ule mradi ulikuwa umesimama kwa muda usiojulikana,jamaa aliniambia kama vipi aniunganishe na timu leader wake anipatie kodi ya kusajili line za simu nami nianze kuwa msajili laini.Jamaa aliniambia ni kazi ambayo ilikuwa na pesa sana ila watu walikuwa wakiichukulia poa.

Steve "Ngoja kesho nitamueleza team leader kama vipi akupe kodi ili uanze kufanya kazi"

Mimi "Kazi inafanyikaje kaka"

Steve "Kazi ni nyepesi sana kaka utaelekezwa namna ya kuifanya"

Kwakuwa kwa muda huo sikuwa na kazi baada ya kusimama kwa mradi,niliona jamaa atakuwa amenisaidia sana ili kuweza kujinasua na ukata ambao ulikuwa ukininyemelea baada kuwa nakula hela nilizokuwa nimezitunza bila kuzizalisha.


............................................................................................



Utajiri wa rafiki yangu ulivyofanya nikamuamini Shetani - 08.


Baada ya siku mbili,yule jamaa aliyekuwa mpangaji mwenzangu aliyeitwa Steve alinifuata akawa ameniambia Team leader amekubali.

Steve "Kaka jiandae kesho nikupeleke maana nilizungumza na team leader akaniambia twende"

Mimi "Sawa kaka"

Kweli,tuliondoka na Steve hadi Buguruni kulikokuwa na ofisi ya Tigo,nilipofika hapo nilikuta kuna vijana wengi wakiwa mchanganyiko(KE & ME) na kiukweli kulikuwa na mabinti wazuri sana,Steve aliniambia nifuatane nae hadi ndani na tulipofika ndani alimuita huyo aliyekuwa Team leader akaja nilipokuwa nimesimama.

Steve "Kiongozi huyu mshikaji ndiye nilikwambia ile juzi anahitaji Code"

Team leader " Aahh ok!"

Aliendelea "Hebu nisubirini kidogo nina mazungumzo nakuja!"

Team leader aliondoka akawa ametuacha pale na Steve,Steve nae akawa yuko bize kupiga stori na washikaji zake wengine ambao pia walikuwa wakifanya kazi ya usajili wa line.Baada ya dakika 20 yule Team leader akawa amerudi.

Team leader "Unaitwa nani ndugu?"
Mimi "Naitwa Umughaka"

Team leader "Kanda ya ziwa nini!"

Mimi "Yeah"

Team leader "Ok,sasa nitakupa line ya Code kwa ajili ya kusajilia,na process zote inabidi ukamilishe muda huu ili uondoke na Steven akakuonyeshe kazi inavyofanyika"

Aliendelea "The more u register customers,the more u get more money"

Team leader "Kwa kanuni za sasa kwenye kampuni ni kwamba,kila freelancer atakuwa anapokea Revenue shares every month within six months"

Aliendelea "Mambo mengine yote Steven atakuelekeza"

Team leader "Steve hakikisha jamaa anakuwa poa"

Steve "Hakuna tatizo kiongozi"

Baada ya ufafanuzi mdogo ambao sikuelewa chochote,Team leader aliingia ndani akawa ametoka na tisheti mbili za Tigo zikiwa mpya zenye maandishi yaliyosomeka "Sajili line yako Tigo hapa",pia aliniletea Kofia, na kizibao,hivi vyote vilikuwa na maandishi yaliyohusu kampuni ya mawasiliano ya Tigo.

Team leader "Ukishaelewa tunavyofanya kazi,wiki ijayo nitakupatia Mwamvuli na meza ili uwe na chimbo lako,au unataka kupiga door to door?"

Mimi "Door to door ndo kitu gani?"

Team leader "Naamanisha uwe unasajili laini kwa kutembea tembea?"

Mimi "Nadhani nipe muda nitakujuza njia ipi kwangu itakuwa bora zaidi!"

Team leader "Ok,hakikisha kila siku asubuhi hukosi hapa ofisini kuanzia saa 1 : 30 uwe hapa maana kila siku kuna kuwa na vikao vya maelekezo"

Mimi "sawa,hakuna tatizo"

Baada ya maelekezo hayo,Team leader alimpatia Steve boksi mpya la laini za simu ambazo hazijasajiliwa na kumtaka anielekeze namna ya kusajili wateja.Tuliondoka na Steve kuelekea Tandika ambako yeye alikuwa akifanyia Shughuli zake huko za kusajili line,sasa tulipofika hapo Tandika jamaa alikuwa na tenti lake kubwa (Gazebo) ambalo lilikuwa la kampuni ya Tigo,tulipofika hapo kuna demu tulimkuta ambaye alikuwa na wateja,yule demu alikuwa akishirikiana na Steve kwenye lile tenti kusajili line.

Wateja walivyokuwa wakija nilikuwa nikielekezwa namna ya kusajili line za simu na kiukweli nilielewa ile kazi kwa muda mfupi sana na nikawa nafanya vizuri sana kuwashinda hata niliowakuta mwanzo.Nifahamu hadi kurudisha line za simu zilipotea na nilifahamu mambo mengi sana na nikawa mnyama sana kwenye ile kazi ya usajili wa line.

Baada ya mwezi kuisha na kupokea malipo,Steve alinishauri niongee na Team leader anipatie Meza na mwamvuli niweke kambi sehemu yenye watu wengi niendelee kupiga kazi.

Steve "Kaka kwakuwa umeshakuwa mzoefu,mwambie Kiongozi akupe mwamvuli na meza upige kazi"

Aliendelea "Au unataka kuparasa?"

Mimi "Kuparasa ndo kufanyaje?"

Steve"Kuparasa ni kupiga door to door,kuna wana wanaita kuparasa"

Mimi "Ni bora nitulie sehemu kaka,hili jua na ishu ya kutembea siyo poa"

Steve "Basi mwambie kiongozi akupe meza na mwamvuli au akupe Gazebo kabisa ila utakuwa unakatwa hela"

Niliona alichokuwa ananiambia Steve ni jambo jema kwasababu nisingeendelea tena kukaa pale kwenye Gazebo lao tukiendelea kugawana wateja.Siku iliyofuata baada ya kufika ofisini pale Buguruni,nilimwambia Team leader anipatie Mwamvuli na meza kama vipi niangalie chimbo ambalo litanifaa kupiga kazi.

Team leader "Sasa umepata chimbo la kuweka meza?"

Mimi "Nitatafuta kulekule Tandika kiongozi"

Team leader "Tandika watu wangu wamejaa sana,kwanini usiende kariakoo maana kule kuna watu wengi pia hii itakuongezea revenue maana kule watu wanahela za kuweka vocha"

Mimi "Ok sawa kiongozi ngoja niingie Kariakoo"

Baada ya kunipatia vitendea kazi(Mwamvuli na Meza) nilipanda gari pale Buguruni kuelekea Kariakoo kwa ajili ya kutafuta chimbo la kufanya kazi.Nilitafuta sana sehemu nitakayoweka meza ili nipige kazi,sasa niliingia mtaa wa Lindi lakini nikakuta kuna jamaa wengi tu wwameweka meza zao za usajili hapo na hivyo nikawa nimekosa eneo.

Nilitembea kuelekea mbele hadi nikawa nimeikamata barabara ya Kamata/Msimbazi road.Sasa kuna duka moja lilikuwa la vyombo vya electronic ambapo pembeni yake kulikuwa na duka dogo la simu,duka hilo ni miongoni mwa maduka ambayo leo yanakitazama kituo cha mwendokasi pale Gerezani,sasa pembeni yake nikaenda kuweka meza,kabla ya kuweka meza nikasogea mpaka kwenye lile duka nikakuta kuna mwanamke wa kiarabu aliyekuwa amejifunika vazi la Nikabu.

Mwanamke "Karibu"

Mimi "Ahsante"

Mimi "Aunt samahani,mimi nafanya kazi ya kusajili line kutoka Tigo,naomba niweke meza hapa pembeni"

Mwanamke "Mmmh hebu tuone"

Yule mwanamke alitoka dukani akawa amekuja nje kuchungulia kuangalia ni eneo lipi ambalo nilikuwa nahitaji kuweka meza na mwamvuli.

Mwanamke "Sawa,utasogeza kidogo pembeni ili usiwakinge wateja"

Mimi "Nashukuru sana Aunt"

Mwanamke "Usijali "

Nilifungua ile meza kutoka kwenye boksi pamoja na ule mwamvuli kisha nikawa nimesimama nasubuiri wateja,changamoto siku hiyo ilikuwa ni kiti,nilipanga kesho yake ningenunua kiti cha kukalia kwasababu pesa nilikuwa nimeacha nyumbani.Japo ilikuwa siku ya kwanza hapo Kariakoo lakini kazi ilifanyika sana na kumbuka nilisajili line 55 kwa siku hiyo moja!.

Maisha yalisonga na nikawa nishakuwa mzoefu sana wa ile kazi,sasa hapo jirani yangu kwenye lile duka la yule dada kulikuwa na huduma za miamala ya kifedha(TIGO,VODA,AIRTEL) ambapo nilipokuwa nikisajili line mteja akihitaji nimuweke pesa kwenye akaunti yake ya Tigo pesa,nilikuwa naingia tu kwenye lile duka!.Ile ilifanya nikazoeleka na taratibu nikawa najulikana.Kuna siku nyingine asipokuwepo yule dada basi utamkuta mumewe,hivyo wote kwa pamoja wakawa wamenizoea.

Niliifanya kazi ya kusajili line za simu kwa uaminifu mkubwa na kwa roho moja kana kwamba ile kampuni ilikuwa ya familia yangu,nilihakikisha naweka na kuhifadhi pesa ili nije nifanye mambo makubwa nilikuwa ninayawaza,nilikuwa nina uchungu sana baada ya Kileri kutafuna pesa yangu ya mtaji niliyokuwa nimempatia.

Sasa kuna siku nikiwa nimetoka kwenye mihangaiko yangu hiyo ya kusajili line nikiwa nimefika pale nyumbani nilikuta kuna zogo la Steve na demu wake.Niliingia zangu ndani kisha nikaingia bafuni kuoga ili nipike nile kisha nilale.Malumbano ya jamaa na demu wake yalikuwa makubwa mno kiasi kwamba jamaa akaja kunigongea mlango huku akilia.

Steve "Kaka njoo unisaidie kunibemebelezea shemeji yako kaka"

Nilimshangaa Steve namna alivyokuwa akitiririsha machozi kana kwamba amefiwa.

Mimi "Kuna nini?"

Steve "We njoo kaka"

Hicho kidemu cha jamaa kilikuwa ni kidemu fulani kilichokuwa kinambabaisha sana jamaa na sikuwahi kuelewa uenda jamaa atakuwa alirogwa kwasababu alikuwaga haambiliki kabisa kwa kile kidemu,nisiseme uongo,kidemu kilikuwa kizuri na kilikuwa na shepu isiyokuwa ya kawaida,sasa labda uenda Steve alichanganyikiwa na kile kishepu,kile kidemu kilikuwa kijitu cha Mtwara kwa mujibu wa Steve na walikutana kwenye pilika zetu hizo za usajili wa line.

Jina la huyo demu alikuwa akiitwa Zubeda ila Steve alikuwa akimuita Zuu.

Niliondoka na jamaa kuelekea hadi ndani kwake ambako kilikuwa chumba kimoja,nilipoingia ndani nilikuta kidemu kimelala kimeweka matako juu huku kinaendelea kuchezea kiswanswadu chake huku hakina habari kabisa na mtu!.

Mimi "Shem mambo vipi"

Zubeda "poa"

Sasa kilikuwa kinajibu huku kinaendelea kuchezea simu.

Mimi "Kuna nini shemeji yangu maana naona jamaa analia tu kama kichaa"

Zubeda "Ndo umwambie akueleze kinachomliza ni kitu gani!"

Muda huo wote naongea nae bado alikuwa bize akicheza na simu yake na akiwa hana habari kabisa.

Mimi "Shem muhurumie mwenzio yawezakana umemkosea"

Zubeda "Nimemkosea kitu gani bwana eeeh na wewe usitake kunichosha"

Aliendelea "Huyo kinachomliza ni wivu tu wakijinga"

Zubeda "Sikia,kuna mwanaume niliwahi kuwa nae kwenye uhusiano na alikuwa akinidai hela yake aliwahi kunipatia mtaji sasa tulipoachana akataka nimrudishie hela yake,ndiyo nikawa nimemuelekeza aje achukue hela yake"

Steve "Mtu mmeachana na bado mnawasiliana nae kila siku usiku anakupigia simu"

Zubeda "Sasa kwani kunipigia simu ndiyo kurudiana nae?"

Steve "Ungeenda sasa kumpatia huko siyo kumwambia aje hapa nyumbani kwangu"

Kwa maelezo ya Steve ni kwamba,huyo jamaa yake na hako kademu kake alikwenda hapo nyumbani kwa Steve wakati jamaa akiwa kazini kwake huko Tandika,ni nilikuka kufahamu ya kwamba kilichokuwa kinamliza Steve ni kuamini huyo demu wake atakuwa ametombewa ndani kwenye gheto lake kwasababu tabia za demu wake alizifahamu kabisa alikuwa hajatulia.

Yule demu alikuwa anambabaisha sana Steve kwa kufahamu alikuwa anampenda,na wewe fikiria pesa zote jamaa ambazo alikuwa akipata kama Kamisheni kwa kusajili laini alikuwa akikapa hako kademu.

Zubeda "Ndiyo maana nimekwambia ngoja niondoke,kwanini unafungia mlango?"

Mimi "Shem hebu yaacheni haya mambo bana"

Zubeda "Mimi unadhani basi nina tatizo shem,ni huyo mwenzio ndiyo ananifikiria vibaya"

Basi baada ya usuluhishi kutoka kwa msuluhishaji wa migogoro ya kimapenzi(Rejea kwa Ema na Deborah) niliyekuwa na uzoefu wa kutosha,niliamua kuondoka mle chumbani kwa jamaa ili wao wenyewe waendelee kupambana.

Kuna muda nilikuwa namshauri Steve aachane na yule demu lakini ni kama nilikuwa nampigia mbuzi gitaa,yule demu alikuwa na sifa mbaya kiasi kwamba kuna masela kadhaa pale mtaani tulipokuwa tunakaa nilikuwa nasikia wanapita nako na kila nikijaribu kumueleza jamaa anajifanya kama ameelewa lakini kumbe yanapitia huku yanatokea kule.

Sasa kuna siku nikiwa kariakoo napiga kazi,kuna dingi mmoja alikuwa na duka pembeni ya ile nyumba akawa amenipigia simu.



............................................................................................




Utajiri wa rafiki yangu ulivyofanya nikamuamini Shetani - 09.


Mwenye duka "Mambo vipi?"

Mimi "Shwari"

Mwenye duka "Jamaa yako anahama nini!"

Mimi "Nani?"

Mwenye duka "Jamaa yako na Mmakonde wake!"

Mimi "Steve?"

Mwenye duka "Eeh!"

Mimi "Wanahama lini?"

Mwenye duka "Naona wanapakia vitu kwenye Suzuki carry"

Mimi "Mbona hajaniambia!"

Mwenye duka "Nyie si marafiki!,ina maana rafiki yako anahama wewe hujui!"

Mimi "Labda wameona waondoke kimya kimya kaka"

Mwenye duka "Sawa bhana baadae"

Baada ya huyo mwenye duka kukata simu nilibaki kushangaa kwasababu zilikuwa ni sababu zipi zinafanya Steve ahame bila kunipa taarifa kama mshikaji wake wa karibu?,nilidhani uenda aliamua kuhama kwasababu alishachoka maneno mengi kuhusu huyo mkewe yaliyokuwa yakizungumzwa hapo mtaani,niliamua kumpigia simu ili kufahamu kilichokuwa kinaendelea na kwanini asiniage kama rafiki yake?

Nilipopiga simu yake ikawa inaita tu bila kupokelewa,nikapiga tena lakini ikawa haipokelewi,baada ya dakika 15 jamaa akanipigia yeye mwenyewe.

Steve "Kaka nilikuwa bize na mteja,nambie mwanangu"

Mimi "Uko Tandika?"

Steve "Yeah niko Tandika"

Mimi "Duuu mi nadhani uko maskani!"

Steve "Mapema yote hii kaka nyumbani nitafute nini?"

Mimi "Kwani pale nyumbani unahama?"

Steve "Nahama?,nahama naenda wapi?"

Mimi "Mbona nimepigiwa simu na mzee beda anasema mkeo anapakia vyombo kwe gari hivyo alidhani mnahama!"

Steve "Unasema?"

Mimi "Mpigie mzee beda umuulize"

Baada ya mazungumzo hayo ambayo ni kama yalimshitua Steve,alikata simu akawa amempigia yule jamaa aliyekuwa na duka kando ya nyumba tulivyokuwa tumepanga.Haukupita muda Steve akawa amenipigia simu tena.

Steve "Kaka ngoja kwanza niwahi nyumbani"

Mimi "Ni kweli?"

Steve "Ni kweli kaka"

Mimi "Anapeleka wapi vyombo au anatoroka?"

Steve "Ngoja niwahi kaka!"

Jamaa alionekana kupagawa sana na asijue ni kitu gani cha kufanya,kiukweli yule demu nilishamshauri sana kama mshikaji wake aachane nae lakini jamaa nikama alikuwa amerogwa,yule demu alikuwa akimfanyia vituko vya kila aina lakini Steve alikuwa haambiliki wala ashauriki,sikuwahi kuelewa ni kitu gani kilimfanya Steve apagawe kwa kile kitoto cha kimakonde.Pasipokuelewa ni kitu gani kilikuwa kinaendelea,mimi niliendelea kupiga zangu kazi kama kawaida.

Ilipofika mida ya saa 11 jioni,Steve akawa amenipigia simu tena akiwa analia kana kwamba kafiwa.

Steve "Kaka Zubeda kaondoka"

Mimi "Acha kulia mwanangu nakuja muda siyo mrefu"

Steve "Kaka Zuu wangu wamemchukua"

Mimi "Nakuja kaka wewe nisubiri"

Jamaa alikuwa akilia kama tahira,sikujua Steve alikuwaga akisimbuliwa na kitu gani kwasababu jamaa alikuwa na sura ya kirembo(Handsome) na kiukweli ungemuona usingedhani kama alikuwa mpumbavu wa kulilia mwanamke kiasi kile.Ilipofika saa 11 : 30 niliamua kukunja ile meza pamoja na mwamvuli nikapeleka mahali ambapo nilikuwa natunzia kila siku,mwaka ule ilipokuwa ikifika saa 12 : 00 jioni na usajili pia ulikuwa unasitishwa,sasa wakati naondoka yule brother wa lile duka la simu(Sitamtaja jina lake halisi kwasababu maalumu,hivyo nitampatia jina la Ally Mpemba) akawa ameniita na mara zote nikiwa pale alikuwa akiniita "Master",alipenda kuniita kwa utani hivyo kwasababu alikuwa akiona shughuli niliyokuwa nikiifanya ndipo akawa ananiita hivyo Master,alikuwaga ananiambia "Aisee wewe nakukubali sana,wewe ni master wa hizi kazi".Kwahiyo ikaenda kimzaha mzaha hivyo hadi akawa ananiita master,jamaa alikuwa ni mpemba lakini vilevile alikuwa mwarabu,nadhani tunafahamu jamaa wanavyokuwaga.

Ally Mpemba "Mbona wawahi kufunga leo,kunani!"

Mimi "Ndiyo muda wenyewe huu kaka"

Ally mpemba "Aaah Master siyo kawaida yako!"

Mimi "Kuna ishu naiwahi maskani kaka"

Ally mpemba "Kesho nikitoka kuswali,tuonane basi!"

Mimi "Tutaonana kaka,si utakuwepo?"

Ally mwarabu "Nadhani nitakuwa kule Aggrey,hapa atakuwepo dada yako"

Mimi "Sawa kaka haina tatizo"

Sasa kumbe mara zote mimi nimekuwa nikifikiria yule Aunt ninayemkuta pale dukani anayependa kujifunika Nikabu ni mkewe kumbe alikuwa ni dada yake;baada ya mazungumzo na Ally niliondoka zangu kwenda kufukuzana na magari ya Gongo la mboto.

Namshukuru Mungu niliingia Gongo la mboto mida ya saa 1 usiku,nilipofika pale nyumbani nilikuta Steve amekaa kwenye mlango wa chumba chake,nilipitiliza moja kwa moja hadi kwa Steve.

Mimi "Vipi?"

Steve "Ali siyo poa kaka"

Niliingia ndani ya kile chumba nikakuta vitu muhimu vyote vimekombwa na yule demu wake,alichokuwa ameacha ni vyombo vya kupikia tu,lakini TV chogo,friji,jiko la gesi,mashuka na vitu vidogo vidogo vyote alikomba.

Mimi "Aiseee,sasa utafanyaje?"

Steve "Nampigia simu zangu hapokei!"

Mimi "Kwani mligombana jana?"

Steve "Tangu siku ile kaka huwezi amini sijagombana nae"

Mimi "Kwani kwao ni wapi?"

Steve "Kwao Mtwara kaka ila yupo dada yake pale Mombasa ndipo alipokuwa anakaa kabla sijamchukua"

Mimi "Dada yake ushampigia simu?"

Steve "Nimempigia akaniambia huyo hawezi kwenda sehemu nyingine zaidi ya kwa bwana ake wa zamani kwasababu hapa mjini hana ndugu mwingine tofauti na yeye"

Mimi "Kwahiyo na wewe umekubali aondoke na vyombo vyako kwenda kwa bwana ake huyo?"

Steve "Sasa kaka nitafanyaje?"

Kiukweli nilitamani kumzibua mabao ya kutosha yule jamaa kwa upumbavu alokuwa akiongea mbele yangu lakini niliamua kuwa mtulivu kwasababu mambo yao yalikuwa hayanihusu,kilichokuwa kinanikwaza ni namna Steve alikuwa akiumia lakini kila ukimuongelea huyo demu vibaya ni kama anachukia,sikujua yule jamaa alipewa nini na yule demu aisee!.

Mimi "Huyo mshikaji wake unamfahamu?"

Steve "Kama ndiye huyo dada yake aliyeniambia namfahamu kaka na mara kadhaa tu nimekuwa nikimfata hapo"

Mimi "Daaah ila wewe jamaa nae,sasa unafahamu kabisa demu wako anakusaliti halafu bado unaendelea nae kweli,hata kama ni kupenda mwanangu wewe umepitiliza"

Steve "Nisindikize kaka mi nikafate vyombo vyangu tu"

Mimi "Ni wapi?"

Steve "Ni hapo Pugu kajiungeni"

Sasa nilitoka nje kwenda kupiga strori kadhaa na yule jamaa wa dukani na kweli alisema ile Suzuki carry ilielekea uelekeo wa njia ya Pugu na jamaa pia alishangaa namna Steve alivyokuwa bwege kiasi kile.

Tuliondoka huo usiku kuelekea Pugu kajiungeni,tulipofika Steve aliamua kuniongoza hadi hapo kwenye hiyo nyumba aliyokuwa anakaa huyo jamaa ambaye alikuwa anamgonga huyo demu wake.Tulipofika Steve akaanza kugonga kile chumba ambacho kilikuwa kimefungwa kwa ndani,baada ya kugonga sana alitoka jamaa mmoja chokoraa tu akiwa kifua wazi.

Jamaa "Vipi"

Steve "Poa,Zuu yupo?"

Jamaa "Zuu?,Zuu yupi?"

Steve "Sadi hebu achana na maswali ya kisenge,ina maana wewe leo humjui Zuu?"

Jamaa "Zuu wapo wengi sijui wewe unamtafuta yupi!"

Steve "Demu wangu"

Jamaa "Sasa demu wako hapa kafata nini!"

Muda huo niko pembeni nasikiliza yale malumbano nilikuwa nimechukia kishenzi,kibaya zaidi kuna majirani ambao nao walikuwa wamepanga kwenye ile nyumba walikuwa nje wakipika huku wakisikiliza na kujionea lile sekeseke.Baada ya kuona wanaigiza niliamua kusogea karibu na kumuuliza swali yule dogo.

Mimi "Wewe zuu unamjua au humjui?"

Jamaa "Brother,huyo Zuu anayemuongelea huyu ni demu wangu"

Mimi "Yupo au hayupo?"

Jamaa "Yupo!"

Mimi "Basi muite"

Jamaa baada ya kuona niko serious alifunga ule mlango akarudi ndani kisha akawa ametoka na kile kidemu.Baada ya kutoka Steve alibaki kujing'ata ng'ata hata kuongea ni kama alishindwa.Baada ya kuona jamaa haongei anabaki kushangaa ilibidi niingilie kati.

Mimi "Vitu vya jamaa viko wapi?"

Zubeda "Vitu gani?"

Mimi "Kwani wewe umechukua vitu gani?"

Zubeda "Vitu nilivyochukua ni vyangu,mmh kuna swali lingine!"

Mimi "Steve hebu pambana na demu wako mi naondoka"

Steve "Kaka usiniache"

Mimi "Kilichotuleta huku ni vitu na unasikia anasema si vyako,sasa hapa tunafanya nini?"

Steve "Zuu hivyo vitu ni vyako unauhakika?"

Zubeda "Nishasema vitu nilivyochukua ni vyangu,vyako nimekuachia nadhani umevikuta"

Steve "Naomba nichukue vitu vyangu nisije kufanya vurugu hapa"

Zubeda "Weeeee ishia hapo hapo,ina maana ulikuwa unanitomba bure!"

Aliendelea "Ina maana ulikuwa unanifira bure?"

Zubeda "Acha ujinga firauni wewe"

Aliendelea "Yaani ulidhani huu mwili niwa kushikwa bure bure tu!"

Yale maneno machafu yalipelekea wale kina mama kuanza kucheka,nilimwambia Steve tuondoke,japo jamaa alikuwa akitetemeka lakini niliamua kumuondoa lile eneo na kuondoka zetu,kiukweli kile kidemu hakikuwaga na aibu hata kidogo na nilikuwa namshangaa sana Steve anawezaje kuwaacha mademu wakali wa pale ofisini akaenda kutembea na kile kichakubimbi.

Mimi "Vitu vinanunuliwa we tuondoke!"

Steve "Kaka ila Zuu nampenda,siwezi kuondoka nikamuacha kaka ni bora nife"

Mimi "Yaani unaona bora ufe kwa ajili ya mwanamke?"

Mimi "Ok,rudi ukafe!"

Niliondoka zangu lile eneo nikamuacha jamaa akiwa amekaa chini machozi yakimtoka kama tahira.Baada ya kufika nyumbani nilipika msosi nikala kisha nikaingia chumbani kulala.



..............................................................................................



Utajiri wa rafiki yangu ulivyofanya nikamuamini Shetani - 10.


Nilishitushwa na sauti ya Steve akiwa ananiita na kunigongea akitaka nimfungulie mlango,nilipochukua simu na kutazama muda ilikuwa imefika saa 4.Niliamka nikaenda kumfungulia jamaa mlango,kiukweli alionekana hayuko kawaida na sikutaka kumpa presha,nilimwambia aingie alale atulize akili.

Namshukuru Mungu kulipokucha,mimi niliwahi kuondoka nikamuacha jamaa akiwa amelala,kabla ya kwenda Kariakoo ilikuwa ni lazima kila msajili line kupitia pale ofisini Buguruni kusikiliza kikao na mambo mapya kisha kuelekea kwenye kituo chake cha kazi,nami ndivyo nilivyofanya!.Nilipofika Kariakoo nilielekea eneo ambalo nilikuwa nikihifadhia vitu vyangu vya kazi na kuja kuanza kupiga kazi.

Sasa wakati nafika pale,lile duka la Ally mpemba lilikuwa bado halijafunguliwa,mi niliweka zangu meza nikaanza kupiga kazi kawa kawaida,kiukweli kwa kipindi kile kulikuwa na wateja wengi mno,yaani ilikuwa ukifungua tu ile saa 2 asubuhi wateja wanaanza.Ilipofika mida ya saa 3 asubuhi,kuna gari aina ya Range Sport nyeusi iliyokuwa na Private Number iliyoandikwa " SALIM " ilisimama pembeni yangu kisha ukafunguliwa mlango akawa ameshuka yule Aunt ndugu yake na Ally Mpemba.

Aunt "Leo umeniwahi"

Mimi "Leo nimekuwahi Aunt,salama lakini"

Aunt "Mie niko salama kabisa sijui wewe huko utokako"

Mimi "Salama kabisa"

Wakati nikiwa naendelea kuzungumza na Aunt ile gari ikawa imeondoka kuelekea Kamata.Yule Aunt pamoja na ndugu yake Ally Mpemba walikuwa wakizungumza kiswahili cha kipwani pwani kama ambavyo wazanzibar wakizungumza!.

Ilipofika mida ya 5 asubuhi,alinipigia simu Steve na akawa ananiambia ya kwamba,yule demu wake wamekubaliana arudi nyumbani na yeye amemsamehe ili mambo mengine yaendelee,mimi kwakuwa nilishamshauri sana kuonekana kama natwanga maji kwenye kinu nilimwambia sawa,hakuna tatizo,sikutaka kabisa kuwashauri kwasababu niliona ni kama nilikuwa napoteza muda.

Mimi "Kwahiyo vitu anarudisha?"

Steve "Ndo naenda kuvichukua kaka"

Mimi "Kwahiyo Leo hujaenda Tandika"

Steve "Leo siendi kaka ngoja kwanza nikamchukue huyu"

Mimi "Poa,kama ukitoka funguo utaniwekea juu ya mlango hapo"

Steve "Leo sina ratiba ya kutoka kaka"

Mimi "Sawa,baadae"

Safari hii niliamua nikae pembeni katika kushuri kwasababu nilichokuja kugundua ni kwamba,mambo yote ya msingi niliyokuwa nikimshauri jamaa kuhusu demu wake,yeye alikuwa akimwambia kila kitu na hivyo mimi kuonekana mchonganishi!,hivyo nikaamua sitokaa tena nimshauri na kama ni kufa yeye afe tu!.

Ilipofika mida ya saa 9 mchana,Ally Mpemba akawa amekuja akiwa ndani ya kanzu nyeupe,alipofika pale nje kabla ya kuingia ndani ya duka lake akawa amenisalimu.

Ally mpemba "Assalam aleykum"

Mimi "Alekom salam"

Ally mpemba "Kwema?"

Mimi "Kwema kaka"

Ally mpemba "Leo wafunga saa ngapi?"

Mimi "Kama kawaida kaka saa 12"

Ally mpemba "Basi utanipa muda wako kidogo Leo sheikh"

Mimi "Sawa kaka"

Sasa mida ya saa 10 alasiri alipokuwa anatoka pale dukani akawa ameniomba kama itawezekana tuondoke wote kuelekea Aggrey.

Mimi "Si hakuna haja ya kutoa vitu vyangu"

Ally mpemba "We viache tu,nishamwambia Farah atakuangalizia usijali"

Niliondoka na Ally kuelekea mtaa wa Aggrey ambako huko nako nilikuta kuna duka kubwa la simu na ndani yake kukiwa na wafanyakazi kama 4 wakisaidiana kuuza,sasa tofauti na kule ni kwamba lile la kule niliko lilikuwa dogo na la pale Aggrey lilikuwa kubwa.

Ally mpemba "Mi huwa nashinda hapa mara zote,nisipokuwa kule basi wanipata hapa"

Mimi "Ok sawa kaka lete maneno"

Ally mpemba "Kuna kazi nataka unisaidie Master"

Mimi "Kazi gani tena kaka?"

Ally Mpemba "Ni kazi ya kawaida tu!"

Aliendelea "Mimi ninahusika pia na mambo ya caterings na nimewaajiri ndugu wa familia na watu wengine lakini ndugu zangu ni watu wa ovyo sana huwa hawapendi kazi za kujishughulisha wao wanapenda kukaa kama hivi unavyowaona"

Ally Mpemba "Sasa kila ninapokutazama nakuona wewe ni mpambanaji mtu wa bara na ndiyo maana nakuita Master"

Aliendelea "Mimi nataka tu unisaidie kitu kimoja na offcouse siyo msaada bali nataka tufanye kazi"

Mimi "Sawa kaka"

Ally Mpemba "Kwani huko Tigo mnalipana shi ngapi?"

Mimi "Kaka kule ninalipwa kwa kamisheni"

Ally Mpemba "Sawa naelewa ni kamisheni lakini malipo yao huwa yapoje?"

Mimi "Inategemea na laini nilizosajili na matumizi ya wateja kwa mwezi husika"

Ally Mpemba "Doo kwahiyo mteja asipotumia laini hulipwi!"

Mimi "Ni mara chache mteja aje kusajili line na asiitumie,sema huwa malipo yanategemea,kuna muda yanapungua na kuna muda yanaongezeka"

Ally Mpemba "Ok sasa mimi nataka unisimamie kwenye mradi wangu hata kwa muda wa mwezi tu Master halafu nikipata mtu muaminifu nitamuweka halafu wewe utaendelea na shughuli zako:

Mimi "Kaka kwanini mimi?"

Allya Mpemba "Mi unajua nilikuwa sikutilii maanani sana,kuna siku Farah akaniambia wewe ni mtu poa sana hata namna unavyo behave,kwa maana nilipokuta umeweka meza yako kando ya duka langu nilimwambia Farah unapaswa utoke pale ila akaniambia wewe ni mtu poa sana"

Aliendelea "Ninachotaka mimi ni kwamba,wafanyakazi wapo ila wewe ukanisimamie tu maana alikuwa anasimamia mama yangu mdogo lakini yuko Unguja anamuuguza me wake!"

Aliendelea "Wewe niambie tu unataka niwe nakulipa shi ngapi?"

Mimi "Kaka unajua sijawa na uzoefu na kazi unayotaka niifanye,hivyo itakuwa ngumu kujua unilipeje kaka"

Ally Mpemba "Sasa fanya hivi,wewe nenda kahifadhi vitu vyako halafu uje twende nyumbani mara moja"

Basi niliondoka zangu kurudi gerezani nikachukua meza,kiti pamoja na mwamvuli nikawa nimerudisha mahali ambapo nilikuwa nahifadhia.Baada ya hapo nikawa nimeondoka hadi Aggrey kisha Ally Mpemba akanichukua kuelekea Msimbazi uelekeo wa kituo cha polisi,tulitembea hadi pale Big Bon ambapo nikaona anatoa funguo wa gari kwenye kanzu yake kisha akabonyeza ile gari ikawaka taa na milango ikafunguka,ilikuwa ni ile ile Range ambayo asubuhi niliona dada yake akiwa anashushwa ambayo ilikuwa na Private Number,sasa kwa mara ya kwanza mwanaume kutoka Kijiji cha Mogabiri huko Ukuryani Tarime nikapanda Range,aisee asikwambie mtu na ndiyo maana kuna watu wako tayari kufanya kila aina ya ovu ili kujipatia fedha wanunue magari,ile ilikuwa ni moja ya gari nzuri kuwahi kupanda katika maisha yangu ya umasikini!.

Tuliondoka lile eneo tukaikamata Morogoro Road kisha safari ikaanza kwa spidi ya wastani,baada ya muda tukawa mbele ya nyumba moja maeneo ya magomeni Mikumi,ile nyumba ilikuwa ya kawaida sana kwa muonekano wa nje ila nilipoingia ndani kiukweli ilikuwa nzuri mno na usingedhani kama muonekano wa nje unasadifu kilichomo ndani!.

Baada ya kupiga honi na kufunguliwa geti gari ikawa imeingia pale uani na kupaki,sasa tulipoteremka kuna vitoto vya kike viwili vya kiarabu(Kipemba) tulivikuta hapo ndani vikawa vinamkimbilia Ally na kumrukia kwa furaha!.

Ally Mpemba " Hawa ni watoto wa Farah "

Mimi "Ooh sawa kaka"

Sasa pale nje nilikuta kuna vyombo vingi sana vya kisasa na majiko makubwa ya Gesi na mkaa,na ndivyo vilikuwa vyombo vilivyokuwa vinatumika kwenye shughuli za catering.

Ally Mpemba "Nimekuleta hapa ili ujionee mwenyewe,na ukishajionea najua utaniambia nikulipe kiasi gani master"

Aliendelea "Sasa wewe kazi yako utakuwa unahakikisha vyombo vyote vinaondoka hadi kwenye events na baada ya hapo utakuwa unahakikisha vyombo vyote vinarudi kama vilivyokuwa,baada ya hapo utakuwa unasimamia ishu ya usafi wa vyombo"

Aliendelea "Kikubwa wewe utakuwa msimamizi"

Baada ya yale maelezo angalau sasa ndipo nikaanza kupata uelewa wa kazi nitakayoenda kuifanya.

Ally Mpemba "Na bahati nzuri ni kwamba,events siyo kila siku,kama kutakuwa hakuna events yeyote wewe utakuwa unaendelea na shughuli zako,mimi nahitaji tu msimazi hadi pale atakaporudi mama mdogo au nitakapompata mtu sahihi,ila nakuomba kwa sasa unisaidie kwenye hili"

Mimi "Sawa kaka nimekuelewa"

Ally Mpemba "Ok sasa niambie niwe nakulipaje!"

Mimi "Wewe nilipe utakavyoona kaka"

Ally Mpemba "Wewe niambie kiasi utakachoona kwako kinafaa maana hii siyo shughuli nyepesi kama unavyodhani!"

Mimi "Tufanye hivi kaka,tukianza kazi ndiyo nitajua,nadhani kwasasa tusubiri kwanza "

Ally mpemba "Ok hakuna tatizo maadamu umeamua hivyo!"

Baada ya mazungumzo yale tuliingia kwenye gari tukawa tumeondoka kuelekea Kariakoo,sasa wakati tunarudi tulipitia njia ya Kigogo na tulipofika pale Karume,jamaa alinipatia elfu 20 ya nauli mi nikashuka kwenye gari yeye akawa ameondoka.Nilienda upande wa pili kupanda gari za Gongo la mboto na kuondoka zangu maskani.



.........................................................................................


Utajiri wa rafiki yangu ulivyofanya nikamuamini Shetani - 11



Nilifanikiwa kufika nyumbani na nikamkuta Steve amemrudisha demu wake kichwa kibovu,kiukweli niliapa sitokuja tena kuingilia au kushauri mahusiano yao,hata kama wangekuwa wanapigana hadi kuuana,nisingethubutu kamwe!.

Sasa nakumbuka siku moja nikiwa pale Kariakoo,alinipigia simu yule jamaa yangu tulikuwa wote tukipambana kwenye vibarua vya ujenzi aliyeitwa Mwakisaka na alinitaka kama nipo tu sina ishu nimfuate kibaha kulikuwa na mradi wa ujenzi wa Ma-Godown na walikuwa wakilipa vizuri.

Mwakisaka "Sawa kaka kama huko unapiga pesa wewe endelea maana riziki popote"

Mimi "Kwahiyo siku hizi unaishi Kibaha"

Mwakisaka " Hapana kaka,huwa naweka tu kambi"

Mimi "Sawa kaka wewe pambana".

Niliendelea kupiga kazi yangu ya usajili wa line za simu kwa uaminifu mkubwa mno,hakuna kazi niliyoifanya kwa moyo wote kama vile ilikuwa ya baba yangu kama ile kazi ya kusajili line,na ndiyo maana hawa madogo wanaosajili line za simu leo ambao huwa wanatembea kwa mguu(Door to door),huwa nikiwaona tu nawaita tunapiga stori mbili tatu kisha nawatia moyo halafu nawaachia hela ya maji kidogo.Kiukweli kwa siku hizi imekuwa kazi ya kudharaulika sana hasa ukizingatia wengi wao wanakosa uaminifu na kuwaibia wateja hao hao ambao wanawafanyia usajili,lakini enzi zangu wakati nafanya ilikuwa kazi muhimu sana na iliyokuwa na maslahi mazuri!,yote kwa yote ni kwamba imebaki kwenye kumbukumbu ya maisha yangu ambayo siwezi kuisahau.

Siku moja nikiwa nimetoka kazini usiku nikiwa nimelala,Ally Mpemba alinipigia simu.

Ally Mpemba "Kaka nakusumbua umelala"

Mimi "Hapana kaka nilikuwa bado niko macho"

Ally Mpemba "Sasa kuna tenda nimeipata usiku huu inapaswa kufanyika kesho jioni pale Osterybay,hivyo jitahidi kesho asubuhi na mapema tuonane ili nikukutanishe na mama mpishi muone mtafanyaje"

Mimi "Sawa kaka"

Ilipofika Asubuhi mida ya saa 2 nilikuwa kwenye gari nikielekea pale Buguruni ofisini kwenye vikao vya kawaida vya kazi yangu ya usajili ambavyo vilikuwa vikifanyika kila siku ili kujua na kufahamu mambo mapya.Sasa niliamua kupita kwanza pale ofisini ili Team leader wangu asije akaona nimezingua kimakusudi;Baada ya vikao kuisha kila mmoja alitawanyika kuingia kazini,mimi nilielekea Kariakoo moja kwa moja,nilipofika sikutaka kuweka meza niliona nimpigie simu kwanza Ally Mpemba.

Mimi " Kaka Asalama aleko"

Ally Mpemba "Aleykum Assalam"

Aliendelea "Kwema?"

Mimi "Kwema kaka,nishafika hapa Kkoo"

Ally Mpemba "Nadhani ungekuja hapa Magomeni maana nimemwambia na Mama mwa-J mnikute hapa"

Mimi "Pale pale tulipoenda siku ile?"

Ally Mpemba "Yeah njoo mpaka hapo"

Mimi "Sawa"

Nilitembea mdogo mdogo hadi karume nikaenda kudandia daladala hadi magomeni,baada ya kushushwa nilianza kutembea mdogo mdogo hadi kwenye ile nyumba ambayo tulifika na Ally siku ile.Baada ya kufika pale nilimpigia jamaa simu kumjulisha ya kuwa nimefika na alinitaka nisubiri kwani muda si mrefu angekuwa amefika hapo.

Haikupita muda mrefu lile geti likafunguliwa akatoka mwanamke mmoja wa kiarabu ambaye alikuwa amejitanda ushungi,baada ya kutoka nje akawa amefunga lile geti na kuondoka.Sikuweza kusalimiana na yule mwanamke kwasababu nilisimama mbali kidogo na ile nyumba.Sasa wakati nikiwa nashangaa pale nje,ile Range iliyokuwa imebandikwa namba binafsi "SALIM" niiona ikiwa inakuja na ilipofika jirani alikuwa ni Ally Mpemba akiendesha ndani akiwa peke yake.

Ally Mpemba "Nisamehe kaka nimekuweka sana"

Mimi " Usijali kaka"

Ally Mpemba "Kwanini umekaa nje?,ungegonga wakufungulie nilishawapa taarifa"

Mimi "Hilo sikulifahamu kaka"

Ally Mpemba "Sema na mimi nimekuwa mzembe kukwambia"

Aliendelea "Mimi nakaa mtaa wa pili kutoka hapa"

Mimi "Mawazo yangu yote nikajua huwa unakaa hapa"

Ally Mpemba "Hapana kaka,Hapa anakaa bi mkubwa na wadogo zangu"

Mimi "Ooh sawa kaka"

Baada ya mazungumzo mafupi,jamaa aligonga lile geti kisha akaja mtu kufungua.Tulipofika ndani jamaa alimwambia dada mmoja mweusi mwenzangu ambaye nadhani alikuwa mfanyakazi ya kwamba atuletee viti tukae nje wakati ambao tungekuwa tunamsubiri mama Mwa -J.

Ally Mpemba "Kuna jamaa yangu mmoja leo usiku atakuwa na sherehe pale kwake hivyo mnapaswa kuweka maandalizi sawa"

Aliendelea "Pia utakuwa unapata uzoefu kuanzia hapo"

Ally Mpemba "Unajua master,nahitaji kuaminika na viongozi wakubwa kwenye haya mambo ya vyakula na nahitaji kuingia kwa miguu yote ndiyo maana unaona nimejipanga!"

Aliendelea "Yaani sherehe zote za viongozi na watu wakubwa nataka tenda niwe nachukua mimi"

Mimi "Kaka hakuna kinachoshindikana,ni malengo tu na jitihada"

Ally Mpemba "Jitahada ninazo kaka na ndiyo maana unaona kila kitu kipo hapa,mambo mengine makubwa ni kwa uwezo wa Allah"

Baada ya dakika 40 yule mama aliyekuwa mpishi aliyeitwa mama Mwa -J alikuwa amekuja akiongozana na mabinti wawili na kijana mmoja.Baada ya salaamu,Ally Mpemba alikuwa akimtambulisha kwangu,baada ya utambulisho ule kumbe yule mama aliwahi kuwa mfanyakazi wa ndani hapo kwo Ally Mpemba kwa miaka ya nyuma.

Ally Mpemba "Wale watu watakuwa 50 na kuna viongozi pale,hivyo naombeni mfanye vema zaidi "

Mama Mwa-J " Bila shaka mdogo wangu unaniamini,kaa kwa kutulia "

Ally Mpemba alichukua simu yake akawa kuna mtu anampigia na kumtaka alete gari.Haukupita muda kuna gari ililetwa ikiwa ni Hiace nyeusi.

Ally mpemba "Hii ndiyo gari ambayo huwa inabeba vyakula pamoja na vyombo,niliinunua kwa ajili ya kazi hii "

Mimi "Ooh sawa kaka hongera maana naona uko vizuri "

Ally Mpemba "Hii mbona kawaida tu"

Kiukweli Ally Mpemba alionekana mtu fulani wa makamo,hakuwa kwenye uzee wala ujana,alikuwa yupo kati.Baada ya mazungumzo ya hapa na pale,yule mama aliondoka na wale mabinti wakaelekea sokoni kwa ajili ya kufanya mahitaji ya vyakula na viungo ambavyo vingetumika kwenye upishi.
Kweli,baada ya siku ndefu ya upishi na kusaidia kuandaa vyakula,ilipofika mida ya saa 11 jioni tuliondoka kuelekea Osterbay mahali ambako kulikuwa na tukio;Ile Hiace ilibeba kila kitu kilichokuwa tayari na tukaondoka,sasa ile Hiace kwa nyuma hakukuwa na siti,kulikuwa tupu na ilikuwa maalumu kwa ubebaji wa vyombo vya vyakula.Ile kazi ya usimamizi ilifanya nikazunguka sehemu karibia zote za ushuani hapa Dar es salaam,pale Osterbay tulipokwenda kiukweli hakukuwa kwa kawaida,mazingira tu ya ile nyumba na mali zake ilitosha kukuaminisha ya kwamba watu walikuwa wanaishi na siyo kuwasindikiza watu kuishi.

Lilikuwa ni tukio la uvalishanaji Pete na baada ya hapo kuliendelea sherehe,sasa Ally Mpemba alikuwa akinipigia simu kufahamu mambo yameendaje na nilikuwa namjulisha mambo yalivyokuwa yakiendelea.Tulikaa pale eneo la tukio hadi mida ya saa 6 usiku,ndipo sherehe ikawa imefungwa rasmi na sisi kupakia vitu na kuvirudisha kule magomeni,sasa kabla ya kuondoka Ally Mpemba alikuwa ameniambia kuna muhusika pale kwenye hiyo sherehe angenipatia milioni 2.5 nimpelekee.Kabla ya kuondoka niliitwa na jamaa mmoja aliyenikabidhi milioni 2.5 kisha akampigia Ally Mpemba akamwambia amenipatia hiyo hela.

Jamaa "Huyu hapa ongea nae"

Ally Mpemba "Master amekupa?"

Mimi "Ndiyo kaka kaniakabidhi milioni 2.5"

Ally Mpemba "Sawa utaniletea "

Basi tuliondoka zetu lile eneo kisha tukawa tumefika magomeni na kuanza kushusha vile vyombo na kuvipanga,Ile ishu ya kupakia na kwenda kushusha vyombo na kuviweka mahali pake ilimalizika mida ya saa 8.Baada ya hapo ile Hiace iliwabeba mama Mwa -J na wale wafanyakazi lakini kabla ya kuondoka nilitaka kufahamu walikuwa wakielekea wapi!.

Mama Mwa - J "Siye tunaenda Tegeta"

Mimi "Mwanangu suka siunarudi?"

Suka "Nikifika ni kupaki kaka sirudi huku"

Mimi "Duuuu sasa nitafikaje maskani!"

Suka "Kwani kwako ni uelekeo upi"

Mimi "Mimi naishi Gongo la mboto "

Suka "Gongo la mboto mbona magari kibao muda huu!"

Mimi "Muda huu?"

Suka "Yeah wewe tembea hadi kituoni magari ni kibao"

Mimi "Basi niache pale kituoni kaka"

Nilipopanda kwenye gari simu yangu ikawa inaita,nilipoitoa mfukoni nikakuta nj Ally Mpemba ananipigia simu.

Ally Mpemba "Mko wapi?"

Mimi "Kaka nipo kwenye gari hapa wananiacha kituoni nielekee Gongo la mboto"

Ally Mpemba "Kaka unajipenda Kweli?kituoni muda huu?"

Mimi "Jamaa ameniambia kuna usafiri"

Ally Mpemba "Mpe simu Jabir"

Nikampa simu yule dereva aliyekuwa akiitwa Jabir wakawa wanaongea kwenye simu na baada ya maongezi jamaa akawa amesimamisha ile Hiace,haukupita muda Ally Mpemba akawa amekuja na ile Range maeneo yale kisha akawa amenitaka nishuke.

Ally Mpemba "Poa nyie ondokeni"

Ally Mpemba "Ingia twende kaka"

Aliendelea " Kaka usiku huu huwezi pata gari za huko kwenu vinginevyo vibaka unataka wakufanye kitu mbaya"

Aliendelea "Twende ukaegeshe kwangu master "

Kweli,tulipofika jamaa anapokaa alishuka akaenda kufungua geti kisha akaingiza gari ndani na kwenda kufunga geti.Ile nyumba ilikuwa nzuri mno na hadi leo ipo ingawaje Ally Mpemba alishaachana nayo anaishi kwingine,ni nyumba ambayo kwa wakati ule ulikuwa unajiuliza mara mbili mbili kwasababu haikuwa ya mchezo mchezo,pale nje kuna gari mbili zilizokuwa mpya na hazikuwa na namba,ni kama zilikuwa zimetoka bandarini.

Jamaa hakuwa na maneno mambo mengi,tuliingia ndani akawa amenionyesha chumba cha kulala kisha na yeye akawa ameelekea kulala chumba chake,kiukweli nililala kidogo tu kukawa kumekucha,kulipokucha Ally aliniambia nisubiri tuondoke wote kuelekea Kkoo,sasa nilitoka nikaelekea sebuleni kukaa na kushangaa namna ambavyo watu walikuwa wakiishi maisha yaliyomstahili mwanadamu kuyaishi.Sasa nilipofika pale sebuleni nilikuta kuna majani ya mchicha na masalia ya Cabbage kana kwamba kulikuwa na mbuzi wamekula na kuacha yale masalia shaghala baghala.

Ally Alipomaliza kujiandaa alikuja akawa kama anashangaa,alielekea ndani akachukua mfagio wa ndani na akaja akafagia na kuzoa,alionekana ni mtu mwenye wasiwasi mwingi lakini alijifanya kufurahi.

Ally Mpemba "Tuondoke sasa "

Aliendelea "Mimi naishi mwenyewe master mke na watoto wako huko Oman"

Mimi "Ooh sawa kaka"

Ally Mpemba "Eeeh bana hivyo ukiona nafanya usafi usinishangae"

Mimi "Ni mambo ya kawaida kaka hata mi naishi mwenyewe"

Ally Mpemba "Bado hujaoa tu!"

Mimi " Bado kaka"

Ally Mpemba "Fanya uoe master,mwanamke na watoto ni baraka "

Aliendelea "Bila ya mke unaweza usifike popote katika haya masuala ya rizki kaka"

Jamaa aliniambia nipande kwenye gari na yeye akawa amerudi ndani,sasa kiukweli nilikuwa naendelea kuyatazama yale magari yaliyokuwa yamepaki namna yalivyokuwa mapya na kwa kuyaangalia tu ilionekana yalikuwa ya gharama kubwa.

Baada ya kutoka ndani aliingia kwenye gari akaitoa nje kisha akarudi kufunga geti tukaondoka zetu.

Maisha yaliendelea huku na mimi nikiendelea kupambana na kazi zangu zote mbili,siku ambayo nilikuwa sisajili line nilikuwa naenda kwenye events na siku ambazo hakukuwa na events nilikuwa nafidia ule muda kwa kusajili line nyingi.

Baada ya kupata pesa ya kutosha nilifungua akaunti NMB nikawa naweka hela zangu nikiwa na malengo ya kununua uwanja ili kwa baadae nianze ujenzi.

Ilifika muda Ally Mpemba akawa ananiamini sana na nikawa mtu wake wa karibu sana,kuna mambo ya familia yake alikuwa ameniambia na hivyo ile familia niliifahamu kuliko walivyodhani,sasa kwakuwa jamaa alikuwa ameniamini na mimi pia sikutaka kumuangusha katika uaminifu.Kuna siku jamaa alikuwa na safari ya kuelekea Unguja ambako aliniambia angekaa kwa takribani wiki moja na kurejea,sasa akawa ameniomba kitu kimoja ambacho sikukielewa kwa haraka haraka.

Ally Mpemba "Kaka nina safari ya Unguja na nadhani itanichukua wiki moja"

Aliendelea "Sasa nakuomba twende nyumbani mara moja kuna kazi ndogo nikupatie"

Mimi "Sawa kaka hakuna tazizo"

Ally Mpemba "Nakuamini sana kaka since day one,tafadhali Linda uaminifu wangu kwako"

Mimi "Kaka hakuna shida,mimi pia nakuamini sana kama wewe ulivyoniamini!"

Baada ya kufika kwake,alipaki gari nje akafungua geti tukaingia ndani,tulipofika ndani Ally Mpemba aliniambia atanipatia funguo wa ile nyumba yake lakini sipaswi kulala mle ndani kama yeye hayupo na kuna chumba alinionyesha ambacho alitaka kila siku saa 1 usiku nihakikishe nakifungua kinakaa wazi na inapofika asubuhi mida ya saa 12 naenda kukifunga.

Ally Mpemba "Utahakikisha kaka unakifungua unakiacha wazi na wewe unaondoka"

Mimi "Kaka hiyo mbona ni kazi ndogo tu!"

Ally Mpemba "Siyo kazi ndogo Master kama unavyodhani "

Mimi "Aaah kaka yaani kufunga chumba na kukifunga kuna kazi gani hapo?"

Mimi "Nitakuwa nawahi asubuhi na magari ya kawe kaka wala usijali"

Ally Mpemba "Hapana,utakuwa unachelewa na mimi nataka saa 12 :00 chumba kifungwe!"

Mimi "Nitakuwa naamka mapema kaka!"

Ally Mpemba "Sasa kama hutojali nakuomba uwe unalala kwenye ile gari nyeusi hapo kwa wiki hii tu kaka ili iwe kazi nyepesi kuliko kutoka huko uliko hadi hapa najua utachelewa"

Mimi "Sawa kaka hakuna tatizo"

Baada ya Ally Mpemba kunipatia maelekezo hayo niliona uaminifu aliyokuwa anaounyesha kwangu basi uenda kuna siku angenikabidhi mali au gari na mimi nivimbe mtaani!.



........................................................................................




Utajiri wa rafiki yangu ulivyofanya nikamuamini Shetani - 12.



Alinikabidhi rasmi funguo wa ile nyumba pamoja kiasi cha Tsh 140,000/= ikiwa na maana ya kwamba kila siku nitakapokuwa hapo nyumbani kwake,basi itanipasa kutumia elfu 20 kwa ajili ya chakula cha usiku,aliniambia sipaswi kabisa kurudi nyumbani kwa muda huo atakao kuwa ametoka.Kabla hajaondoka alinionyesha gari miongoni mwa magari mawili mapya yaliyokuwa yamepaki pale ndani ya fensi.

Kulikuwa na magari mawili mapya, moja lilikuwa Audi A4 nyeusi isiyokuwa na Number Plate na nyingine ilikuwa ni Mercedes benz C63 nyeupe,hii pia haikuwa na Number Plate,hizi gari zite zilikuwa na mpya kabisa.Jamaa aliniambia mimi ninapaswa kuwa nalala kwenye Audi A4.

Baada ya yale maelekezo huku akionyesha uaminifu mkubwa kwangu Ally Mpemba alisafiri kuelekea huko Unguja kama alivyokuwa ameniambia hapo awali.Baada ya jamaa kuondoka,mimi niliendelea na shughuli zangu za usajili wa line kama kawaida na ilipofika mida ya saa 12 jioni niliondoka zangu kupanda gari kuelekea nyumbani kwa Ally Mpemba.

Nilifanikiwa kufika nyumbani kwa Ally Mpemba kabla ya saa moja,nilisukuma geti nikaingia ndani kisha nikalirudishia,sasa nilisogea moja kwa moja hadi kwenye mlango mkubwa wa kuingilia ndani,nilifungua ule mlango na kuzama ndani,nilipofika ndani nilianza kuikagua ile nyumba lakini vyumba vyote nilikuta vimefungwa na yawezekana funguo atakuwa alikuwa ameondoka nazo au aliziweka mahali,chumba ambacho nilikuwa na funguo zake ni kile alichonipa kazi ya kukifungua na kukifunga!.Ile nyumba ilikuwa ni kubwa na ilikuwa niya kifahari,ulikuwa ukiingia ndani kulikuwa na nakshinakshi za gharama kubwa(Nadhani nyumba za waarabu au wahindi huwa mnaelewa zinavyokuwaga).

Ile nyumba ulikuwa ukiiangalia kwa nje ilionekana ya kawaida tu ila kwa ndani ilikuwa nzuri sana na usingeamini kama pale anaishi mtu mmoja.

Ilipofika mida ya saa 1 usiku nilienda mpaka kwenye kile chumba nikakifungua na kiukweli sikuweza kuvumilia ilibidi nisogeze shingo karibu na mlango,niliwasha taa kutazama ndani,nilipotazama ndani nilikuta kuna kitanda ambacho kilikuwa kimetandikwa kwa unadhifu wa hali ya juu,pia kulikuwa na makabati ya nguo pamoja na vitu vingine vya kawaida ambavyo huwa vinapatikana vyumbani.Niendelea kutazama kwa makini lakini hakukuwa na mtu wala,sasa niliamua kuondoka mle chumbani na nilikiacha wazi kama alivyokuwa ameniambia Ally.

Niliwasha taa za nje ya ile nyumba kisha nikafunga mlango,niliondoka zangu usiku ule kuelekea kutafuta chakula ili nile nirudi kulala kama kawaida kwenye gari ambalo Ally Mpemba aliniambia ninapaswa kulitumia kama kitanda.Baada ya kupata chakula,niliamua kurudi kwenda kulala ili asubuhi na mapema niamke niende kukifunga kile chumba,kiukweli sikutaka kumuangusha Ally Mpemba na nilitaka aniamini ili kama kuna mambo makubwa zaidi anionyeshe ili na mimi niweze kufanikiwa.

Wakati natoka kupata msosi ilikuwa mida ya saa 3, sasa nikaona niingie kwenye gari niweze kulala,kwakuwa funguo ya gari alikuwa ameniachia, nilipoingia kwenye gari niliwasha AC ili niendelee kupata kiyoyozi huku nikiutafuta usingizi,nilishusha kiti cha dereva kwa kurudi nyuma kisha nikaanza kuusaka usingizi,sasa wakati nikiwa nimepitiwa na usingizi nilishitushwa ghafla na mlio wa vitu vikiwa vinatupwa mle ndani kwenye nyumba ya Ally Mpemba.

Niliamka na taratibu na kutega sikio kwa makini ili nijiridhishe yawezekana nilisikia vibaya,ile sauti iliendelea na ndipo nikatelemka kwenye ile gari nikaelekea mlangoni kutega sikio vizuri,nilipofika pale mlangoni niliendelea kusikia glass,sufuria za kupikia pamoja na vyombo vingine vikitupwa chini kama vile kulikuwa na watu wanapigana, kiukweli niliingiwa na hali ya hofu sana ikabidi nirudi kwenye gari.Nilichukua simu nikawa namtafuta Ally Mpemba lakini simu yake haikupazikana,niliendelea kumtafuta sana lakini simu yake haikupatikana,sasa niliamua nikae kwenye gari nisitoke hadi asubuhi,muda huo ilikuwa yapata saa 7 usiku,sasa ile hali ya kutupa vitu iliendelea hadi ilipotimu mida ya saa 10 usiku,kiukweli sikupata usingizi hata kidogo na nilikuwa najiuliza kulikuwa na kitu gani mle ndani hadi vyombo kupigizwa kiasi kile,japo nilikuwa jasiri katika mambo mengi ambayo niliwahi kuyapitia lakini kwa mara ya kwanza ile hali ilinitisha sana.

Iilipofika mida ya 12 :00 nilienda kufungua ule mlango kwa umakini mkubwa kisha nikaingia ndani,nilipoingia ndani nikawasha taa ili niweze kutazama vizuri kwasababu kulikuwa bado na giza,sasa ile nimewasha taa na kutazama vizuri,nilikuta uaribifu wa kiwango cha juu sana,kiukweli nimepitia mambo mengi ya kutisha na kushangaza lakini lile tukio lilikuwa ni moja ya matukio yaliyonishangaza sana kwa ile siku.

Nilikuta vyombo vimepigizwa chini kila mahali,glass zilikuwa zimevunjwa vunjwa pale sebuleni hadi jikoni kulikuwa hakutamaniki,kiukweli sikuweza kufahamu ni kitu gani kilikuwa kimefanya uaharibifu kiasi kile.Nilisogea hadi kwenye kile chumba na safari hii sikutaka kabisa kichungulia ndani ilibidi nikifinge haraka.

Baada ya kufunga kile chumba nilitoka nje nikafunga mlango kisha nikarudi kwenye gari kwanza kutulia,kiukweli nilikuwa nina maswali mengi sana ambayo nilikuwa najiuliza lakini sikuwa na majibu.Nilikaa kwenye ile gari hadi mida ya saa 2 asubuhi ndipo nikatoka nikaelekea kwenye bomba kunawa uso na kusukutua maji mdomoni na baada ya hapo nikafunga geti nikaondoka zangu kuelekea ofisini Buguruni kwenye kikao.Kikao kilivyoisha nikaondoka kuelekea Kkoo kazini kama kawaida.

Kwa muda huo yule dada yake na Ally Mpemba aliyekuwa akiitwa Farah hakuwahi kujua kabisa kwa wakati huo kama mimi na Ally tulikuwa tumeshibana kiasi kwamba mpaka Ally kuniachia funguo za nyumba yake,sasa wakati Ally ameondoka,ile Range ilikuwa imepaki nyumbani kwake.

Ilipofika mida ya saa 5 asubuhi simu yangu ikawa inaita na nilipoitazama alikuwa ni Ally akinipigia,niliipokea ile simu kisha akawa ananiuliza maendeleo tangu alipoondoka.

Ally Mpemba "Unaendelea vema lakini wewe?"

Mimi "Kaka naendelea vema lakini jana kuna jambo limetokea pale kwako!"

Ally Mpemba "Usiniambie umefanya ambacho sikukuelekeza"

Mimi "Hapana kaka siyo hivyo"

Ally Mpemba "Mmmh ni nin!,ama umeshindwa nilichokwambia?"

Mimi "Kaka jana wakati nimelala kwenye gari nilikuwa nasikia vitu vinatupwa chini na glass kuvunjwa,nilipoingia ndani asubuhi wakati naenda kufunga mlango nikakuta vyombo vimetapakaa sebuleni hadi Jikoni kaka"

Ally Mpemba "Mtumeeeee!"

Aliendelea "Hiyo TV haijavunjwa kweli?"

Mimi "Hapana kaka,samani za ndani ziko vizuri,vyombo vyote ndo vimetapakaa ndani?"

Ally Mpemba "Umefunga mlango?"

Mimi "Ndiyo kaka nimefunga kama ulivyoniambia"

Ally Mpemba "Vyombo je umevipanga?"

Mimi "Hapana kaka sijagusa kitu maana hukunipa maelekezo mengine zaidi ya yale ya juzi"

Ally Mpemba "Bado uko hapo nyumbani?"

Mimi "Hapana kaka mimi nipo Kkoo"

Ally Mpemba "Ok nakuomba niuazime muda wako master na nitakufidia nikirudi,nakuomba uende sokoni ukanunue kabeji kubwa tano,nunua na mboga za majani kisha nenda nyumbani uingie jikoni ufungue kabati lililoko karibu na friji kwa chini utakuta kitambaa cheupe,hicho kitambaa katandike pale sebuleni juu la ile meza ya kioo na kisha weka hayo mahitaji utakayokuwa umenunua!"

Mimi "Sawa kaka hakuna tatizo"

Ally Mpemba "Nilisahau kukwambia nilivyoondoka,nisamehe sana kaka"

Mimi "Usijali kaka,hizo mboga za majani ni aina gani?"

Ally Mpemba "Nunua zozote kaka ila ziwe za kutosha"

Mimi "Sawa kaka usijali"

Ally Mpemba "Farah hajakuuliza kitu kuhusu mimi?"

Mimi "Hapana kaka,kwanza huwa sinaga stori na mtu kaka mwenyewe unanijua"

Ally Mpemba "Nitakulipa mambo makubwa master kwani wewe ni muaminifu sana,nashukuru sana kwa kuwa muaminifu kwangu?"

Mimi "Usijali kaka!"

Ally Mpemba "Ngoja nimpigie simu Farah kuna hela nimwambie akupe halafu mimi nitamrudishia"

Mimi "Sawa"

Niliamua kufunga na kurudisha meza kule ambapo mara zote nimekuwa nikihifahdi ninapomaliza kazi,sasa nikiwa njiani napeleka kuhifadhi vifaa vyangu vya kazi,Ally Mpemba alinipigia simu.

Ally Mpemba "Nimemwambia Farah akupe elfu 50,itumie hiyo kununua mahitaji hayo niliyokwambia"

Mimi "Sawa kaka Usijali"

Nilirudi hadi kwa Aunt Farah kuchukua kile kiasi cha fedha kisha nikaondoka kuelekea kununua yale mahitaji aliyokuwa ameniambia Ally Mpemba,baada ya kununua mahitaji yote muhimu kama alivyokuwa amenielekeza,nilipanda gari kuelekea Magomeni ambako ndiko alikokuwa akiishi Ally Mpemba,nilipofika nilianza kukusanya vyombo vyote vilivyokuwa chini na vile ambavyo vilikuwa vimepasuka niliamua kuvikusanya na kuviweka kwenye dust bin kule jikoni.

Baada ya kumaliza lile zoezi la kusafisha mle ndani, niliingia jikoni nikafungua ile kabati aliyokuwa amenielekeza jamaa kisha nikatoa kitamabaa cheupe nikaenda kukitandika kwenye ile meza kama alivyokuwa amenielekeza,nilipomaliza kukitandika kile kitambaa nilichukua zile kabeji kubwa 5 pamoja na yale mafungu ya mboga za majani nakiyaweka pale mezani, mboga za majani nilinunua za kutosha na nilinunua na aina karibia zote kasoro matembele!.

Baada ya kumaliza lile zoezi kwa kuwa ilikuwa mapema,niliondoka kuelekea Gongo la Mboto kuoga na kubadili nguo,nilipofika niliamua kulala kabisa kwasababu nilikuwa nina usingizi wa kufa mtu.

Ilipofika mida ya saa 11 jioni niliamua kuondoka kutembea mdogo mdogo hadi stendi ya Gongo la Mboto kisha nikapanda gari za Masaki ili nikashukie Magomeni kisha nielekea kwa Ally Mpemba.

Nilipofika nilifungua mlango nikaingia hadi ndani, sasa kwakuwa muda wa kufungua ule mlango ulikuwa bado kidogo, niliona niwashe Luninga ili niendelee kupoteza muda, sasa wakati nikiwa natazama luninga, kule kwenye kile chumba nikawa nasikia sauti yenye mtetemo.




.........................................................................................





Utajiri wa rafiki yangu ulivyofanya nikamuamini Shetani - 13.




Ile sauti ya mtetemo iliendelea sana kana kwamba hicho kitu kilichokuwa humo chumbani kilikuwa kimekasirishwa,nilisimama taratibu nikatembea kwa kunyata hadi kwenye mlango wa kile chumba,nilipofika kwakuwa muda wa kukifungua ulikuwa bado,nilitegea sikio kwa makini kusikiliza kilikuwa ni kitu gani,nilitulia kimya kabisa lakini ile sauti ya mtetemo ilikoma,niliamua tena kunyata na kurudi sebuleni.

Muda wa kufungua ule mlango ulipowadia nilinyanyuka na kwenda kuufungua,sasa nilipofungua ule mlango kama kawaida niliuacha wazi kisha nikawasha taa za nje nikatoka zangu ndani kuelekea nje.Siku hiyo sikutaka kabisa kutoka kwenda kula kwasababu nilikuwa nimekula muda siyo mrefu hivyo nikawa nimeshiba,kwakuwa bado ilikuwa mapema,niliona nifungue ile gari nikae ndani nitulie hadi nitakapopitiwa na usingizi,nilifungua vioo vya mbele vya ile gari upepo ukaanza kuingia ndani lakini nilipoona mbu wanazidi kuingia kwa kasi nilivifunga kisha nikawasha AC nikaendelea kula upepo.

Ilipofika mida ya saa 3 usiku kukiwa kumetulia,nilianza kusikia sauti ya kitu ambacho sikukielewa kilikuwa ni kitu gani kikiwa kinatafuna kwa sauti na miguno kama ya nguruwe,ile sauti ilikuwa inasikika kwa nguvu sana kiasi kwamba ikabidi nifungue mlango wa gari na kushuka,baada ya kutoka kwenye gari nilisimama kando ili niweze kuisikia ile sauti vizuri.Hali ile hakuna mwanadamu mwenye moyo ambaye asingeiogopa,mimi pamoja na ujasiri wangu wa kikurya lakini ilifika sehemu nikawa naogopa sana lakini niliendelea kuwa mvumilivu na kumdhibitishia Ally Mpemba ya kwamba mimi ni mwanaume na ni mwaminifu,hivyo mategemeo yangu yalikuwa ni ipo siku atanipa fedha au sehemu ya mali zake kutokana na uaminifu wangu kwake.

Ile sauti ilipozidi,nilisogea hadi pale mlangoni kwa kunyata kisha nikawa nasikiliza kilikuwa ni kiumbe wa aina gani aliyekuwa mle ndani,kiukweli ilikuwa ngumu kutambua kama alikuwa mwanadamu au mnyama,kwasababu nilichokuwa najiuliza,kama ni mwanadamu anawezaje kutafuna kwa kasi kiasi kile na miguno kama ya nguruwe?

Kwa watu mliofuga nguruwe au mlioishi na nguruwe nadhani hapa mtakuwa mnanielewa,kile kitu kilichokuwa humo ndani kilikuwa kinatafuna na kuguna kwa utamu kama nguruwe anapokuwa anakula.

Pia kama ni mnyama,Je alikuwa ni mnyama gani?,kiukweli niliendelea kujiuliza maswali mengi yasiyokuwa na majibu,niliona nijiondokee zangu nirudi kwenye gari kutulia,nilipitiwa na usingizi nikajikuta naamka saa 12 baada ya kusikia milio ya magari huko nje,niliamka haraka na kwenda kuufungua ule mlango na kuzama ndani,nilipofika ndani niliwasha taa za pale sebuleni na kukuta kile kitambaa kilichokuwa pale juu ya meza kimetupwa chini na nilipoangalia chini nikakuta kuna ute ute mzito kama ambao hutoa ng'ombe akiwa anatafuna nyasi,zile kabeji pamoja na mboga za majani sikuzikuta hata kipande tu,kiukweli niliingiwa na hofu sana na sikutaka kusubiri nilielekea moja kwa moja mpaka kwenye kile chumba na kukifunga.Nilipokifunga kile chumba angalau sasa moyo wangu ulitulia,niliingia jikoni nikachukua dekio (Mop) nikaenda kusafisha ule ute mzito kisha kile kitambaa nikakirudisha jikoni kama kawaida.

Baada ya kumaliza lile zoezi, nilitoka nje nikafunga mlango kisha kuelekea bombani kunawa,nilipomaliza kunawa uso na kusukutua nilirudi kwenye gari kusikilizia hadi mida ya saa 2 ili niondoke niingie Kkoo kufanya kazi yangu ya usajili.Baada ya muda kufika niliondoka nikaelekea Buguruni ofisini ambako vikao vilikuwa vinafanyika kila siku na ilikuwa ni lazima kuhudhuria,baada ya kumaliza kikao nilichukua box la line kisha nikaondoka zangu Kkoo,sasa wakati nipo kariakoo napiga kazi,Ally Mpemba alinipigia simu na kutaka nimpatie taarifa za usiku.

Ally Mpemba "Assalam aleykum"

Mimi "Alekom salam "

Ally Mpemba "Wajionaje na hali?"

Mimi "Niko vema kabisa kaka"

Ally Mpemba "Mambo yalienda vyema?"

Mimi "Ndiyo kaka hakuna kilichoharibika"

Ally Mpemba "Hakukuwa na usumbufu kama wa jana?"

Mimi "Hapana kaka"

Nilitaka nimuulize jamaa ni kitu gani kilikuwa mle ndani lakini nilikuwa nasita sana na niliona ningemuuliza uenda ningeharibu uhusiano wetu ambao tayari ushaanza kuwa mkubwa,niliamua nipige kimya ili mambo mengine mazuri yaliyokuwa mbele yangu nisiyazibe.

Ally Mpemba "Sasa utamwambia Farah akupe elfu 50 na utafanya kama ambavyo ulifanya jana"

Mimi "Sawa kaka"

Baada ya mazungumzo jamaa akawa amekata ile simu.Ilipofika mida ya saa 10 Alasiri,niliamua nifunge nirudishe vifaa vyangu vya kazi mahali ambapo nimekuwa nikivihifadhi,nilirudi hadi dukani pale nikamwambia yule sister Farah anipatie kiasi cha fedha kama ambavyo Ally Mpemba alikuwa ameniambia.

Farah "Mbona sikuhizi wawahi sana kufunga!"

Mimi "Hata muda wa usajili umebaki mchache na kuna mahali inabidi niwahi"

Farah "Ooh ok nambie"

Mimi "Brother Ally aliniambia unipatie elfu 50"

Farah "Ally kaka yangu au Ally yupi!?"

Mimi "Yes, brother Ally"

Farah "Mbona hajaniambia "

Aliendelea "Ngoja nimtafute nithibitishe"

Baada ya kumpigia Ally Mpemba na kumpata hewani walikuwa wakiongea lakini yule demu nikama alikuwa akimuuliza Ally mimi na yeye tunabiashara gani kwasababu jana alitoa elfu 50 akanipa na leo tena anatoa elfu 50 kunipatia,sikujua Ally Mpemba alimjibu kitu gani,alichukua elfu 50 akanipatia kisha mimi nikaondoka kuelekea sokoni kununua bidhaa kama ambazo nilinunua jana,maelekezo yalikuwa ni yale yale.

Kiukweli kwa muda huo nilikuwa napata sana hela kwasababu kununua mahitaji yote yale nilikuwa natumia chini ya elfu 20 na elfu 30 iliyokuwa inabaki ilikuwa yangu na Ally Mpemba hakuwahi kuiulizia kabisa,kila siku nilikuwa napewa elfu 50 kwa ajili ya manunuzi.

Kama kawaida niponunua bidhaa nilirudi hadi nyumbani Kwa Ally Mpemba na kuyaweka kama ambavyo nilikuwa nimeelekezwa.Ilipofika jioni muda wa kufungua kile chumba,niliamua kufungua pazia la pale sebuleni kisha nikawasha taa,lengo langu ilikuwa ni kuhakikisha siku hiyo nakiona kile kiumbe ambacho sikukifahamu kilikuwa kiumbe cha aina gani!;baada ya kufungua pazia na kuwasha taa,nilienda kuufungua ule mlango na kuacha wazi kisha nikatoka nje.

Niliamua kukaa kando ya lile dirisha la pale sebuleni huku nikiwa na shauku kubwa ya kuona ni kitu gani kilikuwa mle ndani,ilipofika mida ya saa 2 usiku,nilitoka nje nikaelekea kununua chips na soda kisha nikawahi kurudi, nilipofika breki ya kwanza ilikuwa ni kwenye dirisha la pale sebuleni,niliangalia kwa umakini na ndipo niliona zile kabeji na mboga za majani uilikuwa hazijaliwa,hivyo nikaa pale pembeni nikaanza kula huku nikisubiri nione ni kitu gani kilikuwa mle ndani.

Nilikaa sana pale chini hadi mida ya saa 5 usiku lakini kila nikichungulia hakukuwa na dalili ya kitu chochote, niliamua kufungua mlango na kisha kuingia ndani ili nikafunge yale mapazia na kuzima taa,nilipomaliza nilitoka nje kisha nikakaa pale mlangoni na kusikiliza,ndipo haukupita muda nikaanza kusikia utafunaji wa ovyo na papara ukiendelea kama kawaida,niliondoka nikaingia kwenye gari kwenda kulala kama kawaida huku kile kiumbe kikiendelea na utafunaji wake wa sauti kama nguruwe.

Asubuhi kama kawaida niliingia ndani nikafunga ule mlango kisha nikaanza kufanya usafi pale sebuleni kama kawaida,nilipomaliza niliondoka kuelekea kazini kama kawaida.

Sasa ilipofika mida ya saa 3 asubuhi nikiwa tu ndo nimeanza kazi,alinipigia simu Ally Mpemba.

Ally Mpemba "Kaka salama?"

Mimi "Salama kabisa,vipi wewe huko?"

Ally Mpemba "Huku naendelea vema ila narudi wiki ijayo"

Mimi "Sawa kaka,nambie"

Ally Mpemba "Kuna mtu nimempa namba yako atakupigia simu ana mzigo wangu utaenda atakupatia"

Mimi "Sawa kaka ni mzigo gani?"

Ally Mpemba "Ni pesa,hakikisha akikupatia utanipelekea Benki Crdb,nitakutumia vielelezo"

Mimi "Sawa kaka hakuna tatizo"

Ally Mpemba "Pia nimemwambia Farah kuna pesa atakupatia,utachukua utanunua mahitaji yale kama kawaida na itakayobaki utatumia "

Mimi "Nashukuru sana Kaka Ally"

Ally Mpemba "wala huna haja ya kunishukuru, mimi ndiye ninapaswa kukushukuru "

Aliendelea "Nitakufanyia mambo makubwa sana kwa uaminifu wako"

Mimi "Sawa kaka nitashukuru sana"

Baada ya mazungumzo yale mafupi Ally Mpemba akawa amekata simu.

Ilipofika mida ya saa 7 mchana,kuna namba ngeni ikawa imenipigia simu,ilikuwa ni sauti ya mwanamke ambaye alijitambulisha kama Warda.

Mimi "Ndiye mimi"

Warda "Ally kaniambia kuna mzigo wake nikupatie,sijui nakupataje?"

Mimi "Wewe uko wapi?"

Warda "Njoo hapa mtaa wa mkunguni ukifika uniambie"

Mimi "Sawa nakuja muda si mrefu"

Mimi "Aunt Farah samahani naomba unitazamie hapo narudi mara moja"

Farah "Kwani ndo unafunga?"

Mimi "Hapana,kuna mahali nafika mara moja ila nawahi kurudi"

Farah "Ooh sawa kuna hela Ally ameniambia nikupatie,hivyo ukitaka kuondoka utaniambia"

Mimi "Sawa nawahi kurudi"




.......................................................................................




Utajiri wa rafiki yangu ulivyofanya nikamuamini Shetani - 14.



Mimi "Nishafika"

Warda "Umesimama wapi?"

Aliendelea "Ooh ok nishakuona"

Baaada ya nusu dakika alikuja mwanamke mmoja mwenye asili ya uarabuni akiwa amevaa hijab nyeusi ikiwa imempendeza sana kutokana na rangi ya ngozi yake.

Warda "Bila shaka wewe ndiye uliyetumwa na Ally"

Mimi "Yes ndiye mimi "

Warda "Unaitwa nani?"

Mimi "Naitwa Umughaka"

Warda "Mhh mbona Ally hakunitajia jina hilo!"

Mimi "Kaka Ally amezoea kuniita Master,Umughaka ndiyo jina langu halisi"

Warda "Ooh sawa nimekuelewa"

Aliendelea "Ngoja kwanza nimpigie simu halafu nikupe uongee nae"

Alichukua simu yake akaanza kumpigia simu Ally Mpemba na wakaanza kuongea,baada ya kuongea akanipatia na mimi simu ili niongee na Ally,baada ya kujiridhisha aliniambia nifuatane nae.Tulitembea kama hatua kumi kisha tukaingia kwenye nyumba moja ambayo ilikuwa ni ghorofa,ile ghorofa ilikuwa ni Apartment ya watu kuishi na haikuwa kwa ajili ya ofisi.

Baada ya kufika ndani tuliingia kwenye lift nikaona yule dada anabonyeza batani ambayo ilionyesha namba 4,ile lift iling'oa nanga na baada ya sekunde kadhaa tukawa tumefika kwenye floor namba 4,tulipofika tulitembea hatua 3 tukawa tumefika kwenye chumba ambacho baada ya kukifungua tuliingia ndani.

Warda "Nisubiri hapo "

Aliingia chumbani ambako hakutumia muda mwingi akawa ametoka na pochi kubwa ambayo ilikuwa imetuna.

Warda "Hizi ni pesa ambazo Ally amesema nikukabidhi sasa kabla ya kuondoka inapaswa uzihesabu ndipo uondoke"

Alizitoa zile hela kwenye ile pochi kubwa ya kike,kiukweli zilikuwa ni pesa nyingi sana.Nilianza kuzihesabu na kuzipanga ndipo nilipata jumla yake milioni 40.Wakati nazihesabu alikuwa amekaa akiniangalia huku akiendelea kuchezea simu yake.

Mimi "Tayari"

Warda "Umepata bei gani?"

Mimi "Milioni 40"

Warda "Ok uko makini"

Alichukua karatasi pamoja na wino akawa ameweka pale juu ya meza na kuniambia.

Warda "Shika hii"

Aliendelea "Utasaini hapa na hapo chini utaweka dole gumba "

Basi nikafanya kama alivyoniambia na nilipomaliza alichukua simu yake kisha akampigia simu Ally Mpemba.

Warda "Haya nishamkabidhi pesa yako,huyu hapa ongea nae"

Ally Mpemba "Master,huo mzigo nenda kaniwekee benki,nakutumia sasa hivi vielelezo"

Mimi "Sawa kaka"

Warda "Ngoja nikupatie kibegi kidogo,huo mkoba nina kazi nao"

Sasa baada ya kupewa kibegi kidogo,niliziweka zile hela kwenye kile kibegi huku akili yangu ikiwa imechanganyikiwa kabisa,nilipanga nitoroke na zile hela,baada ya kushuka ghorofani nilianza kutembea mdogo mdogo kuelekea mnazi mmoja.

Nilikuwa najisemea uenda ndiyo wakati ambao Mungu aliamua kunitoa kwenye umasikini kupitia zile hela za Ally Mpemba kwa maana hata kama ningeondoka zangu kurudi Mwanza asingepata kwasababu ni mtu tu ambaye nilikutana nae kkoo na halikuwa hanijui kiundani wala haifahamu familia yangu,kiukweli nilikuwa kwenye vita nzito kuhusu zile fedha lakini niliamua nizipelekea Benki ili kuendelea kuonyesha uaminifu wangu kwa Ally,nilisema kama ni umasikini niliandikiwa basi ningekufa masikini tu hata kama ningekimbia na zile hela,pengine ni heri kufa masikini kuliko kuiba cha mtu ambaye ufahamu kakipata vipi,Uaminifu kwangu hata kama usingenilipa lakini ungenijengea heshima kubwa miongoni mwa marafiki na watu wa karibu,hivyo niliamua kuwa muaminifu ingawa nilikuwa nahitaji sana fedha.

Nilitembea kwa haraka sana hadi katikati ya jiji mtaa wa Azikiwe ambapo kwa mujibu wa maelekezo ya Ally Mpemba ilipaswa niende hapo ilipo benki ya Crdb kuziweka hizo fedha.

Baada ya kumaliza kila kitu pale benki,niliondoka zangu kurudi kkoo,nilipofika kwakuwa muda nao ulikuwa umeenda sana,nilimwambia Aunt Farah anipatie kile kiasi ambacho aliambiwa na Ally anipatie ili niondoke zangu kununua mahitaji ya siku hiyo kisha niondoke nikaandae mapema.

Aunt Farah alinikabidhi laki tatu ambazo kwa mujibu wa maelekezo ya Ally Mpemba ni kwamba,laki mbili ningeitumia kwa mahitaji ya vitu kwa siku zilizokuwa zimebaki hadi yeye kurudi na ile laki moja ingekuwa kwa ajili ya matumizi yangu ya kawaida.

Kweli,ile kazi niliifanya kwa uaminifu mkubwa mno hadi siku ambayo alirudi Ally mpemba alikuwa akinishangaa namna nilivyokuwa muaminifu kiasi kile na sikuwahi kumwambia mtu yeyote siri ile.

Ally Mpemba "Kaka kati ya watu na wewe ni mtu!"

Mimi "Kwanini kaka?"

Ally Mpemba "Ndugu zangu si waaminifu kama wewe ulivyo muaminifu"

Aliendelea " Sielewi hata nitakulipa nini!"

Mimi "Usijali kaka haya ni maisha tu!"

Kiukweli nilikuwa najiuliza mle ndani kwa Ally kulikuwa na kitu gani lakini nilikuwa nakosa jibu kwasababu ndani ya siku zote hizo nimekuwa nikiwinda nipate kukiona lakini nilikuwa naishia kusikia sauti tu,mimi sikutaka kuonyesha kama nina wasiwasi,nilichofanya ni kwamba nikiwa nazungumza nae yeye aelewe mimi sifahamu chochote na nilikuwa napotezea mambo mengine ili asije kunoti kitu kutoka kwangu.

Niendelea kupiga kazi yangu ya usajili wa line za simu huku na ile kazi ya usimamizi wa Catering ikiendelea,kiukweli kama kuna muda ambao nilitengeneza pesa ilikuwa ni kipindi hicho,baada ya kupata pesa ya kutosha,nilimtafuta dalali akanitafutia uwanja maeneo ya Chanika Zingiziwa chenye ukubwa wa 25 x 20 nikawa nimenunua Milioni 3.

Nikawa nimepanga nipambane sana ili nikusanye fedha nyinngine nianze ujenzi mdogo mdogo ili nitoke kwenye nyumba za kupanga na mimi niamie kwangu.

Kuna siku tulipata tenda ya kuhudumia chakula maeneo ya Mikocheni,sasa Ally akawa ameniambia siku iliyokuwa inafuata nisiingie kazini ili niende kuwasimamia wale kina mama na vijana kama kawaida yangu maana ndiyo ilikuwa kazi yangu,kiukweli Ally alikuwa akiniamini sana na ilifika kipindi fedha zake zote mimi ndiye nilikuwa nikizipeleka benki,mkurya mimi nikajiona ni mtu mwenye bahati ya kuaminika na na mtu mwenye asili ya uarabu kuliko wakurya wote kutoka Tarime;kweli,siku iliyofuata sikwenda kazini kama kawaida na nilimpigia simu Team leader wangu nikampanga kabisa ili asije akaona baada ya kushika shika vihela nimeanza kuwa na kiburi.

Baada ya maandalizi mimi na timu yangu ya Catering,tukawa tumefika maeneo ya mikocheni kama kawaida,tuliendelea na maandalizi hadi kuhakikisha vitu vyote viko sawa,sasa tukiwa kwenye hiyo shughuli mida ya 2 usiku, Ally akanipigia simu akiwa na kiwewe kisichokuwa cha kawaida.

Ally Mpemba "Master hebu fanya haraka njoo hapa Sinza Mori"

Mimi "Kaka Sinza Mori sipafahamu"

Ally Mpemba "Hebu mpelekee Jabir simu niongee nae"

Baada ya kumpa Jabir simu na kuzungumza nae inaonekana alimwambia Jabir anitafutie muda ule Taxi na akamuelekeza eneo ambalo ningemkuta,sasa baada ya kupata Taxi,Jabir alimpatia maelekezo yule dereva kisha akaniambia niingie kwenye gari tuondoke.

Tulipofika hilo eneo ambalo ambalo Ally alikuwa amesema nimkute pale,nilimpigia simu akaniambia niingie ndani,ilikuwa ni hotel kubwa tu ambayo pia ilikuwa ni bar,nilipoingia ndani nilimkuta jamaa yupo na watu kadhaa wakiwemo mademu wenye asili kama yake wakila na kunywa.

Ally Mpemba "Kaka kanisaidie kufungua chumba,siunajua nimejisahau "

Aliendelea "Aiseee yaani hata sielewi nimejisahau vipi!"

Mimi "Sawa kaka ngoja sasa niwahi!"

Ally Mpemba "Ukishafungua utanirudishia hapa funguo utanikuta hapa hapa "

Mimi "Sawa kaka"

Niliondoka kuelekea kwenye Taxi tukaondoka zetu kuelekea Magomeni,nilipofika nilimwambia dereva Taxi anisubili nje ya geti.Nilifungua mlango kisha nikaingia ndani nikawasha taa,sasa nilipowasha taa sikuona kitambaa cheupe pale kwenye ile meza ya kioo ndipo nilielekea jikoni kwenye kabati nikakikuta ikabidi niende nikitandike kisha nikachukua kabeji na mboga mboga nikaziweka juu ya ile meza,baada ya kumaliza niliondoka zangu nikaenda kufungua ule mlango wa kile chumba.

Sasa nilipomaliza kuufungua ule mlango nikiwa nimegeuza mgongo naondoka ili nitoke ndani nifunge mlango niondoke,aisee nilisikia nimesukumwa na nguvu isiyokuwa ya kawaida,ile nataka kuanguka chini nilimuona kiumbe wa ajabu ananipita kwa kasi ya ajabu akiwa uchi kama alivyozaliwa akikimbilia sebuleni na kuanza kuyafakamia yale makabeji kwa spidi kali mno,nilipokuwa bado naendelea kushangaa na kuhamaki yeye hakuwa kabisa na muda na mimi.

Ndipo nilimshuhudia mwanamke aliyekuwa na asili ya kiarabu lakini akiwa na manywele mengi si kichwani tu hadi kwenye makwapa na sehemu za siri,alikuwa anatoa harufu kali sana ambayo haikuwa ya kawaida. Niliogopa sana na ikabidi nikimbilie nje na kufunga mlango kisha nikaelekea kwenye lile bomba la nje kunawa, baada ya kumaliza kunawa nikatoka nje nikafunga geti nikapanda Taxi kurudi Sinza kumrudishia jamaa funguo, kiukweli roho ilichafukwa sana na niliogopa sana na hata ujasiri niliokuwa nao wote uliyeyuka.

Huruma, majuto na masikitiko vyote kwa pamoja vilinisumbua sana kwa usiku ule; Sasa wakati nikiwa kwenye gari narudi Sinza, Ally Mpemba alinipigia simu akiwa kama mtu aliyepagawa.




........................................................................................





Utajiri wa rafiki yangu ulivyofanya nikamuamini Shetani - 15.




Ally Mpemba "Kaka ...kaka....umefanya nini! Kaka!?"

Mimi "Kuna nini kaka Ally?"

Ally Mpemba "Kaka unataka kuniua?"

Mimi "Kaka Ally uko poa kweli?"

Basi jamaa alianza kulia kwa kwikwi kitu ambacho kilikuwa kikinichanganya zaidi, sikuelewa kama yale maneno aliyokuwa akiniambia yalikuwa ya kwangu au labda kuna mtu alikuwa akimpigia simu bahati mbaya ikaja kwangu!. Nilipofika lile eneo ambalo nilimuacha Ally Mpemba akiwa na rafiki zake sikumkuta hivyo ikabidi nimpigie simu.

Mimi "Kaka nimerudi na sikuoni hapa!"

Ally Mpemba "Nisubiri hapo hapo narudi muda huu"

Haikupita hata dakika 20 jamaa akawa amefika pale akamlipa yule dereva taxi kisha akaniambia niingie kwenye gari yake tuondoke. Wakati tukiwa kwenye gari jamaa alionekana kana kwamba amechukia sana na sikuelewa kilichokuwa kimemchukiza ni kitu gani.

Ally Mpemba "Daah ndugu yangu nilikwambia ufike ufungue tu chumba uondoke sasa wewe umefanya nini?"

Mimi "Kaka nilipofungua chumba ile natoka nielekee nje ndipo yule kiumbe akanipita akikimbilia sebuleni"

Ally Mpemba "Kaka ushaharibu"

Kwa namna ambavyo jamaa alikuwa amechukia niliamua kukaa kimya ili nione atafanya kitu gani, sikutaka kabisa kumuongelesha kwa wakati ule maana niliona ningeendelea kumuudhi, sasa kumbe kile kitendo cha mimi kumuona yule kiumbe wa ajabu kilimshtua Ally Mpemba kule alikokuwa na sikuelewa alijuaje, kiukweli nilibaki na maswali mengi sana ambayo hayakuwa na majibu; Kwakuwa nishakuwa mtu mzima tayari, niliamini hata fedha alizokuwa nazo Ally Mpemba zilikuwa na msukumo wa ushirikina ndani yake, kiukweli niliamua kukaa kimya ili nione ataniambia nini!.

Tulivyofika nyumbani mida ya 4 usiku, nilishuka kwenye gari nikafungua geti kisha jamaa akaingiza gari ndani na kuipaki, alishuka haraka haraka akaniambia hebu njoo ndani, alivyofungua mlango na kuzama ndani tukakuta yule kiumbe amekula kila kitu kilichokuwa pale kwenye meza kama kawaida, sasa Ally Mpemba akaniambia nitoe kile kitambaa nikipeleke jikoni kisha nimsaidie kusafisha pale sebuleni, yeye aliingia chumbani ambako alikaa kwa muda kama wa dakika 5 kisha akawa amerudi pale sebuleni akiwa amevaa kanzu nyeupe akiwa amejifunga na kitambaa, mkononi akiwa ameshika kanzu nyingine nyeupe akanitaka niivae.

Ally Mpemba "Vaa hii tafadhali!"

Mimi "Nivae juu ya nguo zangu hizi?"

Ally Mpemba "wewe vaa hivyo hivyo tu!"

Baada ya kuvaa ike kanzu ambayo ilikuwa ikinukia manukato mazuri, alichukua kitambaa cheupe kama alichokuwa amejifunga kichwani akanifunga na mimi!. Kimuonekano tulifanana kama wale jamaa wa dubai au saudia wanaovaa kanzu na vilemba.
Aliisogeza ile meza ya kioo pembeni kisha akatandika nguo ngumu kama kikoi kisha akanitaka nimsogelee.

Ally Mpemba "Wewe ni rafiki yangu na ninakuamini sana, tafadhali nisaidie!"

Mimi "Nikusaidie nini kaka?"

Ally Mpemba "Nifuate nitakavyokuelekeza"

Mimi "Sawa kaka"

Ally Mpemba alikuwa akitamka maneno ya kiarabu ambayo alinitaka na mimi nimfuatishe, alikuwa akitamka huku tukiwa tumekaa chini ya kile kikoi, baada ya kufanya lile zoezi kwa kurudia rudia kwa muda wa nusu saa tukawa tumemaliza na kisha akatoa kile kikoi akawa amekirudisha chumbani kwake. Aliporudi tena pale sebuleni aliniambia nikae kwenye sofa nami nikaa!.

Ally Mpemba "Kaka naomba ulichokiona ibaki siri yako!"

Aliendelea "Hakuna mtu yeyote anayejua hili jambo isipokuwa wewe"

Mimi "Usijali kaka haya ni maisha tu!"

Ally Mpemba "Mimi nilikuchukua wewe unisaidie mambo yangu kwakuwa wewe una mkondo wa hela"

Aliendelea "Na umekuwa muaminifu nahitaji kukufikisha mbali zaidi!"

Aliendelea "Huyo uliyemuona siyo kiumbe wa ajabu bali huyo ndiye anayenipatia hela na mali hizi unazoziona"

Aliendelea "Siyo mkorofi na akikupenda utamfurahia, huwezi kujiuliza kwanini wewe ndiye nilitaka uwe karibu na mimi?"

Wakati ananiambia mambo yote hayo mimi nilikuwa nimetulia tu nikimuangalia huku nikitikisa kichwa cha kuonyesha ukubali kwenye maswali aliyotaka ukubali wangu.

Ally Mpemba "Wewe una nyota ya utajiri master labda uichezee mwenyewe!"

Mimi "Kweli kaka!?"

Ally Mpemba "Una nyota ya pesa ambayo pesa ikija kwako haitoki labda uitoe mwenyewe au mtu akuchukue uwe unamzalishia pesa!"

Aliendelea "Kaka mjini hapa, ukifa masikini shauri yako, mimi nakushauri kama rafiki yako"

Mimi "Kaka kuna mtu anapenda umasikini? Nahangaika juani ili nipate pesa kaka"

Ally Mpemba "Pesa unatembea nayo nyuma yako harafu unasema unahangaika juani! Watu wa bara hamjuagi kuchangamka!"

Mimi "Kaka nielekeze namna ya kufanya"

Ally Mpemba "Wewe una kifua? Siyo unapenda kupanda tu kwenye Range ukadhani mambo ni mepesi"

Mimi "Kaka kama nimewahi kushika bunduki hakuna jambo litakalonishinda"

Ally Mpemba "Bunduki mwatumia huko bara, hapa mjini twatumia kisomo tu mambo yajipa!"

Aliendelea "Hebu simama unifuate"

Nilisimama nikamfuata Ally Mpemba kisha tukaingia kwenye kile chumba kilichokuwa na yule kiumbe wa ajabu, baada ya kuingia ndani aliwasha taa akasogea mpaka kwenye kabati la ukutani kisha akalifungua, alipolifungua akaanza kuita kwa sauti.

Ally Mpemba "Mayaaa"

Aliendelea "Wewe Maya toka nje nakuita"

Alipokuwa akiita yule kiumbe akawa anaunguruma kwa mtetemo, kiukweli nilisogea nyuma kwa hofu maana haikuwa hali ya kawaida na sikuelewa siku zote jamaa alikuwa akiishi vipi mle ndani peke yake na yule kiumbe bila ndugu zake kujua jambo lolote!.

Baada ya kuita hilo jina la Maya kwa muda kadhaa, yule kiumbe wa ajabu alitoka na alipotoka alipomuona jamaa alimuinamia kama kumsujudu, kiukweli kilikuwa ni kitendo kilichonishangaza sana kwasababu Ally Mpemba kila alichokuwa akimwambia yule kiumbe alionekana kuelewa na kuogopa. Ally Mpemba kuna lugha aliongea nae kisha yule kiumbe aliyekuwa akitoa harufu ya ajabu aliondoka akarudi kwenye lile kabati kisha Ally Mpemba akarudishia lile kabati.

Kumbe kwenye lile kabati kulikuwa kumechimbwa shimo kama la futi sita na ndipo yule kiume alikuwa akikaa, sasa kama ulikuwa ukifungua ile kabati ilikuwa ngumu kumuona kwasababu alikuwa akiingia kwenye lile shimo kulikuwa na ubao ambao ulikuwa ukifunika na hivyo siyo rahisi mtu wa kawaida hata kama ingetokea kuingia mle chumbani kujua kama kulikuwa na mtu mle ndani labda kama ikitokea umeingia yule kiumbe aanze kuunguruma!.

Mimi "Kaka huyu ni nani kwani?"

Ally Mpemba "Nishakwambia huyo ndiye kila kitu kwangu sheikh"

Aliendelea "Watu wa Bara hapa mjini mmekuja kuwashangaa watu"

Aliendelea "Au nawe unataka kuwa msindikizaji?"

Mimi "Hapana kaka"

Ally Mpemba "Kwanza kabla ya kukusaidia inapaswa uslim"

Mimi "Kuslim tu kaka, mbona haina shida hiyo"

Ally Mpemba "Usiseme haina tatizo, usijedhani ni kuslim kama unavyodhani weye!"

Ally Mpemba "Mtu wa kukusilimisha apatikana hapo chumbe"

Aliendelea "Uko tayari mi nimuandae?"

Mimi "Mimi nipo tayari kaka"

Aliendelea "Sawa lakini haya yote uliyoyaona humu ndani yabaki humu humu ndani, utanichukiza sana nikiyasikia sehemu na walahi sitokuacha salama"

Baada ya maneno hayo nilianza kuingiwa uoga na hofu ya ajabu,kiukweli sikujua ni kitu gani kilichokuwa kinanitia hofu muda huo lakini nachokumbuka ni kwamba niliingiwa na hofu. Sasa baada ya majadiliano yale, Ally Mpemba alinipatia funguo za gari ile Aud akanitaka nikalale, sikufahamu ni kwanini vile vyumba vingine ambavyo vilikuwa vimefungwa hakutaka nilale huko hadi aniambie nikalale kwenye gari nje, kiukweli kwa maisha jamaa aliyokuwa akiyaishi ilifika sehemu na mimi nikazamani kuwa kama yeye.

Marafiki muda mwingine hutushawishi hadi kujikuta tunaangukia kwenye maisha mabaya kuliko hapo mwanzo, mimi baada ya kufahamiana na Ally Mpemba nilidhani huenda maisha yangu yangekuwa mazuri kumbe haikuwa kama nilivyodhani, ilifika sehemu nikaacha kazi yangu ya usajili wa line iliyokuwa ikinipatia fedha halali na kudandia maisha ambayo baadae niliyaona ni kero na yenye majuto.

Kiukweli ilifikia hata kazi niliyokuwa nikiifanya niliiona ya kipumbavu baada ya Ally Mpemba kuwa ananipatia fedha nyingi za bure bure ambazo nilizifurahia bila kujua kuna siku zingenigharimu. Tangu nimemfahamu Ally Mpemba na pamoja na yeye kuwa rafiki yangu, sikuwahi hata siku moja kulala kwenye ile nyumba yake na yeye mwenyewe hakuruhusu mimi kulala mle ndani.

Baada ya wiki kama mbili tulijiandaa na jamaa akawa mwenyeji wangu kuelekea kisiwa cha Chumbe Unguja.





........................................................................................





Utajiri wa rafiki yangu ulivyofanya nikamuamini Shetani - 16.



Ukiachilia mbali kile kivuko cha Kigongo - Busisi pamoja na kupanda ile mitumbwi ya shemeji yangu(masamaki) kule kisiwani Ijinga sikuwahi kabisa kupanda Boti ya kisasa, hiyo ndiyo ilikuwa mara yangu ya Kwanza kupanda ile boti nzuri na ya kisasa.

Sababu za mimi na Ally Mpemba kwenda Chumbe zilikuwa mbili, moja; Ni kwamba baada ya mimi kumshuhudia yule kiumbe wa ajabu mle ndani, Ally Mpemba kuna miiko aliivunja kutokana na maelekezo ya mtaalamu wake, hivyo tulienda ili akaone namna ya kurekebisha kabla mambo hayajaharibika, pili; ilikuwa ni mimi kuzitaka mali baada ya ushawishi wa Ally Mpemba, sasa ilifika hatua na mimi nikashawishika na kuona ile kazi yangu ya usajili wa line ilikuwa ikinipotezea muda tu.

Baada ya kufika Unguja hatukutaka kupoteza muda, Ally Mpemba aliniongoza hadi kwa huyo mtaalamu aliyekuwa akimfahamu hapo Chumbe, mawazo yangu nilidhani huenda huyo jamaa angekuwa na makolo kolo kama ambavyo nilizoea kuwaona wataalamu wengi wa mikoani namna wanavyokuwa, ila yeye alikuwa kawaida tu!. Baada ya kufika kwa huyo mtu hatukumkuta na tulimkuta mwanamke aliyekuwa amevaa hijab akamwambia Ally Mpemba kwamba ameenda kuswali na tulichofanya tuliamua kumsubiri pale kwake.

Aliporejea kutoka kuswali alitukuta tukiwa tumekaa kwenye mkeka tukimsubiri, baada ya kumuona Ally Mpemba walisalimiana na mimi pia nikamsalimu. Alimuita Ally Mpemba akamwambia aingie ndani, baada ya mazungumzo ya takribani nusu saa, Ally Mpemba alirudi nje akiwa amebeba Vitu ambavyo sikuvielewa na akanitaka tuongozane nae. Nilimfuata nyuma Ally Mpemba hadi tukaifikia miti pori iliyokuwa kando ya Bahari. Nyuma yetu pia alikuwa akija yule mzee aliyekuwa amevaa kanzu huku mkononi akiwa amebeba Mkeka na vitu vingine, baada ya kufika eneo ambalo yeye aliona ndipo panafaa, alituambia tuvue nguo.

Mzee "Vua nguo zenu"

Mimi na Ally Mpemba tulivua nguo tukabaki kama tulilivyozaliwa, baada ya hapo alinikabidhi kichupa kidogo ambacho kilikuwa cha Gliselin, sasa kile kichupa ndani yake hakukuwa na Gliselin bali kilikuwa na kitu kama damu, baada ya kukipokea akanikabidhi na bangili la chuma(Hili huwa wanapenda kulivaa watu mbalimbali mikononi). Sasa baada ya kukabidhiwa hivyo vitu alitutaka tukae chini kwenye ule mkeka, alitoa kopo kama chetezo kisha akaweka vitu kama tumbaku iliyokauka, baada ya kuona imeenea kwenye kile chombo akatoa kiberiti akawasha, baada ya kuwasha akaanza kuongea kwa kiarabu huku akiwa anatikisa mgongo kwa kwenda mbele na kurudi nyuma. Baada ya kuwasha kile chombo kulikuwa na harufu nzuri sana kama udi lakini yenyewe ilikuwa nzuri zaidi ya udi.

Alipomaliza kusoma kisomo aliniambia nisimame.

Mzee "Waiyona ile bahari?"

Mimi "Ndiyo naiona"

Mzee "Weye nenda pale, ukifika pale chukua hicho kikopo mwaga Baharini ukimaliza chota maji na hicho kikopo uyalete hapa"

Kweli niliondoka zangu kushuka baharini huku nikiwa mtupu kama nilivyozaliwa,yale maeneo hakukuwa na watu kabisa na kulikuwa na miti ambayo isingekuwa rahisi watu kuona mnafanya kitu gani,sikufahamu kama mara zote Ally Mpemba alikuwa akija Unguja analetwa hilo eneo au siku hiyo tulipelekwa tu kwa kazi maalumu.

Nilipofika lile eneo la wazi la bahari nilifanya kama mzee alivyoniambia kisha nikageuza kurudi,nilipofika nilikuta Ally Mpemba akiwa amelazwa kwenye ule mkeka akiwa anapakwa mafuta ambayo sikuyafahamu mgongoni hadi miguuni,sasa alipomaliza ile shughuli kwa Ally Mpemba akaniambia nikae chini kwenye ule mkeka.

Mzee "Sogea kaa hapa"

Baada ya kukaa kwenye ule mkeka akachukua kale kakopo ka Gliselin nilikokuwa nimeweka maji ya bahari akamimina yale maji kwenye chombo kidogo cha udongo kilichokuwa kama chungu lakini kilikuwa kidogo kisha akaanza kuchanganya kwa ndani na mikono,baada ya kumaliza akaanza visomo kwa lugha ya kiarabu,sikuelewa alichokuwa anamaanisha ni kitu gani,sasa baada ya kumaliza akachukua lile bangiri ambalo alikuwa amenipatia mwanzo kisha akalichovya kwenye ule mchaganyiko na kunitaka nivae.

Sasa baada ya kuvaa lile bangili nikasikia limenibana mkono mithiri ya mtu kama kafungwa na waya mikononi, cha ajabu nikaanza kuona damu zinatiririka mkononi, damu zilipoanza kutitirika mkononi akachukua kile chombo kilichokuwa kama chungu akawa anazikinga matone yale yaliyokuwa yakidondoka.

Mzee "Unahisi maumivu?"

Mimi "Hapana"

Mzee "Ukihisi maumivu niambie"

Ile damu iliendelea kutoka kwa mfululizo pasipo kukoma ndipo nikaanza kuhisi maumivu mkononi nikamwambia yule mzee!. Baada tu ya kumwambia nahisi maumivu, alinishika akaanza kuongea maneno yaleyale kisha ile bangili ikalegea na damu zikakoma kutoka. Alichukua kile chombo kilichokuwa kama chungu akakisogeza pembeni kisha akaniambia mimi na Ally tukae chini.

Mzee "Alfwat amekubali toba ya ndugu yako"

Aliendelea "Hakikisha hii hali haijirudii tena na nitamfungamanisha na Alfwat kama ulivyonieleza na atamsaidia kama anavyokusaidia wewe"

Basi baada ya maelezo hayo mafupi, alichukua ile bangili ikiyokuwa imechovya kwenye damu pamoja na mchanganyiko wa dawa kisha akanitaka niivae.

Mzee "Hakikisha hii hauivui mkononi na kama ukipata tatizo inapaswa Ally Mpemba akulete kwangu!"

Mzee "Alfwat amekupenda na nilimueleza hilo suala ndugu yako hapa, unachopaswa kufanya ni kumtunza"

Aliendelea "Kwa ulichokifanya kama asingekuwa amekupenda kitendo cha kumvaa mkononi angekumaliza"

Aliendelea "Jambo la kwanza, inapaswa umvae huyu Alfwat na popote uendapo hakikisha unakuwa nae usimuache na kama nilivyokwambia kukiwa na tatizo utamwambia huyu bwana akulete, usithubutu kukanyaga huku ukiwa mwenyewe"

Mzee "Jambo la pili, hakikisha kila itakapokuwa inafika Ijumaa ya mwisho wa mwezi, utachukua wembe na utajichanja chini ya mkono huu wa kushoto ambao ambao unavaa hii bangili, baada ya kuchanja Alfwat atakuja na utamlisha, akishiba atakuacha na ndipo mambo yako yatashamiri "

Mimi "Nikioga nayo haina tatizo?"

Mzee "Hiyo haina tatizo wala usijali kuhusu kuoga na usije ukajaribu kuivua!"

Mimi " Sawa na nitajuaje Alfwat ameshiba?"

Mzee " Ukiona bangiri inakubana na ukahisi maumivu utashika bangiri na utaipaka mchanganyiko wa damu yako hii ambayo nimekuwekea kwenye kikopo kisha Alfwat atakuachia"

Mimi "Sawa nimekuelewa"

Baada ya maelezo hayo ya kina alituambia tunyanyuke na tukusanye kila kitu na kuondoka kurejea kwake, baada ya kufika kwake hatukukaa sana na tuliondoka kuelekea Unguja ambapo tulifikia kwa bwana mmoja aliyekuwa na asili ya kipemba na nilitambulishwa na Ally kama ndugu yake, tulilala pale kisha kesho yake tukaondoka kurejea Dar es Salaam.

Muda huo nilikuwa nimevaa ile bangiri mkononi na kisha Ally Mpemba akawa ameweka vitu kadhaa ambavyo tulitoka navyo kwa huyo mzee aliyemfahamu yeye.

Baada ya kufika Dar es Salaam nilielekea nyumbani nikaachana na Ally Mpemba pale bandarini, baada ya kufika nyumbani nilichukua kile kichupa kidogo nikakitunza ndani. Niliendelea kupambana kibishi na ile kazi yangu ya usajili wa line huku mkononi nikiwa nimevaa bangiri kama urembo kumbe haikuwa hivyo!.

Sasa ilipofika ijumaa ya mwisho wa mwezi Ally Mpemba alinitaka niende nyumbani kwake.



.....................................................................................





Utajiri wa rafiki yangu ulivyofanya nikamuamini Shetani - 17.




Nikiwa njiani naelekea kwake alinipigia simu akinitaka nipitie pale Big Bon nimsubiri atoke msikitini kisha tuandamane nae hadi kwake. Baada ya muda kupita Ally Mpemba alirudi kutoka msikitini na aliniambia nipande gari yake kisha tuondoke.

Ally Mpemba "Swalama master"

Mimi "Mimi niko poa kaka"

Ally Mpemba "Usiogope mdogo wangu haya ni mambo ya kawaida sana hapa mjini!"

Aliendelea "Wewe nakuona utakuwa mtu mkubwa sana "

Mimi "Kweli kaka?"

Ally Mpemba "Wewe tulia tu utajionea"

Tulipofika kwake niliteremka kwenye gari na kwenda kufungua geti kisha akaingiza gari ndani.

Sasa tulipofika ndani mimi nilikaa pale sebuleni halafu Ally Mpemba yeye akawa amepitiliza moja kwa moja kuingia chumbani kwake, ilipofika mida ya saa 10 Alasiri nikiwa nimekaa pale sebuleni nikisubiri animbie alichoniitia, ndipo nikahisi mkononi nimeanza kubanwa na ile bangiri; Ilibana kwa nguvu huku damu ikaanza kunitoka kwenye mkono ambayo haikuwa nyingi sana, ilipoendelea kubana sana hadi kuihisi maumivu nilichomoa kile kichupa kidogo cha Gliselin kilichokuwa na ule mchanganyiko wa damu na dawa nikaanza kuipaka ile bangili, baada ya dakika 2 hivi ndipo nikahisi ile hali ya kubana inaachia. Kiukweli baada ya lile tukio nilijisikia mwepesi kupita maelezo, kila jambo mbele yangu niliona halina kizuizi chochote.

Nikiwa naendelea kumsubiri Ally Mpemba pale sebuleni nilisikia ule mlango wake ukifunguliwa na ndipo kutazama nikidhani ningemuona Ally Mpemba haikuwa hivyo, alikuwa ni yule kiumbe wa ajabu akitoka ndani ya kile chumba akirudi kwenye chumba chake,sikuelewa alichokuwa amefata ni nini kwenye kile chumba na alionekana kama kushangaa sana!.

Baada ya muda Ally Mpemba nae alitoka ndani kisha akakifunga kile chumba. Sikujua yule kiumbe alipita muda gani kuingia kwenye chumba cha Ally Mpemba wakati nikiwa pale sebuleni kwasababu ile nyumba namna ilivyokuwa imekaa, ilikuwa rahisi mtu akitoka au kuingia chumbani kuonekana, yawezekana alikuwa chumbani kwa Ally Mpemba muda mrefu na Ally Mpemba alipofungua chumba basi alimwambia aondoke aelekee chumbani kwake kulikokuwa na shimo chini ya kabati.

Lakini kilichonishangaza zaidi ni muda Ally Mpemba aliotumia alipoingia chumbani, tulifika hapo nyumbani kwa Ally mida ya saa 8 mchana baada ya kutoka Kkoo, mimi niliendelea kukaa pale sebuleni hadi mida ya saa 10 alasiri ndipo kubwana na ile bangiri ambayo niliambiwa ni Alfwat anakula; kuna masaa kama mawili Ally Mpemba alikuwa chumbani kwake na yule kiumbe ambaye hadi wakati huo nilikuwa simuogopi baada ya kuzoea yale mazingira na kuhakikishiwa na Ally Mpemba usalama wangu wa Kimwili na Kiroho.

Ally Mpemba "Vipi zoezi lako limekamilika?"

Mimi "Ndiyo kaka "

Ally Mpemba "Wewe ni muaminifu sana na ndiyo maana nakupenda sana!"

Aliendelea "Kama nilivyokwambia, wewe utakuwa mtu mkubwa sana kwasababu huogopi kuyatafuta mafanikio"

Aliendelea "wabongo wengi hawafanikiwi kwasababu wanadhani mafanikio hujileta tu kwa kupiga blah blah, mafanikio yanatafutwa kwa nguvu isiyokuwa ya kawaida master"

Aliendelea "Nitakusapoti mwanangu kwakuwa na wewe umenisapoti na umeonyesha uaminifu kwangu tangu nilipokuamini, sikukosea kukuchagua uwe rafiki yangu!"

Aliendelea "Kwasasa hizi ni hatua za awali tu ila nakuona mbali sana, ukiendelea hivi sidhani kama nitakusogelea kwa pesa master"

Kiukweli maneno ya Ally Mpemba yalinichochea sana hadi kuwaza kufanya mambo makubwa ili nipate pesa na mimi niwe mtu maarufu mjini na niendeshe magari ya gharama kama watu wengine.

Baada ya maongezi yale na Ally Mpemba nilimuuliza huenda kulikuwa na ishu yoyote alitaka kuniambia ili niweze kurudi nyumbani mapema.

Ally Mpemba "Hivi unaweza kuendesha gari?"

Mimi "Ndiyo kaka naweza japo sina leseni!"

Ally Mpemba "Ulijifunzia wapi gari master wewe!"

Mimi "Kaka wala sikwenda chuo kujifunza bali kuna mahali nilikuwa napewa kusogeza kidogo tu hadi nikafahamu kimtindo!"

Ally Mpemba "Kwahiyo unaweza kusogeza kimtindo?"

Mimi "Ndiyo kaka!"

Ally Mpemba "Ulikuwa muosha magari nini!"

Mimi "Kwanini kaka?"

Ally Mpemba "Nimeuliza tu maana jamaa wao ndiyo huwa wanaweza kusogeza kimtindo lakini kuendesha kwao ni changamoto!"

Mimi "Hapana kaka, mimi nilijua kusogeza gari miaka fulani nilikuwa mpiga debe"

Ally Mpemba "Duuuu ushawahi kuwa mpiga debe?"

Mimi "Ndiyo kaka!"

Ally Mpemba "Basi kama ndivyo wewe ni faita, kumbe nakuchukulia poa eeeh!"

Mimi "Kawaida tu kaka ni moja ya utafutaji!"

Ally Mpemba "Ok, sasa itabidi nikusajilie ile gari Aud ili uwe unatembelea miradi yangu pamoja na kufanya ishu zako ziwe rahisi!"

Mimi "Kweli kaka?"

Ally Mpemba "Sijawahi kuongopa na ninachoamini wewe unakuja kuwa mkubwa zaidi yangu, jambo la msingi ni kunitunzia siri vinginevyo tusije tukalaumiana!"

Mimi "Kaka kwa hilo tu usijali "

Ally Mpemba "Hapa kwangu umewahi kumuona mtu mwingine zaidi yako kwa muda huu tu ambao nimefahamiana na wewe?"

Mimi "Hapana kaka sijawahi kumuona mtu yeyote!"

Ally Mpemba "Ok, je umewahi kumuona ndugu yangu yeyote hapa kwangu kwa wale unaowafahamu?"

Mimi "Hapana kaka"

Ally Mpemba "Ok uwe unajiuliza kwa nini wewe ninakupa kipaumbele kuliko ndugu zangu!"

Aliendelea "Wewe ni mtu muhimu sana kwangu hivyo usije ukafanya nikakosa uamimifu kwako itakuwa ni mbaya sana katika maisha yako!"

Mimi "Sawa kaka sitokuangusha"

Ally Mpemba "Hivi karibuni nataka kufanya safari ya Oman ila kabla ya kuondoka nitaomba uwe unanisitiri kwa kipindi chote ambacho sitokuwepo!"

Mimi "Wala usijali kaka wewe ushakuwa zaidi ya ndugu!"

Sasa baada ya kusikia jamaa anataka kunipatia ile Aud mpya niwe natembelea, kiukweli nilikuwa nina furaha ya ajabu na nilijikuta nawaza mambo mengi sana na jambo ambalo lilikuwa la kwanza kichwani mwangu baada ya kupata ile gari, safari ya kwanza ingekuwa kwa mjomba Nico kule Ununio ili niende nikaonyeshe taizi la nguvu na kuonyesha siku hizi niko Matawi ya juu, pili nilipanga niwe naingia nalo pale ofisini Buguruni kuwalingishia wale mademu waliokuwa na nyodo na kuniona mimi mshamba!. Kiukweli niliona kama jamaa ananicheleweshea ile mashine na ndiyo maana ilifikia wakati kila jambo alilokuwa akiniambia nilikuwa nikimjibu kwa haraka haraka bila kujiuliza mara mbili mbili madhara ya kile kitu alichokuwa ananiambia.

Ally Mpemba "Unajua maana ya kunisitiri lakini master?"

Mimi "Kaka sitoweza kupayuka kwa watu na kama nikifanya hivyo wewe nifanye unavyoweza"

Ally Mpemba "Mimi simaanishi hivyo master, siyo kwamba sikuamini kwamba wewe ni msiri ila nahitaji uwe unanisitiri kwa kipindi chote hicho ambacho sitokuwepo"

Mimi "Kaka kukusitiri kiaje?"

Ally Mpemba "Umefanya vema kuniuliza na mimi nilisubiri swali lako sema ulikuwa unazunguka!"

Aliendelea "Nadhani wewe waweza kuondoka halafu mambo mengine nitayashughulikia mimi"

Mimi "Kaka hujaniambia lakini kuhusu kusitiri "

Ally Mpemba "Nitakujuza tu wala usijali,siku ya kuondoka nadhani gari nayo itakuwa tayari hivyo nitakujuza"

Mimi "Sawa kaka, basi mimi ngoja niwahi usafiri wetu wa kugombania"

Ally Mpemba "Nisubiri kidogo nakuja"

Baada ya kuniambia nimsubiri, aliingia chumbani ambako hakuchukua muda akawa ametoka na kiasi fulani cha pesa na kunikabidhi nikitumie kama nauli.

Mimi "Nashukuru sana kaka!"

Ally Mpemba "Hupaswi kunishukuru, mimi ndiyo napaswa kukushukuru!"

Niliondoka zangu mle ndani kuelekea nje kisha nikaanza kuhesabu zile hela nikakuta ilikuwa laki 2, kiukweli nilifurahi sana kimoyo moyo na kujiona ni mtu mwenye bahati sana kuwa na urafiki na Ally Mpemba mwenye asili ya arabuni.

Nilipanda zangu gari za Gongo la mboto zilizokuwa zinatokea maeneo ya Morocco, ingawaje zilikuwa zimejaa lakini hakukuwa na namna,nilichowaza mimi nikufika nyumbani sikuwaza uwingi wa abiria. Baada ya kufika nyumbani mida ya saa 12 jioni nilifungua mlango na kuingia ndani, nilipofika sebuleni kwangu niliwasha taa kisha nikawa naelekea chumbani,kama nilivyosema hapo awali ya kwamba, nikuwa nimepanga kwenye nyumba ya vyumba viwili,hivyo kulikuwa na chumba na sebule,ndani kwangu kulikuwa na kila kitu ambacho kijana wa kisasa angetamani kuwa nacho.

Baada ya kufungua chumba na kuingia ndani niliwasha taa, sasa nilipowasha taa kuna hela ambazo zilikuwa mpya noti za shilingi elfu kumi kumi nilizikuta pale kitandani, kiukweli nilishangaa sana zile hela na sikujua ni nani alikuwa ameziweka hapo kitandani, nilidhani huenda ile asubuhi wakati natoka nilizisahau pale kitandani lakini bado haikuingia hakilini kwasababu sikuwa na hela yeyote hapo ndani kwa wakati huo. Niliamua kusogea na kuzikamata zile hela na kuanza kuzihesabu moja baada ya nyingine, sasa wakati nahesabu zile hela nikawa nasikia kuna mtu anagonga mlango!.

Nilitoka chumbani kwenda kuufungua ule mlango, baada ya kuufungua ule mlango kumbe alikuwa ni yule demu wake na Steve.

Zuu "Shem mambo"

Mimi "poa, mambo vipi?"

Zuu "Safi, niazime simu yako nimpigie Steve maana kwangu sina salio!"

Mimi "Ok ngoja nikuletee"

Niliingia ndani nikachukua simu kisha nikampigia simu Steve baada ya kumpata nikampa aongee na demu wake kisha mimi nikarudi chumbani kwenda kuendelea kuhesabu zile hela, nilipokuwa nikiendelea kuhesabu zile hela, demu wa jamaa aliniita niende nikachukue simu, sasa nilipofika nilikuta bado simu haijakata na ndipo akaniambia Steve anaomba kuongea na mimi.

Mimi "Mwanangu niambie!"

Steve "Mwanangu naomba umuazime shemeji yako gesi yako apikie maana kwangu imeisha, nikirudi nakuja kuchukua kaka"

Mimi "Usijali kaka ngoja nimpatie hela akabadili mtungi halafu wewe utanirudishia!"

Steve "Utakuwa umenisaidia sana mwanangu"

Baada ya kuelewana na Steve,niliingia ndani nikachukua elfu 50 kwenye zile hela ambazo Ally Mpemba alinipatia kama nauli nikawa nimempatia demu wa jamaa ili akabadili mtungi wa gesi, baada ya kumpatia mimi nilirudi ndani kuendelea na zoezi la kuhesabu zile hela, baada ya kumaliza kuzihesabu jumla yake zilikuwa milioni 5, kiukweli nilifurahi sana na nikaona mambo yangu yanazidi kunyooka tu bila kutumia nguvu nyingi. Sasa mpango wangu ulikuwa ni kwamba, nichukue zile hela niongezee na ambazo nilikuwa nimedunduliza benki ili nianze kufanya biashara ya viazi mbatata kutoka Mbeya na niachane na mambo ya kusajili line za simu.

Kwakuwa dhamira yangu ilikuwa kuwa mfanyabiashara mkubwa wa viazi mbatata hivyo nikaona nianze kutengeneza koneksheni ya madalali pale soko la Ilala na Mabibo ili kuweza kulifahamu na kuliteka soko, sasa baada ya kujiridhisha bei ya soko nikaona nichukue kale ka hela kangu nilikokuwa nimedunduliza benki pamoja na ile hela niliyoikuta pale kitandani kisha nikapata milioni 7.

Niliamua kumpigia simu team leader na kumdanganya kwamba naelekea nyumbani kulikuwa na matatizo huku lengo langu ni kuelekea mkoani Mbeya kukusanya viazi mbatata na kuvileta mjini ili nipige pesa, lengo la kumuaga team leader ni asiendelee kuniona mzembe katika kazi ile ya kusajili line ili kuendelea kuweka uaminifu asije kuninyang'anya kodi akampatia mtu mwingine,nilitaka ile kazi niiache mdogo mdogo bila kuondoka kwa dharau maana nilichoamini ni kwamba maisha hubadilika.

Niliianza safari ya kuelekea Mbeya kwenda kukusanya viazi na kuvileta mjini.




.......................................................................................





Utajiri wa rafiki yangu ulivyofanya nikamuamini Shetani - 18.



Nilifanikiwa kufika Mbeya na kuanza kuzunguka kukusanya viazi huku nikiendelea kuwatumia madalali ili kufanikisha kwa haraka niweze kurudi mjini kuuza mzigo.

Nilitumia takribani wiki 1 kununua mzigo na kupakia kwenye fuso kisha kuuleta mjini Dar es Salaam, nilipofikisha mzigo mjini hali haikuwa kama nilivyodhani mwanzo, wale madalali ambao niliongea nao tangu mwanzo nilipokutana nao walianza kuniambia mzigo kwasasa umekuwa mwingi na umeshuka bei.

Niliamua mwenyewe kupita na kufanya utafiti kwenye masoko ya Ilala, Buguruni na Mabibo na kugundua ya kwamba wale madalali walikuwa na nia ya kunipiga kwasababu hakukuwa na mzigo mwingi wala nini! Nilichoamua ni kuanza kuuza ule mzigo mwenyewe, ule mzigo kiukweli ulinikata sana na namshukuru Mungu niliambulia kiasi kidogo cha pesa kwasababu kuna magunia mengine ya viazi yalioza kwasababu ya kukaa chini muda mrefu bila kuuzwa.

Nilichogundua ni kwamba wale madalali mwanzo walikuwa wakinipanga ili nilete mzigo mjini na nikisha ufikisha wao ndiyo wanipangie bei ya kuuza, wao wajipatie pesa nyingi kupitia mzigo wangu halafu mimi nipate faida kidogo, sasa nilipowakataa wakasambaza maneno kichini chini kwamba mzigo wangu haufai hivyo kila mteja akawa anaupita tu kama anaaga maiti kiukweli ile hali ilinifedhehesha sana hadi kuna watu ambao ni wema walinishauri niuuze wote kwa jamaa mmoja pale Mabibo ambaye alikuwa ni dalali na alinipatia fedha nusu ya mtaji, kiukweli kwasababu ndiyo ilikuwa mara ya kwanza kuifanya ile biashara sikutaka kabisa kuendelea nayo kwasababu ilikuwa na fitina kubwa mno na mpaka leo sielewi watu wengine wanawezaje kufanya biashara ya viazi.

Baada ya kuona hiyo biashara imenishinda kwasababu ya fitina ya mswahili, niliamua kurudi zangu kwenye usajili wa laini za simu huku nikiendelea na majukumu mengine ya usimamizi wa miradi ya Brother Ally Mpemba.

Baadae nilichokuja kugundua ni kwamba, hakukuwa na fitina za mswahili wala nini, ile hela ambayo nilikuwa nikiipata kila Ijumaa ya mwisho wa mwezi kiukweli kila nilipojaribu kuifungulia biashara iligoma kabisa kwasababu ukiachilia mbali biashara hiyo ya viazi, nilifungua duka la nguo za kike pale Tandika na kuna jamaa mmoja kutoka Iringa nilimuajiri aniuzie, ilikuwa ni siri sana na sikutaka mtu yeyote ajue kuhusu hilo, lile duka halikufikisha hata miezi 6 likawa linaporomoka, mtaji na faida havikujulikana vinapotelea wapi.

Nikajaribu kumchunguza yule bwana mdogo nikadhani huenda akawa ananipiga kumbe haikuwa hivyo, lile duka nikaamua kuliuza na bidhaa baadhi zilizokuwa zimebaki, kwakuwa mwanzo nilipata ugumu kuelewa ila kadiri siku zilivyosonga ndipo akili na ufahamu vikanijia nikafahamu ya kwamba ile hela ilikuwa na matatizo, sasa nilichoamua ni kwamba ile hela niingize kwenye ujenzi wa nyumba yangu nitakayokaa huko Chanika kwenye uwanja wangu(Nitakuja kueleza kilichotokea maana hali ilikuwa mbaya kuliko nilivyodhani).

Sasa kwakuwa nilikuwa na kiasi cha fedha ambacho nilibaki nacho, niliamua kununua ramani ya nyumba na kwenda kuanza ujenzi kwenye uwanja wangu kule Chanika ili ule uwanja usiendelee kuota nyasi, baada ya kupiga msingi na jamvi niliamua kuachia hapo ili niendelee kuvuta nguvu za kupandisha boma.

Sasa kuna siku Ally Mpemba alinipigia simu akawa amenitaka nionane nae pale kwake ili tupange mipango kadhaa kwasababu yeye alikuwa anahitaji kusafiri kama alivyokuwa ameniambia awali, tulikubaliana tungeonana Jumapili ya wiki hiyo pale nyumbani kwake kwasababu pia hata mimi Jumapili mara nyingi nilikuwa napumzika.

Niliondoka zangu kuelekea kwa Ally na bahati nzuri nilimkuta akiwa nyumbani.

Ally Mpemba "Salama?"

Mimi "Salama kaka"

Baada ya salamu na mazungumzo mafupi, jamaa aliingia ndani ambako alichukua muda mrefu kidogo ndipo akawa ametoka.

Ally Mpemba "Pika chakula ule master, hapa ni kama kwako wala usione taabu!"

Mimi "Kaka usijali niko vizuri"

Ally Mpemba "Ulikula muda gani?"

Mimi "Nimekula muda si mrefu!"

Ally Mpemba "Sawa kama ndivyo"

Aliendelea "Mimi nimekuita weye kwasababu hapo awali nilikueleza ya kwamba nina safari ya kwenda Oman, hivyo nikakuomba unisitiri master!"

Mimi "Sawa kaka"

Ally Mpemba "Kuna jambo nahitaji nikwambie na nakuomba Union unionyeshe uaminifu wako kama nilivyokuamini"

Mimi "Kaka ina maana huniamini tu!"

Ally Mpemba "Mimi nakuamini tangu siku ya kwanza ila nadhani unakumbuka nilikutahadharisha ya kwamba kuna mambo ukiyapayuka kwa watu wengine utakachokutana nacho basi utajua mwenyewe!"

Aliendelea "Ndugu zangu siwathamini kama ninavyokuthamini weye, hivyo thamani ninayokupatia ni kubwa mno"

Aliendelea "Hivyo mimi naondoka na itanichukua takribani mwezi mmoja huko, nakuomba usimamie shughuli zangu hasa ile niliyokukabidhi huko kwengine Farah atasimamia!"

Mimi "Sawa kaka nimekuelewa!"

Ally Mpemba "Vipi mambo yako lakini yanakwenda?"

Mimi "Yanakwenda kaka"

Ally Mpemba "Sawa jitahidi ufanye vema kama ulivyoambiwa na nakuhakikishia wewe ukiwa mwaminifu hakika utakuwa mkubwa hapa Bara kote na hata huko pwani hakuna atakaye kugusa kwa utajiri!"

Niliendelea kumsikiliza Ally Mpemba namna alivyonitia moyo kuhusu ile bangili lakini sikutaka kumwambia kabisa kuhusu biashara zangu zote mbili zilivyonipatia hasara ikabidi nikaushe.

Ally Mpemba "Kuna jambo ambalo kabla ya kuondoka naomba ulifahamu maana ni lazima ndipo uweze kufanya maamuzi ya kunisitiri"

Aliendelea "Bila shaka Huyu kiumbe ninayeishi naye hapa kwangu unamfahamu!"

Mimi "Ndiyo kaka namfahamu"

Ally Mpemba "Sasa nadhani unaelewa huwa nisipokuwepo nakuomba unisaidie kumwandalia chakula"

Mimi "Ndiyo kaka"

Ally Mpemba "Naomba leo nikueleze ukweli na usije kujaribu kumueleza mtu, mimi na wewe tumekuwa wamoja na siri yako ni yangu na naomba siri yangu iwe yako, huwezi kufanikiwa kama hutaweza kutunza jambo!"

Aliendelea "Huyo unayemuona hapa she's my blood sister na ndiye mwanamke ninayempenda kuliko wanawake wote duniani, jina lake si Maya kama unavyodhani, jina lake ni Zahra, hakuna mtu yeyote anayejua Zahra yuko hapa ila wewe, hivyo nakuomba uwe makini na siri hii na nakuomba sana!"

Kiukweli Ally Mpemba alionyesha hali fulani ya huruma na upole baada ya kumuongelea Maya, nilikuwa nikimuangalia Ally Mpemba alionyesha usoni ni mtu wa huruma sana lakini kiuhalisia hakuwa kama ulivyomdhania.

Ally Mpemba "Nikitoka Oman nitakuja kukueleza vizuri ila nachotaka ujifunze na unisitiri!"

Aliendelea "Oman sina mke kama nilivyokwambia hapo awali ila kuna jambo kubwa ambalo na wewe utalifanya siku moja, nikirudi nitakujuza ila kwasasa nakuomba unisitiri!"

Kiukweli hali haikuwa rahisi kama nilivyodhani ila kwakuwa nilikuwa tayari nishaingia kwenye mfumo wa Ally Mpemba sikuwa na jinsi ilibidi nitekeleze na kufanya nilichoambiwa ili kuendelea kujipatia pesa.

Ally Mpemba "Nitakapoondoka nakuomba kila ijumaa uwe unalala kwenye chumba changu hicho!"

Mimi " Sawa kaka nimekuelewa"

Ally Mpemba "Naomba usiwe unashituka kwasababu Zahra atakuwa anakuja mnalala naye na atakachokuwa anataka umfanyie naomba umfanyie usiogope!"

Mimi "Hawezi kuniletea fujo kaka?"
Ally Mpemba "Hawezi, yeye akishakula huwa hana shida, hakikisha kila Ijumaa haufungi mlango wa chumba changu, yeye atakuwa anaingia na mnalala nae kisha akitaka chochote mpatie"

Aliendelea "Bila shaka master wewe ni rijali na kama huwezi kabisa basi mimi kuna dawa nitakupatia utakuwa unakunywa ili uweze kuwa imara kitandani!"

Mimi "Hapana kaka wala usijali niko Imara sana!"

Ally Mpemba "Sawa nitashukuru sana kama umeamua kunisitiri!"

Mimi "Kaka asije akajua mimi siyo wewe akaniletea vurugu!"

Ally Mpemba "Hapana hawezi kufanya hivyo, akishaingia chumbani atalala kitandani na wewe nakuomba usipoteze muda wala usione huruma, mshughulikie kikweli kweli, ikifika asubuhi ataamka mwenyewe ataondoka chumbani kwake!"

Mimi "Sawa kaka nimekuelewa!"

Ally Mpemba "Japo anayo harufu ila nakuomba usionyeshe hali ya kujuta maana hiyo harufu ndiyo pesa yenyewe!"

Aliendelea "Ukifanya vema utapata zaidi na utakuwa mkubwa sana"

Mimi "Sawa kaka nimekuelewa kabisa na sitokuangusha"

Ally Mpemba "Usije kuruhusu mtu yeyote kuingia humu ndani zaidi yako!"

Mimi "Sawa"

Ally Mpemba "Sasa jiandae kesho twende pale TRA ukachukue TIN, kuna jamaa pale nishampa hela nitamkabidhi kwako akufanyie mchakato wa leseni ya gari!"

Basi baada ya yale mazungumzo Ally Mpemba alinikabidhi laki 5 kisha akaniambia kesho asubuhi mida ya 2 tuonane ili tuelekee TRA kwa ajili ya ishu ya leseni. Kiukweli nilibaki kushangaa namna Ally Mpemba alivyokuwa na ujasiri wa kulala na dada yake kitanda kimoja na kumuingilia kimwili. Haikuwa kazi ndogo ila niliamua kupiga moyo konde kwasababu nilikuwa ninataka pesa na mimi niliamua kuwa na roho ngumu.

Baada ya siku tatu kufatilia masuala ya leseni, namshukuru Mungu nilijipatia leseni yangu ya kwanza kabisa kwa ajili ya uendeshaji wa gari. Nilipopata leseni Ally Mpemba alinipatia ile gari yake iliyokuwa mpya aina ya Aud A4, kiukweli nilipata kiburi sana kwa kujiona mimi ndiye mimi, sasa kabla Ally hajaondoka kuelekea Oman alinipatia maelekezo namna ya kuimiliki ile gari.

Ally Mpemba "Master nakuomba tu kwenye hii gari mpya ninayokukabidhi ukiamua kuwabeba marafiki zako basi wakae viti vya nyuma,hii siti ya mbele asije akaikalia mtu yeyote labda kama akitokea ndugu yangu,tafadhali sana nakuomba!"

Mimi "Ndugu zako siwafahamu kaka zaidi ya mama yako mdogo pamoja na Farah"

Ally Mpemba "Hao ndiyo ninaomaanisha, kama Farah akikuona na akihitaji lift usiache kumbeba na asikae nyuma bali akae kiti cha mbele, wengine wote usithubutu kuwabeba mbele"

Mimi "Nimekuelewa kaka nitakuwa muangalifu!"

Ally Mpemba "Sawa mimi nadhani Alhamisi ijayo naondoka, hakikisha Jumatano utakuja kulala hapa ili nikiwa naondoka kuna pesa nikukabidhi pia nikukabidhi na funguo"

Mimi "Utachukua muda mrefu huko?"

Ally Mpemba "Haitapungua mwezi!"

Mimi "Sawa kaka"

Baada ya kuniambia niwe muangalifu na ile siti ya mbele nilivuta picha lakini sikupata majibu, lakini nikakumbuka mara zote nimekuwa nikimuona na ile range akiwa amebeba mtu basi huishia kukaa nyuma na siti ya mbele hukaa bila mtu na mimi pia mara zote nimekuwa nikipanda ile Range ndivyo ilivyokuwa!.

Kweli, baada ya siku kufika Ally Mpemba aliondoka akawa amenikabidhi funguo za nyumba yake pamoja na kiasi cha shilingi milioni 3 na akawa ameniambia amempatia Farah maelekezo endapo zikiisha nimuone atanipatia nyingine, pesa aliyonipatia ilikuwa ya matumizi ya kawaida ya kununulia vyakula vya Maya pamoja na matumizi yangu. Nilifurahi sana maana niliona kila kitu sasa kipo mikononi mwangu na nilipanga kiukweli marafiki na ndugu wanitambue mimi ni nani kupitia lile Audi A4.

Baada ya Ally Mpemba Kuondoka hiyo Alhamisi, ilipofika Ijumaa kama kawaida nilienda zangu kazini pale Kkoo kusajili line za simu, ilipofika mida ya saa 10 jioni nilimuaga Farah nikamwambia nitawahi kufunga kuna mahali nawahi.

Farah "Mbona mapema leo!"

Mimi "Kuna mahali nawahi Aunt!"

Farah "Sawa, si unarudi lakini au ndiyo hadi kesho!"

Mimi "Hiyo hadi kesho dada"

Niliondoka zangu nikaenda kununua vyakula vya maya kama kawaida kisha nikaelekea nyumbani kwa Ally Mpemba, nilipofika kama kawaida nilichukua kitambaa kile cheupe nikatandika pale mezani kisha nikaweka vile vyakula, baada ya kuweka vile vyakula nilifunga mlango kisha nikawasha mchuma nikatoka zangu kuelekea kupata chakula ili niwahi kurudi kufungua kile chumba cha Maya.

Nilipomaliza nilirudi mdogo mdogo na ile gari huku nikiendesha kwa madaha kama yangu vile, ilipofika mida ya saa 1 usiku niliwasha taa kisha nikawa nimetoka zangu nje, kiukweli sikutaka kabisa kumuangalia Maya, nilichoamua ni kwenda kuzurura na ikifika mida ya 3 usiku nirudi kulala. Kweli, niliporudi nyumbani kwa Ally Mpemba kama kawaida niliingia chumbani kwake nikawasha taa na sikufunga mlango, kile chumba kilikuwa ni kizuri na kisafi kupita mfano, sikutaka kabisa kuzima taa, niliingia bafuni kuoga kisha nikarudi kujitupa kitandani kulala huku nikiendelea kumsubiri Zahra(Maya)niliyeambiwa na Ally ya kwamba nikiacha chumba wazi ataingia mwenyewe.

Kweli, haikupita hata nusu saa nilimuona Zahra akiingia chumbani akiwa uchi kama ambavyo siku zote huwa.




.......................................................................................





Utajiri wa rafiki yangu ulivyofanya nikamuamini Shetani - 19.



Nilijifanya nimepitiwa na usingizi huku nikiendelea kumtizama Zahra kwa kuibia; baada ya kufika karibu na kitanda alipanda kitandani huku akiwa uchi kama alivyozaliwa!. Sikutaka kabisa kupoteza muda maana Ally Mpemba aliniambia akisha panda kitandani kazi yangu ni kumshughulikia kisawasawa!.

Niliamka taratibu nikavua boxa ambayo nilikuwa nimevaa na singlendi kisha nikarudi kitandani, kiukweli sikuelewa nitaanza vipi kusimamisha uume kwasababu Zahra alikuwa na harufu kali ambayo ilisababishwa na yeye kutokuoga muda mrefu huku sehemu zake za siri zikiwa zimefunikwa na nywele(mavuzi)za kutosha!, nilisogeza mkono nikamshika ili nione kama anaweza kuwa mkali lakini nilipomshika aliendelea kuwa kimya, niliendelea kumshika huku nikimtizama yule mwanamke na kujikuta namvutia picha ya ngono kwa haraka ndipo uume ukasimama kwa haraka kama nyoka aina ya koboko aliyeona hatari na kujiandaa kuikabili, kiukweli baada ya uume kusimama nilimsogelea na kuinyanyua miguu yake kisha nikamchomekea uume taratibu na bila kizuizi ulizama wote nikaanza kumkimbiza mchakamchaka bila huruma!.

Baada ya kumzamishia fimbo ya mnyonge isiyokuwa na huruma hata kidogo, ile harufu kiukweli ni kama nilianza kuizoea huku akili yangu ikimezwa na tamaa ambayo ilifanya nikamuona Zahra(Maya) kama mwanamke wa kawaida wa kiarabu asiyekuwa na tatizo lolote. Hali haikuwa nzuri ni vile tu nilikuwa nina tamaa ya pesa ndiyo ilipelekea mimi kufanya vile.

Niliendelea kumkung'uta Zahra kwa hasira kana kwamba alikuwa ni mwanamke ambaye nimewahi kumtumia nauli akala akashindwa kutokea sasa alipokuja nilipanga nimuonyeshe namna ambavyo watu tuliozoea kula ugali wa uwele na mtama tulivyokuwa na hasira dhidi ya wanawake wala nauli na wenye viherehere wasemao "Tuma na ya kutolea".

Baada ya kufika mlima Kilimanjaro nilitaka kushuka ili angalau nipumue kumbe haikuwa kama nilivyodhani, nilipotaka kuchomoa uume kwenye uke wa Zahra nilijikuta siwezi kwakuwa alikuwa amening'ang'ania kwa nguvu ambazo hazikuwa za kawaida, sikuwa hata na uwezo wa kushindana nae kwakuwa nguvu alizokuwa nazo hazikuwa za kawaida, nilikuwa mpole huku nikiendelea kusukuma taratibu nikitafuta nguvu za kuuanza upya mchaka mchaka!

Baada ya uume kusimama tena niliendelea kumsukumia nyama hadi aliponiachia huku akionekana kulifurahia tendo, baada ya kuona ameanza kuelewa nilichokuwa namfanya niliamua kumgeuza na kuanza kumshughulikia kwa hasira na uchu mwingi, japokuwa hakuwa na akili kama wanadamu wengine lakini uzuri wa yule mwanamke haukupotea, ulikuwa ukimuangalia uligundua kabla ya kuwa alivyokuwa alikuwaga mwanamke mzuri sana! Kiukweli ile staili ya kumgeuza nyuma niliipenda sana na ndiyo nilieendelea kuifanya hadi asubuhi bila kuchoka kwasababu nilikuwa nikimaliza ninapomshika matako koboko anasimama nakumchomekea kisha kazi inaendelea!.

Kule kwenye kile chumba hakuja kulala bali alifata mbolo na mimi sikuwa na hiyana nilimpatia alichokifata.

Ilipofika asubuhi mida ya saa 12 alinyanyuka mwenyewe akaondoka kuelekea chumbani kwake alikokuwa akikaa, mimi niliamka nikatoka kwenda kukifunga chumba chake kisha nikaingia bafuni kuoga. Nilipotoka kuoga nilitoa lile shuka nililolalia na Zahra nikalipeleka kulifua kisha nikaweka shuka jingine.

Baada ya kumaliza shughuli za hapo nyumbanj kwa Ally Mpemba niliamua kwenda zangu Kkoo kuendelea na kazi yangu ya usajili wa line za simu. Kwakuwa ilikuwa Jumamosi, nilipanga nikafanye kazi masaa machache kisha niondoke zangu kuelekea nyumbani kubadili nguo na kujiandaa kwa mambo mengine, siku hiyo sikupita kabisa pale ofisini Buguruni, sasa nilipofika Kkoo nilielekea mahali ambapo nilikuwa natunza vitu vyangu, baada ya kuvichukua niliondoka kueleka sehemu ya kazi, nilipofika muda huo lile duka la Ally Mpemba ambalo mara nyingi alikuwa akiuza dada yake aitwaye Farah lilikuwa bado halijafunguliwa, haikuwa kawaida kukuta lile duka muda huo wa saa 3 kuelekea saa 4 ukute likiwa limefungwa, mimi kama kawaida nilifungua biashara yangu pale na nikaanza kupiga kazi!.

Ilipofika mida ya saa 5 asubuhi nikiwa napiga kazi, sasa nikiwa sina hili wala lile kutokana na ubize, mara ghafla nilisikia sauti ya mwanamke ikinisalimu kwa sauti ambayo haikuwa ya kawaida, nilinyanyua shingo na kumtazama yule mwanamke kumbe alikuwa ni Aunt Farah, dada yake na Ally Mpemba, yeye mara zote alikuwaga akivaa Nicab(Vazi nadhifu lililofunika sura yake).

Mimi "Ooh Aunt Farah, umenishitua!"

Farah "Umeshituka na nini?"

Mimi "Sijui hata nilikuwa nawaza nini!"

Farah "Haya bana, umeamkaje lakini?"

Mimi "Niko poa kabisa, sijui za huko utokako!"

Farah "salama"

Aliendelea "Nilijua utapumzika leo"

Mimi "Ahaa hamna, kama sina tatizo tu la kuniweka nyumbani siwezi kupumzika maana hii kazi hainaga wikiendi!"

Sasa wakati naongea nae yeye alikuwa akiendelea kufungua geti la duka lake, kama mtakumbuka hapo awali niliwaambia ya kwamba, nilikuwa nikifanya biashara zangu kando ya lile duka la Ally Mpemba lililokuwa likitazamana na ambayo leo ni stendi ya Mwendokasi(Kituo cha Gerezani).

Mimi "Leo umechelewa sana hadi nikahisi hufungui!"

Farah "Kuna mahala nilikwenda ndiyo maana nilichelewa"

Mimi "ooh sawa!"

Baada ya mazungumzo mafupi niliendelea na kazi yangu kama kawaida huku wateja wakija mmoja mmoja, kiukweli yule dada sikuwahi kumuona usoni namna alivyo na namna alivyokuwa akifanana! Nilitamani sana siku moja nimuone ili niweze kumfananisha na yule mwanamke aliyetolewa kafara na Ally Mpemba ambaye kwa mujibu wake alikuwa dada yake (Zahra/Maya).

Nilitamani kumuona na kupata uthibitisho kama wanafanana kwa maana walikuwa ni ndugu.

Ilipofika mida ya saa 7 mchana mimi ilibidi nichukue vitu vyangu na kuanza kuvikusanya ili nivirudishe nilikokuwa navihifadhi niweze kwenda nyumbani, kiukweli kwa wakati huo hata utendaji wangu wa kazi haukuwa mzuri kama mwanzo kwakuwa nilikuwa nina pesa ya kutosha hivyo ile kazi nilikuwa ninaifanya angalau nisiweze kukaa tu nyumbani bure. Mara zote ambapo huwa nikiondoka nilikuwaga namuaga Aunt Farah maana nilimzoea kama vile ndugu yangu, sasa kuna jambo ambalo baada ya kumuaga ni kama lilinishitua.

Mimi "Sister mi nakuacha mara moja tutaonana Jumatatu!"

Farah "Mbona mapema sana leo?"

Mimi "Nimechoka tu nahitaji nikapumzike!"

Farah "Sawa mwanaume wa bara mwenye nguvu zake"

Mimi niliondoka zangu bila kumzingatia maana mara zote amekuwa akinitania kwa majina mbalimbali hivyo sikujali.

Nilipofika nyumbani ile nimeingia ndani ya chumba changu cha kulala nilishituka sana baada ya kutazama kitandani na kukuta ile shuka ambayo niliitoa pale kitandani kwa Ally Mpemba baada ya kumkung'uta Maya fimbo za kutosha, kiukweli nilishangaa sana ni nani alikuwa ameifikisha ile shuka pale nyumbani kwasababu baada ya mziki ule wa usiku kucha niliamua kuibadili ili kuweka shuka safi. Nilisogea hadi kitandani nikalitoa lile shuka, cha ajabu hata nililokuwa nimelitandika hapo awali lilikuwa limetolewa na kuwekwa kwenye nguo chafu kana kwamba kuna mtu mle ndani ndiye alifanya vile!.

Baada ya kulitoa nilitandika shuka nyingine safi, nilielekea bafuni kuoga upya ili nirudi nibadili nguo nikiwa na lengo la kuondoka kwenda kuchukua mchuma(Audi )ili nielekee ununio kwa Anko,sasa ile nimetoka bafuni kupiga maji, nilikuta tena lile shuka likiwa limetandikwa kama mwanzo, kiukweli nilitoka mle chumbani kwa haraka nikiwa mwenye hofu kuu, nilisimama pale sebuleni kwa muda nikiwa niNatafakari ni kitu gani kinaendelea, baada ya dakika kadhaa nilirudi chumbani kwa ujasiri kisha nikavaa nguo na kuondoka, lengo ilikuwa ni kwenda hadi Kkoo kwa Aunt Farah ikiwezekana amtafute Ally ili niweze kuzungumza nae maana ile hali sikuielewa kabisa!.

Baada ya kufika Kkoo cha ajabu nikakuta Aunt Farah naye kafunga duka na sikufahamu alipoelekea!. Niliondoka hadi kwa Ally Mpemba Magomeni, nilipofika nilifungua nyumba na kuingia ndani moja kwa moja hadi kwenye chumba alichokuwa akilala jamaa, nilipofungua mlango na kuingia ndani nilikuta tena lile shuka ambalo nimeliacha nyumbani kwangu likiwa limetandikwa kitandani mara hii tena likiwa limetandikwa kitandani kwa Ally Mpemba, kumbuka hii shuka ni ile ambayo niliibadili baada ya kumkung'uta Maya stiki za kutosha ule usiku. Kiukweli nilibaki nikishangaa sana, sasa nilichoamua ni kutoka nje na kuchukua ile gari na kuondoka zangu.

Niliondoka kuelekea Ununio kwa Anko Nico kuwasalimu lakini lengo langu lilikuwa ni lile lile la kuwaringishia ili waone yale waliyokuwa wakizungumza kuhusu mimi hawakunitendea haki. Nilipofika nyumbani kwa Anko nilipiga honi bahati nzuri geti likafunguliwa na kijana mmoja ambaye sikumfahamu, niliingiza gari hadi ndani kisha nikateremka.

Mimi " Mambo vipi "

Jamaa "Safi "

Mimi "kwema?"

Jamaa "Kwema kabisa"

Mimi "Humu ndani wapo kweli?"

Jamaa "Yupo dada Rebecca nadhani"

Niliingia ndani hadi sebuleni kisha nikaa kwenye sofa, kuna mtu bila shaka alikuwa akitazama filamu za kifilipino pale sebuleni lakini baada ya kusikia naingia ndani aliondoka akaelekea chumbani, ile picha niliisoma maana nilikuta luninga ikiwa imewashwa na kwa muonekano tu niligundua kulikuwa na mtu amekimbilia chumbani baada ya kusikia naingia ndani. Baada ya dakika 10 alitoka binti wa Anko Nico ambaye ni mkubwa aliyeitwa Rebecca.

Rebecca "Ooh binamu"

Aliendelea "Karibu!"

Mimi "Ahsante, za hapa"

Rebecca "Nzuri, za utokako!"

Mimi "Huko tuko poa"

Mimi "Mbona nyumba imepoa sana, uko mwenyewe nini!"

Rebecca "Si unajua tena wengine wameenda kanisani!"

Mimi "Oooh aisee hata sikujua "

Mimi " Wanasali mbali?"

Rebecca "Eeeh ni mbali kidogo maana kuna makambi ndiyo wako huko!"

Mimi "Sawa, mimi nilipita kuwasalimu, nadhani utanisalimia Anko na Shangazi wakirudi"

Rebecca "Haukai kuwasubiri?"

Mimi "Nitarudi hata wikiendi ijayo kuwasalimu"

Rebecca "Kaa kidogo maana napasha chakula ule ndiyo uende!"

Mimi "Ok hakuna tatizo!"

Kiukweli nilishangaa sana namna binti wa Anko alivyobadilika kwa muda mchache kwasababu wakati ule nikiwa kwao alikuwa ni mmoja wa watoto wa Anko ambao hawakuwaga na stori na mimi kabisa, nilidhani labda huenda umri ukawa umembadilisha kiakili. Baada ya muda aliniketea msosi nikaanza kuukung'uta kama kawaida kisha nilipomaliza nilimuaga na kumuachia kiasi cha shilingi laki moja kama matumizi yake na kuondoka, alinishangaa sana na kunisindikiza nje kwa bashasha kana kwamba nilimpa milioni moja, mimi lengo langu ni autazame ule mchuma na wazazi wake pamoja na ndugu zake watakaporudi basi awape stori.

Mimi "Mi naenda dada"

Rebecca "Haya binamu uwasalimie huko"

Aliendelea kunisindikiza kwa macho hadi nilipoingia kwenye chombo na kuondoka zangu.

Nilipotoka kwa Anko niliondoka kurudi Gongo la mboto, sasa nilipofika pale Mombasa kuna bar moja niliingia nikapaki gari kisha nikaagiza bia aina ya safari na kuanza kutandika mdogo mdogo, wakati nikiwa ndiyo nimeikamata bia ya pili kuna mtu alinipigia simu, nilipoitazama ile namba ilikuwa ngeni kwenye simu yangu.

Mimi "Halloo"

Yeye "Hello"

Mimi "Nambie"

Yeye "Poa, uko wapi?"

Mimi "Nani?"

Yeye "Farah hapa naongea"

Mimi "Farah!.....Aunt Farah?"

Yeye "Ndiyo"

Mimi "Ooh samahani sana sister hii namba huwaga sina"

Farah "Usijali, uko wapi?"

Mimi "Nipo hapa Mombasa!"

Farah "Ok mimi nipo hapa kwako"

Mimi "Kwangu?"

Farah " Ndiyo!"

Mimi "Wewe si ni Aunt Farah wa Kkoo?"

Farah "Ndiye mimi"

Mimi "Kwangu umepajuaje dada?"

Farah "Nimekuja nikiuliza hadi nimefika"

Kiukweli baada ya maelezo ya Farah nilishituka sana na ile bia nikaanza kuiona chungu, nilishindwa kuelewa alifikaje nyumbani kwangu, na huenda ningekuwa mtu maarufu kiasi kwamba ukiniulizia usingenikosa lakini mimi nilikuwa mtu wa kawaida sana na alivyoniambia eti amefika kwangu kwa kuulizia kiukweli alinichanganya.

Farah "Mbona unashangaa?"

Mimi "Hamna dada!"

Farah "Ally Alitaka kuzungumza nawe ndiyo maana niko hapa"

Mimi "Sawa dada nakuja "

Kilichoniacha hoi ni hiyo statement ya kwamba Ally Mpemba alitaka kuzungumza na mimi, mara zote Ally Akiwaga nje alikuwa akinipigia simu moja kwa moja, ila mimi ndiye nilikuwaga nikitaka kumpigia moja kwa moja simu haitoki. Niliondoka upesi kuelekea nyumbani ili nikaonane na Farah.

Nilipofika pale nyumbani ile gari niliipaki nje ya ile nyumba kwakuwa hakukuwa na nafasi ya kuingiza gari ndani, sasa nilipofika ndani sikumuona Farah ikabidi nimpigie simu.

Mimi "Dada nishafika uko wapi?"

Farah "Nilitoka kidogo nipo hapa dukani nakuja"

Nilifungua mlango nikaingia zangu ndani kuweka mazingira sawa kisha nikatoka nje kumsubiri, sasa baada ya muda aliingia mwanamke mmoja wa kiarabu(Kipemba)aliyekuwa akifanana sana na Zahra/Maya kama mapacha, nilibaki kumtizama kama mtu niliyepigwa na bumbuwazi.

Tangu nimfahamu Farah sikuwahi kumuona uso wake kwasababu mara zote alivaa nicab. Alipokuja kwangu alikuwa amejitanda hijab tu huku uso wake ukiwa wazi kabisa na chini akiwa amevaa suruali nyepesi ya kitambaa pamoja na raba ya converse, kiukweli baada tu ya kumuona namna alivyokuwa akifanana na Maya nilimtambua. Kilichonishangaza zaidi hadi umbo na tembea yake alikuwa ni Maya mtupu, hali ya uwoga ikaanza kuniingia ghafla lakini sikutaka kuonyesha ikabidi nijikaze.

Nilijiuliza maswali mengi sana, ni yeye tu ndiye alifanana na Maya au hadi ndugu wengine ambao sikuwaona nao walifanana na Maya? Na Mbona Ally Mpemba alikuwa hafanani sana na Maya kama ilivyo kwake?

Mimi "Dada Farah karibu"

Farah "Ahsante kijana wa bara mwenye balaa"

Mimi "Karibu ndani!"

Farah "Hapana, ndani siingii!"

Aliendelea "Ngoja nimpigie Ally uongee nae alitaka kuzungumza nawe!"

Mimi "Leo unamtoko nini!"

Farah "Kwanini?"

Mimi "Siyo kawaida yako kukuona hivi!"

Farah "mmmh hujanikuta tu huenda!"

Mimi "Nilikuja dukani mida fulani nikakuta umefunga"

Farah "Kuna mahala inapaswa niwahi hebu zungumza na Ally"

Baada ya kuzungumza na Ally Mpemba alinipatia maelekezo ya kwamba aende kule kwake akachukue ile gari yake(Range Rover) kisha kulikuwa na hela kiasi cha milioni 2 anipatie. Nilimtaka pia Ally Mpemba baadae anipigie simu yangu kuna mambo muhimu nizungumze nae akanianbia usiku angenipigia.

Basi baada ya mazungumzo yale tuliondoka na Farah kuelekea kwenye Audi ili niondoke nimfungulie achukue gari kama jamaa alivyokuwa amenipatia maelekezo, sasa ile Farah anapanda kwenye gari kuna namna aliliitusha hijab yake ambayo ilionekana kumbana,kiukweli nilipomtazama vizuri nilishituka sana baada ya kuona alikuwa na mchoro mkononi kama ambao Maya alikuwa nao kwenye mkono wake wa kuume!



.......................................................................................





Utajiri wa rafiki yangu ulivyofanya nikamuamini Shetani - 20.


Nilikuwa nina maswali kichwani mwangu zaidi ya elfu moja na ambayo hayakuwa na majibu. Iliwezekana vipi mwanamke ambaye hakuwahi kabisa kufika kwangu hata mara moja leo aje tena kwa hoja ya kwamba ameelekezwa kwa kuulizia ulizia? Je, alimuuliza nani huyo ambaye ananifahamu pale mwisho wa lami? Pili, inakuwaje Farah afanane kiasi kile na Zahra/Maya? Sawa yawezekana wangefanana kama ndugu wa tumbo moja, lakini je hadi mchoro mkononi? Kiukweli kwangu ilikuwa ni kama sinema ambayo sikuielewa hata kidogo. Kwakuwa Ally Mpemba amewahi kuniambia Farah ni dada yake, nilidhani huenda Farah na Maya wakawa ni mapacha kwasababu pia Ally aliniambia Maya/Zahra alikuwa ni dada yake pia.

Baada ya kuingia kwenye gari niliiwasha na kuanza kuiondoa taratibu kuelekea Magomeni. Sikutaka kabisa kukaa kimya, niliona niendelee kumdodosa Aunt Farah ili niweze kuufahamu ukweli!.

Mimi "Kwahiyo dada umekuja unaulizia?"

Farah "Mbona unakuwa na mashaka sana leo? Kwanini?"

Mimi "Hapana dada sina mashaka ila nauliza tu!"

Farah "Wewe hukuwahi kumwambia Ally unakaa Gongo la mboto mwisho wa lami?"

Mimi "Nimewahi kumwambia lakini kaka Ally pia hajawahi kufika kwangu".

Farah "Nilipofika hapo mwisho wa lami nimeulizia nikaelekezwa"

Mimi "ooh sawa"

Kiukweli sikutaka kumbishia maana niliona huenda tungekwazana kwasababu sababu alizokuwa akinipa zilikuwa haziniingi akilini hata kidogo, nilijua kabisa alikuwa akinidanganya, pale mwisho wa lami mahali nilipokuwa nikikaa mimi kulikuwaga hakuna watu ninaofahamiana nao sana huenda jamaa mwenye duka pale nje, pia kwa mazingira yale isingekuwa rahisi mtu kunifahamu kwasababu nilikuwaga si mtu wa kujichanganya na ndiyo maana nikasema huenda ningekuwa maarufu pale mtaani hapo angenishawishi kwa ule uongo wake laki kiukweli sikukubaliana naye hata kidogo. Niliamua kukausha tu ili mambo mengine yaendelee maana niliona nikiendelea kulifuatilia hilo suala sana kiundani huenda ningeibua mambo mengine.

Mimi "Dada nikuulize swali?"

Farah "Karibu"

Mimi "Kwenu mmezaliwa wawili tu na Kaka Ally?"

Farah "Kwanini?"

Mimi "Nimeuliza tu maana mara zote nawaona nyie tu"

Farah "Mmh! hapana tupo wengi"

Aliendelea "Wengine hawakai hapa Bongo"

Mimi "Kwahiyo kwa hapa Bongo upo wewe na kaka Ally tu!"

Farah "Hapana wapo wengine!"

Mimi "Ooh sawa!"

Niliamua kukaa kimya sikutaka kabisa kuendelea kuuliza maswali mengi kwakuwa hata yeye pia niliona ananijibu kishingo upande hivyo nikaona nisiingie ndani sana ijapokuwa maswali nilikuwa nayo mengi sana. Sasa kichwani mwangu nilipanga ya kwamba, usiku wa siku hiyo nikamtazame vizuri Maya atakapokuwa akila chakula chake pale sebuleni ili kujiridhisha maana kiukweli walikuwa wakifanana kila kitu na Farah.

Baada ya kufika Magomeni kwenye nyumba ya Ally Mpemba, nilifungua geti na ile gari kuiingiza hadi ndani kwenye sehemu ya kuegeshea. Nilishuka kwenye gari nikaenda kumchukulia ndani funguo ya gari dada Farah ambaye wakati huo alikuwa nje akinisubiri. Baada ya kumpatia ule ufunguo akawa amechukua mkoba wake akatoa shilingi milioni 2 akanipatia.

Farah "Hela hizi hapa"

Mimi "Nashukuru dada"

Hakuchukua muda akaingia kwenye ile Range. Nilisogea nikamfungulia geti akawa ametoka na kuondoka. Sikutaka kabisa kupoteza muda hapo nyumbani niliondoka zangu hadi sokoni kwenda kununua mahitaji ya chakula cha Maya, niliwasha gari nikawa nimetoka zangu kuelekea soko la Ilala, kiukweli wakati huo nilikuwa nimenawiri sana na nilikuwa nanyuka pamba za ukweli, ulevi wangu mkubwa ulikuwa ni kupendeza kwa kuvaa vizuri.

Sasa kuna mahali nilifika nikapaki ile gari kisha nikashuka kuelekea sokoni kununua mahitaji, wakati nikiwa nanunua mahitaji kwa mama mmoja, ghafla nikasikia sauti ya mwanamke mmoja ambaye ilinifanya nikageuka kumtazama, hadi leo sijajua ni kitu gani kilitokea ila huwa najiuliza maswali mengi sana.

Huu ulimwengu hauko kama mnavyodhani ndugu zangu, kuna muda unaweza kuwaona watu wanapendeza na kuishi maisha bora ukadhani ni rahisi lakini si hivyo! Mimi baada ya kupitia mambo hayo machache ndiyo maana leo napambana kwa nguvu zangu kufa na kupona ili kujipatia riziki, sasa kuna watu nikiwaambia mimi ni naendesha bodaboda huwa hawaamini wanadhani natania, japokuwa pia najaribu kuwekeza kwenye kilimo lakini bodaboda hiyo hiyo ndiyo inanipatia pesa ya uwekezaji huo!. Niliamua kupambana na maisha yangu ya udundulizaji kwasababu hakuna maisha ambayo sijapitia, kila baya na jema nishaona, hivyo niliamua kutulia kujipambania, huko mbele mtaelewa vizuri ni kwanini leo naendesha bodaboda.

Sauti ya kike "Mama Eliya nikuletee?"

Mama Eliya "Leo sina hela mwaya!"

Huyo mama Eliya alikuwa ni mama ambaye nilikuwa nimesimama mbele yake nikuchukua kabeji, sasa wakati akiwa kwenye pilika pilika za kunirudishia chenji ndiyo nikawa nimesikia hiyo sauti ikimwambia hivyo, baada ya kumtazama yule mwanamke aliyemuita mama Eliya kiukweli nilibaki nikimtizama. Kiukweli baada ya yule mwanamke kumuita huyo mama niliyekuwa nikinunua mboga kwake nilijikuta tu nageuka kumtazama ni nani na nilipogeuka nilijikuta namtamani baada ya kumtazama, hakuwa mwanamke mbaya, alikuwa ni mwanamke mmoja wa kawaida ila alikuwa na umbo zuri sana.

Mimi "Anauza nini huyo?"

Mama Eliya "Anauza Juisi"

Mimi "Ni nzuri?"

Mama Eliya "Juisi yake huwa tamu kweli sema leo tu ndiyo hali ngumu ila ningechukua"

Mimi "Anauza bei gani?"

Mama Eliya "Anapima kwenye glasi shingi elfu moja"

Mimi "Mwambie akupe"

Mama Eliya "Ahsante mwanangu"

Aliendelea "Nitakunywa baadae "

Mimi "Mwambie aje akupe kabisa maana nyie huwa wajanja, nitakupa hela utaisunda huta nunua,nataka na yeye umuungishe kama mimi nilivyokuungisha"

Baada ya kumwambia hivyo yule mama muuzaji alianza kucheka sana. Nia yangu ilikuwa ni kwamba amuite yule mwanamke asogee kwa karibu nipate kumtazama vizuri maana alikuwa bize na juisi yake na kwangu isingekuwa rahisi kumsimamisha pale sokoni na kuanza kuzungumza nae kwasababu mara zote nimekuwa na aibu kusimama na mwanamke machoni pa watu.

Mama Eliya "Wala usijali baba namuungisha"

Aliendelea "Wewe Ray......Raaaaaay niletee juisi nimepewa ofa"

Baada ya kuita yule mwanamke alijongea taratibu hadi pale nilipokuwa nimesimama kwa mama Eliya.

Mama Eliya "Niwekee glasi moja nimepewa ofa na mwanangu"

Mimi "Mama wewe kunywa hadi utosheke sijakupa ofa yenye kikomo"

Mama Eliya "Mmh nashukuru baba"

Nilifahamu kabisa mama Eliya anaweza kuwa anauhitaji na pesa ndiyo maana ile ofa ni kama alitamani asinywe ili ile hela achukue, sasa mimi nilipanga kumpatia kiasi kidogo kitakachomsaidia.

Mimi "Jusi yako unatengeneza na nini?"

Muuza juisi "Ni mchanganyiko wa Embe, pasheni na parachichi"

Mimi "Ok"

Muuza juisi "Nichangie basi kaka"

Mimi "Haina shida wala usijali, nimepaki gari pale ng'ambo naomba twende ili ikiwezekana nitafute chombo uniwekee"

Muuza juisi "Ninazo chupa kaka"

Mimi "Mbona hapa sizioni?"

Muuza juisi "Kuna mahali nimeziweka nakimbilia mara moja"

Mimi "Ni safi?"

Muuza juisi "Ni safi kaka huwa naziosha na maji moto"

Aliendelea "Au kama hutoridhika basi unywee hapa kaka"

Mimi "Usijali nitanunua"

Basi baada ya mazungumzo mafupi nilimpatia yule mama noti ya shilingi elfu kumi kama malipo ya juisi na itakayobaki achukue yeye, kiukweli alinishukuru sana na nilimwambia wakati wote nitakapokuwa naenda hapo sokoni kununua bidhaa ningekuwa namtafuta yeye.

Niliondoka nikaongozana na yule dada muuza juisi kuelekea nilikokuwa nimepaki gari, mimi nilikuwa mbele na yeye alikuwa nyuma yangu huku mkononi akiwa ameshika galoni ya juisi na kapu la vikombe.Tulipofika nilifungua gari kisha nikamwambia animinie kwenye glasi ili ninywe kwanza niisikie ladha yake.

Mimi "Ni tamu"

Mimi "Unaitwa nani?"

Muuza juisi "Naitwa Rehema"

Mimi "Unaishi wapi Rehema?"

Yeye "Naishi Ubungo Msewe?"

Mimi "Ubungo Msewe iko maeneo gani?"

Yeye "Pale pale Ubungo ni jirani na chuo kikuu"

Mimi "ooh,duuu mbona kama mbali?"

Yeye "Wala hata siyo mbali"

Mimi "Unaona siyo mbali kwasababu ushazoea"

Mimi "Kwahiyo kila siku unamaliza hiyo galoni?"

Yeye "Inategemea, kuna muda nauza hizi galoni hata tatu na kuna siku hata moja haiishi"

Mimi "Ok"

Mimi "Umeolewa?"

Yeye "Sijaolewa ila nina mtu wangu"

Mimi "Mnaishi wote?"

Yeye "Hapana, mi naishi kwa shangazi na yeye anaishi kwao!"

Mimi "Kwahiyo ndiyo umepanga aje awe mume wako?"

Yeye "Hayo sasa ni maajaliwa ya Mwenyezi Mungu"

Mimi "Kwenu anafahamika?"

Yeye "Anafahamika kwasababu ninaye mtoto wake!"

Mimi "Unaye mtoto wake kivipi?"

Yeye "Nimezaa naye "

Mimi "Mbona sasa mimi nakupenda Rehema"

Yeye "Kunipenda wala siyo dhambi kaka, dhambi ni kumtamani mke wa mtu"

Mimi "Mimi sijakutamani Ray mimi nakupenda"

Yeye "Toka lini mwanaume wa Dar akapenda mwanamke? Wewe sema umenitamani tu ili unipate umalize haja zako unikimbie, nyie wanaume hata sinaga hamu kabisa na nyie!"

Mimi "Hebu tuachane na mambo mengi Ray nipe namba yako ya simu nitakupigia"

Yeye "Simu yangu inasumbua betri nimeiacha nyumbani"

Mimi "Mimi nitakupataje ili tutafute mazingira mazuri tuzungumze"

Yeye "Mimi napatikana tu hapa hapa wewe ukija utamuuliza mama Eliya"

Mimi "Lakini umeelewa nilichokwambia Ray?"

Yeye "Lakini nishakwambia ninaye mtu wangu!"

Mimi "Kwani utamwambia?"

Yeye "Siyo hivyo, kumbuka penzi ni kama kikohozi huwa alijifichi!"

Aliendelea "Halafu unataka kuniambia wewe huna mtu?"

Mimi "Ningekuwa na mtu unadhani ningekusumbua?"

Yeye "Mimi nitajuaje! Nyie wanaume kwani mnaaminikaga?"

Mimi "Kwahiyo hata huyo jamaa yako pia humuamini?"

Yeye "Simuamini ndiyo, kwani anapokaa huko ninakuwa nae?"

Mimi "Siko kama unavyodhani Ray"

Yeye "Sawa, ushamaliza kuniongopea? Mimi nataka niwahi kwenye biashara"

Mimi "Sikuongopei ila amini hivyo"

Yeye "Sawa ukiwa na shida basi utanitafuta napatikana hapa hapa sokoni"

Baada ya mazungumzo yale na yule mwanamke ambaye alionekana na msimamo, nilimpatia noti ya shilingi elfu kumi akawa anataka kunirudishia chenji nikamwambia hiyo nimempatia tu.

Yeye "Ahsante"

Yeye "Ila nimesahau kukuuliza jina lako!"

Mimi "Mimi naitwa Umughaka"

Yeye "Sawa nashukuru kukufahamu Umungaka"

Mimi "Siyo Umungaka,ni Umughaka!"

Yeye "Ahahahaa nisamehe jamani una jina gumu, sijui kama nitaweza kulitamka"

Mimi "Kesho nitakuja kukucheki"

Yeye "Saa ngapi sasa ili niwe maeneo jirani?"

Mimi "Mida kama hii"

Yeye "Sawa, msalimie wifi "

Mimi "Wifi tena!"

Yeye "Utakubali sasa!?"

Aliendelea "Haya basi tutaonana!"

Yule mwanamke aliondoka huku namtazama namna alivyokuwa na nyama za kutosha, kiukweli alikuwa mwanamke fulani wa kawaida ila umbo lake halikuwa la kawaida, mara zote ugonjwa wangu kwa wanawake umekuwa ni uleule wa matako makubwa wastani na hips za kuzugia, mara zote huwa sihangaiki na sura kwasababu si sehemu ya hitaji langu kubwa kwa mwanamke, huwa naangalia vinavyo nihusu na visivyo nihusu naachana navyo.

Nilielewa ni kila mwanamke ukijaribu kumtongoza ni lazima akwambie anaye mtu wake ili kujipa thamani lakini mara zote huwa haiko hivyo, hata Rehema nilifahamu kabisa ili ajipe thamani ni lazima angeniambia anaye mtu ingawa nilipomtazama macho yake ilionekana kabisa anasema uongo.

Niliwasha mchuma nikaondoka zangu kuelekea Magomeni kupeleka zile bidhaa na baada ya kufika kama kawaida niliziweka pale mezani kisha nikafunga mlango nikaondoka zangu, sasa kwakuwa ilikuwa bado mapema, nilirudi hadi pale nilipokuwepo mwanzo kwa ajili ya kuendelea na makamuzi ya bia. Muda uliposogea niliamua kuondoka kuelekea Magomeni ili kuweza kuufungua mlango wa Maya, nilipofika nilipaki lile gari kisha nikaingia ndani nikafungua mlango wa kwenye kile chumba cha Maya kisha nikauacha wazi nikatoka zangu nje.

Kwakuwa nilikuwa nimeshiba, niliingia kwenye ile gari nikafunga mlango nikawa nasubiri mida mida ifike ili niweze kumtazama Maya kwa uzuri ili kujiridhisha. Mpaka wakati huo sikuiona simu ya Ally Mpemba wala nini! Niliendelea kusubiri nikidhani angenipigia kama alivyokuwa ameniahidi lakini haikuwa hivyo.

Ilipofika mida ya saa 3 usiku nilianza kusikia yule kiumbe Maya akitafuna kile chakula chake kwa sauti kama mara zote ambavyo huwa akifanya. Nilifungua mlango wa gari taratibu kisha nikasogea hadi dirishani ambako kungeniwezesha kumtizama vizuri kwakuwa nilikuwa nimewasha taa na kufungua lile pazia. Nilisogea hadi pale dirishani kisha nikaanza kumtizama kwa makini sana, sasa wakati namtizama yeye alikuwa amenipa mgongo, nilijaribu kumuangalia kwa umakini mkubwa sana na kiukweli walifanana kila kitu na Faraha, kuanzia urefu hadi umbo, ile alama ya mkononi nilijaribu kuitazama lakini sikuweza kuiona kwakuwa muda wote mikono alikuwa ameshika chakula chake akiendelea kula, hivyo kufanya nisiweze kuitazama vizuri.

Sasa wakati nikiwa namtazama aligeuka ghafla kama mtu ambaye alihisi kitu akawa anaangaalia pale dirishani huku akiacha kutafuna kwa mshangao, nilisogea pembeni ili asinione, baada ya muda nilipochungulia pale sebuleni sikuweza kumuona tena akawa amendoka. Nilirudi zangu kwenye gari nikiwa najiuliza sana maswali mengi, kumbuka pamoja na mambo yote ikiwemo kulala na Maya lakini ni kiumbe ambaye sikupaswa kumzoea na hakuzoeleka.

Ilipofika mida ya saa 5 usiku nilisikia honi ikipigwa getini na ilikuwa ni honi ya lile gari alilokuwa amechukua Farah, niliondoka nikaenda kumfungulia geti kisha akawa ameingiza gari ndani. Aliposhuka kwenye ile gari akawa ameniambia anahitaji kuingia ndani kwenda kujisaidia.

Mimi "Habari za huko dada"

Farah "Nzuri, ndiyo narejea!"

Aliendelea "Nilidhani huenda nisingekukuta ila nimewasiliana na kaka Ally ameniambia upo"

Aliendelea "Ngoja nijisaidie kidogo nimebanwa"

Nilitaka kumzuia asiingie ndani lakini nilishindwa kumzuia kwasababu nilifahamu kabisa ni ndugu yake na Ally Mpemba pia walitoka kuongea muda si mrefu. Hapo awali Ally Mpemba aliwahi kuniambia sipaswi kabisa kumruhusu mtu yeyote kuingia ndani ya ile nyumba yake hata akiwa ndugu yake, kitu alichoniambia Ally Mpemba ambacho naweza kufanya ni kuruhusu ndugu zake tu kukalia kiti cha mbele kwenye gari aliyokuwa amenipatia kupigia misele lakini mtu mwingine hakuruhusiwa.

Sasa kabla hata sijamwambia chochote, nilishitukia kufungua mlango na kuingia ndani, kitu cha ajabu wakati Maya amemaliza kula nilikuwa bado sijasafisha pale sebuleni na mara zote huwa nasafisha asubuhi, sasa nilitaka kumwambia Farah atumie choo cha nje ili asingiingie ndani ambako kungeleta taharuki, niliingia ndani pale sebuleni lakini sikumuona Farah nikiamini huenda alikuwa ameingia chooni, nilianza kusafisha ile meza na pale chini kwa haraka, kabla hata sijamaliza nilimuona anafungua mlango wa chumba cha Ally na kutoka.

Kilichonishangaza zaidi ni kwamba ule mlango nilikuwa nimeufunga na funguo na funguo mara zote zilikuwa zinakaa kwenye kimeza cha luninga, nikajaribu kuzitazama funguo nikakuta zipo pale kwenye kimeza, sasa nikawa najiuliza ule mlango sikuufunga? Na kama nisingeufunga zile funguo zisingechomoka pale mlangoni! Na kwanini ameingia kwenye chumba cha Ally akashindwa kwenda chooni ambako vyoo vilikuwa vinajitegemea?.

Kiukweli hofu ilianza kuniingia na kwakuwa nilikuwa mtu mzima nilitambua fika yawezekana Farah hakuwa mtu wa kawaida.

Farah "Mimi nakwenda!"

Mimi "Sawa dada nikusindikize?"

Farah "Hapana"

Mimi "Sawa dada usiku mwema tutaonana kesho"

Farah "Panapo majaaliwa"

Baada ya kuondoka Farah kiukweli sikuelewa ile hali.

INAENDElea......

Asteria anakusalimia
 
NO BLOCKING BUTTON NO STORY
Kwa hiyo unataka kubadili "terms and conditions" za jamiiforums? Yaani ung'ang'anie kitu uongozi mzima wa jamiiforums ukusikilize wewe! Wewe nani bwana, wewe si bodaboda tu. Hiyo button haitakaa iwekwe kwani inaleta kitu inaitwa 'udikteta' yaani unataka uandike unavyotaka mtu yeyote asiwe na uwezo wa kuku-challenge?
 
Nisikuchoshe na usinichoshe, tusichoshane!.

Kwanza kabisa nipende kuwashukuru wote ambao mmeendelea kuwa na mimi bega kwa bega tangia mwanzo wakati naanza kusimulia visa vya maisha yangu ambayo nimeyaishi na kuyapitia kama mwanadamu.

Simulizi yangu ya kwanza kabisa hapa JF imefahamika kama "TULICHOMFANYA YULE MCHAWI HATOKUJA KUSAHAU KAMWE" hii inapatikana kwenye jukwaa hili la Entertainment, simulizi hii iliangazia namna tulivyopata shuruba ya ushirikina wakati ambao nilienda kumsalimia baba yangu mdogo aliyekuwa mwalimu katika shule moja ya sekondari huko mkoani Tabora, kiukweli ni mkasa ambao sitokuja kuusahau kamwe kwasababu ndipo niliamini wachawi wapo na uchawi upo!

Simulizi ya pili ilikuwa ni muendelezo baada ya hiyo ya kwanza, simulizi hii ya pili niliona nianze kusimulia baada ya mimi kwenda shule ya upili(Advance)na wakati nilipomaliza matokeo yangu hayakuwa mazuri hivyo nikatimuliwa na Mzee(Baba)yangu nyumbani nikaingia mtaani kupambana, simulizi hii inafahamika kama "NILIVYONUSURIKA KIFO BAADA YA MZEE KUNITIMUA NYUMBANI" na inapatikana kwenye jukwaa la Habari na Hoja Mchanganyiko.

Sasa leo nimeona niwaletee na niendelee na masimulizi ya maisha yangu ili kuwapa hamasa vijana wenzangu kuweza kupambana na kutokata tamaa mapema! Dhumuni la masimulizi yangu ni kutoa funzo kwa watu na sipo hapa ili kujipatia fedha kwa njia ya ulagahai, mimi binafsi ninajiweza kwasababu ni mpambanaji na sihitaji hata mia mbovu ya walalahoi wenzangu!.

Mimi binafsi ni mfanyabiashara, nimejiajiri kwa kutoa huduma ya usafirishaji wa abiria almaarufu kama Bodaboda, shughuli zangu huwa nazifanyia hapa Bunju, ingawa ki makazi naishi Mbezi Inn ila kikazi nafanyia Bunju. Sasa kama mtakumbuka kwenye simulizi ya mwisho nilisema ya kwamba, baada ya kuwa tumeuza lile duka la vipodozi ambalo tulikuwa tumefungua na rafiki yangu kipenzi Mtatiro (Kwa sasa anaishi nchini Uganda), tuliamua kugawana fedha kila mtu afe na chake, mimi niliamua kurudi zangu Tarime-Sirari, baada ya kukaa kule kuna ndugu yangu(Mtoto wa Baba yangu mkubwa) tuliwasiliana naye akaniambia nije Dar es salaam ili tufanye biashara ya uuzaji wa vyombo vya ndani kwasababu kwa wakati huo ilikuwa na pesa(Kwa maelezo yake).

Niliianza safari ya kuja Dar es salaam, sasa nilipofika Dar es Salaam pale Ubungo(Kipindi stendi bado haijahamia Mbezi), ile nimefika mida ya saa 5 usiku nikampigia simu mwenyeji wangu lakini majibu toka kwenye simu ni kwamba "Namba unayopiga kwasasa haipatikani, jaribu tena baadae", niliendelea kuipiga ile simu lakini majibu yalikuwa ni hayo hayo!.

Kwakuwa nilikuwa nimechoka, niliamua kumsikiliza moja ya watu ambao walikuwa wakinisumbua ili wabebe mzigo wa begi langu ili niwalipe posho, mpaka wakati huo nilikuwa makini sana kujilinda mimi binafsi pamoja na mzigo wangu, kilichofanya nikawa makini kupita kiasi ni stori ambazo mara zote nimekuwa nikizisikia kuhusu Jiji la Dar es Salaam na vioja vyake.

Mimi " Mwanangu vipi!?"

Jamaa " Poa bro"

Mimi "Mbona mnavurugu, shida ni nini?"

Jamaa " Si huyu msenge, nimemwambia wewe ni wakwangu lakini hataki kusikia"

Mimi "Ok mnasemaje"

Jamaa "Bro we nipe begi mi nikubebee, achana na huyu muhuni atakuibia"

Mimi " Sasa wote mnang'ang'ania mzigo, nimpe nani na nimwache nani?"

Mimi "Sa sikia, begi langu nitalibeba mwenyewe, achaneni na mimi"

Baada ya kusikia lafudhi yangu na namna nilivyochukia nadhani waliamua kutii sheria bila shuruti, waliondoka wakiwa wananiangalia kwa uchungu na maumivu makali ya kukosa posho! Kiukweli muda huo nilichokiongea ndicho nilichokuwa nikikimaanisha, kutokana na sifa mbaya za mkoa wa Dar es Salaam nilikuwa nimesema yeyote ambaye angejitia kimbelembele kunikaba au kuniibia, basi siku hiyo ndiyo ingekuwa mwisho wa maisha yake! Jeuri na kiburi cha kikurya vilinitia morali maradufu na niliwaona wale vijana wa pale stendi ni kama wanawake tu wasiokuwa na uwezo wa kunifanya chochote!.

Niliamua kujisogeza mpaka kwenye geti la kutoka nje, nilipotoka nje nilikuwa nikiendelea kushangaa pilika pilika namna zilivyokuwa za kutosha pale stendi, kiukweli sikuwahi kuona mji uliokuwa na pilika nyingi kama Dar es Salaam.

Mwanza nimekaa lakini hakukuwa na harakati za kutosha kama Dar es salaam. Nilichukua simu yangu nikawa nampigia tena mwenyeji wangu lakini simu yake ikawa haipatikani. Nilichukia sana kwasababu nakumbuka nilivyofika Singida alinipigia simu nikamwambia ya kwamba nimefika Singida na akawa amesema ikifika mida ya saa 2 usiku angekuwa amekuja pale stendi ili anisubiri nikifika tuondoke wote.

Kuna jamaa mmoja alikuwa kando ya geti la kutokea nje ya stendi pale Ubungo nilimsogelea nikawa namuuliza kuhusu Guest House yeyote iliyokuwa karibu ili niende nikalale na ikiwezekana asubuhi niendelee kumtafuta jamaa.

Jamaa "Sasa tutafanyaje ndugu!"

Aliendelea "Mwenyeji wako hajatokea?".

Mimi "Nimempigia simu lakini hapatikani!"

Jamaa "Duuuu mbona ni hatari!"

Aliendelea "Sasa sikia, wewe nyooka na hii barabara, unaona kwenye ile njia?"

Mimi "Ndiyo"

Jamaa "Hebu subiri"

Jamaa " Hassaniiiiiii"

Baada ya ya kuita hilo jina muhusika alifika

Jamaa "Hassani hebu nenda kampeleke huyu jamaa pale kwa Asteria, ukifika mwambie jamaa anataka chumba"

Aliendelea "Kaka nenda na jamaa atakupeleka kwenye Lodge ambayo kuna usalama na vyumba vipo vya kutosha, ila utamlipa maana kuna umbali"

Mimi "Hakuna tatizo"

Basi yule jamaa aliyeitwa Hassan akanichukua akanivusha barabara tukaikamata njia ya Ubungo Maziwa kuelekea kwenye hiyo lodge ambayo nimeambiwa kuna usalama na vyumba vya kutosha. Wakati tunakwenda na Bwana Hassan tulikuwa tunapiga stori za hapa na pale huku mikono yangu ikiwa bize imeng'ang'ania begi kwasababu ndilo lililokuwa na hela pamoja na nguo za kubadilisha, kiukweli nilikuwa nimesema endapo yeyote angejipendekeza kunikaba angejuta kuzaliwa.

Baada ya mwendo mrefu kidogo hatimaye tukawa tumefika kwenye Bar moja iliyokuwa inapiga mziki kwa sauti kubwa huku kukiwa na watu wengi.

Hassan " Nisubiri hapa nakuja"

Nilimsubiri Hassan pale nje baada ya kufika kwenye hiyo Bar na baada ya dakika 15 akawa amekuja kunichukua na kuongozana nae kuingia ndani. Tulipofika ndani ambako kulikuwa na kaunta, Hassan alinichukua tena kuelekea Uani ambako nilikuta kuna vyumba vingi ambavyo vilikuwa havipungui 10.

Sasa baada ya kufika pale Uani alikuja mwanamke mmoja mweusi mnene na ndiye aliyekuwa akiitwa Asteria, alimuita Hassan Pembeni wakawa wanaongea, sikufahamu kitu walichokuwa wanazungumza kwa wakati huo. Baada ya yale mazungumzo Hassan alirudi kwangu.

Hassan "Sasa bro,mimi nadhani nikuache wewe upumzike, niangalizie basi ustaarabu"

Mimi "Chumba changu cha kulala ni kipi?"

Hassan "Atakuonyesha Asteria, wala usijali kaka hapa ni nyumbani"

Baada ya maneno ya kutia moyo ya Hassan nikachomoa shilingi elfu 5 nikawa nimempatia kama posho ya kunipeleka hapo Guest.

Hassan "Aaah kaka hela gani hii?"

Mimi "Hela gani kivipi?"

Hasaan "Aaaah Kaka yaani nikutoe kule stendi na nimeacha shughuli zangu halafu unanipatia buku tano? Hebu ongeza ongeza kaka angalau kesho niamkie supu"

Sikutaka mambo mengi na yule Jamaa ikabidi nizame tena mfukoni nikatoa elfu 5 nyingine nikampatia, hivyo kufanya jumla kuwa elfu 10.

Baada ya jamaa kuondoka lile eneo nikamfuata yule demu aliyeitwa Asteria ili aje anionyeshe chumba niingie kulala kwasababu nilikuwa nimechoka.

Asteria "Kaka ina maana Hujaambiwa huu si muda wa kulala?"

Mimi "Si muda wa kulala?"

Mimi "Si muda wa kulala kivipi?"

Asteria "Kaka hapa huwa hatulazi watu ila tunakodisha!"

Aliendelea "Hivi vyumba vinakodishwa kwa dakika na masaa, labda usubiri mpaka saa 9 wateja wakipungua ndipo tutakukodishia ulale"

Kiukweli baada ya ile kauli niliishiwa nguvu ghafla, sasa baada ya kuniambia maneno yale yeye aliondoka akaenda kuendelea na shughuli zake akaniacha pale Uani nikiwa sijui cha kufanya, sasa ndipo nilikuja kugundua ya kwamba, vile vyumba vilikuwa vinatumika kwenye biashara ya short time(Biashara ya Ngono),sasa kumbe ile Bar niliyopelekwa, pale nje kulikuwa na wanawake wanaouza miili yao(Dada Poa) na vile vyumba vilitumika kwa shughuli ya short time.

............................................................................................


Utajiri wa rafiki yangu ulivyofanya nikamuamini Shetani - 02.

Kwakuwa muda ulikuwa umekwenda sana na kwakuwa nilikuwa mshamba wa jiji, niliona ni vema nisihangaike kuzurura huo usiku bali niendelee kusubiri na kuvumilia hadi muda ambao yule muhudumu aliniambia vyumba vingekuwa tayari kwa kukodishwa.

Sasa pale ndani kulikuwa na madumu ya maji yaliyokuwa na maji na mengine yalikuwa tupu, niliamua kuvuta dumu moja lililokuwa tupu nikakalia, wakati nimekaa nilichukua tena simu yangu nikaanza kumpigia mwenyeji wangu lakini bado hakukuwa na mafanikio, niliwaza nimpigie mama yangu lakini kwakuwa ilikuwa usiku sana sikutaka kumsumbua. Niliendelea kuvumilia pale uani huku nikishuhudia madada poa ambavyo wakibadilisha wanaume kama mvua, ilikuwa kila baada ya dakika moja kuna ambao walikuwa wanatoka vyumbani na wanaume na wengine wakiingia, ilikuwa ni kuingia na kutoka! Kelele za muziki na mioshi ya sigara ilifanya nikalichukia lile eneo kwa ule muda lakini sikuwa na namna ilibidi nivumilie tu angalau pakuche.

Baada ya uvumilivu wa muda mrefu, ilipofika muda wa saa 9 usiku, yule muhudumu aliyeitwa Asteria alikuja akawa ameniambia ni muda sasa wa mimi kuingia kulala!.

Asteria "Kaka chumba hiki hapa nadhani unapaswa ulipie ili uweze kulala"

Mimi "Ni shilingi ngapi?"

Asteria "Ngoja nikuitie mtu anayehusika na vyumba"

Asteria " Aminaaaa"

Aliendelea " Wewe Aminaaa"

Amina "Abeeeee"

Asteria "Haya mteja wako huyu"

Amina " Anataka chumba?"

Asteria "Eeeh"

Amina "Jamani mapema yote hii!"

Asteria "Huyu kaka amesubiri sana msaidie bhana"

Amina "Haya anipe Elfu 20"

Basi kwakuwa nilikuwa nimechoka sikutaka kabisa majibizano na mtu,nilichomoa elfu 20 nikampatia huyo muhudumu kisha nikaingia zangu kwenye chumba nilichokuwa nimeonyeshwa na Asteria.

Nilipoingia mle ndani kwenye kile chumba kiukweli hakustahili mwanadamu mwenye akili timamu kulala kwasababu kilikuwa kichafu sana, uchafu ninaouzungumzia hapa si uchafu wa takataka bali ulikuwa uchafu wa taka mwili, nilikuta kondomu zimetupwa ovyo japo kulikuwa na kidastibini kidogo lakini sijui ilikuwa ni dharau au ni nini maana kondomu zilitupwa tu chini zikiwa na shahawa ndani yake, dirisha la kile chumba pia kulikuwa na pazia lililokuwa chafu kupita kiasi, nilipotazama ukutani ndiyo usiseme, nadhani ule ukuta watu waliokuwa wakiingia mle ndani walikuwa wakiiutemea mate au kuukojolea kwasababu ulikuwa umejaa michirizi ya rangi ya kahawia na njano iliyokuwa imekauka na hivyo kuufanya ukuta kuonekana mchafu.

Godoro lenyewe pia lilikuwa na kava tu llililokuwa limechakaa na lilikuwa limechoka hatari! Kiukweli kutokana na ile harufu ya ule uchafu nilitoka ndani nikaelekea kwenye korido aliyokuwa amekaa yule dada aliyeitwa Amina.

Mimi "Sista mbona kile chumba ni kichafu!"

Amina "Kaka vyumba vyote hapa ndivyo vilivyo kama hutaki kulala unaweza kukaa nje!"

Mimi "Kwani hakuna chumba ambacho angalau ni kisafi?"

Amina "Hebu twende"

Basi yule dada alinyanyuka kwenye kiti akawa ametangulia na mimi nikamfuata nyuma kama mtu na mke wake!.Alianza kufungua chumba kimoja baada ya kingine vile ambavyo havikuwa na watu.

Amina "Je hiki kitakufaa?"

Nilikisogelea kile chumba na kutazama kwa ndani ili nione kama kitafaa.

Mimi "Angalau hiki"

Amina "Sawa"

Niliingia ndani ya kile chumba nikafunga mlango kisha nikakaa zangu kitandani nikiendelea kukitazama. Kile chumba hakikuwa na tofauti kubwa na kile cha kwanza sema hiki cha pili angalau sikukuta kondomu chini na godoro lake halikuchoka sana kama lile la kwanza, japo kulikuwa na kiharufu fulani cha kukera lakini sikuwa na namna ilibidi nivumilie pakuche!. Nilivua viatu kisha nikapanda kitandani kujiegesha, mle ndani hakukuwa na shuka wala taulo, mimi niliamua kulala na nguo zangu angalau zikanisitiri na kiubaridi kile cha Alfajjri.

Mida ya saa 3 asubuhi nilishitushwa na kelele za watu wakiwa wanafokeana hapo nje, niliamka zangu nikavaa viatu kisha nikachukua begi langu nikalitia mgongoni nikatoka nje, nilipotoka nje nikawakuta kina dada wawili wakiwa wanatambiana kwa matusi kedekede! Niliwashangaa namna walivyokuwa wakiporomosheana matusi ya nguoni bila aibu, sikutaka kupoteza muda kwenye mambo ya kijinga, niliondoka zangu kuelekea nje nione nitaianza vipi siku kwenye hili jiji ambalo ndiyo ilikuwa mara yangu ya kwanza kufika!.

Nilichukua simu yangu nikaanza kumtafuta mwenyeji wangu lakini simu haikupatikana hewani kabisa, kiukweli nilibaki najiuliza maswali mengi sana ambayo hayakuwa na majibu. Jamaa ndiye aliyefanya mimi kuondoka Tarime na kuja Dar es Salaam na wakati nikiwa kwenye gari tulikuwa tukiwasiliana naye kutwa nzima, sasa sikufahamu ni kitu gani ambacho kilimpata hadi asipatikane kwenye simu. Niliamua kumtafuta mama yangu na kumueleza kila kitu kilichokuwa kimetokea.

Mama "Sasa utafanyaje?"

Aliendelea "Ndugu wa upande wa baba zenu niliwahi kuwaambia huwa wana tabia za kijinga lakini huwa hamnisikii!"

Mama "Sasa kama mliongea na akajua unaenda kwanini hapatikani kwenye simu?"

Aliendelea "Mpigie mjomba wako Nicholaus"

Mimi "Sinaga namba yake mimi"

Mama "Hebu subiri"

Basi baada ya mazungumzo ya muda mfupi na mama yangu alikata simu, Mama yangu alishangaa sana mimi kwenda Dar es Salaam bila taarifa na kibaya zaidi alikuwaga hapendi kabisa sisi wanae kwenda upande wa baba zetu kwasababu hawakuwaga na msaada zaidi ya masimango na manyanyaso.

Baada ya dakika kama 10 kuna namba ngeni ilinipigia simu ikabidi nipokee kwa uharaka na nilidhani uenda atakuwa jamaa ametumia namba nyingine.

Sauti ya Kiume "Wewe uko wapi?"

Mimi "Nani mwenzangu?"

Sauti ya kiume "Mjomba wako Nico hapa"

Mimi " Ooh Anko shikamoo!"

Anko Nico "Kwahiyo sikuhizi umesahau kikurya hadi uniamkie Kiswahili?"

Mimi "Hapana Anko"

Anko Nico "Haya bhana"

Aliendelea "Wewe unakujaje mjini bila taarifa? Au unadhani hapa ni Mogabiri?"

Mimi "Niliwasiliana na Kileri Anko sema nilipofika nimejaribu kumpigia hapatikani!"

Anko Nico "Huyo Kileri ni nani?"

Mimi "Ni mtoto wa Ba'mkubwa"

Anko Nico "Hapa ni mjini hebu acha ujuaji wa kijinga, sema uko maeneo gani nitume mtu aje akachukue"

Basi nilisogea eneo moja nikamuuliza jamaa mmoja pale ni wapi akawa ameniambia ni Ubungo Maziwa, ndipo nilimpa Anko Nico taarifa.

Anko Nico "Uliza mtu yeyote hapo jirani akuonyeshe jengo la Ubungo Plaza lilipo na uende hapo ukasubiri kuna mtu namtuma anakuja kukuchukua"

Mimi "Sawa anko"

Niliuliza watu bahati nzuri nikawa nimeonyeshwa jengo la Ubungo Plaza na nikaliona kwakuwa lilikuwa refu, nilitembea mdogo mdogo huku nikiwa makini sana na begi langu mgongoni asije kibaka yeyote akanikwapua akakimbia. Nilipofika hapo Ubungo Plaza nilimpigia Anko Nico simu kisha akawa ameniambia kuna mtu amempatia namba yangu ya simu akifika hapo atanipigia simu.



............................................................................................




Utajiri wa rafiki yangu ulivyofanya nikamuamini Shetani - 03


Nilisimama pale kando ya lile jengo la Ubungo Plaza huku nikiendelea kuwa makini sana, baada ya muda wa nusu saa kuna namba nisiyoifahamu ikanipigia.

Mimi "Hallo"

Yeye "Hallo, mambo vipi"

Mimi "poa, nani?"

Yeye " Ah mh! Wewe si ndiye mgeni wa Mzee Nicolaus?"

Mimi "Ndiyo"

Yeye "Ameniambia upo Ubungo Plaza nije nikuchukue"

Aliendelea "Umesimama eneo gani?"

Mimi "Nipo mbele ya hili jengo kaka, mbele kabisa ya mlango wa kuingia"

Yeye "Ok sasa vuka barabara uje upande wa pilipili unaiona hii gari nyeusi Prado imepaki hapa pembeni?"

Aliendelea "wewe si ndo umevaa shati la damu ya mzee na suruali ya kaki?"

Mimi "Ndiyo kaka, umeniona?"

Yeye "Nishakuona, vuka uje nakusubiri"

Nilivuka ile barabara kwa umakini mkubwa huku nikiendelea kushangaa magari namna yalivyokuwa mengi barabarani, wakati nimefika jiji la Dar es Salaam hii barabara ya kutoka Manzese hakukuwa imejengwa miundombinu ya Mwendokasi, hivyo haikuwa rahisi kuivuka ile barabara kwasababu magari yalikuwa rafu sana!. Nilipofika kwenye ile gari jamaa aliyonielekeza niliisogelea kisha nikamgongea kioo akawa amekishusha.

Jamaa "Shwari?"

Mimi "Swari kaka"

Jamaa "Ok Ingia twende"

Nilipanda kwenye ile gari nikaa mbele ili iwe rahisi kuyatazama maeneo ya jiji kwa uzuri zaidi. Wakati tupo kwenye gari hatukuwa na stori sana kwasababu jamaa muda wote alikuwa akiongea na simu.

Baada ya dakika kadhaa tukawa tumefika kwenye nyumba nzuri mno iliyokuwa na geti, ndipo jamaa alipiga honi akawa amefunguliwa geti, baada ya mimi kuteremka jamaa aliondoka na ile gari. Kiukweli ile nyumba ilikuwa nzuri sana na nilipokuwa mwenyeji ndipo niligundua Anko Nico alikuwa akiishi eneo la Ununio -Bahari beach.

Historia fupi ya Anko Nico.

Kiukweli mimi tangu nimekuwa, wajomba zangu nimekuwa nikiwaona Tarime wakiwa wamepita kumsalimia dada yao(Mama yangu), sikuwahi kuzifahamu familia zao na hata makao yao, na mara zote wakati wanapita hapo Tarime huwa wanakuja wenyewe. Hivyo ilikuwa tu ni eidha mama atuambie kuna mjomba wako anaishi sehemu fulani na mwingine yupo sehemu fulani.

Kaka zake mama ambao ni wajomba zangu, wapo wanne(4), Mmoja yupo Serengeti ni muajiriwa wa Tanapa, Mwingine ni Mwanajeshi aliwahi kuwa hapo Lugalo lakini siku hizi amehamishiwa Kigoma, mwingine anaishi na familia yake huko Botswana na mwingine ndiye huyu ambaye nilikuwa kwake, kwa bahati nzuri wote nimewahi kuwaona ila sikuwahi kuishi nao.

Kumekuwa na sintofahamu mara zote katika familia mbili na huwa sifahamu shida ni nini, kwa upande wa kina Baba nilikuwaga nikizingua au kufanya kosa lolote, wakati baba akiniadhibu alikuwa akiniambia nimechukua akili za kipumbavu za ujombani, vilevile mama nae alikuwa akisema upande wa kina baba wana roho mbaya na tabia za kipumbavu, sasa sikuwahi kufahamu ni kitu gani kilikuwa kinaendelea kati ya familia hizi mbili.

Anko Nico alikuwa ni Contractor na Mkewe hadi leo ninapoandika yupo anafanya kazi wizara ya Afya, Anko Nico kwasasa ni marehemu, hivyo mkewe ndiyo kila kitu kwenye familia yake kwasasa.

Nimeona nitoe historia fupi kidogo ili huko mbele maswali yapungue.

Basi baada ya kuachwa pale ndani ya fensi kulikuwa na ukimya wa ajabu, ni ndege tu ambao nilisikia wanalia kwenye miti, kiukweli mazingira yale ungedhani wanakaa mawaziri au viongozi wenye vyeo vikubwa Serikalini kwasababu kulikuwa kuzuri na kutulivu mno! Baada ya muda nikiwa nashangaa, mlango ulifunguliwa akawa ametoka nje binti mmoja aliyekuwa amevalia mavazi ya jikoni(Yale mavazi yanavaliwa na wapishi wakiwa jikoni wanapika).

Yule binti "Karibu"

Mimi " Ahsante"

Yule binti "Unaitwa nani?"

Mimi "Umughaka"

Yule binti "Kumbe ndiyo wewe!"

Tulipofika ndani nikaa kwenye kochi nikawa nashangaa namna watu walivyokuwa wakiishi, wakati naendelea kushangaa mara simu ya mezani ikawa inaita, yule binti akawa amekuja kuipokea.

Yule binti "Eeh amefika baba"

Aliendelea "sawa baba"

Baada ya yale maongezi yule binti akawa ameikata ile simu na kuondoka kwenda kuendelea na alichokuwa anakifanya.

Yule binti alipoivishwa chakula kilitengwa na kunitaka niende nikajisevie, nilinyanyuka zangu nikaenda kupakua msosi na kuanza kula, nilipomaliza kula yule binti alinionyesha chumba ambacho nilipaswa kwenda kuoga na ndipo ningelala kwa siku hiyo, sasa nilipofungua na kuingia ndani nilimkuta mzee mmoja akiwa amelala huku ikionekana kabisa afya yake imedhoofika kwasababu nilikuta amewekewa mpira wa kukojolea, yaonyesha hata kokojoa mwenyewe tu alikuwa hawezi.

Nilipoufungua ule mlango na kuingia ndani akawa ameshituka na kugeuka kwa shida kunitazama.

Mimi "Shikamoo"

Mzee "Marhaba"

Baada ya salamu sikuwa na stori zaidi ya kuendelea kumshangaa mzee huku na yeye akinitazama kwa umakini. Kwakuwa alikuwa amewekewa mpira wa kukojolea nilifahamu kabisa ni mgonjwa na hivyo ikabidi nimpe Pole.

Mimi "Pole sana mzee wangu"

Mzee "Pole ya nini mwanangu!"

Mimi "kwa maumivu mzee"

Mzee "Aaah haya nilishayazoea muda tu"

Aliendelea "wewe ni nani?"

Mimi "Mimi naitwa Umughaka, Nicolaus ni mjomba wangu"

Mzee "Oooh sawa"

Kwa namna mzee alivyokuwa akiongea alionyesha kabisa ni mtu kutokea pande za kaskazini mwa nchi yetu.

Nilivua nguo nikawa nimeingia bafuni kuoga, sasa wakati nikiwa bafuni nikawa nasikia simu yangu inaita mpaka ikakata, nilipomaliza kuoga moja kwa moja nilienda kuitazama na ndipo nikakuta ni mtoto wa baba mkubwa Kileri alikuwa akinipigia. Nilibadili nguo kisha nikampigia.

Kileri "Mwanangu nisamehe sana, uko wapi?"

Mimi "Nipo kwa Anko Nico"

Kileri "Maeneo gani kaka nije kukuchukua"

Mimi "Usijali niko salama kabisa kaka, nadhani nikitoka huku nitakufahamisha"

Kileri "Daaah nisamehe sana kaka, simu yangu huwa inasumbua betri, jana ilizima"

Mimi "Ungetumia hata simu ya mtu kaka"

Kileri "Tatizo namba yako sijaikariri kaka!"

Mimi "Usijali kaka hakuna kilichoharibika"

Kileri "Poa mwanangu lakini hakikisha huchelewi ili tupambane"

Mimi "Nikitoka huku nitakushitua"

Baada ya yale maongezi na Kileri nilitoka mle chumbani nikarudi zangu sebuleni. Nilikaa pale sebuleni huku nikiendelea kutazama luninga, mida ya saa 9 alasiri kuna mabinti wawili waliingia ndani, mmoja akiwa mkubwa na mwingine mdogo, japo kuwa wote walikuwa na miaka zaidi ya 18 lakini kuna mmoja alikuwa mkubwa kuliko mwenzie, wale mabinti walikuwa watoto wa mjomba Niko na kiukweli sikuwahi kuwafahamu na wao walikuwa hawanijui, waliniangalia na mmoja akanisalimia ila mmoja alikula buyu na kuzama ndani!.

Ilipofika mida ya saa 1 usiku, kuna gari iliingia ndani ya fensi ya ile nyumba na haukupita muda akawa ameingia ndani mke wa Anko Nico ambaye nimewahi kumuona mara moja tu pale Tarime wakiwa wamekuja mmewe kumsalimia mama.

Mke wa Anko "Habari ya siku"

Mimi "Nzuri, shikamoo"

Mke wa anko "Marhaba"

Aliendelea "Tarime wazima?"

Mimi "Wazima kabisa"

Mke wa anko "Wifi yupo?"

Mimi "Yupo mzima kabisa"

Mke wa anko "Karibu"

Baada ya salamu yule mke wa anko alizama ndani kwake huko. Ile familia ilikuwa ni familia ambayo ilikuwa haijali kabisa na kila mmoja alijali mambo yake.

Ilipofika mida ya saa 2 mjomba nae akawa amefika.Tuliongea mambo mengi sana na Anko Nico na alitaka kufahamu nimekuja Dar es salaam kufanya shughuli gani kwasababu aliniambia huu mji bila kuwa na kazi ni vema ningerudi Tarime kuliko kudhani kungekuwa na mteremko wa maisha mazuri. Baada ya kumwambia kilichokuwa kimenileta alielewa na akawa kimya.

Maisha ya hapo nyumbani kwa Anko yaliendelea kama kawaida na sasa nikaambiwa niwe namuangalia yule mzee na kumbadilishia mpira, kumuogesha na hata kwenda chooni nihakikishe niwe namtazama, ingawa alikuwa akijiweza kwa kujikokota lakini alihitaji uangalizi, sasa kumbe yule mzee alikuwa ni baba yake na mke wa mjomba Nico.

Niliona nikiondoka pale kwa Anko na kwenda kwa Kileri nitakuwa kama nimewadharau na niliona naweza kupata tatizo halafu ikala kwangu kwasababu ya kuondoka kwa ujuaji, nilisubiri Anko aniambie sasa ni muda wa kuondoka nikaendelee na shughuli zangu baada ya kunifadhili kwa makazi kwa muda.

Kwakuwa muda na siku zilikuwa zimekwenda, Kileri aliniambia kama inawezekana nimuelekeze maeneo nilipokuwa aje achukue ile hela ili akanunue mzigo wa kutosha aongeze kwenye duka kama tulivyokuwa tumekubaliana ili biashara iendelee kufanyika, sikuwa kabisa na shaka kwasababu niliamini ni mtoto wa baba yangu mkubwa na kwetu anafahamika na mimi kwao nafahamika, hivyo niliona ni vema nimwambie aje mpaka Ununio kuchukua ile hela akaendelee kufanya biashara na faida tuwe tunagawana.

Mipango yote ya ufanyaji wa biashara na upatikanaji wa faida tulikuwa tumeisuka tangu nikiwa Tarime, basi jamaa alikuja nikawa nimempatia ile yote milioni 9 akawa ameondoka.

Maisha yalisonga na jamaa akawa ananipa mrejesho kuhusu biashara na kiukweli kwa mujibu wa maelezo yake ilikuwa inachanganya vibaya hivyo sikuwa na shaka.

Pale kwa Anko walikuwa wakiondoka asubuhi nilikuwa ninabaki mimi na yule binti wa kazi huku mimi nikiendelea kumuangalia yule mzee na kuwa kama mtu wa usafi nje ya nyumba. Kadiri siku zilivyokuwa zinasonga ndipo na mambo yalianza kubadilika, kuna siku nilikuwa nikimsalimia mke wa anko anajifanya hajasikia salamu anasepa, nilidhani huenda ilikuwa ni kawaida kwa mtu mzima kuwa na mawazo kumbe haikuwa kama nilivyodhani.

Kuna siku aliporudi kutoka kazini kwake nikawa nasikia anamgombeza sana mjomba huko chumbani kwao na sikufahamu ni kitu gani kilikuwa kikiendelea.



.............................................................................................



Utajiri wa rafiki yangu ulivyofanya nikamuamini Shetani - 04.


Sasa muda ambao mke wa anko anafika pale nyumbani mimi nilikuwa nyuma ya nyumba ambapo kulikuwa kuna kama kibustani kidogo ndani yake kulikuwa kumepandwa miwa ambayo ilikuwa imekuwa mikubwa na hakukuwa na walaji, niliona nikate zangu muwa nikaa chini nikaanza kutafuna, kumbe aliingia chumbani anakolala yule mzee ambaye ni baba yake na akakuta amejisaidia kitandani na hakukuwa na mtu aliyemwangalia na kumjali, kwa mawazo yake yeye alidhani mimi nimemuona yule mzee na nikamuacha kama alivyo ili aendelee kuteseka!.

Akili na mawazo yake yalimtuma vibaya kwasababu sikuwa nimeingia mle chumbani tangia mchana, pia yule mzee alikuwaga kama na kakiburi fulani hivi ambako kalikuwa ka kijinga, anaweza kuwa amebanwa na haja kubwa wala asiite mtu yeyote, utakuta ameinyanyuka ameingia chooni na amechafua vibaya bila hata kuflashi. Inawezekana alifanya makusudi siku ile ili kunikomoa.

Kumbe muda huo Anko anapewa makavu laivu ilikuwa ni hiyo ishu na bahati mbaya sana Anko wangu alikuwaga hakoromi kwa yule mwanamke bali hasira za kugombezwa na mkewe zilikuwaga zinaishia kwa wanae au mimi kwa wakati ule nipo kwake.

Muda huo ambao nipo zangu natafuna miwa sina habari, kumbe alimwambia yule mfanyakazi akaingia mle ndani akatoa yale mashuka akawa amemnyanyua mzee akampeleka bafuni mzee akajisafisha kisha akatandika shuka safi na kuweka mazingira ya chumba poa.

Mimi sikufahamu chochote kwasababu nilipomaliza kula miwa nikazunguka kule mbele ya nyumba ndipo nikakuta gari ya mke wa anko ikiwa imepaki nikajua atakuwa amerudi, sikutaka kuingia ndani kwasababu ilikuwa bado mapema, niliingia stoo nikachukua fagio la nje nikaanza kufagia pale nje.

Nilipomaliza niliingia ndani kuoga na kubadili nguo ili nije nikae sebuleni nitazame luninga, wakati naingia mle ndani nilikuta mzee amelala na kitandani kukiwa na shuka nyingine, sikufahamu kumbe dakika chache zilizopita hali ya mle ndani haikuwa nzuri, sasa huo usiku anko alivyorudi ndipo mkewe akamuamshia mtiti!.

Baada ya hayo malumbano Anko alivyorudi sebuleni alikuwa amebadilika na sikutaka kusema chochote mimi niliendelea kutazama luninga, chakula kilipotengwa alielekea kula na alipomaliza aliingia chumbani kwake!. Mkewe yeye sikuonana nae kwa siku hiyo.

Asubuhi kama kawaida wao waliondoka wakawa wamelekea kazini, pale nyumbani nikawa nimebaki mimi, yule binti wa kazi pamoja na mtoto mkubwa wa anko ambaye naye aliondoka ilipofika mida ya saa 3 asubuhi. Sasa baada ya yule mtoto wa Anko kuondoka, yule binti wa kazi alikuja kuniita nikanywe chai, muda huo nilikuwa nje napambana kung'olea nyasi kwenye maua yaliyokuwa kando ya fensi.

Binti wa kazi " Hivi jana ulikuwa wapi?"

Mimi "Jana?, Jana saa ngapi?"

Binti wa kazi " Aliporudi Mama"

Mimi "Nilikuwa kule Bustanini"

Binti wa Kazi "Jana mama kagomba"

Mimi "Alikuwa anagomba kuhusu nini?"

Binti wa kazi "Aliporudi aliingia chumbani kwa babu akakuta babu kajinyea, alikuwa anakuulizia mimi nikajua labda umetoka!"

Mimi "Alijenyea saa ngapi? Mbona mchana nilipotoka ndani alikuwa tu vizuri"

Binti wa kazi "Alikusema maneno mabaya sana, we acha tu"

Mimi "Mimi siyo mjinga nimuone huyo mzee akiwa anashida niache kumsaidia, mbona siku zote namuosha na kumpeleka chooni na mpira nambadilishia!"

Mimi "Jana nilikuwa bustanini na sikutoka nje kabisa"

Mimi "Kwani kabla sijaja hapa nani alikuwa akimuangalia mzee?"

Binti wa kazi "Nani zaidi yangu? Wanae tu wala hawana time na babu yao"

Baada ya mazungumzo ya muda kadhaa nilinoti kitu kwa yule dada wa kazi ambacho hakutaka kabisa kuniambia, kwa kifupi yule mke wa anko inaonekana alitoa shiti nyingi dhidi yangu, niliamua kutulia na kutafakari.

Sikwenda kwa Anko huenda kwakusema nimepigwa na maisha ili anifadhili la hasha, nilienda pale kwasababu wakati nafika mjini mwenyeji wangu alikuwa hapatikani, sasa kuna muda nilikuwa nashangaa wanavyonichukulia ni kana kwamba nimepigwa na maisha!.

Baada ya kupata kifungua kinywa niliamua nimsubiri Anko akitoka kazini ile jioni nimuage na kesho yake nisepe niwaache wapambane na matatizo yao na roho zao mbaya. Kweli, usiku ule kabla ya kula tukiwa pale sebuleni tukiangalia taarifa ya habari, nilimwambia kesho mimi nitaondoka.

Anko Nico " Utaondoka kwenda wapi?"

Mimi "Nitaenda kwa yule mtoto wa baba mkubwa"

Anko Nico " Sawa siye tupo"

Baada ya hayo mazungumzo niliona kabisa nilikuwa sitakiwi. Ukiachilia Anko, lakini mkewe na watoto wa Anko walikuwa ni watu ambao hawana time na mtu, tangia nimefika hapo hawakuwahi hata kusema na mimi wala kujua hali ya maisha ya shangazi yao, walikuwa ni watu ambao hawakuwa na muda kabisa, pengine uzungu uliwaharibu au walirithi tabia za kwao mama yao.

Kesho yake nilimuaga yule mzee pamoja na yule binti wa kazi nikaondoka zangu, nilipotoka nje nilitembea hadi kituo cha daladala nikapanda kuelekea Tegeta.

Kwakuwa nilikuwa nimeshawasiliana na Kileri akawa ameniambia anakaa Kivule na hivyo ilipaswa nipande magari yatakayonifikisha Ubungo stendi ya daladala na nikifika hapo nipande za Gongo la Mboto nikashukie Banana kisha nichukue za Kivule.

Namshukuru Mungu nikawa nimefika na jamaa akaja kunichukua tukaelekea kwake. Nilipofika kwa jamaa nilikuta anakaa kwenye nyumba ambayo bado haijaisha na nilikuta mafundi wakiwa wanaweka vigae kwenye vyumba baadhi.

Kileri "Karibu wa kwetu, hapa mimi ndipo naishi na familia yangu"

Mimi "Hongera kaka umejitahidi"

Kileri "Kawaida tu, naipeleka mdogo mdogo mpaka itaisha, mjini hapa ukiwa na kwako unaepuka usumbufu wa kodi"

Baada ya mazungumzo ya hapa na pale, jamaa akawa ameniambia kesho yake tungeenda Tandika ambako alidai ndiko anakofanyia biashara ili nikajionee namna biashara ilivyoshamiri.

Ilipofika asubuhi tuliondoka kuelekea huko Tandika kama alivyokuwa ameniambia. Tulipofika hapo Tandika kuna duka moja la vyombo tuliingia lakini kuna kitu kikanishangaza.



..........................................................................................


Utajiri wa rafiki yangu ulivyofanya nikamuamini Shetani - 05


Jamaa wa duka "Oooh poti mtu mbaya"

Kileri "We mpemba acha zako"

Aliendelea "Jamal yuko wapi?"

Jamaa wa duka "Hapo nje hayupo?,alikuwa anaongea na simu hapo nje"

Kileri "Sijamuona"

Jamaa wa duka "Vipi unataka mzigo?"

Kileri "Ngoja kwanza nichonge na Jamal"

Yalikuwa ni mazungumzo kati ya Kileri(Mtoto wa baba yangu mkubwa) na Jamaa mmoja mwenye asili ya Pemba tuliyemkuta kwenye duka kubwa la vyombo vya ndani hapo Tandika.Sasa nilibaki kushangaa yale mazungumzo kwasababu Kileri alichokuwa ameniambia ni kwamba tulikuwa tunakwenda kuliona duka letu(Mimi na yeye) ambalo tulikubaliana kufungua.Nialiamua kutulia uenda hapo tulipita kwa rafiki zake ambao alikuwa akifahamiana nao hivyo tungeondoka muda si mrefu kuelekea kwenye duka lenyewe.

Baada ya dakika kadhaa kuna Jamaa mwingine aliingia dukani ambaye pia alikuwa na asili ya pemba na Kileri alipomuona alimuita ili waongee nje lakini jamaa ni kama akawa anamkataa!.

Jamaa "Tatizo lako poti mpaka tuanze kusumbuana kwenye simu,mzigo tunakupa lakini kona nyingi"

Kileri "Jamal eeh hebu njoo tuzungumze kaka"

Jamal " Kama ni hii ishu ya vyombo sitakuelewa lakini kama ni ishu nyingine sawa"

Kileri "We siunanijua lakini mimi ni mtu wa dili!"

Basi yule jamaa aliyeitwa Jamal alitoka nje na Kileri akawa ameniambia nimsubiri abonge kwanza na jamaa.Mimi nilikaa pembeni ambako sikuweza kusikia walichokuwa wanazungumza,baada ya mazungumzo ambayo Kileri alikuwa anamsisitiza sana jamaa,walimaliza ndipo jamaa(Jamal) alikuja akaingia dukani kisha wakawa wanaongea na Kileri kama mwanzo.

Jamal " Sasa nadhani Poti hesabu zetu tutazipiga mwezi ujao ili tujue tunafanyaje katika gawio,au unasemaje?"

Kileri "Mi nakuamini sana Jamal hapo hakuna tatizo"

Aliendelea "Basi sawa mi naondoka"

Baada ya mazungumzo yale mafupi Kileri aliniambia tuondoke zetu,sasa tukiwa njiani Jamaa alikuwa akinieleza mambo mengi ambayo sikuyaelewa na mimi niliamua kunyamaza ili niuone mwisho wake utakavyokuwa kwasababu wahenga wanasemaga "Njia ya muongo ni fupi".
Kileri "Wa kwetu lile duka ndipo nimeweka mtaji wako na wangu,hivyo hao jamaa mara nyingi ndio ninaofanya nao biashara na niwatu wema sana"

Mimi "Kama ndivyo haina shida"

Mimi "Kwahiyo faida tunagawanaje?"

Kileri "Faida tunaigawana kulingana na mtaji,kama ambavyo duka unaliona lilivyokubwa na bado kuna stock nyingine iko stoo,hivyo kila mtu huwa anapata chake kulingana na mtaji"

Aliendelea "Mimi sikutaka kuwaambia ya kwamba nipo na mdogo wangu ila pesa niliyowapa waiweke kwenye mtaji wao wanafahamu kama niya kwangu,hivyo tukigawana faida sisi ndiyo tutakuwa tunagawanya faida yetu tunagawana"

Mimi "Kama ndivyo ni jambo jema"

Kileri "Pia mwanzo nilikuwaga nachukua vyombo kwa mkopo natembeza barabarani na majumbani lakini baada ya kupata mtaji niliona niongee na jamaa wakakubali na ndiyo maana wakati tunaongea nilikushauri uje huku tuifanye hii biashara kwasababu ina faida sana"

Hatimaye tulipanda gari tukawa tumeondoka kurudi nyumbani,muda huo mimi nilikuwa naendelea kushangaa pilika pilika za watu katika jiji la Dar es salaam.

Tulivyofika nyumbani kwa jamaa,yeye alitoka akawa ameelekea kusiko julikana mimi nikabaki pale nyumbani huku nikiendelea kutazama mazingira ya hapo nyumbani,mafundi siku hiyo hawakuja kuendelea na ujenzi lakini walikuwa wamemaliza kiweka vigae vyumba viwili.

Mke wa Kileri "Shem ingia ndani tule"

Mke wa jamaa baada ya kuivisha chakula cha mchana akawa amenikaribisha ndani.

Mke wa Kileri "Baba Nyangi ameenda wapi?"

Mimi "Tumefika wote lakini naona sijui atakuwa ametoka!"

Mke wa Kileri "Hawezi kuona kuna mgeni akatuliza miguu"

Mimi "Ngoja nimpigie simu uenda atakuwa jirani"

Mimi "Ndugu pande zipi?,msosi tayari huku"

Kileri "Nyie kuleni wa kwetu nimetoka kidogo ila sichelewi kurudi"

Mimi "Sawa kaka"

Basi sie tuliendelea kula chakula kama kawaida.Ilipofika usiku mida ya saa 2 jamaa bado alikuwa hajatokea,nakumbuka baada ya kumaliza kula niliingia chumbani kutulia kwasababu ile nyumba hakukuwa na umeme hivyo walikuwa wanatumia taa ya mafuta au siku nyingine mshumaa,sasa sikutaka kukaa sana sebuleni kwasababu hakukuwa na cha maana zaidi ya kushangaa kenchi.

Sasa nikiwa nimepitiwa na usingizi,niliamshwa ghafla na kelele za mtu akiita kwa nguvu.Nilipoangalia saa ilikuwa mida ya saa 5 usiku.Nilipoendelea kusikiliza kwa makini kumbe ilikuwa ni sauti ya Kileri,sasa kumbe jamaa alikuwa amelewa chakari na alikuwa akimuita mkewe amfungulie.

Kileri "Wewe mama Nyangi "

Aliendelea "Mama Nyangi fungua mlango"

Baada ya mkewe kuwa kimya,jamaa alikuwa akifyonza huku akiendelea kugonga geti kwa nguvu,sikufahamu kama mkewe ni kweli alikuwa hasikii au aliamua tu kujikausha.Ilibidi niamke nitoke kwenda kumfungulia jamaa geti kwasababu ilikuwa usiku.

Mimi "Kaka nadhani shemeji atakuwa amepitiwa na usingizi"
Kileri "Wakwetu ngoja niingie kulala tutaonana asubuhi"

Jamaa alikuwa amelewa sana na hata kutembea vizuri akawa anashindwa.Sasa baada ya kuingia chumbani ile nimenilaza kidogo nikaanza kusikia anamfokea mkewe akitishia kumpiga,mkewe nae hakuwa mnyonge kwani alikuwa akimjibu kwa hasira na namna ambavyo nilielewa ni kwamba,jamaa tabia ya ulevi ilikuwa ni kawaida yake na yule mwanamke alionekana kumchoka kwasababu hakuwa na msaada wowote.Baada ya muda ulipita ukimya na nilifahamu jamaa atakuwa alilala fofofo.

Asubuhi nilipoamka sikumuona jamaa na baada ya kumuuliza mkewe akawa ameniambia aliwahi kuamka saa 12 asubuhi akaondoka.Sasa niliamua kuchukua jembe nikaenda kumsaidia mkewe ambaye alikuwa anapalilia bustani aliyokuwa amelima bamia pamoja na matemebele sasa tukiwa pale bustanini,mkewe akawa ananiambia kuhusu tabia za jamaa na aliamua kuniambia nikiwa kama mdogo wake na ndugu yake wa karibu ikiwezekana nimshauri jamaa.

Mke wa Kileri "Shemeji usingeamka ungeacha alale nje,mimi unadhani naamkaga usiku?"

Aliendelea "Tena nadhani alirudi kwa ajili yako,mara zote akijua amelewa huwa harudi kwasababu anajua hata akirudi nani wa kumfungulia geti?,kuna siku amerudi sikumfungulia alilala nje ndipo akaanza tabia akienda huko kulewa harudi hadi kesho yake"

Mimi "Aisee mbona ni hatari"

Mke wa kileri "We acha tu shemeji napitia mambo magumu sana kama mwanamke"

Mimi "Mbona Kileri hakuwaga na hizi tabia?"

Mke wa Kileri "Wewe kileri umeanza kumjua tangu lini unasema hizo tabia alikuwa hana?"

Mimi "Kileri nimekaa sana kwao maana ni kwa baba yangu mkubwa hivyo ninamfahamu vema na hakuwaga na tabia hizi za ulevi"

Mimi "Labda alipokuja Dar ndipo amenza hizi tabia"

Mke wa Kileri "Ndugu yako amenikuta Nauza dagaa kutoka Mwanza na nilikuwa na mtaji mkubwa tu,nilipoingia na Kileri kwenye mahusiano nikajua ni mwanaume nimepata kumbe nilikuwa najidanganya"

Aliendelea "Nilikuwa nampatia hela nikijua mwenzangu anaongezea mtaji kwenye biashara kumbe pesa yote niliyokuwa nikimpatia yeye alikuwa akiipeleka kwa malaya zake"

Mke wa kileri "Nilipokuja kugundua shem nakwambia ilikuwa ugomvi mkubwa sana,baadae aliniomba msamaha ikabidi nimsamehe tuendelee kuishi ila sikumpatia hela yangu tena"

Aliendelea "Hii nyumba unayoiona niliijenga na kuisimamia mimi kwa pesa yangu ya niliyokuwa naipata kwenye biashara ya dagaa,japo kiwanja ni cha kwake lakini naamini nisingejenga angekuwa amekwisha kiuza"

Baada ya maelezo ya mkewe kidogo nikabaki kushangaa kwasababu mimi niliamini ile nyumba itakuwa imejengwa na ndugu yangu kumbe haikuwa kama nilivyodhani,yule mwanamke alikuwa ni mzuri japo ilionekana kabisa maisha mabaya naya umasikini ndiyo yalikuwa yakimchosha.

Mke wa Kileri " Tangia mwezi uliopita naona analeta mafundi wanakarabati humo ndani kwa kuweka vigae na hata kile choo anekijenga upya maana cha kwanza kilikuwa cha mabati"

Aliendelea "Mimi hata simuulizi shem maana niliyofanya yanatosha,na yeye sasa ni zamu yake"

Mimi "Kwani Kaka yeye ukiacha biashara ya vyombo huwa anafanya kazi nyingine"

Mke wa Kileri "Biashara ya vyombo?,ndiyo alikwambia anafanya biashara ya vyombo?"

Mimi "Ndiyo,hivyo ndivyo ninavyofahamu"

Mke wa Kileri "Biashara ya vyombo alikuwa anaifanya hata kabla hatujaishi wote,kupitia biashara hiyo ya vyombo ndipo mimi na yeye tulikutana kwasababu alikuwa anapenda sana kunipitishia vyombo kwenye banda langu"

Aliendelea "Kwa namna alivyokuwa mpole na mnyenyekevu nikajua mwanaume ndiyo huyu"

Mimi "Kwahiyo auzi tena vyombo?"

Mke wa Kileri "Biashara ya vyombo kidogo impeleke jela shem,kuna vyombo sijui alikuwaga anakopa kwa tajiri sasa kumbe alikuwa anauza na hela hapeleki hivyo mwenye vyombo vyake akataka kumfunga ndipo ikabidi nichukue hela yangu nikampatia alipe hela ya watu na wakati huo ndiyo tulikuwa wapenzi"

Baada ya maelezo ya mke wa kileri kiukweli moyo wangu uliuma sana kwasababu niliamini hela yangu jamaa atakuwa ameila!.

Mke wa kileri "Angekuwa anafanya kazi kila siku tushindie matembele?"

Aliendelea "Binti yake tu hata viatu vya shule saa nyingine ni mtihani,hadi niwapigie simu ndugu zangu nianze kuomba omba"

Mimi "Mimi nilijua anafanya biashara ya uuzaji wa vyombo na hata kuja Dar nimekuja kwa shughuli hiyo!"

Mke wa Kileri "Kama alikwambia hivyo alikudanganya"

Mimi "Jana tulienda Tandika kwenye duka moja la vyombo akadai hela niliyompatia ameiweka hapo pamoja naya kwake ili kuongeza mtaji na faida ikipatikana tutakuwa tunagawana na wale jamaa"

Mke wa kileri "Ulimpatia shi ngapi shem?"

Mimi "Nilimpatia milioni 9"

Mke wa kileri "Mungu wangu!, unasemaaa!"

Mke wa Kileri alipata mshangao baada ya kusikia nimempatia mume wake pesa nyingi kiasi hicho!.

Mke wa Kileri "Mbona mimi sijamuona na hela?"

Aliendelea "Hiyo hela shemeji andika maumivu,hiyo atakuwa amepelekewa hawara yake"

Mke wa Kileri " Ndiyo maana naona anajitutumua kuweka vigae ndani nikawa najiuliza huyu katoa wapi hela"

Aliendelea "Mwanaume hana chochote cha maana anachofanya na watu walishamfahamu hawampi hata kazi kwasababu ya ujuaji wa mjini(utapeli)"

Kiukweli niliumia moyo sana na nilimwambia mkewe akae kimya asimwambie chochote lakini mkewe akuvumilia ile hali akaamua siku hiyo hiyo kumtwangia simu,jamaa alipojua mkewe amefahamu hakuwahi tena kurudi nyumbani kwa takribani wiki mbili.

Kwakuwa sikuwa na kazi ilibidi niingie mtaani kuanza kusaka kazi ya kufanya ili kujipatia kipato.



............................................................................................





Utajiri wa rafiki yangu ulivyofanya nikamuamini Shetani - 06.


Fedha niliyokuwa nimeitafuta kwa jasho na damu na baada ya kuuza mali za duka letu la vipodozi tukawa tumegawana na rafiki yangu kipenzi ikawa imeishia mikononi mwa ndugu yangu ambaye niliamini tungefanya biashara ikashamiri kama alivyokuwa akiniambia lakini haikuwa kama nilivyodhani!.Nilipanga niendelee kuwa subira uenda mwisho wa mwezi angeenda kwa wale jamaa pale Tandika akapewa faida ya pesa aliyokuwa ameweka hapo dukani kama alivyoniambia,niliamua kuupa muda nafasi ingawa Jamaa baada ya kupewa taarifa na mkewe kuhusu hizo hela alikata mawasiliano kabisa kwa takribani wiki mbili.

Sikutaka kabisa kukaa kizembe pale kwa Kileri,niliamua kuzunguka kutafuta kazi ya kufanya angalau nianze kutengeneza pesa,sasa niliamua kutembea mdogo mdogo kama naelekea Banana na kuna mahali nilifika nikakuta jamaa wanafyatua tofali za blocks,eneo lile halikuwa mbali na nyumbani kwa kileri,ilikuwa takribani mita kama 1000 hivi,nilijisogeza mpaka pale nikawa nimeongea na jamaa mmoja ambaye ndiye alionekana kuwa kiongozi wa ule mradi.

Mimi "Kaka kwema"

Jamaa "Kwema,vipi hali"

Mimi "Safi kaka"

Mimi "Naweza kupata angalau kibarua kaka?"

Jamaa "Kibarua kama kipi unaweza!"

Mimi "Chochote tu kaka"

Jamaa "Unao uzoefu wa kufyatua tofali?"

Mimi "Hapana kaka ila kubeba na kupanga naweza"

Jamaa "Unaitwa nani?

Mimi "Naitwa Umughaka"

Jamaa "Ok sawa"

Aliendelea "Sudiiiiiii !"

Jamaa "Sudi eeeh !"

Sudi "Nambie "

Jamaa "Njoo mwanangu"

Sudi "Nambie "

Jamaa "Jamaa anahitaji kibarua,vp kuna sehemu umchomeke?"

Sudi "Hapa nafasi haziishagi ni nguvu zake tu"

Jamaa "Sawa muangalizieni"

Sudi "Mbona kama umependeza,unataka leo leo au ulikuja kucheki kwanza"

Mimi "Kaka nipo tayari kwa kazi"

Sudi " Hizo nguo huzipendi au!"

Mimi "Nitavua nitabaki na bukta"

Sudi "Sawa,twenzetu"

Baada ya maongezi ya muda mfupi,jamaa aliyeitwa Sudi alinichukia mpaka eneo la kazi kisha nikavua nguo zangu nikawa nimebaki na bukta(boksa),sasa Sudi akawa ameniambia nitakuwa nachukua tofali zitakazokuwa zinafyatuliwa na mashine na kisha kwenda kuzipanga kwenye eneo la wazi lililokuwa limetengwa kwa kazi hiyo.

Niliifanya ile kazi kuanzia muda ule hadj jioni mida ya saa 12,kiukweli haikuwa kazi ya kitoto hata kidogo,kwakuwa niloshafanya kazi nzito na ngumu kuliko ile,sikuona tatizo lolote japo jamaa waliponiangalia walidhani mimi ni lele mama lakini nilipoanza kupiga mzigo hawakuamini!.Eneo lile kulikuwa na kinyumba kidogo na kwa nyuma kulikuwa kumejengwa choo pamoja na bafu,hivyo baada ya kumaliza kazi nikawa nimeingia kuoga,nilipomaliza kuoga,yule jamaa ambaye nilienda kumuomba kazi aliinita akanipatia elfu 3 ambayo ni kama posho ya kibarua.Ilikuwa ni hela ndogo sana lakini sikukata tamaa kwakuwa kwa wakati huo sikuwa na kazi yoyote!.

Baada ya malipo niliondoka zangu kwa kutembea kurudi kwa Kikeri ambapo ndipo nilipokuwa nimefikia.

Niliendelea kuifanya ile kazi kwa siku kadhaa,sasa ilikuwa kwamba mteja amiweka oda ya tofali tunapakia na kwenda kushusha tulikuwa tunapewa posho ya upakiaji na ushushaji elfu 2 kila mmoja,hivyo ukijumlisha na ile posho ya ufyatuaji na ubebaji kwenda kuanika ambayo ilikuwa buku 3,kwa siku nilikuwa napata zaidi ya elfu 10,kwasababu kwenye upakiaji na ushushaji kwa siku tulikuwa tunapata oda hata za wateja 3 hadi 4 kwa siku.

Kuna siku nilipomaliza kazi nimerudi nyumbani pale kwa ndugu yangu Kileri nikamkuta yupo,sasa sikutaka kuzungumza nae pale ndanj ilibidi nimwambie shemu tunatoka kidogo.Dhumuni la mimi kumtoa pale nyumbani nilitaka anieleze ukweli kuhusu ile hela kwasababu ilikuwa ni mwezi umekatika na hakukuwa na mrejesho wowote kuhusu faida kama alivyokuwa ameniambia.

Mimi "Ndugu yangu hujanipa mrejesho wowote kuhusu biashara"

Kileri "Kaka wewe acha tu"

Aliendelea "Kiukweli kaka niwe mkweli,wewe ni ndugu yangu sitaki kukuficha"

Kileri "Ile hela ulinipa nilienda kulipa deni nililokuwa nadaiwa na yule jamaa(Jamal) na kuna kiasi cha fedha niliona nijengee choo kilichokuwa cha mabati"

Aliendelea "Juzi kabla hujaja mama yake mke wangu alisema anakuja sasa nikaona nitengeneze angalau vyumba viwili niweke vigae ili kuwe na muonekano kaka"

Mimi "Kaka ni heri ungeniambia tangu mapema nikiwa Tarime kwamba unashida na hela ningekutumia kwakuwa wewe ni ndugu yangu"

Mimi "Lakini kitendo cha kufanya mimi kuja huku nikiamini tunakuja kufanya biashara wakati ni uongo,umenikosea sana ndugu yangu"

Kileri "Nitampigia Marwa nyumbani nimwambie aniuzie vile vi ndama vyangu halafu nitakulipa,wewe ni ndugu yangu"

Mimi "Wewe acha tu,kama ipo ipo tu kaka!"

Mimi "Wala usijali kuhusu hiyo hela"

Kiukweli nilijisikia hasira sana na nilijiona ni mpumbavu sana kumpatia Kileri ile hela ambayo haikufanya jambo la maana zaidi iliishia kwa wanawake zake na utumbuaji wa starehe,sikukata tamaa niliamini kama niliweza kuipata hiyo hela basi nitaweza kuipata nyingine.Japo alijitahidi kunieleza maneno mengi lakini bado nilimuona ni muongo kwasababu mkewe alikuwa ameniambia kila kitu.

Niliendelea kupambana katika ile kazi ya tofali pasipo kukata tamaa,nilikuwa natafuta hela angalau nikapange chumba changu ili niweze kujisogeza zaidi.Kuna siku nikiwa na jamaa zangu kwenye gari tukiwa tunapeleka tofali kwa mteja,kuna jamaa mmoja nae alikuwa mfanyakazi mwenzangu hapo site alikuwa akituambia kama vipi twende kwenye mradi wa nyumba huko kigamboni uliokuwa ukifahamika kama DEGE.

Mwakisaka " Mwanangu kama mko tayari kesho tuibuke Dege kuna jamaa zangu wako kule wanasema kuna hela nzuri"

Mimi "Dege ndo wapi?"

Mwakisaka "Kigamboni huko kuna nyumba zinajengwa kama utitiri!"

Aliendelea "Halafu kule vibarua kwa siku waliniambia wanakula elfu 15"

Zomela "Tatizo kigamboni ni mbali,hiyo hela inaishia tu kwenye nauli"

Mwakisaka "Sasa hiyo nauli kwani unaenda wapi?,watu huko wamepiga kambi halafu wewe unaongelea masuala ya nauli tena"

Aliendelea "Mimi kesho ngoja niende nikacheki"

Zomela "Tatizo huko unaweza kwenda ukakosa na ukirudi huku nako unakuta wameweka mtu mwingine,tena nianze kufanya kazi kutafuta kazi"

Mwakisaka "Kwani utasema unaenda wapi?,kule tunaenda kimya hivyo si rahisi mtu kujua,tukipata ndo hivyo tusipota tunarudi"

Zomela "Hao jamaa zako wanauhakika?,siyo tunachoma nauli tu!"

Mwakisaka "Aliye tayari kesho twende tukikosa tunarudi"

Baada ya yale mazungumzo nilimwambia Mwakisaka mimi nitakuwa tayari kuungana nae na kuelekea huko Kigamboni kusaka kibarua cha elfu 15.

Mimi "Kwahiyo tutakutana wapi?"

Mwakisaka "Kwani siunasimu?"

Mimi "Ndiyo"

Mwakisaka "Nigei namba yako asubuhi nitakushitua"

Nilimpatia namba yangu ya simu Mwakisaka kisha tukaendelea na mambo mengine.

Ilipofika alfajiri mida ya saa 11,Mwakisaka alinipigia simu na akawa ameniambia tuonane pale Banana na nikifika nimwambie,kweli nilianza kuhangaika na usafiri wa kunitoa huko kivule ambao ulikuwa wa changamoto sana,nilihangaika kupambania usafiri hadi saa 12 asubuhi ikanikuta bado sijapata gari,nilikuja kupata gari imejaa ikabidi nining'inie hivyo hivyo kibishi ilimradi nifike.Nilipofika pale Banana nilimpigia Mwakisaka ambaye yeye alikuwa amefika kitambo akinisubiri mimi!.

Mwakisaka "Shwari?"

Mimi "Shwari kaka"

Mimi "Zomela yuko wapi?"

Mwakisaka "Yule hawezi kwenda,ameshapazoea pale kwa Mushi kama kwao"

Aliendelea "Hapa itabidi tupande magari ya kivukoni"

Tulikaa pale stendi tukawa tunasubiri magari ya kivukoni yaliyokuwa yanatokea Gongo la mboto ili tupande tuondoke,gari nyingi zikawa zinapita zimeshona watu kama utitiri,kiukweli nilikuwa nashangaa sana ile hali kwakuwa hata Mwanza sikuwahi kuona gari zinajaa kiasi kile!.

Baada ya muda kupita kuna gari ambalo lilikuja likiwa angalau na nafasi ya kusimama na tukapanda hilo.



...........................................................................................



Utajiri wa rafiki yangu ulivyofanya nikamuamini Shetani - 07.


Kwakuwa Mwakisaka ndiye aliyekuwa mwenyeji wangu sikuwa na hofu kabisa kwasababu ni mtu ambaye tulifanya nae kazi kwa muda mfupi na alikiwa mtu mwema,baada ya kufika kivukoni(feri)tulikata tiketi za kivuko na tukawa tumefanikiwa kuvuka ng'ambo ya pili,baada ya kufika upande wa pili yaani Kigambo,jamaa aliniambia inapaswa tupande gari zilizokuwa zinaelekea Kibada kwa kuwa ndiyo njia yenyewe hiyo.

Tulifanikiwa kufika hapo kwenye mradi mkubwa kabisa uliofahamika kama DEGE ECO VILLAGE,kiukweli nilikuwa nashangaa sana namna ambavyo watu wanatumia fedha,ule mradi ndugu zangu ulikuwa mkubwa mno,na kwa waliobahatika kufika huko au wanaotokea huko watakubaliana nami.

Hatukutaka kupoteza muda kabisa ilibidi Mwakisaka aniambie tuulizie namna ya kupata kibarua kwasababu tulikuta watu wakiwa wanachakalika kinoma.Kuna jamaa tulimfuata tukaanza kumuulizia namna ya kupata kibarua siku hiyo.

Jamaa "Hapa kwetu yupo foreman ambaye ndiye msimamizi wetu,ukienda kule mbele pia wanae foreman wao"

Mwakisaka "Foreman wenu yuko wapi tujaribu kuongea nae?"

Jamaa "Nadhani atakuwa anazungukia maeneo anayosimamia,subirini tu hapa atakuja"

Tulisogea kando tukawa tunaendelea kuushangaa ule mradi wakati huo tunamsubiri mtu tuliyeambiwa ndiye foreman wa hapo tulipofikia.Baada ya muda wa nusu saa jamaa mmoja mweusi aliyekuwa mnene na kitambi cha kutosha akawa amekuja na ndipo yule jamaa alitukonyeza ya kwamba jamaa ndiye foreman wa lile eneo.Tulimfuata na kumjulia hali jamaa kisha Mwakisaka akaanzisha maongezi nae.

Mwakisaka "Kaka tunatafuta kazi ya kibarua "

Foreman "Aliyewaambia hapa tunaajili vibarua nani?"

Mwakisaka "Hakuna mtu aliyetuambia kaka tumekuja kuona kama tutapata"

Foreman "Hapa hatuajiri kwa sasa,siku tukiajiri vibarua mtapata taarifa"

Baada ya yale majibu ya kukatisha tamaa Mwakisaka aliamua akae kimya kisha jamaa akaanza kuondoka kuzunguka nyuma ya yale majengo yaliyokuwa mbele yetu.Sasa yule jamaa aliyekuwa kibarua pale akawa amemuita Mwakisaka akamwambia bila pesa ni ngumu sana kupata kibarua kwasababu hata wao walihonga ndipo kupata kibarua,jamaa akasema twende tukaongee nae kikubwa.Nilimwambia Mwakisaka hiyo kazi ya kuongea na jamaa aniachie mimi,akikataa basi tungerudi zetu kwa Mushi kule kivule kuendelea na ufyatuaji wa tofali.

Niliamua kuzunguka ule upande alokuwa amekwenda yule foreman na bahati nzuri nilimuona akiwa anaingia kwenye jengo moja,nilitembea kwa haraka ili kumuwahi kabla hajafika kwa watu wengi ikawa shida kuzungumza nae.

Mimi "Kaka kakaa"

Foreman "mmmh nambie"

Mimi "Kaka tusaidie ndugu yangu na kama ni chochote tutakupatia"

Foreman "Wewe si ndo upo na yule mwenzio nimewaambia hamna kazi!"

Mimi "Kaka tusaidie ndugu yangu!"

Foreman "Nyie mnatokea wapi?"

Mimi "Wote tunatokea kivule"

Foreman "Kivule?,sasa kivule hadi kuja kufanya kazi huku hamuoni tutasumbuana?"

Aliendelea "Ni bora hata mngekuwa hapa maeneo ya jirani"

Mimi "Tutaweka kambi maeneo haya kaka wala hilo lisikupe taabu"

Foreman "Hapa jirani haturuhusu watu kukaa kwasababu za kiusalama"

Mimi "Sijamaanisha hapa kwenye mradi kaka,tuta tafuta eneo maeneo ya jirani tutaweka kambi"

Foreman "Tukubaliane,mtanipa elfu tano tano kila siku kwa muda wa wiki moja"

Aliendelea "Na iwe siri,ikiwa vinginevyo mi nitawaruka na kuwageuka"

Mimi "Hakuna tazizo kaka"

Foreman "Kamuite mwenzio mje niwakabidhi huku juu!"

Niliondoka kumfuata Mwakisaka na kumueleza kila kitu jamaa alichosema na jamaa akaniambia hakuna tatizo;Tuliondoka kumfuata yule foreman ambaye alituchukua mpaka kwa jamaa wengine akamuacha hapo Mwakisaka kisha akaniambia tena nifuatane nae,mimi pia akawa amenipeleka kwenye kikosi kingine.
Tukaanza kuifanya kazi ya kibarua rasmi na kwa siku tukawa tunapewa elfu 15,ishu ya kula pamoja na maji ya kunywa ilikuwa ni juu ya yako wewe kibarua uzuri ni kwamba,kwenye kundi ambalo mimi nilikuwepo walikuwa wamejitolea kuchanga fedha na kununua vyakula kisha kuna mtu walikuwa wanamlipa anakuja kuwapikia,hivyo na mimi baada ya kuingia kwenye kundi la wale jamaa niliamua kuchangia elfu 10 kwa kila wiki kwa ajili ya huo mpango.

Miongoni mwa wale jamaa pia walikuwa wametengeneza matenti ya maturubai kuishi hapo maeneo ya jirani,niliamua kichangia fedha na mimi ili kukaa hapo,sasa bahati nzuri ni kwamba wikiendi tulikuwaga tunapumzika na hiyo niliitumia kwenda kufata virago vyangu kwa kaka Kileri na kurudi kambini,sikutaka kabisa kuhangaika na mambo ya jiji la Dar es salaam,fokasi yangu ilikuwa ni kwenye kufanya kazi na kutunza malipo yangu kwenye simu.

Nilipopambana ndani ya miezi mitano kwenye ule mradi nilipata kiasi kisichopungua Tsh milioni 1.3,sasa nilimuomba Mwakisaka aniambie ni eneo gani ni zuri kwa kupanga chumba na angalau linakuwa na maisha nafuu kwa hapa Dar es salaam.

Mwakisaka "Mwanangu mimi nakaa Gongo la mboto na nikuzuri sana"

Mimi "Kwahiyo kipindi kile ulikuwa unatoka Gongo la Mboto mpaka Kwa Mushi?"

Mwakisaka " Nilikuwa nakaa kulekule kivule kwa ndugu yangu mmoja"

Aliendelea "Kama unataka chumba we sema nimpigie simu jamaa mmoja pale kitaa akutafutie chumba"

Mimi "Nahitaji kaka"

Mwakisaka "Basi ngoja nitamcheki mshikaji"

Kweli,baada ya Mwakisaka kuwasiliana na jamaa yake na kumjulisha nilikuwa nahitaji chumba jamaa alianza kutafuta na akasema endapo angepata basi angetujulisha.
Baada ya siku tatu yule jamaa aliyepewa kazi na Mwakisaka ya kutafuta chumba akawa amesema nyumba imepatikana maeneo ya mwisho wa lami lakini ni vyumba viwili ambavyo malipo ilikuwa ni elfu 45 kwa kila chumba na ilipaswa kulipwa kwa miezi 6.

Mwakisaka "Jamaa anasema nyumba imepatikana Gongo la mboto mwisho wa lami"

Mimi "Mwisho wa lami ni maeneo ya wapi?"

Mwakisaka "Hapo hapo Gongo la mboto sema ni mbele kidogo"

Mimi "Sawa,na wewe ndiyo unaishi huko?"

Mwakisaka "Hapana,mimi naishi Mzambarauni"

Mwakisaka "Ila jamaa anasema amepata chumba na sebule kwa elfu 45 kwa kila kimoja na inalipwa miezi 6,vp?"

Mimi "Sawa,hakuna tazizo"

Mwakisaka "Ngoja nimwambie amwambie mwenye nyumba atulie kesho kutwa tukakicheki"

Mwakisaka aliwasiliana na yule jamaa akawa amemwambia amwambie mwenye nyumba jumapili tungeenda kukitazama ikiwezekana nilipie kabisa.

Namshukuru Mungu baada ya kwenda kuingalia ile nyumba niliipenda na nikawa nimelipia miezi sita,hela iliyobaki nikanunua godoro na mashuka nikawa nimeyaweka na mimi kufunga chumba kisha kurudi Kigamboni kuendelea na kibarua.

Kila nilipokuwa ninapata hela nilikuwa nikinunua kitu kimoja baada ya kingine na kuweka ndani na hatimaye vyumba vikawa na muonekano mzuri,kiukweli pamoja na mateso ya kushinda juani niliyokuwa nayapitia kule kigamboni lakini nilihakikisha najinyima kiasi kwamba hadi malengo yangu yatimie.

Ule mradi wa Dege kuna muda ukawa umesimama kidogo hivyo kwa muda ule nikaenda kukaa kwangu nilikokuwa nimepanga,sasa pale nilipokuwa naishi kulikuwa na geti na tulikuwa wapangaji kadhaa na kila mtu alikuwa na ishu zake.

Sasa kuna jamaa mmoja alikuwa akiitwa Steve yeye tulitokea kushibana sana na tukawa marafiki,jamaa alikuwa akifanya kazi kampuni ya Tigo kama msajili line za simu,kwakuwa ule mradi ulikuwa umesimama kwa muda usiojulikana,jamaa aliniambia kama vipi aniunganishe na timu leader wake anipatie kodi ya kusajili line za simu nami nianze kuwa msajili laini.Jamaa aliniambia ni kazi ambayo ilikuwa na pesa sana ila watu walikuwa wakiichukulia poa.

Steve "Ngoja kesho nitamueleza team leader kama vipi akupe kodi ili uanze kufanya kazi"

Mimi "Kazi inafanyikaje kaka"

Steve "Kazi ni nyepesi sana kaka utaelekezwa namna ya kuifanya"

Kwakuwa kwa muda huo sikuwa na kazi baada ya kusimama kwa mradi,niliona jamaa atakuwa amenisaidia sana ili kuweza kujinasua na ukata ambao ulikuwa ukininyemelea baada kuwa nakula hela nilizokuwa nimezitunza bila kuzizalisha.


............................................................................................



Utajiri wa rafiki yangu ulivyofanya nikamuamini Shetani - 08.


Baada ya siku mbili,yule jamaa aliyekuwa mpangaji mwenzangu aliyeitwa Steve alinifuata akawa ameniambia Team leader amekubali.

Steve "Kaka jiandae kesho nikupeleke maana nilizungumza na team leader akaniambia twende"

Mimi "Sawa kaka"

Kweli,tuliondoka na Steve hadi Buguruni kulikokuwa na ofisi ya Tigo,nilipofika hapo nilikuta kuna vijana wengi wakiwa mchanganyiko(KE & ME) na kiukweli kulikuwa na mabinti wazuri sana,Steve aliniambia nifuatane nae hadi ndani na tulipofika ndani alimuita huyo aliyekuwa Team leader akaja nilipokuwa nimesimama.

Steve "Kiongozi huyu mshikaji ndiye nilikwambia ile juzi anahitaji Code"

Team leader " Aahh ok!"

Aliendelea "Hebu nisubirini kidogo nina mazungumzo nakuja!"

Team leader aliondoka akawa ametuacha pale na Steve,Steve nae akawa yuko bize kupiga stori na washikaji zake wengine ambao pia walikuwa wakifanya kazi ya usajili wa line.Baada ya dakika 20 yule Team leader akawa amerudi.

Team leader "Unaitwa nani ndugu?"
Mimi "Naitwa Umughaka"

Team leader "Kanda ya ziwa nini!"

Mimi "Yeah"

Team leader "Ok,sasa nitakupa line ya Code kwa ajili ya kusajilia,na process zote inabidi ukamilishe muda huu ili uondoke na Steven akakuonyeshe kazi inavyofanyika"

Aliendelea "The more u register customers,the more u get more money"

Team leader "Kwa kanuni za sasa kwenye kampuni ni kwamba,kila freelancer atakuwa anapokea Revenue shares every month within six months"

Aliendelea "Mambo mengine yote Steven atakuelekeza"

Team leader "Steve hakikisha jamaa anakuwa poa"

Steve "Hakuna tatizo kiongozi"

Baada ya ufafanuzi mdogo ambao sikuelewa chochote,Team leader aliingia ndani akawa ametoka na tisheti mbili za Tigo zikiwa mpya zenye maandishi yaliyosomeka "Sajili line yako Tigo hapa",pia aliniletea Kofia, na kizibao,hivi vyote vilikuwa na maandishi yaliyohusu kampuni ya mawasiliano ya Tigo.

Team leader "Ukishaelewa tunavyofanya kazi,wiki ijayo nitakupatia Mwamvuli na meza ili uwe na chimbo lako,au unataka kupiga door to door?"

Mimi "Door to door ndo kitu gani?"

Team leader "Naamanisha uwe unasajili laini kwa kutembea tembea?"

Mimi "Nadhani nipe muda nitakujuza njia ipi kwangu itakuwa bora zaidi!"

Team leader "Ok,hakikisha kila siku asubuhi hukosi hapa ofisini kuanzia saa 1 : 30 uwe hapa maana kila siku kuna kuwa na vikao vya maelekezo"

Mimi "sawa,hakuna tatizo"

Baada ya maelekezo hayo,Team leader alimpatia Steve boksi mpya la laini za simu ambazo hazijasajiliwa na kumtaka anielekeze namna ya kusajili wateja.Tuliondoka na Steve kuelekea Tandika ambako yeye alikuwa akifanyia Shughuli zake huko za kusajili line,sasa tulipofika hapo Tandika jamaa alikuwa na tenti lake kubwa (Gazebo) ambalo lilikuwa la kampuni ya Tigo,tulipofika hapo kuna demu tulimkuta ambaye alikuwa na wateja,yule demu alikuwa akishirikiana na Steve kwenye lile tenti kusajili line.

Wateja walivyokuwa wakija nilikuwa nikielekezwa namna ya kusajili line za simu na kiukweli nilielewa ile kazi kwa muda mfupi sana na nikawa nafanya vizuri sana kuwashinda hata niliowakuta mwanzo.Nifahamu hadi kurudisha line za simu zilipotea na nilifahamu mambo mengi sana na nikawa mnyama sana kwenye ile kazi ya usajili wa line.

Baada ya mwezi kuisha na kupokea malipo,Steve alinishauri niongee na Team leader anipatie Meza na mwamvuli niweke kambi sehemu yenye watu wengi niendelee kupiga kazi.

Steve "Kaka kwakuwa umeshakuwa mzoefu,mwambie Kiongozi akupe mwamvuli na meza upige kazi"

Aliendelea "Au unataka kuparasa?"

Mimi "Kuparasa ndo kufanyaje?"

Steve"Kuparasa ni kupiga door to door,kuna wana wanaita kuparasa"

Mimi "Ni bora nitulie sehemu kaka,hili jua na ishu ya kutembea siyo poa"

Steve "Basi mwambie kiongozi akupe meza na mwamvuli au akupe Gazebo kabisa ila utakuwa unakatwa hela"

Niliona alichokuwa ananiambia Steve ni jambo jema kwasababu nisingeendelea tena kukaa pale kwenye Gazebo lao tukiendelea kugawana wateja.Siku iliyofuata baada ya kufika ofisini pale Buguruni,nilimwambia Team leader anipatie Mwamvuli na meza kama vipi niangalie chimbo ambalo litanifaa kupiga kazi.

Team leader "Sasa umepata chimbo la kuweka meza?"

Mimi "Nitatafuta kulekule Tandika kiongozi"

Team leader "Tandika watu wangu wamejaa sana,kwanini usiende kariakoo maana kule kuna watu wengi pia hii itakuongezea revenue maana kule watu wanahela za kuweka vocha"

Mimi "Ok sawa kiongozi ngoja niingie Kariakoo"

Baada ya kunipatia vitendea kazi(Mwamvuli na Meza) nilipanda gari pale Buguruni kuelekea Kariakoo kwa ajili ya kutafuta chimbo la kufanya kazi.Nilitafuta sana sehemu nitakayoweka meza ili nipige kazi,sasa niliingia mtaa wa Lindi lakini nikakuta kuna jamaa wengi tu wwameweka meza zao za usajili hapo na hivyo nikawa nimekosa eneo.

Nilitembea kuelekea mbele hadi nikawa nimeikamata barabara ya Kamata/Msimbazi road.Sasa kuna duka moja lilikuwa la vyombo vya electronic ambapo pembeni yake kulikuwa na duka dogo la simu,duka hilo ni miongoni mwa maduka ambayo leo yanakitazama kituo cha mwendokasi pale Gerezani,sasa pembeni yake nikaenda kuweka meza,kabla ya kuweka meza nikasogea mpaka kwenye lile duka nikakuta kuna mwanamke wa kiarabu aliyekuwa amejifunika vazi la Nikabu.

Mwanamke "Karibu"

Mimi "Ahsante"

Mimi "Aunt samahani,mimi nafanya kazi ya kusajili line kutoka Tigo,naomba niweke meza hapa pembeni"

Mwanamke "Mmmh hebu tuone"

Yule mwanamke alitoka dukani akawa amekuja nje kuchungulia kuangalia ni eneo lipi ambalo nilikuwa nahitaji kuweka meza na mwamvuli.

Mwanamke "Sawa,utasogeza kidogo pembeni ili usiwakinge wateja"

Mimi "Nashukuru sana Aunt"

Mwanamke "Usijali "

Nilifungua ile meza kutoka kwenye boksi pamoja na ule mwamvuli kisha nikawa nimesimama nasubuiri wateja,changamoto siku hiyo ilikuwa ni kiti,nilipanga kesho yake ningenunua kiti cha kukalia kwasababu pesa nilikuwa nimeacha nyumbani.Japo ilikuwa siku ya kwanza hapo Kariakoo lakini kazi ilifanyika sana na kumbuka nilisajili line 55 kwa siku hiyo moja!.

Maisha yalisonga na nikawa nishakuwa mzoefu sana wa ile kazi,sasa hapo jirani yangu kwenye lile duka la yule dada kulikuwa na huduma za miamala ya kifedha(TIGO,VODA,AIRTEL) ambapo nilipokuwa nikisajili line mteja akihitaji nimuweke pesa kwenye akaunti yake ya Tigo pesa,nilikuwa naingia tu kwenye lile duka!.Ile ilifanya nikazoeleka na taratibu nikawa najulikana.Kuna siku nyingine asipokuwepo yule dada basi utamkuta mumewe,hivyo wote kwa pamoja wakawa wamenizoea.

Niliifanya kazi ya kusajili line za simu kwa uaminifu mkubwa na kwa roho moja kana kwamba ile kampuni ilikuwa ya familia yangu,nilihakikisha naweka na kuhifadhi pesa ili nije nifanye mambo makubwa nilikuwa ninayawaza,nilikuwa nina uchungu sana baada ya Kileri kutafuna pesa yangu ya mtaji niliyokuwa nimempatia.

Sasa kuna siku nikiwa nimetoka kwenye mihangaiko yangu hiyo ya kusajili line nikiwa nimefika pale nyumbani nilikuta kuna zogo la Steve na demu wake.Niliingia zangu ndani kisha nikaingia bafuni kuoga ili nipike nile kisha nilale.Malumbano ya jamaa na demu wake yalikuwa makubwa mno kiasi kwamba jamaa akaja kunigongea mlango huku akilia.

Steve "Kaka njoo unisaidie kunibemebelezea shemeji yako kaka"

Nilimshangaa Steve namna alivyokuwa akitiririsha machozi kana kwamba amefiwa.

Mimi "Kuna nini?"

Steve "We njoo kaka"

Hicho kidemu cha jamaa kilikuwa ni kidemu fulani kilichokuwa kinambabaisha sana jamaa na sikuwahi kuelewa uenda jamaa atakuwa alirogwa kwasababu alikuwaga haambiliki kabisa kwa kile kidemu,nisiseme uongo,kidemu kilikuwa kizuri na kilikuwa na shepu isiyokuwa ya kawaida,sasa labda uenda Steve alichanganyikiwa na kile kishepu,kile kidemu kilikuwa kijitu cha Mtwara kwa mujibu wa Steve na walikutana kwenye pilika zetu hizo za usajili wa line.

Jina la huyo demu alikuwa akiitwa Zubeda ila Steve alikuwa akimuita Zuu.

Niliondoka na jamaa kuelekea hadi ndani kwake ambako kilikuwa chumba kimoja,nilipoingia ndani nilikuta kidemu kimelala kimeweka matako juu huku kinaendelea kuchezea kiswanswadu chake huku hakina habari kabisa na mtu!.

Mimi "Shem mambo vipi"

Zubeda "poa"

Sasa kilikuwa kinajibu huku kinaendelea kuchezea simu.

Mimi "Kuna nini shemeji yangu maana naona jamaa analia tu kama kichaa"

Zubeda "Ndo umwambie akueleze kinachomliza ni kitu gani!"

Muda huo wote naongea nae bado alikuwa bize akicheza na simu yake na akiwa hana habari kabisa.

Mimi "Shem muhurumie mwenzio yawezakana umemkosea"

Zubeda "Nimemkosea kitu gani bwana eeeh na wewe usitake kunichosha"

Aliendelea "Huyo kinachomliza ni wivu tu wakijinga"

Zubeda "Sikia,kuna mwanaume niliwahi kuwa nae kwenye uhusiano na alikuwa akinidai hela yake aliwahi kunipatia mtaji sasa tulipoachana akataka nimrudishie hela yake,ndiyo nikawa nimemuelekeza aje achukue hela yake"

Steve "Mtu mmeachana na bado mnawasiliana nae kila siku usiku anakupigia simu"

Zubeda "Sasa kwani kunipigia simu ndiyo kurudiana nae?"

Steve "Ungeenda sasa kumpatia huko siyo kumwambia aje hapa nyumbani kwangu"

Kwa maelezo ya Steve ni kwamba,huyo jamaa yake na hako kademu kake alikwenda hapo nyumbani kwa Steve wakati jamaa akiwa kazini kwake huko Tandika,ni nilikuka kufahamu ya kwamba kilichokuwa kinamliza Steve ni kuamini huyo demu wake atakuwa ametombewa ndani kwenye gheto lake kwasababu tabia za demu wake alizifahamu kabisa alikuwa hajatulia.

Yule demu alikuwa anambabaisha sana Steve kwa kufahamu alikuwa anampenda,na wewe fikiria pesa zote jamaa ambazo alikuwa akipata kama Kamisheni kwa kusajili laini alikuwa akikapa hako kademu.

Zubeda "Ndiyo maana nimekwambia ngoja niondoke,kwanini unafungia mlango?"

Mimi "Shem hebu yaacheni haya mambo bana"

Zubeda "Mimi unadhani basi nina tatizo shem,ni huyo mwenzio ndiyo ananifikiria vibaya"

Basi baada ya usuluhishi kutoka kwa msuluhishaji wa migogoro ya kimapenzi(Rejea kwa Ema na Deborah) niliyekuwa na uzoefu wa kutosha,niliamua kuondoka mle chumbani kwa jamaa ili wao wenyewe waendelee kupambana.

Kuna muda nilikuwa namshauri Steve aachane na yule demu lakini ni kama nilikuwa nampigia mbuzi gitaa,yule demu alikuwa na sifa mbaya kiasi kwamba kuna masela kadhaa pale mtaani tulipokuwa tunakaa nilikuwa nasikia wanapita nako na kila nikijaribu kumueleza jamaa anajifanya kama ameelewa lakini kumbe yanapitia huku yanatokea kule.

Sasa kuna siku nikiwa kariakoo napiga kazi,kuna dingi mmoja alikuwa na duka pembeni ya ile nyumba akawa amenipigia simu.



............................................................................................




Utajiri wa rafiki yangu ulivyofanya nikamuamini Shetani - 09.


Mwenye duka "Mambo vipi?"

Mimi "Shwari"

Mwenye duka "Jamaa yako anahama nini!"

Mimi "Nani?"

Mwenye duka "Jamaa yako na Mmakonde wake!"

Mimi "Steve?"

Mwenye duka "Eeh!"

Mimi "Wanahama lini?"

Mwenye duka "Naona wanapakia vitu kwenye Suzuki carry"

Mimi "Mbona hajaniambia!"

Mwenye duka "Nyie si marafiki!,ina maana rafiki yako anahama wewe hujui!"

Mimi "Labda wameona waondoke kimya kimya kaka"

Mwenye duka "Sawa bhana baadae"

Baada ya huyo mwenye duka kukata simu nilibaki kushangaa kwasababu zilikuwa ni sababu zipi zinafanya Steve ahame bila kunipa taarifa kama mshikaji wake wa karibu?,nilidhani uenda aliamua kuhama kwasababu alishachoka maneno mengi kuhusu huyo mkewe yaliyokuwa yakizungumzwa hapo mtaani,niliamua kumpigia simu ili kufahamu kilichokuwa kinaendelea na kwanini asiniage kama rafiki yake?

Nilipopiga simu yake ikawa inaita tu bila kupokelewa,nikapiga tena lakini ikawa haipokelewi,baada ya dakika 15 jamaa akanipigia yeye mwenyewe.

Steve "Kaka nilikuwa bize na mteja,nambie mwanangu"

Mimi "Uko Tandika?"

Steve "Yeah niko Tandika"

Mimi "Duuu mi nadhani uko maskani!"

Steve "Mapema yote hii kaka nyumbani nitafute nini?"

Mimi "Kwani pale nyumbani unahama?"

Steve "Nahama?,nahama naenda wapi?"

Mimi "Mbona nimepigiwa simu na mzee beda anasema mkeo anapakia vyombo kwe gari hivyo alidhani mnahama!"

Steve "Unasema?"

Mimi "Mpigie mzee beda umuulize"

Baada ya mazungumzo hayo ambayo ni kama yalimshitua Steve,alikata simu akawa amempigia yule jamaa aliyekuwa na duka kando ya nyumba tulivyokuwa tumepanga.Haukupita muda Steve akawa amenipigia simu tena.

Steve "Kaka ngoja kwanza niwahi nyumbani"

Mimi "Ni kweli?"

Steve "Ni kweli kaka"

Mimi "Anapeleka wapi vyombo au anatoroka?"

Steve "Ngoja niwahi kaka!"

Jamaa alionekana kupagawa sana na asijue ni kitu gani cha kufanya,kiukweli yule demu nilishamshauri sana kama mshikaji wake aachane nae lakini jamaa nikama alikuwa amerogwa,yule demu alikuwa akimfanyia vituko vya kila aina lakini Steve alikuwa haambiliki wala ashauriki,sikuwahi kuelewa ni kitu gani kilimfanya Steve apagawe kwa kile kitoto cha kimakonde.Pasipokuelewa ni kitu gani kilikuwa kinaendelea,mimi niliendelea kupiga zangu kazi kama kawaida.

Ilipofika mida ya saa 11 jioni,Steve akawa amenipigia simu tena akiwa analia kana kwamba kafiwa.

Steve "Kaka Zubeda kaondoka"

Mimi "Acha kulia mwanangu nakuja muda siyo mrefu"

Steve "Kaka Zuu wangu wamemchukua"

Mimi "Nakuja kaka wewe nisubiri"

Jamaa alikuwa akilia kama tahira,sikujua Steve alikuwaga akisimbuliwa na kitu gani kwasababu jamaa alikuwa na sura ya kirembo(Handsome) na kiukweli ungemuona usingedhani kama alikuwa mpumbavu wa kulilia mwanamke kiasi kile.Ilipofika saa 11 : 30 niliamua kukunja ile meza pamoja na mwamvuli nikapeleka mahali ambapo nilikuwa natunzia kila siku,mwaka ule ilipokuwa ikifika saa 12 : 00 jioni na usajili pia ulikuwa unasitishwa,sasa wakati naondoka yule brother wa lile duka la simu(Sitamtaja jina lake halisi kwasababu maalumu,hivyo nitampatia jina la Ally Mpemba) akawa ameniita na mara zote nikiwa pale alikuwa akiniita "Master",alipenda kuniita kwa utani hivyo kwasababu alikuwa akiona shughuli niliyokuwa nikiifanya ndipo akawa ananiita hivyo Master,alikuwaga ananiambia "Aisee wewe nakukubali sana,wewe ni master wa hizi kazi".Kwahiyo ikaenda kimzaha mzaha hivyo hadi akawa ananiita master,jamaa alikuwa ni mpemba lakini vilevile alikuwa mwarabu,nadhani tunafahamu jamaa wanavyokuwaga.

Ally Mpemba "Mbona wawahi kufunga leo,kunani!"

Mimi "Ndiyo muda wenyewe huu kaka"

Ally mpemba "Aaah Master siyo kawaida yako!"

Mimi "Kuna ishu naiwahi maskani kaka"

Ally mpemba "Kesho nikitoka kuswali,tuonane basi!"

Mimi "Tutaonana kaka,si utakuwepo?"

Ally mwarabu "Nadhani nitakuwa kule Aggrey,hapa atakuwepo dada yako"

Mimi "Sawa kaka haina tatizo"

Sasa kumbe mara zote mimi nimekuwa nikifikiria yule Aunt ninayemkuta pale dukani anayependa kujifunika Nikabu ni mkewe kumbe alikuwa ni dada yake;baada ya mazungumzo na Ally niliondoka zangu kwenda kufukuzana na magari ya Gongo la mboto.

Namshukuru Mungu niliingia Gongo la mboto mida ya saa 1 usiku,nilipofika pale nyumbani nilikuta Steve amekaa kwenye mlango wa chumba chake,nilipitiliza moja kwa moja hadi kwa Steve.

Mimi "Vipi?"

Steve "Ali siyo poa kaka"

Niliingia ndani ya kile chumba nikakuta vitu muhimu vyote vimekombwa na yule demu wake,alichokuwa ameacha ni vyombo vya kupikia tu,lakini TV chogo,friji,jiko la gesi,mashuka na vitu vidogo vidogo vyote alikomba.

Mimi "Aiseee,sasa utafanyaje?"

Steve "Nampigia simu zangu hapokei!"

Mimi "Kwani mligombana jana?"

Steve "Tangu siku ile kaka huwezi amini sijagombana nae"

Mimi "Kwani kwao ni wapi?"

Steve "Kwao Mtwara kaka ila yupo dada yake pale Mombasa ndipo alipokuwa anakaa kabla sijamchukua"

Mimi "Dada yake ushampigia simu?"

Steve "Nimempigia akaniambia huyo hawezi kwenda sehemu nyingine zaidi ya kwa bwana ake wa zamani kwasababu hapa mjini hana ndugu mwingine tofauti na yeye"

Mimi "Kwahiyo na wewe umekubali aondoke na vyombo vyako kwenda kwa bwana ake huyo?"

Steve "Sasa kaka nitafanyaje?"

Kiukweli nilitamani kumzibua mabao ya kutosha yule jamaa kwa upumbavu alokuwa akiongea mbele yangu lakini niliamua kuwa mtulivu kwasababu mambo yao yalikuwa hayanihusu,kilichokuwa kinanikwaza ni namna Steve alikuwa akiumia lakini kila ukimuongelea huyo demu vibaya ni kama anachukia,sikujua yule jamaa alipewa nini na yule demu aisee!.

Mimi "Huyo mshikaji wake unamfahamu?"

Steve "Kama ndiye huyo dada yake aliyeniambia namfahamu kaka na mara kadhaa tu nimekuwa nikimfata hapo"

Mimi "Daaah ila wewe jamaa nae,sasa unafahamu kabisa demu wako anakusaliti halafu bado unaendelea nae kweli,hata kama ni kupenda mwanangu wewe umepitiliza"

Steve "Nisindikize kaka mi nikafate vyombo vyangu tu"

Mimi "Ni wapi?"

Steve "Ni hapo Pugu kajiungeni"

Sasa nilitoka nje kwenda kupiga strori kadhaa na yule jamaa wa dukani na kweli alisema ile Suzuki carry ilielekea uelekeo wa njia ya Pugu na jamaa pia alishangaa namna Steve alivyokuwa bwege kiasi kile.

Tuliondoka huo usiku kuelekea Pugu kajiungeni,tulipofika Steve aliamua kuniongoza hadi hapo kwenye hiyo nyumba aliyokuwa anakaa huyo jamaa ambaye alikuwa anamgonga huyo demu wake.Tulipofika Steve akaanza kugonga kile chumba ambacho kilikuwa kimefungwa kwa ndani,baada ya kugonga sana alitoka jamaa mmoja chokoraa tu akiwa kifua wazi.

Jamaa "Vipi"

Steve "Poa,Zuu yupo?"

Jamaa "Zuu?,Zuu yupi?"

Steve "Sadi hebu achana na maswali ya kisenge,ina maana wewe leo humjui Zuu?"

Jamaa "Zuu wapo wengi sijui wewe unamtafuta yupi!"

Steve "Demu wangu"

Jamaa "Sasa demu wako hapa kafata nini!"

Muda huo niko pembeni nasikiliza yale malumbano nilikuwa nimechukia kishenzi,kibaya zaidi kuna majirani ambao nao walikuwa wamepanga kwenye ile nyumba walikuwa nje wakipika huku wakisikiliza na kujionea lile sekeseke.Baada ya kuona wanaigiza niliamua kusogea karibu na kumuuliza swali yule dogo.

Mimi "Wewe zuu unamjua au humjui?"

Jamaa "Brother,huyo Zuu anayemuongelea huyu ni demu wangu"

Mimi "Yupo au hayupo?"

Jamaa "Yupo!"

Mimi "Basi muite"

Jamaa baada ya kuona niko serious alifunga ule mlango akarudi ndani kisha akawa ametoka na kile kidemu.Baada ya kutoka Steve alibaki kujing'ata ng'ata hata kuongea ni kama alishindwa.Baada ya kuona jamaa haongei anabaki kushangaa ilibidi niingilie kati.

Mimi "Vitu vya jamaa viko wapi?"

Zubeda "Vitu gani?"

Mimi "Kwani wewe umechukua vitu gani?"

Zubeda "Vitu nilivyochukua ni vyangu,mmh kuna swali lingine!"

Mimi "Steve hebu pambana na demu wako mi naondoka"

Steve "Kaka usiniache"

Mimi "Kilichotuleta huku ni vitu na unasikia anasema si vyako,sasa hapa tunafanya nini?"

Steve "Zuu hivyo vitu ni vyako unauhakika?"

Zubeda "Nishasema vitu nilivyochukua ni vyangu,vyako nimekuachia nadhani umevikuta"

Steve "Naomba nichukue vitu vyangu nisije kufanya vurugu hapa"

Zubeda "Weeeee ishia hapo hapo,ina maana ulikuwa unanitomba bure!"

Aliendelea "Ina maana ulikuwa unanifira bure?"

Zubeda "Acha ujinga firauni wewe"

Aliendelea "Yaani ulidhani huu mwili niwa kushikwa bure bure tu!"

Yale maneno machafu yalipelekea wale kina mama kuanza kucheka,nilimwambia Steve tuondoke,japo jamaa alikuwa akitetemeka lakini niliamua kumuondoa lile eneo na kuondoka zetu,kiukweli kile kidemu hakikuwaga na aibu hata kidogo na nilikuwa namshangaa sana Steve anawezaje kuwaacha mademu wakali wa pale ofisini akaenda kutembea na kile kichakubimbi.

Mimi "Vitu vinanunuliwa we tuondoke!"

Steve "Kaka ila Zuu nampenda,siwezi kuondoka nikamuacha kaka ni bora nife"

Mimi "Yaani unaona bora ufe kwa ajili ya mwanamke?"

Mimi "Ok,rudi ukafe!"

Niliondoka zangu lile eneo nikamuacha jamaa akiwa amekaa chini machozi yakimtoka kama tahira.Baada ya kufika nyumbani nilipika msosi nikala kisha nikaingia chumbani kulala.



..............................................................................................



Utajiri wa rafiki yangu ulivyofanya nikamuamini Shetani - 10.


Nilishitushwa na sauti ya Steve akiwa ananiita na kunigongea akitaka nimfungulie mlango,nilipochukua simu na kutazama muda ilikuwa imefika saa 4.Niliamka nikaenda kumfungulia jamaa mlango,kiukweli alionekana hayuko kawaida na sikutaka kumpa presha,nilimwambia aingie alale atulize akili.

Namshukuru Mungu kulipokucha,mimi niliwahi kuondoka nikamuacha jamaa akiwa amelala,kabla ya kwenda Kariakoo ilikuwa ni lazima kila msajili line kupitia pale ofisini Buguruni kusikiliza kikao na mambo mapya kisha kuelekea kwenye kituo chake cha kazi,nami ndivyo nilivyofanya!.Nilipofika Kariakoo nilielekea eneo ambalo nilikuwa nikihifadhia vitu vyangu vya kazi na kuja kuanza kupiga kazi.

Sasa wakati nafika pale,lile duka la Ally mpemba lilikuwa bado halijafunguliwa,mi niliweka zangu meza nikaanza kupiga kazi kawa kawaida,kiukweli kwa kipindi kile kulikuwa na wateja wengi mno,yaani ilikuwa ukifungua tu ile saa 2 asubuhi wateja wanaanza.Ilipofika mida ya saa 3 asubuhi,kuna gari aina ya Range Sport nyeusi iliyokuwa na Private Number iliyoandikwa " SALIM " ilisimama pembeni yangu kisha ukafunguliwa mlango akawa ameshuka yule Aunt ndugu yake na Ally Mpemba.

Aunt "Leo umeniwahi"

Mimi "Leo nimekuwahi Aunt,salama lakini"

Aunt "Mie niko salama kabisa sijui wewe huko utokako"

Mimi "Salama kabisa"

Wakati nikiwa naendelea kuzungumza na Aunt ile gari ikawa imeondoka kuelekea Kamata.Yule Aunt pamoja na ndugu yake Ally Mpemba walikuwa wakizungumza kiswahili cha kipwani pwani kama ambavyo wazanzibar wakizungumza!.

Ilipofika mida ya 5 asubuhi,alinipigia simu Steve na akawa ananiambia ya kwamba,yule demu wake wamekubaliana arudi nyumbani na yeye amemsamehe ili mambo mengine yaendelee,mimi kwakuwa nilishamshauri sana kuonekana kama natwanga maji kwenye kinu nilimwambia sawa,hakuna tatizo,sikutaka kabisa kuwashauri kwasababu niliona ni kama nilikuwa napoteza muda.

Mimi "Kwahiyo vitu anarudisha?"

Steve "Ndo naenda kuvichukua kaka"

Mimi "Kwahiyo Leo hujaenda Tandika"

Steve "Leo siendi kaka ngoja kwanza nikamchukue huyu"

Mimi "Poa,kama ukitoka funguo utaniwekea juu ya mlango hapo"

Steve "Leo sina ratiba ya kutoka kaka"

Mimi "Sawa,baadae"

Safari hii niliamua nikae pembeni katika kushuri kwasababu nilichokuja kugundua ni kwamba,mambo yote ya msingi niliyokuwa nikimshauri jamaa kuhusu demu wake,yeye alikuwa akimwambia kila kitu na hivyo mimi kuonekana mchonganishi!,hivyo nikaamua sitokaa tena nimshauri na kama ni kufa yeye afe tu!.

Ilipofika mida ya saa 9 mchana,Ally Mpemba akawa amekuja akiwa ndani ya kanzu nyeupe,alipofika pale nje kabla ya kuingia ndani ya duka lake akawa amenisalimu.

Ally mpemba "Assalam aleykum"

Mimi "Alekom salam"

Ally mpemba "Kwema?"

Mimi "Kwema kaka"

Ally mpemba "Leo wafunga saa ngapi?"

Mimi "Kama kawaida kaka saa 12"

Ally mpemba "Basi utanipa muda wako kidogo Leo sheikh"

Mimi "Sawa kaka"

Sasa mida ya saa 10 alasiri alipokuwa anatoka pale dukani akawa ameniomba kama itawezekana tuondoke wote kuelekea Aggrey.

Mimi "Si hakuna haja ya kutoa vitu vyangu"

Ally mpemba "We viache tu,nishamwambia Farah atakuangalizia usijali"

Niliondoka na Ally kuelekea mtaa wa Aggrey ambako huko nako nilikuta kuna duka kubwa la simu na ndani yake kukiwa na wafanyakazi kama 4 wakisaidiana kuuza,sasa tofauti na kule ni kwamba lile la kule niliko lilikuwa dogo na la pale Aggrey lilikuwa kubwa.

Ally mpemba "Mi huwa nashinda hapa mara zote,nisipokuwa kule basi wanipata hapa"

Mimi "Ok sawa kaka lete maneno"

Ally mpemba "Kuna kazi nataka unisaidie Master"

Mimi "Kazi gani tena kaka?"

Ally Mpemba "Ni kazi ya kawaida tu!"

Aliendelea "Mimi ninahusika pia na mambo ya caterings na nimewaajiri ndugu wa familia na watu wengine lakini ndugu zangu ni watu wa ovyo sana huwa hawapendi kazi za kujishughulisha wao wanapenda kukaa kama hivi unavyowaona"

Ally Mpemba "Sasa kila ninapokutazama nakuona wewe ni mpambanaji mtu wa bara na ndiyo maana nakuita Master"

Aliendelea "Mimi nataka tu unisaidie kitu kimoja na offcouse siyo msaada bali nataka tufanye kazi"

Mimi "Sawa kaka"

Ally Mpemba "Kwani huko Tigo mnalipana shi ngapi?"

Mimi "Kaka kule ninalipwa kwa kamisheni"

Ally Mpemba "Sawa naelewa ni kamisheni lakini malipo yao huwa yapoje?"

Mimi "Inategemea na laini nilizosajili na matumizi ya wateja kwa mwezi husika"

Ally Mpemba "Doo kwahiyo mteja asipotumia laini hulipwi!"

Mimi "Ni mara chache mteja aje kusajili line na asiitumie,sema huwa malipo yanategemea,kuna muda yanapungua na kuna muda yanaongezeka"

Ally Mpemba "Ok sasa mimi nataka unisimamie kwenye mradi wangu hata kwa muda wa mwezi tu Master halafu nikipata mtu muaminifu nitamuweka halafu wewe utaendelea na shughuli zako:

Mimi "Kaka kwanini mimi?"

Allya Mpemba "Mi unajua nilikuwa sikutilii maanani sana,kuna siku Farah akaniambia wewe ni mtu poa sana hata namna unavyo behave,kwa maana nilipokuta umeweka meza yako kando ya duka langu nilimwambia Farah unapaswa utoke pale ila akaniambia wewe ni mtu poa sana"

Aliendelea "Ninachotaka mimi ni kwamba,wafanyakazi wapo ila wewe ukanisimamie tu maana alikuwa anasimamia mama yangu mdogo lakini yuko Unguja anamuuguza me wake!"

Aliendelea "Wewe niambie tu unataka niwe nakulipa shi ngapi?"

Mimi "Kaka unajua sijawa na uzoefu na kazi unayotaka niifanye,hivyo itakuwa ngumu kujua unilipeje kaka"

Ally Mpemba "Sasa fanya hivi,wewe nenda kahifadhi vitu vyako halafu uje twende nyumbani mara moja"

Basi niliondoka zangu kurudi gerezani nikachukua meza,kiti pamoja na mwamvuli nikawa nimerudisha mahali ambapo nilikuwa nahifadhia.Baada ya hapo nikawa nimeondoka hadi Aggrey kisha Ally Mpemba akanichukua kuelekea Msimbazi uelekeo wa kituo cha polisi,tulitembea hadi pale Big Bon ambapo nikaona anatoa funguo wa gari kwenye kanzu yake kisha akabonyeza ile gari ikawaka taa na milango ikafunguka,ilikuwa ni ile ile Range ambayo asubuhi niliona dada yake akiwa anashushwa ambayo ilikuwa na Private Number,sasa kwa mara ya kwanza mwanaume kutoka Kijiji cha Mogabiri huko Ukuryani Tarime nikapanda Range,aisee asikwambie mtu na ndiyo maana kuna watu wako tayari kufanya kila aina ya ovu ili kujipatia fedha wanunue magari,ile ilikuwa ni moja ya gari nzuri kuwahi kupanda katika maisha yangu ya umasikini!.

Tuliondoka lile eneo tukaikamata Morogoro Road kisha safari ikaanza kwa spidi ya wastani,baada ya muda tukawa mbele ya nyumba moja maeneo ya magomeni Mikumi,ile nyumba ilikuwa ya kawaida sana kwa muonekano wa nje ila nilipoingia ndani kiukweli ilikuwa nzuri mno na usingedhani kama muonekano wa nje unasadifu kilichomo ndani!.

Baada ya kupiga honi na kufunguliwa geti gari ikawa imeingia pale uani na kupaki,sasa tulipoteremka kuna vitoto vya kike viwili vya kiarabu(Kipemba) tulivikuta hapo ndani vikawa vinamkimbilia Ally na kumrukia kwa furaha!.

Ally Mpemba " Hawa ni watoto wa Farah "

Mimi "Ooh sawa kaka"

Sasa pale nje nilikuta kuna vyombo vingi sana vya kisasa na majiko makubwa ya Gesi na mkaa,na ndivyo vilikuwa vyombo vilivyokuwa vinatumika kwenye shughuli za catering.

Ally Mpemba "Nimekuleta hapa ili ujionee mwenyewe,na ukishajionea najua utaniambia nikulipe kiasi gani master"

Aliendelea "Sasa wewe kazi yako utakuwa unahakikisha vyombo vyote vinaondoka hadi kwenye events na baada ya hapo utakuwa unahakikisha vyombo vyote vinarudi kama vilivyokuwa,baada ya hapo utakuwa unasimamia ishu ya usafi wa vyombo"

Aliendelea "Kikubwa wewe utakuwa msimamizi"

Baada ya yale maelezo angalau sasa ndipo nikaanza kupata uelewa wa kazi nitakayoenda kuifanya.

Ally Mpemba "Na bahati nzuri ni kwamba,events siyo kila siku,kama kutakuwa hakuna events yeyote wewe utakuwa unaendelea na shughuli zako,mimi nahitaji tu msimazi hadi pale atakaporudi mama mdogo au nitakapompata mtu sahihi,ila nakuomba kwa sasa unisaidie kwenye hili"

Mimi "Sawa kaka nimekuelewa"

Ally Mpemba "Ok sasa niambie niwe nakulipaje!"

Mimi "Wewe nilipe utakavyoona kaka"

Ally Mpemba "Wewe niambie kiasi utakachoona kwako kinafaa maana hii siyo shughuli nyepesi kama unavyodhani!"

Mimi "Tufanye hivi kaka,tukianza kazi ndiyo nitajua,nadhani kwasasa tusubiri kwanza "

Ally mpemba "Ok hakuna tatizo maadamu umeamua hivyo!"

Baada ya mazungumzo yale tuliingia kwenye gari tukawa tumeondoka kuelekea Kariakoo,sasa wakati tunarudi tulipitia njia ya Kigogo na tulipofika pale Karume,jamaa alinipatia elfu 20 ya nauli mi nikashuka kwenye gari yeye akawa ameondoka.Nilienda upande wa pili kupanda gari za Gongo la mboto na kuondoka zangu maskani.



.........................................................................................


Utajiri wa rafiki yangu ulivyofanya nikamuamini Shetani - 11



Nilifanikiwa kufika nyumbani na nikamkuta Steve amemrudisha demu wake kichwa kibovu,kiukweli niliapa sitokuja tena kuingilia au kushauri mahusiano yao,hata kama wangekuwa wanapigana hadi kuuana,nisingethubutu kamwe!.

Sasa nakumbuka siku moja nikiwa pale Kariakoo,alinipigia simu yule jamaa yangu tulikuwa wote tukipambana kwenye vibarua vya ujenzi aliyeitwa Mwakisaka na alinitaka kama nipo tu sina ishu nimfuate kibaha kulikuwa na mradi wa ujenzi wa Ma-Godown na walikuwa wakilipa vizuri.

Mwakisaka "Sawa kaka kama huko unapiga pesa wewe endelea maana riziki popote"

Mimi "Kwahiyo siku hizi unaishi Kibaha"

Mwakisaka " Hapana kaka,huwa naweka tu kambi"

Mimi "Sawa kaka wewe pambana".

Niliendelea kupiga kazi yangu ya usajili wa line za simu kwa uaminifu mkubwa mno,hakuna kazi niliyoifanya kwa moyo wote kama vile ilikuwa ya baba yangu kama ile kazi ya kusajili line,na ndiyo maana hawa madogo wanaosajili line za simu leo ambao huwa wanatembea kwa mguu(Door to door),huwa nikiwaona tu nawaita tunapiga stori mbili tatu kisha nawatia moyo halafu nawaachia hela ya maji kidogo.Kiukweli kwa siku hizi imekuwa kazi ya kudharaulika sana hasa ukizingatia wengi wao wanakosa uaminifu na kuwaibia wateja hao hao ambao wanawafanyia usajili,lakini enzi zangu wakati nafanya ilikuwa kazi muhimu sana na iliyokuwa na maslahi mazuri!,yote kwa yote ni kwamba imebaki kwenye kumbukumbu ya maisha yangu ambayo siwezi kuisahau.

Siku moja nikiwa nimetoka kazini usiku nikiwa nimelala,Ally Mpemba alinipigia simu.

Ally Mpemba "Kaka nakusumbua umelala"

Mimi "Hapana kaka nilikuwa bado niko macho"

Ally Mpemba "Sasa kuna tenda nimeipata usiku huu inapaswa kufanyika kesho jioni pale Osterybay,hivyo jitahidi kesho asubuhi na mapema tuonane ili nikukutanishe na mama mpishi muone mtafanyaje"

Mimi "Sawa kaka"

Ilipofika Asubuhi mida ya saa 2 nilikuwa kwenye gari nikielekea pale Buguruni ofisini kwenye vikao vya kawaida vya kazi yangu ya usajili ambavyo vilikuwa vikifanyika kila siku ili kujua na kufahamu mambo mapya.Sasa niliamua kupita kwanza pale ofisini ili Team leader wangu asije akaona nimezingua kimakusudi;Baada ya vikao kuisha kila mmoja alitawanyika kuingia kazini,mimi nilielekea Kariakoo moja kwa moja,nilipofika sikutaka kuweka meza niliona nimpigie simu kwanza Ally Mpemba.

Mimi " Kaka Asalama aleko"

Ally Mpemba "Aleykum Assalam"

Aliendelea "Kwema?"

Mimi "Kwema kaka,nishafika hapa Kkoo"

Ally Mpemba "Nadhani ungekuja hapa Magomeni maana nimemwambia na Mama mwa-J mnikute hapa"

Mimi "Pale pale tulipoenda siku ile?"

Ally Mpemba "Yeah njoo mpaka hapo"

Mimi "Sawa"

Nilitembea mdogo mdogo hadi karume nikaenda kudandia daladala hadi magomeni,baada ya kushushwa nilianza kutembea mdogo mdogo hadi kwenye ile nyumba ambayo tulifika na Ally siku ile.Baada ya kufika pale nilimpigia jamaa simu kumjulisha ya kuwa nimefika na alinitaka nisubiri kwani muda si mrefu angekuwa amefika hapo.

Haikupita muda mrefu lile geti likafunguliwa akatoka mwanamke mmoja wa kiarabu ambaye alikuwa amejitanda ushungi,baada ya kutoka nje akawa amefunga lile geti na kuondoka.Sikuweza kusalimiana na yule mwanamke kwasababu nilisimama mbali kidogo na ile nyumba.Sasa wakati nikiwa nashangaa pale nje,ile Range iliyokuwa imebandikwa namba binafsi "SALIM" niiona ikiwa inakuja na ilipofika jirani alikuwa ni Ally Mpemba akiendesha ndani akiwa peke yake.

Ally Mpemba "Nisamehe kaka nimekuweka sana"

Mimi " Usijali kaka"

Ally Mpemba "Kwanini umekaa nje?,ungegonga wakufungulie nilishawapa taarifa"

Mimi "Hilo sikulifahamu kaka"

Ally Mpemba "Sema na mimi nimekuwa mzembe kukwambia"

Aliendelea "Mimi nakaa mtaa wa pili kutoka hapa"

Mimi "Mawazo yangu yote nikajua huwa unakaa hapa"

Ally Mpemba "Hapana kaka,Hapa anakaa bi mkubwa na wadogo zangu"

Mimi "Ooh sawa kaka"

Baada ya mazungumzo mafupi,jamaa aligonga lile geti kisha akaja mtu kufungua.Tulipofika ndani jamaa alimwambia dada mmoja mweusi mwenzangu ambaye nadhani alikuwa mfanyakazi ya kwamba atuletee viti tukae nje wakati ambao tungekuwa tunamsubiri mama Mwa -J.

Ally Mpemba "Kuna jamaa yangu mmoja leo usiku atakuwa na sherehe pale kwake hivyo mnapaswa kuweka maandalizi sawa"

Aliendelea "Pia utakuwa unapata uzoefu kuanzia hapo"

Ally Mpemba "Unajua master,nahitaji kuaminika na viongozi wakubwa kwenye haya mambo ya vyakula na nahitaji kuingia kwa miguu yote ndiyo maana unaona nimejipanga!"

Aliendelea "Yaani sherehe zote za viongozi na watu wakubwa nataka tenda niwe nachukua mimi"

Mimi "Kaka hakuna kinachoshindikana,ni malengo tu na jitihada"

Ally Mpemba "Jitahada ninazo kaka na ndiyo maana unaona kila kitu kipo hapa,mambo mengine makubwa ni kwa uwezo wa Allah"

Baada ya dakika 40 yule mama aliyekuwa mpishi aliyeitwa mama Mwa -J alikuwa amekuja akiongozana na mabinti wawili na kijana mmoja.Baada ya salaamu,Ally Mpemba alikuwa akimtambulisha kwangu,baada ya utambulisho ule kumbe yule mama aliwahi kuwa mfanyakazi wa ndani hapo kwo Ally Mpemba kwa miaka ya nyuma.

Ally Mpemba "Wale watu watakuwa 50 na kuna viongozi pale,hivyo naombeni mfanye vema zaidi "

Mama Mwa-J " Bila shaka mdogo wangu unaniamini,kaa kwa kutulia "

Ally Mpemba alichukua simu yake akawa kuna mtu anampigia na kumtaka alete gari.Haukupita muda kuna gari ililetwa ikiwa ni Hiace nyeusi.

Ally mpemba "Hii ndiyo gari ambayo huwa inabeba vyakula pamoja na vyombo,niliinunua kwa ajili ya kazi hii "

Mimi "Ooh sawa kaka hongera maana naona uko vizuri "

Ally Mpemba "Hii mbona kawaida tu"

Kiukweli Ally Mpemba alionekana mtu fulani wa makamo,hakuwa kwenye uzee wala ujana,alikuwa yupo kati.Baada ya mazungumzo ya hapa na pale,yule mama aliondoka na wale mabinti wakaelekea sokoni kwa ajili ya kufanya mahitaji ya vyakula na viungo ambavyo vingetumika kwenye upishi.
Kweli,baada ya siku ndefu ya upishi na kusaidia kuandaa vyakula,ilipofika mida ya saa 11 jioni tuliondoka kuelekea Osterbay mahali ambako kulikuwa na tukio;Ile Hiace ilibeba kila kitu kilichokuwa tayari na tukaondoka,sasa ile Hiace kwa nyuma hakukuwa na siti,kulikuwa tupu na ilikuwa maalumu kwa ubebaji wa vyombo vya vyakula.Ile kazi ya usimamizi ilifanya nikazunguka sehemu karibia zote za ushuani hapa Dar es salaam,pale Osterbay tulipokwenda kiukweli hakukuwa kwa kawaida,mazingira tu ya ile nyumba na mali zake ilitosha kukuaminisha ya kwamba watu walikuwa wanaishi na siyo kuwasindikiza watu kuishi.

Lilikuwa ni tukio la uvalishanaji Pete na baada ya hapo kuliendelea sherehe,sasa Ally Mpemba alikuwa akinipigia simu kufahamu mambo yameendaje na nilikuwa namjulisha mambo yalivyokuwa yakiendelea.Tulikaa pale eneo la tukio hadi mida ya saa 6 usiku,ndipo sherehe ikawa imefungwa rasmi na sisi kupakia vitu na kuvirudisha kule magomeni,sasa kabla ya kuondoka Ally Mpemba alikuwa ameniambia kuna muhusika pale kwenye hiyo sherehe angenipatia milioni 2.5 nimpelekee.Kabla ya kuondoka niliitwa na jamaa mmoja aliyenikabidhi milioni 2.5 kisha akampigia Ally Mpemba akamwambia amenipatia hiyo hela.

Jamaa "Huyu hapa ongea nae"

Ally Mpemba "Master amekupa?"

Mimi "Ndiyo kaka kaniakabidhi milioni 2.5"

Ally Mpemba "Sawa utaniletea "

Basi tuliondoka zetu lile eneo kisha tukawa tumefika magomeni na kuanza kushusha vile vyombo na kuvipanga,Ile ishu ya kupakia na kwenda kushusha vyombo na kuviweka mahali pake ilimalizika mida ya saa 8.Baada ya hapo ile Hiace iliwabeba mama Mwa -J na wale wafanyakazi lakini kabla ya kuondoka nilitaka kufahamu walikuwa wakielekea wapi!.

Mama Mwa - J "Siye tunaenda Tegeta"

Mimi "Mwanangu suka siunarudi?"

Suka "Nikifika ni kupaki kaka sirudi huku"

Mimi "Duuuu sasa nitafikaje maskani!"

Suka "Kwani kwako ni uelekeo upi"

Mimi "Mimi naishi Gongo la mboto "

Suka "Gongo la mboto mbona magari kibao muda huu!"

Mimi "Muda huu?"

Suka "Yeah wewe tembea hadi kituoni magari ni kibao"

Mimi "Basi niache pale kituoni kaka"

Nilipopanda kwenye gari simu yangu ikawa inaita,nilipoitoa mfukoni nikakuta nj Ally Mpemba ananipigia simu.

Ally Mpemba "Mko wapi?"

Mimi "Kaka nipo kwenye gari hapa wananiacha kituoni nielekee Gongo la mboto"

Ally Mpemba "Kaka unajipenda Kweli?kituoni muda huu?"

Mimi "Jamaa ameniambia kuna usafiri"

Ally Mpemba "Mpe simu Jabir"

Nikampa simu yule dereva aliyekuwa akiitwa Jabir wakawa wanaongea kwenye simu na baada ya maongezi jamaa akawa amesimamisha ile Hiace,haukupita muda Ally Mpemba akawa amekuja na ile Range maeneo yale kisha akawa amenitaka nishuke.

Ally Mpemba "Poa nyie ondokeni"

Ally Mpemba "Ingia twende kaka"

Aliendelea " Kaka usiku huu huwezi pata gari za huko kwenu vinginevyo vibaka unataka wakufanye kitu mbaya"

Aliendelea "Twende ukaegeshe kwangu master "

Kweli,tulipofika jamaa anapokaa alishuka akaenda kufungua geti kisha akaingiza gari ndani na kwenda kufunga geti.Ile nyumba ilikuwa nzuri mno na hadi leo ipo ingawaje Ally Mpemba alishaachana nayo anaishi kwingine,ni nyumba ambayo kwa wakati ule ulikuwa unajiuliza mara mbili mbili kwasababu haikuwa ya mchezo mchezo,pale nje kuna gari mbili zilizokuwa mpya na hazikuwa na namba,ni kama zilikuwa zimetoka bandarini.

Jamaa hakuwa na maneno mambo mengi,tuliingia ndani akawa amenionyesha chumba cha kulala kisha na yeye akawa ameelekea kulala chumba chake,kiukweli nililala kidogo tu kukawa kumekucha,kulipokucha Ally aliniambia nisubiri tuondoke wote kuelekea Kkoo,sasa nilitoka nikaelekea sebuleni kukaa na kushangaa namna ambavyo watu walikuwa wakiishi maisha yaliyomstahili mwanadamu kuyaishi.Sasa nilipofika pale sebuleni nilikuta kuna majani ya mchicha na masalia ya Cabbage kana kwamba kulikuwa na mbuzi wamekula na kuacha yale masalia shaghala baghala.

Ally Alipomaliza kujiandaa alikuja akawa kama anashangaa,alielekea ndani akachukua mfagio wa ndani na akaja akafagia na kuzoa,alionekana ni mtu mwenye wasiwasi mwingi lakini alijifanya kufurahi.

Ally Mpemba "Tuondoke sasa "

Aliendelea "Mimi naishi mwenyewe master mke na watoto wako huko Oman"

Mimi "Ooh sawa kaka"

Ally Mpemba "Eeeh bana hivyo ukiona nafanya usafi usinishangae"

Mimi "Ni mambo ya kawaida kaka hata mi naishi mwenyewe"

Ally Mpemba "Bado hujaoa tu!"

Mimi " Bado kaka"

Ally Mpemba "Fanya uoe master,mwanamke na watoto ni baraka "

Aliendelea "Bila ya mke unaweza usifike popote katika haya masuala ya rizki kaka"

Jamaa aliniambia nipande kwenye gari na yeye akawa amerudi ndani,sasa kiukweli nilikuwa naendelea kuyatazama yale magari yaliyokuwa yamepaki namna yalivyokuwa mapya na kwa kuyaangalia tu ilionekana yalikuwa ya gharama kubwa.

Baada ya kutoka ndani aliingia kwenye gari akaitoa nje kisha akarudi kufunga geti tukaondoka zetu.

Maisha yaliendelea huku na mimi nikiendelea kupambana na kazi zangu zote mbili,siku ambayo nilikuwa sisajili line nilikuwa naenda kwenye events na siku ambazo hakukuwa na events nilikuwa nafidia ule muda kwa kusajili line nyingi.

Baada ya kupata pesa ya kutosha nilifungua akaunti NMB nikawa naweka hela zangu nikiwa na malengo ya kununua uwanja ili kwa baadae nianze ujenzi.

Ilifika muda Ally Mpemba akawa ananiamini sana na nikawa mtu wake wa karibu sana,kuna mambo ya familia yake alikuwa ameniambia na hivyo ile familia niliifahamu kuliko walivyodhani,sasa kwakuwa jamaa alikuwa ameniamini na mimi pia sikutaka kumuangusha katika uaminifu.Kuna siku jamaa alikuwa na safari ya kuelekea Unguja ambako aliniambia angekaa kwa takribani wiki moja na kurejea,sasa akawa ameniomba kitu kimoja ambacho sikukielewa kwa haraka haraka.

Ally Mpemba "Kaka nina safari ya Unguja na nadhani itanichukua wiki moja"

Aliendelea "Sasa nakuomba twende nyumbani mara moja kuna kazi ndogo nikupatie"

Mimi "Sawa kaka hakuna tazizo"

Ally Mpemba "Nakuamini sana kaka since day one,tafadhali Linda uaminifu wangu kwako"

Mimi "Kaka hakuna shida,mimi pia nakuamini sana kama wewe ulivyoniamini!"

Baada ya kufika kwake,alipaki gari nje akafungua geti tukaingia ndani,tulipofika ndani Ally Mpemba aliniambia atanipatia funguo wa ile nyumba yake lakini sipaswi kulala mle ndani kama yeye hayupo na kuna chumba alinionyesha ambacho alitaka kila siku saa 1 usiku nihakikishe nakifungua kinakaa wazi na inapofika asubuhi mida ya saa 12 naenda kukifunga.

Ally Mpemba "Utahakikisha kaka unakifungua unakiacha wazi na wewe unaondoka"

Mimi "Kaka hiyo mbona ni kazi ndogo tu!"

Ally Mpemba "Siyo kazi ndogo Master kama unavyodhani "

Mimi "Aaah kaka yaani kufunga chumba na kukifunga kuna kazi gani hapo?"

Mimi "Nitakuwa nawahi asubuhi na magari ya kawe kaka wala usijali"

Ally Mpemba "Hapana,utakuwa unachelewa na mimi nataka saa 12 :00 chumba kifungwe!"

Mimi "Nitakuwa naamka mapema kaka!"

Ally Mpemba "Sasa kama hutojali nakuomba uwe unalala kwenye ile gari nyeusi hapo kwa wiki hii tu kaka ili iwe kazi nyepesi kuliko kutoka huko uliko hadi hapa najua utachelewa"

Mimi "Sawa kaka hakuna tatizo"

Baada ya Ally Mpemba kunipatia maelekezo hayo niliona uaminifu aliyokuwa anaounyesha kwangu basi uenda kuna siku angenikabidhi mali au gari na mimi nivimbe mtaani!.



........................................................................................




Utajiri wa rafiki yangu ulivyofanya nikamuamini Shetani - 12.



Alinikabidhi rasmi funguo wa ile nyumba pamoja kiasi cha Tsh 140,000/= ikiwa na maana ya kwamba kila siku nitakapokuwa hapo nyumbani kwake,basi itanipasa kutumia elfu 20 kwa ajili ya chakula cha usiku,aliniambia sipaswi kabisa kurudi nyumbani kwa muda huo atakao kuwa ametoka.Kabla hajaondoka alinionyesha gari miongoni mwa magari mawili mapya yaliyokuwa yamepaki pale ndani ya fensi.

Kulikuwa na magari mawili mapya, moja lilikuwa Audi A4 nyeusi isiyokuwa na Number Plate na nyingine ilikuwa ni Mercedes benz C63 nyeupe,hii pia haikuwa na Number Plate,hizi gari zite zilikuwa na mpya kabisa.Jamaa aliniambia mimi ninapaswa kuwa nalala kwenye Audi A4.

Baada ya yale maelekezo huku akionyesha uaminifu mkubwa kwangu Ally Mpemba alisafiri kuelekea huko Unguja kama alivyokuwa ameniambia hapo awali.Baada ya jamaa kuondoka,mimi niliendelea na shughuli zangu za usajili wa line kama kawaida na ilipofika mida ya saa 12 jioni niliondoka zangu kupanda gari kuelekea nyumbani kwa Ally Mpemba.

Nilifanikiwa kufika nyumbani kwa Ally Mpemba kabla ya saa moja,nilisukuma geti nikaingia ndani kisha nikalirudishia,sasa nilisogea moja kwa moja hadi kwenye mlango mkubwa wa kuingilia ndani,nilifungua ule mlango na kuzama ndani,nilipofika ndani nilianza kuikagua ile nyumba lakini vyumba vyote nilikuta vimefungwa na yawezekana funguo atakuwa alikuwa ameondoka nazo au aliziweka mahali,chumba ambacho nilikuwa na funguo zake ni kile alichonipa kazi ya kukifungua na kukifunga!.Ile nyumba ilikuwa ni kubwa na ilikuwa niya kifahari,ulikuwa ukiingia ndani kulikuwa na nakshinakshi za gharama kubwa(Nadhani nyumba za waarabu au wahindi huwa mnaelewa zinavyokuwaga).

Ile nyumba ulikuwa ukiiangalia kwa nje ilionekana ya kawaida tu ila kwa ndani ilikuwa nzuri sana na usingeamini kama pale anaishi mtu mmoja.

Ilipofika mida ya saa 1 usiku nilienda mpaka kwenye kile chumba nikakifungua na kiukweli sikuweza kuvumilia ilibidi nisogeze shingo karibu na mlango,niliwasha taa kutazama ndani,nilipotazama ndani nilikuta kuna kitanda ambacho kilikuwa kimetandikwa kwa unadhifu wa hali ya juu,pia kulikuwa na makabati ya nguo pamoja na vitu vingine vya kawaida ambavyo huwa vinapatikana vyumbani.Niendelea kutazama kwa makini lakini hakukuwa na mtu wala,sasa niliamua kuondoka mle chumbani na nilikiacha wazi kama alivyokuwa ameniambia Ally.

Niliwasha taa za nje ya ile nyumba kisha nikafunga mlango,niliondoka zangu usiku ule kuelekea kutafuta chakula ili nile nirudi kulala kama kawaida kwenye gari ambalo Ally Mpemba aliniambia ninapaswa kulitumia kama kitanda.Baada ya kupata chakula,niliamua kurudi kwenda kulala ili asubuhi na mapema niamke niende kukifunga kile chumba,kiukweli sikutaka kumuangusha Ally Mpemba na nilitaka aniamini ili kama kuna mambo makubwa zaidi anionyeshe ili na mimi niweze kufanikiwa.

Wakati natoka kupata msosi ilikuwa mida ya saa 3, sasa nikaona niingie kwenye gari niweze kulala,kwakuwa funguo ya gari alikuwa ameniachia, nilipoingia kwenye gari niliwasha AC ili niendelee kupata kiyoyozi huku nikiutafuta usingizi,nilishusha kiti cha dereva kwa kurudi nyuma kisha nikaanza kuusaka usingizi,sasa wakati nikiwa nimepitiwa na usingizi nilishitushwa ghafla na mlio wa vitu vikiwa vinatupwa mle ndani kwenye nyumba ya Ally Mpemba.

Niliamka na taratibu na kutega sikio kwa makini ili nijiridhishe yawezekana nilisikia vibaya,ile sauti iliendelea na ndipo nikatelemka kwenye ile gari nikaelekea mlangoni kutega sikio vizuri,nilipofika pale mlangoni niliendelea kusikia glass,sufuria za kupikia pamoja na vyombo vingine vikitupwa chini kama vile kulikuwa na watu wanapigana, kiukweli niliingiwa na hali ya hofu sana ikabidi nirudi kwenye gari.Nilichukua simu nikawa namtafuta Ally Mpemba lakini simu yake haikupazikana,niliendelea kumtafuta sana lakini simu yake haikupatikana,sasa niliamua nikae kwenye gari nisitoke hadi asubuhi,muda huo ilikuwa yapata saa 7 usiku,sasa ile hali ya kutupa vitu iliendelea hadi ilipotimu mida ya saa 10 usiku,kiukweli sikupata usingizi hata kidogo na nilikuwa najiuliza kulikuwa na kitu gani mle ndani hadi vyombo kupigizwa kiasi kile,japo nilikuwa jasiri katika mambo mengi ambayo niliwahi kuyapitia lakini kwa mara ya kwanza ile hali ilinitisha sana.

Iilipofika mida ya 12 :00 nilienda kufungua ule mlango kwa umakini mkubwa kisha nikaingia ndani,nilipoingia ndani nikawasha taa ili niweze kutazama vizuri kwasababu kulikuwa bado na giza,sasa ile nimewasha taa na kutazama vizuri,nilikuta uaribifu wa kiwango cha juu sana,kiukweli nimepitia mambo mengi ya kutisha na kushangaza lakini lile tukio lilikuwa ni moja ya matukio yaliyonishangaza sana kwa ile siku.

Nilikuta vyombo vimepigizwa chini kila mahali,glass zilikuwa zimevunjwa vunjwa pale sebuleni hadi jikoni kulikuwa hakutamaniki,kiukweli sikuweza kufahamu ni kitu gani kilikuwa kimefanya uaharibifu kiasi kile.Nilisogea hadi kwenye kile chumba na safari hii sikutaka kabisa kichungulia ndani ilibidi nikifinge haraka.

Baada ya kufunga kile chumba nilitoka nje nikafunga mlango kisha nikarudi kwenye gari kwanza kutulia,kiukweli nilikuwa nina maswali mengi sana ambayo nilikuwa najiuliza lakini sikuwa na majibu.Nilikaa kwenye ile gari hadi mida ya saa 2 asubuhi ndipo nikatoka nikaelekea kwenye bomba kunawa uso na kusukutua maji mdomoni na baada ya hapo nikafunga geti nikaondoka zangu kuelekea ofisini Buguruni kwenye kikao.Kikao kilivyoisha nikaondoka kuelekea Kkoo kazini kama kawaida.

Kwa muda huo yule dada yake na Ally Mpemba aliyekuwa akiitwa Farah hakuwahi kujua kabisa kwa wakati huo kama mimi na Ally tulikuwa tumeshibana kiasi kwamba mpaka Ally kuniachia funguo za nyumba yake,sasa wakati Ally ameondoka,ile Range ilikuwa imepaki nyumbani kwake.

Ilipofika mida ya saa 5 asubuhi simu yangu ikawa inaita na nilipoitazama alikuwa ni Ally akinipigia,niliipokea ile simu kisha akawa ananiuliza maendeleo tangu alipoondoka.

Ally Mpemba "Unaendelea vema lakini wewe?"

Mimi "Kaka naendelea vema lakini jana kuna jambo limetokea pale kwako!"

Ally Mpemba "Usiniambie umefanya ambacho sikukuelekeza"

Mimi "Hapana kaka siyo hivyo"

Ally Mpemba "Mmmh ni nin!,ama umeshindwa nilichokwambia?"

Mimi "Kaka jana wakati nimelala kwenye gari nilikuwa nasikia vitu vinatupwa chini na glass kuvunjwa,nilipoingia ndani asubuhi wakati naenda kufunga mlango nikakuta vyombo vimetapakaa sebuleni hadi Jikoni kaka"

Ally Mpemba "Mtumeeeee!"

Aliendelea "Hiyo TV haijavunjwa kweli?"

Mimi "Hapana kaka,samani za ndani ziko vizuri,vyombo vyote ndo vimetapakaa ndani?"

Ally Mpemba "Umefunga mlango?"

Mimi "Ndiyo kaka nimefunga kama ulivyoniambia"

Ally Mpemba "Vyombo je umevipanga?"

Mimi "Hapana kaka sijagusa kitu maana hukunipa maelekezo mengine zaidi ya yale ya juzi"

Ally Mpemba "Bado uko hapo nyumbani?"

Mimi "Hapana kaka mimi nipo Kkoo"

Ally Mpemba "Ok nakuomba niuazime muda wako master na nitakufidia nikirudi,nakuomba uende sokoni ukanunue kabeji kubwa tano,nunua na mboga za majani kisha nenda nyumbani uingie jikoni ufungue kabati lililoko karibu na friji kwa chini utakuta kitambaa cheupe,hicho kitambaa katandike pale sebuleni juu la ile meza ya kioo na kisha weka hayo mahitaji utakayokuwa umenunua!"

Mimi "Sawa kaka hakuna tatizo"

Ally Mpemba "Nilisahau kukwambia nilivyoondoka,nisamehe sana kaka"

Mimi "Usijali kaka,hizo mboga za majani ni aina gani?"

Ally Mpemba "Nunua zozote kaka ila ziwe za kutosha"

Mimi "Sawa kaka usijali"

Ally Mpemba "Farah hajakuuliza kitu kuhusu mimi?"

Mimi "Hapana kaka,kwanza huwa sinaga stori na mtu kaka mwenyewe unanijua"

Ally Mpemba "Nitakulipa mambo makubwa master kwani wewe ni muaminifu sana,nashukuru sana kwa kuwa muaminifu kwangu?"

Mimi "Usijali kaka!"

Ally Mpemba "Ngoja nimpigie simu Farah kuna hela nimwambie akupe halafu mimi nitamrudishia"

Mimi "Sawa"

Niliamua kufunga na kurudisha meza kule ambapo mara zote nimekuwa nikihifahdi ninapomaliza kazi,sasa nikiwa njiani napeleka kuhifadhi vifaa vyangu vya kazi,Ally Mpemba alinipigia simu.

Ally Mpemba "Nimemwambia Farah akupe elfu 50,itumie hiyo kununua mahitaji hayo niliyokwambia"

Mimi "Sawa kaka Usijali"

Nilirudi hadi kwa Aunt Farah kuchukua kile kiasi cha fedha kisha nikaondoka kuelekea kununua yale mahitaji aliyokuwa ameniambia Ally Mpemba,baada ya kununua mahitaji yote muhimu kama alivyokuwa amenielekeza,nilipanda gari kuelekea Magomeni ambako ndiko alikokuwa akiishi Ally Mpemba,nilipofika nilianza kukusanya vyombo vyote vilivyokuwa chini na vile ambavyo vilikuwa vimepasuka niliamua kuvikusanya na kuviweka kwenye dust bin kule jikoni.

Baada ya kumaliza lile zoezi la kusafisha mle ndani, niliingia jikoni nikafungua ile kabati aliyokuwa amenielekeza jamaa kisha nikatoa kitamabaa cheupe nikaenda kukitandika kwenye ile meza kama alivyokuwa amenielekeza,nilipomaliza kukitandika kile kitambaa nilichukua zile kabeji kubwa 5 pamoja na yale mafungu ya mboga za majani nakiyaweka pale mezani, mboga za majani nilinunua za kutosha na nilinunua na aina karibia zote kasoro matembele!.

Baada ya kumaliza lile zoezi kwa kuwa ilikuwa mapema,niliondoka kuelekea Gongo la Mboto kuoga na kubadili nguo,nilipofika niliamua kulala kabisa kwasababu nilikuwa nina usingizi wa kufa mtu.

Ilipofika mida ya saa 11 jioni niliamua kuondoka kutembea mdogo mdogo hadi stendi ya Gongo la Mboto kisha nikapanda gari za Masaki ili nikashukie Magomeni kisha nielekea kwa Ally Mpemba.

Nilipofika nilifungua mlango nikaingia hadi ndani, sasa kwakuwa muda wa kufungua ule mlango ulikuwa bado kidogo, niliona niwashe Luninga ili niendelee kupoteza muda, sasa wakati nikiwa natazama luninga, kule kwenye kile chumba nikawa nasikia sauti yenye mtetemo.




.........................................................................................





Utajiri wa rafiki yangu ulivyofanya nikamuamini Shetani - 13.




Ile sauti ya mtetemo iliendelea sana kana kwamba hicho kitu kilichokuwa humo chumbani kilikuwa kimekasirishwa,nilisimama taratibu nikatembea kwa kunyata hadi kwenye mlango wa kile chumba,nilipofika kwakuwa muda wa kukifungua ulikuwa bado,nilitegea sikio kwa makini kusikiliza kilikuwa ni kitu gani,nilitulia kimya kabisa lakini ile sauti ya mtetemo ilikoma,niliamua tena kunyata na kurudi sebuleni.

Muda wa kufungua ule mlango ulipowadia nilinyanyuka na kwenda kuufungua,sasa nilipofungua ule mlango kama kawaida niliuacha wazi kisha nikawasha taa za nje nikatoka zangu ndani kuelekea nje.Siku hiyo sikutaka kabisa kutoka kwenda kula kwasababu nilikuwa nimekula muda siyo mrefu hivyo nikawa nimeshiba,kwakuwa bado ilikuwa mapema,niliona nifungue ile gari nikae ndani nitulie hadi nitakapopitiwa na usingizi,nilifungua vioo vya mbele vya ile gari upepo ukaanza kuingia ndani lakini nilipoona mbu wanazidi kuingia kwa kasi nilivifunga kisha nikawasha AC nikaendelea kula upepo.

Ilipofika mida ya saa 3 usiku kukiwa kumetulia,nilianza kusikia sauti ya kitu ambacho sikukielewa kilikuwa ni kitu gani kikiwa kinatafuna kwa sauti na miguno kama ya nguruwe,ile sauti ilikuwa inasikika kwa nguvu sana kiasi kwamba ikabidi nifungue mlango wa gari na kushuka,baada ya kutoka kwenye gari nilisimama kando ili niweze kuisikia ile sauti vizuri.Hali ile hakuna mwanadamu mwenye moyo ambaye asingeiogopa,mimi pamoja na ujasiri wangu wa kikurya lakini ilifika sehemu nikawa naogopa sana lakini niliendelea kuwa mvumilivu na kumdhibitishia Ally Mpemba ya kwamba mimi ni mwanaume na ni mwaminifu,hivyo mategemeo yangu yalikuwa ni ipo siku atanipa fedha au sehemu ya mali zake kutokana na uaminifu wangu kwake.

Ile sauti ilipozidi,nilisogea hadi pale mlangoni kwa kunyata kisha nikawa nasikiliza kilikuwa ni kiumbe wa aina gani aliyekuwa mle ndani,kiukweli ilikuwa ngumu kutambua kama alikuwa mwanadamu au mnyama,kwasababu nilichokuwa najiuliza,kama ni mwanadamu anawezaje kutafuna kwa kasi kiasi kile na miguno kama ya nguruwe?

Kwa watu mliofuga nguruwe au mlioishi na nguruwe nadhani hapa mtakuwa mnanielewa,kile kitu kilichokuwa humo ndani kilikuwa kinatafuna na kuguna kwa utamu kama nguruwe anapokuwa anakula.

Pia kama ni mnyama,Je alikuwa ni mnyama gani?,kiukweli niliendelea kujiuliza maswali mengi yasiyokuwa na majibu,niliona nijiondokee zangu nirudi kwenye gari kutulia,nilipitiwa na usingizi nikajikuta naamka saa 12 baada ya kusikia milio ya magari huko nje,niliamka haraka na kwenda kuufungua ule mlango na kuzama ndani,nilipofika ndani niliwasha taa za pale sebuleni na kukuta kile kitambaa kilichokuwa pale juu ya meza kimetupwa chini na nilipoangalia chini nikakuta kuna ute ute mzito kama ambao hutoa ng'ombe akiwa anatafuna nyasi,zile kabeji pamoja na mboga za majani sikuzikuta hata kipande tu,kiukweli niliingiwa na hofu sana na sikutaka kusubiri nilielekea moja kwa moja mpaka kwenye kile chumba na kukifunga.Nilipokifunga kile chumba angalau sasa moyo wangu ulitulia,niliingia jikoni nikachukua dekio (Mop) nikaenda kusafisha ule ute mzito kisha kile kitambaa nikakirudisha jikoni kama kawaida.

Baada ya kumaliza lile zoezi, nilitoka nje nikafunga mlango kisha kuelekea bombani kunawa,nilipomaliza kunawa uso na kusukutua nilirudi kwenye gari kusikilizia hadi mida ya saa 2 ili niondoke niingie Kkoo kufanya kazi yangu ya usajili.Baada ya muda kufika niliondoka nikaelekea Buguruni ofisini ambako vikao vilikuwa vinafanyika kila siku na ilikuwa ni lazima kuhudhuria,baada ya kumaliza kikao nilichukua box la line kisha nikaondoka zangu Kkoo,sasa wakati nipo kariakoo napiga kazi,Ally Mpemba alinipigia simu na kutaka nimpatie taarifa za usiku.

Ally Mpemba "Assalam aleykum"

Mimi "Alekom salam "

Ally Mpemba "Wajionaje na hali?"

Mimi "Niko vema kabisa kaka"

Ally Mpemba "Mambo yalienda vyema?"

Mimi "Ndiyo kaka hakuna kilichoharibika"

Ally Mpemba "Hakukuwa na usumbufu kama wa jana?"

Mimi "Hapana kaka"

Nilitaka nimuulize jamaa ni kitu gani kilikuwa mle ndani lakini nilikuwa nasita sana na niliona ningemuuliza uenda ningeharibu uhusiano wetu ambao tayari ushaanza kuwa mkubwa,niliamua nipige kimya ili mambo mengine mazuri yaliyokuwa mbele yangu nisiyazibe.

Ally Mpemba "Sasa utamwambia Farah akupe elfu 50 na utafanya kama ambavyo ulifanya jana"

Mimi "Sawa kaka"

Baada ya mazungumzo jamaa akawa amekata ile simu.Ilipofika mida ya saa 10 Alasiri,niliamua nifunge nirudishe vifaa vyangu vya kazi mahali ambapo nimekuwa nikivihifadhi,nilirudi hadi dukani pale nikamwambia yule sister Farah anipatie kiasi cha fedha kama ambavyo Ally Mpemba alikuwa ameniambia.

Farah "Mbona sikuhizi wawahi sana kufunga!"

Mimi "Hata muda wa usajili umebaki mchache na kuna mahali inabidi niwahi"

Farah "Ooh ok nambie"

Mimi "Brother Ally aliniambia unipatie elfu 50"

Farah "Ally kaka yangu au Ally yupi!?"

Mimi "Yes, brother Ally"

Farah "Mbona hajaniambia "

Aliendelea "Ngoja nimtafute nithibitishe"

Baada ya kumpigia Ally Mpemba na kumpata hewani walikuwa wakiongea lakini yule demu nikama alikuwa akimuuliza Ally mimi na yeye tunabiashara gani kwasababu jana alitoa elfu 50 akanipa na leo tena anatoa elfu 50 kunipatia,sikujua Ally Mpemba alimjibu kitu gani,alichukua elfu 50 akanipatia kisha mimi nikaondoka kuelekea sokoni kununua bidhaa kama ambazo nilinunua jana,maelekezo yalikuwa ni yale yale.

Kiukweli kwa muda huo nilikuwa napata sana hela kwasababu kununua mahitaji yote yale nilikuwa natumia chini ya elfu 20 na elfu 30 iliyokuwa inabaki ilikuwa yangu na Ally Mpemba hakuwahi kuiulizia kabisa,kila siku nilikuwa napewa elfu 50 kwa ajili ya manunuzi.

Kama kawaida niponunua bidhaa nilirudi hadi nyumbani Kwa Ally Mpemba na kuyaweka kama ambavyo nilikuwa nimeelekezwa.Ilipofika jioni muda wa kufungua kile chumba,niliamua kufungua pazia la pale sebuleni kisha nikawasha taa,lengo langu ilikuwa ni kuhakikisha siku hiyo nakiona kile kiumbe ambacho sikukifahamu kilikuwa kiumbe cha aina gani!;baada ya kufungua pazia na kuwasha taa,nilienda kuufungua ule mlango na kuacha wazi kisha nikatoka nje.

Niliamua kukaa kando ya lile dirisha la pale sebuleni huku nikiwa na shauku kubwa ya kuona ni kitu gani kilikuwa mle ndani,ilipofika mida ya saa 2 usiku,nilitoka nje nikaelekea kununua chips na soda kisha nikawahi kurudi, nilipofika breki ya kwanza ilikuwa ni kwenye dirisha la pale sebuleni,niliangalia kwa umakini na ndipo niliona zile kabeji na mboga za majani uilikuwa hazijaliwa,hivyo nikaa pale pembeni nikaanza kula huku nikisubiri nione ni kitu gani kilikuwa mle ndani.

Nilikaa sana pale chini hadi mida ya saa 5 usiku lakini kila nikichungulia hakukuwa na dalili ya kitu chochote, niliamua kufungua mlango na kisha kuingia ndani ili nikafunge yale mapazia na kuzima taa,nilipomaliza nilitoka nje kisha nikakaa pale mlangoni na kusikiliza,ndipo haukupita muda nikaanza kusikia utafunaji wa ovyo na papara ukiendelea kama kawaida,niliondoka nikaingia kwenye gari kwenda kulala kama kawaida huku kile kiumbe kikiendelea na utafunaji wake wa sauti kama nguruwe.

Asubuhi kama kawaida niliingia ndani nikafunga ule mlango kisha nikaanza kufanya usafi pale sebuleni kama kawaida,nilipomaliza niliondoka kuelekea kazini kama kawaida.

Sasa ilipofika mida ya saa 3 asubuhi nikiwa tu ndo nimeanza kazi,alinipigia simu Ally Mpemba.

Ally Mpemba "Kaka salama?"

Mimi "Salama kabisa,vipi wewe huko?"

Ally Mpemba "Huku naendelea vema ila narudi wiki ijayo"

Mimi "Sawa kaka,nambie"

Ally Mpemba "Kuna mtu nimempa namba yako atakupigia simu ana mzigo wangu utaenda atakupatia"

Mimi "Sawa kaka ni mzigo gani?"

Ally Mpemba "Ni pesa,hakikisha akikupatia utanipelekea Benki Crdb,nitakutumia vielelezo"

Mimi "Sawa kaka hakuna tatizo"

Ally Mpemba "Pia nimemwambia Farah kuna pesa atakupatia,utachukua utanunua mahitaji yale kama kawaida na itakayobaki utatumia "

Mimi "Nashukuru sana Kaka Ally"

Ally Mpemba "wala huna haja ya kunishukuru, mimi ndiye ninapaswa kukushukuru "

Aliendelea "Nitakufanyia mambo makubwa sana kwa uaminifu wako"

Mimi "Sawa kaka nitashukuru sana"

Baada ya mazungumzo yale mafupi Ally Mpemba akawa amekata simu.

Ilipofika mida ya saa 7 mchana,kuna namba ngeni ikawa imenipigia simu,ilikuwa ni sauti ya mwanamke ambaye alijitambulisha kama Warda.

Mimi "Ndiye mimi"

Warda "Ally kaniambia kuna mzigo wake nikupatie,sijui nakupataje?"

Mimi "Wewe uko wapi?"

Warda "Njoo hapa mtaa wa mkunguni ukifika uniambie"

Mimi "Sawa nakuja muda si mrefu"

Mimi "Aunt Farah samahani naomba unitazamie hapo narudi mara moja"

Farah "Kwani ndo unafunga?"

Mimi "Hapana,kuna mahali nafika mara moja ila nawahi kurudi"

Farah "Ooh sawa kuna hela Ally ameniambia nikupatie,hivyo ukitaka kuondoka utaniambia"

Mimi "Sawa nawahi kurudi"




.......................................................................................




Utajiri wa rafiki yangu ulivyofanya nikamuamini Shetani - 14.



Mimi "Nishafika"

Warda "Umesimama wapi?"

Aliendelea "Ooh ok nishakuona"

Baaada ya nusu dakika alikuja mwanamke mmoja mwenye asili ya uarabuni akiwa amevaa hijab nyeusi ikiwa imempendeza sana kutokana na rangi ya ngozi yake.

Warda "Bila shaka wewe ndiye uliyetumwa na Ally"

Mimi "Yes ndiye mimi "

Warda "Unaitwa nani?"

Mimi "Naitwa Umughaka"

Warda "Mhh mbona Ally hakunitajia jina hilo!"

Mimi "Kaka Ally amezoea kuniita Master,Umughaka ndiyo jina langu halisi"

Warda "Ooh sawa nimekuelewa"

Aliendelea "Ngoja kwanza nimpigie simu halafu nikupe uongee nae"

Alichukua simu yake akaanza kumpigia simu Ally Mpemba na wakaanza kuongea,baada ya kuongea akanipatia na mimi simu ili niongee na Ally,baada ya kujiridhisha aliniambia nifuatane nae.Tulitembea kama hatua kumi kisha tukaingia kwenye nyumba moja ambayo ilikuwa ni ghorofa,ile ghorofa ilikuwa ni Apartment ya watu kuishi na haikuwa kwa ajili ya ofisi.

Baada ya kufika ndani tuliingia kwenye lift nikaona yule dada anabonyeza batani ambayo ilionyesha namba 4,ile lift iling'oa nanga na baada ya sekunde kadhaa tukawa tumefika kwenye floor namba 4,tulipofika tulitembea hatua 3 tukawa tumefika kwenye chumba ambacho baada ya kukifungua tuliingia ndani.

Warda "Nisubiri hapo "

Aliingia chumbani ambako hakutumia muda mwingi akawa ametoka na pochi kubwa ambayo ilikuwa imetuna.

Warda "Hizi ni pesa ambazo Ally amesema nikukabidhi sasa kabla ya kuondoka inapaswa uzihesabu ndipo uondoke"

Alizitoa zile hela kwenye ile pochi kubwa ya kike,kiukweli zilikuwa ni pesa nyingi sana.Nilianza kuzihesabu na kuzipanga ndipo nilipata jumla yake milioni 40.Wakati nazihesabu alikuwa amekaa akiniangalia huku akiendelea kuchezea simu yake.

Mimi "Tayari"

Warda "Umepata bei gani?"

Mimi "Milioni 40"

Warda "Ok uko makini"

Alichukua karatasi pamoja na wino akawa ameweka pale juu ya meza na kuniambia.

Warda "Shika hii"

Aliendelea "Utasaini hapa na hapo chini utaweka dole gumba "

Basi nikafanya kama alivyoniambia na nilipomaliza alichukua simu yake kisha akampigia simu Ally Mpemba.

Warda "Haya nishamkabidhi pesa yako,huyu hapa ongea nae"

Ally Mpemba "Master,huo mzigo nenda kaniwekee benki,nakutumia sasa hivi vielelezo"

Mimi "Sawa kaka"

Warda "Ngoja nikupatie kibegi kidogo,huo mkoba nina kazi nao"

Sasa baada ya kupewa kibegi kidogo,niliziweka zile hela kwenye kile kibegi huku akili yangu ikiwa imechanganyikiwa kabisa,nilipanga nitoroke na zile hela,baada ya kushuka ghorofani nilianza kutembea mdogo mdogo kuelekea mnazi mmoja.

Nilikuwa najisemea uenda ndiyo wakati ambao Mungu aliamua kunitoa kwenye umasikini kupitia zile hela za Ally Mpemba kwa maana hata kama ningeondoka zangu kurudi Mwanza asingepata kwasababu ni mtu tu ambaye nilikutana nae kkoo na halikuwa hanijui kiundani wala haifahamu familia yangu,kiukweli nilikuwa kwenye vita nzito kuhusu zile fedha lakini niliamua nizipelekea Benki ili kuendelea kuonyesha uaminifu wangu kwa Ally,nilisema kama ni umasikini niliandikiwa basi ningekufa masikini tu hata kama ningekimbia na zile hela,pengine ni heri kufa masikini kuliko kuiba cha mtu ambaye ufahamu kakipata vipi,Uaminifu kwangu hata kama usingenilipa lakini ungenijengea heshima kubwa miongoni mwa marafiki na watu wa karibu,hivyo niliamua kuwa muaminifu ingawa nilikuwa nahitaji sana fedha.

Nilitembea kwa haraka sana hadi katikati ya jiji mtaa wa Azikiwe ambapo kwa mujibu wa maelekezo ya Ally Mpemba ilipaswa niende hapo ilipo benki ya Crdb kuziweka hizo fedha.

Baada ya kumaliza kila kitu pale benki,niliondoka zangu kurudi kkoo,nilipofika kwakuwa muda nao ulikuwa umeenda sana,nilimwambia Aunt Farah anipatie kile kiasi ambacho aliambiwa na Ally anipatie ili niondoke zangu kununua mahitaji ya siku hiyo kisha niondoke nikaandae mapema.

Aunt Farah alinikabidhi laki tatu ambazo kwa mujibu wa maelekezo ya Ally Mpemba ni kwamba,laki mbili ningeitumia kwa mahitaji ya vitu kwa siku zilizokuwa zimebaki hadi yeye kurudi na ile laki moja ingekuwa kwa ajili ya matumizi yangu ya kawaida.

Kweli,ile kazi niliifanya kwa uaminifu mkubwa mno hadi siku ambayo alirudi Ally mpemba alikuwa akinishangaa namna nilivyokuwa muaminifu kiasi kile na sikuwahi kumwambia mtu yeyote siri ile.

Ally Mpemba "Kaka kati ya watu na wewe ni mtu!"

Mimi "Kwanini kaka?"

Ally Mpemba "Ndugu zangu si waaminifu kama wewe ulivyo muaminifu"

Aliendelea " Sielewi hata nitakulipa nini!"

Mimi "Usijali kaka haya ni maisha tu!"

Kiukweli nilikuwa najiuliza mle ndani kwa Ally kulikuwa na kitu gani lakini nilikuwa nakosa jibu kwasababu ndani ya siku zote hizo nimekuwa nikiwinda nipate kukiona lakini nilikuwa naishia kusikia sauti tu,mimi sikutaka kuonyesha kama nina wasiwasi,nilichofanya ni kwamba nikiwa nazungumza nae yeye aelewe mimi sifahamu chochote na nilikuwa napotezea mambo mengine ili asije kunoti kitu kutoka kwangu.

Niendelea kupiga kazi yangu ya usajili wa line za simu huku na ile kazi ya usimamizi wa Catering ikiendelea,kiukweli kama kuna muda ambao nilitengeneza pesa ilikuwa ni kipindi hicho,baada ya kupata pesa ya kutosha,nilimtafuta dalali akanitafutia uwanja maeneo ya Chanika Zingiziwa chenye ukubwa wa 25 x 20 nikawa nimenunua Milioni 3.

Nikawa nimepanga nipambane sana ili nikusanye fedha nyinngine nianze ujenzi mdogo mdogo ili nitoke kwenye nyumba za kupanga na mimi niamie kwangu.

Kuna siku tulipata tenda ya kuhudumia chakula maeneo ya Mikocheni,sasa Ally akawa ameniambia siku iliyokuwa inafuata nisiingie kazini ili niende kuwasimamia wale kina mama na vijana kama kawaida yangu maana ndiyo ilikuwa kazi yangu,kiukweli Ally alikuwa akiniamini sana na ilifika kipindi fedha zake zote mimi ndiye nilikuwa nikizipeleka benki,mkurya mimi nikajiona ni mtu mwenye bahati ya kuaminika na na mtu mwenye asili ya uarabu kuliko wakurya wote kutoka Tarime;kweli,siku iliyofuata sikwenda kazini kama kawaida na nilimpigia simu Team leader wangu nikampanga kabisa ili asije akaona baada ya kushika shika vihela nimeanza kuwa na kiburi.

Baada ya maandalizi mimi na timu yangu ya Catering,tukawa tumefika maeneo ya mikocheni kama kawaida,tuliendelea na maandalizi hadi kuhakikisha vitu vyote viko sawa,sasa tukiwa kwenye hiyo shughuli mida ya 2 usiku, Ally akanipigia simu akiwa na kiwewe kisichokuwa cha kawaida.

Ally Mpemba "Master hebu fanya haraka njoo hapa Sinza Mori"

Mimi "Kaka Sinza Mori sipafahamu"

Ally Mpemba "Hebu mpelekee Jabir simu niongee nae"

Baada ya kumpa Jabir simu na kuzungumza nae inaonekana alimwambia Jabir anitafutie muda ule Taxi na akamuelekeza eneo ambalo ningemkuta,sasa baada ya kupata Taxi,Jabir alimpatia maelekezo yule dereva kisha akaniambia niingie kwenye gari tuondoke.

Tulipofika hilo eneo ambalo ambalo Ally alikuwa amesema nimkute pale,nilimpigia simu akaniambia niingie ndani,ilikuwa ni hotel kubwa tu ambayo pia ilikuwa ni bar,nilipoingia ndani nilimkuta jamaa yupo na watu kadhaa wakiwemo mademu wenye asili kama yake wakila na kunywa.

Ally Mpemba "Kaka kanisaidie kufungua chumba,siunajua nimejisahau "

Aliendelea "Aiseee yaani hata sielewi nimejisahau vipi!"

Mimi "Sawa kaka ngoja sasa niwahi!"

Ally Mpemba "Ukishafungua utanirudishia hapa funguo utanikuta hapa hapa "

Mimi "Sawa kaka"

Niliondoka kuelekea kwenye Taxi tukaondoka zetu kuelekea Magomeni,nilipofika nilimwambia dereva Taxi anisubili nje ya geti.Nilifungua mlango kisha nikaingia ndani nikawasha taa,sasa nilipowasha taa sikuona kitambaa cheupe pale kwenye ile meza ya kioo ndipo nilielekea jikoni kwenye kabati nikakikuta ikabidi niende nikitandike kisha nikachukua kabeji na mboga mboga nikaziweka juu ya ile meza,baada ya kumaliza niliondoka zangu nikaenda kufungua ule mlango wa kile chumba.

Sasa nilipomaliza kuufungua ule mlango nikiwa nimegeuza mgongo naondoka ili nitoke ndani nifunge mlango niondoke,aisee nilisikia nimesukumwa na nguvu isiyokuwa ya kawaida,ile nataka kuanguka chini nilimuona kiumbe wa ajabu ananipita kwa kasi ya ajabu akiwa uchi kama alivyozaliwa akikimbilia sebuleni na kuanza kuyafakamia yale makabeji kwa spidi kali mno,nilipokuwa bado naendelea kushangaa na kuhamaki yeye hakuwa kabisa na muda na mimi.

Ndipo nilimshuhudia mwanamke aliyekuwa na asili ya kiarabu lakini akiwa na manywele mengi si kichwani tu hadi kwenye makwapa na sehemu za siri,alikuwa anatoa harufu kali sana ambayo haikuwa ya kawaida. Niliogopa sana na ikabidi nikimbilie nje na kufunga mlango kisha nikaelekea kwenye lile bomba la nje kunawa, baada ya kumaliza kunawa nikatoka nje nikafunga geti nikapanda Taxi kurudi Sinza kumrudishia jamaa funguo, kiukweli roho ilichafukwa sana na niliogopa sana na hata ujasiri niliokuwa nao wote uliyeyuka.

Huruma, majuto na masikitiko vyote kwa pamoja vilinisumbua sana kwa usiku ule; Sasa wakati nikiwa kwenye gari narudi Sinza, Ally Mpemba alinipigia simu akiwa kama mtu aliyepagawa.




........................................................................................





Utajiri wa rafiki yangu ulivyofanya nikamuamini Shetani - 15.




Ally Mpemba "Kaka ...kaka....umefanya nini! Kaka!?"

Mimi "Kuna nini kaka Ally?"

Ally Mpemba "Kaka unataka kuniua?"

Mimi "Kaka Ally uko poa kweli?"

Basi jamaa alianza kulia kwa kwikwi kitu ambacho kilikuwa kikinichanganya zaidi, sikuelewa kama yale maneno aliyokuwa akiniambia yalikuwa ya kwangu au labda kuna mtu alikuwa akimpigia simu bahati mbaya ikaja kwangu!. Nilipofika lile eneo ambalo nilimuacha Ally Mpemba akiwa na rafiki zake sikumkuta hivyo ikabidi nimpigie simu.

Mimi "Kaka nimerudi na sikuoni hapa!"

Ally Mpemba "Nisubiri hapo hapo narudi muda huu"

Haikupita hata dakika 20 jamaa akawa amefika pale akamlipa yule dereva taxi kisha akaniambia niingie kwenye gari yake tuondoke. Wakati tukiwa kwenye gari jamaa alionekana kana kwamba amechukia sana na sikuelewa kilichokuwa kimemchukiza ni kitu gani.

Ally Mpemba "Daah ndugu yangu nilikwambia ufike ufungue tu chumba uondoke sasa wewe umefanya nini?"

Mimi "Kaka nilipofungua chumba ile natoka nielekee nje ndipo yule kiumbe akanipita akikimbilia sebuleni"

Ally Mpemba "Kaka ushaharibu"

Kwa namna ambavyo jamaa alikuwa amechukia niliamua kukaa kimya ili nione atafanya kitu gani, sikutaka kabisa kumuongelesha kwa wakati ule maana niliona ningeendelea kumuudhi, sasa kumbe kile kitendo cha mimi kumuona yule kiumbe wa ajabu kilimshtua Ally Mpemba kule alikokuwa na sikuelewa alijuaje, kiukweli nilibaki na maswali mengi sana ambayo hayakuwa na majibu; Kwakuwa nishakuwa mtu mzima tayari, niliamini hata fedha alizokuwa nazo Ally Mpemba zilikuwa na msukumo wa ushirikina ndani yake, kiukweli niliamua kukaa kimya ili nione ataniambia nini!.

Tulivyofika nyumbani mida ya 4 usiku, nilishuka kwenye gari nikafungua geti kisha jamaa akaingiza gari ndani na kuipaki, alishuka haraka haraka akaniambia hebu njoo ndani, alivyofungua mlango na kuzama ndani tukakuta yule kiumbe amekula kila kitu kilichokuwa pale kwenye meza kama kawaida, sasa Ally Mpemba akaniambia nitoe kile kitambaa nikipeleke jikoni kisha nimsaidie kusafisha pale sebuleni, yeye aliingia chumbani ambako alikaa kwa muda kama wa dakika 5 kisha akawa amerudi pale sebuleni akiwa amevaa kanzu nyeupe akiwa amejifunga na kitambaa, mkononi akiwa ameshika kanzu nyingine nyeupe akanitaka niivae.

Ally Mpemba "Vaa hii tafadhali!"

Mimi "Nivae juu ya nguo zangu hizi?"

Ally Mpemba "wewe vaa hivyo hivyo tu!"

Baada ya kuvaa ike kanzu ambayo ilikuwa ikinukia manukato mazuri, alichukua kitambaa cheupe kama alichokuwa amejifunga kichwani akanifunga na mimi!. Kimuonekano tulifanana kama wale jamaa wa dubai au saudia wanaovaa kanzu na vilemba.
Aliisogeza ile meza ya kioo pembeni kisha akatandika nguo ngumu kama kikoi kisha akanitaka nimsogelee.

Ally Mpemba "Wewe ni rafiki yangu na ninakuamini sana, tafadhali nisaidie!"

Mimi "Nikusaidie nini kaka?"

Ally Mpemba "Nifuate nitakavyokuelekeza"

Mimi "Sawa kaka"

Ally Mpemba alikuwa akitamka maneno ya kiarabu ambayo alinitaka na mimi nimfuatishe, alikuwa akitamka huku tukiwa tumekaa chini ya kile kikoi, baada ya kufanya lile zoezi kwa kurudia rudia kwa muda wa nusu saa tukawa tumemaliza na kisha akatoa kile kikoi akawa amekirudisha chumbani kwake. Aliporudi tena pale sebuleni aliniambia nikae kwenye sofa nami nikaa!.

Ally Mpemba "Kaka naomba ulichokiona ibaki siri yako!"

Aliendelea "Hakuna mtu yeyote anayejua hili jambo isipokuwa wewe"

Mimi "Usijali kaka haya ni maisha tu!"

Ally Mpemba "Mimi nilikuchukua wewe unisaidie mambo yangu kwakuwa wewe una mkondo wa hela"

Aliendelea "Na umekuwa muaminifu nahitaji kukufikisha mbali zaidi!"

Aliendelea "Huyo uliyemuona siyo kiumbe wa ajabu bali huyo ndiye anayenipatia hela na mali hizi unazoziona"

Aliendelea "Siyo mkorofi na akikupenda utamfurahia, huwezi kujiuliza kwanini wewe ndiye nilitaka uwe karibu na mimi?"

Wakati ananiambia mambo yote hayo mimi nilikuwa nimetulia tu nikimuangalia huku nikitikisa kichwa cha kuonyesha ukubali kwenye maswali aliyotaka ukubali wangu.

Ally Mpemba "Wewe una nyota ya utajiri master labda uichezee mwenyewe!"

Mimi "Kweli kaka!?"

Ally Mpemba "Una nyota ya pesa ambayo pesa ikija kwako haitoki labda uitoe mwenyewe au mtu akuchukue uwe unamzalishia pesa!"

Aliendelea "Kaka mjini hapa, ukifa masikini shauri yako, mimi nakushauri kama rafiki yako"

Mimi "Kaka kuna mtu anapenda umasikini? Nahangaika juani ili nipate pesa kaka"

Ally Mpemba "Pesa unatembea nayo nyuma yako harafu unasema unahangaika juani! Watu wa bara hamjuagi kuchangamka!"

Mimi "Kaka nielekeze namna ya kufanya"

Ally Mpemba "Wewe una kifua? Siyo unapenda kupanda tu kwenye Range ukadhani mambo ni mepesi"

Mimi "Kaka kama nimewahi kushika bunduki hakuna jambo litakalonishinda"

Ally Mpemba "Bunduki mwatumia huko bara, hapa mjini twatumia kisomo tu mambo yajipa!"

Aliendelea "Hebu simama unifuate"

Nilisimama nikamfuata Ally Mpemba kisha tukaingia kwenye kile chumba kilichokuwa na yule kiumbe wa ajabu, baada ya kuingia ndani aliwasha taa akasogea mpaka kwenye kabati la ukutani kisha akalifungua, alipolifungua akaanza kuita kwa sauti.

Ally Mpemba "Mayaaa"

Aliendelea "Wewe Maya toka nje nakuita"

Alipokuwa akiita yule kiumbe akawa anaunguruma kwa mtetemo, kiukweli nilisogea nyuma kwa hofu maana haikuwa hali ya kawaida na sikuelewa siku zote jamaa alikuwa akiishi vipi mle ndani peke yake na yule kiumbe bila ndugu zake kujua jambo lolote!.

Baada ya kuita hilo jina la Maya kwa muda kadhaa, yule kiumbe wa ajabu alitoka na alipotoka alipomuona jamaa alimuinamia kama kumsujudu, kiukweli kilikuwa ni kitendo kilichonishangaza sana kwasababu Ally Mpemba kila alichokuwa akimwambia yule kiumbe alionekana kuelewa na kuogopa. Ally Mpemba kuna lugha aliongea nae kisha yule kiumbe aliyekuwa akitoa harufu ya ajabu aliondoka akarudi kwenye lile kabati kisha Ally Mpemba akarudishia lile kabati.

Kumbe kwenye lile kabati kulikuwa kumechimbwa shimo kama la futi sita na ndipo yule kiume alikuwa akikaa, sasa kama ulikuwa ukifungua ile kabati ilikuwa ngumu kumuona kwasababu alikuwa akiingia kwenye lile shimo kulikuwa na ubao ambao ulikuwa ukifunika na hivyo siyo rahisi mtu wa kawaida hata kama ingetokea kuingia mle chumbani kujua kama kulikuwa na mtu mle ndani labda kama ikitokea umeingia yule kiumbe aanze kuunguruma!.

Mimi "Kaka huyu ni nani kwani?"

Ally Mpemba "Nishakwambia huyo ndiye kila kitu kwangu sheikh"

Aliendelea "Watu wa Bara hapa mjini mmekuja kuwashangaa watu"

Aliendelea "Au nawe unataka kuwa msindikizaji?"

Mimi "Hapana kaka"

Ally Mpemba "Kwanza kabla ya kukusaidia inapaswa uslim"

Mimi "Kuslim tu kaka, mbona haina shida hiyo"

Ally Mpemba "Usiseme haina tatizo, usijedhani ni kuslim kama unavyodhani weye!"

Ally Mpemba "Mtu wa kukusilimisha apatikana hapo chumbe"

Aliendelea "Uko tayari mi nimuandae?"

Mimi "Mimi nipo tayari kaka"

Aliendelea "Sawa lakini haya yote uliyoyaona humu ndani yabaki humu humu ndani, utanichukiza sana nikiyasikia sehemu na walahi sitokuacha salama"

Baada ya maneno hayo nilianza kuingiwa uoga na hofu ya ajabu,kiukweli sikujua ni kitu gani kilichokuwa kinanitia hofu muda huo lakini nachokumbuka ni kwamba niliingiwa na hofu. Sasa baada ya majadiliano yale, Ally Mpemba alinipatia funguo za gari ile Aud akanitaka nikalale, sikufahamu ni kwanini vile vyumba vingine ambavyo vilikuwa vimefungwa hakutaka nilale huko hadi aniambie nikalale kwenye gari nje, kiukweli kwa maisha jamaa aliyokuwa akiyaishi ilifika sehemu na mimi nikazamani kuwa kama yeye.

Marafiki muda mwingine hutushawishi hadi kujikuta tunaangukia kwenye maisha mabaya kuliko hapo mwanzo, mimi baada ya kufahamiana na Ally Mpemba nilidhani huenda maisha yangu yangekuwa mazuri kumbe haikuwa kama nilivyodhani, ilifika sehemu nikaacha kazi yangu ya usajili wa line iliyokuwa ikinipatia fedha halali na kudandia maisha ambayo baadae niliyaona ni kero na yenye majuto.

Kiukweli ilifikia hata kazi niliyokuwa nikiifanya niliiona ya kipumbavu baada ya Ally Mpemba kuwa ananipatia fedha nyingi za bure bure ambazo nilizifurahia bila kujua kuna siku zingenigharimu. Tangu nimemfahamu Ally Mpemba na pamoja na yeye kuwa rafiki yangu, sikuwahi hata siku moja kulala kwenye ile nyumba yake na yeye mwenyewe hakuruhusu mimi kulala mle ndani.

Baada ya wiki kama mbili tulijiandaa na jamaa akawa mwenyeji wangu kuelekea kisiwa cha Chumbe Unguja.





........................................................................................





Utajiri wa rafiki yangu ulivyofanya nikamuamini Shetani - 16.



Ukiachilia mbali kile kivuko cha Kigongo - Busisi pamoja na kupanda ile mitumbwi ya shemeji yangu(masamaki) kule kisiwani Ijinga sikuwahi kabisa kupanda Boti ya kisasa, hiyo ndiyo ilikuwa mara yangu ya Kwanza kupanda ile boti nzuri na ya kisasa.

Sababu za mimi na Ally Mpemba kwenda Chumbe zilikuwa mbili, moja; Ni kwamba baada ya mimi kumshuhudia yule kiumbe wa ajabu mle ndani, Ally Mpemba kuna miiko aliivunja kutokana na maelekezo ya mtaalamu wake, hivyo tulienda ili akaone namna ya kurekebisha kabla mambo hayajaharibika, pili; ilikuwa ni mimi kuzitaka mali baada ya ushawishi wa Ally Mpemba, sasa ilifika hatua na mimi nikashawishika na kuona ile kazi yangu ya usajili wa line ilikuwa ikinipotezea muda tu.

Baada ya kufika Unguja hatukutaka kupoteza muda, Ally Mpemba aliniongoza hadi kwa huyo mtaalamu aliyekuwa akimfahamu hapo Chumbe, mawazo yangu nilidhani huenda huyo jamaa angekuwa na makolo kolo kama ambavyo nilizoea kuwaona wataalamu wengi wa mikoani namna wanavyokuwa, ila yeye alikuwa kawaida tu!. Baada ya kufika kwa huyo mtu hatukumkuta na tulimkuta mwanamke aliyekuwa amevaa hijab akamwambia Ally Mpemba kwamba ameenda kuswali na tulichofanya tuliamua kumsubiri pale kwake.

Aliporejea kutoka kuswali alitukuta tukiwa tumekaa kwenye mkeka tukimsubiri, baada ya kumuona Ally Mpemba walisalimiana na mimi pia nikamsalimu. Alimuita Ally Mpemba akamwambia aingie ndani, baada ya mazungumzo ya takribani nusu saa, Ally Mpemba alirudi nje akiwa amebeba Vitu ambavyo sikuvielewa na akanitaka tuongozane nae. Nilimfuata nyuma Ally Mpemba hadi tukaifikia miti pori iliyokuwa kando ya Bahari. Nyuma yetu pia alikuwa akija yule mzee aliyekuwa amevaa kanzu huku mkononi akiwa amebeba Mkeka na vitu vingine, baada ya kufika eneo ambalo yeye aliona ndipo panafaa, alituambia tuvue nguo.

Mzee "Vua nguo zenu"

Mimi na Ally Mpemba tulivua nguo tukabaki kama tulilivyozaliwa, baada ya hapo alinikabidhi kichupa kidogo ambacho kilikuwa cha Gliselin, sasa kile kichupa ndani yake hakukuwa na Gliselin bali kilikuwa na kitu kama damu, baada ya kukipokea akanikabidhi na bangili la chuma(Hili huwa wanapenda kulivaa watu mbalimbali mikononi). Sasa baada ya kukabidhiwa hivyo vitu alitutaka tukae chini kwenye ule mkeka, alitoa kopo kama chetezo kisha akaweka vitu kama tumbaku iliyokauka, baada ya kuona imeenea kwenye kile chombo akatoa kiberiti akawasha, baada ya kuwasha akaanza kuongea kwa kiarabu huku akiwa anatikisa mgongo kwa kwenda mbele na kurudi nyuma. Baada ya kuwasha kile chombo kulikuwa na harufu nzuri sana kama udi lakini yenyewe ilikuwa nzuri zaidi ya udi.

Alipomaliza kusoma kisomo aliniambia nisimame.

Mzee "Waiyona ile bahari?"

Mimi "Ndiyo naiona"

Mzee "Weye nenda pale, ukifika pale chukua hicho kikopo mwaga Baharini ukimaliza chota maji na hicho kikopo uyalete hapa"

Kweli niliondoka zangu kushuka baharini huku nikiwa mtupu kama nilivyozaliwa,yale maeneo hakukuwa na watu kabisa na kulikuwa na miti ambayo isingekuwa rahisi watu kuona mnafanya kitu gani,sikufahamu kama mara zote Ally Mpemba alikuwa akija Unguja analetwa hilo eneo au siku hiyo tulipelekwa tu kwa kazi maalumu.

Nilipofika lile eneo la wazi la bahari nilifanya kama mzee alivyoniambia kisha nikageuza kurudi,nilipofika nilikuta Ally Mpemba akiwa amelazwa kwenye ule mkeka akiwa anapakwa mafuta ambayo sikuyafahamu mgongoni hadi miguuni,sasa alipomaliza ile shughuli kwa Ally Mpemba akaniambia nikae chini kwenye ule mkeka.

Mzee "Sogea kaa hapa"

Baada ya kukaa kwenye ule mkeka akachukua kale kakopo ka Gliselin nilikokuwa nimeweka maji ya bahari akamimina yale maji kwenye chombo kidogo cha udongo kilichokuwa kama chungu lakini kilikuwa kidogo kisha akaanza kuchanganya kwa ndani na mikono,baada ya kumaliza akaanza visomo kwa lugha ya kiarabu,sikuelewa alichokuwa anamaanisha ni kitu gani,sasa baada ya kumaliza akachukua lile bangiri ambalo alikuwa amenipatia mwanzo kisha akalichovya kwenye ule mchaganyiko na kunitaka nivae.

Sasa baada ya kuvaa lile bangili nikasikia limenibana mkono mithiri ya mtu kama kafungwa na waya mikononi, cha ajabu nikaanza kuona damu zinatiririka mkononi, damu zilipoanza kutitirika mkononi akachukua kile chombo kilichokuwa kama chungu akawa anazikinga matone yale yaliyokuwa yakidondoka.

Mzee "Unahisi maumivu?"

Mimi "Hapana"

Mzee "Ukihisi maumivu niambie"

Ile damu iliendelea kutoka kwa mfululizo pasipo kukoma ndipo nikaanza kuhisi maumivu mkononi nikamwambia yule mzee!. Baada tu ya kumwambia nahisi maumivu, alinishika akaanza kuongea maneno yaleyale kisha ile bangili ikalegea na damu zikakoma kutoka. Alichukua kile chombo kilichokuwa kama chungu akakisogeza pembeni kisha akaniambia mimi na Ally tukae chini.

Mzee "Alfwat amekubali toba ya ndugu yako"

Aliendelea "Hakikisha hii hali haijirudii tena na nitamfungamanisha na Alfwat kama ulivyonieleza na atamsaidia kama anavyokusaidia wewe"

Basi baada ya maelezo hayo mafupi, alichukua ile bangili ikiyokuwa imechovya kwenye damu pamoja na mchanganyiko wa dawa kisha akanitaka niivae.

Mzee "Hakikisha hii hauivui mkononi na kama ukipata tatizo inapaswa Ally Mpemba akulete kwangu!"

Mzee "Alfwat amekupenda na nilimueleza hilo suala ndugu yako hapa, unachopaswa kufanya ni kumtunza"

Aliendelea "Kwa ulichokifanya kama asingekuwa amekupenda kitendo cha kumvaa mkononi angekumaliza"

Aliendelea "Jambo la kwanza, inapaswa umvae huyu Alfwat na popote uendapo hakikisha unakuwa nae usimuache na kama nilivyokwambia kukiwa na tatizo utamwambia huyu bwana akulete, usithubutu kukanyaga huku ukiwa mwenyewe"

Mzee "Jambo la pili, hakikisha kila itakapokuwa inafika Ijumaa ya mwisho wa mwezi, utachukua wembe na utajichanja chini ya mkono huu wa kushoto ambao ambao unavaa hii bangili, baada ya kuchanja Alfwat atakuja na utamlisha, akishiba atakuacha na ndipo mambo yako yatashamiri "

Mimi "Nikioga nayo haina tatizo?"

Mzee "Hiyo haina tatizo wala usijali kuhusu kuoga na usije ukajaribu kuivua!"

Mimi " Sawa na nitajuaje Alfwat ameshiba?"

Mzee " Ukiona bangiri inakubana na ukahisi maumivu utashika bangiri na utaipaka mchanganyiko wa damu yako hii ambayo nimekuwekea kwenye kikopo kisha Alfwat atakuachia"

Mimi "Sawa nimekuelewa"

Baada ya maelezo hayo ya kina alituambia tunyanyuke na tukusanye kila kitu na kuondoka kurejea kwake, baada ya kufika kwake hatukukaa sana na tuliondoka kuelekea Unguja ambapo tulifikia kwa bwana mmoja aliyekuwa na asili ya kipemba na nilitambulishwa na Ally kama ndugu yake, tulilala pale kisha kesho yake tukaondoka kurejea Dar es Salaam.

Muda huo nilikuwa nimevaa ile bangiri mkononi na kisha Ally Mpemba akawa ameweka vitu kadhaa ambavyo tulitoka navyo kwa huyo mzee aliyemfahamu yeye.

Baada ya kufika Dar es Salaam nilielekea nyumbani nikaachana na Ally Mpemba pale bandarini, baada ya kufika nyumbani nilichukua kile kichupa kidogo nikakitunza ndani. Niliendelea kupambana kibishi na ile kazi yangu ya usajili wa line huku mkononi nikiwa nimevaa bangiri kama urembo kumbe haikuwa hivyo!.

Sasa ilipofika ijumaa ya mwisho wa mwezi Ally Mpemba alinitaka niende nyumbani kwake.



.....................................................................................





Utajiri wa rafiki yangu ulivyofanya nikamuamini Shetani - 17.




Nikiwa njiani naelekea kwake alinipigia simu akinitaka nipitie pale Big Bon nimsubiri atoke msikitini kisha tuandamane nae hadi kwake. Baada ya muda kupita Ally Mpemba alirudi kutoka msikitini na aliniambia nipande gari yake kisha tuondoke.

Ally Mpemba "Swalama master"

Mimi "Mimi niko poa kaka"

Ally Mpemba "Usiogope mdogo wangu haya ni mambo ya kawaida sana hapa mjini!"

Aliendelea "Wewe nakuona utakuwa mtu mkubwa sana "

Mimi "Kweli kaka?"

Ally Mpemba "Wewe tulia tu utajionea"

Tulipofika kwake niliteremka kwenye gari na kwenda kufungua geti kisha akaingiza gari ndani.

Sasa tulipofika ndani mimi nilikaa pale sebuleni halafu Ally Mpemba yeye akawa amepitiliza moja kwa moja kuingia chumbani kwake, ilipofika mida ya saa 10 Alasiri nikiwa nimekaa pale sebuleni nikisubiri animbie alichoniitia, ndipo nikahisi mkononi nimeanza kubanwa na ile bangiri; Ilibana kwa nguvu huku damu ikaanza kunitoka kwenye mkono ambayo haikuwa nyingi sana, ilipoendelea kubana sana hadi kuihisi maumivu nilichomoa kile kichupa kidogo cha Gliselin kilichokuwa na ule mchanganyiko wa damu na dawa nikaanza kuipaka ile bangili, baada ya dakika 2 hivi ndipo nikahisi ile hali ya kubana inaachia. Kiukweli baada ya lile tukio nilijisikia mwepesi kupita maelezo, kila jambo mbele yangu niliona halina kizuizi chochote.

Nikiwa naendelea kumsubiri Ally Mpemba pale sebuleni nilisikia ule mlango wake ukifunguliwa na ndipo kutazama nikidhani ningemuona Ally Mpemba haikuwa hivyo, alikuwa ni yule kiumbe wa ajabu akitoka ndani ya kile chumba akirudi kwenye chumba chake,sikuelewa alichokuwa amefata ni nini kwenye kile chumba na alionekana kama kushangaa sana!.

Baada ya muda Ally Mpemba nae alitoka ndani kisha akakifunga kile chumba. Sikujua yule kiumbe alipita muda gani kuingia kwenye chumba cha Ally Mpemba wakati nikiwa pale sebuleni kwasababu ile nyumba namna ilivyokuwa imekaa, ilikuwa rahisi mtu akitoka au kuingia chumbani kuonekana, yawezekana alikuwa chumbani kwa Ally Mpemba muda mrefu na Ally Mpemba alipofungua chumba basi alimwambia aondoke aelekee chumbani kwake kulikokuwa na shimo chini ya kabati.

Lakini kilichonishangaza zaidi ni muda Ally Mpemba aliotumia alipoingia chumbani, tulifika hapo nyumbani kwa Ally mida ya saa 8 mchana baada ya kutoka Kkoo, mimi niliendelea kukaa pale sebuleni hadi mida ya saa 10 alasiri ndipo kubwana na ile bangiri ambayo niliambiwa ni Alfwat anakula; kuna masaa kama mawili Ally Mpemba alikuwa chumbani kwake na yule kiumbe ambaye hadi wakati huo nilikuwa simuogopi baada ya kuzoea yale mazingira na kuhakikishiwa na Ally Mpemba usalama wangu wa Kimwili na Kiroho.

Ally Mpemba "Vipi zoezi lako limekamilika?"

Mimi "Ndiyo kaka "

Ally Mpemba "Wewe ni muaminifu sana na ndiyo maana nakupenda sana!"

Aliendelea "Kama nilivyokwambia, wewe utakuwa mtu mkubwa sana kwasababu huogopi kuyatafuta mafanikio"

Aliendelea "wabongo wengi hawafanikiwi kwasababu wanadhani mafanikio hujileta tu kwa kupiga blah blah, mafanikio yanatafutwa kwa nguvu isiyokuwa ya kawaida master"

Aliendelea "Nitakusapoti mwanangu kwakuwa na wewe umenisapoti na umeonyesha uaminifu kwangu tangu nilipokuamini, sikukosea kukuchagua uwe rafiki yangu!"

Aliendelea "Kwasasa hizi ni hatua za awali tu ila nakuona mbali sana, ukiendelea hivi sidhani kama nitakusogelea kwa pesa master"

Kiukweli maneno ya Ally Mpemba yalinichochea sana hadi kuwaza kufanya mambo makubwa ili nipate pesa na mimi niwe mtu maarufu mjini na niendeshe magari ya gharama kama watu wengine.

Baada ya maongezi yale na Ally Mpemba nilimuuliza huenda kulikuwa na ishu yoyote alitaka kuniambia ili niweze kurudi nyumbani mapema.

Ally Mpemba "Hivi unaweza kuendesha gari?"

Mimi "Ndiyo kaka naweza japo sina leseni!"

Ally Mpemba "Ulijifunzia wapi gari master wewe!"

Mimi "Kaka wala sikwenda chuo kujifunza bali kuna mahali nilikuwa napewa kusogeza kidogo tu hadi nikafahamu kimtindo!"

Ally Mpemba "Kwahiyo unaweza kusogeza kimtindo?"

Mimi "Ndiyo kaka!"

Ally Mpemba "Ulikuwa muosha magari nini!"

Mimi "Kwanini kaka?"

Ally Mpemba "Nimeuliza tu maana jamaa wao ndiyo huwa wanaweza kusogeza kimtindo lakini kuendesha kwao ni changamoto!"

Mimi "Hapana kaka, mimi nilijua kusogeza gari miaka fulani nilikuwa mpiga debe"

Ally Mpemba "Duuuu ushawahi kuwa mpiga debe?"

Mimi "Ndiyo kaka!"

Ally Mpemba "Basi kama ndivyo wewe ni faita, kumbe nakuchukulia poa eeeh!"

Mimi "Kawaida tu kaka ni moja ya utafutaji!"

Ally Mpemba "Ok, sasa itabidi nikusajilie ile gari Aud ili uwe unatembelea miradi yangu pamoja na kufanya ishu zako ziwe rahisi!"

Mimi "Kweli kaka?"

Ally Mpemba "Sijawahi kuongopa na ninachoamini wewe unakuja kuwa mkubwa zaidi yangu, jambo la msingi ni kunitunzia siri vinginevyo tusije tukalaumiana!"

Mimi "Kaka kwa hilo tu usijali "

Ally Mpemba "Hapa kwangu umewahi kumuona mtu mwingine zaidi yako kwa muda huu tu ambao nimefahamiana na wewe?"

Mimi "Hapana kaka sijawahi kumuona mtu yeyote!"

Ally Mpemba "Ok, je umewahi kumuona ndugu yangu yeyote hapa kwangu kwa wale unaowafahamu?"

Mimi "Hapana kaka"

Ally Mpemba "Ok uwe unajiuliza kwa nini wewe ninakupa kipaumbele kuliko ndugu zangu!"

Aliendelea "Wewe ni mtu muhimu sana kwangu hivyo usije ukafanya nikakosa uamimifu kwako itakuwa ni mbaya sana katika maisha yako!"

Mimi "Sawa kaka sitokuangusha"

Ally Mpemba "Hivi karibuni nataka kufanya safari ya Oman ila kabla ya kuondoka nitaomba uwe unanisitiri kwa kipindi chote ambacho sitokuwepo!"

Mimi "Wala usijali kaka wewe ushakuwa zaidi ya ndugu!"

Sasa baada ya kusikia jamaa anataka kunipatia ile Aud mpya niwe natembelea, kiukweli nilikuwa nina furaha ya ajabu na nilijikuta nawaza mambo mengi sana na jambo ambalo lilikuwa la kwanza kichwani mwangu baada ya kupata ile gari, safari ya kwanza ingekuwa kwa mjomba Nico kule Ununio ili niende nikaonyeshe taizi la nguvu na kuonyesha siku hizi niko Matawi ya juu, pili nilipanga niwe naingia nalo pale ofisini Buguruni kuwalingishia wale mademu waliokuwa na nyodo na kuniona mimi mshamba!. Kiukweli niliona kama jamaa ananicheleweshea ile mashine na ndiyo maana ilifikia wakati kila jambo alilokuwa akiniambia nilikuwa nikimjibu kwa haraka haraka bila kujiuliza mara mbili mbili madhara ya kile kitu alichokuwa ananiambia.

Ally Mpemba "Unajua maana ya kunisitiri lakini master?"

Mimi "Kaka sitoweza kupayuka kwa watu na kama nikifanya hivyo wewe nifanye unavyoweza"

Ally Mpemba "Mimi simaanishi hivyo master, siyo kwamba sikuamini kwamba wewe ni msiri ila nahitaji uwe unanisitiri kwa kipindi chote hicho ambacho sitokuwepo"

Mimi "Kaka kukusitiri kiaje?"

Ally Mpemba "Umefanya vema kuniuliza na mimi nilisubiri swali lako sema ulikuwa unazunguka!"

Aliendelea "Nadhani wewe waweza kuondoka halafu mambo mengine nitayashughulikia mimi"

Mimi "Kaka hujaniambia lakini kuhusu kusitiri "

Ally Mpemba "Nitakujuza tu wala usijali,siku ya kuondoka nadhani gari nayo itakuwa tayari hivyo nitakujuza"

Mimi "Sawa kaka, basi mimi ngoja niwahi usafiri wetu wa kugombania"

Ally Mpemba "Nisubiri kidogo nakuja"

Baada ya kuniambia nimsubiri, aliingia chumbani ambako hakuchukua muda akawa ametoka na kiasi fulani cha pesa na kunikabidhi nikitumie kama nauli.

Mimi "Nashukuru sana kaka!"

Ally Mpemba "Hupaswi kunishukuru, mimi ndiyo napaswa kukushukuru!"

Niliondoka zangu mle ndani kuelekea nje kisha nikaanza kuhesabu zile hela nikakuta ilikuwa laki 2, kiukweli nilifurahi sana kimoyo moyo na kujiona ni mtu mwenye bahati sana kuwa na urafiki na Ally Mpemba mwenye asili ya arabuni.

Nilipanda zangu gari za Gongo la mboto zilizokuwa zinatokea maeneo ya Morocco, ingawaje zilikuwa zimejaa lakini hakukuwa na namna,nilichowaza mimi nikufika nyumbani sikuwaza uwingi wa abiria. Baada ya kufika nyumbani mida ya saa 12 jioni nilifungua mlango na kuingia ndani, nilipofika sebuleni kwangu niliwasha taa kisha nikawa naelekea chumbani,kama nilivyosema hapo awali ya kwamba, nikuwa nimepanga kwenye nyumba ya vyumba viwili,hivyo kulikuwa na chumba na sebule,ndani kwangu kulikuwa na kila kitu ambacho kijana wa kisasa angetamani kuwa nacho.

Baada ya kufungua chumba na kuingia ndani niliwasha taa, sasa nilipowasha taa kuna hela ambazo zilikuwa mpya noti za shilingi elfu kumi kumi nilizikuta pale kitandani, kiukweli nilishangaa sana zile hela na sikujua ni nani alikuwa ameziweka hapo kitandani, nilidhani huenda ile asubuhi wakati natoka nilizisahau pale kitandani lakini bado haikuingia hakilini kwasababu sikuwa na hela yeyote hapo ndani kwa wakati huo. Niliamua kusogea na kuzikamata zile hela na kuanza kuzihesabu moja baada ya nyingine, sasa wakati nahesabu zile hela nikawa nasikia kuna mtu anagonga mlango!.

Nilitoka chumbani kwenda kuufungua ule mlango, baada ya kuufungua ule mlango kumbe alikuwa ni yule demu wake na Steve.

Zuu "Shem mambo"

Mimi "poa, mambo vipi?"

Zuu "Safi, niazime simu yako nimpigie Steve maana kwangu sina salio!"

Mimi "Ok ngoja nikuletee"

Niliingia ndani nikachukua simu kisha nikampigia simu Steve baada ya kumpata nikampa aongee na demu wake kisha mimi nikarudi chumbani kwenda kuendelea kuhesabu zile hela, nilipokuwa nikiendelea kuhesabu zile hela, demu wa jamaa aliniita niende nikachukue simu, sasa nilipofika nilikuta bado simu haijakata na ndipo akaniambia Steve anaomba kuongea na mimi.

Mimi "Mwanangu niambie!"

Steve "Mwanangu naomba umuazime shemeji yako gesi yako apikie maana kwangu imeisha, nikirudi nakuja kuchukua kaka"

Mimi "Usijali kaka ngoja nimpatie hela akabadili mtungi halafu wewe utanirudishia!"

Steve "Utakuwa umenisaidia sana mwanangu"

Baada ya kuelewana na Steve,niliingia ndani nikachukua elfu 50 kwenye zile hela ambazo Ally Mpemba alinipatia kama nauli nikawa nimempatia demu wa jamaa ili akabadili mtungi wa gesi, baada ya kumpatia mimi nilirudi ndani kuendelea na zoezi la kuhesabu zile hela, baada ya kumaliza kuzihesabu jumla yake zilikuwa milioni 5, kiukweli nilifurahi sana na nikaona mambo yangu yanazidi kunyooka tu bila kutumia nguvu nyingi. Sasa mpango wangu ulikuwa ni kwamba, nichukue zile hela niongezee na ambazo nilikuwa nimedunduliza benki ili nianze kufanya biashara ya viazi mbatata kutoka Mbeya na niachane na mambo ya kusajili line za simu.

Kwakuwa dhamira yangu ilikuwa kuwa mfanyabiashara mkubwa wa viazi mbatata hivyo nikaona nianze kutengeneza koneksheni ya madalali pale soko la Ilala na Mabibo ili kuweza kulifahamu na kuliteka soko, sasa baada ya kujiridhisha bei ya soko nikaona nichukue kale ka hela kangu nilikokuwa nimedunduliza benki pamoja na ile hela niliyoikuta pale kitandani kisha nikapata milioni 7.

Niliamua kumpigia simu team leader na kumdanganya kwamba naelekea nyumbani kulikuwa na matatizo huku lengo langu ni kuelekea mkoani Mbeya kukusanya viazi mbatata na kuvileta mjini ili nipige pesa, lengo la kumuaga team leader ni asiendelee kuniona mzembe katika kazi ile ya kusajili line ili kuendelea kuweka uaminifu asije kuninyang'anya kodi akampatia mtu mwingine,nilitaka ile kazi niiache mdogo mdogo bila kuondoka kwa dharau maana nilichoamini ni kwamba maisha hubadilika.

Niliianza safari ya kuelekea Mbeya kwenda kukusanya viazi na kuvileta mjini.




.......................................................................................





Utajiri wa rafiki yangu ulivyofanya nikamuamini Shetani - 18.



Nilifanikiwa kufika Mbeya na kuanza kuzunguka kukusanya viazi huku nikiendelea kuwatumia madalali ili kufanikisha kwa haraka niweze kurudi mjini kuuza mzigo.

Nilitumia takribani wiki 1 kununua mzigo na kupakia kwenye fuso kisha kuuleta mjini Dar es Salaam, nilipofikisha mzigo mjini hali haikuwa kama nilivyodhani mwanzo, wale madalali ambao niliongea nao tangu mwanzo nilipokutana nao walianza kuniambia mzigo kwasasa umekuwa mwingi na umeshuka bei.

Niliamua mwenyewe kupita na kufanya utafiti kwenye masoko ya Ilala, Buguruni na Mabibo na kugundua ya kwamba wale madalali walikuwa na nia ya kunipiga kwasababu hakukuwa na mzigo mwingi wala nini! Nilichoamua ni kuanza kuuza ule mzigo mwenyewe, ule mzigo kiukweli ulinikata sana na namshukuru Mungu niliambulia kiasi kidogo cha pesa kwasababu kuna magunia mengine ya viazi yalioza kwasababu ya kukaa chini muda mrefu bila kuuzwa.

Nilichogundua ni kwamba wale madalali mwanzo walikuwa wakinipanga ili nilete mzigo mjini na nikisha ufikisha wao ndiyo wanipangie bei ya kuuza, wao wajipatie pesa nyingi kupitia mzigo wangu halafu mimi nipate faida kidogo, sasa nilipowakataa wakasambaza maneno kichini chini kwamba mzigo wangu haufai hivyo kila mteja akawa anaupita tu kama anaaga maiti kiukweli ile hali ilinifedhehesha sana hadi kuna watu ambao ni wema walinishauri niuuze wote kwa jamaa mmoja pale Mabibo ambaye alikuwa ni dalali na alinipatia fedha nusu ya mtaji, kiukweli kwasababu ndiyo ilikuwa mara ya kwanza kuifanya ile biashara sikutaka kabisa kuendelea nayo kwasababu ilikuwa na fitina kubwa mno na mpaka leo sielewi watu wengine wanawezaje kufanya biashara ya viazi.

Baada ya kuona hiyo biashara imenishinda kwasababu ya fitina ya mswahili, niliamua kurudi zangu kwenye usajili wa laini za simu huku nikiendelea na majukumu mengine ya usimamizi wa miradi ya Brother Ally Mpemba.

Baadae nilichokuja kugundua ni kwamba, hakukuwa na fitina za mswahili wala nini, ile hela ambayo nilikuwa nikiipata kila Ijumaa ya mwisho wa mwezi kiukweli kila nilipojaribu kuifungulia biashara iligoma kabisa kwasababu ukiachilia mbali biashara hiyo ya viazi, nilifungua duka la nguo za kike pale Tandika na kuna jamaa mmoja kutoka Iringa nilimuajiri aniuzie, ilikuwa ni siri sana na sikutaka mtu yeyote ajue kuhusu hilo, lile duka halikufikisha hata miezi 6 likawa linaporomoka, mtaji na faida havikujulikana vinapotelea wapi.

Nikajaribu kumchunguza yule bwana mdogo nikadhani huenda akawa ananipiga kumbe haikuwa hivyo, lile duka nikaamua kuliuza na bidhaa baadhi zilizokuwa zimebaki, kwakuwa mwanzo nilipata ugumu kuelewa ila kadiri siku zilivyosonga ndipo akili na ufahamu vikanijia nikafahamu ya kwamba ile hela ilikuwa na matatizo, sasa nilichoamua ni kwamba ile hela niingize kwenye ujenzi wa nyumba yangu nitakayokaa huko Chanika kwenye uwanja wangu(Nitakuja kueleza kilichotokea maana hali ilikuwa mbaya kuliko nilivyodhani).

Sasa kwakuwa nilikuwa na kiasi cha fedha ambacho nilibaki nacho, niliamua kununua ramani ya nyumba na kwenda kuanza ujenzi kwenye uwanja wangu kule Chanika ili ule uwanja usiendelee kuota nyasi, baada ya kupiga msingi na jamvi niliamua kuachia hapo ili niendelee kuvuta nguvu za kupandisha boma.

Sasa kuna siku Ally Mpemba alinipigia simu akawa amenitaka nionane nae pale kwake ili tupange mipango kadhaa kwasababu yeye alikuwa anahitaji kusafiri kama alivyokuwa ameniambia awali, tulikubaliana tungeonana Jumapili ya wiki hiyo pale nyumbani kwake kwasababu pia hata mimi Jumapili mara nyingi nilikuwa napumzika.

Niliondoka zangu kuelekea kwa Ally na bahati nzuri nilimkuta akiwa nyumbani.

Ally Mpemba "Salama?"

Mimi "Salama kaka"

Baada ya salamu na mazungumzo mafupi, jamaa aliingia ndani ambako alichukua muda mrefu kidogo ndipo akawa ametoka.

Ally Mpemba "Pika chakula ule master, hapa ni kama kwako wala usione taabu!"

Mimi "Kaka usijali niko vizuri"

Ally Mpemba "Ulikula muda gani?"

Mimi "Nimekula muda si mrefu!"

Ally Mpemba "Sawa kama ndivyo"

Aliendelea "Mimi nimekuita weye kwasababu hapo awali nilikueleza ya kwamba nina safari ya kwenda Oman, hivyo nikakuomba unisitiri master!"

Mimi "Sawa kaka"

Ally Mpemba "Kuna jambo nahitaji nikwambie na nakuomba Union unionyeshe uaminifu wako kama nilivyokuamini"

Mimi "Kaka ina maana huniamini tu!"

Ally Mpemba "Mimi nakuamini tangu siku ya kwanza ila nadhani unakumbuka nilikutahadharisha ya kwamba kuna mambo ukiyapayuka kwa watu wengine utakachokutana nacho basi utajua mwenyewe!"

Aliendelea "Ndugu zangu siwathamini kama ninavyokuthamini weye, hivyo thamani ninayokupatia ni kubwa mno"

Aliendelea "Hivyo mimi naondoka na itanichukua takribani mwezi mmoja huko, nakuomba usimamie shughuli zangu hasa ile niliyokukabidhi huko kwengine Farah atasimamia!"

Mimi "Sawa kaka nimekuelewa!"

Ally Mpemba "Vipi mambo yako lakini yanakwenda?"

Mimi "Yanakwenda kaka"

Ally Mpemba "Sawa jitahidi ufanye vema kama ulivyoambiwa na nakuhakikishia wewe ukiwa mwaminifu hakika utakuwa mkubwa hapa Bara kote na hata huko pwani hakuna atakaye kugusa kwa utajiri!"

Niliendelea kumsikiliza Ally Mpemba namna alivyonitia moyo kuhusu ile bangili lakini sikutaka kumwambia kabisa kuhusu biashara zangu zote mbili zilivyonipatia hasara ikabidi nikaushe.

Ally Mpemba "Kuna jambo ambalo kabla ya kuondoka naomba ulifahamu maana ni lazima ndipo uweze kufanya maamuzi ya kunisitiri"

Aliendelea "Bila shaka Huyu kiumbe ninayeishi naye hapa kwangu unamfahamu!"

Mimi "Ndiyo kaka namfahamu"

Ally Mpemba "Sasa nadhani unaelewa huwa nisipokuwepo nakuomba unisaidie kumwandalia chakula"

Mimi "Ndiyo kaka"

Ally Mpemba "Naomba leo nikueleze ukweli na usije kujaribu kumueleza mtu, mimi na wewe tumekuwa wamoja na siri yako ni yangu na naomba siri yangu iwe yako, huwezi kufanikiwa kama hutaweza kutunza jambo!"

Aliendelea "Huyo unayemuona hapa she's my blood sister na ndiye mwanamke ninayempenda kuliko wanawake wote duniani, jina lake si Maya kama unavyodhani, jina lake ni Zahra, hakuna mtu yeyote anayejua Zahra yuko hapa ila wewe, hivyo nakuomba uwe makini na siri hii na nakuomba sana!"

Kiukweli Ally Mpemba alionyesha hali fulani ya huruma na upole baada ya kumuongelea Maya, nilikuwa nikimuangalia Ally Mpemba alionyesha usoni ni mtu wa huruma sana lakini kiuhalisia hakuwa kama ulivyomdhania.

Ally Mpemba "Nikitoka Oman nitakuja kukueleza vizuri ila nachotaka ujifunze na unisitiri!"

Aliendelea "Oman sina mke kama nilivyokwambia hapo awali ila kuna jambo kubwa ambalo na wewe utalifanya siku moja, nikirudi nitakujuza ila kwasasa nakuomba unisitiri!"

Kiukweli hali haikuwa rahisi kama nilivyodhani ila kwakuwa nilikuwa tayari nishaingia kwenye mfumo wa Ally Mpemba sikuwa na jinsi ilibidi nitekeleze na kufanya nilichoambiwa ili kuendelea kujipatia pesa.

Ally Mpemba "Nitakapoondoka nakuomba kila ijumaa uwe unalala kwenye chumba changu hicho!"

Mimi " Sawa kaka nimekuelewa"

Ally Mpemba "Naomba usiwe unashituka kwasababu Zahra atakuwa anakuja mnalala naye na atakachokuwa anataka umfanyie naomba umfanyie usiogope!"

Mimi "Hawezi kuniletea fujo kaka?"
Ally Mpemba "Hawezi, yeye akishakula huwa hana shida, hakikisha kila Ijumaa haufungi mlango wa chumba changu, yeye atakuwa anaingia na mnalala nae kisha akitaka chochote mpatie"

Aliendelea "Bila shaka master wewe ni rijali na kama huwezi kabisa basi mimi kuna dawa nitakupatia utakuwa unakunywa ili uweze kuwa imara kitandani!"

Mimi "Hapana kaka wala usijali niko Imara sana!"

Ally Mpemba "Sawa nitashukuru sana kama umeamua kunisitiri!"

Mimi "Kaka asije akajua mimi siyo wewe akaniletea vurugu!"

Ally Mpemba "Hapana hawezi kufanya hivyo, akishaingia chumbani atalala kitandani na wewe nakuomba usipoteze muda wala usione huruma, mshughulikie kikweli kweli, ikifika asubuhi ataamka mwenyewe ataondoka chumbani kwake!"

Mimi "Sawa kaka nimekuelewa!"

Ally Mpemba "Japo anayo harufu ila nakuomba usionyeshe hali ya kujuta maana hiyo harufu ndiyo pesa yenyewe!"

Aliendelea "Ukifanya vema utapata zaidi na utakuwa mkubwa sana"

Mimi "Sawa kaka nimekuelewa kabisa na sitokuangusha"

Ally Mpemba "Usije kuruhusu mtu yeyote kuingia humu ndani zaidi yako!"

Mimi "Sawa"

Ally Mpemba "Sasa jiandae kesho twende pale TRA ukachukue TIN, kuna jamaa pale nishampa hela nitamkabidhi kwako akufanyie mchakato wa leseni ya gari!"

Basi baada ya yale mazungumzo Ally Mpemba alinikabidhi laki 5 kisha akaniambia kesho asubuhi mida ya 2 tuonane ili tuelekee TRA kwa ajili ya ishu ya leseni. Kiukweli nilibaki kushangaa namna Ally Mpemba alivyokuwa na ujasiri wa kulala na dada yake kitanda kimoja na kumuingilia kimwili. Haikuwa kazi ndogo ila niliamua kupiga moyo konde kwasababu nilikuwa ninataka pesa na mimi niliamua kuwa na roho ngumu.

Baada ya siku tatu kufatilia masuala ya leseni, namshukuru Mungu nilijipatia leseni yangu ya kwanza kabisa kwa ajili ya uendeshaji wa gari. Nilipopata leseni Ally Mpemba alinipatia ile gari yake iliyokuwa mpya aina ya Aud A4, kiukweli nilipata kiburi sana kwa kujiona mimi ndiye mimi, sasa kabla Ally hajaondoka kuelekea Oman alinipatia maelekezo namna ya kuimiliki ile gari.

Ally Mpemba "Master nakuomba tu kwenye hii gari mpya ninayokukabidhi ukiamua kuwabeba marafiki zako basi wakae viti vya nyuma,hii siti ya mbele asije akaikalia mtu yeyote labda kama akitokea ndugu yangu,tafadhali sana nakuomba!"

Mimi "Ndugu zako siwafahamu kaka zaidi ya mama yako mdogo pamoja na Farah"

Ally Mpemba "Hao ndiyo ninaomaanisha, kama Farah akikuona na akihitaji lift usiache kumbeba na asikae nyuma bali akae kiti cha mbele, wengine wote usithubutu kuwabeba mbele"

Mimi "Nimekuelewa kaka nitakuwa muangalifu!"

Ally Mpemba "Sawa mimi nadhani Alhamisi ijayo naondoka, hakikisha Jumatano utakuja kulala hapa ili nikiwa naondoka kuna pesa nikukabidhi pia nikukabidhi na funguo"

Mimi "Utachukua muda mrefu huko?"

Ally Mpemba "Haitapungua mwezi!"

Mimi "Sawa kaka"

Baada ya kuniambia niwe muangalifu na ile siti ya mbele nilivuta picha lakini sikupata majibu, lakini nikakumbuka mara zote nimekuwa nikimuona na ile range akiwa amebeba mtu basi huishia kukaa nyuma na siti ya mbele hukaa bila mtu na mimi pia mara zote nimekuwa nikipanda ile Range ndivyo ilivyokuwa!.

Kweli, baada ya siku kufika Ally Mpemba aliondoka akawa amenikabidhi funguo za nyumba yake pamoja na kiasi cha shilingi milioni 3 na akawa ameniambia amempatia Farah maelekezo endapo zikiisha nimuone atanipatia nyingine, pesa aliyonipatia ilikuwa ya matumizi ya kawaida ya kununulia vyakula vya Maya pamoja na matumizi yangu. Nilifurahi sana maana niliona kila kitu sasa kipo mikononi mwangu na nilipanga kiukweli marafiki na ndugu wanitambue mimi ni nani kupitia lile Audi A4.

Baada ya Ally Mpemba Kuondoka hiyo Alhamisi, ilipofika Ijumaa kama kawaida nilienda zangu kazini pale Kkoo kusajili line za simu, ilipofika mida ya saa 10 jioni nilimuaga Farah nikamwambia nitawahi kufunga kuna mahali nawahi.

Farah "Mbona mapema leo!"

Mimi "Kuna mahali nawahi Aunt!"

Farah "Sawa, si unarudi lakini au ndiyo hadi kesho!"

Mimi "Hiyo hadi kesho dada"

Niliondoka zangu nikaenda kununua vyakula vya maya kama kawaida kisha nikaelekea nyumbani kwa Ally Mpemba, nilipofika kama kawaida nilichukua kitambaa kile cheupe nikatandika pale mezani kisha nikaweka vile vyakula, baada ya kuweka vile vyakula nilifunga mlango kisha nikawasha mchuma nikatoka zangu kuelekea kupata chakula ili niwahi kurudi kufungua kile chumba cha Maya.

Nilipomaliza nilirudi mdogo mdogo na ile gari huku nikiendesha kwa madaha kama yangu vile, ilipofika mida ya saa 1 usiku niliwasha taa kisha nikawa nimetoka zangu nje, kiukweli sikutaka kabisa kumuangalia Maya, nilichoamua ni kwenda kuzurura na ikifika mida ya 3 usiku nirudi kulala. Kweli, niliporudi nyumbani kwa Ally Mpemba kama kawaida niliingia chumbani kwake nikawasha taa na sikufunga mlango, kile chumba kilikuwa ni kizuri na kisafi kupita mfano, sikutaka kabisa kuzima taa, niliingia bafuni kuoga kisha nikarudi kujitupa kitandani kulala huku nikiendelea kumsubiri Zahra(Maya)niliyeambiwa na Ally ya kwamba nikiacha chumba wazi ataingia mwenyewe.

Kweli, haikupita hata nusu saa nilimuona Zahra akiingia chumbani akiwa uchi kama ambavyo siku zote huwa.




.......................................................................................





Utajiri wa rafiki yangu ulivyofanya nikamuamini Shetani - 19.



Nilijifanya nimepitiwa na usingizi huku nikiendelea kumtizama Zahra kwa kuibia; baada ya kufika karibu na kitanda alipanda kitandani huku akiwa uchi kama alivyozaliwa!. Sikutaka kabisa kupoteza muda maana Ally Mpemba aliniambia akisha panda kitandani kazi yangu ni kumshughulikia kisawasawa!.

Niliamka taratibu nikavua boxa ambayo nilikuwa nimevaa na singlendi kisha nikarudi kitandani, kiukweli sikuelewa nitaanza vipi kusimamisha uume kwasababu Zahra alikuwa na harufu kali ambayo ilisababishwa na yeye kutokuoga muda mrefu huku sehemu zake za siri zikiwa zimefunikwa na nywele(mavuzi)za kutosha!, nilisogeza mkono nikamshika ili nione kama anaweza kuwa mkali lakini nilipomshika aliendelea kuwa kimya, niliendelea kumshika huku nikimtizama yule mwanamke na kujikuta namvutia picha ya ngono kwa haraka ndipo uume ukasimama kwa haraka kama nyoka aina ya koboko aliyeona hatari na kujiandaa kuikabili, kiukweli baada ya uume kusimama nilimsogelea na kuinyanyua miguu yake kisha nikamchomekea uume taratibu na bila kizuizi ulizama wote nikaanza kumkimbiza mchakamchaka bila huruma!.

Baada ya kumzamishia fimbo ya mnyonge isiyokuwa na huruma hata kidogo, ile harufu kiukweli ni kama nilianza kuizoea huku akili yangu ikimezwa na tamaa ambayo ilifanya nikamuona Zahra(Maya) kama mwanamke wa kawaida wa kiarabu asiyekuwa na tatizo lolote. Hali haikuwa nzuri ni vile tu nilikuwa nina tamaa ya pesa ndiyo ilipelekea mimi kufanya vile.

Niliendelea kumkung'uta Zahra kwa hasira kana kwamba alikuwa ni mwanamke ambaye nimewahi kumtumia nauli akala akashindwa kutokea sasa alipokuja nilipanga nimuonyeshe namna ambavyo watu tuliozoea kula ugali wa uwele na mtama tulivyokuwa na hasira dhidi ya wanawake wala nauli na wenye viherehere wasemao "Tuma na ya kutolea".

Baada ya kufika mlima Kilimanjaro nilitaka kushuka ili angalau nipumue kumbe haikuwa kama nilivyodhani, nilipotaka kuchomoa uume kwenye uke wa Zahra nilijikuta siwezi kwakuwa alikuwa amening'ang'ania kwa nguvu ambazo hazikuwa za kawaida, sikuwa hata na uwezo wa kushindana nae kwakuwa nguvu alizokuwa nazo hazikuwa za kawaida, nilikuwa mpole huku nikiendelea kusukuma taratibu nikitafuta nguvu za kuuanza upya mchaka mchaka!

Baada ya uume kusimama tena niliendelea kumsukumia nyama hadi aliponiachia huku akionekana kulifurahia tendo, baada ya kuona ameanza kuelewa nilichokuwa namfanya niliamua kumgeuza na kuanza kumshughulikia kwa hasira na uchu mwingi, japokuwa hakuwa na akili kama wanadamu wengine lakini uzuri wa yule mwanamke haukupotea, ulikuwa ukimuangalia uligundua kabla ya kuwa alivyokuwa alikuwaga mwanamke mzuri sana! Kiukweli ile staili ya kumgeuza nyuma niliipenda sana na ndiyo nilieendelea kuifanya hadi asubuhi bila kuchoka kwasababu nilikuwa nikimaliza ninapomshika matako koboko anasimama nakumchomekea kisha kazi inaendelea!.

Kule kwenye kile chumba hakuja kulala bali alifata mbolo na mimi sikuwa na hiyana nilimpatia alichokifata.

Ilipofika asubuhi mida ya saa 12 alinyanyuka mwenyewe akaondoka kuelekea chumbani kwake alikokuwa akikaa, mimi niliamka nikatoka kwenda kukifunga chumba chake kisha nikaingia bafuni kuoga. Nilipotoka kuoga nilitoa lile shuka nililolalia na Zahra nikalipeleka kulifua kisha nikaweka shuka jingine.

Baada ya kumaliza shughuli za hapo nyumbanj kwa Ally Mpemba niliamua kwenda zangu Kkoo kuendelea na kazi yangu ya usajili wa line za simu. Kwakuwa ilikuwa Jumamosi, nilipanga nikafanye kazi masaa machache kisha niondoke zangu kuelekea nyumbani kubadili nguo na kujiandaa kwa mambo mengine, siku hiyo sikupita kabisa pale ofisini Buguruni, sasa nilipofika Kkoo nilielekea mahali ambapo nilikuwa natunza vitu vyangu, baada ya kuvichukua niliondoka kueleka sehemu ya kazi, nilipofika muda huo lile duka la Ally Mpemba ambalo mara nyingi alikuwa akiuza dada yake aitwaye Farah lilikuwa bado halijafunguliwa, haikuwa kawaida kukuta lile duka muda huo wa saa 3 kuelekea saa 4 ukute likiwa limefungwa, mimi kama kawaida nilifungua biashara yangu pale na nikaanza kupiga kazi!.

Ilipofika mida ya saa 5 asubuhi nikiwa napiga kazi, sasa nikiwa sina hili wala lile kutokana na ubize, mara ghafla nilisikia sauti ya mwanamke ikinisalimu kwa sauti ambayo haikuwa ya kawaida, nilinyanyua shingo na kumtazama yule mwanamke kumbe alikuwa ni Aunt Farah, dada yake na Ally Mpemba, yeye mara zote alikuwaga akivaa Nicab(Vazi nadhifu lililofunika sura yake).

Mimi "Ooh Aunt Farah, umenishitua!"

Farah "Umeshituka na nini?"

Mimi "Sijui hata nilikuwa nawaza nini!"

Farah "Haya bana, umeamkaje lakini?"

Mimi "Niko poa kabisa, sijui za huko utokako!"

Farah "salama"

Aliendelea "Nilijua utapumzika leo"

Mimi "Ahaa hamna, kama sina tatizo tu la kuniweka nyumbani siwezi kupumzika maana hii kazi hainaga wikiendi!"

Sasa wakati naongea nae yeye alikuwa akiendelea kufungua geti la duka lake, kama mtakumbuka hapo awali niliwaambia ya kwamba, nilikuwa nikifanya biashara zangu kando ya lile duka la Ally Mpemba lililokuwa likitazamana na ambayo leo ni stendi ya Mwendokasi(Kituo cha Gerezani).

Mimi "Leo umechelewa sana hadi nikahisi hufungui!"

Farah "Kuna mahala nilikwenda ndiyo maana nilichelewa"

Mimi "ooh sawa!"

Baada ya mazungumzo mafupi niliendelea na kazi yangu kama kawaida huku wateja wakija mmoja mmoja, kiukweli yule dada sikuwahi kumuona usoni namna alivyo na namna alivyokuwa akifanana! Nilitamani sana siku moja nimuone ili niweze kumfananisha na yule mwanamke aliyetolewa kafara na Ally Mpemba ambaye kwa mujibu wake alikuwa dada yake (Zahra/Maya).

Nilitamani kumuona na kupata uthibitisho kama wanafanana kwa maana walikuwa ni ndugu.

Ilipofika mida ya saa 7 mchana mimi ilibidi nichukue vitu vyangu na kuanza kuvikusanya ili nivirudishe nilikokuwa navihifadhi niweze kwenda nyumbani, kiukweli kwa wakati huo hata utendaji wangu wa kazi haukuwa mzuri kama mwanzo kwakuwa nilikuwa nina pesa ya kutosha hivyo ile kazi nilikuwa ninaifanya angalau nisiweze kukaa tu nyumbani bure. Mara zote ambapo huwa nikiondoka nilikuwaga namuaga Aunt Farah maana nilimzoea kama vile ndugu yangu, sasa kuna jambo ambalo baada ya kumuaga ni kama lilinishitua.

Mimi "Sister mi nakuacha mara moja tutaonana Jumatatu!"

Farah "Mbona mapema sana leo?"

Mimi "Nimechoka tu nahitaji nikapumzike!"

Farah "Sawa mwanaume wa bara mwenye nguvu zake"

Mimi niliondoka zangu bila kumzingatia maana mara zote amekuwa akinitania kwa majina mbalimbali hivyo sikujali.

Nilipofika nyumbani ile nimeingia ndani ya chumba changu cha kulala nilishituka sana baada ya kutazama kitandani na kukuta ile shuka ambayo niliitoa pale kitandani kwa Ally Mpemba baada ya kumkung'uta Maya fimbo za kutosha, kiukweli nilishangaa sana ni nani alikuwa ameifikisha ile shuka pale nyumbani kwasababu baada ya mziki ule wa usiku kucha niliamua kuibadili ili kuweka shuka safi. Nilisogea hadi kitandani nikalitoa lile shuka, cha ajabu hata nililokuwa nimelitandika hapo awali lilikuwa limetolewa na kuwekwa kwenye nguo chafu kana kwamba kuna mtu mle ndani ndiye alifanya vile!.

Baada ya kulitoa nilitandika shuka nyingine safi, nilielekea bafuni kuoga upya ili nirudi nibadili nguo nikiwa na lengo la kuondoka kwenda kuchukua mchuma(Audi )ili nielekee ununio kwa Anko,sasa ile nimetoka bafuni kupiga maji, nilikuta tena lile shuka likiwa limetandikwa kama mwanzo, kiukweli nilitoka mle chumbani kwa haraka nikiwa mwenye hofu kuu, nilisimama pale sebuleni kwa muda nikiwa niNatafakari ni kitu gani kinaendelea, baada ya dakika kadhaa nilirudi chumbani kwa ujasiri kisha nikavaa nguo na kuondoka, lengo ilikuwa ni kwenda hadi Kkoo kwa Aunt Farah ikiwezekana amtafute Ally ili niweze kuzungumza nae maana ile hali sikuielewa kabisa!.

Baada ya kufika Kkoo cha ajabu nikakuta Aunt Farah naye kafunga duka na sikufahamu alipoelekea!. Niliondoka hadi kwa Ally Mpemba Magomeni, nilipofika nilifungua nyumba na kuingia ndani moja kwa moja hadi kwenye chumba alichokuwa akilala jamaa, nilipofungua mlango na kuingia ndani nilikuta tena lile shuka ambalo nimeliacha nyumbani kwangu likiwa limetandikwa kitandani mara hii tena likiwa limetandikwa kitandani kwa Ally Mpemba, kumbuka hii shuka ni ile ambayo niliibadili baada ya kumkung'uta Maya stiki za kutosha ule usiku. Kiukweli nilibaki nikishangaa sana, sasa nilichoamua ni kutoka nje na kuchukua ile gari na kuondoka zangu.

Niliondoka kuelekea Ununio kwa Anko Nico kuwasalimu lakini lengo langu lilikuwa ni lile lile la kuwaringishia ili waone yale waliyokuwa wakizungumza kuhusu mimi hawakunitendea haki. Nilipofika nyumbani kwa Anko nilipiga honi bahati nzuri geti likafunguliwa na kijana mmoja ambaye sikumfahamu, niliingiza gari hadi ndani kisha nikateremka.

Mimi " Mambo vipi "

Jamaa "Safi "

Mimi "kwema?"

Jamaa "Kwema kabisa"

Mimi "Humu ndani wapo kweli?"

Jamaa "Yupo dada Rebecca nadhani"

Niliingia ndani hadi sebuleni kisha nikaa kwenye sofa, kuna mtu bila shaka alikuwa akitazama filamu za kifilipino pale sebuleni lakini baada ya kusikia naingia ndani aliondoka akaelekea chumbani, ile picha niliisoma maana nilikuta luninga ikiwa imewashwa na kwa muonekano tu niligundua kulikuwa na mtu amekimbilia chumbani baada ya kusikia naingia ndani. Baada ya dakika 10 alitoka binti wa Anko Nico ambaye ni mkubwa aliyeitwa Rebecca.

Rebecca "Ooh binamu"

Aliendelea "Karibu!"

Mimi "Ahsante, za hapa"

Rebecca "Nzuri, za utokako!"

Mimi "Huko tuko poa"

Mimi "Mbona nyumba imepoa sana, uko mwenyewe nini!"

Rebecca "Si unajua tena wengine wameenda kanisani!"

Mimi "Oooh aisee hata sikujua "

Mimi " Wanasali mbali?"

Rebecca "Eeeh ni mbali kidogo maana kuna makambi ndiyo wako huko!"

Mimi "Sawa, mimi nilipita kuwasalimu, nadhani utanisalimia Anko na Shangazi wakirudi"

Rebecca "Haukai kuwasubiri?"

Mimi "Nitarudi hata wikiendi ijayo kuwasalimu"

Rebecca "Kaa kidogo maana napasha chakula ule ndiyo uende!"

Mimi "Ok hakuna tatizo!"

Kiukweli nilishangaa sana namna binti wa Anko alivyobadilika kwa muda mchache kwasababu wakati ule nikiwa kwao alikuwa ni mmoja wa watoto wa Anko ambao hawakuwaga na stori na mimi kabisa, nilidhani labda huenda umri ukawa umembadilisha kiakili. Baada ya muda aliniketea msosi nikaanza kuukung'uta kama kawaida kisha nilipomaliza nilimuaga na kumuachia kiasi cha shilingi laki moja kama matumizi yake na kuondoka, alinishangaa sana na kunisindikiza nje kwa bashasha kana kwamba nilimpa milioni moja, mimi lengo langu ni autazame ule mchuma na wazazi wake pamoja na ndugu zake watakaporudi basi awape stori.

Mimi "Mi naenda dada"

Rebecca "Haya binamu uwasalimie huko"

Aliendelea kunisindikiza kwa macho hadi nilipoingia kwenye chombo na kuondoka zangu.

Nilipotoka kwa Anko niliondoka kurudi Gongo la mboto, sasa nilipofika pale Mombasa kuna bar moja niliingia nikapaki gari kisha nikaagiza bia aina ya safari na kuanza kutandika mdogo mdogo, wakati nikiwa ndiyo nimeikamata bia ya pili kuna mtu alinipigia simu, nilipoitazama ile namba ilikuwa ngeni kwenye simu yangu.

Mimi "Halloo"

Yeye "Hello"

Mimi "Nambie"

Yeye "Poa, uko wapi?"

Mimi "Nani?"

Yeye "Farah hapa naongea"

Mimi "Farah!.....Aunt Farah?"

Yeye "Ndiyo"

Mimi "Ooh samahani sana sister hii namba huwaga sina"

Farah "Usijali, uko wapi?"

Mimi "Nipo hapa Mombasa!"

Farah "Ok mimi nipo hapa kwako"

Mimi "Kwangu?"

Farah " Ndiyo!"

Mimi "Wewe si ni Aunt Farah wa Kkoo?"

Farah "Ndiye mimi"

Mimi "Kwangu umepajuaje dada?"

Farah "Nimekuja nikiuliza hadi nimefika"

Kiukweli baada ya maelezo ya Farah nilishituka sana na ile bia nikaanza kuiona chungu, nilishindwa kuelewa alifikaje nyumbani kwangu, na huenda ningekuwa mtu maarufu kiasi kwamba ukiniulizia usingenikosa lakini mimi nilikuwa mtu wa kawaida sana na alivyoniambia eti amefika kwangu kwa kuulizia kiukweli alinichanganya.

Farah "Mbona unashangaa?"

Mimi "Hamna dada!"

Farah "Ally Alitaka kuzungumza nawe ndiyo maana niko hapa"

Mimi "Sawa dada nakuja "

Kilichoniacha hoi ni hiyo statement ya kwamba Ally Mpemba alitaka kuzungumza na mimi, mara zote Ally Akiwaga nje alikuwa akinipigia simu moja kwa moja, ila mimi ndiye nilikuwaga nikitaka kumpigia moja kwa moja simu haitoki. Niliondoka upesi kuelekea nyumbani ili nikaonane na Farah.

Nilipofika pale nyumbani ile gari niliipaki nje ya ile nyumba kwakuwa hakukuwa na nafasi ya kuingiza gari ndani, sasa nilipofika ndani sikumuona Farah ikabidi nimpigie simu.

Mimi "Dada nishafika uko wapi?"

Farah "Nilitoka kidogo nipo hapa dukani nakuja"

Nilifungua mlango nikaingia zangu ndani kuweka mazingira sawa kisha nikatoka nje kumsubiri, sasa baada ya muda aliingia mwanamke mmoja wa kiarabu(Kipemba)aliyekuwa akifanana sana na Zahra/Maya kama mapacha, nilibaki kumtizama kama mtu niliyepigwa na bumbuwazi.

Tangu nimfahamu Farah sikuwahi kumuona uso wake kwasababu mara zote alivaa nicab. Alipokuja kwangu alikuwa amejitanda hijab tu huku uso wake ukiwa wazi kabisa na chini akiwa amevaa suruali nyepesi ya kitambaa pamoja na raba ya converse, kiukweli baada tu ya kumuona namna alivyokuwa akifanana na Maya nilimtambua. Kilichonishangaza zaidi hadi umbo na tembea yake alikuwa ni Maya mtupu, hali ya uwoga ikaanza kuniingia ghafla lakini sikutaka kuonyesha ikabidi nijikaze.

Nilijiuliza maswali mengi sana, ni yeye tu ndiye alifanana na Maya au hadi ndugu wengine ambao sikuwaona nao walifanana na Maya? Na Mbona Ally Mpemba alikuwa hafanani sana na Maya kama ilivyo kwake?

Mimi "Dada Farah karibu"

Farah "Ahsante kijana wa bara mwenye balaa"

Mimi "Karibu ndani!"

Farah "Hapana, ndani siingii!"

Aliendelea "Ngoja nimpigie Ally uongee nae alitaka kuzungumza nawe!"

Mimi "Leo unamtoko nini!"

Farah "Kwanini?"

Mimi "Siyo kawaida yako kukuona hivi!"

Farah "mmmh hujanikuta tu huenda!"

Mimi "Nilikuja dukani mida fulani nikakuta umefunga"

Farah "Kuna mahala inapaswa niwahi hebu zungumza na Ally"

Baada ya kuzungumza na Ally Mpemba alinipatia maelekezo ya kwamba aende kule kwake akachukue ile gari yake(Range Rover) kisha kulikuwa na hela kiasi cha milioni 2 anipatie. Nilimtaka pia Ally Mpemba baadae anipigie simu yangu kuna mambo muhimu nizungumze nae akanianbia usiku angenipigia.

Basi baada ya mazungumzo yale tuliondoka na Farah kuelekea kwenye Audi ili niondoke nimfungulie achukue gari kama jamaa alivyokuwa amenipatia maelekezo, sasa ile Farah anapanda kwenye gari kuna namna aliliitusha hijab yake ambayo ilionekana kumbana,kiukweli nilipomtazama vizuri nilishituka sana baada ya kuona alikuwa na mchoro mkononi kama ambao Maya alikuwa nao kwenye mkono wake wa kuume!



.......................................................................................





Utajiri wa rafiki yangu ulivyofanya nikamuamini Shetani - 20.


Nilikuwa nina maswali kichwani mwangu zaidi ya elfu moja na ambayo hayakuwa na majibu. Iliwezekana vipi mwanamke ambaye hakuwahi kabisa kufika kwangu hata mara moja leo aje tena kwa hoja ya kwamba ameelekezwa kwa kuulizia ulizia? Je, alimuuliza nani huyo ambaye ananifahamu pale mwisho wa lami? Pili, inakuwaje Farah afanane kiasi kile na Zahra/Maya? Sawa yawezekana wangefanana kama ndugu wa tumbo moja, lakini je hadi mchoro mkononi? Kiukweli kwangu ilikuwa ni kama sinema ambayo sikuielewa hata kidogo. Kwakuwa Ally Mpemba amewahi kuniambia Farah ni dada yake, nilidhani huenda Farah na Maya wakawa ni mapacha kwasababu pia Ally aliniambia Maya/Zahra alikuwa ni dada yake pia.

Baada ya kuingia kwenye gari niliiwasha na kuanza kuiondoa taratibu kuelekea Magomeni. Sikutaka kabisa kukaa kimya, niliona niendelee kumdodosa Aunt Farah ili niweze kuufahamu ukweli!.

Mimi "Kwahiyo dada umekuja unaulizia?"

Farah "Mbona unakuwa na mashaka sana leo? Kwanini?"

Mimi "Hapana dada sina mashaka ila nauliza tu!"

Farah "Wewe hukuwahi kumwambia Ally unakaa Gongo la mboto mwisho wa lami?"

Mimi "Nimewahi kumwambia lakini kaka Ally pia hajawahi kufika kwangu".

Farah "Nilipofika hapo mwisho wa lami nimeulizia nikaelekezwa"

Mimi "ooh sawa"

Kiukweli sikutaka kumbishia maana niliona huenda tungekwazana kwasababu sababu alizokuwa akinipa zilikuwa haziniingi akilini hata kidogo, nilijua kabisa alikuwa akinidanganya, pale mwisho wa lami mahali nilipokuwa nikikaa mimi kulikuwaga hakuna watu ninaofahamiana nao sana huenda jamaa mwenye duka pale nje, pia kwa mazingira yale isingekuwa rahisi mtu kunifahamu kwasababu nilikuwaga si mtu wa kujichanganya na ndiyo maana nikasema huenda ningekuwa maarufu pale mtaani hapo angenishawishi kwa ule uongo wake laki kiukweli sikukubaliana naye hata kidogo. Niliamua kukausha tu ili mambo mengine yaendelee maana niliona nikiendelea kulifuatilia hilo suala sana kiundani huenda ningeibua mambo mengine.

Mimi "Dada nikuulize swali?"

Farah "Karibu"

Mimi "Kwenu mmezaliwa wawili tu na Kaka Ally?"

Farah "Kwanini?"

Mimi "Nimeuliza tu maana mara zote nawaona nyie tu"

Farah "Mmh! hapana tupo wengi"

Aliendelea "Wengine hawakai hapa Bongo"

Mimi "Kwahiyo kwa hapa Bongo upo wewe na kaka Ally tu!"

Farah "Hapana wapo wengine!"

Mimi "Ooh sawa!"

Niliamua kukaa kimya sikutaka kabisa kuendelea kuuliza maswali mengi kwakuwa hata yeye pia niliona ananijibu kishingo upande hivyo nikaona nisiingie ndani sana ijapokuwa maswali nilikuwa nayo mengi sana. Sasa kichwani mwangu nilipanga ya kwamba, usiku wa siku hiyo nikamtazame vizuri Maya atakapokuwa akila chakula chake pale sebuleni ili kujiridhisha maana kiukweli walikuwa wakifanana kila kitu na Farah.

Baada ya kufika Magomeni kwenye nyumba ya Ally Mpemba, nilifungua geti na ile gari kuiingiza hadi ndani kwenye sehemu ya kuegeshea. Nilishuka kwenye gari nikaenda kumchukulia ndani funguo ya gari dada Farah ambaye wakati huo alikuwa nje akinisubiri. Baada ya kumpatia ule ufunguo akawa amechukua mkoba wake akatoa shilingi milioni 2 akanipatia.

Farah "Hela hizi hapa"

Mimi "Nashukuru dada"

Hakuchukua muda akaingia kwenye ile Range. Nilisogea nikamfungulia geti akawa ametoka na kuondoka. Sikutaka kabisa kupoteza muda hapo nyumbani niliondoka zangu hadi sokoni kwenda kununua mahitaji ya chakula cha Maya, niliwasha gari nikawa nimetoka zangu kuelekea soko la Ilala, kiukweli wakati huo nilikuwa nimenawiri sana na nilikuwa nanyuka pamba za ukweli, ulevi wangu mkubwa ulikuwa ni kupendeza kwa kuvaa vizuri.

Sasa kuna mahali nilifika nikapaki ile gari kisha nikashuka kuelekea sokoni kununua mahitaji, wakati nikiwa nanunua mahitaji kwa mama mmoja, ghafla nikasikia sauti ya mwanamke mmoja ambaye ilinifanya nikageuka kumtazama, hadi leo sijajua ni kitu gani kilitokea ila huwa najiuliza maswali mengi sana.

Huu ulimwengu hauko kama mnavyodhani ndugu zangu, kuna muda unaweza kuwaona watu wanapendeza na kuishi maisha bora ukadhani ni rahisi lakini si hivyo! Mimi baada ya kupitia mambo hayo machache ndiyo maana leo napambana kwa nguvu zangu kufa na kupona ili kujipatia riziki, sasa kuna watu nikiwaambia mimi ni naendesha bodaboda huwa hawaamini wanadhani natania, japokuwa pia najaribu kuwekeza kwenye kilimo lakini bodaboda hiyo hiyo ndiyo inanipatia pesa ya uwekezaji huo!. Niliamua kupambana na maisha yangu ya udundulizaji kwasababu hakuna maisha ambayo sijapitia, kila baya na jema nishaona, hivyo niliamua kutulia kujipambania, huko mbele mtaelewa vizuri ni kwanini leo naendesha bodaboda.

Sauti ya kike "Mama Eliya nikuletee?"

Mama Eliya "Leo sina hela mwaya!"

Huyo mama Eliya alikuwa ni mama ambaye nilikuwa nimesimama mbele yake nikuchukua kabeji, sasa wakati akiwa kwenye pilika pilika za kunirudishia chenji ndiyo nikawa nimesikia hiyo sauti ikimwambia hivyo, baada ya kumtazama yule mwanamke aliyemuita mama Eliya kiukweli nilibaki nikimtizama. Kiukweli baada ya yule mwanamke kumuita huyo mama niliyekuwa nikinunua mboga kwake nilijikuta tu nageuka kumtazama ni nani na nilipogeuka nilijikuta namtamani baada ya kumtazama, hakuwa mwanamke mbaya, alikuwa ni mwanamke mmoja wa kawaida ila alikuwa na umbo zuri sana.

Mimi "Anauza nini huyo?"

Mama Eliya "Anauza Juisi"

Mimi "Ni nzuri?"

Mama Eliya "Juisi yake huwa tamu kweli sema leo tu ndiyo hali ngumu ila ningechukua"

Mimi "Anauza bei gani?"

Mama Eliya "Anapima kwenye glasi shingi elfu moja"

Mimi "Mwambie akupe"

Mama Eliya "Ahsante mwanangu"

Aliendelea "Nitakunywa baadae "

Mimi "Mwambie aje akupe kabisa maana nyie huwa wajanja, nitakupa hela utaisunda huta nunua,nataka na yeye umuungishe kama mimi nilivyokuungisha"

Baada ya kumwambia hivyo yule mama muuzaji alianza kucheka sana. Nia yangu ilikuwa ni kwamba amuite yule mwanamke asogee kwa karibu nipate kumtazama vizuri maana alikuwa bize na juisi yake na kwangu isingekuwa rahisi kumsimamisha pale sokoni na kuanza kuzungumza nae kwasababu mara zote nimekuwa na aibu kusimama na mwanamke machoni pa watu.

Mama Eliya "Wala usijali baba namuungisha"

Aliendelea "Wewe Ray......Raaaaaay niletee juisi nimepewa ofa"

Baada ya kuita yule mwanamke alijongea taratibu hadi pale nilipokuwa nimesimama kwa mama Eliya.

Mama Eliya "Niwekee glasi moja nimepewa ofa na mwanangu"

Mimi "Mama wewe kunywa hadi utosheke sijakupa ofa yenye kikomo"

Mama Eliya "Mmh nashukuru baba"

Nilifahamu kabisa mama Eliya anaweza kuwa anauhitaji na pesa ndiyo maana ile ofa ni kama alitamani asinywe ili ile hela achukue, sasa mimi nilipanga kumpatia kiasi kidogo kitakachomsaidia.

Mimi "Jusi yako unatengeneza na nini?"

Muuza juisi "Ni mchanganyiko wa Embe, pasheni na parachichi"

Mimi "Ok"

Muuza juisi "Nichangie basi kaka"

Mimi "Haina shida wala usijali, nimepaki gari pale ng'ambo naomba twende ili ikiwezekana nitafute chombo uniwekee"

Muuza juisi "Ninazo chupa kaka"

Mimi "Mbona hapa sizioni?"

Muuza juisi "Kuna mahali nimeziweka nakimbilia mara moja"

Mimi "Ni safi?"

Muuza juisi "Ni safi kaka huwa naziosha na maji moto"

Aliendelea "Au kama hutoridhika basi unywee hapa kaka"

Mimi "Usijali nitanunua"

Basi baada ya mazungumzo mafupi nilimpatia yule mama noti ya shilingi elfu kumi kama malipo ya juisi na itakayobaki achukue yeye, kiukweli alinishukuru sana na nilimwambia wakati wote nitakapokuwa naenda hapo sokoni kununua bidhaa ningekuwa namtafuta yeye.

Niliondoka nikaongozana na yule dada muuza juisi kuelekea nilikokuwa nimepaki gari, mimi nilikuwa mbele na yeye alikuwa nyuma yangu huku mkononi akiwa ameshika galoni ya juisi na kapu la vikombe.Tulipofika nilifungua gari kisha nikamwambia animinie kwenye glasi ili ninywe kwanza niisikie ladha yake.

Mimi "Ni tamu"

Mimi "Unaitwa nani?"

Muuza juisi "Naitwa Rehema"

Mimi "Unaishi wapi Rehema?"

Yeye "Naishi Ubungo Msewe?"

Mimi "Ubungo Msewe iko maeneo gani?"

Yeye "Pale pale Ubungo ni jirani na chuo kikuu"

Mimi "ooh,duuu mbona kama mbali?"

Yeye "Wala hata siyo mbali"

Mimi "Unaona siyo mbali kwasababu ushazoea"

Mimi "Kwahiyo kila siku unamaliza hiyo galoni?"

Yeye "Inategemea, kuna muda nauza hizi galoni hata tatu na kuna siku hata moja haiishi"

Mimi "Ok"

Mimi "Umeolewa?"

Yeye "Sijaolewa ila nina mtu wangu"

Mimi "Mnaishi wote?"

Yeye "Hapana, mi naishi kwa shangazi na yeye anaishi kwao!"

Mimi "Kwahiyo ndiyo umepanga aje awe mume wako?"

Yeye "Hayo sasa ni maajaliwa ya Mwenyezi Mungu"

Mimi "Kwenu anafahamika?"

Yeye "Anafahamika kwasababu ninaye mtoto wake!"

Mimi "Unaye mtoto wake kivipi?"

Yeye "Nimezaa naye "

Mimi "Mbona sasa mimi nakupenda Rehema"

Yeye "Kunipenda wala siyo dhambi kaka, dhambi ni kumtamani mke wa mtu"

Mimi "Mimi sijakutamani Ray mimi nakupenda"

Yeye "Toka lini mwanaume wa Dar akapenda mwanamke? Wewe sema umenitamani tu ili unipate umalize haja zako unikimbie, nyie wanaume hata sinaga hamu kabisa na nyie!"

Mimi "Hebu tuachane na mambo mengi Ray nipe namba yako ya simu nitakupigia"

Yeye "Simu yangu inasumbua betri nimeiacha nyumbani"

Mimi "Mimi nitakupataje ili tutafute mazingira mazuri tuzungumze"

Yeye "Mimi napatikana tu hapa hapa wewe ukija utamuuliza mama Eliya"

Mimi "Lakini umeelewa nilichokwambia Ray?"

Yeye "Lakini nishakwambia ninaye mtu wangu!"

Mimi "Kwani utamwambia?"

Yeye "Siyo hivyo, kumbuka penzi ni kama kikohozi huwa alijifichi!"

Aliendelea "Halafu unataka kuniambia wewe huna mtu?"

Mimi "Ningekuwa na mtu unadhani ningekusumbua?"

Yeye "Mimi nitajuaje! Nyie wanaume kwani mnaaminikaga?"

Mimi "Kwahiyo hata huyo jamaa yako pia humuamini?"

Yeye "Simuamini ndiyo, kwani anapokaa huko ninakuwa nae?"

Mimi "Siko kama unavyodhani Ray"

Yeye "Sawa, ushamaliza kuniongopea? Mimi nataka niwahi kwenye biashara"

Mimi "Sikuongopei ila amini hivyo"

Yeye "Sawa ukiwa na shida basi utanitafuta napatikana hapa hapa sokoni"

Baada ya mazungumzo yale na yule mwanamke ambaye alionekana na msimamo, nilimpatia noti ya shilingi elfu kumi akawa anataka kunirudishia chenji nikamwambia hiyo nimempatia tu.

Yeye "Ahsante"

Yeye "Ila nimesahau kukuuliza jina lako!"

Mimi "Mimi naitwa Umughaka"

Yeye "Sawa nashukuru kukufahamu Umungaka"

Mimi "Siyo Umungaka,ni Umughaka!"

Yeye "Ahahahaa nisamehe jamani una jina gumu, sijui kama nitaweza kulitamka"

Mimi "Kesho nitakuja kukucheki"

Yeye "Saa ngapi sasa ili niwe maeneo jirani?"

Mimi "Mida kama hii"

Yeye "Sawa, msalimie wifi "

Mimi "Wifi tena!"

Yeye "Utakubali sasa!?"

Aliendelea "Haya basi tutaonana!"

Yule mwanamke aliondoka huku namtazama namna alivyokuwa na nyama za kutosha, kiukweli alikuwa mwanamke fulani wa kawaida ila umbo lake halikuwa la kawaida, mara zote ugonjwa wangu kwa wanawake umekuwa ni uleule wa matako makubwa wastani na hips za kuzugia, mara zote huwa sihangaiki na sura kwasababu si sehemu ya hitaji langu kubwa kwa mwanamke, huwa naangalia vinavyo nihusu na visivyo nihusu naachana navyo.

Nilielewa ni kila mwanamke ukijaribu kumtongoza ni lazima akwambie anaye mtu wake ili kujipa thamani lakini mara zote huwa haiko hivyo, hata Rehema nilifahamu kabisa ili ajipe thamani ni lazima angeniambia anaye mtu ingawa nilipomtazama macho yake ilionekana kabisa anasema uongo.

Niliwasha mchuma nikaondoka zangu kuelekea Magomeni kupeleka zile bidhaa na baada ya kufika kama kawaida niliziweka pale mezani kisha nikafunga mlango nikaondoka zangu, sasa kwakuwa ilikuwa bado mapema, nilirudi hadi pale nilipokuwepo mwanzo kwa ajili ya kuendelea na makamuzi ya bia. Muda uliposogea niliamua kuondoka kuelekea Magomeni ili kuweza kuufungua mlango wa Maya, nilipofika nilipaki lile gari kisha nikaingia ndani nikafungua mlango wa kwenye kile chumba cha Maya kisha nikauacha wazi nikatoka zangu nje.

Kwakuwa nilikuwa nimeshiba, niliingia kwenye ile gari nikafunga mlango nikawa nasubiri mida mida ifike ili niweze kumtazama Maya kwa uzuri ili kujiridhisha. Mpaka wakati huo sikuiona simu ya Ally Mpemba wala nini! Niliendelea kusubiri nikidhani angenipigia kama alivyokuwa ameniahidi lakini haikuwa hivyo.

Ilipofika mida ya saa 3 usiku nilianza kusikia yule kiumbe Maya akitafuna kile chakula chake kwa sauti kama mara zote ambavyo huwa akifanya. Nilifungua mlango wa gari taratibu kisha nikasogea hadi dirishani ambako kungeniwezesha kumtizama vizuri kwakuwa nilikuwa nimewasha taa na kufungua lile pazia. Nilisogea hadi pale dirishani kisha nikaanza kumtizama kwa makini sana, sasa wakati namtizama yeye alikuwa amenipa mgongo, nilijaribu kumuangalia kwa umakini mkubwa sana na kiukweli walifanana kila kitu na Faraha, kuanzia urefu hadi umbo, ile alama ya mkononi nilijaribu kuitazama lakini sikuweza kuiona kwakuwa muda wote mikono alikuwa ameshika chakula chake akiendelea kula, hivyo kufanya nisiweze kuitazama vizuri.

Sasa wakati nikiwa namtazama aligeuka ghafla kama mtu ambaye alihisi kitu akawa anaangaalia pale dirishani huku akiacha kutafuna kwa mshangao, nilisogea pembeni ili asinione, baada ya muda nilipochungulia pale sebuleni sikuweza kumuona tena akawa amendoka. Nilirudi zangu kwenye gari nikiwa najiuliza sana maswali mengi, kumbuka pamoja na mambo yote ikiwemo kulala na Maya lakini ni kiumbe ambaye sikupaswa kumzoea na hakuzoeleka.

Ilipofika mida ya saa 5 usiku nilisikia honi ikipigwa getini na ilikuwa ni honi ya lile gari alilokuwa amechukua Farah, niliondoka nikaenda kumfungulia geti kisha akawa ameingiza gari ndani. Aliposhuka kwenye ile gari akawa ameniambia anahitaji kuingia ndani kwenda kujisaidia.

Mimi "Habari za huko dada"

Farah "Nzuri, ndiyo narejea!"

Aliendelea "Nilidhani huenda nisingekukuta ila nimewasiliana na kaka Ally ameniambia upo"

Aliendelea "Ngoja nijisaidie kidogo nimebanwa"

Nilitaka kumzuia asiingie ndani lakini nilishindwa kumzuia kwasababu nilifahamu kabisa ni ndugu yake na Ally Mpemba pia walitoka kuongea muda si mrefu. Hapo awali Ally Mpemba aliwahi kuniambia sipaswi kabisa kumruhusu mtu yeyote kuingia ndani ya ile nyumba yake hata akiwa ndugu yake, kitu alichoniambia Ally Mpemba ambacho naweza kufanya ni kuruhusu ndugu zake tu kukalia kiti cha mbele kwenye gari aliyokuwa amenipatia kupigia misele lakini mtu mwingine hakuruhusiwa.

Sasa kabla hata sijamwambia chochote, nilishitukia kufungua mlango na kuingia ndani, kitu cha ajabu wakati Maya amemaliza kula nilikuwa bado sijasafisha pale sebuleni na mara zote huwa nasafisha asubuhi, sasa nilitaka kumwambia Farah atumie choo cha nje ili asingiingie ndani ambako kungeleta taharuki, niliingia ndani pale sebuleni lakini sikumuona Farah nikiamini huenda alikuwa ameingia chooni, nilianza kusafisha ile meza na pale chini kwa haraka, kabla hata sijamaliza nilimuona anafungua mlango wa chumba cha Ally na kutoka.

Kilichonishangaza zaidi ni kwamba ule mlango nilikuwa nimeufunga na funguo na funguo mara zote zilikuwa zinakaa kwenye kimeza cha luninga, nikajaribu kuzitazama funguo nikakuta zipo pale kwenye kimeza, sasa nikawa najiuliza ule mlango sikuufunga? Na kama nisingeufunga zile funguo zisingechomoka pale mlangoni! Na kwanini ameingia kwenye chumba cha Ally akashindwa kwenda chooni ambako vyoo vilikuwa vinajitegemea?.

Kiukweli hofu ilianza kuniingia na kwakuwa nilikuwa mtu mzima nilitambua fika yawezekana Farah hakuwa mtu wa kawaida.

Farah "Mimi nakwenda!"

Mimi "Sawa dada nikusindikize?"

Farah "Hapana"

Mimi "Sawa dada usiku mwema tutaonana kesho"

Farah "Panapo majaaliwa"

Baada ya kuondoka Farah kiukweli sikuelewa ile hali.

INAENDElea......
Hivi iliendelea kwel hii na muendelezo wake naupataje
 
Back
Top Bottom