Ndugu huyo wa Roma ambaye hata hivyo alikataa kutaja jina lake, aliliambia gazeti hili kuwa hadi anafikishwa hospitalini hapo, msanii huyo hakuwa katika hali nzuri.
“Huo ndio ukweli ingawa hatujaruhusiwa kushuhudia mahojiano yao, lakini tumeambiwa kapelekwa… kwa kumwangalia ana mikwaruzo, wengine wapo vizuri, lakini Roma kaathirika zaidi, amehojiwa kama shahidi na si mtuhumiwa, polisi ndio wana taarifa zaidi,” alisema.
Hata hivyo, Kamanda Kaganda hakuwa tayari kuzungumza lolote kuhusu tukio hilo zaidi akisema kuwa hadi watakapotoka hospitali.
Wakili wa Roma aliyejitambulisha kwa jina la Jebra Kambole, alisema mteja wake alikuwa anachechemea na ana majeraha mkononi hali iliyomfanya ashindwe kusalimiana naye.
Wakili huyo wakati akisema hayo naye alikuwa hajapata fursa ya kuzungumza naye.
Zaidi alisema Roma na wenzake walianza kuhojiwa saa nane mchana hadi saa moja usiku kabla ya kupelekwa hospitali.
“Hali ya Roma si nzuri, anatetemeka, wenzake wana afadhali kidogo… amehojiwa kama mtu wa kawaida na si muhalifu ili awasaidie polisi katika upelelezi, hadi sasa hakuna shtaka lililofunguliwa dhidi yao, wakimaliza kuangaliwa afya zao wataachiwa huru kwenda nyumbani,” alisema.
Wakati wakili huyo akisema hayo, ofisa mmoja aliyefika kituoni hapo ambaye hakutaka kutaja jina lake gazetini, aliliambia MTANZANIA Jumapili kuwa kuna vitu vimemshangaza kuhusu tukio hilo na kwamba alikuwa akilifuatilia kwa ukaribu.
“Nimetoka humo ndani, lakini kuna vitu sijavielewa, tunataka kuangalia kama ni michezo imechezwa au kweli wanahitaji msaada… tumefanya juhudi nyingi, lakini kuna vitu vimenitia wasiwasi,” alisema ofisa huyo pasipo kuvitaja vitu hivyo.
Ofisa huyo aliliahidi kulipatia gazeti hili taarifa za kina pale atakapokamilisha kulifuatilia jambo hilo kwa kina.
Taarifa zisizo rasmi zilizolifikia gazeti hili, zinaeleza kuwa Roma na wenzake walionekana tangu asubuhi katika mahali ambako hapakuwekwa wazi.
Inaelezwa mtu wa kwanza kupigiwa simu kujulishwa taarifa za kupatikana kwa akina Roma, alikuwa ni Mkurugenzi wa Vipindi wa Clouds Media, Ruge Mutahaba.
Hata hivyo, Ruge ambaye alikuwapo kituoni hapo na baadae katika Hospitali ya Mwananyamala, alilitaka MTANZANIA Jumapili kumuuliza suala hilo Roma mwenyewe na si yeye.
Majira ya saa 3:00 usiku, Roma na wenzake wakiwa hospitalini hapo kuchukuliwa vipimo, askari nao walikuwa wakisubiri majibu yake ili kuyawasilisha kwa Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kinondoni.
Pamoja na hayo, baadhi ya watu wameanza kuhoji tukio zima la kutekwa hadi kupatikana kwa wasanii hao, wengine wakidai kuwa huenda ni mchezo uliochezwa na kiongozi mmoja. ,....
Wanaohoji hilo, wanatilia shaka kitendo cha Diamond kukutana na kiongozi huyo siku mbili baada ya tukio la utekaji kufanyika na kisha kutoa wimbo mpya siku moja kabla ya wasanii hao kuachiwa huru.
Watu hao wamekwenda mbali na kuhoji hatua ya Babu Tale kuhamasisha wasanii kuungana kuwasaka wenzao na zaidi akidaiwa kuwashawishi wakutane na kiongozi huyo ambaye alikaririwa akisema watapatikana kabla ya Jumapili.
- Chanzo gazeti la Mtanzania
Najaribu kuunganisha dots hapo!!! Kuna mengi mengi zaidi yaliyojificha!!! Napata shaka na khofu hali hii ni miaka miwili tu je miaka mingine miwili ijayo hali itakuwaje?