Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam kwa kushirikiana na Timu Maalum ya Kuzuia na Kupambana na Uhalifu wa Mtandaoni, huku ikiwashirikisha Polisi Mkoa wa Morogoro, wamefanya Operesheni maalum kuanzia tarehe 18/05/2022 hadi 26/06/2022 katika maeneo mbalimbali ya Jiji la Dar es Salaam na Mkoa wa Morogoro na kufanikiwa kuwakamata Julius Simon Mwabula @ Kibegi, miaka 20, Mhehe, mkazi wa Ifakara Morogoro na wenzake ishirini na mbili (22) kwa tuhuma za kufanya uhalifu kwa njia ya mtandao.
Watuhumiwa hao wamekuwa wakijifanya wao ni
Wakuu wa shule, Waganga wa kienyeji, Ndugu wa wahanga, Wahudumu wa makampuni ya simu (customer care) au mawakala wa Freemason, ambapo huwatumia watu ujumbe mbalimbali kupitia namba tofauti za simu na kujifanya wanania ya kusaidia watu badala yake huishia kuwaibia ( kuwatapeli).
MFANO WA UJUMBE NI
"
Halo ndugu mzazi mwanao shuleni amepatwa na matatizo na anaumwa sana hivyo tuma pesa haraka ili nimpeleke hospitali” na muhalifu huyo anatoa namba ya kutuma hiyo pesa na ukituma unakuwa umeibiwa.
Watuhumiwa hao wamekutwa wakiwa na vifaa mbalimbali ambavyo wanavitumia kufanya uhalifu huo, vifaa hivyo ni kama ifuatavyo:
- Kompyuta mpakato (laptop) 2,
- Kompyuta ya mezani (desk top) 1,
- Simu za aina tofauti 28,
- Flash 2,
- Modem ya mitandao yote 1,
- Kadi za simu za mitandao mbalimbali zaidi ya 50
Katika Oparesheni hiyo, watuhumiwa wengine wa makosa ya mtandao pia walikamatwa, ambao ni:
Marry Samson Sibora @ ASHA ZUNGU miaka 23, Mzanaki, mkazi wa Sinza Mugabe na
Zainabu Yahaya Omary @ official Manka , miaka 23, Mrangi, mkazi wa Buguruni Wanatuhumiwa kwa
makosa ya usambazaji wa picha za ngono na kuuza mwili kwa njia ya Mtandao ya kijamii ikiwemo facebook, WhatsApp, Tinder na Exotic tz .
Watuhumiwa wote wamehojiwa kwa kina na taratibu za kisheria zinakamilishwa ili wafikishwe Mahakani haraka iwezekanavyo.
Jeshi la Polisi kwa kushirikiana na Mamlaka zingine za kishria, linatoa onyo kali kwa watu wanao jihusisha na uhalifu kwa njia ya mtandao na njia nyingine, kuwa Serikali na vyombo vyake imejipanga kupambana na uhalifu wa aina yoyote, na wahalifu popote walipo watafuatwa, kukamatwa na kupelekwa Mahakamani.
Aidha, Jeshi la Polisi linatoa rai kwa Watanzania wote kutumia mitandao kwa kuzingatia sheria na taratibu zilizowekwa na kuwa waangalifu na vitendo vya utapeli, ikiwemo kuchukuwa tahadhari wakati wa kutuma pesa au kufanya biashara katika mitandao ili kuepuka kutapeliwa, pia watu wajiepushe kufanya biashara haramu mitandaoni kama vile za kuuza mili na ngono.
Muliro J. MULIRO– ACP
Kamanda wa Polisi Kanda Maalum Dar es Salaam.