Yajue usiyoyafahamu kuhusu Vita ya Kagera

Yajue usiyoyafahamu kuhusu Vita ya Kagera

KABLA ya kupambazuka askari wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) walianza kushambulia vilima vya Kikanda, Nsambya na Simba. Majeshi ya Idi Amin yalijua wanajeshi wa Tanzania wangeingia Uganda kushambulia, lakini hawakujua kwa hakika shambulio hilo lingefanyika lini na wapi na kwamba lingefanyika kutokea upande gani.

Kwa jinsi mashambulizi yalivyokuwa makali na ya kushtukiza, Redio Uganda ilitangaza kuwa Uganda imevamiwa na majeshi ya Tanzania na Cuba. Ingawa Cuba ilikanusha habari hizo, Idi Amin aliendelea kuzisisitiza kiasi kwamba jarida la To the point international liliandika, “Dikteta wa Uganda anapiga kelele”.

Kwa mujibu wa kitabu cha War in Uganda, usiku mmoja kabla ya kushambulia vilima vya Simba, baadhi ya makamanda wa brigedi walikutana kwa mazungumzo na kupata kinywaji. Kwa wakati wote huu, kila upande—Tanzania na Uganda—ulikuwa ukijaribu kunasa mawasiliano ya upande wa pili.

Baada ya kupata kinywaji, makamanda wa brigedi walirejea katika vituo vyao na kuanza kucheza kitimbi. Kwa mujibu wa kitabu hicho, makamanda hao walianza kuwasiliana wenyewe kwa wenyewe kwa kutumia redio za upepo.

Mmoja akauliza, “Wacuba wameshakaa tayari upande wa kulia?” Halafu akajibiwa na askari mwingine: “Tayari afande.” Yule wa kwanza akauliza tena, “Waisraeli wameshajiweka tayari upande wa kushoto?” Halafu akajibiwa, “Wako tayari afande.” Kisha akaendelea, “Na je, Wamarekani nao wameshakaa tayari eneo la kati?” Akajibiwa, “Wako tayari afande.” Kisha akasema, “Haya. Twende kazi.”

Majeshi ya Idi Amin yalikuwa yanafuatilia mawasiliano hayo ya redio. Baada ya kusikia mawasiliano hayo, ndani ya dakika chache majeshi ya Uganda yakaanza kulikimbia eneo hilo mmoja baada ya mwingine.

Katika mawasiliano ambayo JWTZ iliyanasa kutoka Uganda walisikia kamanda wa vikosi vya eneo hilo akiwasiliana na makao makuu mjini Kampala akisema, “I see! Kweli wanakuja sasa.” Kisha sauti kutoka Kampala ikajibu, “Sawa. Wapigeni.” Kamanda aliyekuwa akiongea katika mawasiliano hayo alikuwa eneo la vita akiwasiliana na aliyepo makao makuu mjini Kampala. Alipoambiwa wapigeni, yeye akajibu, “Tubadilishane. Wewe njoo huku (vitani) na mimi nije huko (ofisini).”

Siku iliyofuata Idi Amin, kwa kuyaamini maneno ya makamanda wa brigedi waliotaja Wamarekani, Waisraeli na Wacuba, aliingia kwenye studio za Redio Uganda na kuanza kutangaza kuwa nchi yake imevamiwa na Watanzania, Waisraeli, Wacuba na Wamarekani.

Kusikia taarifa hizo, vyombo vya habari vya dunia vikashangazwa na madai ya Amin. Ingawa ilikuwa ni uongo kuwa kulikuwa na Wacuba, Waisraeli na Wamarekani walioivamia Uganda, ukweli ni kwamba Idi Amin alizipata habari hizo kutoka kwa wanajeshi wake ambao nao waliamini kile kitimbi kilichochezwa na makamanda wa JWTZ.

Ni kweli kwamba makamanda wa JWTZ ndio waliosema hayo, na hayo waliyoyasema yakanaswa na redio za mawasiliano za jeshi la Amin ambalo baada ya kuziamini walizipeleka kwa Amin ambaye naye aliziamini na kuitangazia dunia.

Lakini Meja Jenerali David Msuguri, ambaye kwa sasa ndiye alipokea kijiti kutoka kwa Brigedia Jenerali Tumainieli Kiwelu kushambulia majeshi ya Amin, alikemea kitendo cha makamanda hao. Hata hivyo kitimbi hicho kilifanikiwa sana kwa sababu kiliyatia kiwewe majeshi ya Amin.

Mashambulizi makali yakafanywa na JWTZ katika vilima vya Kikanda, Nsambya na Simba. Majeshi ya Idi Amin yalielemewa katika maeneo hayo. Mizinga mikubwa ya Tanzania ikavunja nguvu ya jeshi la Amin.

Upande wa Kaskazini mwa vilima ambako majeshi ya Amin yangeweza kupata mwanya wa kukimbia ulikuwa umezingirwa na brigedi za 201 na 208. Majeshi ya Amin hayakujua yalivyozingirwa.

Walishtukia tu wanashambuliwa na wakastaajabu zaidi kuwa hata walikokuwa wanakimbilia nako kulikuwa kumezingirwa na wapiganaji wa JWTZ. Katika shambulizi hilo moja la siku hiyo moja peke yake, kiasi cha wanajeshi 250 wa Idi Amin waliuawa.

Walipochunguza maeneo waliyoshambulia, makamanda wa Tanzania walitambua kuwa wenzao wa Uganda hawakujua namna ya kutumia vizuri maeneo yaliyoinuka kukabiliana na adui.

Katika kilima cha Nsambya, JWTZ ilikuta handaki moja na simu moja tu ya mawasiliano. Katika eneo la kilima cha Kikanda Watanzania walistaajabu sana walipogundua mizinga mikubwa ambayo makombora yake ndiyo yaliyokishambulia kikosi cha Luteni Kanali Salim Hassan Boma eneo la Mutukula, ilikuwa nyuma ya mlima badala ya juu ya mwinuko.

Wakati mapambano yakiendelea kwenye vilima hivyo, ndege za kivita za Amin zilijaribu kusaidia wanajeshi wake lakini bila mafanikio. Ndege hizo zilishindwa kuokoa jahazi kwa sababu kufikia wakati huo ndege nyingi za Uganda zilikuwa zimeshatunguliwa na JWTZ.

Tangu wapiganaji wa JWTZ walipovuka mpaka na kuingia ardhi ya Uganda Jumamosi ya Januari 20, 1979 na kuteka vilima vilivyotajwa hapo juu pamoja na kiwanja cha ndege za kijeshi cha Lukoma kilichoangukia mikononi mwa JWTZ Jumanne ya Februari 13, Tanzania ilikuwa imeshaangusha ndege 19 za Jeshi la Uganda.

Kilichoanza kumkatisha tamaa Idi Amin ni ile kasi ya Tanzania kuangusha ndege za jeshi lake. Kilichomtia kiwewe zaidi ni kasi ya kukamata silaha kutoka kwa majeshi yake. Baadhi ya marubani waliosikia ndege zao zilivyokuwa zikitunguliwa na majeshi ya Tanzania waliingiwa na kiwewe na hivyo wengine walitoroka kazini.

Kilichofanya Jeshi la Anga la Uganda lifikie katika hali mbaya kiasi hicho ni upungufu—na pengine ukosefu wa wataalamu, upungufu wa vipuri vya ndege na marubani wa ndege za kijeshi kukimbia.

Kwa hiyo wakati mji wa Masaka ukianguka mikononi mwa JWTZ tayari Jeshi la Anga la Idi Amin lilikaribia kuwa mahututi.

Hata hifadhi yake ya silaha nayo ilianza kuwa na mushkeli. Kwenye kilima cha Simba, JWTZ ilikamata vifaru sita.

Baadaye vifaru hivyo vilianza kutumiwa na jeshi la Tanzania. Silaha mbalimbali kuanzia bunduki za kawaida hadi mizinga mikubwa ilikamatwa eneo hilo.

Baada ya kukamilisha kazi ya kuteka vilima vya Kikanda, Nsambya na Simba sasa njia ikawa imesafishwa tayari kwa kuushambulia mji wa Masaka. Nini kilitokea?

Tukutane toleo lijalo
 
Mayunga, twalipo na msuguli. naomba simulizi za Hawa watu katika vita ya Kagera.
 
Mkubwa Niko nashuka na wewe mdogo mdogo mwaga vitu vyote tafadhali
 
Hapa ndiyo tunapofundishwa uongo una madhara makubwa sana...

Kisa chote hiki mpaka kuingia kwenye vita kubwa ni mjenda wa kiganda kuvuka upande wa Tz kuja kunywa pombe na kufuata demu wake...



Cc: mahondaw
 
BAADA ya kuviteka vilima vya Kikanda, Nsambya na Simba, sasa kazi iliyofuata ni kuteka miji ya Masaka na Mbarara. Vikosi vilivyoelekea Masaka havikupata tabu kama vile vilivyoelekea Mbarara. Brigedia Silas Mayunga aliyekuwa akiongoza Brigedi ya 206 ndiye aliyekutana na hali ngumu zaidi.

Kiasi cha kilomita 45 kutoka mpaka wa Tanzania, karibu na mji wa Gayaza vifaru viwili vya Tanzania vya kikosi cha Luteni Nshimani vilipigwa kombora na majeshi ya Idi Amin.

Kwa jinsi Nshimani alivyokasirika, alianza kuwakimbilia maadui waliorusha makombora hayo. Kitabu cha War in Uganda kinasema alipokuwa akiwafukuza kwenye barabara ya kuelekea ufukweni mwa Ziwa Nakivale, Luteni Nshimani aligutuka kuwa alikuwa akielekea kwenye hatari kubwa.

Karibu na kona mmoja ya barabara hiyo alikutana na mzee mmoja mwanamume aliyekuwa akipita eneo hilo. Alimsimamisha na kumuuliza kama ameyaona majeshi ya Amin maeneo hayo. Mzee alimjibu kwamba wote wameshakimbia.

Wakati Nshimani alipogeuka na kuelekea kwenye kona ya barabara hiyo, mtikisiko mkubwa wa milio ya risasi za bunduki za SMG ulitikisa dunia katika eneo hilo. Risasi hizo zilikuwa zikipigwa kutoka pande tatu.

Watanzania walikuwa wameingia kwenye mtego mbaya kuliko wowote katika vita yote ya Tanzania dhidi ya Uganda. Milio ya risasi ilidumu kwa muda fulani, na ilipotulia hatimaye, tayari Watanzania 25 walikuwa wameshapoteza maisha. Haya yalikuwa ni mauaji makubwa zaidi kwa wanajeshi wa Tanzania kuliko wakati mwingine wowote wa kipindi chote cha vita ile.

Shambulio hili lililofanywa na askari wa Idi Amin lilikuwa ni mojawapo ya yale machache waliyofanya kwa umakini mkubwa kipindi chote cha vita.

Shambulio la Ziwa Nakivale likawatia hasira majeshi ya Tanzania, lakini hawakuvunjika moyo. Wakasonga taratibu kuelekea Masaka upande wa mashariki na Mbarara upande wa magharibi. Katika njia nzima kulikuwa na mapigano karibu katika kila kitongoji—mengine madogo na mengine makubwa.

Maeneo ambayo kulikuwa na mapigano makubwa ni pamoja na miji ya Kyotera, Kalisizo, Bukeri, Sanga, Miakitele na baadhi ya maeneo mengine. Wakati wote huu kusonga mbele kulifanyika kwa tahadhari kubwa kuliko ilivyokuwa kabla ya shambulio la Nakivale.

Wanajeshi wa Jeshi la Amin wakawa wanakimbia ovyo na kufyatua risasi ovyo. Wakihofia mizinga ya Tanzania, askari wa Amin walianza kujificha kwenye miji kwa imani kuwa Tanzania ingesita kupiga mabomu maeneo ya raia na hata kama wangepiga mabomu hayo basi raia wa Uganda wangekasirishwa sana na wanajeshi wa Tanzania na hivyo kushirikiana na askari wa Amin.

Lakini hali ilikuwa kinyume. Raia walikuwa tayari wameshaikimbia miji hiyo hata kabla askari wa Amin hawajafika wala wale wa Tanzania. Kutokana na sababu hiyo, wanajeshi wa Tanzania hawakuwa na hofu ya kutumia mizinga yake kushambulia miji hiyo kwa sababu hawakuwa na hofu ya kuwapo kwa raia katika maeneo hayo.

Vikosi vilivyoelekea Masaka havikupata tabu kama vile vilivyoelekea Mbarara. Brigedia Silasi Mayunga aliyekuwa akiongoza Brigedi ya 206 ndiye aliyekutana na hali hiyo.

Kwa mujibu wa kitabu cha War in Uganda: The Legacy of Idi Amin (uk. 82), wapiganaji wa Tanzania walipofika umbali wa kilometa kama 30 kusini mwa mji wa Masaka walikutana na kijana wa Kitanzana ambaye aliwaambia alitekwa na majeshi ya Idi Amin na kupelekwa Uganda sasa alifanikiwa kutoroka na alikuwa njiani kurudi nyumbani. Walipomhoji zaidi aliwaambia wanajeshi hao kuwa ameacha zaidi ya raia 2,000 wa Tanzania katika kambi ya mateso ya Kalisizo.

Lakini walipofika Kalisizo hawakukuta hata raia mmoja wa Tanzania aliyekuwa ameshikiliwa na, badala yake, waliwakuta askari, wapata 600, wa Amin wakisubiri kushambulia. Huenda tayari walikuwa wameachiwa baada ya kupata habari kuwa majeshi ya Tanzania yanakaribia.

Askari wa Amin waliokuwa wakiwasubiri askari wa Tanzania ili wawashambulie, walianza kufanya hivyo. Lakini walipopigwa mzinga wakajikuta wameyeyuka kama samli kwenye kikaango. JWTZ haikuishia hapo.

Ikaendelea kushambulia zaidi kutokea pande tatu. Askari wa Amin wakachanganyikiwa zaidi. Walipoona hali kwao inazidi kuwa ngumu, waliobahatika kukimbia walianza kukimbia ovyo kuelekea Masaka. Zaidi ya askari 200 wa Amin waliuawa siku hiyo katika shambulio hilo moja la Kalisizo.

Walionusurika kuuawa na wakabahatika kukimbia, walikuwa wakipiga mayowe njia nzima kuelekea Masaka. Askari wa Amin ambao hawakuwa eneo la tukio, lakini wakawaona wenzao wakikimbia kwa hofu huku wakipiga mayowe, nao wakajiunga nao na kuanza kukimbia ovyo. Askari wengine waliopata habari za yaliyotukia walivunjika mioyo na wakapoteza hamu ya kuendelea na vita.

Baada ya ushindi wa Kalisizo, Jeshi la Tanzania walikuwa na nafasi nzuri zaidi za kusonga mbele kuelekea Masaka, lakini badala yake walitulia wakaanza kujipanga.

Usiku wa kuamkia Jumamosi ya Febriari 24, 1979, mji wa Masaka ukawa umezingirwa na JWTZ kwa pande tatu na, baada ya muda mfupi, brigedi za 201 na 208 zikaanza mashambulizi. Sehemu ya kwanza kushambuliwa ilikuwa ni kambi ya jeshi ya Kikosi cha Suicide kilichoachwa peke yake kulinda mji wa Masaka. Vikosi vingine vilikuwa vimetoweka kuelekea Lukaya. Walipoelemewa, kikosi cha Suicide nacho kikatoweka, kikakimbilia Villa Maria.

JWTZ walikuwa na amri ya kuiteketeza Masaka. Mji uliteketezwa. Ilipofika jioni ya Jumamosi ya Februari 24, mji wa Masaka ukawa tayari umeharibiwa vibaya, na sasa majeshi ya Tanzania yakaridhika kwamba Idi Amin ameanza kulipa gharama za kuteka ardhi ya Tanzania. Awamu ya pili ya vita ikawa imemalizika. Sasa ikaingia awamu ya tatu. Nini kilifuata baada ya Masaka kutekwa?

Tukutane toleo lijalo.
 
WANAJESHI wa Tanzania walipokuwa wamejipumzisha katika miji ya Masaka na Mbarara waliyoiteka walikuwa pia wakichora mpango wa awamu ya tatu ya vita. Lakini Rais Julius Nyerere, kwa kuhofia lawama za kimataifa alitaka jeshi la Tanzania lisijipeleke mbele sana bali liwaache waasi wa Serikali ya Idi Amin wafanye hivyo halafu JWTZ ije nyuma yao.

Hapo ndipo walipokuja kuingizwa akina Yoweri Kaguta Museveni, ambaye alipewa eneo la Mbarara ambako angewafundisha wapiganaji wake na Paulo Muwanga akapelekwa Masaka. Ingawa Muwanga ni wa kabila la Baganda kama wakazi wa Masaka, alionekana zaidi kuwa ni mtu wa Dk Milton Obote. Baada ya muda mfupi Museveni alifanikiwa kupata wapiganaji kiasi cha 2,000 kutoka Mbarara.

Wakati haya yakifanyika, JWTZ nayo ilikuwa inajipanga upya kutokana na hali ilivyokwenda. Ingawa tayari walikwishateka miji ya Masaka na Mbarara, Idi Amin bado alikuwa madarakani na alikuwa mjini Kampala. JWTZ ikaanza safari ya kwenda Kampala aliko Amin.

Brigedi mbili za Minziro na ya 206 zikaungana kuunda kikosi kazi. Wakati huu ndipo Silas Mayunga alipopandishwa cheo kutoka brigedia na kuwa meja jenerali, kisha akakabidhiwa kikosi kazi hicho. Brigedia Roland Makunda, ambaye alikuwa mkuu wa jeshi dogo la maji alikabidhiwa kusimamia Brigedi ya 206, na Brigedia Ahmed Kitete akakabidhiwa Brigedi ya Minziro.

Baadaye kikosi kKazi kikagundua kuwa Kikosi cha Simba ambacho walikishambulia hawakukiteketeza chote. Baada ya kuukimbia mji wa Mbarara kikosi hicho pamoja na kingine kutoka Kambi ya Mountains of the Moon, walikuwa wamekimbilia Kaskazini mwa mji huo kujiimarisha.

Walishtukiwa baada ya kuanza kuwarushia mabomu wanajeshi wa Tanzania. Lakini JWTZ ilipojibu mapigo, walitoweka.

Jumatatu ya Machi 19, 1979 Redio Uganda iliripoti kuwa Idi Amin aliwatembelea wanajeshi wake “...walioko mstari wa mbele eneo la Mbarara...” na kujadiliana “mambo mengi” na makamanda wa vikosi vya Simba na Chui (Tiger) na kwamba walipanga “mikakati mipya ya kuwang’oa kabisa maadui kutoka ardhi ya Uganda.”

Lakini baadaye ilibainika kwamba redio hiyo ilitangaza uongo. Jambo hilo halikutokea. Lakini angalau hicho kikosi cha Simba kiliendelea kupigana huku kikikimbia. Divisheni ya 20 ya Jeshi la Wananchi wa Tanzania, ambayo ilikuwa inaelekea Uganda, ikakumbana na tatizo jingine la miundombinu wakati kinakaribia eneo la Lukaya, kiasi cha kilomita 40 Kaskazini mwa mji wa Masaka.

Barabara yenye umbali wa kiasi cha kilomita 20 ilikuwa imeharibika vibaya. Kutokana na mvua iliyonyesha barabara hiyo ilijaa madimbwi makubwa ya maji na matope. Hakuna gari lolote lililoweza kupita barabara hiyo, mjia pekee ya kufika huko na kwa kutumia barabara hiyo.

Jijini Dar es Salaam bado Nyerere alikuwa anakuna kichwa. Aiteke Kampala na kumkamata Idi Amin halafu avumilie masuto ya jumuiya ya kimataifa? Au aepuke masuto hayo lakini arudishe majeshi yake nyuma na amwache Idi Amin akiendelea kutawala Uganda?

Idi Amin alijua mpango wa Tanzania wa kuiteka Kampala. Ilisemekana kuwa baadhi ya wanamkakati wake wa kivita walimshauri kuwa ili Kampala isitekwe [kwa urahisi] kama Masaka na Mbarara basi walipaswa kuharibu maeneo fulani ya barabara eneo fulani Kaskazini mwa Lukaya ili kuvunja mawasiliano ya barabara.

Waliambiana kuwa kwa kufanya hivyo kungeyachelewesha zaidi majeshi ya Tanzania kufika Kampala na hivyo majeshi ya Idi Amin yangepata muda mzuri zaidi wa kujipanga upya kukabiliana na maadui. Lakini Idi Amin hakukubaliana na pendekezo hilo, akitoa hoja kwamba ikiwa watavunja madaraja ili Watanzania wasivuke, hatimaye hata yeye mwenyewe hangeweza kuvuka kuwakimbia majeshi ya Tanzania kutoka kwenye ardhi ya Uganda.

Imani ya Idi Amin ya kuwafukuza majeshi ya Tanzania kutoka Uganda ilikuwa kwa kiongozi wa kijeshi wa Libya, Kanali Muammar Gaddafi. Tangu alipopashwa habari kuwa majeshi ya Tanzania yamevuka mpaka na kuingia Uganda, kila mara alikuwa katika mawasiliano na Gaddafi ambaye aliamini kuwa Uganda ni nchi ya Kiislamu ambayo imevamiwa na jeshi ya nchi ya Kikristo.

Kwa hiyo wakati Amin akikataa wazo la askari wake la kuvunja madaraja nchini kwao—kama walivyovunja lile la Mto Kagera—alikuwa tayari amepata ahadi kutoka kwa Gaddafi kwamba alikuwa anamwandalia askari na silaha ambao wangetumwa Uganda kupambana na Watanzania. Hii ilimpa Amin matumaini mapya. Sasa aliamini kuwa hatimaye ushindi ungekuwa upande wake. Kwa hiyo hakukuwa na sababu yoyote ya kuharibu madaraja mazuri ambayo wangelazimika tena kuyajenga baada ya Tanzania kushindwa vita.

Hadi kufikia wakati huu askari wa Libya walikuwa hawajaonekana vitani Uganda. Walioonekana ni Wapalestina waliokuwa wamevaa skafu za PLO na wengine walibeba vitambulisho. Jumanne ya Machi 13, 1979, kupitia Redio Uganda, Idi Amin alitangaza hadharani kuhusu ushiriki wa PLO kwamba, “majeshi ya Palestina yanapigana bega kwa bega mstari wa mbele.”

Kitendo cha Idi Amin kutangaza hadharani kiliwafanya PLO kushindwa kukanusha. Lakini walijaribu kujinasua. Walisema mamia ya watu wao waliopo Uganda walikuwa huko kwa ajili tu ya mafunzo ya kijeshi na si zaidi ya hapo. Lakini hawakuweza kukanusha kama walikuwa wanapigana bega kwa bega na majeshi ya Amin.

Hata hivyo PLO walifadhaika kiasi kwamba waliamua kutuma ujumbe wao mjini Dar es Salaam kusisitiza uhusiano mzuri na mwema na Tanzania. Jumatano ya Machi 21, 1979 ujumbe huo ukaitisha mkutano na waandishi wa habari na kusema, “Hakuna Mpalestina anayepigana bega kwa bega na majeshi ya Idi Amin.”

Lakini hilo halikuondoa ukweli kwamba ushiriki wa PLO katika jeshi la Amin ulikuwa mkubwa. Pamoja na ukweli huo, Rais Nyerere hakuvunja uhusiano kati ya Tanzania na PLO. Ni wakati gani askari wa Libya walliingia.

Tukutane toleo lijalo.

vita%2Bpic.jpeg
 
Wakuu hapa nitawaletea matukio yote muhimu wakati wa vita hii ya Kagera. Sio kama mimi ndiye niliyeandika la hasha! Ninachokifanya mie ni kuwaletea hapa kutoka Gazeti la Mwananchi. Kaa nami upate uhondo huu.

Vita kati ya Tanzania na Uganda, au Vita ya Kagera ilidumu kwa miezi sita kuanzia Novemba 1978 hadi Aprili 1979. Vita hiyo ndiyo iliyouangusha utawala wa Idi Amin Dada uliodumu kwa muda wa miaka minane.

Idd Amin aliingia madarakani Jumatatu ya Januari 25, 1971 alipoiangusha serikali ya Dk Milton Obote na aliondoka Jumatano ya Aprili 11, 1979 wakati majeshi ya Tanzania na ya Uganda yaliposhirikiana kumuondoa.

Mgogoro wa kidiplomasia kati ya Tanzania na Uganda ulianza Jumatatu ya Januari 25, 1971 baada ya Amin kuipindua Serikali ya Dk Obote. Muda mfupi baada ya hapo, Rais wa Tanzania alimpa Dk Obote hifadhi ya kisiasa. Akiwa Tanzania Dk Obote alianza mipango ya kurejea Uganda akitumia ardhi ya Tanzania.

Mambo mengi ambayo yangeweza kusababisha Vita ya Kagera yalikuwa yametendeka tangu Januari 1971 hadi Oktoba 1978, lakini kwa kipindi chote hicho hakuna vita iliyozuka.

Vita hiyo ilianza rasmi siku ileile ya maadhimisho ya Uhuru wa Uganda, yaani Jumatatu ya Oktoba 9, 1978 baada ya mwanajeshi mmoja wa Uganda kuvuka mpaka na kuingia Tanzania kupata kinywaji na kukutana na mpenzi wake ambaye alikuwa raia wa Tanzania.

Kwa mujibu wa gazeti la Daily Monitor la Uganda la Jumanne ya Oktoba 9, 2017, wakati mwanajeshi huyo akiwa mpakani upande wa Tanzania kwa starehe zake, alijikuta akipambana na wanausalama wa Tanzania.

Mwanajeshi huyo alikamatwa na kuwekwa rumande. Mapema asubuhi ya siku iliyofuata, aliachiwa aondoke. Kwa kudhani amedhalilishwa na wanausalama wa Tanzania, alikimbilia kambini kwake upande wa Uganda, akachukua bunduki na kurejea upande wa Tanzania kulipiza kisasi.

Alipofika umbali fulani kutoka kituo alichokuwa ameshikiliwa, alifyatua risasi kwa mbali. Askari wa zamu wa kituo hicho walilazimika kukimbia. Hakuna hata mmoja aliyejeruhiwa.

Alipojisikia vizuri kwa kitendo hicho, aliamua kurejea kambini kwake upande wa Uganda na kumdanganya kamanda wa kikosi chake aliyejulikana kwa jina la Luteni Byansi kwamba alitekwa na askari wa Tanzania, lakini akapambana nao.

Bila kutafakari sana, Luteni Byansi alimpigia simu Kamanda wa Kikosi cha Malire (MMRR) kilichoko Lubiri mjini Kampala, Kanali Juma Ali Oka (alikuwa maarufu kama Juma Butabika).

Bila kuwajulisha maofisa wa ngazi za juu wa Jeshi la Uganda (UPDF), Kanali Butabika aliviamuru vikosi vya jeshi vilivyokuwa Ziwa Victoria kwenda kuongeza nguvu kwenye kikosi cha Luteni Byansi kuishambulia Tanzania.

“Nilikuwa kamanda wa kwanza wa vifaru kuingia Tanzania. Tuliamriwa kushambulia. Tulikaa Tanzania kwa wiki mbili kabla ya kuamriwa kuondoka na kurejea Uganda,” Luteni Muzamir Amule wa UPDF alimwambia mwandishi Faustine Mugabe wa Daily Monitor katika mahojiano aliyofanyiwa mwaka 2015 nchini Uganda.

Kwa maoni yake, Kanali Butabika aliingiza Uganda vita isiyo na ulazima wowote.

“Unawapelekaje vitani wanajeshi kutoka Malire (Kampala) hadi Mutukula (Tanzania) bila kumtaarifu Amiri Jeshi Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi na Usalama au hata kamanda yeyote wa juu wa jeshi?” anahoji Luteni Amule katika habari hiyo.

Ijumaa ya Oktoba 27, 1978, mara baada ya uamuzi wa Kanali Juma Butabika, zilitumwa ndege tatu za kivita aina ya ‘MiG-21’ (Mikoyan-Gurevich) za Kirusi. Marubani bora zaidi wa ndege hizo nchini Uganda, Luteni David Omita, Luteni Atiku na Luteni Abusala walichaguliwa kwa kazi hiyo maalumu.

Kumbukumbu nyingine zinaonyesha kulikuwa na rubani mwingine aliyeitwa Walugembe. Mwaka mmoja kabla, marubani hao watatu—Luteni Omita, Luteni Atiku na Luteni Abusala—walikuwa wamerejea kutoka mafunzoni nchini Urusi.

Uganda ilinunua ndege 20 za aina hiyo mwaka 1977 kuziba pengo la zile aina ya MiG-15 zilizoharibiwa Jumapili ya Julai 4, 1976, wakati makomandoo wa Israel walipoivamia Uganda katika shambulio linalojulikana kama Operation Entebbe.

Ndege hizo zilipaa kutoka Entebbe kwenda kuishambulia Tanzania. Ndani ya muda mfupi zikawa zimeshambulia na kurejea Uganda.

Zilipogeuka, ndege ya Luteni Omita ilipigwa kombora na wanajeshi wa Tanzania. Kombora hilo liliharibu bawa lake la kushoto na ikashika moto. Lakini kati ya sekundi chache kabla ya kushika moto, Luteni Omita alifanikiwa kuruka kwa parachuti.

Hadi wanajeshi wa Tanzania wanafika yalipokuwa mabaki ya ndege hiyo, rubani huyo alikuwa ameshatoweka.

Nchini Uganda, wanajeshi wenzake wakiamini kuwa Luteni Omita ameuawa na majeshi ya Tanzania, walimwona akirejea kambini kwa mguu. Baadaye alipelekwa Entebbe kukutana na Idi Amin ambaye alimpongeza kwa ujasiri wake.

Jumapili ya Oktoba 29, 1978, kwa mujibu wa matangazo ya kituo cha redio cha Voice of Uganda ya Oktoba 30, 1978, Idi Amin aliwapandisha vyeo Omita, Atiku, Abusala na Walugembe kuwa makanali na kuwafanyia tafrija.

Tafrija ya kuwapandisha vyeo ilifanyika mjini Entebbe kwenye Uwanja wa Ndege wa Jeshi.

Wakati Idi Amin akiwa katika sherehe hiyo, Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) lilifanya shambulio lake la kwanza kabisa eneo la Kikagati ndani ya Uganda na kuingia kilometa kadhaa bila ya upinzani wowote.

Itaendelea kesho
Source Mwananchi la leo 10 Dec 2018
Ngoja tuone ila bado kuna vitu vitafichwa bila sababu za msingi.......hususan chanzo halisi cha vita
 
Safi sana...

Ila Nyerere aliichelewesha sana kuwazima Uganda... kila alipokua anaambiwa tuanze, anawasubirisha kutoa amri...



Cc: mahondaw
 
Back
Top Bottom