Zawadi Ya Ushindi

Abdallahking

JF-Expert Member
Joined
Mar 19, 2018
Posts
3,985
Reaction score
10,840



Simulizi : ZAWADI YA USHINDI
Mwandishi : BEN R. MTOBWA
Imeletwa kwenu na: BURE SERIES

Sehemu ya 1

SHANGWE na vigelegele ambavyo viliutoka umati huu mkubwa vilipaa hewani na kujaza anga lote. Sauti za kila aina zilitamkwa kwa kila rangi kiasi

kwamba zilitoa kelele, si kelele za shangwe tena bali mngurumo ambao uliitetemesha ardhi. Naam, ilikuwa siku ya furaha, siku ambayo haitasahaulika, siku ambayo wazee waliusahau uzee wao na kujitoma uwanjani kifua mbele, wakikoroma mikoromo ambayo ilizaa ngurumo ya furaha, siku ambayo vijana waliikumbuka afya yao na kuihadharisha uwanjani kwa kurukaruka huku na huko huku, midomo yao ikiimba nyimbo za ushindi, siku ambayo hata watoto waliukana utoto wao na kujikuta katikati ya wazazi wao wakipiga vigelegele na kucheka.

Naam, siku ya siku! Nani ambaye asingefurahi leo? Siku ambayo mashujaa walikuwa wakirejea







toka katika ile safari yao ndefu ya kumwangamiza nduli, fashisti, dikteta Iddi Amini ambaye alikuwa ameivamia nchi na kuyahatarisha maisha ya mamia ya wananchi wasio na hatia.

Ngoma ziliendela kupigwa ingawa mlio wake ulitawaliwa na vifijo na vigelegele hata visisikike kabisa. Wachezaji waliendelea kucheza na kuimba ingawa macho ya wachezaji yalikuwa juu, kila mmoja akiwatazama wanajeshi ambao walikuwa wakiteremka toka katika magari yao yaliyokuwa yakiendelea kuwasili. Wanajeshi hao walipowasili walijiunga na wenzao katika magoma na vigelegele.

Kila mara mtu mmoja au wawili walionekana wakiiacha ngoma ghafla na kumkimbilia mwanajeshi ambaye ndio kwanza anateremka toka garini. Walimkumbatia na kuviringishana kwa furaha huku machozi ya faraja yakiwaponyoka na kuteleza mashavuni. Pengine alitokea mzee akajikongoja kumkimbilia mtu, alipomfikia alisita ghafla moyoni akinong’ona “siye.”

Hali hiyo iliendelea kwa muda mrefu, lakini hatimaye ngoma zikatelekezwa na nyimbo kusahauliwa, kila mmoja akawa ama kamkumbatia huyu au kaduwaa akimtazama yule.

Waliolia kwa furaha walilia, waliocheka kwa faraja, walicheka. Baadhi walitulia wakitetemeka kwa hofu, mioyo yao ikiwa na imani yenye shaka: Atafika kweli? Atarudi salama? Mungu atajua…

***







Huyu aliteremka polepole, mzigo wake ukining’inia mgongoni. Kama wengine wote alikuwa amevaa mavazi rasmi ya kijeshi, mavazi ambayo yalimfanya aonekane si kama kichaka kinachotisha tu bali kadhalika kama chui anayeranda baada ya kuliangamiza windo lake. Alikuwa akitabasamu. Au tuseme alifahamu mwenyewe kuwa anatabasamu kwani haikuwa rahisi kwa mtu baki kufahamu. Hakuwa mgeni katika mji huu wa Dodoma. Ingawa si mzaliwa wa hapa lakini miaka minne aliyoishi hapa kama haikufaulu kumweka katika orodha ya wenyeji basi ilimfuta katika ile ya wageni. Hivyo, hakuwa na shaka ya kupokewa na watu aliowafahamu. Akatazama huko na huko kwa shahuku. Naam, haukupita muda kabla hajamwona mtu anayemfahamu. Mzee philipo Matayo, mfanyakazi mwenzake, alikuwa akimjia. Akajiandaa kumpokea kwa kuongeza ukubwa wa lile tabasamu lake huku akipanua mikono amkumbatie. Lakini ah! Mzee alimpita bila dalili yoyote ya kumfahamu. Alijaribu kumwita lakini sauti haikufua dafu miongoni mwa kelele nyingi zilizokuwepo. Pengine hakumwona! Aliwaza.
 
2.
Sasa alitokea Luoga, jirani yake, kijana, ambaye kila jioni walizoea kuketi mbele ya nyumba yake wakicheza karata au kuzungumza tu. Huyu alikuwa akimjia huku kamkazia macho. Hakua na shaka kuwa anamwona. Walipokutana Luoga aligutuka kidogo alipoona akikumbatiwa. Akaduwaa katika hali ya mshangao kwa kukumbatiwa na mtu ambaye hakumfahamu







hata kidogo.

“Samahani, nadhani sijawahi kukuona,” alitamka baada ya kujikwanyua toka katika mikono hiyo yenye nguvu.

“Hunifahamu?” mwenzake alihoji kwa mshangao. “Hukumbuki? Humkumbuki mwenzio sikamona?”

Luoga hakuyaamini masikio yake. “Umesema nani? Sika! Ndio wewe sika!” alifoka badala ya kuuliza. Akamkazia macho kwa mara nyingine. Macho yake yalilakiwa na yote yale ambayo kwanza yalimtisha na kumshangaza. Sasa yalimuhuzunisha na kumsikitisha. Kwa muda akajisahau akiwa kamkodolea macho kama anayedhani yanamdanganya na kuota ndoto za mchana.

“Ah!” ikamtoka baada ya kimya hicho kirefu. “Mungu ni mkuu!” Kisha, kama anayetoroka kitisho ama anayeepukwa kutokwa na machozi hadharani aligeuka na kuondoka taratibu huku kajiinamia.

Kitendo cha Luoga kilitonesha au kukumbusha jeraha ambalo Sikamona alikuwa ameanza kulisahau. Hapana, si kulisahau bali kujaribu kufanya hivyo. Jeraha ambalo limekaa katikati ya roho na kuuvisha moyo wake msiba usiovulika wala kufarijika, msiba wa kupotelewa na kilicho chako na kuvisha usicho kitamani, kisichotamanika.

Yale mawazo ambayo yalikuwa yamemjia awali,







mawazo ambayo angeweza kuyatekeleza kama si askari mwenzake kumuwahi muda mfupi kabla ya kuyakamilisha ya kujiua, yakamrudia tena. Naam, ajiue. Angewezaje kuwakabili ndugu zake akiwa katika hali hii? Zaidi ya ndugu zake, Rusia! Angejitokeza mbele yake? Hapana asingekubali kushawishika tena. Lazima atekeleze. Lazima ajiue. Lazima… akafoka kimoyomoyo huku akianza kuondoka kasi.

Alipenya kati ya umati huu mkubwa bila ya kujali chochote. Hakushughulika kujitambulisha kwa waliomjua kadha wa kadha ambao aliwaona. Hakujali alipomwona mtu au watu ambao aliwaona. Hakujali alipomwona mtu au watu ambao waliduwaa wakimtazama kwa mshangao. Wala hakutahabika kuwatazama wale ambao walikumbatiana na jamaa zao wakisheherekea kuonana tena. Alikuwa na yake. Alifanya haraka kwenda asikokujua, akafanya kile ambacho alikijua fika kuwa kingemtenga na macho ya walimwengu milele, na hivyo kumnyima hiyo fursa ya kuchekwa na kusikitishwa kwa wakati mmoja.

Sasa alikuwa mbali kabisa na umati. Akasita kwa muda akijiuliza aende upande upi ambako angepata faragha tosha ya kulikamilisha lengo lake. Wapi? Makore? Tambuka reli? Chamwino? Hapana. Vichochoro vya One Way vinatosha. Silaha? Akafurahi alipokumbuka kuwa bado alikuwa na silaha zake zote. Akaondoka na kuanza kuelekea One Way huku ameridhika kabisa.


“Sika.”
 
3.
Akagutuka kisha akajisahihisha mara moja. Si yeye anayeitwa. Nani awezaye kumfahamu katika hali yake hii mpya aliyonayo? Hakudhani. Akaendelea na safari yake akiwa katika mwendo wake uleule.

“Sika.”

Ilikuwa sauti ya kike. Yaekelea mwitaji alikuwa akimkimbilia. Hata hivyo, hakujishughulisha kugeuka.

“Sika!”

Sasa hakuwa na shaka kuwa ni yeye anayeitwa, kwani mwitaji alikuwa amemfikia na kumshika mkono. Ndipo alipogeuka na kumtazama.

“Rusia.” Akafoka kwa mshangao, bila ya kufahamu anachokifanya. Kiumbe wa mwisho kati ya wote ambao angependa kuonana nao akiwa katika hali hii! Kiumbe ambaye alikuwa hasa ndio kiini cha safari hii ili ajitenge nae milele! Kiumbe ambaye kabla hajaondoka kuelekea huko vitani alimnong’oneza “Utarudi salama… Utanikuta salama ili nikukabidhi zawadi yako…. Ya ushindi…” Kiumbe ambaye… kiumbe…

Hakujua awaze nini. Badala yake alijikuta ameusahau msiba wake na kubaki kimya akimtazama Rusia ambaye pia alisita akitweta kwa mbio alizopiga kumfuata. Uso wake maji ya kunde uliokuwa umezingirwa na nywele nyingi ulimfanya aonekane kama malkia machoni mwa







Sikamona.

“Sika, kwa nini ulikuwa ukinitoroka? Hujui kama siku zote hizi sikuwa na kheri wala afya kwa ajili yako? Sika…” akasita na kumwangukia kifuani. Sikamona akampokea na kumkumbatia kwa nguvu.

Kimya kilichofuata kilikuwa cha faraja. Yote yalikuwa yamesahaulika. Rusia alikuwa amefarijika kwa kumtia Sika wake mikononi baada ya miezi kadhaa ya hofu na mashaka ya kutomuona tena. Sikamona alikuwa ameusahau msiba wake na badala yake kujikuta, kama zamani, yumo katika kifua cha mchumba wake mpenzi. Wakajisahau kama alivyoyasahau macho ya wapita njia.

Kisha, Sikamona akajikumbuka. Akaikumbuka sura yake mpya. Akawaza harakaharaka na kuona kuwa mapenzi yake na Rusia sasa ni ndoto tu, ndoto ambayo kamwe isingetukia kuwa kweli. Ni hapo ambapo alimsukuma Rusia kando polepole na kuanza kuondoka zake.

“Sika! Kwa nini unanifanya hivi? Ni kosa lipi nililokukosea?” Rusia alihoji kwa uchungu ambao ulichanganyika na mshangao.

“Hapana, Rusia. Yaliyopita yamepita. Mapenzi yetu yalikuwa ndoto tu. Ndoto ambayo aslani haiwezi kuwa kweli. Sasa yamekwisha. Sikufahi…” alifoka kwa juhudi ambayo hakujua ilipotoka.

“Yaani… sijakuelewa Sika!” alimjibu kwa sauti yenye majonzi. “Labda huamini kuwa sikuwa na







furaha hata siku moja tangu ulipoondoka hadi leo baada ya kukusubiri kwa hamu kubwa huku nikisononeka mchana na usiku kucha nikilia kama mtoto mdogo. Una nini Sika, jamani?”

Sauti yake ilikuwa na huzuni. Ikamtia Sikamona huruma. Akamgeukia tena Rusia na kumwambia polepole, “Nadhani hujaniona vizuri mpenzi, ebu nitazame.”

Rusia akageuka kumtazama.

Ndio kwanza akashuhudia uharibifu uliokuwa umetendekea katika sura ya Sikamona. Kitu ambacho alikuwa akikitazama hakikustahili kuitwa uso wa binadamu bali kinyago cha Mmakonde ambaye ama hakuwa hodari wa kazi yake au alikusudia kuwashangaza watu. Pua lilikuwa limebomoka na kulalia upande, mdomo mmoja ulikuwa umekatika na kushonwashonwa na wa pili uliambatanishwa kwa shida sana na mashavu yake, jambo ambalo lilimfanya daima mate yawe yakitiririka hadi juu ya kovu hilo jeusi. Jicho moja halikuwepo. Nafasi yake ilimezwa na kovu zito, jeusi, ambalo lilionekana kama lililonona sana.
 
4.
Hayo yalikuwa machache kati ya mengi ya kutisha na kusikitisha yaliyokuwamo katika uso huo. Kwa muda yalimfanya Rusia aduwae akimtazama Sikamona. Kisha ghafla akaangua kicheko.

UCHEKWA! Kisha na mtu kama Rusia! Ni jambo ambalo kamwe halikuigusa akili ya Sikamona.

Kwa kweli, tangu siku ile ambayo alitahamaki na kujikuta kavaa sura hii mpya alifahamu wazi kuwa amekwishakuwa kichekesho miongoni mwa watu. Hata hivyo, kicheko hicho alifahamu kuwa kingekuwa cha kusikitisha. Kila ambaye angemcheka kicheko chake kingekuwa cha uchungu. Wala asingemlaumu yeyote ambaye angemcheka kwani hata mwenyewe alijicheka kwa uchungu siku ile ambayo alijitazama katika kioo kwa mara ya kwanza.

Lakini kilikuwa kicheko cha uchungu. Na kila amchekaye alicheka kwa uchungu. Si kama kicheko na hili tabasamu la Rusia, tabasamu ambalo halina hata chembe ya huzuni kwa kipigo ambacho kimeutokea uso wake. Kwa kweli,







kadiri alivyoyafahamu mapenzi yake, alitegemea kumwona akilia kwa nguvu na aliamini kuwa kilio hicho kingekuwa sherehe ya mwisho kwa mapenzi yao, kwani baada ya kulia angemwepuka daima na kumkwepa kila wakutanapo. Na iwapo ingemtokea kumfumania mahala lazima Rusia angetoa visingizio kadhaa vya kumtoroka, kumbe sababu si nyingine zaidi ya kumwogopa, kumdharau na kutomwamini tena. Sika kwa kuifahamu fika sura yake ilivyo sasa alikuwa ameamua kitambo kuwa asingemlaumu Rusia kwa uamuzi huo.

Ni hayo ambayo yalimshawishi kujiua. Hakutaka kuyaona machozi ya Rusia yakimiminika hadharani kwa ajili yake. Wala hakuwa tayari kushuhudia mwisho wa mapenzi yao ukitokea katika hali kama hiyo. Wala usingekuwa mwisho wa mapenzi yao tu, bali pamoja na ule mwisho wa kumpata mpenzi mwingine yeyote duniani.

Kumbe alikosea. Alikosea kwa yote aliyofikiri. Badala ya mwisho wenye majonzi ambao aliutegemea, umetokea kuwa mwisho wa vicheko na tabasamu, vicheko vya dharau na tabasamu la kashfa. Tabasamu ambalo licha ya kudhihirisha kuwa sura yake haifai kabisa ni ushahidi tosha kuwa asingependeka milele. Kama Rusia kiumbe ambaye alidhani wanapendana, anamcheka watafanyaje wale wasiomjua? Wale ambao hawakuwahi kuitamani sura yake ilipokuwa timilifu? Mawazo hayo yalimwongezea mori wa kujiua upesi ajifiche, asipambane tena na nyuso







zenye huruma, unafiki na tabasamu zenye uchungu. Hakuwa tayari kuendelea kuishi. “Lazima afe… lazima…” alinong’ona kwa uchungu huku akianza kuondoka. Lakini baada ya kupiga hatua mbili tatu kizunguzungu kilimshika, akapepesuka na kuanguka chini. Alijikongoja kuinuka lakini akaanguka tena. Rusia alimuwahi na kumshika mkono, kumwongoza katika kivuli cha mti. Lakini Sikamona hakuhisi mikono hiyo. Wala fikara zake hazikupokea sauti wala ujumbe ambao Rusia alijaribu kumwambia. Badala yake hisia hizo zilikuwa zimehama ghafla na kusafiri maili nyingi nyuma ya wakati zikimfanya aone upya yote ambayo yalikuwa yamemsibu, yote yale ambayo yalimfanya aambulie kuvaa sura kama hii na kuishia kuchekwa na mtu wa mwisho katika wote aliowategemea kumcheka.
 
5.

SIKU hiyo alikuwa ameamka mkakamavu mno. Alihisi afya na kujisikia uchangamfu mwili mzima. Alijisikia akicheka kimoyomoyo. Furaha iliyoje kuwa hai hali

ujana u kamili katika roho na nafsi yako? Aliwaza akichupa toka kitandania na kuvaa mavazi yake harakaharaka. Kisha, alikumbuka kuwa ilimpasa aoge. Kwani jana yake hakuwa amefanya hivyo kwa ajili ya uhaba wa maji. Akavua nguo zake na kujifunga taulo kiunoni. Akavuta ndala toka uvunguni na kuzipachika miguuni. Huyoo, akaelekea bafuni. Huko alikutana na mengine. Maji yalikuwa yamekatika tena. “Haya ndio matatizo ya mkoa huu.” Aliteta moyoni akirejea chumbani ambako alivaa tena nguo zake. Akasugua meno na uso kwa maji ya chupa kisha akaondoka zake kuelekea kazini.

Vinginenvyo, ilikuwa asubuhi njema vilevile,







asubuhi ambayo iliendana vilivyo na hali yake, asubuhi yenye hali ya hewa nyepesi, yenye ule ubaridi unaofariji na kuburudisha.

Kwa mwendo wake wa hatua ndefu aliuacha mtaa wake wa Iringa na kujikuta katikati ya mji wa Dodoma, mji ambao unakusudiwa baadaye uwe Makao Makuu ya Chama na Serikali. Tahamaki akajikuta tayari amewasili kazini kwake CDA, alipita mlangoni na kuiendea ofisi yake huku akipiga mluzi, akiimba wimbo wa mwanamuziki mmoja maarufu duniani.

“Makini kabisa,” alizijibu salamu za wafanyakazi wenzake.

“Vipi! Mbona unaoneka mchangamfu sana leo?” mmoja wao alimtania. “Au ndio umepiga maji alfajiri?”

Alimjibu huku akicheka “Tangu lini nikanywa pombe? Ni kawaida yangu kufurahi na kwa nini ninune? Nna wasiwasi gani mie? Niko huru, katika nchi huru.”

“Wacha, bwana. Mbona jana tu hukutaka kuzungumza na mtu?” Mfanyakazi huyo aliendelea kutania. “Kama hukulewa basi umeshinda bahati nasibu, zawadi ya kwanza.”

Wakacheka kwa nguvu Kisha wakazama kazini.

Saa za kazi zilipokatika Sikamona hakupoteza muda wake. Alifanya haraka kurejea nyumbani kwa mwendo uleule alioujia. Jua lilikuwa kali







na joto jingi, siku zote joto hili lilimuudhi na kumfanya achukie kuishi hapa.

Asingesahau wakati alipotoka kwao Iringa na kuhamia hapa. Siku ile ya kwanza tu alilakiwa na joto kali ajabu. Alipokimbilia bafuni ili aoge alikuta bomba kavu likikoroma kana kwamba linamdhihaki. Usumbufu huo alidhani ungemtia kichaa. Lakini haikutokea kuwa hivyo. Badala yake alijikuta akizoea na kujifunza ustahimilivu.

Lakini leo joto hilo hakuliona hata chembe. Kwani hali ilikuwa ya kawaida, hali ambayo haikuwa na maudhi wala ukatili wowote. Amani, furaha, afya na starehe iliyojaa katika moyo wake ilikuwa vimelimeza kabisa tishio lolote la joto na vumbi ambalo lilikuwa likipeperuka huku na huko.

Kisha, aliishuku furaha yake. Ni kweli kisa cha furaha yote hii ni ujana, uhai na afya peke yake? Haiwezekani. Alijikanusha. Angekuwa mnafiki mkubwa kudai hivyo kwani alifahamu fika asili hasa ya furaha hii ilikuwa ile shahuku ya mkutano wake na Rusia jioni ya leo, mkutano ambao waliuandaa jana ukiwa na ajenda moja tu, kupanga lini wafunge ndoa.
 
6.
Ni hilo ambalo lilizaa furaha rohoni mwake na kufichua afya katika ganzi yake kwani hilo ndilo lililokuwa njaa yake ya kila siku, njaa isiyoshibika kila usiku hakupata usingizi unaomstahili kwa ajili ya kutokuwa na Rusia. Na mchana aliona hauna amani kwake bila ya Rusia kuwa mbele yake. Sasa maadamu siku ya njaa hiyo kudidimia







milele ilikuwa imewadia angekosaje kusahau joto na kudharau jua? Angeshindwaje kuikumbuka afya yake na kuuona ujana wake?

Jioni baada ya kula na kuyaoga yale maji aliyokuwa ameyaifadhi kwa ajili ya dharura alijikuta mitaani. Mguu na njia akielekea Makole kumchukua Rusia. Alijilazimisha kadiri ya uwezo wake kupunguza mwendo ingawa hakufaulu. Mara kwa mara alijifumania kakaza mwendo kupita kiasi hali saa ikimwambia muda walioahidiana ulikuwa mbali.

Njiani alikuta vikundivikundi vya watu wakizungumza kwa sauti ambazo hazikuwa za kawaida. Akahisi lipo jambo lililotokea. Lakini hakuwa na muda wa kujiingiza katika magenge na kuanza maongezi. Aliendelea na safari yake, hatua moja baada ya nyingine.

Mbele yake kulikuwa na watoto wawili. Walikuwa wakienda huku wakizungumza jambo ambalo ingawa hakulielewa, lakini alilisikia kikamilifu.

“Wacha bwana!”

“Kweli kabisa. Atapigwa hadi aone haya.” “Unamtania Idd Amini! Afrika nzima hamna

shujaa kama yeye.”

“Nakwambia atapigwa!” ilikuwa sauti isiyo na shaka. “Ngoja uone. Jeshi letu rafiki yangu ni la pekee. Hivi hujasikia ile methali ‘Debe tupu alihachi kuvuma?’ Ana bahati mbaya sana Amini.

“Siamini.”







“Utaamini tu.”

Sikamona aliwapita na kwenda zake. Maongezi ya Idd Amini yalikuwa yamemchosha siku nyingi, Kwa kadiri alivyofahamu Amini alitawala maongezi si hapa tu bali duniani kote. Vyombo vya habari daima havikukosa cha kuandika juu yake.

Alipoitazama tena saa yake ilimshauri kuongeza mwendo. Akafanya hivyo. Haukupita muda mrefu kabla ya kuwasili mbele ya nyumba yao Rusia. Ule ushujaa aliokuwa nao moyoni ukaanza kudididimia. Siku zote hali hii ilimtokea kila alipokabiliwa na jukumu la kugonga mlango wa nyumba hii, mlango wa akina Rusia. Ukweni, aliwaza akicheka kimoyomoyo. Hata hivyo, baada ya dakika mbili za kujishauri, jitihada zilishinda hofu yake. Akagonga. Bahati ilikuwa upande wake. Aliyefungua mlango hakuwa mwingine zaidi ya Rusia.

Alihisi uso wa Rusia hauna ile hali ambayo huwa nayo siku zote.

Kwa nini? Akajiuliza.

Alikaribishwa ndani ambako aliongozwa hadi chumbani kwa mchumba wake.

“habari za hapa?” alihoji baada ya kuketi kitandani.

“Kidogo nzuri.”

Sauti ya Rusia kadhalika ilikuwa na upungufu fulani katika masikio yake







“Una hakika ni nzuri?” Alihoji tena ili kufukuza ukimya ambao ulianza kutanda.

“Bila shaka, wewe waonaje kwani?” Rusia aliuliza akijiketisha kando yake. Sauti yake ilibishana na maneno yale.

“Sioni kama una hali ya kawaida.” Kimya kikawateka tena.
 
7.
Ni katika kimya hiki sikamona alipoigundua ile siri ambayo siku zote alikuwa akijuliza juu ya mafanikio, siri ya mapenzi yake kwa Rusia, yaani sababu hasa iliyomfaya ampende na kuamua awe mwandani wake milele. Hakupata kuifahamu hadi leo baada ya kumwona Rusia akiwa amenuna kinyume cha kawaida yake.

Kumbe hakuna kilichomvutia zaidi ya ule uchangamfu na tabasamu zake ambazo hazikukoma kububujika kila wakutanapo, kila siku, isipokuwa leo.

Sio kweli kudai kuwa Rusia hakuwa mzuri. Alikuwa mzuri. Mzuri zaidi ya wazuri wengi. Alijaliwa uso mpana ambao ulibeba pua nyofu, mashavu wastani yaliyonona, macho maangavu yanayocheka daima. Umbo lake kadhalika halikuitupa sura. Lilikuwa lile lenye urefu wa kadri na unene wa kadri kama unavyomtshili kabisa mwanamke. Mavazi yake hali kadhalika, yalikuwa kiungo ambacho kilitumika kukamilisha ubora wake. Hakuvaa kiuni wala hakutegemea kuvaa nguo fupi na kujipamba kwa bidhaa zitokazo kiwandani ili kuongeza uzuri.







Siku moja aliwahi kumwambia Sikamona juu ya hilo, “Tabia hiyo ni moja ya utekaji nyara, unamlazimisha mtu akuhusudu bila ihari. Haikuwa uongo, nguo zake zilikuwa za heshima, nywele zake asilia, ngozi yake ya kuzaliwa lakini alimvutia kuliko wengi ambao walitumia maelfu ya pesa kujitengeneza. Machoni mwa Sikamona alivutia kuliko wote.

Hata hivyo, si hayo tu yaliyomfanya Sikamona ajikute hana heri bila kumwona kwani mwenye sura na tabia nyofu kama hiyo hakuwa peke yake. Walikuwa wengi. Wengi tosha. Sikamona aliwastahi wote na kuwahusudu lakini hakuwapenda wala kuwaza chochote juu yao zaidi ya ile hadhi ya kawaida isipokuwa Rusia.

Mapenzi yao na hatimaye, uchumba ni vitu ambavyo vilitokea kama muujiza

***

Ilikuwa asubuhi moja yenye kila hali ambayo Sikamnoa haipendi. Mawingu yalikuwa yametanda angani bila dalili yoyote nyingine ya mvua kunyesha. Mingurumo hafifu ilisikika mara Kusini mara Kaskazini na kuzidi kuchafua mandhari. Sikamona alikuwa njiani kuelekea ofisi ya Waziri Mkuu kwa shughuli za kikazi. Alipoingia ofisi aliyoihitaji alipokelewa na karani ambaye alimlaki kwa namna ambayo hakuwahi kulakiwa huko nyuma. Ukarimu, heshima na zaidi ya ya yote tabasamu laini vilichangia katika kumkaribisha. Ni tabasamu ambalo lilimkoga







Sikamona vilivyo. Lilkuwa tabasamu ambalo lilimfanya ajisikie mwenyeji ghafla kiasi cha kujiona kama yuko nyumbani kwake.

“Naitwa Sikamona.” Alijitambulisa pasi ya kutegemea.

“Ndio. Ndio. Nami jina langu Rusia. Rusia Rashidi.”

Kwa muda Sikamona akajisahau na kujikuta ameketi akimwuliza Rusia habari ambazo hazikuhusiana kabisa na shughuli za kikazi zilizomleta. Baada ya muda alihoji lile swali ambalo lilimtatiza tangu alipokaribishwa “Hivi uliwahi kuniona huko mbeleni?”

“Hapana, kwa nini?”

“Kwa jinsi ulivyonikaribisha. Nilidhani wanifahamu.”

Tabasamu la Rusia likageuka kicheko.

“Hata mimi nilidhani wewe wanifahamu. Niliona uso wako una dalili zote za kujuana.”
 
8.
Wakacheka

Kisha Sikamona akaongeza harakaharaka, “Najua tulikowahi kuonana

“Wapi?” “Ndotoni.” Wakacheka tena

Yalifuata maongezi marefu, wakiongea hili na lile hadi mgeni, ambaye alikuwa akizungumza







na bosi wake Rusia alipotoka na Sikamona kuruhusiwa kuingia.

Aliingia shingo upande. Alipotoka aliaga kwa huzuni na kusindikizwa kwa tabasamu ambalo lilijijenga rohoni mwake, jengo imara ambalo lilimtia kiu ya kuendelea kuonana na Rusia na njaa ya kuliona tena tabasamu lake.

Bila shida maalumu, siku ya pili, Sikamona alijikuta amewasili tena katika ofisi hiyo. Ni siku hiyo ambapo alifanikiwa kumtaka wakutane jioni nje ya ofisi hiyo.

Walikutana. Wakaendelea kukutana.

Tabasamu la Rusia liliufanya kila mkutano ufane na kushawishi mwingine. Wakajikuta tayari wamefahamina tosha.

Rusia alimfahamu sikamona kuwa alikuwa mwana wa mkulima mmoja wa kahawa huko mkoani Iringa na kwamba alikuja hapa Dodoma miaka miwili iliyopita baada ya kuamishwa toka Songea alikokuwa akifanya kazi tangu alipomaliza kidato cha nne.

Naye Sikamona alifurahi kufahamu kuwa Rusia, mtoto pekee wa mzee Rashid alikuwa mzaliwa wa mkulima wa hapahapa Dodoma ingawa asili yao ni huko Tabora. Baba yake alikuwa amestaafu kazi ya ualimu baada ya kuifanya maisha yake yote. Sasa walikuwa wakiishi kwa kutegemea mashine yao ya kusaga nafaka pamoja na kimshahara cha







kima cha chini cha Rusia. Mama yake alikuwa amefariki miaka kadhaa iliyopita. Rusia aliishi na mama wa kambo

Naam, walijuana tosha. Wakazidi kupendana.

Katika moja ya mikutano hii Sikamona alimfichulia mwenzake siri ya roho yake. Kwamba hana hali wala afya kwa ajili yake.

“Sasa?” Rusia aliuliza

“Nakutaka uchumba. Nataka nikuoe.” Alimjibu Tamko hilo lilifanya Rusia aangue kicheko.

Alicheka kwa muda mrefu, kisha akamfahamisha kuwa tangu siku ile walipoonana ofisini kwa mara ya kwanza alikuwa amefahamu kuwa Sikamona alikua amezaliwa kwa ajili yake, na hivyo asijisumbue kusema mengi.

Tabasamu la Rusia likaendelea kuurutubisha uchumba wao kama maji katika bustani. Tabasamu ambalo lilimfanya Sikamona ajisikie afya na furaha kila alionapo. Si furaha tu, bali pamoja na kuwa na hakika ya uhai na kuyapenda maisha, kwani alijisikia kama tajiri mbele ya malkia mzuri kila awapo mbele ya msichana huyu.

***

Naam, siku zote isipokuwa leo tu ambapo Rusia alipoteza kabisa tabasamu na kusahau ule uchangamfu wake, hali ambayo ilimfanya Sikamona akose furaha na kuishuku afya yake.

“Unasema habari nzuri?” alihoji tena. “Mbona
 
9.

waonekaana kama mwenye msiba?”

Rusia alijaribu kuatabasamu, tabasamu ambalo halikuwa kamili. “Kwani kuna mwenye furaha leo hii?”

Akauliza “Kwani kuna nini?” Badala ya kumjibu. “Naona huna habari.” Rusia alimwambia. “Habari ipi?”

“Ya kuvamiwa.” “Kuvamia!”

“Na Idd Amini. Hujasikia kuwa ameteka sehemu ya nchi yetu na kuangamiza mamia ya watu wasio na hatia?”

“Hee? Wacha!” alifoka kwa mshangao “Ametuchokoza. Ameanzisha vita…”



NAKUPENDA kusikia zaidi. Hakuwa tayari.

Vita kwake ilikuwa jambo la mwisho, jambo lenye kila aina ya mikosi, dhiki

na maafa. Ni fursa pekee ambayo, licha ya kusababisha uharibifu wa maisha ya watu wengi, wasio na hatia, hurejesha nyuma maendeleo ya jamii.

Hakupenda vita. Kwa ujumla alivichukia. Hivyo, alimchukia kila mtu ambaye huanzisha au kuwa kiini cha vita.

Ni kweli kuwa viko vita ambavyo huanzishwa na jamii kwa manufaa ya jamii, vita ambavyo hupiganwa na jamii nzima kutokomeza tawala dhalimu zinazoikandamiza. Haja ya vita hivi ni kuinua maisha ya wananchi ili waweze kufaidi matunda ya uraia wao. Vita vya Mau-Mau wa




Kenya, mapinduzi ya Zanzibar, Kyuba, China na Urusi ni mifano dhairi. Hivi kwake vilikuwa vita vitakatifu, vita ambavyo ingawa pia hakuvipenda bado ilikuwa lazima vipiganwe ili jamii hizo ziweze kuwa hapo zilipo. Vita hivyo aliviheshimu kwa kuwa vilitengeneza njia kwa vizazi vya baadaye. Hivyo, waliovianzisha na kuviongoza walikuwa na nafasi pekee katika moyo wake. Kila alipoyafikiria majina yao neno shujaa lilitangulia kila jina.

Lakini si vita kama vile vya Adolf Hitler, vita vya mtu mwenye njaa ya kupanua mipaka yake na kutapakaza jina lake, mtu mwenye kiu ya kumwaga damu, vita ambavyo vilisababisha majonzi makuu na kuyapotosha maendeleo ya dunia nzima.

Mtu kama huyu kwake alikuwa zaidi ya mkatili, mtu ambaye jina lake aliliona karibu zaidi na shetani, kwani ni mtu ambaye hufuraishwa na mateso ayapatayo mtu mwingine, huchekelea aonapo mtu akifa, hutabasamu aonapo mama akilia kwa uchungu wa kuwa mjane na kushangilia pale ambapo umati wa watu huanguka na kufa mbele ya risasi zake. Utu wa mtu kama huyu aliutilia mashaka.
 
10.
Mtu kama Idd Amini! Kiongozi ambaye amejipa uongozi mwenyewe baada ya kuunyakua toka katika serikali halali iliyochaguliwa na wananchi kwa manufaa yao. Ni mtu ambaye alikuwa na sifa zote za ukatili na unyama. Vitendo vyake vya kinyama vilikuwa vingi kiasi cha kuwafanya watu washindwe kuamini kama ni vitendo vya kweli au

hadithi za kubuni.

Baadhi ya vitendo hivyo ni kile cha kumuua kila ambaye alimshuku kuwa ni mpinzani wa uongozi wake. Ukatili haukutokana na kuua tu bali pia mbinu alizozitumia katika mauaji. Aliua kwa namna ya kusikitisha sana, namna ambayo mtu yeyote asingefurahi kuona mwenzake akitendewa, yeyote, isipokuwa Amini pekee na wale ‘wateule’ wake wachache wenye roho ngumu kama yake.

Baaaadhi ya watu ambao dunia iliwafahamu, waliofanyiwa unyama huo na Amini ni marehemu Godfrey Kiggala ambaye alikuwa Waziri wake wa Mambo ya Nje. Huyu alipigwa risasi na kung’olewa macho na ngozi yake kuchunwa. Alipopelekwa hospitali ilikuwa vigumu kumtambua.

Mwingine alikuwa Jemedari wake Brigedia Charles Arube. Huyu aliteswa na kuhangaishwa kupita kiasi. Yasemekana kuwa Amini hakuridhika na mateso hayo. Hivyo, aliifuata maiti hospitali ambako aliwafukuza madaktari na kujifungia peke yake na maiti hiyo chumbani kwa dakika kadhaa. Alichomfanya maiti ni siri yake.

Pamoja na hao, ni maelfu ya watu wengi, wote walipoteza maisha yao kwa namna ya kusikitisha ama kwa amri yake au kwa mkono wake, wengi mno, maaskofu, waumini, wasiojiweza n.k.

Sifa hizo si kwa mauaji tu, ilikuwa pamoja na yale mambo yake ya ajabuajabu. Mara atadai anataka kuikomboa Afrika Kusini, mara atatuma jeshi lake kuwatoa Waizrael katika sehemu







ya Waarabu inayokaliwa kwa mabavu, mara Uingereza ina haki kuzuia Afrika Kusini silaha nakadhalika. Mara mbili aliwahi kuutangazia ulimwengu akidai kuwa ameongea na Mungu, na ameambiwa hivi na vile. Sifa hizi ni pamoja na ile inayosemekana kwamba alijitapa sana kwa kula nyama pamoja na kunyonya damu za watu.

Sikamona hakujua amweke katika kundi lipi mtu kama huyu. Kumwita mkatili ni upendeleo mkubwa kwake, kichaa labda ni kumwonea, nduli ni kumsifu kupita kiasi na dikteta ni kumvimbisha kichwa. Hakujua amwite nani. Kwa kweli, hakujua.
 
11.
Baada ya kuwafanyia unyama usio kadirika wananchi wa Uganda, sasa alikuwa amevuka mpaka na kuja Tanzania kupanua milki yake! Kuiweka sehemu ya nchi yetu chini ya kwato zake! Chini ya jinamizi!

“Tusi lililoje hili!” Sika aliropoka bila ya kufahamu.

Sauti yake ikamzindua yeye mwenyewe. Akaibuka toka katika dimbwi la mawazo. Ndio kwanza akagundua kuwa alikuwa kando ya mpenzi wake, chumbani. Akamtupia jicho ambalo lilikuwa na dhamira ambayo binafsi hakuifahamu. Kisha, aliinuka na kuondoka.

Usiku akiwa amelala chali kitandani, redio yake kaifungua kwa sauti kubwa kuliko alivyozoea, ndipo aliposikia yote aliyoyasikia kwa uhakika zaidi, kwamba jeshi la Idd Amini likiongozwa na







vifaru limeingia nchini kupitia Kagera na kuteka eneo la Tanzania, sehemu ile ambayo tangu aliponyakua madaraka alikuwa akidai kuwa ni eneo lake. Si kuteka tu, bali ilikuwa pamoja na kuwaua kinyama mamia ya wananchi wasio na hatia, kwamba, alikuwa amewashika wananchi, wake kwa waume, watoto kwa wazee na kuwalaza chini kisha akawasaga kwa vifaru pamoja na kubomoa majumba na madaraja, kuiba ng’ombe na kila walichokitamani, na kwamba sasa bendera yake ilikuwa ikipepea katika tarafa hiyo akidai ameikomboa kuondokana na ujamaa!

Sikamona akajigaragaza kitandani kwa uchungu uliochanganyika na hasira. “Aibu iliyoje… ukatili ulioje…” alifoka kwa sauti ndogo. “Na serikali yetu inafanya nini?” Alijiuliza. “Mtu aamue kutuvamia nchi ya amani na haki kama hii, tumtazame tu? Huyu anastahili kufunzwa adabu… serikali yetu inafanya nini?”

Kisha ilifuata ile hotuba ya Amiri Jeshi Mkuu na Rais wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere. Ilikuwa hotuba kali yenye hasira ingawa Mwalimu alizungumza kwa sauti ambayo haikufaulu kuacha huzuni na uchungu hasa kwa kule kufahamu maafa ambayo yangefuatiwa.

“…Tumevamia… Mwendawazimu katuvamia… Katutangazia vita… Na sasa tutampiga… Uwezo wa kumpiga tunao. Nia ya kumpiga tunayo. Sababu ya kumpiga tunayo. Hivyo, tutampiga, wananchi tulieni, msibabaike, sikilizeni muone







vijana wetu watafanya nini…”

Moyo wa Sikamona ulifarijiwa na hotuba hii. Afya na ujana ukamrejea huku akihisi tabasamu katika roho yake. Huu ndio utu, vinginevyo isingekuwa taifa, kuacha ukatili ukineemeka katika ardhi yako! Ingekuwa sawa na mwumini aendaye msikitini bila kutawadha, aliwaza. Polepole usingizi ukamjia. Alafu, ile ndoto yake ya siku zote, kwamba yu pamoja na Rusia, wakizungumza na kucheka, ikamjia tena. Alipogeuka na kujaribu kumkumbatia, kama kawaida ndoto hiyo ilitoweka. Na ilifuatwa na kupaa kwa usingizi. Akabakia macho, akimwaza Rusia.
 
12.
Mara akakumbuka kuwa alikuwa amesahau angalau kumdokeza ile haja iliyompeleka kwao. Haja ya kupanga siku kamili ya harusi yao.



Umesema haja yako ni kujitolea kwenda vitani kumwadhibu nduli aliyeivamia nchi yetu?” Kamanda huyu wa Jeshi la Wananchi, aliyevaa magwanda yenye tepe tatu begani, alimhoji tena huku kamkazia jicho ambalo alihisi lapenya mwili na roho yake hata kuiona roho na

fikra zake. “Ndio, afande.”

“Una hakika uamuzi huo ni wako mwenyewe? Au umeshawishiwa na mtu au kitu fulani?”

“Hapana, mzee,” alimjibu “Nimeamua mwenyewe.”

Unaweza kuniambia kwa nini umeamua hivyo?” Kamanda hakuchoka kuuliza.

Angeweza kutaja sababu nyingi zilizomtuma kuamua hivyo, nyingi mno, kwamba nchi ilikuwa imeonewa, nchi imedharauliwa, nchi imetukanwa,







nchi iko katika hatari ya kuangamia kwa ukatili wa mkatili mmoja. Hivyo, nchi inahitaj kurudisha hadhi yake. Kujikomboa na kumwadhibu mkatili huyu. Yeye kama mwananchi, yeye kama kijana ambaye taifa linamtegemea, angewezaje kuzibia masikio wito wa taifa? Angewezaje kujistarehesha katika mabaa na majumba yote ya starehe hali afya na ujana wake unahitajika na taifa kwa manufaa ya taifa?

Ni hayo, ambayo angeweza kumwambia Kamanda huyo. Lakini licha ya ukosefu wa muda, hakuwa mwepesi wa kuongea mawazo yake. Hivyo, alitamka kwa sauti nyembamba. “Nimeamua kwa kuwa nafahamu ni wajibu wangu kufanya hivyo.”

Kamanda alitabasamu kisha akamwandika jina lake katika ile orodha ya mamia ambao walikuwa wamekwishajiandikisha, “Taifa linawahitaji watu kama wewe. Na lina haki ya kujivunia watu wenye moyo kama wako,” alisema akimuaga.

Sikamona aliondoka katika ofisi hiyo ya CCM hali amefurahi na kuridhika kabisa. Akaelekea nyumbani kwake kufunga virago vyake pamoja na kuagana na rafiki zake.

“Hongera kwa uamuzi wako,” Luoga alimwambia huku wakiwa wameshikana mikono wakati wakitoka nje ya ofisi hiyo. Alikuwa amemwomba amsindikize. “Hata mimi ningeenda iwapo mama yangu angekuwa na mtoto wa pili. Lakini nipo peke yangu naye ni mjane.
 
13.
“Sio lazima twende wote. Kuna mengi ya kufanya







huku nyuma. Sisi tutakuwa mstari wa mbele. Tutategemea sana juhudi zenu mlioko nyuma yetu,” alimjibu ingawa kiasi alimfikiria kama mwoga. Vipi kama kila mmoja angetoa ai hii au ile? Nani ambaye angeikomboa nchi kutokana na nduli mwenye kiu ya damu?

“Mungu akujalie baba…” walimtakia kheri majirani mara ilipofahamika kuwa yeye ni mmoja wa vijana waliokuwa wakijiandaa kufanya msafara huo.

“Nenda na urudi salama.”

“Na… utarudi tu mwanangu.” Zilimfanya Sikamona kiasi aingiwe na hofu.

“Mbona wote wanasema hali wana huzuni? Wanadhani nitakufa?” alijiuliza.

Vipi kama angekufa? Swali hili lilimtia hofu kidogo. Hata hivyo, aliishinda hofu hiyo kwa kujiuliza wangapi wamekwisha kufa kwa ajili ya taifa! Wako wapi wakina Mkwawa, Mirambo, Kinjekitile na askari wao? Wako wapi mashujaa wengi ambao majina yao hata hayakubahatika kuingia katika kurasa za historia? Kwanza hawakufa! Hawakufa kamwe. Majina na hadhi yao vinadumu na vitaendelea kudumu milele kwa ajili ya kujitoa kwao mhanga. Naye akifa jina lake litabaki katika orodha ya mashujaa. Ni bora mara elfu kufa vitani kuliko kukutwa na kifo kitandani au kilabuni.

Mawazo hayo yalimrudishia ushujaa na kumfanya aamue kupigana. Hakuwa na shaka na







uamuzi wake huo.

Sasa kulibaki wajibu mmoja tu, kuagana na Rusia. Asingekwenda bila ya kuonana naye. Kwani moja kati ya sababu ambazo zilimfanya aamue kwenda vitani, ambazo hakumtajia yule Kamanda alikuwa Rusia.

Tangu siku ile ambayo alimwendea kwa haja ya kupanga harusi yao lakini badala yake akaondoka na habari za kuvamiwa, alikuwa amemwendea zaidi ya mara tatu na kurejea bila mafanikio. Siku ya kwanza alimkuta Rusia akiosha vyombo. Akapewa kiti na kukaa kando yake. Kabla hajazungumza chochote Rusia alianza maongezi ya vita kwa sauti ya huzuni. “Ndugu zetu wanakufa bure. Sijui wana hali gani watoto wachanga, wajawazito, wazee, vilema na wote wasiojiweza…”

Sauti yake yenye huruma na majonzi ikamfanya Sikamona ajihisi mwenye hatia kuongelea harusi. Hivyo, aliondoka pasi ya kusema lolote. Safari ya pili walikutana njiani. Kama kawaida Rusia alianzisha maongezi yaleyale ambayo yalikuwa katika midomo ya watu siku zote hizo. Alimweleza Sikamona kuwa amesikia wapelelezi kadhaa wenye mabomu walikuwa wamekamatwa wakiwa katika hatua za kutega mabomu ili kubomoa majengo kadhaa mjini Arusha na hapo Dodoma. Habari hizo zilifuatiwa na nyingine kadha wa kadha zinazosikitisha na kuchukiza.
 
14.
Sikamona alishindwa tena kutamka alichokusudia.



Wala si habari tu ambazo zilimfanya Sikamona ashindwe kutamka haja yake kwa Rusia, kwani nyingi kati ya alizoambiwa alikuwa amekwishazisikia kitambo. Wala si sauti yake yenye majonzi tu ambayo ilimzuia. Alikwishazisikia sauti nyingi zenye huzuni kuliko hiyo. Kilichomnyang’anya uwezo wa kutamka haja yake, hasa ilikuwa ile hali ya ukosefu wa tabasamu katika uso wa Rusia, tabasamu ambalo lilikuwa likimfariji awapo na huzuni, kumchangamsha achokapo, kumfurahisha hauzunikapo na hivyo kumfanya azungumze lolote analojisikia kulizungumza. Kwake lilikuwa kama nuru ambayo humtoa gizani. Hivyo, kukosekana kwa nuru hiyo ndiko kulikomfanya ayasahau maneno yote, pamoja na kuupoteza ulimi wake.

Hata hivyo, siku hiyo hakukubali kushindwa. Alikuwa amemfuata Rusia kazini kwa ajili hiyo. Rusia alimlaki kwa habari ambayo ilikuwa mpya kwake. “Nasikia serikali imewataka vijana kujitolea kwenda kupambana na hili joka. Mashujaa wengi wanajiandikisha…”

Sikamona hakumbuki kama alimjibu au la. Alichokumbuka ni jinsi alivyofanya haraka kutamka kilichomleta kabla hajashindwa nguvu. “Rusia nimekuja ili tupange lini tufunge ndoa.”

Pengine alisikia, pengine hakusikia. Lakini Sikamona alimsikia akiendelea kama anayezungumza peke yake. “Hadhi iliyoje kijana kujitolea kuilinda nchi yake. Ni mchango ambao hautasahauliwa na nchi hii kamwe. Kama







ningekuwa mtoto wa kiume…”

“Nijibu Rusia. Niambie lini unaona tufunge ndoa,” Sikamona alimkatiza na kusisitiza.

Ndipo Rusia alipomgeukia na kunong’ona kwa sauti ya wazi kabisa, “Sikia, twawezaje kuzungumzia harusi yetu wakati nchi nzima imo katika msiba?”

Maneno hayo kama hayakumkomesha Sikamona, basi yalimtosha. Alijihisi mwenye hatia kubwa kufikiria harusi hali ni kweli kabisa taifa lilikuwa katika msiba mkubwa. Watu wasio na hatia walikuwa wakifa na maiti zao kutupwa mapangoni, watoto wakitaabika kwa ukosefu wa wazazi, mali nyingi za thamani zikiharibika!

Aliyaepuka macho ya Rusia, kisha alianzisha maongezi mengine kwa kupoteza lengo, maongezi ambayo hayakupokelewa na Rusia kwani alionekana yuko maili nyingi nje ya chumba hicho.

Hayo na ule mwito wa taifa, hasa kwa vijana waliopitia jeshi la kujenga taifa, kwenda kujitolea kumwadhibu adui, kulimfanya ghafla asikie akipatwa na njaa ya kwenda huko. Maneno ya Rusia aliposema “Hadhi iliyoje kijana kujitolea… ni mchango usiosahaulika…” na… “twawezaje kuzungumzia harusi hali nchi imo katika msiba…” yalikua katika moyo wake kama kengele ambayo ilimwita kwenda vitani. Kengele hiyo ilizidiwa nguvu na lile tamko la Mwalimu Nyeyerere katika hotuba yake akisema… “Tulieni… Sikilizeni







muone vijana wetu watafanya nini…” vijana wanaotegemewa kama yeye si mmoja wao? Alijiuliza.

Ni hapo alipofikia uamuzi.

***

Alimkuta Rusia chumbani kwake, kainama akifanya jambo fulani katika sanduku lake la nguo. Sikamona aliingia kwa kumnyatia. Akamkaribia. Lakini kabla hajafanya chochote alichokusudia kufanya Rusia aligutuka na kumwona. Akalakiwa kwa lile tabasamu lake jipya, dhaifu lisilomsisimua.

“Vipi uko safarini?” “Kwa nini?”

“Naona unafungafunga”

“Ah! Niende wapi. Mimi ni mtu wa hapahapa tu.”

Walizungumza mengi wakibadilishana habari, matukio pamoja na kuambiana yote ambayo kila mmoja alidhani mwenzake angehitaji kujua.

Kisha…

“Wajua Rusia? Nimekuja kukuaga” Sikamona alisema baaadaye.

“Kuniaga! Waenda wapi?” “Uganda,”

“Uganda!”
 
15.
“Vitani.” akasita. “Kesho naondoka kwenda Monduli kupigwa msasa kwa muda mfupi. Baada







ya hapo ndipo nitaelekea mpakani.”

Rusia aliduwaa kwa muda, akimtazama kana kwamba ndio kwanza anamwona maishani mwake.

Ukimya wake ulimtisha Sikamona hata akajikuta akifoka ghafla bila ya kujua anachokifanya.

“Rusia. Sio kosa langu. Ni wajibu ulionilazimisha kuufanya hivyo. Sitakusahau kamwe Rusia. Nitaendelea kukukumbuka daima. Hata kama nikienda kaburini…”

Kama jibu lake Rusia aliinuka na kumkumbatia kwa nguvu. Kwa sauti ya mnong’ono Sikamona alimsikia Rusia akisema, “Usijali mpenzi wangu. Nenda na utarudi salama. Na utakaporudi utanikuta. Na ndipo nitakapokukabidhi zawadi yako maalumu, zawadi ya ushindi.”

Sikamona angependa ainue uso wake. Lakini kwa bahati mbaya hakuuona. Ulikuwa umefunikwa katika kifua chake. Hivyo, alichoambulia ni lile joto la Rusia na mguso wake. Mguso ambao ulimfariji pamoja na kumfanya ajisikie ushujaa ambao alikuwa hajapata kuusikia hapo mbeleni.

ALIPOKUWA mtoto mdogo, kabla hata ya kuanza shule, alikuwa hodari katika michezo yote iliyokuwa ikichezwa na watoto enzi hizo, michezo kama vile ya kukimbizana, mieleka, kutupa mawe na ile miti ambayo waliita mikuki, kujificha porini na kutafutana. Si yeye tu aliyeipenda, bali karibu vijana wote. Michezo ilitawala enzi yao na ilioana na mazingira yao. Hivyo, yeyote kati yao, ambaye aliikwepa wenzake walimtenga na kumdharau wakimwita ‘msichana.’

Ule mchezo wa kujificha na kukimbizana porini ndio uliokuwa maarufu kwao wote. Kila jioni walikwenda msituni na kumteua mmoja wao kama ‘simba’ huyo aligeuka simbamtu na kukabiliwa na jukumu la kuwakamata wengine. Sikamona ilimtukia mara chache sana kukamatwa katika msitu huo ambao aliuzoea hata nao ukamzoea. Alizifahamu vizuri njia na







vitengo vya kila aina ambavyo vilimwezesha kumwepuka ‘simba’ kadhalika, alikuwa hodari wa kujificha katikati ya vichaka vinavyotisha, juu ya miti ambayo matawi yake yalimwezesha kupanda upesiupesi kama nyani ama katika makorongo na mapango yaliyotapakaa huko na huko. Shule ilikuwa imemtenga na michezo hiyo. Hata hivyo, mchakamchaka na gwaride la kila asubuhi ilikuwa badala yake, hivyo, akaipenda shule na kuithamini vilivyo, jambo ambalo lilimfanya achaguliwe kuwa kiranja mkuu akiwa darasa la tano tu na kiranja wa taaluma ya michezo huko sekondari. Kama si kumaliza shule basi ni umri ambao ulimfanya aachane na michezo hiyo kabisa. Akawa akiamka asubuhi na kujikokota kivivu hadi ofisini ambako alishinda kakaa kitini, mafaili yakimtazama kifuani siku zikaja na kwenda.

Halafu likaja Jeshi la Kujenga Taifa. Huko, kwa kiasi fulani, alirudia utoto wake, ingawa kwa njia ya kikubwa zaidi. Licha ya furaha ya kucheza maporini na milimani, alipata fursa ya kujifunza silaha, mbinu za kivita na ukakamavu ambao ulirandana na yale mafunzo ya kuwa ari ya ujenzi wa taifa kiuchumi.

Lakini hayo pia yalichukua muda mfupi tu. Mwaka mmoja baadaye alirejea tena katika maisha yaleyale, maisha ya kitanda na ofisi, maisha ambayo kukimbia mchakamchaka mitaani watu wangekwita mwendawazimu na kupiga gwaride uwani, jirani wangeishuku akili yake.
 
16.
***

Leo alikuwemo tena katika michezo hiyo akijifunza na kujikumbusha yote yale ambayo aliyapitia jeshini na utotoni. Lakini safari hii haikuchezwa kwa ajili ya kujifurahisha, kulazimishwa na umri pamoja na mazingira wala kwa sababu ya kujiandaa tu. Ilikuwa maalumu kwa ajili ya hali halisi ambayo ilikuwa usoni mwa kila mwananchi, maalumu kwa ajili ya kuyaokoa maisha ya wananchi na kurejesha hadhi ya nchi. Hivyo, kama wengine, Sikamona alijifunza au kurudia mafunzo ya silaha na ukakamavu kwa juhudi zote.

Kama kawaida, penye wengi pana mengi. Hivyo, wazembe hawakukosekana ingawa walikuwa wachache mno. Hao, ama kwa ajili ya kutopitia michezo hiyo utotoni, au kwa ajili ya uzembe tu, walilazimika kutoroka ama kuombwa na viongozi warejee majumbani na kuwapisha wenye afya. Ilimshangaza sana Sikamona, mtu mzima kushindwa na jambo ambalo mtu mzima mwingine analitenda.

Ni katika kambi hii ambako Sikamona alikutana na Mdoe. Waliwahi kukutana zamani walipokuwa wanafunzi wa shule ya msingi. Baaada ya kumaliza shule hiyo kila mmoja alizama katika upande tofauti wa dunia, akifuata mkondo wa maisha ulikomwelekeza.

Kumbe mkondo wa Sikamona ulikuwa umemtiririsha hadi katika ukumbi wenye heri na matumaini kuliko mwenzake, elimu ya sekondari,
 
Cookies are required to use this site. You must accept them to continue using the site. Learn more…