Zawadi Ya Ushindi

Zawadi Ya Ushindi

17.
kazi na maisha mema ni baadhi ya heri hizo; si Mdoe ambaye mkondo huohuo ulimsukuma hadi kumdidimiza katika bahari yenye kila aina ya dhiki, majonzi na machungu yasiyo na dalili zozote kukatika.

Alifiwa na mama yake mwaka wa pili tu tangu alipomaliza masomo ya msingi. Halafu, akaangukia katika hifadhi ya mama wa kambo ambaye alikuwa na kila sifa ya u mama wa kambo. Akamlea kwa taabu na kumtunza kwa matusi, masimango na kutumikishwa kitumwa huku akila kwa taabu. Hata hivyo, Mdoe aliendelea kuvumilia kwa kujikumbusha methali inayodai eti, “Baada ya dhiki faraja.” Akawa akiisubiri kwa njaa kubwa siku hiyo, siku ambayo angefarijika na kuneemeka kama wengine.

Faraja aliyoiambulia ilikuwa ile ya kushuhudia kifo cha baba yake kikitokea kwa njia ya ajabuajabu. Alikufa usingizini. Jirani walidai amerogwa hali minong’ono ikisema aliuawa na mke wake ambaye alikusudia kuiba urithi, urithi ambao haukuwa wa haja machoni mwa Mdoe.

Baada ya hapo Mdoe akawa huru katika dunia huru, uhuru uliomtisha na kumbabaisha nusura umtie kichaa, hali ambayo ilimfanya hata adiriki kuutamani ule utumwa wa mama yake wa kambo zaidi ya uhuru huu ambao ulimlazimisha kujitegemea, si kwa chakula na mavazi tu, bali pamoja na mawazo pia.

Hali ambayo iliizeesha mwili na akili zake kabla ya wakati. Akajitoma katika mojawapo ya vijiji vya







kwao Sumbawanga ambako alijijengea kijumba chake na kujilimia mashamba ya chakula. Ni hapo ambapo mawazo yenye matumaini mapya yalianza kuchipua tena katika fikra zake, kwamba huenda angeneemeka na kuwa mtu kama watu wengine, mtu asiye na hofu ya uhuru wala mashaka ya kuishi.

Halafu likazuka hili janga la vita. Likafuatwa na ule mwito wa taifa wa kujitolea kwenda kumwadhibu adui, “Mwito usiopingika” kama alivyowahi kuuita mbele ya Sikamona. Akayaacha yote aliyokuwanayo mkononi na rohoni na kuja kujiunga katika kikosi hiki kilichokuwa kikijiandaa kuelekea katika uwanja wa mapambano.

Sikamona alikuwa amehiari kujitoa mhanga, lakini bado ilimshangaza sana kila alipowaza juu ya watu kama Mdoe na hatua zao za kujitoa. Mara kwa mara alijiuliza kwa nini watu kama hao waliamua hivyo wakati kila mmoja wao alifahamu dhahiri kuwa kitendo hicho ni cha kufa na kupona, kitendo ambacho ni cha kumtoa mtu katika tumaini halisi la maisha yake. Kwa nini? Ushujaa? Labda. Aliwaza. Lakini ushujaa ni nini? Na shujaa ni nani? Mdoe ni shujaa?
 
18.
Hakupata majibu. Badala yake aligundua tu kiasi gani alikuwa hamwelewi rafiki yake Mdoe, pamoja na watu wengine. Pengine ni vigumu mwanadamu kuufahamu undani wa mwanadamu mwingine, kama ilivyokuwa kwake na Mdoe? Ingawa walikuwa wameishi pamoja miaka saba, wakisoma pamoja, kucheza pamoja, kushirikiana







na kugombana, kuchokozana na kupatana n.k lakini bado alikuwa hamwelewi hata kidogo. Hakuifahamu siri iliyofichika katika nafsi yake, siri ambayo ilikuwa imemnyang’anya hofu ya kifokiasi cha kumsukuma kuyanadi maisha yake.

Nyakati kama hizo ilimjia kujiwazia yeye binafsi pia. Ni kipi hasa kilichokuwa kimemtoa hofu ya kifo? Yeye ni shujaa? Ushujaa ni nini? Au inatosha kuwa aliamua kupambana kwa ajili ya uchungu na aibu ya kuvamiwa? Mbona walikuwepo wengi ambao hawakuwa tayari kujitolea? Wengi hata baadhi ya wale ambao wameshuhudia jamaa zao wakichinjwa kama mbuzi na kuzikwa kama mbwa! Yeye ni shujaa? Alijiuliza tena na tena kiasi kwamba si kwamba hakuelewa watu kama Mdoe tu, bali pia hakuwa hata na uwezo wa kujielewa yeye mwenyewe.
 
19.
sasa alikuwa tayari uwanja wa mapambano. Tayari. Tayari kabisa. Tayari kwa lolote. Tayari kufa, tayari kuua.

Giza lilikuwa likikaribia kuimiliki nchi nzima. Nuru hafifu iliyobakia ilimwezesha kuona umbali wa mita chache tu toka katika handaki lake. Alikuwa amelala ndani ya handaki hilo, mtutu wa bunduki lake ukielekea upande ambao uliaminika adui alikuweko. Alikuwa ameipakata barabara silaha yake, tayari kuipa uhai wakati ambao amri ingetolewa. Mavazi yake ya mabaka na kofia yenye muundo wa kichaka vilimfanya awe kama kichaka cheusi kilichoota pangoni.

Aliendelea kutulia, ukimya mwingi ukiwa umetapakaa anga zima, ukimya huo wa kutisha pamoja na kimya kingi ambacho kilitanda huko na huko vilimfanya ajikumbushe jambo moja







lisimtawale. Hofu. Naam, hakuipenda hofu. Kwa ujumla, aliichukia akijua kuwa kuna ujirani mkubwa kati ya hofu na mauti. Hata hivyo, uwezo kamili wa kuishinda ulikuwa ukimtokea kwa vipindi tu. Si sasa ambapo giza lilimfunika na dunia kutulia kama inayoomboleza kifo chake. Si sasa ambapo alikuwa na bunduki mkononi hajui adui yu wapi na iwapo angeweza kweli kumjua adui huyo kabla hajafa yeye. Si sasa wakati ambapo bila shaka jamaa zake huko nyumbani walikuwa wakilia na pengine hata kuomboleza juu yake.

Ni hofu hiyo ambayo ilimrejesha katika yale maswali ambayo siku hizi yalitawala akili yake na kumfanya awe nayo akilini kama wimbo usio na msaidizi, wimbo wa bubu na kiziwi. Kwamba ni kweli kuwa sasa yuko mstari wa mbele! Mbele ya nchi na taifa zima! Mbele ya wazalendo wote, tayari kuua, tayari kufa kwa ajili yao! Ni kweli au ndoto! Kama ni kweli kujinadi nafsi yake kiasi hiki ametumia busara kweli? Swali ambalo alikuwa akijitahidi kulifuta akilini kwa kujihisi mwenye hatia kwa mawazo hayo duni, pamoja na kujikumbusha ujana wake, afya yake na wajibu wake kwa taifa.

Lakini, kadhalika, hayo pia yalikuwa yakimzulia swali jingine. Wajibu ni nini? Hilo lilifuatiwa na lingine. Yeye ni nani na wajibu wake ni upi? Taifa litamlipa nini kwa kumwaga damu yake? Na kwa nini iwe yeye? Kuna maelfu mangapi ya vijana ambao walikuwa wakizurura mitaani?







Labda amekuwa mjinga kuamua kufanya hivyo? La, alijikanusha hima. Ni kufuru kubwa kuwaza hivyo. Yeye ni shujaa, shujaa miongoni mwa mashujaa. Nchi inamtegemea na kuwategemea wote wenye ari kama yake.

Lakini ni kweli yeye ni shujaa? Ushujaa ni nini? Na nini tuzo ya shujaa iwapo atakufa na kuoza kama mzoga? Manufaa yake ni nini? Maswali hayo yaliendelea kuzuka akilini mwake na kuota mizizi. Yalianza tangu usiku ule ambao alijikuta akiparamia lori na kuanza safari ya kuja hapa alipo.

Ulikuwa usiku wenye giza zito kuliko hili la leo, giza la kutisha, giza ambalo lingeweza kuwa ahera iwapo nuru ya taa za umeme katika kambi yao zisingekuwepo na kuunajisi unene wake.

Gari lilikuwa limesimama barabarani likiwasubiri. Wakawa wakiliendea mmoja baada ya mwingine kila mmoja akiwa kamili kwa hali na mali na bunduki zikiwa mikononi, mafurushi makubwa yenye mavazi na mahitaji mengine migongoni. Kadhalika, mioyoni walikuwa wameivaa ile hali ya kusikia furaha na utukufu, hali ambayo humpata yeyote anayefahamu kuwa uhai wake ni tegemeo pekee la wengine.
 
20.
Hata hivyo, pengine hii haikuwa sare katika mioyo yao wote, Sikamona akiwa mfano. Yeye japo alifurahi na kujisifu kimoyomoyo lakini bado hofu haikukoma kupenya katika ari hiyo na hivyo kumfanya awe na mashakamashaka. Wakati wakihutubiwa ile hotuba ya mwisho ambayo







ilikuwa ndefu yenye maneno mengi ndani ya neno moja tu, “Tunawategemeeni” yeye alijisikia kama anayesomewa sala ya mwisho kaburini. Wakati akipanda lori hili alijiona kama anayeingia katika jeneza. Gari lilipoanza kuondoka na kujitoma gizani alihisi kaanza ile safari ya mwisho, safari ya kuzimu. Alitulia akitetemeka kindanindani, macho kayakaza kutazama mandhari ya nchi yake, kwa mara ya mwisho.

Alikuwa akiilinganisha hali hii na ile aliyowahi kuiona miaka michache iliyopita, pindi alipofiwa na mdogo wake. Wakati huo alikuwa bado mtoto, alipendana sana na nduguye huyo, kwa jina Marubu. Kisha, usiku mmoja aliamshwa usingizini kwa ndoto mbili mbaya zinazotisha. Mkono wake wa kushoto ulikuwa umelala juu ya mgongo wa Marubu hali wa kulia kaufanya mto. Kitisho cha jinamizi hilo kilimfanya atetemeke na kutweta. Hivyo, akaanza kumwamsha Marubu kwa kumsuka polepole. Marubu hakuamka. Alimsukasuka kwa muda mrefu bila mafanikio. Akashangaa. Mwisho alimsukuma kwa hasira. Marubu aliviringika kama gogo na kuanguka uvunguni. Lakini bado hakuamka. Hali hiyo ilimjaza Sikamona hofu mpya. Akafanya haraka kuwaamsha wazazi wake ambao baada ya kumtazama mara moja waliangua kilio, kilio ambacho kilithibitisha kuwa Marubu asingeamka tena. Siku ya pili walimshonea sanda na kumlaza katika jeneza. Kisha, wakamchimbia kaburi na kumzika. Sikamona alilia sana akitegemea machozi yamrudishe ndugu yake. Lakini haikutokea.







Akaendelea kulia ingawa si kwa machozi bali majonzi na maombolezo, kilio ambacho kilifufuka kuwa machozi kila alipokumbuka na kuhisi akiona jeneza la Marubu likididimizwa kaburini.

Ndio hali ambayo Sikamona aliihisi wakati alipokuwa anapanda na kuelekea vitani, hali ya kujihisi kamkumbatia Marubu na kushonewa pamoja katika sanda, kupakiwa katika jeneza na hatimaye kuelekezwa kaburini. Na ni hali hiyo ambayo ilimjaza hofu, hofu ya kutisha na kutatanisha, hofu ambayo ilimlazimisha kujiuliza maswali ambayo aliamini ni ya kike kwa wakati kama huo.

Alijisikia kupiga uyowe wa hofu, aruke toka katika jeneza hilo na kujitoma porini, amwepuke Marubu na wafu wengine. Lakini hakufanya hivyo. Hakufanya asilani. Polepole kelele, shangwe na vigelegele toka kwa wenzake viliurejesha moyo na roho yake katika ukumbi wa furaha na utukufu. Akajikuta mshirika katika vigelegele na nyimbo za kuukashifu uvamizi na hekima za mvamizi. Akaupenda sana ule wimbo uliomfafanua Amini kama “mroho” askari zake “Malaya”
 
21.
“Vijana twendeni. Wote twendeni. Tukamtoe nchini mroho wa madaraka.

Tumtoe, tumtoe mroho mwenye njaa ya ukubwa. Tukawatoe nchini Malaya wa Amini.

Tukawatoe, tukawatoe, Malaya, makahaba wa Amini.”







Huo pamoja na nyingine kadha wa kadha zilimfanya abadilike kabisa moyoni na kumaliza safari hali akijiona kama aendaye harusini badala ya vitani.

Ari hiyo iligeuka hasira mara tu alipowasili Kagera na kuushuhudia unyama wa Amini na askari wake katika nchi yao. Alilakiwa na magofu ambayo juzi tu zilikuwa nyumba bora za thamani. Sasa zilikuwa zimechomwa na kubomolewa kwa vifaru, kung’olewa milango na madirisha pamoja na kila chenye thamani.

Si hayo tu, mashamba ya mibuni, migomba na miwa yalikuwa yamechomwa moto pamoja na kuvurugwa hata yakawa kama uwanja ambao ulitumiwa kucheza ngoma ya kikatili. Hayo yalikuwa pamoja na kuharibiwa viwanda, hospitali, shule, barabara na kila kitu ambacho askari hao walifahamu kuwa kina manufaa ama kilimgharimu mwanadamu muda na fedha kukitengeneza. Ukatili ulioje huu? Hasara iliyoje? Alijiuliza huku akitikisa kichwa kwa uchungu.

Eneo hili walilokuwa wamefikia ni lile la Kyaka, ambalo lilikuwa limetekwa na majeshi ya Idd Amini. Kikosi cha Sikamona kilikuwa kimefika kuungana na vikosi vilivyotangulia. Kwa bahati mbaya au nzuri walikuta kazi ya kuyaondoa majeshi hayo ya Amini imekwishatekelezwa. Walichoambulia ni harufu ya vita na mabaki yake. Hata hivyo, walitegemea mashambulizi wakati wowote, na hivyo, walilazimika kuwa makini wakati wote.







Jioni moja Sikamona alitoka kwenda kutembeatembea katika mashamba haya ambayo yaliharibiwa na ukatili wa hao wakatili. Alijipenyeza katika vichaka na migomba iliyosalia. Kisha, macho yake yalivutwa na kitu fulani ambacho aliona kimelala katika kimoja cha vichaka vilivyonusurika. Alikisogelea na kutazama kwa makini. Kelele za hofu au uchungu zingeweza kumtoka. Hakujua kwa nini alifanikiwa kujizuia asifanye hivyo. Badala yake alijikuta akisaga meno na kufunga ngumi kwa nguvu. Alikuwa akiushuhudia unyama wa Amini na askari wake kwa macho yake mwenyewe, unyama wao kwa viumbe wa Mungu. Zile sifa zote ambazo alizisikia kwa maneno sasa alizisadiki baada ya kuona hiki alichokuwa akikiona, maiti ya mwanamke! Ilikuwa imelazwa chali juu ya nyasi. Ukatili si tu kule kumwua, bali njia ambazo zilitumika. Yaonekana alikuwa hakufa kwa silaha ya aina yoyote. Alikufa kwa vidole. Macho yake yote mawili yalikuwa yameng’olewa, ulimi umevutwa nje, sehemu za siri zimetatuliwa na vidole vya mikono na miguu kuvunjwa. Kando yake kitoto kichanga kilikuwa kimelala, maiti vilevile. Hiki ilionyesha kilifariki kwa njaa na kilio kwa kumpoteza mama ghafla.

Sikamona alizitazama maiti hizo kwa muda mrefu. Hasira zikampanda na kisasi kukamilika katika nafsi yake. Haistahimiliki… haivumiliki. Alifoka kimoyomoyo. Ni hapo ambapo alijikuta akijilisha kiapo upya, kiapo cha rohoni kabisa, kwamba asingesita kujitolea kikamilifu kumwadhibu huyu ambaye anafanya vitendo vya







aina hii.

Aliporejea hakujua kuwa alikuwa ametokwa na machozi hadi alipofika mbele ya Mdoe ambaye alikuwa akimsubiri mbele ya handaki lake. “Una nini?” Mdoe alimwuliza kwa mshangao.

“Ninalia!” sikamona pia alishangaa. Kisha, “Ah! Nadhani ni upepo tu.” Alimdanganya.

“Upepo! Tangu lini?” Hakumjibu.
 
22.
ILIENDELEA kutulia katika handaki lake akifanya kila juhudi kuushinda usingizi ambao sasa ulimnyemelea. Angewezaje kualala wakati walikwishaambiwa kuwa

adui hawako mbali na walitarajiwa kupita eneo hilo? Giza ambalo lilikwishaimiliki nchi nzima lilimnyima uwezo wa kuona chochote, hali ambayo ilimfanya aone kama vivuli vinavyotembea na hivyo kurejewa na hofu mara kwa mara. Hakuchoka kupambana na hofu hiyo.

Ukimya ambao ulikuwa umetanda ulinajisiwa na sauti ya bundi ambayo ilianza kulia ghafla. Sikamona alimsikiliza bundi huyo kwa muda, kisha akatabasamu. Alikumbuka ile imani ya kabila lake, kwamba bundi ni ndege wa wachawi na aliapo uwa anabashiri maafa, imani ambayo ilidumu katika nafsi yake hadi mwalimu wake alipoipotosha kwa kuwaambia kwama bundi







ni ndege kama wengine na kwamba imani hiyo ni ya kale isiyotofautiana na zile mila za mtoto kutokula mayai ama mama mjamzito kuambiwa akila samaki asiye na magamba angezaa zeruzeru. Labda ni kweli kuwa imani hiyo ilikuwa duni iliyoachwa nyuma na wakati. Lakini mbona bundi huyu analia hapa, saa hizi, ambazo maafa yako usoni na mashaka yakimchungulia? Mara ngapi mila za kale zimetokea kuwa tunu njema kwa maisha ya kileo? Alinong’ona kimoyomoyo.

Hakuyamaliza mawazo yake. Ile ishara waliyokuwa wakiisubiri ilisikika ghafla. Ikamfanya aduwae kwa muda huku miguu ikilegea na mwili mzima kumtetemeka. Kisha, alizikusanya nguvu zake. Akafanya hima kuiandaa bunduki yake, huku mgongoni akijifunga furushi lake la vifaa.

Walitulia kwa muda ambao sikamona aliuona mrefu kupindukia. Muda ambao ulimrejesha katika hofu. Mikono yake ilitoa jasho huku mwili ukimtetemeka. Alijisikia kwenda haja lakini hakuthubutu. Wala hakujua kama haja hiyo ingemtoka. “…. Tulieni… sikilizeni muone vijana wetu watafanya nini…” yalimrudia maneno ya Mwalimu. Yakamfanya ajisikie aibu na hatia kwa hofu yake, kisha “…Utarudi salama…. Utanikuta… Nikukabidhi zawadi ya Ushindi…” hayo yaliambatana na hali ya kuhisi akiuona uso wa Rusia ukimtazama na kushuhudia alivyokuwa akitweta hovyo. Aibu ikamzidi. Yeye ni kijana. Ujana wake unategemewa sana dakika hii kwa manufaa ya nchi nzima. Vipi aanze hofu na kukata
 
23.
tamaa! La, asingeruhusu uzembe kama huo. Akajikaza kiume na kuahidi na kujikumbusha tena, kwamba ilimlazimu awe imara.

Wakati huo mapambano yalikaribia. Walisubiri kwa dakika kama kumi tu, mara wakawaona maadui waliokuwa wakiwajia kwa kundi kubwa kama la ngombe waendao malishoni. Akainua bunduki yake na kuielekeza katika kundi hilo tayari kuifyatua. Lakini alijisahihisha upesi alipokumbuka kuwa alikuwa hajapewa amri ya kufanya hivyo. Akajilazimisha kutulia. Macho yake kayakaza kuwatazama adui ambao walizidi kuwakaribia.

Kamanda ana nini? Amepatwa na jambo gani hata aache adui kutufikia bila ya kufanya lolote? Sikamona alijiuliza kwa hofu na mshangao.

Halafu, ishara ikatolewa. Ikafuatiwa na ngurumo ya mlio wa bunduki na mlindimo wa risasi ambazo zilimiminwa katika genge la maadui. Maadui hao, ambao bila shaka hawakujua kuwa mbele yao kuna mtego, waliduwaa kwa muda kwa ajili ya mshindo wa wingi wa risasi ambazo zilimiminika toka kila upande. Kisha, kama walivyo askari wote waliofundishwa walijitupa ardhini ghafla na kuanza kupigana. Si mapigano ya kuteka nchi tena, bali kujaribu kuziokoa roho zao.

Ni hapo ilipofuata mvua ya ajabu, mvua ambayo ilikuwa na ngurumo za kutisha, pamoja na vilio vya watu waliokuwa wakihanguka huku na huko.

Haikuchukua muda mrefu kama alivyotegemea







Sikamona. Baada ya dakika kadhaa hali ilirudi kama kawaida. Zile kelele, mingurumo na vilio vilipoa ghafla na nafasi yake kumezwa na ukimya wa hali ya juu. Kama wengine wote, macho ya Sikamona yalitulia juu ya mizoga iliyotapakaa huku na huko pamoja na miili ambayo ilikuwa ikitapatapa kwa maumivu na kukata roho. Miili ya adui.

“Hee, kilikuwa kipigo chema au sio?” Mtu mmoja alitamka. “Kipigo halali yake: chastahili kupewa jina. Kipigo cha kumtoa nyoka pangoni au sio?”

Si kwamba hakumjibu tu, hali kadhalika hakumtazama. Hivyo, hakujua ni nani ambaye alimsemesha. Mawazo yake yalikuwa yamepaa na kutua katika dunia nyingine, dunia yenye huruma na uchungu. Hali hiyo ilimtokea baada ya kuutazama kitambo mwili wa adui mmoja na kushuhudia mateso aliyoyapata. Si hayo tu, alikuwa pia amesikia hata sauti yake ikikoroma na kudai “I am dying for nothing.”

Pengine ni kweli alikuwa akifa bila sababu. Sikamona alijiuliza akitembea polepole toka nje ya umati huo wa mzoga. Bila ya sababu! Kwa vipi? Alilazimishwa kuja vitani? Mtu anawezaje kulazimishwa kufanya jambo kubwa kama hilo?

Hakuwahi kupata muda wa kulijibu swali lake. Kelele za ghafla zilisikika. Alipogeuka aliiona maiti moja ikiinuka na kukurupuka mbio. Hakuwa peke yake, askari mwingine alikuwa akimkimbila. Walikuwa wakimjia. Akaharakisha kuielekeza bunduki yake kifuani mwa adui huyo huku







akifoka, “Simama.” Kabla hajafoka tena mkimbizi huyo alijikwaa na kuanguka chini. Askari aliyekuwa akimkimbilia alimfikia na kumchoma sime mgongoni.

“La, la, acha!” Sikamona alifoka huku akimkimbilia. Alimvuta askari mwenzake mgongoni na kufoka tena. Mwache…”

Askari huyo akainua uso kutazama. Ikamshangaza kukuta si mwingine zaidi ya Mdoe ambaye alimtazama kwa muda. Kisha, kama aliyetishwa na kitu fulani katika macho yake, akafanya haraka kuichomoa sime yake toka katika mwili wa adui huyo na kuondoka zake.

Sikamona akainama kumtazama mateka huyo. Alikuwa ametapakaa damu mwili mzima. Damu ya mtu ilikuwa ikimwagika hadharani. Kwa nini? Alijiuliza. Yeye hakujua kwa nini anakufa? Aliendelea kujiuliza. Hakujua ajipe jibu lipi, hakujua awaze nini. Akayaepuka macho ya mtu huyo na kujivuta tena nje ya uwanja huku askari wenzake wakisogea na kumthibiti adui ambaye aliendelea kutapatapa kama anayekata roho.
 
24.
NDIO nilizaliwa katika nyumba masikini. Labda tuseme ilikuwa na umasikini zaidi ya masikini wengi waliotapakaa huko na huko katika kata yetu, umasikini unaotisha. Ndio, kwani si kwamba ulinifanya nitembee matako wazi tu, bali pia uliniwezesha kuona viraka vilivyoshonana nyuma ya suruali ya baba, wala si kwamba ulitufanya tuishi kwa dhiki tu bali pamoja na kutulazimisha kumfungia baba chooni kila wakusanya kodi walipokuwa wakipita kijijini petu. Ni mengi mno ambayo yalitupata. Mengi kupindukia. Yanatosha kabisa kumfanya mtu aamini kuwa dunia, kama si jehanamu, ni gereza. Sijui kwa nini hali hiyo ilituzidi mno sisi kuliko jirani zetu. Labda ilikuwa kwa ajili ya malazi ya mama mara kwa mara. Ama ilitokana na mapenzi ya baba kwa pombe. Sijui! Kitu nijuacho ni kimoja, kwamba pamoja na umasikini wote huo nilikuwa

na furaha.”







Kiasi Sikamona alimwogopa Mdoe. Akamtazama usoni na kushangaa macho yake yalivyokuwa yakichezacheza na kutoa nuru kali iliyodhihirisha uchungu na simanzi.

“Naam, furaha tosha kabisa. Sikuwa na wasiwasi wowote wa maisha. Sikuuchukia umasikini wala sikupata maumivu yake. Niliyazoea yote. Pengine hali hiyo ilitokana na kule kuwa mmoja miongoni mwa wengi wenye hali kama yetu. Si kuna mtu aliyewahi kusema, kifo cha wengi harusi?” basi mimi pia nilikuwa harusini, katikati ya kundi linalosheherekea, nikicheza ngoma waliyokuwa wakiicheza na kuimba nyimbo walizokuwa wakiziimba, zaidi ya yote hayo nilikuwa na mpenzi.”

Sasa alikuwa kama anayeota na kuzungumza katika ndoto yake hiyo aliposema, “Msichana mzuri mwenye heshima na adabu. Umbo lake lilikuwa na kila ambacho mwanamume anakihitaji. Mwenendo wake ulikamilisha yote ambayo ndoa inayataka. Alikuwa kama nuru gizani, maji jangwani, shibe njaani na faraja matangani. Si kwangu tu, bali kwa kila aliyemwona. Kila mpita njia aliyetazamana naye hakukosa kutazamana naye tena usingizini. Na kila aliyemgusa hakukosa kujikuta akimkumbatia katika ndoto zake. Naam, alikuwa ua la roho, ua lililochanua. Lakini alikuwa wangu. Wangu peke yangu.” Akameza mate kulainisha koo kabla hajaendelea.

“Mapenzi yalianza kama ndoto, ni kweli kuwa alikuwa jirani yangu. Ni kweli pia kuwa alikuwa na hali kama yangu, mtoto wa masikini kama baba yangu.
 
25.

na hali kama yangu, mtoto wa masikini kama baba yangu. Lakini si hiyo sababu ya mapenzi yetu. Ni kitu baki kabisa. Kitu ambacho mpaka leo kinanifanya nishindwe kukifafanua. Ninachojua ni kwamba kitu hicho kilinyang’anya starehe ilipokaa bila ya kumwona, kikanifanya mgonjwa niliposhinda pasi ya kuisikia sauti yake. Nilipojikakamua na kumweleza habari hiyo ikanishangaza aliponifahamisha naye alikuwa na shida kama zangu. Halafu nikaelewa. Yalikuwa mapenzi. Tukawa tukiandamana naye huku na huko. Sikuyaonea aibu matako yangu ambayo yalikuwa wazi kama ambavyo yeye pia hakujali kuvaa gauni lililotatuka kifuani mbele yangu. Mavazi pekee ambayo yangefaa kuitwa mavazi, zilikuwa sare zetu za shule. Tulipofikia umri wa kutosha, matiti yakiwa kamili kifuani mwake, wima kama yanayodhihaki, nilimtajia ndoa. Akanicheka na kunishauri nisubiri tumalize shule.”

“Wakati huo uhuru ulikuwa mikononi mwa mtu mweupe. Ingawa nilikuwa mdogo, lakini nilihisi kasoro katika uhuru huo. Hayo yalinijia baada ya kumsikia baba akifoka kila baada ya kulewa. ‘Tumejidanganya… Tumejidanganya… Uhuru nini kama kodi iko palepale? Uhuru nini kama umasikini uko palepale?’ Ndio nilihisi kasoro kwani nilikuwa nimeshuhudia watu walivyoshambulia kwa nguvu usiku huo wa uhuru. Nikadhani kitakachofuata si kidogo. Lakini sikukiona. Hata hivyo, niliamini umasikini wa baba ulisababishwa na pombe. Hivyo, nikaiepuka na kuapa kwamba







nisingeinywa kamwe. Mara nikaanza kutaabika mawazoni ningepata wapi mahari ambayo ingeniwezesha kumwoa Maida, mpenzi wangu. Huo ukawa mwanzo wa kupotelewa na furaha yangu. Hata hivyo, nilijifariji kila nilipokadiria uzito wa penzi kati yetu. Lazima angekuwa radhi tutoroke tukaishi kokote ambako hakuna ndugu yake wa kudai mahari wala yangu wa kunilaumu. Nikawa nikisubiri kwa kiu kubwa siku ambayo ingenitukia kuwa naye kitanda kimoja nikimkumbatia na kumbusu mwili mzima.”

“Sio kwamba nilikuwa sijamkumbatia. Nilimkumbatia sana, huku nikimshika na kumgusa nipendavyo, nikifarijika na kuburudika nilivyoweza. Lakini ilikuwa ndotoni tu. Njaa yangu ilikuwa lini ndoto hizo kuondokea kuwa kweli.

Sikamona alimwona Mdoe alivyoyaepuka macho yake na kutazama ardhini aliposema, “Haikutokea. Haikutokea ndugu yangu. Maida kwangu alikuwa kama ndoto tu. Ndio, ndoto nzuri na ya kupendeza. Lakini ndoto. Hayo niliyagundua baada ya kumaliza shule. Nilimkumbusha mara kwa mara juu ya ndoa lakini alicheka tu na kuniambia “Tusubiri.” Nikasubiri hadi siku ile ambayo nilikuta… kwao kuna sherehe kubwa. Vipi? Nikauliza.

“Kuna harusi.”

“Ya nani?” Niliuliza kwa wasiwasi. “Maida.”

“Ameolewa!”







“Ndio. Anaolewa na mwalimu wake anaye…”

Sikuweza kumsikiliza zaidi. Sikuwa na hali. Nilijikuta nikipata maradhi ya ghafla. Nikaanguka kwa kizunguzungu. Simjui msamaria ambaye alinizoa na kunipeleka nyumbani juu ya kitanda changu cha kamba ambacho hakikuwa na shuka ya pili. Nijiue? Au nimwue Maida pamoja na mume wake! Nilijiuliza niliporudiwa na fahamu. Kisha, nilipokea barua yake. Ilikuwa na machache yayoeleweka. ‘…kama kweli ulinipenda Mdoe, hutanilaumu kwa uamuzi wangu. Nilijua usingepata mahari. Kadhalika, maisha yetu yangekuwa mabaya mno. Umasikini ungepotosha starehe katika ndoa yetu…’ Ni hapo nilipogundua tusi la masikini. Nikagundua unyonge wa masikini. Hapendezi, hapendeki… ni hapo furaha yangu ilipoingia dosari.”
 
26.
“Kabla sijafahamu kama ningemchukulia Maida hatua ipi, kikatokea kifo cha mama yangu. Kikadhulumu nusu ya furaha na matumaini niliyobakia nayo. Halafu baba akafa. Alikuwa kiungo cha mwisho kati yangu na furaha, matumaini na hamu ya maisha. Nikajikuta nimetua katika dunia ya dhiki, kebehi na misukosuko. Dunia ambayo si kwamba ilininyima chakula na mavazi tu, bali pamoja na kunifanya niwe kichekesho hata kwa mafukara wenzangu. Unyonge ulionijia nusura ungenitia wazimu.”

“Siku moja nilipokuwa nikipitapita katika mitaa ya vichochoroni, nilipita mbele ya kilabu cha pombe. Nikachungulia ndani. Nilimwona







kijana mmoja mwenya hali kama yangu” shati lililotatuka mgongoni, viatu vya magurudumu na suruali yenye viraka visivyokadirika. Alikuwa amelewa barabara na sasa hana habari ingine zaidi ya kucheza na kucheka kwa furaha.”

“Alinivutia kijana huyo. Si kwa ajili ya mchezo wake wala ulevi wake. Ilikuwa kwa ajili ya furaha aliyokuwa nayo. Nimekwishakuambia kuwa niliishiwa na matumaini yote ya maisha mema? Lakini nilichohitaji ni furaha. Nilijua kuhuzunika kwangu kusingenipa mahitaji yangu. Nilihitaji kufurahi ili niendapo kaburini nife mwenye furaha. Furaha ilikuwemo katika ulevi, ulevi ambao uletwa na pombe. Pombe… pombe… pombe… nikajifunza kuinywa pombe. kila senti yangu ambayo niliipata kwa kibarua kigumu ama kuiokota kwa kudra za Mwenyezi Mungu niliitupia katika mkoba wa muuza pombe. Nikawa mlevi mashuhuri mwenye kila sifa ya unywaji pombe, mapenzi kwa kazi hiyo na zaidi ya yote mwenye furaha. Niliyafurahia maisha. Na nikasahau kabisa kudhani kuwa ulevi wa baba ndio uliokuwa kisa cha umasikini wetu. Badala yake niligundua kuwa alijua alichokuwa akikifanya. Ni pombe ambayo ilimsahaulisha uchungu wa kukosa shamba, majonzi ya kutokuwa na kazi na msiba wa kuniona mimi nikifuata mkondo wake. Pombe tu, hakuna zaidi.”

Nzi ambaye alikuwa akimtambaa usoni alimrukia mdomoni. Akamtema na kumponda kwa dole gumba. Sikamona alitamani kucheka.







Lakini kicheko kikagoma kumtoka.

“Hata hivyo, bwana sidhani kama kweli naweza kuiita hali hiyo kuwa ni furaha, kwani furaha ilinitokea kwa muda mfupi tu, muda ule ambao pombe ilikuwa ikielea kichwani mwangu na kunifanya niwe kama ninayeelea katika bahari iliyochafuka. Nyakati ambazo sikupata nilijikuta nikijuta kama kawaida. Nilijuta kuzaliwa, nikajuta kuishi. Nikaanza kumtafuta rafiki mwingine, rafiki ambaye angenitoa katika hili gereza ambalo ni baadhi tu wanaoliita dunia, kifo. Naam, ilikuwa ndio dawa pekee.”

Alisita tena. Safari hii ilikuwa kwa ajili ya kusikiliza nje. Alidhani amesikia sauti ikiita.

“Kifo hakikuja upesi. Na sikuwa shujaa wa kujiua kwa urahisi. Hata hivyo, badala ya kifo ilifuata faraja mpya. Tumaini pekee la mtu kama mimi, Azimio la Arusha.” Alisita na kumtazama Sikamona usoni. “Naam, lilitangazwa. Likatoa sheria mpya na zenye manufaa kwetu ambao tulikuwa na shida na kwa kila mmoja ambaye aliwahurumia watu wote wenye dhiki. Nilifafanua makosa ya uhuru wetu, kwamba ulikuwa kilemba cha ukoka. Uhuru si kubadili rangi ya bendera, bali kubadili mfumo wa maisha, yaani kumfanya kila mwananchi ajisikie huru, si kwa maneno bali kwa vitendo. Huru katika siasa. Huru katika uchumi. Huru katika utamaduni. Likakomesha misingi yote ya baadhi ya watu kukalia uchumi hali wengine wakitaabika. Likafutilia mbali umilikaji wa ardhi, kugawa kazi kwa mjuano na







mabaya mengine kadha wa kadha. Watu wengi walisema mengi. Wengine walilitukana, wengine wakililaumu. Baadhi hata walihama nchi na kwenda nje kwa kulichukia ama kuliogopa. Na ndipo lilipogundua kuwa dunia si mbaya bali wanadamu. Na kwamba taabu yangu haikuletwa na kuishi ila watu tunaoishi nao. Kama si hivyo kwa nini waichukie hata sera ambayo ina nia ya kumtengenezea mwanadamu maisha? Kwa nini waitukane siasa yenye lengo la kuleta uhuru halisi na haki? Kumbe starehe yao ni kutuona tukitembea matako nje na kulala njaa? Waache waseme wapendavyo, waache waame nchi. Mimi binafsi nilimwona Nyerere na wote waliofanikisha mpango huo kama nguzo pekee ambayo mnyonge anaweza kuitegemea. Nikaiacha pombe, nikaacha gofu na kichochoro nilichokuwa nikiishi na kwenda zangu kijijini ambako nilijipatia ardhi na kulima na kiwanja cha kujenga nyumba. Nilifanya kazi kwa bidii ambayo ililetwa na matumaini hadi shamba langu likawa kubwa lenye mavuno bora. Nyumba nyangu pia imepata bati na saruji…”

Alisita ghafla na kumkazia Sikamona jicho kali, jicho ambalo lilimtisha Sikamona nusura kumfanya ainuke na kukimbia. Alistahimili kwa kujikaza tu huku akiusikiliza moyo wake unavyotetemeka ndani ya kifua chake.

“Vipi tumwache mtu ambaye anavamia nchi kwa nia ya kupotosha yote hayo anirejeshe tena katika kundi la ombaomba? Kwamba anataka kuitoa nchi itokane na ujamaa! Tuishi wapi?







Wala si kupotosha maendeleo yetu, bali pamoja na kufanya matumaini ya nchi nzima yawe ndoto. Aharibu maisha, aharibu matumaini ya wenetu. Twawezaje kumwacha? Anastahili adhabu. Anahitaji kipigo. Tena kipigo halali kabisa. Tusipofanya hivyo tutakuwa wasichana badala ya wavulana. Tutakuwa kichekesho kwa dunia nzima. Tuna kazi moja tu, kumpiga.” Akasita tena ghafla kama alivyoanza. Ilikuwa sauti ndogo lakini inayofoka, sauti ambayo ilimfanya Sikamona si amwogope tu bali pamoja na kumwona kama mtu mpya katika macho yake.
 
27.
“Kwa hiyo ndugu yangu,” sasa alikuwa mpole tena, mpole kama kawaida yake, sauti yake ya kuelimisha na kuonya, “Tuna kila haki na wajibu wa kupigana. Tunao uhalali wa kuua. Tusipoua si kwamba tutauawa sisi tu, bali pamoja na matumaini yetu, matumaini ya taifa zima. Lazima hilo uliweke kichwani.”

Kikafuata kimya kirefu.

Ndani ya kimya hicho, Sikamona alihisi hatia. Mdoe alikuwa ameuweka uchi moyo wake. Amezifichua siri za maisha yake, siri za imani yake, siri za matumaini yake, siri ambazo hakuwai kuzitoa kwa mtu yeyote wala hakutarajia kamwe kufanya hivyo. Alikuwa amempa yeye. Kwa sababu gani? Urafiki? La.

Yalianza siku nne zilizopita, tangu baada ya lile pambano lake la kwanza, nafasi yao ya kwanza kuwa katikati ya mizoga ya binadamu, kutazama damu inavyomwagika na kushuhudia







mwanamume anavyotahabika anapokata roho. Hali hiyo ilimtia simanzi kuu. Ikamnyima usingizi kwani kila alipolala alizisikia sauti za wafu wakilalamika kwa uchungu wa risasi. Alishindwa hata kula. Alipojaribu kula nyama alijihisi anakula nyama ya mtu mmoja baina ya maiti kadhaa alizosaidia kuzika. Ndipo akawa mnyonge, mgonjwa si mgonjwa, mzima si mzima. Alijitahidi kuwaepuka watu na kukaa peke yake, akiwaza. Juhudi za akina Mdoe na wenzake kumshawishi ale hazikufua dafu.

Lakini si sasa, baada ya Mdoe kumfunulia undani wake wote, maongezi ambayo hadi yanafika mwisho yalimfanya Sikamona ajisikie analo la kumwambia. Akapanua mdomo kulitamka. Lakini… neno lenyewe liliyeyuka kinywani mwake kama barafu na kutoweka. Badala yake aliduwaa akimtazama kwa macho yasiyomwona.

Kabla hajajua lipi lingefuata ishara ya vita ilisikika ghafla. Mdoe akashangaa kumwona Sikamona akiwa wa kwanza kuinyakua bunduki yake na kuondoka mbio.

Akamfuata.

























10

ALIDUWAA mbele ya mahema. Hawakujua walipaswa kwenda wapi. Kadhalika, hawakumwona hata mtu mmoja. Yaelekea lilikuwa shambulio

la ghafla. Badala ya kwenda kokote walitazama huko na huko na kisha kutazamana kwa macho yanayoulizana swali lilelile, “Ni upande gani?” ngurumo za bunduki na mivumo ya risasi ndio iliyowapa jibu. Ilikuwa imezuka ghafla toka mbele ya kambi yao. Sikamona akaanza tena kukimbia kuelekea huko, Mdoe akimfuata.

“Sika!”

Akageuka kumtazama. Mdoe alikuwa hamtazami. Alikuwa ametoa macho kutazama wanakotoka, nyuma ya mahema yao. Mdomo wake ulikuwa wazi na uso kaukunja kwa makini kama aliyekuwa akiona kitu. Sikamona alitulia kumtazama na kutazama huko na huko bila







ya kuona chochote. “Twende zetu…” alijaribu kumweleza mwenzake, lakini mkono wa Mdoe ambao ulipunga hewani kumnyamazisha ulimfanya si anyamaze tu bali pamoja na kutulia kabisa. Hakujua alichokuwa akikiona Mdoe. Alijaribu kufikiria hicho anachokitazama mwenziwe bila mafaniko. Mawazo yake yalikoma pale Mdoe aliponong’ona bila ya kumtazama. “Adui.”

Akatoa jicho na kulikaza kadiri ya uwezo wake kutazama huko alikokuwa akitazama Mdoe. Bado hakuona wala kusikia chochote. Sauti pekee katika masikio yake ilikuwa ule uvumi wa risasi nyuma yao. “Yu wapi adui?” alinong’ona.

“Nifuate,” Mdoe alitoa amri huku akianza safari ya kurudi walipotoka.

Sikamona alisita kwa muda kabla ya kumfuata. Walitembea kwa kunyata polepole, kisha Mdoe akamwashiria Sikamona kuinama. Baada ya muda Mdoe alimwashiria kulala chini. Wakaenda wakijivuta kifudifudi mfanowa nyoka. Wakayaacha mahema yao na kutokea kwa nyuma. Wakaendelea kujiburuta hadi walipokifikia kichaka ambacho kwa kila hali kilistahili kuwa maficho. Hapo Mdoe alimwashiria mwenziwe kutulia. Wakalala bega kwa bega. Bunduki zao zilikuwa zimeelekea mbele ambako Mdoe alikutazama kwa makini hali Sikamona haoni wala kusikia chochote. “Anaona nini?... Uoga? Kichaa? Au damu ya watu inamdhuru kama ilivyo…” alijiuliza kimoyomoyo.

Mdoe alimkatiza mawazo yake kwa kuelekeza
 
28.






kidole chake mbele huku akimnong’oneza, “Tazama.” Ndipo alipoweza kuviona vichwa viwili vya askari vikiwa vimeinuliwa toka manyasini. Vikitazama upande waliko. Kofia zao zilionyesha dhahiri kuwa walikuwa adui. Sikamona aliinua bunduki yake na kulenga kimoja cha vichwa hivyo tayari kuifyatua. Lakini Mdoe alimzuia akisema, “Hapana, ngoja.”

“Kwa nini?” alifoka kwa mnong’ono, “Unajua wale ni maofisa? Wanajadili mbinu za kutuhujumu.”

“Ndio, lakini subiri.”

Wakatulia wakiwatazama. Vichwa hivyo vilipotazama tena ndipo Mdoe alipomgeukia mwenzake na kumnong’oneza. “Sikia Sika, mbinu zilizotumiwa na hawa jamaa ni za hatari. Hivyo vita vinavyopiganwa huko si vita kamili. Hiyo ni mbinu tu. Wamewatuma hao wenzao, pengine kikosi kidogo ili wakati tukikiangamiza wao watuzingire na kutuangamiza pamoja na kuyateketeza makambi yetu. Hivyo, inatupasa kuangalia sana.” Akasita akifikiri kwa makini. “Sika,” baadaye alisema. “Tuna jukumu kubwa mbele yetu. Kuangamia au kunusurika kwa kikosi chetu kinategemea akili na juhudi zetu. Hivyo bwana, nakuomba unisikie, nenda upesi kwenye mapambano. Mwambie Kamanda hali halisi ilivyo. Mimi nitakuwa nao. Endapo wataanza mashambulio nitakuwa tayari kuwajibu. Sitaruhusu hata kibanda kimoja kiungue. Nenda.”

Sikamona akamshanagaa.







“Unaweza kupambana peke yako na maelfu ya watu? La. Tutakuwa wote. Na kama ni kwenda huko twende wote,” alisema.

“Sika, nasema nenda.”

Kulikuwa na kitu katika sauti ya Mdoe, kitu ambacho kilimfanya Sikamona ainue uso. Ndio kitu hichohicho kilikuwa katika macho yake. Kiliyafanya macho hayo kutoa nuru kali ambayo katika nafsi ya Sikamona ilikuwa amri isiyopingika. Bila kutamka neno jingine alianza kutambaa upesiupesi kurudi alipotoka.

Alikuwa hajafika mbali kabla hajasikia mlipuko wa risasi nyuma yake. Aligeuka na kuanza kurudi. Kisha alijishauri na kuamua kwenda. Amri na maarifa ya kijeshi yote yalimtoka akilini. Badala yake alijikuta akiinuka na kuanza kukimbia akisukumwa na mshindo wa buduki nyuma yake na kuvutwa na uvumi wa risasi mbele yake.

“Simama,” Sauti kali toka kichakani ilimfokea.

Akasimama akitweta. Sauti za risasi zilimdhihirishia kuwa alikuwa karibu ya kuingia katika uwanja wa mapambano aliokuwa akiukimbilia. Kisha, akageuka kutazama ilikotoka sauti hiyo. Aligongana na bastola ambayo ilikuwa imeshikiliwa na MP mwenye cheo cha Koplo.

“Mikono juu,” Koplo huyo alitoa amri nyingine.

Badala ya kutii Sikamona alifoka. “Afande unapoteza muda bure. Adui wako nyuma yetu wametuzingira. Nilikuwa nikienda kumpa







habari mkuu wetu. Kwa hiyo, mwambie hivyo. Tumezingirwa.”

“Muongo wee! Hutoroki mapambano wewe? Hutoki ulipokuwa umejificha na sasa unakwenda huko baada ya kuona adui amejitoa?” Koplo alifoka akimsogelea Sikamona. “Sema ukweli. Ni ujinga kunidanganga kwani…”

“Afande,” Sikamona alinguruma. “Utakuwa na haki ya kubeba hatia iwapo adui atafaulu katika mbinu yake. Nakuomba tena, nenda kampe mkuu wa Kombania habari upesi sana. Mwambie kuna adui nyuma yetu.” Baada ya kusema hayo aligeuka tena, hima kama alivyokuja na kuanza kukimbia.

“Wee! Simama!”

Sikamona hakujishughulisha wala kugeuka nyuma.

Alimkuta Mdoe kalala hatua chache toka pale alipomwacha, bunduki yake ikiwa imeishiwa risasi na sasa anapambana na adui kwa kuwatupia mabomu ya mkono. Damu zilikuwa zikimvuja shingoni, tumboni na usoni. Hali yake ilidhihirisha wazi kuwa alikuwa katika dakika za mwisho za maisha yake.

“Mdoe, unakufa!” Sikamona aliropoka baada ya kumtazama.

Ndio kwanza Mdoe akageuka na kumwona. “Uko hapa bado?” akauliza akifoka. “Hujaenda kupeleka habari? Nenda Sika, nenda haraka.”







Tayari nimeenda na kurudi” alimjibu akitweta. “Unajua Mdoe, unahitaji kumwona daktari upesi.”

“Usijali, bado wakati.”

“Haiwezekani. Lazima…” Kitu cha moto kilipenya katika paja la Sikamona na kuukomesha ubishi wake. Hima, akajilaza kikamilifu na kuiwasha bunduki yake kujibu risasi za adui ambazo zilikuwa zikidondoka huko na huko kama mvua. Iliwachukua dakika kama tano katika shughuli hiyo. Halafu, risasi za adui zikakoma ghafla. Sikamona akafahamu kuwa tayari jeshi lao limewasili. Akainuka na kuwaona adui wakianza kutawanyika mbio kama kundi la kondoo lililovamiwa na nyuki. “Barabara,” alinong’ona.

“Ndio. Tumefanya kazi njema.” Sauti ikamzindua Sikamona. Ndipo alipomkumbuka tena Mdoea. Akainama na kumtazama. Nuru ileile iliyokuwemo katika macho yake. Kisha alikuwa akicheka. “Ilikuwa kazi njema. Wako wapi? Tazama wanavyokimbia. Wengi wao sasa ni maiti, roho zao ziko ahera. Walidhani wangetuweza kwa hila ya kike kama ile?”

Sikamona hakuweza kumsikia. Alikuwa ametishwa tena na hali ya Mdoe. Damu. Damu kila mahali. Damu usoni, damu kinywani, damu mwilini. La, hakuwa mtu wa kupona. “Mdoe twende kambini,” Sika alimwambia akiinama kumwinua.

“Ya nini? Hapa nilipo pananifaa. Najiona niko nyumbani.”







“Usiseme hivyo Mdoe.”

“Ndio, niko nyumbani. Nina furaha kamili. Nitakuwa hapa hadi kiyama, nione kama watainuka hawa waliokusudia kutuhujumu.”

“Hapana Mdoe…” alisema huku akijitahidi tena kumnyanyua. Maumivu katika paja lake yalikuwa makali, hivyo alijikuta akichechemea kwa taabu kubwa na mtu mzito kama Mdoe mgongoni. “Jikaze kidogo basi,” alimwambia.

“Ya nini, Sika?... Usi… Usisumbuke. Niache tu, niko nyumbani.” Sasa hata sauti yake ilikuwa imebadilika, alitamka kila neno kwa kujilazimisha. Sikamona hakumsikiliza bali alizidi kujivuta.

Walipenya msitu na kuacha kelele za vilio na ngurumo za silaha kali nyuma yao. Wakawa wakiikaribia kambi.

“Sika… nitue…” Hakumsikiliza.
 
29.
“Nitue Sika… Nitue…” alifoka kidhaifu. Bado Sikamona hakumkubalia.

“Haya… najua unajisumbua bure. Mimi niko nyumbani… umekuwa mwisho mzuri… mwisho wa kiume… mwisho unaomstahili mwanaume. Au siyo Sika?... Wako wapi? Wako wapi? Na wajitokeze kama wana ndevu…”

Kikafuata kimya kirefu. Sikamona aliona uzito ukizidi. “Mdoe,” akaita. “Mdoe!”

Hakujibiwa. Akagutuka na kumtua chini. Mdoe







alikuwa ametulia kimya, bila dalili yoyote ya maisha. Jambo lililomshangaza Sikamona ni lile tabasamu ambalo lilikuwa bado katika uso wake, tabasamu refu lenye dalili zote za faraja.

Ndipo naye alipohisi upya yale maumivu katika mguu wake wa kushoto, maumivu makali mfano wa moto unaowaka mwilini. Akafahamu kuwa alikuwa na madini ya shaba mwilini mwake. Jasho likaanza kumtoka. Juhudi zake zote za kushindana na maumivu hazikumsaidia. Akajikuta akianguka polepole na kulala kwa utulivu kando ya Mdoe.

























11

LIWASHANGAZA askari wote walioshuhudia tukio hilo, kuona maiti mbili, nje kabisa ya uwanja wa mapambano, zikiwa zimekumbatiana. Kila mmoja aliyefika

katika eneo hilo aliduwaa na kutekwa na huzuni, damu ikiyashurutisha macho yake kuendelea kutazama. Baada ya muda umati mkubwa ulikwisha zizingira maiti hizo.

Kisha, jambo la ajabu zaidi likatokea. Mmoja kati ya maiti hao alionekana akifunua macho. Si hilo tu, bali ilikuwa pamoja na juhudi za maiti huyo kujiinua. Aliposhindwa, alijilaza tena, lakini macho yakiwa wazi. Halafu alionekana kukumbuka jambo. Akajikongoja kuinua mikono yake na kuanza kumsukasuka maiti mwenzake.

“Mdoe, Mdoe…” aliita kwa nguvu. “La, huwezi kufa, Mdoe,” alilalamika kwa sauti ya majonzi. “Mdoe, la…” sasa kilikuwa kilo.







Ndipo watazamaji wakafahamu kilichokuwa kikitokea. Mmoja alikuwa maiti, mwingine mahututi. Wakawainua mmojammoja na kumpeleka Sikamona kwa daktari. Maiti ya Mdoe, kama mashujaa wengine waliopoteza maisha siku hiyo, ilihifadhiwa kwa heshima kusubiri safari ya kurejeshwa nyumbani.

***

Sasa alipigana kishujaa, kwa moyo na nia moja.

Ilikuwa baada ya kupona lile jeraha lililomfanya kulazwa kwa siku kadhaa.

Ari hiyo mpya haikutokana na ile sifa ya ushujaa ambayo alipewa, pamoja na Mdoe, kwa ajili ya kitendo chao ambacho kiliyaokoa maisha ya kikosi kizima na kulifanya taifa lijipatie ushindi mwingine mkubwa. Ingawa walikuwa wamevunja amri zote za kijeshi kwa kitendo chao hicho, lakini bado walisifiwa na majina yao kuingia katika orodha ya mashujaa kati ya mashujaa. Na ni kweli kuwa kila askari ambaye alipishana naye hakukosa kumtupia lile jicho lenye tabasamu inayowakilisha hadhi yake mpya. Lakini bado hiyo haikuwa sababu. Haikuwa sababu kwa kuwa alifahamu kuwa kitendo hicho ndicho kilichomleta katika uwanja wa mapambano. Hakikuwa zaidi ya wajibu ambao aliapa kuutimiza.

Wala haikuwa kwa ajili ya kumuwaza Rusia na kujiambia jinsi ambavyo angemshangilia baada ya kurudi na sifa hizo. Ndio, angelakiwa kwa tabasamu halisi lenye husuda na hongera,







ambalo lingefuatwa na sauti nzuri ikisema, “Mpenzi umefanya jambo kubwa… ipokee zawadi yako…” hilo lilikuwa likimfanya ajiulize swali ambalo limetamba kichwani mwake kwa muda mrefu. Zawadi gani ambayo angepewa? Ingawa hakuifahamu aliendelea kuisubiri kwa hamu kubwa. Lakini bado hiyo haikuwa sababu ya ari yake mpya.

Hasa, ari hii ilikuwa imezuka katika nafsi yake kutokana na kifo cha Mdoe. Kumshuhudia Mdoe peke yake akiunyima umati wa adui njia ya kuingia katika kambi yao, na hatimaye kukata roho mgongoni mwake, kulimfanya azaliwe upya, upya kabisa! Alijihisi mwanamume kamili mwenye ujana kamili, mwili na rohoni timamu. Akili yake ikapambazukiwa na jambo moja tu: kupigana. Usipopigana utakufa. Kila mara alihisi maiti ya Mdoe mgongoni mwake, ikimkumbusha kifo, pamoja na kusikia tena ile sauti yake ya mwisho yenye furaha na majivuno ikisema, “Umekuwa mwisho mzuri, mwisho wa kiume…” Hayo yakaifukuza hofu ya kifo rohoni mwake, yakaiondoa huruma ya kike rohoni mwake, pamoja na kuzitokomeza zile ndoto za jinamizi na uoga wa damu katika moyo wake. Akajitupa katika kila pambano lililofuata kwa hasira na nia halisi, sauti ya maiti ya Mdoe ikimsukuma na kumpa ari zaidi. Alihakikisha mateka ambao walianguka katika miguu yake wanajuta kuzaliwa kabla hawajapelekwa kunakowastahili.

Leo walikuwa wamewateka askari chungu







nzima wa Amini. Kati yao kulikuwa na Waarabu kadha wa kadha. Sikamona alimsogelea Mwarabu mmoja na kumchangamsha kwa teke la tumboni. “Utasema kilichokutoa kwenu na kuja kufanya uharibifu huku.” Akamwambia akiongeza teke la pili. Mwarabu hakusikia Kiswahili. Badala ya kujibu, alilia kwa maumivu. “Sema kilichokuleta huku” Sikamona alimwuliza tena kwa kiingereza huku akimtia ngumi ya kifua. Bado Mwarabu huyo hakumsikia. Lakini alipozidiwa na kipigo aliangua kilio kwa nguvu akitamka neno lililosikika kama “Gadaffi, Gadaffi.”
 
30.
Akamwacha huyo na kumwendea Mganda ambaye alionekana jeuri kuliko mateka wengine. Alikuwa na macho mekundu, sura ya kikatili na umbo la kinyama. Kila kiungo katika mtu huyo kilidhihirisha kuathiriwa na bangi. Alidhoofishwa na gongo pamoja na kutaabishwa kwa kila kitu ambacho ni hatari kwa maisha ya mwanadamu. Sikamona hakumchelewesha. Alimpiga kichwa ambacho kiliyafanya macho yake mekundu yazidi kuwa mekundu. Akamwinua na kumpiga ngumi ya pua. Kisha akamwuliza kilichomtoa kwao na kumleta Tanzania kufanya unyama. Mganda huyo alicheka, jambo ambalo lilimzididhia Sikamona hasira kali. Akamtia vibao vya mfululizo huku akisema, “Utajuta kuja Tanzania.”

“Sijuti,” Mganda alimjibu. “Labda nijute kuzaliwa.”

“Kwa nini?” Sikamona alisita kumpiga na kumwuliza kwa mshangao.







“Nahitaji kura, nahitaji kuishi. Nisingesaliwa nisingehitaji fyote hifyo. Kwa kuwa nilisaliwa lazima niishi. Maisha ni kasi. Mimi nimekosa kila kasi isipokuwa uashikari. Uashikari ni kama imbwa. Niko tayari siku sote kufanya bwana wangu asemafyo. Anasema kamata, nakamata. Ua, naua…”

“Bwana wako nani?” “Idd Amini.”

Sikamona akazidi kushangaa. “Yaani uko tayari kuua kwa kuwa umetumwa kuua? Huna haya wala utu ili uogope kuangamiza kiumbe asiye na hatia?”

Sasa walizungumza kama marafiki.

“Utu utanisaidia nini mbere ya maisha? Haya itanipa chakura? Watu wanafanya kila kasi iri ware. Wengine wanadeki fyoo fya wensao. Wengine wanafua nguo za wensao. Mimi naua. Nahitaji mshahara. Nire.”

“Unaua kwa ajili ya mshahara?” “Askari ni mbwa bwana”

Sikamona hakulisikia jibu lake. Alikuwa hamwulizi Mganda huyo tena, bali akijiuliza mwenyewe. Yawezekana ni kweli mtu kuua kwa ajili ya mshahara? Ni ipi thamani ya maisha basi? Labda ni kweli askari ni kama mbwa? Kama ni hivyo, wakulima na wafanyakazi maelfu kwa maelfu ambao wanataabika katika nchi kadha wa kadha ni wanyama gani? Punda?







Akaacha kumpiga Mganda huyo na kwenda zake huku kainamisha kichwa kwa wingi na uzito wa maswali kadha wa kadha ambayo yalikiteka upya kichwa chake.

Askari ni mbwa!

Wengine wanafagia vyoo, mimi naua ili nile.

***

Halafu ikatokea. Ujumbe wa siri uliijia kambi yao usiku ukiwa na ombi la wananchi wa Uganda kwa Jeshi la Wanachi wa Tanzania, kwamba ukatili na unyama wa Idd Amini ulikuwa umewachosha, wanaomba msaada wa kusaidiwa kuikomboa nchi yao ili watokane na makucha yake, na kuuepuka utawala wake.

Machozi ya furaha yalimtoka Sikamona kwa kule tu kufahamu jambo hilo, kwamba Waganda wameamua. Mdoe angesemaje iwapo angekuwa hai na kuisikia habari hiyo? Alijiuliza.
 
31.

MBI lilikuwa limekubaliwa.

Hivyo, waliingia Uganda mchanamchana, wakifuata barabara na kupenya misitu. Ilimshangaza

Sikamona alipoona raia wa huko wakiwalaki kwa shangwe na vigelegele huku wakiwatupia maua na kuwaita “Wakombozi.” Haikuwa kuwalaki tu, bali pamoja na kuwaongoza katika maficho yote ya askari wa Amini pamoja na vijana kadha wa kadha kujiunga katika “Jeshi la Ukombozi.”

Kilichomshangaza zaidi ni ile furaha waliyokuwa nayo wazee wa huko kila walipokutana na askari wa Tanzania. Walionyesha kuridhika kwa kila kiasi kwamba iliwabidi kutamka mshangao wao kwa maneno.

“Wana adabu, wana heshima…”

“Ndio, na upendo pia. Uliona walivyombeba







mzee Mukasa alipojeruhiwa na bomu walilotega askari wa Nduli?”

“Si hilo tu, ona wanavyotusalimu kwa adabu. Ona wananvyotoa shikamoo kwa raia… uliwahi kuona askari wetu akifanya hivyo?”

Shukrani na moyo huo wa Waganda ukazidisha ari na upendo katika mioyo ya Watanzania. Wakajikuta wakipigana bila ya kujiuliza wanampigania nani. Kazi ikawa rahisi kuliko ambavyo ingestahili kuwa, kwani ilikuwa kama kusafishasafisha askari ambao sio kwamba walikuwa na imani kwa Idd Amini bali walitegemea hongo aliyokuwa akiwapa kwa kuiita mshahara.

Baada ya miezi kadhaa wakawa wameitapakaa Uganda nzima kama nyuki walioingia katika mzinga usiowatosha. Amini akasikika akilalamika, mara atakuja Tanzania kuomba radhi, mara Umoja wa Taifa uingilie kati, lakini ilikuwa kazi bure.

Kama ambavyo alikuwa akichekelea ukatili wake dhidi ya Waganda, ndivyo dunia ilivyotulia ikimcheka.

***

“Kazi mliyotutuma tumeimaliza,” Sikamona alijisikia hivyo. Alikuwa ameegemea mti mkubwa, mbele ya nyumba ya Idd Amini katika kijiji cha Gulu, kijijini kwao baada ya kusafisha nchi nzima. Baada ya kuikomboa Uganda dhidi ya utawala haramu wa kinyama ambao uliathiri maisha na uchumi kwa muda wa miaka minane kazi ilikuwa







imekwisha ila tu kulikuwa na mabaki ambayo yalikuwa yamehama miji na kujificha misituni. Hawa walijipenyeza mijini mara kwa mara na kufanya uhuni ambao hawakuona aibu kuuita, “Kuikomboa Nchi Kutoka Tanzania.” Tatizo hili halikumtia wasiwasi Sikamona. Lilikuwa jambo la kutegemea. Kila vita uwa na mabaki ya aina hii, yakitumia nafasi hii kujineemesha na kujitajirisha huku wakisema hili na lile. Hivyo, Sikamona alifahamu dhahiri kuwa hii haikuwa sababu ya kumnyima furaha.

Lakini hakuwa na furaha.

Hakuwa na furaha kama ile ambayo ingemstahili kuwa nayo baada ya ushindi mkubwa kama huu. Kwa nini? Alijiuliza. Ushindi si jambo dogo. Hasa ushindi dhidi ya kiumbe kama Idd Amini, kiumbe mwenye sifa za unyama, dunia nzima, kiumbe ambaye ulimwengu mzima umeona na kushuhudia alivyoitaabisha Uganda na kuwababaisha majirani. Nchi ngapi zilitumia serikali ya Tanzania salamu za pongezi, zikionyesha furaha yao kwa kuanguka kwa fashisti huyo? Haiyumkini ushindi huu uliifuraisha dunia kwani ulihitajika na dunia nzima.

Hata hivyo bado hakujiskia furaha.

Kwa nini? Ama hali hii ilitokana na kule kupona kwa Idd Amini? Alikuwa ametoroka na kuanza maisha ya udobi katika nchi mojawapo ya Kiarabu. Hakuna mtu yeyote aliyependa kuliona jambo hilo likitokea. Lakini alipona, baada ya kuyapotosha matumaini ya watu na kuwafanya







Waganda wote kutapatapa wakielekea huko na huko, akiwachezesha kama wanawe.

Kwa nini dunia inakua hivi? Mtu mmoja, binadamu wa kawaida kama watu wengine, vipi apate uhuru na nguvu ya kuifanya nchi nzima apendavyo? Vipi ajaliwe uwezo wa kuyatawala maisha ya watu, kunyayasa starehe zao na kukomesha haja zao za maendeleo? Vipi abahatike kupata amri juu ya kuishi na kufa? Uwezo wa kila mwananchi na mamlaka katika kila jambo atendalo?

Baada ya kuchekelea vifo na maisha ya watu wenye dhiki, sasa mtu huyohuyo, yuko salama salimini. Hana shaka lolote, hofu ya mlo wa kesho wala dhiki ya mavazi. Waliokufa wengine, wanaotahabika wengine…

Labda kweli askari ni mbwa…

Kwa vipi? Askari ni kama watu wengine, mwananchi kama alivyo kila mwananchi. Kama kijana basi yu kijana wa taifa, mtoto wa mkulima na mfanyakazi. Kama taifa linaathiriwa na ujinga, umasikini na maradhi basi athari hizo humkumba askari kama zimkumbazo kila mwananchi. Hayo Sikamona aliyafahamu kitambo, kitambo sana, kabla ya Amini kuivamia nchi. Na ni hilo ambalo lilimfanya aingie jeshini. Hakuwa mwanajeshi. Lakini alifahamu fika maslahi yake yalimtaka kuyalinda, kama mwananchi, kama mmoja miongoni mwa wote ambao wanayategemea maslahi yao.







Na askari wa Amini je?

Hapo alijisahihisha mara moja. Alikuwa amekosea. Tafsiri aliyoitoa ilikuwa tafsiri ya askari wa Tanzania. JW “Jeshi la Wananchi” tafsiri halisi kwa maneno na vitendo. Hayo aliyathibitisha kwa macho yake mwenyewe baada ya kushuhudia Waganda wanavyowalaki kwa nyimbo na maua.

Ndiyo, tafsiri hiyo haikuwahusu askari wa Amini kamwe. Idd Amini alikuwa nduli. Alikuwa na kiu kubwa ya kunyayasa na kutesa. Uwezo wa kutimiza kiu yake hiyo hakuwa nao. Alihitaji msaada. Ndipo alipogeuza jeshi la nchi kuwa watumwa wake baada ya kuua waliopinga ujeuri huo na kuajiri aliodhani wangefaa katika kutimiza kiu yake. Aliliamrisha jeshi kuwa sugu katika kuwakandamiza raia, kukomesha nia zao za kujiinua pamoja na kuwasumbua jirani. Kama mbwa wa tajiri, akawashibisha askari hawa kwa vinono zaidi ya chakula cha watu. Akawahonga si malipo tu, bali pamoja na maneno ya uongo hata wakaishiwa aibu na kuwa kama malaya wasio na aibu wala hofu mbele ya wazazi wao. Wakafanya yote ambayo bwana wao aliwaamuru kutenda. Hata wakaritoroka jeshi lake hilo na kwenda kuishi ugenini. Waliosalia miongoni mwao ndio wale waliojiunga na jeshi la ukombozi.

Wala si jeshi tu ambao Amini aliwageuza malaya wake. Viongozi wake wote aliwalazimisha kuifumbia macho haki na halali, wakawa viziwi wasisikie malalamiko na vilio. Hivyo, mkulima akaendelea kuwa mtumwa katika nchi yake
 
32.


mwenyewe, akivuna mavuno mengi na kuambulia faida duni, akifanya kazi ngumu na kulazimika kuona jasho lao likiwastarehesha “wateule” wachache. Kadhalika, mfanyakazi akawa punda asiyejua kuchoka wala kuhitaji malipo halali. Alikesha viwandani na kushinda juani akizalisha faida kubwa ambayo ilimnenepesha Amini, kuimarisha jeshi lake na kustarehesha mabwana zake ndani na nje ya nchi. Hayo pamoja na kule kuiweka Uganda nzima katika jehanamu isiyopungua vilio na maombolezo ndio kisa cha vita. Ndio kisa kilichoifanya Tanzania isisite kuwaunga mkono waganda. Ndio kisa cha adhabu aliyoipata Amini adhabu ya kipigo ambacho kamwe kisingemtoka katika fikra na ndoto zake, kipigo ambacho kimeihakikishia dunia kwamba Waganda walikuwa tayari kununua upya uhuru wao hata kwa bei ya damu. Na kwamba Tanzania ilidhamiria kuleta mapinduzi ya kweli nchini na barani Afrika kwa gharama yoyote, gharama zote, jasho, damu, maisha…

Mdoe!

Umbo na sura yake vilimrudia Sikamona akilini tena. Siku zote kila alipowaza juu ya vita na ukombozi, sura ya Mdoe haikukosa kumjia akilini. Alimwona katika kila hali, mara akiwacheka maadui baada ya kuwazuia kuingia kambini, mara akifoka aliposema “…anastahili kipigo,” na pengine ilimjia ile sauti yake ya mwisho aliponong’ona “…Umekuwa mwisho wa kiume…” hayo yalimfanya Sikamona ajikute akizidi







kumheshimu siku baada ya siku na kuuthamini mchango wake katika kuilinda nchi na kuitetea haki ya Waganda, mchango usiosahaulika, mchango wa maisha, mchango wa uhai kwa hiari!

Nani mwingine anayestahili kuitwa shujaa zaidi ya mtu kama huyu? Mtu ambaye amekuwa tayari kuyapoteza maisha yake kwa ajili ya watu! Kwa ajili ya maslahi, mahitaji na matumaini yao? Mtu aliyezaliwa katika ukoo masikini, akaathiriwa na umasikini na siasa potofu; kisha akaona nuru ikitokea, tumaini la mnyonge, akaitumaini nuru hii na kuanza kuonja matunda yake; kisha giza likatishia kuizima, akaiacha nuru na matumaini na kulipinga giza hata likakubali kuwa limepingwa. Kwa bei ya maisha yake ameinunua nuru upya. Si kwa manufaa yake bali kwa manufaa ya watu wengine, kwa faida ya maisha yao ya baadaye. Kama si ushujaa ni nini basi?”

Kuna watu wengi ambao majina yao yanaishia miongoni mwa watu, kwa ajili ya kujitoa kulisaidia taifa. Akina Lumumba wa Zaire, Nguabi wa Kongo, Mkwawa wa Tanzania, Mao wa China, Lenini wa Urusi n.k. wengi mno. Wote hao majina yao yanaishi kwani matendo yao yalikuwa nuru iliyokusudia kuleta ufanisi palipodorora, faraja penye dhiki na shibe penye njaa. Orodha ya majina yao imo katika fikara za dunia. Jina la Mdoe lilikwishaingia katika kurasa hizo, Sikamona alijikumbusha.

Damu ni nzito kuliko maji. Thamani ya damu ni kubwa, kubwa machoni pa mwanadamu







na Mungu. Haikadiriki. Hakuna aijuaye bei yake. Kama kuichezea damu hiyo, kuchezea maisha, kama alivyofanya Idd Amini ni dhambi isiyosameheka si wazi kuitetea damu na maisha ya utukufu usiosahaulika? Tanzania ni nchi masikini. Pamoja na umasikini wake imejijengea misingi ya siasa ambayo kila mwananchi ataufurahia uananchi wake. Azimio la Arusha ni njia inayomwelekeza huko Mtanzania.

Ingawa bado tumo njiani, lakini mafanikio ambayo yamekwishafikiwa si haba. Yamewafanya si waanze kuyafurahia matunda na uhuru wao tu, bali pamoja na kuwahurumia jirani ambao wanataabishwa zaidi ya wakimbizi katika nchi zao wenyewe.

Hatimaye, wakawahurumia na kuliafiki ombi lao. Baadhi ikawalazimu kufa, akina Mdoe na wenzake. Huu si upendo usio na kifani? Kuacha maisha yenye matumaini! Kuacha uhai! Kwa ajili ya jirani ili kukomesha mkondo wa damu isiyo na hatia uliokuwa umechimbwa na Amini.

Wameukausha! Wameukomesha! Kwa damu yao! Damu isiyo na hatia!

Kama kupanda mbegu ya haki na upendo katika bahari iliyojaa uonevu, chuki na kukata tamaa!
















NAAM. Damu ya Mdoe na wote waliolala katika ardhi ya Uganda haikuwa imepotea bure. Ilikuwa mbegu. Hayo Sikamona aliyafahamu. Lakini bado hakujisikia furaha kama alivyodhani ingemstahili. Kwa nini? Hakulijua jibu. Pengine furaha hiyo ingekamilika hapo ambapo mbegu hiyo waliyopanda itakapotoa matunda, hapo ambapo matunda hayo yatakapoonekana kwa kila mtu na kuwashibisha wananchi labda! Kwani bei ya damu haikadiriki, wala hakuna aijuaye thamani

yake, isipokuwa hapo tu ambapo itachanua.

Akaendelea kuuegemea mti, akiitazama nyumba ya mkimbizi Amini tena na tena. “Baada ya siku itakuwa gofu,” alijiambia akitabasamu kimoyomoyo. Mchana ukatoweka na usiku ukaingia. Akainuka na kujivuta kambini kwao ambako alipata chakula cha usiku. Usiku wa leo







ulikuwa usiku wake wa zamu. Akajivuta hadi mahali pa zamu ambapo alijificha na kutulia akitazama huko na huko.

Kwa Sikamona ulikuwa usiku mrefu, tena wenye kiza kinene zaidi ya kawaida. Hivyo, ilimlazimu kuangalia kwa makini ili aweze kutimiza wajibu uliomleta hapa. Si kutazama tu. Ilikuwa pamoja na kushindana na usingizi ambao uliyatongoza macho yake mara kwa mara. Mawazo yake yakamwacha Amini na ukimbizi wake na kurudi nyumbani, Tanzania. Akawafikiria wazazi wake, akajiuliza watafurahi kiasi gani pindi wamwonapo akirejea salama. Mzima sana, isipokuwa kovu dogo la ile risasi iliyomjeruhi paja! Lakini hiyo ilimfurahisha, kwani kuwepo katika paja lake ni kumbukumbu ambayo kamwe isingefutika, kama shahada ya ushujaa wake.

Halafu akamkumbuka Rusia. Furaha iliyoje pindi watakapoonana tena? Watakumbatiana, watacheka, watashangilia! Atapokelewa kwa lile tabasamu lake makini linalofariji na kuburudisha. Zaidi ya yote atapewa zawadi yake ‘ya ushindi.’ Zawadi… ni zawadi ipi ambayo Rusia alikusudia kumpa? Alijiuliza tena swali hilo. Angepewa kitu gani? Hakuwa na jibu. Badala yake alijisikia ile hamu ya kurejea nyumbani ikimkumba kwa nguvu zaidi. Alitamani aondoke dakika hiyohiyo, apae na kuruka hadi nyumbani. Ndiyo, akatue hadi katika kifua cha Rusia. Lakini akaishia kuhuzunika kwa jinsi jambo hili lilivyokuwa mbali na uwezo wake. Angeruka hapo tu atakapoamriwa kufanya hivyo,
 
33.


siku chache zijazo. Hata hivyo, asingeruka kwa mbawa zake, ingekuwa safari ndefu ya gari.

Aligutuka ghafla. Alihisi ameona kitu kikitambaa katikati ya giza. Akayakaza macho yake kwa makini. La, hakuona chochote. Haiyumkini? Alikuwa amewaza tu. Akaendelea kuwaza hili na lile, akifika huku na kule na kuonana na kila anayemtaka, kimawazo. Kisha alihisi kuona kitu tena. Akayalazimisha macho yake kushindana na giza kulivuka. Naam, hakukosea. Kivuli cha mtu kilionekana kikipenya katikati ya giza hilo, polepole kama wingu. Alikuwa akitoka katika makambi yao! Sikamona alishuku mara moja kuwa huyu hakuwa rafiki wala askari mwenzao. Rafiki asingewatembelea katika muda kama huu na askari mwenzao asingewatembelea kwa mwendo huu bila yeye mlinzi kuwa na taarifa. Akainua bunduki yake na kumlenga huku akipanua mdomo na kutaka kusema “Simama” lakini aliiteremsha bunduki hiyo mara moja baada ya kupata wazo jingine.

‘Bila shaka huyu ni adui,’ Aliwaza. Kama ni hivyo alikuwa ameingilia katika kambi zao kwa upelelezi, ikiwa na maana kuwa alikuwa amegundua yote aliyohitaji kuyagundua na alikuwa akielekea kuwasilisha kwa wakubwa wake. Hivyo, kumwua kusingemaliza ukorofi wao. Haja ilikuwa kung’oa mzizi wa fitina kumaliza vitisho kabisa ili Waganda wapate uhuru wao na kuijenga upya nchi yao. Hivyo, badala ya kumwua alimwacha ili awe daraja ambalo lingemwezesha kuyafikia







maficho yao. Ni wazo hilo ambalo lilimfanya aache kumpiga risasi na badala yake ayaache maficho yake na kuanza kumnyatia kwa adhari na ungalifu kama paka anayemnyemelea panya. Sikamona alifahamu fika kuwa alikuwa akivunja amri zote za jeshi, kuchukua uamuzi huo bila ruhusa. Lakini hakuona kama kulikuwepo na wasaa wa kungoja ruksa.

Waliandamana kwa muda mrefu. Wakauacha mji na kuanza kufuata kichochoro kilichowaelekeza msituni. Hapo Sikamona aligutuka. Aingie porini? Vipi kama angepotea ama kujikuta akitokeza katika umati wa watu? Ni lipi ambalo angefanya kuyaokoa maisha yake? Akaanza kuulaumu uamuzi wake. Labda ingembidi kumwarifu mkuu wa Kombania ili wawafuate pamoja! Lakini huo muda angeupata wapi? Akasita, akiwa hajaamua kama ilimlazimu kuendelea au la.

“Tulieni…. Sikilizeni muone vijana wetu watafanya nini…” maneno ya Rais na Amiri Jeshi Mkuu, Mwalimu Nyerere, yalimjia akilini. Ni nani kijana zaidi yake? Ni kipi wananchi watakachokisikia zaidi ya kitendo kama hiki?”

“…Umekuwa mwisho mzuri… Mwisho wa kiume… Mwisho unaomstahili mwanaume…” si maneno tu aliyohisi kuyasikia bali pamoja na umbo zima la Mdoe likitamka kwa majivuno na faraja.

“…Utarudi salama… Ndipo nitakapokukabidhi zawadi ya ushindi…” kadhalika hakuyasikia maneno ya Rusia tu, bali ilikuwa pamoja na
 
34.

kuhisi uso wake mchangamfu ukimtazama kwa tabasamu. Hayo, kama hirizi ya usalama wake ama taji la ushujaa wake, yakamfanya aanze kumfuata adui huyo kwa moyo wenye ari na matumaini.

Hakukubali kumpoteza. Wala hakuwa tayari adui huyo afahamu kuwa anafuatwa. Alimnyemelea, akajitahidi kadiri ya uwezo wake kuepuka kukanyaga vijiti, visiki na kutumbukia katika korongo. Akaushukuru ujuzi na mazoea yake ya kutembea porini. Zaidi ya yote alilishukuru giza. Zamani alipokuwa mdogo alilichukia na kuliogopa, sasa alilitegemea na kuliona rafiki mkuwa.

Baada ya mwendo wa kutosha waliwasili katika kambi yao. Ingawa giza halikumruhusu kuona lakini kadri alivyozoea, hakushindwa kugundua vibanda vyao vilivyojengwa huku na huko. Kisha, aliweza kuona vichwa vya watu waliokuwa wamesimama hatua kadhaa mbele yake. Walikuwa wakizungumza kwa kunong’ona, asingeweza kusogea tena pasi ya kuonekana. Hivyo, alijifutika katika kichaka huku akimtazama kiongozi wao ambaye aliingia katika kundi hilo. Alihisi wakimlaki kwa shangwe. Akawasikia wakinong’onezana maneno kadhaa. Alihuzunika kwa kule kuwa mbali kiasi cha kutoweza kusikia walichokuwa wakizungumza. Kitu kimoja alikuwa na hakika nacho, kwamba maongezi yao yote yalikusudia kuwaangamiza wao. Laiti angeisikia mipango yao! Akasaga meno kwa uchungu.







Halafu alifahamu kinachotokea. Hujuma hiyo ilikuwa ikipangwa kufanyika muda huohuo! Aliyagundua hayo baada ya kuona vikosi vikitayarishwa na kupangwa tayari. Asingeruhusu hilo litokee, kuacha kikosi chao, ama kijiji chao, kivamiwe ghafla. Ni hilo alilofuata kulikomesha. Hivyo, bila ya kufikiri kwa mara ya pili aliinua bunduki yake na kupiga risasi juu kwa namna ya kuwatahadharisha askari wenzake waliobaki kambini. Mlipuko wa bunduki yake uliwafanya adui wote waduwae na kubaki kimya kwa muda. Lakini mlipuko huohuo uliyafichua maficho yake. Hivyo, wakati adui hao wameduwaa yeye aliinuka na kuanza kukimbia. Hakupiga hatua tatu kabla ya adui mmoja hajafahamu kilichokuwa kikitokea na kuanza kumfuata mbio. Alikuwa adui mwenye mbio nyingi, labda kwa ajili ya kuwa mwenyeji katika msitu huo, kila hatua yake moja alizidi kumkaribia Sikamona. Ndipo Sikamona alipoona kukimbia kusingemfikisha popote. Akasimama na kumgeukia. Adui alipomkaribia , alimpiga risasi na kuanza kukimbia. Lakini sasa alikuwa akifuatwa na kundi zima. Alijua asingefika mbali. Hivyo, aligeuka kuwakabili, hakuwa na muda wa kulala chini. Hakuwa na nafasi ya kufanya hivyo. Wima, kama kisiki, akaiwasha bunduki yake na kuwamiminia adui risasi bila hata ya kulenga shabaha. Wengi walianguka na kufa, wengi wakageuka na kukimbia, lakini ni wengi pia ambao walizidi kumjia kwa uchu kama kundi la mbwa mwitu lililomfumania mwanakondoo. Hatimaye, risasi zikamwishia. Alifahamu







kukimbia kusingemsaidia. Hivyo, alijitosa katika genge la maadui na kuanza kuwapiga kwa sime. Haikumchukua muda kabla hajajikuta angani akipigwa kwa kitako cha bunduki hii na kudakwa kwa singe ile.

Maumivu aliyoyasikia hayakuwa na kifani. Hata hivyo, aliyasikia kwa muda mfupi tu kwani dakika chache baadaye, badala ya kuelekea hewani, alijisikia akididimia polepole katika shimo refu lenye kiza kinene.











alipozinduka alijikuta kalala juu ya kitanda katika chumba chenye harufu tofauti na ile aliyoizoea, harufu ya mchanganyiko wa madawa. Uso wake

mzima ulikuwa umefunikwa na bandeji nzito ambazo zilimzingira hadi mikononi na kifuani. Alipojaribu kujigeuza alalie ubavu alipambana na maumivu makali, maumivu ambayo yalimfanya akikumbuke kile kipigo alichokipata toka kwa adui. “Niko wapi?” aliuliza.

“Kampala. Hospitali,” sauti ilimjibu.

Alipogeuka kuangalia macho yake yaligongana na yale ya Brigedia wake, Chunga. Akagutuka kidogo kwani hakutegemea. Akajaribu kuinua mkono ampigie saluti lakini hakufanikiwa.

“Usisumbuke Sikamona,” Brigedia alimjibu akitabasamu. “Unahitaji kupumzika kwa muda,”







akasita. Kisha, alianza tena, “Umekuwa hapa hospitali bila fahamu kwa siku tatu. Kwa kweli, tulianza kukata tamaa. Sasa hatuna shaka kuwa utapona.” Akasita tena. Kisha akaendelea, “Kitendo chako kamwe hakitasahaulika. Licha ya kuokoa maisha yetu ilituwezesha kuwaangamiza adui ambao walikuwa wakitusumbua sana. Hata hivyo, bado hatujafahamu uliwezaje kufahamu kambi ziliko na kwa nini ulianza kupambana nao peke yako.”

Sikamona angependa kueleza yote, tangu alivyomwona adui, alivyomfuata na hata alipofyatua bunduki ya kuwataadharisha. Hata hivyo, kwa ajili ya maumivu makali aliishia kuongea machache tu. Brigedia alisikiliza kila kitu kwa furaha, huku kasahau tabasamu usoni kwake. Baada ya kusikia yote alitikisa kichwa na kusema. “Ushujaa wako hautasahauliwa. Laiti kila kijana wa kitanzania angekuwa na roho yenye uamuzi na nia kama yako! Nasikitika tulichelewa kidogo kufika hapo ambapo ulikuwa umewadhibiti adui. Hata hivyo, tulifanikiwa kuwateka wote wale ambao walikuwa wamekuzingira na kukukanyagakanyaga kama vifaru wenye vichaa. Nadhani watajuta milele kwa ujinga wao wa kusahau yote waliyostahili kuyakumbuka na badala yake kukuvamia wewe.

Sikamona hakuyasikia yote. Uchungu mkali ulimrudia tena. Vitu kama nyundo vilimpiga kichwani. Ghafla akajiona akididimia tena katika lile shimo refu lenye kiza cha kutisha.







***

Sasa alikuwa hajambo kiasi. Aliweza kukiacha kitanda chake na kujikongoja hatua chache nje ya jengo la hospitali. Aliweza hata kula mwenyewe, ingawa alipata matatizo katika kulenga mdomoni na kutafuna. Alidhani hayo yalisababishwa na plasta zilizomzingira usoni, hivyo yangetoweka mara tu zitakapoondolewa.

Askari wengi walimjia kumpa pole na hongera, wengi sana, wadogo kwa wakubwa, rafiki kwa watu baki. Wote walikifurahia kitendo chake na kumwomba awasimulie tena na tena alivyofaulu peke yake kuwakabili maadui wengi kiasi kile. Lakini Sikamona hakuwa tayari kufanya hivyo. Asingekubali kurejea tena katika ndoto hiyo ya kutisha. Badala yake alikuwa akijiuliza vipi alinusurika katika mapambano chungu nzima, makali mno na kuja kuhatarika katika pambano dogo la mwisho kama hili. Miongoni mwa mapambano hayo ambayo kamwe yasingetoweka katika fikra za Amini na vikaragosi wake ni pamoja na kile kipigo cha Kagera. “Kumtoa Nyoka Nyumbani,” kile cha Lukaya “Asiye Sikia la Mkuu,” kile cha Entebbe “Joka Limekamatwa Kiwiliwili” na kile cha Kampala “Kupondaponda Kichwa cha Joka” yote hayo alishiriki kikamilifu na kuokoka isipokuwa hili. Hata hivyo, huku pia si kupona? Alijikumbusha. Kwani kupona ni nini? Haja si kuweka jina katika historia? Yeye ameongeza uzito wa jina lake katika kurasa za historia!

***







Halafu akawa amepona. Bandeji zikaondolewa na akaruhusiwa kuondoka. Akajisikia furaha kuvaa tena magwanda yake badala ya kanzu za hospitali. Akainua mkono wake ili auguse uso wake ambao alikuwa hajaugusa kwa muda mrefu. Alichokigusa kilimtisha. Alihisi kushika kitu zaidi ya uso wake, kitu baki kabisa, kitu kikavu na kinachokwangua kama kisiki. Ni kitu gani? Akagutuka. Hofu ilimshauri kutoka nje upesi. Huko pia alikutana na mwujiza. Watu wote aliofahamiana nao si walimtazama kwa hofu na mshangao tu, bali pamoja na dalili zote za kutomjua. Akaduwaa kwa muda, kisha alirejea ndani upesiupesi. “Kioo” alifoka akiangaza huku na huko. Ndipo alipokumbuka kioo kilichokuwa bafuni. Hima, akaelekea huko. Alipofika akasimama mbele ya kioo kujitazama. Mbele yake alimwona mwanajeshi mwingine kasimama akimtazama. Kilichomshangaza ni uso wa mtu huyo. Hakujua kama ulistahili kuitwa uso au vipi. Ulikuwa kama kinyago ambacho kilichongwa kwa makosa, kinyago chenye kovu zito na jeusi nusu ya uso mzima, jicho moja, hali la pili limetoweka na nafasi yake kuchukuliwa na kovu hilo, pua lilipondwa na nusu iliyosalia kuinamia upande, mdomo wa juu ukiwa umeng’oka, hali wa chini umerudishiwa kwa kushonwa na shavu ambalo lilisinyaa na kukauka kabisa. Kwa mshangao, Sikamona aliinua mkono kukuna kichwa. Akashangaa zaidi alipoona mtu huyo akifanya vivyohivyo. Kisha akaelewa. Alikuwa akijitazama mwenyewe katika kioo. Mtu wa kutisha alikuwa







yeye!

Ndipo alipoangua kicheko na kuondoka.

Alipofika kambini kwake, Gulu, alilakiwa na nyuso zilezile za mshangao. Hakujali. Alicheka na kuingia hemani ambamo alipata silaha na kutoka tena haraka. Aliifuata njia ileile ambayo alimnyemelea yule adui. Akafuata uchochoro uleule. Hatimaye, akawasili katika msitu wenyewe. Aliufahamu kwa kuona miti ilivyoumia kwa ukali wa risasi. Ni hapo ambapo aliupoteza uso wake. Ni hapo pia ambapo alikusudia kuupoteza uhai wake. Vinginevyo angewezaje kuishi katika hali hii? Angewezaje kustahimili mishangao ya watu? Angewezaje kutazamana na watu waliomjua? Ndugu zake, rafiki na zaidi ya wote Rusia! Mpenzi wake.

Alifahamu fika kuwa amekwishampoteza. Huu si uso ambao ulimfanya Rusia ampende. Hivyo, ni uso ambao utamfanya amdharau. Akajaribu kujikumbusha sura yake ilivyokuwa. Hakuweza kuikumbuka. Ilikuwa imekwishamtoka hata akilini. Alichofahamu peke yake ni kwamba alikuwa na sura nzuri, sura inayowavutia wasichana na kuwababaisha akina mama, sura ambayo ilimfanya Rusia ampende tangu walipoonana kwa mara ya kwnanza. Mara ngapi aliwaona wasichana wakimtazama kwa tamaa? Mara ngapi aliwafumania akina mama wakiteta kuwa ana sura nzuri? Ni yupi tena atakayemtazama kwa namna hiyo? Nani atakayewaza kuwa alikuwa na sura nzuri? Amepoteza kila kitu. Ameupoteza







uzuri, ameupoteza ujana na amempoteza mpenzi.

Jioni ile ambayo kamwe uwa haimtoki akilini ikamrudia tena mawazoni.

Alikuwa amejilaza juu ya kitanda chake akisikiliza redio. Kisha, ikamjia ile hamu yake ya sikuzote, hamu ya kumwona Rusia. Alikurupuka toka kitandani hapo na kumfuata nyumbani. Kwa bahati walikutana njiani. Rusia alikuwa akimjia, pengine kwa kiu ya kumwona vilevile. Wakarudi hali wameshikana mikono, maongezi na tabasamu za Rusia ziliifanya safari yao kuwa fupi zaidi. Walipofika ndani Rusia alijitupa kitandani kujipumzisha. Sikamona akamfuata na kujilaza pembeni yake. Kama kawaida tabasamu la Rusia lilimlaki. “Joto,” Sikamona alinong’ona akivua nguo zake. “Vipi ukilivua hilo gauni Rusia?” Rusia akatii. Ngozi yake laini, nyeusi ilimeremeta kwa namna ambayo iliufanya moyo wa Sikamona upoteze baadhi ya mapigo. Uso wake vilevile, ukisaidiwa na tabasamu laini, ulimfanya aonekane si malaika mzuri tu, bali pia ua zuri lililochanua ambalo linaalika nyuki na vipepeo. Yeye alijisikia kama nyuki anayealikwa. Subira ikamtoka. Akajikuta akimsogelea Rusia na kumkumbatia. Joto la mwili na ngozi laini, matiti yake mororo kifuani na tabasamu lake vilimfanya Sikamona ajihisi mwili wake ukitaka kutoka nje ya ngozi yake. Akapiga hatua ya pili. “La, la, la, Sika, tafadhali…” Rusia alisema bila kumsukuma. Sauti yake haikuwa na hasira, lakini tabasamu lilikuwa limeuacha uso wake.







“Tafadhali Rusia,”

“Hapana. Sio leo, Sika.”

“Kwa nini?” sauti yake ilikuwa na uchungu. Rusia alimtumbulia macho yaliyojaa aibu. Kisha akamwuliza kwa sauti ndogo, “Hujui mwenzio bado bikra?” maelezo ambayo yalimfanya Sikamona si azidi kumpenda tu, bali pamoja na kumheshimu kuliko wasichana wote aliowafahamu. Akaairisha chochote alichokusudia kukifanya. Ndipo tabasamu la Rusia liliporejea. Likamfariji. Wakatulia hali wamekumbatiana, wakiisubiri siku halali kwao wote.”

Kumbe haikutokea siku hiyo. Mapenzi yao yalikuwa yamefikia ukingoni. Ilikuwa kama ndoto, ndoto nzuri ya kupendeza, lakini ndoto ambayo ingeendelea kuwa ndoto. Siku hiyo ingesalia kama kumbukumbu tu katika maisha yake, kumbukumbu katika roho yake. Kumbukumbu ambayo itaandamana naye kaburini na kuishi naye huko kuzimu.

Akairekebisha bunduki yake na kuilekeza kichwani kwake. Akajiandaa kuifyatua. “Kwa heri dunia, kwa heri Rusia…”

“Sikamona.”

Sauti hiyo, kali yenye amri, ilimfanya asite kuifyatua bunduki yake na kugeuka. Alikutana na uso wa Brigedia Chungu pamoja na askari watatu nyuma yake.

“Usifanye hivyo Sikamona” Brigedia alisema
 
35.
walipomfikia. “Sisi tumekuchukulia kama shujaa wetu. Lakini unataka kuuharibu ushujaa wako kwa kujiua. Kujiua ni kitendo cha uoga. Ni tabia ya kukata tamaa. Wewe umekwishaudhihirisha ushujaa wako. Umewashinda maadui zako. Vipi uipoteze heshima yako, kijana? Usiliharibu bure jina lako, bwana mdogo. Huna sababu ya kufanya hivyo. Tafadhali turudi kambini.”

Sikamona akageuka na kuwafuata.

Hakuna sababu ya kujiua? Pengine sura hii ni shahada ya kazi aliyoifanya? Rusia amemkosa, amempoteza. Hayo hakuwa na shaka nayo. Ambacho hakupenda ni kuyaona machozi yake. Asingekuwa tayari kushuhudia maombolezo ya kifo cha mapenzi yao. Hivyo, akaamua kumkwepa maisha yake yote.












HATIMAYE, ule wakati ambao aliuogopa na kuuhofia kuliko nyakati zote ukawa umewadia ,wakati wakukutana macho kwa macho na Rusia akiwa

katika hali hii, wakati ambao hakutaka utokee.

Lakini kumbe hofu yake ilikuwa ya bure. Haikutokea kama alivyotegemea. Rusia si kwamba asingemkubali tu, bali alikuwa amemdharau kiasi cha kumcheka hadharani. Hayo yaliuzidisha msiba wake rohoni na moyoni. Yako wapi machozi ambayo alitarajia kuyaona katika uso wake? Iko wapi huzuni ambayo alidhani ingemkumba? Alikuwa amekosea. Alikosea kila aliloliwaza. Uchungu wa kujua hilo ndio uliomfanya aanguke na kuzirai. Aliporudiwa na fahamu alishangaa kumwona Rusia bado kasimama palepale akimtazama.

“Rusia… kweli Rusia unanicheka?” alifoka kwa







sauti kubwa. “Si kitu. si kosa langu wala lako. Nakuomba jambo moja la mwisho, ondoka mbele yangu na hakikisha hatuonani tena maishani. Nenda.”

Maneno ya Sikamona yakazidi kumshangaza Rusia. Amekuwaje? Akajiuliza. Sikuzote, tangu Sikamona alipoondoka amekuwa akiisubiri dakika hii kwa njaa kubwa, dakika ya kukutana naye tena. Aligundua hilo mara tu baada ya kuondoka kwake. Wala haikuwa hilo peke yake, bali pamoja na kufahamu kikamilifu kuwa asingeona faraja yoyote katika maisha, pasi ya kuwa na Sikamona.

Zamani, kabla hajakutana naye aliishi katika dunia yake peke yake, dunia isiyo na haja ya mpenzi wala mapenzi. Katika dunia hiyo vijana kadha wa kadha wenye kila hali, wakitumia kila aina ya lugha, walimjia na kumtaka mapenzi. Hakukubali. Hakukubali, si kwa kuwa hakutaka tu, bali kwa sababu hakuona hata hicho walichokitaka ni kipi. Maneno yao ya kubembeleza yalipozidi ndivyo alivyozidi kuwachukia. Vitendo vyao vya kumwonyesha mapenzi, yeye vilimfanya awakinai na kuwaona kama wendawazimu.

Lakini alipotokea Sikamona yote hayo yalitoweka katika fikra zake. Huyu hakumtongoza wala kumwonyesha chochote, lakini umbo lake, alipojitokeza mbele yake kwa mara ya kwanza, liliuondoa moyo wake pale ulipokuwa na kuuweka panapostahili, mahali penye njaa na kiu. Si kiu ya maji wala njaa ya chakula. Wala haikuwa njaa ya kupendwa ama kiu ya mapenzi la, ilikuwa kiu ya







kuwa na Sikamona daima, kiu ya kuisikia sauti yake mara kwa mara na njaa ya kuuona uso wake tena na tena. Kiu na njaa hiyo vilikuwa vikitoweka kila walipokutana, akajisikia furaha na faraja kubwa ambayo si kwamba vilimfanya ayapende maisha tu, bali pamoja na kuiona thamani yake.

Hivyo, kipindi hiki ambacho Sikamona alikuwa vitani, Rusia alikuwa taabani akimfikiria. Mara kwa mara alikuwa akizinduka usingizini huku akitetemeka kwa hofu iliyotokana na ndoto mbaya ambazo zilimtisha juu ya maisha ya Sikamona. Hofu yake kubwa ilikuwa pale alipokumbuka kuwa alikuwa ameshiriki kwa njia moja au nyingine kumshawishi Sikamona kwenda huko. Ni hapo alipoapa kuwa kama Sikamona asingerudi, basi angemsubiri hadi ahera ambako wangetimiza ahadi yao.

Wakati mwingine alipata ndoto za kuvutia. Alijiona akiwa na Sikamona katika bustani nzuri zenye maua ya kupendeza, wakiwa wameketi na kukumbatiana. Lakini alipoamka na kujikuta kakumbatia mto badala yake, hofu ilikuwa ikimrudia na machozi kumtoka.

Leo hii, alipopata habari kuwa mashujaa wanarudi, alikuwa wa kwanza kuwahi katika ukumbi ule, muda wote akiangaza macho huku na huku kumtafuta Sikamona. Vipi basi baada ya kumpata akiwa salama, awe na vituko visivyoeleweka? Alijiuliza kwa uchungu na mshangao.

Kwa mshangao huo alimtumbulia macho







Sikamona, macho ambayo yalimshinda nguvu Sikamona, hata akajikuta ametulia akiyatazama, kinyume cha matakwa yake. Kila kitu kilikuwa wazi katika macho hayo, jambo ambalo lilimfanya Sikamona ajikute amemwangukia Rusia kifuani na kumkumbatia kwa mara nyingine, huku kilio cha kwikwi kikimtoka taratibu.

“Mpenzi,” Rusia alikuwa akinong’ona kwa sauti dhaifu. “Nilikuahidi zawadi… Zawadi ya ushindi… ipokee zawadi yako, tafadhali. Nipokee. Tangu leo, mie wako… ukitaka nimeze, ukitaka nitafune…”

Sikamona hakuyaamini masikio yake. Ni kweli kuwa alimwamini rusia na kuliamini kila neno lake. Lakini hakuamini kama bado kulikuwa na uwezekano huo. Kwa nini ampe taabu, aibu ya maisha, msichana huyo mpole? Kwa nini aendelee kuwa kichekesho mitaani na simulizi ofisini maisha yake yote?

“Haiwezekani Rusia,” aliropoka. “Yaliyopita yamepita. Ilikuwa ndoto nzuri… tuendelee kuiacha iwe ndoto. Tusiiharibu…” alimaliza akijikwanyua na kuanza kuondoka tena.

“Sika… tafadhali…” Rusia alisema akizidi kumshikilia mkono. “Sika… sika… mbona sikuelewi?”


TAMATI


Imedhaminiwa kwa hisani ya BURE SERIES
 
Back
Top Bottom