Anga la washenzi na Joana anaona kitu usiku

Anga la washenzi na Joana anaona kitu usiku

*ANGA LA WASHENZI -- 16*
*Simulizi za series*


ILIPOISHIA...

Alisogelea dirisha la sebule, akachungulia ndani. Hakumuona Jona, ila akamuona mwanaume aliyeketishwa kwenye kiti na kufungwa kamba. Hakumtambua mwanaume huyo kwani alikuwa amezibwa na kinyago usoni.
Lakini kinyago hicho kikamgutua. Kilikuwa ni cheusi chenye umbo la fuvu la binadamu. Alikumbuka Miranda aliwahi kumwambia kukihusu. Ya kwamba mwanaume yule aliyemvamia kuchukua kamera, alikuwa amekivaa.
Ina maana ndo’ huyu? Akajiuliza. Anafanya nini hapa akiwa amefungwa kamba?
ENDELEA...

Sasa kidogo Kinoo akaanza kuelewa kwanini Miranda alimwambia 'mchoraji' yule, ambaye ni Jona, hakuwa mchoraji tu, ni mtu mwenye ngebe za mafunzo na ujuzi.
Hakutaka kuingia ndani haraka bali ausome kwanza mchezo, Jona yupo wapi? Na anamfanya nini huyu mtu aliyeonekana dhahiri kuwa mateka?
Akatulia kungoja. Kwa dakika kama nne pasipo kuona wala kusikia jambo la kulituhumu.
Alikuja kushtuka aliposikia chuma cha baridi kisogoni mwake, na sauti ya Jona ikamuamuru:
"Tulia hivyo hivyo! - mikono juu!"
Akatii amri. Kwa uzoefu wake alishajua ni mdomo wa bunduki ndiyo ambao upo kisogoni. Ila alikuwa mkaidi kuwa mpole kirahisi.
Akaanza kufikiri ni njia gani inaweza kumuokoa akaushika mchezo.
Ila kama vile alishtukiwa, akaonywa:
"Ukijitia mjanja, nakutoboa kichwa!"
Akatulia tuli, macho yake yakiangaza angaza kana kwamba mtu mwenye haraka atafutaye ufunguo wa gari.
"Haya ongoza ndani!" Jona akaamuru. Pasipo kubisha, Kinoo akaanza kuchukua hatua kusogelea mlangoni.
Kichwani mwake alitafakari ilikuwaje akadakwa kirahisi hivyo? Alijiona mjinga na mzembe pia.
Endapo asipofanikisha hili, Miranda ataenda kumlaumu sana. Kumtusi na kumshusha vyeo.
Hivyo lazima apate namna.
Alipokaribia mlangoni, upesi akakisogeza kichwa chake kukwepa mdomo wa bunduki kabla Jona hajafanya lolote.
Kisha akautwaa mkono wa Jona na kujaribu kuupoka silaha.
Wakavutana huku na huko nguvu zikitumika. Kinoo akamzidi nguvu Jona, akaiteka silaha akimsukumizia kando mpinzani wake.
Ila kabla hajafanya kitu na bunduki hiyo, Jona akautuma mguu wake, haraka sana, kuutengua mkono wa kulia wa Kinoo uliobebelea bunduki.
Bunduki ikaangukia chini!
Wote wakaitazama kwa macho ya ashki ila wasithubutu kuinamisha migongo yao kwa kumhofia mwenziwe.
Kuinama kunamaanisha kumpa fursa adui akutende atakavyo, hilo kosa hakuna aliyetaka kulifanya.
Wakaachana na bunduki wakitazamana kama mafahari ya ng'ombe ndani ya zizi. Walikunja ngumi wakitegeana.
"Niliwapa onyo, naona hamjataka kulisikia!" Alisema Jona akimkazia macho Kinoo.
"Wewe si wa kutupa sisi onyo. Bado huna hadhi hiyo," Kinoo akajibu kwa dharau kabla hajaguna.
Jona akatabasamu asitie neno. Alipanga matendo yake yaongee sasa na si sauti ya mdomoni.
Kimwili alikuwa mdogo ukimlinganisha na Kinoo, na alijua hilo lina faida na hasaraze. Endapo akiingia mikononi mwa Kinoo basi itamuwia vigumu kuchoropoka.
Faidaye, Kinoo atakuwa mzito kufanya mashanbulizi. Miili mikubwa huchukua hatua kubwa kushurutisha viungo.
Basi akajipanga vema kutumia hiyo faida.
Akachokoza pambano kwa kurusha ngumi mbili za haraka, Kinoo akazikwepa kisha akatuma ngumi yake nzito. Jona akayeya! Ikapita.
Akatuma nyingine na nyingine, Jona akazikwepa kama mchezo wa rede.
Kwa nusu dakika, akausoma mchezo, akapata alichokuwa anakitaka.
Kinoo hakuwa mzuri kwenye kujilinda, alikuwa mzito kukwepa, na alikuwa akiziacha mbavu zake wazi mara kwa mara.
Bila shaka alikuwa anategemea zaidi kushambulia kuliko kujilinda.
Jona akaanza kucheza na mbavu za mwanaume huyo, akilenga kumtepetesha na kumminya uwezo wa kuhema.
Kinoo akarusha ngumi zake kwa mfululizo, Jona akawa anakwepa kisha anakita mbavu za Kinoo kwa ngumi za upesi.
Kila alipopata mwanya, basi akafyatua ngumi tatu ama nne!
Ikafikia mahala Kinoo akachoka kwani alikuwa anatumia nguvu nyingi kurusha ngumi zilizokuwa zinaenda patupu. Ukijumlisha na ngumi alizokuwa antekenywa mbavuni, akashindwa kufua dafu.
Alikuwa hoi bin taaban.
Alikuwa anatamani kuhema kwanguvu, lakini mbavu haizikuruhusu. Ni kama vile alipewa pumu.
Ni wazi alikuwa ameshindwa, ila hakutaka kuingia kwenye mikono ya adui, hivyo basi akatoroka kwa kukimbia.
Aliruka ukuta akazama ndani ya gari lake na kuhepa kwa kasi!
Jona alihofia kufyatua risasi kutoshtua majirani. Hakutaka kuwapa hofu wala makisio na mahisio yoyote juu yake na mambo yake.
Basi akamwacha Kinoo aende. Huko akafikishe habari aliyokumbana nayo.
Yeye akarudi zake ndani na kumtazama Bigo. Akampuuzia na kuendelea na mambo yake. Akaoga na kisha akajipeleka chumbani alipojilaza akiendelea kunywa.
Bigo aliachwa palepale kwenye kiti.

***

Kadiri usiku ulivyokuwa unasonga ndivyo na tafrija ilivyokuwa inanoga.
Sasa ilikuwa ni saa tano inayoelekea saa sita usiku na muziki laini ulikuwa unaburuza eneo wageni wakiserebuka.
Ndani ya eneo hili lililokuwa limesheheni taa kali zilizogeuza usiku kuwa mchana, kulikuwa kuna walinzi kedekede wakiwalinda wanaume na wanawake waliokuwa humo tafrijani.
Watu hawa walikuwa ni 'vibopa', watu wazito wenye nyadhfa zao serikalini ama mahala pengine nyeti kiuchumi.
Karibia wanaume wote walikuwa wamevalia suti, zikipishana tu rangi. Wanawake 'wakila' magauni ya kupendeza na michuchumio ya haja.
Nyuso za wanawake hawa zilikuwa zimerembwa kwa 'make-up' zilizofiti usoni. Waling'aa kama malaika, ila hawagusa kwa mwanamke Miranda.
Alikuwa amependeza haswa. Pia na kujiamini kwake pamoja na kujua kwenda na muda, kulimfanya avutie zaidi.
Kila muziki ulipowekwa alijua kwenda na mapigo. Alifanya watu wamtazame na pia kumwongelea wasijue mwanamke huyu alikuwapo kazini, na lengo lake lilikuwa kumtia kimyani mheshimiwa fulani.
Muziki ulikata, wakarejea kwenye viti vyao. Miranda alikuwa ameketi na BC meza moja. Meza iliyokuwa imechafuliwa kwa vinywaji.
Meza yao ilikuwa inatazamana, kwa umbali kidogo, na meza aliyokuwa ameketi mheshimiwa Boka, waziri wa Afya. Mwanaume mnene mweusi mwenye kitambi kama kiroba cha mihogo.
Alikuwa amevalia suti na tai ya bluu. Mezani alikuwa pamoja na mwanamke fulani mnene, pasi shaka mkewe, pia na kijana mmoja wa kiume mwenye kadirio la miaka ishirini na saba - nane - tisa.
"You did great!" (Umefanya vizuri!) BC alisema akitazama meza ya mheshimiwa Boka. "He was really impressed, now we've to figure the way out to reach him." (Aliguswa sana, sasa tunatakiwa tutafute njia ya kumpata.)
"The problem is his wife," (shida ni mkewe,) alisema Miranda akikunja shingo kutazama penye lengo. "She's very close to him as if she knows our intention. But I will get the way out!" (Amemganda sana kana kwamba anajua lengo letu. Lakini nitapata namna!)
Miranda aliposema tu hivyo, akanyanyuka akijifanya anatengenezea nguo yake vizuri. Mheshimiwa akamtazama, naye akamtazama kukutanisha macho.
Akatabasamu na kutazama kiaibu. Mheshimiwa naye akatabasamu kujibu.
Miranda akaketi. Sasa akajua dhahiri mheshimiwa Boka atakuwa anatazama tazama mezani kwake baada ya hilo tukio.
Basi hakujiweka mbali. Akawa anampa mheshimiwa macho na kajitabasamu.
"The bird's fallen into the trap!" (Ndege ameangukia mtegoni!) Akasema Miranda kwa tabasamu.
"Now take it!" (Sasa mchukue!) BC akashadadia.
Punde Miranda akanyanyuka, akamtazama mheshimiwa, kisha akayaelekezea macho yake upande wa maliwatoni.
Alafu akaelekea huko akitembea kwa madaha ya walimbwende jukwaani. Mheshimiwa akamsindikiza kwa macho ya ukware.
Naye, isichukue muda, akanyanyuka aende huko huko maliwatoni. Basi wakakutana na Miranda kwenye korido.
Mwanamke huyo alikuwa anahangaika na zipu ya gauni huko mgongoni, akijinasibu anahangaika kuifunga.
"Naweza nikakusaidia?" Mheshimiwa Boka akapaza sauti akitabasamu.
'Naona umejileta mwenyewe boya wewe!' Miranda akasema kifuani. Aligeuza uso wake kutazama, akakutana uso kwa uso na waziri. Akaigiza aibu.
"Hapana, ahsante mheshimiwa," akajibu akitabasamu.
"Aaaah bwana mrembo kwanini upate shida hivyo na mie nipo?"
Miranda hakusema kitu. Alitabasamu tu akaendelea kuhangaika na zipu yake. Basi mheshimiwa akaamua kujisogeza, alichukulia ukimya kama 'ndio', akadaka zipu ya Miranda na kuipandisha juu pasi na tabu.
"Ahsante sana, mheshimiwa, na samahani kwa usumbufu!"
"Usijali, mrembo. Unaitwa nani wewe?"
"Flaviana," Miranda akajibu akitazama chini.
"Oooh jina zuri kweli!"
"Ahsante."
Mheshimiwa akatazama mazingira, akajiona wapo wenyewe. Ila alijua fika hawatadumu kwa muda mrefu hapo. Aidha mkewe aje, ama watu wengine waliobanwa na haja, basi akaamua afanye mambo upesi.
"Sasa mrembo nataka tupate nafasi ya kuongea vizuri na wewe. Vipi sasa nitakupataje? - una simu?"
"Ndio ninayo."
"Sawa sawa!" Mheshimiwa akajipekua mfukoni, akatoa kadi ya biashara na kumkabidhi Miranda.
"Utan'chek basi, sawa?"
Miranda akatikisa kichwa. "Sawa, mheshimiwa, n'tajitahidi."
Mheshimiwa akatabasamu na kujilamba lips, akatoka maeneo ya maliwato na kurudi kwenye meza yake.
Baadae kidogo napo Miranda akarudi zake kukutana na BC. Akamwonyeshea kadi aliyopewa na mheshimiwa.
"That's a very big step!" (Hiyo ni hatua kubwa sana!) BC akasema akimpongeza Miranda kwa kumpa mkono. "We have already put him in our store." (Tayari tumeshamtia kwenye ghala.)
Sasa wakanywa kwa furaha wakiendelea kupanga na kusuka mipango yao.
Walikuwa na matumaini makubwa ya kumtia mikononi mheshimiwa Boka, na lengo lao kuu ni kumtumia kiongozi huyo wa kitengo cha Afya kusafirisha mizigo yao kwa kutumia kibali chake.
Huyu kwake alikuwa na faida kubwa kuliko mheshimiwa Eliakimu kwani yeye anahusika moja kwa moja na mambo ya madawa.
Lakini pia gharama yake itakuwa ndogo ama hamna kabisa kwasababu ya kumtumia Miranda kama chambo.
Wakiwa wanelekea ukingoni wa tafrija na sasa wakiwa wanajiandaa kuondoka zao,kwa amani kabisa maana hawajaupoteza usiku, mara kwa mbele yao wanamuona mke wa Mheshimiwa Boka akija.
Kabla hawajafanya kitu, mwanamke huyo alikuwa mbele yao akishikilia kiuno.


*MKE WA MHESHIMIWA ANATAKA NINI?*

*MIRANDA ATAFANIKIWA KUMRUBUNI MHESHIMIWA?*

*VIPI KUHUSU KINOO NA BIGO?*



USIKOSE SEHEMU IJAYO.


*Simulizi za series*
 
*ANGA LA WASHENZI --- 17*

*Simulizi za series*


ILIPOISHIA

Lakini pia gharama yake itakuwa ndogo ama hamna kabisa kwasababu ya kumtumia Miranda kama chambo.

Wakiwa wanelekea ukingoni wa tafrija na sasa wakiwa wanajiandaa kuondoka zao,kwa amani kabisa maana hawajaupoteza usiku, mara kwa mbele yao wanamuona mke wa Mheshimiwa Boka akija.

Kabla hawajafanya kitu, mwanamke huyo alikuwa mbele yao akishikilia kiuno.

ENDELEA…

“Habari binti?” alimsalimu Miranda, kisha akatabasamu.

“Safi, sh’kamoo.”

“Marhaba, umenifurahisha sana. Umeufanya usiku wangu kuwa wa kumbukumbu.”
Miranda akatabasamu.

“Nashukuru sana mama.”

“Usijali, sasa kuna jambo moja nilikuwa nataka tutete mimi na wewe, ningepata faragha?” Alisema mke wa mheshimiwa akimtazama BC. Miranda naye akamtazama BC kabla hajajibu akipandisha mabega.

“Sawa, hamna shida.” Kisha wakasogea kando kidogo.

“Sina malengo ya kukuvunjia heshima, ila nimependezwa nawe na nikaona nastahili kukushirikisha hili kama utakuwa umevutiwa. Unapendelea mambo ya modeling na ulimbwende?”

“Aaaahmm …kiasi.”

“Nina kampuni ya ulimbwende na modeling ambayo inahusika moja kwa moja na mambo ya vipodozi na marashi. Ningependa kufanya kazi na wewe.”

Kidogo Miranda akabanwa na kigugumizi.

“Sitaki unipe jibu lolote kwa sasa, ni jambo nililokushtukiza. Chukua muda wako na ufikirie, utanipatia jibu.”

Mke wa mheshimiwa akafungua pochi yake, akatoa kadi na kumkabidhi Miranda.

“Unajua sikuwa na wazo lolote lile mpaka pale mume wangu aliponishtua na kunishauri. Ni kweli nilivutiwa nawe sema akili yangu ilikuwa kiparty-party zaidi.” Mke wa mheshimiwa alinena akitabasamu.

“Ahsante sana, mama. N’taona namna itakavyokuwa,” akasema Miranda kisha wakapeana mikono na kuagana. Miranda akamrudia BC wakaondoka zao kuelekea kwenye gari.

Miranda akamueleza BC juu ya yale mke wa mheshimiwa aliyomwambia.

“It might be an opportunity.” (Yaweza kuwa fursa) BC alisema akitazama mbele, kisha akauliza: “Do you have any helpful idea from that?” (Una wazo lolote lenye tija toka kwenye hilo?”

Miranda akaminya lips. “Perhaps it may spark later, but for now I take it as a chance for me to be officially closer to Mr. Boka.” (Pengine laweza kutokea baadae, lakini kwa sasa naichukulia kama fursa ya mimi kuwa rasmi karibu na bwana Boka.)

“Yes, but you never know as you will be closer to the wife as well. This game becomes very thrilling, we have to win something out of it!” (Ndio, lakini huwezi jua maana utakuwa karibu na mke vilevile. Huu mchezo unakuwa mzuri zaidi, na tunatakiwa kushinda jambo toka kwenye hilo!”

Miranda hakusema kitu, alikuwa kimya akitafakari.

Gari lilinguruma pasipo watu kuongea mpaka wanafika getini mwa makazi ya Miranda ambapo wanaagana, na Miranda anaingia ndani baada ya kufunguliwa mlango na mlinzi.

“Kuna mgeni yoyote amekuja hapa?”

“Hapana, mam, hamna!”

“Kabisa?”

“Ndio, yupo tu Kinoo.”

“Sasa huyo si mgeni?”

“Samahani, mam, nilidhani labda unaulizia mgeni mgeni yani…”

“Amekuja saa ngapi?”

“Mida kama ya saa tatu hivi kama nipo sahihi.”

“Hajaja na gari?” Miranda aliuliza akiangaza angaza.

“Hapana, alikuja na bodaboda.”

“Alikuwa amebebelea kitu chochote mkononi?”

“Hapana, sijaona zaidi ya simu.”

Miranda akasonya, kisha akanyoosha hatua zake ndefu kuelekea ndani. Alimkuta Kinoo akiwa amejilaza juu ya kiti akijikunyata kana kwamba anahisi baridi kali. Usoni mwake alikuwa na majeraha, na hakuwa nadhifu.

Akamwamsha.

“Vipi, mbona hivi? – umechukua picha?” Akauliza maswali kwa mkupuo. Kinoo akayajibu kwa kutikisa kichwa chake kukataa. Hakutia neno.

“Hujafanikiwa?” Miranda akatahamaki. Alikunja sura yake na kushika kiuno. Akashusha pumzi ndefu kabla hajakaa.

Yalikuwa ni majira ya saa nane usiku sasa. Kulikuwa kimya, kwa mbali kulikuwa kunasikika vijisauti vya vijibwa vikibweka.

“Sijafanikiwa kupata picha,” alisema Kinoo akitazama chini. Alimweleza Miranda namna mambo yalivyotukia ndani ya eneo la tukio. Miranda akashangazwa.

“Nilikuambia Kinoo, na hukutaka kunisikia!”

“Nini sijakusikia?”

“Nilikwambia yule si msanii tu wa kawaida, ni mtu mwenye mafunzo na ujuzi. Ila wewe ukapuuzia, kwa namna ulivyomshambulia ni kana kwamba ulienda kumkamata konda wa daladala!”

Kinoo hakusema kitu, alikuwa anatazama tu chini.

“Huyu mtu ni nani?” Miranda aliuliza akisimama. Aliweka mikono yake nyuma akitambaa na tafakari. “Huyu mtu ni nani haswa? Ni mchoraji tu? Kwanini Bite alimchagua kufanya naye kazi? Kutakuwa kuna sababu yoyote ama ni bahati tu?” Miranda aliteswa na maswali.

Kinoo alimtazama akamwambia:

“Kama ulivyosema hapo awali, mchoraji atakuwa anafuatiliwa na wale watu waliokuja hapa kuteka kamera. Na pasipo na shaka, wao ndiyo watakuwa wanahusika na mipango ya kumuua kwa kutumia gari kama mchoraji alivyokuja kushtaki hapa.”

“Wanataka kumuua,” Miranda alisema akitikisa kichwa. “Wanataka kummaliza, ina maana wanajua mchoraji huyo ana picha hatarishi kwao.”

“Ndio.”

“Sasa tutapataje picha Kinoo? Picha hiyo muhimu sana!”

“Nina wazo – kwanini tusikae meza moja tukaongea na mchoraji yule?”

“Oooh umeona sasa kile nilichokuwa nasema – si kila mara nguvu yatakiwa. Lakini mashaka yangu ni kwa huyo mchoraji, sijui kama atakubali.”

“Nadhani ameshajua sisi hatuhusiki na jaribio la kumuua, anaweza kukubali.”

“Sawa, ila akikubali atataka kujua kuhusu hiyo picha. Atataka kufahamu ina nini na kwanini inatafutwa. Huoni kama hilo ni tishio?”

“Kwani akijua kuna nini?”

“Hapo ndipo mimi naanza kushindwana na wewe. Wewe unajua kilichomo kwenye ile picha?”

“Hapana.”

“Unajua imechorwa nini?”

“Labda…”

“Labda nini? Hatuna uhakika, na pengine tunaweza tukaipata na bado tukashindwa kuing’amua. Endapo kama ina siri kubwa, na ndivyo inavyoonekana kutokana na utafutwaji wake, tutafanyaje? Tutamuua?”

Kinoo kimya.

“Ebu niache nilale. Siku ya leo ilikuwa ndefu sana kwangu,” Miranda alisema akielekea zake ndani ya chumba.

Hakutoka.



***



“Leo unaonekana upo bize kweli ndugu yangu,” Jumanne alimwambia Jona akimshika bega.

Yalikuwa ni majira ya saa mbili asubuhi ndani ya ofisi. Siku ilikuwa imejazwa na shughuli kama kawaida. Magari lukuki yalikuwa yanakatiza huko barabarani kama ilivyo kwenye barabara nyingi ndani ya jiji la Dar es salaam.

“Ni kweli, nimetingwa kidogo,” Jona akamjibu Jumanne pasipo kumtazama. Siku hiyo alikuwa amekuja na tarakilishi yake mpakato na ndiyo alikuwa anahangaika nayo tokea alipokuja.

Pembeni ya tarakilishi hiyo kulikuwa kuna kakibahasha kadogo cheupe, ndani yake kulikuwa kuna picha aina ya pasipoti. Picha moja ilikuwa imetokezea kwa nje.

Jumanne alikuwa anataka kutoka akapate kifungua kinywa, ila akaangaza kidogo alichokuwa anakifanya mwenzake, kile kilichomchukulia muda namna ile.

Akaona Jona yupo mtandaoni, akisoma soma baadhi ya Makala na kupitia baadhi ya picha. Jumanne akapuuzia, ila kabla hajaenda, akaona picha ile iliyokuwa imejitokeza toka kwenye kibahasha.

Aliitazama picha hiyo kwa umakini, haikuwa ngeni. Aliisogelea akaikodolea vema kabla hajamwomba Jona ruhusa ya kuichukua na kuisogeza machoni.

“Unamjua huyo mtu?” Jona akamuuliza Jumanne. Kwa mara ya kwanza aliacha mashine yake akamtazama mwenzake.

“Nahisi kama namjua. Umeitoa wapi?”

“Kuna mtu tu amenipatia. Vipi? – ulimuonea wapi?”

Jumanne alivuta kiti akaketi. Akaendelea kutazama picha hiyo akivuta kumbukumbu.

“Oooh! Sasa nimekumbuka.”

“Ni nani?”

“Huyu ni marehemu Fakiri – aliyewahi kuwa mfanyabiashara mkubwa wa samaki. Alikuwa anasafirisha samaki wa maji chumvi mikoa yote ya Tanzania. Mpaka huko Kongo, Rwanda na Burundi.”

“Ni marehemu?”

“Ndio. Aliuawa mwaka jana.”

“Aliuawa na nani?”

“Aaaah Jona! Unadhani mie n’tajulia wapi sasa? Nawe waniuliza maswali utadhani kachero wa polisi.”

Jona akatabasamu pasipo kutia neno.

“Mie naenda kunywa chai, mzee. Baadae,” Jumanne aliaga akaenda. Joh akaichukua ile picha aliyokuwa anaitazama Jumanne, akaitazama na yeye.

“Fakiri …” Jona alijikuta anaongea mwenyewe. Alitazama nyuma ya picha, akaona maandishi yale ya kichina ambayo yapo kwenye picha zote.

Akaweka picha pembeni na kurejea mtandaoni kwenye injini ya kusaka majibu. Akaandika: ‘Mauaji ya Fakiri’ alafu akabonyeza kitufe cha ‘ok’. Punde majibu yakaja kibao, akaanza kuyapitia moja baada ya moja.

Fakiri aliuawa kwa kunyongwa siku ya tarehe 12, desemba 2016 maeneo ya nyumbani kwake Masaki. Ameacha mjane na mtoto mmoja, ambaye naye alikuja kuuawa juma moja tu baada ya baba yake, yeye akiuawa kwa risasi.

Mpaka sasa hakuna yeyote anayeshikiliwa na polisi kwa mauaji hayo.

Kama juma moja hapo nyuma kabla ya Fakiri kuuawa, alikuwa akikabiliana na kesi ya ukwepaji kodi. Kesi ambayo ilikuwa inaelekea kumshinda na hivyo basi kutakiwa kulipa limbikizo kubwa la kodi pamoja na faini kubwa. Kwa jumla shilingi za kitanzania milioni mia tano! – nusu bilioni.

Pengine ungweza kudhani Fakiri alijiua kwasababu ya kukwepa fedheha hiyo ya biashara yake kufia mikononi, ila hakujiua! Aliuawa! Ni wazi serikali isingeweza kumuua mtu wanayemdai, tena pesa kubwa hivyo.

Sasa nani alimuua? Na alifanya hivyo kwa malengo gani? Na kwanini mtoto wake naye akauawa? Maswali hayo hayakuwahi kupata majibu toka upande wowote ule.

Ila juu yake hayo, Jona anapata tena swali lingine, mbona picha ya Fakiri ilikuwa ndani ya kibahasha cha Bigo? Ina maana yeye ndiye anahusika na mauaji hayo? Kama ndio, mbona ya mtoto wa Fakiri haipo? Yeye aliuawa na nani?



KAZI INAZIDI KUWA KUBWA, SI KWA JONA, BIGO, WALA MIRANDA NA KINOO? JONA ATAGUNDUA NINI?

JE BADO NADE ANAMFUATILIA JONA, ATAGUNDUA NINI?
NINI HATMA YA MIRANDA NA BOKA NA MKEWE?

MKE WA MHESHIMIWA ELIAKIMU JE?

KUNA NAMNA HAYA MAMBO YAKAWA YANAZUNGUKA MDUARANI?
 
*JOANA ANAONA KITU USIKU --- 14*


*Simulizi za series*



ILIPOISHIA



Akapitiwa usingizi akiwa ameshikilia rimoti ya televisheni.



Kwenye mishale ya saa nane usiku, akashtushwa na hodi mlangoni. Alitazama televisheni, bado ilikuwa inaongea na kuonyesha. Akatazama saa, akaona ni saa nane.


Akatazama mlangoni.
“Nani?”



ENDELEA


Akajiuliza. Haraka mwili wake ukaanza kutetemeka kwa hofu. Aliuliza nani yupo mlangoni ila sauti haikusikika. Ilikuwa kavu iliyokithiri woga.


Haraka akili yake ilikimbia akajiuliza: vipi kama ni Moa? Hayo ndiyo majira yake, saa nane za usiku, ina maana amemfuata mpaka Ubelgiji?


Akijiuliza maswali hayo ambayo yalizidi kumpatiia hofu, hodi ikagongwa zaidi mlangoni. Joana alijikuta hajui cha kufanya zaidi ya kutazama tu.


Alikuwa kama zezeta. Alikuwa kama vile hayupo eneo hilo, haoni ilhali anatazama. Ni kama vile alipooza mwili na macho pekee ndiyo yamebakia yakifanya kazi.


Alishtuliwa na mkono wa mama yake uliomdaka bega na kumtikisa tikisa kama dawa ya mbu.
“We Joana! Joana!”


Akakurupuka kumtazama mamaye kwa macho ya kutumbua.


“Una nini?” mama akauliza. “Mbona nabisha hodi unifungulii? Taa zinawaka mpaka muda huu?”


Joana akamwomba radhi mamaye. Akamwambia hakusikia kwani alikuwa amezama kwenye dimbwi la mawazo. Mama akaketi kitako na kuongea naye mawili matatu.


“Una shida gani Joana? Niambie mama yako nakusikiliza,” mama akasema kwa sauti ya upole akimtazama mwanaye.
Alikuwa amevalia gauni jeupe la kulalia, macho yake yakifunikwa na miwani.
Kabla ya Joana hajasema jambo akaanza kudondosha machozi na makamasi. Akalala begani mwa mama yake na kulia kwa sekunde kadhaa kabla hajasema:


“Mama nayakumbuka maisha yangu ya zamani. Natamani yarudi.”


Mama akambembeleza. Akamsihi kila jambo na wakati wake, maisha yanasonga hayasimami. Inabidi sasa atazame na kuzingatia mbele, si nyuma.
“Najua ni ngumu, lakini inabidi sasa ufungue ukurasa mpya wa maisha yako. Wewe bado msichana mdogo sana. Mambo mengi mazuri yanakungoja mbele. Tazama ndoto zako.”


Maneno hayo yakampatia faraja Joana. Mama alimwomba akalale pamoja naye kwa usiku huo. Na kwakuwa baba hakuwepo, hilo halikuwa na shida, akaenda kulala na mama.


Yakapita majuma mawili. Joana akaanza sasa kurudia maisha yake ya kawaida kwa kuwa mtu mwenye furaha akitabasamu na kucheka toka moyoni. Hata mwili wake ulipata uangavu.
Alikula na kunywa vizuri. Lakini pia akajishughulisha na michezo kwa ajili ya kumnyima muda wa kujifungia ndani na hata kuboresha afya yake.


Akajiunga na klabu moja jijini ambayo alikuwa akiambatana nayo kwenye mchezo wa mpira wa pete. Alikuwa anaupenda mchezo huo toka udogoni, na hata alipourejea ilimchukua muda kidogo tu kuwa sawa.


Kwasababu tatizo lilikuwa pumzi, akawa anafanya sana mazoezi ya kukimbia. Aliunda urafiki na wachezaji wenzake. Akajihisi amekuwa mpya.


Alipokuwa akitoka mazoezini alioga na kujipumzisha. Na kwasababu za uchovu wa mazoezi basi akawa haangaiki kutafuta usingizi. Alilala fofofo.
Baada ya mwezi mmoja klabu yake ikapanga safari ya kwenda Paris – Ufaransa ambapo huko kulikuwa kuna mashindao ya mpira wa pete wa kikanda. Joana alikuwa ni mmoja wa wachezaji ambao walijumuishwa kikosini hivyo ilibidi naye aende.


Akaaga wazazi wake. Mama akampatia kiasi kikubwa cha pesa kikamfae huko aendako.


“Fuata wapi furaha yako ilipo,” mama alimwambia kabla hajambusu na kumkumbatia.


Kesho yake mapema, Joana akaungana na wenzake na kukwea basi kuelekea Paris. Ni safari ya masaa matatu au manne, ila kwakuwa hawakuwa na haraka yoyote ile, wakachukua masaa sita kufika.


Walikuwa wanasimama mara kwa mara njiani, kula kunywa na hata kupumzika.
Walipozama ndani ya jiji la Paris wenye kamera zao wakatoa na kuanza kumulikamulika huku na kule, mmojawao alikuwa Joana. Alikuwa anahakikisha kila tukio analipata akalitunze kumbukumbuni.


Ila wakiwa wamebakiza umbali mdogo wapate kufika kwenye hoteli wanayotakiwa kuweka kambi, ghafla tairi la basi likapasuka. Gari likaenda mrama kama jahazi ndani ya bahari iliyochafukwa.


Bahati njema dereva alimudu chombo na kukiweka kando kikiwa kimesababisha uharibifu mdogo. Liligonga gari moja dogo na nguzo moja ya barabarani.
“Nashangaa nini shida. Lilifanyiwa huduma zote kabla halijaanza safari,” dereva alisikika akilaumu.
Alikuwa mwanaume mfupi mnene aliyevalia traki nyekundu na kapelo rangi ya manjano.


Sasa basi kwakuwa umbali ulikuwa mdogo, wakaamua kumalizia kwa kutembea na miguu wakiacha basi linafanyiwa matengenezo.


Wakiwa wanatembea Joana akaendelea na zoezi lake la kupiga picha. Akafotoa huku na huko akiwa anatabasamu. Akawapiga wenzake picha, pia na majengo.


Mara akiwa anafanya zoezi lake hilo, kwa mbali akamwona mtu ambaye hakuwa mgeni. Alihisi amempiga picha mtu huyu kwakuwa kamera yake ilikuwa imeelekea upande wake.


Ila alipotazama kwenye kamera, hakumwona! Akabakia ameduwaa. Akatazama upande ule, hakumwona mtu. Akabakia akiangaza mpaka pale aliposhtuliwa na wenzake nusura agongwe na gari.





****
 
*JOANA ANAONA KITU USIKU*

*Simulizi za series*


ILIPOISHIA

Mara hii alimwona mtu huyu akiwa kwenye bembea mbali sana. Alikuwa haonekani sura vizuri ila mavazi na umbo lake havikuwa vigeni kwa Joana.

Vilikuwa ni vya Moa!

Alijaribu kupmga picha mtu huyo ili amtazame vema akiwa ametulia. Ila hakutokea kwenye kamera. Na alipotazama tena kule kwenye bembea, hakumwona.

ENDELEA

Akashindwa kuelewa, ni mach0 yake ama nini? La hasha! Siyo macho yake bali ni uhalisia, yaani macho yaonyeshe kitu kimoja mara zote hizo?

Basi akakodoa sana macho yake kama atamuona tena mtu huyo, lakini wapi. Hakukuwa na kitu, hakuona jambo mpaka wanafika huko kiwanjani walipoenda kusabahi.

Wakazunguka sana huko na Joana akaendelea kupiga picha. Akafurahia sana na kwa kiasi fulani akasahau shida aliyokuwa nayo.

Marafiki zake pia wakafurahia uwepo wake, wakaweka mapozi mbalimbali Joana awafotoe picha. Wakapiga pia picha ya wote, klabu nzima, kama ukumbusho.

Walichukua muda wa kama masaa mawili ndani ya eneo hilo kabla hawajaondoka. Wakaelekea kwenye hoteli fulani mpya iitwayo La Princessita. Huko Joana akapewa chumba kimoja na mwenzake aitwaye Rosie – mwanamke mnene mweupe.

Kama kawaida chumba hicho kilikuwa kimepakana na dirisha. Na basi kilikuwa katika sakafu ya kumi na mbili ya ghorofa la hoteli ambapo Joana alikuwa na uwezo wa kutazama jiji vizuri kabisa.

Alikifurahia chumba maana kilikuwa kikubwa na chenye samani nzuri za kuvutia. Akapiga picha.

Mwenzake akampatia wazo.

“Kwanini tusiende Eiffel Tower? – kule kuna mandhari mazuri kwa ajili ya kumbukumbu.”

Na kweli. Nani aende Paris: Ufaransa pasipo kutembelea mnara wa Eiffel. Mnara maarufu dunia nzima. Ishara ya Paris na Ufaransa kwa ujumla.

Joana akapendezwa na hilo wazo. Basi wakavaa na kwenda safari. Wakachukua muda mchache sana kufika mnarani kwani hoteli ilikuwa karibu na mnara huo.

Wakapiga picha kadhaa kisha wakaenda mgahawani kula.

“Umeona hii! Imetoka bomba,” alisema Rosie akionyeshea picha mojawapo ndani ya kamera.

“Mie naona zote nzuri,” Joana naye akatia neno wakizikagua picha zingine.

“Joana, nataka nizisafishe picha hizi niwe nazo kwenye nakala ngumu,” akasema Rosie.

“Nataka nikazibandike ukutani mwa chumba changu.”

“Unataka kusafisha ngapi?”

“Zote. Si umesema zote nzuri?”

“Sawa. Twende tukatafute studio.”

Basi wakaenda kuhaha ndani ya jiji. Punde wakapata studio na kusafisha picha. Rosie akalipia na kuchukua picha zake. Joana naye akasafisha kadhaa alizozipenda. Wakazitia bahashani na kurudi hotelini.

Baadae wakaenda mazoezini kwa ajili ya kupasha viungo vya mwili na kuviweka tenge. Wakarejea hotelini kwenye majira ya saa kumi na mbili jioni.

Kwenye majira ya saa mbili usiku baada ya kupata chakula cha usiku, Joana akaketi kitandani na kuanza kupekuwa picha zake. Wakati huo Rosie alikuwa yupo bafuni anaoga.

Zilikuwa nzuri kweli. Zikamfanya mpaka atabasamu.

Alizitazama kwa mara ya kwanza, akarudia kwa mara ya pili. Alipozirudia kwa mara ya tatu, akaona kitu pichani.

Picha ya kwanza … ya pili … ya tatu na ya nne!

Kulikuwa kuna picha ya kivuli cha mtu pembeni yake. Kivuli hichi kilikuwa kimefifia na kuonekana kwa mbali. Kama mtu hautazami kwa karibu huwezi kuona kitu.

Kilikuwa ni kivuli cha mwanaume. Kilikaa upande wa kushoto wa Joana katika kila picha.

Joana akashtuka sana. akatafuta kamera yake na kuanza kupekua picha zote. Haki hakuona kitu. Kivuli hakikuwepo abadani.

Hata pale alipotazama picha zile ambazo alizisafisha, ndani ya kamera hazikuonyesha kivuli. Sasa hichi kivuli kimetoka wapi? Akajiuliza.

Rosie alivyotoka bafuni akamwomba picha zake walizozisafisha azitazame, Rosie akamkubalia na kumpatia. Joana akazikagua zote, hakuona picha ya kivuli hata moja.
Ina maana kivuli alikuwa kwenye picha zake tu. Picha alizomo yeye tu. La haula!

“Kuna nini Jo?” akauliza Rosie akijifuta maji. Alimwona Joana akizikagua picha zake kana kwamba polisi.

“Hamna kitu!” akasema Joana kisha akamkabidhi Rosie picha zake. Rosie akazitazama hizo picha kama zina mushkeli. Hakuona kitu, akazirejesha begini.

Akavaa na kulala akitazama runinga.

Ila Joana hakuwa hapo, alikuwa mbali kimawazo. Aliwaza kile kivuli, kwa namna moja akahisi kinaweza kikawa na mahusiano na taswira aliyokuwa anaiona huku na kule ndani ya jiji.

Akajitahidi kupuuza mawazo hayo na kuhamishia mawazo yake kwenye runinga. Akajumuika na Rosie kutazama tamthilia mpaka mishale ya saa nne usiku. Rosie akalala.

Muda si mwingi naye Joana akapitiwa na usingizi.

Kwenye majira ya usiku wa manane, kukiwa kimya kabisa, Rosie akaanza kutapatapa kama samaki aliyetupiwa jangwani. Alikuwa anahangaika kutafuta hewa kwanguvu zote akibana shingo yake.

Akifanya hayo, alikuwa bado usingizi kwani macho alikuwa ameyafumba.

Alikuwa anataka kupiga kelele lakini sauti haitoki. Alikuwa anataka kufumbua macho lakini kope zilikuwa nzito mno. Akaishia kupapatika!

Jasho lilikuwa linamtoka, na kadiri muda ulivyokuwa unaenda, akawa anapoteza nguvu za kupambana.

Bahati akampiga teke Joana, Joana akakurupuka usingizini na kuangaza. Mara Rosie naye akaamka akishikilia shingo yake, akikohoa na akihema kwanguvu. Joana akatahamaki.

“Vipi Rosie?”

Rosie hakusema jambo. Alikuwa bize anakusanya hewa kwanza. Alipokuja kutengemaa akamwambia Joana alikuwa amekabwa na mwanamke ambaye hakumwona uso wake.

“Alikuaje?” Joana akauliza.

“Alikuwa ana nywele ndefu zikimziba uso!” Rosie akasema kwa sura ya woga. Akatikisa kichwa na kusema: “Nilikuwa nakufa, Joana.”

Tangu hapo Rosie akakosa kukosa usingizi. Yeye na Joana wakabaki macho wakiteta mambo kadha wa kadha. Kila Rosie alipotaka kulala akashtuka na kujilazimisha akae macho.

Alikuwa ana usingizi mzito ila alikuwa na hofu huenda akakabwa tena.

Kwa upande wa Joana yeye alikuwa amekabwa na maswali. Akili yake ilikuwa inawaza huyo mkabaji ni nani? Na je anahusiana na yule mhanga wa ukabwaji kwenye hoteli ya kwanza?

Vipi kama Rosie asingempiga teke? Alikuwa anakufa?

Mawazo ambayo alikuwa ameanza kuyasahau, sasa yanaanza kumrejea.


USIKOSE SEHEMU IJAYO.
 
98bf7d50088f67c6a7fb9f2f343e0865.jpg
 
Back
Top Bottom