Anga la washenzi na Joana anaona kitu usiku

Anga la washenzi na Joana anaona kitu usiku

98bf7d50088f67c6a7fb9f2f343e0865.jpg
Sasa ndo nini hiki...peleka kwenye jukwaa husika please.
 
*ANGA LA WASHENZI --- 18*

*Simulizi za series*


ILIPOISHIA

Sasa nani alimuua? Na alifanya hivyo kwa malengo gani? Na kwanini mtoto wake naye akauawa? Maswali hayo hayakuwahi kupata majibu toka upande wowote ule.

Ila juu yake hayo, Jona anapata tena swali lingine, mbona picha ya Fakiri ilikuwa ndani ya kibahasha cha Bigo? Ina maana yeye ndiye anahusika na mauaji hayo? Kama ndio, mbona ya mtoto wa Fakiri haipo? Yeye aliuawa na nani?

ENDELEA

Akajikuta anashusha pumzi ndefu baada ya kuona ana mlima mkubwa wa kuupanda. Lengo lake lilikuwa ni kumjua tu Bigo ni nani na nani aliyemtuma ila anajikuta anagundua mambo mengine ambayo hakutaraji.

Ayaache? Hapana! Haya mambo yanaweza kumsaidia akaunganisha doti kumjua Bigo hasa ni nani na anamfanyia kazi nani.

Lakini juu ya yote haya, kwanini hawa watu wanataka kumpoteza? Kosa lake ni nini?

Kama angelikuwa bado yu ndani ya jeshi la polisi, basi angesema aliingia kwenye anga zao, ila la hasha! Sasa tabu nini? Alishawahi kuwagusa watu hawa pindi akiwa jeshini? Akajiuliza. Mbona hawakumtafuta muda wote huo?

Masikini hakujua chanzo ni picha. picha tu ndiyo ambayo inataka kumtoa roho. Picha tu ndiyo ambayo inamwingiza kwenye anga la wababe wanaotaka kunyofoa uhai wake kama vile Bite.

Jona anarudishwa ndani ya ulingo wa mapambano pasipo kutarajia. Anarudishwa kazini japokuwa alishakataa hii kazi aendelee na maisha mengine.

Kabla ya kuendelea kuperuzi na kuhangaika juu ya Fakiri, kwanza akapata wazo la kuyatambua yale maneno yaliyokuwepo nyuma ya pasipoti zote za Bigo.

Kwa kutumia alama za kichapio cha tarakilishi zake, anakopi maneno yale kwenye injini ya kusakia majibu mtandaoni kisha anasaka.

Punde yanakuja majibu mengi, anachagua jibu moja na kuliangaza. Anaona maneno matatu: ‘Pumzi ya mwisho’. Kumbe ndiyo maana ya yale maneno.

Moja kwa moja akajihakikishia kumbe wale watu kwenye pasipoti walikuwa kwenye ahadi ya mauaji. Maana yake walikuwa kwenye pumzi zao za mwisho.

Kwanini wauawe? Na ni nani aliyekuwa anataka kuwaua?

Pasipoti zilikuwa mpya mpya. Hilo lilimaanisha orodha hiyo ya mauaji haikuwa ya zamani. Yani kama kwa kukadiria, ina mwaka tu, kama ikizidi ni miezi tu kadhaa.

Kwahiyo wote waliokuwa kwenye pasipoti wameuawa? Au kuna wengine bado wapo hai? Kwanini yeye hayupo kwenye pasipoti ila analengwa kuuawa?

Akili yake ikamwambia yeye alitokea tu kwa dharura, kuna watu waliokuwa kwenye orodha tangu kitambo. Ni nini basi hicho kilichomwingiza kwenye orodha?

Maswali yalizidi kichwa, akaona anahitaji kupumzika. Aliachana na tarakilishi yake kabla hajaidaka simu na kwenda zake nje aliposimama na kuangaza barabarani kana kwamba anahesabu idadi ya magari.

Alitaka kutoka akajipatie kikombe cha chai ila ofisi amwachie nani? Jumanne bado hakuwa amerudi.

Hali hiyo ikamlazimu ang’ae ng’ae macho kabla ya muda kidogo simu yake haijatetemeka kumwashiria ujumbe umeingia. Akaichomoa na kuitazama. Ni ujumbe wa Facebook toka kwa Miriam – mke wa mheshimiwa Eliakimu.

Jona akatabasamu.

‘I think I need your phone number if you don’t mind’ (Nadhani nahitaji namba yako ya simu kama hutojali’

‘It’s just ok, I wanted to ask for it earlier but hesitated.’ (ni sawa, nilitaka kukuomba hapo mapema lakini nikasita.’

Chati yake na Mariam zilionekana hivyo. Yeye alikuwa wa kwanza kutuma ujumbe kuhusu kuomba namba ya simu kabla ya hajajibiwa na Miriam kwamba naye pia alikuwa anataka kuomba.

‘Did you fear to ask?’ (Uliogopa kuomba?)

‘Somehow, you know. You were impressed so I decided to wait.’ (Kiasi, si unajua. Ulikuwa umevutiwa kwahiyo nikaamua kungoja.)

Jona akatuma vimdoli vya kutabasamu, na ndiyo hivyo punde namba ikatumwa na Miriam.

‘At what time am I supposed to find you?’ (Kwa muda gani natakiwa kukutafuta?) Jona akautuma ujumbe kuuliza. Uzuri Mariam alikuwa mtandaoni hivyo akajibu upesi:

‘At any time.’ (Muda wowote.)

‘Really?’ (Kweli?)

‘Yah! Why asking?’ (Ndio! Kwanini unauliza?) Mariam aliambatanisha ujumbe wake na vimdoli vya kushangaa.

‘I didn’t expect that ‘anytime’, aren’t you in relationship? Sorry for asking though.’ (Sikutegemea hiyo ‘muda wowote’, haupo kwenye mahusiano? Samahani kwa kuuliza lakini.)

‘Don’t mind, I am not in relationship that’s why I am free’ (Usijali, sipo kwenye mahusiano ndiyo maana nipo huru.)

‘Better for you! Expect my call n’ messages soon!’ (Ni njema kwako! Tegemea simu na jumbe zangu karibuni!)

‘Wow! Can’t wait.’ (Wow! Nangoja kwa hamu.)

Jona akatoka huko mtandaoni baada ya kuinakili namba ya Bite kichwani, akaitunza kwenye simu yake kwa jina la ‘target no.1’. Kabla hajaendelea zaidi, Jumanne akarejea, basi yeye akaenda kujipatia chai angalau atie joto tumboni.

Akiwa anangoja kikombe cha chai, akaendelea na kazoezi kake.

Akahamishia namba ya Miriam kwenye msako wa lokesheni kwa kutumia GPS. Simu ikaanza kutafuta taratibu. Mara ikaeleza wapi namba ya Miriam inapopatikana.

Jona akajikuta anatabasamu.

“Hadithi imeishia hapa,” akanena mwenyewe.

“Hadithi gani?” mara sauti ikamuuliza na kumfanya atoe macho yake kwenye simu. Alah! Alikuwa mama K akiweka kikombe cha chai mezani.

“Masikio yako yapo kazini muda wote mama K!”

“Kama ilivyo mikono yangu,” mama K akajibu kwa tabasamu, kisha akasema: “Jumanne alisema utakuja.”

“Wapi?”

“Kuna mahali pengine zaidi ya hapa?” Alijigamba mama K ndani ya gauni lake la kale lenye mistari hafifu rangi ya kijani. Nywele zake alikuwa amezifumba na kiremba kikubwa cha pande la khanga, miguu yake ndani ya raba za pinki.

“Amesema ukija utamlipia chai aliyokunywa.”

“Mimi?”

“Sasa hapa naongea na nani? Au sio Jona wewe?”

“Jumanne pumbavu kabisa!” alisema Jona akitikisa kichwa. “Anajifanya mjanja unh?… usijali, n’talipia!”

Mama K akatabasamu kisha akaenda zake.

Akiwa mgahawani, Jona hupenda kukaa mahali panapoweza kumfanya akaona ofisi yake. Hufanya hivi ili asije akakosa ama kupitwa na taarifa yoyote ile toka upande ule wa pili.

Akiwa anakunywa zake chai taratibu, kichwani akiyapangilia mafaili, kwa mbali alikuwa anatazama ofisi na kushuhudia wageni watatu wazungu wakizama ndani.

Jumanne aliwapokea kwa bashasha na punde akaanza kuwaonyesha bidhaa kwa mikono yake iliyokuwa inapanda na kushuka, ikienda kushoto na kulia.

Mpaka Jona anamaliza kunywa chai, wageni walikuwa tayari wameondoka.
Alishika zake njia kurudi ofisini.

Kabla hajafika, ikiwa imebakia takribani kama hatua tatu tu, Jona anamuona mwanamke fulani upande wake wa kushoto hatua kama kumi na tatu kwa umbali.

Mwanamke huyu alikuwa amevalia sketi fupi, topu, koti fupi dogo la kung’aa, viatu virefu vinayokomea magotini, miwani ya jua na wigi refu. Vyote hivi vilikuwa vyeusi kwa rangi!

Mkono wake wa kuume ulikuwa umebebelea simu kubwa. Alikuwa amesimama akichezea hii simu. Ila Jona aliporusha macho yake upande wake, haraka akageuzia sura yake pembeni.

“Nishawahi kumwona huyu mwanamke wapi?” Jona alijiuliza akiingia ndani ya ofisi. Kimo, rangi na shepu ya mwanamke yule kwake havikuwa vigeni. Japokuwa sura hakuwa anaifahamu, ila ‘kapicha’ kalikuwa kyenyeji.

Aliipokutana na Jumanne na kuanza kuongea kuhusu ya mgahawani, akili yake ikampuuzia na kumsahau mwanamke huyo.


***


Kwenye majira ya saa mbili usiku: Mbweni.


Mazingira yalikuwa na rasha rasha za vijikelele vya hapa na pale kama mara nyingi inavyokuwa kwenye nyumba za kupanga ambazo zimesongamana pamoja.

Katika eneo hili, kaya nne zilikuwa ndani ya uzio mmoja mkubwa, kila nyumba ikiwa imejitenga mbali kidogo na mwenzake. Nyumba hizi zilikuwa zinafanana kuanzia rangi mpaka mpangilio wake.

Kama mtu ni mgeni wa eneo basi unaweza kupotea ukachanganya milango.

‘Nisubirie hapo hapo nakuja,’ Kinoo aliyekuwa amesimama getini, kwa ndani, aliupokea ujumbe huo simuni. Akangoja.

Alikuwa amevalia ‘kibody’ cheusi, suruali ya jeans na raba nyeupe.

Punde anamwona Mudy, mwanaume yule aliyekuwa anafanya kazi kwenye kampuni ya Bite, akija. Alikuwa amevalia jezi ya mchezo wa mpira ya taifa la Hispania. Mkononi alikuwa ana simu.

Alimpokea Kinoo wakaongozana naye kuelekea nyumba ya upande wa kushoto mwa geti, kwa nje kulipaki Rav4 nyeupe. Wakazama ndani na kujiweka sebuleni. Baada ya maongezi mafupi, Mudy akaenda chumbani na kurejea na faili moja kubwa rangi ya samawati aliloliweka mezani.

“Kuna nyaraka fulani ya malipo, Bite aliniachia wiki moja kabla ya mauaji yake. Nakumbuka alinisisitizia sana niahakikishe natuma pesa kwenda kampuni fulani ya kusambaza umeme wa jua.”

Mudy akaonyesha nyaraka hiyo kwa Kinoo.

“Ilikuwa kiasi kikubwa sana cha pesa. Ila nilikuwa nimetingwa na kazi nyingi na hata kupelekea kupita siku tatu nikiwa sijatuma pesa hiyo. siku ya nne, Bite alikuja akiwa na mashaka na haraka akaniuliza kama nimetuma ile pesa, nikamwambia hapana lakini nikihofia sana huenda atanikaripia kwani alisisitiza.

Ajabu, akafurahi. Akanambia: ‘Ahsante sana Mudy, usitume tena hiyo pesa. Hao watu ni mafedhuli wakubwa, wezi na wauaji. Acha mara moja!’ kisha akaenda zake.

Huoni kampuni hii ndiyo watuhumiwa namba moja na sababu ikawa ile pesa?” Mudy alimalizia taarifa yake na swali. Kinoo akaunga mkono hoja.

“Ni kweli kabisa!” kisha akauliza: “Na vipi Brokoli? – alichukuliaje hii taarifa?”

Mudy akapandisha mabega juu.

“Sijui! Ila nakumbuka walikaa vikao viwili kama si vitatu mfululizo. Hatukuambiwa wanaongelea nini. Wala hatukupashwa habari kama kuna mabadiliko ama mazingatio yoyote kutokana na vikao hivyo!”


KUNA MCHEZO GANI HAPA? NINI KINOO AMEGUNDUA NA ATAFANYA?

NINI JONA ATAFANYA BAADA YA KUJUA MAKAZI YA MIRIAM – MKE WA MHESHIMIWA ELIAKIMU? NA JE, UPEMBUZI WAKE WA KUMJUA BIGO UTAMPELEKA MPAKA WAPI?

MWANAMKE ANAYEMFUATILIA JONA, NINI MWISHOWE?

Usikose sehemu ijayo

*Simulizi za series*

Sent from my SM-J110F using JamiiForums mobile app
 
*ANGA LA WASHENZI – 19*

*Simulizi za series*


ILIPOISHIA

“Ni kweli kabisa!” kisha akauliza: “Na vipi Brokoli? – alichukuliaje hii taarifa?”

Mudy akapandisha mabega juu.

“Sijui! Ila nakumbuka walikaa vikao viwili kama si vitatu mfululizo. Hatukuambiwa wanaongelea nini. Wala hatukupashwa habari kama kuna mabadiliko ama mazingatio yoyote kutokana na vikao hivyo!”

ENDELEA…

Kinoo akaguna kisha akauliza:

“Unajua wapi Brokoli anaishi?”

“Yah! Najua,” Mudy akajibu akitikisa kichwa.

“Na ulishawahi kuiftuatilia hiyo kampuni ya umeme wa jua?”

“Hapana. Sikufanya hilo kwa kutegemea polisi watalivalia njuga.”

“Sawa, na vipi kama hili jambo likabuma tena huko polisi, upo radhi kwenda umbali gani kutafuta haki ya Bite?”

Kidogo Mudy akasita.

“Una maanisha nini?”

“Unajua Mudy, si kila muda mambo yanaenda kama vile tunavyotarajia ama tunavyotaka. Nadhani uliona namna polisi walivyokuangusha ulivyowapelekea hili jambo. Sasa mimi nataka kujua unaweza kwenda kilomita ngapi kutafuta haki ya Bite?”

“Kadiri ya uwezo wangu.”

“Ahsante sana, hicho ndicho nilikuwa nataka. Njia hii inaweza ikawa ngumu na ndefu, inabidi tujiandae. Aidha kupita njia kuu ama nyinginezo ilimradi haki ipatikane.”

Kinoo akasafisha kwanza koo, akaendelea:

“Kikubwa ninachohitaji toka kwao ni taarifa tu, hayo mengine mimi nitayasimamia. Nitahitaji taarifa mbalimbali toka ofisini mwenu kama hutojali, yote kwa ajili ya Bite.”

“Nitajitahidi kadiri ninavyoweza.”

Wakapeana mikono. Kinoo akaaga.

“Ina maana mgeni unaondoka pasipo kupata chochote kitu?”

“Nashukuru sana, usijali. Leo si mwisho wa dunia. Anyway, unaishi mwenyewe?”

“Yah! Nipo mwenyewe.”

“Nyumba yote hii?”

Mudy akatabasamu. “Ndio, nipo mwenyewe.”

“Aisee!” Kinoo akatahamaki akiangaza huku na huko. Akapandisha mabega yake na kupinda mdomo.

“Haya mzee. Ningependa unipatie hizi nyaraka zako nikajaribu kufuatilia baadhi ya mambo. Pengine naweza nikaibuka na jambo.”

Mudy akamkabidhi.

“Kuwa makini, bado zinahitajika na ni muhimu ofisini.”

Kinoo akaitikia kabla hajaenda zake. Cha kwanza alichokifanya ni kumtafuta na kukutana na Miranda. Alikuwa yupo nyumbani kwake akijipatia kinywaji laini na kutazama televisheni. Alikuwa amevalia bukta ya timberland na blauzi nyeusi.

Akamweleza yale yote aliyoyapata huko kwa Mudy.

“Umefanya kazi nzuri!” Miranda akampongeza akipitisha pitisha macho yake kwenye nyaraka alizokuja nazo Kinoo.

“Lakini … Kinoo, kama vile naijua hii kampuni.”

“Serious?”

“Yah! Serious.”

“Ipo wapi?”

“Kama sijakosea, nilishawahi kuiona ikitangazwa kwenye TV. Tena si zamani, jana tu! … ngoja!” Miranda akanyaka rimoti na kubadili alichokuwa anakitazama toka kwenye movie mpaka chaneli ya kawaida.

“Bila shaka niliona hilo tangazo hapa.”

Alipoweka hiyo chaneli, wakaendelea na maongezi mengine. Wakagusia swala la picha ya Bite iliyopo kwa Jona.

“Nimeona ni vema nikaonana naye binafsi,” alisema Bite akikuna kichwa. “Nadhani nikimwelezea vizuri anaweza akanielewa. Hata kama asiponipa hiyo picha basi anipe wasaa mdogo wa kuitazama.”

“Unadhani atakukubalia?” Kinoo akauliza.

“Hayo yote ni matokeo: kunikubalia ama kunikatalia. Ila angalau nimejaribu. Lakini najua sitashindwa.”

Kinoo akaguna.

“Labda … sijui.”

“Kuna utofauti kati yangu na wewe,” Miranda akasema akimtazama Kinoo. “Tofauti moja kubwa mimi ni mwanamke na wewe ni mwanaume.”

Mara simu ya Miranda ikanguruma na kukatisha maongezi. Miranda akaitazama kujua ni nani kabla hajaiweka sikioni. Alikuwa ni waziri wa michezo; Mheshimiwa Eliakimu Mtaja.

“Tunaweza tukaonana, binti?” sauti ya Eliakimu iliuliza.

“Muda gani mheshimiwa?”

“Kesho majira ya jioni hapa nyumbani kwangu.”

“Sawa.”

Simu ikakata. Lakini ilimkumbusha jambo, kuwasiliana na bwana Boka, waziri wa Afya. Alienda chumbani kwake akarejea na kadi ya biashara aliyopewa na mwanaume huyo, akapiga namba iliyokuwa imeanishwa.

Bahati haikuwa kwake, simu haikupokelewa. Alipiga mara tatu kabla hajaamua kusitisha zoezi hilo.


***


“Kesho atakuja,” alisema bwana Eliakimu akimwambia Nade. Wote walikuwa sebuleni peke yao. Sauti ya televisheni ilikuwa inanguruma kwa mbali ikikosa shabiki wa kuitazama.

Eliakimu alikuwa amevalia suti ya traki ya michezo rangi ya bluu, Nade akiwa amejivalia suruali nyeusi ya kitambaa iliyoendana na koti lake fupi jeusi lenye kola rangi ya pinki.

“Nadhani mipango yetu imeenda kama tulivyotarajia,” alisema bwana Eliakimu. Nade akatikisa kichwa.

“Ndiyo, mkuu. Lakini kuna kajitatizo kadogo kametokea.”

“Wapi huko?”

“Ni kumhusu Maxwell Ndoja. Ameapa kutoshirikiana nasi tena. Amesema inatosha kwa yale yote tuliyoyafanya. Kwa sasa anataka kufungua ukurasa mpya.”

“Ukurasa mpya! Bloody fool!” bwana Eliakimu alifoka. “Anamaanisha nini kusema inatosha?”

Nade akapandisha mabega yake juu.

“Tangu lini pesa ikatosha?” Aliuliza Eliakimu. “Maxwell anataka kunipanda kichwani sasa. inabidi ajue hichi ni kitabu, hakuna ukurasa mpya kama haupo wa zamani, na ukitoa karatasi moja kwenye riwaya basi riwaya nzima inapoteza maana.”

Aliposema hayo akaulaza mgongo wake kwenye kiti akizama fikirani. Kwa dakika kama moja kukawa kimya kabla Nade hajamuuliza:

“Kwahiyo tunafanya nini, mkuu?”

Bwana Eliakimu akanyaka simu yake, akatafuta jina la Max, akaliita. Baada ya muda mchache ikapokelewa.

“Max, tunaweza tukaonana?” bwana Eliakimu aliuliza. Mzee huyu huwa haongei na mtu kwenye simu kuhusu mambo yake. Kuficha taarifa zake huwa anamwomba mtu wake wakutane. Na hupendelea zaidi nyumba yake kama mahali pa makutano.

“Hapana, hatuwezi kukutana,” ikajibu sauti ndani ya simu.

“Kwanini?”

“Kwasababu sina tena sababu ya kukutana na wewe mheshimiwa. Nadhani kibaraka wako ameshakwambia.”

“Max!”

Simu ikakata. Bwana Eliakimu akaitazama kana kwamba haamini.

“Amekata!” akasema akimtazama Nade. “Hivi huyu ananijua ama ananisikia?”

Akashusha pumzi ndefu … akakuna kidevu … akakuna kichwa.

“Hatuwezi tukamwacha huyu mtu hai,” akasema Bwana Eliakimu. “Anajua siri zetu nyingi mno. Hawezi akatoka tu kienyeji namna hii. Tutapataje uhakiki wa taarifa zetu kwake?”

“Hilo ndiyo jambo kubwa. Siri ziko mashakani sasa. hatuwezi jua nini kimemsukuma akajitoa kwenye duara.”

“Kwanini hukummaliza?”

“Nisingeweza kummaliza pasipo idhini yako.”

Eliakimu akanyanyuka akiweka mikono yake nyuma ya mgongo.

“Hakikisha kesho unammaliza huyu punguani. Usibakize ushahidi wowote nyuma!” alisema bwana Eliakimu kwa macho ya kumaanisha.

“Sawa, mkuu. Nitajitahidi,” Nade akapokea kauli.

Eliakimu akaenda zake chumbani. Alikuwa amekunja uso akibinua mdomo.


***


“Kwanini ulimuua Fakiri?” Jona alimuuliza Bigo aliyekuwa hapo kitini kwa masaa ya kutosha sasa. Bigo hakuwa amekula wala kunywa chochote. Tangu alipofungiwa kwenye kiti hakuwa amesogea wala kwenda popote.

Kuepusha asije akapiga makelele na kuzua tafrani, Jona huwa anamfunga mdomo pale anapotaka kulala ama kuondoka.

Bigo alitabasamu akimtazama Jona kwa kebehi.

“Sijui nini unaongelea,” akajibu kisha akalaza kichwa chake kutazama chini.

“Bigo, unapenda kuhangaika na kuteseka namna hii?” Jona aliuliza. “Mimi sina shida na wewe, najua wewe ni kibaraka tu unayetumwa. Mimi nina shida na bosi wako. Na shida yangu ni kujua kwanini anataka kuniua. Kwanini mnataka kuniua?”

Bigo akatabasamu.

“Ngoja nikwambie kitu kimoja, msanii. Sisi huwa hatumfuati wala kusumbuka na mtu asiye na faida kwetu, tunamfuata yule aliye na chetu, yule ambaye ana kitu tunachokitaka.”

“Mimi nina kipi chenu?”

Bigo akatikisa kichwa kichovu.

“Sina haja ya kukwambia, utakuja kujua mwenyewe. Kwa sasa mimi ni wa kufa tu, aidha nifie kwako ama kwa mkuu wangu. Najua hataniacha hai. Kwahiyo sina cha kupoteza, fanya upendacho.”

“Sina haja ya kukuua. Nipe taarifa ninazozitaka.”

“Alafu?”

“Nitakuacha uwe huru.”

Bigo akajaribu kucheka, ila zoezi likashindikana. Hakukuwa na ushirikiano toka tumboni.

“Huru? … siwezi kuwa huru kamwe maisha yangu yote.”

“Kwanini unasema hivyo?”

“Kwasababu najua. Njia pekee ya mimi kuwa huru ni kifo, la hasha sipo huru kabisa. Kwahiyo kama unataka kuniweka huru, inabidi uniue.”

“Sina haja ya kukuua, Bigo.”

“Basi mimi mwenyewe nitajiweka huru.”

“Kivipi? – huwezi kujiua hapo.”

Katika hali ya kushangaza, Bigo akaanza kuvuja damu nyingi mdomoni. Jona akashangazwa sana na hilo tukio. Alimkagua Bigo na macho yake lakini hakuona kama ana mushkeli popote pale.

Mbele ya macho yake, Bigo akalegeza kichwa, akakata pumzi.

Muda mfupi mbele, bado Jona akiwa ameduwaa, ulimi ukatoka mdomoni mwa Bigo na kudondokea chini!

Bigo alikuwa ameunyofoa ulimi wake kwa kutumia meno!


MANENO YAKE ALIYOMWAMBIA JONA YALIKUWA YANAMAANISHA NINI?

NADE ATAFANIKIWA KUMMALIZA MAX ALIYEAMUA KUSILIMU? KWANINI MAX KASILIMU?

KAMA MAX ANAFANYWA HIVI NINI KITATUKIA ENDAPO ELIAKIMU AKIGUNDUA BC NA MIRANDA WANA MPANGO WA KANDO?

KINOO NA MIRANDA WATAFANIKIWA?

Usikose sehemu ijayo.

Sent from my SM-J110F using JamiiForums mobile app
 
Back
Top Bottom