Anga la washenzi na Joana anaona kitu usiku

Anga la washenzi na Joana anaona kitu usiku

Mkuu endelea kutushushia anga la washenzi make imekaa poa sana.
 
*ANGA LA WASHENZI --- 04*

*Simulizi za series*



Moja kwa moja akaenda kwanza chumbani kwake karibia na eneo la kabati, akafunua zulia na kukutana na kamlango kadogo alikokafungua na kuzama chini.

Ilikuwa ni handaki. Tena kubwa tu kutosha kabisa sebule na chumba kimoja. Humo kulikuwa kama stoo kwa kujazwa vitu kadha wa kadha.

Jona akawasha taa apate kuona, kisha kama mtu anayejua anachofanya, akanyookea kwenye kona ya handaki.

Akakuta picha ya Bite. Ilikuwa imefunikwa na kitambaa kikubwa ikiwa imetulia kabisa kama ilivyowekwa.

Jona akashusha pumzi ndefu kwanza. Alijihisi amepata amani ya moyo. Alijikuta mpaka anatabasamu mwenyewe.

Aliifunika tena picha kwa kitambaa na kuirejesha palepale alipoiweka. Alipaona hapo ni salama sasa. Mahali anapopaamini panaweza kumhifadhia jambo lake nyeti.

Bila shaka wavamizi hawakuwa wanajua kama ndani ya nyumba hiyo kuna handaki. Kiufupi, hawakuwa wanajua lolote kuhusiana na nyumba hiyo.

Walidhani ni ya kawaida kama zingine, ujinga ambao uliwagharimu. Walimchukulia Jona kiuwepesi, hawakumpa haswa uzito anaostahili.

Nyumba hii japokuwa i ndogo kwa juu ya ardhi, yani kwenye macho ya kawaida ya binadamu, kiuhalisia ilikuwa kubwa sana kutokana na mambo kadha wa kadha yaliyowekwa katika muundo wa siri.

Ukiachana na handaki ambalo nalo lina sebule na chumba, kuta za nyumba hii zina milango nyuma ya makabati ya vyombo na nguo.
Huwezi ukalifahamu hili kama hujafundwa. Ukisogeza makabati haya pembeni, unakuta milango ya vyumba vidogo vidogo sana ambavyo vinatunza nyaraka na vifaa vya siri.

Chumba kilichopo nyuma ya kabati la jikoni, kilikuwa kina nyaraka na makabrasha yake muhimu. Pia vitu vingine ambavyo hakutaka kuvipoteza, mathalan vifaa alivyokuwa anachezea marehemu mtoto wake. Na hata pia vile alivyokuwa anavipenda mkewe.

Kwahiyo ndani ungekuta mipira ya kuchezea, midoli, marashi mbalimbali, nguo, viatu na kadhalika.

Chumba cha siri kilichojificha nyuma ya kabati lake la nguo la chumbani, kilikuwa kina silaha tu, na si kingine cha ziada.

Silaha hizi zilipachikwa ukutani zikipangiliwa vema. Zilikuwa ni silaha moto na baridi. Bunduki aina kadha wa kadha, mapanga, visu, mashoka, nondo, jambia na kadhalika.

Ila silaha ya kisu ikiwa imetamalaki kuliko zingine. Kulikuwa kuna visu takribani mia moja! Vya kila aina. Vyenye mipini ya kila rangi na muundo wake.

Hii ndiyo silaha Jona anaipenda. Silaha anayoimudu vema. Silaha ambayo hakuweza kwenda vitani pasipo kurandana nayo.

Jona akishika kisu, ni hatari kuliko akishika bunduki.
Kinachomfanya apende silaha ni sababu mbili. Mosi, hufanya kazi pasipo kukoma. Hakuna kusema imeishiwa kama utumiapo bunduki na risasi.

Pili, aliona ndiyo silaha isababishayo maumivu anayoyataka kwa adui. Maumivu ya taratibu. Maumivu makali. Risasi humuondoa mtu haraka. Kuna watu hawastahili kifo cha haraka, aliamini.

Alitoka kwenye handaki akarejeshea vitu kama vilivyokaa, akaenda kuketi sebuleni.

Baada ya kupata picha hiyo sasa alikuwa ametua hofu. Lakini akajitwika mawazo zaidi. Mawazo ambayo aliona yanahitaji ufumbuzi wa haraka.

Alichomoa chupa ya kileo ndani ya jokofu, akamiminia kwenye glasi na kuanza kunywa taratibu akikokotoa mambo kichwani.

Alipomaliza kinywaji kwenye glasi, akabebelea chupa mkononi na kuanza kurandaranda ndani ya nyumba.

Alitazama na kuchambua nyayo za viatu alizozikuta. Alienda nje ya jengo napo akatazama chini. Akaenda pia nje ya uzio.

Akagundua nyumba yake ilivamiwa na watu watatu: mmoja alikuwa mwanamke, mwingine mwanaume. Wa tatu hakujua jinsia yake, yeye alikuwa dereva.

Alijua hilo kwa kutazama alama za viatu vilivyotoka kwenye gari.
Upande wa kulia wa gari, viatu vya kike vilitokea, ila kwa nyuma, si kwa dereva, kama ilivyokuwa kwa viatu vya kiume upande wa kushoto wa gari.

Na viatu hivyo vikarudi na kuingia garini kwa mtindo uleule uliotokea. Gari ikarudishwa nyuma na kutimka. Ndiyo maana ikawa rahisi kwa Jona kujua kuwa dereva hakushuka.

Kama gari lingeenda mbele lisirudi lilipotokea, ingemuwia vigumu kujua kuhusu mambo ya dereva, na watu waliotokea nyuma.

Zaidi akagundua ni aina gani ya gari ilikuja hapo. Si nyingine bali ni ile ile Range Rover Sport. Aling'amua kwa ufananisho wa alama za matairi.

Akarudi zake ndani akifunga milango yote. Akaoga na kujilaza kitandani. Hata hakula.
Akiwa anangoja usingizi umchukue kwa msaada wa kileo alichopiga, akafanya maamuzi. Aliona ana haja ya kurudi kazini.

Aliona ana hitaji la kufanya jitihada za kuutafuta ukweli uliojificha na kugubika swala la hil la picha na kifo cha Bite.

Lakini pia kumsaidia bwana Eliakimu Mtaja, kumwepusha na hadha ya kuwa kama yeye, asiye na mtu anayempenda, maana uchungu wake anaujua.

Lakini kabla hajaanza kuchambua kivipi atayafanyia kazi hayo mambo, usingizi ukampokonya fahamu. Alijikuta asubuhi ya saa kumi na moja.

Kila yanapofika majira haya usingizi kwake hukata hivyo huamka na kuanza kujiandaa kwa ajili ya kukabiliana na siku mpya.

Alihisi njaa sana, ilimbidi atengeneze na kunywa chai, kitu ambacho si kawaida yake.

Alipika chai na mayai. Kulikuwa kuna ubaridi wa mvua siku hiyo, kwahiyo alitaka apate joto.

Akiwa anakunywa chai, mvua ikaanza kunyesha, tena kubwa haswa. Kwahiyo hata alipomaliza ikambidi angojee kidogo kuona kama itapungua.

Alitazama nje akitumia dirisha la jikoni. Alikagua mazingira ya nyumba kwa macho kama mtu ambaye alikosa cha kufanya.

Mvua ilikuwa inamiminika. Na baridi lilikuwa linaongezeka. Alistaajabu ni kwa namna gani ataenda kazini. Alitamani mvua ile ingemkutia akiwa kazini kama ilivyokuwa hapo juzi, lakini haikuwezekana.

Alirudi zake kitandani akajilaza kwa malengo atafakari sasa alichokiachia njiani jana usiku. Alijifunika shuka na kuangaza darini.
Hakukaa muda usingizi ukambeba tena. Hali ya hewa ilimshinikiza. Shuka alilojifunika ukijumlisha na hali ya baridi iliyozuka, hakuweza kujisaidia.

Akalala. Ila usingizi tofauti na ule anaolala kila usiku, usingizi wa kushinikizwa na pombe. Usingizi huu ulikuwa halisi. Usingizi anaoukwepa kila uchwao kwani huwa unamletea matatizo, majinamizi ya kale.

Alidumu kwa takribani dakika kama ishirini usingizini. Mara akaanza kupata njozi. Alijiona akiwa kwenye uwanja wa vita anapambana na watu waliovalia sare za jeshi. Ila hakujua jeshi la wapi.

Watu hawa walikuwa wengi, ila yeye akiwa peke yake. Hakuwa na silaha, alitumia mikono na miguu yake tu. Aliopambana nao walikuwa na bunduki. Lakini akifanikiwa kuwamudu vema.

Alizikwepa risasi. Aliwavunja na kuwatengua maadui pasipo huruma. Alikuwa kila anapommaliza mmoja, anakazana kwenda mbele zaidi kwa kukimbia.

Baada ya muda, akiendekea kupambana kwa juhudi na kusogea mbele, akaona kijumba fulani kidogo, cha mbao chumba ghorofa mbili, umbali wa kama kilomita mbili.

Kijumba hicho kilikuwa kimekaa kwenye mwinuko ulitosha kuona vema kwa chini. Yani kule ambapo yeye na hao watu wengine wanaparangana.

Kwenye sakafu ya ghorofa hiyo, Jona aliona watatu. Hakuwa na uwezo wa kuwaona vizuri, lakini alijua mmoja atakuwa mkewe na mwingine mwanaye.

Alizidi kupambana na kujongea. Kila aliposogea akatupa macho kwenye lile jengo. Punde akaona vizuri. Alikuwa sahihi. Mkewe na mwanaye walikuwepo hapo.

Walikuwa wamefungwa kamba mikono na miguu wakifungwa pia na vinywa. Mwanamke alikuwa amepiga magoti, mtoto akiwa amesimama.

Pembezoni yao alikuwa amesimama mwanajeshi mrefu aliyekuwa amebebelea bunduki ndogo, amewanyooshea mwanamke na mtoto waliofungwa.

Basi Jona akazidi kuchanganyikiwa. Alipambana maradufu. Alizidi kujongea na kujongea. Alipokaribia jengo akasikia sauti kuu inapaza:
"Simama hapo hapo, la sivyo nawateketeza hawa washenzi wako!" Akatii. Alisimama na kusalimu amri. Alipigishwa magoti kwa lazima akinyooshewa midomo ya bunduki.
Macho yake yalitazama familia yake kwa uchungu. Yalivuja machozi. Alitamani kugeuka malaika akawaokoe lakini hakuweza.

Alijitahidi kuwa mpole awanusuru.
Mara giza likagubika asione jambo kabisa. Hakujua limetokea wapi. Punde tu, akasikia milio miwili ya risasi.
Pah! - Pah!

Akashtuka toka usingizini akihema kwanguvu. Alikunja ndita. Macho aliyatoa. Alimeza mate akitafakari. Mara akashtushwa na mlio wa simu iliyoita kandokando yake.

Akaichukua na kuitazama. Alikuwa Mh. Eliakimu Mtaja. Akapokea na kuiweka simu sikioni. "Nakuja mheshimiwa!" Akasema na kujinyanyua.

Mvua ilikuwa imepungua, manyunyu tu ndiyo yalikuwa yanarasha. Bado baridi lilikuwa linapuliza tena kwa kiasi kikubwa.

Jona akavaa koti refu jeusi kisha akatoka. Alitumia usafiri wa daladala kwasababu ya mvua. Baada ya lisaa moja akawa amefika nyumbani kwa Mh. Waziri Eliakimu Mtaja. Alipokelewa wakafanyia maongezi ndani ya nyumba.

"Nipo tayari kufanya kazi. Ila kwa masharti kadhaa," akasema Jona. "Naomba niyasikie," Mh. Eliakimu akatega sikio asikie vema.
"Nataka nifanye kazi hii kwa namna nijuavyo, pasipo kuingiliwa na yeyote yule. Nitakusanya taarifa, nitazichambua, nitazifanyia hariri na kuchukua hatua.
Sitahusika na jeshi la polisi, wala sitashirikiana nao. Nitafanya kazi kwa weledi wa siri mkubwa. Na ningependa iwe hivyo mpaka mwisho.

Lakini zaidi, naomba ushirikiano ulio kamili." Jona akaweka kituo.

Mheshimiwa akashusha pumzi ndefu, akajibu:
"Sawa, nimekuelewa na nimeridhia." Lakini akapendekeza.
"Najua kuna muda utakuwa unanihitaji, aidha nikupe baadhi ya taarifa ama nikusaidie kufanya jambo fulani litakalokusaidia.
Sasa si kila muda nakuwa na fursa, nakuwa nabanwa na kutingwa na mambo mengi tena muhimu. Hivyo basi, kuna mtu ningependekeza uwe naye karibu. Anajua karibia kila kitu kunihusu.

Atakusaidia sana kwenye kufanya kazi yako." Aliposema hayo akaita: "Hey!" Mara tokea ndani akaja mwanamke mrefu aliyevalia sketi ya kaki ya kumbana. Topu nyeusi iliyofunikwa na koti jeusi la kifungo kimoja.

Mwanamke huyu hakuwa mgeni mbele ya macho ya Jona. Alimtambua upesi kuwa ndiye yule aliyekuja nyumbani kwake na kumpatia wito wa Mheshimiwa.

Anaitwa Nade.

Uso wake mpana. Nywele zake nyingi anazozibana. Na miwani ya macho yenye fremu nzito nyeusi, vilimtambulisha upesi.
Alitambulishwa kwa Jona kama mlinzi binafsi wa Mheshimiwa. Jambo hilo likamshtua kidogo Jona. Hakulitarajia.

Mwanamke huyu hakuonekana kama mlinzi. Alikuwa mrembo sana kuwa mlinzi. Aidha kazi ya ukarani ofisini, au mapokezi hotelini ndizo ambazo ungezifikiria punde ungemwona.

Jona alijiuliza ni nini kilichofanya mwanamke huyo apewe kazi kubwa kiasi hicho. Hiyo ikawa mojawapo ya sababu ya kukubali kufanya naye kazi.

Alitamani kumuona akiwa kazini. Alitamani kuona nini kipo nyuma ya ulimbwende wa mwanamke huyo kikamfanya aaminike.

Alitaka kukosoa mawazo aliyoanza kuyajenga kichwani. "Sawa, nitafanya naye kazi," akajibu.

Mheshimiwa akatabasamu. "Hautajutia uamuzi wako," akasema.
.
.
.
.
***
LAKO JICHO!
 
Shukrani sema nashauri usitusahau sana au shusha mbili tatu Mkuu[emoji1][emoji1]
 
*JOANA ANAONA KITU USIKU --- 04*




ILIPOISHIA …




Baadae majira ya usiku, saa tano, Mama akaenda kumgongea mlango Moa. Akaketi pembeni ya kitanda na kumueleza:



“Rudisha bangili hiyo kwa Joana. Umenielewa?”
“Mama ame…”



“Sitaki maneno, Moa. Nimekwambia rudisha hiyo bangili, sawa?” Mama alisema akitumbua macho yake meupe nje. Moa akaogopa.




ENDELEA…




Japokuwa mama yake aliondoka, lakini mwanaume huyu hakulala kwa amani. Sauti ya mama yake ilikuwa inajirudiarudia masikioni mwake na kumgutua. Akafikiria pia kuhusu Joana basi ndiyo akazidi kukosa usingizi.
Akaamua kutoka kitandani na kwenda nje kibarazani. Huko akaegemea kingo ya kibaraza akiangaza mbali, mwili wake ukipulizwa na upepo wa bahari wenye fujo.



Akaendelea kuwaza hapo akitegemea upepo wa bahari unyakue angalau mawazo kidogo na kupumzisha kichwa chake.



Lakini twende mbele turudi na nyuma, mwanaume huyu alikuwa na jambo fulani la kutuweka wazi.



Pasi na shaka.



Ni yeye ndiye alimpokonya bangili Joana baada ya kusimuliwa yale yanayomtukia mwanamke huyo. Je kwanini alimpokonya? Ina maana anajua jambo kuhusu bangili hiyo?



Anadhani pengine ndiyo sababu ya mauzauza ya Joana? Japokuwa hakuwa na uhakika, aliamini bangili hiyo ndiyo adui haswa.



Simulizi za kale alizokuwa anazisikia, tangu akiwa utotoni, kumhusu mama yake kuhusishwa na ulozi zilikuwa zinaingilia sikio moja na kutokea lingine. Hakuwahi kuziamini kamwe.



Alibashiri ni kwasababu ya macho ya mama yake, na kovu kubwa usoni mwake ndivyo vilikuwa sababu ya shutuma hizo. Alikuwa anampenda mama yake, na mama yake alikuwa anampenda vilevile.
Kuna siku moja, akiwa mvulana mdogo wa miaka kumi na miwili, alirudi shule akiwa amechoka mno na mwenye njaa. Alikuwa anaburuza miguu na begi lake la mgongoni akilining’iniza mkononi.
Nyumba siku hiyo ilikuwa pweke asiwepo mtu hata mmoja.



Alimuita mamaye, lakini hakupata majibu. Kabla hata ya kwenda jikoni kutazama chakula kukidhi haja yake ya tumbo, akaenda kwanza chumbani mwa mama yake kutafuta.


Hakuzoea kujipakulia chakula mwenyewe, na hii ni kwasababu ya kudekezwa na wazazi wake tangu yeye ni mtoto wa mwisho.



Aligonga mlango pasipo majibu, akausukuma na kuzama ndani. Akaangaza angaza, hakuona mtu, lakini juu ya meza iliyokuwa imesimama pembeni ya kitanda akaona kisanduku kidogo cha chuma.



Kilikuwa rangi ya bluu iliyokoza. Na kalikuwa wazi.



Akapata hamu ya kutaka kujua kilichomo ndani. Akakisogelea na kutazama, ndaniye akaona bangili nyingi za shepu mbalimbali, na mikufu michache.
Bangili moja ikamvutia kwa kung’aa kwake, michoro na hata umbo lake mithili ya mawimbi ya maji. Basi akainyakua na kwenda nayo sebuleni. Akaichezea na kuijaribishia mkononi.
Ilikuwa inawakawaka!



Kwa muda kidogo bangili hiyo ikamsahaulisha uchovu na njaa aliyokuwa nayo. Alihisi ni ya gharama kubwa sana, na basi pengine kila mtu angependa kuwa nayo. Akaiweka kwenye mkoba wake kwa ajili ya kwenda kuwaonyesha na kuwaringishia marafiki zake shuleni kesho yake.



Baadae mama yake aliporejea, akamkuta akiwa tayari ameshakula na kujilaza na sare zake za shule. Hakugundua kama Moa amechukua moja ya bangili yake, akalaumu tu kwa kukuta kisanduku ki wazi.



“Huyu mzee anapenda kupekua vitu vyangu, kuna siku vitamtokea puani!” Moa alikumbuka namna mama yale alivyolalama. Ingawa alikuwa kwenye usingizi alisikia vema.



Alisikia pia na sauti ya kisanduku cha bangili na mkufu kikifungwa kwanguvu. Muda mfupi kidogo, mama yake akaja kumwamsha na kumtaka akaoge na kubadili nguo.



Kesho yake, asubuhi na mapema ya majira ya saa kumi na mbili kasoro, Moa akaamka kwa ajili ya kujiandaa kwenda shule. Hakuamshwa siku hiyo tofauti na ilivyo kawaida yake mpaka mamaye ampokonye blanketi, tena kwa mbinde.
Ni hamu tu ndiyo ilimkata usingizi na kumgutua – hamu ya kutaka kuringishia bangili kwa marafiki.



Alisugua meno na kuoga, mamaye akamkuta akiwa anavaa sare. Akatabasamu na kumpongeza:
“Umekua sasa, Moa. Ukiendelea hivyo utakuwa mtoto mwenye nidhamu na akili!”



Moa akatabasamu pasipo kutia neno. Alikuwa anakwepa macho ya mama yake mara kwa mara. Alitaka kuondoka haraka kwa kuhisi anaweza kugutukiwa.
Kweli akafanikiwa.



Kitu cha kwanza kukifanya wakati wa mapumziko, ikawa ni kuwakusanya marafiki na kuwaonyesha mali aliyo nayo – bangili. Wote wakatahamaki!
“Umeitoa wapi, Moa? Naweza nikaiona?”
Moa akatamba na kujivuna. Rafiki yake kipenzi aitwaye Filipe akamuazima bangili hiyo aenda nayo na atamrejeshea kesho.



“Nitakupa na zawadi, Moa,” Felipe akaahidi. Moa akasukumwa kumpatia. Kwani si atarejesha? Na zawadi si n’tachukua?



Felipe akaweka bangili mkobani, na wazo lake la kwanza lilikuwa ni kwenda kumpatia dada yake.



Siku iliyofuata, Moa akawahi pia kuamka na kwenda zake shule. Siku hiyo alikuwa anajua anapata zawadi na pia anarejesha bangili nyumbani. Faida maradufu!



Alilenga akishairudisha, basi achukue nyingine na mtindo uwe ule ule kama alioufanya awali. Atatengeneza faida kiasi gani? Aliwaza na kujikuta akijibu kwa tabasamu.



Lakini mbaya alipofika shule, hakumwona Filipe. Hakuwepo darasani wala shule nzima.
Akajihisi vibaya kwa kudhani amedanganywa, na pengine rafiki yake, Filipe, amemzulumu.



“Twende, mi napajua kwao!” Rafiki mmoja akamsahuri Moa. Basi wakakubaliana waende punde tu watakapotoka shule.



Ila kabla muda wa kutoka haujawadia, mwalimu wao wa darasa akaingia darasani na kuwataka watulie maana ana tangazo anataka kuwapatia. Wote wakatii agizo.



“Mwenzetu Filipe amefiwa na dada yake usiku wa kuamkia leo. Amefia huko baharini alipozama na kuokotwa.”
Moa akashikwa na huruma, pamoja pia na marafiki zake, kumbe sasa akajua nini hakikumleta Filipe shuleni, sasa hapo wakaongezeka idadi ya watakaoenda kwa kina Filipe, lengo likiwa kumpa pole.



Wakaongozana pia na mwalimu wa darasa kama mwakilishi wa shule.
Siku hiyo nzima Moa akaipotezea huko. Alimuuliza Filipe kuhusu ile bangili aliyompatia, Filipe akamwambia alimkabidhi dada yake, na hata alivyoenda huko baharini nyakati za usiku, alienda nayo.



Kwahiyo bangili ilikuwa imepotea.
Lakini kwanini dada yake Filipe aende baharini usiku? Yani atoke usiku na kwenda bahari tena pasipo kumwambia wala kumuaga yeyote? Japo Moa alikuwa mdogo, akili yake ilishangazwa sana na haya.



Kwasababu alichelewa mno kurudi nyumbani siku hiyo, mama yake akafungasha safari kwenda shule kumuulizia. Akapewa taarifa za msiba wa Filipe, rafiki yake Moa, akaona heri kwenda huko kumkuta mwanaye.
“Kwanini haukuja nyumbani kun’taarifu kuwa unaenda msibani?” Mama aliuliza kwa hasira.

Aliunyakua mkono wa Moa akaenda naye baada ya Moa kumuaga rafiki yake, Filipe.



Baadae wakiwa nyumbani wanakula, basi Moa akamuuliza mama yake kuhusu yale yaliyokuwa yanamtatiza kumhusu dada yake Filipe.



Namna alivyokufa maji kwa kutoka na kwenda baharini usiku wa saa sita bila kumuaga yeyote, wala kushirikiana na yeyote.



Mama yake akamkazia macho na kumuuliza:



“Kuna yeyote aliyemuona wakati anaenda huko baharini?”



“Ndio,” Moa akajibu. “Filipe alimuona. Akamuita mara tatu lakini hakugeuka wala kujali.”



Mama akanyamaza asiseme lolote lingine. Wakala na baadae wakati wa kulala, mama akaja chumbani kwa Moa.
Usoni alikuwa na ndita za mashaka. Mkono wake wa kushoto alikuwa ameukunja ngumi ukitetemeka.
“Moa,” akaita kabla hajaketi kitako kitandani.



Moa akaamka na kumtazama mama yake.



Uso wa mama ulikuwa na kielelezo kilichompa walakini, kuna jambo halikuwa sawa.



“Moa, umechukua bangili kule kwenye kisanduku chumbani?” Mama aliuliza.
Moa akajikuta anaishiwa nguvu kabla hata hajanena.





***

Sent from my SM-J110F using JamiiForums mobile app
 
Dah steve unatisha kaka....endelea kumwaga sumu.
 
Nashauri tumalizane kwanza na Anga la Washenzi then utaendelea na Joan anaona kitu usiku.
 
Back
Top Bottom