Familia tata

Familia tata

SEHEMU YA 11


Akakutana na picha aliyoipenda sana, alikuwa amepiga na marehemu Juddy, wakati flani wa sikukuu ya Krismas, miaka kadhaa iliyopita, aliipenda picha hiyo kwa vile ilimkumbusha mambo ya siku hiyo, ambayo hawezi kusahau.
SASA ENDELEA…
Ni siku ambayo alimjua mwanaume kwa mara ya kwanza. Alifanya tendo hilo katika vyoo vya ukumbi wa disco, katika ufukwe wa Coco, jijini Dar es Salaam.
“Ninahitaji kuongea na Festo,” alijisemea mwenyewe, akimkumbuka mvulana ambaye alifanya naye kitendo hicho, ambaye walikuwa bado wakiwasiliana, ingawa urafiki wao wa kimapenzi ulikuwa umefifia sana!
Festo baada ya kumaliza shule, alienda India kusomea udaktari, mara ya mwisho walipowasiliana, ni wakati alipompigia simu akiwa Mumbai, akimtaka ampokee uwanja wa ndege wa Heathrow, jijini London alipokwenda kwa shughuli zake. Hiyo ilikuwa mara yake ya kwanza kufika Uingereza na hakutaka kuhangaika. Alimpokea na kumwelekeza sehemu anayoweza kufikia.
Baada ya hapo waliwasiliana tu kwa simu hadi Festo aliporejea Dar es Salaam na kuajiriwa katika hospitali ya Taifa Muhimbili. Asfat akaitoa simu yake ya mkononi, akatafuta jina alilolihitaji, alipolipata akabonyeza kupiga.
“Mambo?” Asfat alizungumza mara baada ya upande wa pili kupokea.
“Poa, umekuja lini mbona kimya kimya,” upande wa pili nao ukajibu.
“Nimepata msiba ghafla, mdogo wangu Santo amefariki juzi kwa kugongwa na gari,”
“Dah, pole sana aisee, mipango ikoje,”
“Tunategemea kuzika keshokutwa hapa hapa Dar,” alisema Asfat.
Baada ya kimya kidogo kupita, Asfat akarudi tena simuni.
“Festo, nina shida sana ya kuonana na wewe, ni muhimu sana katika maisha yangu kwa kweli,”
“Nitakuja msibani kesho, tutaongea.”
“Hapana, sitaki tuzungumzie huku, iwe sehemu nyingine,” Asfat alisema na kumfanya Festo ahamishe hisia zake, akadhani mwenzake alihitaji mazungumzo ya kimapenzi.
“Wapi sasa, hoteli?” akajikuta akiuliza.
“Hapana, sehemu tu tulivu, ninahitaji kuongea na wewe, nina ishu ya muhimu sana kwangu,”
Baada ya kujibishana kwa muda wakakubaliana siku na muda wa kuonana!
Shughuli ya msiba iliendelea, maneno ya hapa na pale yaliendelea kama kawaida ya misiba ya uswahilini. Kwa muda wote, mama Juddy hakubanduka karibu na mama Tonny, alikaa naye na kumfariji kwa kila kilichoendelea. Hali kama hiyo pia ilikuwa kwa mzee Linus na rafiki yake mzee Komba.
Watoto wa familia zote nao walikuwa kitu kimoja, hakuna mtu aliyeonyesha tofauti. Walishirikiana kama kawaida hadi msiba ule ukaonekana wa familia zote.
Hatimaye mazishi yakafanyika katika makaburi ya Nakasangwe, karibu kabisa na sehemu aliyozikwa Juddy, mwaka mmoja na nusu uliopita. Wiki mbili baada ya mazishi hayo, maisha yaliendelea kama kawaida.
***
“Ndiyo hivyo Festo, nataka kulipiza kisasi, nisaidie jinsi ya kuipata hiyo sumu,” Asfat alimalizia kwa kumwambia mpenzi wake wa zamani, baada ya kumweleza mkasa wa familia zao na jinsi ambavyo hakuridhishwa na kifo cha mdogo wake, akiamini Baptist alifanya makusudi.
Walikuwa wamekaa pembeni katika ufukwe wa Kawe, wakiwaangalia watu mbalimbali wakipunga upepo na kuogelea.
Asfat alitaka kulipiza kisasi kwa kumuua ye yote katika familia ya mzee Linus, ilimuuma sana.
“Hapana Asfat, siwezi kukusaidia kutimiza lengo lako, sisi tumeapa kumsaidia mgonjwa na siyo kummaliza, isitoshe, kwa jinsi watu walivyokuwa wakizungumza siku ile pale msibani, inaonekana kabisa ni ajali,” Festo alimwambia Asfat, aliyetoa macho kwa mshangao.
 
SEEMU YA 12


“Hapana Asfat, siwezi kukusaidia kutimiza lengo lako, sisi tumeapa kumsaidia mgonjwa na siyo kummaliza, isitoshe, kwa jinsi watu walivyokuwa wakizungumza siku ile pale msibani, inaonekana kabisa ni ajali,” Festo alimwambia Asfat aliyetoa macho kwa mshangao.
Endelea.. .
“Festo, kumbuka tumesaidiana mambo mengi sana tokea tufahamiane, leo mimi nina shida, kesho itakuwa upande wako na hii ni ahadi tuliwekeana, hata tukiachana kimapenzi tutaendelea kusaidiana na wewe ni mwanaume wangu wa kwanza,” Asfat alimweleza mwenzake.
“Ni kweli tuliwekeana ahadi, lakini sasa hivi mimi ni daktari na nimekula kiapo. Siwezi kufanya hicho kitu unachokisema na ningekushauri uachane kabisa na mawazo hayo, katika dunia hii utaua wangapi kwa visasi?”
Asfat akasimama, akamtazama Festo kwa jicho la hasira, akaanza kutembea akiondoka eneo hilo. Festo alimtazama, naye akasimama, akaanza kumfuata taratibu..
“Asfat,” Festo alimuita akiwa amemkaribia mwenzake ambaye alitembea kwa mwendo wa polepole. Msichana huyo akageuka bila kusema neno, akasimama.
“Umekubali kunisaidia?” alimuuliza.
“Ndiyo,” akamjibu huku akimvuta mkono, akamuongoza kwenye viti vilivyotapakaa katika ufukwe huo wa Kawe. Wakakaaa, akamtazama usoni na kuanza kuzungumza.
Festo alitaka kubadili mawazo ya Asfat, akaanza kumwelezea matukio mbalimbali ya visasi aliyosimuliwa na watu na mengine kuyaona mwenyewe, lakini mara zote, waliotenda visasi hivyo walibainika na kukamatwa. Alimsihi sana kumrejea Mungu, kwani katika maisha, makosa hutokea.
Alimtahadharisha kuwa endapo kitendo chake kitabainika, itamaanisha kusambaratisha kabisa familia zao, kwani tabia ya visasi itaendelea na mwisho wa siku, hakuna atakayekuwa salama.
“Wewe leo unataka kwenda kumuua mtu pale, wakikugundua, na wao watataka kuua mtu kwenu, mauaji hayatakoma, nani atasalimika? Nikushauri mpenzi wangu, amini kuwa ile ni ajali, mbona mama yako anasisitiza ni ajali, kwa nini wewe ung’ang’anie ni kusudi?” Festo alimsisitizia Asfat ambaye kwa muda wote alibaki kimya.
“Haya nimekuelewa Festo, asante kwa ushauri wako, nitauzingatia, ila ninaumia sana, Santo amekufa akiwa bado mdogo sana, alihitaji kufurahia maisha,” hatimaye Asfat alisema.
“Asante kwa kunielewa Asfat. Halafu Uingereza imekupenda sana, umetakata mbaya, nahisi kukupenda upya,” Festo alimwambia huku akimshika kiganja cha mkono wake wa kulia, akikisugua katikati kwa kidole chake.
“Hata wewe umebadilika sana Festo, umekuwa mzuri zaidi, nadhani India ilikuwa poa sana kwako,” Asfat naye alijibu, akimsogelea karibu zaidi.
Wakazungumza mambo yao mengi, wakakumbushana enzi zao na hatimaye, wakajikuta wakikumbatiana, wakabusiana na baadaye, wakaondoka safari yao ikiishia hotelini!
***
Asfat alikuwa katika mtaa wenye pilika nyingi wa Msimbazi, Kariakoo jijini Dar es Salaam, akihama duka moja hadi jingine akitafuta mahitaji kwa ajili ya saluni yake aliyofungua eneo la Tegeta. Alihitaji kununua Stimmer, Dryer, vioo na vitu vingine vidogovidogo.
Ghafla, akiwa ndani ya duka moja la Mhindi, akasikia gari likifunga breki kali, iliyosababisha kelele kubwa ikifuatiwa na mayowe. Akijua mtu atakuwa amegongwa, akatoka nje haraka kushuhudia kilichotokea.
“Pumbavu kabisa wewe, mimi mbwa kama wewe huwa nawapitia kwa tairi tu, shenzi kabisa, bahati yako ningekuua,” sauti kali ilitoka katika gari lililokuwa limesimama baada ya kumkosa kosa mtembea kwa miguu mmoja, ambaye alikuwa anahema, akiwa haamini kama amepona!
 
SEHEMU YA 13

Simulizi hii ilikatishwa mwishoni mwa Februari mwaka huu kwa sababu zilizo nje ya uwezo wetu. Kutokana na maombi ya wasomaji wengi, tunaendelea kuichapisha tena...
Tuliishia pale ambapo marafiki wawili, Mzee Linus na Mzee Komba, ambao wakati huo walikuwa wamewapoteza watoto wao wawili kwa ajali, Asfat na Festo, walikutana nje ya nyumba zao na kuzungumzia uvumi waliousikia kutoka kwa wake zao.
“Lakini kuna kitu kinanisumbua, ambacho bahati mbaya nimejua leo,” wakati akisema maneno haya, macho yake aliyakaza machoni mwa rafiki yake.
“Vipi tena, maneno gani rafiki?” aliuliza mzee Linus.
Mzee Komba aliendelea kumkazia macho rafiki yake, kwa mbali machozi yakaanza kulenga lenga machoni mwake. Hali ile ilimfanya na Mzee Linus naye ajisikie majonzi, akatoa kitambaa mfukoni mwake na kujifuta machozi.
“Kuna maneno nimesikia, sitaki kukaa nayo kwa sababu wewe ni ndugu yangu,” Mzee Komba alimwambia mwenzake, naye akijifuta machozi machoni mwake.
“Yapi hayo ndugu yangu, niambie tujadili,” Mzee Linus alimwambia akiwa na hamu kubwa ya kujua, ingawa hisia zilimpeleka kuhusu mazungumzo yake na mkewe, muda mchache uliopita.
Mzee Komba hakumung’unya maneno, alimweleza kila kitu alichoambiwa na mkewe na kumtaka naye amweleze ukweli kuhusu jambo hilo kama alikuwa na fununu zozote.
“Hata mimi nimesikia leo hii hii taarifa kama hizi kutoka kwa mke wangu, lakini ni tofauti kidogo, yeye anamlaumu Festo kuwa amemuua mwanaye kwa makusudi,” Mzee Linus alimwambia mzee Komba.
“Linu, sisi ni wanaume, hawa ni watoto wetu tumewapoteza, tuelezane ukweli, wewe unalichukulia vipi suala hili, mimi naona ni bahati mbaya tu,” mzee Komba alimweleza rafiki yake.
“Sijawahi kuwa na mawazo yoyote mabaya kuhusiana na maafa yanayotokea, hata mimi najua ni bahati mbaya, sema ninachokiona, hawa akina mama wanaweza kuleta matatizo, ni vema tukawaweka sawa, maana wanaweza kusambaza sumu ikazitesa familia zetu,” mzee Linus alimwambia mzee Komba.
Wakakubaliana juu ya hilo. Wakashikana mikono, wakakumbatiana na wakaanza kutembea kidogo kidogo kuelekea nyumbani kwao!
Shughuli za msiba ziliendelea taratibu, familia zote mbili zikakubaliana kufanya mazishi siku moja, eneo moja.
Siku ya mazishi ikatangazwa, ni siku tatu baada ya ajali ile mbaya na ya kusikitisha. Wote walitakiwa kuzikwa katika makaburi ambayo ndugu zao wawili, Juddy na Santo walizikwa.
Hatimaye siku hiyo ikafika, umati wa watu ulianza kukusanyika katika uwanja uliotenganisha nyumba hizo mbili jirani mapema asubuhi.
Kadiri muda ulivyozidi kwenda, ndivyo walivyoongezeka na hadi ilipofikia saa saba mchana wakati wa chakula, eneo lote lilikuwa limetapakaa watu isivyo kawaida.
Saa nane mchana, miili ya marehemu hao wawili iliwasili ikiwa katika magari mawili madogo kutoka kampuni ya mazishi ya Kwishney Funeral Center na kusababisha eneo hilo kugeuka ghafla kuwa la vilio kutoka kwa akina mama na watoto, huku watu wazima waliokuwa wakiwafahamu marehemu hao wakijifuta machozi!
Baada ya chakula, ibada ya kuwaombea marehemu ilianza ikiongozwa na padre wa Kanisa Katoliki la Tegeta, Jackson Ntandu. Ni wakati akitoa neno baada ya sala hiyo ndipo watu walipojikuta wakibubujikwa na machozi, hasa alipokuwa akirudia msemo maarufu wa ‘hakuna ajuaye siku wala saa’.
“Dakika mbili kabla hawajakutana na vifo vyao, Asfat na Festo walikuwa wazima wa afya na hakuna hata mtu mmoja duniani aliyeweza hata kufikiri kuwa hatutakuwa nao tena.
Rafiki yangu mmoja amenihakikishia kuwa aliwaona wawili hawa walipokuwa wakiingia garini pale Flamingo kurejea nyumbani, lakini zile ndizo zilikuwa dakika zao za mwisho mwisho duniani.
“Wewe leo upo hapa pamoja nasi tunaaga miili yao kwa sababu roho zilishakwenda, hatujui kama zimeenda peponi au motoni, umeshajiandaa kwa ajili ya safari hii ambayo hakuna ajuaje siku wala saa? Jiandae kwa safari ya wakati wowote na maandalizi mazuri ni kwa kufanya ya kumpendeza Mungu,” alisema Padre Jackson na kuwafanya watu wote kuwa kimya.
Baada ya ibada hiyo, kazi ya kuwaaga marehemu ilifanyika na kusababisha vilio vingi kutoka kwa waombolezaji. Baada ya zoezi hilo, kazi ya kuelekea makaburini ilianza kwa misururu mirefu ya watu kuandamana kusindikiza miili iliyokuwa ndani ya magari.
inaendelea.
Chanzo Globalpublishers
 
SEHEMU YA 14


Ilipoishia wiki iliyopita..
Ni saa moja usiku.
Akachukua simu yake, akatafuta jina flani, akabonyeza, ikaanza kuita, wimbo mzuri wa Injili ukisikika!
“Kaka Festo mambo?” Asfat alizungumza.
Sasa endelea..“Aaah Asfat upo? Long time, niambie,” Festo, akiwa anarejea nyumbani kutoka kwenye mishemishe zake, aliipokea simu hiyo kwa mshangao mkubwa, ingawa kila mmoja alikuwa na namba ya mwenzake, lakini hawakuwahi kuwasiliana hata siku moja.
“Uko wapi, home?”
“Hapana ndo narudi, vipi?”
“Nataka tuonane, nina shida kidogo,”
“Wewe uko wapi?”“Niko home, tukutane basi kwa Mzee Mathias,” Asfat alisema na walipokubaliana akakata simu.
Hakukuwa na umbali mrefu kutoka nyumbani kwao hadi kwa Mzee Mathias, kama siyo kukingwa na nyumba kadhaa, mtu angeweza kupaza sauti na kusikika. Kulikuwa na baa moja kubwa na ukumbi maridadi, pia kulikuwa na michezo ya watoto, pool, televisheni kubwa iliyokuwa ikionyesha michezo mbalimbali ya soka la kimataifa.
Badala ya kuelekea nyumbani, Festo akaliongoza gari kuelekea eneo hilo, ambalo hata hivyo, ilikuwa ni uwanja wake wa nyumbani kwa vile kila disko la mwishoni mwa wiki, ilikuwa ni lazima ahudhurie na alifahamika vyema.
Mara tu baada ya kukata simu, Asfat aliinuka na kwenda kumuaga mama yake, akimwambia kwamba anakwenda kwa mzee Mathias kununua chips kwa vile hakujisikia kula ndizi na nyama zilizopikwa nyumbani.
Mama hakuwa na kinyongo, akamruhusu na kumuomba amchukulie kiroba cha konya, akidai alijisikia kama mafua kwa mbali na anadhani akinywa kinywaji hicho, atauondoa ugonjwa huo!
Festo alikuwa wa kwanza kufika kwa mzee Mathias, akalipaki gari vizuri na kuteremka, vijana wachache waliokuwepo eneo hilo, ambao wanamfahamu walimkaribisha kwa bashasha.
Akamwita mhudumu, akamtaka awape kiroba kimoja kimoja cha konya wale vijana wanne waliomzonga, mwenyewe akajiagizia mzinga mzima na kinywaji kisicho na kilevi.
“Vipi kaka Festo,” Asfat alimsemesha baada ya kuwasili na kuungana naye pale alipokaa, kijana huyo akaitika kwa kutingisha kichwa wakati akipeleka fundo la kinywaji kinywani kwa mkono wake wa kushoto, huku akimpa wa kulia kumsalimia!
Haraka, wahudumu wakitambua kuwa wale walikuwa ni kaka na dada, wakasogea kusikiliza nini ambacho msichana angetaka, naye aliagiza kilevi alichokipenda na kuomba aletewe chips kuku, kwani alikuwa anajisikia njaa.
“Niambie Asfat, Uingereza imekupenda sana, umeng’aa, bila shaka utarudi huko kufanya kazi,” Festo alimsemesha dada yake huku akimpa tabasamu la nguvu!
“Hata siendi, baridi kama nini Ulaya, watu hawajui tu wanakimbilia kwa sababu ya ushamba wao.
Mimi nitafanya kazi hapa hapa Bongo, ikibidi kutoka basi itakuwa Afrika, sitaki kabisa Ulaya, kwanza kodi kubwa sana, mshahara wote unaishia kwenye kodi,” Asfat alimwambia Festo.
“Halafu Wabongo bwana, sasa wewe hutaki ukatwe kodi, si ndo inasaidia matibabu na kwenye majanga, kwani mnavyosema sijui Ulaya mtu unatibiwa vizuri na watoto wanasoma bure elimu bora unadhani kwa nini, kwa sababu ya kodi. Huku hamtaki kukatwa kodi halafu mnalalamika huduma mbovu za jamii,” Festo alimchombeza Asfat.
“Kweli lakini kaka Festo unadhani, Ulaya unapiga simu ya dharura, dakika moja tu wamefika na huduma utadhani unalipia, kwa hilo lazima tuwasifu,” alisema msichana.Baada
ya stori mbili tatu za Ulaya na Bongo kutawala, hatimaye Asfat alibadili mazungumzo!“Kaka Festo nina shida kubwa na wewe na ndicho nilichokuitia,” Asfat alisema. Festo akabaki kimya, akiwa na hamu kubwa ya kusikia alichoitiwa, akatingisha kichwa kuashiria aendelee kuzungumza.
“Najisikia kukupenda, nataka uwe mpenzi wangu,” Asfat alisema, akiwa amemkazia sura Festo.
“Whaat?” Festo aliuliza kwa mshangao!
inaendelea
 
SEHEMU YA 15


“Kaka Festo nina shida kubwa na wewe na ndicho nilichokuitia,” Asfat alisema. Festo akabaki kimya, akiwa na hamu kubwa ya kusikia alichoitiwa, akatingisha kichwa kuashiria aendelee kuzungumza.
“Najisikia kukupenda, nataka uwe mpenzi wangu,” Asfat alisema, akiwa amemkazia sura Festo.
Whaat?” Festo aliuliza kwa mshangao! Sasa endelea..
“Hujanisikia kaka Festo? Nakupenda, nataka uwe mpenzi wangu,” Asfat alirudia tena kumwambia kijana aliyekuwa amekaa mbele yake, ambaye kiumri ni mkubwa kwake kwa miaka mitano.
Festo akamtazama vizuri Asfat, ni binti mrembo kuliko wasichana wengi aliowahi kutoka nao, lakini siku zote amekuwa dada yake. Alikuwa ni swahiba mkubwa wa marehemu mdogo wake, Juddy.
Ni dada yake kabisa, anakijua hadi chumba anacholala nyumbani kwao, anamjua kila mtu kwao, ameingia kila chumba nyumbani kwao, anawajua ndugu zake wote..!!
“Kwa nini Asfat?” Festo, baada ya kumtazama huku akitafakari kwa muda mrefu, alimuuliza.
“Basi tu, imetokea. Najua unajiuliza maswali mengi sana, hata mimi nilijiuliza kabla ya kupata ujasiri wa kukuambia kaka,” Asfat alimwambia Festo.
“Dada nadhani iwe hapana, unanijua vizuri kaka yako, sina kawaida ya kutulia na msichana mmoja, mimi bado kijana, siwezi kuruhusu nikufanyie hivyo wewe.” “Utatulia tu, mimi niko hot kaka, utanipenda, lakini hata kama hautatulia, sitajali, kwa sababu nimeamua kukupenda nikijua wazi jinsi ulivyo, usijali,” Asfat alimwambia kaka yake.
Festo alicheka sana, akaagiza bia ingine kwa ajili ya Asfat, akaagiza na mishikaki kadhaa. Asfat hakuelewa kama ombi lake lilikubaliwa au la, lakini kwa kuwa alimfahamu jirani yake huyo kama mtu wa kinywaji, alijua atalipata jibu, tena zuri, kabla hawajaondoka.
Festo akazama katika mawazo. Hakuwahi kufikiria hata siku moja kama angeweza kuwa kimapenzi na Asfat, siyo tu kwa sababu alikuwa rafiki wa karibu sana wa mdogo wake, lakini pia alikuwa ni kama dada yake wa kuzaliwa. Tokea kukua kwao, wameishi kama ndugu. Leo awe mpenzi wake, wataeleweka? Moyo wake ukakataa.
Akamtazama vizuri msichana aliyekuwa mbele yake, alivutia kwa kweli. Kifua chake kilijaa vizuri, sura yake ilitulia na kwa hakika, alikuwa na figa nzuri mno kwa viwango vya Festo. Lakini kitu flani ndani ya nafsi yake, kilikataa kabisa wazo la kuruhusu hisia za kimapenzi.
Asfat alikuwa akimtazama Festo kwa jicho la huba usoni, lakini ndani ya moyo wake alimchukia kupita kiasi, alidhamiria kumuangamiza kwa namna yoyote. Alizijua tabia za walevi, hata kama alijifanya kutomtamani kwa sasa, baadaye angebadilika tu, hivyo akavuta subira na kuzidi kuinywa kwa fujo bia yake ili iishe, aagize nyingine.
Wakahamia katika stori zingine za kimaisha, wakazungumza sana huku wakiongeza kinywaji, Ndovu na Konyagi. Taratibu zikaanza kupanda, kwa makusudi kabisa, Asfat akamshauri kaka yake wahamie katika kibanda kilichokuwa bila taa, akidai mwanga unamfanya alewe haraka.
Ilikuwa sababu ambayo Festo aliielewa na kuikubali, wakahamia sehemu nyingine yenye giza, wakakaa, viti vyao vikiwa karibu zaidi!
Waliendelea kunywa, Asfat katika bia yake ya sita, akajikuta akishindwa kuvumilia, akapeleka mkono wake katika kifua cha Festo, ambaye sasa mzinga wake wa pili ulikuwa unakaribia nusu.
Festo alipenda kufunga shati lake hadi kifungo cha juu kabisa, msichana huyo akafungua vifungo viwili, kisha akauingiza mkono wake na kuanza kuchezea nywele chache zilioota kifuani. Kijana wa kiume alimtazama akiwa haamini kama binti ambaye kwa miaka yote amekuwa dada yake, alidhamiria tendo lile ovu.
“Festo,” aliita kwa sauti ndogo, iliyojaa mahaba!
“Sema,” Festo aliitikia huku akiupeleka mkono wake katika kifua, akabonyeza bonyeza mara kadhaa na kujikuta akivutiwa nayo.
“Hujanijibu ombi langu, nakupenda sana kaka Festo, tafadhali nikubalie, usifikirie kuhusu watu watasemaje, haya ni maisha yetu mimi na wewe,” alisisitiza!
“Hebu punguza munkari mtoto mzuri, mbona una haraka?” Festo alimwambia Asfat, ambaye kwa maneno hayo akajisogeza karibu zaidi, sasa wakawa wanapumuliana.Hadithi
 
SEHEMU YA 16


“HEBU punguza munkari mtoto mzuri, mbona una haraka?” Festo alimwambia Asfat, ambaye kwa maneno hayo akajisogeza karibu zaidi, sasa wakawa wanapumuliana.
Sasa endelea..Katika hali ya ulevi, Festo alijikuta akilegea, kifua cha Asfat kilimpa ushawishi mpya, akajikuta akihemka.
Mikono yake ikafanya ziara isiyo rasmi katika maeneo kadhaa ya binti huyo, ambaye miaka yake minne aliyoishi na kusoma Ulaya ilimfanya azidi kuvutia, akionekana msichana wa makamo, wakati ukweli ni kwamba alikuwa bado mdogo.
“Asfat,” Festo hatimaye aliita, akiwa amemsogeza jirani zaidi, vifua vyao vikiwa vimegusana. Moyoni, msichana akajikuta akiangua kicheko cha ushindi, kasi ya kisasi ikazidi mapigo yake ya moyo.
“Abeee,” Asfat aliitika kimahaba, kitu kilichomuongeza munkari Festo.
“Sikuwahi kufikiria kama tungeweza kufanya hivi, wewe ni msichana, kwa kuwa umeridhia mwenyewe jambo hili, sina kipingamizi, nadhani ulichelewa kuniambia hata hivyo, unaonekana ni hot kweli kama ulivyosema, ooh, I love you,” Festo, asijue alikuwa ameingia kirahisi katika mtego wa Asfat, alijikuta akisema maneno hayo.
“Me too,” Asfat alijibu, naye huku akijiweka karibu zaidi, akiruhusu mwili wake laini uwe mali ya Festo.
Ni saa nne kasoro robo usiku. Mwili wa Festo ulishaanza kuchemka, kinywaji kile kikali, kilionekana kumzidi nguvu. Joto la msichana mzuri kama aliyekuwa pembeni yake, lilimfanya auruhusu mwili wake ufikie tamati ya matamanio yake. Hakudhani kama alihitaji ufundi zaidi, kilichokuwa mbele yake ni kumalizia kazi ndogo iliyoanzishwa na Asfat.
“Nadhani tuondoke, twende zetu sehemu mara moja halafu turudi home, au?” Festo alimwambia Asfat, aliyejibu kwa kutikisa kichwa. Wakainuka, wakalipa fedha walizokuwa wakidaiwa, wakaingia ndani ya gari, Festo akakanyaga mafuta, gari likaserereka na kutokomea kwa kasi.
Vijana kadhaa waliokuwepo wakashangilia kama kawaida yao kila Festo alivyozoea kuendesha kwa manjonjo, wazee wazima wawili watatu waliokuwepo wakatingisha vichwa vyao kwa masikitiko.
Gari likasimama nje ya Hoteli ya Flamingo, iliyopo eneo linalojulikana kama Madale kwa Kawawa. Mhudumu mmoja wa kiume alilifahamu gari la Festo na alimjua fika kijana huyo mpenda mabibi. Akamfuata na kumsalimia.
“Kama kawaida?” alimuuliza baada ya kumsalimia na msichana aliyekuwa naye.
“Unauliza majibu,” Festo alimwambia huku akiweka vitu sawa ndani ya gari lake.
“Inaonekana wewe ni mteja mzuri hapa,” Asfat alimuuliza Festo.
“Nilishakuambia mimi kijana, niliogopa tokea awali kukukwaza, lakini umesema nitatulia, hebu twende ukanitulize,” Festo alisema huku akimpiga busu Asfat, wakashuka garini, wakatokomea ndani.
***
Saa moja baadaye, Festo na Asfat waliibuka kutoka ndani, kila mmoja akionekana kufurahia nafsi yake. Wakatafuta kiti kilichokuwa pembeni kidogo, wakakaa na kuagiza chakula, Festo akiletewa mchemsho wa nyama ya ng’ombe, huku Asfat akila ndizi za kuchoma na mishikaki.
Ilikuwa ni moja ya siku chache ambazo Festo aliwahi kujisikia vizuri baada ya kuwa na mwanamke. Ni kweli, Asfat alikuwa hot. Alihisi kukosa mambo mengi kwa msichana huyu, na kwa mara ya kwanza katika maisha yake ya kimapenzi, akahisi wivu.
Na hata Asfat, alimsifu Festo. Siku zote alimuona kijana mlevi, asiye na dira kimaisha na aliamini kabisa, kwa vyovyote pombe zingemfanya kuwa goigoi kitandani. Alikosea, jamaa alikuwa fundi, muwajibikaji. Akajihisi kumpenda pia, alitamani aanze maisha rasmi na kijana huyo.
Lakini upendo wake kwa mdogo wake Santo, ulilifukuza haraka wazo na kuishi kimapenzi na Festo, alitamani kumuangamiza, wakati wowote akipata nafasi, hata leo hii. Kwa hasira, akaagiza bia!!
Na festo akalazimika kuagiza mzinga mdogo wa konya, wakanywa huku wakihimizana kumaliza ili wawahi nyumbani.
Wakamaliza vinywaji vyao, wakaanza kulielekea gari. Asfat akaomba aendeshe yeye, Festo akamruhusu, akazunguka kushoto, akimuacha msichana akielekea kulia.
Nini kiliendelea? Festo na Asfat wamepona? Usikose kufuatilia muendelezo wa simulizi hii katika toleo lijalo.
 
SEHEMU YA 17


WAKAMALIZA vinywaji vyao, wakaanza kuliekea gari. Asfat akaomba aendeshe yeye, Festo akamruhusu, akazunguka kushoto, akimuacha msichana akielekea kulia.
Asfat aliliondoa gari taratibu na kuliingiza barabarani, akaanza safari ya kuelekea nyumbani kwao, Nakasangwe.
Akili yake yote ilipanga kumuangamiza Festo katika mteremko unaotoka kwa Mzee Mathias kuelekea nyumbani kwao. Kulikuwa na mtaro ambao alidhamiria uwe mwisho wake.
Kila mtu alikuwa kimya, Festo alirejesha kumbukumbu za jinsi alivyotumia muda wake na msichana huyo, miguu yake ikiwa juu ya dash-board, viatu akiwa amevivua. Alifumba macho katika staili flani ya kuuita usingizi. Macho ya Asfat yalikuwa barabarani, akiyakwepa mashimo ya maji, pamoja na mifereji iliyochimbwa kwa ajili ya kupitisha mabomba ya maji kila baada ya urefu mfupi.
Alipofika eneo hilo la kwa Mzee Mathias, wakielekea katika mteremko mkali, Festo akiwa anasinzia, Asfat akaongeza mwendo, akaifuata nguzo moja kubwa ya zege, iliyojengwa kutenganisha ukuta wa shule ya sekondari ya Maendeleo na makazi ya wananchi. Nguzo ilikuwa upande wa Festo, akiwa ameuma meno, akalilenga gari usawa ule ule aliokaa Festo!
Kishindo kikubwa kikasikika, kikafuatiwa na makelele ya gari kukosa mwelekeo na baadaye kidogo, gari hilo likaishia kwenye mtaro ambapo pia lilitoa mshindo mkubwa!!!!!
***
Mama Tonny alikuwa amesubiri sana chips alizomuagiza Asfat, akaona muda unayoyoma. Kwa akili ya utu uzima, hakutaka kujisumbua kumpigia simu kumkumbusha, alijua mwanaye ameshakuwa mtu mzima, mambo mengine siyo ya kumfuatilia sana, akaamua kuingia chumbani kwake kulala.
Na hata alipoungana na mumewe chumbani, hakusema lolote kuhusiana na Asfat. Hawakuwa na kawaida ya kuwaulizia watoto wao, hasa wakubwa, kwani huo ulikuwa ni wakati wao na wenyewe waliamua kuishi maisha hayo. Waliamini vijana wao wanao uwezo wa kujisimamia wenyewe na hivyo ndivyo walivyoishi, hawakuwahi kusikia matatizo yoyote kwao, kuhusiana na maisha yao nje ya nyumba.
Walizungumza mambo yao ya maisha, mipango endelevu ya kipato cha familia yao na hatimaye wakaingia kwenye ulimwengu mwingine usiosimulika, kabla ya kila mmoja kupitiwa na usingizi!!
***
Kevin, kijana mwenye umri wa miaka 19, bitozi, jirani yao akina Festo, alikuwa amejibanza kwenye ukuta wa moja ya nyumba za maeneo hayo, akiwa anazungumza na msichana mpenzi wake, Munira. Hawa ni wapenzi wa muda mrefu, lakini muda mwingi hawako pamoja kwa vile msichana alikuwa akisoma Arusha, katika shule ya kimataifa ya Tanganyika wakati Kevin, ambaye mtaani alifahamika kama Kev, alikuwa akisoma Morogoro High School.
Wakiwa wamekumbatiana ukutani hapo, walisikia gari dogo likiendeshwa kwa mwendo wa kasi kuteremka kuelekea eneo la makazi yao. Mwendo ule uliwatisha, wakaachiana…
“Munny, wale watakuwa ni majambazi wametoka kufanya uhalifu, ule mwendo hawafiki,” Kev alimwambia mpenzi wake, wakiliangalia gari hilo lilivyokuwa likishuka kwa mwendo mkali na wa kutisha.
“Kev, Kev wanakufa hao jamani,” Munira alimwambia mwenzake, sasa akiwa amemkumbatia kwa nguvu, huku akihema!!!
***
Kishindo kile kilikuwa ni kikubwa sana, kilisikika kwa nguvu kwa kila mmoja. Baba na Mama yake Tonny walishtuka usingizini kutokana na mlio ule wa kutisha, wakazi wengine wote wa eneo lile nao walisikia.
Ingawa ulikuwa ni usiku, vumbi kubwa lilionekana kutokea eneo la ajali. Watu wakaanza kusogea taratibu. Kulikuwa kimya, hakuna mtu aliyeonekana ametoka, hakuna sauti iliyosikika kuomba msaada. Wakazidi kusogea, tochi zikiwaka, zikasogea zaidi na kulikuta gari limelala mtaroni!
Je nini kimetokea? Kuna usalama wowote kwa walio ndani ya gari? Usikose kufuatilia katika toleo lijalo ujue kinachoendelea katika simulizi hii ya kusisimua.
 
SEHEMU YA 18


Kulikuwa kimya, hakuna mtu aliyeonekana ametoka, hakuna sauti iliyosikika kuomba msaada. Wakazidi kusogea, tochi zikiwaka, zikasogea zaidi na kulikuta gari limelala mtaroni!
Michirizi ya damu ilionekana ikitoka ndani ya gari na kusambaa katika mtaro.
Mtu mmoja akakumbuka kuangalia namba za gari, alipoziona na kuhakiki, akapiga kelele!
“Festo huyu jamani, atakuwa amekufa, maskini weee!”
Watu wakazinduka, haraka wakalifuata gari ili kulikagua. Wakakuta watu wawili wamekunjwa. Ilikuwa rahisi kumtambua Festo, licha ya kuwa alikuwa amebanwa sana, lakini mwanamke aliyekuwa upande wa dereva, aliwasumbua watu kumtambua mara moja. Hakukuwa na dalili za uhai kwa watu hao, maana wote walionekana wametulia, hakuna aliyeonyesha kuhangaika!
Baada ya kazi kubwa, dakika 45 baadaye, walifanikiwa kuitoa miili ya watu wale wawili waliokuwa ndani. Wanawake walikaa mbali, wakilia, hasa baada ya kutambuliwa kwa Festo, wakabakia wameziba midomo yao wakitafakari mtu wa pili angekuwa ni nani.
Nywele bandia alizovaa Asfat mara ya mwisho, ndizo zilizowafanya waliomuona jioni hiyo, kutambua kwamba ndiye alikuwa abiria mwingine kwenye gari lililopata ajali ile mbaya.
Maiti wale wakapakiwa katika gari, wakakimbizwa hospitalini kwa uhakika zaidi. Katika hospitali ya Mwananyamala, daktari alithibitisha kwamba wawili hao walikuwa wamefariki!
***
Nyumba zile majirani zilipata msiba mkubwa wa ghafla, maneno, kama ilivyo kawaida yakaanza kutolewa na watu wa karibu. Katika miaka yote ya urafiki wao, kujuana kwao, haikuwahi kutokea hata mara moja kwa Asfat na Festo kuwa karibu kiasi hata cha kupanda gari moja. Tukio lile liliwashangaza wengi, akiwemo mama yake Asfat.
“Mume wangu, nina mashaka sana,” Mama Tonny alimuambia mumewe, wakiwa wawili chumbani kwao, wakati ndugu wakiwa nje ya nyumba yao.
“Juu ya nini mama Tonny, usiwe na mawazo sana, tuzidi kumshukuru Mungu,” mumewe alimwambia, akiwa hana wazo lolote kichwani mwake.
“Festo kaniulia tena mwanangu,” Mama Tonny alisema, huku machozi yakiendelea kumtoka. Tokea alipopata taarifa ya kifo cha Asfat, machozi hayakuwahi kukoma kutoka, ilishageuka sehemu ya maisha yake.
“Ni ajali, mbona na yeye amekufa? Usimlaumu marehemu, tuwaombee wote wapate mapumziko mema kwa Mungu,” alisema mumewe.
“Hapana, roho yangu inasita kumsamehe, amemuua makusudi mtoto wangu, alipania kumuua,” Mama Tonny alizidi kulia.
“Kama ni mtu kusababisha kifo, basi ni Asfat ndiye kamuua mwenzake kwa sababu yeye ndiye alikuwa anaendesha,” mumewe alisema huku akifikiria kifo cha mtoto wake mwingine aliyekufa kwa ajali, Santo.
“Asfat aendeshe gari la Festo, wapi na wapi. Lile gari na ule mwendo ni wa Festo, kila mtu anasema ulikuwa ni mwendo mkali sana kama anavyoendeshaga,” Mama mtu alizidi kutoa machozi wakati akizungumza.
***
Katika nyumba ya jirani, kwao akina Festo, wazazi nao walikuwa chumbani kwao, kila mmoja akiwa na yake kichwani. Ni mama ndiye aliyeanza kuzungumza juu ya msiba huo mkubwa.
“Asfat ameamua kulipiza kisasi kwa Festo,” alisema kwa sauti ndogo, maneno yaliyomshtua sana mumewe!
“Kwa nini unasema hivyo, kisasi cha nini?” mumewe aliuliza.
“Yule mtoto hakuwahi kukubali kama Santo aligongwa na gari kwa bahati mbaya, siku zote aliamini Festo alifanya makusudi. Ni dhambi, lakini acha nipate, simpendi kabisa huyu mtoto, ingekuwa amri yangu, maiti yake ningeitupa porini iliwe na wanyama,” mama aliongea kwa uchungu, machozi yakimtoka.
“Wewe ulijuaje?” mzee Linus, sasa akiwa ametoa macho aliuliza kwa shauku.
“Haikuwa siri, kila mtu hapa mtaani alijua jinsi alivyokuwa akimzungumzia Festo,” mama aliongeza.
“Eti?” baba mtu aliuliza tena, sasa akiwa amesimama na kuvuta kumbukumbu kwa hisia kali!
Itaendelea,
 
SEHEMU YA 19


nilivyoaga pale, jamani anakusalimu sana, ila kidogo hali yake goigoi maana alikuwa na homa,” Mama Tony alimwambia mwenzake huku wameshikana mikono, macho yao yalipokutana, kila mmoja alionekana kuamini kuondoka kwa tofauti kati yao.
Sasa endelea...
Maisha ya familia zile mbili yalirejea katika hali yake ya kawaida kama mwanzo, ingawa kulikuwa na aina flani ya hofu kwa kila mwanafamilia. Hisia za kuwa mauaji ya mwisho yalikuwa ni ya kupangwa, yaliendelea kubakia moyoni mwa akina mama wale ambao hata hivyo, waliamua kusamehe kama walivyoahidi.
Marafiki wawili, wao hawakuwa hata na chembe ya mawazo hayo, waliamini kabisa vifo vya watoto wao vilitokea kwa mipango ya Mwenyezi Mungu na si vinginevyo.
Lakini hali ilikuwa tofauti kabisa kwa Stone, kijana aliyekuwa na mwili mkubwa, mpole na asiyependa kuzungumza sana.
Alikuwa na hasira na alitaka kulipiza kisasi. Kisasi chake akihamishie kwa nani ndilo lilikuwa tatizo lake kubwa.
Familia ya Mzee Linus ilisaliwa na watoto watatu, Tonny ambaye ni mdogo kabisa, Maria aliyekuwa na umri kama wa Stone na ambaye alikuwa ndiye mtoto mkubwa pamoja na Ziggy aliyemfuatia. Ingawa familia zao zilikuwa marafiki, Stone hakuwahi kuwa karibu na yeyote kutoka kwa mzee Linus, zaidi ya kuheshimiana na kushirikiana kwenye matatizo na furaha.
“Huyu mama ninamtamani sana kwa sababu najua alikuwa karibu na mwanaye, lazima walishirikiana kupanga mauaji,” Stone aliwaza, akiwa chumbani kwake, wakati akitazama taarifa ya habari ya televisheni.
Lakini pia Tonny, aliyehusika na kifo cha dada yake, Judy, naye aliingia katika orodha. Ingawa aliendelea kuamini kuwa kifo cha ndugu yake yule kilitokea kwa bahati mbaya kweli, lakini muendelezo wa matukio ulimkuta akianza kumchukia mtoto huyo.
“Anyway, ili kwenda sawa, nitawaua wote wawili,” alijikuta akisema kwa sauti. Ghafla, akajikuta akivaa sura ya ukatili, akatamani kuufanya unyama wakati uleule. Akapiga magoti na kupiga ishara ya msalaba, akauzuia uso wake kwa mikono yake, akajikuta akibubujikwa na machozi!
***
Mwaka mmoja ulishapita sasa tokea vifo vya Asfat na Festo. Kila mmoja aliamini kutokuwepo kwa tatizo lolote baina ya wanafamilia, bila kujua kwamba kulikuwa na mtu mmoja miongoni mwao aliyekuwa na malengo ya ajabu.
Kila siku, roho ya Stone ilizidi kuwa mbaya, akatamani kufanya mauaji ya kisasi muda ule ule, lakini jinsi gani atafanya, ili asinaswe, lilikuwa ndilo tatizo kubwa. Mara mbili alishawahi kumvizia Tonny anaporudi toka shule, lakini mara zote aliambatana na wenzake.
Kijana huyo alikuwa na kituo maalum ambacho gari la shule yao lilikuwa likiwashusha. Kuanzia hapo kulikuwa na mwendo kiasi hadi kufika nyumbani kwao. Kabla ya kufika kwao, kulikuwa na vichochoro viwili ambavyo Stone angeweza kumfanyizia.
Stone akaamua kuanza na mikakati thabiti ya kumuua kwanza Tonny, kwa sababu ni rahisi. Akadhamiria kulifanya zoezi lile mapema iwezekanavyo. Alihitaji kuwa peke yake, tena bila silaha. Angeweza kumkaba shingo na kumuua au hata kumpiga ngumi kadhaa shingoni.
Alikuwa na uwezo huo kwa sababu Stone alikuwa ananyenyua vyuma na anafanya mazoezi ya ngumi, alishiba kweli kweli na vijana wengi walimuogopa. Siku hiyo akadhamiria kufanya kweli!
Ilipofika saa moja kasoro, muda ambao Tonny huwa anashuka ndani ya gari lao, akawa maeneo ya karibu amejificha.
Dakika chache baadaye, gari la shule likafika, na kama bahati kwa Stone, kijana yule alishuka peke yake.
Tonny akaanza kutembea taratibu kuelekea kwao, kichwani mwake akifikiria jinsi gani atafanikiwa kufanya home work ya hesabu, somo alilokuwa analichukia kuliko yote, ingawa darasani kwao, yeye ndiye alionekana kiboko yao kwa hesabu.
Akapita uchochoro wa kwanza bila kukutana na mtu, akakaza mwendo maana giza lilishaanza kuingia…
Je, nini kitatokea? Usikose kufuatilia simulizi hii ya kusisimua katika toleo lijalo.
 
SEHEMU YA 20


ambacho gari la shule yao lilikuwa likiwashusha. Kuanzia hapo kulikuwa na mwendo kiasi hadi kufika nyumbani kwao. Kabla ya kufika kwao, kulikuwa na vichochoro viwili ambavyo Stone angeweza kumfanyizia, lakini mara zote hakufanikiwa kwa sababu kijana huyo alikuwa na wenzake.
Endelea..
Kutoka pale alipokuwa, Stone alimuona Tonny akishuka na kuanza kutembea. Kwa hatua za haraka haraka, naye akaanza kujivuta kuufuata uchochoro ule alioingilia. Alipoufikia, tayari windo lake lilishavuka uchochoro wa kwanza, akawa katika uwazi, tayari kuufuata unaofuatia.
Naye akakaza mwendo na giza lilishampa fursa ya kufanya anavyotaka. Mtaa ulikuwa kimya, mapigo ya moyo wake yalikuwa makubwa, kiasi cha kuweza hata yeye mwenyewe kuyasikia, akaongeza mwendo na sasa alikuwa hatua chache tu kumfikia.
Tonny hakuwa na hofu yoyote, kichwani mwake alifikiria kuhusu homework aliyopewa shuleni, siku zote hakupenda kulala na kazi ya shule bila kuifanyia kazi. Alitamani afike haraka nyumbani ili amalizie kiporo chake.
Stone alimnyatia na kujiweka sawa kumrukia. Ghafla, taa kali ya gari ikamulika kutoka mwanzo wa uchochoro kwa nyuma yao, wote wawili wakageuka haraka kutazama, ndipo Tonny alipostaajabu kumuona mtu akiwa karibu yake mno, lakini ambaye hakupata kumsikia kabla taa hazijawaka.
Akapatwa na hofu kubwa, kwa vyovyote hakuwa na nia njema naye. Akageuka na kuanza kutembea kwa haraka kuumaliza uchochoro ule. Alipomaliza, akageuka tena kumuangalia mtu yule ambaye naye alikuwa anakuja taratibu. Mwanga wa gari ulimfanya amtambue aliyekuwa nyuma yake, akazidi kupatwa na hofu kubwa, Stone?
Stone alifadhaika sana, alililaani lile gari na kwa jumla, alijisikia mkosefu mno kwa kilichotokea, alijua wazi kuwa Tonny hawezi kumwelewa.
Chapuchapu akapata wazo, gari lilipopita, akamwita Tonny na kumtaka asimame. Akiwa ameshajenga hofu naye, Tonny akaongeza mwendo, hakumjibu lolote hadi alipofika nyumbani kwao, akaingia moja kwa moja chumbani kwake na kujitupa kitandani, hofu imetawala kichwa chake.
“Alitaka kunifanya nini?” Tonny alijiuliza bila kupata jibu, akaanza kufikiria nyenendo za Stone za siku za hivi karibuni, akaona wazi kuwa alikuwa na nia mbaya dhidi yake!
“Hapana, lazima nimwambie baba, siwezi kukaa kimya,” alijisemea na kuinuka akiwa bado hajabadilisha nguo za shule. Sebuleni, wazazi wake wote walikuwa wamekaa wakinywa kahawa. Akawasalimia na baadaye akawapa mkanda mzima!
“Hebu eleza vizuri maana usije sababisha matatizo bure, mtu hata hajakugusa unasema alitaka kukuua, tukueleweje?” baba yake, mzee Linus alimwuliza, moyoni mwake naye akihisi hatari kutokana na maelezo ya mwanaye.
“Sasa baba, mtu kama anakuja nyuma yako anatembea si unamsikia? Ninaamini kabisa kama siyo zile taa kumulika, kaka Stone alitaka kunidhuru, haiwezekani nimuone hatua moja nyuma yangu bila kumsikia halafu uchochoroni, tena na yeye alishtuka sana kwa zile taa, aligeuka nyuma na kuduwaa,” Tonny aliwaambia wazazi wake.
Mama yake aliyekuwa akisikiliza kwa makini bila kusema neno, akakohoa, ishara kwamba alikuwa anataka kusema, wote wawili wakamwangalia na kusubiri alichotaka kusema.
“Ninahisi harufu ya damu,” alisema na wote wakamkazia macho.
“Kivipi mke wangu,” mumewe alimwuliza.
“Katika siku za hivi karibuni Stone amebadilika sana, mimi nashangaa siku hizi hata hanisalimii, wakati ni kijana ambaye alikuwa rafiki yangu sana, huyu ana jambo anataka kufanya, tujihadhari,” alisema mama mtu.
“Twende kwa wazazi wake tukayazungumze,” alisema mzee Linus, kauli ambayo ilipingwa haraka na mkewe, kwa madai kuwa kitendo hicho kitaanzisha upya chuki baina ya familia zao.
“Hapana, ni lazima twende, halafu lazima akatoe taarifa polisi, nimepata mashaka makubwa sana na simulizi hii, hata mimi naanza kuona hatari, maisha hayako salama kabisa,” alisisitiza mumewe, ambaye baada ya kusema maneno hayo akainuka kuelekea nje ya nyumba yake.
Alipotokeza tu nje ya geti la nyumba yake akiwa na Tonny, macho yake yakatua kwa Stone, aliyekuwa amesimama upande wa pili wa barabara, taa kutoka kwenye nyumba zilizokuwepo mtaani, zilimfanya aonekane bila kikwazo.
Je, nini kilitokea?
 
SEHEMU YA 20


ambacho gari la shule yao lilikuwa likiwashusha. Kuanzia hapo kulikuwa na mwendo kiasi hadi kufika nyumbani kwao. Kabla ya kufika kwao, kulikuwa na vichochoro viwili ambavyo Stone angeweza kumfanyizia, lakini mara zote hakufanikiwa kwa sababu kijana huyo alikuwa na wenzake.
Endelea..
Kutoka pale alipokuwa, Stone alimuona Tonny akishuka na kuanza kutembea. Kwa hatua za haraka haraka, naye akaanza kujivuta kuufuata uchochoro ule alioingilia. Alipoufikia, tayari windo lake lilishavuka uchochoro wa kwanza, akawa katika uwazi, tayari kuufuata unaofuatia.
Naye akakaza mwendo na giza lilishampa fursa ya kufanya anavyotaka. Mtaa ulikuwa kimya, mapigo ya moyo wake yalikuwa makubwa, kiasi cha kuweza hata yeye mwenyewe kuyasikia, akaongeza mwendo na sasa alikuwa hatua chache tu kumfikia.
Tonny hakuwa na hofu yoyote, kichwani mwake alifikiria kuhusu homework aliyopewa shuleni, siku zote hakupenda kulala na kazi ya shule bila kuifanyia kazi. Alitamani afike haraka nyumbani ili amalizie kiporo chake.
Stone alimnyatia na kujiweka sawa kumrukia. Ghafla, taa kali ya gari ikamulika kutoka mwanzo wa uchochoro kwa nyuma yao, wote wawili wakageuka haraka kutazama, ndipo Tonny alipostaajabu kumuona mtu akiwa karibu yake mno, lakini ambaye hakupata kumsikia kabla taa hazijawaka.
Akapatwa na hofu kubwa, kwa vyovyote hakuwa na nia njema naye. Akageuka na kuanza kutembea kwa haraka kuumaliza uchochoro ule. Alipomaliza, akageuka tena kumuangalia mtu yule ambaye naye alikuwa anakuja taratibu. Mwanga wa gari ulimfanya amtambue aliyekuwa nyuma yake, akazidi kupatwa na hofu kubwa, Stone?
Stone alifadhaika sana, alililaani lile gari na kwa jumla, alijisikia mkosefu mno kwa kilichotokea, alijua wazi kuwa Tonny hawezi kumwelewa.
Chapuchapu akapata wazo, gari lilipopita, akamwita Tonny na kumtaka asimame. Akiwa ameshajenga hofu naye, Tonny akaongeza mwendo, hakumjibu lolote hadi alipofika nyumbani kwao, akaingia moja kwa moja chumbani kwake na kujitupa kitandani, hofu imetawala kichwa chake.
“Alitaka kunifanya nini?” Tonny alijiuliza bila kupata jibu, akaanza kufikiria nyenendo za Stone za siku za hivi karibuni, akaona wazi kuwa alikuwa na nia mbaya dhidi yake!
“Hapana, lazima nimwambie baba, siwezi kukaa kimya,” alijisemea na kuinuka akiwa bado hajabadilisha nguo za shule. Sebuleni, wazazi wake wote walikuwa wamekaa wakinywa kahawa. Akawasalimia na baadaye akawapa mkanda mzima!
“Hebu eleza vizuri maana usije sababisha matatizo bure, mtu hata hajakugusa unasema alitaka kukuua, tukueleweje?” baba yake, mzee Linus alimwuliza, moyoni mwake naye akihisi hatari kutokana na maelezo ya mwanaye.
“Sasa baba, mtu kama anakuja nyuma yako anatembea si unamsikia? Ninaamini kabisa kama siyo zile taa kumulika, kaka Stone alitaka kunidhuru, haiwezekani nimuone hatua moja nyuma yangu bila kumsikia halafu uchochoroni, tena na yeye alishtuka sana kwa zile taa, aligeuka nyuma na kuduwaa,” Tonny aliwaambia wazazi wake.
Mama yake aliyekuwa akisikiliza kwa makini bila kusema neno, akakohoa, ishara kwamba alikuwa anataka kusema, wote wawili wakamwangalia na kusubiri alichotaka kusema.
“Ninahisi harufu ya damu,” alisema na wote wakamkazia macho.
“Kivipi mke wangu,” mumewe alimwuliza.
“Katika siku za hivi karibuni Stone amebadilika sana, mimi nashangaa siku hizi hata hanisalimii, wakati ni kijana ambaye alikuwa rafiki yangu sana, huyu ana jambo anataka kufanya, tujihadhari,” alisema mama mtu.
“Twende kwa wazazi wake tukayazungumze,” alisema mzee Linus, kauli ambayo ilipingwa haraka na mkewe, kwa madai kuwa kitendo hicho kitaanzisha upya chuki baina ya familia zao.
“Hapana, ni lazima twende, halafu lazima akatoe taarifa polisi, nimepata mashaka makubwa sana na simulizi hii, hata mimi naanza kuona hatari, maisha hayako salama kabisa,” alisisitiza mumewe, ambaye baada ya kusema maneno hayo akainuka kuelekea nje ya nyumba yake.
Alipotokeza tu nje ya geti la nyumba yake akiwa na Tonny, macho yake yakatua kwa Stone, aliyekuwa amesimama upande wa pili wa barabara, taa kutoka kwenye nyumba zilizokuwepo mtaani, zilimfanya aonekane bila kikwazo.
Je, nini kilitokea?
Endelea mkuu nasubili
 
SEHEMU YA 21

Alipotokeza tu nje ya geti la nyumba yake akiwa na Tonny, macho yake yakatua kwa Stone, aliyekuwa amesimama upande wa pili wa barabara, taa kutoka nyumba za mtaani zilimfanya aonekane bila kikwazo.
Sasa endelea...

Kwa mara ya kwanza tokea azaliwe, mzee Linusu alishtuka na mapigo ya moyo wake yakaanza kupiga harakaharaka. Alimkazia macho kijana yule wa jirani, ambaye naye alionekana kuwa bize na simu yake, akiwa hajishughulishi na mtu yeyote. Tonny naye alishtuka alipomuona Stone lakini akapiga moyo konde akaungana na baba yake kuelekea kwa mzee Komba.

Wakatoka na kupiga hatua kadhaa mbele hadi walipofika getini kwa mzee Komba. Hawakugonga, walilisukuma na kutokezea ndani ambako walikutana na mwanga mkali wa taa za sebuleni. Kwa kuwa walikuwa wenyeji, walisukuma mlango na kuingia ndani ambako walimkuta mzee Komba akiwa amekaa na mkewe. Ingawa walikuwa wamezoeana sana, lakini ujio huu uliwashtua kidogo, wote wakasimama kuwapokea.

“Karibuni, karibuni sana,” alisema mzee Komba huku akimpa mkono mzee mwenzake na baadaye Tonny.

“Asante ndugu yangu, tumekaribia,” alisema mzee Linus na kutoa nafasi kwa Tonny ambaye aliwaamkia wazee wale kisha kukaa kwenye sofa kubwa.
Hakutaka kupoteza muda, mara moja akaanza kusimulia kitu kilichowapeleka pale. Mzee Komba na mkewe walisikiliza kwa makini na kwa mbali, wakaanza kuhisi hatari, maneno ya baba yake Tonny yalikuwa na viashiria vya uvunjifu wa amani.

Baada ya kutoa maelezo hayo, wazazi wake Stone wakabakia wapole, hawakujua waanzie wapi, lakini maneno yale yaliwaingia vizuri na kwa kupima mazingira, hata wao waliona dhamira isiyo nzuri kwa mtoto wao.

***
Stone alipotazama simu yake ya mkononi ili kujua nani anapiga, akajikuta akitamka kwa sauti kidogo.
“Kimenuka” alisema na kupokea simu ya baba yake ambaye bila kumsabahi wala nini, alimtaka kuingia ndani mara moja. Dakika moja baadaye, akaingia sebuleni na kuungana na watu aliowakuta.
“Stone una lolote la kutuambia kuhusu kilichotokea usiku huu wewe na huyu mdogo wako,” baba yake alimwuliza kwa taratibu.

“Tulikuwa tumeongozana wakati tunarudi nyumbani, lakini hatukuongea,” Stone alisema kwa ufupi.
“Nimesikiliza maelezo yake hapa, inaonekana kama kuna kitu kibaya ulitaka kumfanyia, kwa sababu mwanga wa gari ulipowamulika, ulikuwa hatua mbili tu nyuma yake na hakuweza kukusikia wakati ukimsogelea, ulitaka kufanya nini?” baba yake alimwuliza tena.

“Nilikuwa nataka kumtania kwa kumtisha,” Stone naye alisema, lakini uso wake ulionyesha wazi alichokisema hakikufanana na moyo wake.

“Stone, kuna mambo mengi yametokea katika familia zetu hizi, mimi siwezi kukulazimisha useme, lakini naungana na hawa kuwa haukuwa na nia njema kwa Tonny, kama ulikuwa na lengo lolote baya, nakuomba sana mwanangu uliache, hatupo tayari kuona mtu anatuliza makusudi,” alisema baba yake na kumtaka kuondoka sebuleni.

Stone akasimama bila kusema neno na kuingia chumbani kwake.
Mazungumzo mafupi yaliendelea pale sebuleni kabla ya wageni kuaga na kuondoka. Walipofika nje, hawakuingia ndani kwao, bali walipitiliza na kwenda kuchukua Bodaboda, wakapanda kuelekea Kituo cha Polisi cha Wazo.

Katika kaunta ya Polisi, Tonny alianza kuwasimulia askari wawili waliokuwa wakiwahudumia. Baada ya maelezo yake, askari akawauliza maswali kadhaa na kuwaambia wanaweza kuondoka kuelekea nyumbani, lakini wawe makini kwa muda wote.

Saa tano kamili za usiku, geti la mzee Komba likagongwa. Ugongwaji wake ulionyesha ni wa mtu mgeni, kwani ulikuwa ni kwa sauti kubwa. Kwa kuwa alikuwa bado sebuleni wakiwa na mkewe wakiendelea kulizungumzia sakata lile, yeye mwenyewe akasimama na kwenda kufungua.
Ni polisi.

Je, nini kitatokea? Usikose kufuatilia simulizi hii ya kusisimua wiki ijayo.
 
SEHEMU YA 22


Saa tano kamili za usiku, geti la mzee Komba likagongwa. Ugongwaji wake ulionyesha ni wa mtu mgeni kwani ulikuwa ni kwa sauti kubwa. Kwa kuwa alikuwa bado sebuleni wakiwa na mkewe wakiendelea kulizungumzia sakata lile, yeye mwenyewe akasimama na kwenda kufungua.
Sasa endelea...

Ni polisi.
“Shikamoo mzee,” mzee Komba aliamkiwa na askari aliyekuwa amening’iniza bunduki mabegani mwake, mara tu alipofungua geti.

“Marahaba kijana, vipi mbona usiku sana?” aliitikia na kuuliza swali ambalo Polisi hao walimjibu kuwa walikuwa wamekuja kumchukua kijana wake aitwae Stone kwani kulikuwa na malalamiko kidogo juu yake, hivyo walimtaka kituoni kwa mahojiano.

“Malalamiko gani ambayo hayawezi kusubiri kukuche vijana wangu, ninawaombeni kama inawezekana nimlete mwenyewe kituoni kesho asubuhi,” mzee Komba aliwasihi askari.

Askari hao wakakataa na mzee Komba naye akagoma kumtoa kijana wake usiku ule pasipo kwanza kuelezwa kosa la kijana wake. Ubishi ulikuwa mkubwa uliolazimisha majirani kuamka na mjumbe kuitwa.
Ingawa mzee Linus na familia yake waliamka na kutoka nje, lakini alibaki kimya bila kusema lolote wakati rafiki yake alipokuwa akibishana na Polisi. Mjumbe wa mtaa, mzee Masta, aliwauliza kwa busara askari wale, shauri lililopo kituoni linalomuhusu Stone.

“Tumesema tatizo litajulikana hukohuko kituoni, sisi tunafanya ubinadamu mnatuona wajinga, au mnataka tuingia ndani kwa nguvu?” Polisi mmoja, kati ya watatu waliokuwepo alisema. Kutotajwa kwa sababu ya kuja kumchukua Stone, kulichochea vurugu za wananchi ambao sasa walishakuwa wengi.

Hatimaye Polisi walishindwa, wakakubaliana na mzee Komba kuwa ampeleke mwanaye kituoni mapema kesho yake, vinginevyo wangekuja kumchukua mwenyewe.

Polisi walipoondoka, watu waliendelea kujadili kwa muda suala hilo. Kwa kuwa mzee Linus hakuchangia lolote wakati wa mabishano yale, mzee Komba alimfuata alipokuwa amesimama nje ya geti la kuingilia ndani kwake. Akamuuliza sababu ya kutomsaidia katika ishu ile, akasema aliogopa kuisaliti nafsi yake.
“Kuisaliti nafsi yako kivipi?” aliuliza mzee Komba.

“Ni mimi ndiye niliyeenda Polisi kuwataarifu kuhusu Stone kama tulivyokuja kwako jana, tulijadiliana na mama tukaona kama kuna hatari hivi, ni bora Polisi wakajua kinachoendelea,” mzee Linus alisema huku akimtazama mwenzake usoni bila kupepesa macho.

Mzee Komba hakutegemea kusikia maneno yale, alitambua kuwa mkutano wao wa mapema kuhusu suala lile ulishaweka mambo sawa. Hakudhani kama kulikuwa na umuhimu wa kwenda kuripoti polisi tukio ambalo limeshajadiliwa kama familia. Akamtazama kwa macho ya kutoamini, akamuuliza kuhusu maelezo aliyotoa huko, akajibiwa kwamba ni hofu juu ya usalama wa kijana wake kutokana na mwenendo wa Stone.

Taratibu mzee Komba akaondoka kurejea ndani kwake, aliwashukuru watu wachache waliobaki nje wakizungumza kwa kitendo chao cha kutoka nje na kwenda kumsaidia. Ndani, akawakuta mkewe akiwa amekaa na Stone sebuleni.
“Sasa kwa nini hawajasema kosa lake hao Polisi,” mke wake aliuliza, swali ambalo mzee Komba alilitegemea.

“Majirani wameenda kushtaki kuhusu Stone, wanaamini alitaka kumdhuru kijana wao, wamekwenda kutoa taarifa juu ya usalama wa mtoto wao. Kwa hiyo Stone ukae ujipange ujue cha kusema mbele yao.”
Stone akahisi ubaridi umepita ghafla mwilini mwake kabla ya hali yake kurejea kawaida. Akauma midomo yake na kuiachia. Wazazi wake wakatazamana.
***
Waliwahi sana kuamka, Stone akafanya mazoezi kwenye vyuma vyake vilivyokuwepo uani, baba yake naye akajinyoosha viungo chumbani kwake kabla ya wote kuingia bafuni kujimwagia maji, baada ya chai, safari ya kwenda kituo cha Polisi ikaanza.

Ni Stone ndiye aliyekuwa anaendesha gari lao, kila mtu alionekana kuwa na mawazo mengi kichwani mwake, hakuna aliyejua wanachowaza. Walifika kituo cha Polisi Wazo muda wa saa mbili kasoro robo asubuhi.

Je, nini kitaendelea? Usikose kufuatilia katika toleo lijalo.
 
SEHEMU YA 23

Ni Stone ndiye aliyekuwa anaendesha gari lao, kila mtu alionekana kuwa na mawazo mengi kichwani mwake, hakuna aliyejua wanachowaza. Walifika Kituo cha Polisi Wazo muda wa saa mbili kasoro robo asubuhi.

Sasa endelea...

Baba yake Stone alikuwa wa kwanza kushuka garini, akapepesa macho yake kuangalia watu wengi waliokuwa wamejazana kituoni hapo. Watu walikuwa wamejaa pale kwa ajili ya kuwadhamini ndugu zao waliokabiliwa na makosa mbalimbali.

Mzee Komba akatoa simu yake ya kiganjani, akabonyeza namba kadhaa, akaisogeza sikioni. Upande wa pili ukapokea, mazungumzo yalikuwa mafupi, akaikata na kumtaka mwanaye kushuka garini ili waelekee kituoni.

Wakajitambulisha, tayari taarifa zao zilikuwepo, wakatakiwa kuingia chumba kimoja walichoelekezwa, humo wakakutana na ofisa wa polisi aliyevalia kiraia. Akawakaribisha na mara moja akaanza kuzungumza nao juu ya wito wa Stone.

“Jana alikuja jirani yenu kulalamika kwamba wewe ulidhamiria kumfanyia kitu kibaya yule kijana, sasa nataka uniambie, kwa nini ulikuwa unamsogelea kwa kumvizia, tena uchochoroni?” aliuliza yule ofisa wa polisi, ambaye awali alijitambulisha kama Koplo Sam alimuuliza Stone.

Stone alilitegemea swali hili, alishapanga kitu cha kusema, hivyo harakaharaka akajibu.
“Afande, yule ni mdogo wangu, familia zetu ni marafiki kwa miaka mingi, mimi lengo langu lilikuwa ni kumtania kwa kumtisha na wala sikuwa na nia nyingine.”

“Sikiliza Stone, ni rahisi mtu wa kawaida kuweza kukuelewa, lakini siyo watu kama sisi ambao tunasomea namna ya kutambua nia au kusudio la kutenda uhalifu. Katika ishu yako, ukiangalia eneo, muda na namna ulivyomsogelea karibu bila yeye kukusikia, tunahisi ulikuwa na dhamira mbaya,” Koplo Sam alisema huku mzee Komba akijaribu kumtazama mwanaye kwa umakini mkubwa.

“Kweli afande, sikuwa na nia yoyote mbaya,” Stone alijibu tena.
Baada ya majadiliano mafupi, askari aliwaruhusu kuondoka, lakini akimpa onyo Stone kuwa jambo lolote baya litakalomkuta Tonny, yeye atakuwa mtuhumiwa wa kwanza, bila kujali wapi limetokea!
Wakainuka bila mzee Komba kusema jambo lolote, njiani wakiwa garini, akamsemesha kijana wake. Akamtaka kuyachukulia kwa uzito mkubwa maneno ya askari, kwa sababu hata kama jirani yao atadhuriwa na mtu mwingine, itakuwa ni juu yake.

“Lakini hata hivyo Stone, wewe kutaniana na mtoto kama Tonny umeanza lini? Mbona hata mimi napata mashaka na dhamira yako?” alimuuliza Stone ambaye macho yake aliyakaza mbele. Hakumjibu baba yake.

***
Mzee Linus hakupata usingizi kabisa, akili yake yote ilikuwa kwa Stone, hakutaka kuamini maneno yake kuwa eti alitaka kumtania. Kwa mara ya kwanza moyoni mwake, akaanza kuichukia familia ya jirani na rafiki yake wa muda mrefu. Usiku wa saa tisa alikurupuka kutoka usingizini, akawaza sana kabla ya kujikuta akitamka..hawanijui!

Ni kweli, walikuwa hawamjui. Mzee Linus alikuwa mtata tokea utoto wake. Alikuwa na matukio mengi ya kushangaza na kushtusha. Akiwa darasa la pili, aliwahi kumpigilia msumari kwenye goti mtoto wa jirani yao. Msumari huo uliingia vibaya kiasi cha kusababisha binti huyo mdogo kukatwa mguu.

Kijijini kwao alikuwa mtukutu, mwenye kupigana kila siku na wenzake hadi baba yake alipoamua kumpeleka mjini kwa kaka yake, ambaye hakuwa na kijana wa kike. Alipofika huko Singida, haraka sana akazoeleka kiasi cha kuonekana kama ni mtu wa zamani kuliko ukweli wake.

Pamoja na kuwa alikuwa na akili nzuri darasani, lakini nje, alikuwa kwenye makundi ya vijana, wakipora watu usiku na kuwabaka wasichana. Mara tatu alishawahi kukamatwa na Polisi kwa kutajwa na wenzake kwenye matukio, lakini mara zote baba yake mkubwa, aliyekuwa mfanyabiashara aliyefanikiwa, alitoa kitu kidogo na yeye kuachiwa..!

Je, nini kitaendelea? Usikose kufuatilia simulizi hii katika toleo lijalo.
 
SEHEMU YA 24

Pamoja na kuwa alikuwa na akili nzuri darasani, lakini nje alikuwa kwenye makundi ya vijana, wakipora watu usiku na kuwabaka wasichana. Mara tatu alishawahi kukamatwa na Polisi kwa kutajwa na wenzake kwenye matukio, lakini mara zote baba yake mkubwa, aliyekuwa mfanyabiashara aliyefanikiwa, alitoa kitu kidogo na yeye kuachiwa..!
Sasa endelea...

Mzee Linus alishashiriki katika matukio mengi makubwa, ya kupora kwa kujeruhi na hatimaye majeruhi hao kufariki. Hakuweza kukumbuka vizuri watu wangapi walikufa baada ya kundi lao kuwashambulia kwa mapanga.

Kilichomfanya kuachana na tabia hiyo ya uhuni wa kupitiliza, ni siku alipombaka bila kujua, dada yake, mtoto wa baba yake mkubwa. Siku hiyo dada mtu aliondoka nyumbani usiku bila baba yao kujua na kwenda disco. akiwa huko, pamoja na marafiki zake, wakaondoka na wavulana wao kuelekea gesti. Njiani wakakutana na kundi la akina Linus.

Wanaume wakapigwa mapanga na kufanikiwa kukimbia, wasichana wakawekwa chini ya ulinzi. Linus alikuwa wa kwanza kumbaka dada yake ambaye ingawa alimtambua, aliamua kunyamaza ili kujiokoa maana hakujua nini angefanya kama angejitambulisha. Walipomaliza vitendo vile, wakawamulika kwa tochi wale wasichana usoni ili kuwatambua.

Hakuamini macho yake alipomuona dada yake. Akamuomba samahani sana. Dada yake aliamua kumsamehe kwa sababu hakujua angemuambiaje baba yake. Tokea siku ile, Linus akaacha maisha ya mjini, akarejea kanisani..

**
“Huyu dogo nataka nimshughulikie mimi mwenyewe, kama anadhani ule mwili wake unaweza kunishinda mimi, basi ataisoma namba,” mzee Linus alijisemea mwenyewe akiwa amelala kitandani kwake.Alijiwa na mawazo mengi sana kichwani mwake juu ya nini cha kumfanya Stone. Baada ya kufikiri sana, hatimaye akamkumbuka Dayani, mmoja kati ya marafiki zake wa utotoni Singida, ambaye aliendelea na tabia hiyo, hadi akawa jambazi wa kutisha kabla ya kutajirika na kuamua kuachana na kazi hiyo!

Dayani alikuwa anaishi Bunju, nje kidogo ya jiji na Dar es Salaam ambako alijenga nyumba moja nzuri sana na alikuwa na miradi kadhaa ya kumuingizia fedha, ikiwemo baa ya Zanzi ambako alipenda kutembelea mara kwa mara.

Asubuhi na mapema, mzee Linus alichukua simu yake na kumpigia Dayani, kwani ingawa yeye alishaacha mambo hayo, waliendelea kuwa na mawasiliano ya mara kwa mara, alifahamu nyendo zake na wala hawakufichana.

“Haloo,” Dayani aliita mara baada ya kuona simu ya rafiki yake ikiita.
“Chuga, nahitaji kukuona,” alisema mzee Linus simuni bila hata kumsalimia. Aliposikia neno Chuga, mwili wa Dayani ulisisimka, kwa sababu lilikuwa ni jina waliloitana enzi zile za ukabaji, kwani wakiwa kazini hawakutakiwa kabisa kuitaja majina yao halisi hata kwa bahati mbaya. Akajua kuna kazi!
“Njoo tunywe supu Zanzi, utanikuta,” alisema Dayani na kukata simu!

Saa mbili kamili asubuhi, mzee Linus aliingiza gari lake katika eneo la maegesho la baa kubwa ya Zanzi. Ilikuwa ni moja ya baa zilizokuwa zikijaza watu sana na kwa kipindi hiki cha fainali za kombe la dunia, skrini kubwa nne zilifungwa kila upande.

Alimuona Dayani akiwa amekaa akisoma magazeti kwenye kibanda kimoja cha peke yake, akamfuata na kuvuta kiti na kukaa kabla ya kumpa mkono kumsalimia.
Mwenyeji wake akamuita mhudumu ambaye alifika na kuagizwa kuleta mchemsho wa samaki kwa ajili ya mgeni. Mzee Linus aliushambulia haraka haraka mchemsho huo ulipoletwa na alipomaliza, akakohoa kidogo kusafisha koo!

“Lete habari Chuga,” Dayani alimwambia mzee Linus. Wote wawili walionekana umri kuanza kuwatupa mkono. Aliposikia kauli hiyo, mzee Linus akajikuta akicheka kwa sauti!

Je, nini kitatokea? Usikose kufuatilia simulizi hii ya kusisimua katika toleo lijalo.
 
SEHEMU YA 25

“Lete habari Chuga,” Dayani alimwambia mzee Linus. Wote wawili walionekana umri kuanza kuwatupa mkono. Aliposikia kauli hiyo, mzee Linus akajikuta akicheka kwa sauti!
Sasa endelea..

Mzee Linus alimtazama tena mshirika wake wa uhalifu wa hapo zamani, sura yake ilionyesha shauku kubwa ya kusikia habari kutoka kwa mwenzake. Kuona hivyo, mzee huyo akamsimulia kisa chote cha mwanaye, akamwelezea na hofu kubwa aliyonayo, sambamba na historia ya kutatanisha kati ya familia hizo mbili majirani.

“Kama ulivyonisimulia kuhusu huyo kijana ni kweli, basi sitashangaa nikisikia siku yoyote mtoto wetu akikutwa amekufa. Unakumbuka tulivyomzimishaga yule mchaga kule Singida siku zile? Tena ni wewe ndo ulimfuata kwa staili hiyohiyo na hakuliona tena jua, nafikiri tumuondoe mara moja huyo sijui Stone,” Dayani aliongea taratibu, lakini akionyesha msisitizo mkubwa.

Wakakubaliana kuhusu hilo. Dayani aliuliza maswali mengi kuhusu eneo wanaloishi, mazingira yake, nyenendo za Stone na habari nyingine nyingi alizohitaji kujua kabla ya kukamilisha kazi ambayo ilikuwa mbele yake, ambayo hata hivyo, ilikuwa ni ndogo mno kwake.

“Kwa hiyo Chuga, nakulipa shilingi ngapi?” mzee Linus alimuuliza Dayani.
“Acha mambo yako wewe, kwa hiyo mimi nikihitaji msaada wako inabidi nikulipe, nitamalizana na vijana, wewe kapumzike,” alijibiwa.

Waliendelea na mazungumzo yao ya hapa na pale hadi mchana, walipoanza kujipooza kwa bia baridi, kazi waliyoifanya hadi jua lilipozama. Dayani alimpatia kijana wake mmoja amuendeshe kwa gari lake hadi nyumbani kwake, kwani alihofia kwa kinywaji kile, lolote lingeweza kumtokea.

***
Mabadiliko ya uhusiano baina ya familia hizi mbili sasa yalikuwa ni dhahiri. Hakukuwa tena na ucheshi wala uchangamfu kama zamani. Mzee Komba alishaona dalili za rafiki yake wa siku nyingi kubadilika. Kitendo chake cha kumpeleka mwanaye polisi, wakati walishakaa na kuzungumza hakukipenda.
Ili kuhakikisha anailinda familia yake, alikaa chini na mkewe ili kutazama jinsi gani wangeweza kufanya. Walijadiliana vitu vingi, lakini baada ya muda mrefu wa majadiliano, hatimaye wakafikia muafaka kwamba wajilinde kwa dawa za waganga wa jadi.

“Ninamjua mganga anayeweza kufanya kitu kwa ajili yetu na bahati nzuri nilishawahi kuzungumza naye kuhusu hili jambo,” mke wa mzee Komba alimwambia mumewe.
“Unasemaje? Mbona hujawahi kuniambia,” alimwuliza.
Mke wake akamwelezea kwa kifupi kuhusu siku aliyoamua kwenda kwa mganga huyo, ingawa hakumweka wazi jinsi alivyofahamiana naye.

“Basi kesho inabidi twende,” mzee Komba alisema, jambo ambalo lilipingwa na mkewe.
“Hapana, haya mambo yakishaongelewa, jambo lifanyike mara moja, muda bado tunao, tuwashe gari twende, hapo Salasala wala siyo mbali mume wangu.”

Mzee Komba akakubali, wakafanya maandalizi kidogo na muda wa saa kumi na moja jioni siku hiyo, wakatoka na gari yao kuelekea kwa mganga. Nusu saa baadaye walikuwa kwenye foleni wakisubiri kwenda kumuona mtaalamu huyo wa mambo ya giza.

Zamu yao ilipofika, wakaingia na kuketi katika mkeka uliokuwa mbele ya mganga kama ilivyokuwa utaratibu. Baada ya salamu, mganga akawa wa kwanza kuwasemesha.

“Ule mpango wake wa wakati ule, sasa ndiyo wakati wake,” mganga, ambaye alimkumbuka sana mkewe mzee Komba, alisema na mwanamke huyo na mumewe kujikuta wakipatwa na mshangao mkubwa.
“Umejuaje bwana mkubwa,” mwanamke huyo aliuliza.

“Vifaa vyangu vinaonyesha kila kitu, kuna kitu kibaya sana kinaelekea kutokea kwenu wakati wowote kuanzia sasa,” alisema na kuwazidishia, siyo tu mshangao, bali hofu ndani ya mioyo yao!

Je, nini kitaendelea? Usikose kufuatilia simulizi hii ya kusisimua katika toleo lijalo.
 
SEHEMU YA 26

“Vifaa vyangu vinaonyesha kila kitu, kuna kitu kibaya sana kinaelekea kutokea kwenye wakati wowote kuanzia sasa,” alisema na kuwazidishia siyo tu mshangao bali hofu ndani ya mioyo yao.
Sasa endelea...

“Hebu tueleze vizuri bwana mtaalamu, unajua utatuua kwa presha,” mzee Komba alimwambia mganga huyo, kwani maneno yake yalimfanya ahisi baridi mwili mzima.

Mganga akawaelezea kwa kifupi jinsi jirani yao alivyokuwa akipanga mipango ya kuwadhuru na kuwasifu kuwa waliamua wakati muafaka wa kwenda kwake ili aweze kuwalinda. Baada ya maelezo hayo, akataka kusikia kama wana lolote.

“Sisi hatutaki ubaya nao, lakini hatutaki watudhuru, watakachotaka kutufanyia kiwarudie wenyewe,” alisema mkewe mzee Komba na kuungwa mkono na mumewe ambaye alitingisha kichwa kuonyesha kukubaliana naye.

Mganga kusikia hivyo akakubaliana nao na kabla ya kufanya kitu chochote, aliwauliza maswali kadhaa kuhusu familia yao, kama vile idadi ya watoto, kama wana kinga yoyote ya kishirikina waliwahi kupata na vitu vingine kadha wa kadha ambayo yote alijibiwa.

Baada ya hapo akachukua mkeka mdogo, akautandika mbele yao na kuwataka wote kukalia pale, kisha akawafunika kwa kijishuka cheupe, ambacho alikimwagia dawa yenye rangi nyeusi kisha akawanyunyizia na maji huku akizungumza maneno wasiyoyajua, akiwazunguka.

Alipowazunguka kama mara tatu hivi, aliwafunua na kuwataka kurejea walipokaa awali, huku yeye akiendelea kuwafanyia mambo. Nusu saa baadaye aliwakabidhi mfuko wenye dawa kadhaa na kumalizia kwa kuwapa maelezo yafuatayo.

“Usiku huu, chimbieni dawa hii (akiwaonyesha aliyoweka katika chupa nne za soda) katika kona zote nne za nyumba yenu, wewe mama utachimbia za kusini na kaskazini, baba mashariki na magharibi. Hii mnatakiwa kunywa watu wote mnaoishi ndani ya nyumba yenu na hii hapa mtajifukisha kila mtu kwa wakati wake lakini kabla jua halijachomoza.”

Wakaondoka kuelekea nyumbani kwao, ambako walifanya kama walivyoambiwa kabla ya kujitupa kitandani kulala, kusubiri kitakachotokea.
***
Saa tano asubuhi vijana wawili wakiwa kwenye pikipiki walikuwa wanarandaranda katika mitaa ya Nakasangwe wakiwa kama watu wanaomtafuta mtu au nyumba. Waliingia mtaa huu na kutokezea mtaa ule, lakini hakuna hata mmoja aliyewatilia maanani.

Baadaye wakaenda Kwa Big Pub, sehemu moja maarufu sana eneo hilo kwa vinywaji. Wakakaa na kuagiza bia. Walionekana kuwa makini na walichokuwa wakikifanya, lakini hakuna hata mmoja aliyewajua wala kukisia walichokihitaji.

Walikuwa wameifuata nyumba ya mzee Komba na walishaiona. Ni Beka na Shosi, vijana wa kazi ambao hufanya kazi na Dayani. Vijana hawa ni hodari katika kuua na kuharibu. Ndiyo waliopewa kazi, siyo tu kumshughulikia Stone, bali pia kufanya na uhalifu mwingine ili kuitia adabu familia nzima.

“Mungu bwana, yaani jamaa huko aliko anapanga mipango yake, lakini hajui kama jua la kesho hataliona, angejua tupo hatua chache kuichukua roho yake angepotelea huko huko aliko,” Beka, akiwa anakunywa bia yake ya pili alimwambia mwenzake kwa sauti ambayo waliisikia wenyewe tu.

Nia yao ilikuwa ni kumuona Stone, kwani kwa jinsi walivyoelekezwa, hawakuwa wamemuona kijana yeyote aliyefanana na sifa zake. Waliendelea kukaa pale wakiwa na vinywaji vyao huku macho yao yakiwa hayauachi mlango wa mbele wa nyumba ya mzee Komba.

Wakiwa katika bia yao ya nne, mlango wa nyumba hiyo ulisikika ukifunguliwa, gari likaonekana likitoka, Beka akainuka na kuifuata pikipiki waliyoipaki pembeni, Shosi alijua anakoenda, hivyo akabaki kimya pale alipokaa.



Inaendelea
 
SEHEMU YA 27


Wakiwa katika bia yao ya nne, mlango wa nyumba hiyo ulisikika ukifunguliwa, gari likaonekana likitoka, Beka akainuka na kuifuata pikipiki waliyoipaki pembeni, Shosi alijua anakoenda, hivyo akabaki kimya pale alipokaa.
Sasa endelea...


Wakati akipanda juu ya pikipiki na kuiwasha, gari lililokuwa likitoka kwa mzee Komba lilishaingia barabarani likielekea kusikojulikana. Beka alivuta mafuta na kulisogelea gari hilo, alipotupa macho ndani, akakuta aliyekuwa akiliendesha ni mwanamke, mama yake Stone, akapunguza mwendo na kugeuza, akarejea kwenye kijiwe chao.

Hakuna mtu mwingine aliyetoka ndani ya nyumba hiyo hadi gari lililotoka liliporejea. Saa kumi na moja jioni, wakapata wazo jipya.

“Nina uhakika huyu fala atakuwepo ndani, kwa nini tusiwalipue tu kwa petrol nyumba yote wafe?” Beka alimwambia Shosi, ambaye alikubaliana naye, lakini akamtaka kwanza wafanye mawasiliano na bosi wao Dayani.

Walipoongea na Dayani kuhusu mpango huo, naye aliunga mkono na kusema hilo litakuwa jambo zuri zaidi kwani alitaka kuwapa fundisho watu hao wanaomsumbua rafiki yake. Wakamalizia bia zao na kuondoka huku wakiitazama vizuri nyumba ya akina Stone.
***
Mara tu alipomaliza kuzungumza na vijana wake, Dayani alimpigia simu mzee Linus na kumweleza kuhusu mpango mpya, akimtaka kuondoka nyumbani hapo na kuelekea sehemu yoyote, ambako angekaa kwa siku moja au mbili, ili wakati wa tukio hilo, yeye asiwepo karibu.

Mzee Linus akajaribu kuupinga mpango huo, akisema lisingekuwa jambo jema kuwaua wote kwa mara moja, lakini rafiki yake akamsisitiza umuhimu wa kufanya vile, hasa kwa kuwa wangeondoa kabisa matatizo siku za mbele.

Kwa shingo upande akakubaliana naye, lakini moyoni mwake akasikitika sana kwa tukio linalokwenda kutokea. Hakutaka kumwambia jambo lolote mkewe kuhusu mpango huo, lakini akahakikisha watoto wake wote waliokuwepo nyumbani, wakiondoka na kwenda kulala nje ya nyumba yao.

Kulikuwa na watoto watatu nyumbani kwa mzee Linus, Tonny, Brown ambaye alikuwa kaka yake aliyekuwa na umri sawa na Stone na Mwasi, dadake aliyemuachia ziwa. Walipoambiwa kuhusu kuondoka nyumbani kupisha kupigwa dawa ya wadudu usiku, kila mtu kwa nafasi yake walijawa na furaha kubwa.

Mzee Linus na mkewe, wakaamua kwenda kulala hotelini eneo la Tegeta. Kichwani mwake alikuwa na simanzi kubwa, kwani alijua dhambi anayokwenda kuipata.

Mkewe aliona sura ya mumewe, akataka kujua sababu hasa ya kuwaondoa nyumbani, kwani suala la kupigwa dawa halikuwahi kuwa katika mipango yao. Alijua ataambiwa. Lakini mumewe alimsihi kumuacha kwanza apumzike, mambo mengine wangeongea baadaye.
***
Saa sita za usiku, Beka na Shosi wakiwa katika pikipiki mbili walikuwa wanaendesha taratibu kuingia katika eneo la Nakalekwa, ramani yao iliwaongoza vizuri kabisa hadi kwenye nyumba moja hivi ambayo haijamalizika kujengwa, wakasimama.

Wakashusha dumu la petrol lililokuwa kwenye pikipiki ya Beka, wakaliweka chini. Kwa tahadhari kubwa, Shosi akaenda hadi kwenye nyumba waliyoilenga, akaichunguza vizuri, akarudi hadi alipokuwa mwenzake, wakapeana ishara wakaondoka taratibu huku wakitupa macho huku na kule.

Wakafika walipokusudia, wakausukuma mlango wa geti, ulikuwa umefungwa, wakatoa ufunguo Malaya, wakaufungua ukafunguka, wakaingia kimya kimya. Wakaanza kumwaga petrol kupitia kwenye mlango wa mbele wa nyumba, mafuta hayo yakaingia ndani ya nyumba hadi dumu lilipokuwa tupu.

Licha ya ukali wa harufu ya petrol, walishangaa watu waliokuwepo ndani kushindwa kushtuka. Wakarudi mlangoni, wakachukua gazeti walilokuja nalo, wakalikunja vizuri, wakaliwasha moto kisha wakalitupa kwenye mlango wa mbele wa nyumba hiyo na mara moja, ukalipuka ndani.

Wakaanza kukimbia kuzifuata pikipiki zao na walipoziwasha tu, mayowe ya moto, moto, moto yakaanza kusikika, kwani moto ulishakuwa mkubwa na nyumba ilionekana kuteketea.

Simu zikaanza kupigwa huku na huku ili kuwanusuru watu waliokuwa ndani, zimamoto, polisi na kila mahali. Haikusikika kelele ya kitu chochote tokea mle ndani isipokuwa sauti ya moto uliokuwa ukiteketeza vitu.

Sasa watu walishajaa, walijitahidi kuuzima kwa mchanga na maji kwenye ndoo, lakini walionekana kama watu wanaofanya mchezo, moto ulizidi kuteketeza vitu, vilivyosikika vikipasuka kila mara!

Je, nini kitaendelea? Mbona hakukusikika hata mayowe kutoka ndani? Usikose kufuatilia katika toleo lijalo.
 
Back
Top Bottom