Kiranga umeandika mambo mengi muhimu nitadonyoa machache
1. Ni kweli tunahitaji wenye 'hazina' za Historia waandike kama ambavyo hadi leo watu wanatafiti kifo cha Rais Kennedy. Kwasasa ukitafuta vitabu vinavyomhusu Trump utapata zaidi ya 100 na kila kimoja kina jambo lake tofauti.
Ni kwa msingi huu, tuna mnasihi Mohamed kutosema ''Historia yake ni ya kweli' kwani ni kujimilikisha na hilo si sawa. Watu waandike wasomaji wataamua
2. Kwanini tuna vitabu vichache?
Pohamba kagusia vizuri sana. Viongozi wetu wanaogopa kuandika kwasababu ya vizazi vyao.
Mwinyi asingeweza kuandika yote wakati kijana wake alikuwa anavizia nafasi ya Urais Zanzibar.
Mzee Malecela anajua ya Bunge, alipoulizwa uwepo wa COVID-19 alikataa kujibu ingawa aliashiria uwepo wao si kisheria. Mzee alsema ''ili uwe Mbunge lazima uwe na chama'' akiulizwa wapo kimakosa aligoma.
Mzee Malecela anaogopa 'future' ya vizazi vyake, hawezi kusema yote
Dr Salim alijaribu kuandika, '' Wakamshauri' aondoe baadhi ya mambo . Tunajua alitaka kuzungumza siasa za Zanzibar, hilo likaonekana mwiba. Hili nalo ni tatizo la kuingiliwa na '' vyombo''.
3. Sababu nyingine ni mafao ya Viongozi. Hivi kwa mafao anayopata Ndugai unategemea ataandika kitabu gani?
VP, PM na Maspika wanaishi maisha ya 'peponi'', kwao kukaa kimya ni bora kwa sasa na vizazi vyao kuliko kuandika.
Uchawa hauishii kwa vijana, once a Chawa always a Chawa hadi uzeeni.
Nguruvi3,
''...tuna mnasihi Mohamed kutosema ''Historia yake ni ya kweli' kwani ni kujimilikisha na hilo si sawa. Watu waandike wasomaji wataamua.''
Mnaninasihi.
Sijui kwa nini unawajumuisha na watu wengine katika kauli yako hii.
Kwa ni isiwe wewe ndiye unanisihi?
Mimi ninaposema kuwa haya ninayosema ni kweli sababu ni kuwa nayajua ukweli wake.
Ama hili la wasomaji kuamua kama nasema kweli au uongo hili sijaghafilika nalo wala sina shaka na hilo.
Wasomaji wengi wanaamini kwa yote niliyoandika.
Haya niliyoandika wahusika wakuu walikuwa hai na wamesoma na wale walioona wamesoma na hakuna aliyesema kuwa nimesema uongo.
Nakuwekea hapo chini taazia niliyomwandikia Augustino Mrema.
Ndani ya taazia hii nimekuchanganyia mambo.
Mambo haya yatakusaidia kuelewa mengi ambayo naamini hukupata kuyasikia wala kuyajua kabla ya kuyasoma kutoka kwangu:
TAAZIA: AUGUSTINO MREMA (1944 - 2022)
Mohamed Mlamali Adam alimwandikia taazia Thabit Kombo alipofariki.
Kalamu ya Mlamali akiandika kwa lugha yeyote iwe Kiswahili au Kiingereza inastarehesha lakini pia inaumiza kwani inakata kama upanga wa Sayyidna Ali.
Naisoma taazia na kuirejea mara mbili mbili.
Nairejea kwa sababu inanitatiza.
Hii ni taazia au makala ya kawaida tu?
Najiuliza.
Taazia inapitisha kichwani mwangu maisha ya mwanasiasa mkubwa katika historia ya mapinduzi ya Zanzibar lakini sioni kitu hiki ndani ya taazia.
Haikuwa taazia kama taazia zilivyozoeleka kuandikwa.
Kwa nini?
Ninachokiona kinalingana na maneno ya Cassius katika Julius Caesar anapomweleza Brutus ukubwa wa Colossus (sanamu kubwa la mtu) na akilifananisha hilo Colossus na na kiongozi wa Roma, Julius Caesar.
Najiuliza Mlamali anataka kutupa ujumbe gani katika maisha ya Thabit Kombo?
Mimi nalijua Colossus na nayajua maneno ya Cassius:
CASSIUS: Why, man, he doth bestride the narrow world
Like a Colossus, and we petty men
Walk under his huge legs and peep about
To find ourselves dishonorable graves.
Men at some time are masters of their fates.
The fault, dear Brutus, is not in our stars,
But in ourselves, that we are underlings.
(Sawa kwani aitagaa dunia finyu hii
Kama jitu na sisi vijitu vidogo twapita
Chini ya miguu yake na kuchungulia kote
Na kujikuta katika makaburi ya fedheha.
Watu wakati mwingine hutawala sudi zao.
Lawama, mpenzi Brutus, si la nyota zetu
Kwamba tu watu wa chini, bali ni letu wenyewe).
(Kutoka tafsiri ya Julius Nyerere ya ''Julius Caesar,'' (1963).
Mwalimu Nyerere katafsiri ''Colossus,'' kama ''Jitu.''
Kuna mtu alipata kusema kuwa katika tafsiri hii Mwalimu alifanya kazi ndogo sana na tafsiri yote ilimwelemea Sheikh Abdillah Nasir aliyekuwa Mkurugenzi wa Oxford University Press (OUP), Nairobi.
OUP walihamaki sana kwa kauli hii kiasi huyu mwalimu wangu juu ya kuwa alikuwa na msaada mkubwa kwao walimtoa kwenye jopo la kuandika Kamusi ya Kiswahili.
Nilikwenda kumtembelea Sheikh Abdillah Nasir nyumbani kwake Mombasa miaka michache iliyopita na nikamuuliza kuhusu hili.
Sheikh alicheka sana.
Turejee kwa Augustino Mrema.
Siasa za Afrika ukizitafuta katika kitabu kama hicho hapo juu utazikuta humo.
Unachohitaji kufanya ni wewe ujifunze kutafsiri maneno na matukio.
Shakespeare anazungumza kuhusu ''majitu,'' na ''vijitu'' na wale wadogo na wanyonge, watu dhaifu walioko chini miguuni, watu wasio na sauti wala watu wa kuwatetea.
Sasa kinapotokea kifo cha mtu aliyekuwa mkubwa akawa na sauti watu haraka humkumbuka kwa yale yake.
Kuhusu Thabit Kombo alipokufa Mlamali aliandika maneno haya:
‘’The death of Thabit Kombo reminds one of other old grand venerable founding fathers of the ruling party in Tanzania.
The good Samatitan John Rupia whose property was later nationalised.
The nice cheerful Mzee Sampat who toiled for measly wages and died a poor man.
The Sweet Abdul Sykes who risked his job as Market Master under colonial government in order to set up the party.
And others.
They have passed away, their dedication and love of country not quite fully requited.
Thabit, however, has all along had it good.
Neither his power and reputation nor his immense wealth were ever assailed.
How did he do it?’’
(Africa Events October 1986).
Si bure kuwa Mlamali kawataja watu watatu kutaka watu wafanye ulinganisho katika yale waliyoifanyia nchi yao bila kutaka kufaidika binafsi.
Kamtaja John Rupia, Mzee Sampat na Abdul Sykes.
Ikiwa ulipata kuwajua wazalendo hawa utaelewa Mlamali amekusudia kusema kitu gani.
Ukisoma kitabu cha Rais Ali Hassan Mwinyi, ''Mzee Rukhsa Safari ya Maisha Yangu,'' (2021) Rais Mwinyi kamweleza Augustino Mrema (uk. 269 - 273) kwa njia ambayo msomaji atajiuliza ashike lipi?
Kipi msomaji aamini kuwa hivi ndivyo alivyokuwa Mrema?
Mimi nilijiuliza.
Mrema anaingia wapi katika ile kauli ya Cassius ya, ''Jitu'' na ''Vijitu?''
Rais Mwinyi anasema katika kumbukumbu zake kuwa Augustino Mrema ilifikia wakati akiwa Waziri wa Mambo ya Ndani na Makamu Waziri Mkuu aliweza kumfunika Rais wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzania (uk. 270).
Katika utawala wa Rais Mwinyi na uhusiano wake na Augustino Mrema ni pale Mrema alipopambana na Waislam kutokana na sakata la kuvunjwa kwa mabucha yaliyokuwa yanauza nyama ya nguruwe ndiko hakika unaweza kusema hapo ndipo Rais Mwinyi alipopokonywa madaraka na nguvu zake kama Rais.
Sakata hili liliwaumiza watu wengi sana.
Mmoja katika hao alikuwa marehemu Sheikh Kassim Juma mtu aliyekuwa rafiki wa Rais aliyekamatwa akiwa njiani akielekea Nairobi kwenye matibabu.
Nyakati zilikuwa ngumu kwa Waislam.
Kwa mara ya kwanza Waislam waliandamana na kupambana na vyombo vya dola katika mitaa ya Dar es Salaam, Mrema akiwa hayuko mbali katika fikra na vinywa vyao.
Katika kitabu chake Rais Mwinyi kamsifia Mrema.
Mrema alipoamua kujitoa CCM na kuhamia upinzani gazeti la CCM Uhuru, gazeti la chama ambacho Rais Mwinyi alikuwa mwenyekiti wake lilimtangaza na kumpamba Mrema vizuri ukurasa wa mbele kwa wino mweusi uliokoza.
Mrema kwa hili akawa kasimama pazuri sana kwani alikuwa msumari wa moto juu ya kidonda cha Rais Mwinyi.
Rais Mwinyi alipata kumfananisha Mrema na kichwa cha gramophone kilichokwama kwenye santuri iliyomeguka pale alipokuwa akimshambulia yeye katika kesi iliyokuwa mashuhuri ya Chavda.
Mrema kama alivyopanda ghafla na ghafla akafifia aste aste yaani kwa taratibu akawa kama vile hakupata hata kuwepo.
Pamoja na yeye na chama chake ambacho Mrema alikuwa mwenyekiti, nacho kikawa pembeni kikimsindikiza kutoweka pazia lilipoanza kujifunga na wale waliokuwa ukumbini wakiangalia onesho wakinyanyuka vitini kutoka nje ya ukumbi.
Cassius alipata kuzungumza kuhusu "Vijitu," wakichungulia chini ya miguu mikubwa ya "Jitu."
Kipande hiki katika mchezo maarufu wa William Shakespeare, ''Julius Caesar,'' ni
moja ya vipande ninavyovipenda sana.
Tumuage Augustino Mrema kwa salama kwani juu ya yote kaisaidia Tanzania
kujielewa na kuielewa historia yake kwani juu ya yote aliyofanya, Rais Mwinyi kiongozi mkuu wa serikali aliyoitumikia kisha akaiasi kamsifia kwa maneno haya:
''Pamoja na hila zote alizozifanya ili kujisogeza kwenye barabara ya kuendea kwenye urais, Mrema alifanya mengi mazuri katika enzi ya utawala wangu.
Sina budi kukiri deni la hisani kwangu - kama si kwa nia njema basi kwa vitendo vyake.''
Buriani Augustino Lyatonga Mrema.
Nguruvi3,
Naamini kuna mengi hukuwa unayajua.
Ulipata kumsikia Mzee Sampant akitajwa katika historia ya TANU?
Ulipata kusikia historia ya Abdul Sykes anaunda TANU akiwa Market Master Kariakoo?
Umesoma popote historia hii.
Siku zote historia ya TANU na uhuru wa Tanganyika ilikuwa inaanza na Julius Nyerere.
Mlamali alipomtaja Mzee Sampat au Abdul Sykes tumsihi aseme kweli?