Usiku ule baada ya kumaliza gemu wazo la kutaka kumwuliza kuhusu jana yake kuonekana akiwa kwenye gari maeneo ya Point likanijia. Kawaida ya Khumbu alikuwa hapendi mno kuulizwa maswali ya kumtilia mashaka au ya kuonyesha simwamini. Hivyo nilijua nikianzisha hiyo mada tutaishia kugombana. Nikaamua kupotezea.
Maisha yaliendelea na mahusiano yangu na Khumbu yaliendelea mpaka nimemaliza chuo japo hapo katikati kabla ya kumaliza chuo ulitokea ugomvi mkubwa sana uliosababisha tuachane kwa muda.
Kuna siku Khumbu aliniambia amepata kazi benki, bank teller hivyo sasa hivi hatakuwa anapatikana sana kama zamani. Alichokuwa anamaanisha ni kwamba hataweza kuwa anakuja kila nitakampomuhitaji, hivyo siku nikimuhitaji halafu akashindwa kuja inabidi nimuelewe.
Baada ya Khumbu kupata kazi tukawa tunaonana mara moja moja sana. Inaweza kupita hata wiki mbili hatujaonana, sikuona tabu sana maana nilijua kwa sasa ana majukumu ya kikazi. Maisha hayo ya kutokuonana mara kwa mara ndio yaliendelea hadi mwisho wa penzi letu.
Siku moja, ilikuwa siku ya Jumapili, Khumbu alinipigia akaniambia nisitoke nyumbani anakuja kushinda na mimi. Hapo tulikuwa hatujaonana karibia kama wiki mbili hivi, hivyo nilikuwa nimemmiss hatari. Ikumbukwe nilikuwa sina mwanamke yoyote zaidi ya Khumbu hivyo hata siku mbili tu nikiwa sijamuona nilikuwa nammiss hatari, sometimes hisia za Khumbu zikinijia nilikuwa napata mfadhaiko, nakuwa kama mgonjwa. Kwa hiyo kutokuonana na Khumbu kwa wiki mbili ilikuwa mateso sana. Kwanza nilikuwa simuamini kabisa. Nilikuwa najua hizi wiki mbili lazima kuna mtu kama sio watu wanamchakata.
Mida kama ya saa sita akanipigia simu ananiambia yupo getini nikamfungulie. Nikachukua rimoti ya geti nikaelekea getini. Kufika hapo getini nashangaa simuoni ila kuna gari mpya aina Polo Vw ipo hapo getini inataka kuingia. Ikabidi nisogee kabisa hapo getini kuangalia Khumbu yuko wapi. Kikawaida unaweza kufungua geti hata ukiwa umbali wa mita 100, kwa hiyo nilitegemea ningemuona Khumbu kasimama hapo getini hivyo ningemfungulia geti bila ya kwenda kwenye geti, yaani ningebonyeza tu rimoti nikiwa kwa mbali na mgeni wangu angeingia. Nilienda mpaka getini kumwangalia Khumbu pia kuiangalia hiyo gari iliyokuwa pale getini inasubiria kuingia. Kwa mshangao Khumbu ndio alikuwa mwenye ile gari, nilipofika getini alishusha kioo cha gari na kuchungulia ili kunipa ishara ni yeye hivyo nifungue geti aingie.
Aliingia na nikamwonyesha sehemu ya kupaki gari yake. Mmh! Khumbu alikuwa amevaa miwani ile ya kisista du rangi kama ya ugoro hivi, nywele kazibana kwa nyuma. Kavaa blouse mikono mifupi imemshepu kimwili chake vizuri hatari. Chini katupia suruali ya kadeti zile za mabaka mabaka kama za jeshi, hakika alipendeza. Nikamkaribisha ndani huku najiuliza huyu kapata wapi hili gari? Kazi yake ya ubank teller ndio kanunua na gari? Au kuna sponsa?
Inaendelea