Kilimo cha Nyanya: Aina za mbegu, mbinu za kulima na masoko yake

Kilimo cha Nyanya: Aina za mbegu, mbinu za kulima na masoko yake

Aina gani ya Nyanya inastahimili mvua bila kuharibika
 
Wakuu heshima kwenu kwa michango hapa nami nachangia kuhusu Aina za nyanya tu kidogo kadri ninavyozifahamu ili kuongezea akiba ya taarifa.

Money maker: Hii ni aina ya siku nyingi sana ni nyaya za kusimikia mti unabakiza shina moja au mawili mara nyingi zikifikia mikungu 5 au 6 unatakiwa ukate juu. Zinatabia ya kupasuka matunda zikipata maji mengi hasa wakati wa mvua shauri ya ganda laini, hazikai muda mrefu na hazistahimili misukosuko ya safari ndefu!

Roma: Ni nyaya zinazaa sana na ni aina ya mbegu ya enzi na enzi, zinangozi laini, hivyo hazikai muda mrefu mezani kwa mfanyabiashara na zinapondeka kirahisi zinaposafirishwa mbali. Roma ni nyanya tamu sana kwa kachumbari na zina mchuzi mzito lakini zinatabia ya kukauka kitako chake kirahisi sana zinapokabiriwa na ukame au udongo wenye chumvi.

Marglobe: Hii inahitaji kusimamishiwa kwa kufunga kwenye kijiti na mara nyingi hupunguziwa na kuachwa shina moja tu, matunda yake ni makubwa sana na machache nayo inangozi laini haistaimili misukosuko ya kusafirisha.

Tengeru (97?): Hii ni aina ya mbegu zilizozalishwa na watafiti wa kitanzania, inahitaji kusimamishiwa kwa kufunga kwenye kijiti na mara nyingi hupunguziwa na kuachwa shina moja, matunda yake ni makubwa sana na machache hii aina nyanya zake zinaganda gumu hustahimili kusafirishwa na huvumilia magonjwa ya mnyauko, mavuno yake makubwa.

Tanya: Hii ni aina ya mbegu zilizozalishwa na watafiti wa kitanzania, nikifupi cha Tanzania Nyanya. Aina hii haipunguziwi matawi. Ni nyanya nzuri sana zinazokidhi matakwa ya soko inaweza kusafirishwa mbali na inakaa muda mrefu mezani iwapo sokoni. Umbo lake ni matunda marefurefu mfano wa yai isipokuwa ncha zake ni bapa kidogo si mchongoko kama yai.

Ukibahatika kupata mbegu Original ya aina hii utaifurahia kwani matunda yake ni mengi, makubwa na yanavutia sana umbo lake! Angalizo ni kwamba makampuni mengi yanauza mbegu ya Tanya iliyochanganyika kiasi kwamba imefanya wakulima wengi kuichukia mbegu hii! Nimewahi kuilima ilipofikia mavuno nilichoona sikuamini! Ilikuwa ni mchangayiko wa Roma, Marglobe, vigorori na mtepeto, yaani wateja wangu walinikimbia! Ni mbegu nilizonunua kwenye makopo yaliyopakiwa na East African Seed Company, ndugu zangu muwe makini, makampuni ya kibongo yakiishiwa mbegu hukusanya nyanya kwa wakulima na kuzikamua tu! Kuweni macho ikibidi tunzeni mbegu zenu. Mbegu za makampuni ya Kikwetu ninaziogopa sana, utapeli ni mwingi tu na wenye pesa wako above the law!

Cal J: Aina hii haihitaji kupunguziwa matawi, inazaa sana. Ina ngozi ngumu na kwa kweli hustahimili hekaheka za usafirishaji yaani ni mawe, wengine huziita dumudumu, kuna wakati matunda pia hupasuka mvua ikizidi. Hii ni aina maarufu maeneo maarufu ya kilimo cha nyanya.

Rio Grande: Hii ni aina mpya ambayo imekuja kuuwa umaarufu wa Tanya huachwa kutambaa haihitaji kupunguziwa matawi. Aina hii ni aina ya kisasa zaidi inayojibu mahitaji ya soko kwa kuweza kustahimili kusafirishwa masafa na kukaa muda mrefu mezani sokoni (shelf life). Hii ni aina nzuri sana ya nyanya zenye umbo la yai, aina hii humwaga maua na matunda bila kelele, hutoa majani kiasi na inapokunya matunda shambani utaona shambani yanaonekana matunda tupu! Kama ningelima leo ningechangua mbegu hii.

Ornyx: Hii ni aina mpya ambayo imekuja kuuwa umaarufu wa Tanya. Aina hii haihitaji kupunguziwa matawi. Aina hii ni aina ya kisasa zaidi inayojibu mahitaji ya soko kwa kuweza kustahimili kusafirishwa masafa na kukaa muda mrefu mezani sokoni (shelf life).

Aina hii ina matunda makubwa na mengi kuliko Tanya. Matunda yake umbo ni mfano wa yai. Inafanana sana kama Rio Grande, ingawa haifikii uzazi wa Rio Grande. Kwa uzoefu wangu shambani Rio Grande iko juu zaidi ya Orynx.

Nimewahi kuona mbegu za Mkulima Seed Company kopo limewekewa label iliyosomeka 'Rio Grande (Orynx)' ! Inashangaza sana kwa vile hizo ni aina 2 tofauti! Nadhani ni kumpa picha mkulima aliezoea aina mojawapo aone ni ile ile! Yaani aliyezoea Oryx anunue na aliyezoea Rio Grande anunue, lakini huo ni wizi, ni utapeli hizo ni aina tofauti kabisa za nyanya japo zinafanana muonekano wa matunda yake!

Anna F1: Hii ni aina chotara, shina tawi moja au mawili husimamishwa kwa miti, hurefuka urefu zaidi ya mita tano, shina moja huzaa kuanzia kilo 25, ni aina maalum kwa green house ingawa huzalishwa pia nje, unavuna miezi zaidi ya 6, mbegu zake ni ghari sana. (Msifikiri ni hadithi nyingine ya machungwa 4000 kwa mti nina Hand book yake ukipenda niPM nikugawie).

NB: Kusimamishia miti!
Wakati wa masika au umwagiliaji ni lazima kusimamishia miti aina yoyote ya nyanya maana zinapogusana na udongo wenye unyevunyevu huoza.

Unapochagua aina ya nyanya za kupanda angalia soko lako linapenda aina gani ya nyanya ingawa huwa zikiadimika nyanya ni nyanya tu hakunaga kuchagua!

Samahani mimi nami sijuagi kuandika maelezo mafupi msinichoke mwee enh jamani!!
Much love 💕 💕
 
Mkuu Nyamburi asante kutambua uwepo wangu, acha nianze kuchangia na wadau wengine wataendeleza nitakapoishia. Kuna thread moja ilianzishwa hapa kuna mdau alikwama kupata wanunuzi wa nyanya (Dakawa) Dumila Morogoro akaandika hapa kuomba msaada wa kuunganishiwa wanunuzi. Kuna mchango mwingi wa mawazo kule kwenye thread hiyo nadhani hapa ni suala linalojirudia.

NI hivi: 1) Nyanya za kiangazi hufanikishwa na kufaidiwa sana na wakulima wenye mitaji mikubwa ambao huwa wanalima kwa maeneo makubwa sana kuweza kujaza FUSO mwenyewe na kusafirisha masoko ya mbali. Ijapokuwa bei ni ndogo lakini kwa kuwa huwa wanamzigo mkubwa na gharama za uzalishaji ni ndogo sana huwa wanaingiza pesa kubwa sana. Kuna wakulima wengi sana aina hii ukifika msimu wa kilimo cha kiangazi huja kwa wingi sana mkoani Morogoro maeneo ya Dumila, Mbigiri na mabonde ya Kilosa na pia eneo la Doma kuelekea Mikumi. Wakulima hawa ni wenye mitaji mikubwa hasa toka Iringa na maeneo mengine, huja msimu wa kiangazi kulima nyanya hizi kwa wingi sana, na wao hata bei ikiwa ndogo husafirisha kupeleka masoko ya mbali ikiwamo Dar! Mkulima mdogo mdogo akilima msimu huu sana sana ndiyo huishia kuwauzia hao wenye uwezo wa kusafirisha na bei ambayo hupewa ni ya kutupa karibu na bure.

2) Kilimo cha nyanya za kiangazi ni kilimo kisichokuwa na changamoto ukilinganisha na nyanya za masika. Majira ya kiangazi kuna ubaridi na hewa kavu magonjwa hayashamiri sana na nyanya huzaa kwa uwezo mkubwa kuliko majira ya mvua. Nyanya huzaa mavuno makubwa sana kiangazi kuliko majira ya mvua ambako huwa kuna joto linalopukutisha maua na matunda.

3)Hata hivyo uzoefu wangu maeneo ya Morogoro kwa ujumla kwa mfano nyanya zisizokuwa na changamoto ni kuanzia mwishoni mwa mvua na kupitia kipindi chote cha baridi nyanya za mwisho zivunwe mwezi wa nane. Kuanzia mwezi wa tisa huwa kuna changamoto ya ukame ambapo umwagiliaji lazima uwe wa karibu karibu zaidi, pia hutokea wadudu ambao ni nuksi sana, wanaitwa red spider mites, ni kama utitiri mwekundu, hawa ni wabaya sana kuanzia majira ya joto kali yanapoanza. Hawa wadudu ndiyo hupausha majani na matunda yanapoiva kuwa kama rangi ya machungwa. Kuanzia mwezi wa kumi hadi kipindi chote cha joto kali mimea ya nyanya hupunguza sana uzaaji kwani maua huwa yanapukutika tu au hayarutubishwi kwa hiyo nyanya zinazozaliwa ni chache. Na pengine ni kipindi hiki nyanya huanza kuadimika na bei huanza kupanda juu.

Kwa hiyo nahitimisha kwa kusema kuwa kupindi cha kiangazi kina awamu mbili, awamu ya kiangazi baridi ambacho huishia mwezi wa nane na ndicho nyanya huzalishwa kwa wingi sana bila changamoto na awamu ya kiangazi joto kinachoanzia mwezi wa tisa hadi mvua zinapoanza, kipindi hiki ni cha wadudu nuksi, ukame mkali na uzaaji duni wa nyanya shauri ya joto kali linaloathiri uchavushaji na urutubishaji maua. Nawasilisha wakuu !!
Too much respect!!
 
Back
Top Bottom