Habari za jumapili wapendwa,
Leo nina kisa kioja swali...
Kwenye pilika pilika zangu za umesenja nikiwa fildi huko kukusanya dodoso kwa ajili ya miradi kadha wa kadha inayofadhiliwa na watu wa Mashariki ya mbali ndo nilikutana na kioja hiki.
Nilikaribia nyumba ya nne tangu nianze kukusanya dodoso nikiwa nimeambatana na mwenyeji wangu baada ya kunitambulisha yeye aliondoka kuendelea na shughuli zake na kuniacha mie niendelee na dodoso.
Baada ya dodoso kuisha nikiwa nataka kumuaga yule mwenye nyumba nirudi nilipofikia - nyumba ya kulala wageni... yule baba akaniambia mwanangu nina maswali.... nikamsikiliza na kumjibu kwa ufasaha. Akaniambia amejisikia tuu kunisimulia kisa alichokumbana nacho kwenye maisha yake na kumfanya hadi wakati huu hana familia. Ni babu mzee ambaye anajiweza kujimudu ila ndo anaishi mwenyewe na hana mtoto wala mke.
Basi mpenda masimulizi mie nikarudi kuketi nimsikilize babu ananisimulia nini.
Mwanangu, usemi wa kumwambia aliyekuwa mke wangu kipindi hicho umenifanya hadi leo sina familia Maana niliumia sana na sikuwa nimemaanisha alichokielewa mwanamke yule.
Huo mwaka hali ilikuwa ngumu mazao shambani hayakukubali biashara ya samaki mtoni pia ilikuwa ngumu. Nakumbuka siku hiyo nilirudi nyumbani saa kumi alasiri nikiwa sina kitu kwa ajili ya familia kula, nikamwambia mke wangu "FANYA MAARIFA BASI LEO TULE "nimerudi mikono mitupu.
Mke wangu aliguna na kubinjua midomo huku akinitizama kwa jicho la upande.... nakumbuka hakuniambia anaenda wapi ila alijitanda khanga na alitoka. Nilisikia harufu ya marashi aliyopaka baada ya kupiga hatua takriban tatu hivi. Nikakaa uani kusubiri maarifa ya mke wangu, kweli saa 12 jioni alirudi na kibaba cha mahindi, unga na choroko na usiku ukapita. Hilo ndo lilikuwa kosa langu tangu hapo mke wangu alianza kutembea na wanaume pale kijijini akisingizia anafanya maarifa tusilale njaa hata kama nikirudi na kitoweo nyumbani. Hali ile sikuweza kuivumilia nilimrudisha kwao na hatukuwa tumebarikiwa watoto. Tangu hapo sikutaka tena kuishi na mwanamke.
Sasa mwanangu hebu niambie. .. kwanza wewe una watoto? Nikamwambia hapana, umeolewa? Nikamwambia hapana...
Ila hivi mwanaume akamwambia mwanamke wake FANYA MAARIFA huwa mnaelewa kuwa amekutuma ukatembee na wanaume ndo ulete chakula nyumbani? Nikamwambia baba hapana si unaona mie niko kazini hapa ndo nipate mlo wangu japo sina wanaonitegemea.
Wewe unaelewaje?
Nikamwambia ningekuwa mie ningeenda kwa mwanamke mwenzangu pale kijijini aniazime kibaba cha unga na maharage au kunde kisha ukipata namrejeshea na si kwenda kukiuza kwa wanaume.
Haya mwanangu nakutakia kazi njema. Nikamjibu asante baba.
Swali kwa wakaka.....
Huwa inatokea siku hauna kitu na unaomba mwenzi wako aku assist? Anapokeaje ombi lako? Je ni fedheha kwako?
Swali kwa wadada na wamama....
Kufanya maarifa unaelewaje hasa ukiambiwa na mwenza wako siku anapokuwa hana kitu. Ni sawa au unaona si sawa?
Wiki moja baadae nikiwa kwenye sehemu ya umma wa watu wengi, mschana mmoja akiwa anaongea na wenzie akasema... mie bwana angu akiniambia mke wangu leo sina kitu fanya maarifa.... naenda kutembea na bwana nyuma yake tuu hapo mtaa wa pili wala siendi mbali....
Unafikiri kwanini huyu mschana amewaza hivi?
Kasie Mahaba.