Nimeupata ujumbe huu toka kwa mtumishi wa Mungu aliye uweka katika gazeti la mwananchi,kiimani tunaambiwa tuamini chochote kilicho katika kitabu Kitakatifu (biblia),...huyu babu yuko kinyume kabisa na biblia,.....tusikimbilie huko,na kama hatujaona huzi ni nyakati za mwisho!!
Tunaishi nyakati za mwisho.
Neno la Mungu linasema waziwazi kuwa nyakati za mwisho zitakuwa ni siku za hatari, hatari kubwa inayomaanishwa hapa ni watu kujitenga na imani na kufuata roho zidanganyazo 1Tim. 4:1.
Biblia pia inasema, nyakati hizi za mwisho watatokea makristo wa uongo, na manabii wa uongo, nao watatoa ishara kubwa na maajabu; wapate kuwapoteza, kama inawezekana, hata walio wateule Mt.24:23-24.
Ibilisi anahangaika kuwapeleka watumishi wake wengi kwa lengo na kuwavuta na kuwapoteza watu wasikae katika mapenzi ya Mungu, ili hatimaye wakataliwe na Mungu. Kwa sababu hiyo basi, tunapaswa kuwa makini sana na mambo yote yanayotokea nyakati hizi.
Kwa sasa hivi, kwa sababu kanisa bado halijanyakuliwa , mpinga kristo bado hajafunuliwa. Lakini roho yake tayari inatenda kazi.
Neno la Mungu linasema kuwa kutenda kazi kwa roho ya mpinga kristo kunaambatana na ishara na ajabu za uongo ili kuwavuta na kuwapoteza wanadamu 2Thes. 2:7-12, Uf.13:11-14.
Kwa hiyo ndugu zangu, tunapaswa kuwa makini sana katika kila jambo, tusiwe wepesi wa kuchulikwa na kila upepo unaovuma. Hata kama mtu atasema kuwa anatumiwa na Mungu, bado hatupaswi kuwa wepesi wa kukubaliana naye. Kumbuka Yesu alisema wengi watasema siku ile bwana bwana tulifanya miujiza kwa jina lako naye atasema ondokeni sikuwajua ninyi kamwe.
Ninaposema hivyo simaanishi kuwa miujiza yote inatokana na ibilisi, iko miujiza mingi tu inayotokana na Mungu mwenyewe na haina tatizo kabisa.
Kitu cha msingi hapa ni kuwa tunapaswa kuwa na uwezo wa kutofautisha kipi ni kipi ili tusiingie kwenye mtego wa ibilisi.
Mungu wetu ametupa nafasi wa kuyapima na kuyajaribu mambo yote ili tuweze kutofautisha 1Thes. 5:20-22, hatupaswi kuudharau unabii wowote bali kwanza tunapaswa kuupima na kuona kama unatoka kwa Mungu au la. Ikiwa ni wa Mungu tutaushika, la sivyo tutautupilia mbali.
Tunaupima unabii kwa namna gani?
Ni kwa kutumia Neno la Mungu pekee.
Biblia inasema katika Isaya 8:20 kuwa ikiwa watu hawaendi sawasawa na Neno la Mungu, kwao hakuna asubuhi. Asubuhi inamaanisha nuru, na kinyume cha nuru ni giza na giza maana yake ni dhambi. Chochote kile ambacho hakipo sawasawa na Neno la Mungu ni giza, ni dhambi.
Tena Neno la Mungu linasema katika 2Kor.13:8 kuwa hatuwezi tukafanya jambo lolote lililo kinyume na kweli ya Neno la Mungu.
Kuna alama zinazoweza kutusaidia kutambua miujiza ya Mungu.
I. Ishara na miujiza ya Mungu inaambatana na hao waaminio Marko 16:17-18, Luka 10: 17-20. Waaminio ni wale waliompokea Yesu na kumfanya kuwa Bwana na mwokozi wa maisha yao, ni wale waliookoka. Kama mtu hajaokoka kamwe hawezi akatumiwa na Mungu kufanya ishara yeyote. Swali jepesi sasa, huyu babu wa Loliondo ameokoka? (anajua babu mwenyewe yuko upande gani lakini hatu muhukumu kwa hili)
II. Ishara na miujiza huthibitisha Neno la Mungu linalohubiriwa Marko 16:20. Tujiulize, huyu babu anahubiri Neno lolote la Mungu au anagawa dawa tu? Tukumbuke kuwa Mungu wetu anataka kwanza watu wapone roho zao kabla hata ya kuwaza kupona miili yao. Ndio maana akasema utafuteni kwanza ufalme wa mbinguni na mengine mtazidishiwa. Hata kama mtu atapewa hiyo dawa akapona lakini lazima iko siku atakufa tu, sasa akifa atakwenda wapi? Ndio maana Mungu nahitaji kwanza roho zetu zipone. Huyu babu ni sawa na mganga wa kienyeji tu, hana injili yeyote anyohubiri. Anawaza kuponya miili tu wakati Mungu anahitaji tuanze kwanza kuponya roho zetu.
III. Miujiza ya Mungu wa kweli lazima ifanyike kwa jina la Yesu tu Marko 16:17, Luka 10:17, Mdo. 3;1-10. Miujiza ya Mungu haifanyike kwa kutumia mizizi ya miti, ni kwa Neno, ambaye ndiye Yesu Kristo.
IV. Neno linalohubiriwa lazima liwaongoze watu kutubu dhambi zao ili wamgeukie Mungu wao Mdo. 3:19. Sasa pale Loliondo mmesikia kama watu wanatubu dhambi zao na kumrudia Mungu wao au wanapewa dawa tu. Hakuna Mungu hapo, ni uganga tu ndio unaoendelea hapo.
V. Toba ya kweli lazima iwaelekeze watu kwa Yesu Hes. 21:4-9, Yoh. 3:14-15
VI. Mungu hulituma Neno lake ili kuwaponya watu Zab. 107:18-20. Mungu anaponya kwa Neno tu, sio kwa mizizi ya miti au chochote kile.
VII. Yesu Kristo alipokuwa anawatuma wanafunzi wake kwenda kuhubiri na kuponya magonjwa aliwaagiza kuwa mmpewa bure toeni bure Mt. 10:8. Sasa mambo ya watu kutoa mia tano yanatoka wapi sasa? Uzima wa Mungu ni bure kabisa, hakuna biashara yeyote inayofanyika, ni karama ya Mungu tu. Kinachoendelea Loliondo hakipo kabisa katika mapenzi ya Mungu, hata kama duniani nzima ingelihamia hapo.
VIII. Karama za Mungu haziwekwi kwa mtu mmoja tu, dunia hii ni kubwa na Mungu hawezi akaweka mtu mmoja tu kwa ajili ya kazi yake 1Falme 18:20, 19:18. Yule babu kusema kuwa ni yeye peke yake aliyechaguliwa na Mungu kuleta uponyaji, huu ni uongo ulio wazi kabisa, hayo ni masharti ya waganga wa kienyeji kabisa. Karama za Mungu wa Biblia zinaambatana na kuwafundisha wengine jinsi ya kutumiwa na Mungu kama Yesu alivyofanya, sio mtu mmoja tu. Tena, karama za Mungu hazifungiwi na sehemu moja tu. Eti dawa itolewe hapo kijijini tu, hayo ni masharti ya mizimu tu, Mungu hayupo hapo. Yesu alisema enendeni ulimwenguni wote, sio mkae kwenye kijiji kimoja ambacho hata hakifikiki kirahisi Marko 16:15
Ndugu zangu, nawasihi kwa jina la Bwana na mwokozi wetu Kristo Yesu, tusiwaze tu juu ya uponyaji wa miili yetu na tukasahau uponyaji wa roho ambao ndio wa muhimu zaidi. Hata kama tukipona leo, iko siku tutakufa tu. Kwa hiyo lolote tunalolifanya leo ni muhimu tuhakikishe kuwa linakubalika mbele za Mungu wetu.
Suala hapa sio kupona tu, lakini lazima tujue huo uponyaji unatoka wapi. Wagonjwa wengi tu wa ukimwi na magonjwa mengine sugu wameshapata kuponywa kwa njia ya maombezi tu katika jina la Yesu, lakini ajabu ni kwamba habari zao hazikuvumisha kama hili la Loliondo. Wakati wote imekuwa ni vigumu sana kwa vyombo vya habari kutangaza habari njema kama hizo zinatokea makanisani kwa sababu ibilisi hataki watu waufahamu ukweli huo. Hata zinapotangazwa bado, mwitikio unakuwa ni mdogo sana. Lakini hili kwa kuwa ni la kwake mwenyewe ibilisi ndio maana limepigiwa kelele na vyombo vyote vya habari, hata na viongozi wa ngazi mbalimbali serikalini wamekuwa mstari wa mbele kulishabikia na kulienzi. Ni kama upepo fulani unawachukua watu wote bila kujijua na kila mtu anawaza kuwahi kunywa hiyo dawa tu. Tusiwe hivyo ndugu zangu, bali tutafakari na kuyapima yote kwa Neno la Mungu.
Mwisho, Mungu akubariki sana na washirikishe wengine ujumbe huu.
Note:Being an anti-christ does not only mean being against christ,but also imitating to be like christ