Sijaona kwenye amiri za Mungu, inayosema 'usiasi' wala 'usisaliti', lakini kuna amri ya Mungu inayosema 'Usiseme UONGO'.
Kuna maana kubwa sana Mungu kutokataza Uasi na Usaliti, kimsingi kabisa maendeleo yote ya mwanadamu yametokana na 'Uasi na Usaliti'. Kuna wengine tulizaliwa familia masikini na wazazi wasio na elimu, lakini tuliasi na kusaliti historia yetu ya umasikini na kukosa elimu, matokeo yake tumepata maisha bora na maarifa. Isingalikuwa 'uasi na usaliti' wengi tungalikuwa tunaishi maisha yale yale waliokuwa wanaishi wazazi wetu.
Isingalikuwa 'Uasi na Usaliti', dunia leo hii ingekuwa na mfumo mmoja wa kufikiri, kwa sababu watu wangeridhika na aina moja ya mawazo. Lakini sivyo, 'Uasi na usaliti' umefanya dunia imekuwa na aina tofauti za mifumo ya kiuchumi, dini za aina tofauti, lugha za aina tofauti, siasa za mirengo tofauti, na mambo mengine mengi ambayo yanafanya dunia yetu iendelee kuwa ya tofauti na yenye kupiga hatua.
Mpaka hapo, tunaona 'Uasi na Usaliti' umewekwa makusudi na Mungu, ili kuleta mabadiliko ya maisha ya mwanadamu katika ulimwengu huu.
Lakini Mungu, kutukataza 'Kusema Uongo' alikuwa na somo kubwa sana kwamba wanadamu, kwamba tufanye 'Uasi na Usaliti' kwa haki, kwa ukweli na kwa uwazi. Kamwe tusitumie njia za hila, hila ni ulimwengu wa shetani. Na palipo na hila kuna utitiri wa dhambi; rushwa, kusema uongo, mauaji na madhila mengine mabovu.
Hila imetajwa sana kwenye vitabu vya Mungu, ikipigilia msumari ni kitu kisichokuwa na baraka ya kimungu.
"Kwa sababu tunaweza kudanganywa kwa urahisi na mbinu zenye hila za Shetani, ambaye ni fundi katika kufanya mambo yasiyofaa yapendeze, kama alivyofanya alipokuwa akimshawishi Hawa.—2 Wakorintho 11:14; 1 Timotheo 2:14"
"(Ufunuo 12:12) Tusipokuwa waangalifu, propaganda zenye hila za Shetani na watu “wanaodanganya akili” ambao wanatumiwa na Shetani wanaweza kupotosha fikira zetu na kutushawishi tutumbukie katika dhambi.—Tito 1:10. "
"(Ayubu 42:12) Huenda watu wanaotenda kwa hila wakafikiri kwamba wanajinufaisha kwa hasara ya mtu mwingine na hata huenda wakaonekana kuwa wamefanikiwa kwa muda. "
Kwisha kusema hayo, kosa la Halima Mdee na wenzake ni 'Kufanya Uasi na usaliti kwa mbinu za Hila'. Uasi wao hauna baraka za kiMungu kwa sababu, Mungu ametuambia tufanye 'Uasi na Usaliti' tukiwa wakweli kwetu na wanaotuzunguka na kwa njia ya uwazi. Usaliti wao na Uasi umeongozwa na hila za Ibilisi, na kwasababu Mungu amekataa hila, sioni matokeo mazuri ya Uasi na usaliti wa Halima Mdee na wenzake.
Mkereketwa wa nchi ya chama kimoja
N. Mushi